Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! – Sehemu Ya 46. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! – Sehemu Ya 46.

James, Zinda na kina Vai waliondoka nakuacha wote wamepigwa na butwaa. Hakuna aliyekuwa akiamini jinsi mambo yalivyojiweka pamoja. Palizuka ukimya kila mtu akiwaza lake. “Jamani, naombeni msimwambie Nanaa juu ya ahadi ya Zinda kutokea kesho kanisani. Asije akavunjika moyo kesho endapo Zinda hatatokea. Ikitokea anakuja ni sawa. Lakini asipokuja pia ni sawa. Nanaa yupo katika wakati mtulivu. Sitaki tena kumrudisha nyuma na kujiona anapungukiwa kitu.” “Sawa. Lakini mimi nilazima niwahi asubuhi pale kanisani Geb. Inamaana nitaondoka kabla yenu. Nanaa atakuuliza tu. Hajazoea kuona jumapili naondoka peke yangu. Utamdanganya?” Mama G akauliza. 

“Mimi mwenyewe nitajua jinsi ya kuzungumza naye.” “Basi mjitahidi kuamka mapema mumuandae na mtoto. Mnamjua Oliva anavyopenda usingizi wa asubuhi. Lazima mumtoe kitandani mapema ili achangamke, ale. Lasivyo mtakuja naye hajala na amevaa nguo zake za kulalia. Nitaandaa nguo zake za kanisani tayari kabisa. Hapendi..” “Mama! Mama G! Atakuja Liv ameoga na amevalishwa nguo utakazo.” Geb alimkatiza mama yake.

“Bwana nyinyi hamtabiriki bwana! Mnaweza kulala mkapitiliza muda. Mkaniletea mtoto mchafu.” “Wewe usiwe na wasiwasi.” “Lazima niwe nao. Nawafahamu wewe na Nanaa. Hamuwezi kutoka huko chumbani kwenu kwa haraka.” Grace na Danny wakaanza kucheka.

“Jamani! Na sisi tunaondoka. Tutaonana kesho.” Danny akaenda kuchukua wanae chumbani walikokuwa wamelala akaanza kuwapandisha kwenye gari mmoja baada ya mwingine mpaka alipomaliza ndipo akaenda kumwamsha na dada yao anayewasaidia kazi, wakaondoka.

Mama James

Mama James hakutaka kupotezewa muda. Walipotoka tu pale kwenye kikao, akatembea mpaka kituoni, akaenda kupanda daladala kuwahi wateja wake. Alijua kabisa ugomvi utakao kuwa ukiendelea ndani ya gari ya Zinda. Kwani alimuacha Vai na Viola, wakipanda gari ya Zinda. Akajua huo ugomvi humo ndani ya gari, unaweza kumchelewesha kwenye shuguli zake. Akamwachia Zinda ahangaike nao. Akimkuta Vai nyumbani, atajua ameachwa. Asipomkuta atajua Zinda alimchukua.

James.

James alipohakikisha wanatoka tu getini na mlinzi amefunga geti dogo, na yeye akapanda gari yake akaondoka. Hakutaka kujua wanapoelekea wala kinachoendelea. Aliwapita hapo getini na akamuona mama yake anatembea kufuata daladala, lakini hakusimama. Akaamua arudi tu kwake, akapumzishe akili zake. Kwa muda mfupi aliokuwa nao walishampa habari mbaya tupu. Aliondoka pale akimlaumu sana mama yake. Amehusika kwa asilimia zote kuharibika kwa dada zake. Walipo vile kwa umri ule, hawana elimu yeyote na wala hawawezi kuwekwa ndani kama Nanaa na kuwa wake. Hawajui kuzungumza. Hawana adabu. Shule hamna kichwani. Hawana ustaarabu. Hawajui kazi na wazi kabisa wanaonekana ni binti ambao hawajatulia. Wasichana wazuri lakini hawana maadili. Na ndio siku hiyo na yeye James akajua kuwa mdogo wake, Vai alitoa mimba na kuoza karibia kifo! James aliumia sana. Aliondoka pale asijue hatima ya hao dada zake. Alishaishi nao, lakini akashindwa kuwasaidia.

Zinda & Vai

Zinda aliwatoa hapo hao mabinti wawili akiwa amekusudia kabisa kumtoa Vai kwenye maisha yake. Kwanza alishajua hatazaa. Mapenzi ya kitandani pekee hayatamsaidia kitu. Vai hajui kupika wala kusaidia usafi! Vai hataki ndugu! Zinda akawa ameshapata majibu yake yote usiku ule. “Vai hawezi kuja kuwa mke wangu! Uzuri huo hautanisaidia chochote. Utageuka kama mwiba kwangu.” Zinda aliendelea kuwaza wakati akikanyaga mafuta. 

Vai akashangaa wanaelekea nyumbani kwao. Alipokuwa akiishi zamani na mama yake na Viola. Alikuwa amekaa kiti cha mbele. “Umeamua kumrudisha kwanza Viola?” Vai akamuuliza Zinda kwa upole. Alishangaa walivyokuwa wametulia garini. Hawakuwa wakitukanana tena. Kimya. “Zinda?” Vai akauliza tena. “Tafadhali naomba nyamaza. Nyamaza hata kwa dakika chache niweze kufikiria. Unaongea sana Vai, mpaka unanifanya siwezi kufikiria!” “Mbona nimeuliza tu?” NIMEKWAMBIA NYAMAZA! Zinda aligomba kwa sauti kubwa sana mpaka wakaogopa.

“Wewe ni mtu gani huambiliki? Eti Vai? Itakugarimu nini kumsikiliza mtu kidogo tu, na kutii bila kujibu kitu?” Kimya. Zinda aliendesha mpaka nyumbani kwao. “Naombeni mshuke wote.” “Na mimi!?” Vai akauliza kwa upole. “Naomba ushuke Vai. Vitu vyako nitampa kaka yako akuletee.” “Nitabadilika Zinda.” Vai akaanza kulia.

“Nimekusudia kuanzisha familia Vai. Nataka watoto na wewe unaonekana umechezea sana kizazi chako. Huna uwezo wakuzaa.” “Viola amekudanganya.” “Mbona hujashika mimba sasa wakati tumeishi wote kwa miezi takribani mitano sasa?” “Ni kwa sababu nilikuwa nikitumia njia yakuzuia mimba.” Vai alijitetea. Hakuwa tayari kurudi kuishi tena hapo kwenye nyumba ya kupanga ya watu wengi. Kurudi tena uswahilini? Inamaana itabidi aanze kuishi na Viola na kina mama wa pale uswahilini. Mama yao alikuwa busy na baa yake. Kutoka asubuhi kurudi saa nane za usiku.

Kule kwa Zinda alikuwa peke yake na alikuwa akiachiwa pesa kila siku. Anakula atakacho. Anamlipa jirani kuja kumfanyia kazi. Kazi yake ilikuwa kulala akimsubiria Zinda. Leo aje kurudi kuishi na kina Viola tena! Uswahilini! Nyumba ya watu wengi! Hakuwa tayari.

“Njia ipi ya kuzuia mimba uliyokuwa ukiitumia?” Zinda akamgeukia na kumtizama kwa makini. Viola akaanza kucheka. “Mwambie sasa njia ipi ya uzazi wa mpango uliyokuwa ukiitumia kuzuia mimba!” Viola alishabikia. “Naomba utupishe Viola.” Zinda akamgeukia Viola aliyekuwa amekaa nyuma. Akataka ashuke kwenye gari yake. Kwani walikuwa wameegesha nje ya hiyo nyumba waliyokuwa wakiishi. Viola akashuka.

“Umeshanidanganya vyakutosha Vai. Naomba usiendelee kunidanganya. Mimi nilikupenda, nikaamua tuishi wote. Ni kweli wote tulikosa. Mimi nimekusudia kubadilika. Naanza upya bila kinyongo na mtu.” “Na mimi pia Zinda. Nitamuomba Nanaa msamaha. Nitatulia. Hayo ni maisha niliyokuwa nimeishi zamani. Nakuapia Zinda, nimebadilika mpenzi wangu. Tokea nimepata yale matatizo, sijarudi kulala na mwanaume tena. Yaani wewe ndio mwanaume wangu wa kwanza na wala sina tena mpango wa kujichanganya tena.” Vai akaendelea kujitetea.

“Sawa. Lakini tatizo litabaki pale pale Vai. Mimi ndio kaka mkubwa nyumbani kwetu. Nataka familia ambayo wewe huwezi kunipa. Huna uwezo wa kuzaa. Nilikuwa nikikuangalia na kukufuatilia kwa makini sana Vai. Tulifanya mapenzi kwenye siku zote za mwezi. Sijawahi kukuona hata ukipata siku zako! Inamaana walikutoa kabisa kizazi.” “Hapana Zinda.” “Wewe kaa chini jifikirie. Mara ya mwisho kuona siku zako ilikuwa ni lini?” Kimya. 

“Mimi nakufuatilia kuliko unavyofikiria Vai. Kwa kuwa mwenzio naishi na wewe kwa akili nikitaka uje uwe mke wangu kihalali. Lakini si kwamba huzai ila huna kizazi kabisa. Nilishajiuliza sana hilo swali. Inakuaje hupati siku zako? Mwanzoni nikajifariji labda umeshika mimba, lakini leo ndio Viola amenifungua macho. Huna kizazi Vai.  Tena si kwa kuwa umezaliwa hivyo au ni bahati mbaya! Hapana. Ni mambo uliyojitakia. Ni mchezo uliokuwa ukicheza na kizazi chako. Leo unataka na mimi nilipe garama ya maisha uliyoishi nyuma! Hapana Vai. Sitakuwa tayari kufanya hivyo. Siwezi kukuoa. Mwenzio ni lazima niwe na watoto. LAZIMA.” Vai aliumia sana.

Yalikuwa maneno makali ambayo Zinda aliyatamka bila kupindisha. Alijilaumu na kujuta hata kuanza kuishi na Zinda. Pengine kama sio kuanza kuishi naye angemuoa, swala la kuzaa wangelijua mbele ya safari! 

Zinda hakumumunya maneno. Mbele ya uso wake alimkataa. “Nakutakia maisha mema. Mizigo yako itakufuata hapa. Tafadhali usirudi pale kwangu. Nakusihi sana Vai. Tumeshachafuana vyakutosha. Tushapotoshana vyakutosha. Huwezi kuniongoza kwenye jema, na mimi nilishindwa kukuongoza kwenye jema. Wote tumeishi maisha ya kudanganyana tu na kuumiza wengine. Tafadhali shuka kwenye gari yangu.” Vai hakuwa akiamini kama yule ni Zinda aliyekuwa akihangaika kumpa penzi mchana na usiku. Tena wakati mwingine alijituma zaidi ya uwezo wake ili tu kumfurahisha. Leo Zinda anampasukia bila huruma wala aibu!? “Vai!” Zinda akamshitua. Vai akafungua mlango na kutoka. 

Zena Tena Kwenye Maisha Ya Nanaa.

Geb aliingia chumbani akamkuta Nanaa amejilaza kwenye kochi na tv ipo wazi. “Mbona hujalala?” Geb akauliza. “Si umesikia nimefukuzwa pale chumbani kwa mama?” Geb akacheka. “Kwa hiyo hapa navuta muda ili nichelewe kulala, usiku nisiamke.” “Ukiamka, niamshe mimi.” “Nakuonea huruma Geb. Unakuwa umechoka halafu wakati mwingine unatakiwa asubuhi kwenda kazini. Kama leo ndio siku yako ya kulala kwa kuwa huendi kazini na ibada ni saa 4 asubuhi. Naona heri ulale tu. Lakini mama najua hata mchana anaweza kurudi kulala kama asipoamua kwenda kazini.” Geb akakaa.

          “Sasa mbona na simu mkononi?” “Nilikuwa na chat na Zena. Wameamua kuona na Yasini. Wazazi wao wamewakubalia ndoa ya mahakamani. Wamemkubalia kuolewa na mkristo, lakini wamemkataza kubadili dini. Anasema walifanya kazi ya ziada mpaka kukubaliwa na wazazi pande zote mbili. Namuonea wivu!” Nanaa akaongea kwa unyonge. Geb akamtizama na kuamua kuuliza.

“Wivu wa nini?” “Amepata mwanaume anayempenda na anamuoa.” Geb akanyamaza. “Kesho ameniomba nihudhurie kikao chao cha harusi. Kila nilivyojaribu kumkatalia, kama unavyomjua Zena, hajuagi jibu la hapana. Ni nusu saa sasa tokea tuanze kubembelezana. Anasema amenitafuta sana bila mafanikio. Anasema alimuomba Jeff amlete mpaka pale tulipokuwa tukiishi zamani. Mlinzi akawaambia tumehama na hawezi kuwaambia tulipohamia. Alinipigia simu, hakunipata. Si unakumbuka nilibadilisha namba ya simu?  Ukasema nitoe mpaka Whatsapp? Nilitoa mpaka Facebook na Instagram. Leo nimekaa tu hapa nikasema nirudishe Facebook, ndio akaniona online akaanza kuninyeshea mvua za jumbe za kutaka nihudhurie kikao cha kesho.” Geb akabaki kimya anasikiliza.

“Mbona sasa husemi kitu?” “Nakusikiliza Nanaa.” “Nataka kesho kwenda na mimi kwenye kikao chao cha harusi.” Geb akabaki kimya. “Geb?” “Umesema unataka. Sasa sijui natakiwa kusema nini Nanaa! Ndio nakusikiliza. Maana unanipa taarifa. Sijui natakiwa kusema nini?” Nanaa akatulia kidogo. “Basi nimekosea kuongea mpenzi wangu. Nahisi ni kama nimechanganyikiwa, sijui!” “Nini chakukuchanganya?” “Naona wenzangu wote wanaolewa Geb. Mimi nimebaki…” Nanaa akasita kidogo.

“Halafu wote wanakazi! Wameajiriwa! Mimi nipo tu.” Nanaa aliongea kwa kulalamika. “Unataka na wewe kufanya kazi?” Geb akamuuliza taratibu tu. “Sijui! Naona nakaa tu bure. Hamna maendeleo yeyote yale! Nipo tu.” Geb alimjua Nanaa. Muda mfupi tu aliofungulia mtandao, tayari walishamchanganya. Alishapitia page za marafiki zake huko Facebook. Akaona hili na lile. Wengine wakijinadi wamesafiri kikazi nchi hii. Wengine wakionyesha pete za uchumba walizovalishwa na sherehe kubwa. Kuna waliomaliza nao chuo ameona picha zao wakiwa wanaolewa.

“Kama Natuja. Hakuwa hata na mchumba. Nimeona amepata mchumba. Amevalishwa pete ya uchumba. Wakafanyiwa sherehe kubwa. Mwezi uliopita ameolewa. Nimeona picha zao. Alipendeza kweli! Na akatuma picha zao za honeymoon. Sijui walienda wapi!? Lakini zilikuwa nzuri kweli. Zena ndio aliniambia niangalie. Na kesho nae atakuwepo kwenye kikao. Halafu kumbe na Tia naye amechumbiwa! Alipata kazi hapa hapa Dar. Anaishi hapa. Kesho pia atakuwepo kwenye kikao na mchumba wake. Tena nasikia amepata kazi nzuri tu. Yaani anatumia elimu yake na inamwingizia pesa yake.” Geb alibaki akimsikiliza Nanaa anavyolalamika na kujiona ameshindwa na kupitwa na kila mtu.

~~~~~~~~~~~~~

          Pete yake ya uchumba alivalishwa kitandani na Geb. Hapakuwa na sherehe yeyote ile. Wala hakuwa na kumbukumbu ya picha wakati anavalishwa. Alishasahau furaha aliyoipata siku alipoamka na kuikuta ile pete kidoleni mwake. Geb alipomtambua kama ni wake wa milele. Kwa muda mfupi sana alipowasiliana na Zena, akasahu wajibu mkubwa unaomkabili wakati huo. Nanaa alikuwa akiingiza pesa nzuri tu kila mwezi. Ni kama Geb alikuwa akimlipa mshahara bila yeye kujua. Alikuwa akimwambia ni pesa yake ya matumizi. Lakini kwa kiasi kile cha pesa kupewa kila mwezi, Nanaa ambaye hakuwa akinunua chakula wala kulipa kodi na garama yeyote pale ndani, pesa yote ile haikuwa ya matumizi tu. Ulikuwa mshahara kabisa.

Geb alifanya vile ili asijione tegemezi na kujikuta anamuomba pesa mara kwa mara. Alikuwa akimuwekea benki, na nyingine alikuwa akimletea nyumbani. Na bado hakuacha kumgaramia mahitaji yake binafsi. Lakini kama kawaida ya Zena. Aliweza kuingia kwenye akili za Nanaa, na kumshawishi vilivyo. Alijikuta muda wote aliokuwa akizungumza naye Zena alikuwa akimpa maendeleo ya huyu na yule, lakini akashindwa kujisemea chochote. Hakuweza hata kumwambia habari za Oliva na kama anatarajia mtoto mwingine na anaishi na Geb. Aliishia kumwambia, ‘nipo tu.’ Akaonea aibu kila kitu kinachoendelea kwenye maisha yake.

  ~~~~~~~~~~~~~

“Sio kama nalalamika. Nilikuwa nakwambia tu.” Baada ya mazungumzo ya ulalamishi na kugundua Geb ametulia akimsikiliza bila kuongeza neno, akaona atulie. “Zena anahabari za kila mtu. Kwa hiyo ni kama alikuwa akiniambia maendeleo yao.” Nanaa akaendelea. “Anasema hata Jeff naye anatarajia kufunga ndoa.” Akaendelea. “Halafu Jeff na Yasini walifungua biashara yao. Wanashirikiana. Anasema sasa hivi wanapesa sana. Biashara inawaendea vizuri, japo bado wameajiriwa. Ameniambia wakioana tu wanahamia kwenye jumba lao. Anasema Yasini alinunua jumba huko maeneo ya Mbezi beach. Yaani karibu kabisa na baharini. Ilikuwa ikiuzwa kwenye mnada. Nasikia mwenye nayo alishindwa kuilipia, yeye Yasini akainunua. Ipo kwenye marekebisho kidogo tu, wahamie. Anasema kuna mambo hawajayapenda kwenye hiyo nyumba ndio wameona wayabadilishe. Hasa vyumbani na jikoni. Wametafuta ‘contractor’ ndio anayewashugulikia. Hawakutaka hawa mafundi wa kawaida. Mwenyewe Zena anawaita ‘fundi njaa’. Wamekodi kampuni ya ujenzi kabisa ili kushugulikia hiyo nyumba yao.” Geb alibaki akisikiliza.

~~~~~~~~~~~~~

Geb mtoto wa mjini. Anajua pesa. Anajua maisha jinsi yalivyo. Alishaujua udhaifu wa Nanaa wakumwamini Zena hata anapomdanganya, haoni. Habari nyingi alizokuwa akieleza Nanaa pale, alizoambiwa na Zena, zilikuwa na maswali mengi sana, lakini si kwa Nanaa. Nanaa aliendelea kusifia huku akijiona yeye duni.

~~~~~~~~~~~~~

“Na amesema Yasini amemwambia ni kama wameanza nae maisha. Kwa hiyo kila kitu wanachonunua sasa hivi, kinaandikwa majina yao yote mawili. Kama hiyo nyumba, ni ya kwake yeye na Yasini. Wameshashugulikia hati ya nyumba. Ina majina yao yote. Yaani kila kitu chao wanachonunua, ni cha wote wawili. Anasema kasoro gari alilomnunulia ndilo ameandika jina la Zena tu. Ujue sijaamini Geb!? Zena mpanda daladala kama mimi, eti sasa hivi anaendesha gari! Tena gari yake kwa jina lake!” Nanaa akaendelea.

“Lakini wao wameanzia mbali. Si unakumbuka nilivyokusimulia juu yao? Alimkuta Yasini hana kitu. Kwa hiyo kwao wao nirahisi. Yaani kama ni vitu, wameanza kununua pamoja. Inakuwa rahisi. Hakumkuta Yasini na mali yeyote. Nafikiri ndio maana Yasini anamthamini sasa hivi. Ujue sio rahisi kupata msichana anayekuvumilia wakati wa shida mpaka ukafanikiwa?” Nanaa aliendelea kuongea bila kujibiwa, na kwa kuwa alikuwa na mengi yakuongea hakutaka kupoteza muda. Alimjua Geb ni mkimya sana. Ni heri aendelee kuongea tu.

“Sasa nafikiri ndio maana Yasini anamthamini sasa hivi. Anasema alimvumilia sana. Ndio maana sasa hivi anamuenzi. Anasema amemnunuliwa gari nzuri sana. Nimesahau jina. Ila amesema baada ya harusi, wataenda kupumzika nje ya nchi. Wapo kwenye kutafuta ni nchi gani waende kwa fungate. Si unajua wao ni rahisi? Hawana cha mtoto wala Zena hana mimba. Kwa hiyo hawana mtu wakumfikiria ila wao tu. Wanaweza kwenda popote baada ya harusi yao.” Tayari Zena alishafanikiwa kumuonyesha Nanaa kuwa, swala la kuwa na watoto wakati ule ni mzigo. Na yeye hakukosea kutoa ile mimba iliyokaribia kumuua mpaka akalazwa hospitalini, Nanaa akamuhudumia mpaka akapona.

“Yaani Zena amejawa furaha!” Nanaa akaendelea. “Ameniambia nguo zake za harusi na Yasini wanafikiria kwenda kutengenezewa China. Anasema ndugu yake mmoja Yasini amewaambia China wanatengeneza nguo nzuri sana. Na watapata vitu vizuri zaidi vya harusi. Kwa hiyo ameniambia wanatafuta weekend moja wakimbilie China kwa kufanya shopping. Ila Zena ana roho nzuri! Ameniambia kama nataka kumuagiza kitu, nisiwe na wasiwasi. Japokuwa atakuwa na mizigo mingi ya kubeba wakati anarudi, lakini atanibebea na ya kwangu. Yaani Geb, ukimsikiliza Zena, hapo ndipo utajua Mungu yupo. Na humpa yeyote amtakaye. Zena anazungumzia kupanda ndege! Tena sio ndege za lisaa! Ndege ya kwenda nchi yeyote. Yaani kama utani tu. Zena tulikuwa naye kwenye maisha kama haya haya tu. Lakini ona Mungu alivyomwinua!” Tayari Nanaa alishasahau utajiri mkubwa unaomzunguka hapo. 

~~~~~~~~~~~~~

Muda mfupi sana kabla hajazungumza na Zena wala kuingia Facebook, Nanaa alikuwa kwenye shukurani kubwa sana. Aliingia pale chumbani kutokea chini alikowaacha kina Viola. Alipokuwa akijinadi mbele za watu Mungu amempa masikio mengine na mdomo mwingine, yaani Geb. Ameamua kumpumzisha yeye. Aliingia hapo chumbani kwa furaha na shukurani akifurahia vile Mungu alivyombariki kutoka mavumbini mpaka gorofani. 

Akiwa na ndugu mmoja tu James. Aliyekuwa amebeba kofia zote za ubaba, mama, rafiki wa kweli, dada na kaka. Gafla Nanaa anajikuta Mungu amempa mama wa kweli, mama G. Dada ambaye anampenda wala hamuoni kama ni wifi, Grace. Rafiki wa kweli wa wakati wote. Mume na mfariji wake ambaye hawezi kulala mbali naye. Furaha yake ni kumuona yeye anafuraha. Hata akifanya naye mapenzi, alimuonyesha ni kama ndio amebahatika mara ya kwanza ya kulala na yeye mrembo. Na alifanya naye mapenzi kana kwamba hatabahatika tena. Geb. 

Nanaa alikuwa akimshangaa vile anavyofurahia penzi lake hata kama akimkuta bafuni au hapo kwenye kochi. Vile anavyomfurahia mikononi mwake! Hakukosa sababu ya kusifia mchezo aliopewa. Kama hakusifia joto la siku hiyo, basi ulaini wa mwili wa Nanaa, mikononi mwake. Vile alivyofurahia kumshika kila sekunde waliyokuwa wakifanya naye mapenzi. Ilimradi tu, kumfurahisha Nanaa.

Lakini Zena aliyabatilisha yote. Akamfanya ajione na kusahau kila kitu. Akajiona amepitwa. Hana anayemjali yeye kama anavyojaliwa Zena! Akaona mkono wa Mungu juu ya Zena wala si kwake! Akaona maisha yake yeye mwenye mtoto na kupata bahati ya ujauzito tena, si kitu! Nanaa akasahau kabisa orodha ya wasichana wengine wanao jielewa. Wazuri na wasomi waliokuwa wakitamani bahati na heshima aliyopewa yeye na Geb. Kuzaa naye na kumtamka kuwa ndiye mwanamke wa pekee maishani mwake!

Tokea atendwe na msichana. Tena akiwa bado kijana mdogo tu. Chuoni. Geb alipokutana na Nanaa, ndipo anajikuta ni msichana wa pekee anayeweza kuishi naye. Ni kweli alishakuwa na mahusiano na wasichana wengine. Lakini hisia alizozipata kwa Nanaa, akajua ni wake. Na akaelewa ni kwa nini nafsi yake ilikuwa ikimtafuta Nanaa kabla hata hajamuona. Alijikuta popote alipo, yeyote aliyenaye kwa wakati huo, haondoi haja yakutaka kujua pale alipo Nanaa. Alimuulizia mara kwa mara, hata yeye mwenyewe asijue ni kwa nini anamuulizia. 

Alishajua Nanaa alikuwa kwenye mahusiano ya wanaume tofauti tofauti. Lakini hakuacha kuulizia maendeleo yake. Hakuwa akijua ni kwa nini anajikuta anasukumwa kumtafuta James na kumuulizia alipo mdogo wake huyo, mpaka siku alipomuona Nanaa, na kupata nafasi ya kuzungumza naye. Ile hali ya kuwepo na Nanaa kwa mara ya kwanza na kufanya naye mazungumzo mafupi pale beach wakaingiliwa na Grace akimtaka Geb amrudishe mtoto wao Fili nyumbani, iliibua shauku yakutaka kupata nafasi ya kuzungumza na Nanaa zaidi.

Busu alilolipata siku ya kwanza Nanaa akiwa amelala kitandani baada ya Liz kuingia na kumkuta Nanaa anatoa mwiba kidoleni mwake, liliamsha hisia za tofauti! Aliipenda midomo ya mwanadada huyo. Hakuna jinsi au mahali ambapo Geb alitaka kumbusu Nanaa, akajizuia. Aliipenda kuinyonya midomo yake kila wakati. Wakati mwingine Nanaa alimuona akifika kileleni kwa haraka akiwa anambusu yeye.

          Siku ya kwanza kuonja penzi la Nanaa, wakiwa mjini Morogoro, Geb alijua ni kwa nini alimtaka sana Nanaa. Alikata kiu yake na kuibua kiu nyingine ambazo ni penzi la Nanaa pekee lilimwakikishia ndio lina uwezo ya kukata kiu hiyo. Hakuwahi kuchoka kumpapasa pale alipofanikiwa kumuweka mikononi mwake. Macho yake hayakuweza kufunga pale Nanaa alipokuwa uchi mikononi mwake. Akili zake zilitulia kwenye mwili wa Nanaa, nakujikuta hatosheki kutazama pale macho yake yalipoangukia. Nanaa alikuwa akimuona vile anavyofurahia akimpapasa. Alimuona vile hisia kali zilivyokuwa zikiibuka kwa Geb kila ampapasapo. Kwa muda mfupi, Zena alifanikiwa kuweka giza kali kwenye kumbukumbu zote za Nanaa. Akabaki akimuona yeye tu na mafanikio yake.

~~~~~~~~~~~~~

“Naona tulale tu. Najua umechoka.” Nanaa akaona ahitimishe. Hata yeye alishachoka kuongea. Kwanza ni kama aliyamaliza yote. Akasahau kuwa jumapili ndio siku ya familia. Geb aliipenda hiyo siku. Kwa kuwa ndio siku pekee yenye uhakika, mara nyingi hakuwa akihitajika kazini. Aliitumia hiyo siku na Nanaa na Oliva. Siku nyingi za jumamosi alikuwa akienda kazini. Tena wakati mwingine mpaka jioni au usiku.

Akajiweka sawa. Akakaa. “Umeniletea nini hapo. Nataka nile ndio tulale.” Geb akasogolea bakuli alilopewa na mama yake, lilikuwa kwenye sinia na kufunikwa vizuri. “Amenipa mama. Hata sijafungua! Aliniambia nikifika huku nikuwekee kwenye friji.” Nanaa akacheka. “Kweli amekusudia kunifukuza!” Geb akafunua. “Ni matunda.” Kisha akamtizama Nanaa. “Anajua wazi mimi sishibishwi na matunda. Hapo ndio ananitaka nimfuate usiku.” Geb akacheka kidogo. “Lakini haya matunda ni mengi Nanaa.” “Siwezi kushibishwa na matunda hata kidogo. Yaani hicho ni kianzio cha kudhibiti njaa.” Geb alimjua Nanaa jinsi anavyopenda kula. Hata kabla ya ujauzito, Nanaa mpenda kula.

“Kwanza hujanijibu Geb.” “Juu ya nini?” Nanaa aliongea mambo mengi sana mpaka Geb hakujua anatakiwa kujibu nini. “Nazungumzia juu ya kuhudhuria kikao cha harusi. Wala huna haja ya kunipeleka. Ni muda wa jioni. Tukitoka kanisani, tuwe wote. Hiyo jioni nitachukua hata daladala nitaenda na kurudi. Ili wewe upumzike tu.” “Sasa hapo nilitakiwa kujibu nini?” Geb akauliza. “Geb jamani! Labda nilizunguza tu vibaya. Lakini ndio nilikuwa nikikuomba ruhusa mpenzi wangu! Sio kwamba nilikuwa nakutaarifu. Naona umuhimu wa mimi kuwepo. Kwanza itakuwa njia moja wapo yakukutana na wenzangu. Japo naona aibu kidogo.” “Aibu ya nini?” “Si unajua na mimba ya Liv niliibeba chuoni? Walinisema sana. Zaidi Zena na Tia ndio walikuwa viongozi. Wakasema nimeshikishwa mimba halafu nikakimbiwa. Sasa wataniona tena safari hii naenda na tumbo jingine sina ndoa!” Nanaa akaongea kinyonge kidogo.

“Naona labda nisiende tu. Nitulie. Nitamwambia mchango wangu nitatuma.” Akabadili mawazo. “Kwa hiyo unatuonea aibu mimi na watoto wangu?” Geb akamuuliza. Nanaa akashituka kidogo. “Hapana Geb! Siwaonei aibu kabisa. Kwanza namshukuru Mungu kwa ajili yenu. Ni vile naona kuepusha maswali mengi na kujiumiza.” “Kujiumiza!?” Geb akauliza huku akimtizama. Akapoa.

“Nanaa?” “Sio kwa nia mbaya Geb!” “Unaogopa kuonekana na mtoto wangu!? Sijawahi kukukana wewe wala mtoto wangu. Sijawahi kukuonea haya mbele ya mtu yeyote yule Nanaa! Sijawahi kukuficha kwa yeyote! Wakati wote nimekutanguliza wewe na watoto wangu, tena bila kificho! Sina kitu wala mtu ninayemuona wathamani maishani mwangu ila wewe.” “Hata mimi Geb. Samahani kama umeona kama nakukana au nakuonea haya. Ni vile nilitamani nikija kuonana na hao watu angalau niwe nimewafunga midomo katika hili. Sasa najiona ni kama nitaenda kuwapa sababu ya kunisema zaidi. Naomba usinielewe vibaya.” Nanaa akajisogeza karibu ya Geb.

“Nakupenda Geb. Na wewe unajua kabisa sina maisha mengine wala mtu mwingine ila wewe.” “Hayo ulimwambia na Zena?” “Zena ni mbea Geb. Anahamisha maneno hapa na pale. Sikutaka habari zangu na zenyewe ziwe gumzo.” “Au ulijisikia kama huna kitu kizuri cha kumwambia?” Nanaa akababaika sana.  “Nanaa? Au unahisi una maisha mabaya ambayo huwezi kuwaambia watu?” “Hapana Geb. Zena ni mbeya sana. Msambaza maneno. Huwezi amini kwa muda mfupi tu nimezungumza naye amenipa habari za watu karibia darasa zima.” “Kama unalijua hilo, kwa nini unamfungulia mlango mpaka wa moyo wako? Kwa nini unamruhusu kuharibu akili zako? Kwa muda mrefu sana tokea umetoka kwenye mitandao, ulikuwa umetulia Nanaa!”

“Ni juzi tu ulikuwa ukinishukuru kwa fulsa niliyokupa yakukaa nyumbani na kumlea Liv. Ukasema huna mtu ambaye unamfikiria kumwamini kumuachia Liv, kama ikitokea wote, wewe na mama mnatakiwa kwenda kazini! Ulishukuru kwa machozi Nanaa. Nikakwambia tumshukuru Mungu pamoja kwa uwezo aliotujalia. Hasa nguvu. Mimi amenipa nguvu yakufanya kazi, na wewe uwezo wa kumudu hii familia.” Geb akaendelea kumkumbusha.

“Nikakwambia hakuna mtu sahihi ambaye anaweza kulea watoto wetu na kuendesha mambo ya hapa nyumbani vizuri isipokuwa wewe Nanaa. Wote tukakubali huku tukimshukuru Mungu kwa pamoja. Tena tukiwa kwenye kochi hili hili tulilokaa sasa hivi. Unakumbuka tukamshukuru Mungu kwa pamoja na kumsihi Mungu aendelee kubariki biashara zetu, na kutuimarisha sisi wenyewe? Unakumbuka Nanaa?” Nanaa alishaishiwa nguvu. Machozi yalishaanza kumwagika.

“Leo Zena anakufanya uyatupilie mbali maisha Mungu aliyotubariki nayo!” “Hapana Geb. Sijasahau.” “Kweli Nanaa?” Geb akauliza kama kumsuta kidogo. “Labda nimepitiwa tu Geb. Nisamehe mpenzi wangu. Nimepitiwa tu. Sikuonei haya.” Geb akatulia kidogo.

“Unakumbuka nilikuuliza uniambie chochote unachotaka. Ukasema unataka ndoa tu?” Kimya huku akifuta machozi. “Leo unajiita mpanda daladala! Unataka uache magari hapo nje, ukapande daladala! Ili iweje Nanaa? Unajitenga na kila kitu changu! Kutoka kwenye kutambua kuwa hizi mali zote ni zetu. Mungu ametupa kwa upendo, leo imekuwa vyangu kwa kuwa nilianza maisha kabla sijawa na wewe!” “Sijamaanisha hivyo Geb!” Nanaa akajitetea.

“Kweli Nanaa?” “Naomba unisamehe. Na Mungu anisamehe. Unafikiri nimekufuru?” “Ndiyo Nanaa! Umekufuru sana.” Geb alimjibu bila kumumunya maneno. “Naomba unisamehe Mungu wangu. Nimekosa. Nimenung’unika. Nisamehe. Nisamehe mpenzi wangu. Kuna jinsi nimeruhusu maneno ya Zena yaniingie. Nikasahau yale yanayonizunguka. Nisamehe.” Nanaa akajirudi kwa haraka. “Naumia kukuona unanung’unika Nanaa! Najitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu kukuridhisha. Na ninakuomba kama unaona kuna mahali napelea, uniambie.” “Hupelei Geb. Ni kweli unanipa kila ninachotaka na hata mengine sikuwahi kuyafikiria.” Geb akamtizama vizuri.

“Kweli Geb.” Nanaa alijaribu kumuhakikishia. “Naomba uwe muwazi Nanaa. Kama unataka kazi, mimi nafahamiana na watu wengi tu. Naweza kukutafutia kazi. Na ukitaka pia, unaweza pia kuja kufanya kazi pale ninapofanya kazi mimi. Nitamtafutia Oliva mtu wakunisaidia mimi kumtunza mtoto wangu. Nitagawa muda wangu. Kazi na Oliva, ili uwe huru kufanya unachotaka. Sitaki ujihisi mimi na watoto wangu tunakufanya usiishi ndoto zako.” Nanaa alilia sana. Alijua Geb ameshakasirika. “Nisamehe Geb. Nisamehe mpenzi wangu. Nahisi nimekuudhi. Nisamehe. Tafadhali. Naomba nisamehe. Nimekukosea. Nisamehe Geb.” Nanaa aliombeleza akapiga na magoti.

“Nimekuudhi Geb, nisamehe mpenzi wangu! Ninataka kumlea Oliva mimi mwenyewe. Naomba usinikasirikie Geb.” “Hapana Nanaa. Mimi sijakasirika. Ila nataka tuwekane sawa. Sitaki umuone Liv ni mzigo. Huyo mtoto nina mthamini kuliko kila kitu changu. Nampenda sana. Hata huyo aliyekuwepo tumboni namsubiria kwa hamu sana. Binafsi najiita mbarikiwa kwa sababu ya hao watoto pia. Hawapo hapo kwa bahati mbaya Nanaa! Nilipanga na kumuomba Mungu. Kwangu sio mzigo na wala hawapo kwenye maisha yangu kwa bahati mbaya.” “Nisamehe tu Geb. Naomba nisamehe. Hakika nimeongea bila kufikiria. Naomba nisamehe. Nimekiri nimekosa. Naomba yaishe.” Nanaa aliendelea kuomba msamaha wa machozi huku amepiga magoti.

“Nisamehe Geb.” “Yameisha. Ila achana na Zena. Anakuchanganya akili. Kesho unajua ni siku yangu na nyinyi. Siku pekee kwenye juma! Lakini ulikuwa radhi kuniacha kwa aibu ili uende kwake peke yako! Naomba mwombe budget yao ya kikao. Tuchague kitu kimoja, tuwasaidie basi. Lakini sio wewe kwenda huko kesho. Ikitokea unataka kwenda iwe ni siku nyingine ambayo sio siku yangu, na tunakwenda wote. Ni sawa?” “Nimeelewa. Samahani.” Nanaa akarudia.

“Naomba basi ukae hapa na umtumie ujumbe. Atume hiyo budget nzima, halafu umwambia atuambie ni wapi kesho atakuwepo, tukitoka kanisani tumpitishie hiyo pesa au hundi.” Nanaa akabaki amepiga magoti huku ameinama anafuta machozi. “Niangalie Nanaa.” Nanaa alianza kulia tena. “Mimi sitakudanganya, kwa kuwa nakupenda. Nipo kukuongoza na kukusaidia. Hivyo hivyo na wewe kwangu.

Zena sio rafiki unayemuhitaji kwa sasa. Anakuchanganya tu. Umenielewa?” Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Kama unaona muda umekwenda sana, utamtafuta kesho.” Nanaa akajifuta machozi, akavuta simu yake.

Akakuta bado Zena anamtumia ujumbe. “Bado yupo macho. Ametoka kunitumia picha za hoteli wanazofikiria kwenda mara baada ya fungate.” “Basi mtumie huo ujumbe.” Akiwa amepiga magoti vile vile akaanza kutuma ujumbe. ‘Picha ni nzuri Zena. Hongera. Lakini kesho sitaweza kuhudhuria kwenye kikao. Ni siku yangu na familia yangu. Huwa tunaitumia kuwa pamoja na mpenzi wangu, baba watoto wangu na watoto wetu. Ila nimezungumza naye sasa hivi, amekubali kusaidia kwenye harusi yako. Naomba unirushie budget yenu, halafu sisi tutachagua kitu cha kuchangia.’ Akatuma huo ujumbe.

Nanaa aliona kabisa kuwa alisoma. Akamuona anaandika, kisha anaacha. Akafanya hivyo mara kadhaa, mwisho ukaingia ujumbe mwingine. ‘Budget yetu ipo juu sana. Tumeamua kufanya harusi nzuri na ya kisasa. Sidhani kama mtaweza. Hata hivyo hamna haja. Kama hutaweza kufika basi.’ Geb na yeye alikuwa akisoma. Nanaa akamwangalia Geb. “Atakuwa amekasirika.” Nanaa akaongea kwa upole. “Tunaweza kupitia kwenye hicho kikao kesho kwa muda mfupi wakati tunampeleka Liv kucheza. Si lazima mimi na Liv tukaingia. Tunaweza kukusubiria kwenye gari.” “Uliniambia umenisamehe Geb!” “Nakwambia kwa nia nzuri tu. Sina hila ndani yake.” “Sasa kwa nini ubaki kwenye gari tena?” Nanaa akauliza akijua wazi bado Geb anamfikiria anamuonea aibu.

“Hujanikaribisha Nanaa! Wewe ndio umekaribishwa huko. Ukitaka tukusindikize mimi na Liv, tutakufuata. Unajua hakuna sehemu ningependa kuwepo isipokuwa sehemu ulipo Nanaa.” Nanaa akaanza kulia tena.

“Basi naomba mnisindikize Geb. Nitafurahi tukiongozana wote.” Geb akamvuta mkono na kuubusu. “Nakupenda Nanaa.” “Na mimi nakupenda Geb. Nisamehe tu. Sijui niliingiwa na nini! Naona nilishakuwa nimechanganywa na kina Vai, halafu nikaja hapa nikakutana na Zena naye. Nikajirudisha kule Mungu aliponitoa. Nisamehe. Najua unanipenda sana na kunijali Geb. Nimekufuru kujishusha kwa kiasi hicho. Nisamehe.” “Yameisha. Kula basi tulale.” Nanaa akajifuta machozi. 

Akamuona anacheka kama mwanae Liv. “Unacheka nini sasa?” Geb akamuuliza. “Kusimama hapa ndio shuguli. Naona huyu mtoto atatoka mrefu kama wewe. Miezi saba ndio tumbo lote hili!” Geb akacheka kidogo, akasimama na kumsaidia kusimama. “Usikimbilie kupiga magoti bwana! Hukuwa na sababu ya kufanya hivyo.” “Nilijisikia vibaya Geb. Sikutaka nikuumize. Najua unanijali sana na kunihangaikia. Sitaki nikuudhi.” “Yameisha.” “Mbona sasa hata hunikumbatii?” Nanaa akalalamika. “Wewe unajua nikikukumbatia sitakuacha hivyo hivyo. Nataka ule kwanza.” “Mimi nakutaka wewe kwanza.” Geb akacheka. Wakasahau hata habari za Zena. Wakahamia kitandani. Mapenzi yakaanza.

Jumapili.

Nanaa alimka akaanza kumtafuta mama G. “Mbona mama hayupo?” Geb alisahau kumwambia. “Mama alitangulia kanisani. Anamazungumzo na mchungaji.” Nanaa akakaa kama aliyeishiwa nguvu. “Kwani ulitaka nini?” “Kila kitu! Mimi sijui chakufanya hapa ndani bila mama. Atarudi?” “Acha kupaniki Nanaa. Kila kitu ameandaa ndio akaondoka. Tutamkuta huko huko kanisani.” “Na huyo Liv? Ujue ndio anashida humu ndani kuliko kila mtu!” Geb akaanza kucheka.

“Kweli Geb. Huyo mtoto anamuwezea mama tu. Liv hapendi kuchana nywele wala kubadilishwa nguo. Bibi yake ndio anamuwezea.” “Mimi nitakusaidia.” “Haya twende ukajaribu uone. Kwanza kumuamsha hapo ni shuguli. Na akiamka ujue hutamgusa kichwa. Ataishia kukuchekea huku akiweka mikono yake kichwani anakuzuia usimchane. Na unamjua mama. Ukimpelekea mtoto asivyotaka yeye, atakasirika.” “Olivia hawezi kunishinda. Wewe twende tukale, tukiwa tayari tumwamshe.” Wakashuka chini.

Walishakuwa wameoga na kuvaa tayari. Wakala. Ilipofika saa tatu kamili ndipo Geb akaenda kumwamsha Oliva. Alimwamsha mpaka akachoka. Akamtoa kitandani bado amelala. “Si nilikwambia mimi. Huyo shuguli yake mpaka bibi yake. Hapo hatafungua macho mpaka aamue mwenyewe.” Geb akaanza kucheka. “Jamani Liv wewe!? Amka bwana.” Liv aliendelea kulala. “Mimi nambadilisha diaper nambeba hivyo hivyo. Tutambadili mbele ya safari. Hatuwezi kuchelewa kanisani sababu ya nywele. Kwanza hivi alivyo anapendeza tu” “Geb wewe!?” “Sasa wewe unafikiri tutafanyaje Nanaa? Amegoma.” “Shauri yako! Wewe utaenda kupambana na bibi yake.” Geb akacheka huku akimwangalia mwanae. Hakuwa hata na dalili ya kumka.

~~~~~~~~~~~~~

Walifika kanisani mama G nusura aanguke. “Mnanitania nyinyi wawili!?” “Mama, huyu Liv ameamka hapa hapa kanisani. Yaani Geb anazima gari ndio na yeye amefungua macho na kuanza kucheka. Alikataa kabisa kumka.” Nanaa akatetea. Liv alikuwa akipiga makofi huku anacheka. “Liv wewe jamani!” Nanaa hakua akiamini. “Yaani nyinyi watu wazima wawili mnashindwa na huyu mtoto!?” “Mama! Nimemuamsha sana huyo mjukuu wako. Nimemtoa kitandani nikampeleka mpaka sebuleni, lakini akagoma kufungua macho. Nimembadilisha mpaka diaper hajafungua macho. Kama alivyosema Nanaa, ameamka hapahapa.” Liv akamtaka bibi yake. Vimikono vyote juu huku akimwita bibi yake.

Grace akawasogelea akiwa na familia yake. Wote walikuwa wamependeza. “Mbona bado dada ana nguo za kulalia?” Grace akauliza. Nanaa akamkonyeza anyamaze. Grace akacheka. “Watu wazima wawili wameshindwa na mtoto mdogo huyu! Yaani wameniletea mtoto mchafu kabisa huyu. Nywele hazijachanwa halafu waone wao jinsi walivyopendeza! Aibu tupu hii.” “Ni Geb huyo.” Nanaa akamtupia Geb mpira. “Na mimi nilimwambia mama atakasirika.” “Naombeni mnipishe. Mmenikera sana!” “Lakini nimebeba vitu vyake vyote kama ulivyoweka pale kitandani kwako. Hapa ndio nilikuwa nimfungue kumtoa kwenye kiti chake, nianze kumtengeneza. Usikasirike mama yangu.” Geb akajaribu kumtuliza. “Naombeni muondoke, mnipishe.” Grace alizidi kucheka. 

“Sasa amekula?” Grace akauliza tena, Nanaa na Geb wakaangaliana. Mama G akawageukia. “Msiniambie mmemleta huyu mtoto bila kumlisha!” “Nilikwambia alikataa kuamka mama. Liv aligoma kabisa. Yaani nilimnyanyua mpaka kwa mkono mmoja! Akakataa kufungua macho.” “Naomba muondoke Geb.” “Ila tumeleta na chakula chake.” Geb akasisitiza. “Ondokeni Geb.” “Mimi naondoka mama.” Nanaa akasogea pembeni. Geb akampisha pale mlangoni. Mama G akazunguka upande wa pili wa lile gari akiwa na mjukuu wake.

Grace alizidi kucheka. “Liv anakusudi bwana! Mama anatukasirikia bure.” Geb aliendelea kuongea asiamini aliyowafanyia Liv. “Huyo mtoto anakila kitu cha tofauti cha kanisani. Bibi yake ananunua kila leo! Tena ananunua kwa pesa nyingi tu. Sasa leo umletee mtoto na nguo za kulalia! Hamtaelewana.” “Nilimwambia Geb.” “Bwana Liv leo kanikosanisha na mama yangu. Mimi nilijitahidi kweli kumuasha. Tena nikamwimbia na nyimbo zake zote. Lakini wapi!” Wakatangulia kanisani.

Baada ya kama dakika 25 mama G akaingia na Oliva akiwa amependeza sana na cheko lake kama kawaida. Nanaa akamkonyeza Geb ili amwangalie mama yao na Liv. Akawageukia. Liv alishangilia alipoona baba yake anamwangalia. Geb hakuamini. Kwa muda mfupi, yule mtoto alibadilika! Mama G akaenda kuwakabidhi mtoto. “Hivi ndivyo nilitaka aletwe. Na akiwa ameshiba. Nakuja kumchukua sasa hivi.” Akawaambia hivyo na kuondoka. Geb akampokea mtoto huku anatingisha kichwa.

“Sasa mama naye, alitegemea mimi nimletee mtoto akiwa hivi! Naanzia wapi?” Nanaa akacheka huku akiangalia vile huyo mtoto jinsi alivyokuwa amepangiliwa. Kuanzia kichwani mpaka miguuni. Ungependa umshike tu. Lakini cheko hilo la Liv lilikuwa lakibaguzi haswa. Huwapa wachache anaowajua yeye. Akiwa hakufahamu, ujue hutamgusa.

Hayawi Yamekua.

Baada ya kusifu na kuabudu Nanaa akashangaa linatoka tangazo la kwanza la ndoa. Hakuamini. Akamwangalia Geb. “Umesikia!?” Nanaa akauliza kwa kunong’ona. “Ndiyo.” Vigelegele vikasikika. Mama G akiwa anashangilia na wakina mama wengine pale kanisani. Nanaa alijikuta akiinamisha kichwa na kuanza kulia. Hakuwa akiamini. Habari za mwisho alizojua ni kuwa hataweza kuolewa tena kwa kuwa anandoa na Zinda. Geb alimwambia wamsubirie tu Mungu. Alipouliza mpaka lini, hata Geb hakuwa akijua anasubiria mpaka lini. Ila alimsisitiza kutulia. Ukweli moyoni kwa Nanaa hakuwa ametulia. Alitamani sana kuolewa.

~~~~~~~~~~~~~

Hamu ya kumtambulisha Geb kama mumewe ilikuwepo, lakini alikosa ujasiri kabisa. Japo walikuwa wakiishi pamoja na wana watoto. Oliva na huyo aliyekuwepo tumboni, lakini ujasiri wa kumtambulisha kama mume, haukuwepo. Uwezo wa kupaita nyumbani kwa Geb ni kwake, na kutambua mali za Geb kama zake. Tena akiwa amemkuta na kila kitu chake. Magari na nyumba. Pale kwa Geb alikwenda na sanduku lililochakaa na nguo za kawaida sana, ambazo alishatupilia mbali muda mrefu sana Geb alipomfanyia shopping ya nguvu. 

Hata Oliva alimpatia hapo hapo kwa Geb. Kwa ujumla kila kitu anachomiliki kwa wakati huo, alikutana navyo hapo kwa Geb. Utajiri mkubwa uliokuwa ukiongezeka na kumsikia mama yake akimsifia mwanae kuwa anaakili sana ya biashara. Huku akisema ni yeye na Grace wanaendesha hiyo kampuni vizuri sana. Hakuwa akijua hata anatakiwa aongee nini au ajiweke kwenye nafasi gani. Kama mmiliki pamoja na Geb au msikilizaji tu! Anaanzia wapi sasa wakati amevikuta! Hana ndoa na Geb. Umwili huo mmoja unatambulikana wapi!

Japokuwa Geb alijitahidi sana kumfanya Nanaa ajisikie vizuri, lakini haikuondoa ile hali ya kujishuku na kutomiliki moyoni mwa Nanaa. Shauku yake kubwa ni kutaka kuolewa na Geb. Pengine angekuwa hata na ujasiri wa kuulizia mambo fulani fulani. Kuna maswali mengi aliyokuwa nayo juu ya Geb, lakini yalikosa nguvu kwa kuwa alijiona hana haki ya kuyauliza. Kama alivyoachwa Liz na wengineo, ndivyo na yeye alijua angeweza kuachwa siku moja. Hakuwahi kujiaminisha. Amani yake ingetimia tu siku ya harusi atakapotamkwa ni mke halali wa Geb.

Kama mtu angelifungua moyo wa Nanaa, nakujua kilio chake kikubwa mbele za Mungu akiwa peke yake, ilikuwa ndoa. Kila aliyekuwa anamuona anamzunguka, akiwepo kaka yake James, ni kama walishalipuuzia hilo swala. Ilimradi maisha yanaendelea. Nanaa anaendelea kuzaa. Hakuna aliyekuwa akizungumzia swala la ndoa tena. Miezi ilishapita, vikao vya harusi navyo vilishavunjwa. Hapakuwa na dalili ya ndoa tena.

Geb kijana aliyekuwa akiwindwa na historia yake ya nyuma na sasa, alikuwa akimfanya Nanaa asilale usingizi mzuri kwa wasiwasi wa kuibiwa penzi. Ujasiri wa kumuaga asubuhi na kumuacha kwenda kazini kwa amani, ni vile alivyokuwa akimuona Geb anapiga magoti kila siku asubuhi akimuomba Mungu. Alimuona Geb akibadilika na kuwa karibu na Mungu kuliko walivyokutana. Kama Nanaa alishindwa kuamka asubuhi kuomba naye, Geb alihamia upande wa sebuleni hapo hapo chumbani. Basi atasoma neno na kupiga magoti pembeni ya kochi. Akishamaliza kuomba na kuoga. Hapo ndipo alipoenda kitandani na kumshika Nanaa mkono na kuomba naye kwa ufupi kisha kukimbilia kazini. Kidogo ilikuwa ikimtuliza Nanaa.

“Mwanaume anayepiga magoti mbele ya Mungu kwa unyenyekevu hivi, lazima Mungu na yeye atamwinua.” Nanaa alikuwa akiwaza kila alipokuwa akishituka usingizini na kumuona Geb anaomba. Lakini bado haikuondoa shauku ya kuja kuwa mke kihalali. Ashajifikiria mara nyingi ameachika pale na mwanamke mwingine amechukua nafasi yake mle ndani. Alikubali kumsubiria Mungu, lakini kila alipokuwa peke yake hakuacha kumkumbusha Mungu na kumlalamikia katika swala la kuchelewa. Alimwambia Mungu anamchelewesha.

Usiku uliopita ndio ulikuwa mbaya zaidi pale alipozungumza na Zena, na kuambiwa anaolewa. Huku Zena akimpa habari za wenzao waliomaliza nao chuo, vile wanavyoolewa na kufanikiwa. Nafikiri unakumbuka mwisho wake pale jana. Aliishia kupiga magoti na kumuomba Geb msamaha. Akiwa bado na uchungu mwingi moyoni, bado shauku yake ikiwa pale pale, baada ya kuridhishwa kitandani pale na Geb, akajikuta akimuahidi Geb kuwa atakuwa sawa tu hata ikitokea wanaendelea kuishi vile vile. Haikuwa kweli. Lakini ilimbidi kutoa ahadi ile, ili kumridhisha Geb. Alimuahidi kumtambulisha kwa marafiki zake wote hiyo kesho watakapokwenda kwenye kikao.

 ~~~~~~~~~~~~~

Ukweli hakuwa akiamini. Ni kama ilitokea kufumba na kufumbua. Gafla kutoka kwenye kukata tamaa, na kuamua kuacha kabisa kufikiria swala la ndoa, hata masaa 24 hayakuwa yamepita, tangazo lao la kwanza la ndoa likawa limetoka! Bado alikuwa na pete yake ya uchumba mkononi. Waliitwa pale mbele ya kanisa ili waombewe. Bado Nanaa alikuwa ameinama. Mama G alikuja kumchukua Oliva aliyekuwa ameshalala kifuani kwa baba yake wala kelele hazikumsumbua.

Geb akasimama na kumsaidia Nanaa kusimama, wakaenda kupiga magoti pale mbele kuombewa baada ya mchungaji kuuliza kama kuna kipingamizi chochote. Hakukuwepo mtu wa kupinga hilo kwa wakati huo ambapo Mungu ameruhusu. Wakaombewa.

Hakuna sala wala wimbo alikuwa akisikia Nanaa kwa wakati huo. Bado alikuwa amebaki kwenye bumbuwazi. Kilichomshangaza Nanaa ni pale tangazo lake la ndoa lilipotoka siku hiyo hiyo. Mchungaji akatangaza na tarehe ya harusi mara baada ya kuwaombea na watu kumaliza kushangilia. Hasa mama yake Geb ndio alionekana anafuraha zaidi. Nanaa akagundua itakuwa siku ya birthday ya Geb ambayo ilikuwa mwishoni mwa mwezi huo. Hakuweza hata kuzungumza au kuangalia watu kwa machozi yaliyokuwa yakimwagika mfululizo.

Akiwa ameinama palepale mbele kanisani na kushindwa hata kunyanyua uso na kupokea pongezi zake, akasikia sauti ya kaka yake. “Kaka!” Nanaa akanyanyua uso. Akamuona James anacheka. “Usilie sasa.” James akamsogelea na kumpa mkono. “Hongera sana.” Nanaa akashindwa hata kujibu. James alibaki kucheka. Nanaa hakutegemea kumuona kaka yake pale. Ndipo alipojua wote walikuwa wakifahamu hilo isipokuwa yeye tu. Kama alivyomwepesi kucheka ndivyo alivyokuwa mwepesi kulia. Aliendelea kulia mpaka mwisho wa ibada. Wakatoka. Alikuwa kimya huku akifuta machozi wakati wote pembeni mwa Geb.

“Kichwa kitakuuma Nanaa! Usilie bwana.” Grace alimsogelea kujaribu kumtuliza. “Unataka kwenda kula wapi?” Grace alimuuliza lakini Nanaa akashindwa hata kujibu. Geb akamshika mkono na kurudi naye kwenye gari. Mama G alimchukua Liv akaenda naye kwenye gari yake. Grace na familia yake nao wakaingia kwenye gari yao, kadhalika James. Wakaondoka Nanaa asijue wanaelekea wapi.

~~~~~~~~~~~~~

Alipoingia tu kwenye gari Nanaa akajifunika uso na kuendelea kulia kwa uhuru. “Naomba usilie bwana.” Nanaa hakujibu. Baada ya muda akasikia gari linasimama. Akajua labda wamefika nyumbani, akabaki amejifunika uso. Akasikia Geb akishuka, akamfungulia mlango. “Njoo hapa.” Geb akamfungua mkanda na kumgeuza pale pale kwenye kiti akamsogeza na kumkumbatia. “Asante Geb! Nakushukuru sana. Sikutegemea!” Geb alimsikia wakati amemkumbatia. “Nilishakata tamaa. Sikutegemea!” “Nilikwambia tumsubiri Mungu Nanaa. Mungu hakawii wala hachelewi. Hujibu kwa wakati wake. Hakuna siku ilishawahi kupita nisimkumbushe Mungu juu ya shauku yangu.” Nanaa akajitoa na kumtizama.

“Ulifikiri na mimi sina hamu ya kuoa?” Geb akauliza na tabasamu usoni. “Na mimi sifurahii kuishi hivi Nanaa. Na mimi nilitaka kumaliza hili tufikirie mambo mengine. Kitendo cha wanangu kuzaliwa pasipo ndoa takatifu unafikiri ni jambo ninalolifurahia? Unafikiria mimi kama baba naweka mfano gani kwa wanangu? Yaani Liv leo anakuwa mkubwa, halafu anakuja kukuta naishi na wewe bila ndoa! Inamaana namtuma na yeye akafanye hivyo hivyo. Yaani akikua na yeye aende akaishi na mwanaume bila ndoa! Hapana Nanaa. Tumepewa watoto kuwaongoza. Hawatakuwa kingine na kile watakachokiona kwetu au kile tunachowafundisha. Lazima kuweka juhudi za makusudi kuweka mfano wa kuiga.” Akambusu. 

          “Sikutegemea! Mbona sasa hukuniambia?” “Na mimi sikuwa nimetegemea kama Zinda atasimamia ahadi yake mpaka mwisho. Mama alimwambia jana ni lazima aje leo azungumze na mchungaji na wazee wa kanisa kufuta pingamizi lake. Sikutaka kukwambia halafu leo asingetokea, nilijua ungeumia sana.” “Nakushukuru Geb.” Geb akatabasamu.

“Kwa nini?” Akamuuliza huku akimfuta machozi. “Unanilinda na kila kitu. Unahangaika mchana na usiku kwa ajili yangu kuhakikisha mimi na watoto tupo salama na tunafuraha. Hulali kama mimi sinafuraha. Unasimama kwenye nafasi zangu zote za huzuni. Umebeba huzuni zangu zote ili mimi niwe nafuraha. Nakushukuru. Asante.” Geb akambusu. “Asante kama umeona hilo. Na asante kushukuru. Sasa twende tukale. Mama ametuambia tukutane hapa kwa ajili ya chakula cha mchana. Tutakuwa sisi tu kama familia.” Nanaa akajiweka sawa, akaona kila mtu anatoka kwenye gari yake. Wakawasogelea.

Kikao Kingine Cha Familia Kwa Ajili Ya Harusi Ya

Nanaa & Geb.

Walikaa mezani wakila na kuweka mipango ya harusi. Mama G ndiye aliyekuwa akiweka mikakati, alionekana kuhamasika kweli kweli. Danny alirudi kuwa mwenyekiti wa kamati yao ya harusi. Wakakubaliana kuitisha tena kikao kingine. “Lakini sio pale nyumbani.” Geb alitahadharisha. “Naona safari hii tukutane sehemu nyingine kama kwenye hoteli. Na hatutamwitaji Nanaa.” Danny akaongeza. “Mimi niachieni Nanaa. Mambo ya saluni na nguo. Ni mimi na mama.” Grace akaongeza.

“Au labda tusubiri mpaka nijifungue.” “Nanaa please!”Geb akashituka kweli. “Sasa tumbo hili linakua kila siku. Muulize mama. Kila week nanunua nguo mpya. Tumbo linakuwa sana tofauti ya mimba ya Oliva. Sasa hiyo nguo nitanunua ya namna gani? Mpaka siku ya harusi siitabana?” “Hapana Nanaa! Gauni la harusi na lenyewe haliwezi kutuzuia kufunga ndoa. Nunueni mengi hata mkitaka 50. Kuanzia kwa saizi itakayomuenea sasa hivi na makubwa zaidi yake. Sitajali unaonekana vipi hiyo siku ya harusi. Hata ukiwa kama hivyo ulivyo sitajali, nataka kukuoa wewe Nanaa. Sio gauni.” Nanaa akacheka na kuinama.Mama G akaanza kupiga vigelegele. “Basi hapa tutafukuzwa!” Grace akaongea. James akawa anacheka tu.

Walikuwa Grace na familia yake, James, Geb na familia yake tu. “Mimi mwenyewe nimefurahi sana.” Nanaa aliongeza huku machozi yakimtoka. “Siamini! Nahisi ni ndoto! Nilijua sita..” Hapo Nanaa akashindwa kuendelea kuongea. Akanyamaza kama anayefikiria. Kaka yake alicheka tu huku akimwangalia. “Umekuza James. Hongera!” “Asante mama. Mimi mwenyewe siamini hata kama ana watoto! Nikimwangalia Liv hivyo! Siamini kama ni mtoto wa Nanaa!” Kila mtu alikuwa akicheka.

“Mungu ana mambo yake ya ajabu! Yaani nikimfikiria hapa Mungu alipomuweka Nanaa, ungeniuliza miaka 5 iliyopita na kuniambia nitabiri atakuwa wapi baada ya miaka 5, nisingesema hivi hata kidogo! Hiyo siku nikitoka kanisani. Nikahakikisha ameolewa! Nahisi naweza kulala hata masaa 10.” “James! Kwani sasa hivi bado huna amani?” Grace akashangaa. “Huwezi amini Grace. Na yeye anajua. Lazima nimsikie asubuhi na usiku wakati naenda kulala ndipo nipate amani. Nijue ameamka asubuhi salama, na usiku nijue siku yake iliisha salama hamna baya limempata. Ndio napata amani.” Hawakuwa wakiamini. Walibaki wakishangaa.

“Hata anitumie ujumbe wenye mstari mmoja tu, ndipo najua yupo salama. Ikifika saa 4 asubuhi sijamsikia, basi napiga. Ni heri anitumie ujumbe wakusema tu, ‘kazi njema kaka!’ Basi hapo napata amani najua yupo mahali anapumua.” “Sasa wewe si ulishapokea mahari?” Mama G akauliza.

“Mahari sio ndoa mama. Viola alilipiwa mahari na akaachwa na mtoto wake mpaka leo.” James akajibu. “Lakini ni kweli!” Mama G na Grace wakaitika kwa pamoja. “Lakini mimi nilikuhakikishia nitamuoa Nanaa, James! Sijawahi kukudanganya!” “Ikifika kwenye swala la Nanaa, huwa siamini maneno Geb. Hata siku moja. Na kama nilivyokwambia, itabidi kuanza kujifunza na kuzoea. Sijawahi kumuamini mtu yeyote na Nanaa. Huwa nahisi ataonewa tu sehemu. Na kwa kuwa namfahamu kwa kumsikia sauti yake, nakuwa makini sana. Huwezi kunificha ubaya unaomtendea Nanaa, hata umwambie asiniambie. Ukiwa naye pamoja. Kwa kuwaangalia tu, nitajua unaishije na Nanaa. Mama alilijua hilo, kwa hiyo akawa anajitahidi kumuondoa pale nyumbani kila akimfanyia ubaya halafu ajue ninakwenda  hata kama ni kesho yake atamtoa nyumbani.” James aliendelea.

“Kuna siku alimtoa pale nyumbani nikiwa nimemwambia kabisa nitakwenda, lakini nataka kumkuta Nanaa. Nilikwenda baada ya kama siku tatu baada ya kuzungumza naye. Nilifika usiku, sikumkuta Nanaa. Akaniambia amekwenda kwa bibi. Kwa kuzungumza naye tu usiku ule, nikajua kuna kinachoendelea. Nikamwambia nakwenda kwa bibi usiku huo huo, nilazima nizungumze na Nanaa. Nikamwambia nimeota mama mdogo analia sana. Akasema Nanaa mzima, hana shida. Nikamwambia nitapata jibu nitakapo muona Nanaa mwenyewe. Akawa ananizuia sana nisiende kijijini. Kumbe alikuwa amemficha kwa rafiki yake hapo hapo mjini. Akajua nikienda kijijini sitamkuta.”

“Kumbe siku ile nilipompigia simu mama, kabla sijamwambia nakwenda na ninataka kumkuta Nanaa, walikuwa wametoka kumpiga na kumuumiza jicho. Tatizo likawa Nanaa mweupe, jicho lilivilia damu. Walilikanda lile jicho siku tatu mfululizo ili kabla sijafika nimkute mzima. Lakini lile jicho liligoma. Na mama alishajua hawezi tena kunidanganya juu ya Nanaa. Wote walishajua hata Nanaa akinidanganya amejigonga, huwa najua ukweli.” James akatulia.

“Sasa wakafanyaje?” Mama G akauliza. “Haikuwa shuguli ndogo. Ilibidi wanipeleke alipo. Halafu mama akaniwahi kwa kumpigia simu rafiki yake, kuwa nikifika huko na baba, wasifungue mlango, wajidai wamelala.” “Kwa hiyo ukaondoka?” Mama G alizidi kudodosa. “Nakwambia niliota mama Nanaa analia ndio maana nikampigia mama simu kutaka kuzungumza na Nanaa. Wakanidanganya Nanaa hayupo. Kumbe alikuwa nje analia. Akajua nikizungumza na Nanaa nitajua kuna tatizo. Nilipomkosa Nanaa, ndipo nikamwambia sasa nitakwenda na ni lazima nimkute Nanaa nyumbani. Nilishawishika sana kwenda siku ile ile au inayofuata, lakini nilikuwa na kazi ofisini iliyonilazimu niimalize kwanza. Halafu nikajipa moyo kwa mazungumzo yale na mama, inamaana bado yupo hai, hawajamuua.”

“Nikiwa naota mama yake Nanaa analia au yeye mwenyewe analia, huwa najua lazima kuna tatizo limempata Nanaa. Sijui Mungu amefanyaje hiyo! Wala sijawahi kuelewa. Lakini huwa mara nyingi sana, au niseme, sijawahi kukosea. Labda Nanaa mwenyewe aamue asiniambie lakini nikisha ota hivyo, ujue ni kweli. Na nilazima nimuone au nizungumze naye yeye mwenyewe ili nijue kulikoni. Hamna mtu mwingine naweza kuzungumza naye nikaridhika isipokuwa Nanaa mwenyewe.” “Ikawaje sasa?” Mama G akauliza tena.

“Mama kwa kupenda stori!” Nanaa akacheka. “Wewe ndio umenifundisha bwana. Haya ikawaje?” Akamgeukia James. “Muulize Nanaa mwenyewe.” James alijibu huku akicheka kidogo. “Alivunja mlango.” Nanaa akajibu huku ameinama na kucheka. “James wewe!” Grace akashangaa. “Kabisa. Sijui ninakuwa na nini linapokuja swala la Nanaa. Siwezi kufikiria. Yaani siku ile ilikuwa mbaya sana. Nilifanya fujo, mpaka wakamtoa Nanaa. Kwanza walimuumiza jicho vibaya sana. Nikahisi atakuwa chongo. Hilo jicho haliwezi kuja kuona tena. Nilikuwa nimepaniki. Nusura nimpige mama. Ndio baba akaniambia nitajilaani. Nisimguse mama. Heri aolewe, labda na mimi nitaweza kufikiria jambo jingine.” James akamalizia.

“Hutaweza James. Labda uongeze mtu mwingine utakayeweza kumfikiria kama Nanaa, na huku ukiamini sasa hivi anaishi na Geb. Mwanaume anayempenda na kumjali. Hata sisi tunampenda Nanaa. Mwenyewe nahisi kama Mungu amenipa mdogo wa kike.” Grace aliongeza huku akimwangalia Nanaa. “Na mimi hilo nimeliona. Nitazoea tu. Lakini acha afikishwe kwanza kanisani. Akitoka hapo, ndipo labda atatafutwa mwingine wakufikiriwa.” Wote wakacheka.

“Oa mwanangu James. Huyu Nanaa umeshakuza. Tuachie sisi.” James akacheka. “Nitaoa tu mama. Acha hili likamilike kwanza labda ndipo naweza hata kufikiria. Kwanza nahisi hiyo siku nitakayohakikisha ameolewa pale kanisani. Sherehe ikaisha kwa amani. Nafikiri ndio siku ya kwanza kwa muda mrefu sana naweza kulala au hata kuwa na simu iliyoishiwa charge na nikawa na amani, pale Nanaa anapokuwa mbali na mimi.” “We James!?” Bado mama G hayakuwa yakiingia akilini.

“Kweli mama. Huwa ni simu ya Nanaa tu huwa napokea wakati wowote na popote. Na nina hakikisha simu yangu ipo hewani wakati wowote ili isijetokea anashida mahali, halafu akanikosa. Ni namba yake tu niliyoitengenezea mlio wa tofauti kwenye simu yangu. Nikisikia huo mlio hata kama bosi wangu amenisimamia mbele yangu huwa namwambia asubiri kidogo.” “Hata kama anatoa mada mbele ya kikao na wakubwa wapo, simu ya Nanaa ikiingia tu, anaacha kila kitu. James ataomba udhuru na kutoka nje hapo hapo bila yakusubiri jibu la muongoza kikao. Atatoka tu. Anapokwambia simu ya Nanaa haisubiri, ujue hatanii. Mimi nilishaliona hilo, japo hatujawahi kuzungumza naye.” Danny aliongeza na kuzidi kuwashangaza.

“Siku moja tulikuwa kwenye kikao kinachohusu kitengo chetu. Mimi na James tulitakiwa kuelezea mambo yaliyokuwa yanaendelea pale. James alitakiwa aanze, mimi ndio nimalizie. Unajua tulikuwa tunawakilisha kwa wamiliki wa kampuni? Sijui kama unaelewa mama. Walikuwa wamefika hapa nchini. Kwa hiyo na viongozi wote wa zoni zote walikuwepo. Ile James amesimama na kusalimia, ameanza tu, simu ya Nanaa ikaingia. Akapokea pale pale kisha akatuambia anaomba kama dakika tatu hivi, atarudi. Hakusubiri jibu la ndiyo au hapana. Akatoka nje na kutuacha wote tunamsubiria. Ikabidi kutoka na kumuuliza kama ni kwema. Akasema ni Nanaa. Amemuacha nyumbani hajisikii vizuri. Nilimtizama James kama vile nimuulize anajua alichofanya. Lakini nikaona tuokoe muda, arudi ndani amalizie anachohitajika kufanya. Ndipo aondoke.” Kila mtu alicheka. Geb alikuwa akimtizama Nanaa, aliyekuwa ameinama akicheka kwa aibu.

“Nyinyi hamkumuona siku ile asubuhi alipoamka miguu imevimba?” Grace akauliza. “Mimi nilishangaa James amenipita pale mlangoni chumbani kwao hawa, akaenda kumbeba Nanaa na kuondoka bila hata kuzungumza na mtu. Nikabaki kujiuliza kwani alilala hapa au ametokea wapi huyu?” Kila mtu akacheka.

“Ujue siku ile usiku kama panaelekea kupambazuka hivi, niliamshwa na ndoto ya mama mdogo. Mama Nanaa. Nilimuota analia sana. Nikashituka. Na kama nilivyowaambia. Mara nyingi nikiota hivyo, Nanaa analia au yeye mama mdogo analia, nakuwa najua Nanaa anatatizo popote alipo. Na mara nyingi ninakuwa napatia. Hata alipokuwa anaishi na mimi pale nyumbani, nilikuwa nikiota hivyo hata kama ni usiku. Nakwenda kumgongea. Nikienda kumgongea, nakumta hajalala. Labda tumbo linamuuma au anatatizo tu. Sasa nilipoamka baada ya hiyo ndoto, nikaangalia simu. Sikukuta ujumbe wala simu kutoka kwa Nanaa. Nikajiambia itakuwa ni mawazo tu. Kwa kuwa nilimuacha Nanaa usiku uliopita ameshindwa hata kusimama, Geb akambeba mpaka kitandani.”

“Nikasubiria simu na ujumbe wowote kutoka kwa Nanaa. Ikawa kimya. Nikaamua kuoga kabisa kama kujiandaa kama atanipigia. Kimya. Nikajithibitishia ni mawazo tu. Niliposita kumpigia simu ili kumuuliza, nikaamua kurudi kulala kwenye kochi. Sikutaka kuwaamsha. Nafikiri nililala kama masaa mawili tu hivi, simu ya Nanaa ikaingia huku analia. Nikajua tayari. Kwa hiyo kilikuwa kitendo cha kupanda tu kwenye gari ndio maana sikuchelewa kufika.” Kila mtu alishangaa huku akicheka.

“Basi huyu hatakuwa!” “Wala hujakosea mama. Sijawahi kumuona amekuwa hata siku moja. Kila nikimwangalia namuona kama bado mtoto anayehitaji uangalizi wa karibu tu. Siku Geb anamlipia mahari ilikuwa ni kama kengele ya kutolewa usingizini.” Wote walicheka. “Na bado hujaamka!” Grace akaongeza. “Naona naanza kuamka. Nikimuona Liv anacheza vile na nimjamzito tena, najiambia amekuwa sasa.”  Walikaa hapo mpaka jioni. 

“Huyu amelala!” Geb alikuwa amemuweka mwanae kifuani baada ya kucheza na Fili mpaka kuchoka. “Hata hivyo tumeongea mengi. Inatosha. Tukapumzike tu.” Mama G akajibu. “Kuna mahali nataka kumsindikiza Nanaa. Tangulia na Liv nyumbani. Naona amechoka na ishakuwa jioni. Hatutatoka naye tena.” “Hamna shida. Hata hivyo amecheza vyakutosha. Akaoge alale.” Wakaendelea kuzungumza kidogo, wakaagana.

Nanaa na Geb njiani kuelekea kwenye kikao cha harusi ya Zena.

Nanaa afunua ukurasa mpya ulimgusa Geb.

          Akiwa anajua amechelewa, akampigia simu Zena. “Mmeshaanza kikao?” “Bado. Kwani unakuja?” “Tupo njiani. Tutapita hapo kidogo. Si umesema mpo Sinza Bar?” “Ndiyo. Tupo tu hapa nje. Ukishuka kwenye daladala tu, tutakuona.” Zena akajibu. “Basi tupo njiani.” Nanaa akajibu na kukata simu. “Anasema wapo tu nje. Tukifika watatuona.” Nanaa akamwambia Geb wakati anaendesha. Geb akamtizama.

“Unatamani kujua kuendesha gari?” Geb akamuuliza. “Hiyo ni ndoto ambayo lazima nitimize, Geb. Nilimwambia hata kaka. Akaniambia nikimaliza tu chuo nikiwa tayari nimwambie, atanifundisha yeye mwenyewe. Alinikumbusha kipindi fulani kama miezi miwili iliyopita hivi, lakini nikamwambia bado akili hazijatulia. Mambo ya watoto na maisha kwa ujumla. Nikamwambia nataka nikija kujua na mimi niwe nina gari yangu. Sio anifundishe halafu nibakie na ujuzi tu. Unakumbuka kuna siku alikuja kunichukua tukatoka naye kwa chakula cha usiku? Ilikuwa siku ya jumamosi.” Nanaa akajaribu kumkumbusha.

“Nakumbuka.” “Basi siku ile alipowahi alinipitisha pia sehemu wanazouza magari. Nikapata nafasi ya kuangalia magari mbali mbali.” Nanaa akacheka mwenyewe. “Yaani pale ndipo nilipoamini nina ushamba wa magari. Ujue sijui kabisa aina ya magari! Yaani mwenzio nilikuwa najua kuwa kuna magari makubwa na madogo tu. Kumbe tena sijui kuna sijui Toyota, Suzuki, Honda na majina mengi hata sikumbuki. Haya, wakaniambia kuna magari ambayo yanakuwa yanatumia mafuta sana na mengine hayatumii mafuta mengi. Halafu mwenzio nikajua kuwa magari ambayo ni makubwa ndio garama halafu madogo ndio rahisi. Wakaniambia kuna madogo ambayo ni garama sana kuliko hata makubwa. Nikajikuta nachanganyikiwa zaidi.” Nanaa akaanza kucheka tena.

“Basi nikamvuta kaka pembeni. Nikamuuliza mbona hapa sioni magari kama yale ya Geb? Acha kaka acheke. Akaniambia eti magari ya Geb hayo hayauzwi kwenye sehemu kama hizo. Eti unaagiza magari yako nje ya nchi. Halafu akaniuliza swali lililonifanya nifikirie. Akaniuliza eti nishaonana na magari kama yako, wapi! Nikawaza wee, mwishoe akaniambia tuondoke tu. Kwa kufikiria vile bila kutoa jibu la haraka, basi eti nijue ni machache sana hapa nchini. Na pesa yake pia ipo ndefu. Nikajiona nachanganyikiwa tu. Magari yenyewe garama! Halafu hata wakiniuliza nataka lipi, sijui! Nikamwambia kaka niache tu kwa wakati huu. Nifikirie kwanza maswala ya watoto huku tukikusanya pesa. Ameahidi kuniongezea pesa nitakapokuwa tayari.” Nanaa alitabasamu alipokuwa akimalizia na kumwangalia Geb. Macho yakagongana. Kimya.

Ukimya wa muda ukapita. Geb akiendelea kuendesha. Nanaa akafikiria kidogo, akawa hajaelewa kwa nini hachangii kitu. Akaona anyamaze asije akaharibu kama usiku uliopita. Kidogo akaanza kusinzia. “Kwa nini hukuniambia hayo? Au kwa nini nilipokwambia uniambie kitu chochote unachotaka nitakununulia, ukasema unataka tu ndoa? Nilipokuuliza maswala ya gari, ulisema kwa sasa huna haja ya gari. Labda mpaka utakapojifungua. Ukaniahidi popote utakapotaka kwenda, utaniambia mimi nikupeleke au Jeri. Tena ukasisitiza kuwa hata mama atakufaa kwa kuwa huwa anakusindikiza sehemu nyingi tu bila shida. Na imekuwa hivyo wakati wote! Kabla sijamgawia kazi za siku Jeri, huwa nakuuliza kama utamuhitaji!.” Nanaa akakunja uso akajiweka sawa. 

“Nimekutajia kitu ninachojua unaweza kunipa Geb. Ndoa. Sifahamu chochote juu yako isipokuwa mapenzi ya dhati uliyonionyesha. Sijui hata kama una uwezo wa kununua gari jingine hasa baada ya kuninunua kwa mapesa yote yale! Kwanza najisikia vibaya, nashindwa hata kukuuliza kwa hofu la kupata jibu ninalolifikiria. Sijui kama uliua biashara gani kuweza kuninunua kwa mapesa yote yale! Sijui kama nilikufilisi kwa kiasi gani! Sijui ni umbali gani umefika Geb, kuninunua! Naishi mimi na wanangu bure. Tunakula tunachotaka. Navaa kile ninachota na vingine hata sikuwahi kufikiria kama nahitaji. Unanipa pesa kila mwisho wa mwezi, achilia mbali na za matumizi pale nyumbani. Sijui hiyo pesa unatoa wapi! Sijui kama unabiashara gani, isipokuwa zile ninazosikia kutoka kwa mama. Sijui unaingiza kiasi gani kwa mwezi! Sijui kama mwezi huo umeingiza hasara au faida! Kama nilivyokwambia, sijui kama pesa uliyonilipia imekuathiri vipi! Hebu niambie Geb, naanzia wapi kukutwika mzigo wa gari tena?” Nanaa akamuuliza kwa utulivu tu.

“Kuwa mkweli Geb. Hata wewe ungekuwa kwenye nafasi yangu, ungeanza kudai vitu vinavyogarimu mamilioni ya pesa tena? Binafsi siwezi. Nipo huru kutumia ule upande ambao nimekuona upo huru nao kwangu. Na umeufunua kwa umbali ambao sikuwahi kufikiria kama ninastahili. Mapenzi. Umekuwa muwazi na umejitoa kwangu kupita kiasi. Najua chochote nitakachokuomba kwa upande huo, hutasita kunipa. Kwa kuwa najua uwezo wako katika penzi lako kwangu. Utajiri uliopo kwenye mapenzi unaonipa na ambao upo tayari kunipa. Lakini si vinginevyo.” Ulikuwa ukweli mtupu uliomwingia sawia Geb.

~~~~~~~~~~~~~

Ni kweli Geb hakuwahi kuzungumza lolote juu ya utajiri wake kwa Nanaa. Ni jambo ambalo hakuwahi hata kufikiria kama anahitajika kumshirikisha mtu yeyote juu ya pesa yake. Grace mwenyewe alifahamu pesa anayoingiza kaka yake kwa pale kwenye ile biashara tu. Ambayo yeye Grace amewekwa kama msimamizi wa upande wa biashara hiyo inayokusanya mazao mikoani na kuuza pale mjini. Basi.

Geb alikuwa na biashara nyingine. Alikuwa na hilo jengo analokodisha kwa wapangaji wengine. Pesa yake iliingia kwake yeye tu. Alinunua mafuta mikoani na kuyaleta pale jijini. Alikuwa na kiwanda kidogo ambacho kilikuwa kikiyasafisha mafuta hayo na kuyahifadhi kwa ujazo tofauti tofauti ambao aliuza kwa jumla na reja reja. Nayo hiyo biashara yeye mwenywe ndiye aliyekuwa akisimamia. Grace hakuwa akihusika.

Kwenye jengo hilo hilo ambalo kulikuwako ofisi yake na Grace, chini alikuwa na duka kubwa sana ambalo liliuza vinywaji ambavyo havina kileo. Kwa bei ya jumla. Nayo hiyo biashara, ilikuwa ni yeye pekee ndio msimamizi. Grace hakuwa hata akijua kinachoendelea huko. Achilia mbali biashara zake nyingine ndogo ndogo ambazo ungeweza kuzihesabu ni za kipuuzi, lakini si kwa Geb. Alikuwa na vitega uchumi mbali mbali kama alivyokuwa akiambiwa na baba yake akiwa mdogo. Huweki shilingi zote sehemu moja. Unasambaza. Ili upande mmoja ukikwama, uweze kunufaika na kwengine. Nanaa hakuwa akijua analala kitanda kimoja na milionea mkubwa kwa kiasi hicho. 

          Hakuwahi na wala hakuwaza kumshirikisha mtu juu ya pesa anayomiliki. Ila waliojua akaunti zake huko benki, alipoingia kutaka huduma za kibenki, ilibidi meneja wa tawi amuhudumie yeye mwenyewe. Kijana huyo mkimya ambaye usingemkuta kwenye majumba ya starehe isipokuwa nyumbani kwa mama yake na jumapili kanisani, alikuwa amebeba utajiri mkubwa sana. Na alijitahidi kuweka pesa zake kwenye benki tofauti, tofauti.

Aliitafuta shilingi kuanzia chini. Yeye peke yake na shule aliyopewa urithi na mama yake akiwa msaada mkubwa. Anaanzia wapi kumwambia Nanaa maisha yake? Amwambie nini, aache nini? Je, Nanaa anao uwezo wa kumfahamu kwa ukubwa huo? Ni maswali ambayo Geb hakutaka mtu ayajibu kwa kuwa hakutaka kumshirikisha mtu yeyote juu ya hilo. Mali ni zake. Nanaa anampa atakacho. Basi. Inatosha. 

Huo ni upande ambao Nanaa aliona wazi hakuwa tayari Geb kuuzungumzia. Hakuwahi kuzungumza mambo ya kazini akiwa nyumbani. Hata mara moja. Ila Nanaa alikuwa akisikia, ‘kuna mtu nataka kuonana naye leo’ au ‘Jumamosi hii itakuwa ndefu sana. Naweza nikachelewa kurudi nyumbani’. Basi. Hakumsikia akilalamikia mfanyakazi, wala biashara. Ila Grace tu ndiye aliyekuwa akiongea mambo ya kazini anapokuwa na mama yake au anapofanya mambo yake hapo nyumbani. Japokuwa alikuwa na ofisi na wafanyakazi karibu kila mkoa Tanzania, Nanaa hakuwahi kumsikia Geb anazungumza na simu za kikazi nyumbani. Ila Grace. Alitoka nyumbani saa 1:30 asubuhi. Na kurudi saa 11 jioni. Akichelewa sana 6 jioni mwisho. Jumapili ndio hafanyi kazi kabisa. Na wote walijua. Kama kunatatizo, alitafutwa Grace, lakini sio Geb. Ni heri akae kazini siku ya jumamosi mpaka usiku, ilimradi tu, jumapili apumzike.

~~~~~~~~~~~~~

Swala la uchumi ni kipengele kigumu sana kwenye ndoa nyingi. Hupuunzwa lakini ndio eneo kubwa linaloleta matatizo kwenye ndoa nyingi hata kama ndoa ilianza na msingi wa penzi la kweli.

Madhara ya kupuuzwa au kuwekwa misingi mizuri ya uwazi wa kiuchumi kwa wanandoa, huwa haiepukiki. Kama si leo, basi ujue ipo siku lazima watakuja kuona madhara yake.

Mama G atakuja kuzungumzia hilo. Usiache kufuatilia simulizi hili.

Mambo yameanza kunoga kwa Nanaa na Geb. Mambo ya ndoa ndio yanapamba moto. Nanaa yu mjamzito wa miezi 7, anaelekea mwezi wa nane. Geb ataka na yeye ndoa kabla ya mtoto huyo naye hajazaliwa.

Wakiwa ni kama wamevuka vipingamizi vyote, watu hawa wanaona mwanga.

Ni nini tena kitakachowazuia kuhalalisha ndoa yao?

Pengine huu ndio wakati muafaka wa milionea Geb, kuoa na kupumzisha wadada wa mjini. Na kufunga wanaume midomo juu ya Nanaa. Watafanikiwa?

Zena anamsubiria mlalahoi Nanaa, ashuke kwenye daladala ili ahudhurie kikao chake cha harusi.

Asilolijua Zena, maisha ya mtu ni Mungu pekee awezaye kuyabadili.

Haihitaji kikao wala ruhusa kumbariki mtu.

                    Mungu Humpa ampendaye na hakuna wakumuuliza kwa nini?

Endelea kufuatilia.  

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment