“Mama!”
Grace aliita akisikika anaanza kulia. “Nakuja mama. Nilikuwa namuogosha mtoto.”
Wakamsikia analia. “Sasa wewe kamgongee kaka yake na Nanaa. Kumeshakucha hapa.
Na kazi ndio imeanza. Mwambie Nanaa afanye haraka aje hapa.” Danny akatoka,
akaona aanzie chumbani kwa mkewe kwanza amtulize ndipo apandishe juu kwa kina
Geb. Alimkuta amesimama vile vile kama alivyomuacha wala hajajigusa, analia.
“Pole Grace.” “Mama mbona haji
jamani? Sijui nifanyeje?” “Labda nikusaidie kuoga halafu…”
“Namtaka mama, Danny. Nimekutuma
ukamwite mama halafu unanipuuza! Hujali ninachokwambia! Unafikiri hapa
najisikia raha? Sijui kama naumwa njaa au usingizi! Usiku kucha wakati wewe
unakoroma mwenzio nilikuwa nateseka peke yangu. Sasa hivi nakutuma jambo dogo
tu una…” Danny akatoka kwa haraka na
kurudi kwa mama yake.
“Naomba
nipe mimi huyo mtoto mama. Grace atajifungua amesimama. Amelowa machozi na
maji. Na bado amesimama vilevile, palepale. Naomba msindikize akaoge twende
hospitalini. Unajua kuanzia sasa hivi hana atakayemsikiliza ila wewe. Nenda
mama yangu.” Mama G akatingisha kichwa. Alishamvalisha Liv, akamuweka
kitandani. “Wewe muache hapa hapa mpaka mama yake aje, nenda kawagongee.” Grace
alikuwa akilia kwa sauti ya maumivu.
Geb
alishituka sana Danny alipogonga. “Kwema!?” “Grace chupa imevunjika.” Geb
akacheka. “Naona Mzee umeshapaniki.” “Ameshaanza kulia. Hataki hata nimguse!”
Geb akacheka tena. “Mama si yupo naye lakini?” “Ndio ameenda sasa hivi.” “Ngoja
na mimi nivae, nakuja sasa hivi.” “Mwambie Nanaa mtoto alishaamka.” Danny
akaondoka.
Nanaa
aliamini maneno ya mama G. Grace hakuwa hata akitaka mtu mwingine amguse au
kumuongelesha zaidi ya mama yake tu. Mpaka inafika jioni Grace anajifungua,
mama G hakuwa akiweza hata kuongea kwa kuchoka. Geb na Danny walikuwepo
hospitalini, Nanaa alibaki nyumbani na watoto huku akiwasiliana na Geb kujua
kinachoendelea. Mara zote alipotaka kuzungumza na mama G, Geb alimwambia
haitawezekana mpaka Grace ajifungue. Hata wao hawawezi kuzungumza na mama yao
kwa vile Grace alivyomtawala. Hata alipopitiwa na usingizi hapo hospitalini,
alitaka mama yake aendelee kumsugua kiunoni yeye apumzike wakati uchungu
umetulia.
Mama
G na Geb walirudi usiku wote midomo ikiwa imewakauka. “Pole mama.” “Hata maji
kunywa ilikuwa kazi. Hivi alininyweshwa Geb.” “Kwa nini sasa!?” Nanaa akauliza.
“Mikono yote ilikuwa na kazi yakumsugua mzazi. Ikitoka hapo kiunoni au tumboni,
na yeye anaamka nakuanza kulia. Kuja kumnyamazisha tena, ni nusu saa.” Nanaa
akaanza kucheka. “Pole mama yangu. Lakini nimezungumza naye muda si mrefu,
anasikika anafuraha.” “Ndivyo alivyo. Shida ni pale akiwa anataka kujifungua.”
“Na lazima asubuhi mama awepo pale. Azungumze na manesi na kushika wale watoto
wake mpaka aruhusiwe.” Geb akaongeza.
“Na nisichelewe kwenda huko hospitalini. Lasivyo nitakuta analia kama mgonjwa
vile.” Mama G akaongeza, wakacheka. “Pole mama. Kaa hapohapo nikuletee
chakula.”
Mahari Ya Nanaa Yawa Ya Misuko Suko.
Baada
ya kama miezi 3 ya hekaheka ya ulezi wa watoto hao wanne ndani ya nyumba moja,
Oliva akiwa anakaribia miezi 6, na watoto hao wawili wa Grace ambao walikuwa
wanakaribia miezi 3, ndipo James alipiga
simu akimtaka Geb na Danny wakutane nae mahali ili wazungumzie swala la mahari
ya Nanaa. Geb alitoka kazini kwa haraka, akiwa amejawa furaha. Akamkuta Danny
na yeye ndio anaegesha gari yake. Wakasalimiana, wakaingia ndani wakijua James
alitangulia maana gari yake waliiona imeegesha hapo nje.
Wakamkuta
amekaa kwenye meza peke yake, lakini hana furaha. Wakajua ni kazi nyingi tu za
siku hiyo, maana ndio juma lilikuwa lipo ukingoni. “Kwema kaka?” Danny akasalimia.
“Kwema.” James akajibu huku akimvutia Danny kiti. Wakakaa.
“Samahani kukuchelewesha kwenye swala la
mahari Geb. Sio kwamba nilisahau, ila mambo yamekuwa magumu mno. Lakini naomba
usimwambie Nanaa. Hii kitu imezua ugomvi kupita kiasi.” “Ni nini tena!?” Geb
akauliza.
“Daaah!
Sijui niwaambie nini! Lakini gafla sasa hivi kila mtu anamtambua Nanaa, na kila
mtu anataka kupokea yeye hiyo mahari ya Nanaa.” “Kwa nini sasa tusiwape wote?”
Geb akauliza. “Subiri kwanza Geb. Unamaana ulipe mahari ya Nanaa zaidi ya mara
moja!? Kwa nini wasipokee kwa pamoja wakagawana!?” Danny akauliza. “Hawataki.”
James akajibu.
“Mimi
nitawalipa kila mtu. Nataka haya mambo yaishe jamani.” “Basi naona akili ya Geb
ikawa kama yangu. Nikawaambia kila mmoja wao. Yaani bibi na mama. Wanipe tarehe
zao wanazotaka tuwapelekee hiyo mahari. Kila mmoja aandike anachotaka atalipwa
kwa wakati wake. Hapo napo kukazuka maneno. Mama anasema bibi alimkana mama
yake Nanaa na alikataa hata kumwangalia Nanaa mwenyewe. Akamuachia mzigo wote.
Iweje leo atake kulipwa! Nikajaribu kumwambia yeye asihangaike na atakacholipwa
bibi, aniambie anachotaka yeye. Pia akakataa. Akasema kama bibi atalipwa mahari
ya Nanaa, yeye hataki. Ni kama akazira.” “Kwa nini hukuzungumza na Mzee?” Danny
akauliza.
“Hapo
napo pakazua ugomvi wa aina yake. Mama anasema baba naye alimkana Nanaa tokea
mwanzo. Hataki hata kumsikia anamtaja Nanaa. Nimehangaika wee, ndio nikamwambia
basi yeye anipe mahari anayotaka kulipwa. Akasema nimuahidi kuwa bibi hatawahi
kupokea hata shilingi ya Nanaa. Nikamwambia huko siwezi kuingilia. Akazira
karibia siku 20. Nikimsalimia haitikii. Haya, week mbili zilizopita akanipa
orodha ya vitu anavyotaka apelekewe na pesa anazotaka kulipwa kwa ajili ya
kumlea Nanaa. Akanitajia hiyo pesa, nikamkatalia kabisa. Nikamwambia hawezi
kumuuza Nanaa kama ng’ombe! Akasema yeye alikesha akimlea Nanaa, lazima alipwe.
Nikakataa. Akazira tena.” “Anataka kiasi gani?” Geb akauliza akitaka kufupisha
mambo.
James
akabaki anatingisha kichwa huku akisikitika. “Ni kiasi gani?” Geb akauliza
tena. “Nashindwa hata kukutajia Geb. Lakini ujue muda wote huo nimekuwa
nikihangaika kumbembeleza apunguze.” “Umefikia wapi?” Geb aliendelea kuhoji.
“Daaah! Yaani mpaka najisikia aibu kutaja.” “Sema tu James.” Danny akasisitiza.
“Yaani
amepigia hesabu mpaka maziwa aliyokuwa akimnyonyesha Nanaa, kifuani kwake!
Garama za miaka yote aliyokuwepo Nanaa pale nyumbani. Chakula, malazi na mavazi.
Muda uliomgarimu kutofanya kazi na kukaa nyumbani kumlea Nanaa. Akataka…”
“James! Nataka kujua anataka kiasi gani, basi.” Geb alimkatisha. “Daah!” Bado
James alisita kutaja. Waliuona ule ugumu mpaka kwenye macho ya James.
“Naombeni
mnisikilize jamani. Nilazima nitamuoa Nanaa. Kwa garama yeyote ile, nitamuoa
Nanaa, kwa kuwa ndiye mke wangu. Hakuna jinsi nyingine. Kama kazi yote
ninayofanya, kuanzia asubuhi mpaka usiku, haitaweza kulipa hiyo garama ya
Nanaa, basi nitakopa hiyo pesa. Ninachotaka kujua tu, ni kiasi gani?” Geb akasisitiza.
“Nitakusaidia Geb.” James akaongeza. “Unisaidie kumuoa Nanaa!?” Geb akamuuliza
James kwa kumshangaa sana.
“Sitaki
ufikirie ni kama nimekula njama na mama yangu ili kupata pesa kutoka kwako! Na
sitaki uone ni kama unamnunua Nanaa. Ndio maana nataka wewe umlipe nusu, nusu
nitampa mimi na nyingine kama atadai. Kwa sababu hata hicho kiasi, nimemtajia
jana kwa kumsisitiza kuwa ndiyo atakayo lipwa. Si zaidi ya hapo.” “Akakubali?”
Danny akauliza. “Atakubali tu.” “James? Mbona unashindwa kuzungumza? Mama
amekubali hicho kiasi au la?” “Amekubali.” James alijibu akionyesha hana
uhakika.
“Amekubali
kwa kiasi gani?” Geb akauliza tena. “Milioni...” James alitaja kwa upole sana.
“Duuuuh!” Danny alishituka sana. “Lini yupo tayari nilete hiyo pesa?” Geb
akauliza bila wasiwasi. “Utalipa pesa yote hiyo!?” Danny akauliza kwa mshangao.
“Ninamuoa Nanaa. Naomba uniambie ni lini natakiwa kuja kulipa hiyo pesa,
nimalizane nao yaishe.” “Mimi nitakusaidia Geb.” Danny akajitolea. “Asante
Danny. Lakini mimi ndiye ninaye muoa Nanaa. Acha nitalipa mwenyewe tu.” “Lakini
kuna orodha ya vitu vingine vinatakiwa Geb, acha tukusaidie.” “Hapana. Baba
yangu angekuwa hai, hilo ndilo lingekuwa jukumu lake. Lakini hayupo. Na mimi
ndiye Magesa mwenyewe. Nikishindwa kumuoa Nanaa sababu ya pesa, nahisi
sistahili kuwa mtoto wa yule Mzee. Ninachotaka msaada kutoka kwenu ni
kunisindikiza tu. Lakini garama zote ni juu yangu. Nitamuoa Nanaa, mimi
mwenyewe kwa jasho langu.” Danny na James wakanyamaza.
“Kama
hamna kitu cha ziada, naomba mimi niwahi nyumbani. Najua sasa hivi Liv na Nanaa
watakuwa wakinisubiria. Siku hizi Liv akiniona tu ananyanyua mikono yote juu
huku ananichekea akitaka nimbembe. Kwa hiyo naomba niwahi.” Danny na James
wakacheka kidogo. “Basi nitamkabidhi Danny kesho. Nilishindwa kuja na hiyo
orodha kwa kuwa sikujua kama utakubali kulipa hiyo pesa yote.” “Hakuna shida.
Hata hivyo nashukuru sana James. Uwe na usiku mwema. Danny, tutakutana
nyumbani.” Geb akanyanyuka na kuondoka. Alimuacha Danny na James wakifikiria.
Jinsi pesa ilivyo ngumu kwa wakati huo, halafu mtu adai mamilioni yote hayo ya
pesa! Hakika haikuwa ndogo hata kwa tajiri. Waliamini kuwa Geb amekusudia kuoa
kweli kweli.
~~~~~~~~~~~~~~
Na
kweli Geb alipoingia tu nyumbani Liv akaanza kucheka. Moyo wa Geb ulijawa na
furaha ya namna yake. “Njoo mama yangu mzazi. Njoo.” Ile furaha iliyojaa
moyoni, kumuona Liv na mama yake pale nje barazani, wakimsubiria yeye! Tayari
akaona yale mamilioni ya pesa ni kiasi kidogo sana kulinganisha na
anachojisikia kwa wakati ule. “Muone anavyocheka.” Nanaa akamkabidhi kwa baba
yake. Geb akambusu mara kadhaa, akamkumbatia kwa kumuweka kifuani kwake.
“Mmmmh!” Geb alisikika akisikilizia ile raha rohoni mwake. Oliva alizidi
kucheka.
“Dimpozi
kama za mama yako!” Geb akambusu tena mashavuni. “Ananirembulia tokea saa moja.
Ikabidi kumtoa hapa barazani kucheza naye ili asilale bila kukuona.” “Poleni.
Nimechelewa. Nilikuwa nakutana na James.” “Kwema?” Nanaa akauliza. “Kwema. Ni
mambo ya mahari.” Nanaa akatulia kidogo. “Usiwe na wasiwasi. Tutafanikiwa tu.”
“Sidhani Geb. Nahisi kuna kitu kinaendelea tu, lakini kaka hataki kuniambia.
Unajua ni zaidi ya miezi mitatu sasa tokea tumuombe afuatilie mambo ya mahari?
Nilimpigia simu majuzi, akababaika kweli, akashindwa kunipa jibu la moja kwa
moja! Nikahisi kuna kitu ananificha.” “Lakini naona amefikia pazuri. Kesho
amesema atamkabidhi Danny orodha ya hiyo mahari.” Nanaa akanyamaza.
“Tutafanikisha
Nanaa. Usiwe na wasiwasi.” “Natamani iwe hivyo Geb. Na mimi natamani kuvaa
shela! Nisimame na wewe kanisani.” “Shauku yako itatimia hivi karibuni.
Tuendelee kuomba.” Geb akamvuta karibu kwa mkono wake wa kushoto, akawakumbatia
wote wawili. Nanaa na Oliva. Alimbusu Nanaa kichwani. Wakasimama pale kwa muda
wakicheka na mtoto wao, kisha wakaingia ndani.
~~~~~~~~~~~~~~
“Ungechelewa kidogo tu, huyo angelala leo bila
kukuona.” Mama yake alimuwahi wakati wanaingia. “Nimechelewa kidogo leo.
Nilikuwa na Danny na James. Hivi nimemuacha Danny huko huko.” “Kwema?” Grace
akamuuliza. Geb akambusu mwanae. “Kwema. Ni mambo ya mahari.” Alijibu huku
akimwangalia mwanae. Kwa ujibuji ule, Grace na mama yake wakajua hataki maswali
zaidi. Wakaamua wanyamaze.
“Umeshindaje
na watoto?” Geb akamuuliza dada yake. “Wanakazi ya kunyonya tu. Basi hapa hamna
kingine ninachofanya zaidi ya kunyonyesha! Mpaka mgongo unauma!” “Nimekuletea
kitu chakufunga kiunoni. Kusupport mgongo wakati unanyonyesha.” “Afadhali.
Asante.” “Nimeacha kwenye gari. Nitafuata. Ngoja niongee na Oliva kidogo. Eti
mama?” Geb akambusu na kupandisha naye juu chumbani kwake. Nanaa akafuata
nyuma.
~~~~~~~~~~~~~~
Kesho
yake Danny akarudi nyumbani na orodha ya vitu vya mahari anayotakiwa Geb
kulipa. Akataka kumkabidhi Geb lakini
mtoto wake akamuwahi. Aliwakuta nje, Geb na Fili wakicheza. Fili akamkimbilia
baba yake. “Nimemfunga anko.” Akajisifia kwa baba yake. “Hongera mwanangu.
Uendelee kumfunga hivyo hivyo.” Geb akacheka akitingisha kichwa. “Wewe Fili!
Nani kamfunga mwenzake hapa?” “Wewe 3, mimi mbili.” Fili alijibu kwa kujiamini.
“Sasa mimi si ndio mshindi?” “Lakini na mimi pia nimekufunga anko.” Danny na
Geb wakacheka. “Kichwa hicho, hukiwezi kwa hoja.” Danny alimsifia mwanae.
“Kweli simuwezi!” Wakacheka.
“Vipi
huko ndani? Maana nilipigiwa simu nusu saa iliyopita, nikasikia kumechangamka
kweli! Kama wodi ya watoto!” Geb akacheka. “Naona kumetulia.” Geb akajibu. “Afadhali.
Maana nimeambiwa nirudi haraka nije kuchukua wanangu wote.” Geb alizidi
kucheka. “Ndio maana nimemtoa huyu nje. Naona wanamchangamsha kweli Grace!”
Danny akacheka. “Ngoja niwahi ndani kabla ya yeye mwenyewe hajaanza kulia.
Maana hakawii Grace!” Danny akaingia ndani.
Baada
ya muda Geb naye akaingia. “Usingerudi kwanza Geb! Mwanao akikuona, hatakula tena.”
Mama yake alimuwahi. Oliva alivyomuona tu baba yake akanyanyua mikono yote juu
huku anacheka. Chakula chote alichokuwa ameweka mama yake mdomoni kwake,
kikaanza kutoka. “Liv jamani! Cheka gani hiyo mpaka unatema chakula bwana!?”
Nanaa akalalamika. Walikuwa wamemkalisha kwenye kiti chake, wanamlisha.
“Mbona
mwanangu anaonekana hafurahii hicho chakula? Mnamlisha nini?” Geb aliuliza huku
akimsogelea. “Ndio namkazania. Leo siku ya pili tumemuanzishia uji.” “Basi
naona hataki.” “Usiseme hivyo bwana Geb! Huyu mtoto lazima aanze kula.” “Sasa
kama hataki!?” Geb akauliza huku anamchekea mwanae. Tayari Liv alishaanza
kufunga vidole vyake na kuvifungua kama anayemwita baba yake. Geb akamsogelea
na kumbusu.
“Eti
Liv mama?” Mtoto akaanza kujinyanyua pale kwenye kiti ili baba yake ambebe.
“Mwache bwana Geb!” Nanaa akalalamika. “Sasa kama hataki kula hicho chakula
chenu?” “Basi huyo atatonya tu mpaka anaanza shule!” Mama yao aliingilia.
“Atakuja kula bwana mama.” “Lini wakati unamtoa hapo? Mwache mama yake amlishe
kidogo.” “Sasa ananitaka je!” “Haya!” Mama G akaamua anyamaze. “Njoo mama. Njoo
eeh!” Nanaa alibaki akimwangalia Geb na mwanae. “Muone naye anavyocheka! Basi
kazi yake ni hiyo tu. Kucheka. Ukimpa kitu chochote ale, yeye anakuchekea huku
anatema.” Geb akacheka. “Eti Liv. Hutaki kula?” Geb akambusu.
Mahari ya Nanaa, Mzigo mzito.
“Hii
karatasi ya nini?” Grace aliokota karatasi aliyokuwa ameangusha mumewe. “Ni ya
Geb hiyo. Amenipa James nimkabithi. Ina orodha ya mahari ya Nanaa. Nilitaka
kumkabidhi mwenyewe pale nje, Fili akaniwahi na maneno mengi, nikasahau.”
“Afadhali!” Grace akafungua huku akionyesha kufurahia. Wote waliisubiria kwa
muda mrefu sana. “Haleluyaaaa!!” Mama G akaanza kupiga vigelegele vya shangwe.
Akasimama huku anapiga vigelegele.
“Mama!
Utafikiri yeye ndio anaolewa!” Grace alikuwa akimwangalia mama yake asimuelewe.
Nanaa akacheka akasogea. “Hatimaye. Maana nilishaanza kuingiwa na hofu!” Nanaa
alifurahia sana. “Hebu isome. Kesho nataka mkaanze kununua hivyo vitu,
tukalipie. Mchakato wa harusi uanze.” Mama G, akaongeza. “Tulia basi mama!”
Grace alimtaka mama yake akae. Akakaa, Grace akaanza kusoma huku Danny amebeba
watoto wake wote wawili, ametulia kama Geb aliyekuwa amebeba na yeye mwanae.
Kimya, akijua ule mzigo unaomkabili Geb.
Grace
akaendelea kusoma ile orodha. Mwanzoni ilikuwa vitu vya kawaida sana. Alipofika
karibu ya mwisho akatoa macho na kubaki ameduaa. “Nini!? Hebu maliza kusoma
bwana, usinitie presha.” Mama yake akamsisitiza. Grace akasita lakini akaona
asionyeshe wasiwasi mbele ya Nanaa. Akasoma. “Na fidia ya kumlea Nanaa tokea
anazaliwa mpaka anatoka nyumbani kwa mwanangu James!” Kisha akatulia kidogo.
“Iliandikwa Milioni 100. Naona ikafutwa kwa kukatwa
mstari hii tarakimu nzima. Kisha mbele yake imeandikwa hapa milioni 80. Nayo pia
nimeona imekatwa tena. Ikaandikwa tena Milioni 50. Ikafutwa tena kwa kukatwa
mstari. Naona imeandikwa tena Milioni 30 kwa kalamu nyingine, tena sio ile ile
ya bluu. Hii milioni 30 imeandikwa kwa kalamu nyeusi.” Grace alitambua muandiko
wa pili ulikuwa wa James. “Tena ni mwandiko wa James huu!” Ukimywa mkubwa
ukatanda. Nanaa akachukua ile karatasi akaanza kuisoma upya.
Mama
G ndipo akaelewa kwa nini jana yake Geb hakutaka kuongelea swala la mahari.
Walimuona Nanaa anafuta machozi wakati akisoma. Geb akamsogelea. “Njoo.” Geb
alimuita lakini Nanaa akashindwa hata kusogea. Aliendelea kulia huku akisoma.
“Daah! Hii pesa wanayotaka ni ndefu sana jamani! Kwa nini wanafanya hivyo!?”
Grace alilalamika. Danny kwa mara ya kwanza akanyamaza. “Usilie Nanaa. Njoo.” Nanaa
akakataa kwa kutingisha kichwa huku akilia sana.
“Nanaa!” “Hapana Geb. Hii imezidi jamani. Mimi naona
sitaweza tena. Ni heri tuache haya mambo. Heri ukaoe mtu mwingine. Wanakuwa
wananiuza kama ng’ombe jamani! Hii sio haki kwangu. Tena watu wenyewe hata
hawanithamini! Majina yao yenyewe walikataa nisitumie. Sio la baba yake James
tu, hata bibi alikataa nisitumie jina la ukoo wao. Nikaishia kuitwa jina la
mama yangu ndio kama jina la ukoo au la baba yangu! Yaani maisha yangu yote
nimeishia kuitwa Nanaa Wini. Nimekaa kwao nikiwatumikia tokea mtoto huku wakiniambia nalipia
chakula ninachokula na malazi. Kweli mpaka leo hiyo garama yangu sijamaliza
kulipa tu!? Hapana Geb. Inatosha.” “Kwa
hiyo unaniacha?” Geb akamuuliza, Nanaa akazidi kulia.
“Nanaa?”
“Sijui Geb. Lakini hapana. Na
usidhani hapo kwa kaka kuandika hiyo milioni 30 kwa mwandiko wake ni bure. Ujue
wameshindwa kufikia muafaka. Mwandiko huu ni wa
mama mkubwa. Na Grace hujasoma karatasi ya chini. Ameandika fidia anazotaka
alipwe mpaka maziwa niliyomnyonya kwenye matiti yake! Wakati na mimi
alishanilipisha hizi fidia zote, jamani! Alisema haajiri mfanyakazi mwingine
pale ndani sababu mimi natakiwa kulipa fadhila ya hivi vitu vyote alivyoandika
hapa. Alinitajia kila kimoja wapo hapa, Geb. Yaani hii orodha hapa kwangu mimi
sio ngeni. Nimekuwa nikitajiwa mchana na usiku. Kama ilivyo hivi hivi. Tokea
nakua mpaka ananifukuza pale kwa kaka. Naweza kuwatajia hivi vitu vyote hapa
bila hata kusoma, vile vilivyokaa kichwani kwa kuvisikia mara kwa mara. Tena
nikiambiwa nilazima nilipie. Na nilikuwa nalipia kimoja baada ya kingine. Hivi
hivi kama ilivyoandikwa hapa. Hapana. Inatosha Geb. Hivi vitu nilishalipia kwa
mateso mengi sana. Nitadaiwa mpaka lini?”
Nanaa aliendelea kulia.
“Njoo
Nanaa mwanangu.” Mama G na yeye akamwita. “Hapana Mama. Hapana. Kuzaliwa kwangu na kukua kwangu kumekuwa ni shida
tupu mama yangu. Hujui mateso niliyopitia kulipia hii orodha nzima. Nimelipa
kwa machungu makubwa sana. Mama mkubwa hanidai. Nishalipia mimi mwenyewe mama.
Hakika nimemlipa. Heri nisiolewe kuliko kumlipa tena. Nilikuwa wakati mwingine
nafungiwa nje. Usiku. Baridi kali. Nafua nguo za watoto wake, mpaka vidole
vinakuwa vinakufa ganzi kwa baridi. Hapo sina sweta, sijala wala kupumzika
tokea asubuhi. Anasema natakiwa kulipia hiki au kile. Hapana mama yangu. Kama
ni hiyo ndoa basi.” Nanaa akaendelea kulia kwa
uchungu sana.
Kipenda Roho.
Geb
akamkabidhi Liv kwa mama yake, akaenda kumchukua Nanaa. Akamshika mkono,
wakaelekea juu chumbani kwao. Kila mtu alikuwa kimya. “Hapana Geb!” Nanaa
aliendelea kulia. Geb akamkumbatia. Nanaa alilia, huku Geb akimsugua mgongoni.
Wakahamia kitandani. “Nakupenda Nanaa.” “Utapata tu mwanamke mwingine Geb. Mimi hapana.” “Niangalie.” Nanaa alifanya kosa la kumwangalia.
Geb akambusu. Akarudia tena na tena huku amelala naye pale kitandani akimpapasa
taratibu. Aliendelea kunyonya midomo yake mpaka akahakikisha akili ya Nanaa
imerudi pale kitandani.
“Nakupenda
wewe Nanaa.” “Na mimi nakupenda
Geb, lakini…” Geb akamuwahi kwa busu kabla
hajamalizia kisha akaongea yeye. “Unajua kitu ninachotamani kila siku asubuhi
ninapoamka?” Nanaa akatingisha kichwa kukataa. “Kila nikiamka, najua nilazima
niende kazini. Lakini kuanzia muda naondoka hapa nyumbani nakua natamani jioni
ifike, nirudi nyumbani, nikukute wewe na Liv, mkinisubiria mimi pale nje. Zile
dimpozi za yule mtoto anavyozitoa kwangu. Akicheka na kukunjua vile vimikono
vyake akinitaka mimi! Halafu kakitulia hapa kifuani kwangu! Oooh my! Kwangu ni
kitu cha thamani ambacho hakuna kiasi cha pesa kinaweza kununua hiyo furaha
ninayosikia moyoni. Hakuna Nanaa. Nakuahikishia mpenzi wangu, siku utakayokataa
nisikuoe sababu ya pesa, ujue umenimaliza kabisaa.”
“Uwezo
mkubwa nilio nao wa kutengeneza pesa sasa hivi, ni kwa ajili yako mpenzi wangu.
Nimetulia. Akili inafanya kazi vizuri, sababu ya maisha uliyonipa. Sina jinsi
nyingine ya kukwambia ukanielewa. Acha tulipe hiyo pesa, uwe wangu. Hata kama watataka milioni 100, nitawalipa
tu. Waache wakuuze. Uzuri mimi ndio nakununua. Huna chakupoteza. Huingii aibu.
Hiyo pesa itarudi tu. Mungu yupo na sisi.” Nanaa hakuamini.
Aliinama
akaanza kulia tena. “Huwezi kujua kwa nini Mungu ameruhusu hayo yote yakupate.
Lakini maadamu tupo wote, na uwezo upo, mimi nitalipia.” “Labda na mimi nitafute kazi ili nikusaidie
kulipa.” Geb akacheka. “Na kaka yako
James alitaka kunichangia nusu ya hiyo pesa, nimekataa. Mimi nitalipa Nanaa.
Kama nina uwezo wakununua magari ya mamilioni ya pesa, sitashindwa kununua
uhuru wako. Tuwalipe tu ili uwe huru. Tena utakuwa wangu kihalali. Wote
tutakuwa tukiitwa Magesa. Wewe, Oliva na mimi. Wote tutakuwa Magesa.” Nanaa
akacheka.
~~~~~~~~~~~~
“Asante Geb.” “Kavu kavu tu!?” Nanaa akampiga ngumi
kidogo. “Yaani kazi yote niliyofanya ya kukubembeleza naishia kupewa asante
tu!? Nipoze kidogo basi.” Nanaa alicheka mpaka akageuka upande mwingine. “Geb!”
“Kweli tena.” “Mtoto hajala bwana. Baadaye.” “Wewe usijiguse hata kidogo. Na
sikuvui nguo zote. Niruhusu chini tu.” Geb alishapiga magoti na kumfunua
kigauni alichokuwa amevaa.
Akaanza
kubusu mapaja yake huku mikono ikiwa na kazi ya kumtenganisha na nguo ya ndani
nyembamba aliyokuwa amevaa. “My My Myyyy! Uuuuu!” Geb alikuwa akiongea huku
akimtizama Nanaa kwa uchu. Wazi alionekana anafurahia anachokiona. “Hii chupi
ya wapi tena?” “Nilienda leo madukani na mama.” Nanaa aliongea kwa sauti ya
chini iliyojaa kujivunia na kufurahia sifa anazopewa. “Imekupendeza!” “Asante.
Nilijua utaipenda tu.” Geb akabusu juu ya ile chupi. Akapitisha kidole chake
kwenye lastiki ya kiyo chupi kuzunguka kiuno. Mwili mzima wa Nanaa ukasisimka.
Akabaki akisugua mapaja na tabasamu usoni huku akinyonya lips zake.
Midomo
ya Geb ikatua kwenye kitovu chake, akambusu na kuweka kidole chake pale.
“Nakupenda Nanaa.” “Na mimi nakupenda Geb.” Geb alimgeuza kwa haraka. Akamuweka
style ya kupiga magoti akiwa ameinama. “Mmmh! Mh! Mh!” Geb alimpapasa juu ya
kiuno huku akimbusu kila eneo juu ya kino chake. “Hakuna pesa inayoweza kununua
hii.” Tarati Geb alishaingia. Nanaa alimsikia akisugua meno. Akajua anapata
starehe aliyokuwa akitarajia. Akafurahia. Mikono yake ilikuwa imeshika hips za
Nanaa kwa nguvu. Baada ya muda mfupi sana Geb akamaliza.
“Daa! Leo mbona umezidi kuwa wa moto kuliko
siku nyingine?” “Umefurahia?” “Sana. Ukatikaji huo nilishakwambia unanifanya
nashindwa kujizuia.” “Nilitaka umalize haraka, nikamlishe mtoto.” Geb akacheka.
“Mawazo yako kwa Liv, mwili kwa baba yake!” Nanaa akacheka. “Ndio ujue wote
tunakuhitaji. Twende tukamalizie siku, uje unipe mwili na akili zako. Navitaka
vyote viwe hapa. Na hivi kesho nitachelewa kwenda kazini! Basi acha nilifaidi
hilo joto leo.” “Halafu nimepitisha siku zangu Geb.” “Waache waje hao watoto.
Hata kama ni mapacha, tutalea tu.” Nanaa akacheka. Akanyanyuka pale kitandani,
akakimbilia bafuni. Geb akamfuata.
Kule
kumkuta Nanaa yupo uchi huko bafuni akitaka kuoga mara moja ndipo ashuke
akamlishe mtoto, ikawa kosa. Hapo Nanaa akasahau hata mtoto. Walizungushana
huko bafuni, wakajikuta wamerudi tena kitandani huku wameng’ang’aniana. Mapenzi
ya haja yakaendelea pale kitandani. Mpaka waliporidhika ndipo wakatoka hapo
chumbani.
~~~~~~~~~~~~
Walikuta
watoto wote walishaenda kulala kasoro Fili alikuwa anacheza game kwenye simu ya
mama yake huku Grace amempakata na kumbusu kila mara. Alishaogeshwa na kuvaa
nguo za kulalia tayari. “Liv yuko wapi?” “Alishakula, akaoga, nimemlaza muda
tu.” Mama G, akajibu kama anawasuta. Nanaa akainama huku akicheka. “Lakini
kesho nitaenda naye kazini. Nikamfundishe biashara.” Geb akamvuta mkono Nanaa
akamkumbatia. “Ni lini James amesema tukalipe hiyo mahari?” Geb akamuuliza
Danny. “Jumamosi ijayo ndio mama yake amesema atakuwa na nafasi.” “Basi naomba
tujiandae. Jumamosi ijayo tutalipa hiyo mahari.” Geb aliongea akisikika
kujiamini.
“Nimeamua
kukusaidia Geb. Nusu ya hiyo pesa, mimi nitalipa kwa niaba yangu na baba yako.”
Geb akacheka. “Nakushukuru sana mama yangu. Hata James na Nanaa walitaka
kunisaidia, lakini nimekataa. Mimi ndio nitalipia mahari ya Nanaa.
Nitakachoomba ni muwe tu na mimi. Basi.” Mama G akaanza kupiga tena vigelegele.
“Basi
watoto wote wataamka! Mwenyewe nataka muda na mwanangu Fili tu. Nina hamu naye
kweli! Lakini kwa shamra shamra hizi! Wale watoto wawili wa Danny, sijui kama
watalala!” Grace alitaka mama yake anyamaze. “Liv akiamka ndio nitafurahi.” Geb
akajibu huku akicheka vile mama yake anavyocheza. “Mimi sitaki lile jeshi la
Danny liamke bwana! Mgongo wote unauma kwa kubeba!” “Unakumbuka kuvaa ile belti
niliyokuletea lakini?” “Wewe si umewaona wakianza kulia wanavyokuwa? Huwezi
kukumbuka hata kuvaa nguo!” Geb na Nanaa wakacheka. Danny akatingisha kichwa.
“Muulize
mama na Nanaa. Hawa watoto leo asubuhi mpaka waliniliza mimi! Wanalia kama
kengele! Nilikuwa naoga, nimetoka bafuni nakimbia. Nimeshinda na taulo siku
nzima mpaka walipolala.” Geb alizidi kucheka huku akimwangalia dada yake.
“Watakuwa tu. Utapumzika.” “Mmmh! Sioni dalili. Na hivi walivyofanana na Danny
hao, nahisi hizo kelele ni za milele.” “Nakwambia lawama zote ni zangu.” “Kumbe
unafikiri wamerithi kwa nani? Watoto wawili utafikiri jeshi la Iraq! Mpaka
nimekonda wakati nakula kama mchwa! Hongereni mwaya.” Grace alimgeukia Nanaa na
Geb.
“Nanaa!
Ndoa ni nzuri mdogo wangu. Usikubali watu wakakukosesha baraka za ndoa. Kuna
vitu vingine kwenye maisha, vinapaswa kulipiwa garama. Wewe ni wa thamani sana.
Ndio maana kila shetani akikuangalia, anashindwa kukuthaminisha. Anaishia
kuongeza bei tu.” Mama G akapiga tena vigelegele. “Ongea mwanangu Grace.
Umeshindwa shetani!” Mama G akaendelea kupiga vigelegele. “Basi leo hatutalala!”
Grace alifanya wote wacheke.
“Asanteni
jamani. Na samahanini. Ni kweli najisikia vibaya. Ni hivyo sina jinsi
yakufanya.” Nanaa aliongea kinyonge. “Hivi unakumbuka habari ya Yusufu? Yule wa
kwenye bibilia? Unakumbuka aliuzwa na ndugu zake?” Nanaa akatingisha kichwa
kukubali na kuongeza. “Nakumbuka mama.”“Mwisho wake unaukumbuka? Mbali na
mateso mengi aliyopitia, kumbe vyote vile Mungu aliviruhusu ili ajifunze na akomae
hata kiroho chake, ili anapomfikisha sehemu ya juu aweze kuishi na ile baraka.
Ipo sehemu ya juu sana Mungu amekuandalia Nanaa. Na hakuna anayeweza kukaa hapo
isipokuwa ni wewe tu. Kwa kuwa umepitishwa shule kama yako na ukafaulu.
Usipokata tamaa na kuishia njiani kama wengine, ukavumilia mapito yako mpaka
mwisho, hakika utakuja kumshukuru Mungu. Unakwenda kuinuliwa mpaka ushangae.
Utabarikiwa mpaka moyo wako ufurahie na watu wakuite heri.” “Amina mama.
Asante. Nashukuru kwa kuwa na mimi mpaka sasa. Hujanichoka.” Nanaa alianza kulia tena.
“Nikuchoke
tena!? Wala. Tena hata kidogo. Wala usilie. Ukiona mama G amekukatia tamaa,
ujue hata mbingu zimekukataa. Wewe tulia. Furahia. Jiandae kwa moyo mweupe,
ukijua utaolewa tu mwanangu. Ngoja tukalipe hiyo mahari tuanze mikakati ya
harusi. Nitakununulia gauni hilo, ukiingia pale kanisani watu wataulizana.”
“Mama G kwa kupenda shuguli!” Grace alikuwa akimwangalia mama yake, hammalizi.
“Watoto wenyewe nilipewa wawili tu. Wakati unaolewa wewe, sikuwa na uwezo.
Haya, akishaoa Geb, ndio basi tena mpaka Fili. Sasa ni leo hiyo? Heri
nichangamke sasa hivi nikiwa na nguvu.” “Basi mama wakati wewe unashangilia,
sisi tule.” “Kesho asubuhi, Danny na Geb mnaenda kununua vitu vyote kwenye hiyo
orodha. Na msiniletee vitu vya ajabu.” Mama G aliendelea kusherehekea usiku ule
bila kuchoka.
Jumamosi.
Waliamka
siku ya jumamosi. Geb akaenda chumbani kwa mama yake moja kwa moja kumfuata
mwanae. Oliva alikuwa kwenye kitanda chake wakati baba yake anaingia. Akaanza
kucheka huku amenyanyua mikono yake juu. Akifunga na kufungua viganja vyake.
“Njoo mama yangu. Leo tunaenda wote kazini.” “Sasa vitu vya mahari mtaenda
kununua saa ngapi Geb bwana!? Mbona unataka kuniharibia mambo!” “Sikiliza mama
G. Mimi na Oliva tunakimbia kazini mara moja tu. Kuna mzigo unaingia asubuhi
hii. Baada ya muda mfupi tu, narudi. Eti
Liv? Utamsindikiza dad?” “Ana kazi ya kucheka tu huyo mwanao. Ukimuogesha,
anacheka. Ukimlisha ndio kabisaa. Atacheka mpaka chakula kinatoka mdomoni.” Geb
akambusu. Liv akacheka tena.
“Eti
mama? Wewe unacheka tu. Huna tatizo na mtu?” Geb akambusu tena. “Naona unazidi
tu kupendeza. Umemwambia bibi asante? Haya, twende tukampe bibi busu la
asante.” Akaenda kumbusu mama yake kichwani mara mbili. “Hili la Liv, na hili
langu.” “Nataka kutoka kwa Oliva mwenyewe.” Geb akamuinamisha mwanae shavuni
kwa bibi yake. Olivia akamlamba. Wote wakacheka. “Shavu zima limejaa mate!”
“Hapo ndio nimefurahi. Mwache anipake mate atakavyo.” Mama G akajibu akisikika
kufurahia busu la Oliva. Geb akambusu tena Liv, kisha akatoka naye nje.
“Twende
kwa mama. Akupe nyonyo, halafu tukatafute pesa.” Mama G aliwasikia wakiongea.
“Kanywa uji huyo!” Mama G akajibu yeye akiwa bado chumbani. “Mimi ratiba zenu
zinanichanganya. Kwa hiyo mwanangu nyonyo ndio basi?” “Sasa mama yake mwenyewe
haonekaniki, nitafanyaje? Nikampa uji.” Geb akacheka bila kujibu. Tokea
walipoamka walikuwa na Nanaa chumbani. Hakuna aliyemkumbuka mtoto. Hata usiku
walimuacha akalala chumbani kwa bibi yake.
Geb
akatoka chumbani akiwa yeye, Nanaa na mtoto wao. “Basi hivyo, hamtakaa mkarudi
leo. Sasa hapo Nanaa wewe anaenda wapi?” “Kwenda kunyonyesha, mama.” Geb
akajibu kwa haraka. “Mmmh!” Akaguna. “Tunarudi mama, usiwe na wasiwasi.”
“Naomba uwahi Geb. Tafadhali sana. Nina week moja tu ya maandalizi ya hiyo
mahari. Sitaki unitie aibu. Nataka upate muda wakutosha kwenda madukani utafute
vitu vya maana. Kama unaona hutaweza mimi nitaenda mwenyewe.” “Mama! Nimekwambia
sitachelewa kurudi. Usiwe na wasiwasi. Nitaenda kununua vitu vyote. Na
ninakuahidi nitakuletea vitu vizuri kabla usiku hujaingia.” Mama yake
akanyamaza. “Sasa mbona huniitikii?” Geb akamuuliza huku akicheka. “Nitakuona
kama utawahi!” “Sikudanganyi bwana mama. Acha wasiwasi. Nanaa twende.”
Wakatoka.
~~~~~~~~~~~~
Na kweli kabla ya saa nane
mchana, Geb akarudisha familia yake nyumbani. “Mimi nipo tayari Danny. Naomba
unisindikize.” Danny akasimama. “Mbona hamli?” “Acha tu twende. Tutakula
tukirudi. Usiwe na wasiwasi. Ngoja tuwahi wakati hao jamaa wamelala. Nitafanya
haraka kurudi ili wakiamka wanikute.” Danny alijibu akimaanisha wanae. Fillius
na Fillan. “Sitaki mniletee vitu vya ajabu.” Mama G akasisitiza. “Mbona
unarudia rudia mama? Tushaelewa!” Geb alimjibu mama yake wakati anatoka. “Sitaki
unitie aibu.” “Sawa Mama G.” Geb alijibu huku akifunga mlango. Wakatoka kwenda
madukani.
Vitenge
na mablangeti alisema atanunua Mama G mwenyewe. Akawatuma kwenda kuleta vitu
vingine vyote vilivyobaki kwenye hiyo orodha ya mahari ya Nanaa. Walimkusanyia
vitu vyote vya hiyo mahari, wakamletea pale nyumbani. Mama G alianza kupitia
ile orodha. Aliweka alama ya tiki kwa kila kimoja wapo. Akakuta vyote vipo.
Akaanza kuangalia ubora wake, pia akaona wameleta vitu vizuri. Akaridhika.
“Sasa hapa naenda kununua mimi mwenyewe vitenge vya maana na mablangeti. Tena
mablangeti ya nguvu.” Mama G aliongea wakati anaweka vitu vizuri. Angalau Nanaa
akafarijika zaidi kuona mama mkwe wake pia hamuoni mzigo. Yupo bega kwa bega
kuhakikisha mafanikio bora.
Siku Ya Kulipa Mahari Ya Nanaa.
Ilikuwa
siku ya jumamosi ambayo mama yake James alisema angekuwepo hapo nyumbani kwa
James kupokea mahari ya Nanaa. James alipotaka baba yake na bibi wahusishwe,
angalau hata kuhudhuria kushuhudia upokelewaji huo wa mahari, mama yake
alikataa tena akiwa mkali akisema alimlea Nanaa yeye mwenyewe bila msaada wa
mtu, kwa hiyo atapokea hiyo mahari yeye mwenyewe. James hakutaka ugomvi. Akaona
akubali, yaishe.
Alitoka
asubuhi akiwa anaelekea kazini kama kawaida siku ya jumamosi kufanya kazi nusu
siku, kisha alipanga kupitia kwenye biashara zake, akiwa amekubaliana na Grace
aandae watu wakupika, catering, ili hiyo jioni walete chakula hapo nyumbani kwa
James ili wanapomaliza shuguli za mahari, basi waliohudhuria wapate chakula cha
pamoja, kwa kuwa alimjua mama yake hawezi kuwapikia wageni wa Nanaa.
~~~~~~~~~~~~
Danny
alishatuma kwenye group lao la marafiki kuwa jumamosi
hiyo watakwenda kulipia mahari ya Nanaa. Chakushangaza wakaona watu wengi
wanatoa mwitikio. Wengi walikubali kuhudhuria na kuwapongeza Nanaa na Geb huku
wakiendelea kuuliza ni nini cha kusaidia ili kufanikisha shuguli hiyo nzima ya
mahari, lakini Danny aliomba uwepo wao tu, nakuwashukuru.
~~~~~~~~~~~~
Ilipofika
saa 11:45 jioni, James akarudi nyumbani kujiandaa na mapokezi ya wageni.
Walikuwa wamekubaliana wafike hapo saa 12:30 jioni hiyo. Alikuta nyumba chafu
kama kawaida, akasafisha haraka haraka. Mpaka anamaliza kuosha vyombo walivyokuwa
wametumia usiku uliopita na kusafisha nyumba, tayari wageni walikuwa wamefika.
Marafiki wote na wake/waume zao walikuwepo pale. Wafanyabiashara wenzake wa
karibu na Geb, Mama G, Grace, Danny, na marafiki, wafanyakazi wenzake Danny na
James, wote walifika kwa wakati. Nanaa alibaki kwenye gari na Oliva. Mama G
aliwaambia wasubiri mpaka wakimaliza kulipa mahari ndipo wataenda kumchukua
kwenye gari na kwenda kumtambulisha Liv ramsi kwa mama yake James.
“Ngoja
nimuite mama, maana na mimi ndio nimeingia hapa muda sio mrefu.” James aliaga
wageni akiwa vilevile mchafu na akionekana alikuwa na shuguli nyingi hapo
ndani. Kwanza shati lake lenyewe lilikuwa limelowa. Aliingi kwenye chumba
walichokuwa wakilala mama yake, dada zake hao wawili na mtoto wake Viola, lakini
hakuwakuta. Alikuta tv ndio iliyokuwa ikiongea muda wote aliodhani wapo
chumbani wamejilaza huku wakiangalia tv kama kawaida yao. Kumbe waliacha tv
ikiendelea bila wao.
James
akaizima, na kuamua kumpigia simu mama yake. “Wageni
wameshafika, mama. Uko wapi tena!?” “Nyumbani kwangu.” James akatulia kidogo, akitamani asiwe amesikia
alichosikia. “Unamaanisha Moshi!?” “Kumbe nina
nyumba ngapi? Isingekuwa kumlea Nanaa labda sasa hivi ningekuwa na nyumba hata
tatu!” “Si ulisema leo ndio waje kutoa mahari ya Nanaa, kwa nini unafanya hivyo
mama jamani!?” “Kumbe sikuwa nimekwambia? Niliamua leo kuja kumuona baba yako.
Hatujaonana muda mrefu, nina hamu naye.” “Yaani hamu hiyo ya baba inatokea siku
ya kupokea mahari ya Nanaa!?” James akauliza.
“Hamu ni hisia.
Umenisikia James? Huwezi kunipangia lini niwe na hamu na baba yako na lini
nisiwe na hamu naye. Unataka nijenge kwa watu wakati kwangu kunabomoka? Shika
adabu yako. Nikikwambia Nanaa amekuloga, huamini. Ona..” James akakata simu, na kubaki
amesimama ndani ya kile chumba, asijue kuwa wageni wote walikuwa
wakisikiliza.
Watu
wachakula walishakuja, walikuwa
wakisaidiana na Grace kupanga vyakula mle ndani. Grace aliposikia yale
mazungumzo, akabaki ameduwaa. Akamwangalia Danny aliyekuwa amekaa na Fili huku
akisukuma mapacha wao kwenye kigari chao. Wakajikuta wanaangaliana. Wote
wakamgeukia mama yao. James akatoka hajui awaambie nini wenyeji wake, lakini
Mama G akamuwahi. “Jiandae, kesho asubuhi tunakuja kukuchukua, tunaenda
kumfuata mama yako huko Moshi. Unanisikia James?” “Ndiyo mama.” “Saa kumi na
nusu asubuhi, tunaanza safari. Tunakwenda Moshi.” Mama G akasimama.
“Samahanini
sana jamani.” James alikuwa ameishiwa nguvu kabisa. “Watakao weza kula mle,
Grace utatuletea chakula nyumbani. Twende tukajiandae na safari ya kesho, Geb.”
Mama G alikuwa amekasirika sana, akataka kutoka, lakini Malii akamuwahi. “Mama!
Mimi na mke wangu tutawasindikiza. Tutakuja kumpitia James hapa nyumbani kwake
asubuhi sana kama ulivyosema. Halafu tukutane Kibaha.” Kidogo mama G, akatulia.
“Asante
Malii mwanangu. Nakushukuru.” “Na sisi tutawasindikiza. Tutageuza kesho kutwa
jumatatu.” Wengi wao wakaonyesha utayari wa kuungana nao. Wakakubaliana kama
kawaida yao, wakutane Kibaha ndipo waongozane mpaka Moshi. Mama G akatoka. Geb
akafuata nyuma bila yakuweka neno hata moja.
Alipofungua
mlango wa gari tu, Nanaa akamuwahi. “Tayari mama?” Nanaa akauliza na tabasamu
usoni, mara akashangaa Geb anaingia kwenye gari akiwa amekasirika. Nanaa
alianza kuhisi mambo hayakwenda sawa. James naye akatoka, Nanaa akashuka kwenye
gari. “Kuna nini tena, kaka!?” “Mama ameondoka.” Nanaa akatulia kidogo.
“Sijaelewa. Ameondoka kivipi?” “Yaani hayupo hapa. Waliondoka tokea asubuhi
kurudi Moshi. Asubuhi nimeagana nao vizuri, na kuwakumbusha leo ndio siku ya
kulipiwa wewe mahari. Tena nikawasisitiza angalau wanisaidie usafi. Lakini
nimerudi kutoka kazini, sijamkuta mtu hata mmoja na nyumba chafu kuliko
utakavyodhania.” Nanaa aliumia sana.
Akaanza
kulia na kushindwa kujizuia. Akazunguka nyuma ya gari akiendelea kulia. Alilia
mpaka Geb akashuka kwenye gari. Mama G akamfuta na Grace naye akatoka, akasikia
kilio cha Nanaa kule nyuma ya gari, akamfuata. James naye akamfuata. Wakajikuta
wote wamesimama nyuma ya gari hiyo na Nanaa akiendelea kulia kwa uchungu sana.
“Ngoja nikwambie Nanaa, kesho asubuhi tunakwenda Moshi kuwafuata. Na kesho
tutalipa hiyo mahari yote waliyotaka. Wawepo, wasiwepo, tutaiacha hiyo mahari
nyumbani kwao. Na James, waambie wazazi wako, Nanaa ataolewa tu. Wawepo,
wasiwepo, harusi itafungwa. Waache kutuchezea akili. Twende Nanaa ukajiandae na
safari, kesho saa 10:30 alfajiri, tupo barabarani.” Mama G akaongeza.
“Pole sana Nanaa. Usilie. Sisi tupo na wewe,
naamini kila kitu kitaenda sawa. Acha kulia kabisa. Tulia. Turudini nyumbani. Tule,
tupumzike mapema kwa ajili ya safari kesho. Mungu yupo upande wetu. Hakika
tutafanikiwa tu. Usilie.” Grace naye akamtuliza.
Safari ya Moshi tena.
Safari hii ni Nanaa&Geb.
Kama
alivyosema Mama G, ilipotimia saa 12 asubuhi, tayari walikuwa wameshaliacha
jiji la Dar, wakielekea Moshi nyumbani kwao kina James. Yalikuwa magari 13 ya
ndugu, jamaa na marafiki walioungana na Geb kwenda Moshi kulipa mahari. Geb
aliendesha gari lake kubwa, lililoweza kubeba familia nzima. Alikuwepo Geb
mwenyewe, Mama yao, Danny, Fili, Grace, Nanaa, Liv, Fillius na Fillan.
Safari
ilikuwa nzuri na wakafika Moshi mapema tu. James aliwasaidia kupata hoteli
nzuri, walitua mizigo yao hapo hotelini, ndipo wakaelekea tena nyumbani kwa
kina James. James akiongoza msafara mpaka nyumbani kwao. Ilikuwa ni saa 6
mchana wakati wakiegesha magari nyumbani kwa kina James. Kama ilivyokuwa Dar,
Mama G alimwambia Nanaa na mtoto wasubiri kwenye gari. James akawakaribisha
ndani, wakawakuta wote wamekaa sebuleni wanaangalia tv.
“Kwa
nini umeleta watu huku nyumbani bila taarifa!?” Mama yake akashituka sana.
Hakuna kati yao aliyetegemea huo ugeni. James aliamua asiwataarifu tena kuhofia kutorokwa. “Naomba utulie mama,
tumalize hili swala. Hawa watu wote wamekuja hapa wakitaka kulipa mahari ya
Nanaa tu. Naomba tuwakaribishe.” “Unanivunjia heshima. Unaleta wageni nyumbani
kwangu bila taarifa!? Halafu unaniingilia ratiba zangu. Sasa hivi nataka kuanza
kupika.” “Tutasubiri.” Akadakia Mama G.
“Hakuna
mwenye haraka hapa. Kilichotuleta ni ile heshima tuliyonayo kwa Nanaa na kwenu,
basi. Kwa hiyo sisi tutasubiri mpaka umalize shuguli zako zote, tukulipe hiyo
mahari.” Mama G akaongeza. “Ni vile hamjamjua huyo Nanaa.” Mama yake James
akaanza. Kwa kuwa walikuwa wengi, na wenyeji hawakuwapisha viti, wengi walibaki
wamesimama wakisikiliza. James alionekana kuumia mpaka uso wake ulionyesha.
“Mimi
namjua Nanaa ndio maana nimesita kupokea mahari yake. Nanaa ni kama mtoto
niliyemzaa mimi mwenyewe. Amenyonya haya maziwa, tokea anazaliwa mpaka leo.
Namfahamu vizuri sana. Sitaki kuja kudaiwa baadaye mkimrudisha. Nanaa ni mchoyo
sana. Ana roho mbaya hawezi kuishi na watu. Mvivu, hatumiki. Kiburi kimemjaa
mpaka kwenye kope! Ana kasoro kubwa sana ambayo hakuna mwanaume aliyekwisha
lala naye akarudia. Kwanza hazai. Alikaa na mwanaume, akamuacha sababu ya
kutoshika mimba. Huyo mwanaume akalala na Viola mara moja tu, mwenzake amezaa.
Nanaa..” “Samahani Mama James.” Mama G akamkatisha.
“Mimi
ni mama yake Grace na Geb ambaye ndiye mwenzie Nanaa. Wananiita Mama G. Mama G
anatabia yakutopenda kuzungushw...” “Kwani....” Mama James alitaka kumkata.
“Nimekuomba samahani ili unisikilize. Tafadhali nyamaza. Hawa vijana wote unao waona
hapa wengi ni wanangu wakuwalea tokea kina Grace wapo watoto. Tunaheshimiana
sana. Na hawa vijana ni watu na majukumu yao ya msingi sana. Nisingeruhusu
wamsindikize mwenzao Geb kuja kulipa mahari ya
Nanaa, kama simfahamu vizuri Nanaa.” Mama G akaendelea.
“Kama
hufahamu, nimeanza kumuombea mke wa Geb, tokea Geb anazaliwa. Nimekuwa
nikimsihi Mungu kwa kufunga na kuomba kwa ajili ya mke wa Geb, tokea sijakutana
na Nanaa. Nataka ufahamu kuwa, ninaishi na Nanaa nyumba moja. Namfahamu vizuri
sana Nanaa. Na mimi kama mama yake Geb ninakwambia wazi, ni Nanaa peke yake
ndiye mwanamke ninayemuona anamfaa Geb, mwanangu. Kasoro za Nanaa zote
unazozifahamu ujue ni kosa langu mimi. Kwamba sikumuombea vizuri. Inawezekana
kuna mahali nilikosea kuomba. Kwa kuwa sio jana au juzi nilipoanza kumuombea
mke wa Geb. Kama nilivyokwambia ni miaka na miaka nilikuwa nikimuombea huyo
Nanaa. Naomba nikuhakikishie kabisa, usiwe na wasiwasi juu ya mapungufu ya
Nanaa. Niachie mimi kwa asilimia zote.” Mama G alikuwa akiongea kwa kujiamini.
Watu wote walikuwa kimya.
Kisha akaendelea. “Unaona hao vijana wote hao waliosimama hapo mbele yenu? Nimekuza wote hao. Wengine walikuwa yatima, na wengine wazazi wao walikuwa wapo mikoani kama James. Wananiita mama si kwa heshima tu. Ni kwa kuwa nimewalea kama wanangu. Kwa miaka zaidi ya 6 waliyokuwa shule ya sekondari mpaka wanamaliza chuo kikuu, nilisimama nao mimi kama mama. Waliokuwa wakilazwa hospitalini nilikuwa nikiwahudumia mimi mwenyewe mpaka wanapona. Waliishi kwangu kama vile huyu Geb alivyokuwa akiishi kwangu mpaka wanamaliza chuo, tena wakiwa vijana. Lakini nilihakikisha wote wanamaliza chuo, na wanakazi bila hata kuwafahamu wazazi wao." Mama G akaendelea.
“Wote
hao wamesimama hapo, kama wanangu wakuwazaa. Mmoja wao akipatwa na tatizo hapo,
ni langu. Kabla hawajapigia simu wazazi wao mkoani, wananipigia mimi simu
kwanza. Akiwepo mwanao James. Aibu ya mmoja wao hao wote ni aibu yangu mimi.
Wala siwezi hata kutangaza ubaya wa mmoja wao hao, kwa mwenzake. Nabeba huo
ubaya mimi mwenyewe nikimsihi Mungu aingilie kati na kuhangaika nao hao mpaka tatizo
linaisha. Kuna waliooa na wana watoto. Ndoa zao zikiwa na matatizo, nahakikisha
zinarudi kuwa na amani, mimi kama mama yao bila hata kuwasiliana na wazazi wao.
Nahangaika nao mchana na usiku hao vijana wote na watoto wao wananijua mimi
kama bibi yao. Vitoto vyao vimezaliwa mikononi mwangu na kulea mpaka vinakatika
vitomvu, mimi nalea.” Mama G akaendelea.
“Na
hao unao waona hapo ni wachache. Wapo wengi tu na wengine hawapo hapo wapo
safarini kikazi. Ni kina baba, na wanawake na nyazifa walizozipata chini ya
uangalizi wangu. Hapa ninachojaribu kukwambia ni kuwa, HAWEZI kunishinda huyo
Nanaa, mtoto wa juzi tu! Sasa nataka utujibu swali moja tu ili tusizidi
kukupotezea muda. Unapokea mahari ya Nanaa, au hupokei, tuondoke? Na ujue
kabisa, Nanaa ataolewa na Geb. Mpende, msipende, Nanaa ataolewa na Geb. Pesa
yote mliyotudai ya kumlea Nanaa humu ndani, tumekuja nayo. Mpaka malipo
uliyotaka tukulipe kwa Nanaa kunyonya ziwa lako pia tumekuletea.
Kwa hiyo naomba utuambie tunatakiwa kufanya nini ili tusizidi kuwapotezea muda
wenu, muendelee kuangalia tv.” Kulizuka ukimywa mkubwa hapo kama hapakuwa na
mtu.
~~~~~~~~~~~~
Baba
yake James alimwangalia mkewe. Wazi alionyesha kushangazwa na alichokisema mama
G, mwishoni. Yule mama alijua wazi mumewe anamwangalia, lakini akakwepesha
macho. James pia alikuwa amesimama. Hakupata sehemu ya kukaa. Nyumba ilikuwa
chafu, kama hapakuwa na mtu aliyekuwa akiishi humo ndani. Wakati wanawake
watatu wapo hapo wamekaa mbele ya luninga, wametulia kana kwamba hawaoni nzi waliokuwa
wakizunguka mle ndani. Nzi walikuwa wamejaa. Na wenyeji walionekana hawana neno
nao kabisa. Harufu ya kinyesi cha ng’ombe iliyokuwepo hapo ndani, utafikiri
wapo kwenye banda la ng’ombe au ng’ombe wanaishi humo ndani.
~~~~~~~~~~~~
Mama
G alipoona wapo kimya, akaamua aendelee. “Haya, Gozibeth na Danny, kaleteni vitu vyote tulivyoleta vya
mahari.” Gozi na Danny wakatoka na vijana wengine wawili. Wakaanza kuingiza
vitu mle ndani. Baada ya muda mfupi sebule ikawa imejaa vitu vizuri na vya
thamani. Vyote mama G alifanya kwa ajili ya Nanaa. “Asanteni sana.” Mama G
akawashukuru wale vijana waliokuwa wakiingiza mizigo ndani. Akamgeukia Geb.
“Haya Geb! Toa hiyo hundi ya pesa yote waliyodai uwalipe kwa kumlea Nanaa humu
ndani na hundi ya pili ya kumalizia mahari ya Nanaa. Ng’ombe mtanunua wenyewe.
Weka hapo kwenye meza.” Geb akatoa bahasha, akaweka mezani.
“Sasa
hiyo yote ndio mahari na malipo yakumlea Nanaa, kama mama James ulivyomtuma
James. Mkiamua kuitunza sawa, mkiamua kutupa pia ni sawa tu. Ila nawahakikishia
hakuna atakayekuja kuwadai hata kitu kimoja wapo hapo au hata shilingi. Fanyeni
kile mtakachotaka kwenye hiyo mahari na hayo malipo ya Nanaa. James atawapa
tarehe ya harusi ya Nanaa na Geb.” Mama G alikuwa akiendesha mambo yeye
mwenyewe.
“Gozi,
nenda kaniitie Nanaa na Oliva.” Gozi akatoka kwa haraka, baada ya muda akarudi
na Nanaa na Oliva. Mama G akamgeukia Nanaa, “Nanaa, unawatambua hawa?” “Ndiyo.
Shikamoo mama mkubwa na baba mkubwa.” Nanaa alijibu na kusalimia, akiwa bado
amesimama huku amembeba mtoto wake. Gozi alipotaka kumbeba Liv, akakataa.
Akazidi kumng’ang’ania mama yake huku akijificha. Akamuona bibi yake akaanza
kucheka akiwa amebebwa na mama yake. Akanyoosha kimkono chake akitaka bibi yake
ambembe yeye. Mama G akasogea akambeba na kumbusu.Liv akacheka.
~~~~~~~~~~~~
Alijazwa
dhahabu huyo mtoto! Masikioni, mkononi, shingoni na kacheni kadogo alivalishwa
cha mguuni. Kazi hiyo ya bibi yake. Nanaa naye alikuwa amependeza sana.
Aliachia nywele alizokuwa amesukwa, akafanana na Liv kiasi, hasa rangi. Nywele
za Olivia walizichana tu. Zilikuwa zimejaa na kujifinyanga kama mtoto wa
kiarabu. Bibi yake aliweka ua pembeni ya kichwa chake. Hakuwahi kumkata nywele
tokea anazaliwa zaidi ya vincha vya juu tu. Na vile alivyokuwa akicheka,
alipendeza sana. Nanaa alivaa gauni zuri sana. Refu mpaka chini. Hakika
alipendeza. Usingeweza kujua kama ni Nanaa yule aliyekuwa akiishi hapo ndani
kama mfanyakazi wao. Akiwatumikia mchana na usiku.
~~~~~~~~~~~~
Hakuna
aliyeitikia salamu ya Nanaa. Ukimya mwingine ukazuka. “Kuna chochote
tumesahau?” Mama G alivunja ukimywa kwa kumuuliza swali James. “Sidhani mama.
Nashukuru sana kwa kuja na kwa heshima mliyoweka kwa Nanaa. Mungu awabariki.”
James alimsogelea Geb akampa mkono. “Geb! Nakushukuru sana.” “Asante James.
Nashukuru kwa kila kitu. Na samahani kwa usumbufu.” “Hata kidogo. Hujui ni kiasi gani nimefurahi.
Nawashukuru sana.” Akamsogelea mama G. “Asante sana mama yangu, kwa kumpokea
Nanaa. Na samahani kwa usumbufu wote uliojitokeza. Mungu azidi kukubariki.”
“Amina James mwanangu. Na mimi nakushukuru kwa kusimama na sisi kuhakikisha
tunampata Nanaa. Asante kwa kutuamini naye.” Wakapeana mikono. Wazazi wake
hawakusema lolote.
“Haya
wanangu, twendeni.” Walio pata nafasi yakukaa wakasimama wote kwa pamoja. “Na
huyu hapa kwa Kiitaliano anaitwa Olivia, Kiswahili Oliva, nyumbani anaitwa Liv.
Ni mtoto wa Nanaa na Geb. Kwa hiyo jamani, mgumba amezaaa!” Mama G
akaongeza tena huku akimbusu Oliva aliyekuwa akicheka. Alipomuona tu baba yake,
akataka ambembe yeye. Geb akamsogelea mwanae. Akambusu akiwa bado amebebwa na
mama yake. Olivia akanyoosha mikono kama anamwita baba yake. Geb akampokea.
“Twende Nanaa.” Nanaa alitoka huku akilia. “Wala usilie mwanangu. Mungu yupo na
wewe, utafanikiwa tu.” Mama G alisikika akimliwaza. Grace hakuwa ameongea neno
hata moja tangia aingie humo ndani. Alikuwa kimya kabisa akiangalia na
kusikiliza kama wengine.
Baada Ya Mahari.
Hakuna
jinsi ungeeleza furaha ya Nanaa na Geb mara baada ya mahari. Waliporudi tu
hotelini, Geb na Nanaa wakakimbilia chumbani kwao bila kuaga mtu, tena kama
walijiiba. Geb alimshika tu mkono, Nanaa akaelewa. Wakaondoka kimya kimya mpaka
chumbani. Wakajitupia kitandani wakiwa na furaha zote. “Asante Geb. Nashukuru
kwa kunilipia garama yote hiyo. Najua sistahili. Asante.” “Nani anastahili
sasa?” Geb akamvuta karibu. “Kwanza kuanzia leo, wewe ni Nanaa Wini Magesa. Na baada ya harusi tu, tunaenda
mahakamani kubadilisha rasmi jina lako. Na wewe utatambulika rasmi kama Magesa,
kama vile mimi na Liv.” Nanaa akacheka.
“Nimefurahi
tumekamilisha. Na ninamshukuru Mungu kukupa uwezo Geb. Kama isingekuwa hivyo,
sijui ingekuwaje?” Nanaa aliwaza kidogo. “Acha kufikiria mawazo ya ingekuwaje.
Hili limekamilika. Tufikirie lijalo.” Wakati wanaanza kupeana mabusu wakasikia
mlango unagongwa. Geb akakunja uso, akasimama kwenda kufungua.
“Nataka
tumshukuru Mungu pamoja. Tusijisahau jamani! Huyu ni Yesu ndio amefanya.”
Alikuwa mama G na Liv. Geb akampokea mtoto wake. “Ni kweli mama.” Wakatoka
mpaka sehemu ya mapokezi. Wakawakuta watu wote wamekusanyika pale. Ndipo akaona
huo ndio wakati muafaka kuwashukuru wenzie. Aliwashukuru kwa kujitoa kwao bila
kuchoka. Kuacha shuguli zao zote na kumsindikiza mpaka hapo Moshi. “Nawashukuru
sana.” Geb akamaliza.
Wakashikana
mikono, mama G, akamshukuru Mungu. Hakuacha kumkumbuka Zinda. Alimuombea amani
na faraja huku akitubu kwa Mungu kwa chochote alichomkosea. Wakamaliza. Danny
naye akashukuru na kuongeza. “Jumamosi ijayo tunaanza kikao cha kwanza cha
harusi. Nitatuma kwenye kundi. Naombeni wote mkaribie nyumbani kwetu. Muda
nitawajulisha.” “Wapi? Kwako Danny au kwa Geb?” Gozi akauliza. “Kokote
alipokuwepo mama G, hapo ndipo nyumbani kwetu wote sisi. Kwa hiyo ni Tabata
Barakuda, hapo ndipo tutakutana.” Si mama G tu aliyefurahia lile jibu, hata
mkewe alionyesha usoni. Grace akamwangalia mumewe, akanong’ona. “Asante.” Danny
akacheka. Akapa busu la mdomoni.
Ilipofika
kama mida ya saa moja kasoro usiku wakiwa wanaongea na kucheka, James
aliwafuata pale hotelini. “Jamani, nimeshindwa kuvumilia. Naomba tutoke wote
tukasherehekee kulipiwa mahari kwa dada yangu. Twendeni sehemu tukale na
kunywa. Nimepaandaa kwa haraka haraka, hapatafanana na hadhi yenu. Lakini
sitaki mtoke hapa kwetu bila kula. Hii siku niliisubiria kwa hamu sana.” Mama G
akaanza kupiga vigelegele.
“Mama
wewe! Unasumbua wageni wengine! Ona watu wote wamekugeukia wewe!” Mama G
hakuacha. Watu wote walikuwa wakicheka. Wakamalizia vinywaji walivyokuwa
wakinywa pale pale hotelini sehemu ya nje, wakamfuata James nyuma. Alifika hapo
hotelini na taksii, lakini akaondoka na gari la Malii. Walikuwa wamemuacha
James nyumbani kwao tokea mchana walipoenda kulipa mahari.
James
alitafuta mgahawa mzuri tu. Akawaomba wapike chakula kidogo na kizuri kwaajili
ya wageni wake. Alitoa oda ya nyama choma. Alinunua mbuzi mzima kwa ajili ya
shuguli hiyo. Akawaambia wamtengeneze kwa haraka, pamoja na ndizi za kuchoma na kukaanga. Akataka
waongeze na kuku na mishikaki kidogo ya nyama ya ng’ombe. Wakaingia humo ndani,
wakaanza kusherehekea. Hakuna ambaye hakuwa na furaha siku hiyo. Walicheza kila
mziki uliokuwa ukiwekwa ndani ya huo mgahawa aliowaandalia James. Utani
ukaendelea, vigelegele vya mama G, havikukoma. Basi ikawa ni shangwe na
kumshukuru Mungu.
~~~~~~~~~~~~
Walirudi
Dar, salama. Walipoingia tu ndani, Geb
akaomba ushauri. “Nimefikiria, naona nimtafute Zinda na Liz nizungumze nao.
Zinda tumetoka naye mbali sana. Nisingependa akose kitu muhimu kama hiki. Na
yupo sahihi, alikuwa kwenye maisha ya Danny wakati mimi nilipokuwa nchini
India. Sitaki wakosane sasa hivi kwa ajili ya mapenzi yangu kwa Nanaa.”
“Utamwambia nini Zinda!?” Grace akamuuliza.
“Sijui
G. Labda nitaanza kwa kumuomba msamaha, na kujibu chochote atakachotaka kujua.
Lakini naona maisha yetu hayapo sawa bila Zinda. Najihisi tumepoteza ndugu wa
damu.” “Lakini ujiandae Geb. Zinda anahasira sana na wewe.” Danny
alimtahadharisha. “Mimi naungana mkono na Geb. Amtumie ujumbe kabla ya
jumamosi, amuombe wakutane. Ikitokea anakubali wakutane, basi ujue
atakusikiliza. Asipotokea, ujue bado ana hasira. Muache kwanza.” “Sawa mama.”
Wakaagana baada ya kuomba kwa pamoja, kila mtu akaelekea chumbani kwake.
Geb
alimuona Nanaa amenyamaza. Akaongeza ubusy usio wa kawaida. Aliondoka pale
chumbani akaenda chumbani kwa mama G akaanza shuguli kwa mwanae ambazo alikuwa
akifanya mama G wakati wote! Aliingia hapo chumbani na kutoka. Akifanya hili na
lile bila kumaliza. Mama G alibaki akimtizama. Akajua tu lipo jambo. Geb
akashuka kumfuata.
“Leo
Liv analala chumbani kwake kule juu?” Geb akauliza. “Sijui mama.” Akajibu
kinyonge, akatoka. Oliva alishakuwa tayari kwenye kitanda chake. Alivalishwa
nguo zake za kulalia akawa anazunguka tu hapo kitandani kwake chumbani kwa bibi
yake. Aliposikia tu sauti ya baba yake, akasimama. “Ana usingizi huyo.
Ungechelewa kuingia tu hapa, angelala. Naombeni mumuage, mtoke humu ndani
kwangu. Naona shuguli haziishi na mimi nimechoka.” Mama G akajinyoosha
kitandani kwake. “Na huyo Oliva analala hapo hapo. Haendi kokote kule.” Mama G
akaongeza. Kimya.
Nanaa
akahamia kwenye kazi nyingine. Akaanza kukunja nguo za mwanae kabatini bila
kujibu kitu wala kumwangalia mtu. “Basi leo hatutalala!” Mama G akamrushia hilo
neno. “Namalizia tu mama.” “Sasa kwa nini utoe nguo zilizokwisha pangwa huko
kabatini sasa hivi wote tumechoka, halafu uanze kuzipanga upya? Si utoke tu
ukazungumze na huyo Geb yaishe?” Nanaa akaendelea kupanga zile nguo bila
kujibu, Geb akabaki akimwangalia. Na kweli nguo zote zilikuwa zimepangwa vizuri
tu, wala hazikuhitaji kuguswa.
“Wewe
Nanaa?” “Namalizia tu mama.” “Huna unachofanya hapo. Mimi nakujua bwana. Wewe
nenda kazungumze na mwenzio, mtuache mimi na wajina wangu tulale. Maana naona
mnakaribia kumtoa humu ndani. Haya Geb, naomba niwekee mtoto hapo kitandani.
Ongoza njia, Nanaa atafuata.” Geb akambusu mwanae mara kadhaa akamuweka
kitandani akiwa ameshalevya na usingizi vyakutosha.
“Twende
Nanaa.” “Bwana eeh! Nimekwambia utangulie, atakufuata. Mbona hivyo!?” Geb
akamwangalia Nanaa, akamuona amejificha nyuma ya mlango wa kabatini kama
aliyetingwa na shuguli nyingi huko ndani kabatini. “Nenda wee!” Mama yake akamfukuza Geb. “Sawa mama, usiku
mwema.” Geb akatoka. “Haya na wewe njoo hapa.” Nanaa akatoka pale kabatini
akaenda kukaa kitandani kwa mama G. “Sitaki Geb aonane na Liz.” Nanaa akaanza
kuongea tu mara baada ya kukaa. “Mpaka lini?” Mama G akamuuliza taratibu.
“Sijui mama. Lakini mimi simtaki kwenye maisha ya Geb.” Mama G akatulia kidogo.
“Anamtaka
mpenzi wangu mpaka leo! Wakikutana wawili tu halafu akamfanyia vituko? Mimi
simwamini akiwa naye peke yao. Hata kama asipomsamehe Geb, basi. Lakini mimi
simtaki na sitaki Geb awe karibu naye tena.” “Nitamwambia Grace yeye ndio
amtafute azungumze naye kwanza. Kama ataelekea, ndipo Geb naye aungane nao.
Nafikiri wazo lako sio baya. Awepo Grace kwenye mazungumzo yao ili kuwekana
sawa.” Nanaa akacheka.
“Una
wivu wewe!” “Wewe umemsikia Danny anavyosema shetani ni kama simba angurumae.
Akimrarua Geb wangu?” Mama G akacheka sana. “Kazi ipo.” “Wala si ndogo. Hivi
unajua na jina nishabadilishwa? Nasubiri baada ya harusi tu, nikaape
mahakamani.” Nanaa alianza kujisifia. “Ndio utakuwa ukiitwa nani tena mwenzangu?”
Mama G akauliza huku akicheka. “Nanaa Wini Magesa!” “Mwenyewe huyoo!” “Kwa raha zangu!” Nanaa
akaendelea kujisifu. “Halafu wanipokonye tonge mdomoni? Akuu! Waniache mie
Nanaa mtoto wa Wini!” Mama G aliendelea kucheka.
“Hakuna
baya ningefanya Nanaa! Kwanza ningehakikisha nakutana naye sehemu ya wazi.” Geb
aliingia wote wakashangaa. Kumbe alikuwa nje ya mlango akiwasikiliza. “Kwanza
wewe unaongeaje mambo yako na watu wengine kabla hujazungumza na mwenzio!?”
Mama G akamjia juu Geb. Akamgeuka hapo hapo na kicheko kikamwisha usoni.
“Nilijua ni wazo zuri.” Geb alijitetea kwa mama yake.
“Yaani
wazo zuri la kwenda kumtafuta mpenzi wako wa zamani. Aliyekuwa hanipendi na
ananidharau mbele za watu. Unaenda kumbembeleza akubali wewe unioe mimi!”
Kimya. Lile swali likaingia kwa Geb na mama yake. Wakabaki wakitafakari. “Kwanza
unaenda kumbelezaje!?” “Sio kumbembeleza Nanaa!” “Mimi naona nibakie mimi
mwenyewe tu. Wewe nibembeleze mimi tu basi.” Mama G akaanza kucheka.
“Usicheke
mama bwana! Sasa yeye anataka kumfurahisha Liz wa nini, kwa mfano?” “Sio
kumfurahisha Nanaa! Nikutafuta kuwa na amani.” Nanaa akanyamaza. “Mimi naona
tuanze kutafuta amani ya humu ndani kwanza.” Mama G akaongeza. “Sio kwanza
mama. Tutafute amani ya humu ndani tu.” Mama G akacheka tena. “Na amani ya
nje?” Nanaa akapandisha mabega kukataa. Mama G akazidi kucheka. “Hakuna
kutafuta amani na Liz. Mwache kabisa.” “Sawa Nanaa.” Nanaa akaanza kucheka.
“Umefurahi sasa?” Mama G akamuuliza. “Mimi nataka kubakia peke yangu kwa Geb,
mama.” “Upo peke yako na utabakia peke yako daima, Nanaa.” “Hapo nimefurahi.
Sasa hivi twende.” Mama G alicheka mpaka machozi. “Kazi ipo!” “Hamna bwana mama!”
“Naombeni muondoke mniache nilale.” Geb na Nanaa wakatoka huku wakicheka.
Bado Kulia Wivu.
Walipoingia
tu chumbani, Geb akamtumia ujumbe Zinda kumuomba wakutane kesho yake. ‘Kama ni pesa yako nitakuwekea benki. Acha kunisumbua.’ Hayo ndiyo majibu ya Zinda. ‘Sio maswala ya pesa Zinda! Nilitaka tuzungumze.’ Geb akajibu. ‘Unisimulie
vile unavyomfaidi mwanamke wangu? Na Mungu anawaona. Atawalipisha siku si
nyingi. Adhabu yenu inawajia.’ Geb akaona
asiendele. Amwache. Zinda akatuma ujumbe mwingine. ‘Wewe si umeamua pesa yako ndio iongee hapa mjini? Na huyo Nanaa si
anataka wanaume wenye pesa tu? Basi tutawaona mtakapofikia.’ Geb hakutaka kujibu tena. Akam block Zinda kila mahali. Akahakikisha anafungia
mawasiliano yote ya Zinda yasiingie kwenye simu yake tena. Kisha akazima simu
yake kabisa, wakalala.
~~~~~~~~~~~~
Asubuhi
kabla Geb hajatoka kwenda kazini, akamueleza mama yake majibu ya Zinda. “Basi
mwache kabisa. Usimtafute tena.” “Nimemblock kila mahali. Nimeona anazidi
kutuma jumbe za matusi na vitisho.” “Umefanya vizuri. Mpe muda. Labda atakuja
kutulia tu.” Geb akatoka. Danny na Grace walisikia kila kitu. “Yaani Zinda
ameamua kukataa ukweli kabisa jamani!?” Grace akalalamika. “Na sijui kwa nini
anafanya hivyo, wakati anajua ukweli wote! Lakini kama alivyosema mama,
tumuache tu.” Danny naye akaongeza na kutoka akielekea kazini.
~~~~~~~~~~~~
Juma
hilo zima ilikuwa ni maandalizi ya kikao cha kwanza cha harusi ya Nanaa na Geb.
Walihakikisha wanaalika watu wote wakaribu kwa kuwapigia simu. Wakapata idadi
ya watakao hudhuria. Ndipo wakatafuta mtu wa kuwapikia chakula. Catering. Danny
na Malii wakabakiwa na jukumu la vinywaji. Mama G naye alishamtafutia Nanaa
nguo ya kuvaa usiku huo. Akabadilisha mtindo wa nywele. Akawa amependeza yupo
tayari kwa siku hiyo maalumu waliyokuwa wakiisubiria kwa hamu kubwa.
Siku Ya Kikao Cha Kwanza Ya Harusi Ya Geb & Nanaa.
Siku
hiyo ilifika, kila mtu alikuwa na majukumu yake ya kukamilisha kuhakikisha
kikao kinapoanza, mambo yanakwenda sawa. Wageni wao wakae sehemu nzuri, wale na
kunywa kwa kusaza. Hata Geb hakwenda kazini siku hiyo. Alikuwa nyumbani siku
nzima akiandaa sehemu ya kukutania watu. Walikodi viti na meza. Mpaka inafika
saa kumi jioni, kila kitu kikawa kimekamilika.
Kwa
mara ya kwanza mama G alimbana mjukuu wake nywele mafungu matatu. Oliva akawa
amependeza sana. Kama kawaida yake, akamjaza dhahabu kila mahali. Ungependa
kumwangalia. Alihakikisha hata Nanaa anapendeza. Muda wote wa hekaheka za
maandalizi, alimwambia Nanaa apumzike ndani. Asifanye chochote. Kwa hiyo
ilifika jioni Nanaa akiwa na uso uliotulia, kwa kulala siku nzima.
James
alikuwa wa kwanza kufika. Nanaa akafurahi. “Nimefurahi umekuja kaka.” “Siwezi
kukosa hata kidogo.” Waliendelea kutaniana Danny na James huku Geb akiwa
anacheza na mtoto wake. “Anazidi kuwa mkubwa! Namuomba nimshike.” “Ana maringo
huyo mtoto wa Geb! Sijui kama atakubali.” Grace akadakia. “Akimuona baba yake
na bibi yake, hata kwa mbali vipi, mikono yote juu na kuanza kucheka. Lakini
akija mgeni hapa, ananyamaza kimya. Ukimwita, ananyamaza kama sio yeye. Tena
hata hakuangalii.” Wakacheka.
“Mjaribishe
kaka.” James akasimama. Ile kumsogelea tu, akajificha kwenye shingo ya baba
yake, akanyamaza kimya. “Si nilikwambia? Tena anaweza kulala hapo hapo kwenye
shingo ya baba yake.” Wakacheka. “Na hapo kwenye shingo ya baba yake hatoki
mpaka bibi yake amtoe hapo.” Grace aliongeza. “Liv! Liv!” Geb akamwita, akamchungulia.
“Nenda kwa anko.” Geb akawa kama anamvutia kwa James, akamuona ametengeneza
kimdomo chake kama anataka kulia. “Basi mama. Basi.” Liv akarudi shingoni kwa
baba yake. Geb akaanza kumpiga piga mgongoni.
“Daah!
Watoto hawakawii jamani! Ukiambiwa na yeye ameshakuwa mkubwa kiasi cha kukataa
watu!” “Na sisi anatushangaza huyu mtoto! Naona akili yake ndio imekomaa
mapema. Ameanza kujua watu mapema sana. Watu wote wa humu ndani anawafahamu.
Utamuacha hapo kitandani na Fili, utamsikia akicheka kwa sauti tu. Lakini
akiingia mtu asiyemfahamu, anabadilika kama sio yeye!” Mama G akaongeza. “Tena
atakuchekea kama bibi yake au baba yake hawapo karibu na macho yake. Wakitokea
tu, undugu wake na wewe ujue umeisha.” Waliendelea kuongea mpaka wageni
walipoanza kuwa wengi ndipo wakatoka nje.
~~~~~~~~~~~~
Kikao
kikaanza, Geb akiwa amekaa na Nanaa na mtoto wao. Fili akaja kumkalia Nanaa.
Nanaa alimuweka vizuri, kikao kikaendelea. Danny ndiye aliyekuwa akiongoza
kikao. Wakagawana majukumu. Wakaainisha kamati zote. Kama kawaida yao, kwa muda
mfupi sana wakawa wamemaliza kikao kirefu. Walishajuana nani awepo wapi na
atafanya nini, tena bila kusukumana. Kila kiongozi wa kamati akatoa makadirio
ya pesa ya kamati yake. Danny akawa akiandika. Alichoona Geb hatapenda kama
ukumbi na aina ya vyakula, alirekebisha na kushauriana na wenzake. Mwishowe
wakapata makadirio ya juu. Likabakia swala la pesa.
Kama
ilivyo kawaida ya kuulizwa bwana harusi kiasi alichojiandaa nacho cha kuoa.
Akiwa anamjua vizuri Geb, Danny akamtaka Geb azungumze chochote juu ya hiyo
bajeti. “Naombeni niwashukuru sana kwa utayari wa kujitolea. Kikubwa mimi na
Nanaa tunachohitaji ni uwepo wenu tu. Najua mnamajukumu mengi na hali ya pesa
imekuwa ngumu sana. Lakini mimi, Nanaa, Danny, Grace na Mama, tulishajiandaa.
Tulikusanya pesa yakutosha tu anayo Danny. Tunaomba tugaramie kila kitu.
Viongozi wa hizo kamati watakuwa wakiwasiliana na Danny. Danny ndio atakuwa na
pesa yote. Atasaidiana na viongozi wa kamati zote ili kukamilisha hilo.” Geb akamaliza,
lakini pakazuka ukimya mkubwa sana.
Danny
akaona aongeze. “Labda kama hamjamuelewa Geb, ni hivi, majukumu yetu
yamerahisishwa jamani. Sasa hivi tunaingia kazini tu, ili ndani ya mwezi mmoja
tukamilishe maandalizi, hawa watu waoane. Kesho ndio tangazo la kwanza la ndoa
yao. Kwa hiyo, hakuna kuchangishana.” “Hapo ndipo lilipo tatizo Danny. Na sisi
tunawasaidia vipi kwenye matatizo yenu? Ni kama mnatufungia milango ili tukiwa
na shida tushindwe kuwafuata! Hebu mtuambie tu,
kwa hiki mnachofanya nyinyi leo, inamaana kesho Gozi akitaka kuoa
mnamwambia akusanye pesa kwa ndugu zake ndipo atuite?” Malii aliona aongee.
“Huo
haujawahi, wala haujawa utaratibu wetu. Mnataka kuingiza utaratibu mpya na
mgumu sana. Nyinyi mlikaa wanne tu mkachangishana, inamaana mnatuambia
mmetutenga sisi? Wakati wote Danny umehubiri tena kwa kurudia rudia kuwa sisi
ni ndugu. Mbona kama mnatutenga sasa!? Ni kama mnaanzisha matabaka. Au ni
kwamba mnatuona hatuna uwezo?” Gozi naye akalalamika ila yeye akaiweka vibaya
zaidi.
“Naombeni
tusiende mbali. Nia ilikuwa nzuri tu. Kama tumekosea, basi tusameheane. Naomba
tuanze upya. Au unasemaje Geb?” Danny aliingilia. “Kabisa.” Geb akajibu kwa
ufupi tu, akawa amemaliza kama kawaida yake. Lakini wenzake walishamzoea hakuna
aliyetegemea jibu la tofauti. Ndipo wakaanza kufunguka. “Naombeni na mimi
niongee. Sisi tunaomba tuchangie kidogo tulicho nacho, kisha na nyinyi
muongeze. Lakini itakuwa dharau kuacha pesa yetu.” Kila mmoja akaongea lake.
Mwishowe Danny akachukua kalamu na karatasi akamkabidhi Malii. “Basi anza
kuandika pledges au ahadi ya kila mmoja wetu.” Watu wote wakatoa
ahadi zao. Vicheko vikaanza na kutaniana.
Wakati Inaonekana ipo Amani&Utulivu, Ndipo Na Muovu Naye Anapopanga Uharibifu.
Geb
akamuona Nanaa anajishika miguuni mara kwa mara. “Vipi?” “Nahisi miguu inakufa
ganzi, halafu kama inatoa jasho.” “Mshushe Fili. Inawezekana amekulemea.”
“Mmmh! Fili mbona nampakata kila siku? Sidhani.” Geb akamwangalia. “Kweli Geb.”
“Kwa nini usimshushe tu?” Walikuwa wakinong’ona. Alipomuona Nanaa anasita,
akampeleka Oliva kwa mama yake, akarudi kumchukua Fili. Geb ndio akampakata. Nanaa
akacheka. “Wala hamna tofauti!” Geb akamtizama, akaendelea kusikiliza maongezi.
Muda
wa kwenda kula ukafika. “Twende ukachukue chakula. Au nikuletee?” Geb
alimgeukia Nanaa akamuona amebadilika usoni. “Nanaa?” “Miguu imekufa ganzi
kabisa Geb! Siisikii. Hata nikiifinya, sisikii kitu!” Geb akakunja uso kama
haamini. Akampapasa. “Mbona ina maji!? Fili alikukojolea?” Geb akaanza
kumpapasa Fili. “Hapana. Yenyewe ndio nahisi inatoa maji! Gauni lipo kavu
kabisa. Kama Fili angekuwa amekojoa, ningeloa kuanzia hapa juu kwenye gauni!”
“Hebu
simama.” “Siwezi, Geb.” Geb akamtizama kama haelewi. Akamuweka Fili chini,
akasimama mbele ya Nanaa. “Nipe mikono yako.” Nanaa akanyoosha mikono yote
miwili, Geb akamvuta kumnyanyua. Akafanikiwa kusimama. Alipomuachia tu, Nanaa
akaanguka chini kama gunia. Na kwa kuwa alianguka kwa nguvu, kiti kilisogea, akajikuta
yupo aridhini, juu ya ukoka. Geb akashituka sana. Kila mtu akawageukia wao.
“Pole. Umeumia?” “Nimeangukia matako.” Nanaa akajibu huku akijaribu kusimama
akashindwa.
James
akasogea kwa haraka. “Kuna nini?” “Sijui kaka! Lakini miguu imekufa ganzi kabisa
na inatoa maji!” James akainama kuangalia. “Halafu inajaa!” James akashangaa,
watu wote wakamzunguka Nanaa pale chini. Geb akamnyanyua na kumuweka kwenye
kiti. “Inauma?” Geb akauliza. “Nakwambia siisikii kabisa Geb. Naogopa!”
“Usiogope. Twende ndani ukapumzike kwanza.” Geb akambeba. Wakati wanatoka pale,
wakakutana na mama G na yeye anatoka ndani kumbadilisha diaper Oliva.
“Kuna
nini? Mbona mmebebana na Nanaa analia?” Mama G akauliza. “Sijui mama.” Geb
alijibu huku amembeba Nanaa, anamwingiza ndani. Tayari hali ya pale ikawa
imebadilika. Wasiwasi ukawa umetanda. James alikuwa nyuma yao, akawafuata mpaka
chumbani kwa mama G, ndio chumba kilichokuwa karibu. Akamuweka kitandani.
“Naogopa kaka.” Nanaa aliendelea kulia. “Tulia
Nanaa. Labda pumzika kwa kuinyoosha.” James akajibu, Mama G akaingia. “Ni nini!?”
Akauliza. “Sijui mama. Miguu
inatoa maji, halafu imekufa ganzi kabisa. Hata nikiifinya siisikii.” Mama G akasogea karibu. “Geb! Nitolee taulo kubwa
na safi hapo kwenye kabati langu la kushoto.” Mama G akabonyeza mguu mmoja wa
Nanaa. Akashangaa ametengeneza shimo pale alipoweka kidole. “Mmmh!” Akaguna. “Naogopa mama!” Mama G akabaki kimya akiangalia ile miguu. Tayari
muonekano wa kuvimba ukawa bayana.
“Umekula
kitu chochote cha tofauti?” “Hapana
mama! Nimekula ugali niliopika mimi mwenyewe mchana. Ndio na nyinyi wote
mmekula huo huo.” Mama G akabaki akiangalia ile
miguu ya Nanaa. “Ni nini mama?” Geb akauliza kana kwamba mama yake anajibu.
“Mama?” “Na mimi sijui!” “Sasa unakosaje kujua mama jamani!?” Geb alishaonekena
kupaniki. Alianza kulaumu. “Naomba utulie Geb.” “Naogopa mama.” “Nafahamu.
Lakini naomba utulie kabisa. Lasivyo utamuogopesha na Nanaa mwenyewe.” “Naogopa sana mama. Nitafanyaje? Unafiri
nitakufa kabla sijaolewa? Au unafikiri nitakuwa kiwete? Watanikata miguu yangu?
Eti mama!” “Hapana Nanaa mwanangu.” Mama G
naye ni kama akawa amepigwa na kibumbuwazi. Akawa amekamatwa na hofu.
Grace
akaingia akamwangalia mama yake, akamuona ameduaa. Akajua ameshaingiwa hofu.
“Watoto wote nimemuachia Danny huko chumbani. Naomba James ukawatulize wageni
wote. Waambie Nanaa atakuwa sawa, ila sasa hivi anahitaji kupumzika. Wakimaliza
kula, ukamwite Danny chumbani amalizie kikao, wafunge tu na awaruhusu waondoke.
Awaambie tutawajulisha kinachoendelea ila maandalizi yaendelee kama kawaida
tu.” James akatoka bila kujibu.
“Kwenye
hali kama hizi, mama huwa unaomba. Kwa nini na wewe unaingiwa hofu kama Geb na
Nanaa? Naombeni mtulie tuombe.” Mara Fili akaingia. “Siwezi kupakua chakula
mama. Nataka sambusa tu. Naomba twende ukanipakulie.” “Nisubiri kwanz...” Kabla
hajamaliza, Danny akatoka chumbani kwao na watoto wote amewashika wanalia. Geb
akampokea Liv, Grace akamchukua Fillan, Danny akabakiwa na Fillius. Liv
akanyamaza baada ya kubebwa na baba yake. Lakini sio mapacha wa Grace.
Waliendelea kulia kama kengele.
“Njaa
hiyo!” Mama G akakaa pembeni ya Nanaa. “Narudi sasa hivi. Ngoja nikawanyonyeshe
kwanza. Danny kapashe maziwa moto. Fillius atanyonya ya chupa. Lasivyo
hapatakalika hapa.” Danny akatoka na Fillius, pacha mkubwa, ndiye aliyekuwa
akilia sana. Wakaelekea jikoni kufuata maziwa. Grace alikuwa akikamua na kuweka
maziwa yake kwenye friji kama Nanaa tu. Ikitokea wote wanaanza kulia kwa
pamoja, basi mmoja atakunywa kwa chupa na mwingine kunyonya. Grace na yeye
akaelekea chumbani kwao kunyonyesha mtoto mwingine. Fili akabaki amesimama.
Wazazi wote wamemuacha pale.
Geb
akamkabidhi Liv kwa bibi yake, akamshika mkono Fili na kutoka naye nje. Akaenda
kumtafutia chakula. Kukawa na pilika pilika hizi na zile, hakuna aliyeweza kuomba
tena. Geb akarudi na chakula. Nanaa akala, akampandisha chumbani kwenda kulala.
Shetani Hana Usingizi.
Asubuhi
ya siku inayofuata, jumapili, ndio siku waliyokuwa wakiisubiria kwa hamu kwenda
kanisani kwa ajili ya tangazo la kwanza la harusi ya Geb & Nanaa,
waliamshwa na mayowe ya Nanaa. Alikuwa akilia sana. “Mama nisaidie jamani! Mama yangu
nisaidie mimi!” Geb aliruka kitandani akabaki
anatetemeka. Miguu ya Nanaa ilijaa. Ilivimba kupita kiasi. Iliumuka na
kutengeneza malengelenge yaliyojaa maji kama usaha! Kuanzia magotini mpaka
chini kasoro kwenye nyayo tu. Huwezi kujua ni kama aliungua au ni ngozi ya kenge
imefunikwa juu ya miguu yake, lakini ikaongezeka majipu ya usaha. Nanaa alikuwa
akilia hawezi kujiangalia tena. Macho amefunika na kiganja cha mkono wa kulia,
mkono wa kushoto aliutumia kupiga kitanda mfululizo.
“Mama yangu mimi! Jamani nisaidieni!” Ndio sautu ya Nanaa iliyokuwa ikisikika kwenye
jumba hilo.
~~~~~~~~~~~~
- Nini kimempata tena Nanaa?
- Vipingamizi kila mahali! Ndio
wametoka kuvuka changamoto iliyorushwa kwao ya kulipa mahari. Pesa haikuwa
tatizo. Hilo Geb alilikabili bila shida.
- Marafiki nao wamerusha changamoto zao. Lawama, matusi kuitwa wasaliti
na mengine mengi. Hilo nalo halikushinda HEKIMA za mama G. Akawatuliza wote ili
tu, kufikia siku waliyokuwa wakiitamani kwa hamu. Kumsimamisha Nanaa kanisani na
shela ndefu.
Mama G ajipatie mkwe aliyekuwa akimuomba na kujigamba ndiye mwanamke
anayemfaa mwanae. Kwa Geb, ajipatie mwanamke pekee aliyeona atamfaa kumzalia
watoto. Kuendeleza ukoo wa Magesa. Tena akiwa ameanza vizuri sana. Kumzalia
Oliva. Mtoto wa kike aliyekuwa akimsubiria tokea kijana mdogo.
Wakati wote alikuwa akiwaambia rafiki zake, mtoto wake wa kwanza lazima
awe wa kike. Sasa Nanaa ameshusha toto la kike. Binti Magesa. Oliva! Jina la
mama G! Nani kama Nanaa! Katika wooote, amekusudia kuwa na Nanaa. Amefunga
macho na masikio. Ni Nanaa.
Grace na Danny ndio wanafanya kila wawezalo kuhakikisha wanakamilisha
hilo.
Leo Nanaa ameamka na miguu ya ajabu. Geb mwenyewe amemkimbia kitandani.
Nini kitaendelea? Safari hii ni Nani atakayesimama na
Nanaa katika hili nalo? Ataweza kusimama mpaka mwisho? Na nani? Kufunga na
kufungua historia imembadilikia.
Huwezi kuita ni ulemavu hata kidogo. Ni gonjwa lisiloweza kutamkika wala hakuna mtu
angetamani kuwa naye karibu, kwa kutisha.
Ni rahisi sana kuambiana mnapendana kukiwa shwari. Je mambo
yanapokwenda MRAMA?
Usikose kufuatilia ili kujua kitakacho
Endelea.…
0 Comments:
Post a Comment