Akapata. “Hii hapa.” Akamuonyesha. “Ni muongo
jamani huyu kaka!” Nanaa akaangalia ile picha. “Hiki si cheti cha Kenya!?”
“Anasema mlisafiri mpaka Kenya.” James akajibu.
“Muongo kabisa huyu kaka! Huko Kenya mimi
hata sijui kunafananaje! Tena kipindi hiki ndio nilikuwa nikisumbuliwa sana na
kizunguzungu. Nakumbuka ni mwezi huu huu wa kumi ndio kizunguzungu kilinitesa
sana. Nitaenda kuangalia tarehe kwenye mfuko niliokuwa nikiweka vitu vya
hospitalini kipindi mjamzito wa Oliva. Nilikuwa na File maalumu la hospitalini.
Nilikuwa nikiweka kila kitu humo ndani mpaka risiti kama nilinunua dawa au
nililipia kumuona daktari. Nitaangalia kuthibitisha.”
“Nakumbuka kuna weekend moja
ilinilazimu kurudi kumuona daktari sababu nilianguka nikiwa peke yangu kwenye
ngazi, sababu ya kizunguzungu. Nilipoamka tu, nikampigia simu daktari
nikamuomba anione.” Nanaa akaendelea kukumbuka.
“Sasa kwa kuwa yule daktari nilishampa historia
yangu na nikamsihi anisaidie kwa karibu sana ili nisije kufa nikamuacha Oliva
peke yake, basi alikuwa akinisaidia sana. Muda na wakati wowote nilikuwa
nikimpigia simu, anapokea. Ilikuwa siku ya jumamosi. Nakumbuka nilipanda
daladala akaniambia nimfuate alipo. Alikuwa yupo hospitali ya Tumaini.
Nikamwambia nilianguka sababu ya kuona giza. Akaniambia nipime damu. Ndio
akagundua sina damu kabisa. Akataka kunilaza ili niwekewe damu. Ndio
nikamwambia siwezi kulazwa. Kwanza nilikuwa sina pesa. Akasema atanisaidia
lakini lazima niwekewe damu.” Nanaa akaendelea.
“Nikamwambia pia sina mtu wakuanza kuniuguza pale
hospitalini. Maana nilijua yupo busy sana. Asingeweza kuniuguza.
Halafu nikamwambia nipo chuo. Nina mitihani mingi sana, siwezi kulazwa. Baada
ya kumkatalia swala la kulazwa, ndio akaniandikia vidonge, na kuniambia lazima
nipate muda wa kupumzika. Nile vyakula vya kuongeza damu, halafu nirudi kumuona
ili kujua kama damu imeongezeka. Kwa hiyo Zinda ni muongo. Ngoja
nikuletee uthibitisho kaka. Nilitunza kila kitu.” Nanaa akasimama.
Akaelekea stoo alipokuwa amehifadhiwa vitu vyake
vyote vya chuoni. Akaanza kupekua humo ndani. Pale sebuleni palikuwa pamezuka
ukimya mkubwa sana. Nanaa alikuwa akimtaka kumjua mtoa siri zake. Geb
naye akaongezewa mawazo. Akaumizwa kujua Nanaa alikuwa na matatizo ya afya
kipindi mjamzito wa kuyo mtoto aliyezoea kucheza kifuani kwake.
“Faili lenyewe hili hapa kaka.” Nanaa akarudi na
faili kubwa. Macho yake yalikuwa yakisaidia kutafuta. “Amesema tulifunga ndoa
tarehe ngapi?” Nanaa akauliza tena. James akamtajia. “Tena kila kitu
nimekipanga kwa tarehe!” Nanaa akakaa chini huku akitafuta hiyo tarehe.
Akakutana na picha za Ultrasound. Akacheka. “Unataka nikuonyeshe picha
za Oliva wakati yupo tumboni?” Akamuuliza kaka yake. James akacheka. “Hembu
tumuone.” Nanaa akampa kaka yake.
“Na mimi naomba kuona, Nanaa.” Geb akasimama.
Akamsogelea James. James akaangalia, akamkabidhi Geb. Geb akacheka. “Nilikuwa nafurahi
kweli nilivyokuwa nikionyeshwa kwenye machine!” “Nashukuru umezitunza Nanaa.
Ukumbusho mzuri sana.” “Kweli Geb? Maana mimi nilikuwa naweka tu.” “Muhimu
sana. Asante.” Nanaa akamtizama Geb, akacheka.
Akaenda kukaa pembeni yake. “Pole kwa matatizo
yote yaliyokuwa yakikupata peke yako wakati ulipokuwa mjamzito.” Nanaa akacheka
kidogo. “Asante Geb. Namshukuru Mungu kuniwezesha.” Wakataka kupena mabusu,
Nanaa akakumbuka kitu.
“Subiri kwanza kaka. Sasa kama Zinda anasema
alinioa, aliwezaje kuishi na mimi nikiwa na mimba ya Oliva!?” “Anasema
ulimwambia, akakukubalia kuwa atamtunza mtoto.” “Zinda ni mwendawazimu!
Sasa anasema baada ya ndoa ikawaje?” Nanaa aliendelea kuhoji. “Anasema mlienda
kuishi naye.” Nanaa akaanza kucheka.
“Sasa kama nilikuwa nikiishi naye, iweje leo niwe
hapa?” “Anasema ulipokaribia mitihani yeye akiwa nje ya nchi kikazi,
ilikulazimu uhamie hosteli. Ndipo ukajifungua. Ulipojifungua, Geb akajua una
mtoto wake, akaja kukupokonya mtoto. Wewe ndio ukamfuata. Ndio Geb
akakufungia. Ukamwambia..” Nanaa akakunja uso.
“Subiri kwanza kaka. Zinda anaonekana anaongea uongo
unao sindikizwa na ukweli! Hayo mambo ni nani amemwambia!?
Maana hata wewe hukuwa ukijua! Hayo mambo yalitokea kati yangu mimi, mama na
Geb tu. Hakuna mtu mwingine alijua! Ni mambo ya ndani sana. Nani atakuwa
anaongea mambo mazito hivyo, tena ya ndani sana, kwa watu wa
nje!?” Kimya. Nanaa akashangaa watu wote wameinama.
“Naomba nikuombe kitu kaka. Nimekuwa na maswali
ambayo hakuna mtu anayenipa majibu. Kuanzia mtu aliyetaka kuniangamiza,
mpaka mtu anayetoa maneno humu ndani. Hiyo ni tabia mbaya sana.
Kuna mambo ambayo huwa yakitokea, hayafai hata kuja kuzungumzwa tena! Lazima
nijue. Nijue nani anataka kuniangamiza. Na kwa nini! Nani anatoa maneno
humu ndani. Na anayapataje! Maana humu ndani watu wanaokuja ni watu wa
kusafisha. Na wanakuja mara mbili kwa week tu. Na mara nyingi wakija
huwa tunawapisha. Sasa nani anakuwa anatusikiliza? Jibu atakuwa nalo Zinda.
Naomba unisindikize kuzungumza na Zinda. Nitamuomba tuonane naye.
Akikataa nitamfuata hata kwake.” “Akikushitaki?” “Mimi si ni mkewe?” James
akacheka.
“Si ndio vyeti vinavyosema? Sasa nataka
nikazungumze naye. Si ni sawa Geb?” Geb akabaki akimwangalia. Nanaa akajua wazi
huko ndiko kukataliwa. “Naomba usikatae Geb, tafadhali. Zinda hawezi
kuwa sababu ya mimi kutokuolewa na wewe. Au umebadili mawazo.” “Hapana
Nanaa. Unajua jinsi ninavyokupenda. Natamani hata kesho nikuoe.” Nanaa
akacheka.
“Basi sasa kwa nini huniungi mkono katika
swala la kutafuta suluhisho? Au umekata tamaa?” Nanaa aliendelea kumuhoji Geb
taratibu. “Sijakata tamaa Nanaa. Lakini unakumbuka ulimuuliza hata malaika ni nani
amekuweka zile pini, lakini hakukwambia?” “Kwa sababu alikuwa akinielekeza kila
kitu kwako Geb! Mungu anataka wewe ndio uhusike na mimi si vinginevyo.”
“Hudhani kwamba pengine anakulinda? Labda
anadhani haupo tayari na ukweli.” “Sidhani Geb. Mungu amekuamini na
maisha yangu. Anajua wewe utaniongoza vizuri. Ndio maana anataka kila
kitu kizuri, kianzie kwako.” “Una uhakika?” Nanaa akacheka. “Kabisa. Sasa
unafikiri ni kwa nini alitaka wewe ndio uwe chanzo cha uponyaji wangu? Mungu anakuamini
na maisha yangu Geb.” Geb akamtizama.
“Mbona
kama huamini!?” Nanaa akauliza. “Hilo naliamini. Lakini je wewe
unaniamini?” “Nakuamini sana Geb!” “Una uhakika?” “Zaidi ya asilimia 100, Geb.
Mungu amekutumia sana kwenye maisha yangu. Na nimetumia Imani yako kama
ulivyoniambia pale hospitalini nikiwa nimekata tama, nikiwa hata simwamini
Mungu. Lakini nikakuamini wewe, umenisaidia nimerudi kwa Liv. Nakuamini SANA.”
Nanaa asijue anajifunga mwenyewe.
“Basi naomba tulia kwanza kwa sasa hivi.
Acha tutafute njia nyingine yakumaliza hayo matatizo na kufunga ndoa
yetu. Ukitafuta nani amefanya nini sasa hivi, haitasaidia. Utapoteza muelekeo
mzima wa kwa nini upo hapa leo.” Nanaa akatulia kidogo. Hakutegemea jibu la
namna ile kutoka kwa Geb.
Akamgeukia vizuri Geb, akamtizama. “Wewe
unafahamu ni nani amefanya hayo yote?” Lilikuwa swali la moja kwa moja
lililozua ukimya wa gafla. “Geb?” Nanaa akaita kwa upole. “Ndiyo nafahamu.” Geb
akajibu. Wakabaki wakiangaliana. Nanaa akakunja uso, akainama. “Nanaa! Naomba
nipe muda. Nipo kwenye maombi. Namuomba Mungu atusaidie hekima juu ya hili.” “Sasa unajuaje labda kwenda kwangu kwa Zinda ndio msaada
wetu?” Nanaa akauliza huku akifuta machozi.
“Umesikia habari nzima juu ya Zinda. Amekusudia kutukomoa,
Nanaa. Amekwenda umbali mkubwa sana kutengeneza uthibitisho utakaozuia
nisikuoe. Amekusudia. Lazima kuwa makini kwa kila tunachotaka kufanya. Najua
sasa hivi anategemea sisi tufanye mambo fulani fulani kujibu mashambulizi
yake. Na kwa kahika amejipanga. Tena amejipanga vizuri tu. Naomba tupate
muda wa kumsikiliza Mungu. Tujue anataka atusaidiaje katika hili.” Geb
alimvuta mkono.
“Wewe si unasema unaniamini?” Geb akamuuliza.
Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Lakini nataka
kujua. Geb.” “Nafahamu. Basi naomba nipe muda. Sawa?” Nanaa akanyamaza.
“Nanaa?” “Huniamini Geb!” “Nakuamini sana
Nanaa. Lakini naomba tupate muda na Mungu kwanza. Tukikubali kuwa wepesi
wakusikia au kusikiliza kila mtu, nakuhakikishia anguko letu halitakuwa
mbali. Tutaanguka na kutengana kwa haraka sana.”
“Zinda sio adui yetu wa kwanza. Anatumiwa
na shetani. Na usifikiri atakuwa mtu wa mwisho kumtuma kwetu kutuchafua.
Bado tutakutana na makwazo mengi na watu wa aina ya Zinda ni wengi tu. Tukiwa
watu wa haraka kujibu kila mashambulizi, hatutafika mbali.
Umemuona Mungu alivyotutoa kwenye mtego mkubwa sana wa shetani. Amepigana vita
vikubwa sana kwa niaba yetu.” Geb akaendelea.
“Hatuwezi kitu bila msaada wa Mungu. Hatutafika
mbali. Nahitaji muda wetu sisi na Mungu kwanza. Kumbuka kwa nini Mungu ametutoa
hospitalini. Kumbuka kilio chako. Naomba usipoteze muelekeo.
Tafadhali Nanaa.” “Nitasubiri Geb.” Nanaa
akajifuta machozi. “Asante. Nakuahidi kwa wakati unaofaa, nitakwambia kila
kitu. Lakini sio sasa hivi. Mungu ametupa nafasi yakuwa pamoja. Hata masaa 24
hayajaisha tokea upokee uponyaji tuliokuwa tukililia kwa ajili yako mwenyewe na
familia yetu. Naomba urudishe mawazo kwa mtoto aliyekuwepo tumboni na sisi.”
Nanaa akajishika tumbo.
Akamuona anatabasamu. “Halafu kila saa nasahau
hata kama ni mjamzito!” “Kwa kuwa akili yako ina mambo mengi. Naomba
urudishe mawazo humu ndani. Halafu mambo mengine niachie mimi. Sawa?”
Geb alikuwa akizungumza naye taratibu tu. Kila mtu akiwasikiliza. Nanaa akavuta
pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu huku akijirudisha nyuma. Akajiegemeza
pembeni ya Geb. Akambusu begani. “Sawa. Nitatulia kabisa. Chukua hili
faili. Pengine litakusaidia utakapoamua kutafuta ushahidi. Au mimi naweza
kukusaidia.” “Nanaa!” “Basi Geb. Naachana kabisa na hayo mambo.” James
akacheka taratibu. Nanaa akacheka na kuinama.
Geb alibaki akimtizama. “Kweli tena nimeacha Geb.
Sasa hivi natulia na nyinyi tu. Sihangaiki tena. Ilimradi unihakikishie
utakuja kunioa mimi hapa.” Watu wote wakacheka kidogo. “Hapo kafika huyo. Hata
kaka yako alipopiga simu usiku ule ananiuliza sasa iweje akili ije imrudie Geb,
ampigie simu amdai pesa yake! Halafu akukimbie hospitalini!
Nikamuuliza James, huyo Geb akimbilie wapi? Nikamwambia Geb ndio kafika pale.
Hajiwezi kwa lolote. Hata kama mama yake akirudi adai tena pesa nyingine,
atamlipa tu.” “Mama wewe! Naomba temea mate chini, asirudi tena!” Nanaa
alishituka sana. Wakacheka tena kidogo.
“Nimesema ukweli.” Mama G akasisitiza. “Mungu asaidie asirudi tena. Sasa hivi mambo
yake safi. Hata simu zangu hapokei tena. Wamepanga nyumba na amefungua baa.”
“Kaka wewe!” Nanaa akashangaa sana. “Kweli tena. Anashida gani na pesa anayo.
Ashakuuza wewe, sasa hivi ametulia tuli. Amemkimbia baba. Anaishi na
wale wanae wakike.” Nanaa akasikitika sana. “Jamani!” “Lakini waache tu Nanaa.
Mungu yupo.” Wakanyamaza kidogo.
~~~~~~~~~~~~~
Nanaa akamgeukia Geb.
“Asante mpenzi wangu kwa kunilipia garama zote hizo.” Geb akacheka. “Nakupenda
Nanaa. Hakuna thamani inayoweza kulinganisha na yale unayonipa. Ona sasa
hivi nilivyokumbatiwa hapa.” Wakamuona Liv ametulia kifuani kwa baba
yake. Uso ameweka shingoni kwake. Ametulia kimya. Wakacheka.
“Hiyo furaha yake, huwezi kuipima kwa pesa.
Hakuna kiasi cha pesa kinaweza kununua hii hali ninayo jisikia moyoni.” Nanaa
akammchungulia Liv. Mwanae akajitoa pale kwa baba yake, akamwangalia na yeye.
Akacheka kisha akajirudisha tena kwa baba yake. Geb alikuwa akimkuna mgongoni.
Akamgeukia mwanae, akambusu tena. “Umeyabadilisha maisha yangu kabisa Nanaa. Unanipenda
bila unafiki. Umenivumilia hata kipindi kile nipo na Liz!” Nanaa
akainama.
“Unakumbuka kuna siku nilikwambia kwa mafumbo kuwa
upendo huvumilia?” Nanaa akatingisha kichwa, huku akicheka. “Pale
nilikuwa nikikusihi univumilie Nanaa. Ndio nilikuwa nakuomba usimkubali
mtu mwingine, hata Jeff. Unisubiri niweke mambo yangu sawa.” Wakacheka.
“Nilielewa Geb.” “Haiwezekani Nanaa! Sasa
wewe ulielewa nini wakati Liz aliendelea kuwa anakuja kulala pale pale ndani?
Mimi nisingeweza.” Grace akauliza kwa mshangao. “Wakati mwingine
nilikuwa naumia sana. Lakini muda mfupi niliokuwa nikiupata na Geb,
ulikuwa unanifanya nipate moyo wakuendelea kumsubiria.” Wakacheka.
“Kweli! Tulikuwa tukipata muda mfupi mfupi.
Lakini kwa namna fulani, nilianza kujisikia upendo wa Geb kwangu. Kuna jinsi
alivyokuwa akiwa kwangu, hata nilikuwa nikimuona akiwa na Liz hawi
hivyo.” “Sawa sawa Nanaa. Basi kweli kumbe ulikuwa ukimwangalia Geb. Mimi
mwenyewe mpaka nikawa namwambia mama. Huyu Geb anakaribia kukamatwa na
Liz. Alishindwa kabisa kuficha mapenzi yake kwako. Unajua hata siku ile
Marangu Liz alipomuuliza Geb mbele za watu, nilimkonyeza Danny. Nikamwambia,
leo bomu linapasuka. Lakini nikamuona amejikaza sana kutosema.”
Grace akaongeza.
“Aaaah! Ndio maana.” Nanaa akaanza kucheka.
“Nini?” Grace akauliza. “Ujue Geb aliniambia hivi. Baada ya wote kurudi kutoka
Marangu. Siku ile nilikuja kuchukua vitu vyangu ili nihamie kwa Antii. Geb
akanikatalia nisihame. Tukabaki tukizungumza muda mrefu chumbani akinisihi
nibaki. Sasa nikawa nipo kama nimechanganyikiwa tena. Maana ni kama nilimuacha
amekumbatiana na Liz! Hata tumaini dogo nililokuwa nalo moyoni likawa limeisha
kabisa. Nikaamua niondoke kabisa pale kwake.” “Na yeye Geb alijua.” Mama G
akaongeza.
“Kweli mama?” Nanaa akauliza. “Kabisa. Alijua hutasamehe
tena. Wala hutataka kumsubiria tena. Basi muda wote uliomuacha kule
Marangu alishindwa kula wala kulala huyo.” Nanaa hakuamini. “Geb!?” Akauliza
kwa mshangao sana. “Kumbe! Huyo huyo Geb. Hali ilikuwa mbaya sana. Heri
usingeondoka.” “Basi mimi sikuwa hata najua. Niliondoka nikiwa nimekusudia
kuanza upya. Niondoke. Nitulie na shule, basi. Nakumbuka akaingia pale chumbani
kwangu, akaniambia hakuna mtu yeyote kati yetu. Si mimi, wala kaka, au Zinda na
Liz, tuliokuwa tayari kwa ukweli. Ndio maana akaamua kunyamaza tu.”
“Sasa mimi sikumuelewa. Nikamuuliza ni ukweli
gani? Akasema kama nikiamua kubaki naye. Yaani nisihamie kwa
Antii, niendelee kuishi pale kwake, nitajua tu.” “Na unavyopenda umbea
wewe! Hapo ukahisi labda atakuja kukwambia wakati mwingine. Ukaona usipitwe!”
“Kama ulikuwepo kwenye akili zangu mama! Nikasema labda atakuja kuniambia kesho
au baada ya muda mfupi. Heri nibaki tu.” Wakacheka.
“Nanaa kwa kupenda stori! Lakini zitakusaidia
kupata mume.” “Umeona sasa? Ningekimbia wakati ule nisingekuwa hapa.” Kila mtu
akacheka. Lakini Nanaa akashangaa Danny amepooza kabisa. Akahisi kuna
kinachoendelea.
Wakazungumza
mpaka James akaaga. “Sasa na huyo anywe uji ndio akalale.” Mama G akimaanisha
Oliva. “Mpaka uje mtoe hapo shingoni kwa baba yake! Tena kwa kumpa uji! Labda
tumwite Fili ampe pipi.” Nanaa akafanya kila mtu acheke. Fili alishaenda
kulala. Baba yake alimpeleka ilipofika tu saa mbili.
“Fili bwana! Sisi tunajua watoto wanampenda tu,
kumbe anawapa sukari na pipi!” Grace akaongeza. Wakazidi kucheka. “Utamkuta
ametulia nao kitandani wapo kimyaa. Tena huwa ananiambia, ‘usiwe na wasiwasi mama. Wewe nenda tu kaoge. Nitakaa na watoto.’
Basi nikawa najua nimekuza yaya wa Watoto! Kumbe mwenyewe ana
njia zake!” Wakacheka. “Lakini
amekusogezea. Si hao sasa hivi wanakunywa uji? Watakuwa tu.” Mama G akampa
moyo.
Nanaa aliona hali imebadilika. Mazungumzo
hayakuwa kama kawaida. Kulikuwa na hali ya ukimya. Baada ya muda mfupi Danny
akaaga, akaondoka. Wakati Grace anataka kuondoka, Geb akamuita. “Naomba
tuzungumze kidogo.” Grace akamsogelea. “Vipi?” “Unafikiri unaweza kunivumilia
nikaanza kazi jumatatu ijayo? Nataka nitoke na familia yangu kwa kama siku tatu
hivi. Tutarudi jumapili mchana. Jumatatu nitakuwepo kazini. Halafu na wewe
unaweza kuchukua hata siku mbili za mapumziko” “Unataka muondoke lini?” “Kesho
asubuhi.” Geb akajibu. “Hamna shida. Wewe nenda kapumzike na familia yako. Mimi
nitakuwepo.” “Nakushukuru sana.” Geb akamshukuru, Grace akaondoka.
Aluta Kontinua.
Ilikuwa siku ya jumatano
asubuhi wakati Geb akiondoka na familia yake kuelekea mbuga za wanyama Mikumi,
mjini Morogoro. Nanaa alikaa kiti cha nyuma na Oliva. Kwa kuwa walimsubiri
mpaka saa tatu akawa hajaamka, ikabidi kumtoa tu kitandani akiwa bado na usingizi.
Kwa hiyo baada ya kuogeshwa na kunyweshwa uji na bibi yake, alianza kusinzia.
Geb alipomfunga tu kwenye kiti cha gari na kumpa busu, alitoa tabasamu la
kichovu, na kupotelea usingizini. Nanaa aliendelea kuzungumza na Geb njiani
huku Geb akiendesha.
Walifika Mikumi hoteli,
wakachukua chumba. Geb akaanza kutengeneza kitanda cha Oliva walichokuwa
wamekichukua nyumbani. Alikifungua na kurudishia kwenye boksi lake maalumu
akakiweka nyuma ya gari mpaka hapo hotelini. Baada yakupata chumba na kuangalia
sehemu nzuri ya kufunga kitanda hicho cha mtoto, ndipo Geb alipoanza
kukirudisha kwenye muundo wa kulalika. Nanaa alikuwa akimlisha Liv wakati Geb akifunga kitanda.
“Geb!” Nanaa akaita.
“Nimeona kuna tofauti kwa Danny. Kila kitu kipo sawa?” “Hapana.” Nanaa alipata
jibu ambalo hakutegemea. Na Geb akajibu tu kwa kifupi, akaendelea na kazi.
Nanaa akabaki ameduwaa. Akaendelea kumlisha mtoto wake. Akambadilisha nguo na diaper
akabaki akicheza naye.
Geb
akamaliza kila kitu, akaenda kukaa karibu yao. Liv akataka ambembe. “Nanaa,
unajua nimekuja huku kwa kuwa nilitaka muda na nyinyi. Nataka tuwekane
sawa. Tunaishi pale na watu wengi. Ni rahisi mahusiano yetu kumezwa na watu
wanao tuzunguka. Mwishowe tukasahau nafasi zetu kwetu. Namaanisha ikawa
rahisi kupoteza muelekeo. Kwa kifupi, nilitaka kukukumbusha wewe ni nani
pale ndani na kwenye maisha yangu.” Nanaa alikuwa akimsikiliza.
“Nahesabu ni baraka kuwa na wewe mpaka sasa hivi
Nanaa. Sitaki mambo tutakayopambana nayo njiani, yakachukua kile
kilichopo ndani yetu. Naamini bado unanipenda.” “Sana Geb! Wewe unajua kama
nakupenda.” “Basi naomba siku ya leo iwe kwa ajili yangu na Liv tu. Naomba tuwe
wote hapa. Akili zako, mawazo na kila kitu chako. Unakumbuka mapenzi
tuliyofanya mara ya kwanza tulipokuwa wote huku Morogoro?” Nanaa akacheka kwa
aibu.
“Basi nakuomba tena. Nina hamu na wewe Nanaa.”
“Hata mimi Geb. Nakuahidi nitatulia.” Geb akatabasamu na kumbusu.
“Nakuahidi kesho tutapata muda mzuri wa mazungumzo. Nitakwambia kila kitu.
Halafu tutajua kwa pamoja kitu cha kufanya.” “Sawa.” Wakahamia sakafuni kuanza
kucheza na mtoto wao wakati Geb ameagiza chakula hapo chumbani.
~~~~~~~~~~~~~
Mtoto alipolala tu, Nanaa akachangamkia kazi.
Akaanza mabusu kwa Geb. Geb akacheka. “Nina hamu na wewe Nanaa! Nina kiu.”
“Itaisha leo.” Nanaa akamnong’oneza masikioni. Geb akamnyanyua kutoka pale
sakafuni na kumuweka kitandani. Akamfunua gauni yake akambusu tumboni. “Akiwa
wa kiume, nitamuita Magesa Junior.” Mara zote Nanaa alikuwa akisahau kama ni
mjamzito.
“Akiwa wa kike je?” Nanaa
akauliza huku akitoa tabasamu. Macho ya Geb yalikuwa tumboni kwa Nanaa.
Akambusu tena na tena tumboni. “Oliva ulimlea ukiwa peke yako. Huyu nitamlea
mimi. Zamu yangu.” Nanaa akacheka. Hakuwa amepewa jibu lake. Lakini akaamua kunyamaza.
Alijua wazi Geb amesikia swali lake.
“Nataka unitajie kitu kimoja. Kikubwa unachotaka
kutoka kwangu Nanaa. Nitakununulia. Chochote kile. Wala usiwe na
wasiwasi juu ya pesa.” Nanaa akakaa. “Chochote kile?” Nanaa akauliza. “Chochote
kile.” Nanaa akacheka huku akifikiria. “Kwanza niulize kwa nini?” “Kwa sababu
nakupenda.” Nanaa akacheka sana. “Hiyo ndiyo sababu pekee?” “Huniamini?” Geb
akauliza. “Nakuamini Geb. Ila najiuliza kwa nini sasa hivi?” Geb akakaa pembeni
yake.
“Ngoja nikwambie kitu.
Ulipokuwa hospitalini, ndipo nilipojua sina maisha mengine bila wewe
Nanaa. Thamani yako kwangu iliongezeka mara zote pale nilipoona hatari ya kukupoteza.
Nikajiambia Mungu akinipa nafasi ya kuja kuwa na wewe tena, nitakufanyia
chochote utakacho. Lakini kiwe kikubwa kitakacho nigarimu. Ili kila
nikikumbuka, nikumbuke uthamani wako. Si kwa kuwa nitasahau, lakini..”
“Unamaana zaidi ya milioni 50 ulizo nilipia!?” Geb akacheka.
“Namaanisha
kikubwa.” Nanaa akabaki ametoa macho. “Hivi unajua kitu ulichonipa kwenye
maisha yangu? Au unajua kitu ambacho unaendelea kunipa kwenye maisha yangu ni
cha thamani kuliko mtu anavyoweza kufikiria?” “Unamaanisha watoto!?” Nanaa
akauliza. “Ulimpata Liv na kulea mimba kwa mateso ukiwa peke yako. Sasa hivi
nafurahia mapenzi ya huyo mtoto. Hakuna jinsi naweza kukwambia furaha
yake ukaelewa.” Nanaa hakuwa ameelewa.
“Jamani Geb! Mbona
nimesikia watu wengi walikuwa wakitaka kuzaa na wewe!?” “Kwa kuwa walitaka kunitumia
tu! Walitaka kwa faida zao wenyewe. Wengine walijua wakizaa na mimi watanufaika
na pesa yangu. Wengine ni kwa mashindano ili kujivunia kuwa
wamelala na mimi! Wengine walijua wakizaa na mimi watazaa watoto wenye akili
kama zangu! Lakini sio wewe Nanaa.” Geb akawa kama amekumbuka kitu cha
kumwambia.
“Unakumbuka zile siku ambazo tulikuwa hatupo
kwenye maelewano? Kama ile siku ulikuwa umeniomba nikusindikize mahali.
Ukajiandaa kabisa. Akaja Liz, nikaishia kutoka na Liz, nikakuacha wewe?”
Nanaa akanyamaza.
~~~~~~~~~~~~~
Alikumbuka jinsi alivyokuwa ameumia. Alitoka
kwenye birthday aliyokuwa amealikwa na Zena kigamboni. Jeff akamtambia na
mwanamke wake. Akaamua kurudi nyumbani. Akamkuta Geb akiwa anafanya kazi juani.
Akamwokoa na ile hasira. Wakapata muda mfupi, mzuri. Wakakubaliana
watoke. Lakini Geb akaishia kutoka na Liz badala yake yeye ambaye alikuwa
ameshajiandaa. Nanaa aliumia sana, na kuamua kukaa mbali na Geb. Mpaka
mama yake Geb alipombembelezea mwanae, ndipo Nanaa akamtumia ujumbe kwa mara ya
kwanza, Geb akatulia.
~~~~~~~~~~~~~
“Nikiwa nimekuumiza,
ulikuwa unaweza kuweka hisia zako pembeni na kunifikia mimi. Kutaka
kujua ninaendeleaje! Kuhakikisha nipo sawa, ndipo mambo mengine yaendelee.
Wakati wote unaniangalia mimi kama Geb. Uwe katika uzima au matatizo.
Akili zako zipo kwangu mimi kama Geb. Umeweza kutenga hisia zako na mali zangu.
Unanipenda mimi kama Geb.”
“Sijawahi kufanya mapenzi
na mwanamke mwingine kama ninavyofanya mapenzi na wewe Nanaa. Nikiwa nafanya
mapenzi na wewe, moyo wangu, akili zangu na hisia vyote vinafunguka kwa
kuwa najua nafanya mapenzi na mwanamke anaye nithamini. Hamu na wewe haijawahi
kuisha. Ni vile tu kwa kuwa na mimi ni mwanadamu wa kawaida, nachoka.” Geb
alikuwa akiongea naye taratibu na kwa hisia.
“Lakini Nanaa, kiu ya
mapenzi kwako haijawahi isha. Nilikuwa nikikutamani wakati nikiwa na Liz.
Niliacha kufanya naye mapenzi, nikijua wewe ndiye utakayeniridhisha.
Nilijaribu baada ya wewe kuhamia pale nyumbani, lakini nilikuja kushindwa
kabisa. Nilikuwa siwezi kufanya mapenzi na Liz, eti nikijua Nanaa yupo
chumba kingine! Tena pale pale ndani! Nilikuja kushindwa kabisa.” Geb
akacheka kidogo kama aliyekumbuka kitu.
“Kitendo cha kukufikiria
unaweza kuja kuchoka kunisubiri. Ukaamua kuachana na mimi, ukawa na mwanaume
mwingine. Akaona kwa macho kile nilichokuwa nikikitazama mimi na kukitamani.
Nilikuwa siwezi kula Nanaa. Nikijua umetoka mle ndani eti mama aniambie au anitumie
ujumbe kuwa Nanaa ametoka, kazi zilikuwa hazifanyiki!” Nanaa akacheka kidogo.
“Nilikuwa ni kama nashindwa
kufikiria. Kile kitendo cha mimi kumpigia mama simu, nimkute peke yake nyumbani
wakati najua unatakiwa wewe uwepo nyumbani, halafu aniambie umetoka!
Au hata kama nakuwa nimetoka na Liz.
Halafu labda nimtumie ujumbe nimuulize Nanaa anafanya nini sasa hivi, aniambie
ametoka! Pengine kuna mtu ulienda kuonana naye, akili zilikuwa zinavurugika
kabisa.” Nanaa akashangaa.
“Geb wewe! Yaani kumbe ulikuwa ukiniulizia hata
ulipokuwa ukitoka na Liz!?” “Kabisa Nanaa. Nilikuwa nikiondoka lakini moyo
wangu umejaa wasiwasi Najiambia unaweza kupata mwanaume mwingine. Halafu
mama naye alikuwa anakusifia huku akiniambia una bahati sana na wanaume
wenye uwezo. Swali la wewe utanisubiria mpaka lini, lilikuwa likininyima
usingizi na kushindwa hata kula.”
“Basi mimi sikuwa na habari hata kidogo!”
“Nilikuwa na wakati mgumu sana. Unajua mpaka Grace akaniambia ni lazima niweke
kikomo. Najiumiza mimi mwenyewe.” “Sasa Grace alijuaje!?” Nanaa akauliza akiwa
na mshangao wa kilichokuwa kikiendelea bila ya yeye hata kuhisi kama anamtesa
Geb aliyeonyesha maisha yake yanaendelea kama kawaida.
“Yeye alijua
kinachoendelea kwa kuwa Liz alikuwa akimlalamikia. Halafu ujue Grace ni
pacha ambaye ni kama hisia zetu zipo pamoja. Nikiwa kwenye mateso, na yeye anaumia
sana. Anaumia sana Grace akijua kama sina raha. Nikiumwa ndio ujue na
yeye ataumwa. Basi, alipoona vile ndio akaniambia yale sio maisha
ninayotakiwa niendelee kuishi kwa muda mrefu.” “Sasa kwa nini ulikuwa ukiishi
hivyo?” Nanaa akauliza taratibu tu.
“Unaona hiki kinachotokea sasa hivi na Zinda?
Sikutaka wewe ndio utupiwe lawama. Mwanzoni sikutaka Liz ageuke kuwa adui
yako. Nilitaka aje anichukie mimi mwenyewe. Nilitaka kukutoa
kabisa kwenye lawama, ajue mimi ndiye niliyekutaka au kukuchagua. Sio
aje akuzushie wewe.” “Asante Geb. Lakini sasa hivi imekuwa
kinyume. Zinda anasema nimekupendea pesa.” “Sio kweli. Hata watu
hawaamini hilo. Hata Liz hakulaumu wewe. Nilihakikisha anaelewa ni mimi ndiye nimekuchaguwa
wewe.” Nanaa akabaki kimya.
“Niambie nini unataka
Nanaa.” “Nataka niwe mkeo kihalali Geb. Nataka niitwe Nanaa Magesa. Kama mkeo
sio heshima ya kuishi na wewe. Nataka uhangaike mpaka uhakikishe mimi ndio
nasimama na wewe kanisani. Nataka uahidi mbele za watu na mimi mwenyewe kwamba mimi
ndio nitakuwa mkeo mpaka kifo kitakapo tutenganisha. Nataka hata
iweje, nibakie kwako mimi peke yangu. Kwako wewe Geb. Hilo
ndilo NATAKA kutoka kwako. Hiyo ndiyo garama nataka unilipie. Iwe katika
shida na raha. Ukinipa hilo, ndio nitafurahi.”
“Hakuna thamani ya
mali itakayoweza kununua hiyo furaha yake. Nataka uwe wangu mimi Nanaa.
Mimi peke yangu nisiwahi kukushiriki tena na mtu. Na watu wote
wajue Geb ni wa Nanaa.” Hapo ndipo alipoanza kumng’ang’ania Nanaa. Alifanya
naye mapenzi kana kwamba ndio wanaagana na hawataweza kuja kuwa tena pamoja
hapa duniani.
Kwa
hakika siku hiyo ilikuwa ni yao tu. Nanaa na Geb waliweza kuridhishana kila
walipokuwa wakifanya mapenzi. Oliva alipokuwa akiamka walipata muda wa pamoja
naye wakicheza. Walitoka kidogo mida ya jioni kuzunguka hoteli hiyo ya Mikumi.
Geb akiwa amembeba mtoto wake kwa mkono wa kushoto huku wa kulia akiwa
amemshika Nanaa. Wakiongea na kucheka.
Alijitahidi kutuliza akili za Nanaa. Akirudia
rudia umuhimu wake kwake na wanae. Vile anavyomuhitaji. Furaha
aliyompatia kwa kumpa watoto. Tena mtoto kama Oliva mzuri na mwenye uwezo
mkubwa wa kiakili. "Naami hata huyo anayekuja Mungu atamsaidia furaha kama
Liv.” “Hujaniambia kama ni mtoto wa kike tutamuita nani!” Geb akamtekenya
kidogo mwanae, wakacheka. “Eti Liv? Jina la kaka si liwe Magesa Jr?
Utalipenda?” Nanaa akajua Geb anataka mtoto wa kiume. Akaingiwa na hofu. “Iweje nije kuzaa mtoto mwingine wa kike?
Haya mapenzi na sifa zote si vitaisha?” Hofu akafanikiwa kuchukua furaha
yote ya Nanaa.
Kuanzia muda huo mpaka wanaingia kitandani
kulala, Nanaa hakuwa akiongea sana. Geb alikuwa akicheza na Liv. Akajaribu
kumlisha Liv chakula alichokuwa ametayarishiwa na bibi yake. Akala vizuri tu.
Geb akampigia simu mama yake akijisifia kuwa ameweza kumlisha Liv kwa urahisi
tu bila hata kupoteza muda mrefu akimbembeleza.
“Nimezungumza naye tu. Mwanangu
akakubali kukaa kwenye kiti chake, akawa anafungua mdomo. Amekula mpaka
akashiba.” “Mmmh!”
Mama yake akaguna. “Kweli mama.” “Ukute amekula vijiko
vinne tu!” “Ngoja nikuchukulie video uone kibakuli chenyewe.” “Nataka kuona na
tumbo lake. Msije mkamlaza na njaa!” “Sawa mama. Ila ujue mimi
nimewashinda wote. Na mjue mwanangu anaelewa kila kitu. Ni kumwambia tu
ale, anakula.” Nanaa akacheka.
“Unavyojisifia Geb wewe! Ngoja akubadilikie
kesho. Mwanao hatabiriki huyo!” Nanaa akaongeza. “Bwana nyinyi hamjui
kumlisha mwanangu. Mnamkaba badala ya kumkalisha tu kwenye kiti chake ale! Eti
Liv wa Geb?” Geb akakata simu akaendelea na mwanae.
Alimsafisha na
kumbadilisha nguo. Akamuweka kitandani kwake. Akaanza kumsomea kitabu mpaka Liv
akalala. Nanaa alikuwa akimsikiliza wakati anamsomea. Kila mtu alijua Liv
akisomewa kitabu na baba yake alikuwa akilala kwa haraka kuliko yeye mama mtu
au bibi yake. Wakati wao wakimsomea alikuwa akichukua muda mrefu akicheka au
hata kusimama. Mpaka watarudia mara mbili au tatu ndipo anaweza kulala lakini
si baba yake. Wakati mwingine Geb anakuwa hata hajafika mwisho wa kitabu, Liv
anakuwa alishapotelea usingizini. Akamsikia Geb akicheka peke yake. Akajua
anamcheka mwanae. Akatoka.
~~~~~~~~~~~~~
Nanaa alikuwa amejilaza kitandani, Geb alijua
wazi amekosa raha. Akambusu tena na tena. Nanaa akarudisha busu kidogo,
Geb akampa tabasamu. “Unakumbuka nilikwambia huwa napanga mambo yangu, halafu
namwambia Mungu?” Geb akamuuliza Nanaa huku akimtizama vile alivyonyong’onyea
pale kitandani. “Nakumbuka.” Nanaa akajibu taratibu tu akitaka kujua
anapoelekea.
“Basi ni tabia niliyofundishwa na baba
yangu. Aliniambia kamwe nisiwahi kuishi bila kujiwekea mipango. Kisha
nimshirikishe Mungu. Basi ndivyo ninavyoishi. Kila kitu napanga, halafu huwa
namwachia Mungu. Ikitokea inaendana na
mapenzi ya Mungu kwenye maisha yangu, basi huwa inatimia. Na ikitokea...” “Kwa
hiyo ni kweli kama alivyosema Grace? Kuwa ulitaka mtoto wa kike ndio awe wa
kwanza.” Nanaa akawa ameshamuelewa hata kabla hajamaliza.
Kabla hajajibiwa akaongeza swali jingine. “Lakini
unataka awe wa kike mmoja tu?” Geb akajua ameshaingiwa hofu. “Kama
nilivyokuwa nikisema. Nikiona havijatokea kama nilivyopanga, baba
alinifundisha kushukuru kwa kuwa mipango ya Mungu kwa wanadamu ni bora
kuliko yetu. Akanifundisha kupokea kila Mungu atakachonipa.” Nanaa
akatulia.
“Nikweli nilimuomba Mungu kuwa mtoto wangu wa
kwanza awe wa kike. Halafu wa pili ndio awe wa kiume. Akaja Liv. Nikajua mpango
wangu uliendana na wa Mungu. Nilikuvizia siku za mtoto wa kike, na
nikafanikiwa. Tangia umerudi, nilishindwa kuhesabu mzunguko wa hedhi yako.
Nilikuwa siwezi kusubiri siku hata moja ya kutofanya mapenzi na wewe.” Nanaa
akacheka na kujifunika uso.
“Kwa hiyo huyo mtoto wa sasa hivi, ni yule Mungu
atakaye nijalia. Hakuna juhudi zozote nimefanya kumpata wa kiume. Nitampokea
vile atakavyonijalia Mungu. Wewe huusiki na jinsia ya mtoto
yeyote utakaye zaa.” Kidogo Nanaa akatulia. “Niliogopa Geb!” “Nilijua.
Nilikuona vile ulivyobadilika. Huna haja ya kuogopa. Akiwa wa kike,
tutamtafutia jina utakalotaka wewe.” “Ndio maana nakupenda!” Wakajikuta
wameangukia kwenye mapenzi tena.
Wakaendelea usiku huo, wakalala na kuamkia
alhamisi. Siku hiyo na ijumaa wakatumia hapo hapo hotelini wakizunguka tu, kula
na kucheza na mtoto wao huku wakizungumza mazungumzo yasiyoweza kuibua hisia za
majonzi.
Jumamosi,
Mjini Morogoro.
Waliamka siku ya jumamosi
Geb alikuwa amelipia gari ya kuwapeleka mbuga za wanyama. Nanaa alikuwa
akishangaa na kufurahia kila kitu. Kila wakati Geb alikuwa akiwapiga picha yeye
na mwanae. Mwishowe yule aliyekuwa akiwazungusha mbugani akawasaidia kuwapiga
picha kwa pamoja. Wakapata muda mzuri sana huko mbugani. Hasa Nanaa ambaye
hakuwa akijua starehe.
Kwa muda mfupi aliokuwa ameishi na mama G na Geb,
alikuwa akinukia pesa. Kila kitu cha Nanaa kilikuwa kizuri.
Alikuwa akienda kununua vitu na mama G mpenda vitu vizuri. Kwa hiyo hapo alipo
alifanania na Oliva na utajiri wa Geb. “Anasinzia huyo!” Nanaa akamwangalia
Oliva mikononi kwa baba yake. “Naona turudi tu hotelini. Hata hivyo ni kama
tumeshaona wanyama wote.” “Nakushukuru Geb. Nimepata wakati mzuri sana.” Nanaa
akatupia na busu la shukurani. “Nimefurahi kama umepafurahia. Nimefanya hivi
makusudi kwa ajili yako.” “Najua Geb. Asante.” Wakarudi hotelini.
Mpaka wanatoka bafuni kuoga, tayari muhudumu
akawa ameshaleta vyakula pale chumbani. Wakakuta vimeandaliwa vizuri hapo
ndani. “Chumba chote kinanukia chakula!” Nanaa akasifia. “Husikii
kichefuchefu?” “Hata kidogo. Ndio naona njaa inazidi kuuma.” “Vaa basi!” Geb
alianza kucheka. Maana Nanaa alikaa pale pale na taulo lake na kuanza kula.
“Acha kwanza nishibe bwana!” Geb akajua mimba ya safari hiyo haitamsumbua.
Wakakaa na kuanza kula.
~~~~~~~~~~~~~
“Mbona unaniangalia hivyo?” “Kuna kitu nataka
kukwambia.” Nanaa akavuta tena bakuli la matunda, akajisogeza vizuri kwenye
kochi akajiweka sawa. Akakumbuka Geb alimwambia hiyo ndiyo siku atamwambia
ukweli wote. “Umeshiba kweli? Naona bado unajilamba vidole!” Geb akamuuliza.
“Nahisi nina tatizo Geb. Nimeanza kutokushiba! Ile siku tunaondoka nyumbani,
ile asubuhi tulipokaa wote pale nyumbani
na kupata kifungua kinywa, ujue mwenzio nilianzia kula jikoni! Nilikunywa uji
wako pia. Supu ile aliyotengeneza mama. Chapati alizokuwa ameleta Danny jana
yake usiku na yale mayai niliyokula pale mezani. Halafu si ulinisikia njiani
nilivyokuwa nakula?” Geb akaanza kucheka.
“Usinicheke bwana! Sishibi
hata! Yaani ninakula naona sishibi!” Nanaa akaendelea kulalamika. “Kumbuka
unanyonyesha na una mtoto anayekutegemea tumboni.” “Unahisi ndio sababu?” Nanaa
aliuliza huku akimalizia juisi ya matunda iliyobakia kwenye mabuli baada ya
kumaliza matunda yote. Geb akazidi kucheka. “Tuagizie chakula kingine.” “Naona
wazo zuri. Sijashiba hata! Na safari hii waambie walete chips za kutosha Geb.
Wanapunja sana bwana!” “Nitaagiza sahani mbili. Unataka na nini?” “Ndio maana
nakupenda. Sasa moja iwe chips na mayai. Wasiunguze wala kukausha. Waache
mbichi kidogo.” Geb alikuwa akimtizama Nanaa na kucheka.
“Usinicheke bwana! Halafu
sahani ya pili iwe chips na kuku. Walete na kachumbari yenye kila kitu
walichonacho huko jikoni. Na waweke na limao. Sio jingi.” “Sasa kwa maelezo
hayo. Nafikiri niende mimi mwenyewe kuzungumza na mpishi.” “Udumu Geb wangu.
Lakini nahisi nitanenepa sana jamani! Utanichukia?” Geb akambusu. Alipotaka
kumuachia. Nanaa akamng’ang’ania midomo yake.
“Kidogo tu, halafu ndio uende.” “Si umesema una
njaa wewe? Ngoja nikalete kwanza chakula.” “Sio kuwa nina njaa! Ila sijashiba.
Njoo kidogo bwana. Nina hamu na wewe Geb.” Geb hakujivunga. Akachangamkia
penzi. Haikuwa kidogo kama alivyoomba Nanaa. Walihamia kitandani. Nanaa
alinogewa hapo kitandani. Hakutaka Geb amwachie.
“Ni busu tena.” Nanaa aliomba taratibu mara baada
ya Geb kumalizia na yeye. Geb akambusu midomoni kwa muda mrefu kidogo,
akamwachia. Nanaa akajivuta pembeni yake. Karibu kabisa na ubavuni kwake.
“Usilale sasa!” “Nikumbatie kidogo tu.” Nanaa akajigeuza ukutani. Geb akasogea
mpaka nyuma ya mgongo wake. Akambusu nyuma ya shingo.
“Nakupenda Nanaa.” “Nakupenda sana Geb.
Namshukuru Mungu kuwa hapa na wewe. Nashukuru kwa wazo la kuja hapa. Najisikia
vizuri. Sikujua kama nitafurahia hivi. Ni kweli sisi wote watatu, tulihitaji
huu wakati. Asante mpenzi wangu.” “Asante kushukuru.” Geb akapitisha mkono juu
ya kiuno chake. Kiganja kikatua tumboni. Akaanza kumpapasa taratibu, akamsikia
Nanaa ameanza kukoroma taratibu. Akacheka. Akambusu tena mara kadhaa mgongoni.
Akabaki akiwaza.
~~~~~~~~~~~~~
Nanaa alikuwa mwingi wa furaha. Kadhalika Oliva
aliyekuwa akicheka kwa sauti huko mbuga za wanyama. Walipata wakati mzuri sana.
Wakati wote Nanaa alikuwa akimgeukia Geb na kumnong’oneza neno, “Asante”. Akionyesha kufurahia kile Geb alichofanya.
Alikuwa amebadilika usoni kwa furaha. Ni Nanaa aliyekuwa amedidimizwa na
kutamkiwa ni mzigo. Leo Geb amempokea na kuongeza uthamani wake. Nanaa amekuwa
gumzo kwenye jamii! Thamani imeongezwa, kila mtu anamtaka yeye! Mwenye kisu
kikali ndio anakula nyama sasa hivi. Ni Nanaa Magesa.
Joto la mwili wake liliongezeka na kumfanya Geb
kutaka kufanya naye mapenzi kila wakati. Hakutaka kubanduka hapo kwenye mwili
wa Nanaa, ni vile Mungu alifupisha starehe hiyo, na huwa mwili unachoka,
vinginevyo Geb angekesha. Hofu ya kutaka kumwambia kila kitu Nanaa ikaanza
kumwingia. “Nisije kuharibu kila kitu!”
Geb akawaza wakati Nanaa na mwanae wamelala bila hata habari, sababu ya uchovu
wakuzunguka siku nzima mbugani.
Geb akambusu tena
mgongoni huku na yeye amelala kwa ubavu ili kumkumbatia kwa urahisi Nanaa
aliyekuwa na yeye amelala kwa ubavu. Akampapasa tena tumboni mara kadhaa. Hamu
yakutaka kumuamsha apate starehe aliyopewa muda mfupi uliopita ikamjia kadiri
alipokuwa akimpapasa Nanaa.
“Usiku
wa leo utakuwa mfupi. Na hivi amelala mchana!” Geb akawaza na kucheka. “Lakini nikimwambia. Anaweza kuumia sana.”
Wazo jingine likapita. Likamtia hofu kuzungumza yote aliyotaka kuongea na
Nanaa. “Lakini nilazima asikie kutoka
kwangu. Si vinginevyo.” Geb akajirudi. Wakati anawaza, akapitiwa na
usingizi pale pale kitandani alipokuwa amemkumbatia Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~
“Njaa
inauma!” Geb akasikia Nanaa akiongea. Akahisi anaota. “Geb!” Nanaa akamtingisha
kidogo. Akafungua macho. Akakuta giza limeingia mpaka chumbani. Taa ya nje
kwenye balcony, ilikuwa ikimulika kitanda cha Oliva. Chumba hicho kilikuwa
kimejazwa thamani za mbao na viti vizuri vya miti. Geb alichukua kama kinyumba
kidogo, chenye chumba kikubwa kilichogawanywa mara mbili. Kulikuwa na vitanda
viwili humo humo ndani na sehemu kubwa iliyotengenezwa kutoshea meza na viti
vilivyokuwa vimesukwa kwa ustadi mzuri tu. Vyote vilipangiliwa kwenye hicho
kinyumba kilichokuwa kimetengenishwa katika sehemu tatu ndani. Vyumba viwili
na sehemu ya kukaa. Walikuwa na Balcony/
baraza moja kwa nje.
Akamsikia Oliva akiongea
kitandani kwake. “Ameamka huyo!” Geb aliongea akiwa anatoka usingizini.
“Hajaamka muda mrefu. Pole nimekuamsha. Lakini njaa inauma.” “Twendeni basi
wote tukale huko huko sehemu ya kulia chakula. Hata Liv nitaenda kumlishia huko
huko.” Geb akatoka kitandani.
Nanaa alioga hata dakika
haikuisha. “Nanaa!” Geb akashangaa ametoka. “Njaa inauma bwana. Nitaoga vizuri
nikirudi.” Geb akacheka tu. Na yeye akaingia bafuni kwa haraka akatoka.
Alimkuta Nanaa alishavaa na amemtayarisha Liv. “Kweli una njaa!” “Nimeshawapigia
simu. Nikawaambia oda yangu. Nataka nikifika tu, nikute chakula. Siwezi
kusubiri tena.” Akaenda kumpokea Oliva.
Akachukua mfuko wake, wakatoka. Walimbebea cerelac ambayo ilikuwa
niyakuchanganya tu na maji ya vuguvugu.
Walipofika ni kweli
hawakukaa muda mrefu, chakula cha Nanaa kikaletwa. Geb akaagiza maji ya moto na
baridi. Alikuwa ameleta na kiti cha Oliva, maalumu cha kumlishia chakula. Akawa
amemfunga hapo. Amemvalisha na aproni yake. Liv alikaa pale akijua chakula
kinakuja. Alikuwa akimtizama baba yake vile anavyomchanganyia chakula chake.
Kila Geb alipokuwa akimwangalia, Liv alimrudishia tabasamu. Nanaa alikuwa
akiendelea kula kwa juhudi zote wakati Geb akimlisha mtoto huku anazungumza
naye.
Nanaa alikuwa akishangaa
vile Oliva alivyokuwa akila bila shida. “Liv unamakusudi wewe!
Unavyokula kwa bidii kama sio wewe!” “Hamjui kumlisha mwanangu. Mnampakata na
kutaka kumkaba! Liv hapendi fujo mwanangu. Akikaa mwenyewe na kumlisha anakula
vizuri tu. Mnatumia nguvu nyingi bila sababu! Mnaishia kumkera tu. Ndio
maana hali.” “Ngoja niwachukue video nimtumie bibi yake aone ubaya wa mjukuu
wake.” Nanaa akaanza kumchukua video. Liv akacheka. “Tabia mbaya hiyo Liv! Wala
usinichekee.” Oliva alizidi kucheka. “Wala sio mazuri!” Geb alikuwa akicheka.
~~~~~~~~~~~~~
Alipokuwa akilishwa na
bibi yake, wote waliishia kuchafuka. Oliva alikuwa akicheka wakati wote huku
chakula kikitoka. Hakuwa akitaka kutafuna wala kumeza. Mama G akaona awe
anamlisha kwa kumpakata. Oliva alikuwa akipaliwa nakuishia kutapika au kukohoa
na kumlowesha uso mzima bibi yake. Walikuwa wakimlalamikia Geb kuwa mtoto wake
anataka nyonyo tu, hataki kula.
Lakini Geb alikuwa
akiwabishia na kuwaambia jinsi wanavyomlisha Liv, ndio maana hali. Akamnunulia
kiti na kuwaambia watumie njia ya kumuweka ale, napo haikusaidia. Sasa
siku hiyo baba yake alimuweka kwenye kiti chake, akaamfunga vizuri na kumlisha
bila shida. Tena Liv alikuwa akifungua mdomo yeye mwenyewe.
~~~~~~~~~~~~~
Walikuwa na wakati mzuri
sana hapo sehemu ya kulia chakula. Walikuwa wakizungumza mambo yao na kucheka
na mtoto wao huku Nanaa akiendelea kula. Walizungukwa na wazungu watupu hapo.
Wao peke yao ndio walikuwa weusi kwenye eneo hilo la kulia chakula. Nanaa
aliagizia chakula kingine tena, safari hii akawa anaendelea kula taratibu, Geb
akijipanga kuzungumza la moyoni bila kutibua hali ya hewa.
Siri ya kwanza.
“Unajua Danny ni yatima?”
Geb akaanza. “Najua. Alisema na yeye alilelewa kwenye nyumba ya mapadri. Ila
sijui historia yake ni kwa nini ilikuwa hivyo! Na wazazi wake wako wapi!” Nanaa
akajibu huku akiendelea kula, hana habari. “Wazazi wake wote walifariki. Lakini
wote walikuwa wakifanya kazi hapo hapo kanisani. Alianza kufa baba yake wakati
ndio Danny tu amezaliwa. Baada ya kama mwaka mmoja akafa mama yake pia. Lakini
kwa kuwa wazazi wake walikuwa wakitumika hapo kanisani kwa muda mrefu, Danny
alipoachwa peke yake, hao mapadri wakamlea Danny. Ni historia ndefu kidogo.
Lakini ndio hivyo.” “Oooh!” Nanaa akaitikia bila kufikiria. Akaendelea kula.
“Alipofaulu sekondari kwenda Iliboru.” Geb
akaendelea na kumfanya Nanaa amwangalie kwa makini. “Kwani kuna nini tena!?” Nanaa akawaza. “Kwa nini habari za Danny sasa hivi, katikati ya mapumziko yetu!?”
Nanaa akaendelea kujiuliza wakati amenyanyua uso akimtizama Geb aliyeonekana
anataka kuzungumza jambo muhimu.
“Ndipo tukakutana huko. Asilimia kubwa ya
marafiki kwenye lile kundi tulikutana kidato cha kwanza kwenye sekondari ya
Iliboru. Lakini kwenye cubic yetu, au chumba chetu tulikuwa tukilala wanne.
Mimi, James, Danny na Zinda. Tulikuwa tukifuatana sisi wanne. Ndipo Malii na
Goz wakajiunga. Marafiki wengine tulikutana nao kidato cha 5&6. Kundi
likazidi kuongezeka. Wachache hasa wanawake wa lile kundi, tulikutana Chuo
Kikuu Cha Mlimani.” Nanaa akabaki ametulia akimsikiliza, akitaka kujua mwisho
wa yale mazungumzo katikati ya mapumziko yao, yataishia wapi.
“Zinda na Danny wakaanza
urafiki uliowapelekea kuwa kama ndugu. Likizo nyingine kubwa, Danny alikwenda
nyumbani kwa kina Zinda kwanza, ndipo kisha huko kwa hao mapadri, Iringa. James
hakuwa akipoteza muda wowote ule. Shule zilipokuwa zikufungwa tu, alikimbilia
nyumbani ili awe na wewe.” Nanaa akatabasamu.
Akachukua soda yake akanywa. Mara hiyo ya pili,
Nanaa aliomba muhudumu amletee chips na yai. Lakini isikaushwe hata kidogo. Kwa
hiyo hapo alikuwa akiendelea kula kwa kufurahia rojo rojo hilo. Alishamaliza
sahani ya kwanza ya chips kuku, hiyo ilikuwa sahani ya pili aliyokuwa akila
taratibu bila haraka. “Kwa hiyo kuanzia hapo, Danny akawa amepata sehemu mbili
za kuishi. Nyumbani kwa kina Zinda Tabora na huko Iringa, nyumbani kwa wale
mapadri waliokuwa wamemlea tokea mtoto.” “Kwa hiyo kabila la Danny ni muhehe?”
Nanaa akauliza.
“Sina uhakika sana.
Sikuwahi kudadisi hilo. Lakini ni kama wazazi wake walihamia hapo Iringa
kutafuta maisha. Katika hangaika zao, wakajikuta wote wakifanya kazi kwenye
nyumba hiyo ya mapadri. Mama yake alikuwa mpishi. Kama sijakosea. Baba yake
alikuwa akifanya kazi za nje. Usafi, maua na kadhalika. Na nafikiri kama
nakumbuka vizuri, mama yake Danny na yeye alikuwa yatima. Kwa hiyo alikulia
maeneo hayohayo mpaka akaja kukutana na baba yake Danny. Alivyoambiwa Danny ni
kwamba mama yake alishika mimba kabla ya ndoa. Ikamlazimu baba yake kutafuta
chumba na kumchukua. Kumbe baba yake tayari alikuwa na maambukizi ya virusi vya
UKWIMWI. Akamuambuza mama yake. Yaani pale unapomuona Danny ni mtoto
aliyezaliwa na wazazi waliokuwa wameathirika. Kwa kuwa mama yake alikuwa
binti mwaminifu na alilelewa hapo hapo au kwenye mazingira ya namna hiyo,
ikabidi Danny apitie kulelewa kwenye mazingira hayo hayo.” “Maskini Danny!”
Nanaa akamuhurumia.
“Ndio
maana Danny hata mwanamke awe vipi, hawezi kumtaka kimapenzi. Sisi tulijua
atakuja kuwa padre. Tulikuwa naye akiwa hana msichana. Mpaka alipokuja kukutana
na Grace. Kila mtu alishangaa vile alivyochanganyikiwa. Hatukuamini kama ni
Danny.” Nanaa akacheka. Akakumbuka historia ya Danny na Grace.
“Ndio maana anamchunga sana Grace!” Nanaa
akaongeza huku anacheka. “Nafikiri. Anakumbuka kosa la baba yake. Hataki waje
wawaache watoto wao. Wosia wake wakati wote kwa kila mtu ni kuwa makini. Muoga
hata wakuweka pombe mdomoni. Anasema anaogopa kuweka kitu chochote mwilini
mwake kitakachomfanya afanye kitu cha kuja kujutia baadaye.” Nanaa akacheka.
“Kwa hiyo Danny na Zinda, wakageuka kuwa ndugu.
Nikisema ndugu namaanisha ni kama waliokuwa wametoka kwa baba na mama mmoja.
Danny haitaji kualikwa nyumbani kwa kina Zinda. Anaweza kutoka Dar na
kukimbilia Tabora japo kwa siku mbili tu, kuwaona wazazi wa Zinda. Haitaji
kumtaarifu Zinda tatizo la nyumbani kwao ili asaidie. Anatuma pesa nyumbani kwa
kina Zinda kila inapolazimu. Akisikia mama yake Zinda mgonjwa, atawasha gari na
kukimbilia Tabora kumchukua yule mama na kumpeleka hospitalini. Awe na Zinda
asiwe na Zinda, atafanya hivyo. Ndugu wa Zinda hawahitaji ruhusa ya Zinda
kumuomba pesa Danny. Ni kaka yao. Kukiwa na
tatizo nyumbani kwao, wasipompata Zinda kwenye simu, basi Danny
atapigiwa simu.”
“Mimi ndio nimeharibu
mahusiano yao.” Nanaa akajilaumu. Asielewe historia hiyo nzima itakapoishia.
“Wala si wewe Nanaa. Ni Zinda mwenyewe. Zinda alikuwa akijua kabisa ni kwa
kiasi gani nakupenda. Zinda anafahamu. Sijui ni roho gani imemuingia na
kumfanya awe hivyo alivyo. Na ametumia urafiki wake na Danny vibaya au niseme
vizuri, ili kuniharibia mipango yangu.” Nanaa akatulia kidogo. Ni kama akatoka
usingizini. Geb akajua ameanza kupata picha fulani.
“Kama ulivyokuwa ukiona
jinsi Danny na Zinda wanavyoishi. Kufuatana kila mahali. Kuambiana kila
kitu. Kwenye kundi zima wao ndio walikuwa karibu zaidi ya wengine.” Nanaa
akaumia sana. Tayari akawa ameelewa kila kitu. Akainama.
“Kama unavyonijua mimi si
mzungumzaji sana. Lakini hawakuacha kunishirikisha katika mambo yao. Na
japokuwa sikuwa kama wao, wacheshi na mambo mengine, lakini kwa kuwa wote
walikulia pale nyumbani sababu ya Danny, tukajikuta kama ndugu. Hata mimi
nisipokuwepo nyumbani, wao wanaweza kuja tu. Kama alivyosimulia Grace maisha
waliyoishi wakati mimi nipo nchini India. Wote waligeuza nyumbani kwetu kama
kwao.” Nanaa alibaki ameinama.
Geb akaendelea tu. Alikusudia afikishe ujumbe
wake. “Mama na yeye ni yatima kama alivyokwambia. Alipojua historia ya Danny na
mapenzi aliyokuwa nayo kwa Grace, akamfanya Danny kuwa kama mtoto wake.
Anampenda sana Danny. Na kwa kuwa wote wamekutana wacheshi, basi wamekuwa
karibu muda mwingi kuliko hata mimi.” Nanaa akazidi kuumia. Akahisi usaliti
wa hali ya juu.
“Kwa
hiyo mama ndiye aliyemwambia mambo yote Danny, na Danny ndiye aliyemwambia
Zinda?” Nanaa akauliza moja kwa moja na kumfanya Geb atulie kidogo. “Kwamba
mama ametumia uaminifu wangu kwake, akatoa mambo ambayo
nimemuamini nayo, akawa anamwambia Danny!?” Nanaa akatengeneza swali
lake na kulifanya lisikike vibaya zaidi akionyesha maumivu ya usaliti.
“Haikuwa kama hivyo
Nanaa. Unakumbuka siku niliyokufuata hotelini nikiwa na Liv, akilia sana,
kipindi kile cha matatizo yetu?” Kimya. “Unakumbuka hata mama ulimwambia
asimwambie mtu kama una mtoto?” Kimya. “Kwa hiyo hata Grace hakuwa akijua kama
tuna mtoto. Alikuja siku ile ulipokuwa umechelewa kurudi nyumbani. Ukaenda
kulala hotelini kwa kuwa nilikwambia ikifika saa 12 jioni usirudi tena nyumba.
Grace na Danny walipokuja na kukutana na mtoto wasiyemjua. Anafanana na mimi.
Mama hawamjui wala hakuwepo pale. Grace alichukia sana. Akajua moja kwa moja ni
mtoto wangu mimi, halafu yeye akafichwa. Aliumia sana. Alianza
kulalamika ni kwa nini mimi na mama tumeanza kumficha mambo! Ndipo mama ikabidi
amuelezee kila kitu. Wakati akimuelezea alikuwepo Danny na Fili pia.” “Lazima amtetee. Si ni mama yake?”
Likapita wazo kichwani mwa Nanaa, likamchafua kabisa moyo wake.
Geb aliendelea kumuelezea
lakini Nanaa alibaki ameinama. Akaanza kufikiria mambo yote aliyokuwa
akimshirikisha mama G. Akagundua ndio maana Zinda amefanikiwa kutengeneza uongo
unao fanana na kweli. Alijua amepata rafiki wa kweli, na siri zake zipo salama.
Lakini akagundua amemuamini mtu ambaye anaye watu wake. Geb akaendelea
kuongea.
“Kwa hiyo mambo yote anayozungumza
Zinda sasa hivi, ameyatoa kwa Danny, na Danny ameyatoa kwa mama?” Nanaa akanyanyua uso na
kuuliza wakati Geb akiendelea kuongea. Machozi yalishaanza kuchirizika kama
mvua. “Usifikiri kwa hivyo Nanaa!” Nanaa akacheka kwa kuguna huku akifuta
machozi. “Unajua nilimwamini sana mama! Nilikuwa
nikimwambia kila kitu changu! Nikajisikia nimejenga mahusiano mapya!
Nikajiona ni kama nimepata sehemu yangu peke yangu. Kumbe nilikuwa najidanganya
tu! Na sijui ni kwa nini nimekubali kujifanya mjinga wa kiasi hichi jamani!
Nikasahau na kufumbia macho mahusiano niliyoyakuta kwenu! Mna umoja ambao mimi nitabakia
mtu wa nje tu.”
“Sio kweli Nanaa.” “Ni
kweli Geb. Hata kama utatetea familia yako. Mimi nitabakia mtu wa nje tu.
Hata wewe unahaki ya kuwatetea. Mnamahusiano makubwa. Historia zenu zina
mizizi. Mimi nimekuja kwenye maisha yenu hata miaka miwili sijamaliza. Kwanza
nimekuja ni kama nimewatibulia mambo. Mimi nimekuwa mtu wa kuzungumziwa kati
kati yenu. Habari zangu zinazungushwa vile mtakavyo kwa kuwa nimekuwa mgeni
niliyeongezeka na matatizo yangu.” “Unakwenda mbali sana Nanaa.”
Geb akashangaa vile Nanaa alivyochukulia lile jambo. Hakutegemea.
“Usingewatetea, hata mimi
ningekushangaa Geb.”
“Siwatetei Nanaa!” Hamu ya chakula ilishamuisha Nanaa. “Mama anakupenda sana.”
Geb akaongeza. “Kiasi cha kutoweza kunifichia
siri zangu? Kiasi cha kushindwa kunisitiri kama anavyomsitiri
Grace au wewe? Ananipenda kiasi cha kunidanganya?” “Nanaa!” “Nini? Au mimi ndio nakosea sasa hivi? Ni juzi tu,
nimemuuliza mama tena mbele yako na kaka kama ni yeye ndiye ametoa mambo yangu
na kumpa Zinda. Akakataa mbele yako. Au umesahau?” Nanaa aliendelea
kuongea taratibu huku akilia. Sauti yake ilijaa uchungu wa namna yake.
“Hakukudanganya Nanaa! Mama siye aliyetoa maneno
na kuyapeleka kwa Zinda. Danny ndiye aliyetoa hayo maneno.” “Naomba mimi nikapumzike Geb.” “Tafadhali Nanaa!” “Nini Geb? Hakuna nitakachoongea hapa kikawa sawa na kile
unachotaka nifikirie wewe juu ya familia yako. Naogopa hata kuendelea
kuzungumzia juu ya hili jambo. Naomba yaishe.” “Yanaishaje sasa?” “Unataka kusikia nini Geb? Niambie kile unachotaka
kusikia, ili nikirudie uelewe yameisha.” Hawakuwa wakiongea kwa sauti ya
juu, lakini Geb hakupenda kumuona Oliva akimuona mama yake akilia. Alibaki
ametulia kimya akimwangalia mama yake. Kicheko kikaisha kama anayeelewa.
“Naomba twende chumbani Nanaa.” Nanaa akasimama. Akamchukua mwanae, akatangulia
chumbani.
Geb alikusanya vitu vya mtoto wake, na kile kiti
cha Liv, walichokuwa wamekuja nacho, kwa ajili ya kumlishia chakula, akawafuata
chumbani. Nanaa akafungulia maji ya moto. Akatengeneza kwenye beseni la Liv kwa
ajili ya kumuogeshea. Akamtoa nguo. Akaenda naye bafuni. “Nikusaidie?” Geb
akamfuata bafuni. “Hapana. Asante.” Nanaa akaendelea kumuogesha mwanae. Kwa
muonekano wa Liv, Geb akajua mwanae amehisi mama yake hakuwa na furaha. Oliva
alikuwa ametulia akimwangalia mama yake muda wote. Hapakuwa na kucheka
tena. Geb akajua amani imeshapotea.
Akamtoa mtoto wake kwenye
maji, akarudi naye kitandani kwake kumvalisha nguo za kulalia. Akabaki amembeba
kama ambaye hajui chakufanya. Geb akampokea mtoto. “Nanaa! Tafadhali naomba
yaishe.” “Nimekwambia yameisha Geb. Au unataka
kusikia nimeongea nini? Au hata nikisema hayajaisha, unafikiri ndio
itakuaje sasa? Sina chakufanya. Nimeshajua nafasi yangu kwenye familia yenu.
Basi, inatosha.” Geb akanyamaza kidogo akamgeukia Oliva.
Akamuona ametulia kabisa,
nayeye anamwangalia mama yake. Akambusu. “Nakupenda Liv!” Geb akamwambia mwanae
lakini akapata tabasamu badala ya kicheko alichozoea. Mpaka Nanaa
akashangaa.
Geb akamuweka shingoni kama alivyozoea, lakini Liv
akajitoa akamgeukia mama yake, akabaki akimwangalia. Nanaa alipomuona vile,
akahisi kitu kimemkaba kooni. Akanyanyuka akatoka kwenda nje kwenye
baraza. “Kwanza wameninunua kwa pesa nyingi sana. Sina chakufanya.” Nanaa aliwaza wakati amesimama
pale nje peke yake, akiangalia asione chochote kwa mawazo.
“Nilijua nimepata mtu wangu wa
uhakika! Nilijua mama ndio atakuwa kama mama yangu! Lakini naona
nimejidanganya. Hawa watu wana mahusiano yao ambayo hayawezi kuvunjika wala
kuingiliwa. Mimi ni mgeni, na nitabakia kuwa mgeni tu. Kwanza ujio wangu kwenye
maisha yao umesababisha kuvunjika kwa mahusiano yao.” Akaendelea kuwaza. “Nimebakiwa na kaka tu!”
Kila alipojitahidi
kumuongelesha Oliva, alionekana akili na macho yake yapo kule alipoelekea mama
yake. Alibaki akikodoa macho kama anayesubiri mama yake arudi. Geb akajua Nanaa
analia huko nje. Hakutaka kumtoa mwanae pale. Akajua atazidi kumuhuzunisha mtoto
wake. Akamuweka kitandani pamoja na michezo yake, yeye akatoka kule alipokuwa
Nanaa.
Akaenda kusimama
pembeni yake. Akajifuta machozi. “Nataka nikalale.
Usiku mwema.” Nanaa akataka kuondoka. “Nanaa!” Nanaa akageuka. “Naomba
tuzungumze.” Nanaa akageuka vizuri. Akacheka kwa masikitiko. “Unajua nilidhani safari ya kuja huku ilikuwa kwa ajili
yakutaka muda na mimi, kumbe umegaramia pesa zote hizi ili kuja kuwatetea
ndugu zako!” “Sio kweli Nanaa. Naomba hasira zisikufanye hivyo.” Nanaa
akaingia ndani, akabadili nguo. Akapanda kitandani akalala.
Habari nyingi za kukatisha tamaa
na kuharibu moyo wa Nanaa ziliendelea kupita akilini mwake na KUHARIBU THAMANI
NA GARAMA NZIMA ALIYOLIPIWA KUANZIA NA GEB mwenyewe, Mama G kusafiri mbali
akipambana mpaka kumlipia mahari, na kumalizana na mama James tena kanisani. Lile jambo likakuzwa nafsi mwake na
kusahau kabisa na yale MAKUBWA YA UPONYAJI aliyotendewa na Mungu. Moyo wake ukaumia
kupita kawaida, akasahau YOTE, kwa hilo kosa lililomkumbusha makuzi yake
ya uchungu.
~~~~~~~~~~~~~
Maisha Hayatakosa Sababu ya Kukuyumbisha.
Kutoka kwenye
mikakati ya kutulia, macho kwa familia tu, WAPENZI hawa waliokuwa na wakati mzuri
sana mpaka kushuhudia UKUU wa Mungu, leo imetokea sababu nzuri inayoungana mkono na
hasira ya kuvunjika kwa amani.
Usikose
Muendelezo.
Maji
yametibuka..
0 Comments:
Post a Comment