Hilo
nalo Nanaa akasamehe. Akaja kwa msichana wake wa zamani. Frida. Alimuacha
Nanaa, akaishia kufugwa mpaka jela. Napo Nanaa akasamehe wakarudiana. Ikaja
kesi ya Malii tena. Geb akakumbuka kila kitu taratibu. Mara zote aliishia
kuharibu vibaya sana. Akaanza kujichukia nafsi yake, na kuchukia hasira kali
alizonazo, zinazomfanya anashindwa kuzitawala. Zikipanda hasira anashindwa hata
kufanya maamuzi sahihi.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Bado ninaamini Mungu atakusaidia
utatoka salama Nanaa. Uje ulee watoto. Namuomba Mungu akusaidie. Nafikiria
maisha ya watoto bila wewe! Haijalishi nani yupo na hao watoto. Haitakuwa kama
ilivyo sasa hivi. Hii hali ya utulivu hapa. Haijawahi kutokea tokea tuondoke na
watoto. Kwa muda wote huo sikuwahi kurudi nyumbani nikakuta wanangu wapo tu
kama hivi walivyo sasa hivi. Najua ninachoongelea Nanaa. Nimeishi hapo. Hakuna
anayeweza kutuliza hawa watoto kama wewe mwenyewe.” Geb akaendelea.
“Japokuwa
Magesa anaumwa, hakuwa akikufahamu kama mama yake na tupo hospitalini, lakini
upo utulivu mkubwa sana kwetu sisi wote watatu. Ulituona siku mbili tu
zilizopita Nanaa, mimi na wanangu wote tulikuwa hoi! Katika ujinga na mapungufu
yangu yote, na mimi najua umuhimu wako kwenye maisha yangu na wanangu. Naweza
nikawa sijakwambia vyakutosha au sijawahi kukwambia. Labda kila neno linalotoka
kwangu ni tatizo, lakini naomba uniamini katika hili Nanaa, unajua kuishi na
kina Magesa wote. Una jinsi yako yakuleta utulivu fulani katikati yetu.
Japokuwa tunakuwa na ukorofi wetu, mapungufu yetu, lakini unauwezo wa kuwa
katikati yetu na kututuliza na kuweka amani.” Geb akaongeza.
“Kwa
hiyo wakati ukimfikiria Jimmy, naomba utufikirie na sisi. Fikiria jinsi
utakavyotuacha.” “Wewe unaye mwanamke Geb. Maisha yako yanaendelea, kamwe
hayajawahi kusimama.” “Mwanamke gani huyo unayemzungumzia Nanaa!?” “Sara.”
Nanaa alienda moja kwa moja kwenye pointi. Geb akameza mate. Nanaa akamuona
vile alivyobabaika.
“Ni
kweli Sara aliletwa nyumbani. Lakini Nanaa, sijawahi kupata hata dakika moja ya
mazungumzo na yule binti. Na wala mama hakuwahi kuzungumza na mimi juu yake.
Mimi nilijua ni binti aliyekuja pale kumsaidia mama swala la watoto, basi.
Sikujua kama ameletwa kwa ajili yangu na wala hapakuwa na mazungumzo yanayohusu
mimi na yule binti. Nilichokuwa nikijua au nikiambiwa juu yake ni pale
nilipokuwa nikielezwa juu ya watoto. Labda naambiwa wametoka na Sara pamoja na
Jeri, wamepelekwa labda kwa Grace au wanakutana na Danny sehemu ili wacheze na
watoto wao. Nikaona anahusika na watoto wangu na wa Grace kwa karibu sana.
Kuwapeleka sehemu kucheza na kuwazungusha. Ukaribu ukawa wake, mama na Danny
sababu ya watoto. Na ndio kitu alikuwa akipenda kufanya Sara. Au ndio kitu
niliona anafurahia kufanya. Atapenda kutayarishiwa watoto, nakuwapeleka sehemu
za starehe. Lakini si vinginevyo. Sidhani hata kama anajua majina yao. Lakini
Nanaa, nakuapia kwa Mungu wangu. Hata kama angependa watoto na watoto
wangempenda, nisingemuoa yule binti wala sikuwa hata na mawazo yakutafuta
mwanamke. Kwanza nilikuwa nimeumia moyoni.” Geb akaendelea.
“Swala
la mapenzi nilikusudia kuachana nalo kabisa, nilee wanangu tu. Nimejiona hata
mimi sistahili kuwa na mwanamke. Wewe ni shahidi. Nimeweza kufanikisha kila
kitu kwenye maisha yangu, isipokuwa mapenzi. Nimeweza kupanga mambo makubwa na
magumu, nayakafanikiwa. Lakini kila linapokuja swala la mahusiano! Nimekuwa
nikifeli kwa asilimia zote. Nimeamua kuacha niangalie kile ninachoweza kufanya
kwa wanangu tu. Basi.” Nanaa hakujibu kitu.
“Kwa
hiyo Nanaa, kama sio wewe kulea hawa watoto, hakuna mwanamke mwingine atawalea.
Nitabadili maisha yangu. Nitajitahidi mimi mwenyewe kulea wanangu. Kwa shida na
raha. Watakuwa tu. Lakini nakuomba katika mipango unayomfikiria Jimmy na sisi
utufikirie. Mimi na wanangu. Hata kama sio mimi, basi Liv na Magesa. Usikate
tamaa nakufikiria kufa. Naomba tubaki kwenye maombi yakuomba Mungu akuongezee
miaka. Uje ulee watoto wote watatu kwa pamoja.” Nanaa akamwangalia. “Naleaje
watoto wako na wa Malii pamoja, Geb!?” Geb akatulia kidogo.
~~~~~~~~~~~~~~~
Ameshapitishwa
kwenye kashi
kashi za maisha. Akiwa na pesa zake na
jumba au majumba ya fahari, lakini alikuwa hapati usingizi. Alikasirika mpaka
hasira zikamuisha. Nyumba haikuwa na amani. Watoto wanalia mchana na usiku! Akasalimu
amri. Muda mchache aliokuwa na Nanaa pale, aliweza kuwatuliza wanae na yeye.
Liv
alisharudisha kicheko. Nywele alizokuwa hataki mtu aziguse, mama yake aliweza
kumsuka vipande viwili kama minyoosho. Liv akawa amependeza, msafi na ameshiba
vizuri. Japokuwa Geb alikuwa akilala hapo hospitalini, lakini alishapata
utulivu wa namna yake. Kula vizuri, kulala, na akaweza hata kunyoa ndefu.
Magesa hakuwa akilia tena. Garama ya kumpokea mtoto wa Malii ili aishi na
Nanaa, ilikuwa ndogo sana kulinganisha na haso za
maisha alizokuwa akizipata bila Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Nanaa
akajua amemkamata pabaya sana. Geb mtu wa hasira na kutunza mambo moyoni. Sio
mwepesi kusamehe na kuacha mambo yapite tu hivi hivi. “Ilimradi awe anazaliwa
na wewe, haitajalisha, Nanaa.” Nanaa Hakutegemea. Akabaki na mshangao. “Mungu
akipenda, kesho tutaruhusiwa. Nataka kuchukua apartment tena. Pale pale kwenye
ile sehemu tuliishi mimi, wewe na Liv kwa muda mpaka tukahamia pale kwenye ile
nyumba tuliyoikimbia.” Nanaa akanyamaza.
“Na mimi
nataka muda wakutosha na hawa watoto. Nakukaribisha. Kuwa huru kuja kuishi kwa
kipindi chochote unachotaka. Hata kama ni miezi hii michache iliyobaki kabla
hujaenda kujifungua. Njoo upate muda na watoto. Hakuna atakayekusumbua. Hakuna
atakayekuingilia. Ni wewe na watoto tu.” Nanaa akavuta pumzi kwa nguvu.
Akajigeuza upande mwingine. Akamvuta Liv karibu. Akambusu. “Nampenda mama.” Liv
akaongea kwa sauti ya kitoto akiunganisha maneno. Lakini mama yake akaelewa.
“Na mimi nampenda sana Liv.” Liv akafurahi sana akambusu tena mama yake.
~~~~~~~~~~~~~~~
Alimlisha
Liv vizuri. Akampeleka bafuni kuoga ili alale. Wakati yupo bafuni, Geb akaingia
na kiti. Kaa hapa wakati mimi namuogesha. Nanaaa akajikonyeza mwenyewe. Geb
alikuwa akimjali mno, mpaka akashangaa na kucheka nafsi mwake. Akaanza kumuimbia
Liv huku anaogeshwa na baba yake. Liv alikuwa akicheka mpaka Geb alikuwa
akicheka. Aliimba kitoto, ungependa kumsikiliza. Tamaa yakuishi maisha marefu
ili amuone binti yake akikua ikaanza kumwingia. Geb akamtoa bafuni, akamvalisha
na kumuweka kitandani. Wakaomba naye, wakamwambia alale.
Nanaa
akabaki akifikiria. “Unawaza nini?” Geb akavuta tena kiti karibu ya Nanaa. “Liv
atakuwa dada mrembo!” Wakacheka. “Ameanza kuongeza uzito. Angalau
kanatizamika.” “Ni Imani tu Geb. Siku tatu haziwezi zikaonyesha tofauti.”
“Kweli Nanaa! Ndivyo ulivyomkuta huyu mtoto hivi? Kwanza alikuwa hata hacheki.”
Nanaa akanyamaza.
“Unauwezo
wakuendelea kumfanya awe na furaha.” “Mambo yamebadilika Geb. Majukumu
yameniongezekea. Sio kama zamani nakuwa na uwezo wakuamua kwa haraka. Sasa hivi
inabidi kuwa makini zaidi ili nisiwaumize wanangu wote, zaidi Jimmy ambaye hana
kimbilio ila mimi.” “Sasa ni nini unafikiria?” Nanaa akawaza kidogo.
“Sasa
hivi nina biashara inayoweza kuniingizia vijipesa kidogo. Ninaweza kuweka
juhudi kwa hii miezi michache iliyobaki. Nikakusanya pesa zakunitosha mimi na
Jimmy kipindi cha uzazi, au kama sitakuwepo, basi dada Fifi na Jimmy. Kuishi na
dada Fifi kutanisaidia kufanya naye hiyo biashara nakumuweka karibu zaidi na
mimi pamoja na Jimmy. Kuliko eti leo niondoke kwenye maisha yake, nije
kutokezea siku yakujifungua! Nimwachie tu mtoto! Hatapata uzito kama nikiishi
naye pamoja. Akaweza kupata muda na mimi pamoja na Jimmy. Wakawa wanazungumza
kama hivi hata kabla hajazaliwa. Sijui unanielewa Geb?” Geb akabaki kimya.
“Moyo
wangu unatamani sana nije kuishi na nyinyi ili nipate muda na wanangu. Itakuwa
faida kwao lakini hasara kwa mdogo wao, Jimmy. Wao wanalo kimbilio, wewe.
Lakini sio Jimmy. Lazima kumfikiria ndio maana wakati ule nilipoona
mnanikatalia watoto wangu, nikaona ni heri nife naye tu huyu. Hapakuwa na
sababu yakuishi.” Geb akanyamaza.
~~~~~~~~~~~~~~~
Kama ni ahadi alishaziongea zote kwa Nanaa.
Kumfuta machozi, lakini akaishia kumuacha akilia. Kumpenda mpaka kifo. Lakini
alimuacha akijua ni mgonjwa na wala hakuonyesha kujali. Akakumbuka alipomfungia
nje pindi alipojifungua Liv. Tena akalazimishwa na mama yake amfungulie,
akaingia akiwa amelowa damu.
Alipomzalia
mtoto wa pili, akabakwa ndani ya nyumba yake. Akiwa anajua alimtoa hospitalini
akiwa bado mgonjwa. Daktari alimsisitizia lazima atumie dawa na arudi kumuona.
Geb alikumbuka vile alivyomuacha akilia huku amempigia magoti sakafuni
akimlilia asimuache, lakini aliondoka na kumuacha. Tena aliondoka huku
akimshutumu kwa uongo. Akakumbuka maneno makali sana aliyomwambia. Zaidi hataki
tena kuiona sura yake maishani. Akafunga misaada yote, na
kumuacha peke yake kwenye jumba alilofanyiwa unyama mbaya. Tena watu wote
waliokuwepo siku ile wakisikia na kujua anachofanyiwa bila hata kupewa pole na
yeyote yule kati yao. Kana kwamba walikuwa wakishangilia asulubishwe. Ameyataka
mwenyewe. Lipi amebakiza kwa Nanaa?
~~~~~~~~~~~~~~~
Nanaa
akajinyanyua taratibu. “Nashauri leo ulale hapo kitandani Geb. Jipumzishe
mgongo.” Geb akasimama. “Unakwenda wapi tena?” “Nataka nikatembee kidogo ndipo
nirudi kulala. Najihisi kuchoka viungo. Pia nataka nizungumze na dada Fifi.
Nataka kumtia moyo kwenye biashara yetu. Ni mwepesi sana kukata tamaa. Japo
sipo naye kikazi, basi angalau kumtia moyo na kumsaidia kimawazo. Sasa hivi
yupo peke yake. Anapika na kusambaza. Atakuwa anachoka na atakata tu tamaa.
Sasa nikimpigia simu hapa ndani, tukaanza kuzungumza, tutaamsha watoto wote.” Geb akatulia kidogo.
Nanaa
akavuta simu yake. “Nilikuwa nina wazo Nanaa.” Nanaa akamgeukia. “Yeye awe
anapika, halafu Jeri awasaidie kusambaza.” Nanaa akacheka kidogo. “Mbona
unacheka?” “Mawazo yako ni mazuri sana Geb. Na yote yanaonyesha kutoa suluhu
zuri sana, lakini huwa ni kwa muda mfupi sana. Nakushukuru sana. Lakini
hapana. Nimeamua kuanza kujiwekea msingi wa maisha yangu. Nijijenge kuanzia
chini. Ni kwa shida. Lakini naamini nitafika tu. Kama nisipojikaza sasa hivi
nikaanza kitu chakueleweka na chakudumu, nitampa shida Jimmy na historia ya
maisha yangu haitakaa ikabadilika. Itajirudia daima. Na sitakuwa na
wakumlaumu.” Nanaa akaendelea.
“Nimekuwa
nikiishi kwa kusaidiwa kana kwamba mimi ni mjinga, Geb!” “Usiseme hivyo Nanaa.”
“Kweli tena Geb. Niambie ni muda gani umepita tokea nimalize chuo? Nina sababu
gani ya msingi ambayo inanifanya niwe hivi nilivyo? Yaani hata kitanda changu
cha kulalia mimi mwenyewe, sina! Yaani hapa unavyoniona, hata nguo au chupi
ninazovaa ni zilezile ulizokuwa ukininunulia wewe. Sijawahi kutengeneza pesa
yakununua hata kijiko changu!” Nanaa akajicheka.
“Niambie
Geb, kama sio ulemavu wa akili ni nini? Sina tofauti yeyote na wewe au na watu
wengine kama dada yako. Kwa nini mimi niwe hivi na wengine wawe na maendeleo?
Hivi unajua wenzangu niliomaliza nao chuo walipo? Wengi wameolewa. Yaani wana waume
zao. Wametulia makwao na watoto wao. Japo sio matajiri, lakini maisha ya
familia yanaendelea. Niangalie mimi. Mpaka hivi sasa ndio nahangaika kuanza
maisha na nina watoto. Sina rafiki wala familia. Yaani ndio nahangaika na dada
Fifi, mtu niliyekutana naye hospitalini! Ndio amenipa mpaka mashuka
yakujifunika. Niambie ukweli Geb, kama mimi sina tatizo ni nini?” Nanaa
aliongea taratibu lakini kwa makini.
“Kama
ningekuwa nimetulia na nipo makini. Kuanzia kwenye mipango yangu, nina uhakika
wanangu wasingeteseka hivi. Nimeleta watoto duniani mimi kama mama nikiwa
sijajipanga na wala sijielewi nataka nini. Nimekuwa nikijiegemeza kwa watu na
kwenye mapenzi ambayo hayakuwahi kuwepo tokea mwanzo. Lakini nimekuwa kama
mjinga kufungia macho hata yale Mungu aliyokuwa akinitumia ishara kunishitua na
kunieleza sehemu ninazoegemea sio sahihi. Ni dhaifu sana. Lakini nimekuwa nikishupaza shingo. Lakini
sasa hivi ndio kama maisha na majanga yaliyonipata yamenifungua macho.” Geb kimya.
“Nimejiambia
kila siku Mungu atakaponijalia kuamka au kunitoa kitandani, lazima nijikumbushe
mimi ni nani. Nipo wapi! Na nani! Ninakwenda wapi! Najiambia mimi mwenyewe
Nanaa, ndio ninauwezo wakubadili maisha yangu. Sio mtu mwingine. Hata kama
Mungu anataka kunisaidia, hawezi mpaka mimi mwenyewe nitende kazi pamoja
naye. Sitatoka hapa nilipo Geb, kama sitabadilika. Hii misaada ambayo unanipa
leo, kesho ukikasirika unanipokonya au kuniacha, haitanipeleka kokote!
Nawatesa tu wanangu na mimi mwenyewe.” Kama aliyemwagiwa maji, Geb akatulia
kimya.
“Najua
natakiwa kutafuta msambazaji. Naelewa sana. Lakini bado biashara haijakuwa.
Lazima nilipe garama zote sasa hivi nikiwa mgonjwa na wanangu wakinihitaji kwa
kuwa Mungu alinipa nafasi nyingi sana, nikachezea. Inanilazimu kulipa garana
Geb. Nimekusudia sitarudi huko tena. Hata ikinilazimu mapumziko yangu yawe
kwenye daladala nikiwa natoka sehemu moja kwenda nyingine. Iwe kusambaza
maandazi au kuwaona wanangu. Nitafanya hivyo. Kwa kuwa nimeyataka mimi
mwenyewe. Ila najua haitakuwa kwa muda mrefu sana. Nitatoka hapa, na wanangu
watapumzika siku moja. Hata kama sasa hivi nitawapa lisaa limoja kila siku,
lakini namuomba Mungu azidi kuyaongeza hayo masaa. Biashara ikue, niongeze
wafanyakazi ili niweze kuwa na muda na watoto wangu.” Nanaa akaongeza.
“Kwa hiyo Geb, nakushukuru sana kwa kutaka kunisaidia. Lakini hapana. Ila naomba unisaidie kwa upande wa watoto tu. Nakusihi sana, niruhusu kuwa na wanangu pale nitakapoweza. Sitakusumbua uwalete au utume dereva. Nitawafuata popote walipo, kasoro nyumbani kwenu wewe na mama yako, hapo hapana ili nisizidi kuwakera. Kama siku nyingine utaniruhusu hata nilale nao kwangu, nitakushukuru sana. Ukitaka niwalee mimi, pia nitakushukuru mno. Ila tu, nitaomba unisaidie matumizi yao. Sitataka pesa yako hata shilingi. Hilo msiwe na wasiwasi nalo. Nitakuwa nikikuandikia mahitaji yao, au unaweza hata kumtuma Jeri awe analeta hivyo vitu nitakavyohitaji vya watoto ili kuhakikisha au muwe na amani na pesa yenu. Kwangu unakaribishwa muda na wakati wowote ule. Iwe mchana au usiku, njoo ili uje kuona wanao. Nakuachia wewe uamue Geb.” Nanaa akatoka. Usingizi wote ulimpaa Geb. Akabaki kimya pale chumbani na watoto wake akiwaza.
Maisha Baada Ya Kuruhusiwa Magesa Hospitalini.
Kesho
yake Magesa akaruhusiwa kutoka. Geb alipoenda kulipia, Nanaa akakusanya vitu
vyote akaviweka kwenye mifuko ila kwa kutenganisha. Vitu vya watoto wake,
akaviweka sehemu moja, na vyake akaviweka kwengine. Geb akarudi. “Upo tayari?”
Geb akauliza. “Naona nimewafungashia kila kitu chenu kipo tayari. Lakini naona
kama mimi mtaniacha. Bado dada Fifi ana kazi kidogo. Amesema atakuja baada ya
kama nusu saa. Nina mizigo mingi. Vyombo alivyokuwa akileta. Na jana alisahau
kuchukua. Siwezi kupanda navyo kwenye daladala. Ngoja nikusindikize na watoto
kwenye gari, nitarudi huku juu, kumsubiria. Nesi ameniambia hata nikitaka
kulala, naweza kujipumzisha tu.” Nanaa akamalizia kwa kucheka.
“Kwa
hiyo nitakuwa sawa tu. Twende nikusindikize kwenye gari. Nikusaidie kubeba
watoto.” “Twende wote niwapeleke.” Nanaa akatulia kidogo. “Unamaanisha na
watoto?” Nanaa akauliza akiwa hajamuelewa Geb. “Unafikiri nitafanyaje Nanaa?
Magesa ameruhusiwa akiwa bado anatakiwa aendelee na matibabu. Namuona ameshaanza
kukuzoea. Ukimshika wewe, anatulia kwa haraka. Siwezi tena kwenda kumuanzishia
maisha mengine huku ni mgonjwa. Umeona kwa siku chache tu jinsi Liv
alivyobadilika? Mtoto wangu amerudisha kicheko na anakula. Amerudi kuwa msafi,
angalau anatizamika. Acha mimi ndio nilipe hiyo garama, kwa kuwa nimeyataka mimi
mwenyewe. Twende tu. Nitakuachia watoto na nitasaidia kwa kadiri
nitakavyowezeshwa na Mungu.” Nanaa akajawa furaha isiyo kifani.
“Nakushukuru
sana Geb. Nakuahidi nitawalea watoto vizuri. Na kwangu utakuwa hujawapoteza
wanao. Muda na wakati wowote, wewe njoo tu kuwaona. Hata ukitaka kuzungumza nao
kwenye simu, piga muda na wakati wowote ule.” Geb hakujibu kitu katika lile.
“Ngoja
nianze kuweka mizigo kwenye gari. Halafu nitakuja kukuchukua wewe na watoto.
Ila Liv usimbembe. Nitakuja kumfunga kwenye gari yake, halafu nimsukume
mwenyewe. Usiwabebe hao.” “Sawa.” Nanaa alitamani kuruka ruka kwa furaha.
Lakini baada ya Geb kuondoka, akakumbuka chumba chake. Akakaa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Anawaweka
wapi wale watoto wa Geb, waliozoea kulala huku AC ikiwapuliza. Yeye anapepewa
na feni na wakati mwingine anaongeza nguvu yakujipepea na karatasi usiku joto
linapokuwa kali. Watoto waliozoea kulala kwa kujinafasi, tena kwenye vitanda
vyao! Wasiwasi ukamwingia.
~~~~~~~~~~~~~~~
Geb
akamkuta anatuma ujumbe. “Upo tayari?” Geb akamuuliza. “Nilikuwa namtumia
ujumbe dada Fifi, asije tena hapa. Ila anipangie pale ndani. Nimemwambia
nakwenda na watoto. Halafu nataka akaninunulie feni na kapeti ndogo. Nitandike
pale chini ili kama Magesa akitaka kutambaa, asipate shida. Halafu..” Nanaa
akaendelea kumueleza mipango mingi anayotaka kufanya. Geb alijua tu itamgarimu
pesa. Lakini kwa kuwa alishakataliwa kutoa msaada. Akaamua anyamaze.
Akatafuta
sehemu akakaa. Akabaki akimsikiliza. Nanaa alipoona hapati uungwaji mkono, akarudi
kwenye simu yake na kuendelea kutuma ujumbe huku wazi akionekana ameshapaniki.
Geb kimya. Akamaliza. “Nipo tayari. Tunaweza kwenda.” Geb akasimama. Kwa kuwa
alishaingiza vitu vyote kwenye gari, akambeba Magesa mkono wa kushoto, Liv
akawa anamsukuma kwenye kigari chake, mpaka kwenye gari.
Walipoingia
tu kwenye gari, Fifi akapiga simu. “Hivi wewe Nanaa unajua hali yetu ya kiuchumi lakini?” Nanaa kimya. Akatamani kupunguza sauti ya simu Geb
asisikie. “Nanaa!” “Nitakupa pesa
dada. Wewe tumia ulizo nazo.” “Tulizungumza nini jana juu ya kupanua biashara?
Jana tulipanga mambo mengi. Na yote ni mazuri. Ukasema tuache kutumia pesa kwa kujinunulia
vitu ambavyo havitatuingizia faida. Ukanitajia pesa uliyonayo benki. Tukaweka
mipango. Ukaniambia nikubali ile tenda kubwa ya jumamosi. Nimetoka sasa hivi
kuzungumza na mama yake yule bibi harusi. Nimemwambia kama tulivyozungumza. Kuwa tutaweza kuwalisha wote kwenye hiyo sherehe
yao. Leo asubuhi unataka kapeti, sijui feni na mambo mengine. Huo uwezo
tunautoa wapi, mdogo wangu?” Nanaa kimya.
“Tenda tushakubali. Tunatakiwa kuanza kununua vitu. Chupa zakuwekea
chai zinahitajika tano. Haya, tukakubaliana tununue yale mabakuli makubwa ya
chuma cha kuwaka yenye mifuniko yake ya kioo kwa ajili ya kuwekea vitafunio.
Ili tukiyapanga mbele ya watu yaonekane masafi na yavutie. Haya, tukasema na
miko mizuri yakupakulia. Wewe mwenyewe ukasema unataka ya chuma, ili iendane na
sinia. Seti za vikombe, sahani na vijiko. Tumepanga vizuri. Tumeandika.
Ukaniambia niwapigie, niwaambie tutawalisha kwenye kitchen party yao. Sasa mbona tena unageuka?” “Ninakuja na
watoto dada.” Nanaa akaongea kwa upole.
“Wewe kwa sasa huna uwezo wa kulea hao watoto Nanaa! Nimekutana na
wanao. Mazingira mliozalia hao watoto na maisha wanayoishi sasa hivi,
hawatapaweza hapa uswahilini. Kuna mbu na nzi kila wakati! Joto kila wakati!
Hamna nafuu mchana wala usiku hapa. Utakuja kuwaua wanao Nanaa! Hao watoto
hawatapaweza hapa. Hata nikisema nikutolee mizigo yote hapo chumbani kwako,
bado hapatoshi.” Geb aliendelea kukanyaga mafuta,
kuitafuta Kawe.
“Sasa nitafanyaje dada? Nataka kuwa na wanangu.” Tayari Nanaa alishaanza kulia. “Wewe mwenyewe ulinifundisha kuwa kila jambo lina wakati
wake, Nanaa. Huu sio wakati wa kuchukua hao watoto. Ungekuwa umewazaa huku kama
wale wangu, hapo sawa. Au kama huyo Jimmy, hapo sawa. Lakini sio kuwahamisha
kutoka kwao, ukawaleta hapa! Kwanza unakumbuka tunakopikia lakini? Tunapikia
nje. Moshi wote unaingia ndani ya vyumba. Wewe mwenyewe mwenzangu na mimi
ulikuwa unalalamika na kuniambia niwe nahamisha jiko kila pande ya huku uwani,
ili uweze kulala ndani. Sasa ushafikiria hao wanao lakini?” Kimya. Nanaa akabaki akifuta machozi.
“Unataka kuleta balaa bure! Mrudi tena hospitalini. Wewe jiachie tu.
Omba kwenda kutembelea wanao. Kila unapoweza, nenda. Mimi nitakuwa nakusaidia
kazi za hapa ndani, wewe uwe unaenda kutembelea wanao. Hata kama utakuwa
unapika vitu vigumu usiku, ili asubuhi uwe unaenda kwa wanao, pia ni sawa. Mimi
nitahangaika na kusambaza. Lakini sio kuwaleta hapa hao watoto. Jiachie tu
mdogo wangu. Mambo yetu yakiwa safi, tunawafukuza wale wapangaji mle ndani,
tunahamia kwenye nyumba kubwa. Hapo ndipo tunaenda kuwafuata watoto wa
uzunguni.” Nanaa akacheka kidogo.
“Sikutanii Nanaa. Nakwambia ukweli. Umenielewa mdogo wangu?” Nanaa kimya. “Basi ulivyombishi wewe!” “Nafikiria dada.” “Unachofikiria nini sasa?” Kimya. “Wewe Nanaa?” “Nataka kutumia muda niliobakiza na wanangu dada. Magesa
bado mgonjwa.” “Ndio garama watakayolipa hao watoto, Nanaa. Wanasema,
‘tembo wakigombana, manyasi ndio
yanaumia’. Sasa garama yakutokuelewana kwenu nyinyi wazazi, ndio wanalipa watoto
wenu sasa hivi. Lazima wataumia tu. Hamuwezi kuepuka hilo. Watailipa hiyo
garama kwa uzima na ugonjwa. Maumivu yake watayasikia mchana na usiku. Mbaya
huyo mkubwa ambaye mlimlea pamoja. Anauelewa mkubwa sana Liv. Anajua kabisa
kila kinachoendelea. Heri kaka yake. Yeye ataweza kuuguzwa na yeyote na akawa
sawa tu.” Nanaa akazidi kulia, Fifi
akakata simu.
Akasikia
gari linaegeshwa pembeni. “Naomba usilie Nanaa. Sisi tunayemtaka ni wewe. Sitajali
mazingira utakayotaka kuwaweka watoto. Ilimradi wewe ukiamua wawepo hapo,
watakuwepo tu.” “Ni kweli pale
hapatawafaa watoto Geb. Nenda nao tu. Mimi nirudishe kwangu. Nikajipange,
halafu nikiweka mambo sawa, ndipo nitakutafuta tena.” “Basi usilie. Naamini huo ndio uamuzi unaokupa amani.
Tulia. Sitaki Liv aamke, akukute na hali hiyo. Itakuwa ngumu zaidi kumuacha.
Nimeshawatesa wanangu vyakutosha. Nimekubali kulipa garama yeyote ile. Naomba
Mungu anisaidie, kuwasaidia watoto wangu. Naamini watakuwa sawa tu.” Nanaa
akajaribu kutulia, Geb akatoa gari.
Uswazi.
Alimuelekeza
Geb, mpaka wakafika. Kweli nyumba ya mbele ilionekana ni kubwa tu, na nzuri ya kawaida.
“Unaweza kuegesha gari hapo nje tu. Nitamuomba dada Fifi aje anisaidie kushusha
mizigo.” “Tunaruhusiwa kuingia ndani?” Geb akauliza kiungwana. “Kabisa Geb. Karibu.
Nilifikiri unataka mrudi nyumbani ili mkapumzike.” “Hamna neno. Tutakaa
kidogo.” “Ila kuna joto!” Nanaa akamtahadharisha. “Hamna shida.” Geb akafungua
mlango, Fifi naye akatoka.
Wakasaidiana
kushusha mizigo, wakaingia ndani. Fifi alisafisha vizuri chumba cha Nanaa. Ni
kweli kulikuwa na joto, na nzi nje. Ndani Fifi alijitahidi kutoa nzi. Pakawa
hamna nzi wengi. Pasafi ila padogo. Geb akamuacha Liv kwenye kigari chake akiwa
amelala, akamuweka Magesa kitandani kwa mama yake. Yeye akakaa kwenye kochi
refu la mbao lililokuwepo hapo hapo chumbani. Akatulia. Nanaa akababaika
vyakutosha. Kilikuwa chumba kimoja, kilichojazwa mizigo yake yote. Ila kulikuwa
na choo na bafu humo humo ndani. Sakafu
ilikuwa yakawaida tu. Haikuwekwa hata marumaru.
Watoto
wamelala, Geb amekaa kwenye kochi. Hamna tv, wala radio. “Kuna feni. Sijui
niwashe au watoto watakohoa?” “Labda usiwaelekezee.” Geb akajibu taratibu.
Nanaa akawasha feni, akaelekeza upande mwingine. Akabaki akifikiria. “Mbona
hukai?” Geb akamuuliza. “Nataka kupika kwanza. Najua njaa zitakuwa zikiwauma.”
Kimya. “Liv akiamka atataka kula. Ngoja niende nikawashe mkaa. Nitarudi.
Unataka soda au maji?” “Mimi nipo tu sawa. Asante.” Geb akajibu.
Mtihani
ukawa pakuwashia moto. Akajua moshi wote na harufu ya mafuta ya taa vitaingia
ndani alipo Geb na wanae. Fifi akabaki akimtizama. Akahamisha jiko kulia na
kushoto bila kuwasha. “Nahofia moshi utaingia ndani!” Nanaa akajiongelesha. “Si
ndicho nilichokuwa nikikwambia mimi? Mwanaume wa watu hajabisha. Yupo ndani na
wanae. Jasho linakutoka mwenyewe!” “Usiseme hivyo bwana. Nisaidie dada.” “Mbona
hamna shida. Wewe nipishe hapo nifanye vitu vyangu. Dakika 20 tu chakula kipo
mezani.” “Sasa utaniamshia wanangu kwa harufu ya mafuta ya taa.” “Wala si
kuwaamsha tu. Wataondoka hapa wananuka moshi kama wachoma mishikaki.” Nanaa
akacheka.
“Wala
hunisaidii wewe!” “Tatizo lako wewe Nanaa mbishi na huyo bwana hapo
ndani mjuaji. Basi wanaoteseka watoto.” “Sasa mimi ubishi wangu ni upi?”
Fifi akamsogelea Nanaa. “Kinachowashinda kuzungumza mambo mkamaliza na mwenzio
ni nini? Jumba limewashinda, mmelifunga, mmekuja kujibana hapa uswahilini
sababu ya wote hamtaki kushindwa. Wewe mbishi na mwenzio mjuaji. Wote
mmeshika kwenye mpini, watoto wenu kwenye makali!” “Acha kusema hivyo dada!”
Nanaa alizungumza kwa sauti ya chini.
“Nanaa
mdogo wangu. Maisha ni karata. Ukizicheza vibaya tu, imekula kwako. Nilikwambia
tokea mwanzo. Kama Mungu angenipa mimi hata dakika kumi tu na familia yangu,
ningezitumia vizuri sana. Fifi huyu unayemuona hapa, nisingekuwa hivi. Hakuna
garama. Narudia na nilikwambia Nanaa. Hakuna garama itakayonishinda kulipa ili
niwe na familia yangu. Hapa najiuliza hata nikipata mamilioni ya pesa, yana
raha gani? Sina mtoto sina mume. Hata nikivaa dhahabu nikawa na magari tisini, havina raha Nanaa. Maisha
ni watu.” Fifi alitoa machozi.
“Hujakaa
upande wangu ndio maana hujajua ninachoongelea. Niliiacha hii nyumba nikawa
nashinda nazurula kwenye majumba ya watu sababu ya upweke. Nanaa, mimi nilikuwa
naitwa naringa! Huwezi kunikuta napoteza muda na mtu wakati mume na watoto
wangu wapo hai! Kwanza utanikuta wapi na saa ngapi? Sina ujinga na mtu ndio
maana watu na wenyewe walikuwa hawanitaki kipindi nilipobaki peke yangu.” Fifi
akaendelea.
“Na
sio kwamba nilikuwa na ndoa nzuri ya ajabu! Lakini nilikuwa na mwanaume
aliyekuwa akijua kujirudi. Na hivi alishanizalisha, na tumetoka mbali, basi
maisha yalikuwa yakiendelea. Sikuolewa na malaika, lakini tulipendana sana na
Manase. Upendo ulinifunza kuvumilia, kutohesabu na kutojitafutia mambo yangu
mwenyewe. Ndio andiko alilokuwa akilipenda sana Manase. Na hakuacha
kunikumbusha. Hasa yeye akikosa.” Nanaa akacheka huku akilia.
“Usicheke.
Alikuwa akiniudhi, lakini mwenyewe alikuwa ananiambia ni neno la Mungu wala si
lake. Akawa ananiambia nikishaona kunatabia yakuhesabu hesabu kila wakati, ujue
hapo hamna upendo. Nyinyi bado wadogo sana Nanaa. Hivyo hivyo watoto wenu bado
ni wadogo. Wanawahitaji sana. Wewe unaweza kuolewa hata na hilo tumbo lako.” “Dada wewe!” Nanaa
akamfinya.
“Hujaona
wanavyohangaika huko maofisini na wewe? Kila tunakopeleka vitafunwa wanakuomba
wawe baba wa mtoto wako.” “Wale
wana tamaa tu.” “Lakini ndio ujue bado unalipa.
Na mwenzio hivyo hivyo. Wote mnaweza kuendelea na maisha yenu, mkapata wenza
mkawa na furaha tu. Lakini Nanaa, jua wazi, hakuna atakayeweza kulea watoto
wako isipokuwa wewe mwenyewe. Hata baba yao hataweza. Watoto wanaolelewa na
baba peke yao, hawafanani na watoto waliolelewa na mama peke yake. Wapo
tofauti. Na hiyo imeanza tokea mwanzo wa kuumbwa mwanadamu. Uchungu wa mtoto ni
mama. Na haviishi siku yakuzaa tu. Ni mzigo wako huo. Sasa akili kichwani mdogo
wangu. Ujue umama ni garama. Tena garama yakukana nafsi. Hatima ya wanao iko kwako.
Maneno na tabia yako yakuaga aga eti unaenda kufa, ujue utakufa kweli na
uache wanao wanateseka. Shauri yako.” Fifi akataka kuondoka.
“Sasa
itakuaje nikija kujifungua? Nataka tuwe wote hapa ili nikijifungua uweze kuwa karibu
na Jimmy.” “Unaanza kuishi miezi mitatu baadaye wakati hata leo hujamaliza! Si
wazimu huo? Wewe ulizungumza na Mungu akakwambia mimi nitakuwepo hapa duniani
baada ya miezi mitatu ijayo?” “Usiseme hivyo dada!” “Niambie Nanaa. Kesho yangu
wewe unaijua? Nikianguka kesho nikafa? Mimi nilijua kama Manase atakufa siku
ile wakati tulikuwa tukizungumza muda mfupi kabla hajapata ajali!? Unajua
mipango niliyokuwa nayo na Manase juu yetu muda mfupi kabla hajafa? Hakuna
anayejua linalotokea hata baada ya dakika moja kuanzia sasa. Sasa eti wewe
unataka utese watoto wako sasa hivi, kwa ajili ya mtoto unayemtegemea miezi
mitatu ijayo! Huo sio wazimu?” Nanaa akanyamaza.
“Yaani
hawa ulionao sasa hivi ushindwe kuwalea, halafu ujidai unamsubiria Jimmy ambaye
hata hujamshika mkononi! Akizaliwa amekufa?” “Usimtamkie mwanangu mabaya bwana!”
“Mimi nataka kukufungua akili, Nanaa. Wewe bado mdogo. Hujayajua maisha mdogo
wangu. Unadandia treni kwa mbele. Utakufa siku si zako. Haya mama, mimi njaa
inauma. Changamsha mkono huo. Wanao wanaamka sasa hivi. Bwana kakaa ndani.
Haya. Ivisha tule.” “Na huo moshi sasa?” Nanaa akauliza.
“Ndio
watajijua. Si mama yao kaanza maisha! Tena kayaanza maisha kwa kasi zote.
Changamsha mkono sasa.” Nanaa akanyamaza. Alijuta kumsimulia Fifi mkasa mzima
wa Geb. Jana yake mara baada ya kutoka kuzungumza na Geb, akatoka kwenda kumpigia
simu Fifi, nakumueleza kila kitu, akitaka Fifi awe upande wake. Lakini
ameshangaa Fifi amembadilikia! Akaenda kukaa pembeni anamwangalia Nanaa. Baraza
lenyewe lilikuwa na jua.
“Watu
wanakimbia shida, wengine mnazikimbilia!” Fifi aliendelea kuongea kwa mafumbo. “Ona
unavyotokwa jasho hapo juani. Uzuri nimejaza gari yangu mafuta. Ukiangaka tu
hapo, nakutia kwenye gari, nakupeleka hospitalini. Wakakuchome chome sindano,
halafu nakurudisha hapa.” Nanaa akacheka. “Si mbishi wewe! Basi endelea hapo
hapo.” “Njoo unisaidie bwana dada! Kawashe mkaa hapo nje ya geti, halafu uje
upikie ndani.” “Sawa. Mimi sikujaliwa ubishi kama wewe. Ila kumbuka hapo nje
kuna gari ya baba watoto wako. Na ninawasha moto kwa kutumia mafuta ya taa.
Sasa likiwaka moto, ujue chakumueleza!” “Acha kuniogopesha bwana dada! Wewe nenda
kawashie huo moto mbali na hilo gari la watu.” “Sawa. Ila ujue
nilikutahadharisha.” Fifi akatoka na jiko lenye mkaa, mafuta ya taa na
kiberiti.
~~~~~~~~~~~~~~~
Nanaa akarudi ndani. Akakuta wanae wamelala, lakini
wamelowa jasho. Geb alikuwa amepandisha miguu juu ya lile kochi, akiwa bado
amevaa viatu vyake. Amejilaza na kufunga macho. Nanaa akamuhurumia. Akainama na
kumfungua viatu. Akaanza kumtoa taratibu. Geb akafungua macho akabaki
akimtizama. “Pole. Nimekuamsha?” “Hapana. Nilikuwa nimejipumzisha tu. Vipi
wewe?” “Nipo sawa tu. Nimekutoa viatu ili kupunguza joto. Naona unatokwa na
jasho kweli.” “Asante.” Geb akabaki akimwangalia. Nanaa akainama. Geb akamvuta
mkono, akaushika.
“Hongera kwa hatua kubwa. Naona umepambana mpaka
umepata kwako.” Nanaa akacheka. Akakaa vizuri pale sakafuni wakati Geb
amejilaza kwenye kochi. “Mbona unajicheka tena? Kweli mimi nakupongeza.” “Asante
Geb. Lakini kila kitu unachokiona hapa ni cha dada Fifi.” “Taratibu. Kila kitu
utanunua kutokana na uhitaji. Kama hivi unaona wageni wako tunatokwa jasho,
ukipata pesa, unaongeza feni jingine. Taratibu. Huwezi kuwa na kila kitu kwa
wakati mmoja.” Nanaa hakuamini kama yale maneno yanatoka kwa Geb. Bado alikuwa
amemshika mkono akimwangalia.
“Asante kwa kunitia moyo. Naona na wageni wangu
mmekuwa wavumilivu!” Wakacheka na kuwageukia watoto wao. “Unaratiba gani
jioni?” “Sina. Mkiondoka, nitakuwepo tu mpaka usiku ndio nianze kuandaa vitu
vyakupika.” “Unakumbuka lakini kunywa dawa zako?” “Nakunywa usubuhi na usiku
wakati nalala.” Geb akamvuta mkono zaidi. Nanaa akacheka.
“Baadaye
jua likipungua, tunaweza kutoka kidogo na watoto?” “Unataka twende wapi?” Nanaa
akauliza. “Tukatembee kidogo. Tumekuwa kwenye mazingira ya hospitalini kwa muda
mrefu. Kama utaona sawa, tuwapeleke watoto sehemu wacheze kidogo. Hasa Liv.
Hajapata muda wakucheza tokea uondoke. Amekuwa ndani tu. Hata ukimpeleka
mahali, alikuwa hachezi. Au unafikiri utakuwa na kazi nyingi, hutaweza?” Geb
hakutaka kulazimishia.
“Ningefurahi
kuwa nao, Geb. Asante.” “Basi baada ya kula. Wakiamka, twendeni.” Nanaa
akacheka kwa furaha. Wakabaki wamekaa kimya. Nanaa akainama kama anayefikiria.
“Umekata nywele, umependeza.” Nanaa akacheka. “Kweli!?” “Mmmh!” Geb akamshika
kichwani. “Alinikata dada Fifi, hapo nje!” “Alikukata vizuri.” Nanaa akacheka
kwa aibu kidogo huku akijishika shika. “Ngoja nikamsaidie dada Fifi.” Nanaa
akaona atoke tu pale.
Alipotoka
tu, akamsikia Magesa anaongea kitandani. Akarudi. “Magesa!” Mtoto alikuwa
amelowa jasho kama amemwagiwa maji hapo kitandani. “Vipi baba? Pole na joto.” Akamtoa
pale kitandani akampakata. “Amelowa jasho! Kama amenyeshewa mvua! Pole.” Nanaa
akaendelea kuongea, Geb akiwa kimya pale kochini. Akamtoa nguo zote akambakisha
na diaper tu. “Njaa inauma?” Nanaa akamuuliza mwanae. “Ule kwanza, ndio uoge.”
Nanaa akaendelea kuzungumza na mwanae.
Mama
yake akamiminia uji kwenye bakuli, akaanza kunywa. “Nilitaka kumuanzisha
nyonyo, lakini naona sitaweza.” Geb akacheka. “Huyo hana utani na chakula.
Usiposema wewe basi, ujue mwenzio ataendelea kula tu.” Wote wakacheka. Magesa
alikuwa akiendelea kula kana kwamba yupo kijiko cha kwanza, wakati ndio amemaliza
bakuli la uji. Cheko ilimjaa. Alionekana ni mtoto ambae hasumbui. Ilimradi
ashibe. “Naona homa imemuisha kabisa. Amekula vizuri.” Geb akasifia. “Namuonea
huruma jinsi anavyotokwa jasho! Halafu naogopa kumuelekezea feni asije
kukohoa.” Geb kimya.
“Huyo
dada hapo mpaka umtoe. Atalala siku nzima. Na hivi alishiba vizuri kabla
hajalala, hataamka.” Nanaa akacheka. “Liv kwa kupenda kulala! Kama wewe Geb.”
“Naona mwenzangu amezidi. Huyo hata umuweke sakafuni, atalala tu. Hapo alipo
hana habari ya alipo. Mpaka aamke ndio utamuona anahangaika. Kama ni njaa au
kwenda chooni. Lakini sio huo muda wake hapo.” Baba yake akasimama, nakumfuta
jasho. “Naona nimtoe tu hiyo nguo.” Geb akaanza kumtoa. “Mgeuzie na feni
kidogo. Nzi wanamsumbua.” Nanaa akaongeza. Geb hakuchangia.
~~~~~~~~~~~~~~~
Jioni
Geb akawatoa. Akawapeleka sehemu ambayo alijua watoto wake wote watafurahia.
Nanaa hakuwahi kumuona Geb wa namna hii. Alijawa kicheko. Akawa anacheza na
wanae kwa sauti ya juu kabisa. Walikuwa na wakati mzuri sana. Vilijaa vicheko
visivyoisha. Liv ndio alikuwa akicheka mpaka anaanguka chini. Geb alikuwa
akimkimbiza kulia na kushoto, ilimradi tu mtoto wake acheke na kupata wakati
mzuri.
“Naona
Magesa wangu na yeye anaona wivu. Amebaki anaruka ruka tu hapo kwenye gari
yake.” “Ndio akazane kutembea. Eti Magesa?” Geb akamtoa kwenye gari yake
akaanza kumkimbiza Liv huku amembeba Magesa. Magesa alikuwa akicheka kwa sauti
mpaka watu wengine walikuwa wakiwaangalia wao, nakucheka. Kila Geb alipomfikia
Liv, alitumia mkono wa Magesa kumshika. Wote wawili walikuwa wakicheka sana.
Mshikwaji na mshikaji. Magesa na Liv. Mama yao na yeye alikuwa akicheka kama
Geb.
Wakapata
muda wakula pamoja. Walikuwa wamebeba vyakula vya watoto wao. Nanaa akaagiza
samaki wakuchoma na chips. Akataka aletewe kachumbari yenye limao jingi. Geb
yeye akaagiza samaki wa kuchoma kama Nanaa. Akataka tango zima. Lisikatwe.
Nyanya kubwa moja na ugali. Nanaa akacheka. “Hujabadilika tu?” Akamuuliza.
“Nimebadilika mno. Imenibidi kubadilika kwa nguvu. Lasivyo ningekufa kwa njaa.
Hapakuwa na wakumringia tena. Mama alikuwa busy na watoto. Mpaka aje anifikirie
mimi, ilikuwa labda baada ya siku mbili au tatu. Hapo watoto wananiangalia
mimi. Sikuwa na ujanja ila kula kilichopo.” “Pole Geb.” Geb akajicheka na
kunyamaza.
Wakaendelea
kuwalisha watoto wao wakati wanasubiria chakula chao. Geb alikuwa akimlisha
Magesa mpenda kula, Nanaa akamlisha Liv huku wanaongea na kucheka. Chakula chao
kikaletwa. Nanaa akaanza kula. Akamuona anajikatia nyanya na tango, akaanza
kula bila shida. Hakulalamikia ugali wala samaki. Kweli Geb alibadilika. Akala
karibia kumaliza ugali wote. Tango na nyanya vikamwishia. “Nimwite akuongezee?”
“Hapana. Inatosha. Nimeshiba.” Akakusanya sahani zake, akatulia. Alikuwa akila
na kisu na uma, kwa hiyo hakuhitaji kunawa.
Muhudumu
alikuja na bili yao. Nanaa akaiwahi. “Acha mimi nitalipa.” Geb akamuwahi.
“Ngoja tu mimi nilipe.” Nanaa akaendelea kusoma huku ananawa. Muhudumu
akaondoka na vyombo, akisema atarudi kuchukua pesa. “Nanaa! Mimi nitalipa.”
“Acha tu mimi nitalipa.” Nanaa akakazania. “Kwani unataka kushindana na mimi?”
Nanaa akashituka kidogo. “Hapana Geb! Nataka kukusaidia. Umekuwa ukinilipia
mara kwa mara.” “Hayo ni mashindano.” “Hapana. Usinielewe vibaya.” “Mimi ndiye
niliyekuomba tutoke. Haikuwa kwenye ratiba yako wala bajeti yako. Unaposema
nimekuwa nikilipa mara kwa mara, ni kwamba unahesabu. Mimi na wewe tulipofika
hatuwezi kulipana tena. Si kwa wema wala kwa mabaya. Hatutaweza hata kidogo. Hatutafanikiwa.
Hatujengi, tutazidi kubomoa na kuumiza watoto. Niulize mimi, nimejaribu. Najua
matokeo ya unachotaka kufanya, Nanaa. Ni maumivu matupu.” Geb aliongea kwa
utulivu.
Nanaa
akaweka ile bili chini, akamsogezea karibu. “Sio katika hili tu Nanaa. Katika
kila kitu. Naomba kuanzia sasa na kuendelea fanya maamuzi yako ukifikiria
watoto zaidi. Mimi nipo radhi uniadhibu kadiri upendavyo. Lakini sio watoto.”
“Sikuadhibu Geb.” “Unaniadhibu Nanaa. Unaniadhibu kwa mabaya niliyokutendea
tokea mwanzo nakufahamu, mpaka sasa. Jana uliniambia. Lakini najua ninastahili
hayo yote. Lakini Nanaa, nakuomba ufikirie watoto wetu. Tafadhali sana.” Nanaa
akanyamaza.
Muhudumu
akaja, Geb akalipa. “Turudi nyumbani ukanywe dawa, upumzike.” Hawakuwa mbali na
nyumbani kwa Fifi. Walienda Kawe Club. “Nikitoka kusambaza mzigo wa kesho,
nitakuja kukuona na watoto. Ni sawa?” Nanaa akamuuliza Geb wakati wapo njiani.
Safari hii akasema ‘kukuona na watoto’. Na yeye Geb akasikia ametajwa. Geb
akavuta pumzi na kuzishusha taratibu. Akanyamaza kama anayefikiria.
“Nitajitahidi
kuwahi kabla watoto hawajaamka. Halafu nitakaa nao mpaka hata jioni. Ndio
nitaondoka. Unaweza hata kwenda kazini ukaniachia kwa siku nzima.” “Nikichelewa
kurudi je? Maana sijakwenda kazini zaidi ya siku 3.” “Hamna shida. Wewe kuwa
huru tu. Nitakusubiri mpaka urudi Geb. Kama kuna vitu vyakupika, naweza kupika
nikiwa kwako, baada ya watoto kulala. Kisha nikarudi navyo nyumbani tayari kwa kesho. Usiwe na
wasiwasi.” Geb akamtizama.
“Hiyo
‘usiwe na wasiwasi’ unamaanisha au unaongea tu kama sentensi nyingine yeyote.”
“Namaanisha Geb.” “Basi ujue nina wasiwasi Nanaa. Nina wasiwasi wa afya yako.
Ambayo niliipuuza sababu ya hasira. Nina wasiwasi sijui itakuaje kabla na baada
ya kujifungua kwako. Madhara yote hayo najiona mimi ndio nilikusababishia.”
“Hapana Geb! Usifikirie hivyo.” “Niambie kwa nini Nanaa. Kwa nini? Mimi ndiye
niliyemuomba daktari akuruhusu urudi nyumbani. Nikapewa masharti ya jinsi
yakuangalia hiyo presha yako isipande tena na dawa. Kesho yake nikakuacha. Leo
daktari ananiambia madhara yakutokufuata masharti na kutokutumia zile dawa,
kumepanua moyo wako. Wewe mwenyewe una wasiwasi hudhani kama utaishi. Niambie
Nanaa, naachaje kuwa na wasiwasi? Hata kama nina roho mbaya ya namna gani,
nawezaje kwenda kulala, nakukuacha na hali hiyo?” Nanaa hakutegemea kama ndicho
anachojisikia Geb.
“Halafu
kwa vile nilivyokutenda vibaya, watoto wale wale ulikuwa ukiwalilia, unapata
nafasi yakuwa nao, unashindwa! Upo radhi kuacha mtoto mgonjwa, ili tu kuwa
mbali na mimi.” Nanaa akashituka mpaka akamgeukia Geb. “Sio kweli Geb!” “Sasa
ni nini? Mtoto huyo huyo uliyekubali kutoa maisha yako ili azaliwe, leo ni
mgonjwa, haujali, unamuacha akalale bila wewe! Kweli nimekuudhi Nanaa na
umenichukia mimi na watoto wangu.” “Hapana Geb. Nahisi nikuchanganyikiwa tu.
Naona mambo yamekuwa mengi na yote yananiangalia mimi.” “Kwa hiyo hivyo
unavyofanya ndio njia pekee yakutatua hayo mambo mengi?” Nanaa akageukia
dirishani. Akanyamaza.
Wakafika
mpaka nyumbani kwa Fifi. Wakabaki wametulia ndani ya gari. “Geb!” Nanaa akaita.
Geb akamwangalia. “Naomba nishauri kitu.” Moyo wa Geb ukapasuka. “Nataka
kumuomba dada Fifi kama tunaweza kugawana vitu vya kupika. Ili hata nikiondoka
na nyinyi, niwe napika huko huko. Asubuhi nakutana naye mahali. Tunagawa hizo
oda, na kuwapelekea wateja. Unafikiri ni wazo zuri?” Geb akavuta pumzi kama
amepata aghueni. “Hata kama tutakuwa tunabadilishana naye, ili asichoke.
Unafikiri ni sawa? Halafu nimpe yeye nafasi ya kwanza yakuchagua ni nini
anataka kutengeneza.” Nanaa akaendelea.
“Litakuwa
wazo zuri sana. Utakuwa ukiendelea kujiingizia pesa na watoto hawataendelea
kuteseka.” “Ila siku kama ya jumamosi ambayo tunakuwa na tenda kubwa kama kitchen
party, itabidi kulala kwangu. Kwa kuwa tunakuwa tunachelewa kutoka na ninakuwa
nimechoka sana.” Nana akaanza tena. “Naomba tufanyie kazi wazo la kwanza,
kwanza. Tafadhali Nanaa.” “Sawa. Basi kesho nitakuja na jibu lakueleweka. Au
nikizungumza naye, kama bado itakuwa nimapema, nitakutumia ujumbe. Ni sawa?” “Si
sawa.” Geb akajibu kwa haraka kama aliyekuwa akisubiri aulizwe. Nanaa
akashangaa.
“Si
umesema nikazungumze na dada Fifi!?” Nanaa akauliza kama asiyeelewa tena.
“Ndiyo. Na sisi tunakusubiri hapa.” “Geb!” Nanaa akashangaa. “Au ulikuwa
humaanishi?” “Namaanisha. Lakini nahitaji muda wakujiandaa. Nijue nabeba nini
na nini naacha!” “Utahitaji kujiandaa usiku kucha?” Nanaa akanyamaza.
“Sikuharakishi. Ila kama utataka usiku kucha, basi tuingie tukalale mpaka
kesho.” Nanaa hakuamini. “Kwamba na wewe ulale kwenye kile chumba!?” “Si
niliyataka mwenyewe? Ndio garama yakulipa hiyo. Twende.” “Hapana Geb. Sio sawa
kwa watoto.” “Kwa hiyo ni sawa kwa Liv kuamka asubuhi aanze kukulilia? Na ni
sawa kumuacha mtoto mgonjwa?” Nanaa akaona kila kitu kinamgeukia yeye.
“Basi
ngoja nikazungumze naye, nakuja.” “Sawa.” Wakati anashuka, Liv aliyekuwa
akisinzia huku anaangalia cartoons zake akashituka sana. “Mama beba!” “Nakuja
Liv. Nisubiri.” Liv akataka kutoka kwenye kiti huku analia. “Beba mama. Beba!” “Nisubiri Liv. Nakuja sasa hivi, sikudanganyi.” Liv
akazidi kulia. “Hawezi kukubali. Ngoja nimtoe hapo kwenye kiti chake. Atembee
mwenyewe, umshike mkono, uende naye tu. Usimbembe.” Geb akatoa wazo. “Haya
nyamaza mama. Nyamaza twende wote.” Liv akaendelea kulia mpaka akatolewa kwenye
kile kiti, akaenda na mama yake ndani.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Umerudi
nao tena? Hawakuachii hao! Hata ushupaze shingo vipi. Unao hao.” Nanaa
akacheka. Fifi alimpokea na maneno. “Njoo Liv mwanangu. Njoo kwa mama mkubwa.”
Liv akacheka huku anajificha kwa mama yake kama kawaida yake. Nanaa akakaa na
kumpakata. “Sasa inanibidi niende dada yangu. Naomba usijisikie vibaya.” “Mbona
mimi nakuelewa Nanaa. Tena mimi ndio ningekuwa wewe, hata nisingechelewa.”
“Lakini mimi sio kwamba narudiana na Geb. Hapana. Narudi kwa ajili ya wanangu
tu. Tushaharibu sana. Ni ngumu kuja kuaminiana na kuishi tena kama wapenzi.
Kama ni ahadi, tushapena zote tumeshamaliza mimi na Geb. Hatuna jipya. Heri tulee
tu watoto.” “Watu wanakosa na watu wanamapungufu yao Nanaa. Hutakaa ukapata
mwanaume mkamilifu. Wanatofautiana vijimambo tu. Huyu atapungua katika hili na
yule lile.” “Mmmh!” Nanaa akaguna.
“Usigune
Nanaa. Huyu bwana anakupenda mdogo wangu. Kitendo cha kuja kujilaza hapa kwenye
joto na nzi, eti ili awe na wewe, wakati ameacha jumba la maana! Sio kitu
kidogo.” “Hakuwa hapa kwa ajili yangu dada, ni kwa kuwa wanae wananililia.” “Naona
wewe umeamua kufanya maisha kuwa tu magumu. Na sijui shida yako ni nini!” Fifi
alisikitika.
“Mimi
nawajua wanaume dada. Nishadanganywa vyakutosha. Achana na hayo mambo. Naomba
tuzungumzie biashara yetu.” “Unahangaika kulisha wanaume za watu wakati wa
kwako hata hujamshibisha! Tulia Nanaa wewe.” “Nataka pesa dada. Nimeshazungumza
naye, hana neno kwa sisi kuendelea na biashara. Tujipange tu. Leo unaweza
kupika hiki, na mimi nikapika kile. Tunakutana mjini, asubuhi na mapema.
Tunawatengenezea wateja wetu oda zao. Au unasemaje?” “Wazo zuri. Lakini naomba
tuliza mawazo Nanaa. Hizi pesa huwa hazitoshi.” Fifi akasisitiza.
“Sasa
ulitaka niache kabisa! Nitaishije dada yangu? Halafu ikitokea nakuachia Jimmy,
mtafanyaje wakati tutakuwa tumepoteza wateja wote?” “Kwanza ujue hii biashara
ni yako Nanaa. Mimi sasa hivi ukiniambia tuache, naacha nahamia kwenye miradi
yangu ya zamani.” “Dada!” Nanaa akashangaa. “Kweli tena Nanaa. Mimi nakupika
wapi na wapi!?” “Sasa utafanya nini?” “Nilikwambia tulikuwa tunafanya biashara
ya kuku. Niliacha sababu ya kuomboleza.” Wote wakacheka.
“Dada
Fifi wewe! Yaani mimi siku ile unajiliza pale hospitalini nikajua umefiwa jana
yake au hata majuma mawili! Heee! Kumbe miaka!.” “Bwana mimi nimefiwa.” “Acha
bwana dada!” “Si ndio nimeacha sasa. Namsubiria Jimmy wangu, nilee.” “Hayo ndio
maneno. Lakini tenda ya watu tuliyochukua lazima tuitimize. Tusiwe matapeli.”
“Hamna shida. Nimekwambia mimi nakusikiliza wewe. Ila usiache mambo ya wanao,
sababu ya pesa. Shukuru Mungu umepata pakuweka kichwa leo na kula, basi fanya
ya leo. Usiharibu leo, kwa ajili ya kesho. Ukijenga msingi mbaya, hata kama
utaweka gorofa zuri la namna gani juu, ipo siku itakupasukia tu. Kuwa makini.”
“Nimekuelewa dada yangu. Basi ngoja nichukue nguo baadhi, ila kesho kutwa
nakuja tulale hapa, ili tujiandae na hiyo tenda ya jumamosi.” Fifi akacheka.
“Sasa
unacheka nini?” Nanaa akauliza huku anasimama. “Hivi ulisema wanaitwa kina nani
tena?” Fifi akauliza kwa kejeli. “Kina nani?” “Huyo mwanao na baba yake.” “Kina
Magesa?” “Ewaaah! Hao kina Magesa wamekuganda, huthubutu kurudi hapa. Hata kama
utapata tenda ya ikulu, hawatakuachia.” “Nitawapanga dada, ili nipate kijipesa
changu.” “Sawa mama. Tutakuona. Ila ujue mwenzio naanza kufufua biashara
yangu.” “Usinikatie tamaa mapema bwana. Vuta subira.” Nanaa akaingia ndani
kuchukua baadhi ya vitu alivyojua angehitaji.
~~~~~~~~~~~~~~~
Huku
nyuma Geb alishatafuta sehemu ya kwenda kuishi na familia yake kwa muda wakati
wanajiweka sawa. Akabahatika pale pale maeneo ya Msimbazi centre, lakini
apartment tofauti. Akazungumza nao. Kwa kuwa alikuwa akifahamiana na mwenye
apartment, na alishaishi hapo kwa muda, hakupata shida kukamilisha mambo
yakuhamia usiku huo huo.
Awamu Ingine Tena.
Walifika
hapo ilishakuwa usiku wa saa tatu. Liv na mdogo wake walishalala. “Itabidi
kuwafuta, ili niwabadilishe nguo. Liv amejaa michanga kweli.” Geb aliongea
wakati wanaingia ndani. “Nikusaidie yupi?” “Wewe ingia kuoga, upumzike tu.
Nataka kukuona umelala kabisa Nanaa. Ulishakunywa zile dawa?” “Tayari.
Najisikia uchovu!” “Nenda kaoge ulale.” Kulikuwa na vyumba viwili. Akajua
kimoja nilazima kitakuwa cha watoto, na kingine? Akaweka mizigo yake kwenye
chumba ambacho Geb aliweka mizigo ya watoto. Geb alimuona. Hakuongea chochote.
Akatoka na taulo, akaenda kuoga bafu la nje ya hicho chumba. Akatoka ameshavaa
nguo za kulalia, akaenda kujilaza kwenye kochi wakati Geb anabadilisha watoto.
Alipomaliza,
akamfuata pale sebuleni. “Ndio umeshalala?” “Nitalala sasa hivi. Najisikia
uchovu.” “Sasa kwa nini ulale hapo?” “Nimeona nikuachie wewe kule chumbani.
Mimi hapa pananitosha tu. Usiwe na wasiwasi. Nenda kaoge na wewe upumzike.” Geb
akapiga magoti pembeni ya pale alipojilaza. Akavuta mkono wa Nanaa, akaanza
kuomba. Aliomba taratibu, lakini Nanaa alimsikia baadhi ya maneno. Kisha
akasema ameni. “Usiku mwema Nanaa.” “Na wewe. Ila nashukuru kwa
kunipa nafasi ya kuwa na watoto wangu.” “Karibu. Ukitaka kitu chochote usiku,
usiache kunigongea.” “Nitafanya hivyo.” Akaenda chumbani kwake, akamtolea
shuka. Akamfunika vizuri, Geb akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
Maisha
ya pale kwenye apartment yakaanza. Kesho yake Geb hakwenda kazini. Wakashinda
hapo wakicheza na watoto. Vilijaa vicheko siku nzima. Watoto walipolala mchana,
wao walibaki wakiangalia tamthilia na Nanaa kusinzia kidogo. Siku ya kwanza
ikapita, ya pili siku ya ijumaa. Geb pia hakwenda kazini.
Nanaa
akashangaa anamfuata jikoni. Yeye aliamka alfajiri ili kupika vyakula vya wanae
na Geb. Geb naye akawahi kuamka. “Ndio unaenda kazini?” “Nataka kujifunza jinsi
unavyopika uji.” Nanaa akacheka sana. “Usinicheke bwana! Najifunza.” “Haya.
Lakini ndio unatakiwa kusimama hapo jikoni mimi nitakwambia kitu chakufanya.”
“Haaa! Wewe Nanaa ualimu huo umejifunza wapi bwana? Ndio mwanafunzi nimefika
tu, unaniachia kila kitu.” “Kwa kuangalia tu, hutakaa ukaivisha uji hata siku
moja. Kila siku utaona rahisi. Lakini siku ukitaka kupika wewe, utaishia
kumwaga. Wewe shika mwiko na sufuria uanze kufuata maelekeze.” Geb akakubali.
Wakapika mpaka wakamaliza. “Sasa inabidi tule tuonje mapishi.” Geb akacheka.
Wakakaa mezani wakaanza kunywa uji aliokuwa amepika Geb. Wote wakapenda.
“Geb!”
Nanaa akamwita. “Jioni inabidi kwenda kulala kwangu. Ili tujitayarishe na tenda
ya kesho. Kwa kuwa nitachelewa kutoka kwenye hiyo shuguli, nitalala na kesho.
Kwa hiyo nitarudi tena hapa siku ya jumapili. Nitajitahidi kufika asubuhi.”
Kama aliyemwagiwa maji yabaridi, Geb akapooza mpaka usoni, Nanaa akaona.
“Nahitaji
hiyo pesa Geb. Naomba unielewe. Nataka kujifungua Private. Nataka madaktari
wote wawili wawepo hiyo siku ya upasuliwaji. Daktari wangu wa moyo na huyu wa
wakina mama. Nataka niwe na uangalizi wakaribu kama walivyonifanyia kwa Magesa
ndio nataka huduma kama hiyo wakati najifungua Jimmy, ili chochote kikitokea,
niwe na watu wakunisaidia kama kipindi namzaa Magesa. Nilishazungumza na yue
daktari, akasema ni wazo zuri. Ila ni garama sana. Akaniambia kiasi
kilichokugarimu wewe wakati ule wa Magesa. Ni kweli nahitaji kukusanya pesa,
Geb. Sikujua kama ilikugarimu kwa kiasi kile! Yule daktari akasema ndio maana
nilipata huduma nzuri na kwa haraka kwa
kuwa nilijifungulia ‘first class’, lasivyo ningempoteza Magesa na pengine hata
mimi kudhurika vibaya zaidi. Kwa hiyo nahitaji kupambana ili kufikia lengo. Na
hivi nitajifungua kwa upasuliwaji, garama ndio kubwa zaidi.” Geb akanyamaza kwa
muda.
“Kesho
mnahitajika kufika huko kwenye hiyo shuguli saa ngapi?” “Saa 12 ndio wamesema
wataanza kula. Lakini tutataka muda wa ziada wakuandaa meza.” “Unajiangalia
afya yako lakini?” “Nitakunywa dawa. Naamini kwenye saa 4 usiku tutakuwa
tumeshamaliza kila kitu, mpaka kusafisha ili niwahi kurudi kulala.” “Unaenda
kuandaa nini hicho ambacho huwezi kuandaa hapa mpaka uwe kule kwa Fifi?” Geb
alionyesha wazi kutoridhika. Nanaa akakumbuka maneno ya Fifi.
“Hii
biashara ni yangu Geb. Nikizembea mimi, ujue ndio ninaua biashara yangu kabisa.
Lazima nijitoe, ili kufanikisha. Hata kama nitaacha kwa muda, lakini nataka
nikija kurudi, nisiwe niliacha nikiwa nimeharibu. Nitunze wateja wangu. Dada
Fifi amesema ataacha hii biashara. Hapendi kupika kabisa.” “Sasa kama wewe ndio
mwenye biashara, mwambie Fifi yeye ndio aje hapa. Alale hapa, mfanye hicho
ulichotaka mkafanye huko kwake. Lasivyo wote tukalale huko huko kwake.” “Geb!”
Nanaa akashangaa sana.
“Kabisa.
Ni aidha yeye aje hapa, au sisi wote wanne twende kule.” Nanaa alibaki
akimwangalia. “Mpigie simu mwambie akija aje na kila kitu. Mtapikia hapa na
mtaondokea hapa. Kwanza hapa hamtahangaika na maswala ya mkaa. Kuna gesi.
Mtapika kwa haraka na hutatuacha kwa muda mrefu.” Bado Nanaa hakuwa ameelewa. “Yaani
hapa naona ndio nimefika! Geb hataki hata nitoke dakika moja!” Nanaa
akawaza.
“Lakini
lazima nitoke jioni kwenda kununua mahitaji, Geb.” “Unataka nini?” Geb
akauliza. “Kila kitu nimeandika. Lazima niende leo na kuanza kuandaa baadhi ya
vitu mimi mwenyewe.” “Naomba kuona hiyo orodha ya vitu unavyotaka.” Nanaa
akasimama, akaenda kufuata simu yake. Akafungua sehemu aliyokuwa akiwasiliana
na Fifi. Wakitajiana mahitaji mpaka wakafikia muafaka. Geb akaanza kusoma
taratibu.
Wakati
anasoma, na jumbe za Zena zikawa zinaingia. Bila kujua nini kinaendelea kwenye
simu yake. Nanaa amezama kunywa uji kwa bidii kama mwanae Magesa, Geb anasoma
zile jumbe. Akatoka pale kwenye ile orodha, nakuhamia kwenye mazungumzo ya Zena
na Nanaa. Akasoma jumbe za mwishoni, akarudi kwenye orodha.
“Sikujua
kama bado mnawasiliana na Zena!” “Hakuna jinsi yakumkwepa huyo msichana Geb.
Uliponiambia niachane naye wakati ule, nilimfungia mpaka simu zake. Lakini
sijui alifanyaje, akajua kama nimem ‘block’ kila mahali. Akatafuta njia
nyingine yakuwasiliana na mimi. Ila hanisumbui kwa kuwa nimeshamjua kuwa nia
yake nikushindana na mimi. Haniumizi kichwa.” “Sio kweli Nanaa. Zena
amefanikiwa kuingia kwenye kichwa chako. Na anakuendesha kwa vile atakavyo.”
“Sio kweli Geb!” Nanaa akakataa.
“Pale
hospitalini ulipokuwa ukisema wenzako wameolewa, wana watoto, kazi nzuri na
ndoa zilizotulia japo hawana pesa nyingi, ulikuwa ukimzungumzia nani kama sio
Zena? Maana yeye ndio anakuamsha asubuhi hii na habari za ndoa yake na vile Mungu
alivyomjalia mtoto mzuri. Ni asubuhi sasa hivi Nanaa. Hata saa 4 haijafika.
Yupo mtandaoni anajisifia kwako. Hiyo familia anayokwambia ni nzuri, Mungu
amemjalia, anaihudumia saa ngapi? Yuko kila mahali huko mitandaoni anakutag
wewe picha zake na familia yake. Kweli Nanaa?” Kimya.
“Anyway.
Naomba turudi kwenye hii orodha. Hivi vitu naona tunaweza kuvigawa kwenye
makundi mawili. Vyakula na vyombo. Najua vyombo ungependa kununua mwenyewe ili
uchague. Lakini vyakula unaweza kumtuma hata Jeri.” “Hapana Geb. Acha tu
nitafanya mwenyewe!” Geb akamgeukia vizuri.
“Ni
nini Nanaa!? Unafanya nini? Katika maisha huwezi kufanya kila kitu wewe
mwenyewe. Lazima kufika mahali na kukubali kuamini watu ili usaidiwe. Ni siku
ngapi nipo na wewe na watoto? Zaidi ya siku 4. Ni sawa?” Kimya. “Nipo hapa na
pesa yangu inaingia kama kawaida kwa kuwa nimekubali kusaidiwa. Nisingeweza
kufanya kila kitu mwenyewe na niwepo hapa sasa hivi. Unakumbuka kuna kipindi
nilikwambia nahangaika kufanya hii biashara iweze kujiendesha bila hata mimi
kuwepo kila wakati?” Nanaa akatingisha kichwa kukubali.
“Nimefikia
hapo kwa kuwa nilipata muda mrefu wa kuchunguza wafanyakazi wangu. Nikajua
mapungufu yao. Nikajua nani awe wapi na akiwa hapo atanifanikishia mambo yangu
na kwa kiasi gani. Nimejitengenezea timu yangu. Najua nani anacheza wapi na
nimfuatilie vipi. Ndio maana nipo hapa. Nahitaji kupiga simu asubuhi. Wanitumie
mipango ya siku. Grace anipe mipango ya siku nzima ili kujua nini kitaendelea kwa
wafanyakazi wangu wote leo. Napokea ripoti zangu. Nasoma kwa muda mfupi. Najua
kitu gani cha kurekebishwa siku hiyo. Ikifika saa 4 asubuhi, nishajua nini
chakuzungumza na nani. Na jioni nipewe ripoti. Nipo hapa na wewe na watoto
wangu. Biashara zangu naziendesha mimi mwenyewe, kupitia watu wengine. Bila
shida. Lakini kwa kuwa nimekubali kuamini watu.” Kimya.
“Unanielewa
Nanaa?” “Nimeelewa ila nilitaka kufanya kwanza mimi mwenyewe kama wewe
ulivyofanya.” “Mimi sikuwa mjamzito wala mgonjwa. Sikuwa na majukumu ya watoto
kipindi naanza hii biashara. Niliweka mipango yangu kabla hamjaja kwenye maisha
yangu. Niliiona siku ya leo, kabla hamjaja kwenye maisha yangu. Ndio maana
wakati ule uliniona nalala maporini, nasafiri mchana na usiku. Nafanya kazi kwa
bidii ili leo niwe hapa na nyinyi.” Geb akaendelea.
“Nilikwambia
ile ramani ambayo baba yangu aliniachia. Niliifuata kwa bidii sana. Tena
nilipokupata wewe, ndio nikaongeza juhudi ili hiki ninachokifanya sasa hivi
kisichelewe. Namshukuru Mungu nimefanikiwa. Kila kitu kipo kwenye kiganja
changu. Elimu yangu ya kompyuta imenirahisishia kila kitu. Nikitaka kujua nani
yupo wapi na kama anafanya ninachomlipa kila mwisho wa mwezi, nafungua tu simu
yangu. Nawafuatilia bila wafanyakazi wangu wenyewe kujua. Kisha nawapigia simu.
Najua na kufuatilia kila kitu nikiwa hapa hapa na wewe. Najua kama pesa yangu
imeingizwa benki au kuna mtu anachezea sehemu na huwa najua ikiwa kwenye mkono
wa nani kwa muda mrefu, itakuwa hatarini. Najua pesa yangu iwe wapi na kwa
wakati gani. Na nikigundua haipo sehemu na muda uliotakiwa iwepo hapo, basi
ninajua ni nani wakumpigia simu kwa haraka kuhakikisha inapelekwa kwa wakati
huo. Lakini nililipa garama. Na wewe uliona kwa sehemu. Sasa wewe huna huo
muda. Lazima utaumiza familia Nanaa. Kubali kusaidiwa.” Nanaa akanyamaza.
“Namuamini
Jeri kwa asilimia zote. Nilikwambia habari zake. Jeri ni mwaminifu wa hata
ukiacha shilingi sehemu, atakutafuta akupe.
Kwa tabia yake ile, ndio mtu wa pili ninayemlipa mshahara mkubwa mbali
na Grace. Na ndio maana leo unamuona anaendesha watoto wangu. Namlipa kama
meneja wa kampuni fulani. Lakini utashangaa jukumu alilonalo kwa sasa hivi. Ni
Magesa na Liv tu. Hata nimpigie simu saa sita usiku, nimwambie afanye jambo
fulani. Nitarudi kulala bila shida. Kwa kuwa najua Jeri atalifanya kwa
uaminifu. Na ndio huyo nakupa na wewe umtumie. Sasa najua kwa kuwa mimi
umenikasirikia, hutaki kupokea msaada wangu wowote. Umeniziria kila kitu au
kila aina ya msaada nitakao kupa. Lakini nakuhakikishia Nanaa, Jeri atakusaidia
kama ukiamua kuweka mbali tofauti zetu. Atakuwa msaada mkubwa sana kwako. Na
hatakubali kukuharibia kazi. Mtumie kwa ajili yako na watoto. Na kwa kuwa
tayari anakukubali, hamtapata shida.” Nanaa akamfikiria Jeri.
“Kweli
Jeri ni mwaminifu. Japokuwa alikuwa akinihurumia mimi na Liv, vile tulivyokuwa
tukilia. Lakini alisimamia amri yako. Nisimguse mtoto. Alikuwa akinibembeleza huku akiniambia ni
amri amepewa, hawezi kuvunja.” Nanaa
akakumbuka kilio alichokuwa akilia ili amguse mtoto wake, halafu wakamkatalia.
Akaona machozi yanamtoka. Akashindwa kuendelea kunywa ule uji, akaamua atoke
kabisa pale ndani. “Unaenda wapi?” “Nitarudi.” Nanaa akafuta machozi nakutoka
pale ndani. Alishangaa kitu kimemkaba kooni, akashindwa hata kutembea. Akaamua
akae tu hapo nje ya mlango wa ile apartment yao, ajaribu kutulia. Geb akajua
ndio maana bado anahasira naye.
Geb Ajieleza Kwa Nanaa.
Akatoka
kumfuata. “Nilipoondoka siku ile, sikupanga kukupokonya watoto, Nanaa.
Nilimwambia mama lazima upelekewe watoto asubuhi, wakae na wewe kidogo, halafu
warudishwe kwa mama, kisha jioni uletewe tena. Wakishiba, warudishwe kulala.
Sitaki uchonganishi, lakini nataka unielewe na usinifikirie vibaya Nanaa.
Mwanzoni kabisa, kuna siku nilirudi nyumbani mchana nikamkuta Liv analia sana.
Nikamtuma Jeri amlete kwako. Tena nikampa mpaka begi lake lile dogo lenye kila
kitu. Nikamwambia amwache alale na wewe siku hiyo. Jeri akarudi nakuniambia
walinzi walimwambia ni siku ya tatu kujaonekana pale nyumbani. Liv akarudishwa.
Nikawa namtuma Jeri aje kukuangalia pale karibia kila siku, ndipo nikaja kupewa
jibu la kuwa uliamua kuondoka.” Geb akaendelea.
“Nilishangaa
na kuumia zaidi. Nikajiuliza umewezaje kukimbia watoto uliowahangaikia kwa
kiasi kile? Hapo nilikuwa sijui chochote kilichokuwa kikiendelea kwa upande
wako.” “Nilikuachia barua
Geb.” Nanaa akajitetea huku akilia.
“Sikupewa. Na Mungu wangu ni shahidi. Nilikuja kujua habari zako kutoka kwa
babu Nyundo, yule mlinzi. Tena alikuwa akizungumza na mimi kama vile najua kila
kilichokuwa kikiendelea. Mpaka kwamba ulikuwa ukiletewa watoto na hutakiwi
kuwashika. Ni yule babu ndiye aliyeniambia. Ndio maana nikajua sababu ya Liv
kunichukia mimi na bibi yake.” Geb akaendelea.
“Baada
ya yale mazungumzo na yule babu. Na Grace naye akanifuata ofisini na kuzungumza
na mimi sana, nikawa sijui chakufanya Nanaa. Sikuwa nimekusudia utengwe na
watoto. Ile hasira yote niliyokuwa nimeibeba juu yako, ikageuzwa hukumu, nikawa
nashindwa kufikira wala kulala. Ikabidi kuingia kwenye kufunga na kuomba,
kutafuta uso wa Mungu. Angalau anitazame kwa upya, anisaidie nijue chakufanya.
Maana niliweza kuhisi jinsi tulivyokuumiza. Hata mimi nilikasirika sana Nanaa.
Nilitamani kumchukia mama yangu kwa kukutenga na watoto, lakini nikajisuta mimi
mwenyewe. Nikajiambia mimi ndio nina makosa. Nilishindwa kusimama kama
baba kwa watoto wangu. Na nilishindwa kusimama kama mume kwako. Sikuwa na
wakumlaumu. Ila kutubu na kuomba rehema za Mungu.”
“Gafla
watoto wote wakanigeuka. Hawanitaki mimi wala bibi yao. Akianza kulia Magesa,
ujue Liv lazima ataamka. Na akiamka, hamtaki mtu. Anataka ashike ule mtandio
wako tu. Hali wala kunywa. Hataki aguswe na mtu. Akiniangalia ni mara moja,
tena ni kama ananilaumu. Hakuna utakachomwambia akajibu ila matendo tu, tena
akitaka. Hapo sijui pakukupata wala sijui kama kuna mtu anataarifa zako.”
“Nikaendelea
kumuomba Mungu mpaka Jeri akaja kufunguka kwangu. Akaniambia kuwa huo
mnawasiliana, unataka picha za watoto. Ndio nikamtuma akwambie uje uwaone
watoto na unaruhusiwa kuwashika. Siku anakuletea watoto na kukupa ruhusa ya
kuja kuwaona watoto wakati wowote ule, ndio siku niliipata na barua yako.
Ilikuwa imefichwa mahali. Ndipo
nikaisoma na kuelewa kila kitu. Sasa nikamwambia Jeri akutafute ili kusisitiza uwe
unakuja kuona watoto. Ukawa hupatikaniki.” Geb akamueleza mkasa mzima mpaka
walipokuwa wamesimama pale.
“Ni
kweli nilikasirika Nanaa. Uliniumiza sana kwa kutoniambia ukweli. Kama vile
unavyonijua. Huwa napandwa sana na hasira nashindwa kujizuia. Ila nakiri
nilivuka mipaka. Niliongea maneno ambayo yaliletwa na hasira tu. Haikuchukua
hata siku nyingi kujutia nilichokuwa nimekiongea kwako nakujua ni makosa. Tena
wakati ule ambao unanihitaji. Ukiwa umeumizwa na Malii. Nikataka kurudi. Nikiwa
nimejipongeza kuwa angalau katika hasira zangu za safari hii, sikukufukuza.
Nilikuacha pazuri, lakini ukawa umeshaondoka Nanaa.”
“Nikaamua
kurudisha kukuwekea pesa. Muhasibu akaja kuniambia benki wamempigia simu kuwa
cheki zote zimekubali kuingia kwenye akaunti husika, isipokuwa ya kwako. Akaunti
yako ilikuwa imefungwa. Nikampa muhasibu namba yako ya simu. Nikamwambia
akupigie simu, akuombe akaunti yako nyingine. Akaja kunijibu ile namba nayo pia
imefungwa. Hapo nikazidi kukasirika. Kwa kuwa ndio ilikuwa mwanzoni kabisa.
Sijajua hata kwa nini uliondoka. Nikakasirika kuona wewe sio mtu wakuvumilia
wala kutegemewa. Umeweza kukimbia watoto na kubadili mawasiliano kabisa! Kwa
hiyo hayo ndio yaliyokuwa yakiendelea kwa upande wangu.” Nanaa akatulia.
“Simu
iliibiwa kwenye daladala. Nililala, kuja kuamka nikawa nimepitishwa kituo, na
sina pochi.” Wakacheka kidogo. “Ikabidi hapo hapo kuelekea ofisi za Voda ili
kuwaomba wafunge ile namba ili wasiniibie chochote. Nikaomba wanipe namba
nyingine. Nilifunga ile akaunti benki kwa kuwa unakumbuka ile akaunti ni wewe
uliifungua Geb. Unakumbuka nilishakulalamikia makato wanayonikata kila mara?
Ukasema unapenda ile benki kwa kuwa ni waaminifu na unauhakika pesa ipo salama.
Sasa nilipoona umekata matumizi, nikajiambia ni heri nifunge ile akaunti kuliko
waje wanimalizie vijihela vyote vilivyokuwa vimebaki kwa wakati ule. Ndio
nikahamisha pesa zote kwenye ile akaunti niliyokuwa natumia tokea nipo chuoni.
Ni rahisi na hawana makato mengi. Na ndio hiyo nataka nikamuongeze dada Fifi
ili chochote kikitokea apate zakumsaidia yeye na Jimmy.” Geb akatulia
“Nashukuru
kwa msaada unaotaka kunipa wa Jeri.” Nanaa akavunja ukimya. “Kwa hiyo nimpigie
simu nimwambie aje saa ngapi?” “Mapema tu. Lakini mimi itabidi nimpigie simu
dada Fifi aje anichukue tukanunue hivyo vyombo kama ulivyosema.” “Sawa. Naamini
hautachelewa kurudi nyumbani.” “Nitajitahidi.” Wakarudi ndani.
Kulikoungua Mpini.
Wakati
Nanaa anametoka na Fifi, Geb akaamua aende kumsalimia mama yake na watoto.
Alipofika Liv akakataa kushuka garini. “Twende ukamsalimie bibi.” Akabaki
akimwangalia baba yake akiwa amekaa pale pale ndani ya gari kwenye kiti chake.
“Twende halafu tutarudi kwa mama.” Kimya. Geb alishakuwa amemtoa Magesa kwenye
kiti chake. “Liv! Lazima kushuka.” Geb akamkazia sauti. Liv akakunja uso.
“Twende. Na uache kukunja uso.” Liv akanza kutaka kulia. “Haya, shuka hapo.”
Liv akashuka taratibu huku ameshakuwa mwekundu. Geb akafurahi amemuweza mwanae.
Wakati
wanaingia Liv yupo anatembea pembeni ya baba yake, bibi yao akafurahi sana
kuwaona. Akasimama. “Mbona dada amekasirika?” Grace naye aliwaona wakati
wanaingia. Na yeye alikwenda kumsalimia mama yake. “Nenda kasalimie.” Geb
alimpa amri mwanae. “Bibi chapa.” Liv akaanza kutokwa na machozi. Geb akashituka
sana. Yeye na Grace wakamgeukia mama yao. “Mama wewe!” Grace akalaumu.
“Nilimchapa mara moja tu. Tena kibao cha matakoni akiwa na diaper.” Geb
akakasirika sana.
“Kwa
nini ulimchapa, mama jamani?” Grace aliendelea kulalamika. “Nahisi siku hiyo
nilikuwa nimechanganyikiwa tu. Wote walikuwa wanalia na yeye akakataa kutoka
kitandani. Hata mimi nilishangaa nilivyomchapa. Ni kama nikagutuka. Lakini nilimuomba
sana msamaha.” Mama G akajitetea.
“Usingemchapa
mama. Ni heri ungenipigia simu mimi mwenyewe nirudi nyumbani nije kumtoa kitandani
kuliko kuendelea kumwadhibu mwanangu.” “Kumuadhibu au kumfundisha! Nyinyi mngekuwa
hapo bila kuwachapa? Alifanya ukorofi ndio maana nikakasirika. Najua sikutakiwa
kumchapa kwa haraka, lakini nilikuwa namfundisha kutii.” Mama G akawa mkali.
“Ungeelewa
kipindi wanachopitia kwa wakati ule mama! Ulikuwa ukiwapeleka kwa mama yao,
huku hutaki mama yao awaguse! Huoni kama ulikuwa ukiwaadhibu mara mbili?”
“Jamani mama wewe! Ulikuwa ukifanya hivyo tena?” Grace alilaumu zaidi. “Jamani
nyinyi mnamjua Malii jinsi alivyo Malaya yule mtoto. Nilikuwa nawalinda hawa
watoto. Kama Nanaa angekuwa ameathirika, hamuoni kwamba hawa watoto
wangeambukizwa pia kila wanapokwenda kwake na kuwanyonyesha? Leo mnanilaumu kwa
kuwa kila kitu kipo sawa. Lakini wakati ule kama angekuwa ameathirika,
akaendelea kunyonyesha watoto, hakika wote wangeathirika na tungekuwa
tukizungumza habari nyingine sasa hivi.” Kimya kwa muda.
“Ila
ujue huyo mtoto anaakili kama za Geb, mama. Hasahau. Ndio maana nikawa
najiuliza, nini kimetokea kati yako na Liv? Maana alikuwa akikupenda sana.
Gafla akawa kila akikuona anajificha.” Grace akaongeza. “Ni hasira tu na nahisi
nilikuwa kama nimelemewa. Lakini sio kwamba nilikuwa nawatesa watoto Geb.
Nawapenda sana watoto wako, hata nyinyi ni mashahidi.” Geb akanyamaza.
“Nashukuru
kwa kuja kuniona.” Mama G akabadili mazungumzo. Bado Geb alikuwa amesimama.
Hajui kama akae au aondoke. Mama yake alijua ameshakasirika. “Usingemchapa
mwanangu.” Geb akalalamika. “Samahani Geb. Liv, samahani mama yangu. Nisamehe
mama. Njoo.” Liv akamchungulia. “Umependeza! Nani amekusuka?” “Mama!” Liv
akajibu huku anacheka na kujishika kichwani. “Jamani mama Liv anajua kusuka!
Umependeza kweli. Njoo unionyeshe mimi na aunt.” Liv akacheka nyuma ya baba
yake akichungulia katikati ya miguu yake. “Njoo Liv kipenzi changu. Njoo.”
Grace akamwita. Akamwangalia bibi yake na aunt yake akarudi nyuma ya miguu ya
baba yake.
“Nenda
kambusu bibi na anti.” Geb akamwambia mwanae. Liv akaenda kumbusu bibi yake na anti
yake akarudi kwa baba yake. “Twende dad.” Liv alishafika mlangoni. Wakacheka.
“Njoo nikupe zawadi kwanza.” Liv akakataa. “Twende dad.” “Subiri kidogo. Kakae
pale kwenye kochi unisubiri.” Liv akatoka, wakabaki wakimtizama wasijue anaenda
wapi. Kwa kuwa baba yake alijua anaelewa vizuri, hakutilia mashaka na
anapokwenda. Wakamuona anakwenda kukaa kwenye kochi la barazani.
“Japokuwa
Liv anaweza asitamke maneno yote kwa ufasaha na mkamuona ni kama hayupo. Au
hasikilizi sababu ya ukimya wake, lakini nimekuja kugundua anasikia na kuelewa
kila kitu. Chochote mnachozungumza mbele yake, anaelewa na hasahau. Naombeni
muwe makini na kila kitu mnachoongea mbele ya Liv. Na sitaki mtu amchape.
Mkishindwa kumuelekeza kitu, niambieni mimi mwenyewe.” “Sawa baba. Hata hivyo
nilimchapa mara moja tu, tena kidogo.” “Kwa Liv alivyo, anaweza asiwe ameumia
kwa kumchapa, ila ile hasira uliyokuwa nayo wakati ule, ukamuonyesha na kuishia
kumchapa. Na pengine ulimgombesha kwanza wakati ukimlazimisha afanye kitu
ambacho hakutaka kufanya kwa wakati ule.” Geb aliendelea kulalamika.
“Basi
baba. Nipe basi mume wangu nimsalimie. Yeye na mimi hatuna ugomvi.” “Lakini
hatutakaa sana. Nimepita tu kukuona mara moja.” “Nanaa hajambo?” “Anaendelea
vizuri.” Geb akajibu kwa kifupi wakati anataka kumkabidhi mtoto kwa mama yake.
Magesa akamng’ang’ania baba yake kama hataki amshushe. “Hee! Wewe Magesa! Yameanza
lini!? Hebu njoo bwana.” Bibi yake akamsisitiza. Lakini Magesa akafunga mpaka
miguu akimng’ang’ania baba yake, akisisitiza hataki kushuka au kutoka pale kwa
baba yake kwenda kwa bibi yake. Wote wakashangaa.
“Wewe
Magesa ndio wakunikataa mimi! Yaani umeondoka hapa juzi tu, gafla unajidai
hunifahamu!? Hebu njoo bwana.” Yule mtoto akamkataa bibi yake kabisa mpaka
kilio. “Basi baba.” Baba yake akambembeleza akamuweka kifuani. Akakaa naye.
“Labda kwa kuwa ametoka usingizini.” Geb akatetea.
~~~~~~~~~~~~~~~
Kile
kitu kilimuuma sana mama G. Akaumia mpaka watoto wake wakajua. Akabadilika na
kuwa mpole sana. Magesa ni kama mtoto wake. Ni kama alivyomtoa Geb hospitalini
baada ya kumzaa ndivyo ilivyokuwa kwa Magesa. Alimlea kwa mapenzi yote kama
mtoto wake kabisa. Kitendo cha kukesha naye mchana na usiku, kuanzia anazaliwa mpaka
siku tano zilizopita ndio anakuja kumkataa, akasikia kabisa ni hasira ya Mungu
iko juu yake. Magesa ni mtoto ambaye hakujua mapenzi ya mtu mwingine isipokuwa
bibi yake na baba yake. Leo amemkataa! Ilimuuma sana.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Vipi
familia?” Geb akamuuliza dada yake. “Naona Mungu amenipumzisha na ulezi. Bado
Danny anahangaika nao. Utamuonea huruma.” Grace aliongea safari hii akionekana
kama amesharidhika. “Mbona sasa unaongea kama jambo la kawaida?” “Sasa
nifanyaje Geb? Hebu niambie. Nimeshamuomba Mungu kwa kufunga na kuomba zaidi ya
miezi mitano sasa. Heka heka haziishi! Danny kawa kama kapagawa na wale watoto
na huyo Sara. Imebaki kushukuru tu. Lasivyo naona nitachanganyikiwa nishindwe
kuwa na wanangu pale ninapopata nafasi ya kuwa nao.” Grace alieleza taratibu.
“Kwani
wamehama?” “Tupo wote tunaishi humo humo ndani. Tumejaa tele.” Grace aliongea
kama kitu cha kawaida. Geb akamtizama kwa kumshangaa. “Mimi napata muda na
wanangu kama kawaida. Siku za jumamosi na jumapili ndio anatoka na watoto na
mimi napata muda wakufanya mambo yangu binafsi. Hapa nimetoka kutengenezwa
nywele na kucha. Nasubiri saa 10 jioni ifike, niende kwenye masaji. Nikakae
huko nipumzishe mwili wangu, nirudi nyumbani. Jumapili kanisani. Jumatatu
kazini. Tena hivi umeondoka, ndio nafurahia nimepata kitu chakunifanya
nisiwaze. Nafuatilia hata yasiyonihusu huko kazini. Ilimradi jioni ifike,
nikaone wanangu. Basi.” Grace akaongeza.
“Sasa
na wale wadogo?” Geb akauliza. “Danny kapandishwa cheo. Anapesa inayomchanganya,
hana ndugu hana pakuipeleka, zaidi yakunikomoa mimi. Kawatoa watoto nyumbani,
kawaanzisha shule. Pale pale anaposoma Fili, ndiko wapo wadogo zake. Anamwaga
mipesa kama hana akili nzuri. Anatoka na wanae wote asubuhi, anarudi nao jioni.
Siku hizi humo ndani kwetu lugha inayozungumzwa ni kingereza tu, kama tupo
London!” Grace akaongea kama mazuri. Akacheka, lakini Geb akanyamaza.
Wakakaa
kimya kwa muda, kila mtu akiwaza lake. Mwishowe Geb akaona aondoke.
Hakukaribishwa hata maji ya kunywa. “Naona sisi tuondoke, tuwahi kurudi kabla
Nanaa hajarudi nyumbani.” “Mmerudi kwenu?” Grace akauliza. “Hapana. Sio sasa
hivi. Namuacha kwanza. Nimegundua Nanaa anapaogopa sana pale nyumbani.
Anaonekana baada ya lile tukio alishindwa kuja kulala tena. Kwenye mazungumzo
yake, ni kama hajawahi kurudi kulala kwenye kile chumba tena. Sasa, kwa sasa
hivi naona heri atulie pale wakati nikiendelea kumuomba Mungu. Pengine atanisamehe,
atataka turudiane. Hapo ndipo naweza kuzungumza naye swala la kurudi
nyumbani. Lakini kwa sasa namchukulia taratibu sana ili atulie na watoto na
aweze kujifungua salama.” “Umefanya vizuri.” Mama yake akaongea kwa upole.
“Naomba
tuombe kabla sisi hatujaondoka.” “Pole. Mnaondoka na njaa! Sikupika, kwa kuwa
nipo kwenye maombi. Grace naye amekuja hapa, tukaishia kuomba tu, na
mazungumzo.” Mama G akaongeza. “Hamna shida. Naona hamna mwenye njaa hapa. Eti
Magesa?” Geb akamuuliza Magesa aliyekuwa amejiegemeza begani kwa baba yake,
akiangalia nje.
“Liv!”
Geb akamuita. Akaja na kuchungulia. “Njoo tuombe.” Liv akiwa amesimama pale
pale mlangoni, akafunika macho na vimikono vyake viwili, kama yupo tayari kwa
maombi, akainama. Wote wakacheka. “Njoo ndani bwana!” Baba yake akamwita. “Njoo
ukae hapa karibu na mimi.” Akaenda kujificha ubavuni kwa baba yake. Geb akaongoza
yale maombi. Alianza kwa kutubu. Alitubu kwa niaba ya kila mmoja wao pale.
Akawatakasa mpaka watoto wake, akiomba Mungu awarehemu wote. Aliomba Mungu
awabariki na kuwapatia yale yote ambayo pesa na elimu haviwezi kuwapa. Wakaomba
wote watatu kwa kupokezana, mpaka wakamaliza. Geb akaondoka na watoto wake.
~~~~~~~~~~~~~~~
Sababu
ya maombi ya muda mrefu na foleni barabarani wakawa wamechelewa kurudi
nyumbani. Wakamkuta Nanaa alisharudi, Fifi alishaondoka. Liv akamkimbilia mama
yake. “Mama!” “Mpaka nimepatwa na hamu na nyinyi! Mbona mmechelewa kurudi?
Mbusu mama.” Liv akambusu mama yake na kumkumbatia. “Mmetoka kwa sonara? Naona
una hereni na bangili mpya.” Nanaa akamuuliza mwanae wakati Geb anaweka vitu
vya watoto chini. “Bibi!” Nanaa akajua wametoka kwa bibi yao. Hapo hapo na yeye
akabadilika mpaka Geb akajua.
Kwanza Geb hakumuaga kama
atawapeleka watoto kwa bibi yao, nalo likawa kosa lililomuudhi. Amepewa dhahabu
wakati yeye hana uwezo huo. Nalo likawa kosa lililomuudhi. “Anawadanganyishia
wanangu kwa zawadi ili wanikatae mimi, wamtake yeye!” Nanaa akawaza wakati mwanae
akiendelea kumsimulia habari za huko. Akamwambia na auntie yake alikuwepo, ila
Fili hakumuona. Akamuelezea pia kuwa walimuomba Mungu kwa pamoja. Na yeye akaomba
pia.
Geb
alimuona wazi amekosa raha. “Naomba nimshike kaka.” Akimaanisha Magesa. Magesa
akaenda kwa mama yake. Wakaanza kuzungumza pale wote watatu. Yaani Nanaa na
wanae. Akajilaza kabisa kwenye kochi wanae wakawa wamemlalia huku akizungumza
nao. Geb alijaribu kuingilia kwenye hayo mazungumzo akaona yeye anapewa majibu
mafupi mafupi tu. “Vipi huko, mlifanikiwa?” Geb akauliza. “Ndiyo.” Nanaa
akajibu bila hata kumtizama. “Jeri alikuletea vitu vyote unavyotaka?” “Ndiyo.”
Akajibiwa tena kwa kifupi. “Nilidhani Fifi atalala hapa leo ili msaidiane
kazi.” “Atakuja kesho asubuhi.” Geb akaona anyamaze kwanza. Hapakuwa na
maongezi ya ziada.
Wakalisha
watoto na kuwaweka kitandani baada ya kuomba nao. Nanaa alishakuwa amepika
mapema tu, akaoga kabisa. Akachukua mashuka yake chumbani akarudi kujilaza
kwenye kochi. Tena safari hii aligeukia pakuegemezea mgongo hapo kwenye kochi.
Hakutaka kuona sura ya Geb.
Geb
alipotoka kuoga, akakuta taa zote za sebuleni zimezimwa Nanaa ameshalala.
Akajua amekasirika. Akaenda mpaka pale alipolala, akapiga magoti akajiegemeza
kichwa pembeni ya Nanaa, akatulia kwa muda. “Ulipotuacha hapa, nikapata wazo la
kwenda kumuona mama mara moja. Nikaona nisikusumbue kukupigia simu kukwambia.
Nikimbie mara moja na watoto, nikijua nitawahi kurudi kabla yako. Naona sababu
ya maombi na foleni, nimechelewa kurudi na watoto.” Kimya. Geb mbabe sio huyu
wa sasa hivi. Hata Nanaa hakuwahi kuona aina hii ya Geb.
“Umeshakula?”
Geb akauliza. Kimya. “Njaa inaniuma mwenzio.” “Nilijua umekula kwa mama yako. Chakula nilishapika. Nimekirudisha
kwenye friji wakati umeingia chumbani kwako.”
Nanaa akajibu kwa sauti ambayo Geb akajua huko alikogeukia analia.
“Nilienda
kuoga. Lakini Sikula. Nilitaka tuje kula wote.” Geb akajibu kwa upole na
unyenyekevu kama si Geb! Kimya. “Unataka nikupashie moto chakula na wewe, ili
tule huku tunaangalia movie?” Kimya. “Nimekuudhi?” Geb akauliza kwa upole
akibembeleza, mpaka Nanaa akajisikia vibaya. “Naomba nisamehe Nanaa. Sikujua
kama nitachelewa na watoto. Ulitusubiri kwa muda mrefu?” Nanaa akatingisha
kichwa kukubali. “Pole.” Geb akambusu mgongoni.
Akamuona
anageuka taratibu. Akampangusa machozi. “Unarudi kuishi na mama yako?” Nanaa
akauliza huku akitokwa machozi. “Hapa duniani zipo falme mbili tu, ambazo
zinazofanya kazi. Lazima uchague moja ili kuweza kuishi maisha fulani. Hakuna
pande ya katikati. Lazima uchague. Na ukiwa katikati huwezi kufaidi mema ya
famle hizo mbili. Lazima ukubali kumtumikia Mungu kwa uaminifu ili ufaidi mema
yote, au shetani ili akupe yale awapayo wafuasi wake. Hakuna katikati.” Nanaa
hakuelewa anachotaka kuongea Geb. Havikuendana na swali lake.
“Sasa
mimi nimekuwa nikiishi katikati kwa muda mrefu sana. Nikiogopa kwenda kwa
shetani kwa sababu nyingi tu. Lakini sasa hivi nimeamua Nanaa. Nimekusudia
kumfuata Mungu kwa moyo wangu wote na akili zangu zote. Kwa kuwa najua hata
nikirudi kwa shetani, kwa hivi nilivyo, mapungufu niliyonayo, atanichoka kwa
haraka sana, na nitaendelea kuteseka. Ni Mungu mwenyewe ndiye nimemuona anaweza
kuchukuliana na mapungufu yangu na kunisaidia.” Geb akaendelea huku Nanaa
akimsikiliza akiwa amejilaza kwenye kochi.
“Nimeamua
kusoma neno lake, huku nikimsihi Roho wake anijalie kuishi vile neno
linavyosema. Nipo kwenye kujifunza. Najua kutakuwa na kukosea kwingi, lakini
najua Mungu ni mwaminifu na wa haki, kile alichokianzisha ndani yangu,
hatatulia mpaka akikamilishe. Katika kusoma maandiko nikakutana na maandiko
ambayo ni magumu sana kwangu. Na si kwamba ni mageni. Lakini nafikiri Mungu
alitaka au aliona ndio wakati wa mimi kuishi hilo neno.” Geb akakaa.
“Naweza
kuwasha taa?” Akamuuliza Nanaa. Akiwa haelewi, akakubali. Geb akaenda kuwasha
taa, akarudi na simu yake mkononi. Akaenda kunyanyua miguu ya Nanaa ili akae.
Nanaa akataka ampishe, lakini Geb akamzuia. “Nitaipakata tu. Hamna shida.” Geb
akakaa, na kuipakata miguu ya Nanaa. Akaiminya minya kidogo kama kuipapasa. Nanaa alisikia faraja ya
pekee, akauma midomo yake na kutoa tabasamu. “Asante.” Akashukuru, Geb
akamwangalia na kurudisha macho kwenye simu.
“Ngoja
nikusomee kile Mungu anachokiwekea msisitizo kwangu, sasa hivi.” Akafungua
bibilia ya kwenye simu. Akasoma{Mwanzo
2:24 Kwa hiyo mwanamume atamuacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe,
nao watakua mwili mmoja” } “Niliposoma hiyo,
nikatulia kwanza. Roho wa Mungu akanichukua tena taratibu mpaka hapa.” Geb
akafungua tena andiko jingine kwenye bibilia. Akasoma. { Mathayo 19:5-6 Akasema, kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na
mamaye, ataambatana na mkewe, na hao wawili watakua mwili mmoja? hata wamekua
si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, Hapo napo ikawa ni mafundisho magumu zaidi. Maana Mungu alishugulika na
kila eneo la maisha yangu na yale yaliyotokea kwako na mimi nikakuacha. {mwanadamu
asiwatenganishe.} Hapo Mungu
akahakikisha anaparudia sana tena sana.” Geb akaendelea.
“Hapo
ujue nilikuwa kwenye maombi ya siku tatu. Nimefunga. Hata maji sikuwa nakunywa,
natafuta uso wa Mungu tu. Sijui ulipo, sijui chakufanya. Watoto wote
wamenigeuka. Bibilia ndio kimbilio langu. Naisoma mchana na usiku labda Mungu
atazungumza na mimi. Ndio nakutana na hayo maandiko! Mungu hakuishia hapo
Nanaa. Akaendelea tena kwenye hilo eneo. Nikakutana na huu mstari tena. {Waefeso 5:31 Kwa sababu hiyo mtu atamuacha baba yake na mama yake,
ataambatana na mkewe na hao watakua mwili mmoja.} Hapo nikajua lipo tatizo ambalo Mungu ameliona ndani yangu, anataka
nilishugulikie. Hakuna jinsi ungemwambia Geb aachane na mama yake akaelewa.
Wewe unanijua, Nanaa. Umenikuta nalala na mama.” Nanaa akacheka kidogo.
“Nikaanza maombi kumsihi Mungu anifundishe kwenye
hilo eneo. Mungu mwingi wa rehema, akaanza kunifundisha taratibu na kwa upole.
Akanichukua hatua kwa hatua kunifundisha mimi ni nani na nafasi yangu kwake na
kwa jamii ni ipi. Mpaka anamalizana na mimi kwenye hilo eneo, nikaishia kulia
nakuomba toba. Nikajikuta nimeshindwa kusimama kwenye nafasi hata moja wapo.
Kwanza kama mtoto kwa mama yangu. Mume kwako, baba kwa watoto wangu na kijana
kwenye jamii. Vyote hivyo nilikuwa nimevichanganya na kuharibu kabisa mpaka
nikafika mahali, majukumu yangu yote, kasoro pesa ambazo nalo hilo ni eneo
Mungu ameshugulika nalo pia. Bado sijapona, lakini bado ananishugulia. Naamini
nitapona tu.” Nanaa hakuwa ameelewa ni nini ambacho Mungu anatakiwa ashugulike
kwa upande wa pesa kwa Geb. Maana ni kweli alimbariki na pesa. Wakati watu wengine
wakilia njaa, akaunti za Geb zilikuwa zikiingia pesa za halali zisizo na
maswali.
“Kwa
hiyo kama nilivyokwambia, nikagundua nilikuwa nimeshakoroga kila eneo. Majukumu
yote au yale ambayo nilitakiwa kuyafanya mimi, nikawa nimemkabidhi mama yangu,
ndio maana hakuna kilichokuwa kikienda sawa, kasoro pesa tu ambazo niliweka
uangalizi wa asilimia 100, chini yangu. Huwa siamini mtu na mipango yangu ya
pesa, hata Grace. Nikishajiwekea mipango, ni mimi tu ndio nitaisimamia na
kuhakikisha inatimia. Imeniathiri sana, lakini Mungu ni mwaminifu. Na hapo
atanirehemu tu siku moja.” Geb akaendelea.
“Kwa
hiyo Nanaa, umepata jibu la swali lako?” Nanaa akainamisha macho chini kama anayefikiria.
“Nanaa?” “Nimekusikia Geb.” Nanaa akajibu taratibu. “Na je, umenielewa?” Akamuona
analia. “Najua kila kosa lina adhabu au madhara yake, siwezi kuepuka hilo.
Nimeshakukosea mara nyingi sana. Najua hata unatilia mashaka upendo wangu kwako
kwa sababu nimeshindwa kuishi kile nilichokuahidi tokea mwanzo. Umeweka wazi na
kwa vitendo, kuwa upo hapa kwa ajili ya watoto tu. Silaumu. Lakini Nanaa,
kumbuka wewe ni mke wangu. Nilishalipa mahari. Ndoa yetu ilishatangazwa
kanisani mara tatu na tukaenda kuombewa na mchungaji kanisani. Tulishawekeana
viapo mbele za Mungu. Bado tu kuweka viapo mbele za mashahidi ili tupewe hati
za ndoa.” Geb akaendelea.
“Nimeamua
kusimama kwenye nafasi yangu kama mume, baba na mtoto kwa mama yangu. Nasubiri
adhabu yangu iishe ili tuendelee na maisha yetu.” “Mimi sikuadhibu Geb.” Nanaa akajibu huku akifuta machozi. Geb
akamwangalia kidogo, akaendelea. “Kama mume, kusimama na wewe wakati wote.
Sitachoka kukusubiri Nanaa. Nitakusubiri mpaka utakapo nisamehe. Mpaka
utakapoona nafaa kuwa mume wako tena. Mpaka utakapoona ipo sababu ya kuwa na mimi.
Nataka ujue, ninakusubiri.” Nanaa akashindwa hata kumtizama.
“Nitachua
nafasi ya kuwa baba kwa wanangu. Sitamtupia hilo jukumu tena mtu mwingine yeyote,
zaidi mama. Hatakuwa mlezi wa watoto wangu isipokuwa bibi yao. Nitawaongoza
kwenye njia iwapasayo kuishi. Kwa maombi na juhudi zangu zote. Kuwapatia kile
ninachojua wanastahili na kuhitaji. Kwa garama yeyote ile. Iwe pesa au mimi
mwenyewe kutoa uhai wangu kama vile ulivyokuwa ukiwapigania wewe hospitalini
ili wazaliwe. Ndivyo nitakavyohangaika kusimama kuwa baba kwa wanangu kuwapa
kile wanachostahili. Ukiwemo wewe.” Akashika miguu ya Nanaa aliyokuwa
ameipakata.
“Lakini
katika hayo yote, nikakutana na ukweli fulani fulani hapo katikati ambao
nilifichwa, nikaumia sana moyo. Aliyekuwa ameniumiza zaidi alikuwa mama.
Nikataka kumchukia sana. Kwa kuwa ile barua uliyokuwa umeniachia kwa walinzi
ukataka nipewe mimi, Jeri alimpa mama. Mama akaificha. Nilikuja kujua baadaye
sana kama nilivyokwisha kukusimulia. Hasira ikaniwaka ndani yangu. Nikamchukia
mama. Lakini tena, Mungu akanibana.” Geb akamuachia Nanaa. Alikuwa akimpapasa
miguu huku akiiminya minya kwa mkono mmoja. Alijua wazi Nanaa anafurahia.
Akachukua
tena simu yake. Akafungua bibilia. “Akanipeleka sehemu ngumu kweli. {Marko 11:25–26 “Nanyi
mnaposimama kusali, sameheni kila mtu aliyewakosea ili Baba yenu wa mbinguni
apate kuwasamehe ninyi makosa yenu. 26 Lakini
msipowasamehe wengine, basi makosa mliyofanya ninyi hayatasamehewa na Baba yenu
wa mbinguni.”} Hapo
napo pakawa pagumu. Nikakumbuka dhambi nilizonazo. Nikajiambia inamaana nisiposamehe,
na mimi sitasamehewa!” Hapo napo na Nanaa akaanza kuhukumiwa.
“Nikashupaza
shingo kidogo. Kama unavyonijua nilivyo mwingi wa hasira. Lakini Mungu
hakuchoka na mimi. Akaniletea tena andiko jingine. {Matayo 5:23-24 “Basi, kama ulikuwa
tayari kutoa sadaka yako madhabahuni, ukakumbuka kuwa ndugu yako
amekukasirikia, 24 acha sadaka
yako hapo hapo, uende kwanza ukapatane naye, kisha urudi kumtolea Mungu sadaka
yako.”} Kwa
hiyo nikajua hata sadaka zangu hazitakuwa zikipokelewa. Ikabidi kujirudi tu, na
kusamehe. Kwanza Nanaa, kumbuka makosa yalikuwa yangu tokea mwanzo. Sikuwahi
kuachana na mama yangu, na haikutosha, majukumu yangu yote ya nyumbani, nikamkabidhi
yeye. Ikabidi kuwa mpole na kujirudi tu.” Geb akamaliza. Ila yale maneno yote
yalimuingia Nanaa vizuri sana. Na yeye hayo maandika mawili ya mwisho yakawa
yanamuhusu. {Marko11:25-26
na Mathayo
5:23-26} Akabaki kimya.
Geb
akamsugua sugua tena miguu. “Ulitembea sana?” Akamuuliza kwa upendo huku
akimminya miguu kama kumfanyia masaji. Nanaa akakubali kwa kutingisha kichwa.
“Lakini hivyo unavyonifanyia, utanifanya nilale sasa hivi!” Geb akacheka. “Basi
ngoja nilete chakula, tule kwanza ndio ukalale.” “Wapi tena? Mimi hapa ndio
nimeshafika mwenzio. Wala sijisogezi.” “Tupeane zamu yakulala kitandani.”
“Hamna sababu Geb. Mwenzio nafurahia hapa kwenye kochi. Najigeuza nitakavyo,
halafu wanangu wakiamka pale ndani, nawaona. Kwa hiyo wewe furahia tu kitanda.
Mimi nipo sawa kabisa.” Geb akaenda upande uliopo jiko, ambako kuna friji.
~~~~~~~~~~~~~~~
·
Haya, Nanaa amerudi
kuishi na wanae, akionyesha wazi ameshindwa kumpokea Geb kama mpenzi. Kwanza
hana historia yakumuona anaahidi na kutekeleza ahadi zake. Amemwambia wazi bila
kificho kuwa huwa anaanzisha
mambo mazuri na kuishia katikati pindi anapokuwa amekasirika. Lakini Geb huyu anaonekana ni watofauti. Hata
Nanaa mwenyewe amemuona amebadilika. Itakuaje?
·
Usikose kujua
yatakayoendelea kwenye ndoa ya Grace & Danny. Wapenzi wa tokea zamani. Kaburi alilochimba mama G, hakika
ametumbukia mwanae mwenyewe bila kujua, Sara amehamia kwenye ndoa ya mwanae. Je, nini kitaendelea? Grace aliyekuwa ametangaza kumuombea mumewe, ni kama na yeye amesalimu
amri.
Usikose muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment