“Mimi nahisi kuna kinachoendelea kwa yule msichana. Si bure.
Naombeni mfikirie.” Grace akaongeza. “Kwa nini leo atoe vitisho badala ya
kutekeleza kama mwanzo? Kwani mwanzoni kabla hajamdhuru Nanaa, alimuaga Nanaa?
Alimtisha? Si alimdhuru tu?” Grace aliwafanya wafikirie. “Lakini kweli. Lipo
jambo tu. Kama kweli yeye ni mtu wa kutekeleza mambo yake, kwa nini asifanye
kama alivyofanya mwanzo? Inawezekana amekutana na nguvu za Mungu. Kumbukeni
Nanaa alivyosema aliona watu wakipigana. Inawezekana alipigwa vibaya. Uchawi
wake haufanyi kazi tena. Sasa hivi ameamua kutuma vitisho tu.” Mama G
akaongeza. “Sawa sawa mama. Na mimi nahisi hivyo.” Grace akaongeza.
“Lakini kama ni vitisho, basi amefika mbali!” James
akaongeza. “Mimi najiuliza mwisho wa huyu binti utakuwa ni nini!? Mtu aliyehuru
kuingia humu ndani. Mpaka akamfikia Nanaa! Mnafanya naye kazi! Ana uwezo
wakuingia mpaka ofisini kwako na kupiga picha zote hizo! Inamaana ni mtu ambaye
amefanikiwa kuwa karibu sana na nyinyi! Na amekusudia kumuangamiza kweli Nanaa.
Na anaonekana anafanikiwa. Ameanza kwenye miguu. Amekuja kwenye hofu. Nanaa
ameshindwa kuvumilia, amekimbia akiwa na mtoto na ni mjamzito. Sijui yuko wapi!
Na hata kama atapatikana, hamjui ni nini tena atafanya kumdhuru Nanaa na mtoto!
Nashauri mumuache kwanza Nanaa. Mwacheni kabisa. Maana ni kama mtamtafuta
halafu mje mumtie tena matatizoni kwa watu wenu au watu wetu tuliokuwa
nao kwenye maisha yetu! Wote ni mashahidi hapa. Watu wetu wote wamehusika
katika kumuangamiza Nanaa na bado wanamtesa. Si Zinda, si huyo Mira!” James
akaongeza hukumu mioyoni mwao. Likifika swala la dada yake, huwa haumi maneno.
“Mungu naomba unirehemu. Nisaidie hili alilokusudia
kunifanyia shetani lisinipate.” Geb
alikuwa ameinama, wakamsikia akiomba. “Siwezi kuishi bila Nanaa na Oliva. Mungu
nisaidie. Nitachanganyikiwa. Nisaidie Mungu wangu.” Geb alikuwa amejiinamia akiomba. “Pole
Geb!” Grace alimuhurumia kaka yake. “Mungu yupo na wewe. Hata hili atawasaidia
tu.” “Nahisi kuishiwa nguvu G. Sijui chakufanya tena! Ni kweli najiona
nimemwingiza Nanaa kwenye matatizo.” Tayari shutuma za James zilishamwingia na
kumnyima ujasiri.
“Fanya kile ulichokifanya mara ya mwisho ukafanikiwa.” Grace
alimshauri mdogo wake. Na ni yeye peke yake hapo ambaye aliweza kuongea na
James, kwa kuwa hakuwa mtuhumiwa wa moja kwa moja kwenye swala la Nanaa, japo
Mira alimfuata yeye hapo nyumbani. Lakini na yeye linapofika swala la Geb,
lazima asimame naye hata kama atamuonya kwa ukali, lakini huwa anasimama naye
mpaka amuone ametoka kwenye tatizo. Mama G na Danny walikosa ujasiri kwa kuwa
wao ndio walisambaza maneno. Wakaogopa wasije kuchangia hapo, nakuharibu zaidi.
Huwa James hakawii kuwabadilikia.
“Eti Geb? Umepitia changamoto nyingi sana na Nanaa.
Mlishindaje?” “Niliomba G.” Geb aliongea kwa upole huku akimwangalia dada yake.
“Basi omba tena. Wewe umethibitisha nguvu ya maombi. Omba tena. Nanaa na
Liv ni zawadi yako kutoka kwa Mungu. Usikubali kushindwa kirahisi hivi.
Usikubali kutishwa kwa kelele na uongo wa ibilisi. Usikubali kutoa focus
yako au macho yako kwa Mungu.” “Ni kweli. Basi naomba nikaombe.” Geb akasimama
na kuelekea chumbani kwake.
Walikaa
hapo zaidi ya lisaa, hakutoka. James akaaga.
“Tunaomba akikutafuta, utujulishe na sisi.” Mama G alimsihi
James. James akatulia kama anayefikiria. “Tafadhali James mwanangu.” “Najiuliza
ili iweje mama? Mazingira haya sioni kama yapo tayari kumtunza Nanaa na watoto.
Tumetibua sana hali ya hewa. Ni kama hakuna tena utulivu au mazingira mazuri
kwa Nanaa.” “Hapana James. Na wewe usikubali uongo wa ibilisi. Asikutie hofu.
Hakuna vita inayopiganwa na mtu mmoja. Ukidhani unamlinda Nanaa, ujue
utamwangamiza zaidi. Mimi nimemuona Nanaa sasa hivi. Nanaa unayemfahamu wewe
sio Nanaa huyu anayeishi na Geb sasa hivi.” Grace akaingilia mazungumzo ya
James na mama yake.
Akaendelea. “Hawa watu hakuna jinsi wakatengana sasa hivi
eti ukasema maisha yao yatakuwa sawa. Haitakaa ikatokea tena. Si kwa Nanaa si
kwa Geb. Nanaa hatakuwa sawa mbali na Geb. Hata kama ataenda kuanza kazi,
akalipwa mamilioni ya pesa. Au hata kama Geb atakuwa anamtumia pesa, Nanaa
hawezi kuwa na pumziko mbali na Geb. Tafadhali James. Tafadhali sana, naomba
hili nalo lisikukasirishe na kukufanya ushindwe kusimama na Geb. Kama
tulivyomsikia Geb, alifanya yote haya sababu ya kumlinda Nanaa. Si kumficha
Mira kwa Nanaa. Naomba na wewe mlinde Nanaa kwa kumsogeza karibu na Geb
mwanaume anayempenda na kumthamini, sio vinginevyo. Hawa watu sasa hivi ni
familia. Wana watoto, hakuna jinsi ya kuwatenganisha tena. Nakusihi James
usamehe na uwe upande wa kuwajenga. Nanaa anakusikiliza sana wewe. Chochote
utakachomwambia wewe, atasikiliza na kukifanya.” Kwa mara ya kwanza Grace
akamtolea uvivu James. Aliongea kwa ujasiri bila kuweka kituo na kumtaka James
amsikilize.
Mpaka James mwenyewe akatulia. Grace hakuwa mzungumzaji. Kwa
hiyo akiongea ni lazima utamsikiliza tu, kama wewe ni muungwana. “Tafadhali
James.” “Sawa.” Wakashangaa James amekubali kirahisi tu, akaondoka. Danny
alikuwa kimya kabisa, akiwaza vyake. Alishindwa hata kuongeza neno. Majuto
yalikuwa yakimsumbua sana.
Nanaa Ndani Ya
Basi.
Huko kwenye basi majuto yakaanza kumsumbua Nanaa. Akakumbuka
vile Geb alivyokuwa akimuhangaikia. Jinsi alivyougua na kuwa naye pale
hospitalini. Akakumbuka mapenzi ya Geb kwa Oliva. Jinsi alivyokuwa akifurahia
anapokuwa ametoka kazini halafu awakute wakimsubiria barazani. Kitandani
anavyolala akiwa amemshika au kumchora mgongoni. Mabusu ya shingoni na
mgongoni. “Nitalalaje bila Geb!?” Nanaa akawaza. “Nimeondoka kwa
haraka bila kufikiria. Sikutakiwa kumkimbia Geb. Heri ningemuaga tu. Geb
ameniamini na mtoto, leo nimemsaliti!” Nanaa akajikuta
akilia. Aligeukia dirishani, akaendelea kulia. Akaanza kumuhurumia Geb akaamua
kushuka njiani pindi basi litakapo simama.
“Lakini kwa nini amenificha kuwa anafanya kazi
na mwanamke wake?” Wazo
jingine likamjia. “Labda alikuwa na mimi hospitalini kwa kuwa alijua mwanamke wake ndiye
aliyenisababishia yote yale! Dhamira ilikuwa ikimsuta.” Akajikausha machozi. Gari lilisimama
maeneo ya Korogwe. Nanaa akataka kushuka, lakini akapingana na hilo wazo.
“Kwanza nilimuuliza kama anamfahamu ni nani
aliyenifanyia hivyo, akasema anamfahamu. Alishindwa nini kunitajia kama sio
alitaka kumficha mpenzi wake? Geb anapenda kutetea watu wake kama Danny na mama
yake. Heri nikaanze maisha yangu.” Nanaa akatulia kwenye kiti. Akamfunika mwanae vizuri
akajiegemeza kitini, akarudi kulala tena.
Kwa Geb.
Walikaa mpaka saa 11 jioni, Geb hajatoka chumbani kwake.
Grace na Danny nao pia wakaamua kuondoka na watoto wao. Mama G akaona aende tu
kumuangalia. Akamkuta amepiga magoti. Kichwa amekiegemeza kitandani. “Geb!”
Mama yake aliita kwa upole. Geb akanyanyua uso. “Naomba unisamehe mwanangu.
Najiona ninakusababishia maumivu kila wakati. Mara ya kwanza Nanaa aliondoka
akiwa mjamzito, mimi nikiwa sababu. Mara hii ya pili anaondoka tena akiwa
mjamzito, na mtoto juu, mimi nikiwa pia nimesababisha.” Geb akakaa kitandani.
“Njoo ukae hapa.” Mama G akaenda kukaa naye. “Naomba
nisaidie kuomba mama. Naomba tuombe wote.” Mama G alimuonea huruma. “Kwani
umeshindwa kuomba?” “Nimeomba. Lakini naomba tuombe wote tena. Maombi ya watu
wawili wakipatana, yanakuwa na nguvu zaidi. Naomba tumuombee Nanaa wangu na
watoto pia. Nanaa hajala tokea juzi. Alipoteza hamu ya kula kabisa baada
yakuzungumza naye mambo yenu. Jana asubuhi pale hotelini hakula vizuri. Halafu
ni mjamzito na ananyonyesha. Naomba tumuombee ulinzi wa Mungu. Popote alipo,
Mungu amtie nguvu na kumlinda.” Machozi yalianza kumtoka mama G. “Nisamehe Geb. Naona vile
ninavyokutesa mwanangu.” “Hata
hili litapita tu. Naomba tuombe.” Wakapiga magoti.
Wema Huwa Hauozi!
Nanaa alifika Arusha, huku akikumbuka mapenzi ya Geb kwake. Mambo makubwa aliyokuwa akimfanyia. Upendo alio uonyesha kwake. Akakumbuka hakuwa akithaminiwa mpaka Geb alipoweka thamani kwake. Akajirudi. “Hata kama Geb ana mwanamke mwingine, sijawahi kupendwa na kujaliwa kwa kiasi hiki! Geb ananipenda kwa dhati. Anasisimkwa akiniona! Hawezi kulala bila kunigusa mimi. Anafurahi akiniona mimi na Liv.” Japokuwa mawazo mengi tofauti tofauti yalikuwa yakipita kichwani mwake akiwa njiani, lakini hilo ndilo likashindwa kupingwa au kupata upinzani mpaka anafika huko Arusha.
“Haloow?” Geb akaitika. “Geb! Nataka kukutoa wasiwasi. Nimefika salama. Na mtoto hajambo.” Akaweza kutambua kilio kwenye sauti yake. “Nanaa!” “Abeee!” Nanaa akaitika akijaribu kutulia. “Upo salama mpenzi wangu?” “Kuna baridi tu. Lakini nipo salama.” Nanaa akajibu. “Ulibeba nguo nzito za
kujifunika?” Geb
akauliza akisikika kumjali yeye bila kukimbilia lawama au kutaka kujua alipo
kitu kilichomshangaza sana Nanaa na kuzidi kujutia kukimbia mapenzi mazito ya
kiasi hicho. Akazidi kulia.
“Eti Nanaa? Ulibeba nguo nzito za kukuhifadhi usiumie na baridi?” “Hapana.Lakini mtoto nimemfunika vizuri. Usiwe na wasiwasi.” “Ungependa nikuletee nini cha kukusitiri kwa baridi?” Akamsikia Nanaa akiendelea kulia. “Nanaa!” Geb akaita. “Nina hamu na wewe Geb. Sijui nitalalaje leo?” Ndicho kitu Nanaa alifanikiwa kuzungumza. “Naweza kukufuata ili tuwe wote Nanaa.” “Naogopa Geb. Sitaki kufa niache watoto. Acha nianze tu maisha mapya. Nikitulia nitakutafuta. Lakini nisamehe niliondoka bila kukuaga. Niliingiwa na hofu.” “Unaanza maisha mapya bila mimi Nanaa?!” Nanaa akazidi kulia.
“Eti mpenzi wangu?” Geb aliendelea kubembeleza taratibu tu. “Nimeingiwa na hofu Geb. Mira
ameapa kuniangamiza kabisa kama sitaachana na wewe. Amesema atamuua na Oliva
pia.” “Pole mpenzi wangu. Naomba
usilie. Umepata sehemu ya kulala wewe na watoto?” Nanaa alikuwa amembeba Oliva. Akajishika
tumbo. Akakumbuka ni mjamzito. Akajifuta machozi. Mpaka hapo bado Geb hakuwa
akijua Nanaa alipo. Lakini akajitahidi asikurupuke kuuliza hilo swali. Amchote
taratibu tu, kwa upendo.
“Nanaa?” “Ndio nimefika tu. Bado nipo stendi.
Nimepata mtu nimemuomba aniazime simu ili nikutoe wasiwasi. Niliacha simu
nyumbani. Niliitupa kwa hofu Geb.” “Pole sana.” Geb aliongea kwa upole. “Nitakutafuta tena wakati
mwingine. Ngoja nikatafute sehemu ya kulala. Sitaki Liv ashikwe na baridi
zaidi. Nitakupigia wakati mwingine. Narudisha simu kwa mwenyewe.” “Unafikiria
kulala wapi?” Geb
akauliza kwa haraka kabla hajakata simu. “Kwa sasa nitachukua chumba hotelini. Huku
nikitafuta chumba cha kupanga mahali. Nitatafuta kazi. Nakuahidi kukutumia pesa
yako yote. Nitalipa kidogo kidogo.” Machozi yakaanza kumtoka tena.
“Unafahamu hayo mazingira vizuri?” Geb akamuuliza swali la kumtega ila kwa
upendo tu. “Hapana
Geb! Wewe unajua historia yangu. Sijaishi maeneo mengi zaidi ya Moshi na hapo
Dar. Lakini nilikuja huku Arusha kwa sababu Alex, alikuwa au niseme anaishi
huku. Alikuwa anapasifia sana. Anasema ni pazuri. Ndio maana nikaamua kuja
kuanza huku maisha. Nahisi sitasumbuka. Usiwe na wasiwasi na watoto.
Nitahakikisha watakua salama tu.” Nanaa
akajikuta ametamka alipo. Geb akajua.
“Nafahamu hoteli nzuri itakayowafaa wewe na
watoto.” “Mmm! Sitakuwa na hiyo pesa Geb. Najitahidi kubania pesa ili nipate
sehemu nzuri ya kuishi na watoto. Na siku ya kujifungua nisipate shida yeyote
hasa kifedha, kama nitakuwa bado sijapata kazi. Sitaki watoto waje wapate
shida. Acha niende kwenye hoteli za bei ya chini. Halafu namaliza muda wa
maongezi kwenye simu ya watu. Naomba nikuage kwa sasa ili nikatafute sehemu ya
kulala.” “Basi nakata, halafu nitakupigia mimi sasa hivi, ili nisimalize pesa
yake.” “Nataka kuondoka Geb. Hapa kuna kelele na Liv ameanza kutetemeka baridi,
sitaki apatwe na vichomi kama mimi wakati ule mpaka nikalazwa! Nitakupigia simu
wakati mwingine.” Nanaa
akasisitiza.
“Basi chukua taksii, halafu muombe dereva wa
taksii akuazime simu yake. Unipigie, halafu nitazungumza naye pia nimuelekeze
sehemu ya kukupeleka.” “Sawa.” Nanaa
akaitikia kwa haraka ili tu akate ile simu. Na Geb akajua. “Tafadhali usisahau Nanaa.
Niahidi utanipigia ukiwa ndani ya taksii.” Nanaa akajua amekamatwa. Aliitikia bila kufikiria. Na Geb
huwa hapendi kuahidiwa kitu, halafu usitimize. “Sasa
hapo itategemea kama nitapata dereva mwenye muda wa maongezi kwenye simu yake
na kama atakubali, Geb.” “Kabla hujapanda kwenye hiyo taksii, hakikisha
unapanda kwenye taksii yenye dereva mwenye simu.” “Geb! Nina masanduku mawili,
na mtoto! Kwanza nilipanga kupanda daladala ili kubania pesa.” “Hapana Nanaa. Kwenye daladala
utawatesa zaidi watoto. Naomba uchukue taskii.” “Sawa. Nitafanya kama
ulivyosema Geb. Asante na kwa heri.” Nanaa akaaga.
“Nanaa!” Geb akaita. “Abee!” Nanaa akaitika akiwa anakaribia kukata
simu. “Nakuombea
ufanikiwe mpenzi wangu.” Hapo
akaupata moyo wa Nanaa. Akajikuta machozi yakimtoka. “Nakupenda Geb.” “Najua Nanaa. Na mimi nakupenda sana, Nanaa wangu.
Kila kitu kitakuwa sawa. Hakikisha unapanda taksii, na umwambie mwenye taksii anipigie.”
“Nitafanya
kivyo.” Nanaa
akakata simu nakumrudishia mtu aliyekuwa amemuazima simu hiyo. Alikuwa kondakta
wa basi hilo lililofanikisha kumfikisha jijini Arusha salama.
~~~~~~~~~~~~~~
Baada ya kupingana na mawazo mengi akiwa ndani ya basi mpaka
abiria wote wakashuka na kumuacha yeye peke yake na mwanae aliyekuwa
amemkumbatia kama andazi ndipo huyo kondakta akamfuata na kumuuliza kulikoni
kwani pale ndio ilikuwa mwisho wa basi. Na abiria wote walikuwa wameshuka.
Mawazo ya wema wa Geb juu ya maisha yake, yakazidi ubaya wa kutokuambiwa habari
za Mira. Akajikuta kosa la Geb ni dogo sana, kulinganisha na garama alizomlipia
kwenye maisha yake.
Kila alipojiambia kwa
shahada aliyonayo, atapata kazi nzuri. Atalipwa mshahara mzuri. Atakuwa na
uwezo wa kuja kumaliza deni la milioni 50 aliyolipiwa na Geb, lakini akakumbuka
garama ya Geb aliyomlipia maishani si pesa peke yake. Alijitoa kwa hali na mali
pia. Akagundua upendo mkubwa na wa dhati wa Geb maishani mwake. Akagundua kwa
hakika hatakuja kupata mwanadamu anayempenda kama Geb.
Katika wanawake wengi waliotaka kuzaa na Geb, yeye ndio
alichaguliwa na Geb! Ndipo akaona wema wa Geb unazidi ubaya alioleta Mira.
Kwanza hata kama ni mwanamke wake, mbona muda mwingi anakuwa na yeye!? Kwa nini
yeye Mira ndio awe wakutetea mahusiano yao sio Geb!? Hata Nanaa akajiuliza
hilo. Nanaa akakumbuka vile Geb anavyopambana kuona wanakuwa pamoja. Alimuona
anavyomlinda na mama yake mkubwa. Alilipa pesa yote ile ili awe naye.
Akakumbuka visa vya Zinda hata na Liz.
Alimwambia alikubali yeye ndio atupiwe lawama, lakini sio yeye.
“Huyu Mira atakuwa muongo tu. Inawezekana alikuwa mpenzi wa
Geb, lakini Geb alishamuacha, ndio sasa hivi anahangaika na mimi na mwanangu.” Ndio wazo la mwisho alilokuwa amefikia
Nanaa na kuazimia kumtafuta Geb. Ndipo akaazima simu ya Kondakta huyo
kumtaarifu Geb alipo. Lakini hakutaka kurudi kwa Geb, nikutaka tu kumtoa
wasiwasi. Lakini kwenye simu aliyompigia Geb, akaibua hisia zaidi. Akajikuta
anaongea hata ambayo hakupanga kuongea. Akatoa ya moyoni huku akilia. Geb
alimlainisha mpaka Nanaa akaingia kwenye mtego yeye mwenyewe.
~~~~~~~~~~~~~~
Akamrudishia yule kondakta simu yake, kisha akampa pesa
kidogo kama shukurani ya kumshikia mizigo yake, akamuongezea pesa nyingine,
akamwambia akanunua muda mwingine wa maongozi. Alipoona amepewa pesa nzuri,
upendo ukaongezeka. “Naweza kukusaidia kukubebea mizigo mpaka kwenye taksii ili
usisumbuke na mtoto.” “Nitashukuru kaka yangu.” Akambebea mizigo mpaka kwenye
taksii. Nanaa akampa tena pesa nyingine, akaingia na mtoto ndani ya gari. Oliva
alikuwa amejikunja kifuani kwa mama yake kwa baridi.
“Tunaelekea wapi?”
Mwenye taskii akauliza baada ya Nanaa kupanda na mwanae. Lilikuwa swali zuri
sana, lakini hakuwa amejiandaa na jibu lake. Hakujua hata wanakwenda wapi.
Akakumbuka Geb alimwambia ampigie simu mara baada ya kupata taksii. “Naomba
unisaidie simu yako, nimpigie mtu atakuelekeza.” Yule dereva akatoa simu
akampa. Nanaa akapiga. Ikaita mara mbili, akakata. Hapo hapo Geb akapiga.
“Samahani nakusumbua Geb. Lakini tupo kwenye
taksii tayari.” “Hunisumbui hata kidogo. Naomba kuzungumza na dereva.” Akarudisha simu kwa dereva. Akapokea
maagizo kutoka kwa Geb. Akasikia dereva akijibu, ‘nimeelewa’. Kisha
akamrudishia simu Nanaa. “Nanaa!”
“Abee!” “Nimemuelekeza sehemu ya kukupeleka wewe na watoto.” Wasiwasi ukamwingia Nanaa. Alimjua Geb na
maisha anayoishi. Hakuwahi kumpeleka sehemu za bei ya chini. “Unakumbuka swala la pesa lakini?
Naomba isiwe sehemu ya garama Geb! Nabania pesa mwenzio! Sitaki kuja kusumbuka
na watoto.” “Usiwe na wasiwasi. Nimeshawapigia simu ili wawatayarishie chumba,
mkikute tayari. Patakufaa wewe na watoto. Halafu ukishaingia chumbani, unipigie
simu.” “Nimeacha simu nyumbani Geb.” “Hapo hapo chumbani kutakuwa na simu.” Hilo likazidi kumuogopesha.
“Hizo si zitakuwa hoteli zile za garama sana!?”
“Naomba usiwe na wasiwasi juu ya pesa Nanaa. Fikiria usalama wako wewe na
watoto kwanza. Sawa?” Kila
wakati Geb alimkumbusha anao watoto wawili. Hajapuuza ujauzito wake kitu kilichozidi
kumtuliza Nanaa. “Sawa.
Nakushukuru Geb. Na samahani kwa usumbufu. Nakuahidi kukupigia Liv akishatulia.
Sasa hivi anatetemeka baridi. Lakini kama nikikuta umelala, nitakupigia tena
kesho. Umenisikia?” “Sawa.” Geb
akajibu bila wasiwasi. Nanaa akashangaa safari hii hakulazimisha kupigiwa simu.
Ikamuumiza moyoni.
Alitegemea kuambiwa lazima unipigie simu kabla hujalala.
Lakini akaishia kusikia sawa! Ikabidi aage kwa upole. “Usiku mwema, Geb.” “Mama anataka
kuongea na wewe.” Nanaa
akanyamaza. “Nanaa!”
“Bado nipo.” “Nakupa mama.” Kimya.
Akamsikia anaanza kulia. “Nakuomba
usilie tena. Pole mpenzi wangu. Pole sana.” Akamsikia akijaribu kuvuta pumzi mara
kadhaa kujituliza. “Nanaa?” “Nipo Sawa, Geb.” “Utaweza kuzungumza na mama sasa hivi au baadaye?” Geb akatumia hekima. “Ni sawa tu.” Nanaa akajibu.
Geb
akamkabidhi simu mama yake. “Pole
na safari Nanaa, mwanangu.” “Asante mama. Samahani nimeondoka na mtoto gafla.” Mama G hakutegemea, lakini Nanaa alijua
ukaribu wa huyo mama na Oliva mtoto wao. Alimpenda bila unafiki. “Usiwe na wasiwasi mwanangu. Sasa
fanya hivi, ukifika tu hotelini, pale mapokezi waambie wakupe blangeti la
umeme. Nimeshazungumza nao. Wamesema watakutayarishia. Ukifika chumbani,
mwambie muhudumu alichomeke kwenye umeme. Uingie humo ndani na mtoto. Hakikisha
unamnyonyeshea Oliva mkiwa humohumo ndani ya hilo blangeti ili apate joto.
Usimuogeshe leo usiku. Na wewe utulie humo humo ndani ya blangeti kwa muda ili
kutoa vichomi. Umesikia mama?” Nanaa
alikuwa akilia. Mama G alishamuhangaikia mpaka blangeti! Hakutegemea.
Alijua atakuwa amemkasirikia baada ya kuondoka bila kuaga.
Lakini akakuta anabembelezwa! Ilimuingia sana moyoni. Kutoka kwenye maisha ya
kulaumiwa kwa kila jambo, sasa hivi anapata watu wanao mnyenyekea! “Asante mama.” “Pole mwanangu. Jitahidi kunywa hata mtori.
Nimetoa oda jikoni. Nimewaambia wakuletee chumbani.” Mama G akaongeza. Nanaa alishindwa hata
kujibu. Akabaki akilia. “Nakurudisha
kwa Geb.” Mama G
akampa Geb simu yake.
“Nanaa!
Kila kitu kitakuwa sawa mpenzi wangu. Tutaongea tena hivi karibuni. Huyo dereva
mimi ndio nitamlipa. Usimlipe pesa yeyote. Nimemuomba akusaidie kubeba mizigo
mpaka ndani. Usibebe mizigo na watoto. Yeye ndio atakusaidia. Akikufikisha
mapokezi, ndipo anipigie, nikizungumza na wewe, ukiniambia amekufikisha salama,
namtumia pesa yake kwa njia ya simu.” Nanaa aliendelea kulia. “Nanaa!” “Ninazo pesa Geb. Acha tu nitalipia. Nikifika
chumbani nitakupigia.” “Basi mwache akubebee mizigo
mpaka ndani. Naomba niahidi hutabeba hiyo mizigo wewe mwenyewe. Utajiumiza
mgongo na kuhatarisha maisha ya mtoto tumboni.” “Nitamwacha anibebee, asante.” Geb akakata. Nanaa alimkumbatia mwanae
zaidi huku akilia.
Nanaa Hotelini Jijini Arusha.
Baada ya muda, dereva alimwambia wamefika. Nanaa akabaki
ametoa macho. “Hapa si patakuwa pa garama sana!” Nanaa akajikuta anaongea peke
yake huku ametoa macho. “Sitapaweza!” Akaendelea kuwaza wakati dereva akimtolea
mizigo yake. Akashuka kwenye gari. Akaongozana naye mpaka mapokezi. Akamlipa
yule dereva. Akabaki ametoa macho akishangaa uzuri wa ile hoteli ya kisasa mle
ndani huku amebeba mtoto wake mkononi.
Wazungu ndio walikuwa wengi ndani ya hoteli hiyo. Kuashiria
ni ya watalii. Waliokuwa na ngozi nyeusi kama yake, wote aliwasikia wakiongea
lugha ya kigeni.
Kama
sio kingereza, basi ilikuwa kifaransa na lugha nyingine ambazo hata hakuwa
akijua wanazungumza nini. “Can I help you?” Nanaa akageuka. Akakuta muhudumu
ametulia pale mapokezi akimuuliza kama anaweza kumsaidi. Alikuwa dada mrembo
tu. Amevaa sare safi akaonekana nadhifu. Alimpa tabasamu la kumkaribisha.
Tarayi Nanaa alikuwa na wazo la kuondoka hapo. “Karibu.” Yule muhudumu mwenye sura ya kuvutia, akarudia kwa lugha ya Kiswahili baada ya Nanaa kubaki amekodoa macho. Akajua wazi ni mtanzania mwenzake. “Naitwa Nanaa. Nimeambi..” Nanaa akakwama. Hakujua aseme nini. “Nanaa Magesa?”Muhudumu akauliza huku akiangalia kwenye kompyuta.
“Si ni Nanaa Magesa upo na Oliva Magesa?” Si kwamba Nanaa
hakuwa amemsikia tokea mwanzoni. Lakini hakutegemea kusikia akitambuliwa kama
Nanaa Magesa. Moyo wake ukajawa furaha, akamwangalia mwanae. “Ndiyo.” Akajibu na kurudisha macho kwa yule muhudumu.
“Karibu sana. Chumba chenu kipo tayari. Alinipigia tena simu nakuniambia chumba
kiwashwe heater kabisa na blangeti lenu la umeme pia lipo tayari kitandani. Na
lenyewe alisema liwashwe kabisa. Naamini mtafurahia. Subiri kidogo nimwite mtu
wakukubebea mizigo yako. Chakula kitaletwa baada ya muda mfupi. Ukihitaji kitu
chochote, usisite kunipigia hapa mapokezi. Bonyeza namba sifuri tu, nitakuitika.”
Nanaa alibaki ametoa macho, asiamini maandalizi yote yanayomsubiria yeye.
Akabebewa mizigo yake, akapelekwa kwenye chumba chake.
Kilikuwa chumba kizuri sana. Chumba chenyewe tu ni kama nyumba! Ilikuwa na
upande wa sebule. Makochi mazuri sana. Muhudumu alimuuliza mara kadhaa kama
kuna kitu kingine anahitaji, lakini Nanaa alibaki anashangaa tu na mtoto wake
mkononi. Akaamua kuzunguka kila mahali kwanza. Akaelekea chooni na upande
vilipo vitanda. Akabaki ameduaa upande wa vile vitanda. Vilikuwa vimetandikwa
vizuri sana lakini sio vitanda vizuri kushinda alivyoacha nyumbani kwa Geb. Geb
alilalia kitanda kizuri sana.
Mlio wa kufungwa mlango na yule muhudumu ndio uliomtoa
kwenye mawazo. Akajikuta amebaki peke yake na mwanae pale chumbani. Akarudi
pale alipokuwa amemuacha yule muhudumu kuangalia kama mizigo yake ipo au
aliondoka nayo. Akakuta alishaingiza mpaka kule chumbani upande wa makabati ya
nguo. Akapumua kwa nguvu. Akafanya kama alivyoambiwa na mama G, akapanda
kitandani kwa haraka. Akamfunika Oliva huku anamnyonyesha. Oliva alilala pale
pale kwa haraka. Nanaa akajua alikuwa amechoka. Akamfunua tena, akambadilisha
diaper yake. Ilikuwa imejaa sana. Akamuhurumia mwanae. Akajilaumu sana.
“Nimemtesa mwanangu. Pole Liv. Kila kitu kitakuwa sawa.” Akambusu, na kumuweka
sawa. Akahakikisha amemfunika vizuri. Ndipo na yeye akajilaza.
Baada ya muda kidogo, akasikia mlango unagongwa akajua tu ni
mtu wa chakula maana aliambiwa ataletewa chakula. “Karibu.” Akasimama. Ni kweli
alikuwa ameletewa chakula. Akamkaribisha ndani na kumwambia aweke chakula
kwenye meza karibu na makochi. Akaweka na kutoka. Akakumbuka ni zaidi ya dakika
45 tokea azungumze na Geb. Na alimwambia ampigie mara atakapofika hotelini.
Akaangalia. Akakuta kuna simu ya mezani. Akampigia. Haikuwa inapatikana. Akajaribu
tena na tena hakumpata. Akaingiwa na wasiwasi. “Geb amenikimbia!” Nanaa akaanza kulia.
~~~~~~~~~~~~
Alilia na kusahau kuwa yeye ndiye aliyemkimbia Geb.
Akajirudisha kitandani. Alilia na kulia. Akajua amebaki peke yake. Akaanza
kupangia mahesabu pesa alizo nazo. Akapiga simu mapokezi kuuliza bei ya kile
chumba. Akatajiwa kwa dola za kimarekani zisizopungua $185 kwa usiku huo ila
akaambiwa inategemea na huduma ya ziada atakazopewa. “Dola!?” Nanaa akauliza
kwa mshituko. “Dolla 185 na inategemea na huduma kama hivyo ya room service. Ukiletewa
huduma chumbani ni tofauti na kuifuata. Kwa hiyo usijali. Jumla yote itawekwa kwa
pamoja.” Akajaribu kumuelewesha kwa utulivu tu asijue ndio anazidi kumuongezea
hofu. “Haya. Asante.” Akakata simu.
Usingizi wote ulimuisha. “Dola!? Nilimwambia Geb
kuwa sina hiyo pesa! Nitafanyaje na watoto jamani! Watanifunga jela kama nikishindwa
kulipa. Au nilipe ya usiku wa leo tu, halafu asubuhi niondoke? Sitaweza
kuendelea kulala hapa.” Akamuona vile mtoto wake alivyolala vizuri.
Akaridhika moyoni. “Hata kama nitagaramia pesa yote hiyo, angalau mwanangu
amelala vizuri. Baridi inaonekana imemuweza!” Akamfunika vizuri akabaki
akiwaza.
Akaamua kwenda kuoga. Akakutana na mabomba yanayotoa na maji
ya moto huko bafuni. Akafurahia. Akiwa anaoga akakumbuka Mira alimwambia
atamnyonga mtoto wake akiwa usingizini. Akafunga maji kwa haraka, akakimbilia taulo.
Akatoka akikimbia mpaka kitandani alipokuwa amemuacha mtoto wake, akaweka
kidole puani kwake. Akakuta anapumua. Akamshika homa. Akagundua hana homa.
Akamfunua miguuni, pia akakuta miguu yake ipo sawa tu. Akaibonyeza mara kadhaa,
akagundua ipo sawa tu. Akabaki anahema kwa hofu. Akaona pale alipolala hatakuwa
salama. Akaamua amnyanyue mtoto wake alale mikononi mwake. Akakaa pale pale
kitandani akiwa amempakata mwanae. Akapitiwa na usingizi. Kila wakati alishituka
na kuweka kidole puani mwa mwanae kuhakikisha bado anahema.
~~~~~~~~~~~~
Akiwa amepitiwa na usingizi pale kitandani huku amempakata
mtoto wake kwa hofu, akasikia mlango unagongwa. Akashituka sana. Akaangalia saa
ya ukutani, ilikuwa inakaribia saa nne usiku. Akaingiwa hofu ya ajabu. “Labda
wanataka kunidhuru mimi na mtoto wangu!” Nanaa akawaza. Hakuwa ameagiza
kitu chochote kwani hata chakula walichokuwa wamemletea hakuwa amekula. Na
tayari ilishakuwa karibu ni saa 4 usiku. Akavaa rob nyeupe iliyokuwa
imening’inizwa pale chumbani.
Akasogelea mlango. “Nani?” Nanaa akauliza kwa wasiwasi.
Akasikia tena mtu anagonga taratibu bila kujibu. Bado alikuwa amembeba mtoto
wake. Akarudi kwa haraka kwenye simu ya mezani kujaribisha kumpigia tena Geb
ili kuona kama safari hiyo angempata. Safari hii ikaita na kumfariji. Ilipoita mara
ya pili, akapokea. “Samahani
nakusumbua, Geb. Lakini naogopa. Kuna mtu anagonga mlango sasahivi. Hataki
kuniambia yeye ni nani. Nifanyaje? Nipo na mtoto hapa. Kama wanataka kumdhuru
je?” Geb
alihisi hofu iliyomkamata Nanaa. Akamuhurumia. “Usiogope Nanaa. Hakuna mtu
anaweza kukuingilia. Hiyo hoteli wanailinda sana ndio maana nilikuchagulia
hapo. Fungua.” Nanaa
akasita.
“Geb wewe! Unajua Mira amesema atamuua Oliva?”
“Amekuogopesha tu. Ameshindwa tena kwako ndio maana anatumia lugha ya vitisho.
Hawezi kumdhuru mtoto. Usiogope.” “Unafikiri hivyo!?” Nanaa akauliza kutaka uhakika. “Kabisa.
Hebu fikiria Nanaa. Kwani mara ya kwanza alipokudhuru, alikutumia kwanza
vitisho?” “Hapana.” “Basi ujue ameshindwa kufanya madudu yake tena. Ndio maana
akaamua kutumia njia ya kukuogopesha. Hana nguvu hiyo tena juu yetu.
Tumefunikwa na ulinzi wa kiMungu, ndio maana anahangaika.” Kidogo Nanaa akafarijika. “Basi naomba usikate simu, Geb.
Ili kama kuna kitu kibaya kitanipata, ujue halafu uwapigie simu watu wa
mapokezi waje kunisaidia. Umesikia?” “Sawa.” Geb akamkubalia. Ndipo Nanaa akaenda
kufungua mlango huku amembeba mtoto wake. Hakutaka kumuweka chini.
Alumasi Husakwa Chini Kabisa
Aridhini.
Na Atafutaye, Hachoki.
Alipofungua
mlango, macho yake yakagongana na Geb aliyekuwa amesimama katikati ya mlangoni.
Nanaa alirudi nyuma kwa mshituko. Kwa hakika hakutegemea. Akamwinamia mtoto
wake nakuanza kulia. Hakuamini. Akanyanyua uso kuthibitisha kile anachokiona. “Geb!” Geb akaingia. “Umewezaje kufika huku kwa
haraka hivyo!?” “Nilibahatika
kupata ndege. Mara ya mwisho tulipokuwa tukiongea. Ukaniambia utanipigia simu
hata kesho. Halafu ukaongea na mama pia. Pale tulikuwa tayari tupo njiani na
mama ananisindikiza uwanja wa ndege kuja huku. Nilipojua tu upo huku Arusha,
hapohapo nikamtumia ujumbe yule kijana anayekatisha tiketi, huku tunazungumza
na wewe. Tulipoagana kwenye simu mara ya kwanza ukiwa unatafuta taksii, hapo
hapo nikakusanya vitu nilivyojua nitahitaji kwa safari nikaingia kwenye gari
kuelekea uwanja wa ndege. Nikamuomba yule jamaa anayetusaidiaga kupata tiketi
za ndege kwa haraka bila shida. Nikamwambia nipo njiani naelekea uwanja wa
ndege, lazima leo nilale Arusha. Mungu alikuwa upande wangu. Nimefika tu uwanja
wa ndege nikapata tiketi ya ndege iliyokuwa inakaribia kuondoka.” Nanaa bado
hakuwa akiamini.
“Jamani Geb!” Nanaa aliendelea kulia. Asijue kama ni
furaha au mshituko wa kumuona pale mida hiyo. Alijua ameshaachwa na watoto
wake. “Unajua siwezi kulala bila wewe Nanaa.” Nanaa alilia sana. Geb akaweka
mkoba wake chini, akamsogelea Nanaa. “Mbona umembeba huyo?” “Naogopa Geb. Yale maneno ya
Mira kuwa atamnyonga akiwa usingizini, yananisumbua sana.” “Hilo ndilo alilokusudia. Anakutia tu
hofu. Hana chakutufanya tena. Nipe nikupokee.” Geb akamchukua mtoto wake.
Kama kawaida. Akamuweka kifuani na kumkumbatia kwa nguvu
huku akisikilizia furaha moyoni. Akambusu mara kadhaa. Akaanza kumuombea huku
amemkumbatia. “Nakuombea usingizi mzuri Liv. Malaika wa Bwana wakafanye kituo kwako. Ulinzi
wa Mungu ukawe juu yako. Kila ulimi ulioinuka na utakao inuka juu yako, nauhukumu
mkosa. Umeshindwa katika jina la Yesu. Nguvu ya mauti juu yako ninaikataa.
Haina mamlaka wala nguvu kwako, katika jina lipitalo majina yote. Jina la Yesu,
Liv wewe utaishi ili ukayashuhudie na kuyasimulia makuu ya Mungu. Uhai wako
ukafichwe ndani ya Kristo Yesu. Nakutamkia baraka. Umebarikiwa mwanangu, kwa
baraka zote za rohoni na mwilini. Amen!” Geb akamaliza na busu kwa mwanae. Alimtizama kidogo,
akamgeukia Nanaa. Akamkuta ametulia kimya.
“Naomba nimlaze. Apumzike.” “Nimefurahi umekuja Geb. Hofu
imepungua.” “Nataka iishe Nanaa. Hakuna silaha itakayoinuka tena kwetu
ikafanikiwa. Naomba uamini. Ni vitisho tu. Wanataka kukuogopesha.” Nanaa
akatulia. Geb akaenda kumlaza mtoto wake kitandani. Akamfunika vizuri, akarudi
kwa Nanaa.
~~~~~~~~~~~~
“Njoo Nanaa wangu.”
Geb akamvuta. “Nisamehe. Niliingiwa hofu, nikakimbia.” “Nimefurahi sana
ulinitafuta, Nanaa. Asante.” Geb akamkumbatia. “Nina hamu na wewe Geb!” Geb
akambusu kichwani akiwa amemkumbatia. Akamsikia Geb akivuta pumzi kwa nguvu na
kuzishusha taratibu kama aliyepata aghueni moyoni. Akafurahi kuhisi Geb anamtoa
nguo. Akaanza kutoa ile rob ya juu. “Mbona upo na taulo bichi!?” “Nilikuwa
naoga. Nikakumbuka maneno ya Mira, nikamkimbilia mtoto wangu. Niliogopa nisije
nikatoka kuoga, nikamkuta Liv amekufa.” Geb akamuhurumia sana.
“Pole Nanaa. Anakutisha tu.” “Kwani alikuwa mpenzi
wako?” Nanaa akamuuliza kwa upole. “Nimefurahia sana jinsi ulivyouliza hilo
swali. Nimepata moyo kuwa unaniamini.” “Najua hunidanganyi Geb. Hilo
ninauhakika nalo. Najua kwa sasa hivi nipo peke yangu kwako.” Geb alifurahi
sana. Akambusu kichwani, akamtoa lile taulo bichi mwilini mwake, akamfunga tena
ile rob, akamshika mkono, wakasogea mpaka kwenye makochi. Wakakaa.
Siri Ya Pili.
Juu Ya Mira.
“Ni kweli niliishi na Mira nyumba moja.” Geb alianza kwa
utulivu huku Nanaa akimsikiliza. “Lakini ilikuwa mwaka wa mwisho wa masomo
yangu nilipokuwa nchini India. Mwaka huo wa mwisho, niliishiwa pesa. Na kwa
kuwa malengo yangu yalikuwa mwaka huo nimalize masomo yote, na niondoke nchini
hapo na shahada mbili, tena zote nzuri, ilinibidi kujibana sana ili kufanikisha
malengo. Hapo mama alikuwa ameshamaliza kuuza mali zake zote. Hana kitu.
Ukumbuke hapo ni kama alikuwa akisomesha watoto wawili, kwa shahada za juu,
tena kwa ada ya nje, au kimataifa. Haikuwa pesa ndogo, Nanaa.” Geb akaendelea.
“Ikabidi sasa kutafuta watu wakuishi nao ili kubana
matumizi. Ndipo nikapata chumba kwenye apartment aliyokuwa akiishi Mira na
rafiki zake. Pesa ya pango ikapungua. Lakini bado haikutosha. Ikabidi kutafuta
tena mtu wakuishi naye kwenye hicho chumba changu. Nikampata kijana mmoja
kutoka nchini Nigeria. Tukawa tukiishi naye kwenye chumba changu, ndani ya
apartment ya Mira na rafiki zake.” Geb akatulia kidogo.
Kisha akaendelea. “Nilikuwa nipo busy, ungeniona kipindi
hicho, ungenihurumia Nanaa. Unajua kula yangu jinsi ilivyokuwa ya shida. Sasa
ndio ikawa mbaya zaidi. Sikuwa nikikumbuka nilikula nini, wala sikuwa na mpango
wa kula. Mimi na shule, shule na mimi bila kujua watu wananitizama. Mira akaanza
kazi ya kunipikia na kuniwekea chakula. Siku moja nilitoka kujisomea, nikarudi
kama saa tano usiku. Nikamkuta amekaa sebuleni anaangalia tv. Mimi nikajua yupo
na mipango yake, kumbe alikuwa akinisubiri mimi. Akaniambia kipo chakula hapo
mezani. Nile. Basi. Mimi nikakiangalia. Ilikuwa chapati sijui na mboga gani
zile! Kwa kuzitizama tu kwa macho, nikawa nimekinahiwa. Nikachukua chapati
moja, nikaingia chumbani kwangu huku nakula. Sikuwa hata nikijua kama yeye ni
mpishi.” Geb akaendelea.
“Sasa kilichonishitua na kunifanya nijiulize, ni siku ya
pili yake niliporudi pale tulipokuwa tukiishi, yule jamaa niliyekuwa nikilala
naye chumba kimoja akaniambia Mira alikwenda hapo na kuchukua nguo zangu zote
chafu akaenda kufua! Sijaingiza zile habari kichwani vizuri, akaniambia nisiwe na
wasiwasi. Kwani alishazirudisha zote zikiwa zimepigwa pasi. Amenipangia kwenye
kabati langu. Kabla hata sijaongea chochote, akaniambia na ameniletea chakula
hapo chumbani. Ameniomba nile. Nikajua mambo yameshaharibika. Mira hakuwa wa
kwanza kunifanyia hayo. Alishatokea tena na mwingine kama Mira nilipofika tu hapo
nchini. Nikajiapia kuishi peke yangu bila mtu, lakini shida ya pesa ikanifanya
nirudie kosa.” “Kosa gani tena?” Nanaa akauliza.
“Nilipokuwa tu nimefika hapo nchini India, ndio mgeni tu.
Nilikutana na dada mmoja wa kitanzania. Na yeye alikuwa amekwenda kusomea mambo
ya unesi. Akaniambia atanitembeza hapo, kwenye sehemu muhimu. Nikakubali.
Nilijuta Nanaa. Nilikuwa sihemi wala sipumui! Aliniganda mpaka nilihisi
sitaweza kuhema.” Nanaa akacheka. “Usifikiri utani Nanaa! Dada alining’ang’ania
huyo! Tena huku anatangaza kuwa mimi ni mwanamme wake. Wakati mimi ndio
nilikuwa nimetoka kujiapia wanawake tena basi. Ndio nilikuwa nimetoka tu
kutendwa hapo chuo kikuu cha Mlimani. Najua mama yangu ameuza kila kitu ili
nisome. Nikajiambia nina jukumu la kumrudishia vyeti vya maana. Nilijiapia
kutokuruhusu kipingamizi chochote kile. Nikakusudia kujikana haswaa.” Nanaa
akacheka.
“Ukafanyaje sasa?” “Kwa nani? Mira au huyu wa kwanza?” Geb
akauliza. “Wote.” Nanaa akajibu huku akicheka. “Yule wa kwanza ilibidi kuanza
kumkwepa. Lakini haikuwa rahisi. Maana alikuwa akinifuata na kutaka tuongozane
kila mahali. Kwenye kula, sijui kusoma. Mara anifuate nimsindikize shopping.
Ilimradi tu tuwe wote. Ikabidi kumkwepa. Tena kwa wazi kabisa, ili aelewe. Haya,
Mira naye nilipoona shuguli za kufuliwa zimeanza na kuletewa chakula chumbani,
nikaamua niweke kikomo mapema. Nikamwambia yule kijana niliyekuwa nikiishi
naye, asiwahi tena kuruhusu mtu yeyote achukue nguo zangu chafu na kwenda kufua
kama mimi mwenyewe sijaruhusu. Na nikamwambia, asiwahi kupokea kitu chochote
alichopewa aje anipe kutoka kwa yeyote anayeishi pale nchini India. Awaambie
wanitafute mwenyewe wanikabidhi.” Geb akaendelea.
“Lakini yule jamaa akanisihi sana nimvumilie kwa muda mpaka
atakapotumiwa pesa kutoka kwao.” Nanaa akakunja uso. Geb akajua hajamuelewa.
“Yaani yule jamaa niliyekuwa nikiishi naye, aliniomba aendelee kupokea chakula
kwa niaba yangu, ili awe anakula yeye. Kwanza mimi mwenyewe sikuwa nikipenda
vile anavyopika. Sikuwa hata nikila chakula chake. Nilisita sana Nanaa. Hasa
nikizingatia naelewa wazi nia ya Mira kwangu. Nikamwambia yule jamaa, kwa
kuendelea kupokea vile vyakula, ni kama kumwambia Mira, na mimi nimemkubali.
Nikamwambia
haitakuwa sawa aone vyakula vyake navipokea, halafu nije kumkataa baadaye.
Lakini yule jamaa akanisihi sana nimvumilie. Basi. Nikampa muda mfupi. Mambo
yake yalipokaa sawa ndio…” “Subiri kwanza Geb!” Nanaa alimkatisha.
“Inamaana mliendelea kupokea vyakula vyake!?” Nanaa
akauliza. “Ndiyo Nanaa. Lakini baada ya muda mfupi tu, nikaona nikomeshe hiyo
tabia. Nikamwambia Mira tutoke kwa ajili ya chakula cha usiku.” “Geb!” Wivu
ulishamwingia Nanaa. “Nia yakumtoa ilikuwa ni kwenda kuzungumza naye Nanaa. Si
vinginevyo.” Nanaa akatulia. Geb akaendelea.
“Tulipokuwa tukila kwenye huo mgahawa, ndipo ikabidi
kumueleza ukweli wote. Kuanzia mwanamke aliyenisaliti nilipokuwa nipo hapo chuo
kikuu cha Mlimani. Malengo na viapo nilivyojiwekea. Na nikamwambia juu ya
vyakula vyote alivyokuwa akileta pale chumbani, kuwa ni jamaa ndiye aliyekuwa
akila. Tena nakumbuka kumtania kuwa jamaa anasifia sana mapishi yake na yeye
mwenyewe. Akacheka. Sasa nisikilize kwa makini hiyo ndoa ilipotokea.” Nanaa
akajiweka vizuri.
“Alipoelewa kuwa sitanii
wala sina mpango kwenye swala la mahusiano ya kimapenzi. Si kwake tu,
ila ni kwa yeyote yule kwa wakati ule. Akaniomba kuwa, endapo nitafikiria kuoa
mwanamke mwingine basi anaomba nimfikirie yeye. Mungu wangu nishahidi Nanaa.
Sijasahau kitu hata kimoja. Kiiungwana tu, bila kutaka kumuumiza, nikamkubalia
yule dada. Tukazungumza mambo mengine. Tukaachana kwa makubaliano asifuate tena
nguo zangu chafu chumbani kwangu. Yaani nilimuomba asinifulie tena. Wala asinipikie.
Basi. Nikaona ameacha. Mimi nikaendelea na chuo changu. Shule ikachanganya.
Nikamaliza na kuondoka pale nchini. Yeye nilimuacha bado anasoma.” Geb
akaendelea.
“Muda mrefu ukapita bila hata mawasiliano. Akaja siku moja
kuniomba kazi. Hata sijui nani alimpa namba yangu. Sikutaka kujua, nikampa kazi
nikiwa nahitaji mtu pale ofisini kwetu. Grace akamfanyia usahili. Akaniambia
anaona atatufaa. Akaanza kazi. Ninavyokwambia mimi, na ninaomba uniamini.
Sikuwa hata na habari naye. Alikuwa akinisalimia kwa heshima kama wafanyakazi
wengine. Hapakuwahi kutokea na mazungumzo yetu
sisi binafsi hata mara moja. Kwa kuwa yeye ni muhasibu, na yupo chini ya Grace, wala si
mimi. Akiingia ofisini kwangu ujue ametumwa na Grace aniletee kitu ili nikague
au kupitia kama ile ripoti uliyokuwa ukitengeneza wewe. Basi.”
“Huwa hata hatuna mawasiliano mengi mimi na yeye. Inaweza
ikapita hata siku sijawasiliana naye. Kwa kuwa na mimi nina sekretari wangu na
nina shuguli zangu nyingine mbali na ile kampuni unayoifahamu wewe. Kama
ninataka mambo au habari za ile kampuni, nitazungumza na Grace tu, wafanyakazi
wengine wa ile ofisi, wanawajibika kwa Grace, sio mimi. Nina mambo mengi sana
Nanaa. Siwezi kuwa nikizungumza na kila mfanyakazi, lasivyo usingekuwa ukiniona
nyumbani saa 11 jioni au 12. Na wakati mwingine wa mchana tusingepata muda wa
pamoja kama ningekuwa nikiwasiliana na kila mfanyakazi. Ndio maana Grace
anahusika na kina Mira au wafanyakazi wote pale, mimi nafanya mambo yangu
mengine labda Grace awe likizo kama hivi, ndipo atataka nimfanyie baadhi ya
mambo, lakini pia hata akiwa nyumbani, anafanya mambo yake mwenyewe na ndio
maana ulimuona Mira pale nyumbani siku ile ya kikao, alikuja nyumbani jana yake
kumfuata Grace.”
“Ndio Grace anasema akamkaribisha kesho yake kwenye kikao
baada ya Mira kuulizia yale maandalizi pale nyumbani. Lakini sio mimi. Yaani kina James walipotoka kanisani siku ile
ya kikao. Kuzungumza na mchungaji na Zinda. Ndio waliokuja kunishangaza
nakunifanya nianze kukumbuka mambo ya Mira. Nilishasahau kabisaaa.” Nanaa
hakuelewa.
“Sielewi Geb.” “Unakumbuka siku ambayo ndoa yetu ilitangazwa
kanisani halafu Zinda na mama yako mkubwa wakaipinga?” “Nakumbuka.” “Si
unakumbuka kesho yake mama akaomba kikao ili wamsikilize Zinda na kumlipa mama
yako mkubwa pesa aliyokuwa akidai?” “Nakumbuka.” Nanaa akaitika kwa unyonge.
“Basi ndio siku Zinda aliposimulia kuwa Mira ndiye anayekufanyia mambo yote
hayo. Kwa kuwa umemchukulia mume, ambaye ndio mimi. Niliwasihi kina James
wasikwambie kwanza, wakuache. Niliwaambia tutakutoa mawazo yako kwenye
kumtazama Mungu, ukabakia na mawazo ya Mira. Nikawaambia ukweli wote juu yangu
na Mira. Na nikawaambia Mungu atatushindia. Ipo siku nitakwambia. Lakini sio
ukiwa kwenye ile hali.” Geb akaendelea.
“Wakanikubalia. Unakumbuka nilikupeleka Morogoro?” Nanaa
akanyamaza na kuinama. “Nilitaka kupata muda na wewe Nanaa, lakini pia nilitaka
kukwambia juu ya habari za Zinda na Mira. Niliishia kukwambia habari za Zinda
tu, kwa kuwa unakumbuka mwenyewe jinsi ilivyokuwa.” Nanaa akanyamaza. Alikumbuka
jinsi alivyokuwa amepaniki. Alilia. Hata chakula kilimshinda. Ni kweli Geb asingeweza
kuongeza habari nyingine tena.
“Sikutaka kukuudhi zaidi Nanaa. Kumbuka na mimi ulinihesabu
kama msaliti wako. Ukaona nawatetea watu waliokuumiza. Lakini Nanaa, nia yangu
ilikuwa njema tu. Nilikuwa nataka amani. Nilijua wamekosea wao kama binadamu.
Lakini sikutaka mgombane. Nilitegemea ungeumia. Lakini mimi ndio ningekuwa
kimbilio lako kwa kuwa nimekwambia. Lakini ikawa tofauti. Nikaogopa kukupa
habari za Mira kwa haraka. Nikaona nikuache kwanza. Mpaka utulie. Urudishe
imani yako kwangu kama leo, ndipo nikwambie habari za Mira. Lakini jua
hakujawahi kutokea mahusiano kati yetu. Na Mungu wangu ni shahidi. Neno la
kumkubalia kuwa nitamfikiria nitakapokuwa tayari kuoa, ndio anasema niliingia agano
naye na mizimu imejua kuwa nimemkubalia kuwa mimi ni mume wake.” Nanaa
aliyekuwa ameinama kwa aibu, akainua macho kwa mshangao.
“Anasema
mimi na yeye tuna ndoa ya mizimu. Kwa hiyo ndipo aliposimamia hapo.” Geb
akatulia huku akimwangalia Nanaa. “Umenielewa?” Geb akamuuliza. Nanaa
akatingisha kichwa kukubali. “Nataka kujua kama umenielewa na kuniamini Nanaa.
Hilo ndilo la msingi na nguvu yangu. Siwezi kufanya chochote, bila wewe kuwa
upande wangu. Nazidiwa vita. Kwa kuwa najikuta nipo peke yangu bila wewe. Umoja
wetu, ndio nguvu yangu. Kunapotokea tatizo, halafu unanikimbia mimi, ujue
unaniathiri vibaya sana Nanaa. Nataka uniambie kama umenielewa.” “Nimekuelewa Geb.
Na ninaomba unisamehe. Nilikukimbia.” “Ulikimbia, lakini ukanitafuta.
Hilo limenifurahisha sana. Hujui tu.” Geb akambusu midomo yake kwa
kifupi tu. Akamwangalia na kumfuta machozi. “Asante.” Nanaa akashukuru.
“Swala la Zinda na Mira ndilo ninalotaka kujua kama
umenielewa na kuniamini. Kwanza ujue inapokuja swala la kuchagua, wewe utakuwa
wa kwanza. Kwa namna yeyote ile Nanaa. Wewe ndio utakuwa wa kwanza.” Ilimgusa
sana Nanaa. “Na katika swala la kusema kweli. Ujue ni kwako tu ndipo
nitakapojificha uso wangu. Nitasema ukweli wote bila kificho ili ujue ni jinsi
gani utanisitiri. Sina kimbilia jingine ila wewe Nanaa.” Nanaa akajifuta machozi.
“Nimekuelewa
na ninakuamini Geb. Samahani nilikukasirikia tulipokuwa Morogoro. Nilipaniki. Sikutegemea.” “Basi yaishe mpenzi wangu.” Akaanza
kumbusu midomo yake. Akashuka shingoni.
Akambusu shingo nzima. Tena kwa kurudia rudia. Mwili mzima wa Nanaa ulikuwa
ukisimkwa kwa yale mabusu ya mfululizo. Akamgeuzia uso, Geb akapokea midom,
nakuanza kuifanyia kile kitu Nanaa anapenda. Wakahamia kitanda cha jirani. Geb
akakata kiu zao, wakabaki wamekumbatiana hapo kitandani Geb akichezea maziwa yake
taratibu ila si chuchu kuepuka kuzisisimua na kutoa chakula cha Liv. Nanaa
alipenda sana jinsi alivyokuwa akishika maziwa yake, ilimfanya atulie kabisa akisikilizia
raha yake.
~~~~~~~~~~~~
“Sasa
itakuje Geb?” Baada ya muda akauliza. “Kwanza ule. Nimeona vyakula pale hata
hujagusa! Ukiendelea hivyo utajiumiza Nanaa. Kumbuka sasa hivi unaishi kwa
ajili yako na huyo mtoto huko tumboni. Na Liv pia anategemea maziwa kutoka
kwako. Lazima uhakikishe unakula vizuri na kushiba.” Geb akatoka pale
kitandani. Akammiminia mtori. Bado ulikuwa wa moto vile vile. Akampelekea pale
kitandani. “Asante.” Nanaa akashukuru wakati akipokea bakuli la mtori.
“Karibu.” “Na wewe umekula sasa?” Nanaa akauliza. “Wewe unajua siwezi kula kama
haupo au tukiwa hatupo kwenye maelewano Nanaa. Nashindwa hata kujifikiria.”
Nanaa akamuhurumia.
“Nisamehe Geb. Niliingiwa na hofu. Nikaona heri mmoja wetu
alipe garama ili kumnusuru Liv. Kumbuka kile alichonitenda Mira! Sikutaka kimpate
na mtoto. Nikaona ni heri niondoke tu. Nikajua akipata habari kuwa nimeondoka,
ataacha kumfuatilia mtoto wangu.” “Nilikuomba tuwe tunazungumza Nanaa. Ukipata
kitu chochote kinachotaka ufanye maamuzi, naomba unihusishe na Mimi. Usichukue
hatua peke yako bila mimi.” “Samahani Geb. Niliingiwa na hofu ya kupita kiasi.
Nitajitahidi kufanya hivyo.” Wakatulia kidogo.
“Naomba basi na wewe ule.” “Huo mtori sitauweza Nanaa.
Nimeona karoti na maganda ya nyanya vinaniangalia kabisa. Siwezi.” Nanaa
akacheka huku akimtizama. “Basi labda nikutolee hivyo vitu.” “Mmmh! Kwani
siwezi kuagiza chakula hapa?” “Utakula?” Geb akacheka. “Ngoja nijue MENU yao
kwanza. Ndipo nitajua chakuagiza. Kwanza muda umeenda sana.” “Lakini lazima ule
Geb.” Geb akacheka huku akiiendea simu ili kuwapigia watu wa mgahawani. Akapata
kitu anachotaka kula. Akaagiza kiletwe huko chumbani pamoja na chips yai ambayo
haijakauka sana, na nusu kuku. Nanaa akacheka. Akajua ameagiziwa tu yeye.
Ukipenda Boga.
“Sasa itakuaje?” Swali hilo Nanaa alilikazania, akitaka
kujua hatima yake. “Kwanza nataka ujue hivi.” Geb akarudi pale kitandani. “Adui
au niseme shetani, anapenda sana kuishi sehemu isiyo na amani. Baba yangu
alinifundisha kuwa, amani inamtindo wa kukaribisha kila kitu chema ndani ya
nyumba. Na ikiondoka, pia inamtindo wakuondoka na kila kitu chema. Wakati
mwingine mpaka utajiri.” Nanaa akaelewa kile anachotaka kuongea Geb.
“Najua mama amekuumiza Nanaa. Naomba msamehe. Namuombea
mimi msamaha. Amekosa, naomba msamehe. Na kama huna sababu yeyote ya kumsamehe
mama, basi naomba iwe mimi. Msamehe kwa ajili yangu. Naomba yaishe.”
Nanaa akajisikia kuumia zaidi moyoni. “Nimesamehe Geb. Japo ni kweli
sikutegemea! Lakini basi.” Geb akajiweka sawa.
“Naomba usinifikirie kuwa namtetea. Nataka kukwambia ukweli
Nanaa. Mama anakupenda sana wewe. Aliyasimulia hayo yote, akitaka kuonyesha
ubaya wangu kwa Grace baada ya kufika nyumbani, kumkuta mtoto halafu wewe
haupo, umelala hotelini sababu nilikupa masharti ya kutorudi nyumbani
ikishavuka saa 12 jioni. Mama alikuwa akikutetea. Grace alichukia sana. Yaani
wote, mpaka Danny, walinisema usiku ule mpaka nikajisikia vibaya. Wale watu
wanakupenda sana Nanaa. Hakuna hata mmoja wao anae kuchukia.” “Basi Geb.
Yameisha. Nitatafuta kuzungumza na mama pamoja na Danny pia.” “Hapo utakuwa
umefanya vizuri. Nakushukuru.” Geb akatulia.
Suluhisho la Mira.
“Tukirudi kwenye swala la Mira. Huyo ni lazima nikaonane
naye. Ameacha kuja kazini. Hata leo hakuja kazini. Nitaulizia nyumbani kwake,
nita...” “Geb!” Nanaa akashangaa. “Itabidi kufanya hivyo Nanaa. Sina jinsi.
Yapo mambo yakuombea na kumuacha Mungu afanye. Lakini yapo mambo inabidi
kumruhusu Mungu kutenda kupitia wewe mwenyewe. Huyu binti anasema yupo kwenye
ndoa na mimi kwa ahadi niliyomuwekea mimi mwenyewe. Sasa nilazima nizungumze
naye, tuwekane sawa.” “Naogopa Geb!” Nanaa alishaweka mpaka bakuli la mtori
chini, kwa hofu.
“Akikurushia tena madudu yake!?” “Hana nguvu hiyo tena.
Nimekwambia. Hakuna silaha itakayoinuka kinyume yetu, ikafanikiwa tena. Mungu
ameahidi kupigana vita yetu. Alipigana naye au alipigana na madudu aliyokuwa
amekutupia, mpaka ameshinda. Mungu alikuletea ushindi pale pale
hospitalini. Sasa unafikiri ni nini alichobakisha kama sio sisi kuendelea
kutenda kazi pamoja naye?” Geb aliongea kwa kujiamini sana mpaka Nanaa akaanza
kutulia.
“Kuna kitu Grace amekiongea leo. Anasema hadhani kama Mira
yupo sawa. Anasema siku ya kwanza ulipokuwa hospitalini alikuwa na furaha sana
pale kazini. Alikuwa akicheka, akiwa chini mpaka mtu wa juu anasikia. Lakini
siku ya pili yake, alifika kazini kama mgonjwa. Na hajarudi tena. Sasa huwezi
kujua vita hiyo aliyopigana na malaika wa Mungu alishindwa kwa namna gani!
Hutujui yupo kwenye hali gani! Halafu
wanasema yale madudu yanamtindo yakurudia watu. Sasa ukute ubaya aliokutendea wewe,
ndio umemrudi na yeye. Sasa hivi anatapatapa.” “Akirudi huku anakulilia shida?
Au umkute mgonjwa ukamuhurumia? Labda hana kazi anahitaji msaada wako? Halafu
anakukumbusha vile alivyokusaidia nchini India?” Nanaa akauliza.
“Nanaa! Nina jukumu mimi kama baba na mume. Nikishindwa
kuwalinda nyinyi, ujue sistahili kuitwa baba wala mume. Sitaruhusu historia
yangu ya nyuma iwaathiri watoto wangu wala wewe. Nahangaika ili nyinyi msipite
nilipopita mimi. Siwezi kumruhusu tena kuwa karibu na nyinyi. Hata iweje.
Kwanza nikirudi tu Dar, nitakwenda polisi.” “Geb!” Nanaa akashangaa.
“Kabisa Nanaa. Nitaenda kumshitaki kwa vitisho vyote
alivyokutumia. Na kuomba ‘restraining
order’ juu
yake. Kwako na kwa familia yangu. Nitamfuata nikiwa na hiyo ‘restraining order’. Nitampiga marufuku na kumwambia,
chochote kibaya kitakachokupata wewe, watoto wangu na ndugu zangu wote, yeye
ndio atakuwa mtu wa kwanza kukamatwa.” “Akikuomba msamaha je?” “Nitamsamehe au
nilishamsamehe tokea siku nilipojua amekutendea wewe ubaya. Lakini haibadilishi
chochote kile. Bado sitamruhusu kuwa karibu yetu. Nitampiga marufuku na
kumwambia wazi kabisa. Jumbe zake za vitisho na picha zote za mwanangu
alizochukua ofisini kwangu bila ruhusa yangu, vimehifadhiwa polisi na kutaarifu
vyombo vya usalama kuwa, chochote kitakachotupata sisi, yeye ni
muhusika. Hata kazini au kwenye ofisi zangu, hataruhusiwa tena kusogea.
Nikimuona tu, au nikiambia alionekana karibu na nyumbani kwetu au jengo letu
lolote, nitamwakikishia atakuwa hatiani.” Nanaa akaridhika. “Asante Geb.
Angalau moyo wangu umetulia.” Nanaa alisikika ametulia kweli kweli.
Suluhisho Juu Ya Zinda
Akamuona amekunja uso kama amekumbuka kitu. “Nini?” Geb
akauliza. “Itakuaje juu ya Zinda?” Wakasikia mlango wao unagongwa kabla ya Geb
kujibu. Geb akajua wanaletewa chakula. Akasimama. Akavaa rob nyingine iliyokuwa imening’inizwa, akaenda
kufungua mlango. Alikuwa muhudumu aliyekuwa amevalia nadhifu, na sinia la
vyakula. Geb alipokelewa na tabasamu. “Naomba uweke hapo mezani tafadhali.” Geb
akampisha mlangoni, yule muhudumu akapita. Harufu ya chakula, ikaanza kuenea
hapo ndani. Nanaa akasimama.
“Kunanukia vizuri!” Geb akacheka. Alimjua Nanaa jinsi
anavyopenda kula. Geb alimpa pesa kidogo yule muhudumu aliyeleta chakula.
Ilikuwa tip nzuri iliyoonyesha kumfurahisha huyo muhudumu. Alitoa shukurani kwa
Geb kwa kurudia rudia huku akisisitiza kama watahitaji kitu chochote, wasisite
kupiga simu mapokezi na kumuulizia yeye, huku akirudia rudia kujitambulisha
jina lake kwa kirefu na kifupi. Geb akashukuru tena, akatoka.
Akaenda kukaa kwenye kochi alilokuwa amekaa Nanaa. “Umeuliza
juu ya Zinda. Niwe tu muwazi Nanaa, sijapata jibu. Sijajua nifanye nini
juu ya Zinda. Ananisumbua kichwa changu, kwa kuwa nahisi kwa mara ya kwanza
maishani mtu wa karibu yangu, anahusika katika kukwamisha mpango wangu. Au
niseme, kwa mara ya kwanza maishani napanga mpango wa muhimu sana, uliobeba
hatima yangu. Mpango uliojaa furaha yangu, naona unakwama. Na mbaya zaidi sijui
chakufanya. Nimebaki kumuomba tu Mungu.” Nanaa alianza kunywea.
“Kwa hiyo hudhani kama tutafunga tena ndoa yetu?” Nanaa
akauliza. “Sina mpango wa kumfikisha mwanamke mwingine yeyote yule kanisani na
kumpa kiapo changu cha maisha au niseme sina mwanamke mwingine nitakayeweka
naye agano la mpaka kifo, isipokuwa wewe Nanaa. Lakini sijui lini!” “Kwa
nini tusiende kwenye vyombo vya sheria?” Nanaa akahoji. “Nimezungumza na
mwanasheria. Nimemtumia mpaka picha ya kile cheti cha harusi ambacho Zinda
anasema mlifunga ndoa. Yule mwanasheria akasema cheti kinaonekana ni halali,
lakini tunaweza kumshitaki na kumkana. Kesi itapelekwa mahakamani na wewe
utatakiwa kuonyesha ushahidi wako, kumpinga. Yeye anao mashahidi wa muhimu
sana. Mwanamke anayetambulika kama mama yako, yuko upande wake. Achilia mbali
huyo mama yako mkubwa, kina Viola pia wapo upande wake.” “Lakini na mimi nina
ushahidi wa hospitalini! Kuwa siku ile nilikuwa kwa daktari.” Nanaa akaongeza.
“Nilimwambia hivyo huyo mwanasheria. Akasema inawezekana
ukawa ushahidi. Au Zinda akatengeneza stori nyingine.” “Stori gani tena!?”
“Nanaa, hivi unajua hapo Nairobi ni karibu sana? Na wala huhitaji Visa, au
masaa mengi kufika hapo. Na kufungishwa ndoa hakuchukui muda mrefu. Hata dakika
15 ni nyingi. Mnaweza mkafungishwa ndoa na kurudi hapa nchini siku hiyo hiyo.
Kwa hiyo anaweza kusema mlikwenda na kurudi.” Nanaa akapooza na kuishiwa
maneno.
“Wewe ni mjamzito. Sitaki uanze kuhangaika mahakamani,
unashindana na watu waliokusudia kukuangamiza Nanaa. Sitaki tena upitie kwenye
kelele za kina Viola. Sitaki ile hali ya kunyanyasika, ujisikie wanakuonea maishani,
ikurudie tena. Halafu sasa hivi iwe mahakamani, mbele za watu! Sidhani kama
hata na wewe upo tayari kwa hilo. Sasa hivi tuna watoto, tupo pamoja, kitu
kinachowaumiza wao. Ni mke wangu kihalali kwa kuwa nimeshakulipia mpaka mahari,
na Mungu anajua.” “Na hicho ndicho nilijua kitatokea tu Geb. Tukishazaa
ndio basi tena.” Nanaa aliongea kwa kulalamika kidogo.
“Hivi unafikiri ni wewe peke yako ndio unahamu ya ndoa? Au
unafikiri unaweza ukanizalia watoto hawa, halafu nikaamua kuwatafutia wanangu
mama mwingine!?” Nanaa akajifuta machozi. “Siwezi kufanyia hivyo wanangu wala
nafsi yangu. Kwanza natafuta nini tena? Mwenzio katika swala la kutafuta
mwanamke nimeshafunga hiyo shuguli. Kicho kipengele nimeshakitia tiki.
Nimekimaliza. Sasa hivi nasonga mbele. Labda kama wewe mwenzangu bado
unaangalia nje.” “Hapana Geb!” “Basi nakuomba tuwe wavumilivu tu kwa sasa.
Tutunze kile Mungu alichotubariki nacho, huku tukimsihi atuvushe katika hili.
Siku moja tuje kufunga ndoa. Lakini kwa sasa naomba tufurahie hii baraka Mungu
aliyotupa. Upendo wa kweli katikati yetu. Jinsi alivyotuamini na kutupa watoto.
Tufurahie uwezo aliotupa wa kuzungukwa na watoto wetu wenyewe wa kuwazaa. Mungu
anajua nia yetu Nanaa. Hajawahi kushindwa. Na ninauhakika hana mpango wa kuanza
kushindwa kwenye mambo yetu. Zaidi katika hili la ndoa. Maana mengine yote,
ametuonyesha mkono wake upo juu yetu. Tusubiri tu.”
“Nitasubiri Geb. Na ninashukuru kwa kuanza kulifuatilia hata
huko kwa mwanasheria. Na kunifikiria na mimi kutosimama mahakamani na kuendelea
kudhalilishwa na mama mkubwa na watoto wake. Asante.” Nanaa akashukuru kwa
upendo, Geb akajisogeza, na kumbusu begani.
Kwa akili zao, wapenzi hao
wamefika mwisho. Hawajui tena watafanya nini juu ya ndoa yao. Wamebanwa kila
upande. Mazingira yote yamesema hapana kwa kuhalalisha ndoa yao. Nini kitaendelea?
Hata jaribu hilo nalo aliokusudia shetani, kuwasambaratisha, ameshindwa.
Pengine Amani itarejea kwa
kina Magesa kwa kuwa Nanaa amekubali kusamehe, lakini mambo mengine je?
Amani Hutafutwa Kwa
Nguvu Ikiwemo kujishusha, na wakati mwingine hata kukubali mambo yaishe.
Itakuaje Mbeleni?
Mengi, Mazito yanakuja
mbeleni.
Usiache kufuatilia.
0 Comments:
Post a Comment