Hakutaka kumdanganya Nanaa. “Mama yupo nje,
anataka nikazungumze naye. Nakuja sasa hivi. Sitakawia.” “Sawa. Naomba basi
niachie Liv. Niendelee kucheza naye kabla mama hajamchukua.” Geb akaingiwa na
hofu. “Naomba niondoke naye, tafadhali Nanaa. Liv anatambaa. Akienda mbali na
wewe, halafu akataka kushuka, utamsaidiaje na wewe..” Akasita kumalizia. Nanaa
akanyamaza.
Alimuona vile alivyoumia. “Nanaa, unajua sina nia
mbaya.” “Nafahamu. Nenda naye tu.” Nanaa akajibu bila ya kumwangalia. “Naomba
usinikasirikie. Nakupenda mpenzi wangu.” Nanaa akafuta machozi. “Asante.” Akavuta shuka akajifunika vizuri,
asiamini ameshakuwa mlemavu wakushindwa hata kumtunza mtoto wake!
Geb akambusu kwenye kipanda uso, akamnyanyua Liv.
“Nitarudi muda sio mrefu.” Nanaa akatingisha kichwa kukubali. Geb na Oliva
wakatoka. Nanaa alibaki pale kitandani akilia kwa uchungu. Gafla usingizi mzito
sana ukamchukua. Akalala.
Historia ya Mira na Geb.
“Kwa nini mmenitoa kwa Nanaa? Ni kitu gani
ambacho mmeshindwa kuzungumzia ndani!?” Geb aliuliza mara alipofika nje na
kukutana nao wakimsubiri. “Unamfahamu Mira?” Mama yake akaenda moja kwa moja
kwenye swali. Geb akakunja uso. “Mira yupi!?” Geb akauliza. “Wewe unamfahamu
Mira yupi?” Mama yake akauliza tena. “Mira ambaye ni mfanyakazi wetu. Au
muhasibu kwenye kampuni yangu. Kwani vipi?” “Ni msichana wa wapi?” Mama yake
akadadisi tena na kumfanya bado Geb ashangae.
“Kama ni kabila nafikiri ni mtu wa huko kwa kina
Zinda. Kwa sababu anafahamiana na Zinda. Kuna siku, zamani kidogo, Zinda
alikuja pale ofisini kwangu. Mira akawa ameingia pale akitaka niweke saini
kwenye karatasi fulani hivi. Zinda akamtamani yule dada. Nikamwambia amfuate tu
ofisini kwake. Akamfuata. Baadaye Zinda akarudi tena ofisini kwangu na
kuniambia amechukua namba zake za simu na kumbe Mira ni mtu wa kwao kabisa.
Nikamtania na kumwambia ndio aoe kabisa. Akasema ni kama Mira ametokea kwenye
ukoo wa kichawi kidogo. Huko kwao, kijijini kwao Tabora, ukoo wao kina
Mira, hauna sifa nzuri, wazazi wake hawawezi kumruhusu kumuoa. Lakini
akasema atamtafuta tu. Basi. Kwani vipi?” Bado Geb hakuwa ameelewa.
“Hujawahi kuwa na mahusiano naye?” Mama
yake akahoji. “Huyo Mira!?” Geb akauliza kwa mshangao mkubwa sana. “Ndiyo.”
“Hapana mama jamani! Si ungejua?” “Hujawahi kulala naye hata mara moja?”
“Mama!!” Geb akashangaa zaidi. “Si unijibu tu?” James na Danny walikuwepo pale
wakisikiliza. “Hapana! Kwani vipi, mbona maswali ya ajabu!?” Wote watatu
wakaangaliana. “Jamani, naombeni mzungumze. Mimi natakiwa kurudi ndani kwa
Nanaa. Nimemuacha peke yake.” Geb akasisitiza, akionyesha wazi hataki
kupotezewa muda.
“Labda na mimi nikuulize kitu kingine Geb. Nani
alimleta Mira kufanya kazi kwenye kampuni yako?” James akauliza. “Yeye mwenyewe
alinitafuta. Nilikuwa nikifahamiana naye tokea nilipokuwa nchini India.”
“Ooooh!” Wote watatu wakaitikia pamoja. “Kuna nini nyinyi? Mama!?” Bado Geb
hakuwa anaelewa. “Huko nchini India mlikuwa na mahusiano gani na Mira?” Mama
yake akauliza tena.
“Hatuku…” Geb akataka kukana kwa haraka, lakini
akasita kidogo kama aliyekumbuka kitu. Akakunja uso kidogo. “Nini?” Mama yake
akajua amekumbuka kitu. Kisha akatulia gidogo. “Mira ndiye anayehusika na
kumtesa Nanaa? Maana na yeye alikuwepo siku ya kwanza ya kikao! Alikuja
kumletea karatasi fulani Grace. Grace alimwambia azilete ili alinganishe na
ripoti ya mwezi huo. Akaja siku ya ijumaa usiku. Akamkuta Grace yupo na heka
heka ya kupigia watu wa chakula simu. Akiwasisitiza wasichelewe kesho yake.
Tena hata mama utakuwa ulimuona ila utakuwa labda hukumtilia maanani. Watoto
walikuwa wakilia. Grace alimwambia wazungumzie pale nje barazani ili
wasikilizane. Baadaye Grace akaniita na mimi kuniuliza swali, mambo ya ofisini.
Wakati Grace anazungumza na watu wa chakula, Mira alikuwa akisikiliza.
Alipomaliza akamuulizia Grace, kuna nini. Nakumbuka kumsikia Grace akimtania na
kumwambia kuna makulaji kesho kwenye kikao changu cha kwanza cha harusi.
Halafu..” Geb akatulia kama akakumbuka tena kitu.
“Nini?” Mama yake akauliza. “Ni kama akabadilika
kabisa. Sasa hivi ndio nakumbuka sura yake. Ni kama alikosa raha gafla
na mawazo yake hayakuwepo tena pale. Nafikiri ndio maana Grace akamualika aje
ahudhurie kesho yake. Akakubali bila ubishi. Lakini kwani nyinyi mmesikia
nini?” “Subiri kwanza Geb. Mimi nakumbuka kumuona yule msichana siku ya ijumaa,
lakini sio siku ya jumamosi kwenye kikao.” “Alikuwepo mama. Tena alikuwa amekaa
karibu sana na sisi pale.” Geb akatulia kama anayewaza kitu.
“Turudi kwanza mlipokuwa nchini India. Mlikuwa na
mahusiano gani?” Mama yake akaendelea kudadisi. “Nilipofika mwaka wa mwisho
huko huko India, nilikuwa sina tena pesa za kuishi kwenye nyumba yangu peke
yangu au ya watu wawili. Ikanilazimu kutafuta sehemu ya kujishikiza huku
namalizia chuo. Nikapata chumba walipokuwa wakiishi Mira na wasichana wenzake.
Nikahamia hapo mimi na kijana mwingine. Tukawa tukitumia chumba changu. Pesa
niliyokuwa nikilipa hapo kwa ajili ya pango, ikawa ndogo sana. Kwa kuwa kwanza
ilikuwa chumba kimoja tulichokodi kwa kina Mira, halafu tulikuwa na mwenzangu
kwenye hicho chumba. Maisha yakaendelea kwa unafuu.”
“Mira akaanza kuhangaika mara aingie chumbani
kwangu achukue nguo zangu chafu afue, mara atake kunipigia pasi nguo zangu.
Akawa akipika anataka na mimi nile naye. Ikawa heka heka kweli. Nikawa nakosa
utulivu. Narudi chumbani nakuta vitu vyangu vimepangwa, nguo zimefuliwa.
Nikimuuliza yule jamaa, akawa ananiambia ni Mira. Na labda anakuwa ameleta na
chakula. Ameniachia hapo chumbani. Sasa yule jamaa niliyekuwa nikiishi naye kwa
kuwa alikuwa akinijua sipendi kula vile vyakula, yeye akawa anakula. Nikirudi
alikuwa akiniambia, ‘nimekula chakula alichokuwa amekupikia Mira kwa kuwa
nilijua hutakula.’ Nikamwambia ni lazima nimwambie Mira. Ajue ili asihangaike
kunipikia. Mimi sitaki kufuliwa wala kupikiwa. Yule jamaa akanisihi
niache kwa mwezi huo mpaka atakapotumiwa pesa kutoka nyumbani kwao. Hakuwa na
pesa.” Geb akaendelea.
“Tena jamaa mwenyewe alikuwa ni mtu wa kutokea
Nigeria. Basi. Nilipoona heka heka za Mira zinazidi huku anajitangazia kwa watu
kuwa mimi ni mpenzi wake, ikabidi nimtoe kwa chakula cha usiku ili
nikazungumze naye. Tulitoka. Nikwambia ukweli. Kwamba nipo pale kwa sababu nilifeli
chuo sababu ya mwanamke mwingine niliyekuwa nae kabla sijahamia hapo nchini.”
“Nikamwambia kwa wakati huo sipo tayari kabisa
kwa mahusiano na mwanamke yeyote yule. Akaniomba sana tena kwa machozi.
Tena nakumbuka aliniambia, endapo nitafikiri kuoa, anaomba iwe yeye.
Nikamwambia yeye ndio anaanza chuo hapo India. Mimi nimebakiza muda mchache
naondoka hapo, nisingeweza kumuahidi mambo ya mbeleni. Mira akaniambia anaomba
tu hata ahadi ya kuja kumfikiria baadaye. Nikamjibu sawa.
Tukaachana. Yaani leo ndio mnanikumbusha!”
“Hata mwaka jana alipokuja kuniomba kazi ya
uhasibu kuwa alimaliza chuo na akajaribu kuishi sijui ni India sijui wapi! Hata
sikumfuatiliza, alikuja nikiwa na mambo mengi, sikumtilia maanani. Lakini
ninachojua nilikuwa na shida na muhasibu. Nikamuajiri. Yaani hivi leo ndio hata
nimekumbuka hayo mambo yote. Hata nilishasahau kama hata niliishi nyumba moja
na Mira! Kwanza sijui nilikaa kwao muhula mmoja tu. Yaani kama miezi 4 tu!”
“Aaaaahhh!” Danny, James na mama G wakawa
wameunganisha matukio yote. Wakawa wameelewa. “Kwani vipi!?” Wakamsimulia Geb
mwanzo wa kikao mpaka mwisho. Kuanzia mama James, mpaka habari za Mira. Geb
akabaki ametulia. “Kwa hiyo Mira anadai wewe ni mume wake. Na Zinda ametoa uthibitisho
wa kweli kabisa ambao mchungaji amesema hawezi kutangaza tena ndoa yenu.
Na Zinda ameapa pale mbele ya wote, amesema atahakikisha hutamuoa
Nanaa.” Mama yake akaongeza.
“Mimi nitamlilia Mungu wangu, mama. Nimeamua
kutulia kwa Mungu. Nanaa ni mke wangu mimi. Ananipenda na amenichagua
mimi. Waacheni tu, na Mungu aliye hai. Najua kwa hakika atanitetea. Kwa
kuwa nikweli sijamtendea mtu yeyote yule lililo baya.” Geb akajibu.
“Naombeni mimi nirudi ndani kwa Nanaa.” Wote
walibaki kimya. “Kwa hiyo tufanyaje Geb? Mchungaji amesema hatafungisha tena
hiyo ndoa!” “Naomba nipe siku ya leo na kesho Danny. Sasa hivi sina jibu la
haraka. Ndio mmeniambia. Nahitaji muda wa kufikiria. Lakini, naomba mumuache
kwanza Nanaa. Anayopitia sasa hivi yanatosha. Sitaki tena aongezee mambo
mengine.” “Juu ya Mira? Labda ni vyema amjue mbaya wake.” James akaongeza.
“Itasaidia nini?” Geb akauliza huku amekunja uso.
“Haitamsaidia kitu chochote. Sasa hivi Nanaa amefika mahali karibu sana na
Mungu. Nanaa ameonyeshwa na Mungu na amemuahikishia yupo vitani
kwa ajili yake. Nawaomba mumuache Mungu afanye kazi. Mtakapomtaja Mira sasa
hivi kwa Nanaa, mtatoa macho yake kwa Mungu, mtamrudisha kwa wanadamu. Sina
mpango wa kwenda kwa mganga. Naomba nimuachie tu Mungu. Naamini atapigana na
adui zetu. Sijui kama mmenielewa?” Geb akauliza, kimya.
“Labda ni weke hivi, siruhusu mtu yeyote
yule azungumze na Nanaa jambo lolote lile, ila mimi mwenyewe. Kama hivi
mlivyofanya, nashukuru. Umenisikia James?” “Nimeelewa Geb.” “Asante.” Geb
akarudi ndani. Akawaacha wanaangaliana.
~~~~~~~~~~~~~
Alimkuta Nanaa amelala usingizi mzito hata
hakujitingisha wakati wanaingia na Liv. Mama G akaingia. “Anaendeleaje?”
“Ameshinda vizuri tu. Hata ameniomba kama ninaweza kumuombea arudi nyumbani.
Lakini nimemwambia asubiri kidogo.” Geb alijibu huku akimwangalia Nanaa. Danny
na James nao wakaingia. “Nampenda Nanaa, mama. Ni kila kitu
changu kwenye maisha yangu.” “Najua Geb. Mungu atawasaidia.” Geb akabaki
akimwangalia.
“Umemlisha huyo?” Mama G akauliza akimaanisha
Liv. “Nimemlisha wakati mama yake anakula.” “Amekula vizuri?” Geb akanyamaza.
“Geb?” “Alililia nyonyo sana. Mpaka mama yake akashawishika kumnyonyesha.” “Kwa
hiyo amenyonya!?” “Imebidi mama. Wote wawili yeye na mama yake walikuwa wakilia
sana. Nikashindwa chakufanya. Amenyonya na kulala hapo hapo kwa mama yake. Na
ndio Nanaa naye akaweza kupata usingizi wa mchana. Sijui itakuaje mama!” “Wala
usiogope Geb. Naomba urudie ujasiri uliokuwa nao jana na leo asubuhi. Sisi wote
tunakutegemea wewe. Naomba usitetereke. Mwache Nanaa amnyonyeshe mwanae
kama anataka. Mungu alishatuonyesha ulinzi wake kwa huyu mtoto, hakuna
mwanadamu atakayeweza kumdhuru.” Geb akavuta pumzi.
“Kwa hiyo kesho utamrudisha?” Geb akauliza baada
ya ukimya wa muda kupita. “Kama ananyonya, nitamleta na kile kitanda chake
kidogo ili akae na mama yake tu. Na mimi nitakuwepo. Kwa hiyo na wewe unaweza
kuondoka kurudi nyumbani ukapumzike kidogo.” “Siku nitakayorudi kulala pale
kitandani, ni siku nitakayokuwa na Nanaa, mama. Siwezi kumuacha Nanaa
hapa hospitalini, eti mimi nikalale nyumbani! Hapana. Wewe mlete tu Liv na vitu
vyake, ukamsaidie Grace na watoto.” “Sawa. Mungu atawasaidia Geb.
Tunawaombea.” Geb alimkabidhi mama yake mtoto, akamsogelea Nanaa. Akamvuta
mkono, akaubusu.
“Atapona tu.” Geb aliongea huku akimwangalia
Nanaa. “Hakika Mungu atawasaidia. Umebadilika sana Geb! Hakika umenipa somo. Na
ujue najutia mambo anayofanya mama yangu.” “Usijali kabisa James. Ipo siku
tutayaangalia haya yote, yatakuwa nyuma yetu. Tutasahau kabisa. Nashukuru kwa
kuwa na sisi. Hasa Nanaa. Anakutegemea sana wewe. Usikubali uongo
wa Zinda ukakuingia. Nanaa anakutambua wewe kama baba na kila kitu
kwake. Na mimi naliheshimu hilo.” “Nashukuru.” James akaridhika na
kutulia. Alishapoteza ujasiri kwa Geb.
“Jamani!
Ngoja sisi tuondoke. Nitamrudisha huyu
kesho.” Mama G akaaga. “Naomba kukuaga Oliva Magesa.” Geb akamsogelea mwanae na
tabasamu. Liv akacheka. “Useme vizuri wewe Geb! Oliva Magesa tupo wawili hapa
mjini!” Wakacheka. “Namaanisha mrembo wa Geb.” “Hapo sawa.” Mama G
akajibu.
“Haya, njoo mbusu mama.” Geb akamuinamisha Liv
kwa mama yake. “Mwaaa mama Liv.” Geb ndio akaongea kwa niaba ya mwanae.
“Usimsumbue bibi. Ulale mpaka kesho. Sawa?” Oliva akacheka kama kawaida yake.
Geb akamuweka kifuani. Akamkumbatia kwa nguvu.
“Mhhhhh! Nakuombea
usingizi mzuri. Mkono wa Mungu uendelee kuwa juu yako Liv. Ulinzi wa ki Mungu
ukakuzingire. Nakubariki kwa baraka zooote, za rohoni na za mwilini. Uzima wako
umefichwa ndani ya Kristo Yesu. Kila silaha itakayoinuka kinyume nawe,
Liv, ikakutane na uwepo wa Mungu. Mungu apigane na adui zako. Kila ulimi
utakao inuka kinyume nawe, Liv, Bwana auhukumu mkosa. Natamka uzima juu
yako. Malaika wa Bwana wafanye kituo juu yako, Oliva Magesa. AMEN.” Geb
alikuwa akimuombea mwanae huku amemkumbatia. Akamtoa kifuani kwake akamnyanyua
juu. Olivia akaanza kucheka mpaka watu wote wakacheka.
“Mchekaji kama mama yake!” Bibi yake akamsifia.
“Niwasindikize mpaka kwenye gari?” “Hapana bwana! Atakulilia. Kwanza nipe Oliva
wangu.” Olivia alichukuliwa na bibi yake huku akicheka. “Danny, nijie na mizigo
yote.” “Sawa mama.” Mama G akataka kutoka. “Mama!” Geb akamuwahi. Akamkumbatia
yeye na Liv. “Asante sana mama yangu. Nashukuru kwa yooote.” Geb akambusu
kichwani. “Asante kushukuru. Uniagie
Nanaa akiamka.” “Sawa.” Ndipo akatoka.
~~~~~~~~~~~~~
“Geb!”
Danny akamwita. “Vipi?” Geb akamgeukia. “Naomba unisamehe sana. Nahisi
mimi ndiye nimempa nyenzo nzuri sana Zinda, za kukuangamiza.
Naomba unisamehe. Lakini unajua ukaribu niliokuwa nao na Zinda. Ni kama..”
“Danny! Huko sipo akili zangu zipo kabisa. Naomba uniamini sipo hata
kwenye kumlaumu Zinda mwenyewe. Naomba uwe na amani kabisa. Sisi wote
tulikuwa marafiki wa karibu sana. Kutoa neno kwangu na kulipeleka kwa Zinda,
sio kitu ambacho sikutarajia. Nilikuwa nikifahamu.” “Lakini nimekoma.”
Danny aliongeza kinyonge.“Hata mimi nimejifunza sana. Aisee!” James akaongeza.
“Najua kwa hakika Mungu atatuvusha hapa.
Ila sijui ni lini! Lakini najua kwa hakika tutatoka tu. Mungu atatusaidia.”
Geb aliongea huku amerudisha macho kwa Nanaa. “Tunawaombea Geb.” “Asanteni
sana. Nipeni muda na mimi nimuulize Mungu wangu. Nione atanijibu nini juu ya
hili. Najua ipo njia. Ni mimi tu kutulia na kufungua macho ya kiroho ili kuiona
na kuifuata. Mungu hakukusudia kunipa familia nzuri hivi halafu iangamie!
Hapana. Iko sehemu atataka niifikishe familia yangu. Acha nimuulize Mungu
njia.” Hakika Geb alibadilika na kuwashangaza rafiki zake. Wakamuaga, na
kumuacha hapo amesimama pembeni ya kitanda cha Nanaa akionyesha wazi hataki
kutolewa macho yake msalabani kwenye uponyaji nakusikiliza kesi au
majuto yao. Kila walipotaka kumpeleka nje ya Mungu, alirudisha mawazo yake kwa
haraka sana.
Usiku
Wa Pili Hospitalini.
Kwa kuwa walikuwa wameshakula, akaingia kuoga
hapo hapo bafuni. Akatoka. Alivuta kiti pembeni ya kitanda cha Nanaa. Akaanza
kusoma neno la Mungu, bibilia. Kisha akapiga magoti pembeni ya kitanda,
akamshika Nanaa mkono na kuanza kuomba. Geb aliomba kwa muda mrefu. Kwa machozi
huku akimueleza Mungu yote aliyoambiwa yaliyotokea kwenye ofisi ya mchungaji. “Sijui nifanye nini Mungu wangu! Naomba nisaidie. Hakika
nimekwama.” Geb alilia mbele za
Mungu. Alitamani kama malaika wa Mungu atumwe wakati huo huo ajibu kitu. Lakini
hakuona malaika yeyote. Akatamani kama asikie sauti fulani ikimwambia wakati
huo huo kitu cha kufanya. Akajaribu kutulia ili kusikiliza. Lakini kukawa
kimya.
Nesi aliingia, akamkuta amepiga magoti pembeni ya
kitanda cha Nanaa huku ameinamisha uso wake kitandani hapo. Nanaa alikuwa
amelala usingizi mzito haswa hata hakuwa na habari na kinacho endelea. Nesi
alimsafisha vizuri, akamuacha msafi. Akaondoka bila hata kumsemesha Geb.
Aliendelea kuomba mpaka akamaliza, kisha akavuta kiti, akalala huku ameegemeza
kichwa pembeni ya Nanaa. Alijiwekea mkono wa Nanaa juu ya kichwa chake. Hapo
hapo akapitiwa na usingizi.
Ndoto
Ya Pili Ya Nanaa.
“Nanaa!” Alisikia mtu akimuita akiwa usingizini.
Akastuka. Alimuona mtu amesimama pembeni yake akiwa amevaa nguo nyeupe. Akajua
lazima atakuwa ni daktari. “Nimekuja, nimetumwa
kwako.” Nanaa akakaa vizuri ili amtizame. Akajaribu kumuangalia usoni,
akapata shida kumuona. Uso wake ulikuwa ukiwaka sana. Mwanga mkali. “Umetumwa na nani?” Nanaa akauliza huku akijaribu
kufinya macho yake ili kumtizama. “Na Yupo, ambaye
Yupo.” Mwili wa Nanaa ukaanza kutetemeka. Akaendelea kumtizima kwa
shida, asiweze. “Upo tayari?” Akamuuliza. “Umesema umetumwa kufanya nini?” Nanaa
akauliza.
“Kuna vitu vyakutoa miguuni mwako.”
Yule mtu
aliyekuwa amevaa koti jeupe la kidaktari akasogea mpaka miguuni kwa Nanaa.
Akamfunua akawa anaiangalia ile miguu. Nanaa alikuwa anaogopa kuiangalia miguu
yake. “Unajua nimeshindwa kabisa kuingalia hiyo
miguu? Geb mpenzi wangu, ndiye anayenisaidia kuingalia.” Nanaa aliongea
huku amefunga macho kwa kutumia mikono yake. “Leo
ndio mara ya mwisho. Hutaiona tena hivi ilivyo.” “Unauhakika unaweza
kunisaidia? Maana daktari mwenzio aliwatuma hawa manesi kufyonza maji. Lakini
hata jioni hii nimewasikia wakimwambia Geb hapo nje kuwa wamejaribu kunifyoza
tena, imerudi kujaa tena. ” Nanaa
alijieleza.
“Kwa kuwa hawajatoa mzizi wake.
Zipo sindano katikati kabisa ya kila mguu. Aliziweka katikati ya kila mguu
wako. Ndio inabidi kutolewa kwanza.” Nanaa akashituka sana akafungua macho
kujiangalia. “Wapi!?” Alipofungua macho
kuangalia, akagundua kile chumba kimejaa mwanga mkali sana. “Mbona sioni miguu yangu? Punguza mwanga wa taa na mimi
nione.” Nanaa alilalamika huku jasho likimtoka. “Huwezi
kuona. Ni nyuma ya miguu yako. Geb atakapopima ukubwa wa upana wa vidole vyake,
mara moja na nusu kwenye miguu yako. Utagundua kuwa ni katikati ya mguu wako.
Atakapopasua ndani kabisa, ataona sindano katika kila mguu. Zilichomekwa hapo.
Azitoe.” Yule mtu ambaye Nanaa aliyemtambua kama daktari kwa koti jeupe
aliloliona Nanaa kwa shida, akatoa hayo
maelezo. Yakamchanganya Nanaa.
“Sijaelewa ni wapi! Kwanza na nani?
Nani
ameniwekea hizo sindano?” Nanaa
akaanza kulia huku akihangaika kutazama asiweze. Mwanga kutoka kwenye uso mkali
wa yule mtu ulikuwa mkali sana. Aliona akiwa ameshamgeza, na mikono yake
imegusa miguu yake. “Hizi hapa.” Yule mtu
aligusa kwa nguvu kidogo. Alikuwa ameweka kidole sehemu ambayo kwa mara ya
kwanza tokea siku ya kikao chake cha kwanza cha harusi, Nanaa alipopoteza uhusi
wa miguu yake, hapo huyo mtu alipopagusa aliweza kuhisi ameguswa. “Nimehisi vidole vyako katika kila mguu wangu!” Nanaa aliongea kwa furaha sana.
“Basi hapo
ndipo zilipofichwa hizo sindano.” Moyo wa Nanaa ukajawa furaha. “Hakika wewe ni daktari bingwa. Wenzako wamejaribu
kunisaidia wameshindwa. Naomba basi nitoe.” Nanaa alikuwa amelala fudi fudi. “Utanitoa?”
Nanaa akauliza. Lakini kimya. “Tafadhali nisaidie.
Geb anateseka. Nina mtoto mdogo anaitwa Oliva. Bado ananihitaji. Naomba
nihurumie. Hapa nilipo ni mjamzito. Mungu ametubariki mtoto mwingine. Sitaki
niwaache wanangu kama mama yangu alivyoniacha mimi. Tafadhli naomba nisaidie.” Nanaa
alikuwa akilia sana. “Tatizo lako limekwisha.” Yule
mtu akajibu hivyo, kisha kimya. Nanaa akashituka kutoka usingizini. Cha kwanza
akajifunua miguu yake kwa haraka. Akajikuta yupo vile vile.
~~~~~~~~~~~~
Alilia, mpaka Geb akaamka na nesi akaingia. “Kuna
nini?” Nanaa aliendelea kulia. Geb akapanda kitandani, akakaa upande. Akamvuta
karibu akamkumbatia. “Nimeota nimepona Geb.”
Nanaa aliendelea kulia. Alilia kwa muda mrefu. “Kabisa
aliniambia tatizo langu limekwisha.” “Nani?” Geb akamuuliza huku
yule nesi amesimama pembeni akimuhurumia Nanaa. Alijiambia ndio madhara ya
kuomba sana. Alimuona vile Geb na Nanaa wakiomba. Akajiambia wamejiwekea
tumaini la bure! Yule nesi alibaki kimya akisubiri Nanaa atulie, amfunike tena.
“Naomba utulie tuzungumze Nanaa.” Baada ya muda,
Nanaa akatulia. Akamsimulia Geb habari nzima. Mwanzo mpaka mwisho. “Aliniita kabisa, nikashituka kutoka usingizini. Haikuwa
ndoto mpenzi wangu. Naomba uniamini. Nilikaa. Akanishika kabisa.”
Nanaa aliendelea kusisitiza huku akilia. “Hizo ni ndoto za kawaida hasa ukiomba
sana. Akili inajiandaa kwa majibu. Lakini hakuna daktari mpya aliyekuja hapa.
Kwa sababu kama angekuwa amekuja, sisi manesi ndio tungekuwa wa kwanza kum..”
Yule nesi aliingilia. “Naomba unyamaze kwanza.” Geb alimkatisha. “Tafadhali nyamaza.”
Geb akasisitiza.
“Nanaa! Mimi nakuamini. Lakini
aliyekutembelea hakuwa ni daktari. Ni malaika wa Mungu. Hata mimi nimesikia
ndotoni nikiitwa. Nilipoitika, nikasikia tu neno moja, ‘USIOGOPE’.
Nikajua ni akili zangu tu, kwa maombi niliyoomba wakati nimelala. Lakini hakika
ni Mungu.” “Asante kuniamini Geb. Sasa tufanyaje?”
Nanaa akauliza. “Tuchukue hatua ya Imani. Hatuna cha kupoteza. Si
umesema husikii maumivu kwenye miguu yako?” “Bado
sihisi kitu. Imekufa ganzi vile vile.” “Basi naomba unipe tena maelekezo
uliyopewa unipe. Mungu ameniambia nisiogope. Na amekutuma wewe uniambie mimi
ndiye nitoe hizo sindano. Acha nizitoe.” Yule nesi akashangaa.
“Nashauri mumsubiri daktari. Usije ukamtoboa,
halafu kesho ukanitafutia mimi matatizo kwenye uongozi!” Yule nesi akaweka
kipingamizi. “Wewe si umeniambia kila ukimfyoza maji malengelenge yanajaa
tena?” “Ndiyo.” Nesi akajibu kwa kujiamini asijue anaongea na Geb mwenye uwezo
mkubwa sana wakufikiri.
“Basi. Kama hakuna sindano, inamaana nikimaliza,
yatarudi tena vile vile. Naomba kaniletee kitu kikali, ambacho kitakuwa kipo sterilized.
Mimi mwenyewe nitafanya.” Nanaa akambusu Geb. “Asante.”
Geb akarudisha tena busu. “Mungu wetu anaishi Nanaa.” Kwa kuwa Geb
alishawalisha na kuwanywesha. Halafu akawa akiwashukuru kila wakimfanyia kitu
Nanaa, zaidi ya hapo yupo chumba cha peke yake kwenye hospitali hiyo ya
kulipia. Inamaana pesa ipo. Heshima kutoka kwa wauguzi hao, ilikuwepo kwa Geb. Nesi
akatoka.
~~~~~~~~~~~~
Ilikuwa yapata saa nane usiku, wakati nesi
ameleta kila kitu na kumsaidia Geb kumgeuza Nanaa. Nanaa akalala kifudi fudi.
“Naomba urudie tena maelezo yake.” Geb alikuwa tayari amevaa gloves na ameshika
kisu cha upasuaji mkono wa kulia. “Fungua vidole vyako. Gumba na kile
kinachofuata. Nyoosha kabisa. Pima mara moja na nusu, kuanzia chini kwenye
kiungo cha mguu na nyayo kuja juu. Weka hapo kidole. Ninatajua.” Nanaa akatoa
maelekezo kwa hakika.
“Sasa utajuaje akikugusa wakati miguu yako
imekufa ganzi!?” Nesi alitoa neno jingine la kukatisha tamaa. Akamtia wasiwasi
Nanaa. Akasita. “Lakini yeye aliponigusa, nilijua. Pengine na Geb akinigusa
kama ni hapo, nitajua.” Nanaa akajibu huku akitetemeka. “Nanaa! Naomba usiogope.
Hatuna chakupoteza. Tulia nikupime.” Nanaa akarudisha uso kwenye mto. Geb
akaanza kumpima.
Hatua ya kwanza. “Unanisikia? Hiyo ni hatua ya
kwanza.” “Hapo umenigusa?” Nanaa akauliza
huku akilia kwa hofu maana hakusikia chochote. Inamaana yule nesi alikuwa
sahihi. Ni mawazo tu. Haikuwa ndoto au maono kama alivyosimulia. “Lakini ndio
hatua ya kwanza Nanaa. Usiogope.” Geb
akajaribu kumtuliza. “Labda huyo nesi yupo sahihi
Geb. Ni ndoto tu. Sisikii kitu kabisa.” Nanaa aliendelea kulia akisikika
amekata tamaa.
“Niliwaambia mimi. Naombeni muache tu jamani!” Nesi
aliendelea kusisitiza hoja yake. “Mambo hayo mnayaona kwenye luninga tu.
Wachungaji siku hizi wanafanya kama maigizo tu ili kuvutia watu.
Hakuna kitu kama hicho!” Nesi aliendelea. Nanaa akazidi kulia. Geb akaweka kila
kitu pembeni, akarudi kumtuliza.
Akapiga magoti pembeni yake. “Naomba niangalie na
kunisikiliza mimi, Nanaa.” Nanaa alikuwa amejawa jasho, machozi na kamasi uso
mzima, akamgeukia. “Naomba nipe nafasi ya kujaribu mpenzi wangu. Tafadhali.
Uliniahidi utasimamia imani yangu. Basi mimi naamini. Naomba nifanye. Na hata
kama huoni sababu yakufanya hivyo, basi fanya kwa ajili ya Oliva na mtoto.” “Haya.” Nanaa akakubali.
“Haya?” Geb alimuuliza tena kutaka uhakika. “Nitafanya
kwa ajili yako na watoto. Lakini nimeingiwa na hofu Geb. Kama kweli alikuwa
malaika, kwa nini yeye mwenyewe asitoe!?” Nanaa akauliza swali ambalo
lilikuwa ni kweli na maana. “Sijui Nanaa. Ila ninachojua, nataka kufanya.” “Sawa Geb.” Nanaa akakubali.
“Naomba rudisha uso kwenye mto. Tulia tu. Kama
nikigusa, na wewe ukasikia, utaniambia.” “Kama asiposikia, bado utamtoboa?” Nesi
akaingilia tena kwa swali. Geb akamwangalia. “Samahani. Nataka kujua tu.”
“Nitafanya kutokana na imani sio vile atakavyojisikia.” Geb akajibu, na kurudi
kule miguuni. Akapima mara moja na nusu, akaweka kidole. Akabonyeza mara ya
kwanza. “Ni hapa?” Geb akamuuliza Nanaa. “Sisikii
kitu Geb.” Geb akasogeza tena kidole pembeni.
“Hapa?” “Hapana.” “Hapa?”
Geb akagusa tena kwingine. “Sisikii kitu.” Geb
akatulia. Akarudia kupima tena akagundua ni pale alipogusa mara ya kwanza.
Akabonyeza kwa nguvu zote. “Auuuuu!” Nanaa
akalalamika. Geb akaruka. “Umesikia kitu Nanaa!?” “Umenigusa
kwa nguvu! Nimesikia kama sindano.Imenich...”
Nanaa akashituka. “Geb Sindano! Sindano Geb! Sindano!” Nanaa akapiga kelele. Nesi akasogea karibu kushangaa.
Geb alikuwa ameshapapoteza kwa kushituka. Lakini
akarudia tena kupima. Lakini safari hii akarudia kwa ujasiri, akijua ni hakika.
Akaanza kumpima tena. Akafika pale pale. “Ni hapa?” “Bonyeza kwa nguvu Geb.”
Geb akaongeza nguvu. “Sisikii tena.” “Subiri.”
Geb akarudia mpaka akapafikia. “Hapo hapo.”
Geb akakaza moyo. Akaanza kumkata. “Unasikia maumivu?” “Sisikii
kitu kabisa.” Geb akaendelea. Akafika chini kabisa. Akahisi ni kama ule
mguu wa Nanaa umevalishwa limfuko chafu. Akaendelea kukata mpaka chini kabisa.
Ni kweli akakuta kichwa cha sindano kama pini ya ofisini ya kushikilia
karatasi. Akavuta juu. Ikatoka.
“Nanaa!” Geb akaita huku ametoa
macho. Gafla ule mguu ukaanza kupasuka kuanzia juu ya ule uvimbe, mpaka chini.
Maji yakamwagika, ‘pwaa!’ kama maji yaliyomwagwa. Yakatapakaa mpaka sakafuni. “Kuna nini
Geb!?” Nanaa akauliza kwa
mshituko. “Umepasuka! Maji yote yamemwagika! Inauma?” “Hata
kidogo! Sisikii maumivu.” Nanaa akajibu huku akifuta machozi. Geb
akasogea, akamfinya mguu akiwa ameshikwa na mshangao mkubwa usoni.
“Hapo je?” “Hapo
nimesikia.” Geb akaanza kuruka ruka kwa furaha. “Nifanyie
na huo mwingine Geb.” Nesi alikuwa ametoa macho karibu yaanguke. Geb
akafanya kwenye mguu ule mwingine kama alivyofanya mwanzo. Ikawa kama mguu wa
kwanza. Akafanikiwa kupata ile pini, akaivuta. Maji yakamwagika tena. “Naomba
uchukue hatua nyingine ya imani, ugeuke Nanaa.” Nanaa akageuka kwa tahadhari,
huku akilia kwa sauti ya juu. Bado kulikuwa na
ngozi zilizokuwa zikining’inia kwenye miguu yote miwili. Kama matambaa.
Nanaa alikuwa amefunga macho akilia. Wauguzi
wengine wakaja kuangalia kulikoni. Wakabaki wameduaa. Geb alikuwa akijaribu
kutoa yale mangozi yaliyokuwa yamening’inia. “Unaumia?” Geb akauliza. Nanaa
akatingisha kichwa kukataa. Geb akakazana kuyavuta huku akiyatupa sakafuni.
Mwishoe akaamua ayavue kama soksi. Akakwangua kuanzia chini ya goti, taratibu
ili asimuumize, kisha akavuta. Lilianguka ngozi kama la kenge kutoka kwenye
mguu wa kulia wa Nanaa. Geb akapata ujasiri kufanya hivyo hivyo kwenye mguu wa
kushoto. Akavua lile ngozi. Lilikuwa likitisha sana. Akatupa sakafuni.
~~~~~~~~~~~~
Wakati mwingine Mungu huzungumza nasi kwa njia ya
ajabu na tofauti na uelewa wa mwanadamu. Ni rahisi kupuuza na kutotilia
maanani. Hasa unapokutana na vipingamizi vinavyofanana na kweli kama
huyo nesi. Njia za Mungu zipo juu sana. Hazichunguziki kwa akili za
kibinadamu. Bibilia inasema. {1kor 1:25 Kwa maana
upumbavu wa Mungu una hekima zaidi kuliko hekima ya wanadamu, nao udhaifu wa
Mungu una nguvu kuliko nguvu ya wanadamu.}
Wakati mwingine Imani ya mtu mwingine inaweza
kukutoa sehemu moja hadi nyingine. Kukushusha au kukupandisha. Kuwa makini nani
anatembea karibu na wewe. Nani unampa sikio lako! Bibilia inasema {Muhubiri 4:9-11 Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa sababu
wana malipo mazuri kwa kazi yao. Kama mmoja akianguka, mwenzake atamwinua.
Lakini ni jambo la kuhuzunisha kwa mtu yule aangukaye naye hana wa kumwinua!”
Bado Mungu anatenda miujiza. Hajawahi
kuacha. Pengine alishajibu ni wewe kutembea kufikia muujiza wako. Tumekuwa
tukitingwa na mengi nakushindwa kumsikia Mungu au kukubaliana na kile Mungu
anachotujibu kwa kuwa hakileti maana kwenye ufahamu wetu.
~~~~~~~~~~~~
Miguu ya Nanaa ikarudi kuwa kama ya mtoto
mchanga. Laini. Haina hata kipele wala doa! “Sasa
hivi unaweza kufungua macho Nanaa. Mungu amekurejeshea miguu yako.” Geb
mwenyewe hakuwa akiamini zile nguvu alizipata wapi. Akabaki ameduwaa kwa muda
huku machozi yakimtoka kwa hofu ya Mungu iliyokuwa imemkamata. “Nanaa! Fungua macho ushuhudie kile Mungu ametutendea.”
Akaikunja miguu yake na kuinyosha huku akilia. Kisha akafungua macho. Hakuwa
akiamini. Ikabidi yule nesi asimulie manesi wengine kile kilichotokea. Wakaona
na zile pini. Walioweza kuchukua video wakachukua. Lakini Geb akakataa kabisa
Nanaa asichukuliwe video wala asipigwe picha.
“Ninahamu ya kuomba nikiwa nimepiga
magoti, kama wewe Geb.” Geb
akacheka. “Shuka basi kitandani. Nikushike mkono?” Nanaa akatingisha kichwa
kukubali. Geb akaenda kumshika mkono. Akashuka. Akajaribu kutembea, akaweza.
Nanaa alizidi kulia. Hapo hapo akasujudu chini. Alipiga magoti pembeni bila
kujali yale maji machafu pale sakafuni akaendelea kulia huku akimshukuru Mungu.
Geb aliomba wapishwe. Wote wawili walikuwa wakilia kwa furaha.
“Mtataka
nije kutoa catheter?” Nesi akahoji. “Tafadhali.
Halafu nisaidie taulo safi na nguo za kubadilisha. Nataka akaoge. Kisha naomba
utusaidie kusafisha hii sakafu.” “Hizi ngozi nitupe? Au mnataka
niwahifadhie.” Nesi aliendelea kuhoji. “Huo ni uchafu wakutupa tu.” Geb
akajibu. “Na hizi pini? Hamtataka kutunza kumbukumbu?” Nesi alihoji tena. “Sio
mali yetu. Hututahitaji. Ila nitataka nizitupe chooni ili zisije zikatumiwa na
mtu mwingine tena.” Geb akazichukua na kwenda kuzitupia chooni. Aka flush.
Akahakikisha zimeenda ndipo akatoka.
“Njoo Nanaa. Nataka akutoe hiyo catheter ukaoge
vizuri, ukiwa umesimama bafuni. Sio kufutwa ukiwa kitandani.” Geb alimnyanyua
pale sakafuni. Nesi akamchomoa ile catheter na dripu. Geb akamchukua. “Nisaidie
na shuka safi. Nitatandika tu mwenyewe. Nisikusumbue zaidi. Na wewe
ukapumzike.” “Wala usijali kaka yangu. Mimi mwenyewe nimejawa furaha, nahisi
usingizi umetoweka.” Nesi na Geb wakacheka.
Alimsubiria Nanaa akaoga, akamsaidia kumkausha.
Wakatoka wote wakiwa kama wapepigwa na butwaa. “Naomba tuombe wote tena Geb.”
Walikuwa wamekaa kwenye kochi. Wakapiga tena magoti. Wakaanza kuomba. Waliishia
kulia mbele za Mungu. Hofu ya Mungu iliongezeka ndani mwao. Nanaa asiamini kama
amemuona malaika wa Mungu. Na amepokea uponyaji wa namna ile. Magoti
peke yake ikawa haitoshi. Wakainama kabisa kumsujudia Mungu wao kana kwamba
wapo mbele ya kiti cha Enzi cha Mungu. Zilikuwa shukurani zilizojaa Imani
ya ajabu. Iliwachukua dakika 40 kumaliza.
~~~~~~~~~~~~
Wakarudi kukaa. “Unataka kulala kidogo?” Geb
akamuuliza Nanaa. “Nataka kurudi nyumbani.” Geb akaangalia saa. “Ni saa kumi
usiku.” “Sitarudi kulala pale kitandani Geb. Mungu amenitoa hapo. Sitarudi
tena.” “Basi ngoja nikamtafute daktari nizungumze nae.” “Unaniacha!?” Nanaa
akauliza. “Nitarudi baada ya muda mfupi tu.” “Nataka kuwa na wewe Geb.
Usiniache hapa tafadhali.” Geb akamkumbatia kwa muda. “Basi twende wote.”
Wakatoka.
Walizunguka kumtafuta daktari wa zamu. Hata yeye
hakuamini kumuona Nanaa na hali ile. “IMEWEZEKANAJE!?” Akauliza. Geb akasimulia
kwa kifupi. “Kumbe haya mambo ni kweli!” Yule daktari wa kihindi akauliza kwa
mshangao. “Hata sisi ndio mara yetu ya kwanza kushuhudia. Hatukuwahi hata
kushuhudia mtu aliyekuwa na ugonjwa, akipokea uponyaji na sisi tukashuhudia kwa
macho yetu. Ni kitu kipya na kigeni kabisa kwetu. Na wala sisi hatukuwa
tukiishi maisha ya watumishi kanisani. Ni watu wa kawaida tu. Tena..” Geb
akanyamaza. Akataka kusema wenye dhambi. Akakumbuka msamaha wa
dhambi aliopewa na Mungu. “Mungu yupo. Na nguvu zake ni halisi. Hana
upendeleo. Kwa mtu yeyote, wa taifa lolote, anayemcha na kumtii,
hujidhihirisha kwake. Ametuthibitishia hilo mimi na Nanaa.” Geb akamalizia.
Ilibidi daktari awaruhusu tu. Hapakuwa na
sababu ya Nanaa kuendelea kuwepo pale. Kwani tokea awali vipimo vilionyesha ni
mzima. Hana ugonjwa wowote. Ila akamshauri arudi kwa daktari wa wakina mama kwa
ajili ya kliniki. Walishasahau juu ya mtoto. Tangia wafike hapo, Mungu amekuwa
akiwapa yaliyo mema tu. Baraka juu ya baraka. Geb akalipa garama zote. Wakarudi
wodini kukusanya vitu vyote wakiwa wameshikana mkono na Nanaa. Wakawashukuru
manesi, wakaondoka.
Mungu Wa Yasiowezekana Kwa
Wanadamu.
Hapakuwa na maongezi mengi sana kati yao. Ni kama
bado walikuwa kwenye mshituko. Kila mmoja akitafakari lake. Walitembea kimya
kimya mpaka kwenye gari ya Geb huku wameshikana mikono. Geb akamfungulia
mlango. Akamfunga na mkanda. Akasimama pale pembeni yake akimwangalia Nanaa.
Mara Nanaa akamuona machozi yanamtoka. Akatoa mkanda, akamgeukia na
kumkumbatia.
“Sijui maisha mengine tena bila
wewe Nanaa.” Alimsikia
Geb akiongea kifuani kwake. “Mungu amenirudisha tena kwako Geb. Anakusudi na
maisha yetu. Najiuliza kwa nini yule malaika asinitoe yeye zile pini, akanituma
nikwambie wewe ndio utoe?” Geb akatulia kama anayetafakari hilo.
“Si unaona eeh!?Mwenzio ndio swali najiuliza
mpaka sasa hivi.” Nanaa akaongeza. “Umenifanya nifikirie! Sikuwa hata
nimelifikiria hilo.” Geb akajibu. “Panda kwenye gari twende huku tunaongea.
Lakini Geb, naomba nipitishe kwanza kwa kaka.” “Sasa hivi Nanaa!?” “Tafadhali
Geb. Kaka huwa halali vizuri akijua nipo kwenye shida. Na ninajua sasa hivi
ndio kabisa. Kwa hali ile, kuniacha hospitalini! Najua hatakuwa akilala. Naomba
twende akanione ili atulie.”
“Sawa. Hata hivyo anastahili. James
anakuhangaikia sana. Jana usiku ilimlazimu tu kuondoka. Alikuwa akikuangalia
wakati umelala, mpaka machozi yalikuwa yakimtoka. Ilibidi nimtoe. Nikamwambia
sitaki uamke, umkute analia. James anakupenda sana.” “Nafahamu. Mimi ni
kama mtoto wake. Hivi nilivyo, ni kwa ajili yake. Nilikuwa nikiachwa na nepi
chafu kuanzia asubuhi anaponibadilisha wakati anaenda shule, mpaka mchana
anaporudi. Ndio anibadilishe tena na kuniogesha. Ilimbidi kunianzishia uji nikiwa
mchanga kabisa, anasema ilimlazimu ili nisiwe nashinda na njaa wakati yupo
shuleni. Na akirudi, alikuwa akinilisha tena. Amehangaika na mimi kwa muda
mrefu sana. Sijui mapenzi ya mzazi ila kaka.” Waliendelea kuzungumza huku
wakielekea nyumbani kwa James.
“Ungemuhurumia wakati ndio amefika tu pale
shuleni. Tumefika kidato cha kwanza. Unajua tulipangwa cubic au chumba kimoja?
Mimi, yeye, Danny na Zinda. Yeye alikuwa akilala kitanda cha juu yangu. Zinda
juu ya kitanda cha pembeni yetu cha Danny. Alikuwa akitusimulia habari zako
bila kuchoka. Alikuwa na wasiwasi sana na wewe, mpaka akabuni njia ya
kusingizia ugonjwa. Ndio akawa anaweza kurudi nyumbani kukuona. Sisi tukawa na
kazi ya kumsaidia kuandika darasani wakati yeye anakuja kukuona. Hakuwa
akizungumza chochote isipokuwa wewe, Nanaa.” Nanaa akajifuta machozi.
“Umemtaja
Zinda, nimekumbuka. Mambo yaliendaje?” Nanaa akauliza. Geb akatulia kidogo.
“Vipi?” Akauliza tena. “Naomba kwa sasa tufurahie yale Mungu ametutendea kwanza
Nanaa. Mambo mengine tutazungumza wakati mwingine.” Nanaa akajua kuna jambo.
Akaamua anyamaze. Ukimya ukapita. Kila mtu akiwaza lake.
Kwa
James.
Walifika Kijitonyama, alikopangisha nyumba James. Nanaa akashuka kwa haraka. Geb akajua
anataka yeye ndio akagonge mlango. Akatembea nyuma yake taratibu tu. Nyumbani
kwa James hapakuwa na geti. Moja kwa moja wakasogea mpaka mlangoni. Wakaona taa
za sebuleni zinawaka. “Yupo sebuleni.” Nanaa akanong’ona. Kisha akagonga.
Wakamsikia amesimama. Geb akamuhurumia James. Akajua kweli hakuwa amelala. Kwa
kuwa alikuwa akifanya kazi karibu sana na kwake, ule sio muda wa kuamka na
kujiandaa kwenda kazini.
Wakamsikia akifungua ndani, Nanaa akasogea
pembeni kama kujificha. Akabaki amesimama Geb katikati ya mlango. James
akafungua akabaki akimshangaa Geb. “Tafadhali usiniambie kama kuna jambo baya
limempata Nanaa. Nipo kwenye kompyuta yangu usiku kucha natafuta ufumbuzi wa
tatizo lake. Nimepata hospitali mbili nchini Afrika ya kusini. Nataka nikifika
kazini niwapigie simu ili nione kama watanipa appointment ya karibuni,
nimpeleke. Kama umeniletea habari mbaya, naomba
uondoke Geb. Tafadhali sana.” Nanaa alimuhurumia sana kaka yake.
Akajitokeza taratibu.
Alimuona James machozi yakimchirizika.
Alishabadilika rangi kwa hofu mara baada yakumuona Geb mlangoni kwake asubuhi
ile hata kabla hapaja pambazuka. “Kaka!” Nanaa akamuita. James akabaki
amesimama. Akafikicha macho, akayafungua. “Ni mimi kaka. Nimepona.” James
alibaki kimya. Nanaa akamsogelea. Akanyanyua gauni alilokuwa amevaa.
“Ona miguu yangu! Mungu ameniponya muda mfupi
sana uliopita. Hapa ndio tumetoka hospitalini, tukaja kwako moja kwa moja.”
Nanaa aliendelea kujieleza lakini James akabaki ameduaa. Akaweka mikono
kichwani. Akavuta pumzi kama aliyekuwa amekabwa koo. Geb akaingia.
“Naomba ukae James.” Akamshika mkono akamsogeza
mpaka kwenye kochi. Nanaa alianza kulia. Geb akaanza kumueleza mwanzo mpaka
mwisho. Tokea alipoondoka pale wodini, mpaka hapo walipo. James alikuwa akitoa
machozi na kamasi kama mtoto mdogo.
“Mungu ameniponya kaka! Amepigana
vita yangu. Lakini amekataa kabisa kuniambia ni nani aliniwekea zile pini.
Nilijaribu kumuuliza yule malaika. Tena kwa kurudia rudia ili anitajie
aliyeviweka, lakini mpaka anaondoka, hakumtaja.” Nanaa akilalamika.
“Kama Mungu hakutaka umjue
kwa wakati huo, basi ujue ni kwa faida yako Nanaa.” “Kweli kaka?”
“Kabisa. Pokea kile alichokupa. Mengine amejua haupo tayari kuyapokea.” James aliongea kwa
hekima. Geb akamshukuru Mungu kimya kimya. Hakutaka kuanza kutoa habari za Mira
wakati huo. Na kuanza kuleta matatizo kati yake na Nanaa. Wakapata muda
wakutulia wote wawili. Wakajikuta wanacheka.
“Naomba tukapumzike kaka. Geb hajalala.” Geb
akacheka. “Wote hatujalala.” “Ni sawa nikija kukuona jioni?” Nanaa akakunja
uso. “Kwa nini unaniomba ruhusa? Au Geb..” Nanaa akamgeukia Geb kama anayetaka
kuuliza swali. “Unakaribishwa nyumbani muda na wakati wowote ule James.
Huhitaji hata kukaribishwa.” Geb akaongeza kwa haraka. “Ulitaka kunitia
wasiwasi kaka! Nakutegemea na ninakuhitaji sana kwenye maisha yangu, kaka
yangu. Kama Mungu hatabadilisha hii hali, wewe ndio unaweza ukawa ndugu yangu
wa pekee watoto wangu watakao kufahamu.” “Basi nitakuja jioni nikitoka kazini.
Nimefurahi sana. Sijalala usiku kucha nahangaika humo kwenye hiyo kompyuta.
Mpaka nikafikiria nikupeleke Nigeria ukaombewe!” “Pole kaka yangu. Basi
tukuache na wewe ulale hata lisaa. Lakini Mungu ametudhihirishia kuwa yupo
popote pale. Ukimwita, anaitika. Lala kaka. Tutazungumza vizuri
jioni.” James akamsimamisha Nanaa. Akamkumbatia. “Asante Mungu.” Walimsikia
James akishukuru. Wakaagana, wakatoka kuelekea Tabata.
Mungu
Amrudisha Nanaa Nyumbani Kwake Akiwa Anatembea.
Ilikuwa
majira ya saa kumi na mbili kasorobo wakati geti la nyumbani kwa Geb
likifunguliwa na walinzi ili waingie. “Mama anaweza kuanguka kwa mshituko.”
Wakacheka. “Hapo atakuwa anapika ili amtume Danny atuletee chakula
hospitalini.” Nanaa akaongeza na kuzidi kucheka. Wakashuka na kuongozana mpaka
geti dogo la kuingia ndani ya nyumba. Geb akabonyeza kengele.
“Danny! Kamfungulie huyo mlinzi mlango. Sijui
anashida gani? Mimi namalizia hapa jikoni sasa hivi.” Walimsikia mama G
akiongea kwa mbali sababu ya vioo vilivyozungushwa kwenye hiyo nyumba. “Mimi
ndio nipo hapa mama. Danny amerudi chumbani.” Grace akajibu. “Basi wasikilize
ujue wana shida gani.” Wakasikia Grace anafungua milango. Akatoka pale.
“Mamaaaa! Mamaa!” “Nini wewe?” Mama G na Danny
wakatoka wakikimbia. Grace alikuwa akipiga kelele baada ya kumuona Nanaa
amesimama pale. Mama G na Danny walifika pale wakabaki kama sanamu. “Mungu ameniponya
usiku wa saa nane.” Nanaa aliongea na
kujifunua mbele ya taa kubwa iliyokuwa ikimulika hapo mlangoni.
“Oneni.” Akajifunua mpaka juu magotini. Akageuka
nyuma kuwaonyesha. Kwa asili Nanaa hakuwa na miguu minene hata kidogo.
Miembamba na mirefu isiyo na nyama nyingi popote. Lakini ilikuwa mieupe sana
sababu ya kuvaa nguo ndefu wakati wote. Ile miguu ikarudi kuwa kama ya mtoto!
Ngozi safi.
Mama G
akaanza kulia. Alilia huyo mama, mpaka Geb akamtoa pale na kumwingiza ndani.
Badala ya kicheko, pakageuka kilio. Grace na mama G walilia sana. Geb
akawasimulia mwanzo mpaka mwisho. Hofu ya Mungu iliwajaa. Kila mmoja wao mpaka
Danny wakabaki wakitetemeka.
“Umemuona malaika Nanaa!” “Ila nimeshindwa kumtizama
sura mama. Alikuwa akiwaka sana. Mpaka nikadhani ni dokta. Sababu niliona tu
kama amevaa koti jeupe. Nikajua ndoto. Hivi Geb ndiye aliyeniambia ni malaika.
Lakini mama, nilimuhoji sana ili aniambie ni nani amenifanyia ubaya wote
huo lakini hajamtaja kabisa! Aliishia kunipa maelekezo ya nini Geb anifanyie.
Basi. Hakumtaja!” Wote wakanyamaza. Nanaa wala hakuwa akielewa kama
wenzake wanamfahamu.
“Halafu kingine. Najiuliza kwa nini yeye mwenyewe
asinitoe hizo pini akataka Geb ndio azitoe! Tena kwa kurudia rudia kuwa ‘mwambie Geb, afanye hivi’. Halafu huku Geb
akiambiwa kwenye ndoto yake asiogope! Kwa nini Geb!? Tangia nipo
hospitalini najiuliza. Nikasema labda kwa kuwa ndiye aliyekuwa pale! Lakini
roho ikakataa. Nikajiambia labda kwa kuwa Mungu anajua kuwa nampenda
Geb. Lakini pia naona hapana mama. Si Mungu angejifanyia yeye mwenyewe ili
kujipatia utukufu yeye mwenyewe!? Nakumbuka kuna kipindi tulikuwa
tukizungumza mimi na wewe mama. Ukasema Mungu anapenda sana Sifa. Huwa hagawani
utukufu na mwanadamu. Si ni kweli?” “Kabisa. Lakini labda tu alitaka afanye.”
Mama G akajibu. “Hapana mama. Mimi nahisi kipo kitu cha ziada! Moyoni
nashuhudiwa kabisa. Lipo jambo kati ya Mungu na Geb.” Nanaa alikuwa akiongea
kwa utulivu kama akivuta hisia.
“Nashauri Geb aendelee kumuuliza Mungu juu ya
hilo. Mungu amemtumia Geb kufanya jambo la kipekee na gumu sana. Geb
hana elimu ya kidaktari hata kidogo na wala hajawahi kumuombea mtu hata kichwa
tu. Lakini mama, ungemuona vile Geb alivyokuwa amejawa ujasiri! Yaani mimi na
yule nesi tulimkatisha sana tamaa. Nilikuwa nikilia nikimsihi aniache
tu.” “Sababu ya maumivu?” Grace akauliza. “Hapana Grace! Nilikuwa naogopa tu.
Labda sijui niliogopa nisije kukatishwa tamaa kama visingefanya kazi au, sijui!
Lakini alipokuwa kila akinigusa, halafu sisikii kitu, nilikuwa nikimuomba
aniache. Ndipo Geb ikabidi atulie azungumze na mimi kwanza. Tena ni kama alijua.
Akaniambia anaomba kwa wakati ule, nisimamie Imani yake. Yeye atanibeba.” Nanaa
akatulia.
“Mimi mwenyewe sijui ujasiri niliupata wapi! Hata
wazo la kuvua lile ngozi sijui lilitoka wapi!? Nikajikuta navuta lile ngozi
kama namvua Nanaa soksi! Sijui! Ila ninachojua Mungu hutenda kazi na wao
wampendao au wamwaminio.” “Ila huu ugonjwa umenithibitishia kuwa Geb ni
wangu mama.” Kila mtu akacheka. Lakini Nanaa akaanza kulia.
“Nanaaa!” “Kweli
mama. Nilijua Geb ananipenda. Lakini si kwa kiasi hiki! Mungu amejenga kitu
kipya kabisa ndani yangu juu ya Geb. Si upendo tu. Kuna kitu kingine amekiweka
cha tofauti. Bado sijajua, lakini najua moyo wangu Mungu ameugeuza kabisa kwa
Geb, mama.” Nanaa akatulia akijifuta machozi.
“Hata mimi nakubaliana na Nanaa. Geb unampenda
huyu mtoto! Sijawahi kukuona ukiwa hivyo, tokea tunazaliwa. Ulibeba sura
ya tofauti ili kukabiliana na tatizo lililokuwa limempata na halina ufumbuzi
kabisa! Ulimshangaza kila mtu, mpaka James alikuwa akishangaa nakulia peke
yake. Lakini baadaye tukaambiana ni mapenzi ya dhati kwa Nanaa. Utafanya
kila uwezalo kwa huyu mtoto!” Grace akaongeza. Wote wakacheka, mpaka Geb
mwenyewe. Nanaa akamwangalia huku akilia. “Asante
Geb.” Akamshukuru kwa kunong’ona.
“Twende tukapumzike. Hatujalala tokea saa nane
tupo macho! Nanaa najua amechoka. Tutazungumza zaidi baadaye.” “Mle kwanza ndio
mkalale. Msilale bila kula. Hivi ndio nilikuwa nikimalizia kuwapikia.”
“Msipandishe hata juu. Mkae hapo hapo. Napanga chakula sasa hivi.” Mama G akakimbilia jikoni.
“Ngoja nikusaidie mama.” Nanaa akasimama na
kumfuata jikoni kwa haraka. “Wee Nanaa! Hebu nenda kapumzike!” Mama G
akamfukuza pale jikoni. “Usinikataze
mama yangu. Acha tu nifanye. Nilikuwa nikimlilia Mungu anisimamishe tena kwa
ajili ya Geb wangu na wanangu. Amenisaidia, acha nimtumikie tu mpenzi
wangu. Kwa kadiri ya Mungu atakavyonijalia. Nimegundua huu uzima tulio
nao mama si kitu. Unaweza kupokonywa wakati wowote.” Mama G akabaki
akimtizama.
“Usinifukuze mama yangu.” “Haya mwanangu. Uji
wake huo hapo, upo tayari kwenye chupa. Kuna embe kwenye hilo kapu la
hospitalini. Lisafishe tena umuwekee kwenye sinia lake. Na juisi ipo kwenye
friji.” Nanaa akamtayarishia Geb, akamuwekea mezani.
~~~~~~~~~~~~~
“Maziwa yamejaa! Natamani Liv aamke anyonye.”
Nanaa alikuwa akiongea na Geb pale mezani. “Na mwanao huyo kumuamsha ni shuguli
nzito haswa! Akilala amelala.” Mama G akaingilia. “Grace! Wakina kaka
wanaendeleaje?” Grace alikuwa amejiinamia akaanza kucheka. “Anawanywesha uji.
Ndio maana unasikia pametulia.” Mama G akajibu yeye.
“Grace! Si ndio wametimiza miezi mitatu tu!?”
Nanaa akashangaa. “Ndio wametimiza miezi mitatu juzi. Nilichoka Nanaa. Mimi
kelele nyingi vile siziwezi. Nilihisi nitachanganyikiwa.” Nanaa akaanza
kucheka. Akakumbuka vile Grace alivyokuwa akilia wakati wanae wanapokezana
kulia.
“Kwa hiyo
umeacha kuwanyonyesha?” “Niringe?
Wananyonya kama sijui nini vile, na uji pia wanakunywa. Hapa niliamka mapema,
angalau kupata muda na mume wangu kabla hajaenda kazini. Wakiamka nianze
kuhangaika nao. Mpaka saa tatu ninakuwa nimewajaza matumbo yao uji. Hawawezi
hata kulia! Ndio hata nikimuachia hapo mama na maziwa nikienda kazini masaa
mawili, nakuta bado wamelala.” Nanaa akazidi kucheka. “Grace!” “Ningekufa
nikawaacha Nanaa. Heri hivyo.” Grace akaongeza. Geb alikuwa akimwangalia tu
dada yake huku akila.
“Njoo basi ule kabla hawajaamka.” “Na kweli.”
Grace akahamia mezani. “Danny amepigwa na butwaa. Njoo mume wangu ule ndio
uende kazini.” “Namshangaa Mungu!” Danny akasimama na yeye akahamia mezani.
Walikaa pale wakila.
“Zinda..” Nanaa akataka kuuliza. Akamwangalia
Geb, akaona anyamaze tu. Alipoona wote wanaangaliana, akajua kuna
kinachoendelea. “Geb amesema niache habari nyingine. Nipumzike kwanza. Lakini
nilitaka kujua mambo ya Zinda yaliendaje!” “Nanaa!” “Basi Geb. Tutazungumza
tukiamka. Au hata jioni.” Geb akanyamaza. “Si sawa?” “Jioni.” Geb akajibu,
wengine wote wakanyamaza. Nanaa akajua lipo jambo tu ndio maana wengine
hawachangii isivyo kawaida yao.
Alipomaliza kula akaenda chumbani kwa mama G moja
kwa moja kitandani kwa mtoto wake. Akamkuta Oliva amelala hana hata habari.
“Huyu binti Magesa kwa kupenda usingizi! Sasa hapo sijui ataamka saa ngapi?”
Akabaki akijiuliza huku akimwangalia mwanae. Akambusu.
“Huyo mwanao ni wakumuamsha kwa nguvu. Usipomgusa
hapo mpaka saa sita. Nitamuasha kwenye saa mbili. Aoge ndio ale.” “Hakusumbui
kula?” Nanaa akatoka, akamuuliza bibi yake. “Hivyo hivyo. Ana kazi ya kucheka
tu. Tena Fili asiwepo. Akiwepo Fili anataka wacheze. Fili anamtekenya, basi
atacheka hapo wee. Mdomo hautafungwa tena. Na Fili akiondoka analia.” Nanaa
akacheka. “Liv kwa kucheka! Kila kitu yeye kucheka! Na akicheka chakula hakikai
tena mdomoni! Chote kinatoka. Itabidi afundishwe kutabasamu.” Nanaa alifanya
wacheke.
“Nimechoka Nanaa!” Geb akalalamika kidogo.
Akimaanisha wakalale. “Twende basi ukalale.” Akamsogelea Geb na kumsugua kidogo
mgongoni. “Pole.” Geb akamgeukia, akampa tabasamu. “Mama! Asante kwa chakula.”
Geb akasimama, akamkumbatia Nanaa na kumbusu. “Karibu tena nyumbani.” Aliongea
huku akimwangalia Nanaa machoni. “Asante. Nina hamu na wewe Geb!” Nanaa
aliongea sauti ya chini ya kudeka. “Hata mimi.” Pale pale Geb akainama na
kuanza kunyonya midomo ya Nanaa. “Basi hapo tena kazi imeanza!” Mama G
akafanya waanze kucheka. Geb akamnyanyua Nanaa. Akambeba na kupanda naye juu,
kurudi chumbani kwao.
~~~~~~~~~~~
Japokuwa walikuwa na hamu ya kufanya mapenzi.
Kila mmoja alikuwa na uchu na mwenzake, lakini walipofika tu
chumbani, Geb alimuweka Nanaa chini, wakapiga magoti pembeni ya kitanda chao,
wakaanza kuomba. Walimshukuru Mungu kwa kuwarudisha nyumbani salama. Wakaomba
ulinzi wa Mungu juu yao, watoto wao na familia yote kwa jumla. Wakamaliza,
ndipo wakakumbukana sasa.
Walipata wakati mzuri sana hapo kitandani. Kwa
kuwa walikuwa wamechoka, hayakuwa mapenzi ya muda mrefu. Wakaamua kulala. Nanaa
alilala kifuani kwa Geb akiwa amemkumbatia. Alinyanyua uso wake, akambusu mara
kadhaa. “Asante kwa kunipenda Geb.” Geb akiwa na usingizi. Alirudisha
busu, hapo hapo akalala.
~~~~~~~~~~~
Waliamka jioni kwenye saa kumi, nyumba ilikuwa
imetulia sana, kama hakuna mtu. Nanaa akatoka, akaenda chumbani kwa mama G.
Alimkuta Grace na mama yake wamejilaza kitandani. “Mmelala?” Nanaa akauliza.
Akakaa pembeni yao. “Tumepumzika tu, tunaongea. Oliva amerudi kulala muda sio
mrefu.” Grace akajibu. “Nina hamu naye! Maziwa yamejaa mpaka yanauma.” “Labda
ukakamue.” “Natamani anyonye.” “Sasa utanyonyesha mpaka ujifungue?” Nanaa
akacheka. “Nilishasahau kama ni mjamzito!” Nanaa akajishika tumbo.
“Geb kafurahi huyo!” Nanaa akaongea huku
akijiangalia. “Mwenzio anapenda kweli watoto. Usipoangalia, atakuzalisha mchana
na usiku.” Grace alimfanya Nanaa acheke sana. “Hata mimi napenda watoto wengi.”
“Basi hapo mmekutana.” Wakaendelea kuongea wakiwa huko chumbani.
“Nanaa!” Wakamsikia Geb akiita. Nanaa akatoka.
“Utataka kula kitu chochote?” “Nataka kukimbia ofisini mara moja.” Nanaa
akanyamaza. “Sitakawia. Naenda kuangalia mara moja, nitarudi.” Grace akatoka.
“Nimerudi sasa hivi. Nilikuwa huko. Kila kitu kipo sawa Geb. Leo pumzika.” “Una
uhakika? Sitaki usumbuke. Kwa kuwa sasa hivi mimi nipo, nataka urudishe akili
kwa watoto.” “Hayo madume ya Danny hayana neno. Wewe leo pumzika. Kesho asubuhi
ndio uende mwenyewe.” “Mama yuko wapi?” Geb akauliza. “Nipo huku.” Geb akaingia
chumbani kwa mama yake.
“Mzima?” “Nimejinyoosha tu.” “Pole. Najua
unachoka sana.” “Wala. Kama hivi nimelala. Hamna hata ninachofanya!” Geb akakaa
pembeni yake. “Nakushukuru mama.” Mama G akatabasamu. “Asante mama yangu.
Asante sana. Bila wewe naona humu ndani wote tungekuwa tumechanganyikiwa!”
“Namshukuru Mungu kuwa na nyinyi Geb. Uzima huu nilio nao, kama alivyosema
Nanaa, ni wakutumia kwa kadiri tuwezavyo. Kwa hiyo hata mimi ninafurahi kuweza
kuwa msaada.” “Sasa na wewe mambo yako?” Mama G akanyamaza.
“Kwa kuwa Nanaa amerudi, labda kesho uende
ukaangalie kidogo.” “Nitafanya hivyo. Ni muhimu. Akiamka tu huyo dada,
nikishamlisha. Nitatoka mara moja. Nikaangalie biashara inakwendaje. Naamini
Mungu atakuwa amenilindia. Nilikuwa nazungumza na wafanyakazi wangu kila siku.
Hawakuwa wakinipa taarifa mbaya. Ila kuna umuhimu wakwenda kutupia macho.” Geb
na mama yake waliendelea kuzungumza. Nanaa na Grace wakiwa wameenda kukaa
kwenye makochi na wenyewe wanaongea.
~~~~~~~~~~~
Ilipofika saa 11:30 jioni, James akaingia.
“Kaka!” Nanaa akasimama. “Tuone tena hiyo miguu! Maana nilikuwa nahisi naota
siku nzima.” Nanaa akacheka. Akamuonyesha kaka yake. “Imerudi kuwa kama ya
mtoto mchanga!” James akasifia. Mama G, na Geb wakatoka. “Karibu James
mwanangu.” “Asante mama. Za hapa?” “Bado tupo na mshituko wa uponyaji wa
Nanaa!” Wote wakakaa. Geb akaenda kukaa pembeni ya Nanaa. Nanaa akajiegemeza
kwake kidogo, akamvuta na mkono. Danny na Fili nao wakaingia.
“Mbona
huyo macho yamezidi kuingia ndani? Njoo baba.” Grace alilalamika. Fili akaenda
kwa mama yake. “Danny umemfanyaje mwanangu?” Danny akacheka na kutingisha
kichwa. “Maana wewe nakujua. Ukute hapo Fili alikuwa ametulia kwenye gari njia
nzima. Hata hakuimba! Eti Fili mwanangu?” Wakacheka. Fili alikuwa mnyonge.
“Hajala huyo. Mwalimu wake kaniambia tokea asubuhi hajaingiza kitu mdomoni.
Mimi mwenyewe leo mpaka nimemuomba aniimbie huko njiani. Hataki kuongea
mwanao.” Grace akamshika tumbo.
“Eti Fili. Tumbo linauma?” Fili akakubali. “Wewe
Fili? Sijakuuliza mimi njia nzima, ukaninyamazia? Yaani mama yako kakuuliza
kidogo tu, tena hata hajakubembeleza kama mimi, umemwambia!?” “Mwache mwanangu.
Linauma wapi?” Fili akajionyeshea tumbo zima.
“Labda ana gesi. Ngoja nimletee vidonge vya gesi.
Labda litatulia. Si hana homa?” Geb akamuuliza Grace. “Wabaridii.” Geb
akasimama. Akamletea vidonge vya kutoa gesi. Mama yake akampakata vizuri. “Pole
na kazi.” Grace akamgeukia mumewe. “Asante. Naona kimya. Umewapa ugali nini?”
Wakacheka. Danny akakaa. “Niwaletee basi kitu mle.” Mama G akasimama. Nanaa
akafuata nyuma.
“Kwani leo tutakula nini usiku?” “Nilipika
chakula kingi mchana. Tutakula hicho hicho. Wabebee hilo jagi la juisi kutoka
kwenye friji. Weka glasi za kutosha. Ili kila atakayetaka ajimiminie. Sio
tupate kazi ya kusimama kila wakati kufuata glasi.” Nanaa akafanya kama
alivyoagizwa. Akatoka na sinia kubwa lenye jagi ya juisi na glasi. Akaweka kati
kati yao. Kwenye meza kubwa ya hapo sebuleni walipokuwa wamekaa watu wote.
Akamimina kwenye glasi, akawagawia.
“Naenda kumpashia moto chakula, Geb. Kuna
mwingine atataka kula? Naweza kuwaletea hapo hapo.” Nanaa akauliza. “Mimi
naomba supu yangu Nanaa.” Grace akaagiza. “Kama kuna chakula kingi, na mimi
naomba. Sijala leo.” James naye akaongeza. “Sawa kaka.” “Na mimi.” Danny
akaongeza na yeye. “Mimi naona pasha chakula chote, uweke mezani. Watu
wajipakulie wale.” Nanaa akacheka. “Na kweli.” Akarudi jikoni.
Kila
Mwanadamu Mungu Humpa Mlango Wa Kutokea.
“Naombeni
niwashukuru nyinyi wote kwa kuwa pamoja na Nanaa, wakati anaumwa.” James
alivunja ukimya. “Nanaa ni jukumu letu pia James.” Mama G akajibu, James
akacheka kidogo. “Nahisi itanichukua muda kidogo kuniingia hiyo akilini.
Nimemlea Nanaa kwa shida sana, huku nikiona watu wakimuona mzigo.
Hata baba yangu mzazi nilimsikia akikataa katakata kujihusisha naye.”
“Nakumbuka baba alitaka atolewe pale nyumbani.
Mama akaanza kuzunguka naye kama mzigo akitafuta sehemu ya kumtua huku
akilalamika sana. Alizunguka naye kila mahali na kote walikuwa wakimkataa
Nanaa. Nakumbuka mama alirudi naye akiwa amekasirika sana baada hata ya kituo
cha yatima nao kumkataa. Akamuweka kwenye kochi Nanaa alikuwa akilia sana. Mama
akasema hajui atafanya naye nini huyo mtoto. Nakumbuka nikajisogeza mpaka pale
sebuleni alipokuwa amekaa baba na mama, nikawaambia mimi nitamlea Nanaa.
Hawakuamini. Wakajua ni akili za kitoto tu.” James akafikiria kidogo.
“Nikamnyanyua pale kwenye kochi, kwa kuwa
alikuwa akilia mpaka akageuka kuwa mwekundu kabisa. Nilijua kuwa ni njaa.”
James akacheka kidogo. “Nikamuwekea mdomoni, kidole changu hiki kidogo, akaanza
kukinyonya. Alikuwa ananuka mikojo. Nepi imejaa! Nikaenda kumchukulia moja ya
nepi za Viola, nikamwagia maji ya baridi tu. Wala sikuyapasha moto. Nikamkausha
na kumvalisha ile nepi.”
“Nikaenda kumchukulia maziwa ya mbuzi. Pale
nyumbani kulikuwa na ng’ombe na mbuzi. Baba hakuwa akitaka maziwa ya ng’ombe
yaguswe. Sikutaka kesi na mtu. Nikaenda bandani, nikamuomba aliyekuwa akikamua.
Tena alikuwa msichana wa kazi. Akaniwekea kwenye kikombe. Nikaenda kuyapasha
moto. Sidhani hata kama yalichemka vizuri. Nikarudisha kwenye kikombe,
nikampakata Nanaa, nikaanza kumnywesha na kijiko, mpaka akamaliza. Baba na mama
walikuwa wakiniangalia tu.” Kila mtu alikuwa akimsikiliza James.
“Basi. Kuanzia hapo, nikaanza kuhangaika
na Nanaa. Sikumbuki kumpeleka kliniki kwa chanjo yeyote ile wala kuangaliwa
afya yake. Na sikumbuki kumuona anaumwa hata jino. Hakuwahi kunisumbua katika
kukua kwake. Maisha yangu yakabadilika sana. Ilikuwa shule, na Nanaa tu.
Niliachana na marafiki wote. Nikawa na kazi ya kuwa na Nanaa.”
“Nguo au nepi zake nilikuwa nikimkusanyia kutoka
kwenye nguo za Viola. Kama nikiona mama amenunua nguo mpya kwa ajili ya Viola,
namuomba za zamani, namvalisha Nanaa. Basi na yeye akawa ananijua. Hata kama
yupo sebuleni, akisikia tu sauti yangu nimerudi kutoka shuleni. Labda nipo
jikoni, atatambaa kuifuata hiyo sauti mpaka anikute.” James akatulia.
“Kwa nini nimesema yote hayo. Nataka kusema hivi,
sijawahi kuona mtu anamtaka Nanaa kwenye maisha yake yote. Hata
marafiki wa kike wamekuwa wakimsaliti Nanaa. Mpaka majuzi aliponipigia
simu asubuhi amevimba miguu, nikakimbia kumbeba na kumkimbiza hospitalini.
Hakika sikujua kwa hakika kama..” Wakamuona anafuta machozi akanyamaza kidogo.
“Sikutegemea kabisa! Geb
aliponipigia simu nikiwa njiani, alikuwa mkali kidogo kwangu. Lakini asijue ile
ilikuwa faraja. Geb
aliniambia lazima nimtambue na kuheshimu kuwa sasa hivi Nanaa ni jukumu
lake. Zilikuwa ni habari ambazo sikuwahi kuzitegemea kuzisikia maishani.
Au kama ningekuja kusikia, nilidhani nikipindi Nanaa akiwa mzima. Sio akiwa na
miguu ya namna ile! Hata kidogo. Halafu Geb alisema
yupo njiani anatufuata! Lakini bado upande
mwingine sikuamini.” James akajaribu kufuta machozi ili atulie.
“Nilimfikisha Nanaa hospitalini, tukawa tumekaa
naye. Nilikuwa nimeingiwa na hofu, nikijua tumebaki tena wawili. Lakini
Geb akaingia. Kuanzia jinsi alipoingia pale mpaka leo asubuhi anamleta pale
nyumbani, nimesadiki kweli Nanaa ni jukumu ambalo Mungu anaanza kulitoa
kwangu.” “Sio ameanza James. Nanaa ni mke wangu MIMI.
Narudia, na naomba ukubali tu. Nanaa ni jukumu langu mimi.” Wakacheka
kidogo.
“Nakusikia Geb. Na namshukuru Mungu kwa
hilo, ila najua itanichukua muda kuingia akilini.” “Naelewa. Na wala sio kwamba
nakufukuza kwenye maisha ya Nanaa! Hapana. Anakuhitaji sana tu kwenye maisha
yake. Ninachotaka ukijue tu, ni kuwa haupo tena peke yako. Na mimi nipo na wewe
James.” James akavuta pumzi na kucheka kidogo.
“Kwa kweli hilo umelithibitisha kwa
vitendo Geb! Na usifikiri ni kwa ile pesa uliyomlipa mwanzoni mama! Hata
kidogo. Ile wala haikuwa imeniingia akilini. Kwani milioni 30 kwa Geb ni nini
bwana?” Wakacheka kidogo.
“Usinielewe vibaya Geb. Ni pesa nyingi sana.
Lakini najua unayo pesa. Na iliniuma. Lakini si kama ile milioni 20
uliyomlipa tena mama, kwa ajili ya Nanaa aliyekuwa ameharibika miguu!
Unailipa, halafu huku madaktari wanakwambia hawajui jinsi ya kumtibu!
Hapana! Nililia usiku kucha nisiamini kama umefanya hivyo Geb! Danny anakuuliza
juu ya harusi, unasema harusi bado ipo! Ulizidi kunichanganya. Nikasema labda
umechanganyikiwa.” Geb akacheka.
“Kweli kabisa Geb, muulize mama. Nilimpigia simu
usiku wa saa sita. Nilikuwa nikilia kama mtoto mdogo, namuuliza iweje kesho Geb
arudiwe na akili yake, halafu aje adai pesa yake, halafu amkimbie Nanaa pale
hospitalini?” “Haiwezekani James!!” Geb alishangaa sana.
“Muulize mama huyo. Alikesha kwenye simu
akinituliz…” James akanyamaza mara baada ya kumsikia Oliva anaongea kwenye
kitanda chake. Aliongea kwa sauti. Bibi yake aliacha mlango wazi ili kumsikia.
Chumba chake na bibi yake hakikuwa mbali na hapo sebuleni.
Geb akataka kusimama. “Sasa wewe usiende.
Hatanyonya huyo. Mwache sasa hivi ananjaa, mama yake aende akamnyonyeshe.” Mama
G akamzuia Geb. “Ninahamu naye kweli!” “Na yeye atakuwa na hamu na wewe.
Ukimuweka hapo kifuani, hatakubali kutoka tena. Mwache Nanaa aende kwanza.
Nanaa!” Mama G akaita. “Nimemsikia mama. Nakwenda
sasa hivi. Namalizia kuweka chakula mezani.” Nanaa alikuwa akilia.
Alikuwa akiwasikiliza mazungumzo yote.
Geb alipomsikia sauti yake ya kilio, akasimama.
Akamfuata jikoni. “Njoo!” Nanaa akamsogelea. Geb akamkumbatia pale pale jikoni.
Nanaa alilia kwa uchungu sana. Geb akamtuliza, akatulia. Akaanza kumbusu.
“Mtoto anawaita huko chumbani. Wewe Nanaa?” Nanaa akacheka. “Naenda mama.”
Kimya. Mama G akajua wamerudi kupeana mabusu. “Basi hapo mtoto mpaka aanze
kulia, wakati mwenyewe si mlizi!” “Naenda sasa hivi mama yangu. Geb! Niwekee
hivyo vyakula vyote kwenye hiyo meza kubwa
ya huko nje sehemu ya kulia chakula. Kila kitu kama kilivyo.” “Sawa.” Geb
alianza kuhamisha. Nanaa akaenda kunyonyesha.
~~~~~~~~~~~
“Jamani
Nanaa amenipa kazi, nimemaliza. Naombeni tuhamie mezani.” Geb aliwakaribisha.
Fili alishakuwa amelala. Geb akaenda kumchukua. “Ngoja nikammwagie maji mara
moja, aje kula. Wewe nenda kaanze kula Grace.” “Asante. Maana njaa ilishaanza
kuuma.” Grace akamshukuru kaka yake. “Fili! Fili!” Geb akamuita wakati
amembeba. Akafungua macho wakati Geb anampeleka chumbani kwa wazazi wake kumvua
nguo. “Vipi, tumbo limetulia?” Walimsikia Geb akizungumza naye.
Hata dakika 15 hazikuisha, Geb akarudi naye akiwa
ameshamvalisha nguo za kulalia. Lakini anatembea mwenyewe. “Njaa inauma?” Geb
akamuuliza. “Kidogo tu.” Fili akajibu. “Njoo uje ule mwanangu. Naona
umechangamka.” Grace akamuita mwanae. Fili akaenda.
“Shikamoo anko.” Akamsalimia James. “Marahaba
Fili. Za shule?” “Nzuri. Nimepata zote kwenye hesabu.” Fili akajisifia.
“Kumekucha!” Danny akadakia, wakacheka kidogo. “Safi sana. Lazima nikupe
zawadi.” James akamwambia. “Asante anko. Lakini usifikiri nimekosa hata moja?
Nimepata zote. Na sijaigilizia. Halafu nakumbuka mpaka sasa hivi.
Nilimuomba mwalimu niwafundishe pale ubaoni.” “Sasa kazi watakuwa
nayo huko shuleni.” Mama yake akaongea kwa sauti ya chini. Kila mmoja akatamani kucheka, lakini wakajizuia.
“Sasa mwalimu alikuruhusu?” James akauliza.
“Mwanzoni alikataa. Ndio nikamwambia kama hataki basi mimi naondoka, narudi kwa
mama yangu. Nikamwambia ampigie simu mama yangu aje anifuate. Akasema mama
atakuwa kazini. Nikamwambia mama yangu yupo nyumbani na wadogo zangu. Na mimi
najua hesabu zote, anipe chaki niwafundishe. Akakataa. Sasa kuna mtoto mwingine
yeye anapenda tu kulia. Kila mama yake akimshusha pale shuleni, analia tu.
Nikajua atakuwa hajui hesabu. Ndio nikamwambia mwalimu basi nimfundishe yeye,
pia akakataa. Ndio ikabidi ninyamaze.” “Ndio maana ukakataa kula?” Mama yake
akamuuliza taratibu tu.
“Kwani
nilimwambia nataka kufundisha sana? Si kidogo tu! Sasa baadaye akaniambia
nisome. Na mimi nikamkatalia. Nikamwambia najua sana kusoma, lakini na
mimi sitaki kama yeye alivyonikatalia kufundisha hesabu. Nikawa nimekaa
tu kwenye kiti changu.” Hapo kila mtu alianza kucheka. Mpaka Nanaa aliyekuwa akinyonyesha
ndani alisikika akicheka.
“Wewe Fili!” Grace akashangaa sana. “Nilimkatalia
mama. Halafu kila nikinyoosha mkono nijibu swali, hanichagui mimi. Nikaamua
kusimama niongee. Nikamuuliza mbona hanichagui tena? Akasema nimeshajibu sana,
niwape nafasi na wengine. Nikamuuliza mbona sasa hawanyoshi mkono kama mimi?
Hapo hapo nikamjibia mwalimu nikamwambia akiona hawanyooshi mkono, ajue hawajui.
Mimi najua, anichague. Akakataa.” Geb alikuwa akimwangalia Fili huku akitingisha
kichwa.
“Kazi watakuwa nayo huko! Watajuta kumpokea
huyo.” “Na mwanao alivyo na hoja! Kama mwanasheria!” Mama G aliongea huku akicheka
sana. “Sasa kama yeye alinikatalia, kwa nini atake nisome kwa sauti?
Nikamwambia achague mtu mwingine. Mimi sitaki tena.” “We Fili! Hebu njoo
kwanza.” Geb akamuita. Fili akaenda mpaka alipokuwa amekaa anko wake.
“Nisikilize halafu usiongee mpaka nimalize.
Sawa?” Geb akamuuliza. “Hata kama nataka kuchangia?” “Hapana. Mpaka nikuruhusu
kuongea ndio uongee.” “Sawa. Nitanyoosha mkono na unichague.” Kila mtu alikuwa
akicheka. Akanyoosha mkono. “Hapana Fili. Bado sijaanza hata kuongea, na wewe
unataka kuongea! Utasikiliza saa ngapi?” Fili aliendelea kunyoosha mkono bila
kumjibu. Mpaka Geb mwenyewe akacheka. “Haya ongea.” Geb akamruhusu.
“Kesho nataka kwenda na mama shule. Ili amwambie
yule mwalimu aniruhusu kujibu maswali na kufundisha kidogo. Haya sasa hivi
nanyamaza. Na wewe ongea.” Fili akatulia kumpa nafasi anko wake azungumze
naye.
“Cha kwanza ujue unakwenda shule kufundishwa.”
“Anayofundisha mimi nayajua.” Fili akamwingilia. “Nilikwambia nini? Nikiongea,
wewe unanyamaza.” Akatulia. “Na sio kwamba unaenda kufundishwa kusoma tu na
kuandika! Tumekupeleka shule pia ukajifunze kuwa msikivu, heshima, upendo,
utii, vyote hivyo kwa walimu na wenzako. Unatakiwa kujua kuthamini na wengine.
Sio wewe tu.”
“Unaweza kujua kusoma na kuandika, lakini hivyo
vingine inabidi kujifunza pia. Na uelewe. Mwalimu akikwambia kitu, unatakiwa umtii.
Umsikilize kwanza. Acha kujibizana. Hata kama akikwambia unyamaze
wakati wewe unataka kuongea, nyamaza. Hapo ujue unafundishwa kuwa mtoto mtiifu.”
“Akisema uwape nafasi wenzio na wao wajibu, sio
kwamba hakupendi wewe? Anakupenda, lakini ujue kuna watoto wengine wanajifunza
taratibu, wanatakiwa kupewa nafasi wajifunze pia. Ukiwa unanyoosha mkono wewe
tu, halafu unajibu kila wakati, utawanyima wenzio nafasi yakujifunza.”
“Yule mtoto anayemlilia mama yake, unatakiwa
kusaidia kumtuliza na kumuonyesha shuleni ni sehemu nzuri. Mfariji. Mwambie
atulie, atamuona mama yake baadaye. Wakati wakucheza, usimuache peke yake.
Cheza naye ili asiwe mpweke. Umeelewa?” “Hapo nimeelewa anko.” Fili
akakubaliana naye.
“Safi sana. Kwa hiyo kesho ukienda lazima
umuonyeshe mwalimu wewe unaakili kuliko watoto wote. Uwe unanyoosha tu mkono.
Usipochaguliwa, usiongee mpaka akuchague. Akikwambia ufanye kitu chochote,
unafanya. Tena unafanya vizuri sana kuliko kila mtu. Halafu unatulia
kwenye kiti chako. Hakuna kuongea hata na mtu wa pembeni yako mpaka mwalimu
awaruhusu wote kuongea. Kucheza na kuruka, ni nje ya darasani. Sio kupanda juu
ya meza na kuruka darasani. Umesikia?” “Siruki tena kwenye meza anko.” Fili
akajibu kwa utulivu.
“Sasa hapo ndio utakuwa mtoto mzuri na mwenye
akili kuliko wote. Haya kaa sasa hivi, ule chakula chako hapo mezani
mpaka umalize. Halafu uchukue sahani yako urudishe jikoni.” “Bibi Fili
hatanilisha?” Fili akauliza kwa upole. “Hapana. Wewe una akili sana Fili.
Inabidi uonyeshe watu wote kama wewe una akili kwa kuanza kujitegemea
mwenyewe.” Wakamuona anacheka.
“Basi kuanzia leo nitakuwa nakula mwenyewe na
kuwalisha na wadogo zangu. Nitawapa wali, ugali na..” Grace akashituka. “Mimi
naona uanze tu kwanza wewe mwenyewe. Watoto mimi nitawalisha.” Grace akadakia
kwa haraka sana. Watu wakaanza kucheka.
“Naweza mama. Mimi nina akili.” “Kweli wewe
unaakili mwanangu. Lakini naomba watoto niwalishe tu mimi.” “Kwani..” Fili
akataka kubisha, Geb akamuwahi. “Nimekwambia nini juu ya kusikiliza na kutii?
Hamna kumbishia mama. Mama anajua zaidi yako Fili.” “Sawa mama. Nitaanza kwa
kula mimi mwenyewe. Si baadaye utaniruhusu kuwalisha wadogo zangu?” Grace
akanyamaza kidogo kama anayefikiria. Alijua vile Fili alivyo mtundu.
“Cha kwanza, usiwalishe kitu chochote watoto
mpaka umuulize mama au bibi Fili au Nanaa. Wakikuruhusu ndio uwalishe.
Umenielewa?” Geb akamuuliza, akijua hofu ya Grace. “Hata kama nimeachwa na
watoto peke yetu? Labda nimeingia chumbani nikakuta wanalia je? Si naweza
kuwalisha?” Fili akauliza kwa makini. “Uwiii!” Grace alisikika. Watu wakazidi
kucheka.
“Kimbia uje uulize kwanza kabla hujawalisha kitu
chochote.” “Hata Oliva? Maana Oliva yeye ni mkubwa kidogo.” Fili alisisitiza.
“Sasa hapo unamtaka anko wako maneno.” Baba yake akaingilia. Geb akacheka.
“Hata Oliva usimlishe mpaka uulize.” Geb akamjibu.
“Lakini Liv anapenda sana pipi.” “Fili wewe
jamani! Huwa unamlisha Liv pipi!?” Mama yake akashituka sana. “Namlambisha tu.”
Kila mtu alikuwa akicheka. “Basi ndio maana Liv anampenda Fili! Akimuona tu,
anamuita. Kumbe huwa anampa pipi!” Mama G aliongeza
“Nimeelewa anko. Nijilishe tu mimi mwenyewe.
Halafu nikitaka kuwalisha watoto hata pipi ni... “ “Usimpe mtoto yeyote yule
pipi.” Geb alisisitiza wengine walikuwa wakicheka sana. “Hata nikiwa nazo
mbili?” Fili akauliza tena. “Nimekwambia nini juu ya kuuliza kwanza?” Geb
akaumuuliza. “Basi anko. Nimeelewa. Umesema niulize kwanza kabla sijampa mtoto
kitu chochote.” “Safi sana. Hakuna
kuweka kitu chochote mdomoni kwa watoto, mpaka uulize.” “Sawa.” Akakubali.
Akakaa mama yake akamuwekea chakula
kwenye sahani, akaanza kula taratibu. “Sijui wale wawili wao wamelishwa nini
jamani! Naogopa hata kuuliza.” Grace aliongea kwa sauti ya chini. Kila mtu
alikuwa akicheka. “Ngoja mimi niulize.” Mama G akajitolea. “Hivi sijui kina
Fillius wao wanapendaga nini? Ili wakilia niwe nawapa.” Mama G akajidai
kujiuliza kwa sauti. “Walambishe sukari bibi. Ukiwapa
sukari wananyamaza.” “Mungu wangu!!!” Grace aliweka mikono kichwani. Kila mtu
alikuwa akicheka. Mpaka Nanaa akatoka.
“Fili Fili! Kwani huwa unawapa sukari?” Nanaa
akauliza. “Mama akiwa bafuni anaoga, halafu wakilia, nawapa kidogo kidogo.
Hawalii tena. Wanakuwa wanajilamba tu.” “Fili wewe jamani!” “Inasaidia mama. Si
unaona siku hizi hawalii sana?” Fili akajitetea. Bibi yake ndio alikuwa akifuta
machozi kwa kucheka. Mpaka Geb naye alishindwa kujizuia. James na yeye alikuwa
akicheka sana. “Filiiiii!” James aliita akicheka sana. Danny alibaki akimtizama
Fili. “Huyu mtoto ahame kabisa humu ndani.” Mwishoe Danny akaongeza. Hapo
ikabidi bibi yake azungumze naye mpaka akaelewa.
~~~~~~~~~~~
Oliva alipomuona tu baba yake akaanza kunyoosha
mikono. “Nina hamu na wewe Liv mwanangu! Njoo mama.” Geb akamuweka kifuani kama
kawaida yake. Oliva naye akazungusha vimikono vyake kwenye shingo ya baba yake,
akatulia kama anayesubiria kitu. “Mmmmmmmmhhhh!”
Geb alisikika akisikilizia raha ya moyoni huku amemkumbatia mwanae na kufunga
macho. Oliva aliposikia baba yake amemaliza, akajitoa shingoni akamwangalia
huku anacheka.
“Hapo anasubiri mabusu ya baba yake.” Nanaa
alikuwa akiwaangalia. “Baba yake ameshamzoesha. Mpaka ameshajua kinachofuata ni
nini.” Mama G akaongeza. Wote walibaki wakiwatizama. Geb akaanza kumbusu
mfululizo. Oliva alisikika akicheka sana. “Muone anavyofurahia!” Nanaa
akaongeza. “Kazi yake ndio hiyo tu, kucheka.” Bibi yake akaongeza.
Wakakaa hapo na kula kwa pamoja mpaka walipo
maliza. “Kama umemaliza kula Nanaa, naomba tuzungumze.” James alimtaka dada
yake waongee. “Ngoja nimalizie kusafisha hapa mezani.” Nanaa akamaliza.
Wakahamia kwenye makochi, wakati wengine wapo bado mezani wakiongea.
Nanaa Na Kaka Yake.
Nanaa akakaa. Akamuona kaka yake ametulia. “Kuna
nini kaka?” “Nataka uniambie, kwa nini mwaka jana, hukuwa ukitaka tuonane?”
James akauliza. Nanaa akakunja uso. “Mbona nilikwambia kaka? Huniamini?” Nanaa
akauliza. “Hapana. Nataka urudie tena. Na safari hii kwa kina.” Nanaa
akafikiria kidogo. “Unakumbuka baada ya kutoka hospitalini baada ya kufanyiwa
ule upasuaji, na kupata nguvu kidogo, ulikuwa unanifuata kila siku za jumamosi
au jumapili tunakwenda kula nje pamoja?” Nanaa akauliza.
“Nakumbuka, lakini baadaye ukaanza kunikatalia.”
“Samahani kaka. Lakini kama nilivyokuwa nimekwambia. Nia ilikuwa nzuri kaka
yangu. Nakumbuka hata nilipohamia hosteli kutoka kwa Antii, bado ulikuwa
unataka tukutane mahali tule?” “Nakumbuka.” James akajibu. Watu wote walikuwa
wakiwasikiliza pale sebuleni.
“Ukweli harufu za baa zilinza kunishinda kaka.
Nikakwambia tuhamie kwenye migahawa. Nakumbuka ukasema twende kwenye ule
mgahawa wanao uza samaki wazuri wa kuchoma. Pale napo pakanishinda kabisaa.
Nikashindwa kukwambia kwa kuwa wewe ulionekana kupafurahia. Hali ya
kichefuchefu na mabadiliko ya mwili wangu yakanipelekea kununua kipimo mimi
mwenyewe na kujipima mimba. Siku ya jumapili ambayo tulipanga tukutane kwa
chakula cha mchana, ndipo nilipojipima, nikajigundua ni mjamzito.”
“Niliingiwa sana na hofu siku ile. Nikajua endapo
tukikutana tu, utajua kuna jambo ninalokuficha. Ndio nikakutumia ujumbe
kukwambia sitaweza kuja tena. Ukapiga simu ukataka kujua kulikoni. Lakini
niliogopa hata kuongea na wewe kwenye simu. Nikajua endapo utanisikia siku ile,
ungejua kuna tatizo tu. Na ungelazimisha tukutane, nakutaka kujua
kulikoni. Wakati hata mimi sikuwa nikijua nikwambie nini, kwa kuwa sikuwa
kwenye mawasiliano na Geb. Na hapo nilijua Geb amerudiana na Liz. Nakumbuka
nikakutumia ujumbe kukwambia siwezi kuongea kwa wakati huo, nitakupigia
baadaye. Sijui kama ulielewa?” “Nilijua labda unasoma na wenzio.” James
akajibu.
“Nilitaka nikishajua nini chakufanya na mtoto,
ndipo nikwambie. Nikaamua nimwambie kwanza Geb mwenyewe. Akikubali mtoto,
nikajua ndipo nitapata ujasiri hata wa kukwambia. Basi. Nilimfuata Geb
pale alipokuwa akiishi zamani ili kumwambia. Nilimkuta na Liz. Nikashindwa
kumwambia. Au tukashindwa kuzungumza. Nikajua wamerudiana kwa hakika. Nikaogopa
kumwambia ili nisionekane namtumia Liv kama kigezo cha kutaka msaada kutoka kwa
Geb au nataka kuharibu mahusiano yao. Nikaondoka nikiwa nimeamua wewe na Geb nisiwaambie
mpaka nimalize chuo.”
“Nitafute sehemu ya kuishi. Nikipata kazi na
kuweza kujitegemea, ndipo nije kuwatambulisha kwa Oliva. Kumfahamu tu, sio tena
kuwa tegemezi kwako kaka. Najua umehangaika sana na mimi. Sikutaka tena ujue
kama ni mjamzito, halafu ukaanza tena kututunza mimi na Oliva. Nilijiambia
Oliva ni mzigo wangu, nitahangaika naye mwenyewe.” James alikuwa
akimsikiliza kwa makini sana.
“Ndio nikaanza kukupa sababu yakutoweza kukutana
mimi na wewe. Na bahati nzuri ukawa unaelewa, na kuniunga mkono. Lakini pia
mambo hayakwenda kama nilivyotarajia, ndio Geb akaja kugundua nina mtoto wake.
Kukazuka kutokuwa namaelewano kabisa kati yetu. Hapo pia nikaogopa kukwambia
kaka. Kwa kuwa sikuwa nikijua ni lini tena Geb atanifukuza kwake. Nikarudi
sifuri kabisa. Nikawa hata sijui kesho yangu itanikuta wapi.”
“Nilikuwa siruhusiwi
hata kutoka na mtoto labda useme nikuletee umuone! Hapo tena nikaingiwa hofu.
Nikajua ukiniona tena wakati ule ungeumia zaidi kaka yangu. Maana nilijiona
nimefanya kosa ambalo ulikuwa umenionya. Tena kwa kurudia rudia.
Nikaogopa hata kukuona.” Nanaa akafuta machozi.
“Nilikuwa natamani sana kukuona kakak yangu.
Lakini nikajiambia ni mpaka tena nitafute sehemu yangu ya kuishi. Nijijenge
hata kidogo. Wakati nahangaika kujenga uaminifu tena kwa Geb ili
aniamini na mtoto. Nikajiambia akiniamini na kuweza kuniruhusu niwe natoka na
Oliva, ndio pengine nikukaribishe hapo kwangu uje umuone Oliva na uone sehemu
ninayoishi. Lakini Mungu ndio akasaidia, tukapata na Geb. Ndio nikamuomba kitu
cha kwanza, uje nyumbani ili tukutambulishe Oliva. Geb akakubali, ndio
tukakuita wakati ule. Sijui kama unaniamini kaka
yangu. Lakini niliogopa.” Nanaa akaanza kutokwa na machozi.
“Mimi
nakuamini sana Nanaa. Ila nina sababu ya kutaka kujua kwa undani kama hivi.
Nina swali jingine. Katika kipindi hicho chote, ulikutana na Zinda wakati
gani?” James akamuuliza Nanaa. Akashangaa anajaribu kuvuta kumbukumbu.
“Hukumbuki ni lini umekutana na Zinda!?” James akauliza kwa kushangaa. “Mmmh!” Nanaa akaguna akionyesha kutokumbuka
kabisa.
“Labda nikuulize hivi. Koti alilokuazima Zinda
siku ya harusi ya Malii, ulimrudishia lini?” James akauliza. “Unakumbuka siku
moja, ilikuwa jumamosi. Uliniambia kuna nyama ya mbuzi wanachoma vizuri sana
maeneo ya Mbezi ya Kimara. Ukataka tukutane siku hiyo kama kwenye saa tano.
Nikakwambia saa tano natakiwa kwenda dry cleaner ya Sinza. Ukaanza kucheka
ukaniambia, ‘mdogo wangu siku hizi unafua dry cleaner? Mambo yako safi’.
Nikakwambia namchukulia mtu nguo yake. Basi lilikuwa ndio hilo koti la Zinda.
Nilimpigia, nikamuomba tukutane hapohapo kwenye hiyo dry cleaner. Nikamkabidhi
koti lake, akaondoka. Ndio tukakutana na wewe pale Mwenge kituoni, mida ya saa
7 mchana, tukaelekea Mbezi. Sijui unakumbuka?” Nanaa akamuuliza kaka yake.
“Sasa ile si ilikuwa mwezi wa 9 sijui au wa nane
mwishoni?” “Ndio wakati ule ule. Tena umesahau tu kaka. Unakumbuka nilichukua
namba ya Zinda kwenye simu yako? Sema ulikuwa ukiongea na Antii. Sasa sijui
kama ulikuwa ukijua kama nachukua namba ya Zinda! Nilikuomba simu yako
tulipokuwa pale kwa Antii. Ulikuwa umeniletea Calculator. Baada ya ile yangu
kuharibika. Ukasema tukutane kwa Antii ili umsalimie na yeye. Ilikuwa mida ya
jioni, umetoka kazini. Nikachukua namba ya Zinda, nikakurudishia simu yako.” “Basi?”
James akauliza.
“Ukisema, ‘basi’, ndio unamaanisha nini!?” Nanaa
akauliza. “Namaanisha hukukutana tena na Zinda?” James akauliza akitaka
uhakika. “Hapana kaka! Kwanza nilimpigia kwa namba ile ambayo kila mtu alikuwa
nayo. Na nilikuja kuacha kuitumia kabisa ile namba. Sasa hata kama Zinda
atakuwa alikuja kunipigia baadaye, basi hakunipata. Ule ndio ulikuwa mwanzo
na mwisho wa mawasiliano na Zinda. Kwani kuna kitu amesema?” Ikabidi
Nanaa aulize. James akawageukia kina mama G.
“Mbona mnaangaliana na mnasita kuniambia? Maana
nilimuuliza Geb, Geb akaniambia nisubiri kwanza. Eti Geb?” Nanaa akasimama na
kumsogelea Geb pale mezani akiwa anacheza na Oliva. “Unafikiri huu ndio muda wa
kuambiwa? Uliniambia nisubiri. Naanza kupatwa na wasiwasi. Kuna nini?” Geb
akafikiria kidogo. “Mwambie tu James.” Nanaa akageuka, akarudi kukaa pale pale
alipokuwa amekaa na kaka yake.
Nanaa Aambiwa Habari Za
Zinda.
“Zinda ameibua stori mpya inayosababisha
mchungaji kushindwa kutangaza ndoa yenu au kutotambulika uchumba wako na Geb.”
Nanaa akakunja uso. “Stori gani tena!?” Nanaa akauliza huku akimtizama James
kwa makini. James akabaki na yeye hajui aanzie wapi. “Kaka!?” Nanaa akaanza
kupatwa na wasiwasi. “Ameleta
uthibitisho wa cheti cha ndoa.” James akajibu. “Cheti cha ndoa!? Ya nani? Na
inahusiana vipi sasa na mimi kuolewa na Geb!?” Nanaa akazidi kuhoji.
“Ndoa yako wewe na yeye.” Nanaa akatulia kidogo
kama ambaye hajaelewa. “Sijaelewa. Ndoa yangu mimi na Zinda! Au?” “Ndiyo.”
James akajibu. Nanaa akabaki amekodoa macho. “Yaani amesema wewe na yeye
mlifunga ndoa.” “Kwa hiyo anasema mimi ni mkewe?” “Ndiyo.” James akajibu.
“Hivi kaka unajua Zinda sijawahi hata kumshika
mkono? Kwanza siku niliyozungumza naye kwa muda mrefu, ni siku ya kwanza pale
nyumbani kwa Geb pale nje. Tena watu wote walisikia.” “Alipokwambia atakupa
magauni?” Kaka yake akauliza. “Na viatu!” Nanaa akamalizia, watu wengine
wakacheka kidogo.
“Yaani siku ile ndiyo ilikuwa mara yangu ya
kwanza na ya mwisho kukaa chini na kuzungumza na Zinda. Na ninafikiri ndio siku
tuliyozungumza kwa muda mrefu mimi na Zinda. Hata nilipomuomba tuzungumze pale
Marangu, hatukukaa. Tulikuwa tumesimama. Nilimwambia wazi kuwa sipo tayari
kwa mahusiano, kwa kuwa akili yangu haijatulia. Tena nikamwambia
nashawishika sana kukubali ili kupata tu sehemu yakueleweka ya kuishi.
Nikamwambia kama alivyosikia pale, sina mahali pa kuishi. Mimi na kaka
tunatafuta mahali pakuishi.”
“Nikamwambia kwa yeye kuahidi kunipa nyumba na
gari ni kitu kinachosikika vizuri sana kwangu kwa wakati ule ili kupunguza ile dhihaka.
Lakini nikamwambia naogopa sana kumkubalia wakati ule kwa ajili ya kupata
sehemu ya kuishi tu. Tena nikamwambia sitaki aje anipe sehemu ya kuishi
na vitu vyote alivyoniahidi, halafu baadaye nafsi yangu ikapata kila kitu,
nikaja kugundua simpendi. Nikamwambia itakuwa simtendei haki yeye
wala mimi.”
“Akaniomba tena basi tuwe tu kwenye mahusiano.
Nikamwambia kwa wakati ule hata mwili wangu na akili havipo kwenye mahusiano.
Akili zimevurugika. Nikamwambia siwezi kumpa kitu ambacho sina.
Tena nikamalizia kwa kumsisitizia kuwa mimi sio mkewe kabisa. Nikamuomba
msamaha, na kumshukuru kwa nia yake nzuri kwangu. Nikaachana naye. Sijawahi
kukaa tena na Zinda kaka. Hata siku niliyomkabidhi koti lake, tulikuwa
tumesimama. Yeye ndani ya gari yake, mimi nje. Akaniambia twende sehemu tukale.
Nikamwambia wewe unanisubiria twende Mbezi, kwa ajili ya kula nyama choma.
Nikamshukuru kwa koti, nikapanda daladala mpaka Mwenge. Sijamuona tena huyo
Zinda.” Nanaa akamalizia hivyo.
Akafikiria tena. “Tena amedanganya kabisa Zinda.
Maana nilikuwa muwazi kabisa kwake. Sikutaka hata kumzungusha au hata sikuwahi
hata kuwa na hisia na yule kaka.” James akacheka. “Sikudanganyi kaka.
Unakumbuka siku ile nilirudi nyumbani nalia? Nilikuwa nimekuaga nikakwambia
naenda kukutana na Zena Surrender Hotel. Basi siku ile unajua sikukutana na
Zena. Alikuwa amenikutanisha na mwanaume mwingine. Sikuwa tu nimekwambia siku
ile kwa kuwa nilikuwa kama nimechanganyikiwa.” Nanaa akaendelea.
“Nilipofika pale hotelini sikumkuta Zena kama
tulivyokubaliana. Nikampigia simu kumuuliza kulikoni. Akanielekeza kwenye meza
aliyokuwa amekaa mwanaume fulani hivi. Nikamfuata pale nikiwa sielewi.
Nikamwambia Zena ameniambia nimsubirie hapo. Yule kaka akacheka. Alikuwa kaka
labda umri wako hivi au mkubwa kidogo kwako. Alionekana ni kaka aliyetulia na
anajielewa kimaisha. Na alikuwa mzuri tu kwa muonekanao.” James akacheka.
“Usicheke
kaka! Nataka kukwambia kitu cha Zinda ndio maana nakusimulia hii stori. Basi,
yule kaka akaniambia anafahamiana na Zena, alimuomba amtafutie mke. Akasema
Zena amemsifia nimetulia. Na maneno mengi tu. Alijieleza yule kaka kwa muda
mrefu tu. Historia yake ya maisha. Mwanamke aliyekuwa naye mara ya mwisho. Kwa
kifupi alitaka kunioa.”
“Lakini kaka, nilishindwa kabisa
kumkubalia. Yule kaka akanirudisha kwa gari yake, mpaka karibu na nyumbani.
Nilimkatalia asifike nyumbani kwako. Aliniambia nimfanyabiashara. Hapo
alipokuwa alikuwa na gari nzuri tu. Lakini nilichokuwa nikijisikia wakati ule
kwa yule kaka, ni kama nilichojisikia kwa Zinda. Sikutaka hata kumpotezea muda.
Akanishusha, na nikamkatalia namba yangu ya simu, kabisa.” Nanaa akaendelea.
“Nilishuka pale nikiwa nakuja nyumbani huku
nikiwaza. Kwanza nilijichukia kabisa. Yule kaka nilijua angeweza kuniokoa na
shida za wakati ule. Lakini nikajikuta namkataa! Ndio maana nilipokuja
tu nikakukuta umekaa sebuleni ukaniuliza kwa nini nalia, nikakuuliza nitajuaje
kama mtu fulani ndio atakuwa mume wangu? Unakumbuka kaka?” “Nakumbuka.” James
akajibu.
“Tena tukazungumza kwa muda mrefu sana pale
kwenye makochi. Ukazungumza na mimi mpaka nikalala pale pale kwenye kochi mpaka
asubuhi. Unakumbuka?” “Nakumbuka Nanaa.”
James akajibu huku akimtazama dada yake.
“Basi vile vyote ulivyoniambia vile, nilikuja
kuvisikia kwa mara ya kwanza kwa Geb.” Kila mtu alicheka mpaka Geb mwenyewe.
James alicheka mpaka akapiga makofi. “Kabisa kaka. Vile vile. Kila kitu. Tena
nikijua Geb hana kitu. Nikajua ile kampuni ni ya dada yake. Geb anatumwa tu.
Unakumbuka kwenye birthday ya Fili ya
mwaka jana Geb alinifuata nyumbani akasema ametumwa na Grace, aje
anifuate?” “Nakumbuka.” James akajibu.
“Basi mimi mwenzio muda wote nilijua kazi
aliyonayo Geb ni kutumwa tumwa tu na dada yake. Sikujua hata kama
amesoma. Lakini moyoni nikawa najisikia kama vile ulivyoniambia.” Kila mtu
akacheka tena.
“Sasa nikataka kukwambia kuwa vile ulivyoniambia
nitajisikia nikimpata mwanaume ninayempenda, nikataka kukwambia nimejisikia
kwa ndugu yake Grace. Hapo nilikuwa hata sijui kama mlisoma naye. Ndio nikajua
ana mwanamke wake. Nikasema nimuache tu. Lakini bado nikawa namfikiria yeye
tofauti na wanaume wote. Na hapo bado nilikuwa najua anamtumikia dada
yake. Tena kuna kipindi nikajiuliza hivi inawezekanaje mapacha wakawa tofauti
hivyo!? Yaani mmoja asome, mwingine asisome? Au mwingine afanikiwe sana kama
hivyo Grace, halafu mwingine asifanikiwe?” Watu wakacheka. Mpaka mama G.
“Ni kwa vile nilivyokuwa nikimuona Geb anavyojishusha
kwa dada yake! Mimi nikajua hana mbele wala nyuma. Lakini bado moyoni nilikuwa nampenda
kaka.” James akacheka huku akimwangalia Nanaa. “Kama Grace atakumbuka, yeye
ndio aliniambia kuwa Geb anafanya kazi BOT. Nilishituka sana. Tena
nikarudia kumuuliza ‘Geb anafanya kazi BOT!?’ Nikamuuliza kutaka kujua kama
nimesikia na kuelewa vizuri.” “Nakumbuka Nanaa.” “Afadhali. Asante Grace. Tena
nakumbuka ndipo akaniambia hata ile kampuni ni ya Geb. Na akanipa historia fupi
ya maisha ya Geb. Hapo ndipo nikakata tamaa kabisa. Nikajiambia
nilazima nitoe hayo mawazo. Mtu kama Geb hawezi hata kuja kuwa na wazo
na mtu kama mimi.” Nanaa akaendelea.
“Lakini kaka. Japokuwa nilikusudia kuachana
na Geb, lakini nikawa nimepata ile hisia kama uliyokuwa umeniambia.
Nikajiambia kwa hiyo alichoniambia kaka ni kweli. Nikajipa amani hata ya yule
mwanaume niliyemkataa, aliyekuwa amenitafutia Zena. Maana kuna kipindi nilikuwa
nikijilaumu sana kumkataa yule kaka.”
“Haya, wakaja na wengine. Akiwepo na huyo Zinda.
Nikawa natamani kile nilichojisikia kwa Geb, nikipate kwa wengine ili niolewe
na mimi nipate sehemu ya kuishi. Lakini ni kweli kaka yangu sikukisikia
hata kidogo. Ndio maana nilikuwa nikiwakataa moja kwa moja bila kuwapotezea
muda.” Watu walikuwa wakicheka.
“Watu wanaweza kusema nimempendea Geb
pesa, lakini sio kweli kaka yangu. Baada ya kukutana na Geb, nimeshapata
wanaume wengi sana wakinitongoza. Tena wenye pesa nyingi tu. Muulize mama huyo
hapo. Ndio msiri wangu. Huwa namwambia wanaume wote wanao nitongoza. Eti
mama, si wote waliokuwa wakija si hata wewe ulikiri ni matajiri?” Nanaa
akamgeukia mama G, akitaka utetezi.
“Haswaa. Hata yule wa mwisho alionekana
anapesa sana.” Mama G akamtetea. “Si umesikia kaka? Lakini sikuwa napata hisia
zozote.” “Kama ulizokwisha zipata kwa Geb?” James akauliza nakufanya
mpaka Nanaa mwenyewe acheke.
“Hata kidogo. Nilikuwa sisikii chochote zaidi ya
ahadi zao tu. Kwa hiyo Zinda ni muongo kaka. Kwanza amesema tulioana naye
lini?” “Kipindi hicho ulipokuwa na matatizo na Geb.” Nanaa akashituka sana.
“Matatizo gani na Geb!?” “Vile ulivyomfumania Geb na Liz. Anasema baada ya
kumfumania Geb, ukaamua kuachana naye. Kwa hiyo siku ulipomrudishia yeye koti
lake ndio….” “Ngoja kwanza kaka. Yeye Zinda amefahamu vipi mambo yangu ya
ndani hivyo!? Atakuwa amejuaje wakati mimi sikumwambia mtu yeyote. Hata
wewe sijakwambia hata kwa kuropoka kama nilimfumania Geb na Liz. Mtu
anayejua ni mama tu ambaye ndiye msiri wangu. Sijamwambia mtu
yeyote yule! Sasa Zinda ameambiwa na nani mambo makubwa hivyo!?” Nanaa
alishabadilika.
Akamgeukia Geb. “Ni wewe Geb?” Nanaa akauliza.
“Hapana Nanaa.” Geb akajibu. Nanaa akamgeukia mama G huku machozi yakimtoka. “Ni wewe mama? Maana wewe ndio msiri wangu? Wewe ndio
umemwambia Zinda?” “Hapana Nanaa mwanangu.” “Asante
mama. Ningeumia sana. Mwenzio wewe ndio msiri wangu. Sina mtu
mwingine ninayemwambia mambo yangu ya ndani isipokuwa wewe tu.”
Nanaa akajifuta machozi, akatulia.
Lakini kama kitu bado kilikuwa kikimsumbua.
Akaendelea kujiuliza. “Sasa atakuwa ni nani ameweza kutoa mambo makubwa
hivi humu ndani na kumwambia Zinda!? Maana ni kama amempa fimbo ya kutuchapia
mimi na Geb!” Watu wote wakawa wamenyamaza. Nanaa aliuliza swali lililozua
ukimya wa hofu pale sebuleni. Kila mmoja alibaki akiwaza lake.
~~~~~~~~~~~
Geb alikuwa akimuwazia mama yake. Asingependa
Nanaa akosane na mama yake hata kidogo. Mama yake ndiye aliyewasimulia
Grace na mumewe siku walipoenda nyumbani kwake na kukutana na mtoto mgeni kwao,
Oliva, halafu Nanaa hakuwepo alikuwa amelala hotelini baada ya kuchelewa kurudi
nyumbani. Walipouliza mtoto wa nani, na kulikoni Nanaa hayupo ndipo Mama G alipowasimulia
kila kitu. Wakamsema sana Geb, mpaka akamfuata Nanaa hotelini. ‘Sasa Nanaa ataelewa?’ Swali lililoanza
kumsumbua kila mtu.
Danny ndiye aliyetoa maneno na
kuyapeleka kwa Zinda. Danny na Zinda hawakuwa tu marafiki. Walikuwa kama ndugu.
Danny mtoto yatima, alipokelewa kwa kina Zinda kama mtoto wa nyumbani.
Alishafanya biashara na baba yake Zinda kama baba yake. Nyumbani kwa kina
Zinda, Danny hakuhitaji kwenda na Zinda au kukaribishwa. Wakati mwingine
alichukua familia yake na kwenda kusalimia wazazi wake Zinda. Au akisikia mama
yake Zinda ni mgonjwa, alimchukua Geb na kuwahi Tabora kumuwahi mama Zinda na
kumkimbiza hospitalini. Aliweza kutuma pesa kwa kina Zinda bila hata kumwambia
Zinda. Danny alikuwa mtoto wa nyumbani. Kaka wa hiari wa Zinda. ‘Sasa Nanaa ataelewa?’ Ni swali
lililozidi kuumiza vichwa vyao zaidi vile jinsi Nanaa anavyouliza.
~~~~~~~~~~~
“Sasa atakuwa
ni nani ameweza kutoa mambo makubwa hivi humu ndani na kumwambia
Zinda!? Maana ni kama amempa fimbo ya kutuchapia mimi na Geb.” Hilo ndilo likabaki swali
lakuumiza kichwa cha kila mtu hapo sebuleni.
~~~~~~~~~~~
Mungu bado
anatenda Miujiza. Hajawahi kuacha, na wala hana mpango wakuacha. Hana
upendeleo. Habagui wala kuchagua. Hufanya kwa kadiri ya apendavyo.
Nanaa na Geb
wameshuhudia hilo.
KUPOKEA
muujiza ni jambo moja, na KUUTUNZA ni jambo la
pili. Ukifikiri shetani huwa analala au anasinzia, badili fikra.
Hawa
wapenzi wawili ametoka kukutana uso kwa uso na nguvu za Mungu.
Si
kusimuliwa! Hata masaa 24 hayajapinduka tokea Nanaa amuone malaika wa
Mungu, LAKINI tayari shetani ametupa JINGINE.
Nanaa amerudi
nyumbani, anataka kujua wabaya wake.
Sasa je,
yupo tayari na ukweli? Nini kitaendelea kati yao? Alilokusudia shetani safari
hii, watasimama?
Usikose kufuatilia.
0 Comments:
Post a Comment