Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu ya 53. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu ya 53.

Kwa Kina Magesa.

Tokea tukio la kutisha alilosababisha Malii, mahusiano hata kati yao yalivurugika kabisa. Malii alikuwa ni kama amemwaga roho chafu ya kutisha katikati yao. Mahusiano kati ya Grace na mama yake pia yalibadilika kabisa. Akapunguza kwenda nyumbani kwa Geb, labda aitwe. Napo hakuwa akikaa sana. Geb alijua anamkwepa. Hata simu za salamu zikapungua. Mpaka mama yake ampigie tena kwa mambo ya msingi tu. Kwa upande wao hao mapacha. Angalau walikuwa wakikutana ofisini. Mbali ya salamu na kuulizia hali ya watoto, Grace hakuongeza neno kwa kaka yake. Alifanya kazi zake, nakurudi nyumbani kwake. Kimya.

          Yeye Danny ndio hakusikika kabisaa. Tokea siku ya mkasa, walipita na mkewe mara moja tu, hakurudi tena. Tena Danny na watoto wake walibaki kwenye gari hakutaka hata kushuka garini. Mama G naye alikuwa busy na ulezi wa watoto akisaidiana na Sara. Geb yeye ndio alibadilika kuliko kawaida kasoro tu kuchanganyikiwa sababu ya jukumu la watoto na kazi. Ikawa hata ngumu kumuongelesha au kumwangalia usoni. Kupishana kukawa kwingi kati yao kama wanao kwepana. Maisha yakaendelea wasijue yanayoendelea nyumbani kwa Grace na Danny.

Chachu Ndogo, Huchachua Donge Zima.

Kumbe maneno ya Malii yalimuingia na kuharibu akili ya Danny kabisa. Walimtoa pale siku ya tukio, Malii akiendelea kumsema mpaka walipomshusha kwenye mataa. “Wasijekuwa wamenitoa kweli kafara!” Danny aliendelea kuwaza. “Utajiri wa Geb ni kweli umekuwa wa gafla sana. Kwa nini Grace amekazania kufanya kazi huko? Hata ukimwambia kuna kampuni nyingine itamlipa zaidi, au tufungue kitu chetu, hataki! Ukute kweli wameungana pamoja wakifanya biashara kwa njia ya ushirikina wakinitumia mimi!” Danny akaendelea kuwaza.

Ni kweli ‘chachu ndogo, huchachua donge zima’. Danny akaanza kujiwinda nafsi yake na familia ya mkewe. “Wana kijiumoja ambacho hakieleweki eleweki hivi! Inakuwa ni wao tu!” Yale yote yaliyokuwa yakimvutia Danny kwenye familia ya mkewe, yakaanza kuleta maswali. “Kwa nini nimng’anganie hivi Grace!? Kuna walichonifanyia tokea zamani kama alivyosema Malii. Itakuwa ni kweli mimi ndio waliona katika kundi letu wote mimi ndio nina nyota kali, wakanifanyia kweli uchawi kwa kunitoa kafara. Nikawa kama mjinga kwa Grace. Sikuwa hivyo mimi! Sikuwa mtu wa wanawake kabisa! Kwa nini nikawa nimepagawa na mwanamke kama Grace!” Akaendelea kuwaza kila iitwapo leo. Hata mkewe akaanza kumtilia mashaka. Yale mazuri yote ya Grace akaanza kuyaangalia mara mbili mbili huku akijiambia zile sio akili za kawaida. Akaanza kumshusha thamani mkewe.

Matatizo ambayo Grace hakuwahi hata kuwaza yanaweza kumpata ndani ya ndoa yake, yakaanza. Kila kitu anachoongea yeye, Danny anakipinga. Tena kwa ukali sana akiamini ndio anajitoa kwenye ushirikina wa familia ya mkewe. Ukali kwa Grace ukazidi pasipo sababu. Kuchelewa kurudi kutoka kazini bila taarifa kukawa kitu cha kawaida. Yale mambo yakutaka awe na Grace wakati wote yakaisha kabisa kitu ambacho kilikuwa mateso makubwa sana kwa Grace. Akawa anamkwepa sana.

Akimpa hata maji ya kunywa, anayaangalia mara mbili mbili mwishowe anayamwaga hata mbele ya Grace na kwenda kuchukua glasi nyingine na maji mengine au anaacha kabisa kunywa maji. Chakula ndio alikuwa anakikataa waziwazi huku akimtamkia mkewe aondoe limbwata lake, mbele ya macho yake. Akimaanisha aondoe chakula ambacho atakuwa amekiweka madawa ya ushirikina ili kumpumbaza yeye. Grace hakuchoka kumwambia kuwa hajawahi kumloga, lakini napo pia huwa panazuka ugomvi mkubwa zaidi.

Mambo yaliharibika zaidi pale alipojua kuwa Nanaa alipokonywa watoto. Alichukia na kuwa kama amechanganyikiwa kwa Grace. Akawa kama anamlipiza Grace kisasi kwa walichofanya ndugu zake kwa Nanaa. Na yeye ni kama akampokonya Grace watoto. Siku ambazo yeye haendi kazini, anaweza kuchukua wanae kuanzia asubuhi akarudi usiku bila kumtaarifu Grace alipo. Hataaga wala kumtafuta mkewe kumjulia hali au kumwambia walipo na watoto.

~~~~~~~~~~~~~

Ikafika birthday ya kutimiza mwaka kwa mapacha wa Grace, ikabidi kumuomba Geb, watoto wake wahudhurie. Akamfuata ofisini kwake. “Nitamwambia mama. Wataletwa tu. Sidhani kama kutakuwa na shida. Si umesema itafanyika nyumbani?” Grace akabaki kimya kwa muda. “Ndiyo.” Akajibu. “Wewe hutafika?” Grace akauliza. “Najua unanikwepa Grace.” Grace akavuta pumzi na kuzishusha taratibu. “Kwanza nina matatizo yangu binafsi. Pili Sifurahii maamuzi yako na mama Geb. Mnaniumiza nafsi yangu. Ndio maana naona ni heri nikae tu mbali na nyinyi. Siyawezi maisha mnayoishi sasa hivi. Naumia sana hasa nikimuona Liv! Siwezi Geb.” Geb akanyamaza.

          “Najua unampenda sana mama na unamsikiliza kwa kila kitu. Lakini kuna mambo nilazima usimame wewe mwenyewe kama baba, Geb. Wanawake wengi Malaya au niseme wale wachafu kupindukia, au hata mwanamke fukara, akiamua, anaweza kulea watoto vizuri tu. Tena yeye peke yake bila msaada wa mtu, kuliko hata mwanaume msomi na tajiri. Mwanamke mmoja anaweza kulea watoto 10 bila shida. Hata akiwa maskini vipi, anaweza kuwasogeza hao watoto wakafikia ngazi yeyote hata kuwa madaktari au maraisi wa nchi. Lakini mwanaume mmoja milionea anaweza kushindwa kulea hata mtoto mmoja tu. Angalia matajiri wengi na wasomi. Watakwambiwa walilelewa na mama tu. Aidha baba alikimbia au alikufa. Fanya utafiti wako Geb. Utagundua.” Grace aliongea kwa upole sana lakini kinyonge.

“Najua mimi huwa hunisikilizi. Lakini nataka kukwambia ukweli Geb. Unaharibu maisha ya watoto wako. Huyo Sara anayekupikia hapo ndani, hatakaa akawa mama wa Liv, hata ufanyeje Geb.” “Nani amesema Sara atakuwa mama yake Liv?” “Basi fungua macho yako, uone. Sikulazimishi chakufanya. Lakini nakushauri urudi magoti. Umemuacha Mungu Geb. Unaangamia. Mungu pekee ndio atakutoa hapo ulipo. Umekonda. Wewe na mtoto wako Liv, wote mmechoka kama wagonjwa! Umezeeka gafla, umekuwa kama babu wa miaka 80, wakati unaishi na wanawake wawili ndani ya nyumba. Na wote wanakuhangaikia wewe!” Geb akabaki kimya. 

“Vipo viatu vya watu wengine, havivaliki na wengine. Hata ufanyaje. Kuna mapengo huwa hayazibiki daima. Labda kwa rehema za Mungu tu. Mrudie Mungu Geb. Umefanikiwa sana kwenye mambo ya pesa. Unaakili sana upande huo. Kwa nini maisha ya upande mwingine yanakushinda? Jiulize, jichunguze wewe binafsi kabla hujanyoshea mtu mwingine kidole. Inawezekana shida inaanzia kwako. Nakuombea Mungu akusaidie kukufungua macho ili uweze kufanikiwa na huo upande mwingine wa maisha ambao ni muhimu sana hasa sasa hivi ukiwa ni baba. Ninakwambia bila kukuficha Geb. Umeshindwa. Mama hawezi kukwambia ukweli, lakini mimi nakwambia. Umeshindwa kuwa baba kama ulivyoshindwa kuwa kimbilio katika upande wa mapenzi.” Grace akapasua moyo wa Geb.

“Hunitendei haki Grace!” “Ndio maana nakwambia jichunguze Geb. Mimi sitasema mengi kama Danny anavyotusema. Lakini naanza kumuona kwa upande mwingine yupo sahihi. Sisi sio watu wakutegemewa wala wakukimbiliwa wakati wa shida. Tatizo linapotokea, tunajitenga na mtu. Danny anasadiki kwa asilimia mia ni kweli tunamloga! Tunataka watu tunaoona wanatusaidia tu. Tukiona hawana faida kwetu, tunawatupa nje. Anaamini hata yeye tupo naye karibu, tukimshikilia, kwa sababu tuna nufaika naye.” “Ndio maana umekonda hivyo?” Geb akamuuliza dada yake.

“Mimi nakondeshwa na mfungo Geb. Namlilia Mungu wangu. Ipo siku najua atanijibu tu. Hayo mengine najua ni majaribu tu. Lakini Geb, rudi magotini. Vunja roho za kurithi. Muombe Mungu akusaidie urithi mazuri tu kutoka kwa baba. Mabaya uyavunje. Si kwako tu, hata kwa Magesa wako. Ni roho. Nakuhakikishia ipo kwako. Usiposimama imara na kutulia magotini, utakuwa kama baba kwa asilimia zote. Utafanikiwa kipesa, lakini maisha mengine yatakushinda kabisa. Na kama hujagundua, unatesa watoto wako wewe mwenyewe. Ukishirikiana na mama, aliyekuwa kwenye maisha ya baba. Anahamisha maisha ya baba kwako wewe. Nampenda mama, lakini kuna mambo lazima uwe naye makini sana. Kwake haitamsumbua kukuona unayafanya au unaishi maisha fulani aliyomuona baba akiishi.” Grace akaendelea.

“Atakusaidia kuyaishi hayo maisha bila shida. Na atakubariki huku akikufariji na kujaribu kukupa yale yote uliyotakiwa kupewa na mkeo. Atahakikisha unakula na kuvaa vizuri. Atakutafutia mwanamke anayempenda yeye. Umemfikiria Magesa na Liv? Ukishuhudia vile Nanaa anavyoteseka na mimba zake. Inakuwa kufa au kupona ili kuzaa hao watoto. Leo unaungana na mama kumpokonya mtoto wake akiwa hata hajamnyonyesha!” Grace akaanza kutokwa na machozi.

“Tena kwa kosa ambalo alilifanya kwa ajili yako! Hujijui vile ulivyo nahasira Geb. Yule binti alikuficha ili asikuumize au kwa kuwa alikuogopa! Leo unamuadhibu kwa jambo alilolifanya wakati akikuona wewe ukiishi na Liz nyumba moja, ambayo na yeye alikuwa akiishi! Hamkuwa pamoja! Wewe ulikuwa na Liz, na yeye alikuwa huru kuishi maisha yake. Leo mnamuadhibu bila huruma! Unaruhusu wivu wako na hasira zako zitese watoto wako! Na kwa taarifa yako tu, na wewe unateseka. Jiangalie kwenye kioo ndipo utajua.” Grace aliendelea taratibu huku akitokwa na machozi.

“Danny ametuogopa kuliko nitakavyokwambia. Anashindwa kuelewa hata tunawezaje kumtaja Mungu kwa kitendo tulichokifanya kwa Nanaa. Alijua tungemuhurumia na kujutia hata kushindwa kumlinda siku ile usiku! Mlikuwa wanaume wanne pale na walinzi wako. Lakini wote mlishindwa kumlinda Nanaa tuliyekuwa tukimsikia akilia kwa uchungu sana. Leo mnamuadhibu na kumfukuza! Danny ameshindwa kuelewa kabisa. Anatuogopa, hataki hata kutusogelea. Anatuona wote sisi ni wanyama si binadamu. Ananitangazia kuwa inabidi aanze kujiandaa yeye na wanae. Kwa kifupi, Danny anatafuta kuanzisha familia yake. Ndoa yangu ilishaisha Geb. Kinachotufunga sasa hivi ni ile nyumba na watoto, basi.” Grace alifuta machozi.

“Anasema amewekeza pesa zake nyingi sana pale. Hawezi kuondoka na kuniachia ile nyumba. Anatoka na kurudi nyumbani atakavyo.” “Si urudi tuishi wote?” Geb alitoa wazo. Grace akacheka huku akitingisha kichwa. “Hilo ndilo tatizo lako Geb. Kukitokea tatizo linalokuumiza wewe, unakimbia. Hujui kumlipia mtu garama. Hujui kupigania kilicho chako. Hujui na hutaki kujifunza.” Grace akaona asimuache, avute kiti kabisa akae mbele ya meza yake.

“Hivi unakumbuka walimtoa Danny nyumbani kwako huku wakimtukana na kumuaminisha tumemloga? Unakumbuka walimtoa huku wamemshikia risasi ya tumbo na kumwambia wanaenda kumuua? Unakumbuka muda ambao Nanaa alikuwa akilia akiomba msaada na tukashindwa kumsaidia?” Kimya. “Basi Danny anajua mpaka dakika ya mwisho aliyoshuhudia yeye, Nanaa aliyolia akiomba msaada. Danny anajiweka kundi moja na Nanaa. Yatima wasio na msaada. Kuwa familia yetu tunawatumia tu. Anasema wewe umeshapata watoto uliokuwa ukiwataka, basi. Ndio maana tumemtupa Nanaa nje.” Grace akaendelea

“Hivi unajua kuwa James anaogopa hata kumuona Nanaa? Yeye anamaumivu yakushindwa kumsaidia mdogo wake siku ile usiku. Danny anasema James amekonda yupo kama kijiti. Anamwambia Danny, halali. Sauti ya Nanaa akimlilia akimuomba msaada, inamuweka macho. Anasema mdogo wake alimlilia akimuomba amuokoe lakini alishindwa.” Grace akaendelea. Alikusudia kuzungumza na Geb. Akaamua aongee tu hata kama hatajibiwa.

“Sasa Danny yeye anasema haelewi roho hiyo mbaya yakumpokonya Nanaa watoto waliokuwa wakimtesa karibu kufa, sisi tumeipata wapi? Tumewezaje? Anasema ameshindwa hata kumwambia James kama mdogo wake amepokonywa watoto. Anasema kwa hali ya James ilivyo sasa hivi, anaweza kufa kabisa. Anamdanganya kuwa Nanaa yupo na anaendelea vizuri.”

“Kwa hiyo Geb, inawezekana ile nyumba ambayo inamfanya Danny anashindwa kuondoka, ukute ndio muujiza wangu. Sitamkimbia mume wangu. Kwanza mimi naujua ukweli wote. Sijamloga Danny ili anipende. Najua maumivu aliyonayo. Nitamuombea mume wangu. Sitamkimbia kipindi hichi ambacho amechanganywa na maneno ya Malii na matendo yako wewe na mama kwa Nanaa. Mchana na usiku nitamlilia Mungu wangu. Hata kama ameanza umalaya huko nje. Basi, namuombea Mungu amlinde, asipatwe na magonjwa. Naamini ipo siku atanijibu na nitampata Danny na hata kama sitampata tena, sitakuwa na pakulaumu, kwa kuwa ninajua nilivyopambana. Ataniacha nikiwa sina lawama moyoni. Nitajiambia niliomba, nikavumilia, lakini ameshindwa kunipokea tena. Lakini bado sijamaliza kupambana Geb. Nipo kwenye kupigania ndoa yangu mpaka nione huo mwisho. Huwa hatukimbii mmoja anapoanguka. Na  upo usemi unasema, mtoto akinyea mkoni, hukati. Ndoa hazijengwi kwa hisia Geb. Ni upendo. Na unajua sifa za upendo. Nenda kasome bibilia yako kama umesahau tabia za upendo. {1 koritho 13:4-8}.” Grace akasimama na kutoka. Alimuacha Geb hoi. Hakutegemea.

~~~~~~~~~~~~~

Akachukua simu akapiga simu nyumbani. “Mbona Liv analia!?” Akamuuliza mama yake. “Naona ameamka tu vibaya. Lakini ni mzima. Nimempima hana hata homa.” “Amekula?” Geb akamuuliza tena mama yake. “Kidogo sana.” “Naomba kuzungumza naye.” Liv akakataa. Geb akakata simu. Ilikuwa ni saa tano asubuhi. Lakini Geb akaona arudi tu nyumbani. Akaenda kumuaga Grace, akatoka.

Alirudi nyumbani kwa haraka. Akamkuta Liv amekaa chini ya meza, akilia. Maneno na hukumu ya Grace vikaanza kumrudia. Kama aliyefunguliwa macho. Akaona yeye ndio amesababisha machungu yote yale kwa mwanae. Akachuchumaa, akamuona amekaa peke yake mwisho kabisa wa ile meza, ameshika kitambaa cha mama yake alichokuwa akijifunika wakati ananyonya. “Njoo Liv.” Geb akamwita. Liv akaendelea kulia kwa kwikwi, taratibu, bila kutoka pale chini.

 “Njoo mama yangu. Njoo mama eeh!” Liv hata hakujivuta. Akabakia akimwangalia baba yake huku akilia taratibu. Kama aliyekuwa akimuhukumu zaidi. Maneno ya Grace yakaleta maana zaidi. Geb akaingia chini ya ile meza. Liv akajivuta mbali zaidi, akajifunika kitambaa cha mama yake kama kujificha. “Nitakaa hapa hapa na wewe. Sitakugusa.” Liv hakutoka pale. Akatulia vile vile alivyokuwa amejiweka. Mama G alikuwa amekaa kwenye makochi akiangalia.

“Unaumwa?” Geb akamuuliza kwa upendo. Liv kimya. “Unataka twende kwenye ice cream?” Kimya. “Niambie unataka nini Liv, mwanangu.” Kimya. Hata hakunyanyua uso kumwangalia baba yake. Akaamua na yeye kunyamaza. Ukimya wa muda ukapita, Geb akajua ameshalala. Akamtoa pale chini ya meza. “Grace amekwambia birthday ya wanae itakuwa jumamosi hii?” Geb alimuuliza mama yake wakati akipita na mwanae kuelekea chumbani kumlaza. “Amenitumia ujumbe.” Mama G akajibu. Geb akaingia chumbani.

~~~~~~~~~~~~~

“Nataka kumuomba dereva anipeleke saluni. Sijaosha nywele muda kweli!” Geb alimsikia Sara anaaga. “Si ndio umekurudisha sasa hivi?” “Alinisindikiza kwa sonara. Unakumbuka ile pesa uliyonipa jana? Basi nilikuwa naenda kummalizia sonara wangu. Lakini wala sitakawia. Kwanza hamna kitu chakufanya hapa. Huyo mtoto wa kike ndio kagoma. Kaka yake ni maziwa na uji tu. Huwezi kushindwa kummudu huyo, bwana bibi! Acha na mimi nikajisopu sopu nifananie na hapa kidogo. Halafu nimesikia kuna birthday party ya watoto wa Grace. Nataka nikashonee wiving ndefuu, nipendeze. Sio natokea kwenye birthday naonekana wakuja. Au unasemaje bibi!?” Sara akacheka nakutoka bila kusubiri vikwazo.

Baada ya muda akarudi. “Nahisi kama pesa haitanitosha vile! Naomba niongezee kidogo.” Mama G akasimama. Sara akamfuata nyuma. “Yaani pesa yote ile ya jana, umemaliza?” “Bibi na wewe? Pesa gani ile yakujiliza bwana?” “Sio kwamba najiliza Sara. Pesa ngumu.” “Kwa wengine. Hapa pana neema bwana! Acha kubania mipesa hiyo, niache nipendeze bwana! Nataka kushonea wiving original ili ikae muda mrefu halafu nikitokea watu wajue zangu. Uzuri garama bwana.” Sara alisikika akicheka kwa utani. Akapewa pesa, na kutoka na dereva. Geb akatoka taratibu na kurudi chumbani kwake.

~~~~~~~~~~~~~

Maneno ya Grace yakaanza kujirudia taratibu. Miezi mitano ilishapita tokea Nanaa aondoke. Lakini utafikiri ilishapita miaka 3. Geb akarudi chumbani kwake. Kilio cha Liv na maneno ya Grace vilimnyima raha yakurudi tena kazini. Akasogelea kioo nakujitazama. Ni kweli alikuwa amechoka. Akarudi kukaa kitandani akiwa amejawa mawazo. “Mungu nisaidie.” Kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu, Geb akamkumbuka Mungu wake. Akazivuta pumzi kwa nguvu, nakuzishusha taratibu.

Akaamua kupiga magoti kabisa. “Najua unanisikia Mungu wangu. Nisaidie. Ni kweli nimezama.” Ndilo neno aliloweza kuliongea. Akabaki akiwaza jinsi yakujinasua. Aliachana na Mungu lini, ni swali ambalo alishindwa kulijibu. Alikumbuka mara ya mwisho alipokuwa na Nanaa, aliweza kupiga magoti na kuomba. Nini kilimpata? Hasira!

“Liv anaakili kama  za kwangu. Hapotezi kumbukumbu. Bado anamkumbuka mama yake.  Sasa sijui nilaana au ni baraka kwake! Mungu wewe ndio ulimuumba huyu mtoto. Msaidie. Asiendelee kuteseka. Geb aliomba na kuwaza akiwa amepiga vile vile magoti ameinamia kitandani. Alimsikia mama yake anataka kuingia. Lakini alikuwa amejifungia mlango kwa ndani. Hakutaka kumfungulia. Akataka muda wa peke yake mle ndani. Alikaa pale akiwaza asijue aombe nini.

Nanaa!

Mimba ya Nanaa ilipofikisha miezi mitano presha ndio ikazidi kuchukua hatamu. Alirudi kutoka hospitalini, akajitupa kitandani. “Mbona huna raha?” Fifi akaingia na kumuuliza. “Daktari ameniambia hali yangu sio nzuri. Presure ipo juu sana. Hivi hapa ilibidi waniwekee dripu moja ndio nimeweza kufika hapa. Walitaka kunilaza, lakini nimekataa.” “Kwa nini tena na wakati uliniambia mimba zako zote ndivyo zinavyokuwa!?” “Sijui dada. Najiona kama sina nguvu za kupambana tena. Najisikia kuishiwa nguvu kabisa. Sasa sijui kwa kuwa sio mtoto wa Geb? Sijui dada! Nimejiachia tu. Liwalo na liwe. Nikifa au tukifa wote na huyu mtoto, najionea ni sawa tu. Naomba nijipumzishe kidogo.” Fifi alibaki akimwangalia. Nanaa akajigeuza, akalala.

Uzuri hata Fifi alishakuwa mtaalamu wa mapishi. Na kadiri siku zilivyokuwa zikizidi kwenda ndivyo hali ya Nanaa ilivyozidi kuwa mbaya. Presha juu kila wakati. Mikono kutetemeka, mara kufa ganzi. Hawezi kushika chochote. Mbaya zaidi, hakuwa akijali tena. Fifi alijua ni kama amejizira. Alishatafuta msichana mwingine wakuwasaidia. Biashara ikaendelea. Nanaa akiwa nusu nusu. Nanaa aliyeanza hiyo biashara, siye Nanaa huyu. Utafikiri ni watu wawili tofauti. Aliyokuwa akiongea na anavyoishi sasa ni tofauti. Mimba hiyo ilimuharibu akili zake kabisa. Akasahau yeye ni nani, anakwenda wapi na anataka nini. 

Kwa Kina Magesa!

Siku moja kabla ya birthday ya watoto wa Grace, Geb aliwahi kutoka kazini. Akaamua kupitia kwenye nyumba aliyokuwa akiishi na Nanaa. Walinzi walimfungulia geti. Akaegesha gari, akashuka nakutembea taratibu wala asijue kwa nini yupo pale. Akajikuta amekaa pale nje akiwaza. Alikaa kwa muda mrefuu. Mlinzi akamfuata. Geb akamsalimia. Alikuwa ni mlinzi wa muda mrefu hapo. Mzee kwa walinzi wote waliokuwa wakifika hapo kulinda. Wengine walikuwa wakibadilishwa mara kwa mara, lakini yule mzee alikuwepo hapo mara kwa mara. Na Geb alikubaliana na hiyo Kampuni kwa kuwa alikuwa ni mzee aliyejaa busara, ilikuwa rahisi kunyoosha walinzi vijana waliokuwa wakifika hapo.

          “Mambo yanabadilika mwanangu! Na ni kwa kila mtu.” Geb akanyamaza. “Watu wengi wanajua wakishapata majumba makubwa hivi, wakayajaza mavitu ya thamani, ndio maisha yamekamilika. Hawajui nyumba si jengo wala huwa hazijazwi na vitu vya thamani.” Geb akabaki kimya akaendelea kusikiliza tu. “Na mimi wakati wote huwa nawaambia hawa vijana hapa wanaokuja kulinda na mimi. Si hivyo. Maana kutwa wanatamani na wao wangekuwa wamelala ndani, wanalindwa nje. Nawaambia si heri wao asubuhi ikifika au jioni wakitoka kazini, wanaenda kulala kwa wake zao. Japo si kama hapa, lakini wanajua wanarudi makwao. Mke na watoto wanawasubiri. Haijalishi ni wapi. Iwe uswahilini, iwe chumba kimoja, bora maelewano. Sasa waliyaona majuzi hapa wakati mama watoto anakimbia hili jumba. Hawakuamini. Si uliona barua yake aliyokuaga na wewe?” Geb akashangaa kidogo.

“Ulimpa nani?” “Si yule dereva wenu? Jeri! Alileta watoto. Nikamwambia kabisa kuwa asihangaike kuleta tena watoto hapa. Mama yao ameamua ni heri aondoke kuliko yale masharti uliyokuwa umemuwekea. Kwa hiyo..” “Subiri kwanza Mzee Nyundo.” Geb akamkatisha. “Masharti gani na barua gani?” Geb akauliza.

          “Si vile ulivyomwambia awe analeta watoto, lakini asiwaguse? Mwenzio alishindwa vile watoto walivyokuwa wakilia, lakini hawezi kuwabembeleza. Hasa kale karembo kenu. Alikuwa akimlilia sana mama yake. Walikuwa wakilia hapa, kama msibani. Mama mtu analia nje ya gari, basi na mwanae analia ndani ya gari. Na yule dereva naye akasimamia masharti yako bila huruma. Hakuna mtoto kumshika mama yake, wala mama haruhusiwi kumshika mtoto. Kuwaangalia tu dirishani kama anatizama mfungwa jela! Mwishowe naona mwenzio akaona ameshindwa. Akaniaga. Tena hapa mbele ya wale vijana. Akasema hawezi kuendelea kumtesa mtoto wake. Ni heri aondoke tu. Mbona alinipa hata barua yakukuaga! Nilimkabidhi yule kijana wako. Hakukupa?” Geb hakujibu kitu chochote, mpaka yule mlinzi akaamua kuondoka. Lakini na yeye akawa ameongezea kitu kingine.

Geb alikaa kwa muda pale akiwaza. Zilikuwa habari mpya na ngeni kabisa kwake. Akaunganisha hili, akajumlisha nakutoa. Akakumbuka maneno ya Grace. Akajua watu wote wanajua yale yote yanayoendelea kasoro yeye. Akaelewa ni kwa nini watu wanawachukia. Akachukia mateso aliyokuwa akiyapitia Liv na yeye kuwepo kwenye maisha ya huyo mtoto bila taarifa! Akachukia sana. Akajua ndio maana amegeuka kuwa mtoto asiye na furaha. Kwake yalikuwa ni mateso ambayo hakujua ni kwa nini anafanyiwa hivyo na kwa hakika hakustahili. Magesa yeye hakuwa hata na habari na kinachoendelea. Nanaa ni nani? Hakuwa hata na habari na anachokikosa maishani. Bora apewe chakula, maisha yanaendelea. 

Geb akataka kumchukia mama yake, lakini akajua yeye ndio anawajibika kwa asilimia zote. Alishindwa kusimama kwenye nafasi yake kama alivyoambiwa na Grace pia. Alizidi kuumia kushindwa kujua yaliyokuwa yakiendelea na kule walikokuwa wakipitishwa wanae, hasa Liv na yeye akiwepo ila hana habari. Akabaki akiwaza.

~~~~~~~~~~~~~

Alitamani kuendelea kukaa pale hata asionane na mama yake kwa muda ili apate muda na Mungu, lakini akakumbuka watoto wake. Jinsi Sara anavyowalalamikia, hasa Liv. Akaona heri tu arudi, aanze kuwa baba. Akamkuta Magesa analishwa na mama yake. “Nipe nikusaidie kumlisha.” Geb akamsogelea. “Mbona na wewe hauli tokea juzi?” Mama yake akauliza. “Nipo kwenye maombi.” Geb akajibu kwa kifupi tu. Akaendelea kumlisha mtoto wake. Alikuwa akila bila shida. Bibi yake alishamwanzishia uji kwa kuwa alikuwa hashibi. Alikuwa na afya nzuri. Ungependa kumwangalia kila wakati. 

“Kesho ndio ile birthday ya mapacha. Grace anataka iwe mapema.” Mama yake akamkumbusha. “Nakumbuka. Kwa kuwa sitakwenda kazini, tutaongozana tu.” Geb akajibu na kuongeza.  “Kesho nataka na wewe utoke, ukafanye mambo yako. Hata kama utaenda kutengeneza tu kucha, lakini utoke ukapumzike na kujiandaa na hiyo party.” “Sasa nani atakusaidia swala la watoto? Sara si mkaaji ndani.” “Usiwe na wasiwasi. Liv na Magesa hawatanishinda. Wewe chukua mapumziko tu. Hata hivyo nataka muda nao. Nimekuwa na mambo mengi, nimeshindwa kutulia nao.” Geb akaendelea. “Halafu naona nimekuachia majukumu yangu ambayo nilitakiwa kuyafanya mimi mwenyewe kama baba. Unahangaika sana juu ya watoto wangu. Umeacha shuguli zako, upo hapa kwa ajili yao tu! Kweli nakushukuru. Pole na asante mama.” Yale maneno yalimuingia mama G, yakawa kama hukumu tena, wala si faraja. Akabaki kimya kabisa.

Sara!

Ilipofika mida ya saa mbili usiku, Sara akawa anaingia. Alimkuta Geb yupo na mama yake hapo sebuleni. “Nimechelewa kweli sababu ya foleni.” Akajiongelesha. Kimya. “Hata hivyo nimerudi tu. Lakini sijamaliza mambo yangu. Vitu garama kweli! Labda kesho nitamalizia.”  Sara alipita na mifuko yake. “Ukishaweka mizigo yako, nakuomba uje tuzungumze.” Mama G akamuwahi. “Powa, nakuja.” Sara akajibu.

Baada ya muda akatoka. “Kwema?” Akauliza Sara wakati anakaa. “Nimezungumza na shangazi yako, tumeona ni heri urudi tu kuishi kwa wazazi wako.” Sara akashituka mpaka Mama G akamuona. “Kwa nini!?” Sara akauliza. “Naona nimezidiwa na majukumu. Sitaweza kukuangalia wewe na watoto.” “Kwani mimi unatakiwa kuniangalia!? Mimi mtumzima na akili zangu. Nimeishi Morogoro kwa miaka mitatu bila wazazi, sihitaji kuangaliwa na mtu.” “Hilo ndilo tatiza Sara. Mimi nimelea watoto humu ndani. Sijapata ambaye ananirudia saa mbili usiku. Nimekuza bila shida. Nikiheshimiwa. Na..” “Kama ni swala la kuwahi kurudi nyumbani, hilo mbona linazungumzika tu. Wewe niambie saa ngapi unataka niwe narudi nyumbani, nitarudi. Wala usitokwe jasho.” Sara aliongea bila hofu huku akicheka nakutaka kugonga.

“Sioni sababu ya wewe kuendelea kuishi hapa wakati wazazi wako wapo. Unahitaji kurudi kwa wazazi.” “Si nakusaidia swala la watoto!?” “Sara!” Mama G akashangaa maana hata hakuwa akishinda nyumbani. Na anapokuwa nyumbani busy kwenye simu. Hakuwa akitaka kufanya kazi. Kila kitu alimwachia mama G. Ataamka saa 4 asuhuhi au saa tano. Ataoga na kujitengeneza. Kama Jeri yupo, basi atataka amsindikize kila mahali. Zaidi kwa mashoga zake aliomaliza nao chuo, kujionyesha utajiri na gari hiyo yakifahari ya Geb iliyoachwa hapo nyumbani kwa matumizi ya watoto wake. Lakini Sara ndio akaanza kulitumia yeye rasmi baada yakuona muda mwingi Jeri anakuwepo tu pale hana kazi.

~~~~~~~~~~~~~

Kazi kubwa ya Jeri aliyokuwa akifanya na hiyo gari ilikuwa nikuchukua hao watoto kuwapeleka kanisani na nyumbani kwa Grace. Walikuwa wakimpeleka hasa Liv, kwenda kucheza na Fili kabla Danny na yeye hajapora wanae na kuwatawala. Mara kadhaa walikuwa na Sara. Wakati mwingine Sara alipokuwa akifika hapo nyumbani kwao na kuwakosa Danny na watoto wake, alikuwa akimpigia simu. Danny akiwaelekeza walipo, Sara alimwambia Jeri wawe wanawafuata. Lakini mwishowe wakaacha kwani Oliva aliacha kucheza kabisa. Mara nyingine aliishia kukaa kwenye gari tu. Hakuwa akitaka hata kushuka acheze na watoto wa Grace. Hata Fili amfuate ndani ya gari ambembeleze, Liv alikuwa akikataa. Ndipo Jeri akamshauri mama G, waache tu kuwapeleka. Lakini sio Sara. 

Sara alifurahia kule kutoka na kukutana na kina Danny pamoja na watoto wake kwenye mahoteli mbalimbali. Wakati mwingine walikuwa wakipanga na Danny labda jumamosi fulani au siku fulani wapeleke watoto sehemu fulani. Wakikubaliana ndio ikawa furaha ya Sara, ili tu kutoka. Lakini Jeri akaona haina maana. Kwa kuwa walikuwa wakiishia kukaa kwenye gari yeye na Liv, Sara yeye ndiye aliyekuwa akishuka kwenye mahoteli hayo kuungana na Danny na watoto wake. Jeri na Liv watakaa humo ndani ya gari wakisubiri mpaka Sara achoke ndipo wanarudi nyumbani.

Pesa alizokuwa akipewa na mama G hazikuwahi kumtosha. Kila siku alilalamika shida ya pesa. Nywele aliyokuwa amesukia ni ya laki 350. Ametengeneza na kucha. Ukimwangalia unaweza sema mtoto wa kisomali anayetumikiwa na mama G mle ndani. Yeye alionekana bora kuliko hata mama G aliyekuwa amechoka akawa bibi kwelikweli.

~~~~~~~~~~~~~

 “Kweli mama. Sema yule mtoto wenu wa kike ni mkorofi sana. Jeuri, haambiliki. Mtoto mdogo anataka yeye ndio awe kama malkia humu ndani! Anaongea anapojisikia yeye. Akiamua kuwa kisirani, hakujibu kitu.” Geb akasimama, nakuondoka pale. Akawaacha pale wao wawili wakizungumza. Gafla mama G akageuka kuwa mama usiku huo, si bibi tena kwa Sara aliyezoea kumwita bibi. Mpaka mama G, mwenyewe akashangaa.

Siku Ya Birthday

Kesho yake asubuhi Sara aliamka yeye wa kwanza. Akasafisha na kusaidia kazi zote. Mpaka mama G anaamka, yeye akawa amemaliza kila kitu. Mama G hakumuongelesha. Akapita na Magesa wake, akaendelea na shuguli zake. Aliposikia sauti ya mtoto wake, Geb akatoka. “Njoo.” Akamchukua mtoto wake. “Nimeshampikia uji.” Sara akaongea kwa upendo, akimpa taarifa hizo Geb asijue alikorithi Liv. Kimya. Geb hakujibu kitu. “Na dada mkubwa nimemtayarishia vitu vinono. Naamini atakula leo.” Geb akampita nakuelekea sebuleni.

“Umeamkaje? Eti Magesa?” Geb alimuongelesha mwanae. Mara dereva akaingia. “Ndio nimekuja kukuchukua dada Sara.” “Kwenda wapi!?” Jeri akabaki kimya, akamgeukia mama G. “Anakurudisha nyumbani, Sara.” “Mbona nimebadilika mama? Sitakawia kurudi tena. Kuanzia leo nitabadilika.” “Wazazi wanakusubiri nyumbani. Nimeshazungumza na mama yako. Nenda tu. Utakuja wakati mwingine.” Alishaishi na Grace mtoto wa kike wakumzaa. Akawa na adabu zake. Akaja Nanaa, wakawa marafiki. Adabu na msaada bila hata kuombwa. Sara ni waina ambayo hawezi kuvumilia.

Sara aliondoka huku amekasirika sana. Aliongea maneno ya kashfa kabla yakuondoka na kuomba alipwe kwa kazi na muda wote aliokuwa ameishi nao pale. “Karibia miezi mitano sasa! Mmenizubaisha, nikashindwa kuanza kazi ofisini. Ningekuwa napokea karibia milioni mbili kila mwezi. Nikabaki nikiwapangusa mavi watoto wenu! Halafu leo mnanifukuza bila kosa!? Naombeni pesa yangu.” “Unataka kulipwa kiasi gani?” Kwa mara ya kwanza Geb akaingilia.

“Kweli Sara unasahau pesa zote nilizokuwa nikikupa!?” “Shilingi ngapi na wewe? Mtoto wenu yule wa kike kiburi wakati hata choo hajui kutumia! Kumtoa diaper yenyewe anaringa! Halafu hata shuku..” “Unataka ulipwe kiasi gani?” Geb akamkatiza. “Labda milioni.” “Unapokea hundi?” Geb akauliza. “Nitafanyaje sasa kama nyinyi hamna pesa tasilimu na hamuwezi kunirushia kwenye simu yangu?” Geb akamuweka mtoto wake kwenye kiti chake chakulia, akaenda kwenye gari yake. Baada ya muda akarudi na hundi.

“Nakuomba Jeri, usipitie popote pale. Mshushe nyumbani kwao, hakikisha unamkabidhi kwa wazazi wake, ndipo urudi nyumbani moja kwa moja. Kuna kazi nataka kukupa.” Geb akatoa maagizo. “Sawa.” Jeri akatoka na Sara. Sara alikuwa akiishi kwa wazazi wake Kitunda. Akakanyaga mafuta kuelekea Kitunda. Sara alitaka apelekwe benki, lakini Jeri alimkatalia. “Natakiwa kurudi nyumbani mapema.” Jeri akamkatalia  katakata. Akakusudia kumrudisha kwao.

Mama G!

“Mama, wewe usiguse chochote leo. Pata kifungua kinywa. Nenda saluni. Tutakutana kwa Grace. Leo nataka upumzike.” “Naona pia nipitie kwenye biashara zangu. Nikachungulie kidogo, ndipo niende saluni. Sitakawia kufika huko nyumbani kwa Grace.” Mama G alikuwa kama ameokota alumasi. Alikuwa na hao watoto masaa 24. Mpaka alishachoka. Umri ulishakwenda, hana msaada wowote wakusaidiwa watoto wa Geb. Kupata likizo ya siku ile, ilikuwa muujiza aliotamani utokee. Lakini kwa kuwa aliyataka mwenyewe, hakuwa na namna. Ilibidi abebe mzigo wote bila kulalamika huku akimuonyesha Geb inawezekana kabisa na ni rahisi sana.

Hakupoteza muda, wala hakutaka kula. Akaoga na kutoka kwa haraka na gari yake. Hakuwa hata akikumbuka siku aliyotoka humo ndani bila hao watoto. Hata kanisani alishaacha kwenda. Hata kuomba tu yeye mwenyewe alikuwa akishindwa sababu ya watoto na shuguli za humo ndani. Alihakikisha anahangaika sana kumwaminisha Geb kuwa maisha yanaweza kuendelea vizuri tu bila Nanaa. Kumbe asijue garama anayolipa.

Alindwa kukutana hata na marafiki zake sababu ya majukumu ya pale ndani. Hakuwa akienda tena saluni wala kwenye sherehe kama zamani. Hakuwa akijua yanayoendelea huko ulimwenguni. Yeye na watoto tu na shuguli za mle ndani kuhakikisha mambo hayakwami na wala hayaharibiki. Akasahau pia kuwa umri ulishakwenda. Akawa anajituma zaidi ya anavyotakiwa kama binti mdogo, akihakikisha mambo yote ya mle ndani yanakwenda sawa. Chakula cha watoto na Geb mwenyewe, huku akihangaika kumridhisha Sara atulie, ili Geb amuone ni kama binti wa kawaida, amuoe. Kumbe Sara ni mapepe, mtoto ambaye hajui kutulia sehemu moja.

Sirini Mwangani.

Jeri alirudi akamkuta Geb amekaa na watoto wake nje, barazani. Akatoka kwenye gari akaingia mpaka pale barazani. “Mama ametoka?” Akamuuliza Geb. “Ndiyo. Kwani vipi?” Jeri akasita kidogo. “Kwani unashida na mama?” Geb akamuuliza tena alipomuona anasura ya wasiwasi. “Hapana. Ni dada.” “Dada gani tena?” Geb akauliza. “Mkeo!” Moyo wa Geb ukapasuka. “Nanaa!?” Akamuuliza. “Ndiyo. Tumekuwa tukiwasiliana. Anaulizia hali ya watoto wake. Lakini nimekuwa nikimwambia tu wanaendelea vizuri ili nisimuhuzunishe. Alikuwa akilia sana nilipokuwa nikimpelekea watoto na kukataza asiwaguse. Sasa tokea jana ameniomba niwapige watoto wake picha, kisha  nimtumie. Lakini kwanza nilisita kumpiga Liv. Alikuwa akilia sana, karibu siku nzima. Na pili nikaona sio sawa kufanya bila kumuomba bibi yao. Maana aliniambia nisiwe nakwambia wewe chochote, ila yeye.” Jeri akajieleza.

“Lakini kaka, mama ni mama tu. Hata kama anatabia mbaya au chafu, lakini mama anayetaka watoto wake, ni mama mzuri. Mkeo yule ni mzuri sana. Wasura, umbile na moyo. Angeweza kuondoka kwako akaolewa kwingine na asikumbuke wanae. Lakini hajaacha kuulizia watoto wake. Mruhusu awaone wanae, na awashike. Itamsaidia dada Liv. Anazidi kunyongea kila siku. Hafananii hata na mtoto wa humu ndani. Amekonda kama wale watoto wanaoishi kwenye nchi zenye vita! Bado anakumbukumbu zile mbaya za mimi kumpeleka kwa mama yake na kumkatalia asiguswe na mama yake. Ni kumbukumbu mbaya sana kwa mtoto yeyote yule. Najua ni ngumu, lakini bosi wangu, kaza moyo kwa ajili ya wanao. Futa hiyo kumbukumbu mbaya kwa mwanao. Mwache mama yake amshike. Hata kama utataka amshike sehemu ya nje. Hadharani tu. Hata dakika moja tu. Mwache. Mnawaadhibu watoto wenu nyinyi wenyewe.” Kimya.

“Samahani lakini kama nimevuka mipaka. Na mimi ni baba. Tunapitia changamoto kama zenu, lakini zinatofautiana tu majina. Usifikiri mtoto wako huyo ni mdogo. Hapana. Liv ni mkubwa na anaelewa kila kitu. Kama ukimchunguza vizuri, utagundua hanipendi kabisa. Nikiingia tu, na akajua nipo mahali, hataniangalia kabisa, kwa kuwa anajua ubaya niliokuwa nikimtendea yeye na mama yake. Nafikiri anakubali nimchukue akidhani pengine namrudisha tena kwa mama yake, lakini najua kwa hakika asingekubali hata niwe naye sehemu moja.” Jeri akaendelea.

“Na pia nafikiri ameanza kujua ninakompeleka siko kwa mama yake, ndio maana kila nilikokuwa nikimpeleka akaanza kukataa kushuka kwenye gari. Aligoma kushuka mara kadhaa kucheza na Fili na wadogo zake. Kanisani ndio mara ya mwisho ikabidi turudi tu nyumbani. Bibi yake alipomlazimisha kushuka kwenye gari, alilia huyo mtoto, mpaka watu wote waliokuwepo pale nje kanisani walituzunguka pale kwenye gari. Tukarudi nyumbani na hatukuwahi kwenda tena kanisani. Sasa huwezi kujua hata wewe anakufikiriaje, akijua unajua anakopitia, na wewe uko kimya tu! Utamuharibu kabisa mtoto wenu ambaye ni mzuri, sababu ya matatizo yenu. Mmemuadhibu huyo mtoto vyakutosha. Sijui lakini, ni ushauri tu kaka.” Jeri akanyamaza na Geb akanyamaza. Liv alikuwa kimya, akiangalia cartoon zake kwenye tv, pembeni ya baba yake palepale nje barazani, huku Magesa akizunguka kwenye walker yake. Akicheza. 

“Kaka mtu anakua haraka huyo! Anampita dada yake sasa hivi.” Jeri alisifia kama kubadili mazungumzo. “Barua uliyopewa unikabidhi mimi, iko wapi?” Geb akauliza bila maelezo mengi, lakini Jeri alielewa ni barua gani. “Nilimpa bibi. Lakini alinionya nisikwambie. Tafadhali usiniharibie mahusiano yangu na bibi.” “Unaweza kumwambia anaruhusiwa kuja kuwaona watoto.” “Hiyo dada alikataa kwa kuwa bibi alinionya asiwaguse. Na yeye akasema hawezi kumtesa mtoto wake.” “Mwambie utamruhusu kuwashika.” “Kweli bosi wangu!?” Jeri akajisahau. Geb akabaki akimwangalia kwa jicho la tangia lini mimi na wewe tunataniana. 

Lile jicho likamsaidia kurudisha akili za Jeri  kazini. “Ngoja nimtumie ujumbe sasa hivi.” Jeri akajirudi kwa haraka na kutuma ujumbe kwa Nanaa. ‘Kwa nini usije kuwaona tu?’ Akamtumia huo ujumbe Nanaa. ‘Niheri nisiwaone kabisa, kuliko niwaone wakiwa wanalia. Siwezi Jeri. Nitakufa mapema sana.’ ‘Naweza kukuruhusu uwashike.’ Nanaa akakaa kwa haraka. ‘Kweli Jeri?’ ‘Kweli dada.’ ‘Basi nisogezee mpaka nyuma ya ukuta. Sitaingia ndani.’ ‘Kwa nini dada?’ ‘Shida yangu ni watoto Jeri. Sitaki kuja nakuibua matatizo mengine mwishowe nikazuiliwa kabisa hata kuona wanangu. Naomba niletee wanangu kama ulivyoniahidi, tafadhali usinibadilikie.’ ‘Hapana dada, siwezi kubadilika. Wewe njoo. Ukifika unijulishe nitoke.’ ‘Hapa nishatoka nyumbani.’ ‘Sawa dada. Lakini kuwa mwangalifu.’ Geb akamuona Jeri anacheka. 

“Nini?” Akauliza. “Dada anaonekana amefurahi huyo! Tayari yupo njiani. Ona jumbe zake.” Geb akapokea ile simu. Akazisoma na kumrudishia simu yake Jeri bila kuongeza neno. Jeri akarudi kwenye gari kama kulisafisha kidogo ili watoto wa bosi wakiingia wakute pasafi. Baada ya muda Jeri akarudi tena. “Bibi amefanya vizuri kumtoa yule dada hapa. Japokuwa alitaka umuoe, lakini hakuwa akipenda watoto kabisa. Na yeye alikuwa akikuogopa sana. Anasema huingiliki.” Geb akanyamaza. Jeri akaona aondoke tu.

Chako Ni Chako Tu.

Baada ya kama dakika 45 hivi, Nanaa akawa amefika. Akampigia simu Jeri. Jeri akarudi kwa Geb akiwa anakimbia. “Dada amefika.” Geb akamsaidia kuwapandisha watoto kwenye gari. “Naomba kuwa mwangalifu.” “Sawa bosi.” Jeri akatoka na watoto. Geb akarudi ndani kwa haraka sana. Moja kwa moja chumbani kwa mama yake akitafuta barua aliyokuwa ameachiwa na Nanaa. Akahangaika bila mafanikio.

Huku kwa Jeri akazunguka nyuma ya ukuta, akamuona Nanaa. Akashituka sana kumuona na tumbo kubwa, akajua ni mjamzito. Akasimama. “Nakushukuru Jeri.” “Mama!” Liv alishituka sana kumuona mama yake. Nanaa akamsogelea

Liv. “Nina hamu na wewe Liv.” “Beba mama! Beba!” Liv akaanza kulia. Nanaa akaingia ndani ya lile gari akapiga magoti mbele ya kiti cha mwanae, akajikuta akilia sana. Akamkumbatia Liv kwa muda mrefu. “Mama!” Liv akaanza kumbusu mama yake kila mahali. Nanaa alikuwa amekata nywele. Lakini Liv aliweza kumtambua mama yake.

Akamwangalia Magesa wakati Liv akiendelea kumbusu. “Hata siamini kama ni mwanangu huyu! Amekuwa mkubwa sana. Ana afya nzuri! Sidhani hata kama ananijua mimi kama ni mama yake.” Akarudisha macho kwa Liv, alikuwa akimvuta. Nanaa akamtoa kwenye kiti chake huku akifuta machozi. Akahamia naye kiti cha mbele. Akakaa akiwa amempakata.

“Nyonyo!” Liv alivuta gauni la mama yake. “Husahau tu! Maziwa hamna tena Liv. Yameisha yote. Unakula vizuri? Mbona umekwisha hivyo? Tumbo linauma?” Nanaa akamuuliza kwa upendo. Lakini Liv akatingisha kichwa akikataa kuwa haumwi. Akamlalia mama yake kifuani.

“Njaa inauma?” Akakubali. “Naomba kaniletee chakula chake nimlishe. Tafadhali Jeri. Nitakusubiri hapa hapa.” “Nikuache naye!?” “Hata kama ukiondoka naye, lakini kaniletee chakula chake nimlishe mimi mwenyewe.” Kwa kuwa Jeri aliogopa kurudi kwa bosi wake bila watoto wote.  Akamtaka Nanaa amrudishe na kumfunga kwenye kiti chake ili akafuate chakula. Liv alilia sana. Hakutaka mama yake amuache. Mwishowe Jeri akaamua amuche tu na mama yake, akimuomba asiondoke pale. “Siwezi kukimbia naye. Nitakuwa mwaminifu kwako Jeri. Nenda tu ukaniletee chakula chake. Anaonekana ananjaa kweli. Nijie na begi lake la diaper, nimbadilishe kabisa baada ya kula. Nisaidie Jeri.” Jeri akaondoka kurudi kwa Geb.

Geb akashituka sana. “Ameniambia hataweza kukimbia naye. Mtoto amelia sana bosi wangu. Nimeshindwa kumchukua. Lakini amemwambia mama yake ananjaa. Ndio amenituma chakula. Anataka akamlishe, akilala ndio tumrudishe. Sidhani kama ni jambo baya.” “Na siku hizi hali vizuri. Ngoja nikupe chakula chake umpelekee.” Geb aliandaa kwa haraka chakula cha Liv alichokuwa amekataa kula tokea asubuhi. Akakiweka kwenye bakuli lenye mfuniko, akampa Jeri na begi lake. Jeri akatoka kwa haraka huku akiomba Mungu Nanaa awe ametunza ahadi yake asiwe amekimbia na mtoto.

Na kweli, akamkuta Nanaa amesimama na mtoto wake akimsubira. “Asante dada yangu.” “Nisingeweza kukimbia naye.” Nanaa akaingia tena ndani ya gari. Akaanza kumlisha Liv chakula huku yeye amepiga magoti, mtoto wake amekaa kwenye kiti chake. Magesa alikuwa akimwangalia tu mama yake. “Umekua mkubwa baba! Nakuombea sana. Ipo siku Mungu atatupa nafasi yakufahamiana. Umesikia Magesa? Mimi ni mama yako. Na ninakupenda sana.” Jeri alijikuta machozi yakimtoka. “Mungu yupo na nyinyi Liv. Umesikia mama? Kila kitu kitakuwa sawa. Nawaombea kila siku. Mkono wa Mungu upo juu yenu. Hakuna silaha yeyote itakayosimama juu yenu ikafanikiwa.” Nanaa aliendelea kuongea na watoto wake taratibu huku Liv akimwangalia.

          Liv alikula chakula chote huku akimwangalia mama yake kwa makini sana. “Bado unao tu mtandio wako wakunyonyea?” Nanaa akamuuliza huku akicheka kwa upendo. “Huo hauachi popote. Ukitaka alie, mpokonye huo mtandio. Atalia mpaka awe mwekundu.” Jeri aliongeza nakumfanya Nanaa alie sana. “Nirehemu Mungu wangu. Warehemu wanangu. Usiwalipishe wanangu kwa kosa nililotenda mimi.” Jeri alimsikia Nanaa akiomba kwa kuugua sana kwenye hicho kiti cha nyuma alichokuwa wamekaa watoto wake, yeye amepiga magoti. Gari ilikuwa kubwa na ina nafasi yakutosha tu. Kutoka kiti hadi kiti kingine kulikuwa na nafasi. 

“Dada! Naomba usilie. Utaliza na watoto. Muda ulipewa na hao watoto ni mfupi sana. Jaribu kutumia vizuri.” “Ni kweli Jeri. Nakushukuru.” Akamtoa Liv kwenye kiti, akaenda kukaa naye kiti cha mbele baada ya kumbadilisha diaper na nguo iliyokuwa imechafuka kidogo. Alishamfuta vizuri. Akamkumbatia huku akimbusu kila mara. Nanaa alikuwa na namna anayomshika huyo mtoto. Wakati wote alimpapasa mwanae mpaka analala. Na Liv aliitambua mikono ya mama yake tokea mtoto. Akamrudisha kwenye kiti chake. Akamfunga vizuri. Akambusu mara kadhaa, akashuka.

“Mungu wangu akutendee mema Jeri. Akuonekanie siku utakayomuhitaji kama mimi. Nakushukuru sana, tena sana.” Machozi yalikuwa yakimtoka Nanaa. “Amina dada. Unafikiri lini utakuja kuwaona tena?” “Mmmh! Sidhani. Sijui lini nitaamka vipi. Afya yangu kama unavyoniona. Mbaya zaidi nimeishiwa nguvu kutoka ndani. Sina nguvu na sina sababu ya kupambana tena. Sidhani hata kama huu mwezi nitamaliza Jeri.” “Usiseme hivyo dada.” “Kwa jinsi ninavyojisikia na vipimo vya huko hospitalini! Madaktari wenyewe hawajui nimebakisha siku ngapi. Ndio maana nilikuwa nikikusumbua unitumie picha za wanangu niwoane. Sijui kama nitakuja kuwaona tena. Naumwa tokea ndani ya moyo. Nimepigwa haswa, tokea ndani ya nafsi yangu. Lakini Mungu akiniongezea siku, nitakujulisha tu. Nije kuona tena wanangu.”  Nanaa akafuta machozi.

“Nakuelewa dada yangu. Nakuombea uzima. Upone. Uje ulee wanao.” “Amina na asante Jeri.” Akaona Magesa anamwangalia kwa makini sana. Alimsindikiza kwa macho kila mahali na kumtizama kila anachofanya kwa dada yake. “Naomba ni mbembe hata kidogo, kama atakubali.” “Hamna shida.” Jeri akamruhusu. Akaenda kwa haraka kule alikokuwa amekaa Magesa. Akafungua mlango. “Naomba nikubebe kidogo tu mwanangu.” Magesa alitulia kimya huku akimtizama na macho kama ya baba yake. Rangi ya mama, sura kama Geb. Nanaa akambusu, kisha akamtoa pale kwenye kiti. Akambeba kisha akamuweka kifuani. Alipitisha mikono yake yote juu yake, akamkumbatia kwa nguvu sana. 

“Sijawahi kukusahau Magesa mwanangu. Nakupenda na ninakuombea sana.” Nanaa aliongea na mwanae huku amemkumbatia. Alipomuona ametulia, akarudi kukaa naye kwenye gari pale pale mbele. Akamfanyia kama anavyomfanyiaga Liv. Jeri akashangaa analala hapo hapo. Wote wakacheka. “Alikuwa amechoka.” Nanaa akanong’ona huku anashuka. “Ipo nguvu ya ajabu kwenye mikono ya mama, dada yangu. Ni siri ambayo Mungu mwenyewe ndio anajua.” Jeri aliongea kwa hisia huku akimuhurumia Nanaa.

Geb!

Huku nyuma baada ya Jeri kuondoka tena, Geb akarudi tena chumbani kwa mama yake. Akaanza kuisaka tena ile barua. Akaikuta chini kabisa kwenye droo aliyokuwa anasita kufungua tokea mwanzo. Lakini ilibidi ajikaze baada yakufungua na kupekua kila mahali na kuikosa. Kumbe ilifichwa kwenye droo ya chupi na sidiria za mama yake. Alijua wazi Geb hawezi kufika huko.

“Geb!” Ndio neno alilokutana nalo juu ya bahasha. Mwandiko wa Nanaa. Akajua ndio yenyewe. Akaifungua hiyo bahasha kwa haraka kama asiye na imani kama bado ipo. Ilionyesha wazi ilisha funguliwa. Akajua mama yake alishaisoma. Akaipiga picha kwa kutumia simu yake. Mbele na nyuma. Akairudisha vile vile, pale pale alipoikuta. Akatoka kwenda kusoma nje barazani, alipokuwa amekaa na watoto wake. 

~~~~~~~~~~~~~

Wakati anatoka tu, na Jeri naye akawa anarudisha watoto. Geb alimuona kama aliyekuwa akilia. “Kwema?” Geb akauliza huku akitoa watoto kwenye gari. Alianza na Liv. “Amekula vizuri kweli. Mama yake amempakata, akalala.” “Na Magesa naye?” Geb akauliza. “Utashangaa nguvu ya mama. Si unamjua Magesa asivyopenda kushikwa na mtu? Basi leo amemuangalia mama yake mpaka akambeba. Alimpakata na kumbembeleza kama vile Liv. Si unajua vile dada anavyomshikaga Liv?” Geb hakujibu.

Alishachukuliwa na hisia mpaka vile Liv alivyokuwa anapenda mikono ya mama yake, huku akibembelezwa na nyonyo. Hapo anakuwa hana rafiki wala undugu. Mpaka aridhike ndipo anatoka kwenye mikono ya mama yake. “Basi ndio leo alivyomfanyia na Magesa. Alilala hapo hapo mpaka tukamcheka. Lakini…” Jeri akanyamaza. Geb akamwingiza Liv ndani. Akarudi kumchukua kaka yake. Kisha akatoka tena.

“Ulisema lakini. Lakini nini?” “Dada ni mgonjwa. Halafu hivi unajua ni mjamzito?” Nusura Geb aanguke. “Anatetemeka mikono kweli! Hata sijui amefikaje hapa!” Kimya. “Nilimwambia ni lini aniambie atataka kuwaona tena watoto. Lakini nimemsikiliza, ni kama amejikatia tamaa. Ni kama aliyekuja kuaga wanae. Hadhani kama atakuja kupona tena. Anasema ameishiwa nguvu kutokea ndani kabisa. Hawezi kupambana tena. Na huko hospitalini wanamuhesabia siku za kuishi. Inaonekana majibu aliyopewa huko hospitalini si mazuri. Ila dada ni mgonjwa sana. Anaonekana amejikaza tu kufika kuona wanae.” Jeri alimsimulia kila kitu, akamuacha na habari zilizovunja mifupa ya bosi wake. Akamuaga, yeye akarudi ndani.

~~~~~~~~~~~~~

Alipiga magoti nakuanza kulia mbele za Mungu, asijue chakufanya. Ni kweli Nanaa amemuumiza sana. Leo anasikia ni mjamzito wa mtoto wa Malii! Lakini ni mama wa watoto wake. Grace naye alishampitisha kwenye maandiko ya bibilia 1koritho 13:4-8. Geb alibaki amepiga magoti. Asijue afanye nini. Akakumbuka anayo barua kutoka kwa Nanaa. Ipo kwenye simu yake. Hamu yakumsikiliza ikamwingia. Akatoa simu yake, akaanza kusoma akiwa pale pale amepiga magoti.

‘Geb mpenzi wangu, nimekukosea sana. Najua hakuna jinsi unaweza hata kunisikiliza tena, lakini naamini ipo siku Mungu atakupa rehema yakunisamehe. Nashukuru kwa kuniruhusu kuendelea kuishi hapa, lakini Geb, kumbuka hii nyumba tulihamia mimi na wewe. Wote wawili ndio ilikuwa mara yetu ya kwanza kuhamia hapa. Nakumbuka usiku wetu wa kwanza chumbani kwetu, ulinisisitiza na kuniomba nikutengenezee ‘home’. Ukasema hili jengo halina maana kama sisi wote hatutakuwepo humu ndani na kama hakutakuwa na amani. Nakiri kuivunja hii nyumba kwa mikono yangu mimi mwenyewe. Sina chakujitetea. Nakutetea hata mbele za Mungu, ulifanya kwa nafasi yako. Tena kiuaminifu sana. Sijawahi pata mapenzi kama uliyonipa Geb. Nakiri, na ninakutetea mbele za Mungu, hata mbele za watoto wetu hapo baadaye. Hakika huna hatia Geb. Upo sahihi kuniacha. 

Japokuwa nimeshindwa kutimiza nilichokuahidi, lakini nakuahidi kukuombea. Nimetubu. Na nitaendelea kutubu kwa kutokukwambia ukweli wote na kuishia kukuumiza mpenzi wangu. Najua Mungu atanisamehe na kunisikiliza. Nimeambiwa unatafutiwa mke ili uoe. Nakuahidi kukuombea mpenzi. Nitakuombea bila kuchoka ili Mungu akupe mwanamke atakayekupa yale yote niliyoshindwa mimi kukupa. Na asikuumize kama nilivyokuumiza mimi. Nakuombea faraja na amani ile ipitayo fahamu zote, ikufunike Geb. Najua unaweza ukaona haitawezekana kwa yale niliyokusababishia. Lakini Geb, Mungu yupo. Jipe muda tu, ipo siku Mungu atarejesha furaha yako kwa upya.

Hili jengo na vitu vyote vilivyomo humu ndani ni vya thamani sana. Lakini haviwezi kukamilika kama wewe na watoto hampo humu ndani. Sitaweza kuishi humu ndani peke yangu. Hata hivyo naona itakuwa mateso makali zaidi kwa Liv. Analia sana akiniona. Anataka nimshike, wakati umeweka masharti magumu sana kati yangu na wanangu, Geb. 

Ni heri niondoke wazoee kuwa hawana mama, kuliko hivyo wanavyolia nakushindwa kuwabembeleza wanangu. Inaniuma kuliko nitakavyokueleza. Unajua jinsi nilivyokuwa nikiwazaa kwa shida. Ilikuwa kufa nakupona ili wao wazaliwe. Sikubahatika kuwa na mama. Ningependa wanangu wanione. Lakini sio kwa mateso ya kiasi hicho Geb. Sitaki wanangu walipe garama ya kosa langu. Ni heri niondoke tu. Naamini Mungu atawasaidia kwa namna nyingine. 

Sitarudi tena hapa. Kuwa huru kuuza tu. Najua hutaweza kuja kuishi tena humu kwa yale yaliyotokea humu ndani. Hata mimi sijaweza kupata usingizi tangu usiku ule. Imekuwa mateso matupu. Kwa hiyo kuwa huru kufanya chochote na hii nyumba yako. Mimi nakwenda kuanza upya, sehemu nyingine.

Hakika nakushukuru Geb. Asante kwa mapenzi ya kweli uliyonipa. Nakuombea kila la kheri. Mungu akujalie hekima ya kuwalea watoto wetu vizuri. Mungu azidi kukufanikisha katika kila eneo la maisha yako.

Nanaa.’

Hiyo barua haikuwa faraja hata kidogo kwa Geb, ila hukumu ambayo hakujua afanye nini. Alikaa pale akirudia kuisoma bila kuridhika. Alikumbuka pressure kali sana iliyomsumbua Nanaa kipindi ni mjamzito wa Magesa. Lakini akapambana mpaka akamzalia mtoto. Nanaa sio wakutangaza kifo. Hata madaktari walimkatia tamaa, lakini yeye alisimama akitia moyo kila mtu hata wauguzi akiwaambia wasiogope. Lakini leo anasikia amepoteza tumaini kabisa! “Lakini mtoto sio wangu!” Geb akajitetea nafsini kwake.

Ni yeye pekee, mwanamke wa kwanza aliyemuonyesha kumpenda kwa dhati. Hata barua yake ilijaa mapenzi matupu. “Hakuna mwanamke atakayekuja kunipenda kama Nanaa.” Geb akawaza. “Lakini ni muongo, Malaya. Alikuwa akinionyesha kunipenda na kunijali mimi kumbe huku anavulia nguo wanaume wengine na…” Akanyamaza. Akabaki pale chumbani akiwaza hili na kujitetea kwa lile, mpaka muda wa kwenda nyumbani kwa Grace ulipofika.

Kilio cha Liv!

Wakati anakaribia kuamsha watoto wake ili awaandae waende nyumbani kwa dada yake, Liv aliamka nakuanza kumuita mama yake akiwa palepale kitandani. Geb akamsikia. Akajua anaota. Liv alilala akiwa amekumbatia na mama yake, anaamka yupo kitandani kwake, mama yake hayupo! Akaanza kulia akimtaka mama yake. Geb akaenda. Liv alipomuona tu akajisogeza mwisho kabisa wa kitanda chake, hataki baba yake amguse, anamwita mama yake. “Mamaa!”

Kilio kikali chakukataa hata asiguswe na baba yake kikamuamsha Magesa. Akakaa akisikiliza huku akimwangalia dada yake akilia huku akishindana na baba yake asimguse. Hakutaka kabisa Geb amguse. Magesa alipoona ile hali na yeye akaongeza nguvu. Geb yupo peke yake, watoto wote wawili wanamlilia. Liv haonyeshi ushirikiano hata kidogo. Hataki hata baba yake amguse, tena alilia kwa ukali huku akimtizama kama kumuonya asimsogelee. Ndipo akaamini aliyosema Jeri juu ya hasira ya Liv kwa baba yake. Geb alikaribia kuchanganyikiwa. Alikaa hapo zaidi ya nusu saa, Liv akilia kwa uchungu sana. Alifanikiwa kumtuliza Magesa, akamlisha na kumbadilisha nguo. Mpaka anamaliza, Liv alisha jibembeleza na kupitiwa na usingizi pale pale kitandani akiwa amejikunja, na kushikilia mtandio wa mama yake. Geb hakutaka hata kumbadilisha. Akambeba kwa tahadhari, na kumwingiza kwenye gari mpaka nyumbani kwa dada yake.

Nyumbani kwa Danny na Grace.

Alimkuta mama yake na Grace wapo kimya na msichana wa kazi, watoto hawapo. Kulikuwa na vyakula, vinywaji, mpaka keki ya mapacha ilikuwepo. Grace alishaiandaa, lakini hakuwepo Danny wala watoto wao. Geb akawashusha watoto wake, Liv alimuweka kwenye kiti pale pale nje bustanini, na Magesa alimuweka kwenye walker yake akawa anatembea kila mahali huku akimlinda asigonge meza na kuangusha vitu. Liv alijikunja kwenye kiti akanyamaza kimya. Bibi yake alimuita mara kadhaa akitaka ambebe, lakini Liv hata hakumtizama. Wakaamua kumuacha. Kimya kikazuka.

Lisaa la kwanza likapita. La pili na la tatu. Geb hakutaka kuuliza kwani mbali na salamu, hata wenyeji wake walikuwa kimya kama alivyowakuta. Walikaa pale mpaka saa tatu usiku ndipo wakaona gari ya Danny ikiingia getini. Grace akasimama kuwasogelea.

“Mbona umechelewa kurudisha watoto mpaka wamelala, wakati nilikwambia nimewaandalia sherehe hapa?” Grace aliuliza kwa upole tu. Lakini mama yake, Geb na msichana wakazi waliweza kusikia. “Nimekwambia nimechoka na matambiko ya kwenu. Umekusanya ndugu zako mje kuwalisha wanangu madawa yenu? Haitakaa ikatokea tena Grace. Nimekwambia inatosha, naomba uniamini mimi kuwa inatosha. Wanangu wameshasherehekea sherehe yao na watu wakaida. Wamecheza, wamekula na nakufurahi na watu wakaida, inatosha.” Walimsikia Danny akijibu kwa jazba. Grace akanyamaza.

Mara wakamuona Sara anashuka kwenye gari. Alikuwa amevaa nusu uchi. Kikaptura kilifika kwenye hips, na kiblauzi chepesi. “Nikusaidie watoto?” Sara akamuuliza Danny. “Wewe shusha mizigo yako tu. Nitabeba watoto.” Danny akajibu nakumshangaza Grace. Sara akazunguka nyuma ya gari nakuanza kushusha mabegi yake.

“Ni nini kinaendelea Danny? Kwani Sara anahamia hapa?” Grace akauliza tena. “Ndiyo na kumfukuza kama walivyomfukuza mama yako na Geb, hutaweza na sitakuruhusu. Hapa ni kwangu na mimi nina uhuru wa kumwalika nimtakaye. Huwezi kuishi naye, ondoka uniache nifanye ukarimu kwa ninayemtaka. Nenda kaishi na watakatifu wenzako.” Danny akajibu huku akimfungua Fili mkanda.

“Watu msioweza kuishi na watu. Mmezoea kutumia kila mtu! Mkiona hamnufaiki na huyo mtu, mnamfukuza. Mmemfukuza Sara kwa kuwa ameshindwa kuwa kijakazi wenu. Hawezi kuwatumikia kama mlivyozoea kututumia wengine. Mkamfukuza kama mlivyomfukuza Nanaa. Kawazalia watoto, mmeona idadi ya watoto mnaowataka imetimia, tena Mungu naye akafanya kosa la milele. Kawapa wakike na wakiume, harakaharaka. Mmeshamkamua mtoto yatima. Mnayejua hana pakulilia wala kushitaki, mkamnyang’anya watoto wake. Akiwa bado na maumivu yote. Yakuzaa na kubakwa, mkamfukuza kama mbwa! Sasa hapa ndio mmefika. Sara atakaa humu ndani atakavyo yeye. Ni kwangu, na hamna wakuniambia kitu. Nyinyi si mnajidai ni wachawi sana, kalogeni sasa.” Danny alikuwa akiongea kwa jazba. Ukali ulizidi mara tatu yake. Alikuwa akiingia na kutoka huku akiongea.

Alipomaliza, akaenda kupiga teke meza           ya keki. “Mmefanikiwa kunilisha mimi mauchawi yenu, komeni kwa wanangu.” Akaisambaratisha ile keki yote huku wakimwangalia. Akaimwagia na mchanga kabisa. “Marufuku kuja kufanya ibada zenu za matambiko hapa. Mlinipata mimi, sitaki muwafikie wanangu. Komeni kabisa.” Danny akaingia ndani kwa hasira. 

Hapo ndipo walipojua kwa nini hawawaoni watoto wa Danny wala Danny mwenyewe nyumbani kwao. Na kujua kwa nini Grace anakonda. Danny akatoka tena. “Naombeni muwatoe hao watoto nyumbani kwangu. Tafadhali sana. Mnaninyima usingizi.” Danny akaanza tena. “Kwanza nawasifu. Mnaroho mbaya ambazo ni nyinyi tu watatu ambao mnazielewa roho zenu. Na mnajijali nyinyi tu watatu. Hata watoto wenu wenyewe, damu zenu, mnashindwa kuwajali! Halafu eti leo ndio mnakuja nyumbani kwangu mnajidai mnataka kusherehekea birthday za watoto wangu, kama si uchawi wa mchana kweupe ni nini!?” Danny akawasogelea.

“Yaani leo mnajidai mnaupendo wakuwapenda wanangu wakati watoto hao wawili tu, mmeshindwa kuwajali! Liv amekwisha kama kitoto chenye ugonjwa wa mifupa. Mtoto amebaki mifupa mitupu! Mbavu zinahesabika! Halafu bila aibu, mmemjaza dhahabu na magauni ya garama! Nyinyi ni binadamu gani jamani! Hamumuogopi huyo Mungu wenu mnayejifanya mnamfahamu? Watoto wadogo hivyo, mnawatoa kwa mama yao, eti wanalelewa na bibi! Kwa kipi na kwa nini? Ndivyo mganga wenu alivyowatuma nini? Ili muendelea kutajirika. Ukute mlikuwa mnatafuta watoto wakuwatolea matambiko ili muendelee kutajirika.” Danny akaendelea.

“Sasa kama Grace hakuwaambia, ndio nawatangazia wazi kabisa nyinyi kina Magesa. Hamtakaa mkawa karibu na wanangu. Hata iweje, ninawatenga na kuwafuta kwenye maisha ya wanangu. Logeni hao hao watoto wenu. Sitaki niwaone karibu na mtoto wangu hata mmoja. Na nishaongea na walezi wangu, jumapili ijayo nawapeleka Iringa, wakabatizwe kabisa. Watulie kwenye dini iliyonilea mpaka leo. Haya, naombeni ondokeni.” Geb akasimama bila kujibu kitu.

Akambeba Magesa. Akaenda kumfunga kwenye gari, Liv akajua zamu yake inakuja. Hakutaka kushikwa. Akateremka pale kwenye kiti taratibu, akaongoza njia kwenye gari. Geb akamfungulia mlango. Akaanza kuhangaika kupanda akionyesha wazi hataki kusaidiwa. Geb alibaki akimwangalia. Alipambana mpaka akaweza kupanda mpaka kwenye kiti chake. “Naweza kukusaidia kufunga mkanda.” Geb aliongea naye kwa upole. Liv akanyamaza. Geb akajua hata yeye anajua hawezi kufunga mkanda. Akamfunga. Wakati anamalizia, akasikia gari ya mama yake ikitoka getini. Na yeye akapanda gari yake akaondoka. Grace alikuwa kimya kabisa. Hakujibu kitu, akaingia ndani.

Baada Yakuona Wanae.

Nanaa akatoka pale akampigia simu daktari wake anayemuona kliniki. “Nimeamua tu kutoa huyu mtoto kama ulivyoshauri.” “Unauhakika Nanaa?” Lyamu akauliza. Kimya. “Uko wapi wewe Nanaa? Unatetemeka mpaka mimi huku nakusikia! Utakufa barabarani. Hebu njoo huku hospitali ya Tumaini. Chukua taksii.” Nanaa akashuka tena kwenye daladala, akapanda taksii kama alivyoshauriwa na daktari wake. Akaomba apelekwe hospitali ya Tumaini.  

Ukweli alikuwa na hali mbaya. Kila alipokumbuka sura ya Liv, alizidi kulia asijue kama aishi au afe. Kuendelea kuishi na ile mimba nikukubali kufa. Kuitoa, ndio kupona kwake. Presha ikazidi kupanda. Mara nyingi pressure inapokuwa juu, mimba huwa hutoka zenyewe. Lakini sio watoto wa Nanaa, kitu kilichokuwa kikimshangaza kila mtu aliyekuwa akimpima akiwa mjamzito na pressure aliyokuwa nayo. Alizidi kutetemeka, hata yeye akajua safari hii anapata stoke. Yule dereva taksi akamfikisha pale hospitalini, lakini akashindwa hata kumuacha aende peke yake. Akamshika mkono mpaka ndani ofisini kwa dokta Lyamu.

Daktari alipomuona tu akaomba nesi ampe sehemu ya kupumzika. Akaomba achomwe sindano ya usingizi. Lyamu akachukua vitu vyake vyote, akafungia kwenye ofisi yake. “Mwacheni alale leo. Kesho nitakuja kumwangalia.” Daktari akamwandikia dawa. Akamuacha alale.

~~~~~~~~~~~~~

Aliporudi tena kesho yake nakumuuliza swala la kumtoa mtoto anayehatarisha maisha yake, Nanaa akasema amebadili mawazo. “Mbona hata sishangai!” Nanaa akacheka akionyesha amedhoofu. “Sasa hivi nipo tayari kufa. Sina hofu tena.” “Na Liv?” Lyamu akamuuliza akijua kilio chake ni Liv. Nanaa akanyamaza. “Unajua sijawahi kukutana na Nanaa huyu! Nanaa ninayemfahamu mimi ni mpambanaji. Mbishi mpaka kwa kifo! Ni nini kimekupata Nanaa?” “Huyu mtoto sio wa Geb, dokta. Geb hataki hata kuniona. Amenifukuza na kuninyang’anya watoto wangu wote mpaka yule uliyenizalisha wodini.” “Magesa?” Daktari akauliza. “Huyo huyo. Kwani na wewe umenizalisha wangapi?” Lyamu akacheka nakutingisha kichwa.

          “Niliwaona jana kwa kuibiwa na dereva wao. Magesa amekuwa mkubwa, hata hanifahamu. Huyu mtoto nilibakwa na rafiki yake Geb, tena mbele yake Geb. Sina sababu ya kuishi. Sina kinachonibakiza hapa duniani. Kama huyu ananiua, acha nife naye tu, nirudi naye huko alikotoka.” Lyamu akamwangalia Nanaa. Akamuongezea dawa. Akalala.

 ~~~~~~~~~~~~~

Mambo yanazidi kuwa mambo.

Nani amelikoroga na nani analinywa sasa hivi?

Kila nyumba inawaka moto. Hakuna kwenye amani wala utulivu. Si kwa Nanaa aliyebakwa, wala kwa kina Magesa. Sasa hivi Nanaa yupo tayari na kifo huku mwanae Liv, yu mahututi - mzima.

·       Sara aliyetakiwa kuwa mke wa Geb, Sasa yuko na Danny, kwenye nyumba yake na Grace. Kwa makubaliano Yepi? Hata Grace hafahamu.

·       Mama G, amelemewa. Danny amempasukia bila hofu kama aliyetumwa. Umri umeenda watoto wanahitaji ungalizi zaidi, na Liv ndio hawataki kabisa.

·       Geb amejua ukweli wote, lakini akajitetea nafsini kwake kwa yale aliyoumizwa na Nanaa. Lakini Grace alimwambia, kuna mapengo hayazibiki. Hata Liv amemthibitishia hilo. Cheko na dimpozi vya Liv, vimepotea kabisa. Hataki hata baba yake amguse.

Nini kitaendelea? Nani wa Nani kwenye simulizi hili?

Mahesabu yameshapandana.

Grace amesema ndoa yake ilishaisha ila anaendelea

kuomba, mpaka lini!?

·       Sara ambaye alikuwa aolewe na Geb, sasa yupo kwa Danny.

·       Nanaa anasubiria kifo chake hospitalini.

·       Geb ameamua kuwa baba wa watoto wanaonza kumbadilikia. Liv

aliyezoea kuwekwa kifuani na baba yake akisikilizia furaha, huku

akigugumia ‘Mhhhhhh!’ siye Liv huyu.

Nani wa Nani?

Endelea kufuatilia.

 

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment