Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! – Sehemu Ya 42. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! – Sehemu Ya 42.

Nanaa alikuwa amejifunika shuka amelala. Geb na yeye akavua nguo akapanda kitandani. Akamsikia analia taratibu. Akajisogeza karibu naye. Kwa kuwa alikuwa amegeukia ukutani, akajinyanyua mpaka kwenye masikio yake. “Nakupenda Nanaa! Amini ninakupenda na ninathamini kila muda Mungu anao nijalia kuwa na wewe. Unisamehe pale nilipoonyesha upendeleo wowote. Nia yangu ni kuhakikisha kuna amani. Najua mama anakupenda kwa hakika. Ila kuna maisha ambayo tulikuwa tukiishi zamani, hapakuwa na usiri kati yetu. Nahisi ni udhaifu wetu. Na wote wamejifunza kwa hiki kilichotupata. Ndio maana unaona ni kama pale nyumbani amani imepotea. Danny anajilaumu sana. Nilichokuwa nikitaka kutoka kwako ni uwasamehe, yaishe. Sikuwa na nia yakuwatetea. Hata mimi nimeathirika Nanaa. Wamechangia kwa asilimia kubwa kusimamishwa kwa harusi yetu. Lakini namuamini Mungu, atatufanikishia tu. Naomba usinichukie. Nipo upande wako mpenzi wangu. Sipo kinyume na wewe.” Nanaa akanyamaza. Geb alimuona anajifuta machozi, bila kujibu kitu. Akambusu shingoni na kujivuta zaidi karibu yake, akamkumbatia. 

~~~~~~~~~~~~~

Nia ya Geb ilikuwa kuzungumzia mambo mawili. Juu ya hilo la Zinda, Danny na Mama yake, pamoja na la Mira. Lakini kwa jinsi Nanaa alivyopokea habari za watu walioshiriki kutoa habari za ndani na kumpa Zinda, akaona habari za Mira zisubiri kwanza. “Hata malaika alishindwa kumwambia. Heri na mimi ningojee kwanza. Nisije nikaharibu zaidi.” Geb akawaza. Akaamua kulala.

Usiku huo hapakuwa na mapenzi wala busu. Hapakuwa na kuomba pamoja wala Geb hakukumbuka kuomba peke yake. Tayari na yeye alisha changanyikiwa na shutuma alizotupiwa na Nanaa. Nanaa alimuweka na yeye kwenye kundi la wasaliti wake. Hakumuhesabu upande wake kitu kilichomuumiza na kumchanganya Geb zaidi. Mpaka Nanaa analala, amekiri kwake ile safari yote aliyokuwa akiifurahia pale mbugani, akidhani ilikuwa kwa ajili yake ili kumfurahisha, kumbe nia ilikuwa kuja kutetea familia yake. Hilo nalo lilimuumiza Geb. Inamaana furaha yote aliyojenga moyoni mwa Nanaa kwa siku tatu mfululizo, imefutika!

~~~~~~~~~~~~~

Nanaa aliamka asubuhi na mapema. Hiyo ilikuwa siku ya 4, tokea wafike hapo. Ilikuwa ni siku ya jumapili. Geb akamsikia, amekaa kitandani. “Mbona mapema hivyo?” Akauliza. “Si ulisema tunaondoka leo? Ndio nakusanya vitu. Samahani nimekuamsha.” “Hamna neno. Nilifikiria tuondoke hata jioni.” “Kwani kuna kitu kingine tena unataka kuniambia?” “Nanaa!” Geb aliumia zaidi. “Nauliza tu!” “Sikukuleta huku kwa ajili ya kukupa habari zitakazo kuumiza! Nilitaka muda na wewe.” “Naomba usinidanganye Geb.” “Sawa. Nilitaka tuje tuzungumzie na hilo pia. Lakini zaidi nilitaka muda na wewe.” “Basi nitakuwa hapo nje. Nataka nitembee tembee kidogo wakati nyinyi mmelala. Nitarudi baadaye kidogo.” Geb akajirudisha kwenye mto, akafunga macho.

Nanaa alisimama pale kwa muda. Geb hakuwa amesema ndiyo au hapana. “Geb! Natoka nje.” Akamgeukia. “Nakuhitaji Nanaa.” Akamuona Nanaa anavua nguo zote, anarudi kitandani. “Sio kwa namna hiyo Nanaa! Kufanya mapenzi na mimi sio lazima. Sitaki uone unawajibika. Si jukumu unalotakiwa kulitimiza kwangu. Na nikikwambia nakuhitaji sio kwamba nakuhitaji kufanya mapenzi. Nakuhitaji kwenye maisha yangu.” “Sawa.” Nanaa akapanda kitandani, akajifunika shuka, akatulia.

“Nanaa!” Nanaa akageuka, machozi yakimtoka. Akajifuta. “Abee!” “Pole.” Geb aliongea kwa upole na upendo. “Pole sana. Lakini naomba tusitengane sababu ya makosa ya watu wengine. Naomba usinichukie. Kumbuka na mimi nimuhanga wa hayo makosa. Harusi ilikuwa ni yangu pia. Ninataka sana kukuoa Nanaa. Nakuhitaji kwenye maisha yangu.” “Sijakuchukia Geb. Ila nimeumia sana. Sikutegemea. Nilijua nimepata mtu wa kumueleza chochote kinachoendelea kwenye maisha yangu au hata moyoni mwangu. Nimeumia kujikuta narudi kuishia kuwa na kaka tu! Maisha yangu yameshindwa kabisa kuniongezea mtu mwingine!?”  Geb alizidi kuumia. Akaona hata yeye hakutajwa hapo. “Pole.” Ndilo neno aliloweza kujibu akiogopa kuongeza neno jingine asije haribu.

Nanaa alipanda kitandani kwa hasira akiwa uchi kabisa. Kama aliyekuwa akitaka kutimiza wajibu. Lakini Geb akamtuliza. Alimsogelea karibu, akambusu kidogo tu shavuni. “Pole sana.” Akabaki akimwangalia. “Asante.” Akamfunika shuka vizuri. Nanaa akashangaa anajilaza kwenye mto bila hata kumpapasa. “Njaa inakuuma?” Akamuuliza. “Hamu ya kula imeisha kabisa. Nasikia tumbo limejaa. Sina hamu ya kuweka kitu chochote mdomoni.” Geb akajua bado ana hasira. “Basi tulale kidogo. Labda ukiamka utasikia njaa. Na sio lazima tule hapa. Tunaweza kwenda kula sehemu nyingine. Jaribu kupumzika.” Mikono ya Geb ilikuwa juu ya shuka. Akamtengeneza lile shuka vizuri. Kama anayemtayarisha kulala. Nanaa naye akajiweka sawa, akarudi kulala.

~~~~~~~~~~~~~

Waliamshwa  na Oliva saa 4:37asubuhi. Alikuwa akiongea huku akipuliza. Nanaa akacheka. “Fizi zinamuwasha huyo!” “Naomba ukaongee naye kidogo. Jana alijua nimekuudhi. Hakutaka hata kunichekea!” Nanaa akatoka. Alipomuona tu mama yake akaanza kucheka. Akakaa. “Na mimi nina hamu na wewe Liv!” Geb akamsikia anacheka. “Ulilalaje?” Liv aliendelea kucheka. “Njoo upate nyonyo kwanza.” Akamtoa pale kitandani. Akambusu. “Muone unavyotokwa mate! Meno yanataka kutoka ndio maana fizi zinawasha Liv. Pole kipenzi chagu. Ukinyonya nitakupa ile toy yako yakukunia fizi. Sawa?” Oliva alizidi kumchekea mama yake. “Unapendeza ukicheka wewe! Usiwe unanuna bwana. Umesikia Liv?” Geb alisikia wakizungumza. Akabaki akiwaza pale kitandani. 

Alijua kwa hakika Nanaa ameumia sana. Maisha yatakuaje baada ya hapo kati yake na mama yake! Ndio kitu kikaanza kumuumiza kichwa. “Nanaa atarudi kuwa rafiki wa karibu tena wa mama?” Geb akawaza. Kwa ukaribu aliokuwa nao Nanaa na Mama G, ungependa tu uwepo nyumbani kwao. Vilijaa vicheko kila wakati. Nanaa alikuwa akiishi na mama G kama rafiki yake wa karibu wala si mkwe. Alifanya chochote mbele yake bila hofu. Ukiwakuta pamoja, ungeweza kufikiri Geb ndio mkwe halafu Nanaa ndiye kiziwanda cha Mama G. Oliva alilelewa na bibi yake kwa mapenzi makubwa sana. Lakini hapo napo kukatupwa jaribu lake.

Geb akaendelea kuumia. Alichukia ile hali. Wasiwasi ukazidi kumtesa. Kwa Danny haikumsumbua. Nanaa hakuwa karibu sana na Danny, lakini si mama yake. Akabaki akiwaza. Akamchukia shetani na kazi zake zote. Hakuacha wapumzike hata kidogo! Ni jumapili iliyopita tu, siku kama hiyo, Nanaa aliamka na miguu iliyoharibiwa vibaya sana. Huwezi kusema imeoza, kwa kuwa haikutoa harufu. Lakini na jumapili hiyo nayo, wameamka wakiwa wamesambaratishwa mioyo. Nanaa hakumuhesabu upande wake. Akazidi kuumia. Akachukia visasi alivyovianzisha Zinda. Swali la atafanyaje likaanza kumsumbua. Akajua kama harusi haitafanyika kwa haraka, ndio Nanaa ataona madhara yake zaidi. 

~~~~~~~~~~~~~

 “Twende ukamsalimie dad.” Wakamtoa Geb kwenye mawazo. Nanaa akaingia na mtoto wake pale chumbani. Hapakuwa na mlango. Kwa hiyo alipitiliza na kumuweka Liv kifuani kwa baba yake pale alipokuwa amejilaza. Oliva akaanza kumchekea. “Unatoa tu maziwa!” Geb akamfuta. “Naona alikuwa na njaa. Amenyonya kama anakimbizwa!” Nanaa na yeye akajiweka pembeni. “Au ulikuwa na hamu na mama?” Geb alimtekenya kwa kuweka kidole chake kwenye dimpozi yake.

“Halafu fizi zinamuwasha. Anahangaika kweli!” “Hivi tulikumbuka teething toys zake?” Geb akauliza. “Nilibeba. Sema zile anazozipenda, zakuweka kwenye friji ndio niliacha. Nilijua huku hakutakuwa na friji.” Nanaa akajibu huku akimfuta maziwa na mate yaliyokuwa yakimtoka Oliva. Meno ya mbele mawili ya juu na chini yaliyokuwa yakimpendeza sana Liv, yalishatoka tangia anatimiza miezi mitano. Geb akasimama akiwa amemkumbatia mwanae. “Twende tukafuate toys zako nyingine utafune.” Nanaa akaamua kuvaa. Alikuwa amejifunga khanga wakati ameenda kumfuata Liv.

Geb alimuona akivaa. Akatamani aombe penzi la mwisho hapo hotelini, lakini akaamua ajikaze tu. Na yeye Nanaa akajiuliza mbona haombwi tena! “Naona nivae kabisa, ndipo nimuhudumie na Liv.” Akajisemesha akitarajia kuambiwa subiria. “Sawa. Wakati unamvalisha yeye, na mimi nikaoge. Ndipo tukapate kifungua kinywa.” Geb akajibu. Nanaa akatulia kidogo. “Kwani ulitaka tuondoke saa ngapi?” “Najua hamu ya kukaa huku na mimi, imeshakuisha.” “Hapana Geb.” “Naelewa Nanaa. Sikulaumu. Muda wowote utakaotaka tuondoke, tunaweza kwenda tu.” Nanaa akanyamaza. Hakujua ajibu nini.

Dar.

Waliingia jijini mida ya saa kumi jioni. Mlinzi akafungua geti bila kuchelewa. Lakini hawakukuta magari ya watu wengine ila ya Geb. Hapo hapo Geb akampigia simu mama yake. “Uko wapi!?” “Kwa Grace. Namsaidia kuweka mambo sawa. Walirudi kwao jana. Sasa namsaidia usafi, kupika na mambo mengine. Nitarudi kama kwenye saa moja hivi. Vipi nyinyi?” Mama G akauliza. “Salama. Lakini sikujua kama kina Grace wataondoka mama! Hajaniaga!” Geb alilalamika kidogo. “Mwache mwinzio atulie kwake. Ulitaka akae hapo mpaka lini?” “Naona ni mapema sana mama.” “Hivi unajua huyu Grace ni mke wa mtu? Mwache ajenge kwake.” “Watoto watatu bila mtu mwingine!?” Geb aliendelea kulalamika. “Ndio kukua huko. Tutaongea vizuri baadaye.” “Kuna kitu mnataka niwasaidie nije?” Geb akauliza. “Sidhani. Kama kipo watakupigia. Lakini wewe pumzika na familia yako. Mimi nitarudi kwenye saa moja.” “Usichelewe sasa mama!” “Umeanza Geb.” “Naomba usichelewe.” Nanaa alikuwa akiwasikiliza bila ya kuongeza neno.

Alikuwa amekaa kiti cha nyuma na mtoto wake, akamtoa. Liv akafungua macho. “Bado una usingizi?” Nanaa akamuuliza. “Twende ukalale na mama.” Alimbeba mtoto wake mpaka juu chumbani kwake. Akambadilisha diaper na nguo, akapanda naye kitandani. Geb akamkuta amemkumbatia Oliva wamelala. Kitu ambacho sio cha kawaida. Liv alishazoezwa kulala peke yake, kitandani kwake. Kitanda hicho ni cha Geb na Nanaa tu. Akilala hapo Oliva ni mara chache sana, tena wanacheza na baba yake tu. Hata mchana alilala kitandani kwake.

Geb akabaki amesimama pale akimwangalia Nanaa na mtoto wake. Akaamua anyamaze tu. Akaenda kujilaza kwenye makochi. Usingizi wa mimba ulimchukua Nanaa, akalala kama mzigo. Alilala akiwa na mawazo. Na ni kweli alipoteza hamu ya kula kabisa.

Geb alimuasha ilikuwa saa mbili na nusu usiku. Akaangalia pale kitandani Oliva hakuwepo. “Twende ukale.” Geb alimuongolesha kwa upendo. “Nataka nioge kwanza. Najisikia mwili umechoka sana.” “Pole. Labda safari. Ukioga utajisikia vizuri.” Nanaa akajitoa pale kitandani kwa shida, akaenda kuoga. Alipotoka bafuni, Geb hakuwepo pale chumbani. Akaamua arudi tu kulala. Hakujua akitoka pale chumbani, ataenda kuongea nini na mama G. Akaona ni heri arudi kulala tu.

Alipojiweka tu kitandani, akapitiwa tena na usingizi. “Nanaa!” Geb akaingia tena na kumuamsha. “Amka ukale japo kidogo. Mama amerudi na chakula.” “Sijisikii vizuri Geb. Naomba nilale tu. Nitakula kesho.” Nanaa ambaye alikuwa hashibi masaa machache yaliyopita,  gafla hawezi kuweka kitu mdomoni. Hataki tena kula. “Jikaze kidogo tu.” “Nina usingizi sana. Nataka kulala tu. Ila naomba uniletee Liv aje anyonye kabla ya kwenda kulala.” “Sidhani kama ataweza kunyonya. Bibi yake alimpikia ndizi. Amezisaga na samaki. Nimemlisha, naona amekula sana.” Nanaa akacheka kidogo. “Basi kesho. Naomba nilale.” Geb akabaki amesimama pale kwa muda. Nanaa alishafunga macho kuashiria anataka kupumzika sio tena maongezi. Baada ya muda akamsikia Geb anatoka.

Jumatatu.

Akiwa usingizini, kwa mbali akasikia busu la mdomoni. Nanaa akafungua macho. “Nataka kwenda kazini.” “Kwani sasa hivi ni saa ngapi?” Geb akacheka. “Saa moja asubuhi.” Nanaa akakaa kwa haraka. “Sasa umekula nini!?” Nanaa alipitiwa na usingizi, hata uji wa Geb hakuamka kuupika. “Mama alishaniandalia.” “Samahani nimepitiwa na usingizi.” Geb akambusu. “Usijali. Ila uamke hapo kitandani ukale.” “Nitaamka. Maziwa yamejaa, nataka nioge, Liv akiamka anyonye.” “Basi toka hapo kitandani sasa hivi, lasivyo utapitiwa tena na usingizi.” “Nitaamka. Kazi njema.” “Nitarudi mchana tuje tule wote.” Nanaa akatulia kidogo.

“Unataka nikuletee nini?” Geb akauliza. “Nimepoteza hamu ya kula kabisa Geb. Sijisikii kula hata kidogo!” “Labda ni hiyo hali ya ujauzito.” Geb akamshika tumboni. “Labda. Nitamtafuta yule daktari aliyenisaidia wakati wa ujauzito wa Liv.” “Naomba na mimi unishirikishe kwa karibu Nanaa. Nataka tuwe tunakwenda wote.” Nanaa akacheka kidogo. “Sawa. Uwe na siku njema.” Geb akambusu tena, na kutoka.

~~~~~~~~~~~~~

Aliingia kuoga. Akasafisha meno, ndipo akashuka huku akiwaza kukutana na mama G. Hakuwa amemuona tokea watoke safari. Alimsikia akiimba jikoni. Akaingia. “Shikamoo mama.” Hapakuwa na tabasamu wala kicheko. Salamu hiyo aliitoa Nanaa akiwa mlangoni, tena amepooza sana. “Marahaba Nanaa mwanangu. Umeamka salama?” “Ndiyo.” Nanaa akajibu, kisha akanyamaza. “Kaa ule.” “Asante.” Nanaa akaingia ndani. Akasogea mpaka kwenye jiko. Akamimina uji aliokuwa amepikiwa Geb. Akaweka kwenye microwave ili kupasha. Mama G akaona ule ukimya usio wa kawaida. Akajua Nanaa amemkasirikia tu. Wakati anasubiria uji wake upate moto, akaendelea kuchezea simu yake bila kuongea chochote. Kidogo kengele ya kuashiria uji wake umekuwa tayari hapo kwenye microwave ikalia. Akautoa uji, akaenda kukaa mezani. Hapo hapo ndani jikoni. Kimya.

Hakuna Kulala.

Wakati mama G anataka kuzungumza na Nanaa, simu yake ikaita. “Haloo!” Nanaa akapokea. “Ni Nanaa?” Mtu wa upande wa pili akauliza. “Kwani wewe unamtaka nani?” Nanaa akauliza. “Nina shida sana ya kuongea na Nanaa?” “Wewe ni nani?” “Mira.” Akajitambulisha. “Mira!?” Nanaa akauliza akiwa kama hajaelewa vizuri hilo jina. “Ndiyo mimi naitwa Mira.” Mama G akashituka sana. Akaangusha mpaka glasi. Nanaa akamwangalia, na kurudisha mawazo kwenye simu.

“Umesema Mira kama kioo!?” “Ndiyo.” Mira akajibu. “Mmmh! Mbona mimi sikufahamu? Unasemaje?” “Nataka kukutaarifu kuwa mimi ni mke halali wa Geb.” Nanaa akatulia. “Unanisikia Nanaa?” “Nakusikiliza.” “Ndio hivyo. Unatakiwa ujue na uachane na mpenzi wangu. Geb nimetoka naye mbali sana. Tokea tunasoma nchini India tulikuwa tukiishi naye. Aliniacha nchini India nikiwa nasoma. Yeye alipomaliza akaniaga kuwa anarudi kuanza kutafuta maisha huku. Ameniacha na baraka zangu zote. Nikikata tu simu, nitakutumia picha zangu na Geb ili uamini vizuri na ujue sio kwamba nakurusha tu roho. Ni kweli ni mume wangu.” Mira akaendelea.

“Nimemaliza chuo, nikarudi huku akanipa na kazi. Tupo naye kwenye biashara zetu. Maisha yetu yanaendelea kama kawaida. Sitaruhusu wewe wala mwanamke mwingine aingilie mapenzi yetu. Nakuonya ukae mbali na Geb. Tuna maagano ya mpaka kwa mizimu inanitambua mimi kuwa ni mke wa Geb. Nakuonya na kukutaarifu kabisa. Mizimu haitakubali wewe ukavunja agano letu.” Nanaa alibaki akimsikiliza.

“Bila shaka umeshapata onyo la kwanza. Umerudishiwa miguu yako kwa kupewa nafasi ya pili ya maisha. Nakusihi uitumie vizuri. Itakapo kurudia tena, utajuta Nanaa. Hutakaa ukatoka kitandani mpaka kifo chako. Nakusihi acha kucheza na ndoa za watu. Mwache Geb. Kama ni huyo mtoto, tutamlea. Lakini ujue sitarudia kukuonya tena. Kaa mbali na Geb. Ni mume wa mtu.” Mwili mzima wa Nanaa ulianza kutetemeka. Akagundua kumbe mwanamke wa Geb ndio alihusika kumuwekea ukilema! “Kwa nini Geb hakuniambia?” Nanaa akajiuliza na kuumia sana.

Wakati akimsikiliza Mira, akamsikia Oliva akilia. Akakata ile simu, akakimbilia chumbani kwa mama G alipokuwa amelala mtoto wake. Akakuta amesimama. “Kwani umeita sana?” Nanaa akamuuliza mwanae wakati anamchukua. “Pole. Nilikuwa naongea na mtu kwenye simu. Umeamka salama?” Nanaa aliendelea kuongea na mwanae. “Njaa inauma? Eti Liv? Usikasirike bwana. Sikukusikia kipenzi changu. Njoo unyonye, labda utajisikia vizuri.” Akambusu, na kumuweka kwenye ziwa.

Mama G akaingia wakati Nanaa ananyonyesha. Akabaki ameduwaa. Nanaa hakuongeza kitu chochote. Akabaki ameinama akimnyonyesha mtoto wake huku akimchezea nywele. Liv alikuwa akinyonya kwa uchu wote, Nanaa ametulia kimya. Mama G alijua wazi mambo yamebadilika. Nanaa wa zamani angeshaanza kumsimulia juu ya ile simu. Lakini Nanaa huyu alitulia kana kwamba hapakuwa na jambo. Akasimama pale kwa muda mfupi, akaamua atoke.

“Nataka nimuogeshe huyo, niende kwenye biashara yangu mara moja. Sitakawia.” “Hamna neno mama. Wewe nenda tu. Nitamuogesha. Ukirudi ukiona sijamtakatisha mjukuu wako, mtaogeshana tena usiku.” Mama G akacheka kidogo. “Ule basi. Chakula kipo kingi tu kwenye friji. Na cha Oli nimeweka kwenye chupa yake. Leo nimemsagia kiazi na mboga za majani.” “Haya. Asante mama.” Nanaa akarudisha macho kwa mwanae, akanyamaza.

Kwa Geb.

Kitu cha kwanza alipoingia tu kwenye gari yake, akampigia simu Geb. “Kwema?” Geb akauliza. “Hivi ulishazungumza na Nanaa, habari za Mira?” “Hapana mama. Nilianza na kuzungumza naye habari za Zinda kwanza. Mambo ya Mira nimeona yasubiri kwanza.” “Kwa nini!?” Mama G akahoji. “Nanaa ni mjamzito mama. Ametoka kwenye kuumwa, akakutana na habari za Zinda. Zote zikionyesha kuwa wewe ndio umetoa maneno humo ndani. Ilibidi kumuweka kwanza sawa na kuandaa mazingira ya kumwambia mambo ya Mira.” Mama G akanyamaza kidogo.

“Kwa nini unaniuliza?” Geb akauliza, lakini kimya. “Mama?” “Mmmh! Sijui nifanyaje Geb! Nashindwa kukwambia. Asije akasema tena nimekwambia mambo yake.” “Kwani kuna nini? Mbona sauti yako si yakawaida, imejaa wasiwasi?” “Nitakwambia. Lakini naomba uniahidi hutamwambia Nanaa habari hizi.” “Nini?” Geb akahoji zaidi. “Mira amempigia simu Nanaa sasa hivi. Ameongea naye kwa kirefu tu. Nimemsikia akijitambulisha kama yeye ni mke wako na mpo kwenye maagano ambayo hata mizimu inatambua. Amemuahidi kumtumia picha kama uthibitisho wa mahusiano yenu. Na amemwambia alishapewa onyo la kwanza akalazwa mpaka hospitalini. Onyo jingine, amemwambia hatakaa atoke tena kitandani mpaka kifo.” “Mungu wangu!” Geb alisikika kwa sauti ya juu ya kushituka sana.

“Sasa sijui utafanyaje Geb! Ni mbaya sana kwa Nanaa kusikia kutoka kwa Mira. Ni heri angekusikia wewe mwenyewe kwanza. Na nimemsikia akimtambia kuwa anafanya kazi na wewe. Yaani ni kama umemuweka hapo kama mwenzio. Amemwambia ni biashara yenu.” “Mungu wangu nisaidie!”  Geb alisikika akimwita Mungu wake. “Sasa Nanaa amesemaje?” Akauliza tena. “Amenyamaza tu. Anaonekana wazi amenikasirikia. Mbali ya salamu na kuitikia ‘ndiyo’, nakusema atamuogesha Liv yeye mwenyewe, hajaniongelesha kitu kingine chochote.” “Wewe uko wapi?” “Naelekea dukani kwangu. Wamenipigia simu nakuniomba niende. Kuna tatizo kidogo. Ila nashauri usiende sasa hivi. Mwache kwanza kidogo. Fikiria chakufanya au chakuongea naye kwanza.” “Sawa.” Geb akakata simu akiwa amechanganyikiwa, hajui chakufanya. Tokea alipofika kazini siku hiyo, Mira hakuwepo.

Shetani Hana Usiku Wala Mchana.

 Hanaga Usingizi. Hachoki.

Wakati akimvalisha mtoto wake baada ya kumuogesha, akasikia ujumbe unaingia kwenye simu. Akamvalisha mtoto wake haraka haraka, akachukua simu yake. Mira alianza kumtumia picha za Oliva. ‘Huyu mwarabu wako nitamnyonga usingizini kama hutamtoa wewe mwenyewe kwenye maisha ya mume wangu.’ Ulikuwa ujumbe wa vitisho ulio mugopesha sana Nanaa. Alituma picha kama tatu za Oliva, kisha akatuma nyingine alizokuwa amepiga yeye mwenyewe Mira na Geb. Baadhi walikuwa na watu wengine. Mazingira ya pichani, yalionyesha ni kweli walikuwa wote nchini India. Hapo ndipo Nanaa alipomtambua Mira. Akaogopa sana. Mwili mzima wa Nanaa ulikuwa ukitetemeka kadiri kumbukumbu ya Mira ilivyokuwa ikimjia akilini.

Alimuona siku moja kabla ya kikao chao cha kwanza cha harusi, akizungumza na Grace na Geb. Tena akakumbuka waliongea na kucheka. Siku ya kikao, Nanaa akakumbuka vile Mira alipomsogelea kumsalimia. Kwa kuwa alikuwa amekaa na amempakata Fili, Mira alichuchumaa mbele yake baada ya kusalimiana na Geb. Alichuchumaa kumsalimia. Aliongea kwa sauti ya chini ili watu wengine wasisikie. Kuna vitu alizungumza mara kadhaa, Nanaa hakuwa akimsikia wala kumuelewa. Akainama ili kumfikia pale alipokuwa amechuchumaa akampa sikio. Maana Mira aliongea mara tatu bila Nanaa kumsikia. Ndipo akakumbuka kusikia mikono ya Mira ikimpapasa miguuni. Akashituka kidogo na kumuuliza vipi, akamwambia anamtoa uchafu miguuni. Mira alisimama, akaondoka bila Nanaa kumuelewa vizuri. Lakini kwa kuwa alimuona na Grace siku iliyopita, na wakasalimiana na Geb vizuri tu bila tatizo, hakuingiwa na wasiwasi. Akajua ni watu wakaribu ya kina Geb.

Ile picha nzima na yale aliyokuwa akimfanyia Nanaa siku ile, ilianza kumjia vizuri. Kama aliyefunguliwa macho, akawa amejua kabisa. Hata kule kumpapasa miguuni, Nanaa akagundua hakuwa akimtoa uchafu miguuni, bali alikuwa akimuweka zile pini. Nanaa akashituka na kusimama kama mshale, karibia kuanguka. Olivia alibaki akimwangalia mama yake.

Picha zake na Geb wakiwa nchini India ziliendelea kuingia. ‘Huu ndio uthibitisho wa ndoa yangu. Sasa litakalo kupata tena na kifaranga chako, usilaumu. Jua ulionywa.’ Ujumbe mwingine ukaingia. Nanaa alipousoma ni kama alipigwa na shoti ya umeme, akarusha ile simu kitandani. Akabaki akitetemeka huku akimwangalia mwanae kwa hofu.

~~~~~~~~~~~~~

Kwa haraka sana kama aliyekuwa ametumwa, akakimbilia stoo ya ndani ambayo huweka vitu wasivyotumia. Akachukua mabegi makubwa mawili. Akaingia chumbani kwa Oliva na bibi yake. Akaanza kukusanya nguo za mtoto wake na kuziweka kwenye begi moja. Akatoka kwa haraka. Akapiga simu getini na kumuagiza mlinzi mmoja akamchukulie taksii. Akakimbia juu chumbani kwao. Akakusanya baadhi ya nguo zake. Akashuka kwa haraka. “Mungu wangu nisaidie.” Nanaa alikuwa akiongea huku akihema na kukimbia juu na chini ya ile nyumba, kama aliyechanganyikiwa. “Huyu msichana atakuja kuniulia mwanangu. Heri mimi hata nikifa hakuna atakayepata hasara.” Nanaa aliendelea kukusanya vitu vyake.

Simu kutoka kwa mlinzi iliita kumtaarifu Nanaa wamepata taksii. Akaamuru iingie ndani kabisa. Akapandisha mabegi yake mawili kwenye ile taksii, akarudi ndani, akachukua kalamu na karatasi.

 Geb!

Sikuwa nikijua kama una mke ambaye anakuhitaji kiasi cha kunidhuru mimi. Nimeamua kuondoka mapema kabla Mira hajamdhuru mwanangu. Sihofii juu yangu. Kwani hata akiniua mimi, hakuna atakayepata hasara. Najua itakuwa pumziko kwa wengi, lakini si Liv. Nitamtunza na kumlinda na kila hatari. Hata kama itagarimu furaha yangu. Nimeamua kwenda kuanza maisha yangu sehemu nyingine nikiwa na watoto wangu wote. Nina kuahidi kukutafuta nitakapo tulia. Inaweza kuchukua muda kidogo. Lakini nakuahidi kukutafuta nikipata kazi na sehemu nzuri ya kuishi na watoto. Nakuahidi kumpa Liv na mdogo wake maisha mazuri kama unayotamani. Nitahangaika. Naamini nitafanikiwa mapema tu. Niombee uzima na nguvu. Nina kuahidi sitakutenga na watoto wako. Nikitulia nitakujulisha nilipo. Ili kama utapenda, uwe unakuja kuwaona wanao. 

Najua ulininunua kwa pesa nyingi sana. Lakini Geb, nakuahidi kukurudishia pesa yote. Nikianza tu kazi, nitakuwa nakutumia kila mwezi pesa kiasi kupunguza deni. Naomba usiumie ukadhani pesa yako imepotea bure. Nitairudisha kama ilivyo. Tafadhali sana, nakuomba Geb, usimdai kaka. Mimi mwenyewe nitairudisha. Tafadhali nivumilie. Najua hii pete imekugarimu sana. Nakurudishia pamoja na cheni aliyokuwa amenikabidhi mama. Tafadhali mrudishie mama mwenyewe. Naona mimi sio mtu sahihi aliyetakiwa kunipa hiyo cheni iliyobeba historia nzito hivyo. Nashukuru sana kwa kila kitu. Nakuombea uzima na furaha.

Nanaa!

          Akaiweka ile karatasi pale mezani pamoja na cheni na ile pete ya uchumba, akaondoka kwa haraka kama anayekimbizwa.

~~~~~~~~~~~~~

“Tunaelekea wapi?” Yule dereva taksi akauliza. “Stendi ya mabasi yaendayo mikoani.” Dereva akaaondoa taksii. Swali anakwenda wapi baada yakufikishwa stendi, likaanza kumsumbua. Nanaa hakua akijua kokote zaidi ya Moshi alikozaliwa, hapo jijini Dar ambapo napo ni shule ndio iliyomtoa mkoani Moshi na kumfikisha hapo, na Morogoro ambako alipelekwa na Geb.

          Wazo la kukimbilia Morogoro lilipomjia, akapingana nalo kabisa. “Morogoro hapana. Hapo ni karibu sana. Anaweza kunifuata bila shida.” Wazo la kikimbilia Moshi hakutaka hata kulipa nafasi hata kidogo. Ni mkoa ambao haukuwahi kumtendea vyema. Tokea anazaliwa mpaka anaondoka mkoani hapo. Ilikuwa machungu matupu. “Moshi hata kwa fimbo, sitarudi.” Nanaa aliendelea kuwaza wakati dereva taksii akiendelea kuendesha.

Ilikuwa ni saa 4 kamili asubuhi wakati dereva taksii huyo akiingia standi. Mpaka wanaingia hapo, Nanaa hakuwa akijua akimbilie wapi na mwanae. Aliposikia mtu mmoja akiwakimbilia huku akitangaza kuuza tiketi ya mwisho ya basi linaloelekea Arusha muda mfupi sana kuanzia hapo, Nanaa akashawishika. Hakuwahi kufika jijini Arusha. Lakini Alex, mpenzi wake wakwanza, alikuwa akilisifia jiji hilo nakumwambia ipo siku atampeleka huko wakatembee. Lakini mpaka anamsaliti, hakuwahi kumpeleka. Waliishia kulala naye kwenye nyumba za wageni hapo hapo Moshi.

Akamuomba dereva taksii asimamishe gari pembeni ili anunue hiyo tiketi ya kuelekea Arusha. Hakutaka hata kujua ni basi gani. Ilimradi alisikia ni basi litakalomtoa jijini hapo kwa haraka, Nanaa akanunua tiketi. Yule kijana aliyemuuzia akamwambia amebahatika nafasi ya dirishani. Nanaa akamshukuru na kumwambia kwa kumuhakikishia kuwa hamwibii, waongozane mpaka kwenye basi hilo ndipo atakapomlipa hiyo pesa. Yule kijana akiwa anatembea, Nanaa bado yupo ndani ya taksii amekumbatia mwanae kama alumasi anayoogopa asipokonywe, akakubali.

Wakaongozana mpaka kwenye hilo basi. Ni kweli akamsaidia na kupandisha mizigo yote, akamlipa na pesa ya ziada kama shukurani, Nanaa akakaa na mtoto wake huku akihema. Baada ya dakika chache sana, basi hilo lilifanikiwa kumtoa Nanaa na Oliva jijini Dar es salaam, kwa ahadi ya kuwafikisha jijini Arusha salama. Hakuwa akiamini wakati basi hilo linaacha jiji. Akamtizama mtoto wake kama yupo salama. Wakagongana macho. Oliva alikuwa ametulia akimtizama mama yake. Akamshika kichwa kama kupima homa na kuhakikisha yupo salama, akamkuta ni mzima, ila tu ametulia kama anayejua kinachoendelea. “Asante Mungu wangu!” Nanaa alijikuta akishukuru kama aliyeokoka na ajali ya moto.

Akambusu mtoto wake. Oliva alikuwa ametulia tuli. Hata Geb alishamjua mtoto huyo. Ni kama anajua kama mama yake hayupo sawa. Alikuwa mchekaji sana. Lakini mama yake asionyeshe kutokuwa na furaha usoni hata kidogo. Oliva hatacheka hata iweje. “Liv!” Nanaa akamwita kwa upole. “Unakumbuka nilikuahidi hakuna kutengana?” Akamuuliza kama anaelewa. “Basi, bado natunza ahadi yangu. Sitakuacha popote pale mwanangu. Na wala sitakubali mtu akudhuru. Nitakulinda. Umesikia eeh! Usiogope. Kila kitu kitakuwa sawa.” Nanaa alishazoea kuzungumza na huyo mtoto tokea yupo tumboni. Ukiwa nje ya chumba walichopo wao, unaweza fikiri Nanaa anazungumza na mtu mzima. “Lala tu, mama atakukumbatia.” Akamuweka sawa mwanae. Akamkumbatia kama alivyomuahidi. Akamfunika na mtandio wake ambao huwa anamfunika wakati wote akimnyonyesha. Na yeye akajiweka sawa akiwa amempakata vizuri. Liv alilala hata kabla hawajafika mjini Kibaha. Baada ya muda mfupi tu alipomuona mtoto wake amelala na yupo sawa, na yeye akalala.

Huku Nyuma Nyumbani Kwa Geb.

Geb alipata wakati mgumu sana kusubiri kazini mpaka mchana kama alivyoshauriwa na mama yake. Alishindwa hata kumpigia simu Nanaa, kuogopa asije piga na kuropoka na kuharibu mambo zaidi.  Kazi zilikuwa haziendi. Kila wakati macho kwenye simu ya mkononi, ukutani na kompyuta kana kwamba kuna moja inaweza ikampa muda usio sahihi. Ilipofika saa saba mchana, akarudi nyumbani akiwa na makopo ya ice cream mawili. La Vanilla na Chocolate na chakula. Alimnunulia Nanaa kuku wa kuchoma.

Alijua ni mpenzi sana wa nyama. Akafungiwa na Chips, akarudi nazo zikiwa zimefungwa vizuri tu. Akajua hata kama Nanaa hasikii njaa, ile harufu ya yule kuku lazima atamshawishi tu. Alirudi akiwa ameshajiandaa kwa hoja zake zote. Alishazipanga, akazirudia akiwa peke yake mpaka akaridhika kuwa lazima Nanaa ataelewa tu na kusamehe. Alipoingia akakimbilia juu baada ya kukuta nyumba ipo kimya. Akajua atakuwa amelala na mtoto wake chumbani kama usiku uliopita walipotoka Morogoro. Lakini hakuwepo chumbani.

Akampigia simu. Akasikia ikiita chumbani kwa mama yake. Akajua amelala na Oliva chumbani kwa mama yake. Akashuka ngazi akikimbilia chumbani kwa mama yake. Hakumkuta Nanaa. Akapiga tena simu yake, akasikia mlio ukitokea mwisho kabisa wa kitanda cha mama yake, uvunguni upande wa ukutani. Akapanda na kuitoa.

Macho yake yakakumbana na picha zake akiwa na Mira, nchini India. Akaendelea kuangalia. Picha hizo alikuwa ni yeye na Mira. Nyingine akiwa na watanzania wengine. Geb akakaa. Akaendelea kuziangalia. Macho yake yakatua kwenye picha za Oliva. Zote alizitambua ni picha alizokuwa amempiga mwanae na kuzipenda sana. Oliva alikuwa akicheka. Akaenda kuzi print. Akaziweka kwenye fremu nzuri sana na kuzitundika ofisini kwake. Geb alishangaa sana.

“Huyu msichana anaonekana alikuwa akinifuatilia kwa muda mrefu sana bila ya mimi mwenyewe kujua! Ameingiaje ofisini kwangu na kupiga picha, picha za mwanangu!” Geb akaendelea kujiuliza akizidi kushangazwa na kumbukumbu za muda mrefu alizotunza Mira.

Na yeye akakumbana na jumbe za vitisho kutoka kwa Mira. “Hapana. Hapa amefika mbali sana!” Geb aliendelea kuzungumza akiwa peke yake pale chumbani kwa mama yake huku akisoma na kuangalia zile picha kwa kurudia rudia. “Atakuwa amemuogopesha sana Nanaa, ndio maana ametupa na simu. Nanaa atakuwa yuko wapi?”  Geb akasimama nakutoka pale chumbani. 

Ndipo macho yake yakatua juu ya meza aliyozoea kuweka funguo zake za gari kila anapoingia ndani. Wakati ananyanyua zile funguo za gari ili atoke akamwangalie Nanaa huko madukani akidhani pengine alitoka kufuata kitu dukani ndipo akaona karatasi imeandikwa “Geb!” Akajua ni ujumbe kutoka kwa Nanaa. Wakati anaingia, alirusha tu funguo bila kuangalia mezani kwani alikuwa na haraka yakumuwahi Nanaa.

Akaanza kusoma. “No no no noooo!” Alijikuta akikataa kile alichotaarifiwa na Nanaa. Akahisi hakusoma vizuri. Akarudia kusoma tena. “No way! This is not happening to me. No way!” Gafla akahisi dunia imemuangukia. Nanaa ameondoka na faraja yake! Nanaa amebeba mipango mizima ya Geb. Bila kujijua yeye ndiye akawa amebeba ratiba na mipango yote ya maisha ya Geb yaliyobaki hapa duniani. Nanaa ameondoka! Kwa sekunde kadhaa dunia iliacha kuzunguka mbele ya macho ya Geb. Akahisi ni kama giza limemfunika machoni.

Kwa gafla sana kila kitu kikakosa maana hapa duniani. Aliliangalia lile jumba na thamani yote mle ndani. Gafla ikawa ni kama amesimama jagwani kwenye jua kali. Hata kiyoyonzi kilichokuwa kinapuliza mle ndani, hakukisikia tena. Akaanza kuhisi joto kali. Magari yote yaliyokuwa hapo nje ya hilo jumba. Ambalo alilijenga kwa mamilioni ya pesa alitamani yawe msaada kumtoa hapo na kumpeleka alipo Nanaa na watoto wake. Lakini yalishindwa. Yalihitaji kuongozwa. “Amekwenda wapi Nanaa?” Lilikuwa swali ambalo hata hayo magari, yasingeweza kumsaidia, kumtoa hapo na kumfikisha alipo Nanaa.

Akakumbuka mamilioni ya pesa aliyonayo benki. Akajua hayatasaidia kitu chochote kukamilisha furaha yake tena hapa duniani. Yangekuwa na maana tu kama yangeweza kutumika kumwambia Nanaa alipo na watoto wake. Akakumbuka pesa alizolipa kwa ajili ya kumpata Nanaa, siku alipomsahau nje ya ukumbi wa harusi ya Malii. Alimlipa Mlinzi wa benki akamsaidia kwenda naye kwenye kampuni ya simu, akafanikiwa kupata namba ya Antii na kumkuta Nanaa hospitalini. Lakini leo pesa yake imekuwa bubu. Haiwezi kuongea. Nanaa ameacha simu. Labda angekimbilia kwenye kampuni ya simu ili awalipe mamilioni ya pesa wamwambie ile simu inaonyesha ipo wapi kwa wakati ule ili amfuate Nanaa na Oliva, furaha ya moyo wake. “Mungu wangu naomba usiniache!” Akajikuta amepiga magoti pale pale, machozi yakimtoka. Hapakuwa na tumaini tena.

Akarudia tena kusoma ule ujumbe alioachiwa na Nanaa. Akagundua ameelewa kile kilichoandikwa. Akajiambia kabla hajarukwa na akili, watu wasijue ni kwa nini, basi amtaarifu mama yake. Walishaongea muda mfupi kabla hajarudi hapo nyumbani. Mama yake akamwambia yeye bado yupo kwenye biashara yake. Geb alikuwa sawa tu mara ya mwisho alipokuwa akizungumza na mama yake. Lakini safari hii alipiga akiwa analia.

Kwa Mama G.

“Mama!” Geb aliita mara baada ya mama yake kupokea. “Kuna nini wewe!?” Mama G akauliza kwa mshituko. “Nanaa amenikimbia mama. Nimemchelewa kidogo tu!” “Mungu wangu!” Mama G akaweka mikono kichwani. Simu ikaanguka. Geb akarudi kwenye kochi akakaa. Geb yule wa mipango, mwenye majengo yanayoingiza pesa wakati wengine wakilia njaa. Ambaye akifika mahali hata wazee wanasimama. Anayeongoza wanaume na wanawake wasiopungua ishirini kwenye biashara zake tu. Ambao wanategemea kupokea kutoka kwake kila mwisho wa mwezi ili nao watunze familia zao. Geb ambaye walio kwama kifedha wanamkimbilia kukopa mamilioni ya pesa.  Jumatatu hiyo, mchana, siku ya kazi, mwanamke amemfanya apige magoti na kujikuta akilia kama kitoto cha kike.

Kwa James.

Baada ya muda, akampigia simu James kumtaarifu. Ndani ya lisaa limoja nyumba ya Geb ilishakuwa na wageni. James, Grace, mama yake, Danny na watoto wote. Kila mmoja alisoma ule ujumbe kwa kurudia rudia. “Kwa nini hukumwambia Geb? Ujue aliponipigia simu kuniambia mnakwenda Morogoro kupumzika, nikajua mnakwenda kuzungumza!” James akalaumu.

“Kama ulikuwa huwezi kuzungumza naye, ungeniambia tu mimi mwenyewe nikajua jinsi ya kuzungumza naye. Unajua ni mjamzito, halafu ana mtoto. Unafikiri ataishije sasa!? Nanaa haifahamu kabisa hii nchi!” James aliendelea kulaumu kama kawaida yake kwa dada yake.

“Kwa nini hukumwambia Geb? Huyu Mira atakuwa amemuogopesha sana ndio maana ameamua kukimbia.” Grace aliongea kwa unyonge akimuhurumia kaka yake. “Jamani, Nanaa aliyaona mabadiliko ya Danny. Akaanza kuwa na wasiwasi. Akaniuliza mbona Danny hana furaha. Ndipo ikabidi kumuelezea mahusiano ya Danny na Zinda. Nia yangu ilikuwa ni kumtoa hapa, nimpeleke sehemu iliyotulia ili niweze kuzungumza naye. Kwanza ili kujibu maswali yote aliyokuwa nayo Nanaa juu ya ugonjwa aliopata wa gafla, na habari za Zinda.” Geb akaendelea.

“Nilipokuwa nikimuelezea mahusiano ya Danny na Zinda tu, hata sikuwa nimemaliza habari nzima, tayari Nanaa alishakuwa amepata majibu yake. Alilia sana, akihisi amesalitiwa. Ilimchukua muda mrefu sana kutulia. Ilibidi kumueleza taratibu kwa nini maneno yalimfikia Zinda.” “Mimi nilimuona tokea mwanzo jinsi alivyomuuliza mama kama yeye ndiye aliyemwambia Zinda. Mama unakumbuka? Akasema ningeumia sana kama ni mama. Maana mama ndiye msiri wake.” Grace aliongeza.

“Nakumbuka. Na amerudi kutoka safari, ameshindwa hata kuniangalia usoni. Najuta! Unajua Mira alizungumza naye nikiwa hapahapa! Ingekuwa zamani angeniambia. Lakini alinyamaza kabisa. Mpaka namuaga nakwenda kazini, alionyesha yupo sawa tu na hana kitu chakuzungumza na mimi.” “Nimekuta hizi picha na jumbe za vitisho sana kutoka kwa Mira. Mira amemtumia kwenye simu yake. Nina uhakika hizi ndizo zimemkimbiza.” James akachukua ile simu kutoka kwa Geb. Akaanza kuziangalia.

“Mbona ulisema ni kama hamkuwa na mahusiano!?” “James! Huyo dada hatukuwa na mahusiano naye, ila tumeishi naye.” “Picha zako zinaonyesha tofauti Geb! Kama hii mmepiga akiwa amekuegemea begani! Hapa mmekaa karibu kabisa! Na picha za Oliva amezipata wapi!?” James aliendelea kuhoji huku akiperuzi kwenye simu ya dada yake.  “Sidanganyi James. Huyo dada sikuwahi hata kumfikiria kimapenzi. Na Mungu wangu ni shahidi. Na picha zote hizo zimepigwa kwenye mikusanyiko ya watanzania. Sio kwamba nilikuwa nikipiga naye mimi peke yangu! Na picha zote hizo nikiziangalia, nakumbuka kabisa ni picha tulizopiga siku tulizokuwa watanzania tunakutana kwenye sherehe au mikutano ya watanzania. Sasa labda yeye alikuwa akinitega kwa madhumuni yake. Lakini sikuwahi hata kuwa na wazo naye.”

“Amekuja kuomba kazi kwangu, nikamuajiri kama mfanyakazi wa kawaida tu. Muulize hata Grace. Hata sina muda naye. Mungu wangu ni shahidi. Grace ndiye anayemsimamia na tuseme yuko chini ya Grace. Sipo karibu naye kabisa labda atumwe kitu kwangu na Grace, basi.  Nisingemdanganya Nanaa. Nampenda Nanaa. Na picha zote hizo za Oliva ni picha nilizo tundika ofisini kwangu. Hizo mbili nimening’iniza ukutani, pamoja na za Nanaa, na hii ni picha ambayo nimeweka mezani kwangu. Tena ipo nyingine ya Nanaa akiwa amembeba Liv. Muulize Grace. Au twende ofisini kwangu hata sasa hivi utaona. Ofisi yangu imejaa picha za Nanaa na Oliva tu. Nina uhakika ndiko alikoziona hizo picha. Niamini nampenda Nanaa. Siwezi kumchanganya na mwanamke mwingine yeyote yule James. Sithubutu.” Hilo James alilithibitisha pale Nana alipougua. Akanyamaza.

“Sasa unafikiri atakuwa ameenda wapi?” Mama G akamuuliza James. “Sijui! Mimi ndiye familia ya pekee ya Nanaa. Hana pakwenda na hafahamu hii nchi vizuri. Kwanza hana uzoefu wa kusafiri kwenye mabasi. Kwanza hata sikumbuki kama alishawahi kupanda mabasi makubwa kumpeleka sehemu yeyote. Labda HIACE. Kumtoa pale Moshi mjini kumpeleka vijijini. Hata kuja hapa Dar kwenyewe mimi ndiye nilimleta na gari yangu. Nanaa hafahamu mambo mengi na hicho ndicho kinachoniogopesha, tena akiwa ni mjamzito na mtoto juu! Sijui kama anapesa yakumtosha au la!”

“Nanaa anazo pesa. Anapesa nyingi tu. Huwa nampa kila mwisho wa mwezi kama mshahara, kwa matumizi yake binafsi ili asiwe anashida ya pesa. Huwa nampa pesa nzuri tu. Grace akilipa mishahara, nahakikisha na yeye namgawia kutoka kwenye mshahara wangu. Namwingizia asilimia 80 benki halafu 20 huwa namletea hapa nyumbani. Kwa hiyo swala la pesa hilo usiwe na wasiwasi nalo. Na nitaendelea kumuwekea tu, hata kama sitampata.” Geb alijibu kinyonge akisikika amekata tamaa. 

“Kama ni hivyo, ni sawa. Lakini nashauri mumpe muda. Mwacheni atulie tu. Amesema atakutafuta. Basi atakutafuta.” James alisikika amepata aghueni baada ya kusikia dada yake ana pesa. Akasahau pesa si kila kitu.  “Lakini ataishije mwenyewe akiwa na mtoto na ni mjamzito? Hata akiwa na mamilioni ya pesa yanayoingia kila siku bila kuzungukwa na watu wanaompenda na kumthamini, haitamsaidia chochote. Mbaya zaidi akiwa amejawa na hofu! Halafu amejazwa maneno yaliyojaa uongo na usaliti kutoka kwa Mira bila yakusikia upande wangu! Najua sasa hivi amejawa hofu, usaliti na majuto.” Geb alisikika akiwa amenyong’onyea.

“Na lazima atajisikia hivyo. Ameona picha. Halafu amejua unafanya naye kazi siku zote. Kwa nini usimwambie siku zote, mpaka yeye mwenyewe ndiye amekuja kumwambia? Hujui amemwambia nini mbali ya hizo jumbe zakutishia maisha yake na mtoto wake. Nanaa yupo kwenye hofu sana. Ameshuhudia kile huyu anayejiita mke wako, akimtendea yeye. Unyama mkubwa. Lazima sasa hivi anajua hizo jumbe sio za vitisho. Anajua ni kweli ana uwezo wa kuja kumdhuru tena yeye na mtoto wake pia. Lazima aogope na kujiweka mbali. Hasa akijua kwa kutomtaja Mira kwake ni kwa kuwa upo upande wake Mira.” James aliendelea kupalia makaa ya moto.

~~~~~~~~~~~~~

Ni bandika Bandua. Likiisha hili, linaanza jingine.

 Jamani! Nani ni wa Nani?

Hata Nanaa amechanganyikiwa na kupoteza dira, akaamua kuachia gazi.

 Zinda amedai Nanaa ni mkewe, huku Mira naye anadai Geb ni wake!

Geb anamwambia Nanaa amemchagua yeye, huku anapata habari kutoka kwa Mira kuwa ni wa Geb!

Walikuwa mbuga za wanyama kwa takribani siku tatu, kwa nini asimwambie? Alimuona pia na Grace, inamaana hata Grace anamfahamu wifi yake Mira. Usaliti wa namna gani?

Nanaa aliwaza wakati anaondoka.

Anaelekea wapi?

Ø  Ni Nanaa huyu huyu aliyekuwa ametokewa na malaika siku chache zilizopita. Akaamuona mtu akipigana vita yake na kumwambia yupo mtu anayepigana badala yake. Lakini ndio huyu huyu leo anakimbizwa na simu na ujumbe kutoka kwa Mira.

Ø  Alisimamia Imani ya Geb mpaka akapokea muujiza wake, leo ameweka kila kitu chini. Pete ya Geb na cheni ya dhahabu ya mama G, anakimbia na faraja ya Geb, Oliva!

Usikose kufuatilia Visa na Mikasa ya Simulizi hii ya kusisimua.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment