Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu Ya 41. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu Ya 41.

 Nanaa akaendelea kuwaza kwa sauti asijue shida anayowapa wenzake waliomzunguka pale. “Kwanza anasema tulifunga naye ndoa tarehe ngapi? Uliweza kusoma tarehe?” Nanaa akauliza na kuwatoa wote mawazoni. “Nilikipiga kile cheti picha kwa kutumia simu   yangu. Nilifanya      kwa    siri.  Ngoja nikuangalizie.” James akatoa simu yake akaanza kutafuta. “Hii hapa.” Akamuonyesha. “Ni muongo jamani huyu kaka!” Nanaa akaangalia ile picha. “Hiki si cheti cha Kenya!?” “Anasema mlisafiri mpaka Kenya.” James akajibu.

“Muongo kabisa huyu kaka. Huko Kenya mimi hata sijui kunafananaje! Tena kipindi hiki ndio nilikuwa nikisumbuliwa sana na kizunguzungu. Nakumbuka ni mwezi huu huu wa kumi ndio kizunguzungu kilinitesa sana. Nitaenda kuangalia tarehe kwenye mfuko niliokuwa nikiweka vitu vya hospitalini kipindi mjamzito wa Oliva. Nilikuwa na File maalumu la hospitalini. Nilikuwa nikiweka kila kitu humo ndani mpaka risiti kama nilinunua dawa au nililipia kumuona daktari. Nitaangalia kuthibitisha. Nakumbuka kuna weekend moja ilinilazimu kurudi kumuona daktari sababu nilianguka nikiwa peke yangu kwenye ngazi, sababu ya kizunguzungu. Nilipoamka tu, nikampigia simu daktari nikamuomba anione.” Nanaa akaendelea kukumbuka.

“Sasa kwa kuwa yule daktari nilishampa historia yangu na nikamsihi anisaidie kwa karibu sana ili nisije kufa nikamuacha Oliva peke yake, basi alikuwa akinisaidia sana. Muda na wakati wowote nilikuwa nikimpigia simu, anapokea. Ilikuwa siku ya jumamosi. Nakumbuka nilipanda daladala akaniambia nimfuate alipo. Alikuwa yupo hospitali ya Tumaini. Nikamwambia nilianguka sababu ya kuona giza. Akaniambia nipime damu. Ndio akagundua sina damu kabisa. Akataka kunilaza ili niwekewe damu. Ndio nikamwambia siwezi kulazwa. Kwanza nilikuwa sina pesa. Akasema atanisaidia lakini lazima niwekewe damu.” Nanaa akaendelea.

“Nikamwambia pia sina mtu wakuanza kuniuguza pale hospitalini. Maana nilijua yupo busy sana. Asingeweza kuniuguza. Halafu nikamwambia nipo chuo. Nina mitihani mingi sana, siwezi kulazwa. Baada ya kumkatalia swala la kulazwa, ndio akaniandikia vidonge, na kuniambia lazima nipate muda wa kupumzika. Nile vyakula vya kuongeza damu, halafu nirudi kumuona ili kujua kama damu imeongezeka. Kwa hiyo Zinda ni muongo. Ngoja nikuletee uthibitisho kaka. Nilitunza kila kitu.” Nanaa akasimama.

Akaelekea stoo alipokuwa amehifadhiwa vitu vyake vyote vya chuoni. Akaanza kupekua humo ndani. Pale sebuleni palikuwa pamezuka ukimya mkubwa sana. Nanaa alikuwa akimtaka kumjua mtoa siri zake. Geb naye akaongezewa mawazo. Akaumizwa kujua Nanaa alikuwa na matatizo ya afya kipindi mjamzito wa kuyo mtoto aliyezoea kucheza kifuani kwake.

“Faili lenyewe hili hapa kaka.” Nanaa akarudi na faili kubwa. Macho yake yalikuwa yakisaidia kutafuta. “Amesema tulifunga ndoa tarehe ngapi?” Nanaa akauliza tena. James akamtajia. “Tena kila kitu nimekipanga kwa tarehe!” Nanaa akakaa chini huku akitafuta hiyo tarehe. Akakutana na picha za Ultrasound. Akacheka. “Unataka nikuonyeshe picha za Oliva wakati yupo tumboni?” Akamuuliza kaka yake. James akacheka. “Hembu tumuone.” Nanaa akampa kaka yake.

“Na mimi naomba kuona, Nanaa.” Geb akasimama. Akamsogelea James. James akaangalia, akamkabidhi Geb. Geb akacheka. “Nilikuwa nafurahi kweli nilivyokuwa nikionyeshwa kwenye machine!” “Nashukuru umezitunza Nanaa. Ukumbusho mzuri sana.” “Kweli Geb? Maana mimi nilikuwa naweka tu.” “Muhimu sana. Asante.” Nanaa akamtizama Geb, akacheka. Akaenda kukaa pembeni yake. “Pole kwa matatizo yote yaliyokuwa yakikupata peke yako wakati ulipokuwa mjamzito.” Nanaa akacheka kidogo. “Asante Geb. Namshukuru Mungu kuniwezesha.” Wakataka kupena mabusu, Nanaa akakumbuka kitu.

“Subiri kwanza kaka. Sasa kama Zinda anasema alinioa, aliwezaje kuishi na mimi nikiwa na mimba ya Oliva!?” “Anasema ulimwambia, akakukubalia kuwa atamtunza mtoto.” “Zinda ni mwendawazimu! Sasa anasema baada ya ndoa ikawaje?” Nanaa aliendelea kuhoji. “Anasema mlienda kuishi naye.” Nanaa akaanza kucheka. “Sasa kama nilikuwa nikiishi naye, iweje leo niwe hapa?” “Anasema ulipokaribia mitihani yeye akiwa nje ya nchi kikazi, ilikulazimu uhamie hosteli. Ndipo ukajifungua. Ulipojifungua, Geb akajua una mtoto wake, akaja kukupokonya mtoto. Wewe ndio ukamfuata. Ndio Geb akakufungia. Ukamwambia..” Nanaa akakunja uso. “Subiri kwanza kaka. Zinda anaonekana anaongea uongo unao sindikizwa na ukweli! Hayo mambo nani amemwambia!? Maana hata wewe hukuwa ukijua! Hayo mambo yalitokea kati yangu mimi, mama na Geb tu. Hakuna mtu mwingine alijua! Ni mambo ya ndani sana. Nani atakuwa anaongea mambo mazito hivyo, tena ya ndani sana, kwa watu wa nje!?” Kimya. Nanaa akashangaa watu wote wameinama.

“Naomba nikuombe kitu kaka. Nimekuwa na maswali ambayo hakuna mtu anayenipa majibu. Kuanzia mtu aliyetaka kuniangamiza, mpaka mtu anayetoa maneno humu ndani. Hiyo ni tabia mbaya sana. Kuna mambo ambayo huwa yakitokea, hayafai hata kuja kuzungumzwa tena! Lazima nijue. Nijue nani anataka kuniangamiza. Na kwa nini! Nani anatoa maneno humu ndani. Na anayapataje! Maana humu ndani watu wanaokuja ni watu wa kusafisha. Na wanakuja mara mbili kwa week tu. Na mara nyingi wakija huwa tunawapisha. Sasa nani anakuwa anatusikiliza? Jibu atakuwa nalo Zinda. Naomba unisindikize kuzungumza na Zinda. Nitamuomba tuonane naye. Akikataa nitamfuata hata kwake.” “Akikushitaki?” “Mimi si ni mkewe?” James akacheka.

“Si ndio vyeti vinavyosema? Sasa nataka nikazungumze naye. Si ni sawa Geb?” Geb akabaki akimwangalia. Nanaa akajua wazi huko ndiko kukataliwa. “Naomba usikatae Geb, tafadhali. Zinda hawezi kuwa sababu ya mimi kutokuolewa na wewe. Au umebadili mawazo.” “Hapana Nanaa. Unajua jinsi ninavyokupenda. Natamani hata kesho nikuoe.” Nanaa akacheka. “Basi sasa kwa nini huniungi mkono katika swala la kutafuta suluhisho? Au umekata tamaa?” Nanaa aliendelea kumuhoji Geb taratibu. “Sijakata tamaa Nanaa. Lakini unakumbuka ulimuuliza hata malaika ni nani amekuweka zile pini, lakini hakukwambia?” “Kwa sababu alikuwa akinielekeza kila kitu kwako Geb. Mungu anataka wewe ndio uhusike na mimi si vinginevyo.”

“Hudhani kwamba anakulinda? Labda anadhani haupo tayari na ukweli.” “Sidhani Geb. Mungu amekuamini na maisha yangu. Anajua wewe utaniongoza vizuri. Ndio maana anataka kila kitu kizuri, kianzie kwako.” “Una uhakika?” Nanaa akacheka. “Kabisa. Sasa unafikiri ni kwa nini alitaka wewe ndio uwe chanzo cha uponyaji wangu? Mungu anakuamini na maisha yangu Geb.” Geb akamtizama.

 “Mbona kama huamini!?” Nanaa akauliza. “Hilo naliamini. Lakini je wewe unaniamini?” “Nakuamini sana Geb!” “Una uhakika?” “Zaidi ya asilimia 100, Geb. Mungu amekutumia sana kwenye maisha yangu. Na nimetumia Imani yako kama ulivyoniambia pale hospitalini nikiwa nimekata tama, nikiwa hata simwamini Mungu. Lakini nikakuamini wewe, umenisaidia nimerudi kwa Liv. Nakuamini sana.” Nanaa asijue anajifunga mwenyewe.

“Basi naomba tulia kwanza kwa sasa hivi. Acha tutafute njia nyingine yakumaliza hayo matatizo na kufunga ndoa yetu. Ukitafuta nani amefanya nini sasa hivi, haitasaidia. Utapoteza muelekeo mzima wa kwa nini upo hapa leo.” Nanaa akatulia kidogo. Hakutegemea jibu la namna ile kutoka kwa Geb.

Akamgeukia vizuri Geb, akamtizama. “Wewe unafahamu ni nani amefanya hayo yote?” Lilikuwa swali la moja kwa moja lililozua ukimya wa gafla. “Geb?” Nanaa akaita kwa upole. “Ndiyo nafahamu.” Geb akajibu. Wakabaki wakiangaliana. Nanaa akakunja uso, akainama. “Nanaa! Naomba nipe muda. Nipo kwenye maombi. Namuomba Mungu atusaidie hekima juu ya hili.” “Sasa unajuaje labda kwenda kwangu kwa Zinda ndio msaada wetu?” Nanaa akauliza huku akifuta machozi. “Umesikia habari nzima juu ya Zinda. Amekusudia kutukomoa, Nanaa. Amekwenda umbali mkubwa sana kutengeneza uthibitisho utakaozuia nisikuoe. Amekusudia. Lazima kuwa makini kwa kila tunachotaka kufanya. Najua sasa hivi anategemea sisi tufanye mambo fulani fulani kujibu mashambulizi yake. Na kwa kahika amejipanga. Tena amejipanga vizuri tu. Naomba tupate muda wa kumsikiliza Mungu. Tujue anataka atusaidiaje katika hili.” Geb alimvuta mkono.

“Wewe si unasema unaniamini?” Geb akamuuliza. Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Lakini nataka kujua. Geb.” “Nafahamu. Basi naomba nipe muda. Sawa?” Nanaa akanyamaza. “Nanaa?” “Huniamini Geb!” “Nakuamini sana Nanaa. Lakini naomba tupate muda na Mungu kwanza. Tukikubali kuwa wepesi wakusikia au kusikiliza kila mtu, nakuhakikishia anguko letu halitakuwa mbali. Tutaanguka na kutengana kwa haraka sana. Zinda sio adui yetu wa kwanza. Anatumiwa na shetani. Na usifikiri atakuwa mtu wa mwisho kumtuma kwetu kutuchafua. Bado tutakutana na makwazo mengi na watu wa aina ya Zinda ni wengi tu. Tukiwa watu wa haraka kujibu kila mashambulizi, hatutafika mbali. Umemuona Mungu alivyotutoa kwenye mtego mkubwa sana wa shetani. Amepigana vita vikubwa sana kwa niaba yetu.” Geb akaendelea.

“Hatuwezi kitu bila msaada wa Mungu. Hatutafika mbali. Nahitaji muda wetu sisi na Mungu kwanza. Kumbuka kwa nini Mungu ametutoa hospitalini. Kumbuka kilio chako. Naomba usipoteze muelekeo. Tafadhali Nanaa.” “Nitasubiri Geb.” Nanaa akajifuta machozi. “Asante. Nakuahidi kwa wakati unaofaa, nitakwambia kila kitu. Lakini sio sasa hivi. Mungu ametupa nafasi yakuwa pamoja. Hata masaa 24 hayajaisha tokea upokee uponyaji tuliokuwa tukililia kwa ajili yako mwenyewe na familia yetu. Naomba urudishe mawazo kwa mtoto aliyekuwepo tumboni na sisi.” Nanaa akajishika tumbo.

Akamuona anatabasamu. “Halafu kila saa nasahau hata kama ni mjamzito!” “Kwa kuwa akili yako ina mambo mengi. Naomba urudishe mawazo humu ndani. Halafu mambo mengine niachie mimi. Sawa?” Geb alikuwa akizungumza naye taratibu tu. Kila mtu akiwasikiliza. Nanaa akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu huku akijirudisha nyuma. Akajiegemeza pembeni ya Geb. Akambusu begani. “Sawa. Nitatulia kabisa. Chukua hili faili. Pengine litakusaidia utakapoamua kutafuta ushahidi. Au mimi naweza kukusaidia.” “Nanaa!” “Basi Geb. Naachana kabisa na hayo mambo.” James akacheka taratibu. Nanaa akacheka na kuinama.

Geb alibaki akimtizama. “Kweli tena nimeacha Geb. Sasa hivi natulia na nyinyi tu. Sihangaiki tena. Ilimradi unihakikishie utakuja kunioa mimi hapa.” Watu wote wakacheka kidogo. “Hapo kafika huyo. Hata kaka yako alipopiga simu usiku ule ananiuliza sasa iweje akili ije imrudie Geb, ampigie simu amdai pesa yake! Halafu akukimbie hospitalini! Nikamuuliza James, huyo Geb akimbilie wapi? Nikamwambia Geb ndio kafika pale. Hajiwezi kwa lolote. Hata kama mama yake akirudi adai tena pesa nyingine, atamlipa tu.” “Mama wewe! Naomba temea mate chini, asirudi tena!” Nanaa alishituka sana. Wakacheka tena kidogo.

“Nimesema ukweli.” Mama G akasisitiza.  “Mungu asaidie asirudi tena. Sasa hivi mambo yake safi. Hata simu zangu hapokei tena. Wamepanga nyumba na amefungua baa.” “Kaka wewe!” Nanaa akashangaa sana. “Kweli tena. Anashida gani na pesa anayo. Ashakuuza wewe, sasa hivi ametulia tuli. Amemkimbia baba. Anaishi na wale wanae wakike.” Nanaa akasikitika sana. “Jamani!” “Lakini waache tu Nanaa. Mungu yupo.” Wakanyamaza kidogo. 

~~~~~~~~~~~~~

Nanaa akamgeukia Geb. “Asante mpenzi wangu kwa kunilipia garama zote hizo.” Geb akacheka. “Nakupenda Nanaa. Hakuna thamani inayoweza kulinganisha na yale unayonipa. Ona sasa hivi nilivyokumbatiwa hapa.” Wakamuona Liv ametulia kifuani kwa baba yake. Uso ameweka shingoni kwake. Ametulia kimya. Wakacheka.

“Hiyo furaha yake, huwezi kuipima kwa pesa. Hakuna kiasi cha pesa kinaweza kununua hii hali ninayo jisikia moyoni.” Nanaa akammchungulia Liv. Mwanae akajitoa pale kwa baba yake, akamwangalia na yeye. Akacheka kisha akajirudisha tena kwa baba yake. Geb alikuwa akimkuna mgongoni. Akamgeukia mwanae, akambusu tena. “Umeyabadilisha maisha yangu kabisa Nanaa. Unanipenda bila unafiki. Umenivumilia hata kipindi kile nipo na Liz!” Nanaa akainama.

“Unakumbuka kuna siku nilikwambia kwa mafumbo upendo huvumilia?” Nanaa akatingisha kichwa, huku akicheka. “Pale nilikuwa nikikusihi univumilie Nanaa. Ndio nilikuwa nakuomba usimkubali mtu mwingine, hata Jeff. Unisubiri niweke mambo yangu sawa.” Wakacheka.

“Nilielewa Geb.” “Haiwezekani Nanaa! Sasa wewe ulielewa nini wakati Liz aliendelea kuwa anakuja kulala pale pale ndani? Mimi nisingeweza.” Grace akauliza kwa mshangao. “Wakati mwingine nilikuwa naumia sana. Lakini muda mfupi niliokuwa nikiupata na Geb, ulikuwa unanifanya nipate moyo wakuendelea kumsubiria.” Wakacheka.

“Kweli. Tulikuwa tukipata muda mfupi mfupi. Lakini kwa namna fulani, nilianza kujisikia upendo wa Geb kwangu. Kuna jinsi alivyokuwa akiwa kwangu, hata nilikuwa nikimuona akiwa na Liz hawi hivyo.” “Sawa sawa Nanaa. Basi kweli kumbe ulikuwa ukimwangalia Geb. Mimi mwenyewe mpaka nikawa namwambia mama. Huyu Geb anakaribia kukamatwa na Liz. Alishindwa kabisa kuficha mapenzi yake kwako. Unajua hata siku ile Marangu Liz alipomuuliza Geb mbele za watu, nilimkonyeza Danny. Nikamwambia, leo bomu linapasuka. Lakini nikamuona amejikaza sana kutosema.” Grace akaongeza. 

“Aaaah! Ndio maana.” Nanaa akaanza kucheka. “Nini?” Grace akauliza. “Ujue Geb aliniambia hivi. Baada ya wote kurudi kutoka Marangu. Siku ile nilikuja kuchukua vitu vyangu ili nihamie kwa Antii. Geb akanikatalia nisihame. Tukabaki tukizungumza muda mrefu chumbani akinisihi nibaki. Sasa nikawa nipo kama nimechanganyikiwa tena. Maana ni kama nilimuacha amekumbatiana na Liz! Hata tumaini dogo nililokuwa nalo moyoni likawa limeisha kabisa. Nikaamua niondoke kabisa pale kwake.” “Na yeye Geb alijua.” Mama G akaongeza.

“Kweli mama?” Nanaa akauliza. “Kabisa. Alijua hutasamehe tena. Wala hutataka kumsubiria tena. Basi muda wote uliomuacha kule Marangu alishindwa kula wala kulala huyo.” Nanaa hakuamini. “Geb!?” Akauliza kwa mshangao sana. “Kumbe! Huyo huyo Geb. Hali ilikuwa mbaya sana. Heri usingeondoka.” “Basi mimi sikuwa hata najua. Niliondoka nikiwa nimekusudia kuanza upya. Niondoke. Nitulie na shule, basi. Nakumbuka akaingia pale chumbani kwangu, akaniambia hakuna mtu yeyote kati yetu. Si mimi, wala kaka, au Zinda na Liz, tuliokuwa tayari kwa ukweli. Ndio maana akaamua kunyamaza tu. Sasa mimi sikumuelewa. Nikamuuliza ni ukweli gani? Akasema kama nikiamua kubaki naye. Yaani nisihamie kwa Antii, niendelee kuishi pale kwake, nitajua tu.” “Na unavyopenda umbea wewe. Hapo ukahisi labda atakuja kukwambia wakati mwingine. Ukaona usipitwe.” “Kama ulikuwepo kwenye akili zangu mama. Nikasema labda atakuja kuniambia kesho au baada ya muda mfupi. Heri nibaki tu.” Wakacheka.

“Nanaa kwa kupenda stori! Lakini zitakusaidia kupata mume.” “Umeona sasa? Ningekimbia wakati ule nisingekuwa hapa.” Kila mtu akacheka. Lakini Nanaa akashangaa Danny amepooza kabisa. Akahisi kuna kinachoendelea.

          Wakazungumza mpaka James akaaga. “Sasa na huyo anywe uji ndio akalale.” Mama G akimaanisha Oliva. “Mpaka uje mtoe hapo shingoni kwa baba yake! Tena kwa kumpa uji! Labda tumwite Fili ampe pipi.” Nanaa akafanya kila mtu acheke. Fili alishaenda kulala. Baba yake alimpeleka ilipofika tu saa mbili. “Fili bwana! Sisi tunajua watoto wanampenda tu, kumbe anawapa sukari na pipi!” Grace akaongeza. Wakazidi kucheka. “Utamkuta ametulia nao kitandani wapo kimyaa. Tena huwa ananiambia, ‘usiwe na wasiwasi mama. Wewe nenda tu kaoge. Nitakaa na watoto.’ Basi nikawa najua nimekuza yaya wa Watoto! Kumbe mwenyewe ana njia zake!”  Wakacheka. “Lakini amekusogezea. Si hao sasa hivi wanakunywa uji? Watakuwa tu.” Mama G akampa moyo.

Nanaa aliona hali imebadilika. Mazungumzo hayakuwa kama kawaida. Kulikuwa na hali ya ukimya. Baada ya muda mfupi Danny akaaga, akaondoka. Wakati Grace anataka kuondoka, Geb akamuita. “Naomba tuzungumze kidogo.” Grace akamsogelea. “Vipi?” “Unafikiri unaweza kunivumilia nikaanza kazi jumatatu ijayo? Nataka nitoke na familia yangu kwa kama siku tatu hivi. Tutarudi jumapili mchana. Jumatatu nitakuwepo kazini. Halafu na wewe unaweza kuchukua hata siku mbili za mapumziko” “Unataka muondoke lini?” “Kesho asubuhi.” Geb akajibu. “Hamna shida. Wewe nenda kapumzike na familia yako. Mimi nitakuwepo.” “Nakushukuru sana.” Geb akamshukuru, Grace akaondoka.

Aluta Kontinua.

Ilikuwa siku ya jumatano asubuhi wakati Geb akiondoka na familia yake kuelekea mbuga za wanyama Mikumi, mjini Morogoro. Nanaa alikaa kiti cha nyuma na Oliva. Kwa kuwa walimsubiri mpaka saa tatu akawa hajaamka, ikabidi kumtoa tu kitandani akiwa bado na usingizi. Kwa hiyo baada ya kuogeshwa na kunyweshwa uji na bibi yake, alianza kusinzia. Geb alipomfunga tu kwenye kiti cha gari na kumpa busu, alitoa tabasamu la kichovu, na kupotelea usingizini. Nanaa aliendelea kuzungumza na Geb njiani huku Geb akiendesha.

Walifika Mikumi hoteli, wakachukua chumba. Geb akaanza kutengeneza kitanda cha Oliva walichokuwa wamekichukua nyumbani. Alikifungua na kurudishia kwenye boksi lake maalumu akakiweka nyuma ya gari mpaka hapo hotelini. Baada yakupata chumba na kuangalia sehemu nzuri ya kufunga kitanda hicho cha mtoto, ndipo Geb alipoanza kukirudisha kwenye muundo wa kulalika. Nanaa alikuwa akimlisha  Liv wakati Geb akifunga kitanda. 

“Geb!” Nanaa akaita. “Nimeona kuna tofauti kwa Danny. Kila kitu kipo sawa?” “Hapana.” Nanaa alipata jibu ambalo hakutegemea. Na Geb akajibu tu kwa kifupi, akaendelea na kazi. Nanaa akabaki ameduwaa. Akaendelea kumlisha mtoto wake. Akambadilisha nguo na diaper akabaki akicheza naye. 

          Geb akamaliza kila kitu, akaenda kukaa karibu yao. Liv akataka ambembe. “Nanaa, unajua nimekuja huku kwa kuwa nilitaka muda na nyinyi. Nataka tuwekane sawa. Tunaishi pale na watu wengi. Ni rahisi mahusiano yetu kumezwa na watu wanao tuzunguka. Mwishowe tukasahau nafasi zetu kwetu. Namaanisha ikawa rahisi kupoteza muelekeo. Kwa kifupi, nilitaka kukumbusha wewe ni nani pale ndani na kwenye maisha yangu.” Nanaa alikuwa akimsikiliza.

“Nahesabu ni baraka kuwa na wewe mpaka sasa hivi Nanaa. Sitaki mambo tutakayopambana nayo njiani, yakachukua kile kilichopo ndani yetu. Naamini bado unanipenda.” “Sana Geb! Wewe unajua kama nakupenda.” “Basi naomba siku ya leo iwe kwa ajili yangu na Liv tu. Naomba tuwe wote hapa. Akili zako, mawazo na kila kitu chako. Unakumbuka mapenzi tuliyofanya mara ya kwanza tulipokuwa wote huku Morogoro?” Nanaa akacheka kwa aibu. “Basi nakuomba tena. Nina hamu na wewe Nanaa.” “Hata mimi Geb. Nakuahidi nitatulia.” Geb akatabasamu na kumbusu. “Nakuahidi kesho tutapata muda mzuri wa mazungumzo. Nitakwambia kila kitu. Halafu tutajua kwa pamoja kitu cha kufanya.” “Sawa.” Wakahamia sakafuni kuanza kucheza na mtoto wao wakati Geb ameagiza chakula hapo chumbani.

~~~~~~~~~~~~~

 Mtoto alipolala tu, Nanaa akachangamkia kazi. Akaanza mabusu kwa Geb. Geb akacheka. “Nina hamu na wewe Nanaa! Nina kiu.” “Itaisha leo.” Nanaa akamnong’oneza masikioni. Geb akamnyanyua kutoka pale sakafuni na kumuweka kitandani. Akamfunua gauni yake akambusu tumboni. “Akiwa wa kiume, nitamuita Magesa Junior.” Mara zote Nanaa alikuwa akisahau kama ni mjamzito. 

“Akiwa wa kike je?” Nanaa akauliza huku akitoa tabasamu. Macho ya Geb yalikuwa tumboni kwa Nanaa. Akambusu tena na tena tumboni. “Oliva ulimlea ukiwa peke yako. Huyu nitamlea mimi. Zamu yangu.” Nanaa akacheka. Hakuwa amepewa jibu lake. Lakini akaamua kunyamaza. Alijua wazi Geb amesikia swali lake.

“Nataka unitajie kitu kimoja. Kikubwa unachotaka kutoka kwangu Nanaa. Nitakununulia. Chochote kile. Wala usiwe na wasiwasi juu ya pesa.” Nanaa akakaa. “Chochote kile?” Nanaa akauliza. “Chochote kile.” Nanaa akacheka huku akifikiria. “Kwanza niulize kwa nini?” “Kwa sababu nakupenda.” Nanaa akacheka sana. “Hiyo ndiyo sababu pekee?” “Huniamini?” Geb akauliza. “Nakuamini Geb. Ila najiuliza kwa nini sasa hivi?” Geb akakaa pembeni yake.

“Ngoja nikwambie kitu. Ulipokuwa hospitalini, ndipo nilipojua sina maisha mengine bila wewe Nanaa. Thamani yako kwangu iliongezeka mara zote pale nilipoona hatari ya kukupoteza. Nikajiambia Mungu akinipa nafasi ya kuja kuwa na wewe tena, nitakufanyia chochote utakacho. Lakini kiwe kikubwa kitakachonigarimu. Ili kila nikikumbuka, nikumbuke uthamani wako. Si kwa kuwa nitasahau, lakini..” “Unamaana zaidi ya milioni 50 ulizo nilipia!?” Geb akacheka.

          “Namaanisha kikubwa.” Nanaa akabaki ametoa macho. “Hivi unajua kitu ulichonipa kwenye maisha yangu? Au unajua kitu ambacho unaendelea kunipa kwenye maisha yangu ni cha thamani kuliko mtu anavyoweza kufikiria?” “Unamaanisha watoto!?” Nanaa akauliza. “Ulimpata Liv na kulea mimba kwa mateso ukiwa peke yako. Sasa hivi nafurahia mapenzi ya huyo mtoto. Hakuna jinsi naweza kukwambia furaha yake ukaelewa.” Nanaa hakuwa ameelewa.

“Jamani Geb! Mbona nimesikia watu wengi walikuwa wakitaka kuzaa na wewe!?” “Kwa kuwa walitaka kunitumia tu! Walitaka kwa faida zao wenyewe. Wengine walijua wakizaa na mimi watanufaika na pesa yangu. Wengine ni kwa mashindano ili kujivunia kuwa wamelala na mimi! Wengine walijua wakizaa na mimi watazaa watoto wenye akili kama zangu! Lakini sio wewe Nanaa.” Geb akawa kama amekumbuka kitu cha kumwambia.

“Unakumbuka zile siku ambazo tulikuwa hatupo kwenye maelewano? Kama ile siku ulikuwa umeniomba nikusindikize mahali. Ukajiandaa kabisa. Akaja Liz, nikaishia kutoka na Liz, nikakuacha wewe?” Nanaa akanyamaza.

~~~~~~~~~~~~~

 Alikumbuka jinsi alivyokuwa ameumia. Alitoka kwenye birthday aliyokuwa amealikwa na Zena kigamboni. Jeff akamtambia na mwanamke wake. Akaamua kurudi nyumbani. Akamkuta Geb akiwa anafanya kazi juani. Akamwokoa na ile hasira. Wakapata muda mfupi, mzuri. Wakakubaliana watoke. Lakini Geb akaishia kutoka na Liz badala yake yeye ambaye alikuwa ameshajiandaa. Nanaa aliumia sana, na kuamua kukaa mbali na Geb. Mpaka mama yake Geb alipombembelezea mwanae, ndipo Nanaa akamtumia ujumbe kwa mara ya kwanza, Geb akatulia.

~~~~~~~~~~~~~

“Nikiwa nimekuumiza, ulikuwa unaweza kuweka hisia zako pembeni na kunifikia mimi. Kutaka kujua ninaendeleaje! Kuhakikisha nipo sawa, ndipo mambo mengine yaendelee. Wakati wote unaniangalia mimi kama Geb. Uwe katika uzima au matatizo. Akili zako zipo kwangu mimi kama Geb. Umeweza kutenga hisia zako na mali zangu. Unanipenda mimi kama Geb. Sijawahi kufanya mapenzi na mwanamke mwingine kama ninavyofanya mapenzi na wewe Nanaa. Nikiwa nafanya mapenzi na wewe, moyo wangu, akili zangu na hisia vyote vinafunguka kwa kuwa najua nafanya mapenzi na mwanamke anaye nithamini. Hamu na wewe haijawahi kuisha. Ni vile tu kwa kuwa na mimi ni mwanadamu wa kawaida, nachoka.” Geb alikuwa akiongea naye taratibu na kwa hisia.

“Lakini Nanaa, kiu ya mapenzi kwako haijawahi isha. Nilikuwa nikikutamani wakati nikiwa na Liz. Niliacha kufanya naye mapenzi, nikijua wewe ndiye utakayeniridhisha. Nilijaribu baada ya wewe kuhamia pale nyumbani, lakini nilikuja kushindwa kabisa. Nilikuwa siwezi kulala na Liz, eti nikijua Nanaa yupo chumba kingine! Tena pale pale ndani! Nilishindwa kabisa.” Geb akacheka kidogo kama aliyekumbuka kitu.

“Kitendo cha kukufikiria unaweza kuja kuchoka kunisubiri. Ukaamua kuachana na mimi, ukawa na mwanaume mwingine. Akaona kwa macho kile nilichokuwa nikikitazama mimi na kukitamani. Nilikuwa siwezi kula Nanaa. Nikijua umetoka mle ndani eti mama aniambie au anitumie ujumbe kuwa Nanaa ametoka, kazi zilikuwa hazifanyiki!” Nanaa akacheka kidogo. “Nilikuwa ni kama nashindwa kufikiria. Kile kitendo cha mimi kumpigia mama simu, nimkute peke yake nyumbani wakati najua unatakiwa wewe uwepo nyumbani, halafu aniambie umetoka! Au  hata kama nakuwa nimetoka na Liz. Halafu labda nimtumie ujumbe nimuulize Nanaa anafanya nini sasa hivi, aniambie ametoka! Pengine kuna mtu ulienda kuonana naye, akili zilikuwa zinavurugika kabisa.” Nanaa akashangaa.

“Geb wewe! Yaani kumbe ulikuwa ukiniulizia hata ulipokuwa ukitoka na Liz!?” “Kabisa Nanaa. Nilikuwa nikiondoka lakini moyo wangu umejaa wasiwasi. Najiambia unaweza kupata mwanaume mwingine. Halafu mama naye alikuwa anakusifia huku akiniambia una bahati sana na wanaume wenye uwezo. Swali la wewe utanisubiria mpaka lini, lilikuwa likininyima usingizi na kushindwa hata kula.” “Basi mimi sikuwa na habari hata kidogo!” “Nilikuwa na wakati mgumu sana Nanaa. Unajua mpaka Grace akaniambia ni lazima niweke kikomo. Najiumiza mimi mwenyewe.” “Sasa Grace alijuaje!?” Nanaa akauliza akiwa na mshangao wa kilichokuwa kikiendelea bila ya yeye hata kuhisi kama anamtesa Geb aliyeonyesha maisha yake yanaendelea kama kawaida.

“Yeye alijua kinachoendelea kwa kuwa Liz alikuwa akimlalamikia. Halafu ujue Grace ni pacha ambaye ni kama hisia zetu zipo pamoja. Nikiwa kwenye mateso, na yeye anaumia sana. Anaumia sana Grace akijua kama sina raha. Nikiumwa ndio ujue na yeye ataumwa. Basi, alipoona vile ndio akaniambia yale sio maisha ninayotakiwa niendelee kuishi kwa muda mrefu.” “Sasa kwa nini ulikuwa ukiishi hivyo?” Nanaa akauliza taratibu tu.

“Unaona hiki kinachotokea sasa hivi na Zinda? Sikutaka wewe ndio utupiwe lawama. Mwanzoni sikutaka Liz ageuke kuwa adui yako. Nilitaka aje anichukie mimi mwenyewe. Nilitaka kukutoa kabisa kwenye lawama, ajue mimi ndiye niliyekutaka au kukuchagua. Sio aje akuzushie wewe.” “Asante Geb. Lakini sasa hivi imekuwa kinyume. Zinda anasema nimekupendea pesa.” “Sio kweli. Hata watu hawaamini hilo. Hata Liz hakulaumu wewe. Nilihakikisha anaelewa ni mimi ndiye nimekuchaguwa wewe.” Nanaa akabaki kimya.

“Niambie nini unataka Nanaa.” “Nataka niwe mkeo kihalali Geb. Nataka niitwe Nanaa Magesa. Kama mkeo sio heshima ya kuishi na wewe. Nataka uhangaike mpaka uhakikishe mimi ndio nasimama na wewe kanisani. Nataka uahidi mbele za watu na mimi mwenyewe kwamba mimi ndio nitakuwa mkeo mpaka kifo kitakapotutenganisha. Nataka hata iweje, nibakie kwako mimi peke yangu. Kwako wewe Geb. Hilo ndilo nataka kutoka kwako. Hiyo ndiyo garama nataka unilipie. Iwe katika shida na raha. Ukinipa hilo, ndio nitafurahi. Hakuna thamani ya mali itakayoweza kununua hiyo furaha yake. Nataka uwe wangu mimi Nanaa. Mimi peke yangu nisiwahi kukushiriki tena na mtu. Na watu wote wajue Geb ni wa Nanaa.” Hapo ndipo alipoanza kumng’ang’ania Nanaa. Alifanya naye mapenzi kana kwamba ndio wanaagana na hawataweza kuja kuwa tena pamoja hapa duniani.

          Kwa hakika siku hiyo ilikuwa ni yao tu. Nanaa na Geb waliweza kuridhishana kila walipokuwa wakifanya mapenzi. Oliva alipokuwa akiamka walipata muda wa pamoja naye wakicheza. Walitoka kidogo mida ya jioni kuzunguka hoteli hiyo ya Mikumi. Geb akiwa amembeba mtoto wake kwa mkono wa kushoto huku wa kulia akiwa amemshika Nanaa. Wakiongea na kucheka.

Alijitahidi kutuliza akili za Nanaa. Akirudia rudia umuhimu wake kwake na wanae. Vile anavyomuhitaji. Furaha aliyompatia kwa kumpa watoto. Tena mtoto kama Oliva mzuri na mwenye uwezo mkubwa wa kiakili. "Naami hata huyo anayekuja Mungu atamsaidia furaha kama Liv.” “Hujaniambia kama ni mtoto wa kike tutamuita nani!” Geb akamtekenya kidogo mwanae, wakacheka. “Eti Liv? Jina la kaka si liwe Magesa Jr? Utalipenda?” Nanaa akajua Geb anataka mtoto wa kiume. Akaingiwa na hofu. “Iweje nije kuzaa mtoto mwingine wa kike? Haya mapenzi na sifa zote si vitaisha?” Hofu akafanikiwa kuchukua furaha yote ya Nanaa. 

Kuanzia muda huo mpaka wanaingia kitandani kulala, Nanaa hakuwa akiongea sana. Geb alikuwa akicheza na Liv. Akajaribu kumlisha Liv chakula alichokuwa ametayarishiwa na bibi yake. Akala vizuri tu. Geb akampigia simu mama yake akijisifia kuwa ameweza kumlisha Liv kwa urahisi tu bila hata kupoteza muda mrefu akimbembeleza. “Nimezungumza naye tu. Mwanangu akakubali kukaa kwenye kiti chake, akawa anafungua mdomo. Amekula mpaka akashiba.” “Mmmh!” Mama yake akaguna. “Kweli mama.” “Ukute amekula vijiko vinne tu!” “Ngoja nikuchukulie video uone kibakuli chenyewe.” “Nataka kuona na tumbo lake. Msije mkamlaza na njaa!” “Sawa mama. Ila ujue mimi nimewashinda wote. Na mjue mwanangu anaelewa kila kitu. Ni kumwambia tu ale, anakula.” Nanaa akacheka.

“Unavyojisifia Geb wewe! Ngoja akubadilikie kesho. Mwanao hatabiriki huyo!” Nanaa akaongeza. “Bwana nyinyi hamjui kumlisha mwanangu. Mnamkaba badala ya kumkalisha tu kwenye kiti chake ale! Eti Liv wa Geb?” Geb akakata simu akaendelea na mwanae.

Alimsafisha na kumbadilisha nguo. Akamuweka kitandani kwake. Akaanza kumsomea kitabu mpaka Liv akalala. Nanaa alikuwa akimsikiliza wakati anamsomea. Kila mtu alijua Liv akisomewa kitabu na baba yake alikuwa akilala kwa haraka kuliko yeye mama mtu au bibi yake. Wakati wao wakimsomea alikuwa akichukua muda mrefu akicheka au hata kusimama. Mpaka watarudia mara mbili au tatu ndipo anaweza kulala lakini si baba yake. Wakati mwingine Geb anakuwa hata hajafika mwisho wa kitabu, Liv anakuwa alishapotelea usingizini. Akamsikia Geb akicheka peke yake. Akajua anamcheka mwanae. Akatoka. 

~~~~~~~~~~~~~

Nanaa alikuwa amejilaza kitandani, Geb alijua wazi amekosa raha. Akambusu tena na tena. Nanaa akarudisha busu kidogo, Geb akampa tabasamu. “Unakumbuka nilikwambia huwa napanga mambo yangu, halafu namwambia Mungu?” Geb akamuuliza Nanaa huku akimtizama vile alivyonyong’onyea pale kitandani. “Nakumbuka.” Nanaa akajibu taratibu tu akitaka kujua anapoelekea.

“Basi ni tabia niliyofundishwa na baba yangu. Aliniambia kamwe nisiwahi kuishi bila kujiwekea mipango. Kisha nimshirikishe Mungu. Basi ndivyo ninavyoishi. Kila kitu napanga, halafu huwa namwachia  Mungu. Ikitokea inaendana na mapenzi ya Mungu kwenye maisha yangu, basi huwa inatimia. Na ikitokea...” “Kwa hiyo ni kweli kama alivyosema Grace? Kuwa ulitaka mtoto wa kike ndio awe wa kwanza.” Nanaa akawa ameshamuelewa hata kabla hajamaliza.

Kabla hajajibiwa akaongeza swali jingine. “Lakini unataka awe wa kike mmoja tu?” Geb akajua ameshaingiwa hofu. “Kama nilivyokuwa nikisema. Nikiona havijatokea kama nilivyopanga, baba alinifundisha kushukuru kwa kuwa mipango ya Mungu kwa wanadamu ni bora kuliko yetu. Akanifundisha kupokea kila Mungu atakachonipa.” Nanaa akatulia.

“Nikweli nilimuomba Mungu kuwa mtoto wangu wa kwanza awe wa kike. Halafu wa pili ndio awe wa kiume. Akaja Liv. Nikajua mpango wangu uliendana na wa Mungu. Nilikuvizia siku za mtoto wa kike, na nikafanikiwa. Tangia umerudi, nilishindwa kuhesabu mzunguko wa hedhi yako. Nilikuwa siwezi kusubiri siku hata moja ya kutofanya mapenzi na wewe.” Nanaa akacheka na kujifunika uso. “Kwa hiyo huyo mtoto wa sasa hivi, ni yule Mungu atakaye nijalia. Hakuna juhudi zozote nimefanya kumpata wa kiume. Nitampokea vile atakavyonijalia Mungu. Wewe huusiki na jinsia ya mtoto yeyote utakaye zaa.” Kidogo Nanaa akatulia. “Niliogopa Geb!” “Nilijua. Nilikuona vile ulivyobadilika. Huna haja ya kuogopa. Akiwa wa kike, tutamtafutia jina utakalotaka wewe.” “Ndio maana nakupenda!” Wakajikuta wameangukia kwenye mapenzi tena.

Wakaendelea usiku huo, wakalala na kuamkia alhamisi. Siku hiyo na ijumaa wakatumia hapo hapo hotelini wakizunguka tu, kula na kucheza na mtoto wao huku wakizungumza mazungumzo yasiyoweza kuibua hisia za majonzi.

Jumamosi, Mjini Morogoro.

Waliamka siku ya jumamosi Geb alikuwa amelipia gari ya kuwapeleka mbuga za wanyama. Nanaa alikuwa akishangaa na kufurahia kila kitu. Kila wakati Geb alikuwa akiwapiga picha yeye na mwanae. Mwishowe yule aliyekuwa akiwazungusha mbugani akawasaidia kuwapiga picha kwa pamoja. Wakapata muda mzuri sana huko mbugani. Hasa Nanaa ambaye hakuwa akijua starehe. 

Kwa muda mfupi aliokuwa ameishi na mama G na Geb, alikuwa akinukia pesa. Kila kitu cha Nanaa kilikuwa kizuri. Alikuwa akienda kununua vitu na mama G mpenda vitu vizuri. Kwa hiyo hapo alipo alifanania na Oliva na utajiri wa Geb. “Anasinzia huyo!” Nanaa akamwangalia Oliva mikononi kwa baba yake. “Naona turudi tu hotelini. Hata hivyo ni kama tumeshaona wanyama wote.” “Nakushukuru Geb. Nimepata wakati mzuri sana.” Nanaa akatupia na busu la shukurani. “Nimefurahi kama umepafurahia. Nimefanya hivi makusudi kwa ajili yako.” “Najua Geb. Asante.” Wakarudi hotelini.

Mpaka wanatoka bafuni kuoga, tayari muhudumu akawa ameshaleta vyakula pale chumbani. Wakakuta vimeandaliwa vizuri hapo ndani. “Chumba chote kinanukia chakula!” Nanaa akasifia. “Husikii kichefuchefu?” “Hata kidogo. Ndio naona njaa inazidi kuuma.” “Vaa basi!” Geb alianza kucheka. Maana Nanaa alikaa pale pale na taulo lake na kuanza kula. “Acha kwanza nishibe bwana!” Geb akajua mimba ya safari hiyo haitamsumbua. Wakakaa na kuanza kula.

~~~~~~~~~~~~~

 “Mbona unaniangalia hivyo?” “Kuna kitu nataka kukwambia.” Nanaa akavuta tena bakuli la matunda, akajisogeza vizuri kwenye kochi akajiweka sawa. Akakumbuka Geb alimwambia hiyo ndiyo siku atamwambia ukweli wote. “Umeshiba kweli? Naona bado unajilamba vidole!” Geb akamuuliza. “Nahisi nina tatizo Geb. Nimeanza kutokushiba! Ile siku tunaondoka nyumbani, ile  asubuhi tulipokaa wote pale nyumbani na kupata kifungua kinywa, ujue mwenzio nilianzia kula jikoni! Nilikunywa uji wako pia. Supu ile aliyotengeneza mama. Chapati alizokuwa ameleta Danny jana yake usiku na yale mayai niliyokula pale mezani. Halafu si ulinisikia njiani nilivyokuwa nakula?” Geb akaanza kucheka.

“Usinicheke bwana! Sishibi hata! Yaani ninakula naona sishibi!” Nanaa akaendelea kulalamika. “Kumbuka unanyonyesha na una mtoto anayekutegemea tumboni.” “Unahisi ndio sababu?” Nanaa aliuliza huku akimalizia juisi ya matunda iliyobakia kwenye mabuli baada ya kumaliza matunda yote. Geb akazidi kucheka. “Tuagizie chakula kingine.” “Naona wazo zuri. Sijashiba hata! Na safari hii waambie walete chips za kutosha Geb. Wanapunja sana bwana!” “Nitaagiza sahani mbili. Unataka na nini?” “Ndio maana nakupenda. Sasa moja iwe chips na mayai. Wasiunguze wala kukausha. Waache mbichi kidogo.” Geb alikuwa akimtizama Nanaa na kucheka.

“Usinicheke bwana! Halafu sahani ya pili iwe chips na kuku. Walete na kachumbari yenye kila kitu walichonacho huko jikoni. Na waweke na limao. Sio jingi.” “Sasa kwa maelezo hayo. Nafikiri niende mimi mwenyewe kuzungumza na mpishi.” “Udumu Geb wangu. Lakini nahisi nitanenepa sana jamani! Utanichukia?” Geb akambusu. Alipotaka kumuachia. Nanaa akamng’ang’ania midomo yake.

“Kidogo tu, halafu ndio uende.” “Si umesema una njaa wewe? Ngoja nikalete kwanza chakula.” “Sio kuwa nina njaa! Ila sijashiba. Njoo kidogo bwana. Nina hamu na wewe Geb.” Geb hakujivunga. Akachangamkia penzi. Haikuwa kidogo kama alivyoomba Nanaa. Walihamia kitandani. Nanaa alinogewa hapo kitandani. Hakutaka Geb amwachie. “Ni busu tena.” Nanaa aliomba taratibu mara baada ya Geb kumalizia na yeye. Geb akambusu midomoni kwa muda mrefu kidogo, akamwachia. Nanaa akajivuta pembeni yake. Karibu kabisa na ubavuni kwake. “Usilale sasa!” “Nikumbatie kidogo tu.” Nanaa akajigeuza ukutani. Geb akasogea mpaka nyuma ya mgongo wake. Akambusu nyuma ya shingo.

“Nakupenda Nanaa.” “Nakupenda sana Geb. Namshukuru Mungu kuwa hapa na wewe. Nashukuru kwa wazo la kuja hapa. Najisikia vizuri. Sikujua kama nitafurahia hivi. Ni kweli sisi wote watatu, tulihitaji huu wakati. Asante mpenzi wangu.” “Asante kushukuru.” Geb akapitisha mkono juu ya kiuno chake. Kiganja kikatua tumboni. Akaanza kumpapasa taratibu, akamsikia Nanaa ameanza kukoroma taratibu. Akacheka. Akambusu tena mara kadhaa mgongoni. Akabaki akiwaza.

~~~~~~~~~~~~~

Nanaa alikuwa mwingi wa furaha. Kadhalika Oliva aliyekuwa akicheka kwa sauti huko mbuga za wanyama. Walipata wakati mzuri sana. Wakati wote Nanaa alikuwa akimgeukia Geb na kumnong’oneza neno, “Asante”. Akionyesha kufurahia kile Geb alichofanya. Alikuwa amebadilika usoni kwa furaha. Ni Nanaa aliyekuwa amedidimizwa na kutamkiwa ni mzigo. Leo Geb amempokea na kuongeza uthamani wake. Nanaa amekuwa gumzo kwenye jamii! Thamani imeongezwa, kila mtu anamtaka yeye! Mwenye kisu kikali ndio anakula nyama sasa hivi. Ni Nanaa Magesa.

Joto la mwili wake liliongezeka na kumfanya Geb kutaka kufanya naye mapenzi kila wakati. Hakutaka kubanduka hapo kwenye mwili wa Nanaa, ni vile Mungu alifupisha starehe hiyo, na huwa mwili unachoka, vinginevyo Geb angekesha. Hofu ya kutaka kumwambia kila kitu Nanaa ikaanza kumwingia. “Nisije kuharibu kila kitu!” Geb akawaza wakati Nanaa na mwanae wamelala bila hata habari, sababu ya uchovu wakuzunguka siku nzima mbugani.

Geb akambusu tena mgongoni huku na yeye amelala kwa ubavu ili kumkumbatia kwa urahisi Nanaa aliyekuwa na yeye amelala kwa ubavu. Akampapasa tena tumboni mara kadhaa. Hamu yakutaka kumuamsha apate starehe aliyopewa muda mfupi uliopita ikamjia kadiri alipokuwa akimpapasa Nanaa. “Usiku wa leo utakuwa mfupi. Na hivi amelala mchana!” Geb akawaza na kucheka. “Lakini nikimwambia. Anaweza kuumia sana.” Wazo jingine likapita. Likamtia hofu kuzungumza yote aliyotaka kuongea na Nanaa. “Lakini nilazima asikie kutoka kwangu. Si vinginevyo.” Geb akajirudi. Wakati anawaza, akapitiwa na usingizi pale pale kitandani alipokuwa amemkumbatia Nanaa.

~~~~~~~~~~~~~

          “Njaa inauma!” Geb akasikia Nanaa akiongea. Akahisi anaota. “Geb!” Nanaa akamtingisha kidogo. Akafungua macho. Akakuta giza limeingia mpaka chumbani. Taa ya nje kwenye balcony, ilikuwa ikimulika kitanda cha Oliva. Chumba hicho kilikuwa kimejazwa thamani za mbao na viti vizuri vya miti. Geb alichukua kama kinyumba kidogo, chenye chumba kikubwa kilichogawanywa mara mbili. Kulikuwa na vitanda viwili humo humo ndani na sehemu kubwa iliyotengenezwa kutoshea meza na viti vilivyokuwa vimesukwa kwa ustadi mzuri tu. Vyote vilipangiliwa kwenye hicho kinyumba kilichokuwa kimetengenishwa katika sehemu tatu ndani. Vyumba viwili na  sehemu ya kukaa. Walikuwa na Balcony/ baraza moja kwa nje.

Akamsikia Oliva akiongea kitandani kwake. “Ameamka huyo!” Geb aliongea akiwa anatoka usingizini. “Hajaamka muda mrefu. Pole nimekuamsha. Lakini njaa inauma.” “Twendeni basi wote tukale huko huko sehemu ya kulia chakula. Hata Liv nitaenda kumlishia huko huko.” Geb akatoka kitandani. Nanaa alioga hata dakika haikuisha. “Nanaa!” Geb akashangaa ametoka. “Njaa inauma bwana. Nitaoga vizuri nikirudi.” Geb akacheka tu. Na yeye akaingia bafuni kwa haraka akatoka. Alimkuta Nanaa alishavaa na amemtayarisha Liv. “Kweli una njaa!” “Nimeshawapigia simu. Nikawaambia oda yangu. Nataka nikifika tu, nikute chakula. Siwezi kusubiri tena.”  Akaenda kumpokea Oliva. Akachukua mfuko wake, wakatoka. Walimbebea cerelac ambayo ilikuwa niyakuchanganya tu na maji ya vuguvugu. 

Walipofika ni kweli hawakukaa muda mrefu, chakula cha Nanaa kikaletwa. Geb akaagiza maji ya moto na baridi. Alikuwa ameleta na kiti cha Oliva, maalumu cha kumlishia chakula. Akawa amemfunga hapo. Amemvalisha na aproni yake. Liv alikaa pale akijua chakula kinakuja. Alikuwa akimtizama baba yake vile anavyomchanganyia chakula chake. Kila Geb alipokuwa akimwangalia, Liv alimrudishia tabasamu. Nanaa alikuwa akiendelea kula kwa juhudi zote wakati Geb akimlisha mtoto huku anazungumza naye. 

Nanaa alikuwa akishangaa vile Oliva alivyokuwa akila bila shida. “Liv unamakusudi wewe! Unavyokula kwa bidii kama sio wewe!” “Hamjui kumlisha mwanangu. Mnampakata na kutaka kumkaba! Liv hapendi fujo mwanangu. Akikaa mwenyewe na kumlisha anakula vizuri tu. Mnatumia nguvu nyingi bila sababu! Mnaishia kumkera tu. Ndio maana hali.” “Ngoja niwachukue video nimtumie bibi yake aone ubaya wa mjukuu wake.” Nanaa akaanza kumchukua video. Liv akacheka. “Tabia mbaya hiyo Liv! Wala usinichekee.” Oliva alizidi kucheka. “Wala sio mazuri!” Geb alikuwa akicheka.

Alipokuwa akilishwa na bibi yake, wote waliishia kuchafuka. Oliva alikuwa akicheka wakati wote huku chakula kikitoka. Hakuwa akitaka kutafuna wala kumeza. Mama G akaona awe anamlisha kwa kumpakata. Oliva alikuwa akipaliwa nakuishia kutapika au kukohoa na kumlowesha uso mzima bibi yake. Walikuwa wakimlalamikia Geb kuwa mtoto wake anataka nyonyo tu, hataki kula. Lakini Geb alikuwa akiwabishia na kuwaambia jinsi wanavyomlisha Liv, ndio maana hali. Akamnunulia kiti na kuwaambia watumie njia ya kumuweka ale, napo haikusaidia. Sasa siku hiyo baba yake alimuweka kwenye kiti chake, akaamfunga vizuri na kumlisha bila shida. Tena Liv alikuwa akifungua mdomo yeye mwenyewe.

Walikuwa na wakati mzuri sana hapo sehemu ya kulia chakula. Walikuwa wakizungumza mambo yao na kucheka na mtoto wao huku Nanaa akiendelea kula. Walizungukwa na wazungu watupu hapo. Wao peke yao ndio walikuwa weusi kwenye eneo hilo la kulia chakula. Nanaa aliagizia chakula kingine tena, safari hii akawa anaendelea kula taratibu, Geb akijipanga kuzungumza la moyoni bila kutibua hali ya hewa.

Siri ya kwanza.

“Unajua Danny ni yatima?” Geb akaanza. “Najua. Alisema na yeye alilelewa kwenye nyumba ya mapadri. Ila sijui historia yake ni kwa nini ilikuwa hivyo! Na wazazi wake wako wapi!” Nanaa akajibu huku akiendelea kula, hana habari. “Wazazi wake wote walifariki. Lakini wote walikuwa wakifanya kazi hapo hapo kanisani. Alianza kufa baba yake wakati ndio Danny tu amezaliwa. Baada ya kama mwaka mmoja akafa mama yake pia. Lakini kwa kuwa wazazi wake walikuwa wakitumika hapo kanisani kwa muda mrefu, Danny alipoachwa peke yake, hao mapadri wakamlea Danny. Ni historia ndefu kidogo. Lakini ndio hivyo.” “Oooh!” Nanaa akaitikia bila kufikiria. Akaendelea kula.

“Alipofaulu sekondari kwenda Iliboru.” Geb akaendelea na kumfanya Nanaa amwangalie kwa makini. “Kwani kuna nini tena!?” Nanaa akawaza. “Kwa nini habari za Danny sasa hivi, katikati ya mapumziko yetu!?” Nanaa akaendelea kujiuliza wakati amenyanyua uso akimtizama Geb aliyeonekana anataka kuzungumza jambo muhimu.

“Ndipo tukakutana huko. Asilimia kubwa ya marafiki kwenye lile kundi tulikutana kidato cha kwanza kwenye sekondari ya Iliboru. Lakini kwenye kubic yetu, au chumba chetu tulikuwa tukilala wanne. Mimi, James, Danny na Zinda. Tulikuwa tukifuatana sisi wanne. Ndipo Malii na Goz wakajiunga. Marafiki wengine tulikutana nao kidato cha 5&6. Kundi likazidi kuongezeka. Wachache hasa wanawake wa lile kundi, tulikutana Chuo Kikuu Cha Mlimani.” Nanaa akabaki ametulia akimsikiliza, akitaka kujua mwisho wa yale mazungumzo katikati ya mapumziko yao, yataishia wapi.

“Zinda na Danny wakaanza urafiki uliowapelekea kuwa kama ndugu. Likizo nyingine kubwa, Danny alikwenda nyumbani kwa kina Zinda kwanza, ndipo kisha huko kwa hao mapadri, Iringa. James hakuwa akipoteza muda wowote ule. Shule zilipokuwa zikufungwa tu, alikimbilia nyumbani ili awe na wewe.” Nanaa akatabasamu.

Akachukua soda yake akanywa. Mara hiyo ya pili, Nanaa aliomba muhudumu amletee chips na yai. Lakini isikaushwe hata kidogo. Kwa hiyo hapo alikuwa akiendelea kula kwa kufurahia rojo rojo hilo. Alishamaliza sahani ya kwanza ya chips kuku, hiyo ilikuwa sahani ya pili aliyokuwa akila taratibu bila haraka. “Kwa hiyo kuanzia hapo, Danny akawa amepata sehemu mbili za kuishi. Nyumbani kwa kina Zinda Tabora na huko Iringa, nyumbani kwa wale mapadri waliokuwa wamemlea tokea mtoto.” “Kwa hiyo kabila la Danny ni muhehe?” Nanaa akauliza.

“Sina uhakika sana. Sikuwahi kudadisi hilo. Lakini ni kama wazazi wake walihamia hapo Iringa kutafuta maisha. Katika hangaika zao, wakajikuta wote wakifanya kazi kwenye nyumba hiyo ya mapadri. Mama yake alikuwa mpishi. Kama sijakosea. Baba yake alikuwa akifanya kazi za nje. Usafi, maua na kadhalika. Na nafikiri kama nakumbuka vizuri, mama yake Danny na yeye alikuwa yatima. Kwa hiyo alikulia maeneo hayohayo mpaka akaja kukutana na baba yake Danny. Alivyoambiwa Danny ni kwamba mama yake alishika mimba kabla ya ndoa. Ikamlazimu baba yake kutafuta chumba na kumchukua. Kumbe baba yake tayari alikuwa na maambukizi ya virusi vya ukwimwi. Akamuambuza mama yake. Yaani pale unapomuona Danny ni mtoto aliyezaliwa na wazazi waliokuwa wameathirika. Kwa kuwa mama yake alikuwa binti mwaminifu na alilelewa hapo hapo au kwenye mazingira ya namna hiyo, ikabidi Danny apitie kulelewa kwenye mazingira hayo hayo.” “Maskini Danny!” Nanaa akamuhurumia.

          “Ndio maana Danny hata mwanamke awe vipi, hawezi kumtaka kimapenzi. Sisi tulijua atakuja kuwa padre. Tulikuwa naye akiwa hana msichana. Mpaka alipokuja kukutana na Grace. Kila mtu alishangaa vile alivyochanganyikiwa. Hatukuamini kama ni Danny.” Nanaa akacheka. Akakumbuka historia ya Danny na Grace.

“Ndio maana anamchunga sana Grace!” Nanaa akaongeza huku anacheka. “Nafikiri. Anakumbuka kosa la baba yake. Hataki waje wawaache watoto wao. Wosia wake wakati wote kwa kila mtu ni kuwa makini. Muoga hata wakuweka pombe mdomoni. Anasema anaogopa kuweka kitu chochote mwilini mwake kitakachomfanya afanye kitu cha kuja kujutia baadaye.” Nanaa akacheka.

“Kwa hiyo Danny na Zinda, wakageuka kuwa ndugu. Nikisema ndugu namaanisha ni kama waliokuwa wametoka kwa baba na mama mmoja. Danny haitaji kualikwa nyumbani kwa kina Zinda. Anaweza kutoka Dar na kukimbilia Tabora japo kwa siku mbili tu, kuwaona wazazi wa Zinda. Haitaji kumtaarifu Zinda tatizo la nyumbani kwao ili asaidie. Anatuma pesa nyumbani kwa kina Zinda kila inapolazimu. Akisikia mama yake Zinda mgonjwa, atawasha gari na kukimbilia Tabora kumchukua yule mama na kumpeleka hospitalini. Awe na Zinda asiwe na Zinda, atafanya hivyo. Ndugu wa Zinda hawahitaji ruhusa ya Zinda kumuomba pesa Danny. Ni kaka yao. Kukiwa na  tatizo nyumbani kwao, wasipompata Zinda kwenye simu, basi Danny atapigiwa simu.”

“Mimi ndio nimeharibu mahusiano yao.” Nanaa akajilaumu. Asielewe historia hiyo nzima itakapoishia. “Wala si wewe Nanaa. Ni Zinda mwenyewe. Zinda alikuwa akijua kabisa ni kwa kiasi gani nakupenda. Zinda anafahamu. Sijui ni roho gani imemuingia na kumfanya awe hivyo alivyo. Na ametumia urafiki wake na Danny vibaya au niseme vizuri, ili kuniharibia mipango yangu.” Nanaa akatulia kidogo. Ni kama akatoka usingizini. Geb akajua ameanza kupata picha fulani.

“Kama ulivyokuwa ukiona jinsi Danny na Zinda wanavyoishi. Kufuatana kila mahali. Kuambiana kila kitu. Kwenye kundi zima wao ndio walikuwa karibu zaidi ya wengine.” Nanaa akaumia sana. Tayari akawa ameelewa kila kitu. Akainama. “Kama unavyonijua mimi si mzungumzaji sana. Lakini hawakuacha kunishirikisha katika mambo yao. Na japokuwa sikuwa kama wao, wacheshi na mambo mengine, lakini kwa kuwa wote walikulia pale nyumbani sababu ya Danny, tukajikuta kama ndugu. Hata mimi nisipokuwepo nyumbani, wao wanaweza kuja tu. Kama alivyosimulia Grace maisha waliyoishi wakati mimi nipo nchini India. Wote waligeuza nyumbani kwetu kama kwao.” Nanaa alibaki ameinama.

Geb akaendelea tu. Alikusudia afikishe ujumbe wake. “Mama na yeye ni yatima kama alivyokwambia. Alipojua historia ya Danny na mapenzi aliyokuwa nayo kwa Grace, akamfanya Danny kuwa kama mtoto wake. Anampenda sana Danny. Na kwa kuwa wote wamekutana wacheshi, basi wamekuwa karibu muda mwingi kuliko hata mimi.” Nanaa akazidi kuumia. Akahisi usaliti wa hali ya juu.

          “Kwa hiyo mama ndiye aliyemwambia mambo yote Danny, na Danny ndiye aliyemwambia Zinda?” Nanaa akauliza moja kwa moja na kumfanya Geb atulie kidogo. “Kwamba mama ametumia uaminifu wangu kwake, akatoa mambo ambayo nimemuamini nayo, akawa anamwambia Danny!?” Nanaa akatengeneza swali lake na kulifanya lisikike vibaya zaidi akionyesha maumivu ya usaliti.

“Haikuwa kama hivyo Nanaa. Unakumbuka siku niliyokufuata hotelini nikiwa na Liv, akilia sana, kipindi kile cha matatizo yetu?” Kimya. “Unakumbuka hata mama ulimwambia asimwambie mtu kama unamtoto?” Kimya. “Kwa hiyo hata Grace hakuwa akijua kama tuna mtoto. Alikuja siku ile ulipokuwa umechelewa kurudi nyumbani. Ukaenda kulala hotelini kwa kuwa nilikwambia ikifika saa 12 jioni usirudi tena nyumba. Grace na Danny walipokuja na kukutana na mtoto wasiyemjua. Anafanana na mimi. Mama hawamjui wala hakuwepo pale. Grace alichukia sana. Akajua moja kwa moja ni mtoto wangu mimi, halafu yeye akafichwa. Aliumia sana. Alianza kulalamika ni kwa nini mimi na mama tumeanza kumficha mambo! Ndipo mama ikabidi amuelezee kila kitu. Wakati akimuelezea alikuwepo

Danny na Fili pia.” “Lazima amtetee. Si ni mama yake?” Likapita wazo kichwani mwa Nanaa, likamchafua kabisa moyo wake.

Geb aliendelea kumuelezea lakini Nanaa alibaki ameinama. Akaanza kufikiria mambo yote aliyokuwa akimshirikisha mama G. Akagundua ndio maana Zinda amefanikiwa kutengeneza uongo unao fanana na kweli. Alijua amepata rafiki wa kweli, na siri zake zipo salama. Lakini akagundua amemuamini mtu ambaye anaye watu wake. Geb akaendelea kuongea.

“Kwa hiyo mambo yote anayozungumza Zinda sasa hivi, ameyatoa kwa Danny, na Danny ameyatoa kwa mama?” Nanaa akanyanyua uso na kuuliza wakati Geb akiendelea kuongea. Machozi yalishaanza kuchirizika kama mvua. “Usifikiri kwa hivyo Nanaa!” Nanaa akacheka kwa kuguna huku akifuta machozi. “Unajua nilimwamini sana mama! Nilikuwa nikimwambia kila kitu change! Nikajisikia nimejenga mahusiano mapya. Nikajiona ni kama nimepata sehemu yangu peke yangu. Kumbe nilikuwa najidanganya tu! Na sijui ni kwa nini nimekubali kujifanya mjinga wa kiasi hichi jamani! Nikasahau na kufumbia macho mahusiano niliyoyakuta kwenu! Mna umoja ambao mimi nitabakia mtu wa nje tu.”

“Sio kweli Nanaa.” “Ni kweli Geb. Hata kama utatetea familia yako. Mimi nitabakia mtu wa nje tu. Hata wewe unahaki ya kuwatetea. Mnamahusiano makubwa. Historia zenu zina mizizi. Mimi nimekuja kwenye maisha yenu hata miaka miwili sijamaliza. Kwanza nimekuja ni kama nimewatibulia mambo. Mimi nimekuwa mtu wa kuzungumziwa kati kati yenu. Habari zangu zinazungushwa vile mtakavyo kwa kuwa nimekuwa mgeni niliyeongezeka na matatizo yangu.” “Unakwenda mbali sana Nanaa.” Geb akashangaa vile Nanaa alivyochukulia lile jambo. Hakutegemea.

“Usingewatetea, hata mimi ningekushangaa Geb.” “Siwatetei Nanaa!” Hamu ya chakula ilishamuisha Nanaa. “Mama anakupenda sana.” Geb akaongeza. “Kiasi cha kutoweza kunifichia siri zangu? Kiasi cha kushindwa kunisitiri kama anavyomsitiri Grace au wewe? Ananipenda kiasi cha kunidanganya?” “Nanaa!” “Nini? Au mimi ndio nakosea sasa hivi? Ni juzi tu, nimemuuliza mama tena mbele yako na kaka kama ni yeye ndiye ametoa mambo yangu na kumpa Zinda. Akakataa mbele yako. Au umesahau?” Nanaa aliendelea kuongea taratibu huku akilia. Sauti yake ilijaa uchungu wa namna yake.

“Hakukudanganya Nanaa! Mama siye aliyetoa maneno na kuyapeleka kwa Zinda. Danny ndiye aliyetoa hayo maneno.” “Naomba mimi nikapumzike Geb.” “Tafadhali Nanaa!” “Nini Geb? Hakuna nitakachoongea hapa kikawa sawa na kile unachotaka nifikirie wewe juu ya familia yako. Naogopa hata kuendelea kuzungumzia juu ya hili jambo. Naomba yaishe.” “Yanaishaje Nanaa?” “Unataka kusikia nini Geb? Niambie kile unachotaka kusikia, ili nikirudie uelewe yameisha.” Hawakuwa wakiongea kwa sauti ya juu, lakini Geb hakupenda kumuona Oliva akimuona mama yake akilia. Alibaki ametulia kimya akimwangalia mama yake. Kicheko kikaisha kama anayeelewa. “Naomba twende chumbani Nanaa.” Nanaa akasimama. Akamchukua mwanae, akatangulia chumbani.

Geb alikusanya vitu vya mtoto wake, na kile kiti cha Liv, walichokuwa wamekuja nacho, kwa ajili ya kumlishia chakula, akawafuata chumbani. Nanaa akafungulia maji ya moto. Akatengeneza kwenye beseni la Liv kwa ajili ya kumuogeshea. Akamtoa nguo. Akaenda naye bafuni. “Nikusaidie?” Geb akamfuata bafuni. “Hapana. Asante.” Nanaa akaendelea kumuogesha mwanae. Kwa muonekano wa Liv, Geb akajua mwanae amehisi mama yake hakuwa na furaha. Oliva alikuwa ametulia akimwangalia mama yake muda wote. Hapakuwa na kucheka tena. Geb akajua amani imeshapotea.

Akamtoa mtoto wake kwenye maji, akarudi naye kitandani kwake kumvalisha nguo za kulalia. Akabaki amembeba kama ambaye hajui chakufanya. Geb akampokea mtoto. “Nanaa! Tafadhali naomba yaishe.” “Nimekwambia yameisha Geb. Au unataka kusikia nimeongea nini? Au hata nikisema hayajaisha, unafikiri ndio itakuaje sasa? Sina chakufanya. Nimeshajua nafasi yangu kwenye familia yenu. Basi, inatosha.” Geb akanyamaza kidogo akamgeukia Oliva. Akamuona ametulia kabisa, nay eye anamwangalia mama yake. Akambusu. “Nakupenda Liv!” Geb akamwambia mwanae lakini akapata tabasamu badala ya kicheko alichozoea. Mpaka Nanaa akashangaa. 

Geb akamuweka shingoni kama alivyozoea, lakini Liv akajitoa akamgeukia mama yake, akabaki akimwangalia. Nanaa alipomuona vile, akahisi kitu kimemkaba kooni. Akanyanyuka akatoka kwenda nje kwenye baraza. “Kwanza wameninunua kwa pesa nyingi sana. Sina chakufanya.” Nanaa aliwaza wakati amesimama pale nje peke yake, akiangalia asione chochote kwa mawazo. “Nilijua nimepata mtu wangu wa uhakika! Nilijua mama ndio atakuwa kama mama yangu! Lakini naona nimejidanganya. Hawa watu wana mahusiano yao ambayo hayawezi kuvunjika wala kuingiliwa. Mimi ni mgeni, na nitabakia kuwa mgeni tu. Kwanza ujio wangu kwenye maisha yao umesababisha kuvunjika kwa mahusiano yao.” Akaendelea kuwaza. “Nimebakiwa na kaka tu!” 

    Kila alipojitahidi kumuongelesha Oliva, alionekana akili na macho yake yapo kule alipoelekea mama yake. Alibaki akikodoa macho kama anayesubiri mama yake arudi. Geb akajua Nanaa analia huko nje. Hakutaka kumtoa mwanae pale. Akajua atazidi kumuhuzunisha mtoto wake. Akamuweka kitandani pamoja na michezo yake, yeye akatoka kule alipokuwa Nanaa.

Akaenda kusimama pembeni yake. Akajifuta machozi. “Nataka nikalale. Usiku mwema.” Nanaa akataka kuondoka. “Nanaa!” Nanaa akageuka. “Naomba tuzungumze.” Nanaa akageuka vizuri. Akacheka kwa masikitiko. “Unajua nilidhani safari ya kuja huku ilikuwa kwa ajili yakutaka muda na mimi, kumbe umegaramia pesa zote hizi ili kuja kuwatetea ndugu zako!” “Sio kweli Nanaa. Naomba hasira zisikufanye hivyo.” Nanaa akaingia ndani, akabadili nguo. Akapanda kitandani akalala. 

Habari nyingi za kukatisha tamaa na kuharibu moyo wa Nanaa ziliendelea kupita akilini mwake na KUHARIBU THAMANI NA GARAMA NZIMA ALIYOLIPIWA KUANZIA NA GEB mwenyewe, Mama G kusafiri mbali akipambana mpaka kumlipia mahari, na kumalizana na mama James tena kanisani. Lile jambo likakuzwa nafsi mwake na kusahau kabisa na yale aliyotendewa na Mungu. Moyo wake ukaumia kupita kawaida, akasahau yote kwa hilo kosa lililomkumbusha makuzi yake ya uchungu.

~~~~~~~~~~~~~

Maisha Hayatakosa Sababu ya Kukuyumbisha.

Kutoka kwenye mikakati ya kutulia, macho kwa familia tu, wapenzi hawa waliokuwa na wakati mzuri sana mpaka kushuhudia Ukuu wa Mungu, leo imetokea sababu nzuri inayoungana mkono na hasira ya kuvunjika kwa amani.

Usikose Muendelezo.

Maji yametibuka..

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment