Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! – Sehemu Ya 48. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! – Sehemu Ya 48.

Geb alisimama pale nje akifikiria, mwishowe akarudi ndani. Akaenda chumbani kwa mama yake. “Wewe unafikiri Nanaa atakuwa ameenda wapi sasa hivi?” “Usinitanie Geb wewe!” Simu ya Grace ikaingia. “Naomba kukupigia baadaye.” Geb aliongea kwa haraka akitaka kukata. “We Geb! Nisikilize.” Geb akatulia. “Nanaa yupo chumbani kwake amelala. Amesema nisikwambie alipo ila mama tu, ili amletee mtoto anyonye. Hataki kurudi kwako sasa hivi. Nimekwambia tu kabla ya mama ili usipaniki.” “Nakuja.” “Wapi!?” Grace akamuuliza akimshangaa mdogo wake. “Si huko aliko Nanaa!” “Huwezi kufanya hivyo. Mwache alale mpaka kesho.” “Na mimi!?” Geb akauliza kama mtoto anayenyonya. “Aliyekwambia umkorofishe ni nani?” Geb akanyamaza. “Tulia huko huko upate muda wakufikiria.” Grace akakata simu.

Akampigia simu mama yake. “Nanaa yupo hapa kwangu. Anaomba umletee mtoto ili anyonye.” “Nanaa anajua kuniadhibu jamani! Sasa kwa nini anisumbue mimi wakati aliyemkosea ni Geb?” Grace akacheka. “Kwanza kaja analia. Danny anasema amemfungulia mlango alikuwa amekaa chini, hapo nje analia sana. Anaonekana ametembea kuanzia kituoni mpaka hapa. Halafu usiku huu!” “Amekwambia kitu chochote?” “Wala sikumuuliza. Unamjua Nanaa. Hawezi kusema jambo alilomuudhi Geb. Ila aliniomba nisimwambie Geb alipo. Ndio nikamwambia nilazima kumtaarifu alipo ila nitamuomba amwache kwanza.” “Nipe nizungumze naye mwenyewe.” “Subiri.” Baada ya muda akamsikia Grace. “Mama anataka kuongea na wewe.” 

“Mama!” Akamsikia Nanaa. “Sasa mbona unaniadhibu mimi wakati aliyekukosea ni Geb?” Nanaa akaanza kucheka. “Mimi nimechoka bwana. Njoo unyonyeshe mwanao. Na ukichelewa utamkuta amelala.”  “Sijisikii vizuri mama.” “Nini tena?” Mama G akauliza kwa wasiwasi. “Sijui! Lakini sijisikii vizuri. Halafu…” Nanaa akanyamaza akamsikia analia. “Nini Nanaa? Niambie.” “Nimejikuta nimelowa!”  Maji au damu?” “Maji.” “Usilie. Nakuja sasa hivi.” Mama G akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~

Vichomi vilishaanza kumsumbua Nanaa tokea yupo kwenye daladala anaelekea nyumbani kwa Grace. Alipoteremka, akaanza kujihisi kuloa. Alitembea taratibu kutoka kituo cha daladala mpaka nyumbani kwa Grace. Haikuwa shida kupita getini. Walinzi walimruhusu. Alishazoeleka pale mpaka akapewa chumba chake.

Alipofika mlangoni akagonga. Danny alipofungua tu mlango, akasimama na kuacha kulia. Akapitiliza chooni huku akimwambia Danny, “Mimi nina shida na Grace.” “Hata mimi mzima Nanaa!” Danny akamsikia akicheka huku anafunga mlango wa chooni. Grace alishakuwa amepanda kitandani. Akamfuata. “Naomba taulo na nguo ya kulalia.” Bila kuuliza kulikoni, usiku huo nyumbani kwake, akamletea kila kitu kama alivyoagizwa. Tayari Nanaa alishakuwa kwenye moja ya chumba cha wageni, ambacho ni chake. “Naomba mwambie mama aniletee mwanangu anyonye, lakini usimwambie Geb kama nipo kwako.”

“Geb atakuwa na wasiwasi kama hajui ulipo, Nanaa.” Nanaa akanyamaza. “Naomba nimtaarifu kama upo hapa, lakini nitamwambia akuache. Namjua jinsi anavyopata shida kama haupo naye.” Nanaa akanyamaza. Grace akamuona anafuta machozi. Akajua amemuudhi. “Nenda kaoge, halafu upumzike. Nikuletee kitu ule?”

“Hapana. Nasikia tumbo limejaa kama linavichomi. Nataka tu kuoga na kulala nipumzike.” Grace alimjua Nanaa mpenda kula. Kabla hajaulizwa chakula, huwa anaomba mwenyewe. Kwa kukataa vile, akaona amuache. Akaingia bafuni, akaoga na kurudi kitandani kulala, ndipo akazungumza na mama G, baada ya Grace kuwapigia simu.

~~~~~~~~~~~~~

Geb akabaki amesimama pale mlangoni anamwangalia mama yake akifungasha. “Ngoja basi na mimi nikachukue wallet mara moja, nakuja.” “Wapi?” Mama yake akasimama huku amemkazia macho. “Si tunaenda wote kwa Nanaa!” “Geb Magesa, usinitanie wewe mtoto!” “Sasa unafikiria nitayamalizaje kama sitazungumza na Nanaa?” Mama G akamgeukia vizuri.

“Unauhakika upo tayari kuyamaliza?” “Ndiyo mama.” Mama G akamkazia macho. “Nakuuliza Geb, na nataka ufikirie vizuri. Maana mlichogombana na Nanaa si kuondoka nyumbani bila kukuaga au akijua ulimwambia utawahi kutoka kazini ili mtafute pamoja sehemu ya fungate. Mimi na wewe tunajua hiyo ilikuwa sababu tu ya kumkera mtoto wa watu. Hasira zako zimebeba wivu wakuona James anafanya uliyotakiwa kumfanyia wewe Nanaa na kutofahamu cha kufanya na mali zako ukiwa na mtu mwingine ambaye sio hawara ni mke. Unanielewa Geb?” Mama G hakumbakiza.

“Narudia tena, upo tayari kumtoa Nanaa kwa kaka yake na kumpa yote anayopewa na kaka yake? Maana sitakubali umchanganye Nanaa. Nanaa si mjinga, na wala James hatakuruhusu hata kwa sekunde moja. Mimi na wewe tunajua. Yote anayojua mdogo wake anahitaji na kuyastahili, halafu wewe umeshindwa kumpa, ujue James hatatulia mpaka dada yake amepata.” Mama G akaendelea.

“Sasa je, upo tayari? Nataka unijibu kama upo tayari kuona kambi mbili humu ndani? Wewe ukipata mapenzi na watoto, halafu James na dada yake wakiwa timu moja wakitafuta maisha ambayo unajua James alivyo. Atakushinda tu. Na taratibu utajikuta wewe ndio utakosa nguvu na kupoteza kila kitu. Utabakia kuonekana ni mwanaume bahili. Likitokea la kutokea, mimi si Mungu, wewe hufahamu kesho ikoje. Hiyo sura yako utaiweka wapi? Ulimwengu wote utakujua ulimtenga mkeo kwenye mali zako, kaka yake akaanza kumsaidia.” Mama G alizungumza naye bila kumficha.

“Unakumbuka historia ya baba yako na mkewe yule wa kwanza? Sijui alikuhusia nini! Lakini walipomfilisi na kumshitaki mahakamani. Yule mama na watoto wake, walitaka baba yako aondoke kama alivyo. Alikuwa na pakurudia, kwangu, kwa kuwa alihusika kujenga. Hakupata shida hata kuja kumiliki na mimi kwa kuwa alinisaidia kujenga. Kuanzia chini mpaka nilipokuwa. Alipokuwa mgonjwa, nilimchukua na kumleta nyumbani kwetu. Na si kwangu. Palikuwa kwetu. Kwa kuwa aliijenga ile nyumba. Akaweka miradi na alikuwa pia akija kupakarabati, wewe ni shahidi. Japokuwa alirudi kwa mkewe, lakini alihakikisha hakuna linalompita kwenye maisha yangu. Tena kwa kushiriki bega kwa bega. Kama hakuwepo yeye, basi alihakikisha ananiachia mtu anayemwamini.” Mama G akamwangalia tena. Kimya.

“Huwa najiuliza ni kwa nini Magesa hajakupa busara zake, amekupa hayo macho tu ambayo hayakusaidii!” “Unanitukana mama.” Hilo ndilo tusi alilopenda kumtukana nalo Geb, na Geb alijua huwa akifika hapo ndio amechemka, hasira ipo mpaka mwisho. “Sasa nisikilize Geb. Narudia tena. Wewe mtoto wa Magesa, nakuonya. Tena nakuonya sana. Usiniondolee amani na kuniharibia mipango. Mwanamke atakayeishi humu ndani na mimi ni Nanaa tu.” “Kwani mimi nimekataa?” “Basi, kaa chini ujiulize ni nini unataka. Na ukishapata jibu, ndipo ujue jinsi ya kuishi na sisi. Haswa Nanaa. Unanielewa Geb?” Kimya. 

“Nisikuone unanifuata nyuma. Alikufuata chumbani ili muyamalize, ukashindwa. Sasa tulia hapo mpaka ujue chakufanya.” “Mbona nimeshajua cha kufanya?” Mama G akajiweka sawa. “Nakusikiliza.” “Mimi mwenyewe ndio nitamnunulia gari. Nimeshaanza kumtafutia gari. Zuri sana.” “Geb usinitanie wewe mtoto! Mimi muda wote niliokuwa nikiongea hapa nilikwambia Nanaa anataka gari?” “Mengine taratibu mama! Mbona unakuwa mkali kwangu?” “Sasa ndio hivyo. Wakati wewe unajipanga, mwache Nanaa aendelee na kaka yake.”

“Kwa nini na wewe usizungumze naye akawa na subira?” “Aliyekwambia anashida na mali zako ni nani? Ushamsikia Nanaa anakuulizia unaingiza kwa mwezi pesa kiasi gani? Ushamsikia anakuulizia unabiashara gani? Au leo unataka wote tuonekane wehu nikurupuke nianzishe kitu ambacho wala hakikuwepo kwenye akili zake?” Kimya.

“Wewe unasutwa na dhamira yako ndio maana unahangaika hivyo! Naomba mwache Nanaa. Wewe endelea na mipango yako kama kawaida. Na wala sikulaumu. Wapo wanaoishi na wao kama hivyo wewe tu na maisha yanaendelea. Wake zao hawajui chochote kinachoendelea kwenye maisha yao, na ndoa bado zipo. Ila madhara yake naona umeanza kuyaona mapemaaa. Mke utakuwa naye humu ndani, lakini akili zipo kwa kaka yake na wanaume wengine watakaoweza kumsaidia. Ndipo kutoka nje ya ndoa kunapoanza hapo. Atakutana na mwanaume mwingine anayeonekana anajali ndoto zake kuliko wewe. Anamjali na kumsaidia kimawazo. Kwa nini asimpe kidogo ambacho anakugawia na wewe?” Kimya.

“Sasa baki hapa, usinifuate nyuma.” “Mimi siwezi kulala humu ndani bila Nanaa.” “Geb!” Mama yake akamuita kwa kumtahadharisha. “Katika mambo kama haya, wewe unatakiwa uwe upande wangu mama!” “Unanipotezea muda.” Walipogeuka kitandani alipokuwa mtoto, wakakuta Liv alishalala. “Ona sasa!” “Sasa na hapo pia kosa ni langu!? Wewe unamjua Liv jinsi anavyopenda kulala, halafu na wewe ukamuweka kitandani!” “Nenda Geb kabla hujaniudhi zaidi. Kama sio wewe kumkera mama yake mpaka kuondoka, huyu mtoto angelala ameshiba. Amelala na njaa sababu yako wala sio mimi.”

“Basi wewe baki hapa na mtoto mimi niende kwa Nanaa.” “Geb!” “Ni wazo tu mama!” Geb akacheka kidogo.  “Sitaki mawazo yako. Jishauri mwenyewe na balaa lako. Wewe utabaki hapa na mtoto, mimi ndio nakwenda kwa Nanaa.” “Mwambie namsubiria tulale.” “Hakika sitamwambia. Kwanza naona akae tu huko huko kwa Grace mpaka akili yako itakapokukaa sawa au mpaka siku ya harusi.” “Haa! Tafadhali sana mama. Hapo ndipo utakaponifanya nitembee uchi barabarani.” “Unatembea uchi vipi wakati unapesa za kununua nguo? Hebu nipishe hapo mlangoni.” Akamsukuma mwanae akapita ili aondoke.

Geb akatumia akili ya haraka kumtuliza mama yake. “Ukirudi na Nanaa leo, mzigo wa jumamosi ijayo nitakulipia mimi. Nitamwambia dereva akushushie mzigo halafu pesa yote namlipa mimi, Grace.” Akamuona amegeuka. Akajua tayari amenasa. Kabla hajafikiria vizuri, akamkatalia, Geb akamchanganya zaidi. “Tena nitawaambia wakushushie oda yako kama ilivyo, wasikupunje.” “Na sitaki mchele mbaya kwa kuwa ni wa bure.” “Sio bure, si ndio unaenda kumleta Nanaa!” “Usinichanganye Geb!” “Basi mama yangu. Nitamwambia akuchagulie mchele mzuri.” “Sasa mchele tu!?” Geb akaanza kucheka huku anatingisha kichwa.

“Kweli mama unapenda pesa!” “Sio kupenda pesa. Wewe kama umeamua kutoa hongo, toa hongo zakueleweka sio hongo za kitoto!” Mama G alishatulizwa. “Basi nakuongezea na lita 20 za mafuta, kama utazungumza na Nanaa swala la kukasirika, halafu anaondoka nyumbani. Mwambie akikasirika awe anatulia nyumbani tuzungumze.” “Unamaanisha ukimkera, asiondoke?” Geb akacheka zaidi.

“Ukitaka nizungumze naye hivyo labda unipe lita 40 za mafuta ya alizeti.” “Mama!” Geb akashangaa sana. “Basi utaonana na Nanaa siku ya harusi. Kwanza nataka apumzike.” “Jumatatu nitamtuma dereva akuletee mafuta halafu jumamosi mchele.” Mama G akageuka na kuanza kuondoka. “Hujisikii vibaya?” Geb akamtupia swali. “Hata bibilia inasema, ‘kila mtenda kazi anastahili ujira wake’. Wewe unaharibu, mimi nina kazi ya kujenga. Soma bibilia wewe mtoto wa Magesa.” Mama G akajibu huku anatoka. “Usichelewe sasa!” “Unataka kuniongezea na malipo ya kuniharakisha?” “Hapana mama. Wewe nenda, nitasubiri tu. Utanifilisi bure!” Akamsikia anacheka huku anafunga mlango. 

Kila Kazi Na Malipo Yake.

Nyumbani kwa Grace na Geb hapakuwa mbali sana. Wote waliishi Tabata. Alipofika, akamkuta Grace anamsubiria sebuleni. “Nanaa analalamika vichomi, mama. Hajala.” Mama yake akaingia chumbani. Akamkuta amejifunika. “Vipi?” “Nasikia vichomi mama. Nahisi naendelea kuloa.” “Tuone.” Mama G akamfunua. Akakuta ameloa. “Hii sio ishara nzuri. Twende hospitalini moja kwa moja.” Grace akamtolea nguo, akavaa. Wakatoka Grace, mama yake na Nanaa.

Njiani akampigia simu Geb. “Sasa sio uanze kupaniki. Tunampeleka Nanaa hospitalini kwa checkup.” Mama yake akaanza kwa kumtahadharisha. “Kwa nini tena?” Geb akauliza. “Tutajua tukifika huko.” “Hapana mama. Nataka kujua kwa nini anaenda hospitalini usiku huu!?” “Hajisikii vizuri.” “Hilo jibu halitoshi.” Mama G akatulia kidogo. “Mama?” Geb akaita. “Kwa nini usisubiri mpaka tumuone daktari!” “Nipe Nanaa mwenyewe nizungumze naye.” Mama G ndiye aliyekuwa akiendesha, akampa simu Nanaa aliyekuwa amejilaza kiti cha nyuma. “Geb anataka kuongea na wewe.” Nanaa akafungua macho akapokea

simu.

“Geb!” Nanaa akaita. “Vipi?” Akamsikia ameanza kulia. “Pole. Nini kinauma?” “Sijui! Lakini nasikia vichomi vikali, sijisikii vizuri, halafu maji yameanza kutoka.” “Unamaanisha maji ya kumtunzia mtoto!?” “Sijui Geb! Nimeona tu naloa.” “Naomba usilie Nanaa. Tulia kabisa. Mungu yupo na sisi. Hatuwezi kumpoteza huyo mtoto.” “Naomba uniombee.” “Nakuombea mpenzi wangu. Pole. Kila kitu kitakuwa sawa.” Nanaa akarudisha simu kwa mama G. “Unipigie mkishafika tu hospitalini.” “Sawa.” Mama G akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~

Hapo hapo Geb akaanza kubeba vitu vya mtoto wake na kuingiza kwenye gari. Akaenda kumtoa mtoto pale kitandani na kumfunga kwenye kiti chake kwenye gari, akaondoka mpaka nyumbani kwa Grace na mumewe. Danny akamfungulia mlango. “Naomba nimuache hapa Liv. Haitaji chochote ila sehemu ya kulala mpaka bibi yake atakapokuja kumchukua. Ila hataamka mpaka kesho saa nne asubuhi kama ikitokea bibi yake hatawahi kurudi.” “Hamna shida.” Geb akamkabidhisha kwa Danny na yeye akatoka kwa kasi akiwahi hospitalini.

~~~~~~~~~~~~~

Nanaa alifikishwa hospitalini mapokezi. Alipoangaliwa, ni kweli maji ya kumtunzia mtoto yalikuwa yakitoka na presha ilikuwa juu. Wakashauriwa alazwe ili apate mapumziko na ashushwe ile presha. Wakati anaingizwa wodini, na Geb naye akawa ameshafika. Mama yake akamueleza kwa kifupi. Wakaelekea kwenye chumba alichopata cha kulazwa. 

          “Pole Nanaa!” Geb akarudia. “Asante. Naogopa Geb! Itakuaje kama mtoto akitoka?” Nanaa aliuliza huku akilia. “Nimeambiwa presha ipo juu Nanaa. Naomba uache mawazo yatakayokusababisha izidi kupanda. Huyo mtoto hatukumuweka sisi. Aliyemuweka atamtetea. Naomba tufanye kwa upande wetu tu. Sasa hivi wewe unahusika kumtunza. Naomba jitahidi kwa upande wako kutulia ili na presha nayo itulie, yeye awe salama. Hilo ndilo tunaweza kufanya kwa sasa. Basi. Sawa?” Nanaa akatingisha kichwa kukubali. 

“Bado una mamumivu?” Geb akamuuliza huku akimpapasa tumbo taratibu. “Sio sana.” “Lakini bado yapo?” “Kama vichomi. Wameniambia wamempigia simu daktari wangu. Aje, na kufanya ultrasound na mengineyo, ili kujua ni nini kinachosababisha. Ila nimemsikia nesi akisema kama presha ikizidi kuwa juu daktari anaweza kulazimika kumtoa mtoto. Lakini sitaki Geb. Nimebeba miezi yote hiyo nakaribia kumaliza 8, sitaki kumpoteza mtoto ambaye hata sijamjua! Sijui kama ni wakike au wakiume! Hata sijamfurahia mwanangu! Hapana Geb. Mimi sitaki waje wamtoe huyu mtoto.” “Basi naomba usilie, tumwambie Mungu.” Geb akapiga magoti pembeni ya kile kitanda huku amemshika mkono Nanaa.

“Nakushukuru Mungu kwa heshima uliyotupa mimi na Nanaa. Si kwa kustahili kwetu ndio maana umetupa Oliva na kaka yake.” Mama G akafungua macho akamtazama Geb. Hakuna aliyekuwa akijua jinsia ya huyo mtoto. Kumbe wakati wote yeye alijua jinsia ya mtoto! “Wakati huu Magesa anahitaji msaada ambao sisi hatuwezi kumpa, na madaktari wanaonekana kushindwa. Namuombea mtoto wangu. Nakataa kifo cha Magesa kabla hajatimiza kusudi lake hapa duniani. Magesa ataishi aje asimulie makuu yako wewe Mungu. Natubu kwa lolote nililosababisha mimi binafsi mpaka kufikia hapa. Nakataa roho ya uharibifu. Natakamka uzima juu ya mtoto wangu. Nakiri kuwa Magesa ataishi wala hatakufa. Najua uweza ulioweka kwenye damu yetu. Kwa kuwa na yeye amebeba damu yangu, ninaamini uliweka uwezo wa upambanaji ndani yake. Atapambana na hali yeyote inayomkabili sasa.”

“Nakuamuru Magesa, utulie mpaka siku zako za kukaa tumboni mwa mama yako zitakapotimia. Hutatoka sasa hivi ili utunzwe kwenye vyombo vilivyoumbwa na kazi ya mwanadamu. Utakaa pale Mungu alipokusudia ukae kwa miezi 9 kamili ndipo utakapotoka na nikuone. Tunakupenda na tunakuombea ulinzi wa kiMungu ndani yako. Kila silaha itakayoinuka juu yako, mimi ninaingamiza katika jina la Yesu Kristo. Kila ulimi utakao tamka mabaya juu yako na kuleta uharibifu wowote, mimi baba yako na mama yako, usiku wa leo, tunautengua na kuufuta katika ulimwengu wa roho, sasa hadi siku utakapokamilisha kusudi lako hapa duniani. Natamka uzima ndani yako. Kila kilichoanza kufa kwenye maisha yako, nakijenga na kukitamkia uzima na baraka. Mungu akutunze na akujalie ukuaji mkamilifu huko tumboni. Ili mama yako afurahie ukaaji wako.” Geb akaendelea.

“Nakuombea uzima Nanaa mke wangu. Mungu akuponye. Amani ile ipitayo amani zoote, ikatawale moyoni mwako. Umebarikiwa Nanaa kwa kuwa unafanya kazi kubwa ya kuleta kusudi la Mungu hapa duniani. Nakuombea uzima ili ufurahie huduma hii ya umama. Nakuombea uwezo wa Mungu ukawe juu yako ili ukaweze kustahimili kila kitu mpaka mwisho. Naomba Mungu unijalie uwezo wa kuwa msaada kwa Nanaa na watoto wangu. Naomba amani kati yangu. Nisamehe pale ninapokuwa kwazo. Nisaidie niweze kusimama kwenye nafasi yangu. Amina.” “Amen!” Kila mmoja akaitikia.

“Ulijuaje kama ni mtoto wa kiume!?” Nanaa akauliza mara baada yakusema Amen. “Tokea ultrasound ya kwanza. Nilichukua namba ya simu ya yule….” “Ngoja kwanza Geb. Si tulisema tusubiri?” “Wewe ndio ulitaka kusubiri Nanaa. Mimi nilitaka kujua.” Grace na mama yake wakaanza kucheka. “Geb wewe!” “Kweli tena.” “Umenizunguka bwana!” Mama G alizidi kucheka kuonyesha amefurahi. “Hataa! Wewe ulitaka kusubiri. Nikakwambia sawa. Na ili nisiharibu matakwa yako, baadaye mimi nikapiga simu kuulizia. Wakaniambia. Nikabaki na jibu langu. Leo nilitaka ujue kwa kuwa ulionyesha kujutia kutojua jinsia yake mpaka leo.” “Lakini nimefurahi sana. Nilikuwa natamani mtoto wa kiume, kupita kiasi.” Nanaa akajishika tumbo.

“Kwa hiyo huyo ndio Magesa?” Mama yake akamuuliza. “Haswaaa! Magesa G. Magesa.” “Geb! Mpaka umempa mtoto jina kamili!?” Grace alishangaa. “Nilimuomba huyo mtoto baada ya Oliva tu kuzaliwa. Nilimuomba Mungu anijalie mtoto wa kiume angalau mmoja tu. Nikamuomba na mengineyo. Nilipojua Nanaa ni mjamzito. Kwanza nilishituka kwa kuwa sikuwa nimempigia mahesabu ili ashike mimba ya mtoto wa kiume. Nikajua atakuwa ameshika tena mimba ya mtoto wa kike. Lakini alipoonyesha anampango wa kuendelea kuzaa hata baada ya huyu, nikajifariji. Nikamkumbusha tena Mungu kuwa mtoto wangu wa tatu basi awe wa kiume. Kumbe jamaa alishakuwa ametulia ndani. Nilipoambiwa ni wa kiume, nilitamani kuruka ruka.” Geb aliongea akicheka.

“Geb wewe ni msiri sana! Mimi nisingeweza. Ningeshamwambia kila mtu.” Geb akacheka. “Mnakumbuka siku ile niliwaambia mnisindikize kituo cha watoto yatima kule Mburahati ili nipeleke chakula na pesa?” “Mimi nilijua kuna kilichokufurahisha tu ndio maana unatoa sadaka. Lakini sikujua kama ni hilo. Maana niliona kuna kulazimishwa. Kila nikikwambia tufanye juma linalofuata, nikaona unakuwa mkali. Na unataka kila mtu awepo mpaka watoto kina Fillius!” Mama G akaongeza nakumfanya Grace acheke zaidi.

“Mimi nilimwambia Geb, muda huo ndio watoto wanakuwa wamelala, nikaona amenikasirikia. Akawa mkali. Anataka watu wote tuwepo hata kama watoto watakuwa wamelala, twende nao hivyo hivyo. Nikamwambia mama hii sadaka ya safari hii ni ya kibabe!” Wote wakacheka. “Pale nilikuwa nafuraha, sikutaka mtu anicheleweshe kumtolea Mungu sadaka yangu ya shukurani. Na hapo nilikuwa nimeshaandaa jina kamili. Kwa hiyo pale tunakwenda kule kituoni, nilishakuwa na jina. Nikafanya kama mama alivyotufundisha kabla ya kutoa sadaka kuzungumza na Mungu. Nikamtajia Mungu jina la mtoto wangu, na nikamuombea baraka zote za siku ile, ziwe juu yake. Basi.” Geb akamalizia.

“Hongereni sana. Hongera Nanaa kwa kutuongezea kina Magessa. Usiogope. Huyo ni mbarikiwa. Na asili ya kina Magessa ni wapambanaji. Utakuja kumuona tu mwanao. Jiandae kunyonyesha mchana na usiku.” Nanaa akacheka. “Asante mama. Lakini tutamuombea aje kuwa kama dada yake. Usiku tuwe tunalala.” Wakacheka. “Dume hilo! Huoni unavyokula sasa hivi?” “Lakini leo sikula vizuri. Hata nilipokuwa na kaka, niliagiza chakula ninachokipenda, nikashangaa kinanishinda!” “Kwa kuwa hukuwa ukijisikia vizuri. Watakuangalia. Wakijua tatizo na kulitibu, utarudia hali yako. Nashauri ulale sasa hivi. Pumzika kabisa. Hakikisha unapumzisha akili na moyo wako ili hiyo presha ishuke. Tutakuona kesho.” “Asanteni mama na Grace.” “Punguza mawazo Nanaa. Kila kitu kitakuwa sawa.” “Asante Grace. Nitajitahidi kutulia.” Grace akamkumbatia na kumbusu. Nanaa akajisikia machozi yanamtoka. “Asante Grace.” “Damu ya Yesu ukifunike Nanaa. Nakuombea amani na furaha.” “Asante.” Grace akamfunika vizuri, akatoka nje.

“Kesho nitakupigia kujua daktari anasemaje. Kama wataendelea kukupumzisha, nitakuletea Liv.” “Nitashukuru mama. Asante.” “Haya.” Mama G na yeye akatoka. Geb akawafuata nyuma. “Asanteni mama na Grace. Nashukuru kwa kila kitu.” “Mungu atawasaidia Geb. Na sisi tunarudi nyumbani, lakini njiani tutakuwa tunawaombea.” “Asante mama. Usiku mwema. Akiamka Liv mlete tu.” “Sawa.” Wakaondoka Geb akarudi chumbani alipokuwa Nanaa.

Nanaa & Geb!

Akavuta kiti na kukaa pembeni yake. “Nakupenda Nanaa.” “Sasa tatizo ni nini Geb?” “Nilikosa tu. Nahisi sijui napatwa na wivu!” “Wivu na kaka James!?” “Naona ananiingilia Nanaa. Wewe ni mke wangu sasa. Natamani alijue na kuliheshimu hilo. Mahusiano yenu kwa sasa sio kama zamani. Mimi na wewe ni kitu kimoja. Kitendo cha kukutoa kwangu na kupanga naye mipango ya maisha bila mimi kuhusishwa moja kwa moja, inanikera.” Nanaa akatulia.

“Lazima James aelewe hilo na kuliheshimu Nanaa. Sio sawa kumchukua mke wa mtu na kaunzisha mambo unayojua yatatugawa.” “Sidhani kama anania hiyo Geb.” “Sasa kwa nini akupe wazo la kufanya naye biashara. Wewe peke yako angali akijua mimi nipo na ninafanya biashara? Anaona kama vile mimi nakutenga kwenye mambo yangu?” “Sidhani Geb. Nafikiri kaka anania ya kunisaidia tu.” “Kwani ulimwambia una shida?” “Hapana!” “Sasa!?” Nanaa akanyamaza. 

“James ananifahamu vizuri zaidi yako Nanaa. Si sawa kufanya anayofanya.” “Labda hiyo ndiyo sababu inayomfanya afanye anayofanya. Anaona mimi sikufahamu na huna mpango wa kunifahamisha. Ukweli mimi na wewe tunatoka kwenye ulimwengu mbili tofauti Geb. Umeanza kushika pesa nyingi kabla yangu. Ni ngumu kunifikiria kama mwenzako katika maswala ya uchumi. Mimi naelewa. Na nafikiri hata kaka anafahamu hilo ndio maana anajaribu kunisaidia. Siwezi kubakia hivi milele kama mama yake Oliva tu! Oliva hatanyonya maisha. Watoto wote watakuja kwenda shule na watakuwa na kwao. Nini itakuwa hatima yangu?” Wote walikuwa wametulia wanazungumza taratibu.

          “Mimi nipo Nanaa.” “Sasa hivi upo. Hujui kesho yako Geb. Halafu mimi sijui kukaa bure. Unanijua nilivyo muhangaikaji. Nitakapomaliza hili la kuzaa na kulea, nitahitaji kitu chakufanya. Nitafanya nini, ndio kaka anajaribu kunisaidia. Sidhani kama ni sawa eti nije kuanza maisha mapya nikiwa nimeshazeeka! Nafurahia hivi mambo yote yanavyokwenda kwa pamoja. Wewe unafanya mambo yako. Na mimi nifanye ya kwangu na kaka, wakati ninalea. Amesema atanisaidia kwa asilimia kubwa tu ili nisihangaike na mambo ya biashara wakati nina watoto.” Geb akawa anatingisha kichwa kukataa.

“Nini?” Nanaa akauliza. “Sasa unafikiri mimi nitakuwa nahangaika kwa ajili ya nani?” “Sijui Geb! Mimi nitajuaje? Labda unahangaika kwa ajili ya watoto wako! Hatujawahi kukaa chini tukazungumza chochote juu ya maisha mengine mbali ya mapenzi.” “Basi ni kuchelewa tu. Lakini mimi sihesabu eti kuwa mali zote nilizo nazo eti zote ni za kwangu peke yangu. Nanaa hahusiki. Kazi ya Nanaa ni kuzaa tu! Hapana Nanaa. Mimi nimekuchagua wewe kwa makusudi kabisa. Ni mtu ambaye najua tutaishi mpaka tuzeeshane. Hakuna mipaka kati yetu. Kama unaswali lolote wewe niulize tu nitakujibu.”

“Sina sababu yakufanya hivyo Geb. Wewe ukiwa tayari na ukiona ni sawa kunishirikisha mambo yako, itakuwa sawa. Na kama ukiona hivi tunavyoishi ni sawa, pia sitalalamika. Ila ujue ni lazima na mimi nifanye kitu.” “Mbona unafanya mambo makubwa na mazuri Nanaa? Unaendesha mambo ya nyumbani. Hapo ulipo upo kwa ajili ya kuhakikisha huyo mtoto anazaliwa salama.” “Unajua namaanisha nini Geb. Yule nesi aliyenipokea pale na kuniwekea hii dripu, na yeye ni mjamzito kama mimi. Anapete ya ndoa kidoleni. Ameniambia ana watoto wengine wawili wa kiume, walikuwa wanatafuta mtoto wa kike. Ndio hiyo mimba aliyonayo sasa hivi. Na yupo hapa kazini, usiku huu, amenihudumia mimi.” Geb akanyamaza kwa muda. Kisha akaongeza.

“Naomba ujue, nahangaika pia kwa ajili yako Nanaa.” “Asante.” Nanaa akajibu kwa kifupi. “Mbona kama huamini?” “Ulitaka nifanyaje Geb? Mimi nimekushukuru.” “Nataka uamini, kuwa vyote nilivyo navyo ni vyetu sisi na watoto wetu. Na naomba ujue, sifurahii vile James anavyotugawa.” Nanaa akanyamaza. “Hawezi kufanya biashara na wewe bila mimi. Wewe huna kitu chako na mimi sina kitu changu. Yale magari pale nje sio ya kwangu. Ni yetu. Chukua lolote utakalo uendeshe.” “Hata kama sijui kuendesha?” “Mimi ndio nitakufundisha, sio James.” Nanaa akacheka huku akimtizama asiamini. Tayari akaona amenaswa katikati ya mapenzi ya marafiki hao wawili. Kaka yake na Geb.

          “Kweli wivu umekupata Geb! Ni kwa nini?” “Sitaki kuingiliwa na wewe. Mimi nina mipango yote ya maisha yetu?” “Mipango gani? Kwa nini sasa huniambii?” “Utashika mangapi Nanaa?” “Unajua nini ninamaanisha Geb.” “Nilifikiri tumegawana majukumu. Wewe mambo ya nyumbani, mimi mambo ya kazini?” “Wewe unajua majukumu yangu yote Geb. Lakini mimi sifahamu unachofanya zaidi ya kile anachokifanya Grace. Nasikia tu kutoka kwa mama kuwa unabiashara nyingi. Nashindwa hata kumuuliza. Naona ni kama wewe hutaki mimi nijue.” “Sio kweli bwana Nanaa.” “Sawa.” Mara nesi akaingia.

 “Samahani. Naomba usiku wa leo umpishe alale. Pressure yake ilikuwa juu sana. Anahitaji mapumziko haswa. Nimekuja kumchoma sindano ya usingizi. Anatakiwa alale kabisa. Wala hatajua aliyekuwepo pembeni yake. Sisi tutakuwepo kumsaidia kama akihitaji msaada.” Nanaa akacheka huku akimwangalia Geb. “Unafurahia mimi kufukuzwa?” “Wewe si umeniombea amani na furaha? Ndio ujue nina amani kwa lolote lile.” “Mimi nitanyamaza. Sitamuongelesha tena. Wewe mchome sindano.” “Una uhakika?” Yule nesi akamuuliza, Geb akabaki akimtizama. “Hatarudia kukujibu alilokwisha kwambia wala hataondoka hapo alipokaa. Unaona kile kibegi kidogo pale na begi la laptop? Ni mizigo yake yote ile. Yaani hapa ndio amefika.” Yule nesi akacheka kidogo huku akitazama mizigo ya Geb. “Wewe nichome hiyo sindano, ukapumzike.” Akamchoma sindano, akampima tena na kumwangalia maji.

“Jitahidi kupumzika.” “Asante. Kwani pressure umeonaje?” “Bado ipo juu. Sio vizuri hasa ukiwa kwenye hatua hiyo.” “Asante. Nitalala ili kutulia. Usiwe na wasiwasi. Nikitaka kitu, atakuja kukuita.” “Na sisi tutakuwa tukipita kukuangalia mara kwa mara.” “Asante.” Nesi akatoka.

“Usiku mwema baba Liv!” Nanaa akamtania. Geb akacheka na kutingisha kichwa. “Usimpigie simu James mpaka mimi mwenyewe nitakapoamua.” Nanaa akazidi kucheka. “Unajitesa bure mpenzi wangu.” “Sitaki kuingiliwa.” “Haya Geb! Lakini ujue akijua nimelala hapa leo bila yakumwambia, hatafurahi.” “Ndio aanze kuzoea kuwa wewe ni jukumu langu hakuhusu tena. Mtu anajua mpaka idadi ya watoto tutakao zaa kabla yangu mimi mwenyewe!” Nanaa akazidi kucheka.

“Anachukua mke wangu na kumpa mipango bila idhini yangu!? Hapo amenikosea sana.” “Nia yake nzuri.” “Hainihusu mimi. Sasa hivi nitakuwa makini naye sana.” “Mwenzio nimeanza kusinzia hapa. Na usiondoke hapo. Nikiamka nikukute hapo hapo.” “Si ulinikimbia wewe?” “Kwa muda tu ili utulie Geb. Ulikuwa umekasirika sana. Nilishindwa kukutuliza.” “Kwa hiyo ungerudi?” Nanaa akacheka na kufunga macho. Hapo hapo akapitiwa na usingizi.

Nanaa na Bedrest

Aliamshwa asubuhi na madaktari waliokuwa wanapita round. “Unajisikiaje?” Nanaa akafikiria kidogo. “Vizuri. Lakini..” Akasita tena huku akijipapasa. “Nini?” Geb akamsogelea. Alikuwa amesimama pembeni kuwapisha madaktari ili wamwangalie.  “Nahisi nimelowa.” Nanaa aliongea huku machozi yakimtoka. “Mnafikiri mwanangu ni mzima?” Nanaa akauliza kwa kilio. “Cha msingi utulie kabisa. Tutakwenda kumwangalia kwenye Ultrasaound ili tujue anaendeleaje.” Daktari aliyekuwa akimuona kwenye kliniki aliongeza. “Jana ulimsikia akicheza?” Daktari akauliza tena. “Asubuhi. Lakini mida ya usiku sikumsikia kabisa. Na anamtindo wakucheza kila siku asubuhi. Ni kama ndiye anayeniamsha.” Nanaa alijibu huku akijishika tumbo. “Unafikiri atakuwa salama kama maji yakiendelea kutoka hivi?” Nanaa akauliza tena.

“Cha msingi ni kuhakikisha hiyo pressure yako inashuka, kwanza. Tutamwangalia mtoto, kisha tutajua jinsi ya kumsaidia yeye na wewe. Sawa?” Nanaa akatingisha kichwa. “Hakikisha unatulia kabisa. Pata mapumziko ya kutosha. Na sisi tutatafuta njia ya kukusaidia ili pressure ishuke na mtoto atunzwe humo ndani mpaka akomae zaidi. Anaweza kutolewa na kuwekwa kwenye chupa ya kumkuzia, lakini humo tumboni kwako ndio sehemu ya pekee na salama kwake. Kwa hiyo kwa namna yeyote ile, hakikisha umetuliza mawazo kumsaidia mtoto. Tutakuwa makini na vyakula unavyokula, ili visizidishe hiyo pressure. Ukitoka kwenye chumba cha Ultrasound nitarudi kuzungumza na wewe zaidi.” Wale madaktari na wanafunzi wanaosomea udaktari walizungumza na Nanaa pamoja na Geb kuwafariji na kuwatia moyo. Ndipo wakaondoka.

Walipotoka tu, Geb akavuta kiti mpaka pale kitandani. “Usiogope Nanaa. Mungu yupo na sisi. Hajawahi kutuacha. Hawezi kuanza leo.” Akaweka mkono tumboni kwa Nanaa. Akasogeza mdomo pale tumboni kwa Nanaa. “Magesa! Hakuna sehemu sahihi unaweza kukaa sasa hivi isipokuwa huko ulipo, tumboni mwa mama yako. Lazima utulie. Mungu yupo na wewe, atakushindia. Una damu ya kupambana. Huu ndio wakati wako. Lazima upambane na kila upinzani unaopitia humo ndani. Hakikisha wewe ndio unashinda na unabaki huko mpaka siku ambazo Mungu amekuamuru ukae. Nakuombea na mimi nipo na wewe. Haupo peke yako. Lazima tutashinda. Kwa kuwa Mungu ametuahidia ushindi.” Akambusu Nanaa tumboni na kumpapasa mpaka yule mtoto akaanza kucheza.

Nanaa alianza kucheka mpaka akalia. “Mungu wangu! Anacheza Geb!” Nanaa aliendelea kulia. “Asante Yesu. Anacheza!” “Safi sana. Usiwe unanyamaza ukamtia mama hofu.” Geb akambusu tena kisha akamsogelea Nanaa. “Huyu hatoki humo. Ni mpambanaji, hawezi kushindwa.” Akambusu Nanaa. Nanaa akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha kama aliyepata aghueni. Walikuja kumtayarisha kwa ajili ya ultrasound, kisha wakaenda akiwa amelala vile vile kitandani.

~~~~~~~~~~~~~

Baada ya ultrasound daktari akashauri Nanaa asitoke pale mpaka siku ya kujifungua. Geb alitamani kuchanganyikiwa. “Tuna harusi baada ya siku 13 tu!” Geb alijikuta akiropoka mbele ya yule daktari aliyewafuata pale chumbani. “Geb!” Nanaa akashangaa. “Kweli Nanaa. Lazima tufunge ndoa siku na muda tuliopanga. Hakuna kusubiri tena.” “Mtoto wenu ni mkubwa sana. Kuanzi urefu mpaka uzito wake huyu mtoto, ni mkubwa. Na Nanaa amepoteza maji mengi. Akitoka tu hapo kitandani, ipo hatari ya huyo mtoto kutoka. Ni lazima apate total bed rest. Tena ya hapa hospitalini wala si nyumbani.” Daktari akasisitiza.

“Basi tutamleta mchungaji hapa hapa atufungishe ndoa.” “Hapana Geb. Tusubiri tu. Mimi ndoto zangu tokea zamani ni kusimama kanisani nikiwa nimevaa shela ndefu. Sio nikiwa hapa kitandani tena hospitalini! Hapana.” “Unaweza kabisa kuvaa shela ndefu ukasimama na tukafunga ndoa hapa hapa pembeni ya kitanda. Mimi nataka kukuoa.” “Hapana Geb. Sio hapa. Kama unataka kunioa mimi, basi subiri.” “Nasubiri mpaka lini Nanaa? Nimesubiri vya kutosha. Hatuwezi kuahirisha tena. Oliva amezaliwa bila ndoa na Magesa pia aje akute nacheza michezo ya kihuni!

Hapana Nanaa, tunaoana.” Nanaa na Geb wakaendelea kubishana palepale mbele ya yule daktari na nesi anayemsaidia Nanaa.

“Haya ndio moja ya mambo ambayo itamlazimu Nanaa ajitenge nayo.” Wote wakanyamaza. “Itawalazimu kuhakikisha mnafanya kwa upande wenu na sisi kwa upande wetu ili kuhakikisha tunafikia lengo.” Daktari alijaribu kuzungumza nao kiuungwana. Mama G akaingia na mtoto wao. Bila salamu Geb akamchukua mtoto wake na kutoka. Mama G akabaki na mshangao. Daktari naye akaaga na kutoka. Nitarudi tena jioni kukuangalia. “Asante sana.” Nanaa akashukuru.

~~~~~~~~~~~~~

“Haya, kwema? Maana naona nimenyang’anywa mtoto bila salamu.” Mama G akauliza. “Kakasirika.” “Nini tena?” “Eti mama, Geb anataka tufungie ndoa hapa.” “Kwa nini?” “Ndio ushangae sasa!” “Hapana Nanaa. Nauliza kwa nini mfunge ndoa hapa na si kanisani?” Mama G hakuwa anataarifa na kinachoendelea. Nanaa akamsimulia majibu ya vipimo vyote. “Kwa kifupi Magesa ni mzima. Lakini nimeambiwa ni mrefu sana na mzito ndio maana nilikuwa nasikia sana maumivu.

Hapa sitoki mama mpaka mtoto atimize siku zake, azaliwe. Au angalau amalize hii miezi 8 yote. Ikishindikana na pressure ikikataa kushuka, wanamtoa.” Mama G akakaa.

“Sasa mbona husemi kitu?” Nanaa akamuuliza mama G. “Nafikiria.” “Nini?” “Geb hakiwezi kile chumba bila wewe. Inamaana mtakaa hapa kwa karibia mwezi mzima!” Nanaa akanyamaza. “Geb anakupenda Nanaa. Anakupenda sana. Hakuna sababu utakayompa asikuoe wewe au asiwe karibu na wewe, akaridhika. Shida yake kubwa ni kuwa na wewe. Hafikirii kama akikuoa hapa hatavaa suti au hatafika ukumbini kwenye sherehe. Shida yake ni kukufanya uwe wake. Basi.” Nanaa akaanza kulia.

“Jipeni muda wa kufikiria. Msiharakishe majibu.” “Ndoto zangu ni kuvaa shela ndefu kama ile aliyoninunulia Grace, mama. Nataka na mimi kusimama kanisani. Nikiolewa hapa, ndio basi. Nitakuja kuolewa tena lini?” Nanaa aliendelea kulia. “Naomba utulie Nanaa. Umeniambia pressure bado ipo juu. Lazima utulie ili ishuke. Isiposhuka watamtoa huyo mtoto. Si ndivyo ulivyoambiwa?” “Sasa nitafanyaje mama? Sitaki kumuumiza Geb, na mimi natamani kutimiza ndoto yangu!” “Hizi habari ndio mmepewa sasa hivi. Mambo mengi yanapita kichwani kwenu. Maisha yenu yatabadilika kwa mwezi mzima, kitu ambacho sio wewe wala Geb aliyetarajia. Mnahitaji muda. Naomba tulia kabisa. Geb alinitumia masharti yote ya vyakula unavyotakiwa kula kuanzia sasa. Nimeleta uji, Grace ataleta chakula baada ya muda mfupi tu. Kunywa uji ulale.” “Nataka kumnyonyesha kwanza Liv.” Mama G akasimama na kutoka. 

~~~~~~~~~~~~~

 “Nanaa anataka kumnyonyesha huyo kabla hajalala.” Geb akamkabidhi mtoto mama yake. “Niangalie mimi Geb.” Geb akageuka. “Nataka ujijibu haya maswali. Unamtaka mtoto wako azaliwe salama? Maana maombi peke yake hayatatosha kama usipokubali kutenda kazi na Mungu. Lazima. Nasisitiza, ni lazima ufanye mazingira matulivu kwa Nanaa ili mpate mtoto wenu.” “Nanaa hataki nimuoe mama.” “Tangia unazaliwa mpaka sasa, sijakuona ukitaka kitu. Na ukamshirikisha Mungu, ukashindwa kupata wewe Geb Magesa. Mwambie Mungu haja ya moyo wako. Weka hasira pembeni. Mtunze mwenzio. Namfahamu Nanaa. Mtafikia tu muafaka. Nanaa ni muoga sana wa ugomvi. Ndio maana jana ulipomgombeza tu kidogo, tayari pressure imempanda. Ukitaka atulie, ni akuone na wewe umetulia.” Geb alipata faraja ya namna yake. Akajisikia ametulia kabisa.

~~~~~~~~~~~~~

Wakarudi chumbani. Geb akamsogelea          Nanaa.“Samahani.Nahisi nimepaniki.” Nanaa akamuonea huruma. “Na mimi nataka unioe Geb!” “Najua. Naomba upumzike. Tutapanga kila kitu pamoja, baadaye. Sasa hivi naomba upumzike.” Nanaa akajisikia na yeye furaha. “Asante.” Wala hakunyonyesha tena, hapo hapo akalala. Usiku walipobaki peke yao Nanaa akaanza.

“Geb!” Geb alikuwa akila pembeni. “Vipi?” “Asante kwa kuwa hapa na mimi.” Geb akasimama. “Hakuna sehemu natamani kuwepo isipokuwa wewe ulipo Nanaa. Nakupenda.” Ilimgusa sana Nanaa. “Basi naomba unioe tu.” “Na shela?” Geb akauliza. “Naweza kusubiri Nanaa. Hamna shida.” “Moja ya ndoto zangu nyingine ni kuolewa na mwanaume anayenipenda. Maadamu nimekupata wewe, naona nisiendelee kusubiri. Acha tuoane tu.” Geb akainama na kumbusu. Alimbusu kwa muda mrefu bila kupumzika.

“Asante Nanaa. Na samahani. Nina tatizo la kupanga mambo yangu. Baada ya kushindwa kukuoa wakati ule, nikamuomba Mungu anisaidie niweze kukuoa kwenye siku yangu ya kuzaliwa. Na kweli Mungu akafanya hivyo. Naomba iwe hivyo. Kwangu inamaana kubwa sana. Sitajali utaonekana vipi mpenzi wangu. Nakutaka wewe. Naomba tukamilishe hili. Nakuahidi tutafanya sherehe mara baada ya Magesa kuzaliwa.” Nanaa akatingisha kichwa kukubali huku akifuta machozi. “Asante. Basi nitazungumza na uongozi wa hospitali kama tunaweza kufunga ndoa yetu siku hiyo. Sitataka watu wengi sana. Ni familia yetu na marafiki zetu wa karibu. Basi.” Nanaa akatabasamu baada ya kumuona Geb amechangamka.

~~~~~~~~~~~~~

Ndugu zao ndio walikuwa wametoka hapo. James, Danny na familia yake yote, Mama G na Oliva. Na wote wakajua Nanaa hatatoka hapo mpaka ajifungue. James alipouliza swala la ndoa, hakupata jibu. Kila mtu akanyamaza. Lakini baadaye Nanaa alimwambia kaka yake yeye ameamua kusubiri mpaka ajifungue. Kwa hiyo wote waliondoka tena na taarifa kuwa harusi hiyo inaahirishwa tena.

~~~~~~~~~~~~~

Geb akampigia simu James wa kwanza. “Tutafunga ndoa hapahapa hospitalini. Kesho nitazungumza na uongozi wa hospitali tuone watakachosema.” Akamsikia James anacheka. “Daah! Umegoma kusubiri?” “Hapana aisee. Acha nioe James. Mtoto wa pili huyu! Wote watakuja kujua ni kama sikuwa na malengo kabisa bwana! Halafu Dume langu linakuja! Anakuja anamkuta baba yake hajaoa! Sio sawa. Nitakuwa siweki mfano mzuri. Nilishakosea tokea mwanzo, basi maadamu Mungu ametupa neema, acha niitumie vizuri. Nisiendelee kukosea. Naomba baraka zako. Utuunge mkono katika hili tafadhali.” “Tupo pamoja.” Hata James alisikika akiwa

amefurahia.

“Nani atawasimamia sasa?” James akauliza. “Wale wale. Nitaongea na Malii kama bado wanaweza kutusimamia yeye na mkewe hapahapa hospitalini. Naona ndiye rafiki wa kweli niliyebaki naye na angalau tunaendana.” “Sidhani kama Malii atakataa. Kwa umbali tuliotoka naye, lazima atasimama na wewe, popote. Labda tatizo lije kuwa mkewe.” James akatahadharisha. “Nitazungumza naye kesho, tuone. Lakini sidhani kama kufungia hapa hospitalini itakuwa kikwazo kwao.” “Sidhani. Wewe wasikilize. Kila la kheri.” James akatoa baraka zake. “Asante. Sitakuwa na watu wengi. Ni ndugu tu. Nanaa akijifungua, ndipo tutafanya sherehe na marafiki, kumshukuru Mungu. Kwa hiyo kama mama na kina Viola wangependa kuhudhuria hapa hospitalini siku hiyo nikimuoa Nanaa, wakaribishe tafadhali. Naweza kuwatumia dereva akaenda kuwachukua.” James akanyamaza kwa muda. Geb akaona aage. “Siku njema.” “Asante na wewe.” Wakakata simu.

~~~~~~~~~~~~~

Mama yake akawa wapili kupigiwa. “Naoa mama!” Mama G akaanza kucheka na kupiga vigelegele. “Subiri kwanza mama. Nisikilize.” “Niache nifurahie kwanza. Usinikere wewe mtoto!” Mama G akaendelea kupiga vigelegele. “Si usikilize kwanza ndio uendelee kusherehekea?” “Usianze kunipa masharti ya hiyo harusi Geb. Maana wewe nakujua.” “Hatutaki watu wengi mama. Ni ndugu tu.” “Hee!” Mama G akashangaa.

“Nanaa akishajifungua ndipo tutafanya sherehe na utaalika watu wote unaotaka wewe. Lakini sasa hivi ni familia tu kwa kuwa tutafungia hiyo ndoa hapa hapa chumbani. Naomba usubiri.” Nanaa akaanza kucheka. “Yaani huo ni msamiati wa kichina kwa mama G. Hawezi hata kidogo. Wewe msikilize tu umsikie. Alivyopania hiyo harusi!” Nanaa aliongeza akiwa anawasikiliza.

“Kwa nini mfungie ndoa chumbani? Kwani Nanaa yupo mahututi? Usiniharibie shuguli kabisa!” Geb akajua tayari ameshapokonywa shuguli nzima. “Sasa wewe ulitakaje?” “Nitakuja mwenyewe kesho kuzungumza na uongozi wa hospitali.” Geb akashangaa. “Mama!” “Kumbe! Wewe unafikiri hawana kumbi za kufanyia mikutano hapo? Unataka mashoga zangu wakose harusi?” “Si watahudhuria sherehe baadaye!” “Nataka wahudhurie vyote. Ndoa na sherehe. Sasa wewe niachie kila kitu.” Akamsikia anaanza kupiga vigelegele tena.

“Huna utakalomwambia mama akaelewa juu ya hiyo harusi. Wewe mwache tu.” Nanaa akaongeza. “We Geb!” Geb akamsikia mama yake akimwita. “Nipo mama.” Geb akaitika. “Tena nitataka kuonana na huyo daktari wa Nanaa. Aniambie masharti yote juu yake. Ukaaji wake na..” “Mama, Mamaa!” Geb akaita. “Nini?” “Nilishazungumza na daktari. Nanaa anatakiwa alale asikae.” “Wewe niwekee miahadi na huyo daktari. Nitakuja kuzungumza naye mwenyewe. Wewe vipi bwana!?” Akaendelea kupiga vigelegele kwa muda. 

“Ngoja nimpigie Grace sasa hivi, ili tujue tunafanyaje?” “Juu ya nini mama? Acha hii iwe ndogo tu!” “Naomba usinipangie kitu cha kufanya kwenye harusi ya mwanangu. Wewe angalia swala la ugonjwa, basi. Mimi na Grace tutajua maswala mengine.” “Nilitaka kumpigia mimi kwanza ili nimtaarifu.” “Kwani mimi nimekuzuia nini? Mimi nampigia na maswala yangu na wewe mpigie na yako.” Akaendelea kupiga vigelegele. “Naomba yasiwe maswala mengi mama. Kumbuka hapa ni hospitalini.” Geb aliongea akisikika kuishiwa nguvu, akamsikia mama yake amekata simu. 

“Daah!” Geb akabaki na mshangao. Nanaa akazidi kucheka. “Nilikwambia mimi.” “Yaani shuguli nzima ameipora yeye! Ishakuwa shuguli yake yeye, mwenye mtoto. Kesho anakuja kuzungumza na uongozi wa hospitali na daktari wako! Anataka marafiki zake wote wawepo. Tena isifanyikie hapa! Hiyo ndoa anataka ikafungwe kwenye ukumbi.” Geb alikuwa akieleza huku ameshikilia simu yake haamini.

“Nilijua tu. Mama hana dogo.” “Najuta! Heri yeye ndio ningemfanyia surprise.” Geb aliendelea kuwaza. “Na hapo mama Magesa huna utakachomwambia tena. Kashashika usukani kwenye shuguli nzima. Utamsikia akitaka umlipe pesa yake tu.” Nanaa alizidi kucheka. “Sio kwamba anakuomba kwanza?” Nanaa akauliza. “Umcheleweshe kwenye mipango yake? Hathubutu. Atanunua vitu vyote anavyotaka kwa pesa yake, baadaye ndio anakuletea risiti umlipe pesa yake. Subiri utamuona. Kesho tu, risiti zake zitaanza kuingia hapa. Hajuagi kusubiri kwenye mambo yake. Akipanga mipango yake leo, ujue inaanza hapo hapo.” Nanaa alizidi kucheka.

“Kanikatia simu ili yeye ndio awe wa kwanza kumwambia Grace! Namwambia asubiri kwanza, hataki. Mama! Tena anasisitiza eti mimi nisimuharibie shuguli!” Geb aliendelea kulalamika huku akishangaa. “Hana jambo dogo hata iweje. Wewe muache tu afurahie. Ni siku yake.” “We Nanaa!? Siku yake au yangu mimi na wewe?” “Si ndio amekwambia yeye ndio mwenye mtoto?” “Daah!” Geb akavuta kiti na kukaa pembeni ya Nanaa.

~~~~~~~~~~~~~

 “Asante Nanaa.” “Asante ya nini tena?” Nanaa akauliza huku akijiweka sawa. “Kukubali kuweka matakwa yako pembeni, na kuolewa  ukiwa hapa. Nimefurahi sana.” Nanaa akamwangalia Geb. “Unahitaji msaada wa kiroho, Geb. Wewe ni mtu gani huwezi kubadilika hata kidogo!?” Geb akacheka. “Eti siku nzima umepooza hata kuongea, huongei kwa kuwa huoi siku uliyopanga wewe!” “Magesa hawezi kuja akakuta baba yake bado sijaoa, Nanaa! Ni fedhea ilioje!? Halafu eti aje ajue yeye ndio alisababisha! Unataka mwanangu ajilaumu?” “Unajua kufikiria mbali wewe! Mimi hilo wala sikuwaza.” “Ndio hivyo. Wanangu watakuja kuniona baba muhuni. Eti Magesa.” Akamshika Nanaa tumbo na kumbusu.

“Utavaa suti yako?” Nanaa akamuuliza. Geb alikuwa amefurahi sana mpaka uso ulionyesha. “Kabisa. Naoa mwenzio. Lazima nivae suti.” Nanaa akacheka kidogo na kufikiria. Geb akamuona. “Vipi? Unataka kubadili mawazo nini?” “Hapana. Nafikiria tu.” “Nini?” Geb akamuuliza na kumbusu kwenye kipanda uso. “Ningumu kuyatabiri maisha. Sikujua kama nitapata mtu anayenipenda na kutaka kunioa kwa kiasi hiki! Haya, nilipokupata, sikujua kama nitafunga ndoa hospitalini.

Tena nikiwa nimelala kitandani!” “Unajuta?” “Hapana Geb. Hata kidogo.” Nanaa akatulia kwa muda.

“Mchana nilipomwambia kaka kuwa nitasubiri mpaka nijufungue, nilikuona vile ulivyohuzunika. Sio kukasirika kama jana. Nikakusikia ukiongea na Grace ukimwambia umekubaliana na mawazo yangu, utasubiri mpaka nitakapokuwa tayari. Lile neno likaniingia sana. Nikajiuliza ni ‘lini nitakuwa tayari?’ Nikakumbuka ni miezi michache tu iliyopita, nilikuwa hapahapa hospitalini. Kasoro chumba tofauti. Nikiwa nimeoza miguu. Na bado ulikuwa na mimi ukitaka kunioa vile vile.” Nanaa akaanza kulia.

“Maisha yangu yamekuwa hayatabiriki Geb. Lakini mapenzi yako kwangu hakika ni ya halisi. Unanipenda kwa dhati tena bila sababu. Wakati wote unasisitiza unanipenda mimi vile nilivyo, hujali ninaonekana vipi. Sina sababu yakunifanya usinioe Geb. Kama ni gauni lenye shela ndefu, nitalivaa hata hapa kitandani tu. Sitajali tutakapofunga ndoa, ilimradi wewe upo, na ndiye utakayeapa mbele ya Mungu utanichukua kama mkeo, hadi kifo! Hiyo itatosha kwangu. Nakushukuru.” Geb akasimama na kukumbatia pale pale alipokuwa amelala.

  ~~~~~~~~~~~~~

Walikumbatiana kwa muda, mabusu yakafuata. “Docta amesema hakuna mapenzi Geb. Niache.” Geb akahema kwa nguvu na kumuachia. “Daah! Hali mbaya.” Nanaa akamcheka. “Amesema mpaka lini tena?” “Nijifungue!” Nanaa alijibu huku anacheka. “Daah!” Geb alilalamika. “Sasa fungate tutafanya nini?” Nanaa akauliza.

Geb akarudi na kukaa kwenye kiti. “Tutarudi hapa baada ya kila mtu kuondoka. Tutapata muda wa kumshukuru Mungu. Siku tatu mfululizo, sitawasha simu wala kompyuta. Sitaenda kazini hata kidogo. Tutakuwa wote siku tatu mfululizo. Mimi na wewe tu.” “Na madaktari na manesi.” Nanaa akaongeza. “Na hao basi. Tutapata muda mtulivu wa kuzungumza. Hapo ndipo utapata nafasi ya kumfahamu mumeo vizuri. Ndani na nje. Maswali yako yote, yatapata majibu ya wazi na kina. Utapata nafasi ya kushauri chochote katika yote tutakayozungumza. Nitahakikisha baada ya hizo siku tatu, tunakuwa kitu kimoja. Kimwili, kiakili na kiroho tunakuwa pamoja. Mtu akikuona wewe, anakuwa amemuona Geb Magesa.” Nanaa akacheka.

“Unacheka tena?” “Hapo haiwezekani Geb.Nimewasikia watu wakinong’ona siku ile pale kwenye kikao cha Zena.” “Juu ya nini?” Geb akauliza. “Haupo kama ninavyokujua Geb. Wewe sio mwenzangu hata iweje.” “Kivipi Nanaa!?” “Walikuwa wakisema wewe ni milionea wa hapa mjini.” Geb akacheka. “Wewe hufahamu watoto wa mjini. Wanakuza kila kitu.” “Jeff anafanya kazi benki. Alisema anahusika na moja ya akaunti zako.” Geb akacheka kidogo. “Yaani dakika moja niliyokwenda kukununulia chakula, tayari waliongea kila kitu!” “Wewe hukuona walivyokuwa wakituangalia?” “Walikuwa wakikuangalia ulivyopendeza bwana!” Nanaa akampiga ngumi kidogo.

“Umoja wetu hautakuwa na mipaka Nanaa. Yale yote Mungu aliyonibariki mimi, yatakuwa ni yako pia. Na yale yote Mungu aliyokubariki wewe, tutayashiriki pamoja. Au unafikirije?” Tayari machozi yalishakuwa yakimtoka Nanaa. “Si ndivyo hivyo?” “Mimi sina hata kitu Geb! Utanufaika kwa lipi?” “Sina pesa inayoweza kumnunua Oliva na Magesa. Pesa sio kila kitu Nanaa. Umenipa nyumba yenye amani na utulivu. Una upendo wa dhati kwangu. Unanifikiria. Umetulia. Mwaminifu kwangu. Hivyo vyote vinathamni kuliko pesa, mpenzi wangu. Na huwezi kuvinunua, hata uwe tajiri wa namna gani. Wewe sio mwanamke wa kwanza kuwa na mimi. Lakini wewe ni mwanamke wa kwanza kunivumilia na kunipenda.” Geb aliendelea.

Vya Sirini Vikiwekwa Mwangani Haibakii Kama Ilivyokuwa.

 “Sitasahau jinsi ulivyeweza kunisubiria kwa uchungu wakati nalala na Liz, chumbani kwangu wakati na wewe upo palepale! Nilikuwa najisikia vibaya. Sikuwa na jinsi. Halafu mama akawa ananiambia vile ilivyo hatari ya kuendelea kuchelewa kufanya maamuzi. Akawa anazungumza kwa mafumbo. Lakini nilielewa kuwa ulikuwa una watu wanao kutongoza mbali na Zinda na Jeff. Nilijua kuna wanaume wengine ulikuwa ukienda kukutana nao, Nanaa.” Nanaa akashituka kidogo. Akataka kukana.

“Nilikuwa najua Nanaa.” Nanaa akanyamaza. “Kuna siku ulitoka mapema kidogo kazini. Ilikuwa siku ya ijumaa. Ulibadilisha nguo ofisini tena baada ya kumuaga Grace. Ulifuatwa na mwanaume alikuwa na gari ndogo, nyeupe. Ulivaa gauni fupi mpaka kwenye magoti. Lilikuwa la rangi nyeusi. Lilichanua kuanzia chini ya maziwa. Ukabadili na aina ya nywele. Vile ulivyokuwa umebana asubuhi wakati unaenda kazini, haikuwa kama ulivyotoka. Ulibadili na viatu. Ukavaa viatu vya wazi, lakini vilikuwa vya juu kidogo. Halafu ulitokea mlango wa nyuma. Stoo. Kama ambaye hukutaka mtu akuone. Kwa kuwa hata nguo ulibadili baada ya kumuaga Grace.” Nanaa alishindwa hata kumwangalia Geb.

          “Nilipomuuliza Grace unakwenda wapi, akaniambia hajui, lakini ulimuomba ruhusa tangia saa 6 mchana. Nilijiuliza ni wapi unakwenda ambako ilikulazimu uvae vile na usitake mtu akuone! Nilijua kama umebadili nguo kwa kuwa nilikuona wakati unatoka nyumbani asubuhi. Halafu nikakuona wakati unatoka ofisini na kupanda gari ya yule Jamaa. Na mimi nilikuwa nimefika pale ofisini. Lakini sikuwa nimeshuka kwenye gari. Nilikuwa nikizungumza na mtu kwenye simu ndani ya gari.” Nanaa akanyamaza. 

“Unakumbuka?” Geb akamuuliza. “Lakini sikuchelewa kurudi nyumbani.” Nanaa akajitetea. “Sawa sawa. Hukuchelewa hata kidogo. Ulirudi nyumbani muda ule ule unaorudi na Grace. Kama mliingia tu pamoja. Lakini ulirudi nyumbani ukiwa umevaa tena nguo zile zile ulizokuwa umevaa asubuhi wakati ukienda kazini na ukarudishia mtindo wa nywele vile vile kama asubuhi. Ulinikuta nje, ukashindwa hata kunisalimia kama kawaida yako. Ukapita kwa haraka, ukaingia ndani. Ulisema kichwa kinakuuma, hukuweza hata kula. Ukalala mpaka asubuhi.” Geb alikuwa na hicho kitu moyoni. Hakuwa amemwambia mtu yeyote yule. Akabaki nacho huku akiumia tu. Wakati huo na yeye alikuwa na Liz.

“Nilijaribu kumuuliza mama kwa makini ili asijue. Lakini nilitaka kujua kama alijua kama ulitoka na ulikwenda wapi. Lakini mama alionyesha hajui naongea nini na alisema siku hiyo hamkuzungumza kabisa. Alipokupigia simu mida ya jioni, hukupokea kitu ambacho sio kawaida yako. Lakini ukamtumia ujumbe kuwa upo sehemu hutaweza kuzungumza. Utampigia baada ya muda mfupi. Hukupiga ila saa 12 kamili ukawa unaingia getini.” Nanaa alibaki kimya.

~~~~~~~~~~~~~

Mwanzo wa Geb ulikuwa mzuri sana. Nanaa hakutegemea kama ataishia hapo. Nanaa alipanga hiyo safari kwa siri sana. Hakuwa hata amemwambia mama G mshauri wake. Siku hiyo aliamua kufanya kile akili yake imemtuma. Hakuchelewa kurudi, na wala hakukosea kurudi nyumbani na nguo za tofauti na zile alizokuwa ameondoka nazo. Muda wote aliokuwa na Geb, hakujua kama amebeba hilo jambo moyoni. “Sasa atakuwa amebeba mangapi?” Nanaa akajiuliza.

~~~~~~~~~~~~~

 “Najua sikuwa na haki ya kuumia au kuona wivu. Lakini nilishindwa kulala Nanaa. Swali la ulikuwa wapi ambako uliweza kuwa huru kubadilisha nguo na kurudisha nywele vile zilivyokuwa asubuhi, ndilo lililokuwa likinitesa sana.” Kimya. “Nanaa?” Geb akamwita. “Abee!” “Tunakaribia kuanza maisha mapya. Si sawa kuanza kuwa na siri kati yetu. Najua hili lingeweza kusubiri, lakini nataka tuingie kwenye ndoa wote tukiwa kwenye ukurasa mmoja na tukiwa na amani. Nataka kujua ukweli.” Nanaa alitamani asingezungumzia hicho kitu. Hakutaka mtu ajue kabisa. “Nataka kujua ulikuwa wapi na ulikuwa na nani?” Geb alisisitiza kwa utulivu bila jazba.

 “Naomba uniamini, siku ile hakuna kilichotokea Geb.” Geb akakunja uso. “Sivyo nilivyokuuliza Nanaa. Nataka kujua ulikuwa wapi na ulikuwa na nani. Basi.” “Naomba tusizungumzie hicho kitu Geb. Tukiache kama kilivyo. Lakini naomba uamini hakuna nilichofanya.” “Mbona unanitia wasiwasi!?” “Tafadhali Geb. Naomba tuyaache kama yalivyo. Nakuomba. Tafadhali sana. Naomba maisha yetu tuliyoishi zamani, kama hayatatuathiri sasa hivi, basi tuyaache kama yalivyo. Tuanze upya mimi na wewe.” Nanaa alisisitiza.

“Tunaanzaje upya kukiwa na maswali ya nyuma ambayo hayataki kupewa majibu?” “Geb! Najua huna asili ya kutaka kupitwa na mambo. Lakini katika hili, nakusihi acha tu.” “Naachaje Nanaa!?” “Wewe unataka kuibua mambo ambayo hayaleti amani hata kidogo.” “Labda hujaelewa Nanaa. Hili jambo nimejaribu kulisahau lakini limekuwa likinisumbua sana. Kwa kifupi hiyo amani unayozungumzia, haipo. Na sitaki tuingie kwenye ndoa katika hali hii. Kwangu ndoa sio mchezo. Ni kweli tutakuwa mwili mmoja. Nataka iwe hivyo kiukweli. Nimekwambia utanifahamu kwa asilimia 100. Watu wakikuona wewe, watakuwa wakiniona mimi. Nitajifunua kwako kwa asilimia zote.”

“Sasa na wewe huoni kama unahitajika kufanya hivyo hivyo? Huoni kama haitakuwa sawa, eti mimi unifahamu mambo yangu yote. Mpaka wanawake niliokuwa na mahusiano nao, halafu nikupe ruksa ya kuniuliza tena chochote! Na ahadi ya kukwambia ukweli, halafu wewe ukatae kujibu swali kama hilo? Ni nini unaficha ambacho ni cha hatari sana!?” Nanaa alitamani hilo lipite tu. Lakini Geb alionekana halitaweza kupita kamwe. 

~~~~~~~~~~~~~

Zikiwa zimebaki siku chache sana za kutimiza ndoto zao, Geb ana ibua siri kubwa sana iliyokuwa imefichwa na kuendelea kufichwa Nanaa. Hata mama G, msiri wake hakuwa amemwambia. Hakutaka mtu ajue. Kumbe Geb analo

moyoni. Leo anataka ukweli kwa Nanaa ambaye presha inamsumbua.

Tena yupo hospitalini.

Nini kitaendelea?

Nani alikuwa na Nanaa?

Geb & Nanaa wataweza kufuata masharti ya daktari kusaidia kuzaliwa mtoto aliyekomaa huku wakiwa wamejawa wivu, hasira na Kutojizuia?

Hapo nyuma vikwazo vilikuwa vinatoka NJE. Walimudu. Sasa ni wao wenyewe.

Itakuaje!?

 Usikose muendelezo…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment