Nanaa alikuwa amejifunika shuka amelala. Geb na
yeye akavua nguo akapanda kitandani. Akamsikia analia taratibu. Akajisogeza
karibu naye. Kwa kuwa alikuwa amegeukia ukutani, akajinyanyua mpaka kwenye
masikio yake. “Nakupenda Nanaa! Amini ninakupenda na ninathamini kila muda
Mungu anao nijalia kuwa na wewe. Unisamehe pale nilipoonyesha upendeleo
wowote. Nia yangu ni kuhakikisha kuna amani.”
“Najua mama anakupenda kwa hakika. Ila kuna
maisha ambayo tulikuwa tukiishi zamani, hapakuwa na usiri kati yetu.
Nahisi ni udhaifu wetu. Na wote wamejifunza kwa hiki kilichotupata. Ndio
maana unaona ni kama pale nyumbani amani imepotea. Danny anajilaumu
sana. Nilichokuwa nikitaka kutoka kwako ni uwasamehe, yaishe. Sikuwa na nia
yakuwatetea.”
“Hata mimi nimeathirika Nanaa. Wamechangia
kwa asilimia kubwa kusimamishwa kwa harusi yetu. Lakini namuamini Mungu,
atatufanikishia tu. Naomba usinichukie. Nipo upande wako mpenzi wangu.
Sipo kinyume na wewe.” Nanaa akanyamaza. Geb alimuona anajifuta machozi, bila
kujibu kitu. Akambusu shingoni na kujivuta zaidi karibu yake,
akamkumbatia.
~~~~~~~~~~~~~
Nia ya Geb ilikuwa kuzungumzia mambo mawili. Juu ya
hilo la Zinda, Danny na Mama yake, pamoja na la Mira. Lakini kwa jinsi Nanaa
alivyopokea habari za watu walioshiriki kutoa habari za ndani na kumpa Zinda,
akaona habari za Mira zisubiri kwanza. “Hata
malaika alishindwa kumwambia. Heri na mimi ningojee kwanza. Nisije nikaharibu
zaidi.” Geb akawaza. Akaamua kulala.
Usiku huo hapakuwa na mapenzi wala
busu. Hapakuwa na kuomba pamoja wala Geb hakukumbuka kuomba peke yake. Tayari
na yeye alisha changanyikiwa na shutuma alizotupiwa na Nanaa.
Nanaa alimuweka na yeye kwenye kundi la wasaliti wake. Hakumuhesabu
upande wake kitu kilichomuumiza na kumchanganya Geb zaidi. Mpaka Nanaa
analala, amekiri kwake ile safari yote aliyokuwa akiifurahia pale mbugani,
akidhani ilikuwa kwa ajili yake ili kumfurahisha, kumbe nia ilikuwa
kuja kutetea familia yake. Hilo nalo lilimuumiza Geb. Inamaana
furaha yote aliyojenga moyoni mwa Nanaa kwa siku tatu mfululizo, imefutika!
~~~~~~~~~~~~~
Nanaa aliamka asubuhi na mapema. Hiyo ilikuwa siku
ya 4, tokea wafike hapo. Ilikuwa ni siku ya jumapili. Geb akamsikia, amekaa
kitandani. “Mbona mapema hivyo?” Akauliza. “Si ulisema tunaondoka leo? Ndio
nakusanya vitu. Samahani nimekuamsha.” “Hamna neno. Nilifikiria tuondoke hata
jioni.” “Kwani kuna kitu kingine tena unataka kuniambia?”
“Nanaa!” Geb aliumia zaidi.
“Nauliza tu!” “Sikukuleta huku kwa ajili ya kukupa
habari zitakazo kuumiza! Nilitaka muda na wewe.” “Naomba usinidanganye
Geb.” “Sawa. Nilitaka tuje tuzungumzie na hilo pia. Lakini zaidi nilitaka muda
na wewe.” “Basi nitakuwa hapo nje. Nataka nitembee tembee kidogo wakati nyinyi
mmelala. Nitarudi baadaye kidogo.” Geb akajirudisha kwenye mto, akafunga macho.
Nanaa alisimama pale kwa muda. Geb hakuwa amesema
ndiyo au hapana. “Geb! Natoka nje.” Akamgeukia. “Nakuhitaji Nanaa.” Akamuona
Nanaa anavua nguo zote, anarudi kitandani. “Sio kwa namna hiyo Nanaa! Kufanya
mapenzi na mimi sio lazima. Sitaki uone unawajibika! Si jukumu
unalotakiwa kulitimiza kwangu. Na nikikwambia nakuhitaji sio kwamba nakuhitaji
kufanya mapenzi. Nakuhitaji kwenye maisha yangu.” “Sawa.” Nanaa akapanda
kitandani, akajifunika shuka, akatulia.
“Nanaa!” Nanaa akageuka, machozi yakimtoka.
Akajifuta. “Abee!” “Pole.” Geb aliongea kwa
upole na upendo. “Pole sana. Lakini naomba tusitengane sababu ya makosa
ya watu wengine. Naomba usinichukie. Kumbuka na mimi nimuhanga wa
hayo makosa. Harusi ilikuwa ni yangu pia. Ninataka sana kukuoa Nanaa.
Nakuhitaji kwenye maisha yangu.” “Sijakuchukia
Geb. Ila nimeumia sana. Sikutegemea. Nilijua nimepata mtu wa kumueleza
chochote kinachoendelea kwenye maisha yangu au hata moyoni mwangu. Nimeumia
kujikuta narudi kuishia kuwa na kaka tu! Maisha yangu yameshindwa kabisa
kuniongezea mtu mwingine!?” Geb
alizidi kuumia. Akaona hata yeye hakutajwa hapo. “Pole.” Ndilo neno aliloweza
kujibu akiogopa kuongeza neno jingine asije haribu.
Nanaa alipanda kitandani kwa
hasira akiwa uchi kabisa. Kama aliyekuwa akitaka kutimiza wajibu. Lakini Geb
akamtuliza. Alimsogelea karibu, akambusu kidogo tu shavuni. “Pole sana.”
Akabaki akimwangalia. “Asante.” Akamfunika
shuka vizuri. Nanaa akashangaa anajilaza kwenye mto bila hata kumpapasa. “Njaa
inakuuma?” Akamuuliza. “Hamu ya kula imeisha kabisa. Nasikia tumbo limejaa.
Sina hamu ya kuweka kitu chochote mdomoni.” Geb akajua bado ana hasira.
“Basi tulale kidogo. Labda ukiamka
utasikia njaa. Na sio lazima tule hapa. Tunaweza kwenda kula sehemu nyingine.
Jaribu kupumzika.” Mikono ya Geb ilikuwa juu ya shuka. Akamtengeneza lile shuka
vizuri. Kama anayemtayarisha kulala. Nanaa naye akajiweka sawa, akarudi kulala.
~~~~~~~~~~~~~
Waliamshwa na Oliva saa 4:37asubuhi. Alikuwa akiongea
huku akipuliza. Nanaa akacheka. “Fizi zinamuwasha huyo!” “Naomba ukaongee naye
kidogo. Jana alijua nimekuudhi. Hakutaka hata kunichekea!” Nanaa
akatoka. Alipomuona tu mama yake akaanza kucheka. Akakaa. “Na mimi nina hamu na
wewe Liv!” Geb akamsikia anacheka.
“Ulilalaje?” Liv aliendelea
kucheka. “Njoo upate nyonyo kwanza.” Akamtoa pale kitandani. Akambusu.
“Muone unavyotokwa mate! Meno yanataka kutoka ndio maana fizi zinawasha Liv.
Pole kipenzi chagu. Ukinyonya nitakupa ile toy yako yakukunia fizi. Sawa?”
Oliva alizidi kumchekea mama yake. “Unapendeza ukicheka wewe! Usiwe
unanuna bwana. Umesikia Liv?” Geb alisikia wakizungumza. Akabaki akiwaza pale
kitandani.
Alijua kwa hakika Nanaa ameumia
sana. Maisha yatakuaje baada ya hapo kati yake na mama yake! Ndio
kitu kikaanza kumuumiza kichwa. “Nanaa
atarudi kuwa rafiki wa karibu tena wa mama?” Geb akawaza. Kwa ukaribu
aliokuwa nao Nanaa na Mama G, ungependa tu uwepo nyumbani kwao. Vilijaa vicheko
kila wakati. Nanaa alikuwa akiishi na mama G kama rafiki yake wa karibu wala si
mkwe. Alifanya chochote mbele yake bila hofu. Ukiwakuta pamoja, ungeweza
kufikiri Geb ndio mkwe halafu Nanaa ndiye kiziwanda cha Mama G. Oliva alilelewa
na bibi yake kwa mapenzi makubwa sana. Lakini hapo napo kukatupwa jaribu
lake.
Geb akaendelea kuumia. Alichukia
ile hali. Wasiwasi ukazidi kumtesa. Kwa Danny haikumsumbua. Nanaa
hakuwa karibu sana na Danny, lakini si mama yake. Akabaki akiwaza. Akamchukia
shetani na kazi zake zote. Hakuacha wapumzike hata kidogo! Ni
jumapili iliyopita tu, siku kama hiyo, Nanaa aliamka na miguu iliyoharibiwa
vibaya sana. Huwezi kusema imeoza, kwa kuwa haikutoa harufu. Lakini na jumapili
hiyo nayo, wameamka wakiwa wamesambaratishwa mioyo. Nanaa hakumuhesabu
upande wake. Akazidi kuumia. Akachukia visasi alivyovianzisha Zinda.
Swali la atafanyaje likaanza kumsumbua. Akajua kama harusi haitafanyika kwa
haraka, ndio Nanaa ataona madhara yake zaidi.
~~~~~~~~~~~~~
“Twende
ukamsalimie dad.” Wakamtoa Geb kwenye mawazo. Nanaa akaingia na mtoto wake pale
chumbani. Hapakuwa na mlango. Kwa hiyo alipitiliza na kumuweka Liv kifuani kwa
baba yake pale alipokuwa amejilaza. Oliva akaanza kumchekea. “Unatoa tu
maziwa!” Geb akamfuta. “Naona alikuwa na njaa. Amenyonya kama
anakimbizwa!” Nanaa na yeye akajiweka pembeni. “Au ulikuwa na hamu na
mama?” Geb alimtekenya kwa kuweka kidole chake kwenye dimpozi yake.
“Halafu fizi zinamuwasha. Anahangaika kweli!”
“Hivi tulikumbuka teething toys zake?” Geb akauliza. “Nilibeba. Sema zile
anazozipenda, zakuweka kwenye friji ndio niliacha. Nilijua huku hakutakuwa
na friji.” Nanaa akajibu huku akimfuta maziwa na mate yaliyokuwa
yakimtoka Oliva. Meno ya mbele mawili ya juu na chini yaliyokuwa yakimpendeza
sana Liv, yalishatoka tangia anatimiza miezi mitano. Geb akasimama akiwa
amemkumbatia mwanae. “Twende tukafuate toys zako nyingine utafune.” Nanaa
akaamua kuvaa. Alikuwa amejifunga khanga wakati ameenda kumfuata Liv.
Geb alimuona akivaa. Akatamani
aombe penzi la mwisho hapo hotelini, lakini akaamua ajikaze tu. Na
yeye Nanaa akajiuliza mbona haombwi tena! “Naona nivae kabisa, ndipo
nimuhudumie na Liv.” Akajisemesha akitarajia kuambiwa subiria. “Sawa. Wakati
unamvalisha yeye, na mimi nikaoge. Ndipo tukapate kifungua kinywa.” Geb
akajibu. Nanaa akatulia kidogo. “Kwani ulitaka tuondoke saa ngapi?” “Najua hamu
ya kukaa huku na mimi, imeshakuisha.” “Hapana Geb!” “Naelewa Nanaa. Sikulaumu.
Muda wowote utakaotaka tuondoke, tunaweza kwenda tu.” Nanaa akanyamaza. Hakujua
ajibu nini.
Dar.
Waliingia jijini mida ya saa kumi jioni. Mlinzi
akafungua geti bila kuchelewa. Lakini hawakukuta magari ya watu wengine ila ya
Geb. Hapo hapo Geb akampigia simu mama yake. “Uko
wapi!?” “Kwa Grace. Namsaidia kuweka mambo sawa. Walirudi kwao jana.
Sasa namsaidia usafi, kupika na mambo mengine. Nitarudi kama kwenye saa moja
hivi. Vipi nyinyi?” Mama G akauliza. “Salama.
Lakini sikujua kama kina Grace wataondoka mama! Hajaniaga!” Geb alilalamika kidogo.
“Mwache mwinzio atulie kwake. Ulitaka
akae hapo mpaka lini?” “Naona ni mapema sana mama!” “Hivi unajua huyu Grace ni
mke wa mtu? Mwache ajenge kwake.” “Watoto watatu bila mtu mwingine!?” Geb aliendelea kulalamika. “Ndio kukua huko. Tutaongea vizuri baadaye.” “Kuna kitu
mnataka niwasaidie nije?” Geb akauliza. “Sidhani.
Kama kipo watakupigia. Lakini wewe pumzika na familia yako. Mimi nitarudi
kwenye saa moja.” “Usichelewe sasa mama!” “Umeanza Geb.” “Naomba usichelewe.” Nanaa
alikuwa akiwasikiliza bila ya kuongeza neno.
Alikuwa amekaa kiti cha nyuma na mtoto wake,
akamtoa. Liv akafungua macho. “Bado una usingizi?” Nanaa akamuuliza. “Twende
ukalale na mama.” Alimbeba mtoto wake mpaka juu chumbani kwake. Akambadilisha
diaper na nguo, akapanda naye kitandani. Geb akamkuta amemkumbatia Oliva
wamelala. Kitu ambacho sio cha kawaida. Liv alishazoezwa kulala peke yake,
kitandani kwake. Kitanda hicho ni cha Geb na Nanaa tu. Akilala hapo Oliva ni
mara chache sana, tena wanacheza na baba yake tu. Hata mchana alilala
kitandani kwake.
Geb akabaki amesimama pale akimwangalia Nanaa na
mtoto wake. Akaamua anyamaze tu. Akaenda kujilaza kwenye makochi. Usingizi wa
mimba ulimchukua Nanaa, akalala kama mzigo. Alilala akiwa na mawazo. Na ni
kweli alipoteza hamu ya kula kabisa.
Geb alimuasha ilikuwa saa mbili na nusu usiku.
Akaangalia pale kitandani Oliva hakuwepo. “Twende ukale.” Geb alimuongolesha
kwa upendo. “Nataka nioge kwanza. Najisikia mwili umechoka sana.” “Pole.
Labda safari. Ukioga utajisikia vizuri.” Nanaa akajitoa pale kitandani kwa
shida, akaenda kuoga. Alipotoka bafuni, Geb hakuwepo pale chumbani. Akaamua
arudi tu kulala. Hakujua akitoka pale chumbani, ataenda kuongea nini na mama G.
Akaona ni heri arudi kulala tu.
Alipojiweka tu kitandani, akapitiwa tena na
usingizi. “Nanaa!” Geb akaingia tena na kumuamsha. “Amka ukale
japo kidogo. Mama amerudi na chakula.” “Sijisikii vizuri Geb. Naomba nilale tu.
Nitakula kesho.” Nanaa ambaye alikuwa hashibi masaa machache
yaliyopita, gafla hawezi kuweka kitu
mdomoni! Hataki tena kula. “Jikaze kidogo tu.” “Nina usingizi sana.
Nataka kulala tu. Ila naomba uniletee Liv aje anyonye kabla ya kwenda kulala.”
“Sidhani kama ataweza kunyonya. Bibi yake alimpikia ndizi. Amezisaga na samaki.
Nimemlisha, naona amekula sana.” Nanaa akacheka kidogo. “Basi kesho. Naomba
nilale.” Geb akabaki amesimama pale kwa muda. Nanaa alishafunga macho
kuashiria anataka kupumzika sio tena maongezi. Baada ya muda akamsikia Geb
anatoka.
Jumatatu.
Akiwa usingizini, kwa mbali akasikia busu la
mdomoni. Nanaa akafungua macho. “Nataka kwenda kazini.” “Kwani sasa hivi ni saa
ngapi?” Geb akacheka. “Saa moja asubuhi.” Nanaa akakaa kwa haraka. “Sasa
umekula nini!?” Nanaa alipitiwa na usingizi, hata uji wa Geb hakuamka
kuupika. “Mama alishaniandalia.” “Samahani nimepitiwa na usingizi.” Geb
akambusu. “Usijali. Ila uamke hapo kitandani ukale.” “Nitaamka. Maziwa yamejaa,
nataka nioge, Liv akiamka anyonye.” “Basi toka hapo kitandani sasa hivi,
lasivyo utapitiwa tena na usingizi.” “Nitaamka. Kazi njema.” “Nitarudi mchana
tuje tule wote.” Nanaa akatulia kidogo.
“Unataka nikuletee nini?” Geb akauliza. “Nimepoteza
hamu ya kula kabisa Geb. Sijisikii kula hata kidogo!” “Labda ni hiyo
hali ya ujauzito.” Geb akamshika tumboni. “Labda. Nitamtafuta yule daktari
aliyenisaidia wakati wa ujauzito wa Liv.” “Naomba na mimi unishirikishe kwa
karibu Nanaa. Nataka tuwe tunakwenda wote.” Nanaa akacheka kidogo. “Sawa. Uwe
na siku njema.” Geb akambusu tena, na kutoka.
~~~~~~~~~~~~~
Aliingia kuoga. Akasafisha meno,
ndipo akashuka huku akiwaza kukutana na mama G. Hakuwa amemuona tokea watoke
safari. Alimsikia akiimba jikoni. Akaingia. “Shikamoo mama.” Hapakuwa na
tabasamu wala kicheko. Salamu hiyo aliitoa Nanaa akiwa mlangoni, tena amepooza
sana. “Marahaba Nanaa mwanangu. Umeamka salama?” “Ndiyo.” Nanaa akajibu, kisha
akanyamaza.
“Kaa ule.” “Asante.” Akaingia hapo
jikoni. Akasogea mpaka kwenye jiko. Akamimina uji aliokuwa amepikiwa Geb.
Akaweka kwenye microwave ili kupasha. Mama G akaona ule ukimya usio wa kawaida.
Akajua Nanaa amemkasirikia tu. Wakati anasubiria uji wake upate moto,
akaendelea kuchezea simu yake bila kuongea chochote. Kidogo kengele ya
kuashiria uji wake umekuwa tayari hapo kwenye microwave ikalia. Akautoa uji,
akaenda kukaa mezani. Hapo hapo ndani jikoni. Kimya.
Hakuna Kulala.
Wakati mama G anataka kuzungumza
na Nanaa, simu yake ikaita. “Haloo!” Nanaa
akapokea. “Ni Nanaa?” Mtu wa upande wa pili
akauliza. “Kwani wewe unamtaka nani?” Nanaa
akauliza. “Nina shida sana ya kuongea na Nanaa?”
“Wewe ni nani?” “Mira.” Akajitambulisha. “Mira!?”
Nanaa akauliza akiwa kama hajaelewa vizuri hilo jina. “Ndiyo mimi naitwa Mira.” Mama G akashituka
sana. Akaangusha mpaka glasi. Nanaa akamwangalia, na kurudisha mawazo kwenye
simu.
“Umesema Mira kama kioo!?”
“Ndiyo.”
Mira akajibu. “Mmmh! Mbona mimi sikufahamu? Unasemaje?”
“Nataka kukutaarifu kuwa mimi ni mke HALALI wa Geb.” Nanaa
akatulia. “Unanisikia Nanaa?” “Nakusikiliza.” “Ndio
hivyo. Unatakiwa ujue na uachane na mpenzi wangu. Geb nimetoka naye
mbali sana. Tokea tunasoma nchini India tulikuwa tukiishi naye. Aliniacha
nchini India nikiwa nasoma. Yeye alipomaliza akaniaga kuwa anarudi kuanza
kutafuta maisha huku. Ameniacha na baraka zangu zote. Nikikata tu simu,
nitakutumia picha zangu na Geb ili uamini vizuri na ujue sio kwamba nakurusha
tu roho. Ni kweli ni mume wangu.” Mira akaendelea.
“Nimemaliza chuo, nikarudi huku akanipa
na kazi. Tupo naye kwenye biashara zetu. Maisha yetu yanaendelea kama
kawaida. Sitaruhusu wewe wala mwanamke mwingine aingilie mapenzi
yetu. Nakuonya ukae mbali na Geb. Tuna maagano ya mpaka kwa mizimu
inanitambua mimi kuwa ni mke wa Geb. Nakuonya na kukutaarifu kabisa.
Mizimu haitakubali wewe ukavunja AGANO letu.” Nanaa alibaki akimsikiliza.
“Bila shaka umeshapata onyo la kwanza.
Umerudishiwa miguu yako kwa kupewa nafasi ya pili ya maisha. Nakusihi uitumie
vizuri. Itakapo kurudia tena, utajuta Nanaa. Hutakaa ukatoka kitandani
mpaka kifo chako. Nakusihi acha kucheza na ndoa za watu. Mwache
Geb. Kama ni huyo mtoto, tutamlea. Lakini ujue sitarudia kukuonya tena.
Kaa mbali na Geb. Ni mume wa WANGU.” Mwili mzima wa Nanaa ulianza kutetemeka. Akagundua
kumbe mwanamke wa Geb ndio alihusika kumuwekea ukilema! “Kwa nini Geb hakuniambia?” Nanaa akajiuliza na kuumia sana.
Wakati akimsikiliza Mira, akamsikia Oliva akilia.
Akakata ile simu, akakimbilia chumbani kwa mama G alipokuwa amelala mtoto wake.
Akakuta amesimama. “Kwani umeita sana?” Nanaa akamuuliza mwanae wakati
anamchukua. “Pole. Nilikuwa naongea na mtu kwenye simu. Umeamka salama?” Nanaa
aliendelea kuongea na mwanae. “Njaa inauma? Eti Liv? Usikasirike bwana!
Sikukusikia kipenzi changu. Njoo unyonye, labda utajisikia vizuri.” Akambusu,
na kumuweka kwenye ziwa.
Mama G akaingia wakati Nanaa ananyonyesha. Akabaki
ameduwaa. Nanaa hakuongeza kitu chochote. Akabaki ameinama akimnyonyesha
mtoto wake huku akimchezea nywele. Liv alikuwa akinyonya kwa uchu
wote, Nanaa ametulia kimya. Mama G alijua wazi mambo yamebadilika.
Nanaa wa zamani angeshaanza kumsimulia juu ya ile simu. Lakini Nanaa
huyu alitulia kana kwamba hapakuwa na jambo. Akasimama pale kwa muda
mfupi, akaamua atoke.
“Nataka nimuogeshe huyo, niende
kwenye biashara yangu mara moja. Sitakawia.” “Hamna neno mama. Wewe nenda tu.
Nitamuogesha. Ukirudi ukiona sijamtakatisha mjukuu wako, mtaogeshana tena
usiku.” Mama G akacheka kidogo. “Ule basi. Chakula kipo kingi tu kwenye friji.
Na cha Oli nimeweka kwenye chupa yake. Leo nimemsagia kiazi na mboga za
majani.” “Haya. Asante mama.” Nanaa akarudisha macho kwa mwanae, akanyamaza.
Kwa Geb.
Kitu cha kwanza alipoingia tu kwenye gari yake,
akampigia simu Geb. “Kwema?” Geb akauliza. “Hivi ulishazungumza na Nanaa, habari za Mira?” “Hapana mama.
Nilianza na kuzungumza naye habari za Zinda kwanza. Mambo ya Mira nimeona yasubiri
kwanza.” “Kwa nini!?” Mama G akahoji. “Nanaa
ni mjamzito mama. Ametoka kwenye kuumwa, akakutana na habari za Zinda. Zote
zikionyesha kuwa wewe ndio umetoa maneno humo ndani. Ilibidi kumuweka kwanza
sawa na kuandaa mazingira ya kumwambia mambo ya Mira.” Mama G akanyamaza
kidogo.
“Kwa nini unaniuliza?” Geb akauliza, lakini kimya.
“Mama?” “Mmmh! Sijui nifanyaje Geb!
Nashindwa kukwambia. Asije akasema tena nimekwambia mambo yake.” “Kwani kuna
nini? Mbona sauti yako si yakawaida, imejaa wasiwasi?” “Nitakwambia.
Lakini naomba uniahidi hutamwambia Nanaa habari hizi.” “Nini?” Geb akahoji zaidi.
“Mira amempigia simu Nanaa sasa hivi.
Ameongea naye kwa kirefu tu. Nimemsikia akijitambulisha kama yeye ni mke wako
na mpo kwenye maagano ambayo hata mizimu inatambua. Amemuahidi
kumtumia picha kama uthibitisho wa mahusiano yenu. Na amemwambia alishapewa onyo
la kwanza akalazwa mpaka hospitalini. Onyo jingine, amemwambia hatakaa atoke
tena kitandani mpaka kifo.” “Mungu wangu!” Geb alisikika kwa sauti ya juu
ya kushituka sana.
“Sasa sijui utafanyaje Geb! Ni mbaya
sana kwa Nanaa kusikia kutoka kwa Mira. Ni heri angekusikia wewe mwenyewe
kwanza. Na nimemsikia akimtambia kuwa anafanya kazi na wewe. Yaani ni kama
umemuweka hapo kama mwenzio. Amemwambia ni biashara yenu.” “Mungu
wangu nisaidie!” Geb alisikika akimwita Mungu wake. “Sasa Nanaa amesemaje?” Akauliza tena.
“Amenyamaza tu. Anaonekana wazi amenikasirikia.
Mbali ya salamu na kuitikia ‘ndiyo’, nakusema atamuogesha Liv yeye mwenyewe,
hajaniongelesha kitu kingine chochote.” “Wewe uko wapi?” “Naelekea dukani
kwangu. Wamenipigia simu nakuniomba niende. Kuna tatizo kidogo. Ila nashauri
usiende sasa hivi. Mwache kwanza kidogo. Fikiria chakufanya au chakuongea naye
kwanza.” “Sawa.”
Geb akakata simu akiwa amechanganyikiwa, hajui chakufanya. Tokea alipofika
kazini siku hiyo, Mira hakuwepo.
Shetani Hana Usiku Wala Mchana.
Hanaga Usingizi. Hachoki.
Wakati akimvalisha mtoto wake baada ya kumuogesha,
akasikia ujumbe unaingia kwenye simu. Akamvalisha mtoto wake haraka haraka,
akachukua simu yake. Mira alianza kumtumia picha za Oliva. ‘Huyu mwarabu wako nitamnyonga usingizini kama hutamtoa wewe
mwenyewe kwenye maisha ya mume wangu.’ Ulikuwa ujumbe wa vitisho ulio
mugopesha sana Nanaa. Alituma picha kama tatu za Oliva, kisha akatuma
nyingine alizokuwa amepiga yeye mwenyewe Mira na Geb.
Baadhi walikuwa na watu wengine. Mazingira ya
pichani, yalionyesha ni kweli walikuwa wote nchini India. Hapo ndipo Nanaa alipomtambua
Mira. Akaogopa sana. Mwili mzima wa Nanaa ulikuwa ukitetemeka kadiri kumbukumbu
ya Mira ilivyokuwa ikimjia akilini.
Alimuona siku moja kabla ya kikao chao cha kwanza
cha harusi, akizungumza na Grace na Geb. Tena akakumbuka waliongea na kucheka.
Siku ya kikao, Nanaa akakumbuka vile Mira alipomsogelea kumsalimia. Kwa
kuwa alikuwa amekaa na amempakata Fili, Mira alichuchumaa mbele yake
baada ya kusalimiana na Geb. Alichuchumaa kumsalimia. Aliongea kwa sauti ya chini
ili watu wengine wasisikie. Kuna vitu alizungumza mara kadhaa,
Nanaa hakuwa akimsikia wala kumuelewa. Akainama ili
kumfikia pale alipokuwa amechuchumaa akampa sikio. Maana Mira aliongea mara TATU
bila Nanaa kumsikia.
Ndipo akakumbuka kusikia mikono ya
Mira ikimpapasa miguuni. Akashituka kidogo na kumuuliza
vipi! Akamjibu anamtoa uchafu miguuni. Mira alisimama, akaondoka
bila Nanaa kumuelewa vizuri. Lakini kwa kuwa alimuona na Grace siku
iliyopita, na wakasalimiana na Geb vizuri tu bila tatizo, hakuingiwa na
wasiwasi. Akajua ni watu wakaribu ya kina Geb.
Ile picha
nzima na yale aliyokuwa akimfanyia Nanaa siku ile, ilianza kumjia vizuri
akilini. Kama aliyefunguliwa macho, akawa amejua kwa HAKIKA. Hata
kule kumpapasa miguuni, Nanaa akagundua hakuwa akimtoa
uchafu miguuni, bali alikuwa akimuweka zile pini. Nanaa akashituka na
kusimama kama mshale, karibia kuanguka. Olivia alibaki akimwangalia mama yake.
Picha zake na Geb wakiwa nchini
India ziliendelea kuingia. ‘Huu ndio uthibitisho
wa ndoa yangu. Sasa litakalo kupata tena na kifaranga chako, usilaumu. Jua
ulionywa.’ Ujumbe mwingine ukaingia. Nanaa alipousoma ni kama
alipigwa na shoti ya umeme, akarusha ile simu kitandani. Akabaki akitetemeka
huku akimwangalia mwanae kwa hofu.
~~~~~~~~~~~~~
Kwa haraka sana kama aliyekuwa
ametumwa, akakimbilia stoo ya ndani ambayo huweka vitu wasivyotumia. Akachukua
mabegi makubwa mawili. Akaingia chumbani kwa Oliva na bibi yake. Akaanza
kukusanya nguo za mtoto wake na kuziweka kwenye begi moja. Akatoka kwa haraka.
Akapiga simu getini na kumuagiza mlinzi mmoja akamchukulie taksii. Akakimbia
juu chumbani kwao. Akakusanya baadhi ya nguo zake. Akashuka kwa haraka. “Mungu wangu nisaidie.” Nanaa alikuwa
akiongea huku akihema na kukimbia juu na chini ya ile nyumba, kama
aliyechanganyikiwa. “Huyu msichana
atakuja kuniulia mwanangu. Heri mimi hata nikifa hakuna atakayepata hasara.”
Nanaa aliendelea kukusanya vitu vyake.
Simu kutoka kwa mlinzi iliita
kumtaarifu Nanaa wamepata taksii. Akaamuru iingie ndani kabisa. Akapandisha
mabegi yake mawili kwenye ile taksii, akarudi ndani, akachukua kalamu na
karatasi.
Geb!
Sikuwa nikijua kama una mke ambaye anakuhitaji kiasi cha kunidhuru
mimi. Nimeamua kuondoka mapema kabla Mira hajamdhuru mwanangu. Sihofii
juu yangu. Kwani hata akiniua mimi, hakuna atakayepata hasara. Najua itakuwa
pumziko kwa wengi, lakini si Liv. Nitamtunza na kumlinda na kila hatari. Hata
kama itagarimu furaha yangu. Nimeamua kwenda kuanza maisha yangu sehemu
nyingine nikiwa na watoto wangu wote. Nina kuahidi kukutafuta nitakapo tulia.
Inaweza kuchukua muda kidogo. Lakini nakuahidi kukutafuta nikipata kazi na
sehemu nzuri ya kuishi na watoto. Nakuahidi kumpa Liv na mdogo wake maisha
mazuri kama unayotamani. Nitahangaika. Naamini nitafanikiwa mapema tu. Niombee
uzima na nguvu. Nina kuahidi sitakutenga na watoto wako. Nikitulia
nitakujulisha nilipo. Ili kama utapenda, uwe unakuja kuwaona wanao.
Najua ulininunua
kwa pesa nyingi sana. Lakini Geb, nakuahidi kukurudishia pesa yote. Nikianza tu
kazi, nitakuwa nakutumia kila mwezi pesa kiasi kupunguza deni. Naomba usiumie
ukadhani pesa yako imepotea bure. Nitairudisha kama ilivyo. Tafadhali
sana, nakuomba Geb, usimdai kaka. Mimi mwenyewe nitairudisha. Tafadhali
nivumilie. Najua hii pete imekugarimu sana. Nakurudishia pamoja na cheni
aliyokuwa amenikabidhi mama. Tafadhali mrudishie mama mwenyewe. Naona mimi sio
mtu sahihi aliyetakiwa kunipa hiyo cheni iliyobeba historia nzito hivyo.
Nashukuru sana kwa kila kitu. Nakuombea uzima na furaha.
Nanaa!
Akaiweka
ile karatasi pale mezani pamoja na cheni na hiyo pete ya uchumba, akaondoka kwa
haraka sana.
~~~~~~~~~~~~~
“Tunaelekea wapi?” Yule dereva
taksi akauliza. “Stendi ya mabasi yaendayo mikoani.” Dereva akaaondoa
taksii. Swali anakwenda wapi baada yakufikishwa stendi, likaanza
kumsumbua. Nanaa hakua akijua kokote zaidi ya Moshi alikozaliwa, hapo jijini
Dar ambapo napo ni shule ndio iliyomtoa mkoani Moshi na kumfikisha hapo, na
Morogoro ambako alipelekwa na Geb.
Wazo
la kukimbilia Morogoro lilipomjia, akapingana nalo kabisa. “Morogoro hapana. Hapo ni karibu sana. Anaweza kunifuata bila shida.”
Wazo la kikimbilia Moshi hakutaka hata kulipa nafasi hata kidogo. Ni mkoa ambao
haukuwahi kumtendea vyema. Tokea anazaliwa mpaka anaondoka mkoani hapo. Ilikuwa
machungu matupu. “Moshi hata kwa fimbo,
sitarudi.” Nanaa aliendelea kuwaza wakati dereva taksii akiendelea
kuendesha.
Ilikuwa ni saa 4 kamili
asubuhi wakati dereva taksii huyo akiingia standi.
Mpaka wanaingia hapo, Nanaa hakuwa akijua akimbilie wapi na mwanae. Aliposikia
mtu mmoja akiwakimbilia huku akitangaza kuuza tiketi ya mwisho ya basi
linaloelekea Arusha muda mfupi sana kuanzia hapo, Nanaa akashawishika. Hakuwahi
kufika jijini Arusha. Lakini Alex, mpenzi wake wakwanza, alikuwa akilisifia
jiji hilo nakumwambia ipo siku atampeleka huko wakatembee. Lakini mpaka
anamsaliti, hakuwahi kumpeleka. Waliishia kulala naye kwenye nyumba za wageni
hapo hapo Moshi.
Akamuomba dereva taksii asimamishe gari pembeni
ili anunue hiyo tiketi ya kuelekea Arusha. Hakutaka hata kujua ni basi gani.
Ilimradi alisikia ni basi litakalomtoa jijini hapo kwa haraka, Nanaa
akanunua tiketi. Yule kijana aliyemuuzia akamwambia amebahatika nafasi ya
dirishani. Nanaa akamshukuru na kumwambia kwa kumuhakikishia kuwa hamwibii,
waongozane mpaka kwenye basi hilo ndipo atakapomlipa hiyo pesa. Yule kijana
akiwa anatembea, Nanaa bado yupo ndani ya taksii amekumbatia mwanae kama
alumasi anayoogopa asipokonywe, akakubali.
Wakaongozana mpaka kwenye hilo basi. Ni kweli akamsaidia na kupandisha mizigo yote, akamlipa
na pesa ya ziada kama shukurani, Nanaa akakaa na mtoto wake huku akihema. Baada ya dakika chache sana, basi hilo
lilifanikiwa kumtoa Nanaa na Oliva jijini Dar es salaam, kwa ahadi ya kuwafikisha
jijini Arusha salama.
Hakuwa akiamini wakati basi hilo linaacha jiji.
Akamtizama mtoto wake kama yupo salama. Wakagongana macho. Oliva alikuwa
ametulia akimtizama mama yake. Akamshika kichwa kama kupima homa na kuhakikisha
yupo salama, akamkuta ni mzima, ila tu ametulia kama anayejua kinachoendelea. “Asante Mungu wangu!” Nanaa
alijikuta akishukuru kama aliyeokoka na
ajali ya moto.
Akambusu mtoto wake. Oliva alikuwa ametulia tuli.
Hata Geb alishamjua mtoto huyo. Ni kama anajua kama mama yake hayupo
sawa. Alikuwa mchekaji sana. Lakini mama yake asionyeshe kutokuwa na furaha
usoni hata kidogo. Oliva hatacheka hata iweje. “Liv!” Nanaa akamwita kwa
upole.
“Unakumbuka nilikuahidi hakuna kutengana?”
Akamuuliza kama anaelewa. “Basi, bado natunza ahadi yangu. Sitakuacha popote
pale mwanangu. Na wala sitakubali mtu akudhuru. Nitakulinda.
Umesikia eeh! Usiogope. Kila kitu kitakuwa sawa.” Nanaa alishazoea
kuzungumza na huyo mtoto tokea yupo tumboni. Ukiwa nje ya chumba walichopo wao,
unaweza fikiri Nanaa anazungumza na mtu mzima.
“Lala tu, mama atakukumbatia.” Akamuweka
sawa mwanae. Akamkumbatia kama alivyomuahidi. Akamfunika na mtandio wake ambao
huwa anamfunika wakati wote akimnyonyesha. Na yeye akajiweka sawa akiwa
amempakata vizuri. Liv alilala hata
kabla hawajafika mjini Kibaha. Baada ya muda mfupi tu alipomuona mtoto wake
amelala na yupo sawa, na yeye akalala.
Huku Nyuma Nyumbani Kwa Geb.
Geb alipata wakati mgumu
sana kusubiri kazini mpaka mchana kama alivyoshauriwa na mama yake. Alishindwa
hata kumpigia simu Nanaa, kuogopa asije piga na kuropoka na kuharibu mambo
zaidi. Kazi zilikuwa haziendi. Kila
wakati macho kwenye simu ya mkononi, ukutani na kompyuta kana kwamba kuna moja
inaweza ikampa muda usio sahihi. Ilipofika saa saba mchana, akarudi nyumbani
akiwa na makopo ya ice cream mawili. La Vanilla na Chocolate na chakula.
Alimnunulia Nanaa kuku wa kuchoma.
Alijua ni mpenzi sana wa nyama. Akafungiwa na Chips, akarudi nazo
zikiwa zimefungwa vizuri tu. Akajua hata kama Nanaa hasikii njaa, ile harufu ya
yule kuku lazima atamshawishi tu. Alirudi akiwa ameshajiandaa kwa hoja
zake zote. Alishazipanga, akazirudia akiwa peke yake mpaka akaridhika kuwa
lazima Nanaa ataelewa tu na kusamehe.
Alipoingia akakimbilia juu baada ya kukuta nyumba
ipo kimya. Akajua atakuwa amelala na mtoto wake chumbani kama usiku uliopita
walipotoka Morogoro. Lakini hakuwepo
chumbani.
Akampigia simu. Akasikia ikiita chumbani kwa mama
yake. Akajua amelala na Oliva chumbani kwa mama yake. Akashuka ngazi
akikimbilia chumbani kwa mama yake. Hakumkuta Nanaa. Akapiga tena simu
yake, akasikia mlio ukitokea mwisho kabisa wa kitanda cha mama yake, uvunguni
upande wa ukutani. Akapanda na kuitoa.
Macho yake yakakumbana na picha zake akiwa na
Mira, nchini India. Akaendelea kuangalia. Picha hizo alikuwa ni yeye na
Mira. Nyingine akiwa na watanzania wengine. Geb akakaa. Akaendelea kuziangalia.
Macho yake yakatua kwenye picha za Oliva. Zote alizitambua ni picha
alizokuwa amempiga mwanae na kuzipenda sana. Oliva alikuwa akicheka. Akaenda
kuzi print. Akaziweka kwenye fremu nzuri sana na kuzitundika ofisini
kwake. Geb alishangaa sana.
“Huyu msichana anaonekana alikuwa
akinifuatilia kwa muda mrefu sana bila ya mimi mwenyewe kujua! Ameingiaje
ofisini kwangu na kupiga picha, picha za mwanangu!” Geb akaendelea kujiuliza
akizidi kushangazwa na kumbukumbu za muda mrefu alizotunza Mira.
Na yeye akakumbana na jumbe za vitisho
kutoka kwa Mira. “Hapana. Hapa amefika mbali sana!” Geb aliendelea
kuzungumza akiwa peke yake pale chumbani kwa mama yake huku akisoma na
kuangalia zile picha kwa kurudia rudia. “Atakuwa amemuogopesha sana Nanaa,
ndio maana ametupa na simu. Nanaa atakuwa yuko wapi?” Geb akasimama nakutoka pale chumbani.
Ndipo macho yake yakatua juu ya meza aliyozoea
kuweka funguo zake za gari kila anapoingia ndani. Wakati ananyanyua zile funguo
za gari ili atoke akamwangalie Nanaa huko madukani akidhani pengine alitoka
kufuata kitu dukani ndipo akaona karatasi imeandikwa “Geb!”
Akajua ni ujumbe kutoka kwa Nanaa. Wakati anaingia, alirusha tu funguo bila
kuangalia mezani kwani alikuwa na haraka yakumuwahi Nanaa.
Akaanza kusoma. “No no no noooo!” Alijikuta
akikataa kile alichotaarifiwa na Nanaa. Akahisi hakusoma vizuri. Akarudia
kusoma tena. “No way! This is not
happening to me. No way!” Gafla akahisi dunia imemuangukia. Nanaa
ameondoka na faraja yake! Nanaa amebeba
mipango mizima ya Geb. Bila kujijua yeye ndiye akawa amebeba ratiba na mipango yote ya maisha
ya Geb yaliyobaki hapa duniani. Nanaa ameondoka! Kwa sekunde kadhaa dunia
iliacha kuzunguka mbele ya macho ya Geb. Akahisi ni kama giza
limemfunika machoni.
Kwa gafla sana kila kitu kikakosa maana hapa
duniani. Aliliangalia lile jumba na thamani yote mle ndani. Gafla ikawa ni kama
amesimama jagwani kwenye jua kali. Hata kiyoyonzi kilichokuwa kinapuliza
mle ndani, hakukisikia tena. Akaanza kuhisi joto kali. Magari yote yaliyokuwa
hapo nje ya hilo jumba. Ambalo alilijenga kwa mamilioni ya pesa alitamani yawe
msaada kumtoa hapo na kumpeleka alipo Nanaa na watoto wake. Lakini yalishindwa.
Yalihitaji kuongozwa. “Amekwenda wapi Nanaa?” Lilikuwa swali ambalo hata
hayo magari, yasingeweza kumsaidia, kumtoa hapo na kumfikisha alipo Nanaa.
Akakumbuka mamilioni ya pesa aliyonayo benki.
Akajua hayatasaidia kitu chochote kukamilisha furaha yake tena hapa
duniani. Yangekuwa na maana tu kama yangeweza kutumika kumwambia Nanaa alipo na
watoto wake. Akakumbuka pesa alizolipa kwa ajili ya kumpata Nanaa, siku
alipomsahau nje ya ukumbi wa harusi ya Malii. Alimlipa Mlinzi wa benki
akamsaidia kwenda naye kwenye kampuni ya simu, akafanikiwa kupata namba ya
Antii na kumkuta Nanaa hospitalini. Lakini leo pesa yake imekuwa bubu.
Haiwezi kuongea.
Nanaa ameacha simu. Labda angekimbilia kwenye
kampuni ya simu ili awalipe mamilioni ya pesa wamwambie ile simu inaonyesha ipo
wapi kwa wakati ule ili amfuate Nanaa na Oliva, furaha ya moyo wake. “Mungu wangu naomba usiniache!” Akajikuta amepiga
magoti pale pale, machozi yakimtoka. Hapakuwa na tumaini tena.
Akarudia tena kusoma ule ujumbe alioachiwa na
Nanaa. Akagundua ameelewa kile kilichoandikwa. Akajiambia kabla
hajarukwa na akili, watu wasijue ni kwa nini, basi amtaarifu mama yake.
Walishaongea muda mfupi kabla hajarudi hapo nyumbani. Mama yake akamwambia yeye
bado yupo kwenye biashara yake. Geb alikuwa sawa tu mara ya mwisho alipokuwa
akizungumza na mama yake. Lakini safari hii alipiga akiwa analia.
Kwa Mama G.
“Mama!” Geb aliita mara baada ya
mama yake kupokea. “Kuna nini wewe!?” Mama G
akauliza kwa mshituko. “Nanaa amenikimbia mama. Nimemchelewa kidogo tu!” “Mungu
wangu!” Mama G akaweka mikono kichwani. Simu ikaanguka. Geb akarudi
kwenye kochi akakaa. Geb yule wa mipango, mwenye majengo yanayoingiza pesa
wakati wengine wakilia njaa. Ambaye akifika mahali hata wazee wanasimama.
Anayeongoza wanaume na wanawake wasiopungua ishirini kwenye biashara zake tu.
Ambao wanategemea kupokea kutoka kwake kila mwisho wa mwezi ili nao watunze
familia zao. Geb ambaye walio kwama
kifedha wanamkimbilia kukopa mamilioni ya pesa. Jumatatu hiyo, mchana, siku ya kazi, mwanamke
amemfanya apige magoti na kujikuta akilia kama kitoto cha kike.
Kwa James.
Baada ya muda, akampigia simu James kumtaarifu.
Ndani ya lisaa limoja nyumba ya Geb ilishakuwa na wageni. James, Grace, mama
yake, Danny na watoto wote. Kila mmoja alisoma ule ujumbe kwa kurudia rudia.
“Kwa nini hukumwambia Geb? Ujue aliponipigia simu kuniambia mnakwenda Morogoro
kupumzika, nikajua mnakwenda kuzungumza!” James akalaumu.
“Kama ulikuwa huwezi kuzungumza naye, ungeniambia
tu mimi mwenyewe nikajua jinsi ya kuzungumza naye. Unajua ni mjamzito, halafu
ana mtoto. Unafikiri ataishije sasa!?
Nanaa haifahamu kabisa hii nchi!” James aliendelea kulaumu kama kawaida yake
kwa dada yake.
“Kwa nini hukumwambia Geb? Huyu Mira atakuwa amemuogopesha
sana ndio maana ameamua kukimbia.”
Grace aliongea kwa unyonge akimuhurumia kaka yake. “Jamani, Nanaa aliyaona
mabadiliko ya Danny. Akaanza kuwa na wasiwasi. Akaniuliza mbona Danny hana
furaha. Ndipo ikabidi kumuelezea mahusiano ya Danny na Zinda. Nia yangu ilikuwa
ni kumtoa hapa, nimpeleke sehemu iliyotulia ili niweze kuzungumza naye. Kwanza
ili kujibu maswali yote aliyokuwa nayo Nanaa juu ya ugonjwa aliopata wa gafla,
na habari za Zinda.” Geb akaendelea.
“Nilipokuwa nikimuelezea
mahusiano ya Danny na Zinda tu, hata sikuwa nimemaliza habari nzima, tayari
Nanaa alishakuwa amepata majibu yake. Alilia sana, akihisi amesalitiwa.
Ilimchukua muda mrefu sana kutulia. Ilibidi kumueleza taratibu kwa nini maneno
yalimfikia Zinda.” “Mimi nilimuona tokea mwanzo jinsi alivyomuuliza mama kama
yeye ndiye aliyemwambia Zinda. Mama unakumbuka? Akasema ningeumia
sana kama ni mama. Maana mama ndiye msiri wake.” Grace aliongeza.
“Nakumbuka. Na amerudi kutoka safari, ameshindwa
hata kuniangalia usoni. Najuta!
Unajua Mira alizungumza naye nikiwa hapahapa!
Ingekuwa zamani angeniambia. Lakini alinyamaza kabisa. Mpaka
namuaga nakwenda kazini, alionyesha yupo sawa tu na hana kitu chakuzungumza na
mimi.” “Nimekuta hizi picha na jumbe za vitisho sana kutoka kwa Mira.
Mira amemtumia kwenye simu yake. Nina uhakika hizi ndizo zimemkimbiza.”
James akachukua ile simu kutoka kwa Geb. Akaanza
kuziangalia.
“Mbona ulisema ni kama hamkuwa na mahusiano!?”
“James! Huyo dada hatukuwa na mahusiano naye, ila tumeishi naye.” “Picha zako
zinaonyesha tofauti Geb! Kama hii mmepiga akiwa amekuegemea begani! Hapa
mmekaa karibu kabisa! Na picha za Oliva amezipata wapi!?” James aliendelea kuhoji huku akiperuzi kwenye simu ya dada
yake.
“Sidanganyi James. Huyo dada sikuwahi hata
kumfikiria kimapenzi. Na Mungu wangu ni shahidi. Na picha zote hizo zimepigwa
kwenye mikusanyiko ya watanzania. Sio
kwamba nilikuwa nikipiga naye mimi peke yangu! Na picha zote hizo nikiziangalia, nakumbuka kabisa ni picha
tulizopiga siku tulizokuwa watanzania tunakutana kwenye sherehe au mikutano ya
watanzania. Sasa labda yeye alikuwa akinitega kwa madhumuni yake. Lakini
sikuwahi hata kuwa na wazo naye.”
“Amekuja kuomba kazi kwangu, nikamuajiri kama mfanyakazi wa kawaida
tu. Muulize hata Grace. Hata sina muda naye. Mungu wangu ni shahidi.
Grace ndiye anayemsimamia na tuseme yuko chini ya Grace. Sipo karibu naye
kabisa labda atumwe kitu kwangu na Grace, basi.
Nisingemdanganya Nanaa. Nampenda Nanaa. Na picha zote hizo za
Oliva ni picha nilizo tundika ofisini kwangu. Hizo mbili nimening’iniza
ukutani, pamoja na za Nanaa, na hii ni picha ambayo nimeweka mezani kwangu.
Tena ipo nyingine ya Nanaa akiwa amembeba Liv. Muulize Grace. Au twende ofisini
kwangu hata sasa hivi utaona. Ofisi yangu imejaa picha za Nanaa na Oliva tu.
Nina uhakika ndiko alikoziona hizo picha. Niamini nampenda Nanaa. Siwezi
kumchanganya na mwanamke mwingine yeyote yule James. Sithubutu.”
Hilo James alilithibitisha pale Nana alipougua. Akanyamaza.
“Sasa unafikiri atakuwa ameenda wapi?” Mama G
akamuuliza James. “Sijui! Mimi ndiye
familia ya pekee ya Nanaa. Hana pakwenda na hafahamu hii nchi
vizuri. Kwanza hana uzoefu wa kusafiri kwenye mabasi. Kwanza hata sikumbuki
kama alishawahi kupanda mabasi makubwa kumpeleka sehemu yeyote. Labda HIACE.
Kumtoa pale Moshi mjini kumpeleka vijijini. Hata kuja hapa Dar kwenyewe mimi
ndiye nilimleta na gari yangu. Nanaa hafahamu mambo mengi na hicho
ndicho kinachoniogopesha, tena akiwa ni mjamzito na mtoto juu! Sijui kama anapesa yakumtosha au la!”
“Nanaa anazo pesa. Anapesa nyingi tu. Huwa nampa
kila mwisho wa mwezi kama mshahara, kwa matumizi yake binafsi ili asiwe
anashida ya pesa. Huwa nampa pesa nzuri tu. Grace akilipa mishahara,
nahakikisha na yeye namgawia kutoka
kwenye mshahara wangu. Namwingizia asilimia 80 benki halafu 20 huwa
namletea hapa nyumbani. Kwa hiyo swala la pesa hilo usiwe na wasiwasi
nalo. Na nitaendelea kumuwekea tu, hata
kama sitampata.” Geb alijibu kinyonge akisikika amekata tamaa.
“Kama ni hivyo, ni sawa. Lakini nashauri mumpe muda. Mwacheni atulie tu. Amesema
atakutafuta. Basi atakutafuta.” James alisikika amepata aghueni baada ya
kusikia dada yake ana pesa. Akasahau
pesa si kila kitu. “Lakini ataishije mwenyewe akiwa na mtoto na ni mjamzito?
Hata akiwa na mamilioni ya pesa yanayoingia kila siku bila kuzungukwa na watu wanaompenda
na kumthamini, haitamsaidia chochote. Mbaya zaidi akiwa amejawa na hofu! Halafu amejazwa maneno yaliyojaa uongo
na usaliti kutoka kwa Mira bila yakusikia upande wangu! Najua sasa hivi
amejawa hofu, usaliti na majuto.” Geb alisikika akiwa
amenyong’onyea.
“Na lazima atajisikia hivyo. Ameona picha. Halafu
amejua unafanya naye kazi siku zote. Kwa nini usimwambie siku zote,
mpaka yeye mwenyewe ndiye amekuja kumwambia? Hujui amemwambia nini mbali ya
hizo jumbe zakutishia maisha yake na mtoto wake. Nanaa yupo kwenye hofu sana. Ameshuhudia
kile huyu anayejiita mke wako, akimtendea yeye. Unyama mkubwa.
Lazima sasa hivi anajua hizo jumbe sio za vitisho. Anajua ni kweli ana uwezo wa kuja kumdhuru tena yeye na mtoto wake pia. Lazima aogope na kujiweka mbali.
Hasa akijua kwa kutomtaja Mira kwake ni kwa kuwa upo upande wake Mira.” James
aliendelea kupalia makaa ya moto.
~~~~~~~~~~~~~
Ni bandika
Bandua. Likiisha hili, linaanza jingine.
Jamani! Nani ni wa
Nani?
Hata Nanaa
amechanganyikiwa na kupoteza dira, akaamua kuachia gazi.
Zinda amedai Nanaa ni mkewe, huku Mira naye
anadai Geb ni mumewe!
Geb
anamwambia Nanaa amemchagua yeye, huku anapata habari kutoka kwa Mira kuwa ni
wa Geb!
Walikuwa
mbuga za wanyama kwa takribani siku tatu, kwa nini asimwambie? Alimuona pia na
Grace, inamaana hata Grace anamfahamu wifi yake huyo Mira.
Usaliti wa namna
gani?
Nanaa aliwaza
wakati anaondoka.
Anaelekea
wapi?
Ø Ni Nanaa
huyu huyu aliyekuwa ametokewa na malaika siku chache zilizopita. Akaamuona mtu
akipigana vita yake na kumwambia yupo mtu anayepigana badala yake. Lakini ndio
huyu huyu leo anakimbizwa na simu na ujumbe kutoka kwa Mira.
Ø Alisimamia
Imani ya Geb mpaka akapokea muujiza wake, leo ameweka kila kitu chini. Pete ya
Geb na cheni ya dhahabu ya mama G, anakimbia na faraja ya Geb, Oliva!
Usikose
kufuatilia Visa na Mikasa ya Simulizi hii ya kusisimua.
0 Comments:
Post a Comment