Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu Ya 36. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu Ya 36.

James aliingia bila kubisha hodi , akawakuta wenyeji wake wamekaa kama wanamsubiria. “Shikamoo mama.” James akasalimia na kukaa, bila kusubiria ajibiwe salamu yake, akaanza. “Hili swali nilimuuliza Grace, na wewe nakuuliza Geb, unakumbuka jambo lolote nililowahi kukusimulia juu ya Nanaa?” “Nakumbuka.” Geb akajibu kwa utulivu tu. “Sidhani kama mnakumbuka jamani!” Nanaa akaingia na kubaki amesimama nyuma ya kochi alilokaa kaka yake huku akionyesha hofu kubwa. 

“Wewe Geb tokea tunakutana sekondari, kidato cha kwanza, mpaka mwaka jana hamjamchukua Nanaa kuishi naye hapa, nilikuwa nikikwambia habari za Nanaa. Kwa wazi bila kukuficha. Ni kwamba mnasahau au mmeamua kupuuza?” “Nakumbuka kila kitu James.” “Kwa hiyo ni  umeamua kupuuza tu? Maana usingefanya unayoyafanya. Mnajua kuwa Nanaa ni kama yatima. Hana pakwenda, na alipolelewa nako wanamsubiria akosee mahali ili wanibeze au wamcheke. Leo umezaa na mdogo wangu, unamvalisha pete uchochoroni na kumficha hapa kwa kuwa unajua hana pakwenda!? Katika kuishi kote hapa duniani ndivyo unavyoona watu wanafanya? Yaani unazaa na binti ya watu, unamvalisha pete, halafu unamficha, ndio inakuwa basi? Unaishi naye kama mkeo kwa ruksa ya nani?” “Ndio maana upo hapa leo, James! Sijakusudia kumficha Nanaa.” Geb alianza akiwa ametulia tu.

“Unakumbuka nilikufuata ofisini kwako nikakwambia kuwa nampenda Nanaa?” “Ndio ulikuwa ukiomba ruhusa ya kumzalisha?” James akauliza kwa jazba, Geb akatulia kidogo. Hakuna aliyejua kama Geb alishamfuata James kumwambia maswala ya Nanaa. Wote wakabaki kimya wakisubiria kuona mwisho wa Geb na James. “Nakufahamu Geb. Wewe sio mtu wakukosea. Kumbuka ni kama tumekuwa pamoja.” “Sikujua kama Nanaa ni mjamzito. Alinikataa, akaondoka kwangu akiwa mjamzito bila kuniambia. Alinipiga marufuku nisimtafute tena maishani, kama vile na wewe ulivyonifuata rasmi na kunionya nisisogee pale chuo kikuu cha Mlimani kumfuata Nanaa, labda niende kwa shuguli zangu.” James alianza kutulia. Nanaa hata hakuwa akijua kama kaka yake alimkataza Geb asimtafute.

 “Sasa kwa kuwa ulikuwa mwaka wake wa mwisho chuoni, nikakubaliana na onyo lako na nikaona ni vyema kumuacha, nisimbugudhi. Sikukutana na Nanaa, mpaka miezi miwili iliyopita, akiwa na mtoto wangu. Alijifungua, akamtafuta mama nakumuomba amuhudumie kwa siri. Nilipoona nyendo za mama hazielewiki ni kama za siri, ndipo nikamfuatilia. Alikuwa akitoka asubuhi na vyakula, anarudi usiku. Ndipo nilipoingiwa na wasiwasi. Ndio siku moja nikaamua kumfuatilia mpaka hosteli za Mlimani ambako alikuwepo mtoto wangu na Nanaa. Kwa kuwa Nanaa hakutaka kunihusisha na mtoto wangu, nilimchukua mtoto wangu kwa nguvu, ndipo Nanaa akanifuata nyumbani. Nilimkatalia mtoto kwa makusudi ili Nanaa abaki nyumbani, atulie.” Geb akaendelea.

“Tulikuwa kwenye hali mbaya sana James. Nisingeweza kumwambia mtu yeyote juu ya Nanaa au mtoto kwa wakati ule, kwa kuwa sikuwa najua hatima yetu. Tumepata na Nanaa, na kuwekana sawa, hata week haijaisha! Jana ndio tumerudi kutoka kwenye apartment. Tulikuwa tukiishi huko na ndiko tulikopatana na Nanaa. Leo upo hapa ili kukutambulisha mtoto, lakini pia kutaka kujua taratibu za kulipa mahari. Nimekusudia kumuoa Nanaa, na wewe unanijua James, huwa sidanganyi.” James akabaki kimya kwa muda.

“Usingemzalisha kwanza, Geb! Si ungesubiri!” “Nanaa asingekubali nimuoe James. Na wala leo asingekuwa hapa na  mimi. Muulize mwenyewe. Hata alivyorudi na mtoto, alijaribu kunitoroka. Nakuhakikishia na nyinyi watatu wote mnanijua kasoro mama, nisingezaa na Nanaa kama sina nia ya kumuoa. Weka hasira pembeni James, halafu kuwa mkweli. Unanijua mimi, huwa sifanyagi kosa kama hilo.” Geb akajitetea tena. Kwa kuwa James alimjua Geb, akatulia kidogo.

“Pole sana mwanangu, lakini mtoto mwenyewe ungemuona, ingekusaidia. Nanaa katuletea toto la nguvu. Damu nyeupe peee. Kitu hadimu kwenye ukoo wetu.” Kidogo James akatabasamu.“Yuko wapi?” “Amelala, lakini ngoja nikuletee labda utafurahi kidogo.” Mama G akasimama kwa  haraka.  “Nashindwa kukuomba msamaha James, nitakuwa nakudanganya tu. Haikuwa bahati mbaya. Hivi ilivyo, ndivyo nilikusudia iwe. Nisaidie kunipa tu taratibu inayofuata ili kukamilisha utaratibu wakumfanya Nanaa kuwa mke wangu wa halali.” James akacheka, akatingisha kichwa. 

“Unajua siamini kabisa! Aisee Geb wewe niking’ang’anizi! Labda ndio maana umefanikiwa kuliko sisi wote.” Angalau watu wakacheka. “Nilikuwa namuonya Geb huku nimemtolea macho, aachane kabisa na Nanaa. Yaani nilikuwa namkaripia mpaka mwenyewe najua. Lakini ukakazana tu! Nilikuwa najua sana kama ulikuwa ukikesha pale kwa Antii wakati Nanaa alipotoka hospitalini.” Geb akacheka. “Nilimsihi sana Antii asikwambie.” “Asingeweza. Lakini nikamwambia akuache tu.” Kidogo Nanaa akapumua.

“Sijui kwa nini tokea unaanza kumsimulia Nanaa tukiwa shule, nikaanza kujiona na mimi nawajibika kama wewe! Unakumbuka Danny?” “Nakumbuka vile James alivyokuwa anadanganya shuleni anaumwa ili arudi kumuona Nanaa. Wakati huo Nanaa kalikuwa hakajatimiza hata miaka 5.” “Nilimuacha nyumbani ndio ameingiza miaka 4. Nikamuomba Mzee anihamishie shule ya sekondari ya Old Moshi, mama akakataa. Nilikuwa nakaribia kuchanganyikiwa! Maana ndio kalikuwa kadogo. Halafu likizo nzima ile ya darasa la saba, nilikaa naye kama yaya wake. Kumlisha, kumuogesha na kumfanyia kila kitu. Sasa matokeo kutoka, naambiwa natakiwa kwenda kusoma bweni! Nilihisi nitarukwa na akili. Maana tokea kanatolewa hospitalini mimi ndio nilikuwa nakitunza. Wakati mwingine natoka shule nakikikuta kimelowa, inabidi kukibadilisha. Hapo nipo la 5. Nanaa hajui mtu ila mimi. Nahisi ndio maana nilipokutana na nyinyi nilikuwa nikimuongelea sana Nanaa ili kujifariji tu. Nilikuwa na wasiwasi naye kweli.” “Labda na mimi ndio maana nilianza kumfuatilia kwa kumuonea huruma.” Geb akaongeza.

“Lakini Geb ulikazana! Unakumbuka James?” “Sana tu. Unakumbuka mpaka tukalizungumzia hili?” James akauliza. “Nakumbuka. Kila mtu alijua kama Geb anamfuatilia Nanaa.” Danny akaongeza. “Sasa utata ukaja pale ulipoanza mahusiano na wanawake wengine. Nikajiambia labda ni upendo wa kikaka.” Wote wakacheka. “Lakini hata mimi nilidhania hivyo hivyo mwanzoni. Kuwa ni upendo kama wa James kwa Nanaa. Lakini kadiri siku zilivyozidi kwenda, ndivyo nikawa nikimfikiria Nanaa kwa zaidi. Mambo yaliharibika nilipokuja kumuona Nanaa mwenyewe. Ndio nikajua ni mke wangu.” Walizi kucheka.

“Nisaidie tu kujua hizo taratibu za mahari.” “Nitaongea na mama, tuone atasemaje.” “Asante kaka, na samahani sana kwa kutokukwambia mapema.” Akamgeukia Nanaa. “Daah! Ushukuru kwa kuwa ni Geb. Sijui tungejificha wapi!?” “Samahani kaka yangu.” James akatingisha kichwa na tabasamu usoni. “Umekosea pazuri.” James akajibu, wakacheka.

~~~~~~~~~~~~

          Mama G akatoka na Oliva, akamkabidhi James. James akaanza kumwangalia kwa makini kisha akauliza. “Una uhakika huyu mtoto ni wa Geb wewe Nanaa?” “Kaka wewe!” Wote wakacheka. “Mbona mtoto kama wakiarabu!?” James alijawa na tabasamu kila mtu aliliona lile tabasamu. “Wangu huyo, James. Angalia nywele hiyo. Hata umpe mchina miaka 7 hawezi kuitoa nywele kama hiyo kiwandani. Na akifungua macho, utafikiri Fili.” Geb alijisifia huku na yeye akimsogelea yule mtoto.

“Fungua basi hayo macho mama, ili wakuone!” Geb alimuongelesha mwanae taratibu huku akimkuna miguu. “Na anajua kulala huyo!” Mama G aliongeza. “Hongereni sana.” James akawapongeza. “Asante.” Mama G akadakia yeye kwa haraka. 

“Mama wewe! Mtoto wa kwako!?” Grace akamuwahi. “Kumbe wako? Huyo mtoto anajina langu na ninamlea mimi mwenyewe tokea anazaliwa. Mama yake hajawahi hata kumuogesha huyu mtoto! Muulize. Anajua kunyonyesha tu, kazi nyingine zote za huyo mtoto ni mimi.” “Basi na biashara pia imemshinda, mama huyo! Anakazi yakulea tu” Grace aliongeza nakumfanya James acheke.

“Mama umeacha kazi?” “Kazi zipo James mwanangu. Nikienda kesho au kesho kutwa, nitaikuta tu. Lakini huyu wajina wangu, siku ikipita moja, ujue haitakaa ikarudia milele. Sitaki kupitwa.” James alijisikia vizuri sana. “Asante sana mama kwa kumpokea Nanaa. Nafarijika nikiona mnamjali, anahitaji familia. Nitaenda kuzungumza na mama kujua taratibu za mahari.” James alikuwa akiongea huku macho yote yakiwa kwa huyo mtoto. 

~~~~~~~~~~~

Chakula kiliwekwa mezani, Nanaa akawakaribisha watu wote pale mezani. Akakaa pembeni ya kaka yake. Akaonekana kama ana kitu anataka kumwambia. James akamwangalia. “Vipi?” Nanaa akacheka kisha akainama. “Unataka tutoke tukaongee hapo nje?” James akauliza. Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Sasa si umuache mwenzio amalize kula?” Mamaa G akaingilia. “Chakula hakitapita huyu. Namfahamu akiwa na jambo lake. Twende.” James akaweka kijiko kwenye sahani, akasimama na dada yake. Wakatoka nje, wakakaa barazani.

“Ni nini?” James akamuuliza. “Namuhofia Zinda.” Nanaa aliongea kwa sauti ya chini, lakini Danny ndani akaanza kucheka kwa sauti. “Yaani Danny ni mbea wewe mume wangu! Sasa si ungenyamaza tu?” Grace naye alikuwa akicheka. James naye akaanza kucheka. “Mimi naona mje tu mmalizie hayo mazungumzo humu humu ndani. Dada yako hajuagi kunong’ona huyo!” Mama G akaingilia kila mtu akaanza kucheka, mpaka Geb. 

“Kweli tena James mwanangu. Nanaa hajui kunong’ona hata. Sisi wote tulijua tutasikia tu.” Nanaa alikuwa akicheka. James akamshika mkono wakarudi ndani. Bado James alikuwa akicheka. “Bwana mimi sipati picha! Zinda lazima akumind Nanaa. Umemkataa! Tena alishakuwa amekununulia bangili za dhahabu, ukaenda kuzaa na Geb!” Danny aliongeza kichochezi. “Mimi sikujua kama alininunulia!” Nanaa akajitetea nakufanya watu wazidi kucheka. “Kwa hiyo ungejua kama amekununulia bangili za dhahabu, ungemkubali?” Danny akamuuliza. “Akuuu!” Nanaa alikataa kwa kupandisha mabega juu. Watu wakazidi kucheka.

“Yaani sijui utamwambia nini Zinda! Maana zile sababu zako ulizompa, ni kinyume kabisa na ulichoenda kufanya!” Danny alizidi kumuogopesha. “Sio mimi ni Geb huyo!” Hapo mpaka Grace alipaliwa. Mama G, ndio alikuwa akicheka mpaka machozi. “Acheni kumuogopesha mpenzi wangu jamani. Zinda alikuwa akijua tokea zamani kuwa nilikuwa na nia ya dhati kwa Nanaa. Kwanza nilikuwa nikimshangaa alivyokuwa akihangaika na Nanaa wakati alijua wazi mimi ndio nilikuwa na nia naye. Wala usiwe na wasiwasi Nanaa. Hakuna baya ulilolifanya. Rafiki zake James wote walikuwa wakijua nilikuwa nakufuatilia tokea tupo Iliboru sekondari. Tena kuna kipindi mpaka Malii akaniulizia juu yako. Kwa hiyo wanajua sana.” Geb akamtuliza. 

“Afadhali. Maana nilikuwa naogopa kweli. Nilisema wasije wakakuona wewe umewasaliti. Wakati ni mimi mwenyewe niliamua.” Nanaa aliongeza taratibu kama anayefikiria. “Wala msingemtuliza huyu. Aliyemwambia amdanganye mwanangu Zinda ni nani? Mngemuacha Zinda aje amsute.” “Mwaya mama sijui yukoje! Saa nyingine anakuwa rafiki yangu saa nyingine ananirusha roho!” Kila mtu alicheka. “Ule uongo wako kwa Zinda mwanangu, ndio huo unaniuma mimi.” “Hayo mambo ya kale mama. Sasa hivi kuwa upande wangu mimi.” “Nimgeuke Zinda mwanangu aliyeingia mpaka deni la kununua dhahabu!?” Nanaa akacheka sana.

“Yaani kumbe mpaka alikopa?Asingefanya hivyo!” Nanaa alizidi kucheka na kufanya wengine wacheke zaidi. “Kumbe je? Si anakupenda.” “Mimi nilishasema Zinda simpendi. Kwanza anakunywa pombe. Mimi sipendi harufu ya pombe. Muulizeni hata kaka.” Kila mtu akacheka. “Sasa si ungemwambia mwenyewe?” Mama G, akamuuliza. “Hata mimi nimemuhurumia Zinda. Amehangaika kweli, halafu akaja kuambiwa shule kwanza! Hata mwezi haujaisha, nashangaa Geb amekubaliwa!” Danny aliongeza Nanaa akazidi kucheka huku amejificha uso. 

“Mimi Geb ndio nilikuwa namtaka tokea mwanzo.” Nanaa akajibu, nakufanya mpaka James acheke na kushangaa. “Nanaa!?” “Kweli kaka. Wala sio Zinda.” Nanaa alizidi kujitetea. “Haya dada yangu. Mimi nitamalizana na Zinda. Wala usiwe na wasiwasi.” James akamalizia. “Asante kaka yangu. Angalau nikikutana naye nitakuwa sijifichi.” Viliendelea vicheko kati yao mpaka James alipoaga. Aliondoka kila mtu akajua ameridhika.

Penzi lililokusudiwa na kusubiriwa kwa hamu!

Penzi la Nanaa na Geb ndio likaanza rasmi. Moto uliokuwa ukiwaka ndani yao, ni wao wawili tu ndio walijua. Muda wa kitandani ukawa mfupi. Hilo wote walikiri na kulalamika kunapambazuka mapema, na weekend haina huruma kwao. Iliisha bila wao wawili kufaidi vilivyo. Nanaa alikuwa akisubiri muda wa kurudi kwa Geb nyumbani, kana kwamba anasubiri kutunukiwa ulimwengu wote! Kila alipowasili Geb kutoka kazini, alianza mabusu kwa Nanaa, popote atakapomkuta binti huyo. Na hayakuwa mabusu ya sekunde kadhaa, mabusu yakumtoshea. Kisha wataongozana kwenda kuoga. Haijalishi muda. Huo wakati atakao fika Geb, ndio wakati wa kuoga kwao. Napo hapakuchukua muda mfupi. Mpaka wapangaji wao walikuwa wakiwasahau kama wapo humo ndani. Wakipandisha juu, watatumia muda wakutosha, ndipo Geb atashuka chini kuzungumza na mama yake na watu wengine.

Geb awapo nyumbani, alikuwa nyuma ya Nanaa wakati wote. Atamshika na kumkumbatia. Hata akiwa yupo kwenye sinki la jikoni, basi Geb atamfuata na kuanza kumpapasa pale anapoweza au kuzungumza naye. Ilimradi tu mikono yake iwe juu ya mwili wa Nanaa. Muda mwingi walitumia chumbani. Na kwa kuwa muda mwingi Oliva alikuwa na bibi yake, basi Nanaa alikuwa huru. Jumbe za mapenzi na simu za kujuliana hali kilikuwa kitu cha kawaida sana kwao. Muda mwingi walikuwa waki chat. Wakati Geb yupo kazini, Nanaa yupo nyumbani.

‘Umevaa nini sasa hivi?’ ‘Upo wapi sasa hivi?’ ‘Piga picha nikuone.’ ‘Nina hamu na wewe!’ ‘Asubuhi muda ulikuwa mfupi, bado nakuhitaji.’ ‘Naomba kusikia sauti yako.’ ‘Liv ananyonya? Naomba kuona.’ ‘Nikirudi sasa hivi, tunaweza hata kupata nusu saa tu tukiwa peke yetu?’ ‘Tengeneza mazingira ya kumuachia mama mtoto. Nakuja nipo njiani, nikukute chumbani.’ ‘Kumbuka leo ni ijumaa, Nanaa. Hakikisha unalala mchana. Ili usiku tupate muda wa pamoja.’ ‘Na wewe hakikisha hujichoshi.’ Hizo zilikuwa jumbe zisizoisha kati yao. 

~~~~~~~~~~~~~

“Mimi naona huyu James alete tu hizo taratibu za mahari. Watu walipe hiyo mahari, tupumzike.” Geb na Nanaa wakacheka. Grace aliwakuta jikoni wanapeana mabusu mfululizo. “Halafu mimi nashauri honeymoon ya hata mwezi mzima. Angalau kuwe na amani humu ndani.” Danny alidakia akiwa nje ya jiko. “Mimi pia nitachangia hiyo honeymoon. Wakae hata miezi 3. Watu tupumzike! Maana jikoni hapafikiki, wenye nyumba kutwa wamekumbatiana. Ukisema ukakae barazani, na wenyewe wapo wamepakatana. Ukipita koridoni, na wenyewe wapo wamekumbatiana!” Geb na Nanaa wakazidi kucheka. 

“Sasa nikienda honeymoon miezi 3, si tutarudi tumekuwa masikini?” “Kwani hata sasa hivi kuna unachokifanya kule ofisini?” Grace akauliza. “Grace unapata dhambi wewe!” Geb akashangaa. “Kutwa upo kwenye simu Geb. Mpaka sekretari wake amehamishia kazi zake kwangu. Na akianza simu zake kwa Nanaa, hataki mtu aingie ofisini kwake. Basi kama kuna kitu cha muhimu, inabidi yule mama aje anifuate mimi, mimi ndio niingie huko ofisini kwake. Siku hizi anasaini cheki bila hata kuuliza maswali kwa kuwa akili zote zipo nyumbani. Dakika moja yupo, dakika ya pili anakugongea ofisini anakwambia anatoka kidogo. Ukipiga simu nyumbani, unaambiwa yupo chumbani na Nanaa. Bora aoe, aende akapumzike labda akirudi akili itakuwa imetulia.” Grace aliongeza. 

“Hapa nyumbani napo kazi ni hiyo hiyo. Simu mkononi kila wakati. Sasa iite, halafu yeye yupo mbali. Utamuonea huruma. Unaweza ukadhani atavunja mguu.” Mama G akaongeza. “Sasa unakuta mwenzio ameacha kazi zake zote, anakupigia wewe! Lazima kuheshimu hilo.” “Mmmh!” Mama G akaguna, kila mtu akacheka. 

Mwenye Kisu Kikali, Ndio Mla Nyama.

Mambo hayakwenda kama alivyotegemea James na kina Magesa. Zinda alilalamika sana kuwa Geb ametumia pesa yake au utajiri wake kumnyang’anya mwanamke wake. Ambaye ni Nanaa. Alilalamika bila kuchoka. James alipoona wameshindwa kuelewana na Zinda ikabidi kumuita Danny. Wakakutana na Zinda baa. Danny akaanza kumkumbusha tokea zamani. “Unakumbuka wakati tupo “O” Level? Kipindi James anaenda kwao kumwangalia Nanaa? Geb ndiye aliyekuwa akimwandikia masomo yote darasani kama anakosa vipindi. Na yote hayo alifanya kwa ajili ya Nanaa.” Danny akatetea. “Kwani mimi sikumsaidia James wakati tupo shuleni? Mlijua kuwa nafanya kwa ajili ya nani?” Zinda aliuliza akiwa na hasira. “Au leo ndio mnajidai kuniruka sababu sina pesa kama Geb?”

“Hapana Zinda. Wewe unajua mimi ni mtu wako!” Danny alijaribu kumtuliza. “Acha kunidanganya Danny. Umemuoa dada yake, lazima utamtetea tu.” “Simtetei Geb! Kumbuka vile Geb alivyoendelea kumfuatilia yule mtoto kwa karibu hata alivyokuwa India? Hakuacha kumfuatilia.” “Wewe unajuaje kama na mimi sikuwa nikimfuatilia?” “Sema umekasirika tu Zinda. Lakini sikumbuki wewe binafsi kumuulizia Nanaa kwangu kama Geb.” James akaingilia.

“Utaacha vipi kutetea wakati dada yako anaolewa kwenye neema, James? Unajua atafia pazuri kwenye majumba ya maana sio mimi. Lakini kumbukeni mimi nimekuwa na nyinyi tokea zamani sana. Geb alishawaacha hapa akaenda kusoma nje ya nchi, mimi nilikuwa na nyinyi. Danny wewe tumekuwa kama ndugu. Mama yangu mimi ndio mama yako wewe. Leo pesa inakutoa ubinadamu unaniruka! Sikuchagua kuwa masikini.” “Acha hizo Zinda!” “Kwani uongo? Tuambizane ukweli sisi wote hapa. Kama mimi ndio ningekuwa Geb, nina pesa kama alizonazo Geb. Kila mkiwa na shida ninawakopesha. Na Geb angekuwa mimi. Leo mngenifuata kunituliza wakati amenichukulia mwanamke wangu?” “Hapo unatutukana Zinda!” James akaingilia.

“Hapana. Kuweni tu wakweli. Nanaa ananikataa mimi kwa kuwa sina pesa. Na James umeamua kumpa baraka zako Geb kwa kuwa unajua undugu utakolea, atakusaidia popote ukikwama. Na..” “Nisikilize Zinda. Najua umekasirika. Lakini unapokwenda, unakaribia kuvuka mipaka, na sitaruhusu. Huwezi kumtukana dada yangu. Huwezi kusema amempendea Geb pesa.” “Kwani uongo? Alinikataa mimi kwa kunidanganyia maswala ya shule. Mimi nimekaa nimetulia, sijatafuta hata mwanamke! Namsubiri Nanaa amalize shule tuzungumze naye tena. Kumbe alikuwa akinitoa njiani tu na nyinyi wawili mkinikejeli!” “Kivipi Zinda!?” Danny akauliza.

“Sio nyinyi wawili niliowashirikisha nia yangu kwa Nanaa? Mlijua ninaingia deni la pesa nyingi tu kwa ajili ya Nanaa. Mlijua nimekopa pesa yakumnunulia Nanaa vitu. Danny ulinisindikiza mpaka kwa sonara. James na wewe ukaungana na sisi kwenda kununua nguo, viatu na vitu vingine! Tena mkijua ni kwa pesa niliyokopa! Hamkusema kitu! Mlinyamaza kimya. Kumbe James unang’ata meno. Hunitaki mimi mkopaji. Unataka dada yako akaolewe na tajiri!” “Zinda jiangalie!” James alimtahadharisha.

“Kwa lipi James? Naweza nikawa masikini, pengine sijui hata kutongoza lakini si mjinga. Unakumbuka wakati tupo njiani kwenda Marangu niliwaomba nyinyi wawili mnisaidie kuniunganisha kwa Nanaa? Haswa wewe James. Nilijua wazi hakuna utakachomwambia Nanaa, asikusikilize. Lakini ukajibaraguza kama mtoto wa kike ili tu kunikwepa huku ukimsogeza mdogo wako kwa Geb. Umemtoa kwako ukamuhamishia nyumbani kwa Geb ili tu akambebee mimba Geb, kisha wapate sababu ya..” James alirusha ngumi ikampata Zinda sawia.

Danny alisimama kwa haraka akamshika James. “Nakwambia ukweli ndio maana unakasirika James. Ubinadamu unakuisha wewe na dada yako sababu ya pesa!”  James alitaka kumrukia tena, lakini Danny akamshika kwa nguvu. Kelele zilifanya watu wengine waanze kuwatizama na kutaka kujua kulikoni, lakini Danny akamvuta James nje. “Naomba ondoka James. Tafadhali sana. Ondoka.” Danny akamsihi James. Bila kuongeza neno, James akaingia kwenye gari yake akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~

Katika yote hayo Zinda hakuwa amelewa hata kidogo. Alionekana wazi ameumizwa. Danny alirudi kule alikokuwa amemuacha Zinda. Akakuta ameshaagiza bia. “Tumetoka mbali sana mimi na wewe Danny. Walishakufukuza hao nyumbani kwao, mimi nikakupokea. Nilikukaribisha kwetu ukiwa huna pakwenda. Leo unanigeuka mimi! Tena nikiwa nimekuomba unisaidie kumpata Nanaa!” “Zinda umekasirika. Angalia sana maneno yanayokutoka ukiwa na hasira.” Danny akamsihi.

“Kwani ni uongo kuwa walikufukuza?” “Sikuwahi kufukuzwa nyumbani kwa kina Geb hata siku moja. Mimi mwenyewe niliondoka kwao kipindi kile tulipo maliza wote chuo, sababu sikutaka kushuhudia Grace akiolewa na mwanaume mwingine. Yule mama tokea zamani alinipokea kama mtoto wake.” “Utaacha vipi kuwatetea wakati wanakuweka mjini? Geb ndiye anakulisha na kukulaza wewe na mkeo nyumbani kwake, utaachaje kumtetea? Hata mimi ningelipa fadhila ya kumsogezea Nanaa.” Danny alipandwa na hasira. 

“Ila nakutuma kwao Danny, na wewe Kibara wao usikie. SITAKUBALI hata kidogo. Nitafanya nini na lini, hiyo mtaona matokeo. Hakika mtalipa kwa usaliti wenu. Nyinyi wote. Nyinyi si mnapesa sasa hivi? Geb ameshakuhonga na kukusaidia kukamilisha mjengo wako? Sasa hivi zamu ya James. Na yeye atasaidiwa kukamilisha kinyumba chake alichokuwa akihangaika nacho miaka yote hiyo. Sasa mimi nitawakomesha Danny. Kawafikishie ujumbe wangu. Na wewe sitaki kukuona tena kwenye maisha yangu. Msaliti mkubwa wewe. Nenda, labda na wewe utapewa na hilo jina la Magesa. Wewe na mkeo wote muitwe Magesa.” Danny hakutaka kujibu kwa kuwa alikuwa amekasirika sana, akaamua kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~

Danny alirudi nyumbani mkewe akajua kabisa amekasirika. Aliingia isivyo kawaida yake, akasalimia na kupitiliza chumbani. Maneno ya Zinda ya kumkashifu kuwa anatuzwa yeye na familia yake, na Geb, yalimuumiza sana. Yaliharibu akili zake na kuchafukwa kabisa moyo. Kwa kuwa ni kweli alikuwa akiishi nyumbani kwa Geb. Tokea wahamie hapo kwa mara ya pili hakuwa hata akikumbuka lini alinunua chakula hapo ndani. Hata chumvi! Aliamka akakuta chakula kimeandaliwa, na aliporudi jioni alikuta chakula mezani. Yeye na familia yake walikula na kusaza hapo ndani bila hata kufikiria mara mbili.

Leo Zinda ameibua kitu kipya. Ikamfanya ajifikirie. “Kumbe ndivyo jamaa wote wanavyonisema hivyo!” Danny akawaza, akiyachukua maneno ya Zinda kama ndio kauli ya kila mtu. Akajidharau sana. Akajua wenzake wote wanamsema hivyo kuwa anatunzwa na Geb. Aliumia zaidi kwani kwa sehemu ilikuwa ni kweli. Lakini ni kwa ajili ya maisha waliyokuwa wakiishi hapo. Waliishi kama ndugu bila kuhesabiana. Wewe fanya hiki, mimi kile, ilimradi siku iende warudi nyumbani wakutane wacheke. 

Lakini haikuwa hivyo kwenye macho ya Zinda rafiki au kama mtu wa karibu sana kwa James. Aliibua kitu cha tofauti ndani ya Danny, tena hakutegemea wala hakuwa tayari kwa wakati ule ambao mkewe anakaribia kujifungua na hawana msaada wa msichana wa kazi. Akajuta hata kwa nini alimkubalia James atoke naye mapema kazini kwenda kuzungumza na Zinda. James na Danny walitoka kwenye hicho kikao, Zinda akiwa amewachafua mioyo yao vibaya sana. Aliwadhihaki na kuwakashifu kila mmoja kwa vile alivyowajua na akagonga msumari palepale, kuhakikisha anawafunga midomo na wao waonje maumivu anayojisikia.

~~~~~~~~~~~~~

Grace alimuona vile mumewe alivyoingia, wakaangaliana na mama yake. Grace akageuka kulia na kushoto, kutafuta balance ya kusimama huku akigugumia akiashiria anafanya kazi ngumu mpaka akafanikiwa kusimama. Hata hivyo alikuwa amechoka. Ndio na yeye alikuwa amerudi nyumbani kutoka kazini. “Hiyo siku ya kutoa hawa watoto huko tumboni, naisubiri kwa hamu sana!” Mama yake akacheka. “Waache wakomae wajukuu zangu!” “Basi ujue mwanao ndio nazidi kukoma. Heri uniombee watoke tu. Watakomaa hukuhuku nje.” “Siku zimebaki chache. Jikaze.” “Mmmh!” Grace akaguna huku akielekea chumbani kwao.

Aliingia chumbani akamkuta mumewe anasoma jumbe kwenye simu yake huku anatingisha kichwa. “Kwema?” Grace akauliza huku akipapasa tumbo lake. Akajivuta mpaka alipokuwa amesimama mumewe. “Vipi? Mbona macho kwenye simu hata huniangalii!?” Grace akauliza kwa kulalamika. “Samahani bwana. Nahisi nimechanganyikiwa. Vipi nyinyi? Mmeshindaje?” Danny akamgeukia mkewe, akamgusa tumbo.

“Tupo tu.” “Umeweza kunywa maji?” Danny akamuuliza mkewe. “Ndio ilikuwa kazi ya leo hiyo. Mama kila akipiga simu ananikumbusha kunywa maji. Angalau nimepitisha lita mbili. Ila mbavu zinauma!” “Pole. Lakini si ndio siku za lala salama hizi?” “Mmmh! Bado. Ndio nimeanza mwezi wa 9!” “Utafika tu mama. Jikaze.” Danny akambusu mkewe. “Nini kinakuchanganya?” Grace akauliza. “Wewe ingia huko kwenye group letu la Whatsapp, utajionea na kujisikilizia mwenyewe.” Danny alijibu wakati anajitupa kitandani na viatu vyake.

“Vua bwana viatu Danny! Wewe ndio umemfundisha Fili! Anacheza na viatu kitandani!” “Wewe soma hizo jumbe humo ndani ya group, ndio utajua kwa nini napanda na viatu kitandani.” “Kaniletee basi simu yangu. Nimeacha sebuleni.” “Basi tumia ya kwangu.” “Sitaki bwana Danny! Nenda kaniletee yangu. Nikianzia kusoma kwenye yangu ndio vizuri.” Danny akatoka, akakutana na Geb naye anasoma huku akitingisha kichwa. “Njoo huku huku sebuleni Grace. Nilitaka kumficha Geb, lakini naona ameshapata ujumbe wake.” Danny akamuita mkewe. “Kuna nini tena!?” Akauliza mama G, baada ya kutoka chumbani kwake akiwa na Oliva na Fili. Nanaa alikuwa ameinama wakati anasikilizishwa jumbe alizojirikodi Zinda na kutuma kwenye group.

Alia Wivu!

Hasira ya Zinda ikaendelea. Akaanza kusambaza sumu ya chuki katika kundi lao la marafiki. Wale waliokuwa pamoja tokea wapo sekondari mpaka sasa wakiwa wameoa. Lilikuwa kundi kubwa tu. Kwani walitafutana baada ya chuo kuisha wakawa wakishirikiana. Waliongeza hata wake zao kwenye kundi hilo. Kwa hiyo kama kulikuwa na jambo lolote lile, liwe la kheri au la simanzi, walishirikiana na kuwasiliana kwa kutumia kundi hilo. Wakaweza kukutanika mara moja na kushirikiana kwa wepesi. Na Danny ndiye aliyekuwa kiongozi wao.

Zinda alijirekodi kuanzia mwanzo wa mahusiano yake na watu wote waliokuwepo mle ndani. Alieleza vile alivyojua wao ni ndugu. Wakisaidiana bila hila. Akaeleza vile alivyojitoa kwao, hata pale Geb alivyokuwa hayupo kwenye maisha yao, lakini yeye alikuwepo. Zinda alieleza kusikitishwa na usaliti wa watu waliopo humo ndani. James na Danny ambao waliheshimiana sana. Akaeleza vile walivyojua tokea mwanzo anakusudia kukopa na wakajua amekopa pesa nyingi kwa ajili ya kununua zawadi za Nanaa. Aliwakumbusha watu wote mle ndani juhudi zake zote safarini kuelekea Marangu mpaka walipofika Marangu. Wao wakiwepo, na Geb akiwepo na Liz. Tena walilala chumba kimoja kama wapenzi.

Akawakumbusha usaliti wa familia hiyo kwa Nanaa. Jinsi walivyomdhalilisha kule Marangu na James kuonekana kukasirishwa na kitendo kicho. Akawakumbusha ule mkasa mzima. Nanaa hakuwa hata amejua kama kulitokea ugomvi alipoondoka Marangu, ndio siku hiyo na yeye akasikia hapo kwenye malalamiko ya Zinda. Akanyanyua uso kumtizama Geb, lakini Geb hakutaka kukatiza. Akataka kuendelea kusikiliza rikodi hiyo ya Zinda.

Zinda akamlaumu sana Geb kutumia mali zake kumnyang’anya mwanamke wake. Tena watu wote kwenye hilo kundi wakijua hilo. Aliendelea kusema wakati Geb akimfaidi Liz, yeye Zinda kwa mara ya kwanza akaonyesha nia ya kuwa na mtu wake maishani. Akataka kutulia na Nanaa.

Zinda anasema yeye anafahamika kuwa hakuwahi kuwa na mwanamke wa maana. Au aliwakumbusha wote kipindi anamtongoza Nanaa, hakuwa na mwanamke. Ila Geb alikuwa na Liz. “Kwa kutumia pesa zake, Geb amehakikisha mimi ambaye sina kitu. Sina mwanamke, ananichukulia mwanamke wangu. Leo Danny na James kwa kuwa wananufaika na pesa ya Geb, wanatoa baraka zao kwenye ukatili kama huu! Wanasema Geb alimpenda Nanaa tokea zamani wakati wote tulishuhudia Geb akimkana Nanaa mbele yetu wakati tupo Marangu! Geb alikuwa akilala na Liz wakati Nanaa alikuwepo! Mimi nahangaika kumtongoza Nanaa, na kumfanya awe wangu, Geb akiwa anamsaidia Nanaa na kaka yake, kimali, akanipokonya mwanamke wangu.” Zinda aliendelea kwenye rikodi yake.

“Ubinadamu unawaisha watu niliohesabu kama ndugu sababu ya pesa! Danny akiwa kama kiongozi wetu na ndugu yangu mimi wa karibu, leo sababu ya kutunzwa hapa mjini yeye na familia yake na Geb, anaamua kufumbia macho hilo, anamtetea Geb! Anasema Geb alimpenda Nanaa tokea mwanzo! Mbona sikumuona Geb akimsubiria Nanaa? Akaendelea kuwa na mahusiano ya wanawake watatu tofauti tofauti! Tena mmoja alitaka mpaka kujiua kwa ajili yake wakati tupo chuo kikuu cha Mlimani! Najiuliza mapenzi hayo kwa Nanaa alianza lini wakati Nanaa alikuwepo kabla ya wanawake wote hao kuwepo kwenye mahusino na Geb? Ni kipi kigumu watu wameshindwa kukiona na kuwa wawazi? Jamani pesa ya Geb isitufumbe macho na kusahau mambo!” Akaendelea kulalamika akisikika na uchungu mwingi.

“Ni juzi juzi tu, kwenye harusi ya Malii, huyu huyu Geb mwenye sifa ya kutosahau, alimsahau na kumuacha nje ya ukumbi mwanamke anayesema anampenda! Akapigwa na baridi zaidi ya masaa manne mpaka Nanaa akaugua karibia kufa! Nanaa aliugua na sisi tukimuuguza bila familia hiyo ya matajiri, kina Magesa. Eti gafla leo James na Nanaa wamelisahau hilo!” Zinda akaendelea.

“Kweli leo Geb haoni hata aibu kutudanganya sisi watu tunaomjua kabla hata hana kitu! Tena akiwa masikini wakutupwa, kama paka la mtaani tu anadanganya bila aibu! Anadiriki kusema anampenda Nanaa!  Anamchukua mwanamke wangu wakati nyinyi wote mnajua nilikuwa nikisubiri Nanaa amalize chuo nizungumze naye tena! Mpaka leo nimetunza zawadi nilizomnunulia Nanaa na ni mwezi uliopita tu ndio nimemaliza kulipa deni ya pesa niliyokopa kununulia zawadi hizo! Na nyinyi wote mnajua! Lakini mnashindwa kuwa upande wangu mimi ambaye sijawahi hata kuonekana na mwanamke! Leo mnakuwa upande wa Geb aliyekwisha kuwa kwenye mahusiano tena yakueleweka na wanawake wengine, tena hata Nanaa mwenyewe akiwepo! Kama sio upendeleo wa waziwazi tu sababu ya pesa yake ni nini?” Zinda aliendelea kulalamika.

“Mapenzi gani hayo ya dhati kwa mwanamke huyu, huku ukitaka kujiua kwa mwanamke yule!? Geb anatumia pesa yake kukandaniza watu. Aliyempa yeye pesa, ndiye aliyetunyima sisi. Na kwa kuwa ni Mungu, basi Mungu atatuhukumu kwa haki. James mpe dada yako huyo Geb, lakini nakuhakikishia, pesa sio kila kitu. Mtanikumbuka tu. Upo umbali nimeshakwenda na nyinyi, nina uhakika Geb hawezi kwenda na nyinyi. Danny wewe ni mnafiki, ndumi la kuwili. Na Mungu atakulipa kabisa. Najitoa rasmi kwenye maisha yenu. Sitaki tena mnitafute. Sitaki kupigiwa simu na yeyote. Nyinyi mliojaliwa unafiki endeleeni kuwakumbatia hao kina Magesa ili waendelee kuwakopesha pesa. Wengine hatukujaliwa unafiki. Na tutawaona mtakapoishia na hao kina Magesa. Wakiwageuka, msinitafute. Na yatakayowapata pia, msinitafute. Leo ndio mwisho wenu na mimi.” Zinda akamaliza rikodi yake. 

Akaongeza na baadhi ya jumbe zakuzidi kulalamika. Na kutukana watu wa mle ndani. Tena kwa majina.

 ‘Najua hata Malii utatetea kwa kuwa nusu ya bajeti yako ya harusi alibeba Geb. Hata gauni la harusi la mkeo, yeye ndio alilinunua, wote tunajua.’ Ujumbe huo ukawa wa Malii. ‘Danny wewe ndio siongei kabisa. Kwa kuwa mnalishwa na kulala bure hapo kwa Geb. Una kazi yakupiga picha vyakula unavyolishwa na Geb, na kuturingishia sisi mboga moja. Hata mimi ningelipa fadhila. Lazima uwe upande wake.’ Na huo ujumbe nao akaurushia kwa kundi. 

‘Na wewe James, najua unafurahia kuwa Neema imemshukia dada yako. Kwamba na wewe utaponea hapo hapo. Labda atakusaidia kumalizia kile kijumba chako ulichokuwa ukihangaika nacho miaka yote. Unamshikilia vizuri ili akutoe kwenye nyumba za kupanga. Lakini wanaume sisi tunapambana kivyetu. Hata kama hatujateremsha magorofa hapa mjini. Tunakula na kulala makwetu. Hatufungwi macho na pesa.’ Akatuma ujumbe mwingine.

‘Na wewe Jerome. Mzee wa kuchomekea. Kutaka makuu, pesa huna. Najua lazima utatetea tu kwa kuwa Geb anakudai na huna mpango wa kulipa pesa yake. Lakini ujue wazi mkeo anajitongozesha kwa Geb. Masela wanakuchora tu. Wote wanajua kuwa mkeo anamtaka Geb. Kundi limejaa unafiki. Wanashindwa kumwambia ukweli, wamebaki kukucheka pembeni wewe na mkeo.’ Na huo nao akaurushia hapo kundini.

‘Na wewe Tuli, jamaa kashakuonyesha hakutaki. Acha kujichekesha kwake kwa mambo ya kipuuzi. Najua hata hili utataka kumfariji nalo kwa cheko lako lakijinga. Fungua macho uone na ujue majira. Tafuta mwanaume wako akuoe. Acha kuomba omba ujinga na kujikiria Geb ni mumeo. Geb alishakiri kwetu hajawahi kuwa na wazo na wewe wala hana mpango na wewe. Kama masela wangekuwa waungwana wangeshakwambia. Wanakuchora tu. Tena wanasema unamtakia vijisenti vyake.’ Huo nao Zinda akaurushia hapo hapo.

“Anaandika ujumbe mwingine. Ngoja nimtoe kabla hajazidi kuharibu.” Danny alipoona anaandika tena, akaamua kumtoa kabisa kwenye kundi kabla hajatuma ujumbe mwingine na kuzidi kuchafua watu. Akatulia. Yeye Danny ndiye alikuwa akiwasomea wote pale sebuleni. Wakawa wanasikiliza. “Mmmh!” Grace alisikika akiguna. “Sijui nijibu nini humu ndani!?” Danny akauliza. “Hapana. Usijibu kitu chochote. Tulia kwanza.” Mama G akatoa wazo. Wote wakamwangalia mama yao.

~~~~~~~~~~~~~

“Nisikilizeni kwa makini sana. Shetani anataka kuwafarakanisha. Anajua wazi kila kwenye umoja, ndipo Mungu anapoamuru baraka zake. Someni kitabu cha Zaburi 133:1-3.” Geb akafungua bibilia yake ya kwenye simu. “Zaburi 133:1-3 Inasema hivi, {{1.Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, kwa umoja. 2.Ni kama mafuta mazuri kichwani, Yashukayo ndevuni, ndevu za Haruni, Yashukayo mpaka upindo wa mavazi yake. 3 Kama umande wa Hermoni shukao milimani pa Sayuni. Maana ndiko BWANA alikoamuru baraka,Naam, uzima hata milele.}” Geb akamaliza. “Nataka na Danny naye asome. Taratibu tu. Kwa makini. Neno kwa neno.” Mama G akataka Danny arudie kusoma. Danny akasoma.

“Sijui kama mmeshatambua hila ya muovu? Shetani ni muongo. Na hakuitwa muongo kwa bahati mbaya. Anayoongea yanayofanana na kweli kabisa. Ni mfitini. Hawezi kuruhusu zile baraka Mungu anazoamuru juu yenu kama mstari wa 3 kwenye hiyo zaburi, itimie kati yenu. Hawezi. Na hatalala mpaka awafarakanishe. Danny wewe umebeba jukumu zito sana. La kundi zima na hapa nyumbani pia. Ukiruhusu tu hayo maneno yakuingie, ujue utavuruga umoja kati yetu na kundi zima. Sio Geb wala wewe ambaye anaweza kufika hapo mlipo bila mmoja wenu. Geb anakuhitaji sana kwenye maisha yake, na wewe hivyo hivyo. Siku utakapomtizama Geb kama Zinda anavyotaka uanze leo, nawaambia kabisa, hakuna kati yenu atakaye simama. Si Geb wala wewe Danny.” Mama G akaendelea.

“Pesa ya Geb itakuwa na thamani tu, sisi wote tukiwa kwenye maisha yake. Na yeye amejitahidi kutuonyesha hivyo kwa vitendo. Si kweli Danny?” “Kweli mama. Na Mungu wangu ni shahidi. Si mtetei Geb. Amekuwa mnyenyekevu kwetu sisi wote. Kwanza hazungumzi.” “Nashukuru kwa kuwa mkweli Danny. Nakusihi mwanangu, usilisahau hilo, ukakubali uongo wa ibilisi. Sina utofauti kati yako wewe na Geb. Hata Nanaa nilimwambia. Nitamlilia Mungu juu yako kama nitakavyomlilia Mungu juu ya Geb. Haupo hapa sababu ya shida. Ni umoja na amani ambayo Mungu alitujalia. Wewe ni shahidi. Alipita Liz hapa, alishindwa kuwa na sisi. Shetani ameshindwa kumtumia Nanaa kututenganisha, leo anatutumia nguvu ya nje kutusambaratisha. Msikubali.” Mama G aliongeza.

“Kwa nini leo ndio iwe ni siku ya kujulikana mabaya yote kama kweli yalikuwepo? Kwa nini leo ndio tukumbushwe mabaya tuliyomtendea Nanaa? Tena akiwa Nanaa mwenyewe na kaka yake wamesamehe na wala hawajatuhesabia? Ipo hila, na msikubali.” “Daah! Afadhali mama umeongea. Nilishafikiria kesho nirudi nyumbani kwetu na mke wangu na mtoto. Nilikuwa najiambia nitajua mbele ya safari hapo Grace atakapojifungua. Nikajiambia hapa nilazima nitoke.” “Basi ndio shetani angekuwa ameshinda. Usiruhusu neno hata moja likuingie Danny. Sio kweli kama wewe unamtegemea Geb sasa hivi. Una mshahara wako mzuri tu. Na hata mkiondoka leo, sisi tutapika humu ndani na kutaliwa. Na hicho chumba mnacholalia kitabaki na kitanda chake na AC itaendelea kupuliza hata kama nyinyi hamta itumia. Unanielewa Danny?” “Nimeelewa mama.” “Basi tulia.” Danny akavuta pumzi kwa nguvu.

“Nijibu nini kwenye group?” Danny akauliza. “Tulia kwanza. Sasa hivi kila mmoja wenu ana hasira na Zinda. Mwacheni kwanza. Tumwiteni Mungu ataingilia kati hii hali.” Nanaa alibaki ameinama tu. Zinda alizungumza ukweli mtupu. Tayari na yeye akaanza kusononeka moyoni. Mama G akamwangalia.

“Nanaa!” Nanaa akanyanyua uso akamwangalia. Tayari machozi yalishakuwa yamejaa machoni kwake. “Unakumbuka uliniuliza kitakachokufanya usitulie sasa hivi wakati unaye Geb na Oliva, ni nini?” Akashindwa kujibu. “Basi mambo kama haya ndiyo yatakufanya usitulie. Shetani ameshakuona umeingia humu ndani, umetulia. Sasa anahangaika kukufanya mateka wa fikra zako. Amecheza na hisia zako. Ameshaingiza uongo unaofanana na ukweli. Amerudisha mambo ya nyuma, aliyojua yalikuumiza ili kukutesa. Ni kweli wote tulikukosea kwa namna moja au nyingine. Na ukasamehe. Kwani ulisamehe sababu ya pesa?” Mama G akauliza.

“Hapana mama.” Nanaa alijibu kinyonge. “Sasa!? Sisi wote tumekuona jinsi unavyompenda Geb. Na ulitaka kujitenga kabisa na mali ya Geb mpaka sisi tulipokulazimisha usitafute kwako, hapa ndio kwako.” “Tena mimi ndiye niliye kulazimisha Nanaa. Kwa kuwa mimi ndiye nakupenda. Nilikusimulia kila kitu. Tafadhali Nanaa, usinichukie sababu ya makosa ya nyuma ambayo Zinda anayatumia sasa hivi. Tafadhali mpenzi wangu.” Geb alimkatisha mama yake, akapokea usukani wa kusihi. Nanaa akafuta machozi, akainama.

“Nanaa!” Geb akamuita. “Abee!” “Umenielewa?” Geb akamuuliza kwa upole. “Niamini nakupenda Nanaa, sina sababu yakudaganya. Naomba uniamini mimi kuliko maneno ya hasira ya Zinda. Zinda amekasirika tu, lakini anajua ukweli wote. Naomba niamini mimi Nanana. Tafadhali.” Kila mtu alijua Geb ameingiwa na hofu. Na ni mara chache sana Geb akiwa katika hali hiyo. Akajikuta amekamatwa kwenye ukweli uliotengenezewa hila kali ya kumuaminisha yeyote yule hata ambao walikuwa wakijua ukweli wangeweza kubadili walichokuwa wakikifahamu na kuelewa ukweli mpya wa Zinda na kumuona kweli Geb ni mbambaishaji tu. Sio mkweli. Zinda alimbana Geb kwa vile anavyomfahamu mpaka Geb akatingishika na jeuri yote ikamuisha. Hata mama yake akamuona. Ile haiba ya kunyamaza ikamtoka gafla akabaki akijitete akibabaika. “Tafadhali mpenzi wangu. Mimi nakupenda kwa dhati.” “Najua Geb. Nafahamu kama unanipenda. Laki…” Nanaa akaanza kulia kwa kuumia sana.

 “Njoo Nanaa.” Mama G akamuita. Nanaa akamsogelea. “Kaa hapa.” Akakaa pembeni ya mama G. “Niambie chochote kile unachosita kuongea.”“Mimi najijua nina mkosi mama. Naona nimeanza kumuingizia Geb na Oliva pia! Hawa watu walikuwa kwenye umoja mzuri tu. Ona mimi nilivyoleta machafuko! Haya, jana uliniambia unataka Oliva abarikiwe jumapili hii inayokuja. Ukasema utamfanyia tafrija. Mwanangu anaanza mwanzo wa maisha yake kwenye machafuko hivi! Najisikia vibaya mama yangu.” “Usilie Nanaa. Kwanza nataka ufute hiyo kauli kwamba wewe unamkosi. Nanaa wewe ni mbarikiwa. Maisha yako yalianza siku ile nilipokuongoza sala ya toba. Soma bibilia Geb. Fungua 2 koritho 5:17.” Geb akaanza kusoma. “{Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; yakale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.}” Geb akamaliza.

“Umesikia Nanaa? Hata kama ulikuwa na mkosi, siku ulipomkabidhi Yesu maisha yako, ameondoa kila kitu. Kama ulivyoaminishwa wewe unamkosi, ndivyo unavyotakiwa kuamini kuwa wewe ni mbarikiwa. Umenielewa?” “Nimeelewa mama.” “Sasa kwa taarifa yako tu, vita yako ndio imeanza. Kama ulifikiri kufika hapa ndio utamaliza, basi ulikosea Nanaa. Umama ni kazi kuliko kazi yeyote ile hapa duniani. Hivyo unavyoumia kwa Oliva kwamba anaanza kwenye machafuko, huwa haviishi na wala havitakuwa na nafuu. Badala ya kulia, unajiweka na kusimama kwenye nafasi yako. Ukijua wewe unaye Simba wa kabila la Yuda. Atakupigania, hutashindwa. Faida yake ni moja tu, humtegemei shetani na kazi zake, zenye mateso mengi. Mara kwa mganga wa kienyeji au hata kutizama mambo kwa jicho la wengine wanavyotazama mambo. Wewe kimbilio lako ni magoti. Kumtwika Yesu fedheha zako zote. Mlilie Mungu katika kila hali. Mwambie hofu yako. Amuru mambo yasiyoonekana katika ulimwengu wa Roho, yadhihirike katika ulimwengu wa mwili. Niliwaambia wewe na Geb, hamtasimama, kama hamtamtanguliza Mungu. Umeona sasa?” Mama G aliwaangalia wote.

          “Mungu pekee awe kimbilio lenu Nanaa na Geb, ndipo mtaweza kusimama. Mtajaribiwa sana, lakini mkimtanguliza Mungu mtashinda tu. Unanisikia?” “Nakusikia mama, lakini mimi nataka Liv abarikiwe hiyo jumapili kama ulivyopanga mama! Hata kama watu wasipokuja, sisi wenyewe tutatosha. Na kaka James.” “Safi sana. Hayo ndiyo mambo. Maisha yetu hayasimami sababu za hila za ibilisi. Tunasonga mbele. Nitazungumza na mchungaji. Sasa hii itakuwa tofauti. Si Nanaa unaniruhusu kufanya kile ninachotaka na Oliva.” “Chochote mama yangu. Wewe fanya kile unachojua kitampendeza Mungu. Si ni sawa Geb?” Nanaa akamgeukia Geb. “Sawa.” Geb akakubali.

“Basi. Nashukuru. Sasa huyu shuguli yake nataka iwe tofauti. Tumuombee baraka, kwa kuwabariki watoto wengine. Geb utaenda kituo kile cha watoto yatima kilichopo pale Mwenge. Nataka ukazungumze na uongozi. Waombe wakuandikie mahitaji yao yote. Hata kama ni ujenzi wa kitu, wewe waambie waandike tu. Tukishapata mahitaji yao yote. Tutakuja kukaa hapa kama familia. Tutachagua vitu tutakavyoweza kufanya sasa hivi. Kabla ya jumapili, tutawapelekea. Ndipo tukamuombee Oliva baraka kwa Mungu siku ya jumapili halafu tutaenda kula chakula na hao watoto yatima hiyo siku ya jumapili.” Nanaa akaanza kucheka.  

“Ndio maana nakupenda mama yangu.” Wakacheka kidogo. “Halafu mahitaji mengine yatakayo baki, tutamwamini tena Mungu kukamilishia hicho kituo, wakati tunaenda kutoa sadaka ya shukurani wakati hao wakina kaka wakishazaliwa. Au unasemaje Danny?” “Maana nilishaanza kuona wivu!” Danny akajibu. Wakacheka. “Ni wazo zuri sana mama. Tumekuwa tukitapanya mapesa huko kwenye birthday zao hawa! Kwanza hata wenyewe hawaelewi! Bora hata umri wa Fili huo.” Danny akaongeza.

“Na kama tukiweza kumaliza mahitaji yote, sasa kwa wanangu wakizaliwa tutawapelekea nini?” Grace akahoji akionyesha wasiwasi kidogo. Gafla wazo la mama G likawa lamaana kila mtu analitaka. “Grace, hao watoto ni yatima. Wanaishi kwa kusaidiwa tu na watu. Hawawezi kuishiwa mahitaji yao kwa msaada wa mara moja tu. Hata kula yao ni ya msaada. Sidhani kama wanawadhamini wakutosha kukidhi mahitaji yao. Usiwe na wasiwasi. Huu ni mwanzo tu. Na kila jambo tujue Mungu anatuletea kwa wakati. Tushirikiane sasa hivi tukamilishe hili la hiyo jumapili na tuendelee kufanya ili kuwafundisha Fili, Oliva na wadogo zao, kujali yatima.” Danny na Grace wakaridhika. 

“Mama! Kibinafsi mimi nakushukuru kwa kweli. Sikuwahi kujiona nina upungufu wa wazazi tokea nimekuwa na wewe. Umeniongoza vizuri sana. Nakiri bila wewe, pengine nisingekuwa hapa. Sijui kama unakumbuka wakati nataka kuacha chuo ili nitafute kazi nimtunze mwenyewe Grace?” “Nakumbuka Danny mwanangu.” “Lakini ukataka nivumilie, huku ukinihudumia kwa jasho lako, kama ulivyofanya kwa Geb, mpaka nikamaliza shule yangu. Ni kweli upendo wako kwangu ni kama wa Geb tu. Kwa muda mfupi nilichanganyikiwa. Zinda akanichanganya kabisa. Lakini nimekaa hapa sasa hivi, ni kama Mungu amenirudisha hatua kwa hatua. Akanionyesha jinsi ulivyohangaika na mimi bila kuchoka. Tena nikiwa mkorofi kuliko hata watoto wako ulio wazaa.” Grace na Geb wakacheka. “Kweli! Si mimi mwenyewe najijua. Nakushukuru mama yangu. Asante kunituliza.” Danny alisikika akiwa ametulia kabisa.

“Basi na mimi namshukuru Mungu kwa hilo. Haya, njooni wote tushikane mikono tuombe.” Wakasogea wakashikana mikono mama G akaongoza maombi. Alianza kwa kutubu. Aliwatakasa wanae kwa majina. Kila mmoja wao akiowaombea toba na utakaso. Akaomba amani iliyokuwepo kati yao, iendelee kudumu. Akabariki kazi za mikono yao kila mmoja wao. Akamuombea Fili, Oliva na watoto walioko tumboni mwa Grace na wengine watakao kuja. Akaomba hekima  juu yao yakupambana na changamoto zote zitakazo wakabili maishani. Kisha akaomba ulinzi juu yao. Wakamaliza wote wakiwa wametulia.

~~~~~~~~~~~~~

Baada tu ya maombi Geb akamgusa Nanaa. “Naomba twende tukazungumze.” Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Naomba Nanaa anyonyeshe kwanza.” Wakacheka. “Mara moja tu, tutarudi!” “Hapana Geb. Mimi nawajua nyinyi. Hamtarudi leo. Huyu mtoto lazima ale ndio arudi kulala, hawezi kusubiri.” Mpaka Grace akacheka, Geb akatingisha kichwa. “Mama anakosa imani na Geb!” Danny akachokoza. “Mimi nawajua hawa. Watakuachia mtoto hapa kwa ahadi ya kurudi baada ya muda mfupi sana. Tena Geb ndio ataingia hapa anakimbiakimbia akijifanya anaharaka, anataka akazungumze kitu kwa muda mfupi tu na Nanaa. Basi wapandishe hizo ngazi! Hutakaa ukawaona tena. Na yeye mtoto wa watu asivyo na makuu, analala kimya na njaa yake. Wazazi hawa utawasikia wanacheka juu.” Geb alimtizama mama yake kama haamini.

“Mama!” Geb akashangaa. “Mama nini! Mwache mwenzio anyonyeshe.” “Basi na huko kazini ndio hivyo hivyo. Utaagwa. Anakwambia anarudi baada ya muda mfupi sana. Unamkumbusha watu watakaokuja hapo ofisini. Tena walioweka miahadi ya kumuona labda hata siku tano kabla. Anakwambia sitakawia. Ujue usahau. Na utafute kitu cha kuzungumza na hao wageni wake. Harudi Geb. Ukipiga simu huku nyumbani kumtafuta, unaambiwa yupo chumbani kwake, simu kazima. Yaani hapo ndio ujue ananifikishia ujumbe kuwa nimalizane na watu wake mimi mwenyewe. Wenye kukasirika wanakasirika, wanaona wamepuuzwa. Wenye uvumilivu wanaomba miahadi mingine tena ili wajaribu kama watakuja kuonana na Geb mwenyewe.” Geb akarudi kukaa huku akitabasamu bila kukanusha. 

“Basi nanyonyesha kwanza mama!” “Au twende naye juu. Tuongee wakati unanyonyesha.” Geb akatoa wazo. “Hapana Geb. Wewe tulia hapo kwenye kochi, mwenzio akanyonyeshe hapo chumbani kwangu. Mtoto akishiba nyinyi nendeni kokote mnakotaka, hakuna hata atakaye wasumbua. Haya Nanaa nyanyuka nenda.” Danny alizidi kucheka.

“Kwani wewe mama unahisi mtoto anaweza kwenda kulazwa bila kula?” “Yaani Danny kwa kupenda kushabikia mambo!” Mkewe alimjua. “Si nimeuliza tu!?” Danny alizidi kucheka.  “Hapana Danny. Wewe nyamaza tu mume wangu.” “Sawa. Lakini kwani wewe mama unahisije?” Kila mtu alianza kucheka upyaa. “Mwanangu Danny, mimi huwa nashinda humu ndani na huyu mtoto. Acha tu alishwe sasa hivi, nimuogeshe ndio alale. Maana wakati mwingine kama baba yake akirudi hapa mchana, basi mwanae ndio aandike maumivu. Utasikia ‘Nanaa, njoo mara moja.’ Hapo yeye kashapandisha ngazi yupo juu kule. Basi bibi huyu naye akishasikia jina lake limetajwa, popote ulipo, anakuletea mtoto, au utamsikia anakwambia ‘Nimemuacha Liv hapo kitandani. Narudi sasa hivi.’ Basi huyo mtoto atalala hapo, kuja kukumbukwa na mama yake ni baada ya baba mtu kuondoka. Utafikiri alilishwa ugali kabla ya kuachwa.” Danny na Grace walikuwa wanacheka, Nanaa akajificha uso.

“Ni mazungumzo ya muda mfupi tu!” “Hapana Geb. Acha hayo mazungumzo yasubiri. Haya Nanaa, chukua mtoto, nenda kanyonyeshe.” Nanaa akasimama kwenda kumchukua mtoto. “Labda ungempa muda kabisa wakutulia humo ndani.” Grace akamfinya mumewe. “Ukoje Danny wewe!?” “Nazungumzia ushibaji wa mtoto Grace mke wangu! Si unajua mawazo yakiwa yamegawanyika! Nanaa anaweza asinyonyeshe vizuri.” Nanaa akakimbilia chumbani na mwanae.

“Wala usiwe na wasiwasi. Atashiba tu mjukuu wangu. Hivi ninavyohangaika kumnywesha supu huyo Nanaa, mbona atatulia hapo mpaka mtoto ashibe. Nikiridhika ndio ataenda kwenye hayo mazungumzo.” “Mama bwana!” Danny alizidi kuchochea. Angalau utani ukazidi. Wakaanza kucheka.

  ~~~~~~~~~~~~~

Mara James akaingia akionekana amepaniki haswa. Akakuta pale ndani kumejaa vicheko, asielewe. “Karibu James mwanangu.” “Asante mama.” Akakaa. Akamwangalia Danny, Geb na Grace akaona wametulia na tabasamu usoni. “Mnacheka nini?” James akauliza. “Danny anamchokoza Geb na Nanaa.” “Grace naye hana siri!?” “Umezidi wewe.” “Sio wewe uliyekuwa ukitusimulia habari za Geb hapa? Kwamba jamaa ofisi kahamishia nyumbani? Mimi kosa langu kuuliza maswali?” “Mchochezi Danny. Anataka kukuza visa.” Wakaendelea kubishana Danny na mkewe.

“Subirini kwanza. Hivi nyinyi mmesikia yanayoendelea kwenye kundi?” “Kuna mapya mbali ya yale ya Zinda?” Danny naye akauliza. “Kwa hiyo mmesikia kila kitu!?” James akauliza kwa kushangaa. “Si nilimtoa?” “Bwana si padogo humo ndani. Liz amemrudisha. Wamejaza kurasa za matusi. Nahisi kama nimevuliwa nguo zote.” Wote wakacheka na kumshangaza James.

“Wameamua kuungana?” Danny akauliza huku akicheka. “Yaani mpaka sasa hivi hapa, wanapokezana kuandika. Hakuna walichobakiza naona wanarudia rudia.” James akaongea. “Naombeni msimwambie Nanaa tafadhali. Itamchanganya sana.”

“Mbona anajua! Ameingia ndani sasa hivi kwenda kunyonyesha.” Mama G akajibu bila wasiwasi. “Mbona sasa nyinyi hamna paniki yeyote!?” James akauliza akiwa haelewi.

“Tumemuachia Mungu.” James akakunja uso huku akimwangalia Danny. “Kweli tena James. Wewe jiulize tu mwenyewe, shutuma zote anazokushutumu Zinda ni kweli?” “Hata kidogo Danny! Na wewe ni shahidi. Sijamuuza Nanaa kwa Geb mimi sababu ya pesa. Kwanza sikuwa hata nikijua kinachoendelea wakati ule wa mambo ya Marangu. Nilimsindikiza Zinda kununua vitu bila hila nikitaka Nanaa mwenyewe aamue japo nilijua wazi Nanaa hawezi kumkubali Zinda sababu ya pombe. Nanaa hapendi kabisa harufu ya pombe. Na ndio maana kama utakumbuka wakati tumemsindikiza Zinda, nilimsihi sana asubiri kwanza, asinunue kitu chochote mpaka azungumze na Nanaa. Unakumbuka Danny?”

“Basi mimi nilijua na wewe hicho kipengele umesahau. Nikajiuliza kwa nini pale baa hukumkumbusha wakati analalamika na kukutukana?” “Nilikuwa nimeshakasirika, maneno hayatoki tena. Nikaona heri nimrushie tu ngumi ya mdomo anyamaze.” James alijibu wakacheka. 

“Ujue siku ile pale kwa sonara ulipompa lile wazo, kuwa asinunue mpaka azungumze na Nanaa, nilitaka kukuuliza pale pale, kwa nini, lakini unakumbuka Zinda akakubishia kwa haraka sana wala hakutaka kukusikiliza?” “Tena alikuwa mkali haswa! Nikaamua ninyamaze nimwache na ubishi wake. Leo analaumu kwamba tulimuacha aingie garama bure wakati nilikuwa na mpango wakumuuza kwa Geb! Mjinga sana Zinda.” James akaongeza kwa hasira kidogo. “Kwani pesa Geb kapata leo? Tangia nampiga Geb marufuku kuwa karibu na Nanaa, Geb si alikuwa na pesa! Wewe, Malii na Zinda wote mlijua jinsi nilivyomfukuza Geb na kumpa onyo kutokuwa karibu na Nanaa.” Grace akamgeukia mumewe.

“Sasa nini Grace?” “Kwa nini hukuniambia?” “Kweli mke wangu? Ulitaka nije kukwambia kuwa James ameniambia amempa ONYO kaka yako asimuone mwanamke pekee ambaye wote tunajua anampenda?” Grace akanyamaza. “Nilijua ingekuumiza tu. Tena baada ya wote kumkosea Nanaa! Niliona wewe na mama mlivyoumia wakati Nanaa mgonjwa. Nilijua ningekwambia wewe, na wewe ungemwambia mama, mkazidi kuumia. Zaidi mama ambaye alikuwa akimuomba Geb msamaha kila siku kwa kusababisha kukimbiwa na Nanaa. Nisingeweza kukwambia. Ingekuwa ni kama nawaongezea hukumu.” Grace akaridhika. “Asante kutufikiria Danny. Kweli ingetuongezea hukumu tu.” Danny akatoa tabasamu kwa mkewe.

“Sasa ndio najiuliza, hayo yote Zinda amesahau kweli au ni hasira tu?” James bado hakuwa ameelewa. “Nisikilize James mwanangu. Ndio maana mimi nilifundisha wanangu kunyamaza wakati umekasirika. Ukiwa na hasira unaweza kuongea chochote kile. Zinda amekasirika. Akija kutulia, atakuja kukumbuka hayo yote, na atajua amekosea. Kumjibu sasa hivi, hakutasaidia hata kidogo. Mpeni muda wa kupokea taarifa za Nanaa kuzaa na Geb. Mpeni muda tu. Atakuja kuzikubali baadaye. Lakini kwa wakati huu, mwacheni.” “Sasa na Liz je!? Maana naye analalamika sana. Ananiita majina mabaya kweli huko mtandaoni likiwepo Msaliti!” James akaongeza akisikika kuumia.

“Shauku ya Liz ilikuwa ni kuzaa na Geb tokea zamani. Na aliniambia alishamuomba Geb kama hana mpango wa kumuoa basi angalau wazae naye mtoto hata mmoja tu. Geb hakusema ndiyo au hapana. Si ni kweli?” Grace akamuuliza Geb. Geb akanyamaza. “We Geb?” Dada yake akamuuliza tena kwa msisitizo. “Ni kweli.” Geb akajibu kifupi tu. “Aaaaah! Basi ndio maana anasema hivyo huko kwenye group!” James akadakia akikumbuka shutuma za mtandaoni. Wakataka kumuuliza amesema nini, lakini wakaona ni heri wanyamaze tu. 

“Nashauri mtulie.” Mama G akasisitiza ushauri wake. “Nisijaribu kumtafuta Liz ili nizungumze naye?” James akauliza. “Naomba mimi nikwambie James.” Grace akawahi kabla ya mama yake. “Japokuwa sijasikiliza rikodi alizotuma huko kwenye kundi letu au hatujasoma jumbe zake, lakini mimi namfahamu sana Liz. Nafahamu jinsi anavyojithamini mwili wake. Na mnajua kwa Liz, hakuna mwanamke bora na wa thamani kama yeye mwenyewe. Kwa hiyo naweza kuhisi chuki yake ipo wapi. Kitendo cha Geb kukataa kuzaa na yeye, na kujua wazi ameamua kuzaa na Nanaa! Tena watu wote tunajua kuwa Geb hakukosea. Maana wote sisi tunajua tabia ya Geb. Kufikiria, na kupanga mambo yake kabla hajatenda jambo lolote. Wote tunajua huwa halali na mwanamke kwa kukosea, na halali na mwanamke yeyote bila kinga. Kwa yeye kuzaa na Nanaa na si Liz, watu wote wanajua Geb alikusudia. Na ni kama kumdhalilisha Liz kwa hali ya juu wakati watu wote tunajua Liz alishambembeleza sana Geb azae naye, lakini japokuwa Geb hakusema hapana, minong’ono ilizuka kuwa Geb alikataa. Hata Danny alisikia. Si ni kweli Danny?” Grace akauliza akitaka uungwaji mkono wa mumewe.

“Mimi nilikuta wanamcheka. Sijui nani alifikisha hizo habari kwa kina Goz na Malii. Wakawa wanamcheka waziwazi kwamba anataka urithi. Lakini Liz akasema ni wivu tu, yeye anataka mbegu ya Geb kwenye maisha yake. Akasema anataka kuzaa mtoto mwenye akili nzuri. Kwa kuwa yeye anaakili na Geb anaakili sana, kwa hiyo anauhakika akizaa mtoto na Geb, atakuwa tishio ulimwenguni. Goz akawa anamcheka. Liz akaondoka kwa hasira, ndio mimi nikauliza kulikoni. Ndio Malii akanisimulia kuwa Liz anamkataa Goz kwa kuwa hana akili kama za Geb, anamtaka Geb. Sasa Goz akawa anamcheka Liz kuwa hata afanyaje Geb anapita tu kwake, ni heri amkubali yeye. Yeye atamuoa na kumthamini.” Geb alibaki kimya.

“Si umesikia James?” Grace akauliza. “Mimi hilo mbona najua? Goz mwenyewe alishaniambia kuwa anamtaka Liz, lakini Liz anamng’ang’ania Geb sababu ya pesa. Kwa hiyo najua. Hata sasa hivi huko kwenye kundi, Goz anatuma picha za watu wanaocheka mpaka machozi.” James alijibu nakufanya wacheke. “Gozibeth ni chizi! Anafanya makusudi tu kuwacheka Liz na Zinda.” Danny aliongeza. “Ndio kazi yake hapo. Liz akituma tu ujumbe, na yeye anatuma katuni na ile video ya yule mtoto mdogo anayecheka sanaaaa.” Wakazidi kucheka.

“Sasa kwa hali kama hiyo, Liz akiwa na hasira hivyo, unafikiri utamwambia nini akaelewa? Liz hajawahi na wala hafikirii kushindwa. Kwa Nanaa kufanikiwa kuzaa na Geb, wewe tayari ni adui mkubwa sana kwa Liz. Nashauri umwache tu atulie. Wote wanahitaji muda wakuingiza hizo habari akilini. Watatulia tu kama mama alivyosema.” Grace akamaliza.

“Sasa hali ya Nanaa?” Akili ya James ikarudi kwa dada yake. “Mzimaa. Katulia. Hivi hapa anataka mwanae akabarikiwe jumapili.” James akacheka. “Kweli nimekuza!” James akajisifia. “Mimi nilikuwa nakuja kumtuliza!” “Ametulia tuli. Na wewe tulia tu. Wala usimuonyeshe wasiwasi. Mtie tu moyo na msaidie mpaka afunge ndoa yake.”  “Nahangaikia hizo taratibu mama. Hivi sikutaka ajue ugumu ninaopitia ili tu kuweka mazingira ya mahari yake kupokelewa huko nyumbani.” “Ni nini tena!?” Mama G akauliza.

“Daah! Naomba nisiongee mama yangu. Lakini naomba mniombee. Hili jambo sio rahisi kama nilivyodhani. Lakini Mungu yupo nami. Atanisaidia tu. Sijawahi kutulia tokea Nanaa analetwa nyumbani kutoka hospitalini akiwa ametoka kuzaliwa na mama yake amefariki, mpaka leo! Na hili najua nitalikamilisha tu.” Hata uso wa James ulishabadilika akaonekana kuna kinachoendelea.

“Unajua tokea mama yake amekuja pale nyumbani kwetu akiwa mjamzito, mpaka yule mama anapelekwa hospitalini kujifungua, alikuwa akilia sana! Sitamsahau. Halafu kalikuwa kabinti kadogo sana. Kila nikimfikiria najiuliza sijui alikuwa akiogopa! Au kwa kuwa alikataliwa na mwanaume aliyempa mimba! Au sijui kwa kuwa alifukuzwa nyumbani kwao! Hakika sijui! Lakini sura yake akiwa analia akiwa amekaa nje peke yake, haijawahi kunitoka mpaka leo. Na kila nikimkumbuka, ndivyo ninavyojitahidi kumsaidia Nanaa, asipitie kule alikopita mama yake. Sitaki hata awe na uchungu au awe na mawazo huyu mtoto. Wakati mwingine nahisi nakuwa over protective kwake. Sitaki hata mtu amuudhi kidogo.” James alikuwa akiongea huku akionekana kufikiria.

“Mungu atakusaidia na kukubariki James. Umebeba jukumu la Nanaa ukiwa bado mdogo sana. Mungu hatakupungukia kwa hilo. Kila ulichofanya kwa Nanaa, ujue umemkopesha Mungu.” “Amina mama. Kwa hiyo msione kimya. Napambana kupata taratibu za mahari. Nikikamilisha tu, nitawajulisha. Sitaki waje wapate sababu ya kunilaumu au kumlaumu Nanaa. Naomba tusubiri ili tufuate hatua zote.” “Usijali James. Mimi nitasubiri tu. Na ninakuahidi nitamuoa Nanaa, na nitamtunza vizuri tu. Hutasikia tatizo lolote.” Geb akaongeza. “Nashukuru Geb. Asante sana.” Wakati wanamalizia mazungumzo yao tu, Nanaa akatoka.

“Kaka!” Nanaa akaonyesha kufurahi. “Shikamoo.” “Marahaba. Vipi mtoto?” “Alikuwa anakula. Naona anarembua tu. Anataka kulala.” Akamkabidhi kaka yake. “Anakua kama uyoga! Unamlisha nini?” “Namkazania kunyonya.” Mama G akadaikia wote wakacheka, Grace akatingisha kichwa. “Mama wewe!” “Kumbe uongo? Mimi ndiye namkazania kunyonyeshwa. Mambo ya huyo mtoto yote, niulize mimi James mwanangu.” James akacheka. “Na mimi nimeona mama.” “Tena umbile kachukua langu kabisa.” “Mama wewe! Sio mama yake?” “Hata kidogo! Hapo Nanaa katupa rangi tu. Mimi nina damu kali kweli! Basi na yeye huyo Oliva akija kuzaa, atazaa watoto kama mimi!” Grace alikuwa akimwangalia mama yake hammalizi. Kila mtu alikuwa akicheka.

“Sasa Geb itabidi apandishe huo ukuta. Maana kama huyo mtoto atakuwa kama mke wangu! Jasho litawatoka.” Danny aliongeza kwa kumsifia mkewe. “Wala si ukuta huo wa kazi ya mikono ya mwanadamu. Huyo nitamuwekea ukuta wa kiroho. Maisha yake naenda kuyatoa wakfu kwa Bwana! Akaombewe. Nguvu ya Mungu imzingire kila aendapo. Nataka…” “Mama hamalizagi na mipango ya huyo mtoto! Akianza hapo, tutakesha. Naombeni tule jamani.” Grace alianza kuhangaika kusimama. “Wivu tu!” Mama G akasimama na kwenda kumpa mkono Grace ili asimame. “Hivyo ulivyokonda mama yangu! Nitakuumiza tu.” “Nakuhurumia. Nipe mkono nikusaidie kusimama.” Mama G akanyoosha mkono ili amsaidie Grace kusimama. Danny akasimama, akamsadia mkewe kusimama. Wakacheka.

Kikao kikahamia mezani. Wakaanza kucheka. Hakuna aliyekumbuka tena kashfa zinazowakabili. Danny aliendelea kuwachekesha, mpaka James alipotaka kuaga. “Oliva anabarikiwa, kaka.” “Nimeambiwa. Hongera.” Nanaa akacheka. “Si utakuwepo?” Nanaa akauliza. “Lazima. Siwezi kukosa.” Nanaa akafurahi. “Lakini tutaenda kuwabariki watoto yatima kwanza siku ya jumamosi, ndipo jumapili tunafanya ibada.” Nanaa akamuelezea kaka yake mpango mzima. “Mpango mzuri sana. Basi na mimi  nitataka kushiriki.” James akasisitiza.

“Mimi nashauri hivi. Sijui kama itakuwa ni sawa. Geb akishapata hayo mahitaji yote. Danny aandae tangazo dogo tu la mwaliko. Litakaloeleza ratiba nzima kuanzia jumamosi huko kituo cha watoto yatima, mpaka jumapili. Alitume hilo tangazo kwa marafiki wote, pamoja na mahitaji yote. Atakayetaka kuchangia, ajibu palepale kwenye kundi. Ili kushirikisha watu wote hizo baraka. Vitakavyo baki vyote, itakuwa sisi. Danny na Grace nyinyi iwe chakula. Mtanunua vyakula kwa ajili ya kituo. Kadiri muwezavyo. Mahitaji mengine ni Geb na Nanaa. Na wengine tutachagua hapo. Au mnaonaje?” “Mbona mimi nilishafurahia hilo wazo kabla hujauliza!” James alifanya wacheke. Wakakubaliana hivyo.

Ubarikio wa Oliva Magesa.

Geb alifanya kama alivyoshauriwa na mama yake. Akakusanya mahitaji yote kutoka kwenye hiko kituo cha watoto yatima. Wakakusanyika tena kama familia. Wakayapitia, ndipo Danny naye akaamua kufanya kama alivyoshauriwa na mama G. Akayatuma kwanza kundini kabla wao hawajachagua, ili kusiwe na kulalamika tena. Alituma kwenye kundi lile lile walilotukanwa, bila kujibu shutuma. Tokea watukanwe ndio Danny anarudi na ujumbe wa kumshukuru Mungu na kuwataarifu juu ya kubarikiwa kwa mtoto wa Geb na Nanaa. Alieleza mpango mzima wa kubariki kituo cha watoto yatima, na kuwaambia na wao wanakaribishwa. Atakayependa kuungana nao, basi achague kitu hapo na aandike hapo hapo, ili wasirudie kununua vitu vilevile.

Hapo hapo  Zinda na Liz wakatoka/left kwenye lile kundi. Danny akatulia tu, hakujibu kitu. Lakini wakashangaa kuona watu baadhi wanajibu na kuchagua vitu vya kuleta siku hiyo. Danny akashukuru na kuwataarifu muda wa kukutana siku hiyo ya jumamosi kwenye kituo hicho cha watoto yatima, sehemu ya kuegesha magari kabla hawajaonana na uongozi. Vitu vilivyobaki kina Magesa wakamaliza wao wenyewe.

Jumamosi hiyo walipokutanika kwenye kituo hicho cha watoto yatima, mama G akaomba waombe kwanza. Wakashangaa maombi ya mama yule ni juu ya watoto hao yatima na watoto wao tu. Akawaombea baraka watoto wao wote. Kisha ndio akasema waingie ndani. Hakutaka kuuliza mambo yaliyopita, na wala kina Danny hawakuweka mazingira yakuzungumzia shutuma za Zinda na Liz. Kwa hiyo hapakuwa na hayo mazungumzo kabisa.

Watu walifanya kilichowapeleka pale, na kesho yake baada ya ibada, Oliva alipobarikiwa akiwa amesimamiwa na bibi yake, walirudi kunywa na kula na watoto hao yatima. Napo pia walishangaa baadhi ya marafiki zao waliwaunga mkono. Walifika kanisani na kwenye chakula cha mchana. Hilo nalo wakafanikiwa kulimaliza. Lakini wazi kulikuwa na ukimya wa namna yake. Kama kuwindana hivi! Hakuna kutizamana machoni. Hapakuwa na vicheko vingi, na walifika wachache. Mama G aliwashukuru walioweza kufika, wakaagana.

 ~~~~~~~~~~~~~

-       Hawa watu walikuwa ni marafiki wa muda mrefu sana. Wamekua pamoja, wakageuka kuwa kama ndugu. Leo kumeingia tatizo ambalo kwa mara ya kwanza hawajui watalitatua vipi katikati ya jambo ambalo baadhi yao waliliona ni la heri.

-       Kwa Mara ya kwanza James anamuona dada yake akiwa na furaha nakupokelewa kwenye familia inayomjali. Anamjua Nanaa. Anajua wazi wale ndio watu ambao Nanaa angewahitaji maishani. Alimuona jinsi mdogo wake akihangaika tokea anazaliwa. Leo amempata Geb, lakini kumeingia dosari kubwa sana. Tena akiwa ametupiwa shutuma zinazo fanana na kweli!

-       Zinda akiwa ndiye kama ndugu wa Karibu wa Danny, leo ndio anampa maneno machungu ya kiasi kile. Kejeli na matusi yaliyogusa hisia za Danny. Zinda anamuhesabu ni msaliti kwake. Amesimama na Geb wala si yeye. Amempa ujumbe wa vitisho kuwafikishia kina Magesa. Ameahidi kutokukubali na litakalo wapata wasimtafute.

-Nini Zinda atafanya?

-Nini kitaendelea kwa vijana hao waliokuwa pamoja?

Mama G aliwahusia hawa wapenzi wawili, {Geb & Nanaa}, juu ya vita inayo wakabili mbeleni. Aliwasihi wamtangulize Mungu katika kila jambo, lakini mapenzi yamenoga. Hakuna anayetosheka na mwenzake. Si mchana, si usiku, penzi tamu haswaaaa!

-       Je, wataweza kuendelea kusimama katika kila kombora litakalotupwa kwao wakiwa na msingi imara wa kitandani tu?

Wote wanaujua mchezo wa kitandani vilivyo. Tena hakuna asiyetosheka na mwenzie wawapo kitandani. Ndio maana kazi hazifanyiki tena kwa Geb, mikono yake inataka kushika mwili wa Nanaa wakati wote! Hakuna sehemu nimeona wakiomba pamoja kama walivyoshauriwa zaidi ya penzi.

-       Nini kitaendelea kati ya penzi hilo zito la Nanaa & Geb?

 

USIKOSE MUENDELEZO. Mambo ndio kwanzaaaa Yanaanza.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment