Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu ya 50. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu ya 50.

Ikawa tayari kuna hali ya mtafaruku ndani ya hicho chumba, hapo hospitalini. Mambo mengi yenye maswali tena ambayo hawakuyategemea kwa kila mmoja wao hapo yakawa yametokea kwa wakati mmoja, bila majibu. Kabla hawajapata majibu ya kwa nini Malii na mkewe hawasimamii harusi, na ni nani atasimamia harusi hiyo! Kwa Nanaa akijiuliza kama harusi aliyokuwa akiiringia kama bado ipo au la! Ni nini kinaendelea kwa wanandoa hao wawili, Malii na mkewe! Likaja la Nanaa ambaye hawakutegemea kupata mtoto siku hiyo ambayo pressure iliyokuwa imetulia, ipo juu sana, chupa imevunjika na bado anaendelea kuomboleza!

 “Tafadhali Geb. Kabla sijaingia chumba cha upasuaji naomba nikusikie kuwa umenisamehe. Naweza nisitoke tena. Naomba angalau nife nikiwa najua nimekuacha na watoto wangu ukiwa huna hasira na mimi.” Manesi walishaanza kusukuma kitanda kumtoa Nanaa pale ndani, daktari akionyesha hataki kupoteza hata dakika moja mbeleni. “Geb please!” Nanaa akasisitiza huku akilia. Geb akawasogeza wale manesi kwa haraka, akainama pale kitandani na kumbusu Nanaa midomoni. Nanaa alisikika akiendelea kulia, wasijue ni furaha au uchungu.

          Alimbusu kwa muda kidogo. Akamwangalia. “Nilishakusamehe Nanaa. Lakini lazima utoke, ujue nakusubiri tufunge ndoa.” “Bado utanioa!?” “Kabisa. Nilitaka kukufanyia surprise. Nilitunza busu langu mpaka siku ya harusi yetu.” Nanaa akazidi kulia. “Nilijua umenikasirikia Geb! Ungeniambia.” “Ilikuwa surprise Nana! Magesa ndio ameharibu.” Nanaa akacheka huku akifuta machozi. “Siogopi tena.” Nanaa akaongea nakufanya kila mtu acheke. 

“Lazima twende sasa hivi.” Daktari akarudi pale walipokuwa wamesimama. “Nimemwacha mtu ameshikilia lifti. Twendeni tuwahi.” Daktari akasisitiza. “Naruhusiwa kuingia na mimi tukifika chumba cha upasuaji?” “Hapana! Ingekuwa ni labor, hapo sawa.” “Daah!” Geb akasikitika. “Nitakuwa nikikusubiri nje ya chumba cha upasuaji. Ukijifungua tu, tunafunga ndoa, tunaenda kupumzika.” Kila mtu alikuwa nyuma ya hicho kitanda wakimsindikiza Nanaa, kutoka chumba alichokuwa amelazwa kwa mapumziko hapo hospitalini, chini kwenda chumba cha upasuaji jengo hilohilo lakini gorofa ya juu. Walikuwa wakiiendea lifti ili iwatoe hapo wodini.

          “Tutawaacha watoto, wakati tunaenda honeymoon?” Nanaa akauliza huku akikunja uso. “Mama atabaki nao. Vipi mbona unakunja uso?” Geb akajibu na kuuliza. “Nasikia maumivu makali.” Nanaa alianza kulalamika huku akilia. “Nasikia mtoto wangu anatoka jamani!” Nanaa aliongeza sauti iliyojaa kilio. “Mtoto wangu mimi!” “Nisikilize Nanaa. Pressure ipo juu sana. Tumaini pekee alilobakisha Magesa ni wewe kutulia ili akitoka awe salama na wewe akukute. Unaweza kutulia.” Nanaa akatingisha kichwa na kufunga mdogo hapo hapo huku akifunga miguu.

“Hapana Nanaa. Huwezi kufanya hivyo.” Daktari akarudi kutoka ilipokuwepo lifti. Ilishakuwa imejifunga. Kuashiria inatumika kwenye magorofa mengine. Walichelewa. Daktari akaingiza mkono ndani ya ile shuka.

“Nimeshika kichwa! Hatutafika chumba cha upasuaji. Turudini chumbani kwake.” Kwa haraka wakageuza kile kitanda kurudi chumbani kwa Nanaa. Hapakuwa mbali sana na hapo kwenye lifti. “Naombeni wote mnisubiri hapo nje.” Daktari alitoa amri hiyo akionyesha wasiwasi usoni. “Geb njoo. Nimeanza kuogopa tena.” Nanaa akamuita akiwa amenyosha mkono. “Wewe unaruhusiwa.” Daktari alimgeukia Geb. “Usiogope Nanaa. Kila kitu kitakuwa sawa.” Geb akamshika mkono na kumbusu. Nanaa ndio alikuwa amebeba hatima ya mtoto wake. Mtoto aliyetabiriwa tangia Geb ni mtoto mdogo. Ilimlazimu Geb kutulia sana, ili kuwa faraja kwa Nanaa, ili kuhakikisha kusudi la Mungu linatimilika. “Tunakuombea Nanaa, wifi yangu. Na ujue tunakusubiri hapa hapa nje.” “Asante Grace.” Nanaa alijibu huku akiingizwa ndani ya kile kile chumba alichokuwa amelazwa. Mama G akakimbia na kumbusu Nanaa. “Nakusubiria mwanangu. Jikaze. Umefikia mwisho wa hayo mateso. Wewe nitolee tu, nitalea mwenyewe.” Nanaa akacheka huku anafuta machozi. Akatoka na kuwapisha.

~~~~~~~~~~~~~~

Kila mtu alikuwa kimya akimwita Mungu aingilie kati kwenye ile hali. Mtoto alikuwa anatoka huku kwa kiutalamu, Nanaa mwenye pressure iliyo juu sana, hawezi kuzaa kwa njia ya kawaida tena kwa wakati huo. Funga na kufungua chumba cha Nanaa kilishajaa madaktari. Alikuwa amelazwa first class, kwenye hospitali hiyo ya garama za juu sana nchini. Kwa hiyo hata uangalizi wake ulikuwa wajuu. Manesi wenyewe walikuwa wakimuheshimu kwa kuweza kumudu chumba hicho tena kwa mapumziko ambayo Geb alikuwa tayari kulipia kwa siku 21 ambazo Nanaa angetakiwa awepo mpaka ajifungue.

Chakula na usafi wa hospitalini hapo, ungeona. Ungejua ipo pesa inayofanya kazi. Alikuwa akihudumiwa kwa hali ya juu sana. Uzuri ni kuwa, daktari huyo huyo aliyekuwa akimuhudumia kipindi cha ujauzito wa Oliva, aliyekuwa amempata kwenye hospitali ya bure ya taifa, kumbe alikuwa akifanya na hapo kama ‘part time’. Kwa hiyo Nanaa alibadilisha tu mazingira, ila huduma ya daktari wake aliyekuwa amemzoea tokea zamani ilikuwa ile ile. Kutoka kwenye kumtibu bure na kumsaidia vitu vingine, safari hii daktari huyo anavuna wema wake kwa kula pesa ya Geb, aliyemwambia ahakikishe huyo mtoto anazaliwa salama na Nanaa anaishi. 

Alishazungumza naye baada ya kutoka kliniki. Wakati mimba ya Nanaa bado ndogo tu. Geb akiwa amemfuata kwa siri kujua jinsia ya mtoto huyo. Alipomtajia kuwa ni wakiume, Geb akamwambia yule daktari kuwa huyo mtoto anaitwa Magesa. Alishatabiriwa na babu yake tokea hata yeye mwenyewe Geb hajakuwa kijana mkubwa. Kwa hiyo afanye juu chini, kuhakikisha kwanza huyo mtoto anazaliwa salama. Na mama yake awe salama ili aje amlee huyo mtoto.

          Mwanzoni dokta Lyamu alijibu bila shida kwani Nanaa alikuwa mzima kabisa. Alimtoa hofu Geb. Na kumwambia alishamuona Nanaa akibeba mimba akiwa hana damu. Na akajifungua bila hata yeye kuwepo, na akajifungua salama tu. Hofu yao ilikuja pale mwishoni pressure ilipoanza kumsumbua Nanaa akiwa na miezi karibia kumaliza 8. Hapo hofu ndipo ilipomwingia huyo daktari na ahadi aliyokuwa amempa Geb, ambaye walishaanza kuzoeana kwa kukutana mara kwa mara hapo hospitalini wakati Nanaa alipowekwa mapumzikoni. Kila ushauri aliotaka Nanaa afuate, alimtumia Geb kuweka msisitizo kwa Nanaa, kwa sababu Nanaa alikuwa mbishi sana. Kwenye hatari, yeye ndiye aliyekuwa amkimsisitiza dokta  Lyamu akimwambia asiogope. 

Mwenye Hatima Ya Kila Kitu Ni Mungu.

Hapo nje ya chumba alicho lazwa Nanaa kila mtu alikuwa ameshikilia roho yake kwa hofu, wakati ndani kukisikika  kuna heka heka zakutia hofu zaidi. Geb alikuwa ndani na Nanaa, kitu alichofurahia kama alivyokuwa amepanga kwamba huyo mtoto azaliwe yeye akiwepo. Baada kama ya dakika 8 hivi, kilio cha mtoto kikasikika kutoka ndani ya kicho chumba. Mama G akawa kama amechanganyikiwa. Akaanza kupiga kelele. Grace alijikuta machozi yakimtoka. Oliva alimka kwa kelele za bibi yake. “Amka mama. Umepata mdogo wako.” Mama G alimtoa kutoka kwenye kiti chake. James alikuwa akipumua kwa hofu. Hakufurahia kama wengine, alibaki kimya tu.

Baada ya muda alitoka nesi. James akamkimbilia kwa haraka. “Vipi Nanaa?” James akauliza akionyesha wasiwasi. “Anaendelea vizuri. Usiwe na wasiwasi. Mtoto mwenyewe naona ametoka bila shida. Hajahangaika sana kuzaa. Ila madaktari ndio wanahangaika kushusha pressure yake na kushonwa. Alichanika sana. Mtoto alikuwa mkubwa sana. Ila na yeye mzima, amepakatwa na mama yake huku akihudumiwa.” James akapumua kwa nguvu. 

“Anafananaje? Namaanisha huyo mtoto.” Grace akamsogelea na yeye huyo nesi, akauliza. “Ana macho kama hayo yako. Dume la nguvu. Mrefu kama baba yake.” Wote wakacheka. Mama G akaendelea kuruka ruka. “Jamani Magesa amezaliwa!” Akaendelea kupiga vigelegele huku amembeba Oliva. “Mama tulia bwana! Unapiga sana kelele!” Grace alijaribu kumtuliza bila mafanikio.

Geb akatoka akiwa amembeba mtoto. “Nanaa amesema nikuletee kidogo umuone ndio akashugulikiwe.” Haraka haraka akamkabidhi Oliva kwa James. “James mwanangu, nishikie mara moja.” “Hapo shuguli imempata mama!” Grace aliongeza na kumpisha mama yake. Geb akamsogezea mama yake mtoto, akamkabidhi. “Magesa mzungu amezaliwa jamani!” Mama G aliendelea kupiga kelele. “Basi mpaka Nanaa amekusikia mama, kwa kelele!” Grace aliongea huku akimsogelea na yeye ili kumuona Magesa. Mama G akampokea na kumyanyua juu. “Umebarikiwa Magesa. Wewe ni shujaa. Utaishi maisha marefuuuu, usimulie makuu ya Mungu.” Machozi yalikuwa yakimtoka Grace na Geb. “Baba angekuwepo, angefurahi sana kumuona Magesa.” Grace aliongeza huku akifuta machozi ya furaha.

“Hongera Geb!” Grace alimpongeza kaka yake. “Asante. Nimefurahi sana. Siamini! Nahisi kama sikuwa nimejiandaa vizuri! Nilijua siku bado!” Geb aliongea akimtazama mtoto wake. “Sikutegemea kama angekuja anikute bado sijaoa!” Aliongea kwa kulalamika kidogo. Akamsogelea tena mwanae. “Hebu tumuone, mama.” Mama G akamuweka vizuri, wote wakamsogelea. Wakawa wamemzunguka mama yao, wanamwangalia Magesa kwa karibu na makini. “Amefanana sana na mimi, kasoro rangi tu.” Wote wakacheka.

“Nanaa anadamu kali sana ya rangi. Lakini huyu ni Geb mtupu. Anaendeleaje?” “Wanamsafisha na kujaribu kushusha pressure. Ila wanataka alale kabisa. Wanaamini akija kuamka tena, atakuwa sawa tu. Amejitahidi sana mpenzi wangu. Hata daktari amemsifu. Angechelewa kidogo tu, Magesa angekosa hewa. Kumbe alishaanza kutoka bwana!” “Maskini mwanangu Nanaa! Sasa hapo ni kukazana na vyakula. Anakuwa na kazi ya kunyonyesha watoto wawili! Na dume hili, sio mchezo.” Mama G aliongeza huku akimuweka vizuri Magesa.

“Ngoja nirudi ndani kwa Nanaa.” Geb aliaga huku akimchukua mtoto wake. “Mwambie Nanaa asante kuniletea mtoto. Nimefurahi sana. Mpe pole. Mwambie namsubiria kwa hamu nimpe pongezi zake, mwanamke wa shoka!” Mama G aliongeza, wakacheka.

Geb akarudi ndani na mtoto. Wakati akishonwa ndipo Nanaa alipomwambia atoke na mtoto nje. Ampelekee mama G aliyekuwa akimsikia akipiga kelele.  Geb alirudi akakuta nesi aliyekuwa akimuhudumia Nanaa ameshamaliza kila kitu. “Nimekurudishia mkeo kama binti mdogo!” Geb na Nanaa wakacheka. “Nakushukuru sana. Asanteni kunisaidia.” Nanaa akashukuru tena. “Karibu. Pole na hongera. Pumzika ili ujisikie vizuri. Kazi ndio imeanza. Mapumziko ya mwisho hayo! Si unamuona mwanao ameshaanza kunyonya kidole?” Nanaa akacheka. “Nipe nimuone tena, Magesa wangu.”  Nanaa akajiweka vizuri. “Mama kafurahi huyo!” “Nimemsikia akipiga kelele.” “Ameshindwa hata kukaa.” Nanaa akacheka huku akimpokea mwanae. 

“Magesa ni mzuri sana. Mkubwa! Ndio maana ulikuwa ukiniumiza mwanangu! Urefu huu unaupeleka wapi?” Nanaa alimgusa mwanae kwa upendo. Akambusu. “Nimefurahi sana kukuona.” Nanaa akaanza kulia nakushangaza hata madaktari waliokuwa wakijadiliana juu ya pressure yake. Muda wote wa kuzaa alikuwa jasiri akikazana kusukuma kwa makini kama alivyokuwa akielekezwa na daktari wake ili asiipandishe pressure zaidi na asimdhuru mtoto ambaye alishatanguliza kichwa. Alitoka na nywele nyingi sana kama za baba yake.

“Usilie bwana Nanaa! Unatakiwa ufurahi.” Geb alijaribu kumbembeleza. Nanaa alikumbuka siku alipojifungua Oliva, akiwa peke yake hospitalini. Hofu ya itakuaje ikimuandama. “Namuomba Liv.” Nanaa akamgeukia Geb. “Naruhusiwa kuwaita watu ndani?” Geb alimuuliza dokta Lyamu. “Hali yake bado haijatengemaa. Anatakiwa alale kabisa.” “Kwa muda mfupi tu tafadhali. Namtaka mtoto wangu.” Lyamu akatabasamu huku akimwangalia Nanaa. “Unanichanganya wewe! Yaani muda unaotakiwa uwe unalia, huwa unacheka. Muda wa kucheka ndio unalia!” Nanaa akacheka huku akifuta machozi.

Akainama kumwangalia mtoto wake. Akamuweka kwenye ziwa ili anyonye. Magesa akaanza kuvuta ziwa kama aliyezaliwa na ujuzi wa kunyonya. “Asante kwa kunisaidia na kunivumilia.” Nanaa akamshukuru Lyamu, daktari wake. “Kumbe unajijua ulivyo mkorofi?” Nanaa akacheka. “Asanteni wote jamani. Isingekuwa nyinyi wote kuwa hapa na mimi, wala nisingeweza. Nawashukuru sana, tena sana.” Nanaa akashukuru wauguzi wote pale ndani. “Karibu. Pole na hongera.” Wakaitikia huku wakiendelea kukusanya vifaa vilivyokuwa vikiingizwa mle ndani wakati wa kujifungua Nanaa, ili kuacha chumba hicho kisafi na nafasi ya wageni wake.  

“Kabla hamjatoka, naombeni mnipe muda mfupi sana nimshukuru Mungu pamoja na nyinyi.” Geb akawasimamisha wote. “Sitachukua muda mrefu. Wewe Nanaa andelea tu kunyonyesha.” “Ni kweli Geb. Mungu anastahili kupewa sifa kwa huu muujiza.” Nanaa akaunga mkono. Hapo hapo Geb akaanza kuomba tena akiwa amepiga magoti. Akashangaa anashukuru na machozi yanamtoka. Akamshukuru sana Mungu kwa ule muujiza pale. Akamtambua kuwa bila mkono wake, Nanaa asingeweza. Akawaombea baraka wale wauguzi wote waliomsaidia Nanaa na Magesa. Baada ya muda mfupi sana akawa amemaliza. Akawapa mkono kila mmoja. Kwa kurudia kuwashukuru. Kwani aliwaona jinsi walivyokuwa wakihangaika. 

Utabiri Juu Ya Magesa.

Mama G alikuwa na furaha isiyo kifani. “Magesa aliniambia habari za huyu mtoto. Ndio maana nilikuwa nina hamu sana yakujua kama Nanaa amebeba mimba yake au bado niendelee kusubiri.” “Ndio maana ulitaka kumrubuni Nanaa mkaangalie jinsia halafu umlipe milioni?” Grace akauliza. “Kabisa. Maana nilikuwa namsubiria kwa hamu huku nikimuomba Mungu nisife kabla sijamuona. Maana Magesa alisema alishamuombea sana. Nikamuuliza kwa nini asimkazanie Geb ambaye ndio mtoto pekee wa kiume na tumeshamuona? Akasema Mungu alimuonyesha huyu mtoto. Akampa kabisa na jina lake yeye mwenyewe. Akasema nihakikishe Geb anakuwa katika njia nzuri, ili aweze kumlea huyu Magesa.” Mama G akaendelea kueleza huku wamerudi kukaa kwenye viti, wakisubiri waingie kumuona Nanaa.

Kila mtu alikuwa akimsikiliza mpaka mke wa Malii. “Sasa siku ile usiku tulipomleta Nanaa hapa hospitalini. Geb akatukuta hapa na kuanza kumuombea. Akamtaja ni Magesa..” “Ndio maana ukashituka sana mama!” “Kumbe unakumbuka Grace? Nikamwambia Mungu asante kwa kuweza hata kuona ujauzito wake. Sasa kuja kusikia Nanaa anasumbuliwa na pressure itahatarisha maisha yake na mtoto, ndipo maombi ya kufunga na kuomba yalipoanza. Kuharibu kazi ya ibilisi. Maana kila tulipokuwa tukimpeleka Nanaa kliniki, tulikuwa tukiambiwa ni mzimaa. Iweje karibu na mwisho uzuke ugonjwa mkubwa hivyo wakati hata mama mtu hakuwahi kuwa nao!? Sasa leo kumsikia Magesa analia hapo ndani, hakika nimemtukuza Mungu wangu.” Mama G akafuta machozi.

“Hongereni sana.” Mke wa Malii aliwapongeza kinyonge. “Asante Manka.” Grace alijibu. “Ndio maana Nanaa alikuwa akipata sana maumivu. Mtoto mkubwa sana. Hapo hata hajatimiza siku zake lakini yuko hivyo!” Grace aliongeza. “Nakwambia huyo ni Magesa mtupu.” Mama G akasifia. “Ni mzuri kama dada yake! Nywele na macho utafikiri ni mapacha! Nanaa amebahatika sana.” Manka mke wa Malii akaongeza. James alikuwa na Oliva amempakata. Wote wakamgeukia. “Hongera James mwanangu. Umekuza. Naona nazidi kuletewa wajukuu! Zote hizo ni juhudi zako baba. Hongera na asante.” James akacheka. Wazi alionekana amefurahi na yeye. Akamwangalia Oliva aliyekuwa ametulia tu akionyesha bado ana usingizi.

Madtari walitoka na manesi nao pia wakatoka wakiwa wanasukuma kigari kilichojaa vifaa vingi walivyovitumia wakati wa kujifungua Nanaa. “Asanteni sana jamani. Mungu wangu awabariki.” Mama G akasimama kwa haraka akawakimbilia wale madaktari na manesi. “Asanteni sana, tena sana. Naombeni mrudi jioni, ili tule na kunywa tumshukuru Mungu pamoja.” Mama G akaongeza.

“Mimi sitakuwepo mama. Natakiwa kwenye hospitali nyingine. Naomba mfurahie kwa niaba yangu.” Lyamu akajibu kwa upande wake. “Basi naomba mwanangu Danny akusindikize.” Danny alijua mkwewe anachomaanisha. “Nyinyi wengine naomba mpitie chakula chenu hapo kwenye ofisi ya manesi. Grace atahakikisha wote mnapata chakula na vinywaji. Mmefanya kazi kubwa sana ambayo lazima Mungu aliwahitaji kuwatumia ili kukamilisha ujio wa mjukuu wangu. Hatuna jinsi nyingine ya kuwashukuru ila kusema asante.” Grace naye akasogea na kuongeza. “Asanteni sana.” Wote waliwapa mkono wa kushukuru.

“Ila Nanaa anahitaji muda wa kupumzika. Bado pressure ipo juu.” Lyamu akaongeza kabla yakuondoka. “Na sisi hatutakaa sana. Tunamuona tu na kutoka, mpaka usiku ndipo tutarudi. Asante baba.” Mama G aliendelea kushukuru.

“Nanaa anamtaka Liv.” Geb akatoka. Ndipo wote wakaelekea chumbani. James ndiye alikuwa amembeba Oliva. Oliva alipomuona tu baba yake akanyanyua mikono. “Dadii!” “Njoo mwanangu, nikutambulishe kwa kaka yako.” Geb akampokea. Mama G alishaingia ndani akaenda moja kwa moja kitandani kwa Nanaa. Nanaa akaanza kulia. “Nimechanika sana mama!” Nanaa alinong’ona kwenye sikio la mama G. “Utapona Nanaa mwanangu. Pole mama. Umefanya kazi ngumu tena ukiwa mgonjwa.” “Basi pole hiyo ingeenda na bakuli la uji.” Kila mtu akacheka. “Na mzazi tumempata!” Mama G akaongeza. 

“Mchukueni huyo mtoto, nimkumbatie Nanaa wangu.” James akampokea Magesa, mama G akamkumbatia Nanaa. “Hongera sana Nanaa. Hongera mama.” “Asante mama yangu. Nimefurahi sana.” Grace naye akamsogelea na kumkumbatia. “Pole wifi yangu.” Nanaa akacheka. “Nimefurahi umeniita wifi.” Wote wakacheka. “Kwa kuwa anaandaa harusi mwenyewe ndio maana na uwifi umenoga.” Mama G akaongeza.

“Jamani pole na maandalizi! Basi mimi nilijua hamna tena harusi. Geb aliacha kuzungumzia kabisa.” “Surprise!” Geb akaongeza. “Na ni surprise kweli. Mbona utapenda?” Nanaa akacheka. “Mniombee uzima.” “Utapona mama. Utapona tu na utalea wanao.” Mama G akamfariji.

Manka mke wa Malii akamsogelea na yeye. “Hongera sana Nanaa. Hakika Mungu amekubariki.” Nanaa akajikuta machozi yanamtoka. Furaha ya ajabu ilimjaa moyoni. Hakuwa anaamini kama ni yeye Nanaa. Gafla akaona vile Mungu alivyoweza kuongeza uthamani wake. Bado hakuwa akiamini yanayomtokea. “Asante Manka. Na wewe umebarikiwa.” Akacheka kwa kuguna kama asiyesadiki. “Usigune Manka mwanangu. Sema amina. Umebarikiwa.” “Mmmh mama! Tuyaache tu kwa kuwa sasa hivi tunafuraha ya mtoto. Acha tufarijike kwa hili. Bado Mungu anajidhihirisha yupo na wala hajaacha kutenda miujiza. Ni dakika chache tu hapa tulikuwa tunazungumzia hatari ya kifo iliyokuwa inatukabili. Lakini ona furaha aliyotushushia Mungu! Ni kwa neema na upendeleo mkubwa alionao kwa Nanaa.” Mwisho wa hayo maneno ya Manka, ukafanya kutulie kidogo, wasijue wajibu nini tena.

“Amina! Nashukuru Mungu. Geb namuomba Liv wangu.” Nanaa akavunja ukimya uliotaka kuzuka mle ndani na kumgeukia Geb. Nanaa akampokea na kuanza kulia tena. “Kama ni hivyo namchukua mtoto.” Geb alimsogelea Nanaa. “Mwaka jana, siku kama ya leo wakati najifungua Liv nilikuwa peke yangu Geb. Nikiwa nimejawa hofu. Sijui itakuaje na nitamuweka wapi. Nilikuwa nikimuhurumia kweli. Acha nikae naye kidogo nifurahie.” Nanaa alikua akiongea huku akimwangalia Oliva ambaye na yeye alikuwa akimtizama na macho ya kusinzia.

“Jamani watu wamesahau birthday ya dada mkubwa! Mama Mzazi!” Grace akashituka sana. “Jamani Liv wangu! Pole mama, nimekusahau!” Bibi yake akaongeza. Geb alikuwa kama ameduwaa kwa muda. “Nimewezaje kusahau hili!” “Wala usijilaumu Geb. Tangia sisi tumeingia hapa ile saa moja mpaka sasa, ilikuwa ni heka heka tu. Akili zako zilikuwa hazijatulia.” “Hapana Mama, sikutakiwa kusahau birthday ya Liv. Namuomba.” Geb akamchukua. 

“Happy birthday Oliva Magesa.” Oliva akacheka huku akimtizama baba yake. Akambusu mara kadhaa kisha akamuweka vizuri ili kumuombea. “Nakupenda mwanangu na ninakuombea heri kwenye maisha yako yote. Uwezo wa kimungu ukawe juu yako daima. Ukafanikiwe kwa kila utakachogusa. Kila utakapopita wakamwite heri mwanamke aliyekuzaa wewe. Nakuombea ulinzi katika kila jaribu atakalokutupia muovu. Mungu akakushindie. Wakati wote wewe ndio ukasimame mshindi. Nakuombea afya njema na baraka zote za mbinguni na duniani zikawe juu yako. Hatua zako ziongozwe na Bwana. Amen!” “Amen!” Kila mtu aliitika na kuanza kumpongeza Oliva.

“Jioni tukileta vyakula, nitaleta na keki yake aje akate hapa hapa mbele ya mama yake.” Grace akatoa wazo liliondelea kumgusa Nanaa. Bado machozi yalikuwa yakimtoka Nanaa. “Pole Nanaa mwanangu. Mungu anakufuta machozi sasa hivi.” “Kweli mama. Kaka! Umemuona Magesa?” James akacheka. “Mwenzio alikuwa na wasiwasi na wewe huyo! Ndio anacheka sasa hivi.” “Jamani kaka yangu! Pole.” James akamwangalia Nanaa. “Pole wewe.” “Asante kaka. Pole na wewe kwa wasiwasi.” Nanaa akajibu na kufuta machozi. James akarudisha macho kwa Magesa aliyekuwa amemshika. “Mtoto mzuri sana, Nanaa. Hongera.” James alirudia huku akimtizama yule mtoto. “Asante kaka.” Oliva akataka arudishwe kwa mama yake. Nanaa akampokea na kumbusu mara kadhaa. “Happy birthday Liv!” Oliva akacheka na kuhamia kwenye ziwa la mama yake.

Oliva akataka nyonyo. “Mchukue bwana asinyonye ili amwachie mwenzie kwa hizi siku mbili. Akianza kunyonya huyu ni mpaka ahakikishe amemaliza.” Geb akataka kumchukua Oliva akaanza kulia. “Jamani Liv! Nenda bwana. Maziwa ya mtoto. Nenda bibi akupe uji.” Akajificha uso kwa mama yake. “Basi tabia hizo za baba yake. Akitaka jambo lake mpaka apate. Jasho litakutoka.” Wote wakacheka. Mama G akamsogelea. “Bibi! Bibi!” Oliva akamwangalia bibi yake, akacheka na kurudisha uso kwa mama yake akajificha. “Basi akikuchekea hivyo, utafikiri amekukubalia. Kumbe ndio anakwambia hadanganyiki.” Mama G aliongeza.

Manka, Mkewe Malii, Atoa Siri Nzito.

Manka akasimama. “Jamani, naombeni mimi nitangulie kabla jua halijawa kali sana.”  “Si umpigie simu Malii!? Jua limeshakuwa kali Manka. Huwezi kutembea sasa hivi wakati gari ipo!” Grace alimuwahi. “Gari ile ni ya Malii, wifi yangu. Mimi nimeambiwa nilikwenda pale na daladala, nisijitie ufahari wa ukubwani. Acha tu niende.” Manka alifanya kila mtu ashangae. “Subiri kwanza Manka. Huyo aliyekwambia hivyo ni Malii mwenyewe au nani!?” Gafla Mama G akawa hajaelewa.

 “Mwanao Malii huyo.” “Haiwezekani!” “Mmmh! Acha tu mama. Mimi mwenyewe ningeambiwa kabla, nisingeamini. Hivi ni bibilia ndio ilionya mwanadamu asiolewe na mnyama au ni mimi tu mwenyewe nimepata huo msemo?” Manka akaanza. “Usiseme hivyo Manka mwanangu.” “Nakwambia nimejiingiza kwenye ndoa na mnyama mama. Mwanadamu wa kawaidia hawezi kuwa kama Malii.” Kama aliyekuwa amepewa ruhusa. Akarudi kukaa.

Ni kama aliyekuwa amekabwa na kitu kooni. Akaanza kuongea bila kificho kina Danny, James, Geb, Grace na mama G, wakisikiliza. “Mimi huwa najiuliza labda yule mwanaume nilibadilishiwa siku ya harusi! Si wakawaida hata kidogo! Hivi ushawahi ona mwanaume mshenzi hapa duniani?” Manka akauliza. “Manka!” “Basi ni kwa vile yupo mmoja tu hapa duniani, na ninaishi naye mimi. Malii.” Manka akajiweka sawa. Mama G akamkabidhi Nanaa bakuli la uji. “Kunywa wakati huyo anasinzia.” Nanaa akapokea.

“Kwanza mimi nilikuwa najua naolewa na mwanaume mcha Mungu. Kumbe naolewa na mnyama ambaye hana Mungu ndani yake na wala hajui kama yupo Mungu aliye muumba! Akianza kunitukana, utafikiri mie mke mwenzie.” “Kwa nini!?” Mama G akauliza kwa mshangao. “Weusi! Nakwambia mwanaume anachukia rangi yangu hii, utafikiri hakuniona kabla hajanioa au utafikiri nilikuwa na Mungu wakati ananiumba, nikafanya kosa la kuchagua niumbwe mweusi.” Grace na Danny wakatizamana. Grace na mama yake pia walikuwa weusi. 

“Malii jamani! Amepatwa na nini?” Mama G akauliza. “Ni mshenzi tu yule mama. Samahani kusema hivyo. Lakini hujawahi ona mtu kama Malii. Ila nashukuru Mungu, nishakuwa na wanaume wanosifia rangi yangu, kwa hiyo nimejua tatizo wala sio rangi, anapepo chafu sana. Na asiposaidiwa mapema, hakika atakufa kifo kibaya. Sio kawaida.” Manka akaongeza. “Kwa nini?” “Sema kuna watoto mama. Na mimi nataka kuondoka. Lakini ujue wazi, pale nimenawa mikono, naondoka hivi karibuni.” Manka akasisitiza.

          Akataka kusimama, akawa kama amekumbuka kitu. “Ujue mie mwanzoni nilikuwa simfahamu huyu Nanaa. Mara ya kwanza kumsikia ni kwa Malii mwenyewe tukiwa tunafanya mapenzi.” Nanaa akashituka sana. Akapaliwa na kuanza kukohoa mfululizo. “Samahanini jamani. Lakini acheni tu niongee. Amenichosha nafsi na roho.” Geb akampa Nanaa maji ya kunywa. Kila mtu akabaki ametoa macho. Grace akawaangalia wanae. Wote walikuwa wamelala. Fili alikuwa amepakatwa na baba yake tokea zamani.

Hata mama G akashindwa kuhoji. Akabaki kimya. “Basi mwanaume yule akamtaja Nanaa. Nikamuuliza Nanaa ni nani? Akakataa katakata kuwa yeye hajasema Nanaa. Akaniambia alikuwa anagugumia nananaa! Wakati mimi nilisikia kabisa ni kama jina Nanaa. Nikanyamaza kwa kuwa sikuwa namjua. Nikajiambia labda ni mwanamke wake wa zamani. Hapo hata hatujaoana. Sikutaka ugomvi, siku ile ikapita. Lakini ukweli nikaumia sana. Nikajiambia huyu mwanaume anafanya mapenzi na mimi huku akimuona mwanamke mwingine! Basi nikatulia.” Manka akaendelea.

“Kwani iliishia hapo. Ukaanza mchezo wa kusifiwa wanawake weupe, wanalinganishwa na weusi. Kama utani vile. Mimi nikawa nacheka. Najua utani! Huwezi amini mama, usiku ule wa honeymoon, alikuwa anatajwa Nanaa tu. Mpaka kesho yake ikabidi nimkalishe chini nimwambie aniambie ukweli. Akaanza kuniambia atakuwa ameropoka tu. Nikamkazania na kumwambia si kwa kurudia mara zote hizo tena usiku wetu wa kwanza wa ndoa! Nikamwambia anitajie Nanaa ni nani na kama ni mwanamke wake ambaye yupo naye kwenye mahusiano. Basi ndio safari yangu ngumu ya ndoa ikaanza hapo. Nilitamani kuondoka pale hotelini mama yangu, lakini aibu. Narudije nyumbani nilikoacha wazazi wangu na mimi ndio nimeolewa hata masaa 24 hayajapita!” Manka hakunyamaza. 

Akasahau kama ndio yeye aliyesema siku hiyo wafurahie tu baraka kutoka kwa Mungu. Manka akaendelea. “Tukarudi nyumbani, nikaanza kulinganishwa sasa na Nanaa. Chuki ikanijia juu ya huyo Nanaa. Shauku ya kutaka kumjua Nanaa, anayetajwa mpaka kwenye kitanda changu cha ndoa, ikaibuka. Nikaanza kuuliza taratibu. Nikaanza na Goz. Maana Goz kidogo ndio akawa amebaki na sisi baada ya kundi letu kusambaratika na uzuri Gozi ni mtu wakuhamisha maneno. Nikajua hataninyima majibu yangu kama na yeye anamfahamu huyo Nanaa. Nikamuuliza unamfahamu Nanaa? Gozi akacheka sana. Akasema , ‘siku hizi Nanaa ndio habari ya mjini!’ kama mnavyomjua Gozi. Utani haumwishi, maneno mengi. Akaendelea. Akasema, ‘sasa hivi Nanaa anawaendesha akili wahandisi wa mjini, hapashikiki. Kampiga chini Miss Africa, jasho linamtoka!’. Akimaanisha Liz. Mimi si sipo kwenye hilo kundi lenu la Whatsapp!” Manka akaendelea.

“Acha Gozi anipe mikasa ya mjini. Kinachoendelea. Na yeye akaanza kusifia. ‘Nanaa anawaka kama jua, kiuno ng’e! Wanaume walio liana amini, na kuapiana urafiki kama undugu, wanashikana mashati sasa hivi!’. Aliposema tu Nanaa ni mweupe, nikajua tayari. Ndicho alichomkamatia Malii. Nikamuuliza kwani huyo Nanaa anaishi wapi, au wazazi wake wako wapi? Nyinyi mmemfahamuje? Na iweje marafiki wote wamgombanie mwanamke mmoja? Sasa hivi yuko na nani? Si ndio akasema mwenye kisu kikali ndio anayekula nyama! Kafichwa na milionea wa mjini. Nikamuuliza nani? Na yeye akaniuliza kwani mamilionea vijana hapa mjini ambao hawajaoa, mimi ninao wajua ni wangapi? Hapo tena macho yakanitoka. Kama anavyojisemeaga Malii. Mwanamke mimi wa migombani. Mamilionea wa jijini nawajulia wapi? Nikabaki nawaza.” Manka alikuwa amekaa kwenye kochi hapo hapo chumbani mbele ya Nanaa.

Anaongea huku akimtizama mama G. Watu wote wakimsikiliza. Nanaa akaendelea kunywa uji taratibu. James kimya. “Basi. Sasa hapo mimi hata sikujua kama Geb ndiye milionea! Lakini jina hilo halikuwa geni. Nilikuwa nimeshalisikia hilo jina mara nyingi tu. Wakitaka kukopana pesa, wanaambiana mpigie simu Milionea. Basi, ndio Goz akasema ni Geb. Nikashikwa kama na bumbuazi. Akaniuliza vipi? Nikawa kama nimemsahau tena Geb! Maana Geb ninayemfahamu mimi ukikutana naye anakusalimia kwa kukupa mkono. Halafu akiwa katikati ya watu, hazungumzi kabisa. Katulia wakati wote wala sikuwahi kumjua kama ni yeye milionea. Ndio Gozi akaniambia ndiye huyo huyo alisimamia harusi yetu na Miss Africa sijui mwenyewe anamwita Face of Africa. Kuna jina lao wenyewe wamempa Liz.” Manka akaendelea.

“Ndio nikaambiwa na habari za Liz zote. Mtoto asiyejua shida. Hataki maskini, ananyata kama malaika. Sasa nikaambiwa, ndio kwa mara ya kwanza akapata kiboko yake, ambaye ni Nanaa. Hamu ya kumfahamu huyo Nanaa ikaongezeka. Nikauliza kwani huyo Nanaa na yeye yupo kama Liz? Ndio nikapewa tena habari za James. Kuwa James ndio mama, baba, dada na kaka ya Nanaa. Wanaume hao ambao wote waliapishana katika shida na raha, wamesambaratishwa na Nanaa, waliyemsikia kutoka kwa James tokea anamiaka sijui 4, sijui hata sikumbuki vizuri maana na yeye Gozi alikuwa na mengi ya kuongea na mimi nilitaka kusikiliza. Wote nasikia walikuwa shule ya bweni huko jijini Arusha, Iliboru.” Manka akaendelea kama asiyetaka kukatishwa.

“Gozi akasema mate yaliwatoka paleee, James alipowatambulisha huyo Nanaa. Unaambiwa mpaka wanaoweza kutumia tunguri walitumia. Kila mtu akadai Nanaa wake. Gozi akasema kuna ambao hawakutaka kuingia kwenye ugomvi mkubwa, lakini nasikia pia walimfuata huyo kaka mtu, sijui mzazi mtu wa Nanaa, yaani James. Kulalamika nakuomba James awaunganishie kwa Nanaa. Akasema sasa hivi watu hawazungumzi hapa mjini sababu ya Nanaa. Nikamuuliza vipi na yeye? Akasema yeye mnyonge. Hata akisema, hamna atakayemsikia. Nikamwambia niambie mimi. Akasema yeye ni machozi ya samaki. Haitasaidia. Gozi akamalizia kwa kusema, ‘Nanaa maji marefu mama!’ Akaondoka kama mnavyomfahamu Gozi.” Nanaa alikuwa ameinama kimya.

“Basi tena pale ikabidi na mimi niwe mpole. Niunge msafara wa Gozi. Nikajinyamazia kimyaa. Lakini mama! Mmmh! Usiombe. Malii mnyanyasaji! Akianza kutukana viungo vyako vya mwili, utajuta kuzaliwa mwanamke. Halafu taratibu mwenyewe hana haraka. Hapo karudi nyumbani, kalewa. Basi atakuchambua wewe, mpaka utashindwa kulala. Halafu anamalizia kukwambia hataki kukugusa amechoka. Heri tu alale. Mara ya kwanza nilitamani ninywe sumu nife.” “Usifanye hivyo Manka mwanangu.” “Sasa hivi siwezi kufanya hivyo tena mama yangu. Nimeshamuelewa. Hanisumbui tena.” Manka akaongea.

“Afadhali. Maana unaweza kujikuta unachuki na watu bure.” “Wala nisiseme uongo mama. Nilimchukia Nanaa kupita kiasi. Sasa nikawa sijui kama alishakuwa na mahusiano naye au la. Nilionyeshwa picha yake. Nikakumbuka ndiye msichana wa mwisho kukutana naye siku ya harusi yetu wakati tunaingia ukumbini. Tulimkuta amesimama pale nje. Bwana msichana alikuwa amependeza huyu! Mpaka Malii alishindwa kujizuia. Mbele yangu alimsifia kama amependeza sana. Basi ile picha ndio ikawa inanitesa. Nikajua ni mwanamke wake Malii. Alikuwa anamsubiria pale nje ili waonane na mpenzi wake.” “Hapana Manka mwanangu. Usiingie dhambini. Sisi ndio tulimsahau Nanaa pale nje. Pale alikuwa amezuiliwa kuingia ukumbini.” Mama G akamueleza kwa kifupi.

“Kumbe! Basi mimi na hilo nikalibeba. Nikawa najiambia kama sio Nanaa kumuonjesha penzi Malii, wala tusingekuwa hapa. Sasa akanipa kubwa kuliko! Acha Malii anivue nguo mbele ya watu mama!” “Nini tena?” Mama G akauliza. “Bwana mwanaume yule nimemvulia kofia. Asiende kuanzisha mahusiano na yule msichana aliyenisimamia harusi! Sio kulala naye mara moja, mahusiano haswa. Na yule dada alikuwa rafiki wa tokea watoto. Tulizaliwa kijiji kimoja pale Marangu. Yaani wazazi wake ni kama wazazi wangu. Tumelelewa pamoja. Ila mwenzangu akapewa rangi nyeupe. Yule dada ndio akageuka kuwa mke wa Malii. Mama! Walinitoa jasho.” Manka akacheka na kupiga makofi.

“Yule Mary si mnafanya naye kazi ofisi moja!?” “Sawa sawa wifi yangu. Basi walinichezesha ngoma nilizokuwa sijui kuzicheza. Nakwambia mapenzi ya wazi wazi. Malii anamfuata kazini kwenda kula mchana.” “Si ameolewa? Yule aliyemsimamia Malii si ni mumewe yule?” “Bwana kumbe wifi Grace unakumbukumbu! Sasa yule bwana wake hana kitu. Hali yake kama yangu. Alijisemea Malii. Kwetu tunalalia machalali na kuamkia mtori tu. Hamna chakula kwetu. Basi yule kaka uwezo wake mdogo. Lakini walikuwa wanasikilizana sana na Mary mpaka nikawa nawaonea wivu. Nikienda kwao nilikuwa nawaambia waniombee na mimi nipate ndoa kama yao. Haaa! Malii si akaingilia kati. Nikamwambia nimempongeza. Maana Mary na uzuri ule aliwaliza wanaume, lakini mapenzi ya dhati ndio yakamfanya aolewe na Chalii. Tena nakumbuka Malii akanijibu kwa kiburi kuwa yeye ni mwanaume wa shoka, hatongozi na kukataliwa. Nikamtupia swali la haraka ili kujiridhisha, nikamwambia mbona Nanaa anamtoa jasho? Akajibu na ndipo nilipojua Nanaa alimkataa. Akasema, ‘atafutaye hachoki, akichoka kashapata’. Hapo ndipo nilipojua bado anahangaishwa akili na Nanaa.” Manka akaendelea. Hakuna aliyemkatisha.

“Sasa Malii akaniambia Geb anaomba tukutane naye kwa chakula cha mchana hotelini. Atakuwa na Nanaa. Akasisitiza nivae vizuri nisije mtia aibu. Nisivae nguo zangu za migombani. Kwa kuwa Geb akikutoa kwenda kula mahali sio kwenye chips vumbi. Ni hoteli za maana. Mimi nikacheka tu. Tulipofika hapo, ndipo nikamuona kwa karibu dada huyo!” Manka akamnyoshea kidole Nanaa.

“Mjamzito wa huyu mtoto wake mpya. Mwenyewe kapendeza. Kajaa dhababu mwili mzima. Alivaa kigauni chake cheusi mwenyewe, mpaka magotini. Bwana Nanaa alipendeza mpaka nikasema leo Geb atamkamata Malii. Bwana yule alikuwa akihangaika, basi bibi huyu katulia kimya. Anawaka kama alivyosema Gozi. Akiongea tu, mashavu yanabonyea! Mbona niliamini alichokisema Gozi! Lakini tena mimi mwenyewe pale nikawa kama sijielewi. Hoteli kama ile sijawahi kufika. Soda kwenye glasi! Kwa nini bwana!?” Kidogo watu wakacheka.

“Kumejaa visu na vijiko vya kila namna. Meza imekuwa kama kabati la vyombo! Basi pale mimi nikasema heri nikapumzikie chooni. Nikaaga, nikawaacha hapo mezani ili nikirudi, angalau nikute wameshika vile vifaa pale mezani, nijue wanatumiaje. Nikakaa huko weee, kurudi nikakuta kila mtu ana kisu na uma kasoro Nanaa kashikilia paja lake anakula kwa mkono.” Kila mtu akacheka. “Kwa msosi huyu! Hawezi kutumia kisu na uma! Vitamchelewesha.” Danny alimchokoza.  Nanaa akacheka tu huku akimpapasa mwanae aliyekuwa ameshalala na yeye alishamaliza uji wake, akawa amejilaza pembeni yake. Geb alishampokea bakuli tupu alilokuwa amemalizia uji.

 “Basi pale na mimi nikasema nimwige Nanaa. Nilipaliwa, pale, Geb alipotuomba tumsimamie harusi. Hakika nilipaliwa mama. Muulize Nanaa na Geb. Mpaka ilibidi niletewe maji ya kunywa. Bwana Malii alikasirika nusura apasuke.” “Kwa nini sasa?” “Wakati tupo njiani tunarudi nyumbani ndipo akaniambia nimemtia sana aibu.” “Jamanii!!” Grace na mama G wakaongea kwa pamoja.

“Nilishamzoea hanipi tena shida. Hapakuwahi kuwa na mapenzi pale. Hata sijui ni kwa nini hata alinioa! Lakini ukweli nilishituka sana. Nikasema huyu kaka na akili yake yote anataka kumkabidhi fisi bucha! Asichokiona na kutojua ukweli kutoka kwa Malii rafiki yake ni nini mpaka kumfanya awe msimamizi wake!? Nikakumbuka majigambo ya Malii akisema, ‘atafutaye hachoki, na lazima atampata tu Nanaa. Kwanza Nanaa alishampenda yeye, lakini akazinguliwa na pesa ya Geb.’ Akasema walikuwa kwenye mahusiano ya muda mrefu sana na Nanaa. Mpaka Nanaa alishamtamkia anampenda sana. Lakini sijui Nanaa alihamia nyumbani kwa Geb sijui, ndio Geb akamzidi mahesabu! Kuna kajistori alikizungumza, sikukielewa vizuri kwa kuwa alikuwa amelewa sana siku akinisimulia. Alikuwa anachanganya maneno, lakini ni kitu kama hicho. Na yeye alitoa malalamishi yake hapo juu ya Nanaa.” Manka akazua ganzi mwilini mwa Nanaa.

“Sasa nikajiambia Geb anafanya kosa la mwaka. Anamrudisha Nanaa kwa Malaya yule! Lakini nikajirudi, nikamkumbuka shoga yangu Mary. Nilimuomba anisimamie harusi yangu, akiwa rafiki wa karibu sana kwangu. Mwaminifu niliyekuwa nikimwamini na chochote, lakini akaishia kuwa mke mwenzangu. Nikajiambia wanadamu hawatabiriki. Nikasema nisubiri nione mwisho wake. Basi Malii akawa amefurahi kweli. Akawa anatamba kuwa tunasimamia harusi, halafu tutalipwa.” “Hee! Kumbe ilikuwa uwalipe?” Mama G akamgeukia Geb.

“Alisema tarehe hiyo angetakiwa asafiri kikazi. Anabiashara yake sehemu. Akasema asipoenda weekend hiyo atapoteza hiyo pesa. Ndio nikamuuliza ni kiasi gani aka..” “Muongo. Tena tapeli mkubwa mwenzio yule. Alikuwa anakupangia pesa kubwa ili umpe amalizie mambo yake. Pale alipo hana cha biashara wala nini! Bado tunaishi kwenye nyumba ya kaka  yake yule aliyehama hapa nchini na familia yake. Basi ile nyumba yake, ndio sisi tunaishi hapo mpaka leo. Tunaishi bureee. Pesa yake yote, starehe. Tena kuna wakati mama yake alikuja kutusalimia hapa mjini. Akakutana na hali hiyo ya mwanae. Yule mama alienda sokoni Kariakoo kununua vyakula kwa uchungu. Akiondoka asubuhi Malii hajali hata huku nyuma mama yake anakula nini.” Manka alimkatisha Geb akaendelea yeye.

“Mimi nilishamzoea. Haachi pesa pale ndani. Na akirudi anakuwa ameshiba na kalewa. Ni matusi tu kwenda mbele mpaka mnalala. Sasa mama yake akawa anaumia kuona vile. Mimi kimya. Nanunua ninachoweza, nampikia namwachia hapo, naenda kazini. Na kwa kuwa nilishamjua ni mshenzi, nikaanza kupanga mipango yangu mingineee! Ikikamilika tu, atanisikia mitandaoni. Sitaki ujinga.” Manka akajisifia.

“Kwa hiyo mama wala usinione nimekaukwa mdomo bure. Sina cha mimba wala nini. Yule bwana hanigusi, kwanza hata nishasahau mara ya mwisho ni lini. Ila,

Mungu atamlipa Malii. Atamlipa vibaya sana.” “Mama yake alijaribu kuzungumza naye?” Mama G akahoji.

“Kwani unafikiri mama yake aliishia hapo? Alirudi kwao, akarudi tena pale na baba yake Malii. Na yeye akajionea. Malii alijitahidi siku mbili tatu, akashindwa. Akarudia wehu wake vilevile mbele ya wazazi wake. Yule Mzee alikuwa anaongea kichaga kitupu, Kiswahili kilimpotea. Mpaka ungemuhurumia. Walimuonya sana. Yule baba alimwambia asipobadilika, atakufa bado mdogo. Ni mchafu yule, mama! Hujawahi kusikia. Hakuna mwanamke mweupe anayempita. Mpaka unamuhurumia. Analala kwenye kochi kwa kuchoka kwa pombe na wanawake. Kwa hiyo Geb! Ni Mungu ndio alikusaidia kututoa kwenye harusi yenu. Ulikuwa unatumbukia shimoni. Toa sadaka kanisani. Analala akimuota Nanaa yule. Wala sio siri. Hakuna siku asimtaje Nanaa. Hata Gozi anajua hilo ila anasema hatakwambia. Hataki kuonekana mchonganishi. Na ameapa atampata Nanaa tu. Sasa Nanaa jiandae.” Manka akataka kusimama.

 “Aendelee kuota hivyo hivyo. Hatawahi kunipata hata iweje.” “Kwani wewe Nanaa ulikuwa ukimfahamu Malii kabla ya Geb!” Grace akauliza, Nanaa akanyamaza kidogo. James akamgeukia vizuri.

“Nanaa?” James akamuuliza kwa ukali kidogo. “Abee.” Akamwitikia kaka yake, James akabaki akimtizama. “Ndiyo na hapana.” Nanaa akajibu akiwa anaangalia chini. “Ndio nini!? Ulishakuwa na mahusiano naye?” James akauliza kwa ukali kidogo. “Hebu subiri kwanza James. Unawezaje kumuhoji mke wa mtu maswali kama hayo? Huko ni kunivunjia heshima. Mnavuka mipaka na sitaruhusu. Nanaa ni mke wangu mimi. Nashauri James uanze kuelewa hilo na kuliheshimu. Anawajibika kwangu tu, si kwa mtu mwingine yeyote.” Geb akawabadilikia. Kila mtu akabaki kimya.

“Hata hivyo muda wakumuona umeisha. Daktari ameshauri alale.” Geb aliongeza na kumfunika vizuri Nanaa. “Lakini jioni nilitaka tuje kula chakula cha usiku pamoja, baba. Kama kumshukuru Mungu na kusherehekea birthday ya Oliva.” Mama G akajua ameshakasirika. Akaongea naye kwa upole. “Naomba tuwasiliane kwanza mama. Akiamka nitawajulisha hali yake ilivyo. Bado pressure yake ipo juu. Anahitaji utulivu. Kwa nini tusisubiri akitoka ndipo tukamshukuru Mungu pamoja nakufanya hiyo sherehe ya Liv?” “Hata hivyo mimi mwenyewe nitarudi baadaye kuleta vyakula na kumwangalia Nanaa. Nataka kujua anaendeleaje.” Kimya. “Hata mimi pia nitarudi baadaye.” Grace akaongeza. Nanaa hakujibu.

James akamkabidhi Magesa kwa Nanaa, wakatoka. Geb na yeye akamchukua Liv pale kitandani akamsindikiza mama yake akiwa amembeba. Nanaa akaanza kumnyonyesha tena. Nesi akaingia tena, akampima nakutoka akiwa ameonyesha uso wa wasiwasi. Nanaa akajua majibu ya presha aliyompima hayakumfurahisha. Hakujali. Akaendelea kumnyonyesha mtoto wake huku amejawa furaha na hofu ya Malii.

Magesa alinyonya bila kumaliza. Nanaa akajua hashibi sababu Liv alishanyonya maziwa yote muda mchache uliopita. Geb akarudi baada ya kuhakikisha amemfunga vizuri mtoto wake kwenye gari. Akamfunika nakumbusu mara kadhaa. Liv alikuwa amelala. Akawaaga mama yake na dada yake na watoto, akarudi chumbani kwa Nanaa.

 ~~~~~~~~~~~~~

“Naona hapati kitu huyu. Anavuta bila kupumzika.” Nanaa akamuwahi Geb mara alipoingia. “Liv huyo! Amemaliza maziwa yote.” “Sijui nitamfanyaje ili kumuachisha ziwa. Na hasahau! Hata mkitengana siku tatu, akirudi analilia nyonyo.” “Lakini itabidi aachishwe kwa nguvu. Hutaweza kuwanyonyesha wote wawili. Na hivyo alivyo Liv, na ninavyomuona kaka yake, utachoka sana.” Geb akaongeza huku akimsogelea karibu mtoto wake. Nanaa akamuona anacheka.

“Nini?” Akamuuliza. “Nilikuwa nikimsubiria kwa hamu huyu? Nilikuwa natamani sana kumuona. Nilijua atafanana na mimi na baba.” “Hata hivyo naona mmefanana.” Geb akamtizama vizuri. “Sidhani. Una rangi kali sana Nanaa. Huyu mtoto atakuwa kama Liv. Naona wanakuwa kama mapacha!” Nanaa akabaki akimtizama mwanae kwa makini. “Kweli atakuwa kama Liv. Natamani aniangalie.” Nanaa akaongeza. “Macho yangu hayo.” Geb akaongea kwa kujisifu. “Na manywele kama dad. Kila kitu ni wewe Geb, nahisi ni rangi tu. Ngoja tumsubirie tuone.” Wakaendelea kuongea huku mtoto akisikika kunyonya kwa kutoridhika.

Mara daktari wake akarudi. “Lazima kumuweka chini huyo mtoto ulale, Nanaa. Naomba safari hii unisikilize. Umempata huyo mtoto kwa bahati sana. Usifikiri ndio umepona. Nesi amenipigia simu, imebidi nirudi. Presha bado haijashuka. Naomba upate muda wa kupumzika kabisa.” “Akishiba huyu, nitalala. Nahisi maziwa hayatoki.” Nanaa akajitetea.

“Ndio hicho nimekuja kuzungumza na nyinyi. Najua Nanaa hupendi maziwa ya kopo. Lakini safari hii itabidi tu ukubali. Kwanza sababu ya aina ya mtoto uliyejifungua. Ni wakiume. Na nilikwambia tokea yupo tumboni, mwanao anaonekana ni mlaji.” Nanaa akacheka. “Alikuwa akila vidole hapa.” Nanaa akaongeza huku akimwangalia.

“Ehee! Sasa nataka kwa siku saba mfululizo, ulale tu. Utapata muda na mtoto wako. Utamnyonyesha, lakini najua kwa sasa hatashiba. Lazima aongezewe maziwa ya kopo, kuepusha kuamka wewe mara kwa mara. Katikati ya usiku na mchana. Nataka uwe unapata masaa yasiyopungua 8 usiku. Bila kuamka. Kulala moja kwa moja. Nitakuwa nakupa dawa. Na mchana pia..” “Nitamnyonyesha mwanangu na nitalala.” Nanaa akaingilia.

“Umeanza ubishi Nanaa.” “Sasa kwa nini mwanangu ale maziwa ya ajabu wakati mimi nipo? Ningekuwa nimekufa hapo sawa.” Nanaa akabisha. “Naomba unisikilize mimi Nanaa. Mimi ndio daktari wako kwa sasa, na kesho nitakuletea daktari wa mambo ya moyo azungumze na wewe labda yeye utamuelewa vizuri.” “Mimi nakutaka wewe.” “Hapana Nanaa. Mimi huwa hunisikilizi. Acha nikuletee daktari ambaye ni mgeni kwako, labda utamuelewa. Geb!” Akamgeukia Geb.

“Hali ya Nanaa si nzuri. Sikutaka kuwatia wasiwasi, lakini lazima ujue presha yake sio nzuri. Anaweza hata kupata kichaa cha mimba, kifafa na mengineyo, hata kifo. Kama hamtanisikiliza, atakuachia hawa watoto wakiwa bado wadogo sana.” Hapo ndipo Nanaa akatulia. Daktari akaanza kuwaeleza kwa utulivu. Mpaka Geb akaelewa. Aliuliza maswali mengi na yule daktari akayajibu na kuwaahidi daktari wa kesho yake atazungumza nao zaidi. 

“Usiwe na wasiwasi. Mimi nimeelewa. Na Nanaa atapumzika. Kama kuna maziwa yeyote unayojua ni mazuri kwa Magesa, niandikie nikayanunue sasa hivi.” “Kwa sasa nesi atakuja kumchukua mtoto. Atoke kabisa hapa. Watamlisha na kukusaidia kila kitu. Ukienda kuwaletea hayo maziwa, utawakabidhi wao. Watakuwa wakimuhudumia wakati wote. Watakuwa wakimleta kwa mama yake kwa masaa fulani. Ili amnyonyeshe na kukaa naye kidogo, kisha watamchukua ili Nanaa apumzike kabisa. Akiruhusiwa, anaweza kuacha kumpa hayo maziwa ya kopo. Akaendelea kumnyonyesha kama alivyofanya kwa Liv.” “Nimeelewa na nitahakikisha anafuata masharti yote. Muda mwingi nitakuwa naye hapa. Atapumzika tu.” Geb akatoa matumaini.

~~~~~~~~~~~~~

Alikuwa ni daktari aliyekuwa akimuhudumia Nanaa tokea yupo chuoni. Nanaa alimzoea sana. Na kwa kuwa alijua historia ya kuzaliwa kwa Nanaa, akajikuta ni mgonjwa wake anayemuweka karibu sana. Na utundu wa Nanaa, ukawafanya wazoeane kwa karibu. Kasoro alisumbuka na ubishi wa Nanaa. Angalau Geb alipoingia kwenye picha, kidogo ikaleta nafuu.

~~~~~~~~~~~~~

Mtoto alipokuja kuchukuliwa na nesi kama alivyoongea daktari, akamtaka Nanaa alale kabisa. Geb naye akatoka kwenda kununua maziwa aliyoagizwa na daktari. Nanaa akalala usingizi mzito. Lakini baada ya muda akashituliwa na ndoto yake na Malii. Akaogopa sana. Akabaki akiwaza pale kitandani. Picha ya akiwa na Malii na yale aliyoyafanya naye siku ile wakiwa wawili tu yakaanza kumsumbua. Akajua kwa hakika ndio maana Malii anateseka mpaka sasa. Alimkatili vibaya sana. “Nimwambie ukweli wote Geb?” Nanaa akawaza huku amejilaza hapo kitandani. Palikuwa pametulia sana. Hapakuwa hata na dalili ya kuwepo mtu.

“Geb akijua ukweli wote, atachanganyikiwa. Heri niache tu.” Nanaa akakataa wazo la kumwambia ukweli wote Geb. Walipokutana na Malii, kabla hajamkatalia penzi, ni mengi yaliendelea kati yao kabla ya hatua ya penzi. Lakini Nanaa akajiambia hatathubutu kumueleza yote Geb. “Kama busu tu lilimfanya apige teke kiti! Akijua yote atarukwa na akili.” Nanaa akakusudia kunyamaza. “Hata hivyo hatukwenda mbali san..” akasita kidogo.

~~~~~~~~~~~~~

Ni nini kilitokea kati ya Nanaa na Malii kinachomchanganya Malii kwa kiasi hicho? Geb Hapendi Siri, Nanaa anaogopa kumwambia ukweli, itakuaje mbeleni atakapojua ukweli ambapo hakuna siri duniani?

Malii aliyeapa lazima atampata Nanaa hata iweje, atafanyaje akiwa ameshatoka kwenye maisha yao ramsi hata usimamizi wa harusi amekataliwa na Geb?

Usipitwe…

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment