“Ni nini hicho kikubwa unachokificha
kwa mtu kama mimi ambaye nipo tayari kusimama na wewe kila mahali, na kwenye
kila hali!? Nimekuthibitishia kwa vitendo kuwa ninasimama
nawewe hata iweje! Ulitaka nifanye nini tena ili uniamini?” Ikageuka lawama,
lakini wazi Nanaa alimjua hayupo tayari na huo ukweli. Lakini kwa jinsi
alivyomjua, alijua hakuna jinsi ya kupambazuka hapo, kama hatajua
alichokianzisha. “Eti Nanaa? Mpaka unanitisha! Nani huyo mwenye thamani kubwa
hivyo, yakufichwa kuliko mimi kujua ukweli?” “Mimi nakujua Geb ndio maana
nimeamua kukulinda. Hauwezi kubaki hivyo ulivyo ukiendelea kuchimbua haya mambo.
Yalitokea tukiwa hatuko pamoja, yaliisha, nakusihi Geb, yaache kama yalivyo.” Nanaa
naye akamsisitiza, tena kwa kumtahadharisha kwa wazi kabisa.
“Katika hili sitaki ulinzi wako. Wewe niambie
tu.” Nanaa akamtizama vile ambavyo ameshabadilika. “Nanaa?” “Naomba maji kwanza.”Akampa
na kuyanywa. “Umetosheka?” Akatingisha kichwa kukubali na kuanza. “Kuna siku
usiku kabla ya kulala, nilipata simu. Iliita sana. Kwa kuwa ilikuwa usiku na
sikujua namba yake, Sikupokea.” Geb akarudi kukaa. Nanaa akasita. Akamwangalia tena
kwa makini. “Naomba uniahidi hutafanya kitu Geb.” “Mbona unanipa masharti
wakati hata hujaanza kunisimulia habari yenyewe? Ni nani unayemtetea hivyo!?”
“Sio kumtetea. Nalinda amani.” “Naomba endelea Nanaa.” Geb alisikika kutotaka
kupotezewa muda.
“Akatuma
ujumbe. Akajitambulisha kama yeye ni secret admire wangu!” Nanaa akaendelea. “Tuka chat usiku ule kwa
muda mrefu tu. Vichekesho tu na mambo ya kawaida. Siku hiyo ikapita. Kesho yake
akaniamsha na ujumbe mzuri sana. Tuka chat kidogo, tukaagana. Mchana ikawa
hivyo hivyo na usiku, mpaka ikajengeka tabia. Kila nilipokuwa nikimwambia
anitajie yeye ni nani, hakutaka kuniambia.” “Kwa hiyo ukaendelea ku chat na mtu
usiyemjua!?” Geb akauliza kwa wivu akionekana kama anashangaa.
“Yalikuwa
mambo ya kawaida tu, sikuona ubaya wake. Alikuwa akituma jumbe za kujengana,
faraja na mambo mengine ambayo hata wewe ungependelea kuyajua.” “Ulimwambia
mama?” Geb akauliza. Nanaa akababaika sana. “Nanaa?” “Hapana.” “Kwa nini?”
“Sikuona sababu Geb. Mara nyingi nilikuwa nikizungumza na mama yale mambo
niliyokuwa nikimtaka ushauri tu. Mwanzoni Malii alikuwa akituma jumbe za
kawaida tu.” “WHAT!!??” Geb alishituka mpaka akasimama. Nanaa aliropoka
jina, hakutaka kumtaja mpaka mwisho wa stori nzima.
“Naomba
ukae chini Geb na utulie. Hakuna kilichotokea kati yetu. Tafadhali Geb.” “Hivi
unajua Malii alikuwa anajua kuwa nakupenda? Malii ndiye mtu pekee niliyemtamkia
kwa wazi tokea tupo sekondari kuwa ninavutiwa na habari zako anazozisimulia
James! Nikamwambia ninaguswa na wewe kwa namna ya tofauti sana. Nikamwambia
nina upendo wa ajabu sana kwako. Tena akaniuliza nampendaje mtu ambaye
sijamuona, nikamwambia kuna kitu cha tofauti najisikia kila ninaposikia habari
zako. Iweje leo aje kinyume nyume akutake wewe?” Geb alishakuwa amekasirika.
“Sasa
hivi ndio naelewa ni kwa nini hakutaka nimwajiri mdogo wake tena, japo mimi
nilikuwa tayari kumuajiri mpaka nikabadili mawazo. Nafikiri yule mdogo wake
alipokuona na kukupenda, alimwambia Malii kwanza kabla hajaja kwangu kukuulizia
baada ya Malii kumnyima habari zako. Malii akaamua amtenganishe mdogo wake na
wewe ili asimzibie yeye. Akanitumia ujumbe ambao ulinishangaza, akisema nisimwajiri
tena mdogo wake. Nilipomuuliza ni kwa nini, hakutoa sababu za kueleweka. Ila kwa
kuwa alishafanyiwa usahili na Grace, ikawa lazima aje nikutane naye na mimi. Kesho
yake alipokuja ofisini na kuanza kukuulizia kwangu, ndipo nikamnyima kazi. Lakini
sikuwa nikijua nia ya Malii kwa wakati huo kuwa ni wewe kwa kuwa tayari
alikuwa kwenye mahusiano na huyo mkewe!”
“Ndio
maana sikutaka kuendelea naye Geb!” “Kuendelea naye!? Kwani mlifikia wapi!?”
“Nitakusimuliaje hivyo ulivyo hamaki? Unaniogopesha mpaka mimi mwenyewe Geb!
Naomba utulie usikilize mpaka mwisho. Tafadhali. Na sasa hivi nilazima ukae
unisikilize ili usibakiwe na habari nusu nusu.” Geb akabaki amesimama.
“Geb!
Naomba ukae.” Nanaa akamlazimisha kwa ukali kidogo. Akawa kama anayejishauri na
kiburi chake, Nanaa akabaki akimtizama, mwishoe akarudi kukaa. “Na hakuna
kuficha kitu.” Geb akaongeza kwa hasira. Wivu ulishaibua hasira zote ndani
yake. “Naomba tulia Geb. Mimi huwa sikudanganyi.” “Uliishia pale anakufurahisha
kwa jumbe zake za faraja na kukujenga.” “Geb!” Nanaa akashangaa. “Ndio nataka
uanzie hapo. Maana unamtindo wa kusema ‘kwa
kifupi’. Nataka habari nzima.” Nanaa akajua hapata kuchwa usiku huo utakuwa
mrefu haswa.
“Endelea
sasa.” Geb akasisitiza. “Ndio tukaendelea ku chat mpaka nika, au niseme
tukapanga kukutana.” “Tafadhali sana Nanaa. Naomba malizia sentensi yako. Mpaka
ukafanyaje?” “Nilivutiwa naye Geb! Kwanza ukumbuke mimi sikuwa nawafahamu
rafiki zake wote kaka James. Hata Malii sikuwa nikimfahamu kihivyo. Basi. Siku
ya kwanza tukakutana. Ilikuwa siku ya jumapili. Nyinyi mlikwenda kanisani, na
mimi nikaenda kanisani kwetu. Wakati ule kabla hatujaanza kuabudu kanisa moja.
Na nilisikia Liz akisema mchana mtakwenda sijui kwa ndugu yake gani sijui,
alikuwa na sherehe ndogo. Aliamua kuifanya mapema kwa kuwa kesho yake ilikuwa
siku ya kazi. Liz alikuomba muongozane siku ya jumamosi, tena mlikuwa mmekaa
sebuleni, halafu mimi na mama tulikuwa tumekaa sehemu ya kulia chakula,
ukamkubalia kuwa mkitoka kanisani utamfuata muende.” Geb akanyamaza.
Hakukanusha wala kukubali.
Nanaa
alipoona kimya, akaendelea. “Mimi nilivyotoka kanisani, nikaenda kukutana na
Malii. Tulizungumza mambo mengi na mazuri tu. Ndipo akanitamkia kuwa
ananipenda.” Nanaa alimtizama Geb vizuri. Alishakuwa amebadilika mpaka macho
yalikuwa mekundu. “Lakini katika mazungumzo yetu nikaanza kufikiria nilimuona
wapi? Ndio nikamwambia aniambie kwa hakika alipata wapi namba yangu. Akaniambia
hataniambia ila alisisitiza anataka nijue kwa hakika ananipenda na amekuwa
akinifuatilia kwa muda mrefu ndio maana ameamua kuvunja ukimya.” Nanaa
akaendelea.
“Nilipomuuliza
ni wapi aliponifahamu mpaka akapata moyo wa kuendelea kunifuatilia, akasema
hataniambia. Ndipo nikamwambia bila hivyo sitataka kuwasiliana naye tena.
Nikasimama na kutaka kuondoka. Ndipo ikabidi aniambie yeye ni rafiki ya kaka
James. Tukazungumza mambo mengi. Tukaagana. Lakini jumbe zikaendelea kama
kawaida. Kwa kweli mwanzoni nilianza kuvutiwa Geb. Naomba nikiri. Alikuwa mwema
sana kwangu. Upendo. Na wakati wote alihakikisha ananijulia hali na kutaka
angalau kunisikia.” Nanaa akanyamaza akasita. Akanyamaza.
“Nakusikiliza
Nanaa.” “Siku ile ya ijumaa, ile uliponiona nimetoka. Tulipanga tokea siku ya
jumatatu. Aliniambia ijumaa ni birthday yake. Nikamuuliza angependa zawadi
gani, akaniambia angependa kuniona siku hiyo mapema kidogo, kwa kuwa jioni nilazima
awe na wazazi wake, walikuja kutoka Moshi.” “Wewe kwa nini hukushangaa kwa nini
hakukukaribisha huko kwa wazazi wake?” Nanaa akanyamaza.
“Ikawaje
sasa?” Geb akaendelea kuuliza. Lakini wazi alishaonekana amekasirika sana. “Si
ndio mambo hayakwenda kama tulivyotarajia nikarudi nyumbani.” “Nanaa please.
Unajua kabisa mimi sipendi hivyo unavyokuwa unafupisha maneno. Inamaana kuna
kitu unaficha.” “Umekasirika mpaka nashindwa kukwambia kila kitu.” “Lazima
nikasirike Nanaa. Malii amenizunguka na wewe ulinificha.” “Alinisihi sana
nisikwambie Geb. Akasema nikikwambia nitakuwa nimeharibu kila kitu. Ndio maana
mimi sikutaka hata kwenda Marangu. Sikutaka hata kuja kumuona tena.” Geb
alikunja uso.
“Naomba
urudi nyuma Nanaa. Tafadhali sana. Nina hali mbaya kuliko ninavyoweza
kukueleza.” “Sasa kwa nini uwe hivyo Geb na wakati kwanza ni historia ya nyuma!
Hatukuwa kwenye mahusiano na wala…” “Naomba usiendelee kuniumiza Nanaa.
Ulishajua nakupenda.” “Hapana Geb! Mimi ndio nilijua nakupenda. Mapenzi yangu
kwako ndio yalinifanya nikatae kila mtu.” “Kama kweli ulijua unanipenda, sasa
kwa nini ulitoka na Malii?” Geb akauliza.
“Hiyo
ilikuwa mwanzoni kabisa nilipokukatia tamaa Geb! Nilikupenda kabla sijajua kama
hata una kazi ya kueleweka. Kuja kukujua sivyo ninavyokufikiria kuwa ni mlala
hoi, na kampuni ninayofanyia kazi ni yako! Nikaja kumuona na Liz. Anatambulika
kwenu na mama yako anampa baraka zake, nilikata tamaa Geb. Malii alikuja wakati
niliokuwa nikihitaji mtu.” “Kwa kuwa alikuwa akijua kinachoendelea. Alikusudia
kunizidi mahesabu. Alijua ndio kipindi changu cha mabadiliko na yeye ndio aka…”
Geb akasimama na kupiga teke kiti alichokuwa amekalia, na kutoka nje.
Mwili Ni Udongo.
Nanaa
akaanza kujisikia vibaya. Akabonyeza kengele kumuita muuguzi. “Samahani. Naomba
nipime tena pressure. Sijisikii vizuri.” “Hata hivyo muda umefika wa kukupima
tena.” Yule nesi akaleta mashine ya kupimia, akampima pressure. Ilikuwa juu
sana, ikabidi daktari wa zamu apigiwe simu. Akafika.
“Hii
pressure ipo juu sana, Nanaa. Huwezi kuendelea kumbeba huyu mtoto. Lazima
atolewe lasivyo utahatarisha maisha yako.” “Huyu mtoto hatatoka humo ndani.
Wewe nipe dawa nyingine ya usingizi, nilale.” Dokta alibaki akimwangalia Nanaa.
“Ila ninachoomba. Uache maagizo kuwa haruhusiwi mtu yeyote kuja kuniona kwa
muda wa siku tatu mfululizo. Nataka nilale tu. Lazima huyu mtoto azaliwe siku
zake zitakapotimia. Ila sio leo wala kesho. Kama mkiweza kuniwekea dripu ya maji
kwa ajili ya kuupa mwili wangu nguvu, ningeshukuru zaidi ili hata nisiamke
kula.” Akajua labda Nanaa hajamuelewa.
“Labda
hujaelewa Nanaa. Kwa hali yako hiyo ukiendelea hivyo, huwezi kuishi.” “Niamini
mimi nikikwambia kuwa huyu mtoto hajaja kwa ajili ya kuniua. Kama kuna mahali
unataka nisaini kuwa nimekataa nisitolewe mtoto, nipe nisaini. La sivyo mimi
hapa nimefika na wala sitakufa. Hujaniona nikiwa nakaribia kufa wewe. Hapa sipo
hata robo yake. Wala usitie shaka. Nipe dawa.” Hakutaka kubishana naye, kwanza
alijua daktari wake atafika hapo, watamalizana. Yeye amalize zamu yake huo
usiku, atoke. Akaandika dawa ambazo angetaka atumie, mara Geb akaingia.
“Kuna
nini!?” Geb akauliza kwa mshituko mara baada yakurudi pale chumbani, na kukuta
daktari na wauguzi wawili. “Naomba umpe ule ujumbe uliosema utawapa ndugu zangu
wote.” Nanaa akamrushia mpira dokta. “Ujumbe gani!?” Geb akauliza. “Pressure
yake ipo juu sana. Hataweza..” “Hapana. Huo sio ujumbe ninaotaka uwape. Hujui
uwezo nilionao dokta. Hujui ni nini naweza na nini siwezi. Wewe waambie kwa
muda wa siku tatu, haruhusiwi mtu kuja humu chumbani isipokuwa madaktari na
wauguzi tu.” “Haiwezekani Nanaa!” Geb akashangaa.
“Sasa
unataka kubaki hapa ili ufanyeje? Huna unachokifanya zaidi ya kunikorofisha tu.
Nimekusudia kumzaa huyu mtoto akiwa mzima na siku zake zikiwa zimetimia kama
Liv. Hakuna mtu wala mazingira yatakayonizuia. Kwa kuwa umeshindwa kuwa msaada
wangu, naomba unipishe nitimize jukumu langu kwa mtoto wangu. Kwa sasa
ananihitaji mimi kuliko wewe Geb. Daktari anafikiria atolewe humu ndani,
akidhani anahatarisha maisha yangu. Nimekusudia kumpa uhai mtoto wangu.
Nitapambana mimi mwenyewe kama nilivyofanya kwa Liv, ndivyo nitakavyofanya kwa
Magesa, bila wewe. Kwa kuwa wewe umeshindwa Geb.” Nanaa
alishakasirika.
“Sasa
nataka kujua, unanipisha ili nitimize jukumu langu au mimi nikupishe nikatafute
njia zangu za kumuokoa mtoto wangu? Halafu nitakuletea nikishamzaa, kama Liv.” Geb
hakuamini. Nanaa alimbadilikia kama sio yeye. Alikuwa ni kama simba anayetetea
mtoto wake. “Nitatulia Nanaa.” “Hapana. Kwa sasa tulipofika ni pabaya. Ni aidha
wewe utoke au Magesa ndio atoke. Sasa mimi nimemchagua yeye abaki, wewe ndio
utoke hapa. Maana Magesa hana kimbilio. Wewe unalo kimbilio. Una kitanda kizuri
na cha fahari kinakusubiri nyumbani.”
“Hivi
unajua watakapomtoa mtoto wangu sasa hivi ni wapi wataenda kumueka? Udongoni.
Mtalia na kunyamaza, mimi nitaachwa na jeraha ambalo halitapona maishani mwangu
kote. Mtasema alikuwa mtoto ambaye hajakomaa au mtoto si riziki. Kwangu mimi
Magesa ni mtoto kama Liv. Sitaruhusu mwanadamu yeyote aharibu kusudi la Mungu
kwenye maisha yangu. Umeshindwa kupambana pamoja na mimi, mimi ndio
naanza mapambano. Na siwezi kuwa na wewe kwa kuwa unanishika miguu. Naomba
uondoke Geb. Na uwaambie watu wote, nahitaji mapumziko ya siku 3 mfululizo.
Sihitaji mtu yeyote aje anione wala aniletee chakula. Nitakula chakula cha hapa
hospitalini.” Geb alibaki kama haamini.
“Na
Liv je!? Nitamleta anyonye.” “Hapana. Liv atasubiri. Yeye anaweza kula ugali,
mdogo wake hana tumaini jingine isipokuwa mimi. Anaweza kuishi bila kunyonya,
kaka yake hawezi. Usiku mwema Geb.” Nanaa akajiweka sawa. Kila mtu mle ndani ya
chumba alikuwa kimya wakisubiri wamalize. “Naombeni tuanze matibabu jamani.
Mnichome hiyo sindano, nilale.” Geb akakusanya vitu vyake akamsogelea Nanaa. “Samahani.”
Nanaa hakutaka kujibu. Akanyamaza kimya bila hata kumwangalia. Akabaki
akiangalia shuka alilojifunika. Geb akambusu kichwani. Akatoka. Ilishakuwa saa
sita usiku. Nanaa akachomwa sindano, hapo hapo akapitiwa na usingizi.
~~~~~~~~~~~~~~
Ni
kweli pressure ya Nanaa ilikuwa juu sana. Hata daktari wake aliyekuwa
akimuhudumia kipindi ni mjamzito wa Oliva, dokta Lyamu, alipopita kesho yake na
kusoma matokeo ya pressure ya siku iliyopita na asubuhi hiyo, alimshauri mtoto
atolewe. Akamwambia kwa miezi ile, wanaweza kumuweka mahali na anaweza akakua
tu. “Siku zake alizoandikiwa na Mungu kukaa humo ndani bado. Wewe niandikie
dawa za kutumia. Na waambie manesi waache kupita kila baada ya nusu saa na
kunipima pressure. Wananifanya nashindwa kulala. Wanapishana humu chumbani
kwangu mchana na usiku!” Dokta Lyamu alimfahamu tokea ujauzito wa Liv, akawa
amemjua Nanaa na mpaka wakatengeneza kama udugu sababu ya kumuonea huruma juu
ya historia ya kifo cha mama yake na kumuacha akiwa mchanga kabisa. Halafu kabila
likawa moja na mama yake. Akaishia kuwa daktari kama mjomba wa Nanaa.
“Huyu
mtoto hamtamtoa. Hilo wala halipo kwenye mjadala. Tuendelee na jingine.” Akacheka
na kutingisha kichwa. “Nanaa! Naomba unisikilize. Tatizo la mimba ile ya
kwanza, sio kama sasa hivi. Sasa hivi ni serious. Ni kweli utakwenda.” “Siendi
popote. Mimi nipo hapa na wewe mpaka baada ya week 3 mbele. Siwezi kukubali
mumtoe mtoto wangu halafu mje mniambie sijui joto la huko mlipomuweka lilipanda
au likashuka, akafa! Au sijui alizidishiwa dawa, sijui nini! Hapana.
Hapa alipo yupo salama. Mwache mtoto wangu.” “Wapo watu maalumu wakuhudumia
watoto wa aina hiyo.” “Wangapi wanatoka salama huko?” “Wengi tu!” Akamjibu kwa
kujiamini.
“Lakini
kuna wanaokufa. Si ndio?” Kimya. “Sasa Magesa hatakuwa kwenye idadi ya hao
wachache, wanaopatwa na bahati mbaya na kufa huko. Yupo hapa kwa makusudi. Wewe
endelea kuhangaika na hii nyumba yake, ambayo Mungu amemuweka. Nitibuni mpaka
muone nimekufa, ndipo mumtoe sasa. Lakini kwa kuwa kwa sasa yupo humo ndani.
Umemuangalia, na kufanya vipimo vyote. Wewe mwenyewe ukaniambia yupo salama
kabisa. Sasa hakuna atakayemtoa humo.” Waliposhindwa kumshauri madaktari hao
waliokuwa wamepita round akiwepo na daktari wake wa kliniki, wakajadiliana
jinsi ya kutatua tatizo hilo la pressure ili mtoto akae humo ndani.
Wakazungumza kwa muda mrefu huku wanafunzi wengine wa udaktari wakisikiliza kwa
makini na kumuuliza maswali mpaka Nanaa alipochoka, na kuwaambia analala.
~~~~~~~~~~~~~~
Ni
kweli zilipita siku tatu mfululizo Nanaa hajaonana na mtu yeyote. Alikuwa
akilala tu bila kuongea na mtu yeyote yule mbali na wauguzi wanao mtibu. Mungu
bariki siku ya tatu, pressure ya Nanaa ilishuka ikarudi kuwa ya kawaida.
Alijitahidi kutulia na kutowaza kitu chochote zaidi ya mwanae Magesa.
Akakumbuka jinsi alivyokuwa akizungumza na Oliva wakati yupo tumboni. Akaanza
kuzungumza na huyo mtoto kana kwamba ni mtumzima, wanaonana. Wakati wote mikono
ilikuwa tumboni akimpapasa mtoto wake.
Alikuwa
amefungiwa mashine ya kupima mapigo ya moyo ya mtoto. Nayo iliwapa matumaini ya
huyo mtoto kuendelea kuwa humo ndani salama bila shida. Daktari alimtaka pia
awe anakula, sio kuishi kwa dripu kama alivyotaka. Nanaa alikuwa akiletewa
chakula maalumu cha pale pale hospitalini na kula. Hakumuona mama G wala wanae
na wajukuu zake. Hata kaka yake hakuja kumuona. Akajua Geb alifikisha ujumbe.
Kwa hiyo akapata mapumziko ya kweli.
~~~~~~~~~~~~~~
Alipomaliza
siku tatu, siku ya nne alfajiri na mapema akiwa usingizini akahisi mtu
anamchora mgongoni. Alikuwa amegeukia ukutani. Akafungua macho bila ya kugeuka.
Akajua ni Geb tu. Akanyamaza. “Nina hamu na wewe Nanaa.” Akasikia sauti ya Geb.
Akanyamaza. “Samahani nilikosea. Sikutakiwa kuwa mkali kwako.” Kimya. “Au
tuseme sikutakiwa kuyaanzisha yale mazungumzo kipindi hichi ambacho unahitaji
msaada wangu. Ningesubiri tu. Naomba unisamehe.” Kimya. Geb alijua kuwa Nanaa
anamsikiliza. Akaendelea kumpapasa mgongoni.
“Daktari
ameniambia bado hutaki kumuona mtu yeyote, unahitaji muda zaidi wa kumpumzika.
Naomba tuwe wote. Nakuahidi nitabadilika. Sitakukera kwa maneno yeyote yale.”
Kimya. “Nanaa please!” Kimya. Geb akatulia kwa muda, akaanza tena. “Pia daktari
aliniambia Magesa anaweza kuzaliwa kuanzia baada ya siku 20 kuanzia sasa na akawa
sawa tu. Naomba tumalize wote hizo siku.” Kimya. Nana hakutaka hata kugeuka.
Akabaki amenyamaza. Geb alikaa hapo kwa muda bila kujibiwa kitu.
“Bado
hutaki uletewe kitu chochote kutoka nyumbani?” Kimya. “Liv anakutafuta Nanaa.
Anatambaa kila mahali, mama anasema anakutafuta wewe. Hachoki kwenda kwenye
kochi alilozoea kukuona umelala. Naomba nimlete baadaye. Japo kwa muda mfupi tu,
anyonye.” Hapo akamsikia analia taratibu. “Sitakaa sana. Nitamleta, akuone
kidogo tu. Ukiweza kumnyonyesha ni sawa, ukishindwa basi angalau mpate hata
nusu saa na yeye. Naomba usimwadhibu mtoto kwa kosa langu. Nakuahidi
sitazungumza chochote. Ni wewe na mtoto tu. Sawa?” Nanaa akatingisha kichwa
kukubali. Bado alimpa mgongo.
“Naweza
kukaa hapa kidogo?” Kimya. “Sitaongea Nanaa. Nakuahidi. Nakaa tu.” Kimya. Geb
akanyamaza. Baada ya muda mfupi sana akamsikia anakoroma. Akajua alikuwa
amechoka. Inamaana siku hizo zote tatu hakuwa amelala vizuri. Akageuka
kumwangalia. Bado alikuwa amekaa kwenye kiti, pembeni ya kitanda chake. Kichwa
amekiegemeza kitandani. Amelala hana habari. Nanaa akacheka mwenyewe.
Akampapasa kidogo kichwani. Na yeye akapitiwa na usingizi.
~~~~~~~~~~~~~~
Alipoamka
hakumkuta Geb. Alishaondoka. Akajua amekwenda kazini. Baada ya kusaidiwa usafi
wa asubuhi, akakaa ili ale. Akaona muuguzi mwingine anaingia na maua mengii na
kopo la icream. Nanaa akacheka. Akajua yanatoka kwa Geb. Alikuwa na hamu ya ice
cream. Akaomba apewe kijiko aanze kuila hiyo ice cream. Alikula ndio akasoma na
kadi. Ilikuwa kadi kutoka kwa Geb akiomba msamaha. Akaomba yule nesi amuwekee
maua yake kwenye chupa. Akamuwekea pembeni ya meza na kadi yake. Akala na
kurudi kulala.
Ilipofika
jioni Geb akaingia na Oliva. Oliva alifurahi sana kumuona mama yake. Kwa mara
ya kwanza alisema mama nzuri, bila kukosea au kuunganisha maneno na kumfanya
mpaka Nanaa alie. Akakaa na kumpokea. “Mama!” Oliva aliita huku akitoka kwa
baba yake na kutaka mama yake ampokee. “Na mimi nina hamu na wewe Liv.” Tayari alishamsogelea kifuani. “Husahau kunyonya tu!?” Nanaa alimuuliza mwanae huku akifuta machozi.
Oliva alianza kunung’unika akiashiria kutotaka kuchelewesha. Mama yake akamlaza
pembeni yake. Alionywa asiwe anambeba kwa wakati huo.
Kwa
hiyo wote wakalala pale kitandani. Akaanza kumnyonyesha. Alinyonya huku
akimtizama mama yake. Nanaa alikuwa akimwangalia kwa upendo. Ilisikika milio
yake akimeza maziwa ya mama yake kwa nguvu zote. “Umependeza Liv. Bibi ndiye
amekusuka?” Nanaa aliuliza kana kwamba atajibiwa. Oliva alibaki akimwangalia tu
mama yake huku akinyonya.
“Ni
Grace ndiye amemsuka. Alikuwa kwake tokea asubuhi anacheza na Fili.” Nanaa hata
hakumwangalia. Geb akanyamaza akajua bado Nanaa hataki kuzungumza naye. Swali
la kama harusi bado ipo au la, aliogopa hata kumuuliza Nanaa. Kuhofia jibu la
hapana. Akabaki kimya.
“Asante
kwa maua na Ice cream. Nilikuwa na hamu nayo!” Nanaa akavunja ukimya. Nusura
asimame. “Naweza kuleta tena usiku.” “Naomba usitafute sababu ya kurudi kuja
kulala hapa.” Geb akacheka. “Nitakuletea na nyama choma.” Tayari Nanaa akaanza
kushawishika. Nanaa mmpenda kula alikuwa akiletewa vyakula visivyo na chumvi!
Tena vyakula vya wagonjwa! Nyama choma ikasikika vizuri mpaka rohoni. Halafu hata yeye alikuwa na hamu na Geb. Mara
nyingi usiku wakiwa kitandani wao wawili walikuwa wakipata wakati mzuri sana.
Vicheko na stori za hapa na pale. Tena mara nyingi baada ya kupeana penzi zito.
Hata wakiwa hapo hospitalini, bado walitumia muda wao vizuri. Walipeana mabusu
ya haja huku wakiliwazana vyakutosha. Hakuna jinsi Nanaa aliyesumbuliwa na
wanaume, pamoja na ndugu waliomuona mzigo eti leo umwambie akae mbali na Geb
muda mrefu akafurahia. Hata kidogo. Bado hakuzoea kuhitajika kwa kiasi kile.
“Sijui
nilete na chips au ndizi za kuchoma?” Geb akajidai anajiuliza kwa sauti. Akajua
Nanaa ameshaingia line. “Halafu nimenunua movie nzuri. Naweza kuleta wakati
nakuletea ice cream na nyama choma. Ila sasa sijui nilete na nini!?” Geb akaendelea kutangaza hongo. “Kwani
ukileta vyote kuna shida gani!?” Nanaa akajibu nakumfanya Geb acheke. Akajua
ameshanasa kama mama yake. “Bwana usinicheke kwa kuwa unajua napenda kula!”
“Mimi nimefurahi tu.” Nanaa akamwangalia. Alikuwa akiishi na wanawake hao
wawili. Mashoga haswa. Nanaa na mama G. Na ndio wanawake aliowapenda sana.
Aliwajua udhaifu wao wote wawili. Mama yake mmpenda pesa, hiyo ikawa hongo
yakumtuliza. Na Nanaa chakula.
“Nimekumiss
Geb!” “Mwenzio hata silali vizuri. Nimekuwa kama mlinzi huko nyumbani.”
“Nimekuona ulivyokuwa unakoroma hapa asubuhi.” “Si unihurumie usiku nije tu
kulala hapa?” Nanaa akacheka. “Ukichelewa utanikuta nimeshalala.” “Naenda tu
kumshusha huyu, narudi.” “Sasa sio urudi mikono mitupu!” Geb alicheka huku
anatingisha kichwa. “Nanaa kwa chakula! Sitasahau mama. Najua hiyo ndio tiketi
yangu ya kuingilia hapa?” Nanaa akacheka.
Usiku.
Geb
alirudi akamkuta Nanaa amelala. “Nanaa!” Akafungua macho. “Nimepitiwa na
usingizi sasa hivi. Nilikuwa nasubiria hiyo nyama choma kwa hamu! Halafu Liv
ameninyonya mpaka ameniacha na njaa! Nikaona nisile chakula cha hapa
hospitalini ili nije kufaidi nyama.” “Atakuwa alikuwa tu na hamu na wewe. Grace
anasema alikula vizuri tu. Wala hakumsumbua kula.” “Aliamka njiani?” Nanaa
akauliza huku akijiweka sawa.
“Hapana.
Atakuwa alikuwa amechoka pia. Amecheza sana na Fili. Na hivi anataka kutembea
kama mwenzie, utamuonea huruma.” Nanaa akacheka. “Naomba umrudishe tena kesho.
Leo ameniita mama!” “Nimemsikia. Juzi ameniita mimi da-da.” Nanaa akacheka
sana. “Dada tena!” “Mimi sijali. Ilimradi najua ni mimi, nimefurahi sana.” Geb
akajibu.
Baada
ya chakula, Nanaa akaanza tena. “Geb! Najua bado unataka kujua nini kilitokea
kati yangu na Malii.” Geb akanyamaza. “Ungependa nimalizie?” “Sitaki iibue
mambo mengine Nanaa. Nataka huyo mtoto azaliwe mimi nikiwepo. Maana sasa hivi
mimi ndio nimegeuka mkosaji wala sio wewe! Naomba tuache tu. Tutakuja
kuzungumza wakati mwingine.” “Sasa mimi nilikosea nini Geb!? Mwanzoni sikujua
kama mnafahamiana na Malii! Pili hatukuwa kwenye mahusiano mimi na wewe!”
“Nanaa please! Naomba tuache tu. Ulijua nakupenda. Na ulijua kama ni kosa ndio
maana ulijificha hukutaka hata mama ajue na wala uliponikuta pale nje,
ulishindwa kuniangalia usoni. Ulisalimia na kuingia ndani moja kwa moja kwa
kuwa ulijua ulinikosea Nanaa. Dhamira ilikusuta kwa ulichotenda.” Geb
alisisitiza kukosewa.
“Siku
ile nilishindwa kukuangalia sababu ya kushindwa kufanya nilichotaka kufanya si
sababu ya kufanya unachofikiria. Nilijichukia kwa kushindwa kufanya kile mwili
wangu ulitaka kwa wakati ule sababu ya kubeba hisia za mwanaume ambaye alikuwa
mpenzi wa mtu mwingine! Tena ambaye nilijua siku hiyo hiyo usiku, mpenzi wake
anakuja kulala naye, humo humo ndani ya nyumba niliyomo mimi. Tena nikiwepo
chumba cha jirani! Wakifanya kile mimi ninachoshindwa kufanya wakati
huo.” Nanaa alianza kutokwa na machozi.
“Nikweli nilikwenda kukutana na Malii. Gari uliyoiona ilikuwa ni ya
dereva taksii. Nilishazungumza naye na kumwambia aje anichukue na kunipeleka
sehemu tuliyokubaliana na Malii. Haikuwa nyumba ya kulala wageni. Aliniambia ni
nyumbani kwa rafiki yake. Ni kweli nilishavutiwa na Malii. Kwa jumbe alizokuwa
akinitumia, alionyesha kunijali na kunihitaji. Nilifika kwenye hiyo nyumba,
tukala na kunywa. Lakini mimi sio mtoto Geb. Nilijua mwisho wa yote ni mapenzi.
Na nilikusudia kufanya hivyo. Siwezi kukudanganya.” Nanaa
alimfanya Geb abaki akimtizama.
Nanaa
akajifuta machozi. Akaendelea akiwa ametulia kidogo. “Na sio kwamba sikumwambia
mama kwa kuwa niliogopa! Mama alijua upo na Liz. Na aliona vile Liz alivyokuwa
akija kulala pale na wewe. Nilijipa muda ili nione tutakapoishia mimi na Malii.
Malii alikuwa tofauti na wote niliokuwa nikimwambia mama. Ni mtu niliyekuwa
nikifurahia mahusiano yake. Nilitaka kumchunguza kwa muda mpaka nione mwisho
wake ndipo nimtambulishe kwa mama na kwa kaka. Sikutaka ushauri wa mtu, kwa
kuwa nilikuwa nimekusudia kuwa naye. Malii ni mtu wa nyumbani. Hicho pia
kilikuwa kigezo kingine kilichonifanya nivutiwe naye kwa haraka kuona ni kabila
moja.” Nanaa akaendelea.
“Baada
ya kula na kunywa, ulifika wakati ambao hata mimi nilikuwa nikiusubiria kwa
hamu. Malii alininyanyua, akanikumbatia na kunibusu.” Nanaa alimuona Geb
amefunga macho na kutingisha kichwa. “Naomba acha Nanaa. Tafadhali sana.”
“Hapana Geb. Naomba nimalizie. Umeyataka wewe mwenyewe. Nilikubembeleza sana
tuyaache, ukakataa. Sasa tulia nimalizie ili uamue leo kama bado unataka kunioa
au utanihukumu kwa maisha niliyoishi zamani.” “Ukisema hivyo unakosea Nanaa.”
“Kweli Geb. Huyu mtu nilikuwa naye kabla yako. Na hata hatukuwa kwenye
mahusiano kwa muda mrefu.” “Kwamba unayatambua kuwa ni mahusiano!?” “Naomba
nisimulie mpaka mwisho Geb. Tafadhali sana.” “Mimi najihisi sipo tayari
kuzungumzia hili swala tena. Naomba tuache tu.” “Tunaachaje Geb?” Geb
akasimama.
“Hunielewi
Nanaa. Malii alinifanyia makusudi.”
“Makusudi kivipi wakati ulikuwa na Liz, Geb!?” “Huelewi Nanaa.” “Naelewa. Na
yeye alinisimulia kwa upande wake ndio maana na mimi nikakubaliana na swala la
kunyamaza, nisikwambie.” “Alikwambia nini?” Geb akauliza. “Ndio ukae sasa ili
nikusimulie ukweli wote.” “Naumia Nanaa.” “Unaumia
nini sasa?”“Malii amenigeuka.” “Hajakugeuka Geb. Wewe kaa chini.” “Wewe
zungumza tu.” Nanaa alijua ujeuri wa Geb umesharudi. Alibadilika. Akajua kiburi
chote kimerudi vile vile.
Akabaki
akimwangalia. “Wewe si unataka kumalizia? Malizia sasa. Uliishia kuwa mlikuwa
mmekumbatiana, mnakisi.” “Unatafuta kujiudhi bure Geb.” “Sio natafuta.
Nimeshakasirika sana Nanaa. Malii amenifanyia ubaya.” “Ubaya gani? Sio yeye
aliyekuuliza juu yangu?” Geb akakunja
uso.
“Malii
hakukuuliza utafanyaje juu yangu na Liz?” Kimya. “Unakumbuka jibu ulilompa?”
Kimya. “Sasa kama hukumbuki, Malii alikurikodi na akanisikilizisha.” “Eti
nini!?” Geb alishituka sana. “Ndio ujue hata mimi niliumia Geb. Lakini niliamua
kunyamaza tu. Malii alinisikilizisha mazungumzo yenu yote, mliyokuwa
mmezungumza siku ile. Niliyasikia majibu yako yote uliyokuwa ukimjibu Malii juu
yangu. Kwa hiyo hakuna aliyekuzunguka Geb. Malii alifanya kwa haki, kwa yale
uliyomjibu juu yangu.” “Kwa hiyo alinitega wakati ananiuliza ili anirikodi aje
kukwambia?” Geb akauliza, lakini wazi alionyesha kuishiwa nguvu. Kumbukumbu juu
ya mazungumzo yake na Malii juu ya Liz na Nanaa, ilimjia sawia kama
alivyojaliwa na Mungu kutosahau. Akakumbuka kila kitu.
“Hakuwa
amepanga kunisikilizisha. Ila baada ya kunibusu kwa muda, nilimwambia aniache
tu. Akauliza kwa nini, nikamjibu, ‘hapana’ tu. Ndipo akajaribu kunibembeleza
sana, lakini nilishindwa Geb. Hisia ambazo nilikuwa nikizisikia nikiwa na wewe,
hata ukiniongelesha tu, sikuzipata kwa Malii siku ile. Ila sikumwambia.
Aliniona nalia. Akadhani alikosea kitu. Nikamwambia hapana ni mimi mwenywe ndio
nina tatizo. Kumbuka Malii sio mwanaume wa kwanza kumkataa tokea nikuone wewe
na kukupenda Geb. Muulize mama. Lakini Malii nilitaka ndio nitulie naye baada
ya kukukatia wewe tamaa.” Geb akarudi kukaa.
“Malii
hakuwa ameelewa tatizo langu ni nini na mimi nilishindwa kumwambia. Ningeanzia
wapi? Namwambia vipi nampenda mwanaume anayenihifadhi nyumbani kwake? Tena
inajulika wazi mpaka kwa familia yake kuwa ana mpenzi? Tena anayekuja kulala
hapo hapo na ni rafiki ya dada yake!? Nilishindwa kumwambia Malii na
nilishindwa kuendelea hata kumruhusu anikumbatie kwa kuwa nilishajua zipo hisia
za kweli ndani yangu. Kuendelea kufanya chochote na Malii, itakuwa
nikutomtendea yeye haki na nafsi yangu pia. Nikabaki nikifikiria, nisijue cha
kumwambia.” Nanaa akaendelea.
“Kwanza
nilijisikia vibaya. Kwa kuwa aliniambia ile sehemu aliihangaikia makusudi kwa
ajili yetu siku hiyo. Kwa hiyo sio kwamba alinishitukiza alichotaka tukifanye!
Tulishazungumza na mimi nilimuonyesha kuwa nipo tayari. Sasa iweje tena
nimbadilikie wakati tulikubaliana na yeye alikuwa tayari kabisa kwa mapenzi?
Nikabaki nikifikiria na yeye akijiuliza kulikoni wakati ndio ulifika wakati
mwafaka ambao wote tulikuwa tukiuusubiri kwa hamu? Nilikataa hata asiendelee
kunishika. Ndipo akaropoka gafla na kuniuliza kwa kunishitukiza akasema, ‘au sababu ni Geb?’ Hapo ndipo nilishituka
mpaka akajua jibu ni ‘ndiyo’. Maana
ndio na mimi nilikuwa nikikufikiria.” Nanaa akaendelea. Hapo hata Geb hakutia
neno.
“Alinicheka
kwa dharau sana. Akaniambia wala nisijisumbue hata kukufikiria. Wewe huna
mpango na mimi. Na wanawake kama mimi tunaokufikiria wewe na kusubiria labda
siku moja utatukubali, akasema tuko wengi sana. Akanitajia majina baadhi
ya wanawake wanaokusubiria na ambao hata walishakutongoza. Akaniambia wengine
mlikuwa nao pale chuo kikuu cha Mlimani. Akanihakikishia kabisa huna mpango na
mimi. Na kuweka msisitizo juu ya hilo ndipo akanieleza mahusiano yenu. Kuwa
nyinyi mpo karibu sana kuliko watu wengine. Na huwa mnazungumza mambo mengi.”
Nanaa akaendelea.
“Ukweli
alikuwa muwazi kwangu vya kutosha. Aliniambia pia alikuwa na mwanamke ambaye
anataka kumuoa. Lakini baada ya kuniona, akavutiwa na mimi. Alisema nyinyi wote
mnanifahamu kutokana na stori alizokuwa akisimulia kaka James. Wewe ulikuwa
mstari wa mbele kuniulizia. Kwa hiyo aliponiona na kuvutiwa, akakumbuka swala
la kwako la kunifuatilia kwa karibu. Ndipo akakuuliza vipi juu yangu?
Akakuuliza, ‘kuniuulizia kule kulikuwa na
maana nyingine yeyote, au ni undugu tu?’
Nikasikia akikuuliza tena, ‘ile hisia uliyosema
unajisikia juu yangu na kukufanya kuniulizia wakati ule hata kabla hujaniona,
imebadili chochote baada ya kunioana?’.
Unakumbuka alikuuliza tena, ‘itakuaje juu
ya Liz baada ya mimi kutokea?’ Nafikiri
unakumbuka majibu yako yote kwa kuwa huwa husahau Geb.” Nanaa aliona vile Geb
alivyotulia. Akajua wazi amekumbuka kila kitu.
“Nisikilize
Nanaa. Mimi nilimjibu vile Malii kwa kuwa nilijua vile Malii alivyokuwa karibu
na watu wengine. Nikajua jibu lolote nitakalompa ni kama nitakuwa nimetangazia
uma. Ni kweli Malii nipo naye karibu kuliko wengine wote kama alivyokwambia,
lakini huwa simwambii kila kitu. Na Malii najua yupo karibu yangu kwa sababu zake.
Nazifahamu. Ndio maana haishiwi maswali kwangu kuliko marafiki zangu wengine
wote. Kama umeshatuangalia, ni kama wengine wananiogopa kidogo. Ni sababu ya
kuwa sana mkimya. Huwa nipo sana makini na kila neno linalotoka kinywani
mwangu. Na wote wale najua tupo karibu, lakini wanamaswali mengi sana juu
yangu. Mengine wanashindwa kuniuliza moja kwa moja. Niligundua huwa wanamtuma
Malii kupata majibu fulani fulani kutoka kwangu kwa kuwa Malii amewahakikishia
kuwa huwa nipo muwazi sana kwake.” Geb akaendelea.
“Lakini huwa hajui. Huwa namjibu kutokana na
kile ninachojua anapenda kusikia au ni sawa hata akiwarudishia majibu wenzie.
Malii alishahangaika sana kuiba biashara zangu. Alishakuwa karibu sana na mimi
ili kujua nini nafanya, ili afanye kama mimi ili anizidi. Kwa kuwa nilishamjua
anahila ndani yake, kila alilojaribu kuuliza, nilimjibu kwa kiwango kidogo
sana. Akidhani amefanikiwa, akaanza kuagiza malori nje ya nchi ili afanye
biashara kama ninayofanya mimi na mbaya zaidi, kwa kutumia wateja wangu wale wale.
Sikumuonyesha najua wala sikumuuliza japo nilijua kuwa ameingiza nchini hayo
malori mawili kwa siri na kuanza kupigia simu wateja wangu. Alisajili kampuni
kama yangu na kutafuta jengo kubwa.” Nanaa alitulia kumsikiliza.
“Vyote
hivyo anafanya kushindana na mimi. Asijue mwenzie nilianzia wapi. Yeye akaanza
kwa kishindo, tena kwa pesa ya wizi. Kampuni aliyokuwa akiwafanyia kazi ilikuwa
ikihusika na mambo ya mtandao hapa nchini. Walikuwa wakimlipa vizuri sana. Kuja
kushituka, Malii alikuwa akiwauzia huduma makampuni mengine, kwa kutumia vifaa
vya hapo hapo kwenye hiyo kampuni, lakini aliwauzia kwa jina la kampuni yake
kwa siri. Wamiliki wa ile kampuni walipokuja kumgundua, walimshitaki.
Hawakutaka kesi kubwa ili wasiharibu jina la kampuni yao, lakini Malii akafilisiwa
kila kitu mpaka yale malori na nyumba aliyokuwa amejenga.” Nanaa alibaki ametoa
macho.
“Pale
alipo Malii ni kama ameanza upya maisha. Kazi aliyonayo sasa hivi, nilimsaidia
kumuunganisha na jamaa mmoja, ndipo wakampa kazi kwenye kampuni yao bila maswali
mengi kwenye usaili kwa ajili yangu. Kwa kuwa pia ni mtendaji kazi mzuri,
hakuna aliyejuta. Pale alipo hafahamu kama nafahamu alichokuwa akitaka
kunifanyia. Niliamua kumuacha tu kwa kuwa nilishajua ni mtu wa namna gani.” Geb
akaendelea.
“Naomba
ujiulize Nanaa. Hata kama mimi nilimjibu kuwa wewe ni kama wasichana wengine
tu kwenye maisha yangu, kama ni mtu mzuri kwetu, mimi au wewe, akijidai mimi ni
rafiki yake, kwa nini anirikodi? Na kwa nini akusikilizishe mazungumzo yetu?
Alishindwa nini kujitengenezea njia ya kukupata mpaka anichafue mimi?” Kimya.
“Eti
Nanaa?” Geb alimuuliza. “Mimi sijui Geb. Lakini nakwambia kile nilichomwambia
na yeye. Sijali unanifikiria nini, na sijali upo na nani. Sijui kwa nini hisia
zangu zimekuwa kubwa kwako. Na nilimwambia pia sijui kwa nini iwe kwako.
Akasema labda pesa. Nikamuhakikishia sio swala la pesa, kwa kuwa nilikupenda
kabla hata sijajua kama wewe una pesa. Nilimwambia ninachojua nakupenda kwa
dhati. Sijawahi kupata hisia za namna hiyo kwa mwanamme mwingine yeyote ila
wewe Geb. Ila nilimwakikishia kuwa, endapo itatokea ukanipa hiyo nafasi,
nitaitumia ipasavyo. Si kwa ajili yako tu, ila kwa ajili yangu mwenyewe.
Nilimwambia nimekusudia kuupa moyo wangu kile kinachopenda. Nikamwambia
nitakusubiri. Akitokea mwingine atakayeweza kuamsha hizo hisia kama zilivyoamka
kwako, na akanifungulia mlango, nikamwambia sita, sita. Awe tajiri, awe fukara
nitajitupia kwake.” Nanaa akaendelea.
“Aliponiambia
niyape muda mahusiano yetu, nikamwambia nina uhakika sio yeye. Kwa kuwa wewe
sikuwa nimekupa hata nafasi. Lakini nilipokuona tu, nikavutiwa mno. Nilimwambia
mara ya kwanza nilishindwa hata kulala vizuri, nikitamani nije kukuona tena
wakati mwingine. Haikuwa ni kwa muonekano tu. Nilimwambia nishatongozwa na
wanaume wazuri sana kimuonekano. Waliobeba baadhi ya vigezo nilivyodhani
navihitaji kwa mume wangu. Lakini nilipokutana na wewe, ilikuwa tofauti. Kwa
mara ya kwanza, nilisikia kitu cha tofauti moyoni mwangu. Sina jinsi
nikamueleza mtu, akanielewa. Lakini nikamwambia nilipojua uwezo wako na yupo
Liz kwenye maisha yako, niliamua kukaa mbali kabisa na wewe, lakini bado hisia
zangu ziligoma kubadilika. Nilijikuta unajengeka utayari wa kusubiri kitu
ambacho sio kawaida yangu. Nikamwambia kwa kunishika siku ile na kunibusu,
nimehakikisha yeye siye na wala hatakuwa ndiye. Tukaachana kwa makubaliano
yaishie pale na wala tusitafutane tena. Akasema atamuoa mwanamke wake. Nikamtakia
kila la kheri. Tukaachana.” Nanaa akamaliza. Geb akatulia kidogo.
“Kwa
hiyo sijui umenielewa Geb? Mimi sikujua mahusiano yenu mpaka siku hiyo
alipojifungua kwangu. Sikumwambia mama kwa kuwa aliniambia wanamahuasiano ya
karibu sana na mama G. Akaniomba nisiwaambie, yasije kuharibika mahusiano yenu.
Nilipomuuliza kama ningemkubali, je angeendelea kuwaficha? Akanijibu kwa wazi
kabisa. Akaniambia wewe uko karibu sana na mama yako. Na upo makini sana kwenye
maisha. Huwa huropoki. Kwa kumjibu vile yeye, inamaana hata mama G anajua hilo.
Sio siri kuwa mimi unaniona kama mtu tu wakawaida tu. Na unanisaidia pale kama
mdogo wake James.” “Sasa kwa nini akukataze tena kusema?” Geb akauliza.
“Kwa
vile nilivyokuwa nimemwambia nitakungoja tu mpaka nitakapopata mtu mwingine au
mpaka wewe utakaponipa nafasi. Na nilimuhakikishia Geb. Na ndivyo nilivyofanya.
Nilimwambia ikitokea unanipa nafasi maishani mwako, nitahakikisha nitaitumia
ipasavyo kwa kuwa nitakuwa nimepata uhakika kutoka kwa Mungu. Nitakupenda kwa
dhati kwa kuwa ninajua wewe ni wangu, ambaye Mungu amenipa. Nilimwambia Malii,
hakuna sababu ya wewe kuja kunipenda mtu kama mimi. Kwa kuwa umezungukwa na
kila kitu unachokihitaji. Wanawake wazuri wanakugombania. Wengine mama alikuwa
akinionyesha mpaka picha zao huko Facebook na Instagram. Nikamwambia, ukija
kwangu nitajua wewe ni wangu kwa hakika. Malii alinitazama kama hivyo
unavyonitazama wewe. Lakini alisema kama ningemkubali yeye, angenitambulisha
kwenu bila shida, kwa kuwa ulishakataa mahusiano yetu kimapenzi.
Ulimwambia baada ya kuniona, ukagundua ilikuwa ni huruma tu iliyokuwa
ikikupelekea kuniulizia tokea zamani, ndio maana uliamua kuendelea kumsaidia
kaka James, kwa kuishi na mimi.” Geb akatulia kidogo.
“Naomba
nikuulize swali Nanaa. Na naomba uwe muwazi.” “Nini?” Nanaa akauliza.
“Umeshawahi kutilia mashaka mapenzi yangu kwako hata mara moja?” “Ninachojua
kwa hakika, nakupenda Geb. Hilo sijawahi kulitilia shaka hata mara moja.” “Kwa
hiyo mimi umenitilia mashaka.” “Siwezi kusemea moyo wako Geb! Mdomo unaongea
mengi. Inawezekana na mimi unanipa majibu ya yale unayojua ningependa kuyasikia
kutoka kwako kama unavyofanya kwa Malii!” “Nanaa!!” Geb akashangaa sana.
“Kweli
Geb. Mimi nawezaje kuusemea moyo wako?” “Basi naomba uyasemee matendo yangu
kwako.” “Kwa matendo hapo naweza kukusemea.” “Nakusikiliza.” Nanaa akacheka.
“Mbona unawasiwasi?” “Nataka kujua unafikiri nini juu yangu, Nanaa. Mengi
yamesemwa. Si Malii tu, hata Zinda. Aliongea mambo mengi akithibitisha kuwa
sikupendi kwa kuwa nilikuwa na Liz wakati nikiwa naishi na wewe.” “Mimi hayo
siyajali. Na hata mama nilimwambia. Ilimradi nilikupata, inatosha. Mimi
nilikuwa na maisha yangu ya mahusiano kabla yako. Sema mahusiano yangu yaliisha
kabla ya kukutana na wewe. Na wewe mahusiano yako yaliisha baada ya kukutana na
mimi. Mimi naona ni yale yale tu.” Nanaa akaendelea.
“Na
huwa nakutetea hata kwa watu. Hata Grace alishaniuliza hilo swali. Mimi sio
mwanamke wa kwanza kwenye maisha yako. Usingeweza kukurupuka kwangu mara baada
ya kuniona na kuacha wanawake zako wote.” “Ni Liz tu, Nanaa.” Nanaa akacheka.
“Huyo huyo Liz. Eti ukamuacha bila hata kunifahamu mimi ni nani! Nina tabia
gani! Kama kweli nakupenda wewe kwa dhati au nipo kama wanawake wengine wanaopenda
hayo macho yako na pesa.” Geb akacheka.
“Si
ni kweli?” Nanaa akauliza. “Nakupenda Nanaa. Niamini nikikwambia nakupenda na
nilikusudia wewe ndio uwe mke wangu. Hamna sababu yeyote inayonifanya niwe hapa
sasa hivi na wewe. Au uwe na watoto wangu kama mimi sikuamua Nanaa. Nilikwambia
na ninarudia, mimi sikurupuki. Hasa kwenye mambo yanayohusu maisha yangu.
Watoto unaozaa na mimi sio bahati mbaya. Nimekusudia. Nimekuchagua wewe uwe
kwenye maisha yangu yote hapa duniani. Lasivyo ungenikuta nilishaoa au
nilishakuwa na watoto tokea zamani maana wewe sio mwanamke wa kwanza kuwa na
mahusiano ya kimapenzi na mimi. Niliamua watoto wangu wote watokane na wewe.”
Geb akasisitiza.
“Malii
aliniambia majuzi tulipokutana na mkewe tukizungumzia swala la kuwa ukurasa
mmoja kwenye harusi, wao kama wasimamizi wetu wa harusi. Unakumbuka pale
hotelini mkewe alikwenda chooni na wewe ukatoka kwenda kuzungumza na simu? Mlituacha
mimi na Malii pale mezani. Unakumbuka?” Geb alibaki akimtizama Nanaa, akitaka
aendelee ili ajue ni nini tena kilitokea. “Geb?” “Nakumbuka Nanaa.” “Basi
aliniambia unanioa kwa sababu ya rangi yangu tu. Au rangi ya ukoo wetu, wala si mapenzi.” Nanaa akaongeza na kumuudhi
sana Geb.
“Yeye
ndio alikuwa akipenda wanawake weupe tokea zamani. Hata alipotutambulisha huyo
mkewe, kabla ya kumuoa, tena nakumbuka hata Danny aliongea hili. Akamwambia
ugonjwa wake tokea tupo shule ni wasichana waupe. Malii hajawahi kuwa na
msichana mweusi hata mara moja. Tena alikuwa anasema wasichana weusi wote
anawaona kama dada zake wakuzaliwa tumbo moja. Hawezi hata kuwatongoza. Liz
alishawahi kumpiga na kiatu sababu ya kusema hivyo siku moja tukiwa pamoja.”
“Danny alimwambia nini?” Nanaa akauliza.
“Danny
alimtahadharisha na kumwambia ndoa ni kifungo cha maisha. Yeye hajawahi kuwa na
mwanamke mweusi hata mara moja. Tena akiwa amekusudia sio kwa bahati mbaya
kuwakosa wanawake weusi. Ni alikuwa hawatongozi kabisa. Akimuona msichana
mweusi anayempenda yeye, au yupo karibu naye, alikuwa akiwafanya marafiki tu.
Alikuwa akisema anaogopa kuwatongoza kabisa. Sasa Danny akamuuliza iweje leo
aoe mwanamke mweusi? Akasema yule dada ni watofauti. Amembadili mtazamo kabisa.
Anasifa zote za kuwa mkewe. Danny akamuuliza je yeye anasifa za kuwa mumewe?
Akasema amebadilika, sasa hivi ametulia. Atakuwa mume mzuri. Kumbe huku nyuma
anakutongoza wewe! Mimi sikuwahi kuchagua mwanamke kwa rangi hata siku moja.
Mbona Liz alikuwa mweusi? Kwanza naweza kusema mama ndio alivutiwa na rangi
yako kuliko hata mimi mwenyewe.” Nanaa akacheka sana.
“Namsikia
anavyosema nimeleta damu nyeupe kwenye ukoo.” “Basi ujue ni mama na Grace ndio
wanakusifia rangi yako kuliko hata mimi mwenyewe.” “Kwa hiyo wewe hupendi rangi
yangu!?” Nanaa akauliza kwa kulalamika kidogo. “Nanaa!” “Wewe sema tu.”
“Nilishakwambia nilikupenda hata kabla sijakuona. Nakupenda Nanaa. Nakupenda
sana mpenzi wangu. Na nilizidi kukupenda baada ya kukuona. Sasa sijui kama na
rangi ilichangia, lakini jua nakupenda.” Nanaa akacheka kuonyesha kuridhika.
“Kwani
kaka hakuwahi kuwaonyesha picha zangu?” Nanaa akauliza huku akijirudisha kulala
vizuri. “Kwani wewe ulishamuona kaka yako akipiga picha?” Nanaa alicheka sana.
“Kweli bwana! Kaka hapendi picha. Utambembeleza week nzima kumpiga picha ndio
anakubali.” “Basi umepata jibu. Ila nakumbuka kumdadisi kidogo tu baada ya
kuona hisia zinanisumbua, nikamuuliza kama mnafanana naye. Akasema labda rangi
tu. Lakini akasema hata sura hufanani na mama yako kabisa.” Nanaa akafikiria.
~~~~~~~~~~~~~~
“Eti
Geb. Unafikiria ni sawa nije kumtafuta baba yangu?” “Sio vibaya. Lakini kwa
jinsi alivyonisimulia James, hata na wewe pia, mlisema alikana mimba na wewe
mwenyewe wakati ni mtoto mdogo kabisa. Sasa hutaumia ukimtafuta halafu akukatae
tena?” Nanaa akafikiria tena. “Lakini safari hii sitamtafuta kwa mahusiano.
Nikutaka tu kumuona. Nimfahamu. Sihitaji kitu kutoka kwake. Angalau nijue
nafanana na nani, kabila langu na mambo ya kawaida tu. Wala sitamuomba
mahusiano.” “Sawa. Tutazungumza na James.”
“Asante Geb.” Nanaa akashukuru.
“Lakini
Nanaa, nimeamua Malii na mkewe hawatatusimamia tena harusi.” Nanaa
akabaki kimya akimtizama. “Malii bado anaonekana anakutaka na hatatulia mpaka akupate.”
“We Geb! Yaani unamaanisha nitamkubali!?” Nanaa akashituka sana. “Ujue mimi sio
muhuni? Hata kama hukunikuta bikra, ila ujue najiheshimu sana. Acha..” “Hapana
Nanaa! Subiri kwanza. Acha kupaniki. Sijamaanisha hivyo.” Geb akamkatisha maana
Nanaa alishabadilika.
“Unamaanisha
nini sasa?” “Namaanisha ataendelea
kutusumbua sana. Hasa wewe. Hatakata tamaa. Mimi namfahamu Malii kwa wanawake.
Na zaidi wawe wangu na ni mweupe! Itatusumbua tu.” Kimya. “Sasa mbona husemi
tena kitu!?” “Unataka kunisikia nikisema nini Geb? Mimi sijali nani
anatusimamia harusi. Ilimradi wewe uwepo siku hiyo, basi.” Geb akacheka kidogo.
“Kwa
hiyo bado unataka nikuoe?” Nanaa akamwangalia na kucheka kwa kuguna kidogo.
“Wewe ni mkorofi sana Geb.” Geb akacheka. “Mimi ndio mumeo bwana. Ni hasira
tu.” “Unakasirikaga bila hata sababu!” “Nilijua utasema unaomba nibadilike.”
“Aiii! Mama yako alinisimulia habari za baba yako. Anasema alikuwa hivyo
hivyo.” Geb alicheka sana. “Mama bwana! Anapenda kuniharibia!” “Ndio ukweli
wenyewe. Wakati mwingine unakasirika mpaka nakuhurumia. Na mara zote mimi ndio
sababu!”
“Basi
usiwe unaniudhi.” “Nitafanyaje Geb jamani? Hutaki nitoke na kaka yangu. Hutaki
niwe kwenye mitandao. Hutaki niwe na marafiki. Nikichelewa kurudi nyumbani,
nikikukuta wewe ni shida. Hata kama nitarudishwa na kaka au Grace dada yako pia
ni shida!” “Nakuwa naacha mambo yangu ili nirudi nyumbani tuwe wote, halafu na
wewe sikukuti! Hata wewe usingefurahia Nanaa.” Nanaa akabaki akimwangalia.
“Wewe
niangalie hivyo hivyo. Lakini nataka niwe nakukuta nyumbani.” “Ndio ukampiga
marufuku na mama kutembea na mimi jioni?” “Mimi nilimwambia kwa vizuri tu.
Shuguli zake za jioni za kina mama, wewe hazikuhusu. Asiwe anakuchukua, akuache
nyumbani na mtoto.” Nanaa alicheka na kutingisha kichwa. “Unashida wewe! Mpaka
kwa mama yako mzazi!” “Wewe ukianza heka heka za mama G, mambo ya nyumbani
yatakushinda. Wewe mwache azunguke mwenyewe. Nimemwambia akitaka mtoke, iwe
asubuhi, ili jioni uwepo nyumbani.” Nanaa akapumua kwa nguvu. “Mbona hujibu?”
“Hilo mbona kila mtu alishalielewa. Hata nikiwa na Grace mahali inabidi
anirudishe haraka nyumbani kabla ya saa 11 na nusu jioni. Kila mtu ananikwepa
kwa masharti yako, Geb!” Geb akacheka.
“Unafikiri
nivizuri? Unakuwa mkali kwa kila mtu! Utafikiri wanaenda kuniuza kwa wanaume
wengine wakati ni ndugu zako!” “Mama na Grace wanashuguli nyingi sana wale.
Hutaweza. Kila weekend wanashuguli! Mara Kitchen party,
sijui wagonjwa hospitalini. Mambo kibao. Hapana. Nimewaambia mara moja moja
tena iwe muhimu.” “Sawa baba.” Nanaa akaitika na kulala vizuri.
“Lakini Geb, Nataka
kukuhakikishia swala la Malii. Tafadhali usiwe na wasiwasi juu yangu. Japo
anaonekana anania na mimi, lakini naomba uniamini. Hakuna kilichotokea na
sita…” “Kipo kilichotokea Nanaa. Naomba tusikatae ukweli. Malii alikuchukua
ukiwa na mimi. Mkatafuta sehemu ya siri ya kwenda kufanya naye mapenzi.
Mkaishia kukiss. Hilo sitalisahau na wala sitalipuuza. Malii amembusu na
kumkumbatia mke wangu. Ndilo nitakalobakia nalo. Awe alitumia kigezo kuwa
sikutaki kimapenzi au la. Lakini ujue wazi, alifanya kusudi akijua ukweli na
ndio maana alirikodi mazungumzo yetu na kukukataza usiseme.” Geb akasimama.
Akamfunika
Nanaa shuka vizuri. “Na kuthibitisha hilo, ndio maana anahangaika na wewe mpaka
leo. Malii ni mpinzani wangu wa wakati wote. Wala hataishia kwako.” “Kwa hiyo
unanilaumu?” Geb akanyamaza. Nanaa akapata jibu lake. “Naomba unisamehe Geb!”
Geb akamtizama. “Nisamehe. Na ninakuahidi hakuna kitu kingine nitakachofanya
kwa siri tena. Nakuhakikishia Geb. Mimi sina tabia yakutoka nje ya mahusian..”
“Nanaa! Naomba uishie kwenye msamaha tu. Basi.” “Lakini..” Nanaa akaona
anyamaze tu, akubali yaishe.
“Basi
Geb. Nimekubali kosa. Nilienda kwa Malii, huku nikijua kile kinachoendelea kati
yetu, japo hatukuwa tumezungumza. Lakini nilijua hisia zako kwangu. Naomba
nisamehe, na ninakuahidi na kwa msaada wa Mungu, sitarudia tena.” Akamuona
kidogo ametulia. Geb huwa hakubali kushindwa na chochote maishani. “Nisamehe
Geb. Nilikosa.” “Basi, yamekwisha.” Geb akajibu. “Yameishaje?” Akanyamaza.
“Mbona huniambii kama umenisamehe?” Nanaa akalalamika. “Sasa mbona
unalazimishia majibu unayotaka wewe, Nanaa? Wewe umeomba msamaha. Nimekusikia
na kukwambia yameisha. Naomba tuache yaishe hivyo.” Nanaa akaona anyamaze tu.
Alimfahamu Geb. Akajiingiza ndani ya shuka vizuri, akalala bila hata kupewa
busu.
Ukweli Huwa Ni Mchungu.
Baada
yakujua ukweli, kweli mambo yalibadilika. Mabusu yalikoma kati yao. Kitu
kilichomshangaza sana Nanaa. Alimuona akimuhudumia vizuri. Kumletea vitu
vizuri, lakini sio kumbusu. Hakuonyesha hasira wala kuzungumzia chochote. Kabla
ya kwenda kazini asubuhi, aliamka na kumsaidia kumsafisha pale pale kitandani.
Alihakikisha amekula vizuri ndipo alipomuacha na kwenda kazini. Wakati wa
mchana alirudi na Oliva ili apate muda na mama yake.
Nanaa
alikuwa akicheza na mwanae pale pale kitandani akimsikiliza maneno mapya
aliyoweza kuzungumza wakati Geb akiendelea na shuguli zake. Kama ni kupiga simu
au kurudi kwenye ipad au laptop yake na kufanya kazi baadhi humo mpaka jioni
anapomrudisha Oliva nyumbani.
Usiku alikuwa akirudi akiwa ameshaoga na vyakula
ambavyo anajua Nanaa anapenda. Na baadhi ya DVD ambazo anajua Nanaa angefurahia
usiku huo na kesho yake anapomuacha kwenda kazini. Wataangalia hizo movie
usiku. Atamfunika tu, nakujirudisha kitini kuendelea na shuguli zake mpaka
analala. ~~~~~~~~~~~~~~
Juma
moja lilishapita tangia Geb abadilike. Hofu ikaanza kumuingia Nanaa. Ile midomo
aliyokuwa na hamu ya kuinyonya akigugumia kama anakula pipi, aliikwepa kama sio
yeye. Hakuendelea kuzungumzia habari za harusi wala hakuwa amemuona mtu yeyote
kutoka nyumbani kwa kina Geb. Ila kaka yake alishapita hapo mara kadhaa. Akiwa
anaelekea kazini na jioni alimpitishia vitu vidogo vidogo vyakula.
Kwa
kuwa Geb alisema yameisha. Na Nanaa alimjua Geb, akisema jambo amesema.
Hakutaka kurudia yale mazungumzo na kumuhoji kama bado anahasira. Alishindwa kudai
mabusu, kwani Geb alionyesha wazi hahitaji busu lolote. Alizungumzia mambo ya
kawaida kabisa, zaidi watoto wake hao wawili Nanaa anaomzalia. Alimuonyesha
Nanaa video alizokuwa akimchukua Oliva akifanya mambo mapya kila siku na
kumuonyesha kumfurahia binti yake. Alimwaga sifa za Oliva pasipo kuchoka.
Hapakuwa na mazungumzo ya mapenzi kati yao. Ilikuwa ni kula na kuangalia movie
basi.
~~~~~~~~~~~~~~
Wasiwasi ukazidi kumtesa Nanaa. “Kuna kuolewa kweli hapa!” Nanaa
akawaza nafsini mwake. “Au ndio
nitaishia kuzalishwa tu?” Ndio swali lililozidi kumuumiza Nanaa. “Au
anaona kinyaa baada ya kumwambia Malii alinibusu? Maana tangia nimwambie hivyo,
hajanibusu wala kunikumbatia tena!” Machozi yakazidi kumtoka Nanaa
kila anapokuwa peke yake, asijue wakumuuliza. Mwanzoni yeye ndio alionyesha
hayupo tayari, Geb akabembeleza. Safari hii uliwekwa ukimya wa namna yake.
Zilikuwa habari za watoto tu. Mama G wakumuuliza hakuwepo asubuhi wala mchana.
~~~~~~~~~~~~~~
Uzalendo
ukamshinda, mwishoe akaona aulize tu. “Mbona mama na Grace hawaji kuniona?”
Nanaa akauliza usiku huo wakati Geb alipoingia. Alisubiri mpaka akachoka.
Ilikuwa siku ya ijumaa. Hakuletewa mtoto. Geb alimuaga asubuhi na kumwambia
siku hiyo atakuwa busy sana. Ila atarudi usiku. Arudi mchana. Akamletea ice cream,
akionyesha anaharaka. Hata hakukaa sana, akatoka wakati Nanaa anakula.
Alirudi
usiku huo akionyesha amechoka sana. Alionekana alitokea nyumbani, kwani
alinukia vizuri. Kuonyesha alishaoga na yupo tayari kulala. Nanaa alibaki
akimtizama. “Kwanza umeshindaje?” “Vizuri. Nimelala siku nzima.” “Afadhali.
Magesa ameshalala?” Geb akauliza huku akisogelea tumbo la Nanaa. “Alikuwa akicheza
hapa muda sio mrefu. Naona na yeye amemsubiri dad mpaka amechoka.” “Nilikuwa na
siku ndefu sana leo.” Geb akambusu tumboni na kupapasa taratibu tumbo la Nanaa.
“Nina
hamu na mama!” Nanaa akarudia. “Niliwaambia wakuache upumzike, kama ulivyokuwa
umeomba.” Geb alijibu na kujirudisha kwenye kiti. “Ilikuwa ni kwa kipindi kile
tu!” Nanaa akajitetea kidogo. “Basi kama unataka waje, nitawaambia ili kesho
waje kukuona.” Nanaa akanyamaza kwa muda.
“Wamefanya
ultrasound leo.” “Daah! Nimepitwa. Magesa anaendeleaje?” Geb akauliza. “Daktari
anasema anaendelea vizuri. Namshukuru Mungu nimebakiza siku 12 tu. Nimeshachoka
kukaa hapa.” “Naelewa. Kukaa sehemu moja inachosha. Pole.” Geb akajibu hivyo
tu. Akatulia kidogo. “Kwa hiyo maji hayatoki tena?” Akauliza tena Geb.
“Nilisahau kuuliza. Lakini ni kama alisema yapo maji yakutosha kumuweka mtoto
kwa hizo siku 12.” “Afadhali. Basi tuombe halafu tulale. Nimekuwa na siku ndefu
sana. Nipo hoi.” “Pole.” Nanaa akaongea kwa kunyongea. Akionyesha kukosa raha
kabisa.
Wakaomba
kwa pamoja. Geb akamshukuru Mungu kwa ripoti nzuri aliyopewa na daktari.
Akamuombea mtoto wake huyo Magesa. Kisha akamuombea na Nanaa huku akiwa
amemshika mkono, yeye amepiga magoti pembeni ya kitanda. Akamuombea na
kumbariki Nanaa. Ndipo akamuombea na Oliva huku akimwaga sifa za huyo mtoto
mbele za Mungu kana kwamba Mungu hamfahamu huyo mtoto. Akamsifia na kumuombea.
Akamaliza.
“Asante
kwa maombi mazuri.” Nanaa alishukuru wakati Geb akisimama. “Na mimi nakushukuru
kwa kulipa garama ya kuwa hapa kama kifungoni kwa ajili ya mtoto wangu.
Unajua ndio mbeba jina la Magesa?” Nanaa akacheka kidogo. “Huwa namfikiria baba
yangu. Nasema angekuwa hai, angekuthamini sana. Aliniambia alisharidhika na
watoto wake wakike. Hakutegemea kama Mungu angemzawadia mtoto wa kiume wa
kuendeleza jina lake. Alijua angekufa, halafu jina lake lingepotea tu. Hapo
ndipo nilipojua ni kwa nini alikuwa akizungumza sana na mimi.” Geb akarudi
kukaa.
“Alikuwa
akinifundisha mambo mengi sana mpaka nilikuwa nashangaa. Ni kama alitaka aache
picha yake halisi hapa duniani. Japokuwa tulikuwa watoto wa nje ya ndoa, lakini
alijitahidi sana kuwekeza kwangu. Nilikuwa mdogo kuliko wote, lakini alikuwa
akinihusia mambo mengi kana kwamba sitamuona tena kesho yake. Hakuwahi kuniona
mimi ni mtoto. Grace ndio alikuwa kiziwanda wake, mpaka mama alikuwa
akinihurumia. Siku ambazo nilikuwa siendi shule, alikuwa anakuja kunifuata pale
kwa mama. Alfajiri sana. Tunaenda kwenye kazi zake. Halafu alikuwa mtu wa kazi
za mikono sana. Basi nitakuwa naye huko mpaka jioni, ndipo ananirudisha kwa
mama.” “Kumbe ndio maana unafanya sana kazi!?” Geb akacheka.
“Sijui
maisha ya kubahatisha. Yule Mzee aliniambia bahati zangu zote, zitakutana
na juhudi zangu. Akaniambia nimfundishe na Magesa hivyo hivyo.” Nanaa akashangaa
sana. “Haiwezekani Geb! Yaani baba yako alikwambia jina la mtoto wako wa kwanza
wa kiume!?” “Kabisa Nanaa. Ndio maana nilikuwa makini sana katika swala la
kuzaa. Sikutaka kuzaa hovyo. Baba aliniambia mtoto wangu wa kiume wa kwanza,
nimpe jina la Magesa. Hao wengine nipo huru kuwaita majina nitakayo. Akamuombea
kabisa. Na akaniambia nimfundishe katika misingi ya kimungu. Aliniambia siri ya
mafanikio yote ni kwenye kanuni za kibibilia. Alikuwa akifanya kazi huku
akitumia maandiko ya kimungu. Yule Mzee alikuwa akifanya kazi Nanaa! Hujawahi
ona. Na alikuwa na bahati sana. Hakuna alichofanya asifanikiwe.” “Unahisi ndipo
uliporithi?” Nanaa akauliza na kumfanya Geb acheke kidogo.
“Sijui!
Labda.” Geb alijibu huku akicheka. “Sema ukweli.” “Kwa kweli siwezi kulalamika
au kukufuru. Naona mkono wa Mungu katika kila eneo la maisha yangu. Wakati
mwingine najiambia labda kwa kuwa nafanya kama baba alivyonifundisha! Sijui!”
“Ndio unafanyaje?” Geb akacheka tena. “Leo una maswali!” “Nataka kujua.” Nana
akasisitiza.
“Sio
vitu vigeni. Ni zile zile kanuni ndogo ndogo tu za maisha zinazojulikana na
kila mtu. Lakini huwa ni rahisi kuzipuuza. Sasa hizo baba alinifundisha na
kunisisitiza nisijaribu kuzipuuza hata mara moja.” “Zipi?” Nanaa alizidi
kuuliza. “Moja wapo aliniambia hakuna pesa ndogo. Milioni moja haikamiliki bila
shilingi moja. Akasema kama ninajiwekea malengo ya kuwa kila mwaka niwe na
kiasi fulani cha pesa. Tuseme, milioni 50. Aliniambia kila mwanzo wangu wa
mwaka nitakaochagua mimi. Sio lazima ikawa mwezi wa kwanza. Hata kama nikisema
nafunga mwaka kila mwezi wa sita. Lakini lazima niweke malengo ya kiasi cha
pesa ninachotaka nifunge nacho mwaka.” Geb akaendelea.
“Akasema.
Kama nitataka kufunga mwaka na milioni 50, lazima ndani ya huo mwaka niheshimu
kila senti na kuitafuta kwa bidii. Hata kama itakuwa ni biashara ya kuuza
karanga stendi ya daladala, nihakikishe ninauza kwa bidii, ili nipate hiyo
shilingi moja ya kukamilisha malengo ya milioni 50. Akaniambia nisiwahi
kuridhika kuvuka mwaka kama sijatimiza malengo. Hata kwa kupungukiwa na hata shilingi
moja. Akasema huko ni kushindwa, ambako kutakaribisha kushindwa kwenye mambo
mengi zaidi.” Nanaa alibaki ametoa macho. Ndipo akajua siri ya Geb.
“Kumbee!”
Geb akacheka baada ya Nanaa kuhamaki. “Lala Nanaa. Acha kupenda stori.” “Ndio
maana watu wanakuita mfanikiwa! Kumbe unasiri hivyo! Kesho niambie
nyingine.” “Nyingine ya mwisho, aliniambia, nisilale hata dakika moja, kama
sijatimiza malengo ya siku hiyo. Lazima kila siku iwe nimejipangia malengo
yangu ambayo nihakikishe ninayatimiza. Nisilale mchana au usiku, kama
zijatimiza malengo ya siku hiyo. Lasivyo nikukaribisha kushindwa. Inamaana
malengo ya siku hiyo, yatakutana na malengo ya kesho. Yataenda kujilundika
mpaka yatafika ya mwaka mzima. Ndipo kupuuza kutakapoingilia kati maana itabidi
kuyaacha ya jana ili nifanye ya leo. Halafu nitashindwa kuweka malengo mapya
sababu ya kupambana kukamilisha malengo yazamani. Wakati kila siku Mungu
anayotupa, baba aliniambia inakuwa ni mpya. Kila siku Mungu anaweka baraka
mpya. Siwezi kutembea na malengo ya jana kwa kutumia baraka za leo. Nitashindwa
vibaya sana.” “Magesa unasikia mwanangu?” Nanaa akajishika tumbo. Geb alicheka
sana.
“Yaani
sasa hivi ndio naelewa kila kitu! Ujue una mambo yako Geb wewe! Mpaka Grace
anakuita mkoloni. Unakanuni ambazo utafikiri Mzee! Ukiamua jambo umeamua.”
“Kwa kuwa sikurupuki Nanaa. Na hilo baba alinitahadharisha. Kutokuyumbishwa na
matukio.” Nanaa alimwangalia Geb hakummaliza. “Kwa hiyo na huyu Magesa atakuwa
kama wewe?” “Zaidi ya mimi. Ataijua bibilia zaidi yangu. Kama babu yake
alivyoniambia. Atatembea katika neno mchana na usiku.
Namuombea uzima na roho ya utii.
Mambo mengi nimemwandikia. Akikua na kuweza kusoma, atakutana na wosia wa babu
yake. Nimemuandikia mambo mengi sana. Yale aliyoshindwa babu yake, alisema
nimwambie ili na yeye asije pita huko.” “Geb wewe!” “Kweli tena. Mimi ni mjumbe
tu. Napitisha ujumbe kwa vizazi vya Mzee Magesa.” Geb alijibu huku akicheka.
“Umenifanya
nijisikie wa muhimu! Kumbe nimebeba kitu cha maana hivyo!” Nanaa aliendelea
kujipapasa tumboni. Geb akacheka. “Ndio maana ulivyonifukuza siku ile
nilishindwa hata kulala. Lazima huyo azaliwe mimi nikiwepo. Mbeba ukoo huyo!”
“Sasa mama yako anajua?” Nanaa akadadisi. “Kwa sehemu. Yale baba aliyokuwa
akimuhusia juu yangu. Hasa shule. Alimwambia ahakikishe nasoma kwa garama
yeyote ile. Halafu ahakikishe nakua kanisani. Alimwambia nimebeba ujumbe wa
muhimu sana. Lazima ahakikishe sipotei.” Geb akacheka kama anayefikiria.
“Unafikiri
mama alikuwa anafurahia maisha ninayoishi na wanawake pale ndani? Hasa Liz? Hata
kidogo. Mama anampenda Yesu, Nanaa. Anajua ninaishi maisha ambayo hayampendezi
Mungu. Lakini anasema ni afadhali nimlete msichana pale ndani ili awe anamfahamu,
kuliko niishie nao nje. Alikuwa akitaka kumjua kila mwanamke ninayekuwa kwenye
mahusiano naye na alijitahidi kumfahamu huyo binti mpaka kwa wazazi wake.
Anasema ni kwa faida zake mwenyewe. Kwa hiyo ilinifunga nisiwe natembea hovyo
na wanawake. Kwa kuwa inabidi mama ahusike. Ni Liz tu ndio walishindwa na mama.
Lakini wengine wote walikuwa karibu na mama.” “Wa ngapi?” Geb alicheka sana.
“Usiwe na wasiwasi. Hakuna msafara mrefu sana. Ila wewe ndio kiongozi wa wote,
mbeba ukoo.” Nanaa akaguna.
Jumamosi.
Ilikuwa
siku ya jumamosi walipoamka baada ya maongezi marefu ya usiku uliopita. Geb
akimuelezea Nanaa juu ya baba yake. Alimsaidia Nanaa kuoga, lakini pale pale
kitandani kama alivyokuwa amefundishwa na manesi. Akambadili nguo, akaruhusu
manesi waingie wabadili mashuka, wakabaki wamekaa wakizungumza. Bado hapakuwa
na mabusu wala mambo ya mapenzi kati yao.
Mama
G, Oliva, Grace na familia yake wote wakaingia. Nanaa akajikuta machozi
yanamtoka. “Mlinisusa.” Akalalamika. “Wala sio sisi. Geb alipiga marufuku
kila mtu. Akasema tusije, wala tusikupigie simu.” “Simu yenyewe alishachukua.” Nanaa aliongeza huku akifuta machozi. “Haya. Kumbe
unajua? Basi Grace akamwambia, kama hataki upigiwe simu, akifika hapa yeye
apige tukusalimie. Kama unavyomjua Geb, akajibu ‘inategemea’. Na nini? Hakusema. Tukabaki tunasubiri. Jana usiku
kanitumia ujumbe kwamba leo tunaruhusiwa kuja kukuona.” “Tena mimi kaniandikia
kwa msisitizo, ‘kwa muda mfupi’.” Grace akamkatisha mama yake.
Nanaa akacheka.
“Hata
mimi nimeambiwa naruhusiwa kuja, lakini ni kwa muda mfupi. Nikampigia simu
Grace, nikamwambia leo tuamkie hapa hapa hospitalini. Asubuhi tuwe tumefika
kabla madaktari hawajapita.” Mama G akamaliza huku anaweka vitu chini. Nanaa
akacheka, Geb alikuwa kimya kama hazungumziwi yeye. Alishamchukua mtoto wake.
“Mbona
huyu anasinzia!?” Geb akauliza. “Hujanisikia? Nimekwambia tuliamua kuamkia
hapa. Kwani huu ndio muda wa mwanao kuamka?” Mama yake akamuuliza. “Liv kwa
kupenda usingizi!” Nanaa akaongeza. “Hapo nimemuogesha huku amelala. Na
ameshindwa pia kula.” “Basi mlete nimnyonyeshe.” “Ndio atalala kabisa.” Bibi
yake aliongeza huku akienda kumchukua kutoka kwa Geb ili amkabidhi mama yake.
“Nina
hamu na wewe Liv! Jana hukuja kuniona.” Nanaa alilalamika. “Nilimvalisha na
kumwandalia begi lake kabisaa. Baba yake ndio hakutokea. Na mimi kumleta
nikaogopa nisije nikamkorofisha mtoa masharti.” “Nilikuwa na kazi nyingi sana
jana.” Geb akajibu. Nanaa akajifunika nakuanza kumnyonyesha mwanae.
“Mbona
Fili wangu leo hana raha?” Fili alikuwa ametulia sana, kitu ambacho si kawaida
yake. “Danny huyo!” Nanaa akacheka. Alimjua Fili na baba yake. “Nisalimie Fili
kipenzi changu.” Fili akaanza kulia. “Njoo mwaya. Panda hapa kitandani ulale na
mimi. Nyamaza mtoto mzuri.” “Wakati mwingine masikio yake huyo anayahamishia
miguuni.” Danny aliongeza. “Njoo Fili.” Fili akamwangalia baba yake kama
anayeomba ruhusa. “Nenda sasa. Unaniangalia nini?” Fili akaenda kupanda
kitandani kwa Nanaa. Akajilaza vizuri kwenye mto. “Mfunike mama. Anaonekana ana
usingizi.” Bibi yake akamfunika.
“Basi
ndio haya tuliyokuwa tunakatazwa kuja hapa. Sasa na huyu naye atakutwa amelala
hapa hapa!” Grace akaongeza. “Na Liv naye akilala, nitamlaza hapa hapa.” “Na
wewe?” Mama G akauliza. “Nitalala pembeni yao.” “Hata hivyo hawatakaa muda
mrefu.” Geb akaongeza, mama yake akaguna. “Bwana waache. Ninahamu na nyinyi
kweli! Mlienda kwenye kichen
paty ya Suzy?” Nanaa akauliza. “Mama wewe umepitwa! Ilikuwa
si mchezo. Muulize Grace. Tuliserebuka mpaka Grace akanitoa pale mbele.” Nanaa
akaanza kucheka.
“Yaani
mama! Utafikiri ndio alikuwa mama yake bibi harusi!” Grace aliongeza. Nanaa
akazidi kucheka. “Ngoja nikuonyeshe picha.” Mama G akatoa simu. Nanaa akaanza
kuangalia huku Liv ananyonya ndani ya mtandio ambao Nanaa aliozoea kumfunika
wakati akimnyonyesha, huku wamelala pale pale kitandani. Fili pembeni, Oliva
kati kati na Nanaa pembeni. “Mlipendeza!” Nanaa akasifia.
Maji Yametibuka.
Mara
wakaingia James na Malii pamoja na mkewe. James na Malii walikuwa wakicheka.
Nanaa akawaangalia kidogo tu akarudisha macho kwenye simu. Wakasalimiana. “Mbona
midomo imekukauka mwanangu?” Mama G alimuuliza mke wa Malii. “Mama wewe!” Grace
akashituka sana. “Nauliza tu. Mimi ndiye mama yake Malii. Sasa kama ameanza
kumnyima chakula, aniambie nimuweke Malii sawa.” “Hapana mama. Unajua ulinilea
vizuri. Siwezi kumnyima mke wangu chakula.” “Mbona unamjibia wakati nimemuuliza
yeye? Eti mama?” Mama G akasisitiza swali lake. “Hapana mama. Nakula.” Alijibu
na tabasamu la kinyonge.
“Au
mambo tayari?” Mama G akauliza tena. “Mama Magesa Wewe!” Grace akashangaa kwa
kushituka. “Bwana wee! Kila mtoto anakuja na vyake. Kuna mimba nyingine
zinakuja hutaki chakula kabisaaa.” “Sio Nanaa.” Danny aliongeza na kufanya wote
wacheke. “Maana mjamzito huyu na msosi! Hatari.” “Naomba niache Danny. Mwenzio
ni mjamzito.” “Basi ndio sababu yake hiyo! Ngoja ujifungue tuone.” “Si nitakuwa
nanyonyesha! Lazima kula chakula kingi!” Kila mtu alicheka zaidi. “Basi sababu
hazimwishi. Hajali wembamba wala unene. Namwambia unatakiwa kuwa model,
msichana mwembamba. Lakini wapi! Hapo James una dada!” James alikuwa akicheka
tu huku akimwangalia dada yake.
“Kwanza
hapa njaa inauma. Kaka mtu anakula huko ndani, na dada yake anakula hapa nje. Mimi
wembamba huo naupatia wapi!?” “Kula mwanangu. Ushakuwa mama. Utapungua
wakishakua hao. Sasa hivi hakikisha wanapata chakula chakutosha. Mambo ya diet
mpaka wajukuu zangu wakue.” “Ndio maana nampenda mama yangu. Haya, nimiminie
uji basi.” Kila mtu akacheka.
“Na
wewe mama unywe kidogo. Naona hujala bwana.” Mama G akimaanisha mke wa Malii.
Akamkabidhi kikombe. “Hapana mama. Mimi nipo tu sawa. Mwachie tu mgonjwa.”
“Huyo sio mgonjwa. Wewe kunywa tu. Upo mwingi. Kaa hapo ule bwana. Utasimamiaje
harusi ukiwa kama mgonjwa? Kula kidogo angalau umfikie mwili bibi harusi wako.”
Mama G akasistiza. “Heri upokee tu. Mama hajui jibu la hapana. Pokea tu unywe.”
Mke wa Malii akapokea huku akicheka.
“Hayo ndio mambo. Kula ili kwenye harusi na
wewe utokee mwanangu. Watasema unateseka kwenye ndoa bure.” Mama G akasisitiza.
“Hawatasimamia tena harusi yetu.” Geb aliongeza na kufanya kila mtu amgeukie.
“Unamaanisha Malii na mkewe!?” Mama yake akauliza. “Si ndio hao tuliokuwa
tumewaomba wasimamie harusi yetu! ” Geb akajibu, tayari hasira zilionekana
kumpanda. Hakuwa ameongea neno lolote tangia
kina Malii wanaingia hapo, wala hakuwasalimia.
“Kwa nini!?” Malii akamuuliza Geb kwa mshangao.
“Kwa sababu mimi nimesema hivyo.” Alijibu kwa jeuri, kila mtu aliona na
kushangaa. Alijawa na hasira za gafla. Nanaa ndipo alipoiona hasira ya Geb
waziwazi. Akanyamaza na kuendelea kuangalia picha kwenye simu ya mama G. Bado
walikuwa wakimwangalia. Akarudisha macho kwa mama yake aliyekuwa bado amekodoa
macho. “Sasa ni nani anasimamia?” Mama yake akamuuliza na kumwangalia yeye na
Nanaa kwa zamu. Alipoona hata Nanaa hamtizami, akajua kuna jambo la ziada na
hatajibiwa tena. Alishaishi na baba yake Geb, kwa hiyo kwa kumtizama tu Geb,
akajua amekasirika sana na hataongea tena. Akageukia upande mwingine, na Geb
akainamia simu yake. Pakazuka ukimya wa gafla.
“Vipi
mtoto na wewe mwenyewe?” James akabadilisha mazungumzo. “Naendelea vizuri. Jana
walimwangalia mtoto. Wanasema mrefu kweli!” James akatabasamu. “Ila hajambo?”
“Hajambo kabisa. Hapa anacheza. Na siku hizi akigeuka hata kama upo usingizini
utaamka tu.” “Unapata maumivu?” Mama G akauliza. “Sana mama.” “Umemwambia
daktari?” “Ndio maana ikabidi kuangalia tena. Wameniambia kila kitu kipo sawa,
ila napata maumivu sababu mtoto ni
mkubwa sana.” “Hata hivyo siku zimebaki chache. Jikaze mwanangu.
Tunakuombea.” “Asante mama.” Pakazuka ukimya mwingine.
Geb
akasimama na kutoka upande wa barazani. Malii akamfuata. “Vipi!?” Wakamsikia
Malii akiuliza. Kimya. “Mbona unabadilisha mambo kienyeji? Ni jana tu James
ametoka kuzungumzia swala la sisi kusimamia harusi hapa hospitalini. Mimi na
mke wangu tukakubali. Leo unasema hatusimamii tena harusi! Halafu hutaki kutoa
sababu? Ni nini?” Kimya. “Geb!” “Usiniguse tafadhali.” Wakamsikia Geb akijibu.
“Kwa nini unanipuuza? Nakuuliza hunijibu, ni kama hunisikii!?” “Kwa kuwa
unarudia maswali ambayo nilishajibu pale ndani.” Geb akajibu, mama yake
akasimama kwa haraka akatoka nje kuwafuata pale barazani.
“Malii!
Naomba utulie kwanza.” “Hapana mama! Geb ananidharau. Iweje jana James aniambie
tusimamie hapa hospitalini, halafu leo Geb anifanyie hivi? Tena kwa kiburi!
Yeye mwenyewe na Nanaa ndio waliotufuata kutuomba. Leo analeta jeuri!? Kwa nini
anatufanya sisi kama watoto wadogo? Anatuzungusha vile atakavyo!”
James
akatoka. “Jamani naomba mnisamehe. Mimi nilizungumza na Malii bila kuwasiliana
na Geb mwenye shuguli. Kwa hiyo Malii, naomba unisamehe bwana. Kama kuna garama
yeyote mliingia, mimi nitalipa.” “Kwa nini unafikiria swala la pesa tu na
kuondoa ubinadamu? Kwani kinachomshinda Geb kutuambia sababu ni nini?” “Jamani
nashauri mtulie. Geb ameshajibu kwamba ameamua hivyo. Kwa kufanya fujo hapo,
wala haitasaidia kubadili jibu lake. Nashauri Malii uliache hilo jambo liishie
hapo.” “Hapana mama. Huko ni kumwendekeza Geb. Hiyo ni dharau.” Malii
aliendelea kulalamika.
Geb
alikuwa ameshageukia upande wa bustanini. Akionekana pale alishahama wala
hasikilizi tena. Malii alimtizama kwa hasira. “Usije wahi kunitafuta tena. Leo
iwe mwisho.” Malii alitoa onyo kali. Hata Geb hakujisumbua kumtizama.
Alimuonyesha jeuri na kana kwamba hilo onyo ndio kitu alitamani kitokee kati yao.
Akarudi ndani kwa mkewe.
“Twende.” Malii alimuongelesha mkewe kwa jeuri. “Wewe tangulia na gari yako.
Mimi namalizia kunywa uji.” Kila mtu akashangaa.
“Sasa
unaniangalia nini? Wewe umekuja na gari yako. Umeniambia mimi nipande daladala,
nikufuate hapa. Kwa nini kunitoa hapa kwa hasira wakati hata usafiri hatutumii
pamoja! Mimi siondoki sasa hivi. Nasubiri fujo za daladala zipungue na jua
litulie, ndipo nitarudi nyumbani.” Kila mtu akabaki anashangaa. Mkewe
akaendelea kunywa uji wake taratibu.
Malii
akabaki bado amesimama. “Hakika mimi siondoki sasa hivi. Wewe tangulia tu. Hapa
nilipo nimechoka kwa kutembea. Unataka nitoke tena hapa nianze kutembea wakati
mimi ndio nimefika! Hata Malii! Acha nipumzike. Kwanza huwezi jua, naweza
nikabahatika lifti hapa hapa, nikasogezwa hata karibu ya kituo cha daladala
kama sio nyumbani kabisa.” Walizidi kushangaa. Malii alikuwa na usafiri. Iweje
watoke nyumba moja, halafu mkewe atembee wakati Malii alikuja na gari!
James
aliyeingia nao akabaki ametulia pale nje. Alimkuta Malii amekaa ndani ya gari,
mkewe yupo nje ya gari. Akasema ndio amefika. Kwa haraka James akajua ndio wote
wamefika, maana hata Malii alisema ametokea nyumbani. “Malii mwanangu, mimi
nitakusaidia kumrudisha nyumbani. Mwache azungumze na wenzie na amalizie huo
uji.” Mama G akaingilia. Malii akatoka. Mkewe akaendelea kunywa uji taratibu
kama hamna kinachoendelea.
~~~~~~~~~~~~~~
Madaktari
waliingia nakukuta kitandani kwa mgonjwa, wamejaa watoto. “Unaendeleaje Nanaa?”
Daktari wake, Lyamu, alimuuliza baada ya kusalimiana na kila mtu. Geb
aliposikia sauti ya dokta Lyamu, akaingia ndani. “Naendelea vizuri.” Nanaa
akajibu kinyonge huku ameangalia chini. Dokta Lyamu aliyemzoea Nanaa mcheshi
akaona mabadiliko. Akavuta chati ya Nanaa na kuanza kusoma. “Naona tangia
nikuache jana, mambo hayajabadilika. Pressure ipo vizuri, hata ya asubuhi
imeonyesha vizuri.” Daktari aliongea huku akiendelea kusoma ile chati ya Nanaa.
“Endelea
kupumzika na kujtahidi kunywa maji mengi.” “Sawa.” Nanaa akajibu. “Naomba
nikupime tena kidogo kabla sijaondoka.” Daktari akamsogelea. “Ngoja nimtoe
mtoto.” Geb akasogea pale kitandani ili kumtoa Oliva. “Bado dada ananyonya
vizuri?” Daktari akauliza. Alikuwa ni daktari wake Nanaa tokea ni mjamzito wa Oliva.
“Zile siku tatu za kumwachisha ili kaka yake anyonye peke yake sijui kama
itawezekana. Ananyonya kama mwenye njaa ya mwaka mzima!” Lyamu akacheka. “Ndio
vizuri. Bado anahitaji maziwa.” Geb akamtoa Oliva na kwenda kumfunga kwenye
kiti chake. “Ngoja nimtoe na huyo kaka yake.” Danny akasogea. “Hamna shida.
Hapo alipo hanizuii.” Daktari Danny kumtoa mtoto.
Nanaa
akatoa mkono, daktari akapima. Watu wote wakiwa wamenyamaza kabisa
wakimwangalia daktari. Wakamuona amekunja uso. Akamtoa kile kipimo. Akaminya
mkono wa Nanaa kidogo, na kurudishia ile mashine tena. Akapima, wakamuona
amekunja tena uso.
“Usiogope,
mimi nitakuwa sawa.” Nanaa alisikika akimwambia daktari. “Vipi?” Geb akasogea.
“Usifanye mchezo Nanaa!” Daktari akasisitiza. Nanaa akanyamaza. “Umekula
ng’ombe mzima, umebakisha mkia tu. Sina dawa nyingine ya kukupa, lasivyo
itabidi tumtoe huyo mtoto. Hata hivyo ameshakomaa.” “Nimekwambia usiogope. Hizo
siku 11 tulizobakisha na huyu kaka, zitafika tu.” Nanaa alisisitiza huku
akishika tumbo lake. “Kwani pressure ikoje?”
Geb akauliza tena. “Ipo juu sana. Yaani imerudi vilevile! Lakini kwa
sasa, huyu mtoto ameshakomaa. Ni heri atolewe tu. Jana nilimwangalia, ni mtoto
anayeonekana ana nguvu. Kumuacha huko ndani ya mama yake, ni kuhatarisha maisha
yake bila sababu. Tafadhali zungumza na Nanaa. Hamna sababu ya kumuweka huyo
mtoto huko. ” James akaingia akamsogelea Nanaa.
Mipango Ya Mungu Si Ya Wanadamu.
“Vipi?”
Kaka yake akamuuliza. “Nataka kwenda chooni. Naomba nisaidie nisimame niende
chooni.” Akimaanisha kutaka msaada wa kutolewa Fili pale kitandani ili atoke.
Danny akaenda kumtoa mtoto pale kitandani, Nanaa akashusha miguu kitandani.
Akasikia kichomi kikali sana kinapita tumboni. Akakunja uso huku ameshika
tumbo. “Vipi mama?” Mama G naye akamsogelea kwa haraka na Geb pia. “Kimepita
kichomi hapa.” Nanaa akaonyeshea tumboni kwake. “Pole. Kimepita?” Geb akauliza
huku akijaribu kumshika tumboni. Nanaa akabaki amejishikilia tumbo. “Ngoja
niende chooni.” Akasimama.
Aliposimama
tu, maji mengi sana yakamwagika. Chupa ikavunjika. “Haa!” Nanaa akashangaa, na kumwangalia yule daktari. Kama
aliyechanganyikiwa yule daktari akabonyeza kengele kuita manesi. Akapiga simu
chumba cha upasuaji kwa haraka. “Nakuja na mama mzazi. Hawezi kuzaa. Pressure
ni 170 kwa 110. Naomba mniandalie kila kitu. Nakuja sasa hivi.” Tayari manesi
walishafika. Wakamrudisha Nanaa kitandani.
“Nimeingiwa na hofu. Mtoto atakuwa salama?” Nanaa akamuuliza daktari kwa sauti ya chini kuhu
akilia. “Nitajitahi wote mtoke chumba cha upasuaji salama. Usiogope.” “Kama ikikulazimu kuchagua kati yangu na
mtoto, naomba iwe mtoto tafadhali.”
“Nanaa!” Geb akamsogelea. “Usiogope. Kila kitu kitakuwa sawa. Umesikia?” “Nisamehe Geb. Tafadhali nisamehe mpenzi
wangu. Sikukusudia kukuudhi.” Nanaa aliendelea
kulia. Hakuna aliyeelewa. Tayari hofu ilishajaa ndani ya kile chumba. Hofu ya
kumpoteza mtoto na Nanaa mwenyewe. “Nini
kinaendelea?” Ndilo likawa swali la
kila mtu katika kile chumba kwa wakati ule.
Nanaa
alikuwa akilizwa na mengi. Alihofia anaweza kwenda huko chumba cha upasuaji na
asitoke tena. Hofu juu ya mwanae aliyemuhangaikia pia ilimsumbua. Pia alijua
ameshapoteza penzi la Geb. Hilo ndilo lilipoteza hata ladha ya kila kitu.
Alitarajia mtoto aje akiwa ameshaolewa. Lakini hapakuwa na mazungumzo tena ya
ndoa. Ni week ilishapita, hajapata hata busu kutoka kwa Geb.
~~~~~~~~~~~~~~
Nini kitaendelea? Nini hatima ya Nanaa na Magesa? Pressure ipo juu
sana. Na pressure ikiwa juu, mama mjamzito hawezi kuzaa kwa njia ya kawaida,
kuepuka kusukuma kwa nguvu wakati pressure imeshakuwa juu.
Geb je? Siku hiyo ndipo
Nanaa aliona hasira iliyokuwa imejificha ndani
yake. Hakujua kama harusi imesitishwa au la! Si mama G wala
Geb mwenyewe waliozungumzia tena swala la harusi kwa Nanaa, zaidi ya
kumsikia Geb akiwakataa wasimamizi wa harusi.
Hata akipona, je bado atamuoa?
Mke wa Malii naye azua jingine jipya.
Je, ni nini kinaendelea kwa wana ndoa hao?
Usikose. Muendelezo
0 Comments:
Post a Comment