Geb naye alikuwa akilia kama mtoto pembeni ya
kitanda. Bado mama G alibaki ameduwaa. Grace akamfunika shuka Nanaa kama
kumsitiri, maana usiku uliopita Geb alimsaidia kumbadilisha nguo za kulalia. Na
nguo hiyo yakulalia ilikuwa ni kama imemuweka nusu uchi. Ilikuwa nyepesi sana.
Danny naye
akaingia. Grace akasimama na kuwatizama kwa zamu. “Kwanza naombeni wote mtoke.
Hasa wewe Geb na Danny. Nataka nimsafishe na kumbadilisha nguo. Nikikuita hapa
Geb, nataka uwe umetulia kabisa. Nisione chozi hata moja. Ukoje lakini, unakuwa
kama Fili!? Haya naomba mtoke. Danny na Geb tokeni.” Wakatoka.
Mama G akabaki amesimama kama sanamu. Hajajigusa
wala kuongea. Grace akamgeukia na yeye. “Kweli mama jamani!? Ni nini sasa!?”
Grace akamshangaa. “Yaani huu ndio unafikiri ndio muda wa wewe kuchanganyikiwa
wakati wote tunakuangalia wewe? Nanaa anakulilia na wewe ndio upo kwenye hali
hiyo! Hebu acha bwana!” Mama G ndio akawa kama aliyeamshwa kutoka usingizini. Akaingia bafuni
kwa Geb na Nanaa, akatayarisha maji kwenye beseni akatoka nayo kumfuta Nanaa
aliyekuwa akilia pale pale kitandani.
Wakati
ndio wanamalizia kumsafisha na kumbadili nguo, wakamsikia James ameingia. “Yuko
wapi?” “Juu chumbani kwao.” Danny akamjibu. Wakamsikia James anapandisha ngazi
huku anakimbia. Akagonga na kuingia. “Kaka mimi nakufa!” James
akaangalia ile miguu, haraka sana akambeba kumtoa pale kitandani.
“Unampeleka wapi James!? Ndio
tumemaliza kumsafisha mwili na kumvalisha. Hata chai bado hajanywa.” James
hakujibu, akatoka amembeba dada yake. “James!?” Grace akamuita. “Nampeleka
hospitalini.”“Hospitali gani?” “Nitawajulisha.” James akajibu huku akiendelea
kushuka ngazi huku amembeba Nanaa aliyekuwa akilia. Baada ya muda mfupi sana
wakasikia gari ya James inatoka getini kwa kasi. Ndipo akili zao zikaanza
kufanya kazi sasa. Bado Geb alikuwa kwenye nguo zake za kulalia
~~~~~~~~~~~~~
Geb
akakimbilia chumbani kuoga na kubadili nguo kwa haraka, akatoka huku anakimbia
na yeye. “Unijulishe mtakapokuwa Geb. Nikimlisha Liv, nitakuja.” Geb
alimwitikia mama yake huku anatoka bila hata kujua hospitali aliyopelekwa
Nanaa. Njiani ndipo akampigia simu James. Iliita zaidi ya mara tatu bila
kupokelewa. Hapo ndipo jasho lilipoanza kumtoka Geb. Hakuwa akijua aelekee
wapi. Akajaribu tena.
Ikapokelewa.
“Uko wapi James?” “Bado nipo njiani.” “Unaenda hospitali gani?” Kimya. James hakujibu ila akamsikia Nanaa akilia
sana. “James?” “Nafikiria.” James akajibu. “Kwa nini tusimpeleke..” “Nisikilize Geb. Nimekwambia nafikiria. Nataka
nimpeleke sehemu atakayopata huduma kwa haraka. Acha kuniita mara kwa mara,
nashindwa kufikiria.” “Namimi nataka unisikilize James. Nanaa ni mke wangu mimi. Sasa hivi yupo chini yangu mimi. Nataka
ulitambue hilo na uniheshimu.” Kimya.
“Sasa mimi
natangulia Agakhani, nataka umlete mke wangu pale.” Kimya. “Unanisikia James?” “Naona mimi nitakutangulia. Sipo mbali na hapo.”
“Basi baada ya muda mfupi sana na mimi nitakuwa hapo.” Geb mwenyewe hakuamini kama safari hii amemmudu
James. Ikifika kwenye swala la Nanaa, James anakuwa mkali sana. Pengine ni yale
mamilioni ya pesa aliyopokea mama yake siku chache zilizopita ndiyo yamempunguza
ujasiri James! Au ameshatambua Geb haepukiki! Nani ajuaye! Lakini kwa mara ya
kwanza alimkubalia Geb.
Walifika
mapokezi, Nanaa akaanza kufanyiwa huduma ya kwanza. Alipimwa homa na pressure
wakati wanasubiri kumuona daktari. Muuguzi waliyemkuta hapo aliwaambia kila
kitu kipo sawa kabisa. Hakuwa na homa na pressure yake ilikuwa nzuri tu. James
alikaa na Nanaa pale nje wakisubiria kumuona daktari. Bahati nzuri hawakukuta
watu wengi sana siku hiyo ya jumapili. Wakajua kwa vyovyote vile watamuona
daktari kwa haraka. Wachache waliowakuta pale wakabaki wakiangalia miguu ya
Nanaa kwa kujiiba. Aliwekwa kwenye wheelchair. James akamuomba muuguzi ampe
shuka amfunike. “Naogopa kaka.” Nanaa aliongea wakati kaka yake akimfunika huku
akiendelea kulia. “Pole Nanaa. Lakini naona kuna dalili nzuri. Mpaka sasa kila
kitu kipo sawa. Hawajakukuta na tatizo. Mungu atakusaidia. Usiogope.” James
alijaribu kumtuliza lakini hata yeye aliingiwa hofu. Haikuwa hali ya kawaida.
Mara
Geb akaingia. Akaenda moja kwa moja kwa Nanaa. “Pole.” “Naogopa
Geb! Naogopa sana.” Midomo ya Nanaa ilikuwa ikicheza kama yupo kwenye
baridi kali sana. Yeye na kaka yake wote walishabadilika rangi wakawa wekundu
kama moto. Geb akapiga magoti, akambusu palepale alipokuwa
amekaa kwenye wheel chair. Akambusu midomo yake kidogo, kisha akamkumbatia huku
akiongea naye sikioni taratibu. “Usiogope. Kila kitu kitakuwa sawa. Sawa?”
Nanaa akatingisha kichwa. “Nitakuwa hapa na wewe wakati wote.” “Naogopa
kujiangalia.” Nanaa alikuwa akitetemeka sana mpaka meno yalikuwa
yakigongana. “Basi usiangalie. Nitakufunika wakati wote ili usione. Huna haja
yakuangalia. Mimi nitakusaidia kila kitu. Na nitakuwa hapa na wewe wakati wote.
Hautakuwa peke yako.” Geb alizungumza naye huku amemkumbatia. Akatingisha
kichwa.
“Haya,
niangalie Nanaa.” Nanaa akamwangalia. Akamfuta machozi. “Naomba uinue imani
yako kwa upya. Jua hata hili tutalipita tu. Sawa?” “Pamoja!?” “Mimi na wewe, Nanaa.” Watu wote walikuwa
wakiwasikiliza. James alikuwa kimya ameinamisha kichwa. “Nikifa?” “Sio sasa hivi na wala si kwa hili. Bado
hatujafanya mambo mengi sana. Mungu hawezi kukuchukua sasa hivi. Kwanza
unakumbuka hata bado hatujafunga ndoa?” Nanaa akaanza kulia tena.
“Sasa tunafungaje ndoa nikiwa
hivi? Wakinikata miguu? Nikifa?”
“Unakumbuka tulimuomba Mungu na mama akatuombea, Mungu atusaidie tufunge ndoa?”
Nanaa akatingisha kichwa kukubali huku akilia. “Basi naomba tuwe na imani kuwa
atajibu maombi. Uwe na miguu usiwe na miguu, lazima Mungu atatujalia tutafunga
ndoa yetu.” Watu wote wakapata ujasiri wa kuwageukia vizuri kuwasikiliza. “Kweli
Geb!?”
Nanaa akauliza kama asiyeamini. “Kabisa. Kwa hiyo naomba utulie. Tujue
kuwa sasa hivi tupo hapa tunahitaji msaada wa madaktari. Tusubiri tuone
watakacho tuambia. Lakini naomba kabisa ujiambie na tukatae kuwa hili sio
jaribu la kututenganisha wala la kutushusha chini.” Kidogo Nanaa akaanza
kutulia.
“Hili sio jaribu lakunishusha
wala kunitenganisha na wewe Geb.”
“Mbona kama sijakusikia vizuri, Nanaa? Au huna uhakika?” Geb akamfuta machozi,
akambusu tena midomo yake kwa muda kidogo, kisha akamuachia. Nanaa akavuta pumzi kwa nguvu na
kuzishusha taratibu. “Hili sio jaribu la
kunishusha wala la kunitenganisha na Geb.” Geb
akatabasamu. “Hapo sawa na usilie tena kama umeamini hilo. Sawa?” Nanaa
akatingisha kichwa kukubali. Geb akambusu tena na tena. Akasimama.
“Niliingiwa
na hofu. Nikajua utaniacha. Maana uliruka kitandani, ukanikimbia.” “Nisamehe
Nanaa. Nilishtuka sana. Unajua tulilala nikajua tukiamka utakuwa sawa tu. Sasa
kuja kukutana na picha hiyo, ndio nikashituka sana. Akili iliponirudia,
nikajuta sana. Nikajua nilikuogopesha zaidi.” Nanaa akacheka kidogo.
“Usinicheke bwana. Kwanza niambie
kama inauma?” “Hata kidogo. Wala sijihisi kama nina miguu.” “Utakuwa tu sawa.
Pole na samahani kwa kukuogopesha.” “Nimefurahi umekuja.” Wakaanza kucheka.
Nanaa huyu siye aliyetoka nyumbani. Alianza kuongea na James na Geb akijaribu
kujituliza.
Geb
alikuwa akiandaa maneno ya kuzungumza naye akiwa njiani huku akimuomba Mungu
amtie nguvu. Ni kweli Nanaa alikuwa anatisha sana. Geb alijitahidi kuzungumza
naye ili kumtoa mawazo yake kwenye ile miguu. Aliifunika vizuri ili Nanaa asiiangalie
tena au hata ikitokea anainama, asiione. Na Nanaa naye hakutaka hata kufanya
kosa hata lakugusa magoti. Mikono aliiweka juu tu, na macho yaliangalia pembeni
wakati wote. Hakujitizama. Wakati mwingine Geb alikuwa akiishika mikono yake na
kuibusu, huku akiisugua mikono hiyo iliyokuwa ikitetemeka sana, mpaka Nanaa
akatulia.
“Pole kaka. Nilikuogopesha.” “Pole wewe.
Lakini nimefurahi hofu imeisha. Ikiwa hivyo, itakusaidia kupona haraka.” Nanaa
akacheka, akisikika ametulia kwa asilimia kubwa. Dimpozi zikaonekana. Geb
akaweka kidole chake, Nanaa akamgeukia akacheka. “Asante Geb.” Nanaa
akanong’ona. Geb akampa tabasamu akamshika mkono wake na kuanza kubusu viganja
vyake tena. Kwa mapenzi hayo, huwezi kuogopa tena.
~~~~~~~~~~~~~
Zamu
yake ya kumuona daktari ikafika. Nesi akamuita jina lake. Geb akamsukuma mpaka
kwenye chumba cha daktari huku James akiwafuata nyuma. Hata daktari mwenyewe
alishituka alipoona ile miguu. “Ameungua na maji ya moto au mafuta ya moto!?”
Akauliza. “Hapana. Imeanza jana akiwa amekaa. Akaniambia miguu yake inakufa
ganzi. Alikuwa amempakata mtoto. Nikamchukua yule mtoto nikidhani labda
amelemewa na uzito wa mtoto, maana mtoto mwenyewe ni wa miaka sita. Baada ya
muda nikataka asimame ndio akaniambia hawezi. Tukaenda kulala, ameamka akawa
hivyo.” Geb alijieleza. Nanaa alikuwa akiangalia pembeni huku machozi
yakimtoka.
“Hii
kitu ni ngeni kabisa! Au amekula kitu ambacho kimemkataa?” Daktari akauliza.
“Hajabadilisha chakula.” Geb akajibu. “Basi inabidi afanyiwe vipimo. Itabidi
alazwe wakati tunamfanyia uchunguzi.” “Kuna jinsi yeyote yakumpatia chumba
chake yeye mwenyewe? Sitaki wawe hata wawili kwenye hicho chumba.
Nisingependa watu wageni au
nisiowafahamu mimi wawe wanaingia humo kwenye hicho chumba halafu wamtie hofu.”
“Ila garama itaongezeka.” Daktari akamtahadharisha. “Hamna shida. Ilimradi yeye
atulie tu.” Geb alijibu bila wasiwasi.
“Nimebanwa na mkojo. Nitafanyaje Geb?”
Nanaa alinong’ona huku akilia. “Kwanza naomba usilie Nanaa. Ndio maana tupo
hapa hospitalini ili kupata msaada. Hayo yote watatushauri nini chakufanya.
Usiwe na wasiwasi kabisa. Sawa?” Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Basi
naomba usilie.” “Siwezi. Naona
machozi yanatoka tu.” “Basi nitakufuta. Jitahidi
kuondoa hofu moyoni.” Nanaa akatingisha kichwa. Daktari na James walikuwa
wakisikiliza tu. Geb akamtizama huyo daktari kama kutaka asimshangae Nanaa, na
afanye wajibu wake. “Inabidi avalishwe catheter. Itamsaidia kutoa mkojo bila shida
ya yeye kuhangaika kwenda chooni. Watamvalisha na diaper.” Daktari akatoa huo
ushauri ulimfanya Nanaa kuongeza kulia.
“Hiyo
itakusaidia Nanaa.” “Nakuwa kama Liv jamani! Watu wanaanza
kunisafisha!” “Sio watu. Ni mimi. Usiwe na
wasiwasi. Unakumbuka nilikwambia tutakuwa wote wakati wote? Geb alijaribu
kumtuliza kwa kumuuliza swali. Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Sitakubali
udhalilike Nanaa. Mimi nipo na manesi watakuwepo. Usiogope.” Kidogo Nanaa
akatulia. Lakini alijua wazi maisha yake ndio yameshabadilika. Kutoka
kujitegemea, akifika atakapo kwa uhuru wote. Gafla ameanza kuwa tegemezi! Mpaka lini? Ni swali lililoanza kumsumbua kabla hata hajapewa
kitanda pale hospitalini.
Nanaa Akiwa Hospitalini.
Alichukuliwa
damu kwa ajili ya vipimo vingi sana huku daktari akisisitiza lazima kufanyiwa
culture ili kujua kinachoendelea kwa undani. Majibu mengine aliambiwa watapewa
siku hiyo hiyo mengine waliambiwa yanaweza kuchukua mpaka majuma mawili. Geb
hakuwa na wasiwasi, ilimradi kijulikane kinachomsumbua Nanaa. “Labda hayo majibu mengine nikasubirie
nyumbani.” Wasiwasi wa garama ukamwingia.
“Nanaa! Ndio tumefika tu sasa hivi, tayari unataka kuondoka mpenzi wangu!
Naomba tuwape muda wa kukufanya uchunguzi wa kutosha.”
“Itakuwa pesa nyingi sana Geb! Maadamu majibu ya awali yameshaonyesha
hakuna tatizo kubwa. Tukipata na haya ya leo, mimi naona tuondoke tu.” Nanaa akaongeza kabla Geb hajajibu. “Halafu nitakaa hapa peke yangu mpaka lini? Mwanangu?”
Tayari ile hofu ilionekana imerudi tena usoni. “Niangalie Nanaa. Nilikwambia
mimi nitakuwepo hapa na wewe muda wote. Yale yote tuliyokuwa tukiyafanya
nyumbani, tutayafanya tukiwa hapa. Na kama unavyomuona mama hayuko hapa, kwa
kuwa yupo na Liv. Na unamjua Liv anampenda sana bibi yake.” “Naona kuliko hata mimi!” Geb akatabasamu. “Si unaona sasa? Usilie bwana! Hakuna
kitakachobadilika.” “Na wewe kazini?” “Naomba usianze kuniwekea vikwazo vingi Nanaa.
Nimekwambia tutakuwa wote hapa.”
“Lakini itabidi uwe unaenda kidogo. Sitaki huu ugonjwa ukufilisi.” “Kila kitu kitakwenda vizuri tu. Kwanza ujue Grace
atakuwepo ofisini muda wote. Kitu kitakachonihitaji mimi atafanya yeye au
tutajua kitu chakufanya muda huo utakapofika. Naomba sasa hivi utulie kabisa.
Acha mawazo mengii, tena ya baadaye. Naomba tukabiliane na la sasa hivi
kwanza.” Nanaa akatulia.
Alishakuwa
amewekewa catheter kwa hiyo mkojo ukawa unatoka tu. Mama G akapiga simu,
akataka kuzungumza na Nanaa. “Vipi Liv wangu?”
“Anakazi ya kucheka tu mwanao.” Angalau Nanaa
akafarijika. “Vipi na wewe?” “Nasubiri majibu
ya vipimo mama.” “Lakini nimefurahi umetulia. Nitakuja muda sio mrefu.
Namalizia kazi hapa ndani ili nikimuachia watoto Grace, asiteseke peke yake.
Danny yupo njiani. Nimemtuma uji wenu.” “Mimi sioni umuhimu wa kunywa huo uji tena mama.
Nitarudi kula vyakula vya kawaida bila kula
vitu vya kuongeza maziwa. Sitaki Liv aje aninyonye tena. Sijui nimepatwa
na gonjwa gani! Sitaki kumuambukiza mwanangu. Naona mumuanzishie tu maziwa ya
kawaida.” Nanaa alianza kulia tena. Mama G
akanyamaza.
Hata yeye aliona ni kweli. Hawakujua ni nini
kinamsumbua Nanaa. Kimemuathiri kwa kiasi gani! Hawakujua kama ni gonjwa
ambukizi au la. Nanaa aliendelea kulia pale kwenye simu, mama G akiwa kimya.
Geb akachukua simu, akazima. “Hata hivyo amenyonya vyakutosha. Miezi sita bila
kula kitu ila maziwa yako tu, nafikiri amepata kinga yote. Atakula vyakula
vingine. Usiwe na wasiwasi.” “Nilitaka
anyonye mpaka hata miaka miwili.” “Haaa!
Yote hiyo! Na mimi?” Geb aliropoka mbele ya James. Nanaa akacheka nakujificha
uso kwa mto. James akatoka.
“Heri
nimegundua hila zoko, Nanaa.” “Geb wewe!” “Miaka miwili si michache Nanaa.
Ngoja nimwambie mama aanze kufikiria kitu cha kumnywesha huyo mjukuu wake. Hapa
biashara ndio imekufa.” Nanaa alizidi kucheka. “Sasa utamwambia nini mama?”
“Tunatumia huu huu ugonjwa.” “Ujue Geb huna akili wewe!” “Weee, nimevumilia
sana. Acha na yeye anipishe.” Nanaa alikuwa akicheka. “Inasaidia kinga na
kujenga akili.” “Anaakili zakumtosha yule mtoto. Naona hayo maziwa yako
yameshamjenga vyakutosha. Aache utani na mimi kabisa! Kwanza pale alipo
anakumbukumbu ya mtoto wa miaka 2, inatosha. Acha aanze kupewa ugali.”
Waliendelea kuongea huku wakicheka.
Akaingia
James na Danny. “Afadhali kama Nanaa anacheka. Maana nilikuwa nimeingiwa hofu
kweli!” Nanaa akamwangalia Geb. “Atakuwa tu sawa.” Geb akajibu. Wakaendelea na
stori nyingine. “Sikuwa hata nimejua kikao kiliishaje jana!” Geb aliingiza
mazungumzo ya kikao. “Watu wameahidi pesa ya kutosha bwana. Mpaka nikashangaa!
Ila watu wana wasiwasi na Nanaa.” Danny akaongeza. “Waambie Nanaa anaendelea
vizuri, na harusi ipo palepale kama tulivyopanga.” Danny akamtizama Geb kama
haamini.
“Vipi?”
Akamuuliza Danny kama na yeye anamshangaa kwa kusita kwake. “Naona kama
tungesubiri tujue hatima ya Nanaa.” Danny akashauri. “Miguu ya Nanaa
haitanizuia kumuoa Nanaa, Danny. Siku na tarehe ile ile tuliyopanga kufunga
ndoa, ndio hiyo hiyo. Iwe hapa hospitalini au kanisani, namuoa Nanaa.
Sitasubiri tena. Ninachotaka kutoka kwenu ni ushirikiano tu. Nitamuomba mama
aniombee kwa mchungaji aliyeahidi kutupa mafundisho ya ndoa, aje hapa
hospitalini atupe hayo mafundisho mimi na Nanaa. Tena kwa muda uleule ambao
kanisa limepanga wa mafundisho, ndio huo huo tutafundishwa. Wapi harusi
itafungwa, ndio itategemea na wapi bibi harusi atakuwepo siku hiyo. Basi.”
James na Danny wakaangaliana kwa muda wakiwa hawajaelewa. Nanaa hakuwa
akiamini.
“Unauhakika
Geb?” James akauliza. “Juu ya nini!?” Geb naye akamuuliza. “Kumuoa Nanaa akiwa
kwenye hali hiyo?” “Ipi?” Geb akauliza tena. “Mengi yaweza kutokea Geb.”
“Lini?” Geb akauliza tena, akiwa ametulia tu. James akanyamaza. “Naomba
unielewe James. Sina uwezo wakujua kesho inakuwa nini. Na siwezi kuruhusu hofu
ndio itoe tathimini ya maisha yangu. Sipo hivyo na wala sijawahi kuwa hivyo.
Mimi ni mtu wa mipango. Napanga kila kitu, halafu namuachia Mungu. Kwa mfano,
leo nilipanga kuwa Nanaa. Imetimia. Nipo na Nanaa. Lakini ni wapi, hapo Mungu
amepanga yeye kuwa nitakuwa naye hapa. Japo mimi nilijua ningekuwa naye mida
hii kanisani. Nikiwa nimembeba mtoto wangu pembeni ya familia yangu. Sehemu,
sio kama nilivyotarajia, lakini nipo naye hapa. Na baadhi yenu nyinyi kama
familia tupo pamoja. Kwa hiyo kwa sehemu kubwa mipango yangu imekamilika.” Geb
alizungumza akiwa anaonekana anajielewa.
“Mipango
yangu ni kuwa Nanaa ndiye atakayekuwa mke wangu kihalali. Sitaruka hatua hata
moja. Nimekamilisha kwa wazazi. Bado kanisani tu. Mipango yangu siku hiyo ya
harusi yetu ni niwe nimesimama naye kanisani. Baada ya hapo twende ukumbini
tukafurahie na watu watakaoweza kuhudhuria. Tena isizidi siku 40 tokea jana.
Nimepanga hivyo. Na nitasimamia hivyo. Mengine namwachia Mungu. Ninayemtaka ni
Nanaa tu. Wapi, na kwa staili gani, nitaona mbele ya safari, siku itakapofika.
Naomba mnielewe katika hilo. Sijawahi na sitaki kuyumbishwa na matukio.”
“Nimekuelewa Mzee.” Danny akajibu. James akatoka tena pale chumbani. Nanaa
akabaki amejifunika akilia.
“Wala
usilie Nanaa. Na hili tutavuka tu. Tutavuka kwa staili gani, hatujui. Tumuachie
Mungu. Yupo pamoja na sisi. Umesikia?” Nanaa akatingisha kichwa ndani ya shuka.
Geb akamfunua. “Naomba usilie hata kidogo. Kulia ni kumtangazia shetani
ameshinda. Hajawahi kushinda, na wala hataanzia kwetu kushinda. Nimuongo
tu. Sasa hivi ananguruma, kwa vitisho vya macho haya ya nyama.
Anakutupia vitu vya kukuogopesha tu. Lakini alishashindwa.” Geb akamfuta
machozi huku Danny akiwasikiliza asielewe ule ujasiri Geb aliupata wapi! Nanaa
hakuwa akitizamika miguuni. Tayari taulo alilokuwa amewekewa chini yake na
shuka la juu vilishalowa. Geb akamwita nesi. Akaja kubadilisha, wakamfunika
tena. Nanaa akawa ametulia.
~~~~~~~~~~~~~
Baada
ya muda, Mama G akaingia. “Hivi Grace amegoma kubaki. Tumekuja na watoto wote,
wapo kwenye gari. Utafikiri amefungua shule ya chekechea hapo kwenye gari.”
Danny akacheka. “Ngoja nikampokee.” Daktari akaingi. “Vipi?” “Anaendelea
vizuri.” Geb akamjibu yule daktari. “Sasa nimerudi na baadhi ya majibu ya
vipimo tulivyovichukua.” “Naomba usubiri kwanza nimwite kaka yake kabla
hujatuambia. Ndio kama baba yake Nanaa.” Geb akampigia simu James. “Njoo, daktari yuko hapa, anamajibu ya Nanaa. Nataka na wewe usikie.” Geb akakata simu.
Baada
ya muda mfupi sana, James akaingia. Macho yake yalikuwa mekundu sana. Wazi
alionekana alikuwa akilia. “Majibu yakoje?” James akamuuliza daktari mara
alipoingia. “Vipimo vyote vinaonekana Nanaa hana tatizo lolote. Hata mkojo ni
msafi kabisa. Ila tumekuta ni mjamzito.” “Asante
Mungu wangu kwa faraja. Hata wakati huu umetukumbuka. Asante Yesu wangu. Asante
ku…” Geb aliendelea kumshukuru Mungu akaacha kila mtu
kimya.
Zile
habari zilimshtua kila mtu pale ndani. Kwa hali ya Nanaa ilivyo, halafu kusikia
ni mjamzito tena, hata mama G, akashituka sana. Lakini ikawa tofauti kwa Geb.
Zile shukurani alizokuwa akizitoa huku akifurahia, kulianza hata kubadilisha
moyo wa Nanaa. “Si umeona Nanaa? Katika hili pia Mungu ametukumbuka. Ametutumia
faraja.” Hata yule daktari akabaki kimya.
“Hivi unaona hali yangu Geb? Mimba hiyo naibebaje? Mtoto huyo anakujaje
sasa hivi?” Nanaa akauliza huku akilia.
“Nanaa! Hivi wewe unafikiri Mungu hakuwa ameiona siku hii ya leo? Hakuna jambo
linalotokea sasa hivi eti likamshangaza Mungu! Hata kidogo. Alijua leo
tutakuwepo hapa tukiwa kwenye hali hii ya ugonjwa, ndipo akaamua kutukumbusha
kuwa yupo na sisi. Ametubariki na mtoto mwingine. Hiyo ni faraja Nanaa. Jiulize
kwa nini huyo mtoto aje kwetu wakati huu? Au unafikiri ni bahati mbaya?” “Na
maradhi haya Geb!?” Nanaa akauliza.
“Mbona
kama unasahau Nanaa wewe!? Unakumbuka mimba ya Liv? Unakumbuka ulivyougua mpaka
ukafanyiwa na upasuaji! Madawa uliyokuwa ukinywa! Lakini mwangalie Liv sasa
hivi. Anakuwa kwa haraka kuliko watoto wa umri wake! Si kwa nguvu zako wala
uweza wa madaktari tumekuwa na Liv. Mungu ametaka kukuhakikishia yeye ni Mungu.
Na humpa amtakaye. Hata huyo naomba tumuachie Mungu, na tuchukue kama faraja.
Hakuna jinsi Mungu angekupa pole, ukaelewa kama si kukupa huyo mtoto sasa hivi.
Jua hiyo ndio pole ya kipekee kutoka kwa Mungu. Na anatujulisha bado
mkono wake uko juu yetu.” Geb akaendelea.
“Kama
unafikiri huyo mtoto amekuja kwa bahati mbaya, uliza wanaolala mahospitalini na
makanisani wakililia kushika mimba. Muulize Sara mke wa Ibrahimu, mama yake
Isaka kwenye bibilia atakwambia vile ilivyo shida kushika mimba. Muulize Hana
mke wa Elkana kwenye kitabu cha 1 samweli 1. Mama yake Nabii Samweli. Kama ungepata bahati ya
kukutana na hao wanawake wawili tu. Waliokuwa wameolewa na wanaume wema, safi
mbele za Mungu. Ndipo ungetambua na kuelewa hichi Mungu alichokutendea wewe.”
Geb akaendelea.
“Sio
kitu kidogo kilichotokea kwetu Nanaa! Usipuuze hata kidogo. Usikubali hii hali
ya leo ikakufanya ushindwe kuona baraka na faraja Mungu aliyotutumia.
Tumshukuru Mungu kwa majibu haya ya kwanza kuwa huna tatizo. Damu yako safi.
Inamaana hata mtoto yupo salama huko tumboni. Nalo hilo ni la kumshukuru Mungu.
Naomba Danny akatuletee vinywaji, tusherehekee mtoto wangu. Leo tunahabari
njema tu. Tuna mtoto anayekuja na hawajakuta tatizo. Umenielewa Nanaa?” Nanaa
akatingisha kichwa huku akifuta machozi.
“Ni
kweli unaamini Nanaa? Mbona sikusikii ukisema kitu?” Nanaa akavuta pumzi kwa
nguvu na kuzishusha. “Leo ni habari
njema za mtoto wetu na kuwa sijakutwa na tatizo lolote.” Nanaa akarudia. “Mbona kama sikusikii vizuri?
Halafu bado unalia? Naomba hizi habari ziingie moyoni, na zipate nafasi kama
habari nyingine zozote zile.” Kila mtu alikuwa akisikiliza, nakushindwa
kuchangia. Daktari mwenyewe alikuwa kimya. Geb akamfuta machozi na kumbusu
kichwani. “Leo ni habari njema za mtoto wetu na kuwa sijakutwa na tatizo.”
Nanaa akarudia tena kwa sauti iliyotulia. “Ewaaa!” Geb akainama na kumbusu
midomoni. “Naomba utulie na uingize habari njema tu. Kwa ajili yako na mtoto.
Basi.” Nanaa akatingisha kichwa kukubali.
Akamgeukia
mama yake. “Umemsikia Mungu wetu tunayemuabudu? Amegeuza huzuni yetu kuwa
kicheko! Oliva amepata mdogo wake.” Mama G akaendelea kujifuta machozi,
asiamini ni nini kimempata Geb. Alihisi ni kuchanganyikiwa kwa hali ya Nanaa.
Lakini kila alipokuwa akiongea, alionekana anajua anachokizungumza. Danny na
James walikuwa kama wamepigwa na butwaa. “Danny! Naomba chakula kizuri na
vinywaji mpaka kwa manesi. Vije humu ndani. Mwambie Grace alete watoto humu
ndani. Lipo jambo Mungu ametutendea mimi na Nanaa. Lazima tumtukuze yeye Mungu.
Na nitamrushia mchungaji sadaka yetu ya shukurani. Tunaitoa leo leo.
Haitangoja.” Geb alibadilisha ile hali ya huzuni, wakaanza kutulia.
“Nitakusindikiza
Danny.” James akaona na yeye atoke tu, ili wasiharibu hali ya pale iliyojaa
furaha na shangwe tupu. Ukweli wote walikuwa na hofu. Lakini sio Geb. Hata mama
yake hakuwahi kumuona Geb huyu. Alijawa kujiamini na yeye ndiye alikuwa
akiongea mistari ya bibilia kama Grace! Mama G akaanza kuona amekuza vijana.
Tokea asubuhi Grace aliingilia ile hali ya Nanaa, akamsaidia wakati yeye
amepatwa na mshtuko asijue chakufanya. Kufika hapo hospitalini, anakutana na
Geb naye ametulia. Ikabidi na yeye atulie tu.
~~~~~~~~~~~~~
“Ni sawa
watoto wadogo kuwepo humu?” Geb akauliza kabla daktari hajatoka. “Mpaka
sasa hakuna hatari yeyote ile ya maambukizi. Kama nilivyowaambia, damu na mkojo
wake ni visafi kabisa. Hakuna ugonjwa wowote kwa mkeo.” Daktari alijibu lakini
wazi alionekana yupo kwenye mshangao. Geb alielewa. “Nakushukuru sana.” Geb
akampa mkono. Akatoka. “Naomba ukaniletee Liv, mama.” Mama G akatoka kimya
kimya bila hata kuongeza neno.
“Msamehe
mama. Hivyo ndivyo anavyokuwa wanae wakiwa wagonjwa. Utampenda hekaheka zake mtu
mwingine akiwa mgonjwa! Lakini asiwe mwanae. Hapo akili itakuja kumrudia
baadaye.” Alibaki Geb na Nanaa pale chumbani. “Alishaniambiaga tokea kipindi
kile tulipohamia kwenye apartment. Halafu nikamuona wakati wa uchungu wa
Grace.” Wakacheka kidogo. Wakamkumbuka mama G alivyokuwa amechanganyikiwa
wakati Grace anahangaika na uchungu. “Basi ndivyo alivyo. Ujanja wote huwa
unamwisha.” Akamuona Nanaa ametulia akiwaza.
~~~~~~~~~~~~~
James,
Danny, na mama G wote wakajikuta wamesimama kwenye gari alilokuwepo Grace.
“Mbona wote mpo kama mabubu?” Grace akawauliza huku akiwaangalia kwa zamu.
Kimya. “We Danny?” Grace akatoa mkono nje akamsukuma kidogo mumewe. “Sijawahi
kumuona Geb yule tuliyemuacha mle ndani!” Danny aliongea kama anajaribu kuvuta taswira.
“Au amechanganyikiwa?” James akauliza. “Na mimi nilidhani hivyo. Lakini
hasikiki kama mtu aliyechanganyikiwa hata kidogo.” Danny akajibu wakati mama G
amejiegemeza kwenye gari pembeni.
“Amefanyaje?”
Grace akauliza. “Bwana ametulia. Na anasema mipango yao ya harusi inaendelea
kama ilivyo!” Danny akajibu. “Sasa nyinyi mlitaka iweje!?” Grace akauliza kwa
kushangaa. Wote wakamgeukia. Wakamuona Grace anawaangalia. “We Danny? Ulitakaje?
Asimuoe Nanaa!?” “Sio asimuoe. Angalau asubiri aangalie hatima yake.” “Kumbe
nyinyi mmeishi na Geb lakini hamjamfahamu! Geb sio mpangaji wa mipango halafu
asihakikishe inatimia. Labda Mungu aseme hapana. Na ndio maana hanaga mipango
mingii na hanaga mipango ya kijinga hata
mmoja. Hajui kuahidi kitu anachojua hataweza kukisimamia. Akisema anamuoa
Nanaa, ujue hajakurupuka. Na ni lazima atamuoa Nanaa, labda Nanaa afe kabla ya
hiyo siku. Na akiamua kuwa hatakuwa na watoto nje ya Nanaa, ujue hata Nanaa
akishindwa kuzaa mjue Geb hatawahi kuwa na watoto hapa duniani. Ndio Geb alivyo.
Na labda ndio maana anafanikiwa san..” “Kwanza Nanaa amekutwa ni mjamzito.”
James akamkatisha.
“Jamani
Mungu ni mkubwa! Ona katika hili pia amewatumia faraja!” Wote watatu wakasogea
pale dirishani wakabaki wakimwangalia Grace mpaka mama yake. “Nini!?” Grace
akashangaa. “Kweli nyinyi ni mapacha! Geb naye amesema hivyo hivyo! Yaani
maneno hayo hayo kama uliyosema wewe! Ndio maana tunakwambia amechanganyikiwa.”
“Heee! Amechanganyikiwa tena!? Hakika huyo ni Mungu, Danny! Si mtu mwingine.
Ameamua kumfariji Nanaa katika kipindi hiki kigumu.” Grace aliendelea
kushangilia huku akimtukuza Mungu.
“Mimi
naona tuondoke James.” “Mnaenda wapi badala turudi ndani tukasherehekee?” Wote
wakarudi kumwangalia tena Grace. “Nyinyi vipi jamani!?” Grace akashangaa.
“Mbona mpo hivyo!? Shetani hana uwezo wakutoa vitu vizuri hata siku moja.
Kelele zake huwa zinaishia kama vile mnavyoona miguu ya Nanaa.
Basi. Hawezi kutoa baraka hata siku moja. Huyo ni Mungu ameamua kujidhihirisha
kwetu kama kutuonyesha mkono wake bado upo juu ya Nanaa.” Grace akaendelea
kurudia aliyozungumza Geb.
“Basi
nahisi sisi ndio tumechanganyikiwa!” Danny akaafiki. “Kwa nini?” Grace
akauliza. “Maana mwenzio huko ndani anaongea maneno kama hayo hayo
unayozungumza wewe! Utafikiri mmeambizana! Hapa tumetumwa vyakula kwa wauguzi
wote wanao muhudumia Nanaa, na sisi.” “Usisahau na vinywaji Danny. Tumeambiwa
tukalete vinywaji vyakutosha, tusherehekee mtoto aliyekuwepo tumboni.” James
akamalizia wakacheka kwa pamoja.
“Haya,
watoto wa Danny, mjiandae tunatoka. Fili vaa viatu tunaenda kwa anti Nanaa. Ana
mtoto mwingine tumboni.” “Kama vile Fillius na Fillan walivyokuwa tumboni kwako wanacheza?” Fili
akamuuliza mama yake huku akitafuta viatu vyake. “Eheee! Lakini wa aunt
hawajaanza kucheza. Bado wadogo. Umefurahi?” “Sana mama. Mimi ndio kaka mkubwa.
Nitakuwa nacheza na wadogo zangu wote. Nitawafundisha kuruka ngazi.” “Nini?”
Danny akashutuka sana na kumgeukia mwanae. “Mbona anko Geb anasema ni sawa tu.”
Fili akajitetea. “Wewe ruka peke yako na anko wako. Usifundishe wenzio kuruka.
Unataka kunichanganya akili wewe Fili. Sitaki wawe watundu kama wewe.” “Anko
amesema mimi ni brave. Nina uwezo wa kuthubutu mambo magumu na
sishindwi.” Fili alijibu kifasaha. Grace akaanza kucheka.
“Sasa
hapo Grace unacheka nini bwana?” “Wewe usinigeukie mimi. Endelea kupambana na
Fili.” Grace akaendelea kucheka. “Hicho kichwa kwa hoja, ukiwezi.” James
akaongeza na kuondoka kuelekea lilipokuwa gari yake. “Danny na maneno yote,
hapo kwa Fili amefika mwisho. Haya dad, unalanyongeza?” Grace akazidi
kumchokoza mumewe. “Hamna kufundisha wenzako kuruka ruka kama wewe. Unanisikia
wewe Fili.” Danny aliongea kibabe kidogo.
“Kwa
nini?” Fili akauliza kwa utulivu na macho yake kama mama yake. “Wataumia.”
Danny akajibu. “Mbona mimi sijawahi kuumia? Naruka kwa kutumia akili dad.
Siruki kijinga. Na nitawafundisha kuwa makini kabla hawajaanza kuruka.” Grace
alizidi kucheka mpaka akainamia usukani. “Mimi naona niondoke tu.” Danny
akaanza kuondoka.
Mpaka
mama G akaanza kucheka. “Danny! Danny mume wangu!” “Sitaki Grace. Mimi naenda
kuleta vitu vya sherehe. Geb ataanza kupiga simu sasa hivi, kuulizia.” Danny
akaelekea alipokuwa ameegesha James gari yake. Wakaondoka.
“Njoo
mama G.” Grace akamuita. “Niambie mama yangu. Kibumbuazi kimekuisha?” “Mmmh!
Naona nyinyi watoto mmenipita. Imebidi kiishe tu. Maana huko ndani ukiingia,
hata ukiwa na huzuni zako zinaisha.” Grace akacheka. “Kwa nini?” “Huyo Geb!
Kila neno analoongea ni kinyume na hofu. Anasema yale shetani aliyokusudia kuwa
mabaya, Mungu anayabadilisha kuwa mema. Anasema kilio chao, Mungu
amekibadilisha na kuwa kicheko. Amefurahi huyo! Kama Nanaa amepona!” “Jambo la
kumshukuru Mungu mama! Unafikiri kama yeye angeendelea kupaniki kama vile
asubuhi, wewe ungekuwa kwenye hali gani? Ingekuwa mbaya zaidi!”
“Na ni kweli. Ila Grace, umekuwa mwanangu.
Sikutegemea kama ungekuwa shupavu hivyo! Yaani leo asubuhi pale chumbani kwa
Geb na Nanaa, niliona sura ya Magesa hivi. Nikasema katika hali hii ngumu,
Mungu amemrudisha Magesa kupitia wewe. Ulifanya kama vile baba yako angefanya!
Utulivu usoni mwako, maneno ya kutokatisha tamaa, na kuchukua hatua kwa haraka
kwenye wakati mtatanishi kama ule ambao wote tulikuwa hatujui chakufanya!” Mama
G akacheka.
“Unacheka
nini sasa?” Grace akamuuliza. “Ulimuona Geb lakini?” Wote walizidi kucheka.
“Lakini Nanaa anatisha mama! Kuamka na kukutana na miguu ya hali ile! Mimi
mwenyewe sijui ujasiri nilipata wapi?” “Nikaona kwa masaa machache wewe ukawa
Magesa, basi kiziwanda wangu akawa kama mama yake!” Wakazidi kucheka. “Lakini
ukimuona humo ndani sasa hivi, utafikiri Magesa amefufuka. Mimi mpaka
nimeondoka. Alivyosimama! Anavyoongea! Ule ujasiri! Ni Magesa mtupu! Na sura
ile na macho, hakika utafikiri Magesa mwenyewe Mungu amenirudishia.” “Sasa
Nanaa yupo na hali gani?” “Ametulia kabisa. Hayo mabusu anayopewa!” Grace
akacheka sana.
“Na
Geb anavyojua kubembeleza!” “Basi na maneno yake hayo, mpaka Nanaa ametulia.
Lakini Geb ameomba afunikwe ile miguu asiione kwa sasa hivi. Habari walizonazo
humo ndani wanasema ni njema tu. Nanaa amepimwa hajakutwa na tatizo na Mungu
amewabariki mtoto mwingine. Basi.” “Afadhali. Twende basi.” “Ujue nilitumwa
nimpeleke Oliva?” “Hivi wewe mama ukoje bwana!? Naomba ubadilike. Nanaa alikuwa
anakulilia na wewe ukabaki umeduaa!” “Bwana ananijua huwa naishiwa nguvu.
Anajua sana.” “Hapana bwana.”
“Basi
sasa hivi nguvu zimerudi.” “Kweli? Maana sio turudi tena ndani, uanze tena kufa
ganzi na kugeuka kuwa bubu wakati haya ndiyo mambo yako ya kuombea.” “Halafu
hatujaomba hata mara moja, Grace!” “Shetani huyo. Jana nilitaka kuanza kuomba,
Danny akaingia na jeshi lake.” Wakacheka. “Lazima leo tupige maombi ya nguvu.”
“Kabisa.” Mama G akafungua mlango. “Kumbe wote wapo macho!?” “Wameshiba hapo.
Liv nilimlisha tena, na hao kina kaka nimewapa uji.” “Wewe Grace!?” “Kweli
mama. Nimeona hawashibi. Huoni walivyotulia? Nimewapa uji wa Liv.” “Umewalevya
bwana!” “Heri hivyo walivyolewa. Na mimi nipumzike.” Mama G akacheka.
“Hawajakataa?”“Wapo
kama Danny hawa watoto. Naona hawa sitasumbuka nao kama Fili. Wamekula mpaka
nikaona basi. Hapo nimewawekea nyimbo za watoto, wanaangalia huku wanasinzia.
Kimyaa, kila mtu anashuguli zake.” Mama G akatingisha kichwa. “Nilijua
nikiwaambia wewe na Danny, mngekataa.” “Kwa hiyo ukaona ufanye siri?” “Kumbe!”
“Watoto wadogo hao Grace. Ungewaanzishia maziwa mengine.” “Hayakai tumboni.
Bora wanywe uji na kunyonya. Nitachanganyikiwa mama. Wananiliza kila siku! Sina
hata muda na Danny wangu? Hapana mama. Namtaka mume wangu.”
“Na
watoto?” “Watakuwa tu. Nikiona huo uji umewakataa, basi. Nitatafuta njia
nyingine. Yaani sina muda na mume wangu hata kidogo! Watoto wakilala, na sisi
tumechoka. Hapana mama. Ni mwezi unaenda watatu huu, hata hatujapata muda na
Danny!” “Ni hivi tu limetokea hili. Ningekushikia hata kwa masaa matatu mrudi
kwenu kwa muda mfupi mpumzike, ndio mrudi pale.” “Mbona itabidi ufanye tu.”
“Grace wewe mtoto?” “Kweli mama. Na hivi wameshaanza kunywa uji. Baadaye
tukirudi nyumbani, nitatoka na Danny kidogo.” Mama G akatingisha kichwa.
Liv
alipomuona tu bibi yake akaanza kuhangaika pale kwenye kiti huku anacheka na
kunyanyua vimikono vyake juu. “Muone alivyofurahi kukuona.” Mama G akacheka.
Akapita mpaka kiti cha nyuma kabisa alipokuwa amekaa Oliva. Grace alinunuliwa
na mumewe gari nyingine ya Toyota Van. Yenye njia ya katikati. Kwa hiyo ilikuwa
rahisi kufikia kiti chochote. Ilikuwa ni gari ya viti 7. Waliita gari ya
watoto. Waliwaweka kwenye viti vyao na kuwafunga mikanda. Wakawa wakizunguka
nao bila shida ya kupakatana.
Akambusu
Liv. “Salamu kwanza Oliva. Wewe vipi bwana?”
Bibi yake alimwambia. “Anataka umbembe?” Grace akauliza huku akiwatoa
wanae Fillius na Fillan, na kuwaweka kwenye kigari chao cha kuwasukuma wakati
wakitembea. Na chenyewe kilikuwa cha mapacha watatu. Wakati mwingine walimuweka
Liv humo kama bibi yake na baba yake hawapo. Wakiwepo, atataka wambebe tu, sio
kumsukuma kwenye kigari.
“Nakwambia!
Anataka salamu hiyo tupeane nikiwa nimembeba! Haya njoo.” Mama G akamtoa Liv
kwenye kiti chake akambeba, kisha akambusu. Liv akaanza kucheka huku akiongea
kwa lugha ya kitoto. “Unamtaka dad?” Mama G akamuuliza. Liv akacheka. “Haya,
twende kwa dad yako.” Wakatoka pale, Fili akiwa anafuraha zote.
~~~~~~~~~~~~~
Walimkuta Geb anaomba na Nanaa. Maombi yalikuwa ya shukurani tu. Isivyo kawaida, Oliva alivyoingia tu akamtaka mama yake na wala si baba yake. Nanaa alianza kulia kwa uchungu sana. Kwani mkono mmoja alishawekewa dripu ya maji ili kufidia yale maji anayopoteza kwa wingi miguuni. Oliva alilalamika akimtaka mama yake mpaka Geb akamtoa nje. Hapo ndipo alipoanza kulia. Mama yao naye akatoka. “Labda ni njaa mama.” “Hana njaa. Amekula vizuri tu. Labda anahamu na mama yake. Mweke pale akae naye tu.” “Nanaa anaogopa mama. Hataki amuambukize.” “Mweke kidogo tu hata kifuani atulie. Unamjua mwanao yupo kama wewe. Hawezi kutaka kitu akatulia mpaka akipate. Muweke kwa mama yake.” Wakarudi ndani.
Liv alishakuwa mwekundu. “Mshike kidogo tu, atulie.” Geb akamuweka kwa mama yake. Akamlalia mama yake kama alivyokuwa akimlalia baba yake kifuani, Nanaa akamkumbatia kwa mikono yote miwili. Nanaa ndiye aliyebaki akilia. “Nitakufa nimuache mwanangu!” Nanaa alisikika akilia taratibu.
“Nisikilize
Nanaa. Uzima na mauti upo kwenye kinywa chako. Unachokiri ndicho kitakacho
kuwa. Ukikiri mauti, na kweli mauti ndiye atakayekuja. Ukikiri uzima, uzima
ndiye atakayekuja. Pambana. Tena pambana sana kwa ajili yako na wanao. Una
sababu kubwa ya kupambana. Kama si kwa ajili yako basi ya wanao. Liv, na huyo
ambaye yupo tumboni anayekutegemea kwa asilimia zote. Ujue sasa hivi unaishi
kwa ajili yako na huyo mjukuu wangu. Nataka upambane haswa. Kiri uzima. Jiambie
hutakufa bali utaishi. Ambia hiyo hali hutakufa, hutakuwa kilema, iambie
utaishi uyashuhudie matendo makubwa ya Bwana. Umenisikia Nanaa?” Mama G
akaongea kijasiri, Nanaa akatingisha kichwa.
“Hapana
Nanaa. You
can do better than that.” Geb akaingilia. “Sitakufa, bali nitaishi. Niyashuhudie makuu
ya Mungu.” Nanaa akarudia. “Hiyo ni kwa
ajili yako. Sasa iambie hali yako. Na lazima kuwa jasiri. Tena ongeza kuwa, ‘uhai wangu umefichwa ndani ya Kristo Yesu’.” Geb akasisitiza. “Tena bila machozi.” Mama G
akaongeza. Geb akamsogelea nakumfuta machozi. Nanaa akatulia na kurudia.
“Sitakufa. Bali nitaishi. Niyashuhudie makuu ya Mungu. Si mimi ninayeishi, bali
Kristo ndani yangu. Na uhai wangu umefichwa ndani ya Kristo Yesu.” Nanaa
aliongeza na kufanya mama G na wanae wacheke na kumpigia makofi.
“Safi
sana. Sasa tumwite huyo aliyeficha uhai wako. Tumkumbushe juu ya afya yako.
Hakuna atakayetulia tena, mpaka tuone Bwana atakavyotujibu katika hali ya
kulalamika kwetu. Tuombe.” Yakaanza maombi pale chumbani. Mama G ndiye
aliyekuwa akiongoza. Waliomba bila kupumzika. Danny na James walipoingia na
vyakula, na wao wakaungana nao kuomba mpaka
wakamaliza.
“Tumeshagawa
vyakula na vinywaji kwa wauguzi wote wa hii gorofa.” “Nashukuru sana Danny.
Asante.” Wakakaa wote wakamshukuru Mungu na kuanza kula huku Oliva amelala
kifuani kwa mama yake. Kila walipotaka kumtoa, Nanaa alikataa. Alibaki
akimpapasa mgongoni huku wengine wakiendelea kula na kuzungumza. Wakamaliza
kula wakabaki wakizungumza tu.
~~~~~~~~~~~~~
Mambo
yakaanza kubadilika pale Geb alipoaga. Akamsogelea Nanaa. “Nitarudi baada ya
muda mfupi. Nakimbia nyumbani mara moja.” “Utarudi?” Nanaa akauliza.
“Sitakawia.” Geb akajibu. Tayari Nanaa alishaanza kutetemeka kwa hofu. “Najua
utarudi tu. Si ndio?” “Nitarudi Nanaa!” Nanaa akaanza kumpigapiga mtoto wake
mgongoni kama anayembembeleza, wakati Oliva alikuwa ameshalala. “Najua. Najua
unaenda mara moja tu, halafu utarudi. Hutachelewa.” Watu wote wakatulia.
James
akamsogelea. Akajua ameingiwa na hofu. “Nipe nikupokee mtoto.” “Geb anakwenda
nyumbani mara moja kaka. Atarudi.” “Ndiyo Nanaa.” James akamjibu kwa upole
kutaka atulie. Maana hata midomo yake ilishaanza kucheza kama aliyeshika baridi
kali. “Nanaa! Nanaa! Niangalie.” Geb akamuita. James akamchukua mtoto. “Kuna vitu
naenda kuchukua mara moja nitarudi baada ya muda mfupi sana.” Geb akarudia
taratibu akijaribu kumtuliza “Hata mimi najua utarudi Geb. Huwezi
kuniacha hapa peke yangu.” Nanaa alianza
kutokwa machozi huku akitetemeka sana. Akavuta shuka akajifunika mpaka mabegani
huku machozi yakimtoka. “Nenda tu. Mimi
nitakuwa hapa hapa nakusubiri Geb. Nitakusubiri. Hamna neno kabisa.” Kila mtu alikuwa akimwangalia kwa kumuhurumia.
Wakajua ameingiwa hofu.
“Nanaa!”
“Nenda tu Geb. Nakuamini
utarudi.” Geb akamshika mkono. Akakaa
pembeni ya kitanda. “Kwani unataka nini huko nyumbani?” Grace akauliza.
“Begi langu lile la kazini. Lenye
laptop. Na..” “Nenda tu kachukue
Geb. Nitasubiri.” Nanaa akarudia huku bado midomo
ikimcheza. “Naona nitamtuma Grace akanikusanyie vitu ninavyovitaka, halafu..”
“Mimi nitarudi navyo.” Akawahi James kwa kumkata Geb na kuendelea. “Mimi niende
na Grace. Anipe hivyo vitu vyako vyote. Nitakuletea Geb.” James aliongea
kinyenyekevu sana kama anayesihi na kuomba Geb abaki tu na dada yake. “Nafikiri
hilo wazo ni zuri. Halafu tumuache Nanaa sasa hivi apumzike.” Mama G akaongeza.
Geb
akamfuta machozi, akamwinamia pale kitandani nakuanza kumbusu pale mbele za
watu. Nanaa akaanza kutulia. “Lala mimi nitakuwa hapa hapa.” “Niliingiwa na
hofu Geb. Samahani.” Geb akambusu tena kwenye kipanda uso, akampa na tabasamu.
“Nenda tu.” Walimsikia Nanaa akiongea akisikika akiwa ametulia kidogo. Bado Geb
alikuwa amemwinamia. “Naelewa. Usijali. Hata mimi sitaki kuondoka tena.”
“Kweli?” Nanaa akamuuliza kwa upole. “Nikitoka hapa, tutatoka wote.” “Sasa kazini?” Nanaa akauliza. “Mimi nitakuwa
nikienda hata kama ni nusu siku. Ili kuhakikisha kila kitu kipo sawa. Usiwe au
msiwe na wasiwasi.” Wote wakamgeukia Grace mpaka mumewe.
Grace
akacheka. “Nitawabeba wanangu wala msiwe na wasiwasi. Wakiamka vizuri, tunaenda
asubuhi. Wakiamka na akili kama za baba yao, naenda nao mchana. Tutakuwa
tunawasiliana Geb. Wewe tuliza mawazo tu hapa hospitalini. Mambo mengine
yatakuwa sawa.” Geb aliinama kwa muda kama anayefikiria. Kisha akamgeukia tena
Grace. “Nakushukuru sana Grace. Asante. Asante sana.” “Asante Grace.” Nanaa
naye akaongeza. “Wala msijali. Kwanza
likizo yenyewe ilikuwa imeshaisha. Nilikuwa nikivuta tu muda huku nikitafuta msichana
wa kazi. Watoto wenyewe wameshakuwa.” Grace akaongeza. “Afadhali. Utakuwa
umempunguzia mwenzio mzigo mkubwa sana. Hata yeye atatulia.” Mama G akaongeza.
Geb akamgeukia tena Nanaa, akamvuta mkono na kuubusu.
Hakuna Msiba Usio Kuwa Na
Mwenzie.
Wakiwa
wanataka kutoka, mchungaji akampigia simu mama G. “Upo sehemu nzuri tunaweza kuzungumza?”
Mchungaji akauliza. “Nipo na wanangu. Tunaweza
kuongea tu.” “Mlikumbuka kama leo ndio lilikuwa tangazo la kwanza la harusi ya
Geb na Nanaa?” “Tunakumbuka mchungaji. Lakini tumepata matatizo. Hapa tupo
hospitalini ndio maana tumeshindwa kuja kanisani. Ulifanikiwa kutangaza?” Mama G akauliza. Wote walikuwa wakisikiliza.
“Kabla
sijakwambia kilichonifanya nikupigie, niambie kwanza nani ni mgonjwa?” Mchungaji akahoji tena. “Kuna nini tena?” Mama G akauliza. “Nafikiri
ushugulike na tatizo moja baada ya jingine.” Mchungaji akashauri. “Mpaka sasa
sijaona tatizo lakunifanya nishindwe kukabiliana na changamoto nyingine,
Mchungaji. Tafadhali niambie tu. Kuna nini?”
Mama G aliendelea kusisitiza. Mchungaji akasita. “Au tuonane?”
“Hamna shida. Sasa hivi tupo hapa hospitalini ndio tunajiandaa kuondoka.
Naelekea nyumbani. Lakini kabla hatujapanga muda na wakati wa kukutana, nataka
kujua tunakutana kwa ajili ya nini! Na tafadhali usinifiche.” Mama G akasisitiza zaidi.
“Tangazo la
kwanza tu, limepata kipingamizi.”
Mchungaji akaongea. “Unamaanisha nini?” Mama G akauliza.
“Leo wakati natoa tangazo la kwanza la ndoa ya Geb na Nanaa, nikapata
vipingamizi viwili. Wapo watu wawili wanaopinga hiyo ndoa isifungwe. Kwa hiyo hatuwezi
kuendelea mpaka tufikie muafaka.”
Mama G akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu.
“Vipingamizi
kutoka kwa nani?” Mama G akauliza. “Labda tukutane. Ili tuzungumze.” Mchungaji akasisitiza. “Kwa nini ulinipigia simu?” Mama G alishabadilika. “Kama sijakosea, ulinipigia simu ili kunijulisha. Simu ni nusu ya
kuonana. Tafadhali tusiendelee kupoteza muda zaidi.” Mama G aliongea
kwa ukali kidogo huku wote wakimsikiliza. “Ni kweli.” Mchungaji akajishusha. Mama G akaweka ile simu
kwenye speaker ili kila mtu asikilize.
“Kipingamizi
cha kwanza kinatoka kwa mama yake Nanaa.” “Nanaa ni yatima, mimi ndio mama
yake.” Mama G akajibu kibabe. “Amekuja hapa mama mmoja. Wakati natangaza, yeye na kijana mmoja
wakapinga kuwa ndoa isifungwe. Ndipo baada ya ibada ikabidi kukaa nao ofisini.
Huyo mama amejitambulisha kwa jina la ‘Mama James’. Anasema yeye ndiye
aliyemlea Nanaa tokea mama yake amefariki. Amemlea kwa tabu sana. Alipowaambia
anataka alipwe fidia, mmemkatalia.” “Subiri kwanza. Mama James amesema tumemkatalia
kumlipa!?” “Labda sijaongea vizuri. Amesema mmemkatalia kumpa pesa
aliyowadai, mmemlipa kidogo sana.”
“Mungu wangu mama!” James alisikika akisikitika.
“Amekwambia
yeye alitaka kiasi gani?” “Anavyodai alitaka
milioni 100. Akamtuma mwanae kwenu. Mkaomba mpunguziwe mpaka milioni 50.
Akakubali. Matokeo yake mmempa hundi ya milioni 30 tu. Tena anasema alipoenda
benki wamemkatalia kumpa hiyo pesa.” “Mama
James hasemi ukweli mama.” Geb aliingilia. “Jumatatu tulipokuwa Moshi. Tena
kabla hata hatujaondoka Moshi, meneja wa tawi la benki alilokuwa amekwenda
kuchukua hiyo pesa, alimpigia simu meneja wa benki yenye akaunti yangu hapa
Dar. Tena huyo Mzee naheshimiana naye sana. Naweza hata kuwapa namba yake.
Alinipigia simu kuniuliza kama kweli nimehidhinisha hiyo pesa itolewe kutoka
kwenye akaunti yangu huko Moshi. Akaniambia yupo kwenye simu nyingine na meneja
wa tawi la Moshi, yaani bado hajakata simu. Na mama yake James yupo hapo
ofisini na binti mwingine.”
“Tena alinisomea jina kamili la mama yake Jemes
kutoka kwenye kitambulisho chake. Maana huyu meneja wa hapa Dar alimwambia
akitoe kopi kitambulisho cha huyo mama amtumie saa hiyo hiyo kwa Fax.
Nikamwambia ampe hiyo pesa. Mimi ndiye nimemwandikia hiyo hundi. Lakini
nikamsisitiza ahakikishe wanasahihishana vizuri, halafu wanitumie kopi zote.
Yule meneja wa hapa alinipigia simu baadaye akaniambia ameshakamilisha kila
kitu na kopi zote za kuthibitisha amechukua malipo, anazo. Nikipata muda niende
ofisini kwake nikachukue. Sijakwenda mpaka leo, kwa kuwa nimekuwa na mambo
mengi. Kwa hiyo amechukua hiyo pesa.” Geb akamaliza kujitetea.
“Umesikia
mchungaji? Kwamba kithibitisho kipo?”
Mama G alikuwa kwenye spika. “Nimesikia. Sasa na
hilo salio?” Mchungaji akauliza. “Salio gani tena!?” Mama G
akauliza. “Amesema aliwadai milioni 50,
lakini mkampa milioni 30. Hivi amesema yupo hotelini amekuja kudai malipo yake.
Anasema mmemchukua Nanaa, mnaishi naye bila kumlipa. Amelalamika kuwa yeye
ndiye aliyehangaika naye tokea mtoto, lakini nyinyi ndio mnafaidi matunda yake.
Amesema hatatulia, mpaka apate haki yake. Atafanya lolote na kwenda popote
mpaka apate haki yake.” “Mungu wangu mama!” James
alikuwa ameshika kichwa. Nanaa ndiye alikuwa akilia sana.
~~~~~~~~~~~~~
Kila
James alipokuwa akitizama hali ya dada yake pale kitandani, haikuwa ikifanania
kabisa na mamilioni ya pesa waliyokuwa wakidaiwa. Nanaa alikuwa akivuja maji
pale kitandani! Vipimo vya awali vilishaonyesha hana tatizo. Inamaana
ataendelea kuwepo hapo ili lijulikane tatizo na ndipo matibabu yaanze. Akajua
na hapo tena kwenye hiyo hospitali yakulipia, patagarimu pesa nyingi sana. Sasa
wanalipaje tena mamilioni ya pesa ya mahari wakati pale tu alipolala dada yake,
James alijua ni pesa nyingi sana zitamtoka Geb!?
Chumba
alicholazwa Nanaa na huduma alizokuwa akipewa ni za hali ya juu sana. James
alijua ni mapesa mengi yatamtoka Geb. Japokuwa yeye mwenyewe alikuwa akilipiwa
matibabu na kampuni yake, lakini alijua hata kama angelazwa kwenye hospitali
hiyo, kampuni hiyo ingemudu kumuweka kwenye chumba cha angalau watu wawili tu.
Sio chumba cha peke yake kama vile.
Ni
mapenzi ya dhati kwa dada yake kutoka kwa Geb ndiyo yamemlazimu kumlaza Nanaa
pale. Ili kupata huduma ya haraka na makinifu. “Hawa watu watajitoa hivi kwa Nanaa mpaka lini? Mwishowe watamchoka au
wataanza kumuona ni mzigo.” James aliwaza.
“Hali yangu hii sio yakulipiwa
mamilioni ya pesa. Geb atashindwa. Ataniacha.” Nanaa aliendelea kulia huku akiwaza. Alijifunika
shuka akawa analia kwa uchungu sana.
Ni
kweli mtu huchagui uzaliwe wapi na nani. Na wala huchagui uzaliwe kwenye
mazingira yepi. Huchagui ndugu, wala kabila. Sasa kwa nini Mungu anaweka
wengine kwenye mazingira kama ya Nanaa? Nanaa alizaliwa na kujikuta mikononi
kwa mama yake James. Hakumbuki alipokuwa akilia wakati mchanga! Hakumbuki siku
wala muda alipokuwa akinyonya ziwa la mama huyo analodai malipo ya pesa nyingi
hivyo! “Kwani mimi nina mkosi gani jamani!?”
Ndilo swali ambalo Nanaa hakuweza kupata jibu lake.
~~~~~~~~~~~~~
Ukimya ulikuwa umetanda pale chumbani
wakimsikiliza mchungaji. “Huyu mama anaonekana anamaanisha
anachoongea mama G. Amesema bila kulipwa pesa yake, hiyo harusi haitafungwa na
wala hakuna atakayeweza kufaidi jasho lake.” “Anamaanisha nini?” Mama G akauliza. “Alikuwa
akiongea kwa jazba sana. Ilichukua muda kumtoa hapa ofisini kwani alikuwa
akionyesha vitisho.” “Vitisho gani?” Mama G aliendelea kuhoji. “Ni mambo mengi. Ikabidi kumtoa tu hapa. Maana watu hata wamtaani
walinza kujaa hapa kanisani. Lakini amesisitiza kama hatalipwa hiyo pesa yake
yote, hakuna mtu atakayefaidi matunda yake.” Wote wakavuta pumzi.
“Na mwingine ni
nani?” Mama G akahoji. “Kijana mmoja
amejitaja kwa jina moja tu, Zinda. Anasema Nanaa ni mkewe ila Geb amempokonya.”
“Amekuletea cheti chake cha ndoa aliyofunga yeye na Nanaa?” Mama G alitumia akili ya haraka sana. Akauliza
hilo swali. “Amesema atakileta kama tutataka
uthibitisho. Lakini na yeye amesema hiyo ndoa isifungwe, kwa kuwa Nanaa ni mke
wake kihalali. Ila Geb anatumia pesa yake kumrubuni mkewe.” Wote wakashangaa.
“Umesema amekwambia anacho cheti
chao cha ndoa?” Mama G akauliza tena
kuthibitisha. “Ndiyo.” Mchungaji
akajibu.
“Ndoa
aliyofunga yeye na Nanaa!?” Mama G akahoji
tena kwa mshangao. “Amesema nikikihitaji kwa
uthibitisho zaidi, atakileta. Na anasema kama sitachukua hatua maalumu,
anakwenda kwenye vyombo vya sheria. Na amesisitiza na yeye kuwa, Nanaa hatakaa
akaolewa na Geb, labda kama yeye sio mwanaume.” Hapo ndio kila mtu akabaki
anajiuliza ni mchezo gani Zinda anataka kucheza! Mama G akavuta pumzi kwa
nguvu.
~~~~~~~~~~~~~
Bado mambo yanazidi kumuwakia moto Nanaa. Hata hapo kitandani bado
changamoto zinaendelea kumfuata tu. Mwanzoni Geb
alionekana akiweza. Akalipa milioni 30 kwa haraka sana. Sasa
zinahitajika milioni 20 nyingine kwa ajili ya Nanaa aliyeoza
miguu na kuvuja maji hapo hospitalini.
- Je, bado ipo thamani ya kuendelea kulipia mipesa
yote hiyo? Pengine ndio kimya cha Geb akitafuta thamani hiyo na kujishauri kama
akimbie au abaki!?
Zinda naye amedai Nanaa ni mkewe halali na anacho Kithibitisho.
- Kipi? Maana ni kweli Nanaa alipotezana na familia hiyo ya
Magesa na kaka yake, akatokezea na
Liv.
- Alikuwa wapi?
- Ni kweli alifunga ndoa na Zinda?
- Je ni kweli Zinda anacho kithibitishi?
- Hao wote walijuaje kama siku hiyo ndiyo siku ya Tangazo la kwanza la Ndoa
ya Nanaa na Geb wkati hawakuwepo siku ya kikao cha kwanza cha harusi?
Kikulacho, kinguoni Mwako. Nani Ndumi
La Kuwili?
Usikose kufuatilia ili kujua.
0 Comments:
Post a Comment