Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu ya 51. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu ya 51.

Geb akaingia kwa tahadhari kama asimuamshe. Nanaa akamwangalia. “Umeambiwa ulale Nanaa. Hata dawa hazifanyi kazi!” Nanaa akacheka kidogo. “Labda ukilala pembeni yangu halafu ukanikumbatia, ndipo nitalala.” “Wewe unataka nifukuzwe hapa.” “Hawawezi bwana. Shida yao wanataka nilale. Ukinishika shika, ndio nitalala vizuri. Nina hamu na wewe Geb. Hatujalala wote muda mrefu!” “Hata mimi. Basi ngoja nikawaweke sawa hao manesi. Nakuja.” Geb akatoka. Akazungumza na manesi. Kwa kuwa kilikuwa chumba chake tu, wakamruhusu.

“Wamesema hamna shida.” Geb akarudisha jibu. “Muone alivyofurahi!” “Hata mimi nataka kukushika. Unafikiri nilikuwa sina hamu na wewe?” Nanaa akacheka. “Ila ujue ndio nimejifungua leo.” “Nakumbuka Nanaa! Siwezi kuvuka mipaka bwana. Nashika tu.” Nanaa akacheka sana. Geb akapanda kitandani upande usiokuwa na dripu, mabusu yakaanza. Baada ya muda, wakaona walale tu, hali ilishakuwa mbaya.

~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda mlango ukafunguliwa. Mama G alikuwa amerudi na Grace wakiwa na vyakula. “Sasa hapo si alitakiwa kulala mtoto!?” Nanaa akaanza kucheka. “Mwache mama. Amechoka.” “Basi kazi unayo. Liv naye akija anataka alale hapohapo! Baba yake naye alale hapohapo! Magesa naye alale…” Mama G kama akakumbuka kitu. “Kwanza mtoto mwenyewe yuko wapi?” “Wamemchukua. Maziwa hayatoki mama. Alikuwa ananyonya, lakini hashibi. Ndio daktari amesema aanzishiwe ya kopo. Halafu wamesema atakuwa analala huko huko. Watakuwa wakimleta kidogo tu. Presha bado ipo juu. Wanataka nilale.” “Pole Nanaa. Ni kweli utahitaji kula vizuri na kulala.” Wakakaa.

“Lazima ule sana. Utakuwa ukikamua kama kwa Liv. Halafu nitakuwa nikiwapelekea hao manesi, wawe wanampa ya kwako wala si ya kopo. Najua hupendi.” “Ndio maana nakupenda mama yangu.” “Ndio ukazane kula sasa.” “Kwani hilo unawasiwasi nalo mama yangu?” Mpaka Grace akacheka. “Nanaa!” Grace akatingisha kichwa. “Hapa tuzungumze, huku nakula.” Nanaa akatoa wazo. Mama G akacheka.

“Hapana Nanaa. Unatakiwa kula na kurudi kulala. Sio uzungumze.” Geb aliongeza akiwa amelala pale pale kitandani kama mgonjwa. “Kumbe upo macho! Haya aamka na wewe ule.” Geb akakaa. “Nitaomba msaada kwa mtoto mama. Uwe unakwenda kumwangalia.” “Wala usijali. Mbona hapa nishaweka mipango yote. Liv anahamia kwa Grace kwa muda. Nikitoka tu hapa naenda kumwangalia walipomuweka mume wangu.” Mama G akacheka kidogo. “Alivyofurahia!” Grace akamtizama mama yake.

“Kumbe! Mtoto yupo kama Magesa, mme wangu! Kasoro rangi tu.” “Naomba kusikia hiyo mipango mpaka mwisho mama.” Geb alimkatiza. “Haya baba. Mwenzio ninafuraha ya ajabu. Kwanza sikutegemea. Nilivyo..” “Mama wewe! Si umeambiwa useme mipango kwanza? Acha kuzungumzia furaha zako kwanza, bwana. Mweleze Geb hiyo mipango.” Grace alimkatiza. Nanaa akawa anacheka tu.

“Haya. Nitaenda kuchukua ratiba nzima ya huyo mtoto. Nijue saa ngapi anaogeshwa. Muda gani anakula na muda gani anatakiwa aje huku. Hata kama ni asubuhi, nitakuwa nakuja kumuogesha mwenyewe na kumpa maziwa. Nikiona yupo sawa, ndio namuacha mpaka jioni. Lakini hapo nitahakikisha namuacha na maziwa yakutosha. Kwanza natamani kama wanipe niende naye kabisa.” “Mama!” Nanaa akashangaa. “Ndio vizuri nilee mwenyewe. Kwanza ndio nitakuwa na amani na usafi wake, maziwa anayopewa, na nitaweza kuwa na wote wawili pamoja na dada yake. Naweza kukuletea asubuhi na jioni.” Wazo likasikika zuri.

Geb na Nanaa wakaanza kushawishika. “Kwanza huwezi jua. Wanaweza kuanza kuchanganya vitu vyake na watoto wengine waliozaliwa na magonjwa hatarishi. Halafu akaambukiz..” “Bwana mama acha kutuogopesha.” Geb alimkatisha. “Sasa ulifikiri wanahuyo mtoto mmoja tu huko kwenye wodi za watoto!? Siku hizi hakuna kunyanyapaa. Watoto wote wanachanganywa pamoja.” “Mama wewe? Hapa ni hospitalini wapo makini bwana. Acha kuwatia hofu Geb na Nanaa.” “Na manesi wenyewe wanakuwa wanachoka. Swala la kupitiwa ni ubinadamu kabisa. Huwezi kuwalaumu chochote kikitokea.” Mama G akasisitiza.

“Kwa hiyo umesema unaweza kukaa naye nyumbani?” Geb akauliza. Mama G akafurahia moyoni. Akajua mtego wake umenasa. Aliwaogopesha kwa makusudi. “Mkitaka wenyewe. Sitaki kuingilia.” Akajibu mama G, kiuungwana. “Eti Nanaa?” Geb akamgeukia Nanaa. “Kwanza hapa nishaanza kuwaza kama bado yupo salama! Unaweza kuta watoto wako wengi, akalia mwanangu wakampuuza. Naomba ukazungumze na daktari wamruhusu tu aondoke na mama. Si wamempima wanasema ni mzima kabisa?” “Ndivyo walivyoniambia.” Geb akajibu. “Basi naona aende tu na mama.” Bila kuongeza, Geb akasimama na kutoka nje.

Wakamuona Nanaa analia. “Umeona umemuogopesha Nanaa? Bwana usilie Nanaa wifi yangu. Mwanao atakuwa mzima.” “Nalia kwa furaha mwenzio. Ujue mimi nilipozaliwa tu, mama akafariki. Hakuna aliyetaka kunichukua. Sasa kuona hivi mnawapokea wanangu, nimefurahi sana. Asante mama. Kumbe hata ningekufa wanangu wangelelewa vizuri tu!” “Kwanza wala usilie. Kufa haufi. Maneno yote yale yalinitoka ili kumuogopesha Geb, chaubishi. Nilijua bila kumtia hofu ya maradhi kwa mwanae, wala asingekubali niondoke na huyo mtoto wakati mimi namtaka sana huyo mtoto.” Wote wakacheka.

“Hivi mama wewe ukoje? Kwa nini kutumia lugha ngumu hivyo? Si ungesema tu kama unataka kuondoka na mtoto kuliko kutia watu hofu?” Grace alilalamika. “Kwani wewe humjui Geb? Hapa nilikuwa nimepanga kumtia hofu zaidi mpaka akubali. Ni hivyo tu kakubali haraka. Nilimwandalia maneno ya hofu zaidi ya haya.” Nanaa alizidi kucheka. “Mbishi sana Geb, kama baba yake! Akiamua jambo ndio basi. Habadiliki kirahisi. Sasa mimi huwa namjua pakumpatia.” Mama G akawa amefurahia kweli kuwa mtego wake umenasa.

“Sasa utawaweza wote wawili!?” “Wala usitie hofu. Ninavyomtaka huyo Magesa. Acha nikahangaike nao tu. Asubuhi na jioni utakuwa na wanao hapa. Mchana nakuacha upumzike.” “Nakushukuru mama yangu. Nahisi hata presha itashuka.” Wakaanza stori. Mama G akiwa amechangamka kweli. Furaha ilionyesha usoni. Kila mtu akajua.

Geb akarudi. Mama yake akanyamaza. “Unacheka kwa sauti sana mama jamani! Nanaa anatakiwa kupumzika.” “Heee! Hata kucheka haturuhusiwi?” “Si ndio maana ameachwa hapa? Nanaa akiendelea hivyo tutachelewa kutoka hapa. Na mimi nataka arudi nyumbani kwa watoto.” “Kwani wamenikubalia kuondoka na Magesa?” Mama G akahoji. “Wamesema daktari wa watoto ametoka kumuona sasa hivi. Anaonekana kila kitu kipo sawa. Hata wao wameona ni wazo zuri kama kuna mtu wa kumwangalia kwa karibu, achukuliwe tu.” Mama G akajisahau tena, akaanza kushangilia.

“Punguza sauti mama bwana!” Geb akalalamika. “Halafu uwe unamleta kama ulivyosema. Usije ukajisahau naye.” Geb alimtahadharisha. “Sasa maziwa nitapataje na wewe!? Mbona kama hufikirii.” Mama yake akambadilikia. “Hapa nitaletwa na mawili. Kuleta chakula kwa mama yake, na kuchukua maziwa. Nyinyi nikamulieni hayo maziwa. Myahifadhi vizuri, nikiwa nakuja, nakuja kuyafuata.” “Mama alivyofurahi! Mipango mingiii. Kazi tena basi?” Grace akauliza. “Nimepata kijana mwaminifu sana. Atanishikia kwa muda. Acha nimlee mume wangu.” “Na kwa Liv ulisema hivyo hivyo.” “Sasa yule si ndio mwenyewe? Alelewe na nani kama sio mimi?” Geb akabaki akimwangalia na kutingisha kichwa.

Mama G alijawa mipango mingiii, wote wakabaki wakimsikiliza. Aliacha vyakula hapo hospitalini. Cha Nanaa, Geb na wauguzi wote waliomsaidia Nanaa kujifungua. Akapewa mtoto, wakaondoka na kumuacha Nanaa na Geb. Wakala, na kurudi kulala.

~~~~~~~~~~~~~

Maisha yakaanza. Watoto wanaletwa asubuhi na jioni. Nanaa akawa akiwanyonyesha wote wawili huku akiwa na uhakika wa maziwa mengine ya Magesa kwenye chupa. Mida ambayo anajua Nanaa analala mchana muda mrefu, Geb alitoka kwenda kazini. Wakati mwingine mpaka jioni. Anarudi hospitalini kulala na Nanaa, akiwa ameshapitia nyumbani. Anaoga na kubadili nguo. Wakati mwingine alichukua nyumbani nguo za kesho yake kazini.

Magesa na Liv walikuwa wakiletwa hospitalini wakiwa wasafi na wanavutia. Ungependa kuwaangalia. Mama G alishika usukani wa hao watoto, hata Nanaa hakuwa na wasiwasi. Kwanza aliona wanalelewa vizuri na mtu mwenye uzoefu zaidi yake. Na ni bibi yao. Aliyekuwa akiwapenda sana. 

Baada ya siku tatu tu, Geb akamwamisha Jeri, dereva wake wa kazini wa muda mrefu sana, nyumbani. Jeri alikuwa mwaminifu na aliheshimiana na Geb. Yeye ndiye aliyemuona anafaa kumuweka kuwa dereva wa watoto wake tu. Alimwambia kila siku asubuhi awe anaripoti nyumbani, kwa mama G. Atamwambia kitu gani chakufanya siku nzima. Kama ni kumtuma mahali au kazi za pale pale ndani. Basi afanye kwa wakati huo yeye na Nanaa wakiwa hospitalini. Akakabidhiwa ile gari ya Geb ya kifahari, yenye viti 8, waliyosafiri nayo kwenda Marangu kwenye harusi ya Malii. Kwa hiyo Jeri ndio akawa dereva wa nyumbani. Mama G akawa akikaa nyuma na watoto, Jeri anawapeleka atakapo na hao watoto.

Yeye Geb akahamia kwenye gari yake ndogo nyingine yenye milango miwili tu. ‘Sport Car’ nzuri ya rangi ya maruni na nyeusi. Hata hilo gari pia lilikuwa la garama sana na ya starehe tu. Mtu wa kawaida asingeweza kununua kwa garama yote hiyo, ikiwa haina uwezo wa kubeba watu wengi, isipokuwa starehe tu. Starehe ya Geb, ilikuwa ni magari na kitanda. Alimwaga pesa kwenye magari na vitanda vya kifahari bila kufikiria mara mbili. Alijiambia ni lazima alale sehemu nzuri, na afikishwe anapotaka na usafiri mzuri.  Katika hilo ndipo ungeweza kuona utajiri wa Geb. Lakini si vinginevyo. Wakati mwingine aliporudi nyumbani alibadilisha gari hiyo nakutoka na gari nyingie. Inategemea na aina ya safari. 

~~~~~~~~~~~~~

Nanaa akawa anapata muda mwingi wamapumziko. Hakuwa na majukumu mengi isipokuwa yeye na akiletewa watoto kwa muda mfupi. Kilichomshangaza na kumchanganya Nanaa zaidi ni pale Geb aliponyamazia na kutozungumzia kabisa juu ya yale aliyoongea Manka, mke wa Malii. Hakujua kinachoendelea kichwani kwa Geb. Hiyo ilizidi kumsumbua Nanaa na kumuongezea wasiwasi kila akikumbuka mkasa wake na Malii. Kila wakati maneno ya mkewe Malii yalikuwa yakijirudia na kujisikia hofu.

Matibabu yakaendelea. Baada ya siku chache, presha ikaanza kushuka. Alikaa hospitalini siku 11. Ndipo daktari akawaruhusu warudi nyumbani. Nanaa na Geb walifurahia sana. “Lakini bado unahitaji mapumziko Nanaa. Sijajua ni nini kinachofanya presha yako isirudi kuwa yakawaida kabisa. Vipimo vyote vinaonyesha huna tatizo lakukufanya usipone kabisa. Kwanza wewe bado mdogo. Hutakiwi kuwa na maradhi ya pressure.” Daktari huyo wa mambo ya moyo alikuwa akizungumza na Nanaa alipokuwa akipita kumwangalia.

“Labda kwa kuwa nipo mbali na wanangu.” Nanaa akaongeza huku akificha ukweli wa kile kinachoendelea moyoni mwake. Hakuna aliyejua hofu iliyomjaa Nanaa. Malii aliapa ni lazima atampata. Hilo hakulisikia kwa mkewe Malii tu, hata Malii mwenyewe alishamwapia. Na wala hazikuwa siku nyingi. Lakini pia hakumwambia Geb. Kitendo cha kumsikia mkewe akirudia mbele za watu, akajua Malii hatanii. “Asije kuja kumwambia Geb ukweli wote!” Hiyo ndio iliyokuwa hofu iliyokuwa ikimuweka macho Nanaa.

“Tuombe Mungu hiyo ndio iwe sababu. Sio vizuri kuanza kusumbuliwa na pressure kwa umri wako. Hata hivyo kesho nitakuruhusu, pengine itasaidia. Lakini nilazima upunguze mawazo na ukapumzike huko nyumbani.” “Nitafanya hivyo.” Nanaa akajibu.  

Nanaa Atolewa Hospitalini.

Nanaa aliamka akiwa na nguvu na amechangamka  kweli kweli kwa furaha yakurudi nyumbani kwa watoto wake. Oliva na Magesa. Tena Magesa aliyekuwa amebebewa utabiri. Nanaa hajawahi pata shida ya kushika mimba. Anazaa kutokana na anavyotaka Geb! Alitaka wa kike, Nanaa akamtolea binti wa nguvu. Haya Mzee Magesa alitabiri juu ya Magesa, bila ya kuhangaika, Nanaa akatoa Magesa wa nguvu! Mungu ampe nini Nanaa? Nani mwanamke kama Nanaa? Nanaa anaheshimika kwenye ukoo huo. Nanaa muendelezo ukoo! Umesikia sifa za Nanaa hata kutoka kwa mke wa Malii, Manka. Unaambiwa, ‘Nanaa maji marefu’. Marafiki walioliana amini, leo wanashikana mashati kwa ajili ya Nanaa yule aliyekuwa akivaa jalalani! Mungu amempandisha juu, na amemjaza dhahabu! Gari ya kifahari inamngojea hapo nje ya majengo hayo ya hospitalini, dereva ni Geb, ili amrudishe kwenye jumba la thamani! Utamwambia nini Nanaa?

          Akaingia bafuni kuoga. “Mbona sikuoni kama unavaa kitu zaidi ya chupi tu?” Geb alimfuata bafuni. “Nilishamaliza mwenzio. Hapa nipo safi.” Nanaa akajibu huku akitaka kuvaa. “Mbona sasa hukuniambia!?” “Wewe Geb! Tupo hospitalini.” “Nimebanwa Nanaa. Nisaidie mpenzi wangu. Kidogo tu.” “Hapa hapa kwenye bafu la hospitalini!” “Kidogo tu, tutamalizia nyumbani.” Geb akaendelea kubembeleza. Nanaa akacheka.

Geb akajua ndio amekubaliwa. Akaanza kumfaidi Nanaa hapo hapo bafuni. Hata Nanaa alikuwa na hamu na Geb. Alikuwa mtundu na mtulivu sana kwenye mapenzi. Popote na wakati wowote alipomshika Nanaa, alifurahia penzi lake. Mpaka akakamilisha raundi ya kwanza, ndipo akamwachia. “Daah! Asante Nanaa wangu. Hali ilikuwa mbaya!” “Hata mimi nilikuwa na hamu na wewe. Asante kunivumilia Geb. Tokea wakati ule wameniweka bed rest mpaka leo! Unastahili pongezi. Tukifika tu nyumbani, tupandishe juu. Kama lisaa tu, ukate kiu yote ndio tukakae na watoto.” “Lisaa tu!? Nitamwambia mama tunahitaji muda Nanaa. Ni siku nyingi sijalala na wewe mpenzi wangu. Bado mwenzio nakuhitaji. Akili yangu haijatulia.” “Basi nitaenda kukutuliza. Usijali.” Geb akamkumbatia na kumbusu kwa muda nakumuachia.

Nanaa akaanza kuvaa. “Nakushukuru kwa kunizalia watoto wazuri, Nanaa. Na pole kwa shida unazopitia mpaka kuwaleta hapa duniani. Unapambana kweli bila kuwakatia tamaa. Ndio maana wanazaliwa wazima. Asante.” Geb aliongea kwa upendo mpaka ikamwingia moyoni Nanaa. Akamgeukia. “Na mimi nakushukuru kuwa na mimi hapa hospitalini, Geb. Hujui nikiasi gani unanifariji. Ungeweza kuniacha hapa, ukawa na watoto nyumbani. Na ingeeleweka tu. Lakini umenichagua mimi. Umeniweka kwenye chumba 
kizuri. Madaktari wazuri. Najua inakugarimu sana. Nakushukuru. Asante.” Geb akacheka.

“Nakupenda Nanaa. Nakuthamini kuliko nafsi yangu. Sijawahi kupenda hivi. Amini nakupenda. Wewe ni wangu. Si kile kitanda wala nyumba inayoweza kukalika kwa furaha, kama wewe haupo. Nikilala pembeni yako ndio naweza kulala vizuri.” Nanaa akacheka. “Asante.” Nanaa akashukuru kwa upole huku akimfikiria Geb. Alitamani kumwambia kila kitu asimfiche chochote kile. Lakini akaogopa. “Anaweza kubadilika. Ukweli unauma! Heri nijiachie tu.” Nanaa akawaza.

~~~~~~~~~~~~~

Akaruhusiwa, Geb akaenda kulipia, akarudi chumbani kumchukua Nanaa. Walitoka pale chumbani wakimshukuru Mungu wao. Hawakuacha kuwashukuru wauguzi wote, tena kwa kuwashika mikono. Ndipo wakatoka hapo. Wakati wapo kwenye gari Geb akaanza. “Naomba nikuombe kitu Nanaa.” “Nini?” “Tuingie mahali kidogo tupumzike hata masaa manne tu.” “Geb! Na watoto?” “Mama alishachukua maziwa yakutosha asubuhi. Tukifika nyumbani watakuganda. Heka heka zakulea zitaanza. Mimi tena itabidi nisubiri. Naomba twende kwa muda huo mfupi tu. Angalau na mimi unipe hayo masaa machache. Nipumzike tena kifuani kwako. Nilale hata masaa mawili bila kelele. Nikiamka ndio twende.” Nanaa akamuhurumia.  

Alijua tabia ya Geb yakutafutia usingizi mwilini mwake. Hasa kifuani. Akishalala ndipo alipokuwa akitoka kifuani kwake, nakulala kwenye mto. Tena baada ya Nanaa kumchezea nywele na masikio. Alikuwa akilala usingizi mzito. “Au umechoka?” “Hapana Geb. Hata mimi nitafurahia wakati mtulivu na wewe. Twende tu.” Geb akatoa gari hapo kwenye viwanja vya hospitalini mpaka kwenye hoteli aliyojua italeta utulivu. Palikuwa kimya, na ipo maeneo mbali na barabara kubwa. Akalipia, wakapata chumba, akarudi kwenye gari. Akamchukua Nanaa na kuelekea kwenye hicho chumba.

Geb & Nanaa

Hapa ndipo Nanaa alipojua kama Geb alikuwa na hamu naye. Alihangaika na mwili wake bila papara, akiwa anafurahia kila kitu. Walifanya mapenzi kwa muda mrefu. Nanaa akafananisha na uchu aliokuwa nao mara ya kwanza mjini Morogoro, wakiwa ndio wamepata fursa kwa mara ya kwanza kufanya mapenzi. Alifanya mapenzi na Nanaa kwa taratibu na tahadhari, mpaka aliporidhika. Ndipo akajilaza hapo kitandani, nakupitiwa na usingizi mzito huku amemshikilia Nanaa.

Alipoona amepotelea usingizini, akajivuta pembeni na kuchukua simu ya Geb, akamtumia ujumbe mama G. ‘Ni mimi Nanaa. Bado unamaziwa yakutosha?’ Baada ya kama dakika 13 akajibiwa. ‘Kwani mnakuja saa ngapi? Mwanao anakazi ya kula tu. Hana kingine anachokifanya hapa.’ ‘Geb ndio amelala. Sijui ataamka saa ngapi!’ ‘Sasa wewe muendekeze huyo, ulezi utakushinda.’ ‘Amechoka sana.’ ‘Sawa.’ Nanaa akacheka baada yakusoma ile ‘sawa’ ya mama G.

‘Akiamka tu, tunakuja bwana mama. Wewe mpunguzie kula.’ ‘Mtoto unahatari mbaya wewe! Yote hayo ili baba yake asisumbuliwe?’ ‘Kumbe? Walitukuta hao!’ Nanaa akajibu. ‘Basi umama umeshakushinda.’ ‘Hamna bwana. Nakuja mama yangu.’ ‘Tena uje kweli. Ikifika saa 12 jioni hajaamka, lazima umwamshe huyo. Uje nyumbani. Acha kumfuatiliza Geb. Anapenda kupendwa kama huyu mwanae hapa anayenirembulia macho. Njoo Oli wangu.’ Nanaa akacheka huku akimsikiliza akimwita mjukuu wake. ‘Bye. Nitakuona baadaye.’ Nanaa akaaga. ‘Na uwahi Nanaa. Usinitanie.’ ‘Nakuja mama. Usiwe na wasiwasi.’ Alipotuma huo ujumbe wa mwisho, Nanaa akazima simu kabisa. Akajilaza pembeni ya Geb. Mpaka saa 12 jioni ndipo wakaamka.

Nyumbani.

Walirudi nyumbani wote wakiwa wametulia na mawazo yapo kwa watoto wao tayari kwa ulezi. Walikuta marafiki na familia zao wakiwasubiria. Geb akamwangalia mama yake nakutingisha kichwa. “Nichakula cha usiku tu baba. Nilitaka watu waje, tumshukuru Mungu pamoja. Basi.” Mama G akajitetea kwa Geb. “Kwani huwa huwezi kusubiri mama jamani? Yaani ndio Nanaa amerudi tu. Hata hajapumzika, ushaita watu!” “Si mmetoka kupumzika nyinyi!?” Geb akajua hawezi kushindana na mama yake. Akanyamaza.

Walikuwepo hapo marafiki wa Geb, wakike na wakiume. Waliosoma pamoja na baadhi wa ofisini kwake. Mama G alitaka walete na watoto wao. Kwa ajili ya kusherehekea birthday ya Liv na huyo Magesa ambaye alishaanza kuchangamka. Sababu ya kucheza sana na Fili, Oliva alishaanza kutembea bila hata ya kuanguka. Wengi walisema aliwahi kutembea. Mama G alimuomba mama mmoja ambaye ni rafiki yake anayefanya mambo ya catering. Akamletea chakula kizuri sana hapo nyumbani. 

Walimwimbia Oliva, akakata keki kwa mikono yake bila kisu. Akaanza kumlisha kila mtu aliyeambiwa na anti yake. Grace ndio alikuwa akimwambia amlishe nani na baada ya yupi. Basi Oliva alifanya huku akicheka. Walimchukua video nyingi tu huku akipigwa picha. Vilijaa vicheko. James naye alikuwepo.

Nanaa alirudi kukaa kwenye kochi na watoto wake. Liv akimchezea nywele huku akimwangalia Magesa. Hakuna furaha ungemwambia Nanaa ipo ya zaidi ya vile anavyojisikia wakati ule. Alizungukwa na watoto hao wawili, ambao kila mtu alikuwa akimsifia na kumpongeza. Mara nyingi watu walimuomba kumshika Magesa, nakumrudishia. Mwishowe bibi yake akataka akalazwe. “Hata hamu haijaniisha mama jamani!” “Kelele sana hapa, ndio maana anashituka shituka. Kesho siku nzima nitakuachia.” Nanaa akacheka na kumkabidhi.

Wakabaki wakiangaliana na Oliva. Akamuona Liv ameshuka kutoka kwenye kochi, anakwenda kuchukua kitambaa kama mtandio aliozoea kumpa mama yake ajifunike ili anyonye. Akarudi nao. Akasimama mbele ya Nanaa huku akicheka. “Liv wewe! Huoni aibu mbele za watu? Bwana umeshiba. Nimemuona dad akikulisha. Nenda kacheze na Fili.” Liv akabaki amesimama mbele ya mama yake. “Nenda kacheze kidogo Liv. Huna njaa bwana! Haya nenda mama yangu. Nenda eeh!” Nanaa akabembeleza lakini Liv akamgomea. Japo alikuwa katikati ya wenzake. Wakicheka na kelele nyingi, lakini macho yake wakati wote yalikuwa kwa Nanaa, mpenzi wake. Geb akawaona.

Akawasogelea. “Eti Liv anataka nyonyo jamani wakati ameshiba!” “Huyo sio kwamba anataka nyonyo sababu ya njaa. Liv anahamu na wewe. Akiwa na hamu na wewe, ziwa pekee ndilo linamfariji huyo mwanao, kama hujamjua. Ameona wamemchukua mtoto, ndio akaona na yeye amepata nafasi.” Geb akamjulisha Nanaa. “Kumbe!” “Wewe huoni leo hataki kucheza na yeyote. Hata Fili amemkatalia kucheza. Anataka awe hapo karibu na wewe tu.” “Jamani Liv wangu! Hata mimi nina hamu na wewe mama yangu. Sasa kwa kuwa wewe ni mtoto mzuri, twende chumbani ukanyonye vizuri, halafu unipe habari za hapa.” Liv akacheka.

Geb akataka kumnyanyua, akakataa. “Mama hawezi kukubeba Liv. Mimi nataka kukubeba tu ili nikupeleke huko chumbani. Namsaidia mama.” Nanaa alikuwa amesimama. Liv akajificha kwenye gauni alilokuwa amevaa mama yake. Alilivuta upande, akajifunika usoni. “Huna utakalomwambia huyo akakubali. Akishaamua kitu huyo, kaamua.” Mama G akatoka akamkuta Geb anaongeleshana na mwanae. “Njoo mtoto mzuri.” Geb alimjaribisha tena. Akamchungulia kutoka kule alikokuwa amejificha uso, akamcheka baba yake akarudi pale pale. Mpaka Nanaa akacheka.

“Na tabia yake ndio hiyo hiyo. Unaweza dhani cheka yake ndio anakukubalia! Kumbe wala. Anakuchekea huku anakukatalia. Wewe mshike mkono mpande naye hizo ngazi. Wala usimbembe.” Bibi yake  akatoa wazo. Nanaa akainama. “Eti Liv?” Bado alikuwa akicheka. “Muone vidimpozi vyake! Haya twende.” Wakaanza kuondoka. Wakamuona Geb anawafuata nyuma. “We Geb! Hebu rudi hapa. Wote wapo hapa kwa ajili yenu. Sasa sio muende mkajifungie huko!” Geb akacheka. “Narudi mama. Nawasindikiza tu.” “Mmmh!” Mama G akaguna. Mpaka Grace naye akacheka.

Geb alirudi kwa rafiki zake, akamuacha Nanaa anamnyonyesha Liv huku wakizungumza. “Nilikuwa na hamu na wewe Liv!” Liv akamwangalia huku ziwa la mama yake lipo mdomoni. Akaendelea kunyonya. “Unampenda Magesa?” Nanaa akamuuliza. Liv akatingisha kichwa kukubali. “Wewe ni dada mzuri Liv! Lazima umpende sana mdogo wako. Umesikia Liv? Akilia tu, unambembeleza nakumpa chupa yake yamaziwa.” Nanaa akaendelea kuzungumza naye taratibu huku wamejilaza kitandani. Liv ananyonya huku akimsikiliza mama yake. Nanaa alikuwa akimchezea nywele taratibu huku akimshikashika kwa upendo mpaka wote wakalala.

~~~~~~~~~~~~~

Geb alikuja kumuamsha ili anywe dawa. “Kaka hajaamka?” Nanaa akauliza huku akimsogeza Liv. “Alivyojikunja hapa, kama kitoto cha paka!” “Huyo mtoto anakupenda sana Nanaa. Ukikosekana hata siku mbili tu, anabadilika. Kila mtu anajua.” “Jamani Liv wangu! Sijui ni vile nilivyokuwa nikizungumza naye sana wakati yupo tumboni?” “Ni Mungu tu amekupa mtoto anayekupenda.” “Namuombea na mdogo wake awe hivyo hivyo. Lakini sijisikii vizuri hivyo anavyokuwa anapewa maziwa ya chupa. Hana connection na mimi! Hatakuwa na hisia kwangu. Kuanzia kesho namwachisha kabisa maziwa ya kopo. Namrudisha kifuani.” “Utachoka Nanaa. Magesa ni mlaji. Wewe muulize mama. Anakula kama mchwa.” Nanaa akacheka. 

“Kwa kuwa umerudi mwenyewe, jiongezee muda naye. Mnyonyeshe, lakini pia usimwachishe na chupa. Utachoka kuamka usiku kila mara.” “Nitaangalia. Sina kazi nyingine kwa sasa isipokuwa hawa watoto Geb. Nachoshwa na nini?” Geb akafurahia kuona akili ya Nanaa imetulia na anafikiria tu watoto au mambo ya pale nyumbani. “Mbona pako kimya?” “Ujue sasa hivi inakaribia saa 4 usiku? Watu wameondoka kasoro Danny nafamilia yake, James na Gozi ndio wapo bado wanazungumza. Naona Gozi alikuwa na haraka, lakini gafla yeye ndio amegeuka mwendesha kikao. Maneno hayamwishi. Ila nimemsikia Grace anataka waondoke.”

“Tumelala sana na Liv.” “Kwani hotelini hukulala?” “Sio sana. Nahisi nimekuja kumaliza uchovu wote hapa. Sasa hivi najisikia vizuri.” “Afadhali. Sasa itabidi huyo atoke hapo. Arudi kitandani kwake, mimi nichukue nafasi yangu.” Nanaa akacheka. “Ngoja nikamshukuru Grace kwa kumsaidia mama na kazi ya hawa watoto. Twende.” Geb akambeba mtoto. Wakatoka.

~~~~~~~~~~~~~

“Sasa huyo amebakisha maziwa ya mdogo wake kweli?” Grace akauliza, Nanaa akacheka. “Nilishakamua wakati nilipokuja tu. Nimempa mama tayari.” Nanaa akakaa. “Naomba nikushukuru Grace wifi yangu. Asante kwa kumsaidia mama na shuguli za hawa watoto. Nashukuru pia kwa kuja kuniona hospitalini.” “Karibu Nanaa. Nakuombea upone na Mungu akupe hekima uwe mama mzuri kwa wanao. Umejaliwa watoto wazuri sana. Kazi ni kulea tu.” “Asante kama unaniombea, maana ni kweli nahitaji maombi.” Nanaa akajibu.

“James anazidi kuzeeka!” Danny akatania. “Si mchezo! Wajukuu au maanko wawili! Mzee umekua dingi.” Gozi akaongeza wote wakazidi kucheka. Geb akarudi kukaa pembeni ya Nanaa baada yakumlaza mtoto. Mama G akamletea mtori. Bila kujivunga akaanza kula kwa juhudi zote. “Asante mama yangu. Mbona sasa Geb wangu hali?” “Nilikuwa na njaa kama sijala mwaka. Nimekula wakati mmelala na Liv.” Nanaa akamwangalia na kucheka. Akakumbuka shuguli waliyokuwa nayo hotelini.

Wakati Kunapoonekana Kuna Amani,

Ndipo Na Uharibufu hunyemelea.

Wakati stori zikiendelea kupamba moto, mida ya saa nne na nusu hivi, hata Danny na Grace walishasahau kama walishaaga, mlinzi akapiga simu. “Vipi?” Geb akapokea. “Malii yupo hapa getini na vijana wanne. Anasema ni marafiki zake.” Geb akanyamaza kidogo na kuangalia saa ya ukutani. Ukweli muda ulishakwenda. Wageni karibia wote walishaondoka. “Kuna nini?” Mama yake akamuuliza. “Malii yupo getini.” Geb akajibu. “Kwani ulizuia Malii asiruhusiwe kuingia humu?” “Hapana. Ila mlinzi anasema ana vijana wanne ambao Malii amewatambulisha kama rafiki zake. Amewaangalia kwenye orodha ya watu, hawapo kwenye system ndio maana anauliza.” “Labda ameona alete watu baki mje kuzungumza. Hamkuachana vizuri pale hospitalini wakati mmekuwa pamoja kwa muda mrefu sana. Ni bora kumsikiliza. Pengine anataka myamalize” Geb akasita kidogo.

“Wewe msikilize tu. Usiache kumsikiliza. Halafu maamuzi ndio fanya kwa wakati wako. Lakini si sawa kumzuia kuingia getini.” Mama G akasisitiza. Akiwa anasita sana rohoni Geb akaona asimkaidi mama yake pale mbele za watu wote. “Waruhusu waingie.” Geb akamjibu mlinzi, akakata simu na kurudi kukaa.

Moyo wa Nanaa ulipasuka kama kulikoangushwa chuma sakafuni. Tayari akakosa raha. Alitamani amwambie Geb asimruhusu, lakini hakujua atasema ni kwa nini. Akakumbuka ndoto mbaya aliyoota wakati yupo hospitalini, alipoota akiwa na Malii. Akahisi si kwema. “Naomba nikamalizie chakula changu chumbani.” Akamnong’oneza Geb. “Nisubiri twende wote.” Geb akamjibu taratibu. Nanaa hakuwa na ujanja. Ila kubaki.

Wakasikia kengele mlangoni. Geb akasimama kwenda kufungua. Wote walikuwa kimya kabisa. Wametulia wakimsubiria Malii na hao rafiki zake. Aliingia na vijana wakubwa na wageni kabisa kwao. Hawakuonekana na sura za kirafiki hata mmoja wao. Malii alipita kukaa, lakini wale vijana wakasimama.

“Kwema?” Akaanza mama G. “Tutajua yote baada ya kukamilisha kilichonileta.” Malii akajibu. Lakini si kama walivyomzoea. Alikuwa na sura ya tofauti waliyomzoea kumuona nayo. Mara nyingi mida ya jioni huwa anakuwa alishaingiza mwilini bia za Safari kadhaa. Lakini muonekano wa leo haukuwa wa

‘Safari’. Ni zaidi yake.

“Funga mlango na kushusha mapazia.” Malii akatoa amri kwa mmoja wa kijana aliyekuja naye na kuogopesha wenyeji. “Hee! Kwani vipi Malii mwanangu?” Mmoja wa wale vijana akamsogelea mama G nakumpiga ngumi ya nguvu kwenye shavu. Mama G akatema damu nyingi, kuashiria kupasuka kwa ndani. Hapo ndipo Geb akataka kusimama ili kumtetea mama yake, na yeye akapigwa teke la nguvu la tumbo, lililomtupa sakafuni. Hapo ndipo wakajua hali si shwari.

“Mimi ndio nimewafuata. Nimewaambia nataka kuzungumza na nyinyi. Acheni dharau zenu. Sijaja kumdhuru mtu. Ila mkileta ukorofi, na kusimama katikati ya kusudi langu, hakika sitasita kuwaumiza. Tulieni kimya. Nataka muda na Nanaa.” Kila mtu akamgeukia Nanaa na kurudisha macho kwa Malii. Hofu yakupitiliza ilishatanda mahali pale. Wote walishatoa risasi wakazishika mkononi.

“Naombeni muwafunge wote na muwasogeze wote pale pembeni. Sitaki kuingiliwa”


Malii akaamuru. Walitoa tape. Gundi kali ya plastiki nyeusi. Kubwa na pana. Wakawabandika mdomoni ili wasiongee au wasisikike hata kama wakitaka kupiga kelele. Waliwafunga wote mikono yao kwa nyuma. Ndipo wakawafunga tena kila mmoja, miguu yote miwili kwa pamoja, kwa kutumia gundi hiyo hiyo, kasoro Nanaa. Malii alimvuta kutoka pale alipokuwa amekaa kwenye kochi, akabaki amemshikilia huku wamesimama.

“Ukitulia, sitakuumiza.” Malii alizungumza naye akiwa amemkumbatia kiunoni. Akambusu, Nanaa akamkwepa. “Leo ndio unanikana mbele za watu!?” Malii akauliza nakushangaza kila mtu. “Mimi sio kama Zinda.” Malii akaanza. “Mimi ni mtu wa action. Vitendo tu. Sasa nimekuja kuchukua kilicho changu.” Malii akaendelea. “Nyinyi wote hamjui kilichokuwa kikiendelea kati yangu na Nanaa, baada ya Geb kutamka wazi wazi kuwa hamtaki Nanaa. Wewe James, ukiwa rafiki wa karibu. Mtu wa nyumbani. Umezuzuliwa na vijisenti vya Geb, ukaamua kumpa dada yako ili upate pakuvunia pesa, ukasahau kuwa Geb alimkana Nanaa.” Malii akatulia.

“Labda niwaeleze kwa kifupi. Mimi nilijua wazi hisia za Geb kwa Nanaa. Kwa kuwa mimi nilikuwa karibu sana na Geb kuliko nyinyi wote. Tuseme alikuwa akizungumza na mimi kuliko nyinyi wote. Nilijua alikuwa akimfuatilia Nanaa. Miaka yote tulikuwa tukisikia habari za Nanaa, lakini James alikuwa akimficha huyu dada yake mpaka siku ile ya birthday ya Fili ndio kila mtu akamuona Nanaa, nakusahau kama Geb alikuwa akimfutilia Nanaa. Lakini sio mimi. Mimi sikupagawa. Nikasema nifuate utaratibu. Kwa kuwa Geb ni mtu wangu, tumetoka mbali. Na wote tulijua kama Geb alikuwa akimfuatilia Nanaa.” Malii akaendelea.

“Usiku uleule. Sikutaka hata kupoe. Wakati watu wanaondoka. Mimi nikamwita Geb pembeni. Nikamuuliza, itakuaje juu ya Nanaa na wakati ule yupo kwenye mahusiano na Liz? Haya ndio yalikuwa majibu yake.” Malii akatoa simu aliyokuwa amemrikodi Geb akijibu juu ya Nanaa, na Liz. “Hamna kitu bwana. Mimi nilikuwa nikimuulizia tu.” Geb alisikika akijibu.

“Kiuungwana tu. Ili nisikanyage waya za umeme nikiwa nimeloa. Nikasubiri kuona kitakachoendelea. Nikasikia watu wakisema. Tena sio watu, ni huyo Gozi. Akaniambia Geb kavuta kifaa ndani. Yaani Nanaa. Nikashituka sana. Nikaamua kumtafuta tena Geb. Nikamuuliza, ‘Nasikia umemuhamishia Nanaa nyumbani kwako. Ndio umeamua kuchukua hatua?’ Haya ndio yakawa majibu ya Geb. “Acheni uzushi jamani. Nanaa yupo kwangu kwa kuwa James aliwaomba Grace na Danny waishi nae kwa muda. Sihusiki na Nanaa kuwepo nyumbani kwangu. Anasaidiwa tu na kina Grace. Yeye na kaka yake James wakiweka sawa mambo yao, ataondoka.” Geb akasikika akitoa jibu.

“Binafsi nikajua hilo jibu ni la jumla sana. Nikaamua kuwa muwazi kwa Geb. Nikamuuliza. Hakuna hisia zozote za kimapenzi? Kama mnavyomfahamu Geb, jeuri imemjaa. Akanyamaza. Nikaweka msisitizo. Nikauliza tena kutaka uhakika ili kusije kuwa na lawama baadaye. Nikauliza, ‘Unauhakika hakuna hisia za kimapenzi kwa Nanaa?’ Geb akanihakikishia kuwa yeye alikuwa akimfutilia Nanaa kama mdogo wa James tu, na si vinginevyo.” Malii akaendelea.

Nanaa alikuwa akilia sana. “Naomba niache Malii. Usiniguse.” Malii akacheka. “Nimekuhakikishia ukitulia, sitakuumiza Nanaa. Usifanye fujo. Hakika nitakuumiza.” Nanaa akaendelea kulia. “Tokea juzi najifunza kuvuta bangi kwa ajili yako. Usinikorofishe, nakuahidi sitakuumiza. Tulia.” Akaendelea.

“Basi. Kwa kuwa milionea Geb akawa amekiri hana shida wala hisia zozote kwa Nanaa, kama na nyinyi mlivyomsikia kwenye rikodi yake ya mwisho, mimi nikaanza kutupa ndoano kwa Nanaa. Tukaanza akiwa hanifahamu. Lakini jumbe na simu za hapa na pale kati yangu mimi na Nanaa zikaendelea. Kila siku nilikuwa nikipata nguvu yakuendelea na maisha baada ya kuwa kwenye ukurasa mmoja na Nanaa. Akasisitiza tufahamiane kwa kuonana. Nikaweka mipango. Tukaonana.” Malii akaendelea.

“Tulipokutana, nikajitambulisha bila kumficha. Nilimwambia kuwa nilimfahamu tokea tupo sekondari kwa kupitia kaka yake. Nikamueleza kila kitu. Nikamwambia hata siku ile ya birthday ya Fili na mimi nilikuwepo na nilimuona. Sema watu tulikuwa wengi pengine hakuniona vizuri. Nanaa akasita kabisa. Siku ya kwanza tukaachana akiwa anaonekana wazi anataka kukatisha yale mahusiano. Mimi niliendelea na jumbe zangu za kuomba radhi kwa kutojitambulisha vizuri tokea mwanzo huku nikimfariji kwa jumbe, mpaka Nanaa akasamehe. Mawasiliano yakarudi. Ninazo jumbe kibao zangu na Nanaa. Sitawaonyesha kwa heshima ya Nanaa.” Malii akaendelea.

“Nilimwambia ninaye mwanamke nataka kumuoa. Ila akinikubali, sitamuoa huyo mwanamke. Hapo napo Nanaa akasita lakini hakukataa moja kwa moja kwa umbali tuliokuwa tumefika mimi na yeye Nanaa. Ilikuwa ni week ya birthday yangu. Nikamwambia Nanaa. Akaniuliza ninataka zawadi gani, nikamwambia namuhitaji yeye. Tukazungumza sana na nikambembeleza. Nanaa akanikubalia tukutane, tukafanye mapenzi.” Kila mtu akamgeuka Nanaa, akainama huku akilia.

“Akaletwa na taksii mpaka nyumbani kwa Gozi. Nilimuomba aniachie funguo kipindi kile anakwenda Japan kwenye mambo yake ya kikazi. Basi, tukapata muda mzuri sana na Nanaa. Vilijaa vicheko, habari za hapa na pale. Nikajua Nanaa amenikubali kwa hakika.” Malii akaendelea.

“Kumbuka ombi langu la mwisho lilikuwa ni akubali nimuoe. Kuwepo pale kukamilisha mapenzi na mimi, nikajua nimepata mke. Sikutaka kupoteza muda zaidi, nikamvutia chumbani. Romance ikaendelea tukiwa kwenye ukurasa mmoja. Nikiwa nishamvua nguo zote, yupo kitandani, akiniona hali yangu mbaya kabisa, nilazima nilale naye, eti akanibadilikia! Akakaa na kujifunika. Hakika alinikatili vibaya sana Nanaa. Nililia kama mtoto nikimsihi angalau anisaidie tu. Ameshanionyesha mwili wake, amenibadili hali yangu, sijiwezi tena, anisaidie. Nanaa akakataa kata kata bila hata huruma hakuwa nayo.” Malii akaendelea.

“Hakuna mwanaume ambaye atafanikiwa kuona mwili wa Nanaa akabaki alivyo. Nanaa anavutia ndani bwana!” Nanaa akampiga kibao cha mdomo kwa haraka. “Kaka yangu yupo hapa. Mshenzi wewe!” Nanaa akaongea kwa hasira. Malii alimrudishia kofi la nguvu, likamsindikiza Nanaa sakafuni. “Wewe ndio mshenzi Nanaa.” Malii akamjibu kwa hasira akiwa ameshakasirika zaidi usoni.

          “Unajua madhara uliyonisababishia lakini? Kila mwanamke ninaye lala naye, nakuona wewe. Umeharibu ndoa yangu. Kila nikimshika mke wangu, au niseme aliyekuwa mke wangu. Maana nishampa talaka yake. Tena ni kwa sababu yako Nanaa. Nimeshindwa hata kufanya naye mapenzi kwa kuwa hafanani na wewe. Silali mchana wala usiku bila kukuona ukiwa umelala uchi kitandani. Unaniumiza kupita unavyofikiria. Nilikwambia siku ile tulipokutana mimi, wewe, Geb na Manka. Walipotoka nikakuomba. Nikakwambia nisaidie basi hata mara moja tu ili niweze kuendelea na maisha yangu kwa kuwa uliniacha pabaya. Unakumbuka uliondoka na kuniacha kama mbwa?” Malii akamuuliza Nanaa aliyekuwa akilia pale chini.

          “Nilikwambia wazi Geb hakupendi. Anachokupendea labda ni hiyo rangi na kiuno tu. Geb anapenda wanawake smart kama Liz. Ukanijibu kwa jeuri hata wewe ni smart. Kama wewe ni smart na kama kweli Geb anakupenda na kukuzalisha watoto wawili, ameshakuoa? Unaweza kusema hapana sababu ya hili au lile. Basi ni jibu hata kama anakushirikisha katika mali zake. Hata unajua anakiasi gani benki!? Unajua anamiliki biashara ngapi? Unajua anatengeneza kiasi gani kwa mwezi? Unajua anapokwenda kila siku asubuhi anapokuaga kuwa anakwenda kazini? Wewe unajua huwa anakwenda kwenye biashara ipi? Mtoto wa kichaga unayeijua pesa, unakubali kugeuzwa Fala! Anakufanya kama mbwa tu, hana hisia zozote zakimapenzi na wewe. Anachotaka ni hichi. Mashine ya kumfyatulia watoto, basi. Huna thamani yeyote kwake. Mimi ndio nilikupenda kwa dhati.”  Nanaa aliendelea kulia.

“Sasa sitaki tupotezeane muda. Nimefuata haki yangu, ili maisha yangu yaendelee na wewe nikuache hapa hapa ili uendelee kula na kulala bure. Maana ndio shida aliyojua Geb unayo wewe na kaka yako. Huna pakuishi, wala kaka yako hana uwezo wa kukulisha tena. Mchaga huyu wa kiume, amefilisika na amechoka kupambana hapa mjini ili aweze kukutunza wewe dada yake ndio maana amekusukumia hapa kwenye pesa ili ule na kulala bure. Huku akikubali uzalishwe bila ndoa wakati yeye mwenyewe James, hathubutu kuvulia nguo mwanamke yeyote yule. Anamsubiria mkewe.” Malii akacheka.

“Hakika James wewe ni mshenzi sana. Unatudhalilisha wachaga, James. Sisi ni wahangaikaji bwana! Huwezi kushindwa kuyamudu maisha kwa kiasi chakuuza dada yako! Yaani umeshindwa kumtunza dada yako mwenyewe, umeamua aje alalwe hapa ili ale na kula bure!?  Kweli wewe kiboko! Sasa kwa kifupi, nimeamua kuanza maisha mapyaaa. Nikatulie mahali kimyaaa. Lakini siwezi kuanza nikiwa na Nanaa kichwani mwangu. Nimekuja tumalize tulichoanza, ili..” “Haiwezekani Malii! Huwezi kunifanyia hivyo.” Nanaa alizidi kulia. 

“Labda hujanielewa Nanaa. Unanigarimu maisha yangu, kupita utakavyodhani. Hapa nilipo sina kitu wala mtu kwa sababu yako. Nimeuza kila kitu ikiwemo nyumba ya kaka yangu niliyokuwa nikiishi na Manka, ili niweze kuwalipa hao vijana, waje wanisaidie kukamilisha ndoto zangu. Natembea kama mjinga humo mabarabarani sababu yako! Nimezidisha pombe kwa ajili yako! Napenda ngono, lakini nayo siifaidi sababu yako! Kwa kifupi nimekuja kujikomboa na maisha yangu. Nimetangaza kufa leo, au kupona. Ilimradi unitimizie ulichokuwa umekianza mwilini mwangu. Sijaja kuomba. Ni heri nitoke maiti hapa, kuliko mzima ambaye hujanikamilisha. Wewe ndio unahatima yangu. Kufa au kuondoka hapa nikiwa tayari kuanza maisha yangu mapya nikiwa nimetulia akili.” Malii aliendelea.

“Hao vijana wanne, nimewalipa pesa za kifo chao. Niliwatahadharisha kuwa ni kazi ya kifo. Pesa waliyonitajia, huwezi amini. Lakini nimekubali kuuza kila kitu. Mpaka gari yangu, ili niwalipe kabisa. Waache urithi kwa ndugu zao kabla hatujaja hapa. Hawana chakupoteza tena. Lililotuleta hapa ni mimi kufanya mapenzi na wewe Nanaa. Basi. Na ninakuhakikishia, leo nitalala na wewe mpaka nitosheke ndipo nitakapoondoka hapa. Kwa hiyo naombeni mtulie.” Malii akawageukia wengine.

“Kilichotuleta hapa ni Nanaa tu. Na Geb.” Akamsogelea karibu Geb. “Usithubutu kufanya chochote, hakika nitakumaliza. Unajua nina hasira na wewe. Umenidhalilisha vyakutosha. Umemchukua Nanaa kutoka kwangu ukiwa huna mapenzi ya dhati kwake ila tu kututhibitishia wewe unayo pesa. Hakika tulia. Lasivyo utawaacha watoto wako wakiwa bado wadogo sana. Ninachuki na wewe, kukuua haitanisumbua.” Akampiga teke la nguvu kwenye miguu, kisha akamtemea mate. “Mshezi mkubwa wewe Geb. Leo nakuonyesha pesa sio kila kitu.”

          Akawageukia wengine. “Sasa nisikilizeni, hao vijana nitakao waacha hapa, wapo kikazi. Hamuwajui, hawawajui. Washachukua pesa zangu zote. Wameapa kunisaidia kukamilisha lengo langu. Hawatasita kuwadhuru kwa namna yeyote ile. Tulieni kimya ili mimi na Nanaa tukamalizane. Nitamwacha hapa hapa na yeye Geb aendelee kujifidia misaada yake.” Akamvuta Nanaa.

“Naomba niache Malii.” Nanaa alizidi kulia. “Unakumbuka ulivyonianza kwa mbwembe mpaka ukaniamsha na ukaniacha nakulilia? Sasa leo unaenda kumaliza ulichokianza mwilini mwangu. Ila nakupa uhuru wa kuchagua. Hapa kwenye kochi mbele ya kaka yako na Geb, au chumbani kwa Geb. Maana hapa sio kwako hata iweje. Geb anathamini mali zake kuliko mtu wala kitu chochote hapa duniani. Hutakaa ukamiliki chochote kwa Geb. Labda hao watoto aliokuzalisha. Mimi namfahamu Geb.” Nanaa akashika kochi kwa nguvu.

“Ooh! Kumbe unataka hapa hapa kwenye kochi? Basi mmfungeni hapo hapo kwenye kochi mimi niendelee kukata kiu.” Vijana wawili wakamsogelea. “Hapana Malii. Naomba nisamehe tafadhali. Nisamehe kwa ukatili niliokufanyia na nisamehe kwa kila kitu. Lakini usinibake tafadhali Malii.” Nanaa aliendelea kuomboleza wakati Malii akivua nguo pale pale mbele za watu. “Hakuna kitu cha ajabu utanipa tofauti na unachompa Geb.” Nanaa akampigia magoti. Malii akabakiwa na nguo ya ndani tu. Alishavua mpaka soksi. 

~~~~~~~~~~~~~

Malii amekuja kudai na yeye haki yake kwa Nanaa.

Tena ndani ya jumba hilo lililojazwa mali za thamani na ulinzi wa nguvu wa masaa 24. Thamani ya pekee hapo ni Nanaa peke yake. Ameuza kila kitu ili tu

kukamilisha alichokianzisha Nanaa sirini. Yupo na wanaume wa nguvu wanne, waliokubali kuyatoa maisha yao kwa ajili ya kutimiza azma yake.

Nanaa hana mtetezi. Aliokuwa nao wote wamefungwa, hawawezi kujitetea hata wao wenyewe. Geb alishapigwa teke, mama G anavuja damu za mdomo.

Upo wapi ulinzi wa Geb?

Unaweza kufikiria hali ya Geb moyoni mwake kwa wakati huo pale sakafuni akiugulia maumivu ya teke, mama yake amepigwa, anavuja damu, hawezi kumtetea, na kudhalilishwa mbele ya watu?

Sababu ni Nanaa aliyemficha ukweli tena akiwa amembembeleza kwa kurudia rudia awe anamwambia ukweli wote hata kama anajua utamuumiza sana.

Sasa kuja kujua ukweli wote kutoka kwa Malii, akiwa ameyatoa maisha yake

kwa kiasi hicho kwa Nanaa. Walikuwa wote hospitalini

muda wote huo,  na bado Nanaa alimficha ukweli!!

Usikose kujua yatakayojiri.  Nani wa Nani?

Endelea kusoma…

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment