Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu ya 54 - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu ya 54

Huku kwa Geb.

Geb alilala usiku huo akiwa amefunga siku ya tatu. Akamuota Nanaa analia sana. Akashituka. Akakaa. Akakumbuka vile James anavyokuwa anamuota Nanaa akilia, na anakuwa kwenye shida. “Lakini haiwezekani. Hiyo kitu ni ya James tu.” Geb akabishia ndoto yake. Akajitetea na mikasa mikali ya masaa machache yaliyopita. Kuanzia vile Jeri alivyomsimulia hali aliyomkuta nayo Nanaa na jinsi alivyomuhurumia mpaka kulia. Akakumbuka matusi makali ya Danny mpaka kumfukuza nyumbani kwake. Akajua kwa hakika nafsi yake imeingiwa hofu nakushika tu hukumu, ndio maana akaota ile ndoto. Akajifariji.

Maneno ya Danny. Tukio la kuwatukana matusi mazito vile. Wote watatu. Bila hofu. Kwa  maneno yanayoendana na kweli! Maelezo ya Jeri juu ya Nanaa. Barua ya Nanaa. Kilio cha uchungu cha Liv, nakumuonyesha wazi amemchukia. Mtoto aliyekuwa akikimbilia kifuani kwake, nakulala! Vyote hivyo vilimnyima usingizi Geb. Alikaa kitandani kwake kimya akiwaza. 

~~~~~~~~~~~~

Kwani walirudi nyumbani baada yakutoka pale nyumbani kwa Danny, walishindwa hata kuongeleshana. Mama yake alishindwa hata kumtizama Geb. Alimchukua Magesa. Akamlisha na kumbadili nguo. Liv alishushwa kwenye gari, akakataa hata kushikwa mkono. Akarudi ndani, akajilaza kwenye kochi huku akiangalia tv. Baba yake hakumuuliza kitu. Akamkabidhi chupa yake ya maziwa.

Akaanza kuivuta taratibu huku amejilaza kwenye kochi, amekumbatia mtandio wa mama yake, anaangalia tv. Alipopitiwa na usingizi, ndipo Geb alipombadilisha diaper na nguo, akaenda kumlaza kitandani kwake, na yeye akarudi chumbani kwake.

~~~~~~~~~~~~

Kesho yake Jeri alipofika tu kazini, yaani nyumbani kwa Geb, akamuita nje. Akamwambia amtumie ujumbe Nanaa, ajue anaendeleaje. Jeri akafanya hivyo. Lakini ikawa kimya. “Hata ujumbe unaonekana haujafika!” “Endelea kujaribu. Lakini usimwambie mama. Nyamaza kabisa. Usiropoke hata ujio wa Nanaa jana.” “Sawa bosi.” Jeri akapata kazi yakutunza siri kwa mabosi wake wote wawili. Geb na mama yake.

Geb alipofika tu kazini akampigia simu Jeri kujua kama alimpata Nanaa. “Hapana. Naona bado simu imefungwa.” “Endelea kujaribu.” Geb akasisitiza. Mchana tena akampigia simu Jeri. Majibu yakawa yale yale. Usiku wakati analala, Jeri amerudi kwake, akampigia tena simu.“Bado simu yake inaonekana imefungwa.” Jeri akamjibu bosi wake.

~~~~~~~~~~~~

Juma zima likapita. Bila kumpata Nanaa. Geb akaanza kupaniki sasa. Akaona aanze kumsaka yeye mwenyewe. “Akija kufa, Liv wangu atateseka sana na hatakaa akanisamehe.” Geb akawaza. “Ni kweli nimekuwa kama baba! Grace hajakosea. Alipoteza binti zake wawili sababu yakumuacha mama yao. Baba amekufa bila wale watoto wake.” Hofu ikamuingia Geb. “Lakini Liv bado mdogo sana. Hawezi kuja kukumbuka.” Akajifariji.

Juhudi za kumtafuta Nanaa zikaendelea huku akijiambia anafanya kwa ajili ya Liv. Mchana ukaenda na usiku haukuwa mbali. Kadiri siku zilivyozidi kusogea Nanaa hapatikaniki, akajiongezea sababu zaidi ya kuendelea kumsaka. Safari hii akawa akimtafuta sababu ya watoto wote wawili. “Magesa atakuja kunilaumu sana. Atakuja kunichukia kwa kumtenga na mama yake. Liv naye hatanisamehe kabisa. Bora tu nimtafute, nijue hali yake kwa ajili ya wanae tu.” Akajiambia huku akiendelea kupiga simu ya Nanaa bila mafanikio.

Huku Kwa Grace Na Danny.

Maisha ya Sara yakaendelea ndani ya nyumba ya Danny bila shida. Kuamka anavyotaka bila hata kujigusa na chochote ila urembo wake tu. Alitoka bila kuaga, labda kama Danny yupo. Tena wakati mwingine alitoka na Danny na watoto. Heshima hamna kwa Grace wala kwa msichana wa kazi wa Grace. Grace alishazungumza na msichana wake wa kazi. Kwa hiyo yule dada naye akawa anampuuza tu.

Na kweli, baada ya kama siku 10 hivi Danny, Sara na watoto wote wakasafiri. Grace alipotaka kuwasindikiza kwenda huko Iringa, kwenye nyumba ya mapadri, alikokuzwa mumewe, Danny alimkashifu na kumwambia ni mahali pa chini sana na watu anaoenda kukutana nao ni duni mno. Matajiri kama kina Magesa hawawezi kufika huko wala hataweza kuchangamana na wao. Hataki kiwingu, amuache tu. Grace alishuhudia wanae wakiondoka na Sara kama mama yao.

Alisimama akitizama wanae wakiondoka siku hiyo asubuhi, na yeye akapanda gari kuelekea kazini. Njia nzima alikuwa akimlilia Mungu wake amrehemu. Alilia Grace mpaka anafika kazini kwake. Hakuwa hata akikumbuka ni lini alikula. Alikuwa akifunga mfululizo. Alikaa sehemu ya kuegesha magari, mwishowe akaamua aingie tu ndani aanze majukumu ya pale yanayomtoa kwenye mawazo.

Geb akaingia. Alipomuona na sura ya kulia, akamuhurumia. Asijue ampe pole au samahani. Ni kama yeye na mama yake ndio wamemuingiza kwenye yale matatizo. Akabaki amesimama mlangoni kwake kwa muda akifikiria. Grace alijua wazi kama kaka yake amesimama pale, lakini hata hakumtizama. Aliendelea kuandika kwenye komputa yake.

Simu ya mama yake ikaanza kuita mfululizo. “Mama anawasiwasi na wewe G. Zungumza naye hata kidogo. Amenituma nikuombe upokee simu zake.” Grace akapokea. “Unaendeleaje Grace?” Mama G akauliza. “Namshukuru Mungu. Lakini ujue tu, mke uliyemtafutia Geb, amekuwa mke wa mume wangu. Tunapozungumza hapa, wapo njiani na wanangu wanakwenda Iringa. Kaburi ulilomchimbia Nanaa, nimetumbukia mimi.” Grace alijibu na machozi yakimtoka. Mama yake akakata simu. Geb akaondoka bila kuongeza neno.

  ~~~~~~~~~~~~

Geb alirudi ofisini kwake akabaki amekodoa macho. Nyumbani hapakaliki. Kilio cha wanae, kazini nako kilio cha dada yake. Magesa naye alishaanza kulia usiku. Lala ya Geb ilishaanza kuwa ya shida. Akamuhamishia mwanae chumbani kwake ili usiku awe anamlisha yeye mwenyewe ili asiendelee kumtesa mama yake.

~~~~~~~~~~~~

Binafsi Geb hakuwa akimlaumu mama yake hata kidogo. Alijilaumu yeye mwenyewe kushindwa kuwa baba kwa watoto wake na kusimama kwenye nafasi yake kama Grace alivyomwambia. Akachukuliwa na jazba. Akajikuta yeye na mama yake wako ukurasa mmoja. Hakuna wakumsaidia mwenzie. Wakahama na watoto. Akamuachia mama yake majukumu yote ya watoto, yeye akaanza maisha yakujihurumia kuwa amedanganywa na kuumizwa na Nanaa. Mama G ndio akashika usukukani. Anaamua watoto wafanyiwe nini na nani. Yeye akiwepo hapo hapo akijihurumia hana habari na kinachoendelea.

~~~~~~~~~~~~~

“Danny anahaki yakukasirika. Ni kweli tumekuwa zaidi ya wanyama.” Geb akawaza nafsini mwake akianza kujilaumu sasa. Akaamua kumpigia tena simu Nanaa bila mafanikio. Ndipo wazo lakumtafuta daktari aliyejua huwa anamtibu Nanaa kila akiwa mjamzito likamjia. Alikuwa na namba yake, kwani walikuwa karibu sana kipindi Nanaa ana ujauzito wa Magesa. Yeye ndio alimwibia siri ya jinsia ya mtoto aliyekuwa amembeba Nanaa, Magesa, bila hata Nanaa mwenyewe kujua.

Kwa Dokta Lyamu.

Akaitafuta kwa makini kwenye simu yake, akaipata. Akampigia. “Namuulizia Nanaa. Huwa anakuja kukuona?” Geb akauliza. “Ndiyo. Hivi hapa yupo kwenye matibabu. Lakini safari hii sio Nanaa unayemfahamu wewe. Amejikatia tamaa. Na siunajua uponyaji unatoka ndani? Sasa Nanaa hataki kujikaza kabisa. Dawa zinamkataa. Suluhisho pekee ni kumtoa mtoto, lakini pia hataki kama unavyomjua. Lakini safari hii si kama watoto wake wengine. Huyu wasafari hii amekata tamaa kabisa.” Lyamu akamuelezea Geb.

“Yuko wapi?” Akauliza. “Nilikuwa nimemlaza hapa hospitali ya Tumaini, lakini nikaona nimrudishe tu hospitali ya Muhimbili.” “Kwa nini!?” “Hapa nilimuweka kwa juma zima nikijaribu kumshauri jinsi ya kupona, lakini hakuwa akitoa ushirikiano. Nikaona tunaingia garama ya bure. Heri tuhamie kwenye hospitali ya bure, tuendelee kubembelezana.” “Usingemkatia tamaa.” Geb akajisikia kuumia, akajisahau na kulalamika. 

“Sio mimi! Ni Nanaa mwenyewe.” “Naomba nielekeze alipolazwa.” Akamuelekeza mpaka kitanda alicholazwa. “Na mimi mwenyewe naelekea huko sasa hivi.” Geb akakata simu na kutoka pale mbio bila hata kuaga. Hata muda wakuona wagonjwa ulikuwa bado haujafika wakati Geb akiegesha gari yake katika hospitali ya Muhimbili. Ilikuwa saa 9 mchana. Hakuruhusiwa kuingia. Akakumbuka daktari alimwambia na yeye anaelekea huko. Akampigia simu. “Naomba nisaidie kama unaweza kuniombea nikaingia kumuona Nanaa.” “Nipo huku kitengo cha mambo ya moyo. Najaribu kuzungumza na wataalamu juu ya hali yake. Nitakuja muda sio mrefu.” “Nakushukuru sana.” Geb akakata simu na kubaki amesimama pale nje ya wodi, akitamani aruhusiwe tu aingie amuone Nanaa.

Atafutaye Hachoki.

Kadiri dakika zilivyozidi kwenda, ndivyo shauku ya kumuona Nanaa ilivyomuongezeka. Sababu ya kumtafuta Nanaa kwa ajili ya watoto wake, ikabadilika. Ikawa ni yeye ndio mwenye shida na Nanaa kuliko hata wanae wanao lia huko nyumbani. Alikaa pale akimsubiria kwa hamu kubwa dakatri aje aingie naye.

 Kama baada ya dakika 20, ndipo Lyamu akafika pale. “Twende.” Wakaongozana mpaka alipokuwa amelazwa Nanaa. Alikuwa amelazwa kitanda cha mwisho kabisa. Alikuwa amelala huku jasho likimtoka sana. Daktari akamvuta mkono, akaanza kumpima presha. “Bado ipo juu!” Daktari aliongea huku akiendelea kusoma.

“Anatokwa na jasho jingi!” Geb akaanza kumfuta na kitambaa chake. Nanaa akafungua macho, akamuona Geb. Akamtizama kwa muda, akarudi kulala. Geb akajua anafikiri anaota. “Mungu atakusaidia utapona Nanaa. Pole sana.” Geb alijikuta akiongea. “Acha tuombe.” Geb akapiga magoti pale pale pembeni ya kitanda, akaanza kuomba. Aliomba mpaka Nanaa akaamka.

“Geb!” Aliita kwa upole huku akilia. “Nimechoka. Natamani Mungu anipumzishe. Nimechoka sana.” “Pole Nanaa. Pole sana.” Nanaa akavuta pumzi. “Lakini Nanaa wewe ni mpambanaji. Sio mtu wakuita kifo! Usikate tamaa.” “Safari hii nimepigwa vibaya sana. Mpaka nafsi yangu imepondeka. Siwezi tena.” “Sio wewe Nanaa.”

“Kweli Geb. Siwezi. Natamani kupumzika tu. Nimepambana na haya maisha vyakutosha. Sina nilichobakiza.” “Ni kwa sababu umekata tamaa mapema.” Nanaa akavuta tena pumzi kwa nguvu. Akafunga macho. Geb akamfuta machozi.

“Asante.” Akashukuru huku amefunga macho. “Karibu.” Geb akajibu. Lyamu alibaki akiwasikiliza huku akiandika kwenye jarida la Nanaa. “Nitarudi baadaye tena kidogo. Ngoja nikazungumze na wenzangu. Sijui nitakukuta?”  Baada yakumaliza kuandika, Lyamu akaaga. “Mimi nitakuwepo tu. Utanikuta kama hawatanifukuza.” Geb akajibu. “Nitazungumza na manesi basi ili wasikutoe. Kwanza muda wakuona wagonjwa umekaribia.” Akatoka.

~~~~~~~~~~~~

“Geb!” Nanaa akaita kwa upole. “Naam!”  Geb akaitika. “Lile tukio lilinisababishia nikapata mimba. Hapa nilipo ni mjamzito.” “Nafahamu Nanaa. Najua.” Geb alimjibu nakumfuta machozi. “Lakini Nanaa, naomba umchukulie kama ni mtoto wako. Uliyepewa dhamana na Mungu umlete hapa duniani. Kama ulivyoniambia kwa Magesa. Unakumbuka?” Nanaa akatingisha kichwa akilia. “Basi naomba ufanye kwa nafasi yako. Kama ulivyofanya kwa Magesa ndivyo ufanye na kwa huyu. Najua unaweza Nanaa. Mungu hakuwa amekosea alipompitisha huyo mtoto kwako. Si unajua wapo wengi wanalilia kupata watoto na wameshindwa?” “Kwa hiyo Mungu ameniamini mimi?” Nanaa akauliza. “Kabisa. Anajua uwezo aliouweka ndani yako. Pambana, utoke hapo. Usikubali kushindwa bila kupambana. Umenisikia?” Nanaa akatingisha kichwa kukubali.

“Lakini mwili wangu umechoka sana!” “Unakumbuka umeshika mimba mara baada yakujifungua tu Magesa? Tena hukua hata umepona vizuri. Mwili wako haukuwa umepumzika hata kidogo. Bado ulikuwa upo kwenye madawa. Lazima mwili uchoke. Unachohitaji ni mapumziko tu. Unahitaji mapumziko yakutosha, utakuwa sawa tu.” “Basi narudi kulala. Naomba ukiondoka, ukifika nyumbani unisalimie Liv na mdogo wake.” “Nitafanya hivyo.” Akasinzia kidogo, akashituka.

“Geb!” “Bado nipo.” Akatulia kidogo huku amefunga macho. “Asante kwa kuja.” “Karibu. Pumzika kidogo.” “Ila nina kiu sana. Sijanywa maji siku nyingi na sina mtu wakumtuma maji ya kunywa.” Geb akaumia sana. “Chakula je?” “Huwa wanapitisha cha wagonjwa wote, hichi kinachotolewa na hospitali. Lakini mara nyingi nakuwa nimelala. Nashindwa kula.” Geb akazidi kumuhurumia. Akajua anachoshwa na mengi. “Basi nisubiri nakuja. Unahamu yakula nini?” “Chochote tu. Sichagui.” Akajibu kinyoge. Geb akatoka kwa haraka sana.

~~~~~~~~~~~~

Kwa kuwa alijua Nanaa si mchaguzi wa chakula. Anakula chochote. Akaenda kwenye maduka ya hapo nje ya hospitali. Akanunua chupa ya chai, thermos, akakimbilia baa aliyojua atapata tu chakula laini. Akapata mtori. Akachukua na fanta orange aliyojua Nanaa anaipenda. Akabeba na chupa za maji mbili, akarudi hospitalini kwa haraka.

          “Nataka kukukalisha ili ule.” “Nimechoka Geb. Mwili hauna nguvu. Mikono inatetemeka.” “Mimi nitakulisha. Nakusaidia kukaa.” Geb akamvuta, akamuegemeza kwenye mto. Akakaa mbele yake, huku akiwa ameshaweka mtori kwenye bakuli. Akaanza kumlisha taratibu. Alionekana alikuwa na njaa sana. Alikula ule mtori wote. Akafungua macho. “Asante. Nahisi njaa ndio ilikuwa ikinichosha zaidi.” “Pole.” Nanaa akajiinamia.

“Nilikuletea na soda yako unayoipenda.” Nanaa akaiangalia na kutoa tabasamu. “Asante. Nitainywa sasa hivi ikiwa bado yabaridi.” Akamfungulia. Akaanza kumpa akiwa anavuta na mrija. Alikuwa amemshikia. “Nakushukuru sana Geb. Asante.” “Karibu. Lakini bado mikono inakutetemeka.” “Itapona tu.” Geb akacheka. “Huyo ndio Nanaa ninayemfahamu mimi. Sio Nanaa anayeita kifo.” Akacheka nakuinama kama anayefikiria. 

“Kesho asubuhi nikuletee nini?” Nanaa akanyanyua uso na kumwangalia vizuri, akaona machozi yakimtoka. “Kwani utarudi tena?” Nanaa akauliza. “Ndiyo.” Nanaa akainama nakuanza kulia. “Lazima kujaribu kutulia Nanaa ili presha ishuke.” “Lakini nina mimba ya Malii!” Nanaa akarudia kwa kumtahadharisha. “Nafahamu Nanaa. Najua. Unataka nikuletee nini kesho?” “Chochote tu utakachoweza.” Nanaa akajibu nakujifuta machozi huku akijua wazi itabidi anunue chakula. Geb hakujua kupika hata kidogo.

“Kabla hujaondoka, naomba nikuombe kitu. Samahani lakini.” “Unataka nini?” “Sijui hata simu yangu ilipo. Lakini yupo dada ninayeishi naye. Hajui nilipo tokea siku niliyomuaga nakwenda kuona wanangu. Sijarudi tena nyumbani. Atakuwa na wasiwasi sana. Naomba nimpigie.” Geb akamtolea simu. Nanaa akampigia.

Kwa Fifi.

“Ni mimi dada Fifi!” “Nanaa!” Fifi akauliza. “Ndiyo dada.” “Kwa nini unanifanyia hivyo mdogo wangu? Nimekwenda mpaka polisi! Nimezunguka mpaka mahospitalini. Nimekuwa kama mwehu! Usinifanyie hivyo Nanaa. Watu wananipotea mimi kama upepo. Leo nakuwa na huyu kesho wananipotea. Sina mtu.. Akamsikia analia. “Pole dada. Pole dada yangu.” Nanaa akajaribu kumtuliza.

“Uko wapi sasa? Au umerudi kwa baba watoto wako?” “Hapana dada. Haitakaa ikatokea tena. Nilishakusimulia kila kitu, sikuwa nimekudanganya. Hata kama ingekuwa hivyo, nisingehama bila kukutaarifu dada yangu. Unisamehe.” “Uko wapi sasa?” “Hali ilikuwa mbaya. Si unakumbuka nilitoka nikiwa sijisikii vizuri, nikakwambia nilazima nikawaone wanangu?” “Na wosia ulishaniachia.” Nanaa akacheka.

“Usicheke bwana Nanaa! Umenipeleka mpaka vyumba vya maiti!” “Dada Fifi wewe!” “Sasa je? Ulivyoondoka ukiniaga kuwa unaweza usirudi tena kwa vile unavyojisikia. Heri ukaone wanao angalau kwa mara ya mwisho. Halafu nisikuone tena! Sasa unafikiri ningeanza kukutafutia wapi?” “Si wodini!” “Aliyekwambia sijafika huko mawodini ni nani?” Nanaa akacheka tena. Nanaa huyu alishapewa mtori na soda. Tena alilishwa na Geb! Hata sauti ilishaanza kutoka.

“Nimelazwa dada.” “Wapi!? Kweli nimezunguka mimi mpaka wodi za wanaume. Na hivi ulikata nywele!” Nanaa alicheka tena. “Na tumbo hili?” “Kwani hujaona wanaume wenye vitambi na maziwa, bwana? Hebu niambie ulipo, ili nije. Umekula?” “Nilikuwa nimedhoofu. Kumbe ni njaa. Presha pia ipo juu sana.” “Tulia Nanaa mdogo wangu. Wanao bado wadogo mama. Usikiri kufa. Tulia ulee wanao. Tulia presha nayo itulie.” Nanaa akaanza kulia.

“Unanisikiliza lakini?” Kimya. Nanaa aliendelea kulia. “Umenitoa wodini kwa maneno yako ya imani. Umebadili maisha yangu. Naomba hiyo imani yako itumie na kwako, mdogo wangu. Toka hapo ulipo. Samehe, maisha yaendelee. Leo umekataliwa watoto. Hujui kesho. Uliniambia unapambana ili wanao wakija kukutafuta, wakukute hai, sio waonyeshwe kaburi. Ukaanza vizuri. Umejua ni mjamzito tu, mambo yote yamebadilika. Hutaki kila kitu! Unajiandaa kufa! Umefikiria wanao uliokwisha wazaa?” Nanaa aliendelea kulia.

“Nanaa!” “Nilikata tamaa dada.” “Hapana bwana. Hizo ni kauli za kishamba kweli wakati wewe mtoto wa mjini.” Nanaa akaanza kucheka tena. “Niletee uji kesho asubuhi. Njaa imeanza kunisumbua.” “Afadhali kama hamu ya kula imerudi.” “Niletee na chai, sambusa, chapati na maandazi.” Akamsikia Fifi anacheka. “Wewe si ulikuwa ukitaka nile?” “Nakwambia nitajuta!” Nanaa akacheka. 

“Naomba mimi ndio niwe wakwanza bwana! Ndio ukasambazie wengine.” “Hapa nahangaika kupika. Kutwa nilikuwa nakutaja. Nasema huyu Nanaa kaanzisha mambo anayoyajua yeye, halafu ananiacha.” “Kama nakuona jinsi ulivyokuwa unaongea peke yako hapo jikoni.” “Naongea, nakulia kama mwehu!” “Pole dada yangu. Basi kesho unianze mimi.” “Lazima. Kwanza nishapatwa na hamu na wewe. Sina mtu wakunisikiliza. Ngoja nimalize kupika, nitakupigia tena kabla yakulala.” “Lakini hii simu sio yangu dada. Nimeazima kwa mtu.” “Mmh! Sasa nakupataje?” “Wewe ndio wakupotea Muhimbili wakati ndio maeneo yako haya!?” Fifi akacheka sana. Nanaa akamuelekeza alipo, wakaagana.

 ~~~~~~~~~~~~

“Asante Geb. Nakushukuru sana. Ila naomba usihangaike tena. Maadamu dada Fifi amejua nilipo, ataleta tu vyakula.” Geb akamwangalia. Nanaa akainama. “Jilaze.” Akajinyoosha vizuri. Akamfunika. “Mnaishi wapi?” “Kawe mwisho.” Nanaa akajibu. “Fifi ameolewa?” Geb akauliza. “Mumewe na watoto wake wakike wawili, na binamu wa mumewe, walipata ajali mbaya, wakafariki papohapo. Kwa hiyo tunaishi sisi wenyewe, kwenye nyumba ya uwani. Mumewe alimuachia mali nyingi ikiwemo hiyo nyumba ambayo tunaishi sisi. Ila nyumba yao kubwa wanaishi wapangaji wengine. Amepangisha familia moja tu, ndio wanaishi nyumba yake kubwa ya mbele. Nipazuri tu na yeye ni dada mzuri sana.” “Nimemsikia.” Nanaa akacheka.

“Ukijitahidi ukapona, nitakuwa nakuletea watoto, ukae nao kwa muda unaotaka wewe.” Nanaa akaanza kulia asiamini. “Kweli Geb!?” “Lakini mpaka daktari akuruhusu. Anihakikishie upo salama. Ndio nitakuwa nikikuletea watoto.” Nanaa hakuamini. Alijifunika shuka mpaka kichwani akaanza kulia tena. Geb akamfunua. “Kulia hakutasaidia kushusha presha Nanaa. Jaribu kutulia kabisa. Jipe muda wakutuliza mawazo. Ukijua watoto wanakusubiri upande wa pili. Umesikia?” “Nakushukuru Geb. Asante. Halafu pia usiwe na wasiwasi hata ukiniacha nao. Walishanipima UKIMWI na magonjwa yote hatarishi. Zinaaa na mengine yote ambayo ningeweza kuambukizwa. Lakini wameniambia sina. Nipo salama kabisa.

Nakuhakikishia hata ukiniachia watoto, watakuwa salama.” Geb akanyamaza. Hayo yalikuwa ni maneno ya mama yake, sio yeye. “Nitakuona kesho Nanaa. Ngoja nimuwahi Liv.” “Nisalimie sana wanangu. Nakushukuru sana Geb. Asante.” Geb akamfunika vizuri, nakuondoka. Nanaa alilia kidogo, akakumbuka anatakiwa kupona. Akajituliza kimya pale kitandani.

Siku Inayofuata.

Asubuhi ya saa 12, Geb alikuwa wakwanza pale wodini. Nanaa alikuwa anatoka chooni wakati Geb anangia. “Geb!” Nanaa akashangaa asiamini macho yake. “Mbona mapema!?” “Ndio muda wakuona wagonjwa huu.” “Sikujua.” Nanaa akajibu. “Vipi? Ulilala vizuri?” “Kama mtoto mchanga!” Wakacheka. “Asubuhi hii wamenipima na kunipa dawa. Naona sio mbaya sana. Karibu. Twende kwenye kitanda changu, au unawahi kazini?” “Bado ni mapema sana. Nimeacha bado wamelala.” “Mpaka Magesa?” Nanaa akauliza wakati wakirudi kitandani kwake.

“Yeye ndio anaratiba ngumu. Inabidi usiku niwe namuhamishia chumbani kwangu ili mama awe anapumzika usiku, mchana aweze kushinda nao vizuri. Lazima aamke mara mbili. Na akiamka anaanza kupuliza na kulia. Bibi yake anahisi ameanza kuotwa meno. Fizi zinamsumbua.” Nanaa akafikiria kidogo. “Nimemuona ana afya nzuri.” “Alikuwa mlaji mzuri sana, ila ameanza kubadilika. Alikuwa akila kila kitu. Lakini naona anaanza kuwa kama Liv. Liv anasumbua sana kula. Anaweza akaamka saa nne, akakataa kula kitu chochote mpaka wakati mwingine inabidi niwe narudi mchana kumbembeleza kula kitu chochote.” “Nimemuona. Amekuwa mwepesi sana. Kamebaki nywele tu!” “Nazo hataki kuchana pia. Hataki mtu amshike kichwa. Amekuwa mkali kweli!” Kwa mara ya kwanza Geb akajikuta anatoa dukuduku lake.

“Pole kwa kulea.” Geb akamtizama, akanyamaza.“Nakuombea Geb. Sijaacha kukuombea.” “Unaniombea nini?” “Kila kitu Geb. Nakuombea amani, faraja, kufanikiwa, kila kitu.” “Basi naona Mungu hajayasikia hayo maombi yako. Hamna chochote kinachoendelea vizuri. Si unaniona?” Geb alijibu kwa kujidharau. “Umepitia kipindi kigumu sana Geb. Jipe muda. Mungu atakutendea. Mungu hawezi kukuacha. Jipe muda tu, kila kitu kitakuwa sawa. Pole.” Geb akanyamaza, akabaki akifikiria. Alikuwa amesimama kati kati ya kitanda cha Nanaa na mgonjwa mwingine kwenye wodi hiyo ya wazazi.

Fifi!

          Fifi akaingia. Wakamsikia akisalimiana na manesi wa hapo kama mashoga zake wa mtaani tu. “Huyo unayemsikia mwenye kelele, ndio dada Fifi.” Akasalimiana na manesi wote na utani kidogo, ndipo akaenda kwa Nanaa. “Umenitesa Nanaa wewe!” “Pole dada. Pole sana. Hali ilikuwa mbaya. Nilianzia hospitali ya Tumaini, baada ya kama week hivi, yule daktari akanihamishia hapa. Nahisi yeye ndio mwenye vitu vyangu vyote. Nilifika pale nilikuwa sijiwezi!” Akamsimulia kila kitu. Kuanzia alipotoka pale mpaka siku hiyo.

“Pole mdogo wangu. Pole sana. Lakini si umshukuru huyo bwana kama amekubali hata ushike watoto? Maana wanaume wengine ni washenzi, wangekutosa baharini.” Fifi akaanza taratibu. Nanaa akatamani kumkonyeza kwa kuwa alimjua. Hana breki ya mdomo. Fifi akaendelea. “Lakini naye anajishaua! Kinachomfanya amtume dereva wake ni nini, asiyeleta wanae yeye mwenyewe? Nakwambia ingekuwa mimi mbona ningemzidi mahesabu. Hakika ningetoroka na wanangu. Asilete wazimu wake! Anajua uchungu wa mwana yeye? Azae basi kama yeye anajitia mwanaume kweli! Kwanza wewe ulibakwa. Kosa lako nini?” Geb alikuwa kimya katulia na simu yake mkononi akiperuzi taratibu.

“Mimi sijawahi kuona mwanaume anayeshindwa kumlinda mkewe, halafu eti ajidai kununa! Achana naye mdogo wangu. Huyo bwana hakupendi. Nakwambia mimi mume wangu kwanza angekuomba msamaha. Tena wewe ungeombwa msamaha wa herufi kubwa. Yaani umebakwa kwa kosa la kukataa kulala na rafiki yake! Anakuadhibu nini kama sio wehu huo ni nini?  Kuna watu tunaishi nao mdogo wangu, ni vichaa wale wakulazwa mahospitalini. Hatuwajui tu. Jambo kama hilo likitokea, ndipo unapojua uzima wa akili ya mtu.” Nanaa alitamani kumfunga mdomo, lakini Fifi alionekana na jazba. Akajua wagonjwa wote wameshajua kama alibakwa.

Bado Geb aliendelea kuchezea simu yake. “Au hakuwahi kukupenda? Ulijilazimishia tu mdogo wangu? Maana hayo nayo yamo! Mwanaume hakutaki unajilazimishia unajua atakuja kubadilika baadaye. Yamemshinda, ndio kapata sababu yakukufukuza. Mimi nayajua mapenzi bwana. Tena nayajua mapenzi yakupendwa, si yakusimuliwa! Upendo unatabia ya kusitiri wingi wa dhambi mdogo wangu! Upendo unavumilia! Tena wanasema hautafuti mambo yake yenyewe! Nenda kasome sifa za upendo, ndio utajua kama huyo bwana alikupenda au alikuwa anakutumia tu!” 

“Ila mimi nakwambia Nanaa mdogo wangu, huyo bwana ni MUONGO. Kakutafutia tu sababu. Achana naye. Wala usife sababu yake. Hakustahili hata kidogo.” Nanaa akajitahidi kumkonyeza lakini wapi.

“Kama ni hilo jumba hata mume wangu alikuwa nalo. Kafa, kaniachia lote. Mwenyewe pia likanishinda mpaka uliponipa wazo la kulikodisha. Achana naye. Atakuja kufa aliache hilo jumba na magari yake. Kama alijua atazikwa nayo, basi amechemka. Aniulize mimi. Wewe jikaze, utoke hapa. Zaa. Nikabidhi mimi huyo mtoto kama tulivyokubaliana. Mimi ndio mama yake Jimmy. Au unasemaje Jimmy wangu?” Fifi akainama na kumshika tumbo Nanaa. 

“Nisalimie mwanangu. Sema na mama yako mkubwa basi.” Akampapasa tumbo Nanaa mpaka mtoto akacheza. “Mambo si ndio hayo mwanangu? Utasoma baba. Tena utakuwa msomi kuliko watoto wa matajiri wote hapa duniani. Tutauza sambusa na chapati mpaka uwe daktari, uje ututibu presha mimi na mama yako. Na kingereza utajua tu. Kwani ada shilingi ngapi bwana! Kama mamilioni na sisi tutakuwa nayo tu. Tutauza hata ile nyumba usome mwanangu. Wasitubabaishe.” Fifi akaendelea. 

Nanaa akamvuta kidogo kama kumtuliza. “Sasa je! Wewe tulizana, nizalie huyo mtoto uone atakavyokuwa kama uyoga! Mapenzi yote tutampa. Na kama utataka mwanaume wa kukuoa mbona utapata tu. Wapo kibao na mdogo wangu unalipa! Au vipi?” Akamgeukia jirani ya Nanaa. Mama aliyekuwa amelazwa kitanda cha jirani. “Eti unamuonaje mdogo wangu?” “Si mchezo.Hapo mwenyewe mjamzito na bado anavutia. Unalipa kabisa.” Fifi akafurahi sana.

“Heri mwambie wewe atakuamini. Nikimwambia mimi huwa anasema ooh, dada Fifi wewe maneno mengi, sijui nini! Umesikia sasa?” Fifi akamgeukia vizuri Nanaa. “Kwanza yule jamaa yako anayekutaka, ambaye akikuona anachanganyikiwa, leo nampelekea sambusa 30. Kaniambia anataka wewe ndio uende ili akakuunganishe na mfanyakazi mwenzie, anataka tuwapikie kwenye kichen party ya mwenzao. Sasa changamka mdogo wangu. Mimi nikienda, nitamwambia Nanaa atakuja siku nyingine kama akitoa oda nzuri. Najua kwa kuwa atataka kukuona, lazima aongeze oda kubwa na atupe tenda yakuchanganyikiwa mtu. Sasa mama, changamka hapo. Toka tukatafute pesa za Jimmy. Nataka mwanangu asome. Tena awe gumzo hapa duniani. Au unasemaje?” Fifi akaweka kituo, Nanaa akavuta pumzi. Akafurahia lile swali.

“Eti Nanaa mdogo wangu? Tia neno basi!” Fifi akasisitiza. “Huyo hapo ndio Geb!” Fifi akatulia kwanza. Geb akamtizama. “Geb kwamba anafanana jina na yule baba watoto wako?” Fifi akauliza kwa sauti iliyoishiwa nguvu. Nanaa akatingisha kichwa kukataa. Fifi akajua amekamatwa. Akaweka kapu la chakula chini, akaondoka bila kuaga. “Kakamatwa vibaya! Maneno yote yamemwisha.” Yule mgonjwa wa kitanda cha jirani akaanza kucheka. “Yaani maneno yote yale aliyokuwa akiongea, kumbe bwana mwenyewe hata sura hamfahamu!” Yule mama alizidi kucheka. Nanaa akabaki akicheka kimya kimya huku akifikiria pakuanzia.

~~~~~~~~~~~~

“Angalia ni nini ameleta, ili kama vimepungua nikanunue kabla yakuondoka.” Nanaa akavuta lile kapu. Alileta kila kitu alichomuomba na zaidi. “Naona kila kitu kipo, asante.” Nanaa akataka kujimiminia, Geb akamsaidia. “Naomba ule kidogo Geb. Huo uji ni mwingi sana.” “Hapana. Wewe kula tu. Mimi nitarudi nyumbani. Nitakula, ndio niende kazini.” Nanaa akamwangalia, akanyamaza. “Si kwa sababu nyingine yeyote ile, Nanaa. Nataka uwe na chakula cha kukutosha siku nzima. Ili ukisikia njaa tena, ule. Umenielewa?” “Nimeelewa. Naamini nitatoka.” “Ila naomba usilazimishie. Acha wakuruhusu wenyewe.” Nanaa akanyamaza.

“Unanielewa? Kama ni swala la kuwahi watoto naweza kuwa nakuletea hata hapa.” “Hapa sio sehemu sahihi kwao. Bado wadogo sana. Sitaki waje hapa wachukue magonjwa. Nitakuwa sawa tu Geb. Acha nitoke hapa nipate muda na wanangu. Magesa hanifahamu kabisa! Na Liv naye bado anaonekana hanielewi kwa nini sipo naye. Nakuwa napotea kwenye maisha yake na kurudi kwa sekunde chache, halafu napotea tena. Unakumbuka muda niliokuwa hospitalini wakati wa ujauzito wa Magesa?” “Nakumbuka. Alikuwa anahangaika kweli kukutafuta. Hata sasa hayupo sawa kabisa.” “Nimemuona. Naogopa itamuathiri zaidi. Kama umenipa nafasi yakuwa naye, acha niitumie vizuri. Nitajitahidi kunywa dawa na kupunguza au kugawa muda wa kazi. Ili niwe nao.” Nanaa wa mipango akarudi.

“Unafanya kazi gani?” “Tunatengeneza vitafunwa na kusambaza maofisini na kwenye masherehe.” Geb akanyamaza. Nanaa akaendelea kula. “Mchana ungependa nikuletee nini?” “Usihangaike juu yangu Geb. Umekuja hii asubuhi, inatosha. Maadamu dada Fifi amejua nilipo, sitakuwa na shida tena. Atanihudumia tu. Halafu pia ana gari. Hata nikiruhusiwa, atanisaidia usafiri. Kwa hiyo nikiruhusiwa hapo baadaye, nitamtafuta Jeri, nimtaarifu kila kitu. Halafu nitamuelekeza kule tunapoishi ili awe anawaleta watoto.” Geb alijua ndio hajakaribishwa hivyo.

“Lakini kama watanitoa leo, nikarudi nyumbani kwangu salama, nitajitahidi kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya watoto. Usafi na kupanga vizuri ili kuwe na nafasi yakutosha. Ili wanangu wakija hata kwa masaa machache, wapate pakucheza. Ni padogo, lakini najua patatosha tu.” Nanaa akakumbuka kitu.

“Itabidi nikitoka hapa, nimuombe dada Fifi anipitishe madukani kwanza ili ninunue tv kwa ajili ya Liv. Ili akija akitaka kuangalia cartoons zake, asikose. Halafu itabidi ninunue na feni. Ili..” “Nanaa! Naomba utulie.” “Sitaki wanangu waje wajisikie wapo kwenye mazingira ya ajabu sana. Japokuwa hayatakuwa sawa na kwao, lakini angalau wapate vitu vya muhimu.” “Wanakutaka wewe. Acha kufikiria mambo mengii. Kitu cha msingi na maana ni uzima wako kwao. Basi. Wakukute unafuraha, ili wapate pumziko. Jitahidi kufuata masharti ya madaktari, hilo ndilo la msingi.” Nanaa akanyamaza.

Akaendelea kula. “Hujanijibu unataka kula nini mchana.”“Naomba usihangaike Geb. Dada Fifi ata..” “Hutaki nirudi tena hapa?” “Nakuonea huruma Geb. Najua una mambo mengi. Umechoka. Unahitaji kupumzika.” “Nitapumzika ukitoka hapo kitandani.” Nanaa akaona machozi yanamtoka. Akakumbuka vile Geb anavyokuwa naye wakati wote anapokuwa hospitalini. Tena bila kuchoka.

“Bado unapenda vanila Ice cream au unataka nikubadilishie?” “Nakula kila kitu Geb. Sichagui.” “Basi mwambie Fifi, nitaleta chakula cha mchana.” “Sina simu. Labda kama daktari atapita mapema, nimuombe vitu vyangu.” “Nikitoka hapa, nitampigia kuzungumza naye juu yako, nitamkumbusha juu ya simu yako.” “Nakushukuru Geb.” Nanaa akashukuru.

“Basi ngoja nikamuwahi na Magesa. Napenda kumlisha mimi mwenyewe uji wa asubuhi kabla sijaenda kazini.” “Dada mkubwa bado anaamka saa 4?” Nanaa akauliza. “Bado mpenda usingizi vile vile ila hali kabisa.” Nanaa akabaki kimya, anafikiria. Akavuta pumzi kwa nguvu. Geb akaona anazishusha taratibu. Huku anafuta machozi.

“Nawahurumia wanangu! Wanalipa garama ya makosa yangu.” Nanaa akaanza kutokwa na machozi. “Huwezi amini jinsi Roho wa Mungu alivyokuwa akinisisitiza nikwambie ukweli wote lakini hofu ilinishika kabisa, nikaogopa kukwambia. Hakuna siku inapita bila kujutia Geb. Najuta kupita nitakavyokwambia. Ila basi tena. Najua itakuwa ngumu kuniamini tena, lakini sikukusudia kukuumiza Geb. Ni hofu ndio ilinikamata. Niliogopa usije ukani…” Nanaa akaona haitasaidia tena. “Daah! Basi tena. Mungu awarehemu wanangu tu sasa. Sina jinsi tena. Nilishaharibu mimi mwenyewe.” Nanaa akaona anyamaze tu. Wakabaki kimya kwa muda kila mtu akiwaza lake.

~~~~~~~~~~~~

Geb ndio alikuwa anajua sasa matokeo au athari ya anachokiongelea Nanaa. Anaona shida wanayopitia watoto wao kwa wakati ule bila mama yao. Mama yake alishachoka kwa hakika. Ule moto alioanza nao wakati anapokonya watoto wa Nanaa, hata Geb aliuona ni kama umeisha wote. Si kupungua tena, nikuisha kabisa. Ni kama alishalemewa. Watoto wawili wadogo! Mmoja aliyekuwa akiyajua mapenzi ya mama aliyekuwa anauchu wa kuzaa mtoto na kumpa mapenzi yote aliyokosa yeye. Ambaye ni Liv. Liv aliyajua mapenzi ya mama yake kwa kushikwa na kuongeleshwa. Ungemkuta Liv mkononi mwa mama yake, au akiwa na mama yake! Huwezi kuiga jinsi ya kuishi na huyo mtoto. Ni kule maisha yalikompitisha Nanaa peke yake, ndiko kulikomuwezesha kumlea Liv kwa namna ile.

Magesa alitolewa kwa mama yake hata kitovu kilikuwa hakijaanguka. Mtoto anayehitajika mapenzi ya mama kwa masaa 24. Ratiba zake za kulala zilikuwa bado zinabadilika. Wakati mwingine mchana ndio usiku, usiku ndio mchana. Tena hata ulalaji wake ni wa masaa machache machache, kwa kuwa alikuwa bado anakula vyakula vyepesi. Akikojoa tu, tayari njaa. Ziwa la mama yake ndilo lilikuwa kitulizo.

Siku chache alipokuwa amezaliwa, haikuwa ikimsumbua mama G. Hata kama atakesha naye usiku, basi alijua asubuhi atampelekea mama yake hospitalini. Atamnyonyesha mpaka alale ndipo anarudi naye nyumbani. Akiamka hata akilia, ni kwa muda mfupi, tena akizidisha kusumbua atampa maziwa ya chupa na kumrudisha hospitalini kwenye nyonyo ya mama yake, anatulia. Akiwa na shuguli zake, anawaacha watoto wote hapo hospitalini kwa wazazi wao. Anakwenda kufanya shuguli zake. Akirudi, watoto wanakuwa walishalishwa mpaka chakula cha usiku.

Tena wakati mwingine Geb alikuwa ameshawaosha hata nakuwavalisha nguo zakulalia. Anamuwekea watoto kwenye gari, anakwenda kuwalaza akisaidiwa na Jeri. Asubuhi anawarudisha kwa wazazi wao, Nana ana Geb. Au Jeri anawarudisha hospitalini. Maisha yakawa rahisi sana.

Wakati anampokonya Nanaa, watoto walikuwa wameshiba. Usiku uliopita walikuwa na wazazi wao. Liv aliambiwa mama yake anarudi siku hiyo nyumbani. Akasaidia matayarisho yote yakumpokea mama yake. Akaambiwa atakuwa akiendelea kunyonya na mdogo wake. Hapakuwa na shida.

Mambo yalianza kumbadilikia mama G, mara tu watoto wale walipoamka nyumba nyingine, bila mama yao. Waswahili husema, ‘mtoto wa mtu, mtamu akiwa amelala!’. Hayo ndiyo aliyopambana nayo bibi huyo. Liv alitolewa kwa mama yake akiwa amelala. Ndani ya gorofa lenye kiyoyozi na mazingira mazuri sana. Akahamishiwa kwenye gari ya thamani, akapelekwa kwenye nyumba nyingine ya baba yake. Iliyojazwa thamani kama yazamani. 

Geb alihakikisha kila kitu cha nyumba aliyokuwa akiishi na Nanaa, kipo kwenye ile nyumba nyingine ili watoto wake wasione tofauti. Aina ya vitu vya nyumba ya kwanza vikanunuliwa kwenye nyumba hiyo waliyohamia. Tena na thamani zaidi, lakini bila Nanaa.

Yeye na mama yake walijua wale watoto ni wa Nanaa tokea siku wanaamka upande wa pili, bila mama yao. Ubabe ndio uliwasaidia siku za mwanzoni wakiamini watoto wale watazoea maisha mapya na kuwa sawa. Nyumba ilikuwa ikijaa vilio kuanzia asubuhi mpaka asubuhi. Ndio maana wakati mwingine mama G alipokuwa akilemewa, alikuwa akimtuma Jeri awapeleke kwa mama yao lakini asiwaguse.

Kidogo Magesa akaanza kuzoea. Akawa akipewa chakula kingi mpaka tumbo linasalimu amri, inabidi kulala tu. Ila sio Liv aliyekuwa akimfahamu mama yake. Geb na mama yake walihangaika na huyo mtoto mpaka wakasalimu amri. Vicheko vilikoma. Zile dimpozi walizozoea kuziona kutoka kwa Liv zilikoma kabisa. Akawa mtoto mnyonge sana.

Afya ya mama G nayo haikukawia kumkumbusha umri wake. Wakati akipambana kubeba watoto ili kuwatuliza na kumuonyesha Geb kuwa kila kitu kipo sawa, mgongo haukukawia. Kutokulala vizuri na vilio vya watoto wawili mchana na usiku. Na pia alimuongeza Sara kwa haraka ili kuziba pengo la Nanaa. Akidhani pengine atasaidia ile hali, lakini kumbe ndio akawa ameongeza tatizo jingine. Mtu mwingine anayemtesa kwa wasiwasi. Akihangaika kufunika makosa yake kwa Geb, huku akiteswa na wasiwasi huko anakokwenda siku nzima na kurudi amechelewa! Binti mdogo, aliyekabidhiwa na wazazi wake kwa heshima. Akipatwa na matatizo huko anakokwenda, itakuaje? Wasiwasi ukaongezeka kwa mama G. Akazeeka siku si zake. 

Geb mwenyewe hakuna usiku aliokuwa akilala masaa zaidi ya matano mfululizo sababu yakumuhurumia mama yake usiku na mtoto mchanga. Wakati mwingine akimsikia ameamka, inamlazimu na yeye kwenda kusaidia. Akirudi kulala na yeye, usingizi hauji kwa haraka. Alishazoea kubembelezwa na Nanaa ndipo alale. Nanaa alimzoesha kumshika shika mwili wake hasa kumchezea nywele mpaka analala. Ikabidi aanze tena kujizoeza kujibembeleza kulala mwenyewe. Mpaka usingizi unarudi tena, na muda wakuamka tena Magesa unakuwa umefika na kuhitajika kwenda kazini. Hamna tena kulala. Zilikuwa zimejaa fujo kwenye maisha ya familia hiyo ya Magesa, Nanaa hakuwa na taarifa. Kwa upande mwingine ni heri hata ya yeye Nanaa alikuwa akilala usiku na kuendelea kuwaza watoto wake siku nyingine inapoanza. Tena wakati mwingine hata mchana alilala sababu ya usingizi mzito wa mimba.

~~~~~~~~~~~~

Wakajikuta wote wapo kimya, kila mtu anawaza lake. Ni hawa hawa wapenzi wawili Mungu alishawatumia kujidhihirisha nguvu zake za uponyaji kwa kuwatumia wao. Alithibitisha kwao kuwa upo mkono wake juu yao, hilo halikuwa swali. Lakini bado walikuwa na vitu wamebeba mioyoni mwao. Nakujisahau kwingi.

“Pata muda wakupumzika. Jilaze. Nitakuona baadaye.” Geb akagutuka kutoka mawazoni, akaona ni heri aondoke pale awahi kurudi nyumbani. “Njoo mara moja Geb.” Geb akasogea. “Kaa hapa kwenye kitanda tuombe.” Geb akamwangalia, akakaa. Nanaa akataka kumshika ili amuombee, kama aliyekumbuka kitu, akamuachia. “Tuombe.” Nanaa akafunga macho. “Mungu wangu na baba yangu. Najua hata sasa unatusikia! Tunatambua uwepo wako hata sasa, mahali hapa.” Nanaa akaanza kuomba akiwa amefunga macho. Akahisi Geb amemshika mikono. 

“Tunakupa sifa na utukufu kwa jinsi ya vile tu ulivyo. Tunatubu na kujitakasa…” Nanaa akaendelea. Mwili mzima ulikuwa ukitetemeka kwa kushikwa na Geb. Lakini akaendelea kuomba. “Tunaipokea siku ya leo kwa shukurani. Namkabidhi Geb mikononi mwako. Mlinde na kila hila ya muovu. Mpe faraja na amani moyoni mwake. Mbariki, mpe nguvu na shauku ya kuendelea kukupenda wewe. Msaidie..” Akamuombea mpaka akamaliza. “Amen!” Geb akafungua macho, yakagongana.

“Asante kwa maombi mazuri.” Nanaa akatoa tabasamu ambalo halijawahi kuongopa moyoni mwa Geb. Ni kweli akaanza kupokea faraja yake ile aliyoikosa kwa hasira kali na kumkimbia Nanaa. Akaona maombi ya Nanaa yameanza kujibiwa. Bado alikuwa amemshika mikono. “Naamini utakuwa na siku njema.” “Nakuombea na wewe Nanaa.” “Asante. Nisalimie wanangu.” Geb akasimama. “Nitakupigia picha. Nikuletee umuone Magesa, na dada yake akiwa amelala.” Nanaa akacheka. “Nitashukuru.” Geb akaondoka.

 ~~~~~~~~~~~~

Hata kama una presha ya namna gani, lazima upone. Geb aliyerudi sasa hivi amepoa na amemkubali mpaka mtoto wa Malii! Shida kwa Nanaa inatoka wapi tena? Watoto ataletewa. Ahadi ya Geb kurudi mchana ipo. Tena anarudi na picha za watoto wao! Na ice cream juu! Mungu ampe nini? Presha ikaanza kujitengeneza yenyewe. Akajigeuza mara mbili, ya tatu usingizi ukamchua. Akalala kama mtoto mchanga.

~~~~~~~~~~~~

Haikuwa hivyo kwa Geb mara aliporudi nyumbani. Wakati Nanaa anauchapa usingizi wa furaha kule hospitalini, yeye alipokelewa na kilio cha Magesa. Alimkuta akilia mpaka dada yake akawa ameamka anasikiliza kilio cha kaka yake. Sura ya mama G ilikuwa imebadilika. Alionyesha wazi anaweza kupokea msaada wowote ambao angeweza kupewa. Alichoka, na wazi alionyesha ana maumivu.

Geb akampokea mtoto maana walikuwa wakizunguka nyumba nzima. “Mlete nikupokee.” Bila hata kujivunga, akamkabidhi kwa haraka, akaanza kujinyosha. “Ni nini Magesa?” Geb akamuuliza kwa kumuhurumia mtoto wake. Alikuwa mwekundu kama moto kwa kulia. “Au tumbo limejaa gesi?” Alipogeuka kupata jibu kutoka mama yake, hakumkuta. Alishaondoka zamani. Akawa amebaki na watoto wake wawili. Swali la kama amekula au la, lilishapata jibu. Hakuona kibakuli chochote pale kwenye kiti cha Magesa. Na ndio ilikuwa saa mbili asubuhi wakati Geb anaingia hapo ndani. Kwa hali ile, Geb akajua kilio chake huko chumbani alipokuwa amemuacha amelala, ndicho kilichomuamsha mama yake, na ndio walikuwa wakibembelezana wakati wote.

“Twende nje tukambembeleze mtoto.” Alimwambia Liv. Liv akamtizama baba yake, akarudisha macho kwenye tv aliyokuwa amejiwashia mwenyewe baada yakuamka nakumkuta bibi yake anabembelezana na mdogo wake. Geb akajua amemsikia na kumuelewa, ila hataki. Hata hivyo akajua hana nguvu. Alilala bila kula. Geb akatoka yeye na Magesa. Akazunguka na huyo mtoto hapo nje akilia huku akimpiga piga mgongoni, mpaka akalala.

Ilichukua kama dakika 10 mbele ndipo akanyamaza. Tena akiwa anapingana na wazo lakumpeleka hospitalini wakamwangalie ni nini kinamsumbua. Alirudi kukaa naye pale barazani akiwaza, mwishowe akaamua amrudishe kulala. Yeye akatoka nje.

~~~~~~~~~~~~

Cha kwanza akampigia simu dakatri wa Nanaa, Lyamu. “Inagarimu nini kumrudisha Nanaa kwenye hali yake yazamani?” Ndilo swali la kwanza alilouliza Geb, mara daktari wa Nanaa kupokea simu. Lyamu akatulia kidogo kama anayefikiria pakuanzia, Geb akatulia tu. Kisha akaanza. “Zipo njia mbili. Japo sio kwamba ndio atapona kabisa lakini itasaidia. Ya kwanza ambayo Nanaa anakataa au ambayo hajawahi kuikubali ni ile yakutoa huyo mtoto. Hapo atapona kwa haraka. Kwa kuwa mimba na matatizo aliyonayo sasa hivi ndio vinachangia kupandisha presha yake. Ata..” “Na ya pili? Maana hiyo najua haitakaa ikatokea. Nanaa hawezi kukubali.” Geb akamkatisha.

“Kuna dawa nimeshauriwa na daktari wa mambo ya moyo. Wamesema ni nzuri au zitakuwa salama kwake na mtoto pia, zinaweza kumsaidia. Japo ni garama sana. Ndio najiandaa kwenda kuzungumza naye. Ili..” “Naomba uzungumze na mimi.” Geb akamuwahi.

“Samahani Geb. Naelewa kwa sehemu mlipo wewe na Nanaa kwa sasa. Amenieleza kwa sehemu kile mnachopitia. Ameniambia  hampo tena pamoja. Na kama chochote kikitatokea kwake, na mtoto akapona, Frida au Fifi kama anavyomuita yeye, ndio anadhamana na huyo mtoto. Wanaonekana wamekubaliana kwa maandishi. Na amemuweka Frida kama mtu atakayeingia naye chumba cha kujifungua. Wamelipia garama za ‘private delivary’. Kwamba niwepo mimi muda wa kujifungua na nilazima Frida awepo kwenye hicho chumba atakachojifungulia. Ndiye mtu anayemleta kliniki pia.” Moyo wa Geb ulinyong’onyea kabisa. Akapooza.

“Kwa hiyo hatima yake kwa sasa naomba nikazungumze na yeye mwenyewe.” Daktari akaendelea. “Nimeelewa. Lakini unafikiri kama atakubali hizo dawa, anaweza kuruhusiwa lini?” Geb akauliza. “Wewe unamjua Nanaa. Sitashangaa nikamkuta ananisubiri hata sasa hivi hapo kwenye mlango wa wodini, aniage.” Geb akacheka kidogo. “Lakini kama angekuwa mgonjwa mwingine ungefanyaje?” Geb akaendelea kuuliza.

“Angeanzishiwa dawa mpya. Kisha akapewa siku hata mbili mbele zauangalizi akiwa hapo hapo hospitalini. Ili kujua kama dawa zinafanya kazi au la. Lakini kwa Nanaa utajua kama zinafanya kazi kwa kuwa hatanitafuta tena. Au zimemkataa kwa kuwa atarudi akiwa anakaribia kufa, huku ana masharti yake. Kwa hiyo kwa Nanaa, tutajua mbele ya safari. Ngumu kusema na kutabiri. Lakini Geb!” “Nakusikiliza.” “Safari hii Nanaa ni mgonjwa. Sio sababu ya mimba tu, lakini moyo wake umepanuka. Unakumbuka mara ya mwisho mlipokuwa naye hospitalini nilikutahadharisha madhara yakutofuata masharti ya zile dawa?” Geb akanyamaza. 

Akakumbuka wakati anamtoa Nanaa hospitalini baada ya kujifungua Magesa, daktari alimsisitizia kumfuatilia Nanaa kwa karibu sana. Kuhakikisha anatumia dawa kama alivyoandikiwa. Matokeo yake kesho yake tu alimuacha na kumpokonya kabisa watoto, nakumuongezea madhara zaidi. Alishindwa hata kumjibu dokta.

“Sasa moja ya madhara ya kukaa na presha ya juu sana bila kuitibu kwa muda mrefu, ni hayo. Moyo wa Nanaaa umeanza kusumbua. Kwa jinsi alivyozungumza na yule daktari wa moyo hakuwa hata akijua dawa zenyewe zilikuwa wapi. Kwa kifupi hakuendelea na matibabu yeyote yale.” Geb akakumbuka aliziacha kwenye gari lake. 

~~~~~~~~~~~~

Kumbukumbu ilimjia siku wanatoka hospitalini. Yeye ndiye aliyekwenda kuchukua dawa hizo na kulipia garama zote za Nanaa na Magesa. Akaenda kuzifungia dawa hizo mbele ya gari, kwenye dashboard draw, mbele ya kiti cha abiria. Jioni waliporudi nyumbani wakakuta watu wakiwasubiria. Sherehe ya kukaribishwa Nanaa na Magesa nyumbani pamoja na birthday ya Liv, vikachanganya. Akakumbuka Nanaa alikwenda kulala. Akamuamsha ili ale chakula ndipo ampe dawa. Wakati Nanaa anakula ndipo Malii akaingia na kusababisha maafa. Hakujali presha hiyo ya Nanaa hata baada ya kubakwa kwake, akijua wazi aliruhusiwa akiwa bado mgonjwa. Lakini alisisitiza mpenzi wake aruhusiwe tu, atahakikisha anafuata masharti ya daktari, atatumia hizo dawa na yeye mwenyewe Geb, akatoa  ahadi ya kumrudisha Nanaa hospitalini kila inapotakikana ili kumuona daktari wa moyo.

Ni kesho yake tu baada ya kumpa huyo daktari ahadi hizo, ndipo alipoondoka kikatili sana akimuacha Nanaa akilia sakafuni. Hakukumbuka dawa wala ugonjwa wa Nanaa, ila hasira kali juu yake. Hapo ndipo daktari anamkumbusha juu ya hizo dawa alizotakiwa kumpa Nanaa. Aliishia kuzinunua na kuzifungia kwenye gari.

Akajua kwa miezi hiyo sita, zitakuwa pengine zilishatupwa wakati ameenda kusafishiwa gari yake. Kwanza alishabadili aina ya gari alilokuwa akitumia. Lile alikuwa akilitumia mara chache sana anapokuwa na Nanaa tu. Lilikuwa ni lile gari lenye milango miwili. Lilitolewa pale alipokuwa akiishi Nanaa, na kuhamishiwa nyumba waliyorudi kuishi na mama yake na watoto, akalisusa hapo kwa kuwa lilimkumbusha Nanaa kila anapoingia humo. Akaona alitelekeze kabisa. 

~~~~~~~~~~~~

“Kwa hiyo mbali na ujauzito alionao, tayari Nanaa ana matizo ya moyo.” Daktari akamalizia. “Ameniambia unaweza ukawa na simu yake.” “Ninayo. Niliificha kwa makusudi ili apumzike. Ilikuwa ikiita nakuingia jumbe kila baada ya dakika. Ikabidi kuizima ili angalau alale. Ila leo nitampelekea vitu vyake vyote. Sijui kwa nini, lakini hisia zangu zote zinaniambia hatalala leo hospitalini! Ataondoka tu.” Geb akacheka kidogo. “Na mimi nitarudi huko baada ya muda mfupi sana. Sitachelewa.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~

Geb akarudi ndani akakaa pembeni ya Liv. “Unataka kunywa uji au maziwa?” Kimya. “Liv?” Hata hakugeuka kumwangalia baba yake. Akabaki kimya macho kwenye luninga. “Twende nikakubadilishe diaper.” Geb akaendelea. Baada ya sekunde kadhaa Liv akashuka pale kwenye kochi kuelekea chumbani kwao. “Tunaenda kwanza kuosha uso na meno.” Geb akaendelea kuzungumza naye akiwa nyuma yake. Mpaka anamalizia hiyo sentensi, Liv alishafika bafuni. Akamuosha vizuri na kumbadilisha nguo. Wakatoka.

Akarudi kukaa kwenye kochi. Geb akamfuata. “Naenda kumuona mama Liv, unataka twende wote?” Liv akamwangalia, akavuta mtandio wa mama yake vizuri. Akaushika nakurudisha macho kwenye luninga. Geb akafikiria kidogo. Akamvuta na kumbeba. “Pole Liv.” Liv akajiegesha vizuri pembeni ya shingo ya baba yake, akatulia. Geb akaona atoke naye. Akamchulia begi lake lenye vitu baadhi vyakubadilisha, akatoka naye, kuelekea hospitalini alikokuwa amemuacha Nanaa.

Katika swala la uelewa, Geb hakulitilia mashaka. Japokuwa hata miaka miwili hakuwa ametimiza, lakini Oliva alikuwa na uelewa wa hali ya juu. Hakuna aliyekuwa akizungumza naye kama mtoto mdogo. Eti zile sauti za kitoto, kwa Liv hawakumfanyia. Walizungumza naye kama mtu mzima, na yeye alielewa.

~~~~~~~~~~~~

Akiwa anaingia kwenye geti la hospitalini. Ilishakuwa saa tano asubuhi. Hakuwa akikumbuka cha ice cream wala chakula cha mgonjwa. Simu ya Nanaa ikaingia. “Ni mimi Nanaa.” Geb akacheka nafsini mwake. Alikuwa na namba yake, alipewa na Jeri. “Vipi?” “Nilipiga kukutaarifu kuwa ninatoka hospitalini.” Geb akakumbuka maneno ya Lyamu. “Nanaa!” Geb akashangaa. “Hapa nilipo nipo nasubiria dawa tu, niondoke. Nimempigia simu dada Fifi. Atakuja kunichukua.” “Subiri kwanza Nanaa. Umeruhusiwa au umeamua kuondoka?” Geb akauliza.

“Nina mambo mengi sana yakufanya Geb. Sina muda wakulala hapa Muhimbili.” “Uko wapi?” Nanaa akamuelekeza alipo. “Mpigie simu Fifi, mwambie mimi nitakuchukua. Ndio nipo hapa getini.” Nanaa akatulia kidogo, kama aliyeshangazwa na ujio mwingine tena wa Geb. “Nanaa?” Geb akaita. “Nampigia sasa hivi.” Wakaagana.

          Alimuona kwa mbali amekaa na mizigo yake yote, kuashiria hatarudi tena wodini. Akampigia simu. “Geuka.” Nanaa akageuka vizuri. Akamuona yupo ndani ya gari yake kubwa aliyokuwa akitumia Jeri kwa ajili ya watoto. Akampungia mkono. “Njoo.” “Bado sijapata dawa, Geb! Nasubiria waniite jina langu.” “Njoo mara moja tu.” Nanaa akaanza kutembea kumfuata. Wakakata simu. Kadiri alivyokuwa akiwasogelea, ndivyo tumaini jipya lilivyokuwa likijengeka moyoni mwake. Geb alisikia moyo unajaa furaha.

“Nilikwambia usihang..” “Mama!” Kabla Nanaa hajamaliza sentensi yake mara alipofika kwenye gari upande wa dirisha alipokuwa amekaa Geb, Liv aliyekuwa amekaa kiti cha nyuma, akamuona mama yake. “Liv wangu!” Nanaa akazunguka upande wa pili akafungua mlango. “Beba mama! Beba.” Liv alishaanza kulia. “Usilie. Ndio nakufungua nikubebe.” Nanaa akajaribu kutulia lakini akashindwa. Machozi yakamtoka. Akamtoa pale kwenye kiti chake, akamsimamisha pale pale pembeni ya kiti chake akamkumbatia. Liv alimbusu mama yake zaidi ya mara tano. Kichwani, usoni mwa mama yake alimpa hayo mabusu bila kuchoka. Geb akabaki akimshangaa Liv. Liv huyu siye wanaye ishi naye yeye na mama yake. Ni watofauti kabisa anapokuwa na mama yake.

“Tumbo linanguruma njaa. Hebu tulione.” Liv akanyanyua gauni. Mama yake akamtekenya, Liv akacheka. “Hili tumbo halina kitu Liv. Lazima ule.” “Nyonyo!” Nanaa na Geb wakacheka. “Nyonyo hamna tena. Imeisha yote. Lakini ninao uji na mtori. Tuanze kwanza uji.” Liv akatingisha kichwa kukubali. “Beba.” “Nakubeba Liv. Lakini nisubiri nakuja sasa hivi. Nimeacha mizigo yote pale…” “Mmhhh mama! Beba. Beba mama!” Liv akaanza kulia tena. “Nitarudi sasa hivi Liv! Sidanganyi.” Liv akazidi kulia akimshikilia mama yake. Nanaa akambeba. “Basi ngoja mimi nikafuate. Wewe kaa hapo mbele, umpakate. Hawezi kuamini tena.” Geb akateremka na kwenda kuchukua yeye hizo dawa. Nanaa akambeba huku akilia. “Pole mwanangu. Pole sana Liv.” Nanaa akaendelea kumbembeleza wakiwa wamekaa kiti cha mbele.

Akashangaa Geb amechukua muda kidogo kurudi. Maana ilikuwa ni kitendo chakuchukua kikapu na kugeuza tu. Akahisi aliyemwachia mizigo yake amwangalizie amemkatalia. Kumbe Geb alifika pale akakuta ndio na jina la Nanaa likitajwa akachukue dawa. Nanaa akampigia. “Nalipia dawa.” Geb akajibu mara baada yakupokea. “Acha usilipe. Nakuja sasa hivi. Ninazo pesa.” Nanaa akamuwahi. “Nimeshawakabidhi pesa. Usiwe na wasiwasi.” Geb akakata simu.

Akarudi baada ya kuchukua kila kitu. “Samahani Geb. Nakuingiza garama zisizo kuhusu. Naomba nipe pochi yangu hapo nyuma, pembeni ya kiti cha Liv, nikurudishie pesa yako. Najua ni garama sana.” Geb akakunja uso. “Kweli naomba nikulipe tu Geb. Ninazo pesa. Huna sababu yakunisaidia.” Alipoona bado Geb anamtizama tu, akageuka yeye mwenyewe akiwa bado amempakata Liv, akavuta pochi yake nakutoa wallet yake kutoka kwenye hiyo pochi, akatoa pesa. “Nashukuru.” Akawa anamkabidhi Geb. Geb akabaki akimwangalia. “Tafadhali naomba upokee Geb.” Nanaa akasisitiza huku ameshika ile hela.

          “Naomba upokee ili nimlishe mtoto.” Geb alikuwa amesimama nje upande aliokuwa amekaa Nanaa na mtoto wake. Akazunguka upande wake wa dereva bila kupokea pesa, akakaa kwenye kiti chake. “Nimuwekee nini huyo?” “Tafadhali naomba upokee Geb.” Nanaa alisisitiza akiwa bado ameshikilia zile pesa. “Naomba chukua tu. Ninazo pesa. Nina uwezo wakujitunza sasa hivi.” “Ndio maana na jina umebadili? Umerudi kujiita jina la mama yako, ukatoa Magesa. Na kumuweka Fifi kama mtu wako wa karibu? Yaani unaingia chumba chakujifungulia na Fifi!?” Nanaa akajua ameshazungumza na Lyamu.

“Naomba usinilaumu Geb. Unakumbuka mara ya mwisho unaniacha pale kwako uliniambia hutaki kuja kuiona sura yangu tena, na wala nisiwahi kukutafuta tena? Unakumbuka Geb?” Kimya. “Kana kwamba haitoshi, kuweka msisitizo wa ulichozungumza kwangu, mwezi uleule ukakata pesa uliyokuwa ukinipa ya matumizi yangu binafsi ya kila mwezi. Sikuwa nimepanga kubakwa wala kushika mimba. Yote yamenitokea bila hata kutarajia! Hapa ninapozungumza na wewe, sijui kaka alipo wala sijamsikia tokea siku ile. Hivi unavyoniona nilivyo, ndivyo nimemaliza. Sina ndugu wala rafiki.” Nanaa akaanza kutokwa na machozi.

“Mungu alinipa dada Fifi nikiwa nimelazwa hapa hapa hospitalini. Nililazwa pembeni yake.” Nanaa akamsimulia historia yake na Fifi kwa kifupi mpaka siku hiyo walipoonana hapo hospitalini, tena Fifi akimtukana Geb. “Niambie Geb, ningetakiwa kufanya nini kama sio kushika pale Mungu aliponiletea msaada? Najiitaje tena Nanaa Magesa!? Naanzia wapi mimi? Na mtoto atakayezaliwa wa Malii naye aitwe James Magesa?” Nanaa akauliza akiwa analia kwa uchungu sana. Geb akajua amebeba mtoto wakiume.

“Watu wote kwenye maisha yangu hawatabiriki! Wanatoka na kurudi vile wanavyojisikia wao. Sina mtu anayeweza kusimama na mimi kipindi cha shida yangu. Sasa hebu niambie Geb, nikifa chumba cha kujifungulia! Au hata nikaja kufa siku chache baadaye, huyu mtoto anakwenda wapi? Mimi niliangukia nyumbani kwa mama mkubwa. Yeye ataangukia wapi? Ilikuwa nilazima kumtafutia pakwenda. Na imani ikaongezeka kwa dada Fifi kwa kuwa kwanza hana familia, halafu akamtawala mwanangu hata kabla sijamuomba. Anamsubiria huyu mtoto kama ulivyomsikia leo asubuhi.” Geb akabaki kimya. Akageuka pembeni akiangalia nje ya dirisha. Nanaa akaziweka zile pesa pembeni yake. Akajifuta machozi. Akatulia kwanza.

“Naomba unimiminie uji, nimlishe kwanza ndio tuondoke. Anaonekana ana njaa.” Geb akamimina uji na kuanza kupoozesha. “Geb!” Nanaa akamwita, Geb akamgeukia. “Nakushukuru sana, kuniletea Liv. Nahisi ndio dawa pekee nilihitaji leo. Nimefurahi sana.” “Na mdogo wake naona na yeye amenibadilikia! Nimemkuta analia sana. Amekuwa mwekundu kwa kulia muda mrefu.” “Ungemleta tu na yeye.” “Unatakiwa kupumzika Nanaa!” “Napumzika vipi huku najua wanangu hawana furaha, Geb? Natoa wapi hilo pumziko?” “Kumbe ningejua nisingekwambia!” “Hapana. Ni heri umeniambia, ili nijue chakufanya. Kama sio kuwaona, basi kuwaombea. Nashukuru.” Geb akamkabidhi uji.

“Liv mama, usilale bila kula. Amka.” Nanaa akambusu. “Anasinzia.” “Ameamshwa na kaka yake. Alikuwa akilia sana.” “Pole mama eeh! Kaa vizuri ule.” Liv akambusu mama yake, akajirudisha kulala. “Namimi nakupenda Liv. Haya kaa ule kwanza.” Akajiegemeza kwa mama yake akaanza kula. “Naomba na wewe ule, Geb.” “Na njaa inauma kweli. Asubuhi nilijivunga nikijua nitakula nikifika nyumani, lakini sikukuta hata uji wangu.” “Pole. Kula kitu chochote humo. Nikifika nyumbani mimi nitapika tena.” Nanaa akajiuliza huku akiwaza moyoni. “Kwa nini huyo mke aliyemsikia ametafutiwa Geb, hakumpikia? Au ndio alikuwa akibembeleza mtoto?” Nanaa akawaza wakati akiendelea kumlisha Liv, na Geb akila.

~~~~~~~~~~~~

Liv alimaliza kula bila shida. Akamfuta vizuri. Akabaki akimwangalia. “Unataka kulala?” Liv akamwangalia mama yake. “Macho hayo yamejaa usingizi. Lala.” Liv akalala wakati mama yake akimpapasa kama kawaida yake. “Anapenda kupendwa huyo! Hivyo unavyomfanyia anapenda kweli ndio maana anakukumbuka.” “Jifunze na wewe umfanyie.” Nanaa alitoa ushauri. “Anaakili huyo. Muone hivyo hivyo. Hakubali mtu amshike hivyo ila wewe tu.” Nanaa akambusu, akaendelea kumbembeleza.

Alipolala kabisa, akamfunga kwenye kiti chake akarudi kiti cha mbele, pembeni ya Geb. Akatulia kidogo. “Geb!” Akamuita. Geb akamgeukia. “Sasa hivi nataka kwenda nyumbani. Tumepata oda kubwa siku ya kesho. Nataka nikasaidiane na kina dada Fifi, ili kukamilisha.” Geb akabaki akimtizama. “Naweza kumuachia dada Fifi na huyo msichana mgeni wafanye peke yao pengine nipumzike. Lakini nazitaka sana hizo pesa kabla sijajifungua. Nataka nikusanye pesa yakunisaidia kipindi hicho nipo na mtoto nyumbani. Nitajipa mapumziko ya kama mwezi mmoja, angalau mpaka mtoto achangamke, ndipo niendelee na biashara na kutafuta kazi. Lakini kwa hii miezi mitatu iliyobaki, nataka nijitume sana. Ili nisiishiwe katikati.” Nanaa alijieleza vizuri sana, kifasaha.

Geb akageukia dirishani akafikiria kidogo, akamgeukia. “Hivi sasa hivi mtoto ambaye umebaki ukimfikiria ni mmoja tu? Huyo aliyekuwepo tumboni?” Nanaa akakunja uso. “Eti Nanaa?” Nanaa hakuwa ameelewa. “Hivi umesikia neno lolote nililokwambia juu ya Magesa na Liv? Unaona afya ya Liv ilivyo?” Kimya. “Nanaa?” Geb akaita tena. 

“Naona na nimekuelewa Geb. Nitajitahidi kugawa muda.” “Kwa hiyo hivi unavyoniambia ni kwamba, umeshamalizana na Liv. Umeshamnywesha uji. Niondoke naye. Akalale, akiamka alie tena mpaka kesho, nikuletee tena, umyweshe uji, niondoke naye tena, wakati wewe unauza sambusa?” Nanaa akawa hajui tena anatakiwa afanyaje wakati alinyang’anywa watoto.

“Unakumbuka kitu chochote nilichokwambia juu ya Magesa?” “Nakumbuka Geb, lakini sijui natakiwa nifanye nini?” “Kweli Nanaa? Nakwambia mtoto analia sana, wewe unaniambia unataka ukauze sambusa ili upate pesa! Kweli?” Nanaa akaona machozi yanamtoka. “Hivi unawataka tena hawa watoto au ndio umeniziria? Na wewe umeamua iwe zamu yako, unikomoe? Usipokee msaada wangu tena, uniachie watoto. Hata wakiteseka, haikuhusu tena kwa sababu nilikupokonya na sasa hivi mtoto anayejaliwa ni mmoja tu. Liv na Magesa hawana tena maana.” “Unavyonifanyia sio haki Geb! Sio sawa.” Nanaa aliongea huku akilia.

“Kwa hiyo unataka usawa na mimi? Na wewe ukasirike kama nilivyokasirika mimi. Uweke hasira mbele, utafute kunikomoa kwa kuwa nilikukosea! Tuendelee kutesa watoto. Halafu wewe ukimaliza, na mimi nitafute tena kosa lako, nikulipize.” “Geb!” Nanaa akashangaa, asielewe. “Ndicho unachotaka kukifanya, kwa kuwa unaona nilichokifanya mimi nikizuri sana. Kimeninufaisha mimi mwenyewe. Ndio maana afya yangu nzuri. Nimependeza sana. Na nikanufaisha watoto pia. Ndio maana wanaendelea vizuri. Sasa hivi ni zamu yako. Unikomoe.” Geb akambadilikia Nanaa.

“Uliniudhi Nanaa! Ukweli ulinikosea sana. Tena baada ya kukusihi uwe unaniambia ukweli. Nilikwambia hata kama unajua huo ukweli utaniumiza kwa kiasi gani, nilikuomba uniambie ukweli tu kuliko kunidanganya. Haya, yakatokea yakutokea. Unanijua kabisa ninatatizo la hasira. Nimefanya maamuzi mabaya, si kwamba yameathiri tu watoto! Mimi mwenyewe nipo kama mgonjwa niliyekimbia hospitalini. Najirudi kwako, nikiwa na watoto, na wewe unanipa mipango yako yakunionyesha unamaisha yako. Hata kama mimi hunitaki tena, ndio nakuuliza, na hawa watoto wawili pia huwataki tena?” “Nawataka Geb. Tena nawataka kwa garama yeyote ile, nawataka.” “Ki vipi?” Geb akauliza.

“Niambie Nanaa. Unampango gani na hawa watoto? Nimesikia mipango yako kwa James au Jimmy. Mpaka umemtafutia mtu wakumchukua ukifa. Sasa naomba kujua mipango ya Liv na Magesa.” Nanaa akajifuta machozi, akatulia kabisa na kuanza kufikiria akijieleza kwa makini. “Inategemea utakuwa ukiwaleta saa ngapi na kwa muda gani. Hapo ndipo nitajua jinsi yakujipanga. Lakini nakuhakikishia Geb, wanangu wanakuja kwanza ndio mengine.” Nanaa akajibu.

“Nikiamua kukupa kabisa? Yaani nikaamua wewe ndio uishi nao. Utafanyaje na biashara hiyo uliyoanza? Si utashindwa au utaanza kuwaona mzigo?” “Sitashindwa kuwa na wanangu Geb. Na ninakuhakikishia sitawashindwa na wala sitawaona ni mzigo. Wewe nipe kwa majaribio hata ya siku tatu tu, utaona.” “Hawa watoto wanahitaji uangalizi wa masaa 24, Nanaa. Mama mwenyewe kazi zake zote zimesimama tokea siku anawachukua hawa watoto. Mpaka juzi nimemuonea huruma nakujisuta moyoni, nikamwambia atoke kidogo. Nikabaki nao nyumbani. Hawa watoto tulizaa karibu karibu na ni jukumu letu. Kama wewe unaingia kwenye biashara kama mimi, itabidi mimi nijipange upya. Lakini nimekataa, na nimejionya, hawatalelewa na mtu mwingine tena isipokuwa mimi au wewe kuhusika moja kwa moja. Nakiri nilizidisha hasira, nakuchukua maamuzi yaliyowaumiza watoto. Lakini nimekusudia kubadilika. Kama wewe upo busy basi itabidi mimi nihamishie ofisi nyumbani kwa muda, mpaka angalau wakue kidogo.” Nanaa akavuta pumzi nakuzishusha. Geb amejirudi. Amekuwa muwazi bila kificho.

“Basi naomba mimi mwenyewe niwalee, lakini unisaidie pesa kidogo. Sio kwa ajili yangu mimi. Ni kwa ajili yao tu. Kwa ajili ya chakula chao, mavazi na kama ikitokea wanaugua, basi niwe nina pesa za matibabu mazuri na ya haraka. Ila malazi ninapo sehemu yakuwahifadhi. Nilishamlipa dada Fifi kodi ya miezi sita mingine. Nilimpa miezi 6 ya kwanza. Kabla haijaisha, nikamuongezea mingine 6. Kwa hiyo pakuishi hapata sumbua. Nipe miezi hata mitatu tu, uangalie. Na si lazima ukawa ukinipa mimi pesa. Wanunulie tu vitu wanao, uwe unaniletea. Hamna haja yakunipa pesa kabisa.” “Sasa na wewe utaishije?” Geb akauliza.

Nanaa akafikiria tena kwa haraka na kujibu. “Mimi nitafanya shuguli zangu kama kawaida. Nitakuwa nikipika usiku wakati watoto wamelala, asubuhi wanaenda kusambaza, mimi nabaki na watoto.” Akamuona Geb amenyamaza. “Au nimekosea? Wewe nikosoe chochote juu ya huo mpango wangu, nitafanya tu. Ilimradi niwe na wanangu.” Geb akaonekana hana hoja. “Ngoja nifikirie.” Nanaa anaye akanyamaza. 

Walikaa pale kwa muda, mwishowe Geb akawasha gari. “Naomba nielekeze huko unakoishi sasa.” Geb akaondoa gari. “Geb!”  “Naam!” Geb akaitika. “Najua umeniambia unafikiria, lakini naomba leo ukinishusha nyumbani, uniachie Liv kidogo. Angalau akiamka leo, akutane na sura yangu.” “Sawa.” Geb akakubali bila shida. “Nilikuwa bado sijamaliza.” Geb akamtizama.

“Naomba urudi nyumbani, ukamwangalie Magesa. Kama bado analia tumpeleke hospitalini.” “Kwa hiyo kama amenyamaza, ndio inakuaje?” “Nashindwa chakusema Geb. Umeniambia unafikiria mpenz…” Nanaa alitaka kusema mpenzi wangu. Akasita. Wakanyamaza kidogo. “Lakini Geb, hata ukiniambia unishushe sehemu, nikusubiri wakati unaenda kunichukulia mwanangu, nitakushukuru sana.” “Unamaanisha sasa hivi?” “Kabisa. Mimi niache hata kituo cha daladala pale karibu na kwako, nitawasubiri wakati unaenda kumchukua Magesa.” Akaona gari inageuzwa, kutafuta njia ya Tabata. Nanaa akajua hata wao wamelemewa. Akawacheka moyoni nakujiambia, debe limevuja, nafuu kwake mchukuzi. Anapata wanae wote wawili bila shida.

Debe Limevuja.

“Utataka nikuchukilie nini?” Geb akamuuliza mara alipokaribia nyumbani kwake. “Nguo ndio kitu cha muhimu. Mengine yote, sio lazima. Ila naomba nishushe hapo soko dogo ninunue vitu vichache vyakupika wakati unaenda kumchukua kaka.” Geb akamshusha, yeye akaondoka na Liv akiwa amelala. Wakati anakaribia nyumbani, akaona mama yake anampigia simu. Akapokea. Akasikia sauti ya Magesa, akilia. “Huyu analia sana, nizaidi ya nusu saa sasa. Na homa imeanza kuwa kali. Naona nimpeleke tu hospitali.” “Nakuja, nipo hapa karibu tu. Nitayarishie begi lake, mimi nitampeleka.” Geb akakata simu.

Hapo hapo akampigia Nanaa. “Naomba usinunue vyakula. Mama anasema Magesa homa ni kali, inabidi tumpeleke hospitalini. Nisubiri nakuja sasa hivi.” “Sawa.” Nanaa akatoka barabarani. Hata dakika 10 hazikuisha, akaona gari ya Geb. Akasogea. Wakati anafungua mlango, akasikia kilio cha Magesa. “Naomba nimshike. Asilie peke yake mpaka hospitalini.” Magesa alikuwa amefungwa kwenye kiti cha nyuma. Pembeni ya dada yake. “Kaa basi, nimfungue. Nitakupa.” Gafla wakajikuta wamekuwa wazazi wakujielewa. Akili zimewarudia.

Magesa alikuwa akilia kama kengele. Geb akamtoa kiti cha nyuma, akamkabidhi mama yake pale mbele. “Pole baba. Pole sana. Nini kinauma?” Nanaa akaanza kumbembeleza nakumuongelesha kama ataelewa. Akajifunga yeye mkanda, akamlaza kifudi fudi tumbo lake mapajani huku akimsugua mgongoni. Akaanza kutoa hewa. “Pole Magesa mwanangu. Ni tumbo ndio linauma?” Magesa alianza kupunguza sauti kama ambaye ameanza kupata nafuu, huku baba yake anaendesha.

“Haya, mwangalie mama.” Nanaa akamnyanyua. “Pole sana.” Akambusu na kumuweka kifuani, akamkumbatia vizuri huku akimbembeleza. Mpaka wanafika hospitalini, Magesa alishalala. Geb alikuwa kimya kabisa. Mawazo yalikuwa mbali, hata hakuwa akijua ni muda gani huyo mtoto alinyamaza.

Baada ya vipimo vingi, Magesa akagunduliwa ana UTI. Ugonjwa ambao mara nyingi unachangiwa na kinyesi, kuingia njia ya mkojo. “Inamaana alikuwa hasafishwi vizuri!?” Wazazi hao wakajiuliza kimya kimya. Nani wakulaumiwa? Geb au bibi? Labda mama mtu! Hakuna ajuae. Ilibidi aanzishiwe matibabu kwa haraka, na kwakuwa homa ilishakuwa kali sana, ikabidi alazwe ili waishushe kwa haraka isije leta madhara zaidi. Wanafanyaje na Liv? Lazima wachukue chumba chao peke yao. Watajua wao wenyewe wakishapewa chumba.

Uzazi Ni Kazi.

Nanaa akakabidhiwa chumba yeye na wanae. Magesa akapewa dawa yakushusha homa, akamlaza kitandani upande mmoja, upande mwingine Liv. Wakabaki wamekaa yeye na Geb. Wazo likamjia Nanaa. Akampigia simu Fifi. “Naomba niletee chakula huku hospitali ya Agakani.” “Wewe Nanaa! Asubuhi ulikuwa Muhimbili, ukaniambia umeruhusiwa, nije nikufuate. Mara ukaniambia nisije tena, umepata lifti ya Geb. Sasa hivi upo hospitali ya Agakani! Wewe mtoto vipi?” “Wakati tupo njiani tunarudi nyumbani, Geb akapata simu kuwa Magesa anaumwa. Ikabidi kumfuata, ndio tumelazwa hapa hospitalini. Sasa nataka chakula cha Liv. Na yeye yupo hapa. Nataka akiamka ale. Ule mtori watokea asubuhi, sasa hivi utakuwa umeharibika.” “Umeona akili yako ikikurudia unavyokuwa mama mzuri?” Nanaa akacheka.

“Ona sasa hivi unaweza kulea na wanao! Haya, na wewe unataka kula nini?” “Chochote kile dada yangu.” Geb akamgusa. “Subiri dada.” Nanaa akamgeukia Geb. “Wewe nitaenda kukununulia.” Geb akaongea kwa sauti ya chini. “Kwa nini usimuache dada Fifi akaleta, ili wewe upumzike?” Nanaa akamjibu Geb. “Ni lini mara ya mwisho umekula mbuzi wa kuchoma?” Nanaa akacheka sana. Fifi akasikia. “Na unibakishie Nanaa. Sio tena ule huyo mbuzi peke yako.” “Dada Fifi kwa nyama!” “Ndiyo. Sasa kaka mdogo naye atakula nini?” “Wamesema wataniletea chakula chake akiamka tu. Sasa sijui watamletea nini!? Naomba na uji mzuri. Ili akishindwa chakula cha hapa, nimuongezee uji. Lakini pole dada yangu, nakusumbua!” “Wala usijali. Nakuja sasa hivi. Ngoja nikupikie, nilete kabla hawajaamka.” “Ndio maana nakupenda.” Fifi akacheka nakukata simu.

~~~~~~~~~~~~

Geb akatoka. Baada ya muda akarudi na nyama ya mbuzi yakuchoma. Nyingi pamoja na chips na ndizi zakuchoma. Soda 4, na maji ya kunywa. “Narudi nyumbani kuoga, nibadili nguo. Nitarudi kulala na nyinyi.” “Naomba tuombe kwanza Geb. Mungu ametukutanisha pamoja. Japo ni hospitalini, lakini ipo haja yakushukuru nakumuombea Magesa.” Nanaa na Geb niwazuri sana wamaombi wanapokuwa kwenye shida.

Wakashikana tena mikono wakaomba. Nanaa alitubu kwa popote yeye na Geb walipozembea kwa watoto hao ambao Mungu aliwapa kwa upendo. Akashukuru kwa nafasi nyingine Mungu aliyowapa na watoto hao. Kisha akaomba amani na uponyaji kwa Magesa na Liv. Waliomba mpaka kila mmoja wao akajisikia vizuri. “Amina.” “Amen! Asante kwa maombi mazuri, Nanaa. Nitarudi sasa hivi.” “Nashauri upumzike kidogo Geb. Kalale kidogo, ndipo urudi. Jua watoto wapo salama, na mimi nipo. Naomba ulale kabisa. Hata ukija kwa kuchelewa, hamna shida. Ila unahitaji kupumzika.” Geb akafikiria kidogo, akatoka.

Kuliko Ungua Mpini.

Mama G akashangaa Geb anaingia bila watoto. “Vipi!?”Akamuuliza akisikika na wasiwasi. “Magesa amekutwa na UTI. Wamemlaza.” Geb akajibu kwa kifupi. “Nilivyokuwa nikijitahidi kumbadilisha diaper! Sijui kapataje huo ugonjwa! Sasa umewaacha na nani?” Mama G akauliza tena huku akijisikia vibaya. “Wapo na mama yao.” Geb akajibu nakuingia chumbani kwake. Mama G akabaki ameduaa kama dakika tano. Hajui aseme nini. 

Ndipo akamfuata Geb chumbani. “Asubuhi nililemewa nikakusahau chakula. Ila nimekupikia. Uje kula.” “Nataka kama lisaa limoja tu lakulala. Nitakuja kula kabla sijarudi hospitalini.” “Niwapikie nini huko?” “Usipike kitu chochote. Wewe pumzika tu.” Geb akajirusha kitandani vile vile na viatu akalala. Alijirushia hapo kitandani saa 8 mchana, akaamka saa 11 jioni. Akaingia kuoga harakahara, akatoka akiwa na haraka.

“Naomba tuongozane.” Mama G, alikuwa akisubiria kwenye makochi. “Naomba uje kesho mama. Leo pumzika tu.” Mama G akajua hatakiwi. “Basi kula kwanza.” Geb akafikiria kidogo, akarudi kukaa. Akatoa simu nakumpigia Nanaa. “Vipi?” “Safi tu.” Nanaa kajibu. “Nilipitiwa na usingizi.” “Ndio vizuri umepumzika. Daktari alirudi tena, wameona wamwanzishie dripu ya maji. Wamemuwekea na dawa humo humo. Wameniambia itamsaidia kwa haraka, hata akikataa kula itamsaidia. Kwa hiyo amerudi kulala. Halafu niliwaomba waniletee kitanda cha mtoto. Crib. Wameleta. Naona dada nitamlaza hapo.” “Anafanyaje sasa hivi?” “Amekula vizuri kweli! Nimemuogesha, yupo hapa tumepakatana, anaangalia cartoons zake.” Geb akatulia kidogo.

“Sasa si utakuwa na wewe umechoka?” “Hapa nimejilaza kwenye kochi. Dada amejiegemeza kwangu huku anaangalia tv. Nilikuwa nasinzia. Yaani wewe ndio umeniamsha.” “Pole. Nikuletee nini?” “Nimeshiba. Dada Fifi alikuwa hapa. Akaongeza tena vyakula. Tumekula ndio akaondoka. Nipo tu sawa. Wewe pumzika. Tutaonana hiyo kesho.” Geb akakata simu. Akala vizuri akashiba, akatoka baada yakumuaga mama yake nakumuelekeza hospitali na chumba alicholazwa Magesa.

Njiani akampigia simu Grace. “Naomba uendelee kushikilia kazini. Nitakuwa hospitalini na Magesa. Amelazwa.” “Poleni Geb. Basi mwambie mama aniambie nini anataka niwaletee hospitalini.” “Mama yupo nyumbani.” “Kwa hiyo upo mwenyewe hospitalini!?” Grace akaendelea kuhoji akimuhurumia kaka yake. “Sasa hivi wote wawili wapo na mama yao huko hospitalini. Mimi ndio naenda huko sasa hivi.” Grace akapatwa na kigugumizi. “Mama yao Liv na Magesa au mama yetu sisi?” Grace akahoji zaidi. “Wapo na Nanaa.” Grace akanyamaza, Geb akakata simu.

Baada ya muda Grace akapiga tena simu. “Wamelazwa wodi gani?” Geb akamuelekeza hospitali waliyopo na chumba. “Lakini naomba labda uje kesho. Naomba leo tuwaache kwanza. Hasa Liv. Anataka muda na mama yake.” “Sawa.” Geb akakata simu.

~~~~~~~~~~~~

Liv alikuwa akicheza mwilini mwa mama yake huku akiangalia cartoons zake wakati baba yake anaingia. Nanaa alikuwa amejilaza chali kwenye kochi. Liv alipomuona tu baba yake ameingia, akajificha nyuma ya mama yake. Nyuma kabisa. “Wala sikuchukui. Nataka tu unisalimie. Njoo.” Liv hakutoka hapo nyuma. “Njoo uchukue ice cream.” Liv alikataa kabisa. Akaendelea kujificha. “Nimekuletea na wewe ice cream.” Nanaa akakaa. “Hata hivyo ameshiba. Amekula sana.” Nanaa akatetea.

Mama G Na Grace.

Asubuhi wakati Nanaa na Geb wanaomba. Mama G na Grace wakaingia. Walimkuta Geb na Nanaa wamepiga magoti pembeni ya kitanda kingine kidogo alichokuwa amelazwa Magesa. Hawakugeuka wakati wanaingia. Wakaomba kama dakika tano mbeleni, ndipo wakamaliza. Geb akamsaidia Nanaa kusimama. Ile kuamka, mama G na Grace ndipo wakagundua Nanaa ni mjamzito. Wakabaki wameduaa. “Shikamooni.” Nanaa akasalimia, nakuchukua kipochi chake akatoka. Hata yeye aliwaona jinsi walivyomshangaa.

Alipotoka tu, Geb akamfuata. “Nanaa!” “Nitarudi Geb. Nawapa nafasi na watoto.” “Naomba usiondoke tafadhali.” Geb alisisitiza wakiwa wamesimama nje tu ya mlango. “Hawa watu wamekuja kuona watoto, sio mimi. Ndio nawapa nafasi au uhuru na watoto. Watakapo ondoka, unaweza kunipigia simu, nikarudi. Sitaki uwepo wangu uwe kero.” “Haiwezekani Nanaa. Naomba uje. Wewe sio kero.” Nanaa akakunja uso akageuka vizuri.

“Geb! Naweza nikawa vitu vingi, lakini mimi sio mjinga. Tafadhali, naomba watoto wangu wakiamka na ndugu zako wakiondoka, nipigie simu nitarudi.” “Nanaa! Si tumetoka kuomba sasa hivi!? Unafikiri maombi yetu yatajibiwa vipi kama unashindwa kusamehe.” “Nani amekosa ambaye anahitaji msamaha wangu na nimeshindwa kumsamehe!?” Kimya.

“Hakuna aliyenikosea na nikashindwa kusamehe Geb. Iwe nimeombwa msamaha au la. Huwa nasamehe kwa ajili yangu mimi mwenyewe. Sina kinyongo na mtu. Ila nimeijua nafasi yangu na nimeamua kutojidanganya tena. Hao wote wawili waliniacha kitandani nikilia maumivu ya kubakwa wakati nimetoka kujifungua! Grace alishindwa hata kuja kunipa pole, au hata kuja kuangalia niliumia kiasi gani ajue jinsi yakunisaidia au hata kunisitiri. Alibeba watoto wake, akaondoka. Akajua mmenipokonya watoto wangu, yeye anayejua uchungu wa watoto, akaniona nilivyoteseka, alinyamaza kimya. Ndio namuona leo, ananishangaa na mimba yangu.” Nanaa akaendelea

“Mama yako ndio sitaki kurudia matusi yake. Na wewe ulikuwepo. Yeye ni mwanamke kama mimi. Anajua uchungu wa kuzaa. Nilimwamini kwa kumsogeza karibu yangu. Nikampa moyo wangu. Akatumia uyatima wangu kama fimbo yakunichapa siku nilipokuwa na shida. Hata kama ningekuwa mbaya kiasi gani, kama siku ile mimi ningekuwa Grace, nimefanyiwa vile, kweli angenitukana kiasi kile na kunichukulia wanangu? Nililia usiku kucha na yeye ananisikia. Asubuhi ananipokonya watoto niliowazaa kwa kumwaga si damu tu, ila uhai wangu! Watoto nilio wazaa kwa kukubali kufa! Ananiambia mimi, mama yao ni mchafu, sistahili kugusa wanangu!”

“Hakika nimesamehe, Geb. Na nimemuachia Mungu. Sina kifua chakubeba uchungu wa ubaya mlio nitendea. Sina. Na ndio maana nimeyaweka yote madhabahuni kwa bwana. Sina neno lolote juu yenu, Mungu atashugulika na nyinyi wala si mimi. Lakini ndugu zako sio watu watakaorudi kuwa sehemu ya maisha yangu.” Nanaa aliongea taratibu bila jazba, lakini alisikika.

“Kama Grace alivyoamua kuniacha siku ya msiba wangu, hakutaka kusumbuka na mimi. Basi. Naahidi hatakaa akarudi kwenye maisha yangu. Mama yako analilia pesa zako! Anasema kinachonisumbua ni pesa zako! Amenitukana matusi ya nguoni siku ile ya maombolezo yangu! Akachukua watoto wangu bila hofu mbele za Mungu! Mtoto wangu akiwa analilia ziwa langu! Hivi unajua jinsi nilivyoteseka na yale matiti? Yaligeuka kuwa kama majipu Geb. Maziwa yalikuwa yanajaa, mwanangu anashindwa kunyonya, kwa sababu mnaniadhibu mimi! Niliumwa mpaka homa, kwa ajili yakumkatili mwanangu. Alimpa mtoto wangu maziwa ya kopo, akijua ni kitu napingana nacho tokea kwa Liv. Lakini aliamua kufanya ili kunikomoa mimi.” Nanaa alifuta machozi.

“Siku ya shida yangu, alisimama kama mtesi wangu. Aliwatesa wanangu na mimi. Watoto wadogo wasio na hatia aliwatenga na mimi kwa hila kabisa. Huku akiwatafutia mama mwingine! Lakini Geb, hawa watoto ni wangu. Tena Mungu alinipa mimi kwa upendo tu. Si wewe Geb, wala mama yako mtakao weza kunipokonya. Mungu ambaye ni Baba wa yatima. Aliyenipa mimi hao watoto, ndio atakayenipigania. Atawarudisha mikononi mwangu kwa kuwa sikuwatenda ubaya mkubwa wa kiasi hicho, ila tu nilitaka kutunza mahusiano yenu, yangu na Malii. Hakuna cha ajabu sana nilichokifanya ambacho nyinyi wote watatu hamkuwahi kufanya, chakustahili adhabu mliyowaadhibu wanangu Geb. Mmemnyima Magesa mapenzi yangu, kwa makusudi. Liv wangu ananililia mchana na usiku, mnamwangali tu!  Hamjali kilio cha mwanangu, eti kwa kuwa sikusema yote yaliyotokea kati yangu na Malii!” Nanaa akapata jukwaa.

“Hakika nimewasamehe. Mungu wangu anajua. Sina nguvu ya kupambana na nyinyi. Kwanza yeye Mungu ameweka mkono wake juu yenu katika kila eneo la maisha yenu. Kwenye fedha, Mungu amewafanikisha. Utakatifu, amewafanikisha. Hamna dhambi. Nyinyi ni wema sana. Ndio maana hamna hofu na watu kama sisi na mnaweza kuhukumu kwa wepesi. Siwezi kushindana na nyinyi. Nilimwachia Mungu wangu ambaye alinileta hapa duniani, akaninyima yale aliyowabariki nyinyi. Hakika nimemuachia Yesu. Yeye ndio atashugulika na nyinyi, wala si mimi. Sina kinyongo na hata mmoja wenu. Lakini hawatakaa kurudi kuwepo kwenye maisha yangu. Tutaonana kama hivi ikitulazimu. Na kama ni wanangu, nitalea kwa upendo wote, na unyenyekevu pale mama yako ATAKAPO KURUHUSU unipe niwalee. Lakini si vinginevyo.” Nanaa akaondoka.

Ujumbe uliwafikia vizuri sana. Nanaa alihakikisha haamshi wanae, lakini wengine wote ujumbe unawafikia. Na kwa hakika ulifika. Geb alibaki amesimama pale mlangoni. Hajui aingie ndani au atoke kwa muda. Akabaki amesimama pale, mpaka akamsikia Magesa ananung’unika. Akaingia. “Vipi baba!” Geb akamsogelea. Akamshika kichwa. “Vipi homa?” Mama yake akauliza. “Bado ipo juu. Lakini walituambia akipata dozi ya leo pia, inaweza kushusha homa.” “Poleni Geb.” Grace aliongea kwa upole. “Atakuwa sawa tu. Eti Magesa? Pambana baba. Pambana tutoke hapa.” Geb alimbembeleza kwa kumshika shika.

“Nilileta chakula chenu wote. Mpaka uji wa dada.” Mama G akaongeza. “Usihangaike tena mama. Yupo dada anayeishi na Nanaa, naona ndiye anayemuhudumia Nanaa. Tokea Nanaa mwenyewe alipokuwa hospitalini. Ndiye..” “Kwani Nanaa alikuwa amelazwa?” Grace akamkatisha. “Yaani hata kwake hajarudi. Alikuwa amelazwa hospitali ya Muhimbili karibu ya mwezi. Nimemtoa hapo, na kuhamia hapa kumuuguza Magesa. Kwa hiyo hajapumzika.” “Alikuwa anaumwa nini?” “Presha.” Wakanyamaza.

“Kwa hiyo usingaike kupika. Huwa anamwagiza huyo dada chakula anachotaka Liv ale, ndio anapika halafu kikiletwa anakula naye. Kama leo alishapita alfajiri sana. Ndiye aliyetuamsha. Ameshamletea chakula cha asubuhi, na amemuagiza       chakula cha mchana pia. Kwa hiyo usisumbuke. Tumia huu muda kupumzika, mama.” Mama G, akanyamaza.

Magesa akaanza kulia taratibu. Geb akaendelea kumbembeleza lakini akazidi kulia mpaka Liv akaamka pale kwenye kitanda. Akafungua macho. Akawaangalia kwa zamu watu wote waliokuwepo pale ndani. Hakumuona mama yake. Akakaa. “Njoo nikubebe.” Bibi yake akamsogelea. Liv    akajivuta mpaka mwisho kabisa wa hicho kitanda chake kama anamkatalia. Tayari machozi yakaanza kumtoka. “Mama anakuja Liv. Wala usilie.” Geb akamuwahi, lakini alishachelewa. Liv alishavuta mtandio wake, akajifunika kabisa huku kamekunja miguu yake.

“Mimi naona tuondoke mama, ili Nanaa aje awe na watoto wake. Inatosha.” “Kwa hiyo naruhusiwa kuja kuwaona watoto?” Mama G akauliza. “Tokea ujauzito ule wa Magesa mpaka leo, presha inamsumbua sana Nanaa. Mnakumbuka ilibidi kumuombea atolewe tu hospitalini baada ya kujifungua Magesa, ili arudi nyumbani awe na watoto? Walimruhusu kwa kuwa niliwapa ahadi yakumrudisha hospitalini mara kwa mara kwa vipimo na kumuona dakitari. Huku nikiwaahidi nitasimamia unywaji wake wa dawa. Wote niliwaambia. Mnakumbuka?” Kila mtu kimya.

“Ndio yakatokea yakutokea. Tukamuacha bila uangalizi wowote. Hata dawa alizokuwa ameandikiwa atumie, niliondoka nazo. Nikazifungia kwenye ile gari ndogo. Jana ndio daktari wake alinikumbusha. Na mbaya zaidi, hata Nanaa hakujua kama alitakiwa kutumia hizo dawa. Alipoulizwa na daktari kama alikuwa akitumia zile dawa, hakuwa hata akijua huyo daktari alikuwa akizungumzia nini, kwa kuwa mimi ndiye niliyekuwa nimechukua maagizo yote ya dawa na dawa zenyewe. Daktari wake ameniambia kutotumia zile dawa na Nanaa kuendelea kuwa na pressure ya juu kwa muda mrefu bila kuitibu, imesababisha madhara makubwa zaidi kwenye moyo wake.”

“Hapo alipo moyo wake umepanuka. Presha ipo juu sana. Dawa ya kwanza na ya haraka inayoweza kumsaidia kwa sehemu, nikumtoa huyo mtoto. Lakini amekataa. Daktari anayemtibu sasahivi ameniambia kwa hali aliyonayo sasahivi hawezi kuzaa tena kwa kawaida. Akifanikiwa kufika hiyo siku zakutimia umri wa kukaa mtoto huko tumboni, kabla uchungu haujaanza, watamfanyia upasuaji. Hana uwezo wakusukuma tena mtoto. Sasa kuna dawa amepewa ndizo anatumia sasa hivi na ndizo zinamfanya aweze kuwepo hapa na watoto na kumsogeza mpaka hizo siku za kujifungua. Naomba tumuache kwanza.” “Mmmh!” Mama G akaguna. 

“Naomba mpe pole. Mtie moyo mwambie Mungu atamsaidia atapona, na kumrudishia muda wake wote aliopoteza na wanae. Na wewe msaidie ili atulie na watoto, mimi nitakuwepo kazini. Usiwe na wasiwasi. Binafsi sitambugudhi kabisa, ili atulie. Ila ukipata nafasi yakuzungumza naye, naomba niombee msamaha. Mwambie ni kweli najutia. Najuta sana, lakini nampenda na ninamuombea.” Grace akatoka. 

“Sasa nikiache hiki chakula au niondoke nacho?” Mama G akauliza. “Kitamwagwa tu mama. Nenda nacho. Asante.” Mama G akabaki amesimama. “Na wewe?” “Kama kipo chakula changu, naomba niachie tafadhali. Mtoto akiendelea vizuri, jioni nitakuja kukuangalia nyumbani. Lakini kapumzike tu.” Mama G akaacha kapu lote akatoka.

~~~~~~~~~~~~

Geb akampigia simu Nanaa. Ikaita mpaka ikakata. Baada ya muda Nanaa akapiga. “Vipi?” Geb alimuwahi mara tu baada yakupokea. “Namsikia Magesa analia. Naruhusiwa kuja?” Nanaa akauliza kwa sauti iliyosikika alikuwa akilia. “Naomba usilie Nanaa. Uzima wako ni muhimu sana kwa hawa watoto. Naomba utulie.” Kimya. “Uko wapi?” “Sipo mbali. Kama unaniruhusu kurudi, naweza kuja sasa hivi. Sitachukua muda mrefu.” “Naomba uje basi. Na Liv naye ameamka. Amejifunika, anakulilia.” “Basi nakuja.” Wakakata. Geb akaendelea kubembeleza watoto wake.

~~~~~~~~~~~~

Nanaa akashindwa kuelewa kama yeye ndio mgonjwa au Magesa. Akili na mawazo ya Geb vyote vilikuwa kwake. Hapakuwa na ahadi wala maneno mengi, lakini kila wakati alimuuliza anavyojisikia. Kama ameshiba, amekumbuka kunywa dawa na kumtaka ajilaze, halafu anamuwekea watoto pembeni yake. Alimfuata mpaka chooni kama atakawia kutoka. Na akienda kuoga, alienda kusimama humo humo bafuni. Hata kama hatamuongelesha, lakini Nanaa alishitukia anaingia nakujiegemeza hata kwenye sinki na macho kwenye simu yake. Akifunga tu maji, Geb anamchukulia taulo na kumsogezea. Atamsaidia kujikausha mgongoni au miguuni, kwamba asiiname. Ilimradi Nanaa akamuona anajishugulisha naye.

Akabaki akijiuliza baada ya mtoto kuruhusiwa, itakuaje? Ndio itakuwa mwisho wake na wanae? Akabaki kimya akiwaza. Geb akamuona amepotelea mawazoni. Ilikuwa jioni ya siku inayofuata mara baada ya ujio wa mama G, na Grace. “Nikupe maji ya kunywa?” Geb akamsogelea. “Naona nakunywa maji mengi! Nina kazi ya kwenda chooni kila saa!” “Lakini unahitaji maji mengi. Jitahidi kunywa. Ikifika kwenye saa 12 jioni ndio iwe mwisho.” Liv alikuwa amemkalia mama yake huku akiangalia tv.

Ukimya ukapita kidogo. “Unawaza nini?” Geb akavuta kiti karibu na alipokuwa amejilaza Nanaa. “Nafikiria tu.” “Nini?” Nanaa akafikiria kidogo. “Nafikiria baada ya hapa, nitakuwa nawaonaje tena wanangu?” Nanaa akaona machozi yanaanza kumtoka. “Naona Magesa ni kama ameanza kunizoea! Sasa hivi hata nikimshika mimi anatulia. Nina wasiwasi tukija kupotezana tena kwa muda mrefu, atanisahau tena.” “Kwa nini mpotezane tena?” Geb akauliza.

“Eti Nanaa?” “Sijui Geb! Hata sielewi tena! Hakuna kinachoeleweka tena. Nimebakiza siku chache tu wanifanyie huo upasuaji ambao sijui kama hata huo moyo utakubali kufufuka tena baada ya hapo! Sijui kama baada ya hapo nitawaona wanangu tena!” “Tunamuomba Mungu Nanaa. Naomba na wewe ujipe moyo.” “Sijui kwa nini Geb? Nimeingiwa na hofu sana.” Nanaa akavuta pumzi na kujaribu kutulia.

“Nimemwambia dada Fifi kuanzia siku moja kabla sijalazwa kwa ajili ya huo upasuaji, asichukue oda yeyote ile. Nataka niwe naye hospitalini wakati wote. Kuanzia mwanzo mpaka mwisho awepo. Nikitoka tu hapa, nataka niende naye benki. Nikamuweke kama mtu wa pili kwenye akaunti yangu. Ili chochote kikitokea kwangu, apate pesa za kujikimu na mwanangu siku hizo za mwanzoni mpaka mtoto atakapochangamka. Ndipo atajua mwenyewe chakufanya na huyo mtoto. Nimejitahidi kuandikia mambo mengi juu yangu na maisha yangu. Kwa ajili yake yeye dada Fifi na Jimmy. Ili nisije kuondoka vibaya kama mama alivyoniacha mimi. Naamini Jimmy akija kuwa mkubwa hatakuwa na maswali mengi, kama mama alivyokuwa ameniacha nayo.” Geb akajua yapo mengi yanayoendelea ndani ya kichwa na moyo wa Nanaa. 

~~~~~~~~~~~~

Akatamani atoe ahadi, akakumbuka ameshamuahidi ahadi nyingi sana, na amekuwa akizivunja muda mfupi sana mara baada yakumuahidi. Siku aliyobakwa Nanaa, alikuwa naye hotelini zaidi ya masaa matatu akimwaga ahadi tele kwake. Usiku wake alipobakwa, hata pole hakumpa. Akaishia kumpokonya watoto na kukata msaada wa pesa alizokuwa akimpa kila mwezi. Na kumpokonya watoto. Leo anarudi na ahadi gani tena!?

Akakumbuka ahadi zote alizokuwa akimuahidi tokea hawana hata mtoto mmoja, nakuishia kuzivunja vibaya sana. Tena alimuacha akiwa anamaumivu na inakuwa ni muda mfupi sana baada ya ahadi zake kwake. Anarudi kwa kuomba msamaha, nakurudia tena kuahidi? Hakujua kama atubu na kuahidi tena au anyamaze. Maana ni jana yake tu, Nanaa alimtahadharisha nakumwambia yeye sio mjinga. Akaona anyamaze.

~~~~~~~~~~~~~~~

Mambo yanazidi kuchanganya. Maji yamezidi unga kwa kina Magesa.

Nanaa naye amewaambia amewaacha madhabahuni kwa

Bwana, Yeye ndiye atashugulika nao. Amejipatia wanae lakini wakiwa dhaifu, na Magesa mgonjwa.

Geb anakutana na Nanaa aliyejeruhiwa sana. Anamipango mizito ambayo yeye wala pesa yake  haihusishwi.

Nani wa Nani?

Endelea kusoma kujua kitakachoendelea….


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment