Geb alibaki akifikiria, wakati
Nanaa akiendelea kulia. James alikuwa ameinamisha kichwa pale alipokuwa amekaa.
Amekishikilia kana kwamba
kinataka kuanguka. Walimsikia na yeye akivuta kamasi kama aliyekuwa akilia.
Ukimya ukatanda tena. Kila mmoja akiwaza lake. Mchungaji akakata simu. Bado jua
lilikuwa likiwaka nje. Hakuna aliyekuwa na wazo hata lakuangalia saa. Wazi
walijua ndio mida ya ibada kuisha. Inamaana hata bado hapo kanisani hapajapoa
tokea mama yake James na Zinda waamshe sakata la kipingamizi cha ndoa ya Nanaa
na Geb.
Kwa
alivyo mzungumzaji mama yake, James alianza kupata picha moto aliowawashia hapo
kanisani. Kwa fujo alizozifanya siku ile pale baa na matusi aliyokuwa
akiyamwaga kwenye kundi lao la whatsapp, Danny akaanza kupata picha sakata
alilolipeleka Zinda pale kanisani. Wote walibaki kimya.
~~~~~~~~~~~~
“Milioni
20 nyingine!?” James alisikika akirudia kwa
sauti iliyojaa huzuni huku akifuta machozi. Mtoto huyo wa kiume, alifikishwa
mahali hajui atafanya nini na dada yake huyo hapo kitandani. “Labda nitafute mteja wa kiwanja changu na
ile nyumba ninayojenga. Nimlipe mama. Haya mambo yaishe.” James aliendelea. “Naombeni wote muondoke jamani. Nataka kubaki tu peke yangu.” Nanaa naye akaongeza. “Naombeni mniache. Geb, nakushukuru kwa kila
kitu. Lakini kwa sasa nataka niachwe peke yangu, tafadhali.” Nanaa alisisitiza huku akilia. “Nimechoka.
Naona inatosha. Naomba niachwe kabisa.”
Nanaa akaendelea.
“Nilikwambia
sitaondoka hapa hospitalini bila wewe Nanaa.” “Mimi sikutaki tena Geb. Sitaki tena mahusiano na wewe.” “Naomba usiwahi kurudia kuniambia hivyo tena
Nanaa.” Nanaa aliendelea kulia. “Mimi na wewe tuna maagano ya milele ambayo
hayavunjiki kwa changamoto za njiani.” “Tutafanyaje Geb!?” “Hilo ndilo
swali ulitakiwa kuuliza Nanaa. Sio kunikana!” “Naona mambo yanazidi Geb! Sina thamani ya milioni 50 mimi. Waambieni
hao wote waje wanione sasa hivi kama bado wataendelea kuning’ang’ania. Nimeanza
kuoza nikiwa hai. Hakuna mwenye haja na mimi zaidi yakutaka kunikomoa tu.
Unafikiri Zinda atanitaka sasa hivi jinsi nilivyo? Au huyo mama mkubwa
unafikiri atavuna matunda gani hivi nilivyo? Mwambieni aje anichukue muone kama
atanikubali. Wameamua kunikomoa tu.”
Nanaa aliendelea kulia huku akiongea.
“Hawajui wanadai nini. Hawajaniona.”“Mimi
na wewe Nanaa, ni mpaka kifo kitakapotutenganisha. Hakuna pesa itakayokutoa
kwangu. Pesa yeyote wanayotaka nitawalipa. Kwa vyovyote ulivyo na
utakavyokuwa, wewe ni Nanaa Magesa. Ni wangu sasa hivi na ni jukumu langu. Nitanunua
uhuru wako kwa bei yeyote ile. Nakupenda wewe, na nimekuchagua wewe. Hata
iweje, utakuwa wangu tu. Wala pesa isikulize.” Geb akamgeukia Grace.
“Kitabu
cha hundi ya akaunti yangu mimi binafsi, sio ya kampuni, kipo kwenye mkoba wa
laptop yangu. Mpe mama aniletee kesho wakati anamleta Liv hapa hospitalini
nishinde naye. Nitaweka saini tu bila kuandika kiasi ili mama aende nayo wakati
anakutana na mama James. Nataka kesho tufikie hatima ya hiyo pesa mama. Nataka
tumalize kumlipa huyo mama kiasi cha pesa atakachoridhia yeye. Jaza hiyo hundi,
hakikisha anasaini mahali kukubali amepokea, kisha mkabidhi, yaishe. Tafadhali
mama, naomba hakikisha kesho iwe mwisho wa hayo madai. Sitaki kusikia tena.”
Geb alitoa hayo maagizo.
“Mimi
nitakuongezea pesa kiasi Geb. Ninayo akiba.” “Nakushukuru James. Lakini hapana.
Umeshahangaika sana na Nanaa mpaka kumfikisha hapo alipo. Inatosha.
Nilishawalipa mahari yenu. Mkakubali. Nanaa ni mke wangu mimi. Nina jukumu la
kumlinda kwa namna yeyote ile. Hapo alipo ni mjamzito na mgonjwa. Naomba mambo
mengine yote kuanzia leo niambiwe mimi tafadhali. Nataka yeye ajifikirie yeye
na mtoto aliyekuwepo tumboni tu.” “Usisahau harusi pia.” Grace akaongeza
wote wakamgeukia kama kumshangaa. “Ni kweli Grace. Ajifikirie yeye mwenyewe,
mtoto na harusi. Basi.” Geb akakubaliana na dada yake.
“Mengine
yote, yaishie hapo nje ya huo mlango. Sitaki matatizo mengine yeyote yale
yaingizwe tena ndani ya hiki chumba. Nitamlinda Nanaa kwa kila namna.” Geb
aliongea kwa kutulia. Akaendelea. “Na ninaomba, mtu yeyote yule, asiambiwe hali
ya Nanaa. Sitaki mtu yeyote mbali ya nyinyi aje kumuona Nanaa. Sitaki
wageuze hapa ni mbuga za wanyama. Sitaki waje washangae na kuzidi kumtia
hofu. Danny, naomba endeleza mipango ya harusi kama kawaida. Marafiki wote
habari watakazopewa ni za harusi tu. Wakitaka kujua hali ya Nanaa, waambieni…”
“Nanaa amewekwa ndani anatayarishwa kwa ajili ya harusi.” Mama G akadakia na
kumalizia.
Wote
wakamgeukia. “Kabisa. Hakuna mtu atakayemuona Nanaa mpaka siku ya harusi yake.
Kila mtu ajue hivyo. Mafunzo yao ya ndoa yataendelea hapa hapa ndani mpaka siku
yao ya harusi kama alivyosema Geb. Mimi na Grace tutakuwa tukija kuzungumza na
Nanaa juu ya ndoa. Hatutataka mtu mwingine amfundishe kitu chochote Nanaa,
isipokuwa mimi na Grace.” Mama G akaongeza. “Asante mama.” Nanaa akashukuru.
“Nakushukuru mama.” Geb naye akaongeza.
“Na
James, tafadhali sana. Hata mama yako naomba asijue hali ya Nanaa. Niacheni tu
mimi mwenyewe. Nitamlilia Mungu wangu mpaka atakaponijibu. Na ninajua atajibu
tu. Sitaki mtu yeyote yule ajue. Maana hata wakijua, haitasaidia kitu.” Geb
akaongeza. “Inawezekana wanajua kinachoendelea sana tu. Inawezekana mmoja wao
ndio anahusika na kukuweka hapo Nanaa.” Mama G aliongea, wote wakamwangalia.
“Nawaambia kweli kabisa. Nyinyi mmeshawahi kuona ugonjwa kama huo? Upo mkono wa
mtu juu ya miguu ya Nanaa. Lakini mimi sitanyamza Geb.” Mama G akaongeza wote
wakabaki wakimwangalia.
“James,
mimi nakutuma kwa mama yako. Mwambie kama anahusika na ugonjwa wa Nanaa,
ahakikishe huyu mtoto anapona. Huna haja ya kumwambia anaumwa nini na yupo wapi,
ila mwambie nataka atoe mkono wake kwenye maisha ya Nanaa. Tutamlipa pesa yake,
aachane na Nanaa. Anaanza vita kali sana, ambayo mwambie namwakikishia
hatashinda. Pesa yake yote tutampa kesho. Mwambie aje ofisini kwa mchungaji
majira ya saa 11jioni. Nitazungumza na mchungaji ili aite na wazee wa kanisa,
washuhudie tukimalizana na mama yako.” Mama G akamgeukia Geb.
“Geb!
Mpigie simu huyo meneja wa benki, mwambie anitayarishie kopi zote za malipo ya
hiyo milioni 30 aliyochukua mama James. Nitapita hapo benki kesho kuchukua hizo
kopi zote, wakati naelekea kanisani.” Mama G akanyanyua tena simu akapiga
mchungaji. “Naomba mwambie Zinda, kesho
akuletee hicho kithibitisho cha ndoa yake na Nanaa. Kaka yake Nanaa, ambaye ni
James, mimi, mwanangu Danny tutakuwepo hapo kanisani saa 11 jioni kuangalia
hicho kithibitisho na aseme ni nani alimlipa hiyo mahari ya kumuoa Nanaa. Na
tafadhali sana mchungaji.” Mama G akaendelea.
“Ili kusiwe na
kupindisha maneno hiyo kesho na baadaye, naomba unisaidie kunitafutia baadhi ya
wazee watakaoweza kuwepo kesho kwenye hicho kikao.” “Ni wazo zuri mama. Poleni
kwa matatizo.” “Nashukuru. Lakini mpaka sasa, sijaona tatizo. Hatuna tatizo
hata kidogo. Hiyo ndoa itafungwa tu. Na ili kufanikisha hilo, naomba usimwambie
Zinda kama sisi tutakuwepo hapo. Anaweza asitokee. Nataka afike hapo, ndipo
atukute tukimsubiri. Nimemuomba na mama James pia awepo tumlipe pesa yake. ”
“Sawa mama. Mungu azidi kuwalinda.” “Amina.”
Mama G akaagana na mchungaji. Akakata simu.
“Asante
mama.” Geb alisikika akiwa amepata aghueni. “Mungu yuko na wewe Geb. Uamuzi
uliochukua ni wa busara. Binafsi nikushukuru. Hisia nilizonazo kwa Nanaa, ni
kama mtoto niliyemtoa tumboni kwangu. Huwa najiambia ndio kiziwanda wangu.”
“Mama wewe! Sio mimi tena?” Wote wakacheka mpaka Nanaa na mama G, wakacheka.
“Kweli tena. Nampenda Nanaa, kwa moyo wangu wote bila unafiki. Na Nanaa,
utasimama tu siku yako ya harusi. Na utalea wanao mwenyewe. Wala usiogope.”
Nanaa akaanza kulia tena.
“Kulia
ni kukubali kushindwa Nanaa. Sasa hivi simama kama Simba, ukitetea wanao. Kilio
cha Oliva leo kikutie shauku ya kurudi kwako na kulea wanao. Usikubali
kushindwa kizembe hivyo. Simama mchana na usiku ukimlilia Mungu, akutoe hapo
kitandani. Najua inaogopesha. Lakini jiambie tunae…” “Simba wa kabila la Yuda.
Atanguruma tu. Na akinguruma, kila agano na kila madhabahu iliyohusika
na kuweka agano la hicho walichokutupia, hakika Yesu atakipindua. Sitanyamaza,
mpaka Mungu, mume wa wajane. Baba wa yatima, atakaponijibu. Hakika atajibu
Nanaa mwanangu. Wala hapo hutakaa muda mrefu. Utatoka tu.” Mama G alimkatisha
mwanae Grace, akaendelea yeye akiwa amejawa ujasiri.
“Umesikia
Nanaa? Usilie tena.” Grace akaendelea. “Ila hakikisha ukitoka hapo unaushuhuda
mkubwa. Kukaa kwako hapo isiwe bure. Lile baya alilokusudia shetani juu yako,
Bwana akutendee mema. Badilisha hiyo historia. Jiambie hapo upo kwenye shule.
Lazima ukitoka hapo uwe watofauti. Mungu amekutenga kwa muda. Badilisha mtazamo
wako weka kwa Yesu tu. Kuanzia sasa, mwambie Mungu aseme nawe kwa kuwa umekaa
chini, umetulia, unamsikiliza yeye tu. Inawezekana ulikuwa na mambo mengi. Wewe
na Geb. Wote mmeshindwa kumsikia Mungu. Sijui kama mlikuwa mkipata muda wa
pamoja kumuomba Mungu?Japo mama alishaniambia aliwafundisha.” Grace aliwatizama
wote wawili kutaka kujua.
~~~~~~~~~~~~
Wapenzi
hao wawili walijawa kiu iliyokuwa haiishi kati yao. Kila walipokuwa wakipata
muda wao peke yao, ilikuwa ni mapenzi tu. Na tena kila walipomaliza,
waliwekeana ahadi ya kuendelea baadaye kana kwamba hawakutumia masaa na masaa
hapo kitandani au kwenye kochi lao hapo chumbani. Na kwa kuwa walikuwa wakilala
peke yao juu gorofani, walifanya mapenzi kwa raha zao zote wakijinafasi.
Chumba
chao kilikuwa na sebule ndogo tu. Geb alitengeneza sebule hiyo iliyokuwa
ikiangalia baraza kubwa la nje, la huko huko gorofani. Lililokuwa
limezungushiwa vyuma vizuri sana vya urembo na kioo kizito. Mwanga wa jua
ulikuwa ukimulika sebule hiyo ndogo iliyokuwa imetenganishwa na milango ya
kusukuma ya vioo. Mtu wa nje hakuweza kuona ndani ila wa ndani tu. Kuliwekwa tv
kubwa sana ambayo wakati wote walijiambia wanakaa hapo kuangalia tv, na kuishia
kufanya mapenzi kwa muda mrefu huku movie ikiendelea.
Ndani
ya hicho hicho chumba chao, kulikuwa na chumba kikubwa tu cha nguo na viatu.
Upande wa Geb, na upande mwingine wa Nanaa. Napo huko walikutana wakati wa
kuvaa baada ya kutoka kuoga. Kila walipotizamana, walianza upya ndani ya chumba
hicho hicho na kujikuta wanarudi tena kuoga ambapo na huko bafuni kulikuwa na
sinki kubwa la kuogea pamoja na bafu. Na sehemu kubwa yenye sinki la kupigia
mswaki lenye vitu vyao baadhi. Upande wa Geb, kulikuwa na vifaa vya kunyolea
ndevu na mafuta yake. Upande wa Nanaa, vitu vya kike. Mbele ya hilo sinki
kulikuwa na kioo kikubwa sana ukutani. Napo pia Geb alijikuta akichelewa kutoka
humo maliwatoni kuwahi kwenye majukumu yake ya kila siku.
Kwani
kila alipokuwa huko akimalizia kujisafi, huku Nanaa naye amejifunga taulo
akitaka na yeye kujipodoa mbele ya sinki hilo lenye kioo kikubwa upande wake
kisha atoke ili akasaidie kazi za humo ndani au hata mtoto wake tu, Geb
aliishia kumkodolea macho kwa kupitia kioo hicho, mwishowe uzalendo humwisha,
na kuishia kukwapua taulo hilo mwilini mwa Nanaa, nakuomba kuagwa ili aweze
kutulia kazini. Huku akimuahidi Nanaa, akimpa penzi la mara ya mwisho hapo hapo
bafuni, ataondoka kuwahi kazini. Mchana hatarudi mpaka jioni akitoka kazini.
Lakini
mchezo ukawa ni huo. Kazi zikipungua kazini mida ya mchana, Geb anarudi huku
akimwambia Nanaa, asubuhi wakati wanaagana, hakufaidi hiki au kile. Anamtaka
kidogo tu huko chumbani ili angalau akatulize mawazo kwenye kikao chake cha
jioni huko kazini na watu muhimu. Na kwa penzi alilokuwa akipewa Nanaa. Sifa
alizokuwa akipewa kuanzia nguo ya ndani atakayokutana nayo Geb muda huo, Nanaa
alikuwa akiomba Geb arudi tu, amfunue, afurahishwe. Hata yale mapungufu
aliyokuwa nayo Nanaa, kama mwanamke, akitamani Mungu asingemuumba nayo, Geb
alijigamba na kumwambia ndio starehe ya macho yake. Akimuona tu hivyo,
hajiwezi. Kwa hiyo hakuna jinsi ungemwambia Nanaa, asimvulie nguo Geb, muda na
wakati wowote akakubali.
Maombi,
kusoma neno la Mungu, vyote vilisubiri. Ushirika wao na Mungu kama
walivyofundishwa na mama yao, walisogeza mbele. Kila wakati waliambiana
wataanza kesho. Walishapanga mikakati. Walishaweka mipango ya kuanza kusoma
bibilia kwa pamoja. Waanzie wapi, waishie wapi. Geb alipokuwa kazini, Nanaa
alipata ‘bible plan’ nzuri sana kwa wapenzi au wanandoa, kutoka online.
Akaichukua ili waanze kusoma pamoja na kuomba. Jioni hiyo baada ya Geb kutoka
kazini, Nanaa alipokuwa akimuelezea Geb juu ya hiyo ‘bible plan’, wakiwa chumbani kwao,
akimwambia waanzie hapo, walijikuta wakihema pembeni, baada ya shuguli nzito na
tamu ya mapenzi.
Geb
alikuwa akiangalia midomo ya Nanaa wakati akimuelezea, huku amejilaza kwenye
kochi hapo chumbani kwao. Mikono ya Geb ilikuwa ikitembea mwilini mwa Nanaa,
wakati Nanaa ameshika simu yake anamsomea hiyo ‘bible plan’ kutoka kwenye
bibilia. Geb alikuwa amekaa, Nanaa amemuegemea kiwili wili cha juu. Waliishia
kufanya mapenzi. Geb akamsifia kwa kazi nzuri aliyoifanya ya kutafuta plan hiyo,
na mkakati wa kuanza kusoma na kuomba pamoja, akamwambia lazima kesho
yake waanze. Kesho haikuwahi kufika, mpaka hapo Grace anapowauliza.
~~~~~~~~~~~~
Alipowaona
wanaangaliana, Grace akapata jibu lake. “Nanaa na Geb, shetani yupo na nguvu
zake ni halisi. Msifanye mchezo jamani. Mkiishi hivyo mbali ya nguvu za Mungu,
atawachezea kwa kadiri ya uwezo wake. Na yeye huwa hachoki. Atatuma attack kutoka nje. Akiona mnashinda na mmeshikana kama
sasa hivi, ataanza kuwajaribu nyinyi kwa nyinyi. Ombeni bila kukoma. Ombeni
msiingie majaribuni. Ombeni myashinde majaribu. Yapo. Yatakuja. Msipuuze hata
kidogo.” Grace alikuwa akiongea nao kwa taratibu.
Dada
huyo mkimya, lakini kumbe alibeba nguvu ya ajabu. Akianza kuzungumza mambo ya
Mungu, utapenda kumsikiliza. Kwa kuwa alijitolea mfano na kuwaambia ni maisha
anayoyaishi yeye. “Mnadhamana ya roho mbili sasa hivi kama sio tatu. Maana
hatujui Nanaa ana watoto gani humo tumboni. Kama ni mapacha au mmoja. Hizo roho
mtadaiwa na Mungu! Mtazitolea hesabu siku moja. Msizembee. Simameni kwa ajili
yenu na watoto wenu.” Grace akamaliza na kunyamaza.
“Mmeelewa
Geb na Nanaa? Huu muda mtakao kuwepo hapa, utumieni vizuri kama alivyosema
Grace. Shetani hapendi familia. Ndio maana wakati wote anasimama kupinga ndoa.
Anajua akimpata mama au baba, amepata taifa la kesho. Ambao ni watoto.
Mmesikia?” “Nimeelewa Grace na mama. Nawaahidi kufanyia kazi. Hii ni ‘wake up call’ yetu. Akimaanisha kengele ya kuwaamsha kutoka usingizini.
Hatutatoka hapa kama tulivyoingia. Si ndio Nanaa?” Geb alimsogelea Nanaa,
akainama na kumbusu. Nanaa akatingisha kichwa akikubali.
“Basi
kabla hamjaondoka, naomba tuombeni tena pamoja.” Geb akapiga magoti pembeni ya
kitanda cha Nanaa. “Nipe mkono wako.” Nanaa akampa mkono ule ambao haukuwa na
dripu. Geb akaushika. Hakuna aliyemuona Geb akiomba vile. Japokuwa hakuwa
akiomba, lakini alikuwa akimuona mara zote vile mama yake alivyokuwa
akimuombea. Usiku wakiwa wanalala na mama yake. Enzi akilala na mama yake kabla
Nanaa hajaanza kuishi nao. Mama G alikuwa akimshika Geb mikono usiku anaomba.
Mama huyo hakuacha kutubu kwa niaba ya mwanae huku akimsihi Mungu amtakase.
Wakati wote alibariki mikono ya mwanae, nakumuombea katika kila eneo. Geb
aliishia kusema ‘Amen’. Na kulala bila hata kuongeza neno. Lakini siku
hiyo aliomba kama mama yake.
Aliomba
mpaka Nanaa akashangaa. Akafungua macho na kumtizama Geb aliyekuwa amezama
kwenye uwepo wa Mungu. Alishakuwa ametubu kwa ajili yake, Nanaa na Oliva.
Akamtakasa na mtoto au watoto waliokuwepo tumboni. Akaomba uwepo wa Mungu.
Danny mwenyewe hakuamini. Aliomba kwa muda wa dakika 36, bila kupumzika. Ndipo
akamaliza. Mama G akafurahi sana.
“Sasa hapo, hata nikiondoka sitakuwa na
wasiwasi. Najua kiziwanda wangu yupo kwenye mikono mizuri.” “Kweli mambo
yanabadilika! Nanaa amenipokonya nafasi yangu hivi hivi!” Angalau wakaanza
kucheka. “Muda wakudeka umeisha Geb. Unaingia kazini.” “Ni kweli. Nilishazoea
kuombewa na mama.” Wakacheka.
“Mama!”
Geb aliita. “Naomba asubuhi Liv akiamka, ukishamlisha, umlete. Sitaki akae
mbali na mama yake. Hajawahi kuwa mbali naye. Na sitaki aone tofauti. Mimi na
mama yake wote hatupo! Haitakuwa vizuri. Kwa kuwa mimi nitakuwepo tu hapa,
mlete nishinde naye.” Watu wote wakanyamaza. “Nini?” Geb akauliza. “Kwa nini
usimuache kwa muda mpaka mama yake apone?” “Nitachanganyikiwa mama. Naomba aje
tu. Akiwa hapa akili ndio itatulia.” Nanaa aliongeza. “Sawa nitamleta. Lakini
sio asubuhi. Angalau tumuache apate na ule usingizi wake wa saa tano. Akiamka
hapo, ale chakula kwanza. Halafu nitaenda naye benki kuchukua hizo karatasi,
ndio nije naye hapa. Sitaki akae hapa hospitalini muda mrefu. Atataka kutambaa.
Na sidhani kama kuna mazingira hayo, hapa.” “Basi ukija uje na kile kigari chake
chakutembea.” “Hapo sawa.” Wakakubaliana.
James
akamsogelea Nanaa. “Nitakuona baadaye kidogo. Ngoja nikafuate vitu vya Geb.”
“Tutaongozana James. Na mimi naondoka sasahivi.” Grace akaaga. “Asante kaka.” Nanaa akaanza kulia. James akasimama pale kwa muda
akimwangalia dada yake kwa kumuhurumia. “Pole sana Nanaa. Pole. Nitakuona baada
ya muda kidogo.” James akaaga. “Na wewe Nanaa uletewe nini?” Mama G akauliza. “Uji wa Geb, na chakula chake. Hajala vizuri
mama. Anaweza kulala na njaa.” “Basi itabidi
James asubiri kidogo huko nyumbani, nipike haraka haraka.” “Asante mama yangu.”
Nanaa akashukuru. Kila mtu akacheka. “Asante Nanaa.” Geb akamshukuru. Nanaa
akatabasamu huku akifuta machozi mashavuni.
“Mwenyewe
anamkumbuka Geb hata akiwa na matat….”Danny akashindwa kumalizia. Akanyamaza
kwa muda. “Nanaa na Geb, upendo una nguvu ya ajabu sana. Mkiendelea hivyo.
Mkichanganya na maombi. Mkajisogeza karibu na Mungu. Hakuna litakalo washinda.”
“Kama wewe na Grace?” Nanaa akadakia. Wakacheka. “Na sisi mtuombee tuwe kama
nyinyi.” Nanaa aliongeza kwa upole. “Mungu ameshawasaidia Nanaa. Yupo na
nyinyi.” “Amina na asante Danny.” Wakaagana. Wote wakaondoka.
Usiku
Wa Kwanza Nanaa Akiwa Hospitalini.
Geb
alijitahidi sana kumliwaza Nanaa. Usiku huo aliutumia kumuwekea viapo vya
milele. Daktari alishapita. Na nesi naye akawa amechukua vipimo vyote. Nanaa
hakuwa amepandisha homa wala pressure. Kila kitu kilikuwa sawa tu. Daktari
alimwambia nesi aliyekuwepo zamu, ajaribu kufyoza yale maji kutoka kwenye
malengelenge ya miguu yake. Ili baadhi ya maji hayo yakafanyiwe vipimo. Yule
nesi alishangazwa na yale malengelenge. Alivyoyafyonza maji, muda ule ule
yakajaa tena na kurudi kama yalivyokuwa! Kwa mshituko akaongea pale pale mbele
ya Nanaa na Geb. Nanaa akaanza kulia.
Nesi
alipoondoka, Geb akamfuata. “Tafadhali sana. Naomba maendeleo yote ya ugonjwa
wa Nanaa nijulishwe mimi. Naomba yeye aachwe kwa sasa. Sitaki aanze kupandisha
pressure na ujauzito alio nao. Nataka atulie. Sijui itawezekana?” Geb aliongea
kiugwana sana. “Samahani. Nikatika hali ya mshituko tu kaka yangu. Sijawahi ona
kitu kama hicho! Samahani sana. Nitajulisha na wengine.” “Nitashukuru. Unaweza
kunipa mataulo ya ziada ili niwe nambadilisha mwenyewe. Kuwapunguzia usumbufu
usiku.” “Basi nitakuletea. Lakini lazima kuja kubadilisha mfuko wa mkojo na
kumwangalia tena homa na pressure yake.” “Hamna shida.” Geb akarudi chumbani
alipokuwa Nanaa.
Bado
alimkuta akilia. “Itakuwaje Geb?” Nanaa akauliza huku akilia sana kwa hofu. “Sijui
Nanaa! Lakini najua kitu kimoja.” “Nini?” Nanaa akauliza kwa shauku kama
aliyejua Geb anamajibu yote. “Ukiacha kulia nitakwambia.” “Niambie tu Geb.” “Nataka unisikie ukiwa umetulia.” “Siwezi. Naogopa. Itakuaje maisha yangu yaje
kuishia hapa kitandani?” “Tumezungumzia nini juu ya swala
la hofu Nanaa?” Geb akamuuliza. “Umesema ndio njia ya kuzidi kumfungulia shetani mlango. Lakini unajua
kama binadamu nashindwa Geb.” “Nakuelewa
Nanaa. Na sikulaumu. Acha imani yangu ikubebe kwa sasa. Nitaamini kwa ajili
yako. Mungu atatenda tu. Naomba usiangalie hii hali sasa hivi. Tuangalie ahadi
za Mungu tu.” Geb akajaribu kumtuliza.
“Lakini itakuaje kama nikibakia hivi hivi nisipone? Utafanyaje?” Nanaa akauliza. “Ninachojua kwa hakika ninakupenda
wewe Nanaa. Na nimekuchagua wewe uwe mke wangu. Tutazikana. Kwa hali yeyote
ile, wewe ni wangu. Tupo hapa kusubiri majibu ya vipimo vyote walivyochukua.
Yakitoka na kusema kila kitu kipo sawa, tutakubaliana nayo. Tutaondoka hapa na
kurudi nyumbani kwetu. Maisha ya aina nyingine yataanza. Nikijua unahitaji
msaada wa karibu zaidi, haswa mimi ninapokuwa kazini. Na hapo ndipo
itakaponilazimu kutafuta msadizi wa kutusaidia mimi na Grace. Ili niwe na wewe
muda mwingi. Basi. Hakuna kitakachobadilika kati yetu Nanaa. Mungu akizidi
kutubariki siku, tutafunga ndoa yetu. Wakati tukiendelea kumsubiria mtoto
wetu.” Nanaa akavuta pumzi kwa nguvu akijaribu kutulia.
“Kwa hiyo niwe na uhakika kuwa hutaniacha peke yangu?” “Naanzia
wapi Nanaa? Niende kwa nani?” “Sijui
Geb!” “Haitakaa ikatokea. Ni kifo tu
ndicho kitatutenga mimi na wewe mpenzi wangu. Na nitamlilia Mungu atupe umri
mrefu mimi na wewe.” “Nakushukuru Geb.” Geb akambusu.
“Lakini
nikuombe kitu Nanaa.” “Nini?” Geb akavuta shuka na kumfunika vizuri. “Najua upo
kwenye wakati mgumu sana. Uelewe hata mimi nipo kwenye wakati mgumu. Nakuhitaji
kuliko unavyofikiria wewe. Nakuhitaji sasa hivi. Ukiwa kwenye hali hiyohiyo
ujue nakuhitaji. Wewe ndio faraja yangu. Naomba isitokee ukanikana tena.” “Sitarudia tena Geb. Niliingiwa hofu na hiyo
pesa. Ni nyingi sana.” “Naelewa. Lakini naomba katika
kila changamoto, tusimame pamoja. Leo ni wewe wanadai hiyo pesa, je ikitokea ni
mimi?” “Unajua sitawahi
kukukimbia Geb. Nakupenda.” “Basi endelea
kuonyesha kwa vitendo na maneno yako. Nahitaji kusikia hivyo hata nyakati za
shida. Tafadhali Nanaa. Inaniogopesha kukuona upo tayari kuachana na mimi
kirahisi hivyo!” “Nisamehe Geb.
Tafadhali nisamehe mpenzi wangu. Nimepata habari ngumu ngumu kwa wakati mmoja.
Nikaona nikupunguzie mzigo. Labda tukiachana, utapumzika. Nimeona vimezidi Geb!”
“Hakuna pumziko mbali na wewe. Wewe ndio
pumziko langu.” Nanaa alilia sana.
Alijifikiria
hali aliyonayo wakati ule. Na maneno aliyokuwa akiyasikia kutoka kwa Geb,
vilimgusa sana. Ndipo akasadiki kuwa Geb ana mapenzi naye ya dhati. “Nakushukuru sana Geb. Asante mpenzi wangu.
Sasa hivi nimethibitisha. Maisha yangu yote nimejua ninaye kaka tu. Lakini
angalau sasa hivi najua umeongezeka na wewe. Asante mpenzi wangu.” Geb akamvuta karibu akaanza kumbusu huku
amemkumbatia. Alimnyonya midomo yake kwa utulivu akiwa amelala palepale
kitandani na dripu yake ya maji mkononi. Alimnyanyua kiwiliwili kidogo tu,
akahakikisha amemudu kumkumbatia vizuri.
“Nakupenda
sana Nanaa.” “Nimeamini Geb. Asante. Nakushukuru kuwa hapa na mimi. Asante
kunilipia garama kubwa sana kutoka kwa mama mkubwa.” “Karibu.” “Nakupenda Geb.”
Geb akatabasamu. “Asante Nanaa.” Akaanza kumbusu tena mpaka nesi akaingia
kuleta mataulo. Akamkabithi Geb, na boksi la gloves. Akatoka.
“Nataka
upumzike. Leo umekuwa na siku ndefu sana. Kesho tutaanza kutafuta majina ya
mtoto.” Nanaa akacheka. “Sawa.” “Nilimisi hizo dimpozi!” Geb akamshika
mashavuni. “Usilie tena bwana. Unajua ni jambo moja kujaribiwa. Lakini kukosa
au kupoteza tumaini ndio mbaya zaidi. Naomba amani yetu idumu. Amini kunamahali
Mungu anatupeleka mimi na wewe. Tupo hapa tunaandaliwa. Unasikia Nanaa?”
“Sitalia tena Geb. Sasa hivi nitarudisha furaha kwa ajili yako na wanangu.
Sitaki Liv aje kesho anikute nalia au sina raha.” “Kabisa. Na huyo wa tumboni
sitaki ahisi anakuja kwenye mazingira ambayo hayajaandaliwa.”
“Nitabadilika Geb. Nakuahidi kupambana kwa ajili yako na wanangu. Na ninajua
hapa kitandani nitatoka tu.” “Sasa hapo unaanza kuongea. Endelea
kidogo.” Nanaa akampiga ngumi kidogo.
“Kweli
tena. Rudia Nanaa. Mpaka hiyo hali isikie. Akili ielewe. Na moyo upokee muujiza
wa maneno yako. Kumbuka mama alivyokwambia. Uzima na mauti upo kwenye kinywa
chako. Jitamkie uzima.” “Nitapona Geb. Nitamlilia Mungu kwa ajili yako na
wanangu. Nataka kulea watoto wangu mimi mwenyewe.” “Basi tushikane mikono tena
tumwambie Mungu. Aturehemu.” Geb akamwekea mito nyuma ya mgongo. Akapandisha
kitanda upande wa kichwani. Wakaanza kuomba. Waliomba, kila mmoja akimsihi
Mungu kivyake. Ndipo Geb akamwacha alale.
“Na
wewe utalala wapi?” Nanaa akamuuliza kwa kumuhurumia. “Najua usiku wa leo
utakuwa mgumu sana kwangu Nanaa. Nimeshazoea kulala na wewe.” Nanaa
akamuhurumia sana mpenzi wake. “Nishazoea kukusikia mwilini mwangu, hata nikishituka
usiku nakukuta pembeni yangu. Lile kochi wameniambia linaweza kugeuka kitanda.
Lakini pale napaona mbali sana na wewe.” Nanaa akajifuta machozi. “Nitavuta
kiti angalau nilale hapo pembeni yako. Uniguse tu. Labda nitalala.” “Labda ukilaze kichwa hapa pembeni yangu.” Nanaa akatoa wazo. “Labda hivyo.” Akavuta kiti
mpaka karibu kabisa ya kitanda cha Nanaa. “Hapa sawa. Ngoja nikasafishe meno,
nije tulale.” Nanaa alibaki akimwangalia kwa kumuhurumia.
Ndoto Ya Kwanza Ya Vita Ya Nanaa.
Walilala
wameshikana mikono. Nanaa akageuka upande aliokuwa amekaa Geb. Alimchezea
nywele mpaka akamsikia anahema kama aliyepotelea usingizini. Na yeye akafunga
macho. Akiwa anapitiwa na usingizi, akaona amechukuliwa kutoka pale kitandani
mpaka juu kabisa ya mlima. Akawa amesimama peke yake. Hali ya mahali pale
akaifurahia sana. Mara akasikia mshindo na kelele kama ya watu wanaopigana sana
chini ya ule mlima aliosimama. Kwenye bonde. Akataka kushuka ili akaangalie
kulikoni, sauti ikamwita na kumkataza asishuke. Akiwa katika hali ya
kutofahamu, kwa kuwa sauti ya vita ilizidi kupanda kutoka bondeni, sauti ya
mapanga makali yakisikika yakisuguana, ile hali ya utulivu pale juu mlimani
ikaanza kupotea. Nanaa akakosa raha kabisa.
Akatamani
kuondoka kabisa sehemu ile kwa hofu, kwani cheche za moto zilianza kupanda
kutoka chini kuashiria ni misuguano mikali ya yale mapanga. Akageuza uso wake
ili akimbie akiwa na hofu kubwa, akasikia sauti ikimwambia, “Usiogope. Yupo anayepigana badala yako.” Nanaa
akashituka kutoka kwenye yale maono. Akakaa huku machozi yakimtoka.
Akamwangalia Geb, alikuwa amelala kabisa. Akatamani kujifunua miguu yake ili
ajiangalie. Akaogopa. Akabaki amekaa akitafakari kile alichoona. Asijue kama ni
ndoto, au ni maono. Lakini bado mwili wake ulikuwa ukitetemeka asijue afanyaje
na ile ndoto. Akatamani angekuwa na simu, ampigie mama G, lakini Geb alishazima
simu ya Nanaa tokea mchana, ili asisumbuliwe na mtu yeyote.
Akamwangalia
tena Geb. Akatamani amwamshe ili amsimulie, lakini Geb alikuwa amelala kabisa.
Tena alionekana amechoka. Nanaa akamuhurumia. Akakumbuka siku nzima alikuwa na
kazi ya kumliwaza yeye na kuzungumza na madaktari na kila muuguzi aliyekuwa
akimuhudumia yeye. “Anahitaji
kupumzika.” Nanaa akawaza.“Mimi ndiye
niliyeambiwa nisiogope. Lazima nitulie. Nitafakari mimi mwenyewe. Niombe?”
Nanaa mtoto aliyezoea kwenda kanisani tokea mtoto, hakuwa akijua cha kufanya.
Tokea yupo mdogo, akiwa nyumbani kwa mama yake mkubwa, ilikuwa ni lazima siku
ya jumapili kwenda kanisani. Lakini hakuwahi kuwa na mahusiano binafsi na
Mungu. Hata hakuwa akijua ikitokea anakutanishwa na Mungu, anatakiwa afanye
nini.
Akatamani
aombe. Lakini anaombea nini? Ndilo swali likaanza kumuumiza.
“Au nimuombee yule niliyeambiwa anapigana vita kwa ajili
yangu? Akishindwa?” Hofu ikaanza kumsumbua. Lakini
akakumbuka aliambiwa asiogope. “Inamaana
atashinda?” Akajiuliza. “Kwanza ni
nani anayepigana vita badala yangu?” Akazidi kuwaza. Akili zikaanza kufanya
kazi. Akaanza kutafakari mahusia aliyokuwa akihusiwa na Grace, mama G na Geb.
Akaanza kutafakari kitu kimoja hadi kingine.
Machozi
yakaanza kumtoka taratibu. “Huu ni wakati wangu wakusimama mimi kama
Nanaa. Lazima nipambane kwa ajili yangu, Geb na watoto wangu.” Akakumbuka mimba aliyonayo. Akajishika tumbo. Maneno
ya Geb kuwa Mungu amemtumia kicheko wakati wa huzuni yake, yakamrudia.
Kwa mara ya kwanza, akiwa hajiwezi, Nanaa mbele za Mungu wake apata
muda wakushukuru.
Machozi
ya faraja yakaanza kumtoka. Moyoni akajisikia kushukuru. Akajikuta akitamka
shukurani zake mbele za Mungu huku akilia. Alitamani ile hali ya shukurani
ingemjia masaa machache kabla hajapata yale maradhi. Ili aweze kupiga magoti,
kumsujudia Mungu wake kwa matendo makubwa maishani mwake. Akajaribu kusogeza
miguu, akagundua bado imekufa ganzi. Hakutaka kujifunua ajiangalie. Akakumbuka
ni muda mfupi tu kabla Geb hajalala, aliweka taulo safi. Akaona atoe mawazo
yake kwenye ile hali, ampe Mungu wake shukurani juu ya maisha yake.
Akamtizama
Geb, mwanaume aliyemzuri wa sura na akili. Ameacha kitanda cha mamilioni ya
pesa nyumbani kwake. Amelala kwenye kiti pembeni yake. Machozi yalizidi kumtoka
Nanaa. Akakumbuka wanawake wengi aliosimuliwa waliokuwa wakimtaka Geb. Tena
wengine waliomba kuzaa naye tu, bila kutaka matunzo ya huyo mtoto kutoka kwa
Geb. Ila mbegu zake tu. Lakini Geb amemchagua yeye! “Huyo ni wewe tu Mungu. Hakuna mwingine.” Nanaa
aliendelea kulia pale kitandani huku akimtizama Geb, aliyekuwa hana hata
habari.
Picha
ya Oliva akicheka ikamjia. Akakumbuka jinsi alivyokaa tumboni kwake akiwa
mgonjwa. Akafanyiwa upasuaji huku anapewa madawa mengi ya kukausha maji ya
mapafuni kwake. Na bado Oliva akazaliwa akiwa mzima. Hakuwahi kuumwa hata mara
moja mpaka pale alipofika na miezi 6. Uelewa mkubwa alio nao wakati ni mtoto.
Kila Geb alipompeleka kliniki, alirudi na habari kuwa mtoto wao yupo mbele ya
hatua anazotakiwa awepo.
Alianza
kutambaa akiwa bado mdogo. Alianza kumtambua mama yake na watu wote aliokuwa
akiishi nao mle ndani akiwa bado mdogo sana. “Hakika
huyo ni wewe tu Mungu. Si kazi ya mikono ya mwanadamu.” Nanaa
aliendelea kushukuru. Akajishika tumbo. Hofu ya ukuaji wa yule mtoto tumboni
kwake ikaisha. “Ulinipa Liv kwa upendo. Hakuna
daktari aliyejua, wala mimi kusema kuna kitu tulifanya ili mwanangu azaliwe
vile. Lakini Mungu, umethibitisha mkono wako juu ya Oliva. Natubu kwa hofu
iliyoniingia. Ulishanionyesha kuwa unaweza kunitetea hata kabla sijakuomba.
Umeshanionyesha wewe ndiye unapigana vita kwa ajili yangu. Hakika wewe ni Baba
yangu. Naomba nisamehe kwa kukutilia mashaka.” Nanaa akatubu sana. Akamsihi
Mungu amsamehe.
Hali
ya shukurani juu ya kile kiumbe kilichopo ndani yake ikamjia. Akajikuta
akicheka huku machozi yakimtoka. “Bado unanionyesha
unaniamini. Na nina uwezo wa kubeba uhai wa kiumbe kingine. Kwa nini mimi!?
Kama sio upendeleo wako kwangu? Nakushukuru Mungu wangu.” Nanaa
akamshukuru sana Mungu.
Akakumbuka
maono aliyoyaona muda mfupi uliopita. Akiwa juu sana. Ile hali ya utulivu na
amani aliyojisikia akiwa pale juu mlimani. Akakumbuka alikuwa amesimama!
Akacheka. Wazo likamjia na kumkumbusha, vita inayopiganwa kwa ajili yake,
ilikuwa mbali kabisa na yeye. Chini sana. Akakumbuka akiambiwa asiogope. Yupo
anayepigana kwa ajili yake. “Vita si yangu. Nasubiri ushindi wangu. Mungu wangu
hujawahi kushindwa. Nasubiria vita yangu iishe, nishuhudie ushindi wangu kwa
macho haya ya nyama.” Nanaa akawaza huku akicheka.
Akatamani arudishwe tena kule kwenye ile vita ili ajue inaendeleaje. Lakini
akajikuta macho yanakuwa mazito, akalala.
Asubuhi Ya Jumatatu Nanaa Alipokuwa Hospitalini.
Alihisi
mtu akimnyanyua miguu yake. Akashituka. “Geb!” “Pole, nimekushitua.
Nakubadilisha. Umelowa.” Akatulia. Akakumbuka miguu yake ndiyo inavuja maji.
Akatulia kidogo. Hofu ikataka kumsumbua. Akakumbuka usiku uliopita. Mwanga wa
jua ulikuwa umeshaingia ndani, kuashiria kumepambazuka. “Hata hivyo unatakiwa
kuamka Nanaa. Umelala sana.” Nanaa akacheka. Geb akamwangalia asiamini. Ile
furaha ya Nanaa ilitoka ndani, si usoni. Geb akamfunika vizuri. Akavuta kiti
akakaa pembeni yake.
“Naona uso mwangavu! Inaelekea ulilala
vizuri.” “Namshukuru Mungu, nimelala vizuri sanaaaa.” Geb akacheka. “Kweli
naona ni sanaaaaa. Danny amepitisha vyakula hapa, tumezungumza kidogo,
naona hata hujashituka!” “Sikuwa hata na habari!” “Ndio vizuri.” “Naomba ni
busu hapa.” Nanaa akionyeshea shavuni. “Kwa nini shavuni?” “Si ndio nimeamka
tu! Kinywa kitakuwa kinanuka.” Geb akasimama. Akambusu mdomoni.
“Asante
sana Geb. Namshukuru Mungu kwa ajili yako. Hata kama sababu zote hapa duniani
zikiisha zakumshukuru Mungu, lakini wewe, Oliva na huyu mtoto, mtabaki kuwa
sababu pekee maishani mwangu, ya kumtukuza Mungu wangu. Nyinyi ni muujiza wa
kwanza kwenye maisha yangu. Na ninajua Mungu ataniletea miujiza mikubwa zaidi
maishani mwangu.” Geb aliona kitu cha tofauti kwa Nanaa. Akabaki akimsikiliza.
“Nakupenda Geb. Na kitendo cha kuwa na mimi hapa, wakati huu ukinihudumia bila
kuchoka, hakika nitakienzi milele. Na Mungu atakubariki.” Ilimgusa sana
Geb.
“Kuna
kitu cha tofauti kwako Nanaa! Nini kimetokea huko usingizini?” Geb aliuliza na
tabasamu. “Usiku wakati umelala, nimepata muda mzuri sana na Mungu wangu.
Lakini ni baada ya yale Mungu aliyonionyesha.” Akamsimulia Geb kila kitu. “Sala
zetu zimefika mbele za Mungu, Nanaa. Mungu amekutumia mtu wa kupigana vita
yako.” Geb na yeye akajawa na furaha sana. “Hakika ipo nguvu ya maombi Geb.
Natamani tungeanza zamani!” “Nafikiri hatujachelewa. Kila jambo lina wakati wake.
Naamini huu ndio wakati uliokubalika na bwana. Kuna jambo mama alinifundisha
juu ya ndoto.” Geb akajiweka sawa.
“Aliniambia
kila unapoota ndoto. Kama ni nzuri, unajiunganisha nayo. Na kumuomba Mungu
akulinde mpaka ushuhudie kwa macho, yale uliyoyaota. Kama ni mbaya, unaikataa
na kumuomba Mungu aifute kwenye maisha yako. Basi tuombe kwa kifupi, kisha
nikusafishe kinywa, upate kifungua kinywa. Mama amekupikia vitu kama mzazi!”
Nanaa akacheka. “Amepiga simu na kusisitiza unywe. Maziwa yakitoka, tukamue halafu
tuyamwage. Anasema tusiache yakauke. Ili Oliva aendelee kunyonya ukitoka hapa.”
Nanaa akatulia kidogo. “Umeambiwa usiogope Nanaa. Na yupo mtu anapigana kwa
ajili yako. Amini hapa hatutakuwepo kwa muda mrefu. Utatoka, na Oliva
ataendelea kunyonya kama ulivyopanga.” “Na mtoto huyu wa tumboni?” “Atamkuta
dada yake akinyonya.” Wakacheka. “Haya tuombe.” Geb akapiga magoti palepale
pembeni ya kitanda, akamshika mkono Nanaa, wakaanza kuomba pamoja.
~~~~~~~~~~~~
Nanaa
na Geb walishinda vizuri. Madaktari walipita kumungalia Nanaa. Bado hawakujua
jinsi ya kumsaidia kwa kuwa vipimo vilizidi kuonyesha hana tatizo. Na Nanaa
mwenyewe alikataa kunywa dawa yeyote kwani alisema hana maumivu popote.
Ikabakia kipimo kimoja ambacho ni cha yale maji yaliyotolewa na kwenda
kufanyiwa uchunguzi.
Walikuwa
wakiongea mambo yao huku wakicheka. Walipata muda wakusoma neno kwa pamoja. Geb
akawa anaendelea kufanya kazi zake kwenye kompyuta yake huku akiongea na watu
wa ofisini kwake. Alipiga simu huku na kule. Nanaa akamsikia akizungumza na
Grace pia. Akajua mambo yanakwenda vizuri. Akabaki ametulia pale kitandani.
Mama
G akaingia na Oliva akiwa amelala. Nanaa akacheka alipomuona. “Umemsuka vizuri!
Kimependa ki binti Magesa!” “Nimeona tunasumbuana kuchana. Nikaamua kumsuka
hayo mabutu sita. Grace alimnunulia hivyo vibanio muda mrefu tu. Leo ndio
tumemfunga.” “Hakulia?” “Anavyopenda urembo huyo! Alikuwa ametulia tuli.
Alivyokuwa akitaka kujishika kichwani, Grace alikuwa akimwambia subiri kwanza
mpaka amalize. Basi akawa anacheka kama anayeelewa vile! Mpaka tukamaliza.
Grace akamuweka hivyo vibanio bila shida. Akawa anamwambia asivitoe. Naona
hajatoa.” Nanaa akacheka. “Amependeza kweli! Asante mama. Naona na hereni
mpya!” “Sasa hujamuona shingoni na mkononi. Unamtaka bure. Usicheze na kina
Oliva Magesa. Tupo wawili tu mjini.”
Mama G akaanza kujisifia. Nanaa akacheka sana.
“Mwenyewe
huyo!” “Kumbe! Ushakutana na Oliva Magesa mwingine?” “Hata mara moja. Ni nyinyi
tu wawili.” Nanaa akajibu. “Ndio maana yake, na wala hatakaa akatokea
mwingine.” Nanaa akazidi kucheka huku Geb akimsikiliza mama yake anavyojisifia.
Akasogea kumchungulia mwanae aliyekuwa akisifiwa. Bado alikuwa amelala pale
kwenye kigari chake. Akavuta kidogo ile cheni shingoni kwa mwanae ili aione,
akabaki akiangalia. “Nzuri sana mama. Asante.” Geb akashukuru. “Karibu.” Mama G
akajibu.
Kisha
akamgeukia Nanaa. “Haya vipi Nanaa. Naona uso wa furaha. Mambo yameendaje?”
“Mwenzio nimeona maono mama. Nusu nikupigie simu usiku.” “Sasa kwa nini
hukupiga!?” “Geb alichukua simu yangu. Amezima. Amesema nitulize mawazo.”
“Haya. Anza.” Nanaa akaanza kucheka. “Unanicheka?” “Mama na wewe unapenda stori
kuliko mimi!” “Sikufikii Nanaa. Wewe unaweza kuweka mtoto chini ili usikilize
umbea.” Wakacheka.
Nanaa
alimsimulia mama G kila kitu. Akamuona machozi yanamtoka yule mama. “Mungu wetu anaishi Nanaa. Hasinzii wala
hachoki kama sisi. Mungu wetu yupo vitani. Amekuahidia ushindi.” “Kabisa mama. Yaani sina hofu hata.” Wakacheka
kidogo, mama G akajifuta machozi. “Nakuona. Na hiyo ndio silaha kubwa sana ya
kumshinda shetani. Kutokuwa na hofu. Na ndio uponyaji wako ulipo.” Mama G
akakaa na Nanaa na kuzungumza naye sana huku akimtia moyo yeye na Geb.
~~~~~~~~~~~~
Baada
ya masaa mawili Oliva akafungua macho. Akakuta baba yake akimwangalia. Akacheka
akiwa anatoka usingizini kama ambaye hakutegemea kukutana na sura ile.
“Umependeza Liv! Umependeza sana binti yangu. Hakika wewe ni mrembo.” Geb akamsifia.
Liv akazidi kucheka huku akionekana na usingizi. Bado Geb alikuwa akimtizama na
tabasamu usoni. “Mlimpiga picha?” Geb akauliza. “Si unajua Grace anavyopenda
kumpiga picha? Kampiga picha nyingi kweli.” “Njoo mama yangu mzazi. Nina hamu
na wewe!” Geb akamtoa kwenye kiti chake. Akamuweka kifuani kwake, akamkumbatia
kwa muda huku akisikilizia ile furaha. Liv alishazoea kufanyiwa hivyo na baba
yake. Wakati wote Geb alimuweka kifuani kwake na kumkumbatia kwa muda huku
akigugumia. “Mmmmmmmmmh!” Kisha
anambusu mara kadhaa. Liv hucheka sana huku akimwangalia baba yake. Ndipo
mengine yanaendelea.
“Sasa
mimi niwaache. Nitarudi baadaye kuja kumchukua huyo dada. Nikamalizane na mama
James. Na huyo Zinda anayejidai ni mumeo.”
“Pole kwa usumbufu mama.” “Wala usijali. Yataisha tu Nanaa. Na wewe
utapumzika kwako. Siku moja utasahau yote haya.” “Naamini hivyo mama yangu.
Nakuombea hekima ya Mungu ili ukafanikishe kila kitu huko kwenye hicho kikao.”
“Na kweli nahitaji hekima ya Mungu. Na nimefunga kwa makusudi kwa ajili hiyo.
Maana wamenikera kweli! Naweza nikaenda kuwachachafya, wasikae wakanisahau
maisha. Heri Mungu akaingilie kati.” Nanaa akacheka. “Nakuaminia mama yangu.”
Mama G akacheka. Geb akabaki akimwangalia mama yake.
“Leo
nikirudi hapa, nataka niwe nimefika mwisho na Zinda. Kama na mahusiano
yanakufa, acha yafe. Amefika mbali sana. Sitaruhusu aharibu maisha yenu.” “Utafanyaje
mama?” “Tutampa muda wa kutoa vithibitisho vyake. Na kujieleza. Tutakapofikia
mwisho wa ushahidi wake, ndipo nitakapomuomba nizungumze naye. Hakika hatakaa
akanisahau. Yeye si anajidai mlevi? Sasa leo atapambana na mimi. Hana adabu
kabisa.” Nanaa aliendelea kucheka.
“Wewe
cheka tu. Mumeo anakuita.” “Akuuu! Mimi mume wangu Geb. Hata wakisema
nimempendea pesa, sawa tu. Lakini mwambie mimi mke wa Geb. Akubali, akatae.
Atajijua mwenyewe!” “Mimi naona twende wote.” “Sitaki mama.” “Si ndio ukamkatae
mbele za watu!” “Mimi nakuaminia mama yangu. Wewe nenda ukaniwakilishe.” Mama G
akacheka na kutoka.
Kikao Cha Kesi Ya Kipingamizi Cha Harusi Ya Nanaa&Geb.
Mama James!
Mama
G alifika pale kanisani akiwa nje ya ofisi ya mchungaji akasikia sauti ya mama
James akiongea ofisini kwa mchungaji. Alilalamikia hili na lile juu ya Nanaa.
Jinsi alivyo binti mbaya. Muhuni. Hana shukurani na mambo mengi ya kumchafua.
Wakati anataka kuingia ndani, akaona gari ya James na Danny na zenyewe
zimeongozana. Wakaingia ndani ya uzio wa kanisa. Wakaegesha magari yao pembeni
ya gari ya mama G. Wakashuka wote wakamsogelea mama G.
James
akamsikia mama yake ndani akiongea vibaya sana. Akaingia kwa haraka bila hata
kumsalimia mama G. “Naomba unyamaze mama. Tafadhali sana. Nyamaza.” “Nataka
pesa yangu.” Mama G akaingia. Akamkuta mchungaji na wazee wa kanisa mle ndani.
Wote walikuwa kimya wakimsikiliza huyo mama. James alijisikia vibaya sana.
“Jamani naombeni mumsamehe mama yangu. Sijui amepatwa na nini!” “Shika adabu
yako James.” Mama yake alimkatisha.
“Jamani,
naomba tusiendelee kumpotezea muda mama James. Aongee kiasi cha pesa anachotaka
alipwe. Tumalizane leo.” Mama G akawakatisha wote. “Eti mama James? Umekataa
kuwa hukupokea kiasi cha milioni 30 kama malipo yako ya kumlea Nanaa?” “Mimi
nilitaka milioni 100. Ndio mkaomba niwapunguzie. Nikawafanyia milioni 50.
Nashangaa mnanizungusha! Mnataka Nanaa aolewe bila kunilipa! Mnafaidi matunda
ambayo hamkupa…” “Kwa hiyo ulipokea milioni 30 au hujapokea?” Mama G
akamkatisha kwa kumuuliza tena swali. “Iko wapi sasa hiyo nyingine?” Mama James
hakutaka kukiri.
“Mama,
wanataka kujua kwanza juu ya ile pesa waliyokuletea Moshi. Wanataka ukiri wako
kama ulipokea au la. Maana jana ulimwambia mchungaji hukupokea.” James naye
akaingilia. Yule mama akaanza kuwaka kama mkaa. “Huo ndio umbea. Mchungaji
anatakiwa awe na kifua cha kubeba mambo siyo..” “Nisikilize mama James. Hakuna
mwenye muda wakupoteza hapa. Nataka kujua kama ulipokea hiyo pesa au la. Basi.
Hatutaki fujo hata kidogo. Wote tunakuheshimu. Na binafsi ninakushukuru kwa
kumlea Nanaa.” Kidogo yule mama akatulia.
“Maana
mnaweza kusema natanguliza pesa mbele. Sio utu.” “Hapana. Wewe tuambie kama
pesa ya kwanza ulipokea?” “Ndiyo. Bado milioni 20. Ni jasho langu. Nilihangaika
sana kumlea huyo mtot..” “Basi. Pesa yako iliyobaki hii hapa.” Mama G akatoa
ile hundi. Akaiandika vizuri. Akamuonyesha. Akataka kuipokea. “Kabla hujaipokea
hii pesa. Nataka upokee kalamu na karatasi kutoka kwa mchungaji. Andika majina
yako yote. Na ueleze kuwa tarehe ya leo umepokea kiasi cha milioni 50. Kwa
malipo ya kumlea Nanaa. Humdai tena Nanaa.” Mchungaji akampa kalamu na
karatasi. Yule mama akapokea kwa haraka sana bila hata shida. Akaanza kuandika.
James alibaki akimwangalia mama yake, asiamini anachokifanya.
Akamaliza.
“Naomba pesa yangu.” Yule mama akanyoosha mkono. Mama G akapokea kwanza ile
karatasi. Akasoma. Akaridhika nayo. Akamwangalia. “Sasa nakupa onyo, mama
James. Nanaa ameokoka. Na analindwa na Mungu. Usithubutu kumsogelea kwa aina
yeyote ile. Iwe kichawi au..” “Mimi nilipo hapa, hata mganga simjui! Mdomo
wangu ndio mganga wangu na Yesu wangu.” Mama James alijibu kwa kujiamini. Kila
mtu akatingisha kichwa kwa kumsikitikia. Lakini mama G akawa amepata jibu kuwa
Mama James hausiki katika ushirikina.
“Hundi
yako hii hapa. James atakupa tarehe ya harusi ya Nanaa. Tungependa kukuona.”
“Ili mniringishie?” Mama James akauliza kishari huku akisimama. “Sina shida.
Nimekabidhi mzigo. Simtaki huyo mtoto. Kwanza anamkosi. Simtaki karibu yangu
wala wanangu.” Yule mama akatoka.
Ukimywa
wa muda ukatanda. “Naombeni mtusamehe mimi na mama yangu. Samahanini sana.”
“James, wala usiwe na wasiwasi. Hilo limeshapita. Kuwa na amani kabisa
mwanangu. Mimi bado nakuhesabu kama mtu muhimu sana kwenye maisha yetu. Na ujue
Nanaa anakuhitaji sana, zaidi sasa hivi. Usikubali hili jambo likakuondolea
ujasiri wa kuwa karibu na Nanaa. Umemsikia akikutaja wewe kama baba yake.”
“Daaah! Lakini najisikia vibaya sana mama! Sipati usingizi. Natamani kama
ningesaidia kidogo tu. Lakini uwezo sina mama yangu.” “Nanaa sio jukumu lako
tena James. Mlishapokea mahari. Kimila Nanaa ni mke wa Geb. Huwezi kuendelea
kutunza mke wa mtu. Geb hawezi kukubali hata kama ungekuwa na uwezo.
Halafu ujue kabisa, nafasi ya Nanaa kwenye maisha yetu ni kubwa
kuliko unavyofikiri.” Mama G akakaa.
James
akamwangalia mama G, kama asiyeelewa. “Geb ndiye mtoto wa kiume wa pekee kwa mzee
Magesa. Yeye ndiye anayebeba jina la baba yake. Kwa Nanaa kuendelea kumzalia
watoto vile, kwa Geb ni fahari kubwa sana. Kama hufahamu hilo, nataka
leo uelewe. Kwake Nanaa ni mtu wa thamani sana. Anaendeleza ukoo
wa Magesa kitu kilicho muhimu sana kwa Geb na kwetu pia. Hakuna
pesa atakayoiona ni kubwa Geb kwa Nanaa. Na ujue Geb anafanya kama vile baba
yake anamwangalia. Yupo makini sana na kila hatua anayochukua. Kwa hiyo
ujue anafanya kila kitu kwa ajili ya heshima ya baba yake. Hawezi akaruhusu
mtu aingilie hilo, hata iweje. Hata ungekuwa wewe ni milionea wa vipi,
Geb asingekubali umlipie Nanaa pesa. Anaona kuruhusu hilo ni kumwaibisha
baba yake, au kumwambia baba yake wosia wote na mambo yote aliyomfundisha ameshindwa
kwa kiasi cha juu sana.” Mama G akaendelea.
“Magesa
alimpata Geb kipindi cha uzee wake. Alijua atakufa na Geb akiwa ndio mtoto wake
wa pekee wa kiume. Alikuwa akimfundisha Geb kwa maneno na vitendo. Mchana na
usiku. Hata alipokuwa amelazwa hospitalini, Magesa alikuwa akizungumza
na Geb kana kwamba anaongea na mtu mzima. Walikuwa wakiachana jioni, anamwambia
akirudi kesho yake, arudi na maswali yote ambayo anafikiri atahitaji kumuuliza
miaka labda 10 au hata 20 ijayo. Yoyote yale. Uchumi, mahusiano, kila swali
alimtaka Geb aulize. Na kweli Geb alikuwa akimpa maswali mazito mpaka
wakati mwingine nilikuwa nikimtoa Grace nje ili kuwapa nafasi yakuzungumza.
Naweza kusema Magesa alizungumza na Geb kuliko mtu yeyote yule, au hata zaidi
yangu. Mpaka kifo chake, Geb alikuwa pembeni ya baba yake akimsikiliza.
Nahisi ndio maana akili ya Geb ilikomaa mapema sana, sababu ya baba yake.” Wote
walikuwa wakimsikiliza mama G.
“Kwa
hiyo naomba uwe na amani kabisa. Hata Danny alitaka kumsaidia, Lakini amekataa
kabisa. Mimi mwenyewe amekataa nisimsaidie hata nusu ya mahari yake kwa Nanaa.
Pesa za mablangeti na vitenge nilivyokuwa nimenunua kwa pesa yangu,
amenirudishia yote kama ilivyo. Aliniambia ni baba yake ndio alitakiwa kumlipia
mahari. Kwa kuwa baba yake alimpa yeye jukumu la ukoo, basi yeye mwenyewe
atalipa mahari ya Nanaa. Kwa hiyo uwe na amani tu. Wala usijisikie mnyonge. Hakuna
utakachofanya tena kwa Nanaa, Geb akakuruhusu. Ameshajihesabu jukumu la
Nanaa ni lake kama vile alivyo Oliva. Jana aliniambia anasubiri mambo yatulie, akambadilishe
Nanaa jina, aitwe Nanaa Magesa. Ndio ujue mawazo ya mwenzio yalivyo.” Kidogo
watu wakacheka, na James akatulia. Maongezi mengine yakaendelea wakati
wanamsubiri Zinda.
Hakuna Msiba Usiokuwa na Mwenzie.
“Zinda.”
Wakati
wakizungumza wakasikia mlango unagongwa, Zinda akaingia akiwa na sura ya
hasira. “Huu ndio uthibitisho kuwa Nanaa ni mke wangu halali.” Zinda akatupa
cheti cha ndoa mezani, bila salamu wala tabasamu. Kila mtu akashangaa.
Hawakutegemea. “Sasa semeni jingine.” Akaongeza. Mchungaji akaokota kile cheti,
akaanza kukisoma. Kilikuwa cheti cha ndoa halali. Na kilionyesha walifunga ndoa
mahakamani.
“Ni
kweli hiki cheti kinaonyesha Zinda ni mume halali wa Nanaa.” Mchungaji aliongea
huku akiendelea kukikagua kile cheti. “Naomba kukiona na mimi.” James akasimama
na kwenda kukifuata. Moja kwa moja akakimbilia kwenye tarehe. Akasoma kwa
makini. Wakaona anacheka. “Kweli unatumia urafiki wetu vizuri sana Zinda.”
James aliongea huku akimkabidhi Danny kile cheti.
“Tokea
siku uliponisaliti wewe na Danny, mkijua jinsi nilivyohangaika na Nanaa. Lakini
kwa kuwa mimi sina pesa kama Geb, mkaamua mumtoe Nanaa kwangu na kumpa Geb
mwanamke wangu, mmetangaza vita na mimi, James. Mimi sio rafiki yenu. Na
ninawahakikishia, tutapambana kufa na kupona hapa mjini. Nitafika popote
itakaponilazimu, lakini nawaambia Geb hatamuoa Nanaa.” Zinda alibadilika.
Hakuwa Zinda wanae mfahamu.
Danny
na James walibaki wakimtizama. Danny akarudisha macho kwenye kile cheti.
Akatingisha kichwa. “Jamani mimi nina swali kwa Zinda. Sijui naruhusiwa
kuuliza?” Danny akaongea. “Karibu.” Mchungaji akamruhusu. “Unamkaribisha Danny
kuuliza swali hapa kama nani?” Zinda akaingilia. “Basi hakuna shida. Ila naomba
mchungaji zingatia mambo yafuatayo kutokana na hichi cheti cha ndoa, na
ninaomba muulize wewe Zinda haya maswali. Kutokana na tarehe hii iliyopo kwenye
hichi cheti cha ndoa, inaonyesha tarehe
hii 23/10/2017, nchini Kenya, ndipo Nanaa na Zinda walipofunga ndoa yao. Kitu
ambacho nakuhakikishia sio kweli. Nanaa alikuwa yupo chuo kikuu cha Mlimani.
Anamalizia shahada yake ya mwisho! Tena akiwa mjamzito wa mtoto wa Geb. Nanaa
asingeweza kusafiri akiwa mjamzito wa mtoto wa mwanaume anayempenda, Geb, na
kwenda kufunga ndoa na Zinda. Hiyo ni moja. Kutoka tu kwenye hiki cheti.” Danny
akaendelea.
“Pili.
Nanaa kama msomi wa chuo kikuu, kwa nini hapa aweke saini ya dole gumba, badala
ya saini yake halali? Achana na swali atakalokuja kuuliza James, yeye ambaye
Nanaa anamtambua kama baba yake, atauliza mahari hiyo kama mila ya kitanzania,
alimpa nani mpaka akapata ruhusa ya kumuoa Nanaa? Naomba umuulize hilo swali
Zinda.” Danny akamaliza na kumpa kile cheti cha ndoa mama G.
Mama
G akaanza kukiangalia. Kilionyesha ni cha kutokea nchini Kenya. Mama G akaanza
kutingisha kichwa. Zinda alikuwa ametulia kana kwamba hakumsikia kabisa Danny.
Mchungaji akayaweka yale maswali sawa, akamuuliza Zinda. “Naomba kama utaweza
kukaa, ukae Zinda ili tuzungumze vizuri.” Mchungaji alizungumza kiustarabu.
“Mimi nipo sawa tu. Naweza kuongea wakati nimesimama.” Zinda akajibu kwa jeuri.
“Kujibu
swali lako la kwanza mchungaji ni hivi, baada ya Nanaa kuniambia hatutaweza
kuwa na mahusiano wakati ule, nikatulia. Siku moja ya harusi ya aliyekuwa
rafiki yetu, Malii. Nanaa akiwa ameachwa nje, usiku kwenye baridi, na hawa watu
wote hao wanajidai sasa hivi ni ndugu zake Nanaa, pamoja na Geb anayedai Nanaa
ni mkewe, mimi nilimkuta Nanaa nje peke
yake. Nilitoka ukumbini, nikiwa naelekea msalani. Watajwa wote hapo juu
walikuwa wakila na kucheza ndani wakati Nanaa wamemsahau nje ya ukumbi.
Nilimkuta akiwa anateseka nje na baridi. Nikamvalisha koti langu. Nikamwambia
anisubiri wakati naelekea msalani ili nikitoka nimuingize ndani. Lakini
sikumkuta. Nikauliza, nikaambiwa alishaondoka. Kumbe alizidiwa akaokwatwa na
watu wakampeleka hospitalini. Hao wote hapo, mpaka huyo anayejiita baba yake
Nanaa, walikuwa wakisherehekea ndani wakati wamemsahau nje ya ukumbi, Nanaa
wanayejidai kumgombania leo.” Zinda aliongea vizuri bila hofu.
“Kufupisha
habari ndefu, Nanaa ambaye ni mke wangu, akiwa hospitalini, alihudumiwa na
huyo mwanamke aliyemuoka siku hiyo
walipomsahau nje mpaka akapona na kuhamia nyumbani kwa huyo mama kuishi naye.
Awali alikuwa akiishi nyumbani kwa hawa
matajiri unao waona wamekaa hapo, nyumbani kwa Geb. Lakini Nanaa akaamua
kuhama kwao na kwenda kuishi kwa huyo mama sababu ya ubaya wa hawa watu
waliomtendea. Akakata mawasiliano na hao wote walio kaa hapo, mpaka na Geb
aliyekuja kumfumania baadaye.” Danny na James hawakuwa wakiamini.
“Nanaa
akiwa ameumia sana, akanitafuta ili anirudishie koti langu nililokuwa nimempa
siku ya harusi akiwa ameachwa nje. Nafikiri mnakumbuka. Aliniomba tukutane kwa
chakula cha mchana. Tukakutana. Tulipata muda mzuri sana. Akanieleza masikitiko
yake ya usaliti aliofanyiwa na hao watu wote. Kuanzia mama yake Geb aliyekuwa
ndiye muhusika wa kwanza, aliyemuacha nje. James ambaye alidhani ni
kama baba yake. Geb aliyekuwa amemdanganya anampenda, lakini akamfumania
na mpenzi wake aliyekuwa amemdanganya Nanaa waliachana. Kumbe Nanaa
alikuja kugundua ilikuwa ni janja ya kumuweka tu kitandani. Nanaa akaniambia
baada ya Geb kufanikiwa kulala naye, ndipo alipoanza kumfanyia vitimbwi. Hakuwa
akimjali kwa dhati. Ikiwemo kuwepo kwenye kumbi wa harusi na mpenzi wake, badala
yake yeye Nanaa. Nanaa alijua wazi Geb alifanya makusudi kutomwingiza
ukumbini. Waligawa kadi kwa watu wote. Mpaka marafiki wa karibu, kasoro
Nanaa, ili asiingie ukumbini, awe na Liz mpenzi wake. Na mama yake Geb analijua
hilo.” Mama G alibaki akimtizama Zinda asiamini.
“Hata
ukitaka ushahidi wa Liz nitaleta. Liz alikuwa mpenzi wa halali wa Geb. Na
alikuwa akienda kulala nyumbani kwa Geb, mama yake Geb akiwepo! Nanaa pia
alikuwa akiishi hapo hapo. Na ndugu zake Geb. Hata huyo anayetambulishwa kwenu
kama baba yake Nanaa, anajua kama Liz alikuwa mchumba wa Geb, na walikuwa ni
kama wakiishi pamoja! Sasa utawauliza kwa wakati wako mapenzi au mahusiano hayo
ya Geb kwa Nanaa yalianza lini? Wakati Geb alikuwa akilala na mpenzi wake
kwenye nyumba hiyohiyo aliyokuwa akiishi Nanaa na wote hawa kasoro huyu
anayejiita kama baba yake Nanaa, japo alikuwa ni kama akiishi hapo maana kula
yake pia alitegemea hapo nyumbani kwa tajiri yao Geb?” Zinda akawa amemtukana
na James kwa makusudi tu, akionyesha wote wapo mjini kwa nguvu ya
Geb, mwanaume mwenzao. Hawakumuingilia, wakamuacha tu aendelee.
“Turudi
kwenye habari yangu mimi na mke wangu.” Danny alicheka na kutingisha kichwa. “Siku
hiyo Nanaa aliponiomba tukutane ili anirudishie koti langu, tulipata muda mzuri
sana kama nilivyotangulia kusema. Penzi jipya likazaliwa. Yakaanza mahusiano
kati yetu, lakini alinisihi nisimwambie hata James, kwa kuwa hawakuwa
kwenye mawasiliano yeyote yale. Na akasema hamtaki tena James kwenye
maisha yake. Nikakubali, sisi tukaendelea.”
“Nanaa
alipojigundua ana ujauzito wa Geb, aliogopa sana. Akataka kuitoa ile mimba.
Nikamwambia asiue kiumbe kisicho na hatia kwa kosa la baba yake. Nikamwahidi
kuwa nitakuwa tayari kumtunza yeye na mtoto. Na kumuhakikishia hivyo,
nikamwambia nipo tayari kufunga naye ndoa.” Zinda akaendelea. “Swala likawa
jinsi ya kulipa mahari. Nanaa akakataa kata kata nisimshirikishe kaka yake
huyu, ambaye mmetambulishwa kwenu kama baba yake. Akanipeleka kwa mama
yake mkubwa Moshi. Ndipo nilipolipa mahari.” “Haiwezekani Zinda!
Unadanganya kabisa.” James akamkatisha. Zinda akatoa simu yake. Akapiga namba
fulani, ikapokelewa. “Naomba uingie ndani mama.” Akakata simu.
Hata
dakika moja haikuisha mama James akaingia. “Haiwezekani mama!” James akashituka sana. “Juu ya nini!?” Mama
James akauliza bila hofu. “Mama aliyemlea Nanaa tokea anazaliwa huyu hapa.
Muulize kama hajapokea mahari yangu.” Mchungaji alimwangalia yule mama, akabaki
ameduwaa. “Unafanya nini mama yangu!? Ni mchezo gani unataka kumfanyia Nanaa?
Hujatoka kulipwa pesa ya kumlea Nanaa muda mfupi uliopita?” James akamuuliza
akiwa anaonyesha kuumia sana mpaka uso wake ulibadilika.
“Mmenilipa!
Kwani nimekataa? Si ndio mnamtumia sasa hivi huyo Nanaa! Sasa mlitaka mfaidi
matunda msiyoyapanda wala kupalilia? Zinda aliletwa na Nanaa nyumbani.
Akamtambulisha kama mumewe mtarajia. Zinda akalipa mahari yote. Na picha za
ulipwaji mahari hizi hapa.” Yule mama akafungua mkoba. Akatoa picha. Wakaanza
kuzisambaza pale ndani kwenye ofisi ya mchungaji. “Nanaa yuko wapi hapa kwenye
hizi picha? Mbona kwenye picha zote mnaonekana wewe, Viola, Vai na Zinda tu?”
James akauliza.
“Kwani mwanamke muda ule anapolipiwa mahari
anakuwepo? Si anakuja baadaye baada ya taratibu za mahari kukamilika! Ungekuwa
umeoa, ungeyajua hayo.” Mama James alimjibu mwanae bila hofu wala kubabaika. Picha
zile zilionyesha vitu vyote vya mahari kama alivyotoa Geb. Yule mama na wanae
hao wa kike walionekana wakivipokea vile vitu hapo pichani.
“Ngoja
kwanza mama. Zinda anasema alitoa hii mahari Moshi. Sio kweli. Wewe na hao
wanao wa kike wote mlikuwepo nyumbani kwangu karibia mwaka jana mzima. Kwa nini
mnadanganya?” “Hayo yakuwa Moshi sifahamu. Ila ninachojua mimi Zinda
ndiye mume wa Nanaa kihalali. Kwa kuwa alinilipa mimi mahari, na kwenda kufunga
ndoa na Nanaa, nchini Nairobi Kenya. Tena Nanaa mwenyewe akisisitiza usiambiwe
kabisa.” Yule mama akamjibu James bila kupepesa kope.
“Kama
hamna la nyongeza, nataka kuondoka.” Alimgeukia Zinda. “Nakushukuru sana mama
yangu. Asante.” Zinda akampa mkono mama James. “Labda kabla mama James
hajaondoka. Naomba mchungaji muulize kama anakumbukumbu ya kupokea mahari ya Nanaa
hapo majuzi kutoka kwa Geb.” Danny akawahi. “Na kweli. Maana tulimfuata mpaka
Moshi kwenda kulipa mahari ya Nanaa. Na mimi nilikuwepo kupokea hiyo mahari
kutoka kwa Geb. Ni kwa nini alipokea mahari mbili mbili?” James naye akaongezea
swali, kwenye swali la Danny.
“Hivi
wewe James unalipwa na huyo Geb? Umekuwa wazimu wa kunigeuka hata mimi mama
yako? Nimesikia anakujengea na nyumba. Ndio sababu ya kunivunjia heshima mbele
za watu!? Unanihoji kutaka kunidhalilisha mimi! Sasa nakuonya James, shika
adabu yako. Utatembea uchi hapa mjini. Endelea kumtumikia mwanaume mwenzako.
Hata baba yako atasikitika sana.” Yule mama aliwaka kama sio yeye. Na alikuwa
akifanana na James, hakuna jinsi James angeweza kumkana mama yake pale
mbele ya watu. Alimrisisha rangi ya weupe. Alikuwa mweupe sana kama James.
Urefu na sura ya duara kama mwanae James.
James
alibaki akimtizama mama yake asiamini. “Ni nini mama yangu unafanya!? Huyu
Zinda amekulipa kiasi gani, kinachokufanya ukose utu kiasi hicho!?” “Sina shida
na kulipwa. Kwa taarifa yako tu, nina nyumbani kwangu hapo Ubungo maziwa.
Naishi na wanangu. Ninatarajia kufungua baa, ambayo itakuwa ikipigwa miziki Live
kila siku. Sasa nina shida gani? Kwa nini nipokee pesa kutoka kwa mkwe
anayejiheshimu kama Zinda? Na umwambie Nanaa, tamaa itamponza. Atahama nyumba
moja hadi nyingine sababu ya kupenda pesa. Mkumbushe kiapo alichomwapia mumewe
Zinda.”
“Subiri
kwanza mama. Yaani hii pesa uliyolipwa hapa majuzi na leo na Geb, ndiyo hiyo
inakufanya umwache baba peke yako huko Moshi, uje uanzishe biashara hapa mjini!?
Kwa nini usiende kufanyia biashara kulekule Moshi?” “Kwa hiyo unanipangia na ni
jinsi gani pia ya kuishi!? Kweli umelaaniwa wewe mtoto. Sasa kabla sijakuvulia
nguo hapa mbele za watu, naona niondoke.” Yule mama akatoka.
Walimuona James ameweka mikono
kichwani, machozi yakimtoka. “Sasa narudi kwako mchungaji. Ukitangaza tena ndoa
ya mke wangu. Ukitaka aolewe kwa mara ya pili. Ujue unatangaza vita na mimi na
vyombo vya sheria. Sitakubali. Nitakushitaki kwa kupokea hongo kutoka kwa hao
mamilionea. Najua unaweza kuingia tamaa kwa kuwa umeona wameweza kumlipa mama James
bila shida. Nashauri usifanye hivyo. Kanisa hili litafungwa. Nanaa ni mke wangu
kihalali. Awe ameweka saini ya dole gumba au ameandika, hilo ni juu yangu mimi
na Nanaa mwenyewe. Haimuhusu mtu yeyote. Na kuanzia sasa, sitaki usumbufu.”
Zinda akataka kutoka.
“Naomba
nikuulize swali la mwisho kabla ya kuondoka Zinda.” Mchungaji akamuwahi.
“Karibu.” Zinda akarudi. “Imekuaje kwa muda wote huo mkeo alikuwa akiishi na
Geb?” “Mpaka leo anaishi na Geb.” Danny aliongezea kwenye hoja ya mchungaji.
Wote wakamgeukia Zinda. “Kumbe sikumaliza habari nzima? Samahani sana.” Zinda
akajiweka sawa. “Baada ya ndoa yetu. Nikawa nikiishi na Nanaa nyumba moja huku
amechukua chumba hosteli. Tunalea mimba huku anasoma. Mimi ndiye niliyekuwa
nikimpeleka Nanaa chuoni na kumrudisha. Alipokaribia kujifungua, nikapata
safari ya gafla. Ikanibidi nisafiri lakini huku tukijua nitawahi kurudi kabla
Nanaa hajajifungua. Ndipo ikamlazimu Nanaa kuhamia tena hosteli ili asipate
shida ya usafiri.”
“Siku
ya pili yake baada tu ya mimi kuondoka, Nanaa akajifungua. Geb alipojua kama
Nanaa amejifungua, Nanaa akiwa kwenye mtihani, Geb akamwiba mtoto. Ndipo
ikabidi Nanaa amfuate nyumbani kwa Geb. Nanaa alinipigia simu nikiwa safarini
na kunisimulia mkasa mzima. Kuwa Geb amemfungia mtoto. Na kuweka ulinzi mkali
sana. Akampa sharti kuwa, anakaribishwa kumlea mtoto wake hapo ndani, lakini
haruhusiwi kutoka na huyo mtoto.” Zinda alijieleza bila shida.
“Niliporudi
safari tukaonana na Nanaa. Akaniambia ukatili anaofanyiwa mle ndani na Geb.
Lakini akanisihi tukubali tuvumilie tu, mpaka angalau atakapomuachisha mwanae
kunyonya ndipo atarudi nyumbani. Kwa hiyo tukawa tukiwasiliana na Nanaa, na
kukutana kila tunapoweza. Mwezi uliopita, Nanaa alinitafuta tena akiwa analia.
Akasema Geb anamlazimisha kufunga ndoa, lasivyo anamfukuza mle ndani. Kwa kuwa
hata hivyo mtoto ameshakuwa mkubwa, mama yake anaanza kumuanzishia mjukuu wake
chakula cha kawaida. Hana haja ya kunyonya tena. Kwa hiyo akamwambia Nanaa, kitakachomuweka
karibu na mtoto wake ni kama atakubali amuoe, lasivyo anamfukuza mle ndani.
Nikamtuliza Nanaa, na nikamwahidi kumtetea. Kwa hiyo mchungaji, nakutuma kwa
Geb. Mwambie hatakaa amuoe Nanaa. Mvua inyeshe, jua litoke. Hatamuoa Nanaa.
Kama nitamkosa mimi Nanaa, ajue na yeye atamkosa.” Hapo ndipo wakahisi pengine
Zinda anahusika na ugonjwa wa Nanaa.
“Kwa
hiyo wewe ndiye unayemtesa Nanaa sasa hivi?” Mama G akarusha swali. “Siwezi
kumtesa mke wangu! Hata hivyo kwa kuhamia kuishi kwa Geb, ameshajitengenezea
adui mmoja mkubwa ambaye ni mke halali wa Geb, katika ulimwengu wa kiroho. Geb
aliingia maagano na Mira. Katika ulimwengu wa roho Mira ni mke halali wa Geb.
Sasa labda huyo ndiye anayemtesa Nanaa. Mimi sihusiki na ugonjwa wake.” Bila
kujijua Zinda akajikuta akiropoka.
“Umejuaje
kama Nanaa ni mgonjwa Zinda!?” James akauliza akiwa ameshituka sana. Kimya.
“Zinda? Maana hakuna mtu yeyote anayejua kama Nanaa ni mgonjwa. Wewe umejuaje?”
Kidogo Zinda akababaika. Wote wakamwangalia. “Mchungaji, nimemaliza, naondoka.”
“Subiri kwanza Zinda. Mira ni nani?” Mama G akauliza. “Kamuulize mwanao. Lakini
ujue, ndiye mkweo wa halali. Hata mizimu inamtambua kama ni mkewe. Waliingia maagano.
Sasa kama ni mizimu inamrudi Nanaa, kwa kuvunja agano la watu, shauri
yenu. Sihusiki.” Zinda akatoka akiwa amezua jambo jipya kabisaa.
~~~~~~~~~~~~
“Mira ni nani?” Mama G akamgeukia Danny na
James. “Mimi simfahamu!” Danny akajibu. “Na wewe James?” “Na mimi ndio namsikia
leo. Sijawahi kumsikia hata mara moja.” James akajibu. Pakazuka ukimya. Kila
mtu alikuwa akiwaza lake. Zinda aliongea mambo yote kwa hakika na uthibitisho.
Nani anakana? Ni kweli kuna kipindi Nanaa alikataa kuonana na kaka yake James.
Walipoteza mawasiliano kwa muda mrefu tu. Alikuwa wapi? Zinda aliibua mambo
mengi yanayofanana na ukweli mtupu kama kuwasuta mama G, Danny na James. Na
kweli aliwafunga mdomo.
Waliishiwa
maneno kabisa. Vijana hao walikuwa marafiki wa muda mrefu sana. Tena waliokuwa
wameshibana. Hakuna walilokuwa wakifichana. Analolijua Danny ndilo atakalolijua
James, Zinda, Malii, Geb na kundi lao wote. Waliambiana na kushirikishana kila
kitu kwenye maisha yao. Angalau Geb alikuwa mkimya sana. Lakini kwa kuwa
alikuwa karibu na Danny mzungumzaji, hata yeye habari zake zilifikishwa na
Danny kwa kundi hilo. Bila kujijua, walijikuta hata mambo yao ya ndani sana ya
siri, yanajulikana na kila mtu zaidi Zinda ambaye ndiye alikuwa rafiki mkuu wa
Danny. Waliheshimiana kama ndugu wa damu. Danny hakuwahi kumnyima neno Zinda.
Walijua
kwa hakika Zinda anadanganya. Lakini ilikuwa ni ngumu kumkamata uongo wake kwa
kuwa aliongea uongo unao fanana na kweli tupu. Na kila neno aliloliongea
alilipata kutoka kwa Danny au James mwenyewe.
Au alishuhudia yeye mwenyewe. Walibaki wamekaa pale kwenye viti kila
mmoja akijiuliza lake. “Labda ni siku
ile nilivyomsimulia Zinda…?” Kila mmoja alijiuliza kimya kimya.
~~~~~~~~~~~~
“Jamani!
Kama mlivyoshuhudia kuwa Zinda ni mume wa halali wa Nanaa. Hatutaweza kutangaza
tena habari ya ndoa ya Nanaa na Geb labda
mpaka mtakapoleta uthibitisho
mwingine. Kama hati ya talaka ya Zinda na Nanaa.” Mama G akacheka. Akasimama. “Nashukuru
kwa muda wenu. Mungu awabariki.” Mama G akatoka. Danny na James wakamfuata.
~~~~~~~~~~~~
Wakajikuta
wamesimama pale nje kimya kila mtu akiwaza lake. “Zinda ametuweza. Ametumia
ukarimu wetu kwake, vizuri sana.” Mama G aliongea huku akiwaza. “Najuta!” Danny alijikuta akiropoka.
“Nahisi wewe hujuti kama mimi. Naumia sana.” James akaongeza. “Nisikilizeni
James na Danny. Zinda hakuwa adui. Zinda alikuwa ndugu yenu. Ndugu ambaye ni
rafiki wa karibu. Kuna mambo mengine mliongea kwake kwa imani mliyokuwa nayo
kwake. Leo amemruhusu shetani kutumia uaminifu wenu kufanya uovu.” “Halafu
umesikia mama? Mungu amemuweka wazi mbaya wa Nanaa?” Danny akaongeza. “Lakini
huyo Mira ni nani!?” James akauliza. “Geb ndiye atakayekuwa na jibu. Twendeni
tukamuulize.” Mama G akatoa wazo.
“Lakini naomba isiwe mbele ya Nanaa. Tutazidi kumuumiza.” James naye akatoa wazi.
“Basi tukifika, tumpigie simu Geb atoke nje. Tuongee naye.” Wakakubaliana na
wazo la mama G.
~~~~~~~~~~~~~
Zinda amewakilisha ushahidi wake. Mume halali wa Nanaa na mama James
kama mzazi husika wa Nanaa, amekubaliana naye. Nanaa hayupo kwenye nafasi ya
kupinga, ndoa imesitishwa.
Mira, ndiye anayemtesa Nanaa? Ni nani?
Usikose Muendelezo wa Kusikitisha na Kuumiza.
0 Comments:
Post a Comment