Alisimama
baada yakumuona Nanaa. “Umependeza sana Nanaa.” Nanaa akacheka. “Asante. Na
wewe amependeza kama kawaida yako. Hujikosei!” Zac akacheka. “Nilirudi
nyumbani, nikajiandaa rasmi kukutana na wewe.” Nanaa alizidi kucheka. “Kwa hiyo
hapo umevaa hivyo kwa ajili yangu?” “Unafanya mchezo nini? Nimevunja kabati
kama mtoto wa kike!” Nanaa akazidi kucheka. “Basi umepatia.” “Afadhali kama
juhudi zangu sio bure.” Wakatizamana kwa muda kama wasio amini.
“Nina hamu na wewe Nanaa!” Zac akaanza. “Naomba unisamehe
mpenzi wangu. Nilikosa.” Nanaa alibaki kimya kwa muda, akabadili mazungumzo.
“Umerudi lini?” “Hata sijamaliza week. Nimerudi kwa ahadi ya kazi. Baba
aliniunganishia kwenye kampuni moja ya mambo ya simu. Nimefanya usahili huko,
wameonekana kuvutiwa na mimi, wamesema watanipigia simu. Lakini ikitokea
sijabahatisha, nataka kurudi shule, nimalize kabisa mpaka PHD. Kwanza nani
alikwambia kama sipo nchini?” Nanaa akatabasamu. “Nilikutana na Tondi, yule
rafiki yako. Ilikuwa maeneo ya Posta Mpya, akawa ananilaumu, eti
nilikuchanganya mpaka ukakimbia nchi.” Wote wakacheka.
“Lakini hakukosea. Niliingiwa na chuki. Nikajichukia sana kwa
kitendo nilichokifanya. Unajua japokuwa sikuwa nimekutambulisha nyumbani,
lakini kila mtu alikuwa akikufahamu na wakajua lazima nikuoe. Tena niliwaambia
tutafunga ndoa ukiwa mwaka wa pili. Kwa hiyo kila mtu alijua naoa mwaka ule
unaofuata baada ya kumaliza. Sasa kuja kuharibu, nikaona heri nikaanze
kwingine. Nilijilaumu sana.” Nanaa akanyamaza kwa muda kama anayefikiria.
Alishamuagizia kinywaji alichojua Nanaa anakipenda. Aliagiza
mara alipopokea ujumbe kutoka kwa Nanaa akimtaarifu kuwa Geb amefika nyumbani,
avute subira kidogo, ataungana naye muda si mrefu. Yeye alikuwa amefika hapo
lisaa kabla ya Nanaa kufika hapo. “Nanaa!” “Kwa
nini ulinisaliti, Zac?” Nanaa akauliza huku machozi yakianza kumtoka. “Uliwezaje kusahau ahadi zote na mipango yote
tuliyowekeana mimi na wewe!? Ni nini nilikuudhi au nilikunyima ukakipata kwake?
Ulikuwa na mahusiano naye kwa muda gani? Mara ngapi ulilala naye kabla
sijawafumania? Mliendelea naye baada yakuwafumania? Alikuwa mzuri kitandani
kuliko mimi? Ilikuaje Zac?” Nanaa akajikuta yale maswali aliyokuwa
akijiuliza siku zote juu ya Zac, yanatoka bila kituo.
“Uliwezaje kunisaliti ungali ulijua nilikuwa nikikuhitaji
kiasi kile? Uliwezaje kunionyesha mapenzi yote yale, halafu ukaweza kulala na
msichana mwingine? Na yeye ulikuwa ukimfanyia kama ulivyokuwa ukinifanyia mimi
kitandani? Na yeye ulimwambia unampenda? Hivi uliwezaje hata kudiriki kumvulia
nguo msichana mwingine ambaye sio mimi!? Tena akijua mimi nipo! Halafu na yeye
alikuwa anamchumba wake! Akitoka kwako, anarudi na kwa mpenzi wake, halafu
mnaniacha mimi peke yangu! Uliwezaje kunisaliti Zac? Uliwezaje kusaliti
makubaliano yote yale? Au yalikuwa ni maneno ya uongo kwangu? Pengine ndiyo
maneno uliyozoea kuwaambia wasichana wote!” Nanaa hakuwa akisubiri
ajibiwe.
Aliendelea kuuliza tu. “Hivi
unakumbuka kuwa kile kitanda ulichokuwa ukilala na mimi, ndicho ulichokuwa
umelala na yule msichana!? Ni nani uliyekuwa ukifanya naye mapenzi wakati wote
ulipokuwa na mimi? Uliona upo na Nanaa kweli au ilikulazimu unifikirie mimi
ndiye yule msichana uliyekuwa ukitembea naye kila mahali huku ukiniaminisha ni
mwanafunzi mwenzako kama wanafunzi wengine tu? Uliiona sura yangu wakati
ukifanya mapenzi na mimi au ni ya yule msicha wako? Eti Zac?”
“Kwa nini ulinidanganya na kunivua nguo zangu
bila penzi la kweli? Umenisababishia ugonjwa mkubwa sana maishani. Nashindwa
kupenda na kuamini mtu yeyote! Umenisababisha kutupa mbali penzi la kweli
lililokuwa limekuja kwangu mara moja katika maisha yangu, sababu ulivunja
uwaminifu wako kwangu. Wanaume wote nawaona waongo! Tena mbaya zaidi ulinitenda
nikiwa nimekusimulia usaliti niliotendwa na mwanaume niliyekuwa naye kabla yako!
Ukanifurahisha kwa muda mfupi, halafu ukarudia kosa lile lile! Tena na mtu
wakaribu yetu! Uliwezaje kunitendea ubaya wa kiasi kile? Nilikufanyia nini
kibaya cha kunilipa kwa kiasi kile?”
Nanaa alijikuta akitokwa na maswali yaliyosindikizwa na machozi kama mvua.
Alimnyeshea mvua ya machozi na maswali, Zac akabaki amenywea
hajui aanzie wapi kujibu. Hasira za kusalitiwa zilimrejea Nanaa, alilia asijue
atajisaidia vipi. Ukweli hakuwa tayari kupokea jibu hata moja kama alivyodhania
hapo awali. Bado hakutaka kudanganywa na wala hakuwa tayari na ukweli. Zac
alitaka kumfuta machozi, Nanaa akakwepesha uso akasimama mbali zaidi. “Nakutakia maisha mema Zac. Lakini sio na mimi. Tafadhali
usinitafute tena hata kwa ujumbe. Leo ndio nakuaga rasmi. Na kama kweli
ulishawahi hata kunipenda maishani mwako, utaheshimu maamuzi yangu. Kwa heri.”
Nanaa akaondoka bila hata kunywa kinywaji chake. Hakugeuka nyuma, na wala
safari hii Zac hakumfuata.
Tangia mchana wake anakutana na Zac, mpaka muda mfupi kabla ya
kuja hapo, walikuwa wakiwasiliana vizuri sana na Nanaa. Akajua Nanaa amesamehe,
nikwenda kuwekana tu sawa, waanze upya na kuendeleza penzi lao. Lakini Nanaa
alibadilika gafla. Swali la kwanza na la pilli alionekana ametulia. Lakini
kadiri alivyoendelea kuzungumza ndipo Zac alivyozidi kuona jeraha kubwa
alilomsababishia moyoni mwake. Akaamini na kukubali huo ndio mwisho wake na
Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~
Akiwa bado amekaa palepale gizani, akimuonea wivu Zac
anavyofaidi na Nanaa wakati huo, akashangaa mlango unafunguliwa kwa tahadhari.
Kidogo alishituka akijua mwizi. “Mwizi na funguo?” Geb akajiuliza. “Atakuwa
ni Nanaa? Lakini mbona mapema hivyo! Hata nusu saa haijaisha!” Geb akatulia
baada ya mwanga wa nje, ulipoingia kwa kupitia mlango, na kumsaidia kumuonyesha
Nanaa. Geb akashukuru Mungu. Nanaa naye alishukuru baada ya kuingia hapo ndani
na kukuta giza. Akajua Geb alishakula, akaenda kulala. Asubiri nini tena,
wakati walishapoteza mtiririko mzima wa maongezi yao! Alimuonyesha wazi
mahusiano yao yalikufa akabaki Liv tu kati yao.
Akaingia mpaka jikoni kwa tahadhari kama asiyetaka kusumbua
mtu, akakaa chini kabisa sakafuni. Akajikunja hapo na kuanza kulia taratibu.
Nanaa alikuwa mzoefu wa kulia. Tokea mtoto mpaka hapo, hakuwahi kunyimwa na
maisha sababu ya kulia. Maisha yalijua kumpiga, nakumliza bila huruma. Alijua
jinsi ya kutawala sauti yake. Akiamua mtu mwingine asijue kama analia, hutajua.
Ataruhusu kutoa machozi bila sauti, ili kuruhusu uchungu wake moyoni utoke,
angalau baada ya hapo aendelee na maisha mengine.
Geb alijua wazi analia, japo hapakuwa na sauti. Alimuhurumia
Nanaa, asijue ni nini tena kimemsibu. Akaamua kutoka sebuleni, akasogea jikoni
taratibu kama asiyetaka kumshitua. Alipofika tu jikoni, Nanaa akashituka sana.
Akasimama. Ilibidi Geb awashe taa, ndipo akaona vile Nanaa alivyojaa machozi
kila mahali. Nguo hiyo nyeupe ilikuwa chapachapa kwa machozi. “Samahani nimekusumbua.” Nanaa aliongea huku
akijipangusa machozi kwa viganja vyake. “Hata kidogo.” Nanaa alibabaika kidogo
asijue aseme nini. “Samahani sikujua kama umekaa
kwenye makochi. Nilijua umeshakwenda kulala.” Geb akamsogelea.
“Hujanisumbua, Nanaa. Ila sikutaka ukae hapo chini peke yako.” “Liv aliamka hata mara moja?” Tayari akabadili
mazungumzo. Geb akavuta pumzi kwa nguvu akabaki akimtizama.
“Nimechelewa sana?” Nanaa akauliza kwa upole baada ya kuona kimya. “Samahani kwa kuchelewa.” Akarudia kuomba tena
msamaha. Tena safari hii ulikuwa wa unyonge, na machozi juu yake. Geb akazidi
kuumia. “Liv hajaamka Nanaa. Na hujachelewa hata kidogo. Hujamaliza hata dakika
30, tokea uondoke mpaka sasa. Upo sawa?” “Ndiyo. Basi ngoja nikaoge ili niwe
tayari akiamka, nimnyonyeshe moja kwa moja.” Akapita pembeni yake, akaingia
chumbani kwenda kuoga na kubadili nguo. Geb akasimama pale kwa muda, akaamua na
yeye kwenda kuoga angalau kutoa uchovu wa siku nzima.
~~~~~~~~~~~~~
Nanaa alioga, akapanda kitandani, akajilaza pembeni ya
mwanae. Geb alimaliza kuoga, akapitia simu yake, akajibu jumbe mbili tatu
kutoka kwa marafiki zake, akatoka nakukuta nyumba imetulia. Akajua lazima Nanaa
yupo chumbani kwake analia. Akaamua kumfuata chumbani kwake. Akabaki
akimwangalia vile Nanaa alivyomkumbatia Liv kwa mapenzi huku amelala.
Akamuhurumia na kuzidi kuhukumiwa. Nanaa alichoka na mizunguko ya siku nzima,
ukichanganya na kilio, hakuhitaji kubembelezwa na chochote au yeyote ili alale.
Alijikuta hata anashindwa kulia tena, ila kupitiwa na usingizi muda na sekunde
aliyopitisha mkono juu ya mwanae.
Geb alibaki amesimama akimwangalia. Nanaa akashituka akamkuta
bado Geb akiwaangalia. Geb alimuona vile alivyoingiwa na hofu. Alikumbuka vile
Geb alivyomwambia asilale na mtoto kitanda kimoja, amzoeshe kulala kitandani
kwake. Akakaa huku akijaribu kumsogeza Liv mbali kidogo kama kuepusha ushahidi.
“Alikuwa amelala kitandani kwake, nikamtoa hapo ili nijaribu kumbadili diaper
nikidhani ataamka ili anyonye, lakini hajaamka. Nilitaka kumrudisha kitandani
kwake, lakini nimepitiwa na usingizi.” Nanaa akajitetea huku akionyesha uso wa
wasiwasi, kama aliyefumaniwa.
“Naona Liv mwenyewe anapenda hivyo mnavyolala.” “Lakini
naweza kumuweka kitandani kwake tu.” “Hamna shida. Nyinyi laleni tu. Vipi
lakini na wewe?” Nanaa akajiweka vizuri, akakaa. “Anaendelea vizuri. Homa
iliisha kabisa. Alikuwa akitoa kicheko tu kwa bibi yake.” Nanaa akajibu huku
macho yote yakiwa kwa mwanae, mikono ikimpapasa kwa tabasamu zito. Geb akatulia, akijua wazi Nanaa ameelewa
swali ila anakwepa. Ujumbe ukaingia kwenye simu ya Nanaa, ikatoa mlio mara
kadhaa, kulazimisha kupewa na yenyewe kipaumbele. Ilikuwa pembeni kwenye meza.
Wote wakaingalia ile simu.
Kabla hajafikiria chakufanya, ukaingia ujumbe mwingine
uliotoa sauti kama ya mara ya kwanza. Ukaingia ujumbe wa tatu na wa nne.
Ikamlazimu Nanaa kuchukua simu yake. Akaanza kuzisoma zile jumbe taratibu. Zote
zilitoka kwa Zac. Geb aliona machozi yakimtoka mara kadhaa na kuyapangusa,
kisha akataka kujibu, lakini simu ikaingia. Iliita mara kadhaa huku Nanaa
akiangalia sura ya Zac juu ya simu yake. Akafikiri kwa haraka, akapokea huku
akijiandaa kutoka ili akazungumze na simu yake nje.
“Nanaa mpenzi! Nashukuru umepokea simu yangu.” Zac alisikika upande wa
pili. “Naomba subiri kidogo.” Nanaa akaongea kwa
upole huku akitaka kutoka hapo chumbani. “Huna haja
yakutoka. Mimi ndio natakiwa kutoka.” Geb akatoka, akafunga mlango,
akamuacha Nanaa ameduwaa na simu yake sikioni, Zac upande wa pili. “Nanaa!” “Nipo Zac.” Nanaa akajibu kwa utulivu huku
akijirudisha kitandani.
“Naomba nafasi ya kunisikiliza. Tafadhali mpenzi
wangu. Naomba nisikilize tu. Naweza nisiwe na majibu ya maswali yote kwa kina,
lakini nipe nafasi mpenzi. Siwezi kuruhusu mwisho wa machozi kwako. Hata kama
nimeshindwa mengine, basi naomba nipe nafasi ya kutimiza ahadi moja
niliyokuwekea, sitakubali kuyaona machozi yako tena, zaidi mimi nikiwa
nimesababisha. Nipe nafasi. Nisikilize tu. Hata kama tunaagana, tuagane tukiwa
tuna amani. Nakuahidi safari hii tukimaliza mazungumzo yetu, ukanipa masharti,
nitafuata, ila kwa sharti moja tu. Kama tutaagana ukiwa una amani na mimi, na
sivinginevyo.” Nanaa aliendelea kufuta
machozi, huku akisikilizia faraja moyoni.
“Nanaa!”
Kimya. “Tafadhali mpenzi wangu.” “Utaniambia nini Zac, ambacho hujawahi kuniambia? Naogopa
kuumia zaidi.” Nanaa akajibu kwa uchungu na machozi yakizidi
kumbubujika. “Nakuomba nipe nafasi mpenzi. Nisikilize
tu.” Kimya. “Sasa hivi nimeshaondoka hapo.
Lakini kesho siku nzima nitakuwa hapo kwenye huo mgahawa nikikusubiri. Ukipata
nafasi muda wowote, iwe jioni, au asubuhi, jua nipo hapo nikikusubiri. Naomba
urudi tuzungumze.” Nanaa akafikira kidogo. Akakata ile simu na kuizima
kabisa. Geb aliyekuwa nje ya mlango akisikiliza aliposikia kimya, akaondoka kwa
haraka ili kama Nanaa anatoka asimkute pale nje. Akaenda kusimama jikoni.
~~~~~~~~~~~~~
“Kweli jamaa
ameamua kupambana! Akifanikiwa tu kufikia moyo wa Nanaa, ndio nimekwisha na
mwanangu.” Geb aliwaza. Akajua sababu ya Nanaa kumpenda Zac, ni kujua
kumbembeleza kitu alichoshindwa yeye. “Mama yupo sahihi, Nanaa ataondoka au
watamzalisha, nibakie na Oliva wangu nikiteseka.” Geb aliendelea kuwaza.
Geb mtoto wa mama. Kijana mwenye pesa. Mzuri na yeye anavutia kwenye macho ya
wanawake. Amezoea kubembelezwa na sio kubembeleza. Kwa swala la mchezo wa
kitandani, hata yeye alijua ni hodari. Aliujua mchezo wa mapenzi, hata Liz
alizunguka lakini ilimlazimu kurudi kukata kiu kwa Geb. Kila alipokuwa akijishauri
kuachana na Geb moja kwa moja, alikumbuka penzi la Geb, akajikuta akijirudisha
mwenyewe. Liz alishakiri hata kwa mashoga zake, hakuna mwanaume aliyewahi
kuutendea haki mwili wake huo wa thamani, kama Geb.
“Bwana Geb akikuvua nguo, hujuti!” Ndio ilikuwa kauli ya Liz
kwa mashoga zake wakati wote. Japokuwa hakuwahi kufanya naye mapenzi bila
kinga, kama wanaume wengine waliokuwa wakipagawa na kuchanganyikiwa mara Liz
akiwakubali, nakuona kuvaa kondom ni kupoteza ladha nzima ya kimwana huyo,
lakini alifaidi penzi la Geb, alilokuwa akipewa pipi kwenye ganda lake.
Kilichokuwa kikimpagawisha zaidi, ni ule uwezo wa Geb kumfikisha kileleni hata
mara 4, kwenye mchezo mmoja, tena akiwa ametulia, bila heka heka nyingi katika
eneo la tukio.
~~~~~~~~~~~~~
Geb alitoa chakula alichokuwa amewekewa na Nanaa, akataka
kula, akashindwa. Akataka hata kunywa uji wake kama dawa, lakini pia
akashindwa. Akataka kurudi chumbani kwa Nanaa, lakini akagundua Nanaa
alishazima taa, amelala. “Hata nikiingia, nikamuamsha, nitamwambia nini
wakati wazi nilimuonyesha simjali? Sijui kama anakula au la. Nilishamuonyesha
kumsusa muda mrefu sana. Ndio maana anashindwa hata kujibu maswali yangu. Kesho
ndio hatima ya Zac, Nanaa na mimi. Zac anayejua kumbembeleza Nanaa, akifanikiwa
kukutana na Nanaa kesho tena, mimi ndio niandike maumivu. Au nimkataze asiende?
Naanzia wapi? Sina mamlaka hayo tena juu yake. Mama hajakosea. ‘I sow
a seed for my own destruction’. Lazima
kujishusha kama mama alivyosema. Nanaa alinitamkia kuwa kwa mara ya kwanza
maishani amejikuta akipenda. Ni mimi ndiye aliyenipenda. Mimi ndiye nipo kwenye
nafasi nzuri na kubwa kuliko Zac. Ananipenda na nimefanikiwa kumzalisha. Kesho
tukiamka salama, nitatumia silaha zangu zote mpaka kieleweke.” Geb
aliendelea kuwaza akijaribu kuweka mikakati aliyokuwa akijikatisha nayo tamaa.
“Hakika kesho lazima nichukue changu mapema.” Akazidi kujiwekea mikakati mingi, akachukua simu na kumtumia
ujumbe mama yake. ‘Mama, naomba kesho usiingie ndani.
Niachie chakula cha Nanaa hapo mapokezi nitakifuata. Naomba nipate muda na
Nanaa. Nampenda sana Nanaa, na sipo tayari kumpoteza. Naomba uende kazini uwe
na Grace kumsaidia kazi. Kesho sitaki kutoka kabisa humu ndani. Nitahakikisha
narekebisha makosa yangu yote. Nitajishusha kama ulivyonishauri wewe mama yangu.
Siwezi kumpoteza Nanaa. Nahisi nachanganyikiwa mama. Sijui lakufanya! Siwezi
kula, wala kulala wakati nimechoka. Nimeshindwa hata kuacha kuangalia mlango
alipolala mwanamke ninayempenda. Naumia kuona anathaminiwa na kuonyeshwa mapenzi
na mwanaume mwingine wakati mimi nilikuwa nikilala naye nyumba moja! Mwanaume
ambaye hata nakosa ujasiri wakumwita ni mpinzani wangu, kwa kuwa mwenzangu
amenipita mbali sana kwa Nanaa. Lakini mama, nilikuwa au ninayo mipango mikubwa
na ya kudumu kwa Nanaa. Ni hasira tu ndizo zimenifanya kupitisha kipimo.’
Mama yake alisoma huo ujumbe kwa makini.
Akaamua kumjibu. ‘Ulijisahau na
kumpuuza Nanaa, Geb. Ulijua atakuwepo wakati wote kwa kuwa ana shida. Mwenzio
anatumia matatizo ya Nanaa kumpata Nanaa. Na kumfanya awe karibu naye. Lakini
wewe umeyatumia matatizo ya Nanaa kama fimbo ya kumchapia mwanamke mtulivu,
asiye na makuu, aliyehitaji kupendwa tu! Nanaa sio kama hao wanawake zako
wengine waliokuwa wakitaka mali zako tu, bila kukujali. Japokuwa ulikuwa ukimfanyia
ubaya, lakini huyo mtoto alihakikisha halali bila ya kuhakikisha una chakula,
Geb. Huendi kazini bila kula! Ulijua hilo na ukapuuza.’ Mama G aliandika
huo ujumbe akautuma kwa mwanae.
Geb akasoma majibu ya mama yake na kuzidi kuhukumiwa moyoni. ‘Nimetambua kosa mama. Kesho nitarekebisha.’
Akarudisha majibu kwa mama yake. ‘Kama bado hujachelewa!’
Mama yake nae akamjibu kwa kifupi. ‘Naomba usinikatie
tamaa mama. Wewe ndio nguzo yangu. Kila ninapokosea wewe ndio unakuwepo
kuniinua. Hujawahi kunitupa, naomba usinitupe sasa hivi. Nitachanganyikiwa
zaidi ya hivi.’ Geb alijikuta akizidi kukosa nguvu kila alipokumbuka
ukali kutoka kwa mama yake kila linapokuja swala la Nanaa. Wazi mama yake
alionekana kuwa upande wa Nanaa kila wakati kitu kilichokuwa kipya na kigeni
kwa Geb.
Alizoea kuonwa kama malaika na mama yake. ‘Mama! Nimekuomba usinitupe. Nimekukosea, nimekosea kila mtu,
naomba mnisaidie wewe na Grace, kwa namna yeyote ile nimpate tena Nanaa.’ Jumbe zote aliona zimeingia kwenye simu ya
mama yake, akaona wazi amesoma, na hataki kujibu. Geb alizidi kuumia. ‘Tafadhali mama yangu. Naomba usinitupe sasa hivi!’
Geb alituma ujumbe mwingine akiendelea kusihi.
Japokuwa alikuwa amemkasirikia mwanae, ikabidi ajirudi
kidogo. Akamuhurumia. Akajua amekuwa mkali sana kwake. Alimjua jinsi anavyoweza
kuchanganyikiwa na kuwa hata mgonjwa. Alikumbuka madhara makubwa aliyoyapata
kwa msichana aliyemkimbia kwa ajili ya mwanaume mwingine akiwa chuoni. Akaogopa
historia kujirudia, akarudisha ujumbe kwa haraka, ‘Geb!
Penye nia pana njia. Sijawahi kuona ukishindwa jambo. Sasa hivi naingia kwenye
maombi kukuombea mwanangu. Hujawahi kunidanganya, na ninaamini ulichosema kuwa
unampenda Nanaa. Tulia, hakikisha unapata usingizi wakutosha ili kesho uwe na
familia yako. Nitakuletea vyakula asubuhi, na kwenda ofisini kwako kumsaidia
kazi Grace. Usiku mwema.’ Ilikuwa kama dawa, moyoni kwa Geb. Alifurahia
sana, akarudi chumbani kwake moja kwa moja. ‘Asante
sana mama yangu. Usiku mwema.’ Alituma huo ujumbe, akabaki akiwaza.
Wakati akiwaza huku, Nanaa naye alikuwa akiwaza, na Zac hivyo hivyo.
Kwa Zac!
Z |
ac naye alianza kupanga
sera zake. Akajiapia kurudisha penzi la Nanaa. Akapanga maneno ya kumwambia
huku akijaribu kukumbuka maswali yote aliyoulizwa na Nanaa jioni hiyo. Akaanza
kuyafanyia mazoezi majibu yake. Huku akiyapa hisia kutokana na kile alichojua
Nanaa angependa kusikia, na kugusa hisia zake kwa haraka. Alijiambia endapo
kesho atabahatika kukutana naye tu, basi atahakikisha anauza sera zake kama
mwanasiasa. Kwa utulivu sana bila papara ili asiharibu akiweka hisia nzito,
mpaka Nanaa ataingia kwenye anga zake. Akakusudia kumbana katika kila eneo
alilojua Nanaa anaweza kutaka kumponyoka. Na kwa kuwa alimjulia Nanaa, hakika
alijua atashinda tu.
Akaweka mkakati wa kumuoa kwa haraka sana hata ikimlazimu
ndoa ya serikalini ambayo alijua haitakuwa na mlolongo mrefu. “Jamaa
kaniwahi kwa mtoto, mimi namuwahi kidoleni.” Akajisemea Zac usiku huo. “Halafu
namfungia. Nikishamfungia, simtoi humo ndani mpaka nihakikishe amebeba mtoto
wangu na mimi.” Akaendelea kujiwekea mikakati. “Lakini jamaa anaonekana
mambo yake safi. Nanaa ana hali nzuri. Nitaweza kweli kushindana naye?” Akajivunja
tena moyo. “Hapana. Hata kama anapesa za kunizidi mimi, mbona Nanaa
anaonekana bado hana furaha? Jamaa anaonekana ni kweli hamjali. Mimi bado nipo
kwenye nafasi nzuri tu.” Akajitia
tena moyo. Akapandisha ujasiri. Akajitia morari zaidi.
“Kama kweli angekuwa yupo kwenye mikono sahihi, nina uhakika asingetulia
mikononi mwangu kwa kiasi kile. Ni kweli nimechezea shilingi chooni. Lakini
bado najiona nina nafasi kubwa sana kwa Nanaa. Mimi ni Zac bwana! Mtoto wa
mjini. Lazima nikieleweshe.” Akachukua simu,
akamtumia ujumbe Nanaa. ‘Usiku mwema mpenzi wangu.
Nitakuona kesho.’ Mpaka anapitiwa na usingizi, ujumbe haukuonekana
kufika.
Kwa Nanaa!
“Nakosea
wapi kwa hawa wanaume jamani!?”
Nanaa aliwaza huku machozi yakimtoka gizani pale alipokuwa amelala na mtoto
wake. “Geb amenionyesha wazi hanihitaji, nipo
hapa kwa ajili ya mtoto. Mpaka lini? Ikitokea anaoa kesho, inamaana nitabaki
humu ndani na mkewe kwa ajili ya kunyonyesha tu. Nitaweza? Heri niendelee na
maisha yangu. Peke yangu? Oliva wangu je? Nimuache kweli? Zac alinipenda sana
na bado anaonekana kunihitaji. Alikosea wapi? Ni nini kilimsababishia
anisaliti? Alipatwa na nini? Nimpe nafasi nyingine tena?” Nanaa
aliendelea kuwaza huku akifuta machozi.
“Labda nikamsikilize ili nijue. ‘jini likujualo, halikuli, likakwisha’.” Nanaa alijiambia. “Heri nirudi kwa Zac ninayejua
ananipenda, hata kama ananidanganya, lakini hajawahi kunifanyia unyama kama
Geb. Geb hanihitaji mimi maishani. Nisije nikamkataa Zac sasa hivi, Geb
akanifukuza, nikaishia kuwa peke yangu. Sitaki kuja kuanza mahusiano na
mwanaume mwingine tena. Kwanza Zac alinionyesha wazi amempokea Liv.” Nanaa
akajifariji, ili tu kujitia moyo kwenye maamuzi yake.
“Hata kama nikiondoka hapa, Geb akanikatalia kuondoka na
mwanangu, nitamuomba kazi ya kumlea mwanangu, mimi mwenyewe. Niwe naingia
asubuhi, natoka usiku wakati Oliva wangu analala. Nitahakikisha hatahisi kama
sipo naye. Nitashinda na mwanangu siku nzima! Usiku narudi kwangu na Zac.
Nianzishe familia yakueleweka na Zac.”
Nanaa aakaanza kujiwekea mikakati. ‘Lakini itakuaje kama Zac akiamua
tuondoke nchini? Itakuaje kama Geb akinikatalia kuondoka na Liv? Hata iweje
sitawahi kutengana na mwanangu. Labda kifo pekee.’ Tayari akaanza kuona
ugumu wa mikakati yake. Lakini
akaendelea kuwaza.
~~~~~~~~~~~~~
Akaamua kuwasha simu yake, akakutana na ujumbe wa Zac.
Akausoma na kuamua kurudisha majibu kumwambia Zac usiku mwema na yeye. Wakaanza
kuchat tena kwa muda mrefu. Nanaa akitoa vipingamizi vyote anavyoona vipo mbele
yake hata kama akimsamehe. Zac naye alitumia hiyo nafasi vizuri sana. Akijibu
na kumtoa Nanaa wasiwasi. Alimpa mikakati kabambe, endapo watakuwa pamoja. Nini
watafanya wakiwa pamoja ili kuwa na amani na pia wasimpoteze Oliva.
Alimbembeleza Nanaa na kumuonyesha anamuhesabu kwenye maisha yake. Vile
anavyomuhitaji. Vile maisha ambavyo hayajakuwa sawa tokea waachane! Akampanga mpaka
Nanaa akaanza kuingia kwenye mstari. Akajikuta wanakubaliana, kesho kuonana
tena ili wazungumze zaidi.
~~~~~~~~~~~~~
Kikubwa alichokuwa akikwepa ni upweke. Alijiapia hatawahi
kuja kuwa peke yake maishani. Kwa garama yeyote ile, ataolewa na kuanzisha
familia na mwanaume yeyote atakayekuja kuwa tayari kumuoa. Yeye kama yeye Nanaa
hakuwahi kufungulia moyo wake kwa wanaume ila mwili tu. Angalau kwa Geb alihisi
kupenda kwa mara ya kwanza, lakini Geb alimuonyesha hamuhitaji!
~~~~~~~~~~~~~
Oliva alianza kuhangaika, akamtoa mama yake kutoka mawazoni,
akakaa kwa haraka. Moyo wake ulijaa furaha mara baada yakuwasha taa, na Liv
kumpa tabasamu. “Nina hamu na wewe Liv mwanangu! Punguza kulala basi ili tuwe
tunaongea! Muone unavyojinyoosha. Utaachika! Mwanamke gani unapenda kitanda
hivyo? Eti Liv mama? Njoo kipenzi changu. Njoo eeh!” Geb akamsikia Nanaa
akiongea na mtoto, akajua ameamka. Na yeye akapata sababu ya kuamka.
“Na
mimi naomba nimuone. Nina hamu naye!” Nanaa alishitukia Geb anaingia, akakuta
ananyonyesha. Macho yake yakatua kwenye matiti yaliyokuwa yakimpa usingizi
kabla Oliva hajayamiliki. Nanaa akamuona amekodolea macho matiti yake, akavuta
mtandio wake aliozoea kumfunikia Oliva wakati akinyonya, akajifunika yeye na
mtoto. Geb akagutuka akaona ajibaraguze tu. “Ukimaliza kumnyonyesha utaniita
basi. Nipo hapo chumbani.” Oliva akaanza kuhangaika mle ndani. “Amesikia sauti
yako naona hataki kunyonya tena, anakutafuta.” Nanaa akamtoa, akaona vile Geb
alivyofurahi. “Nimshike kidogo. Ninahamu naye kweli! Asubuhi niliondoka akiwa
amelala.” Geb akajisogeza.
“Njoo mama. Njoo mama yangu mzazi.” Geb akampokea, akambusu,
nakumuweka kifuani. Nanaa alimuona akifunga macho kama anayesikilizia furaha
moyoni, akanyanyua mkono wake akaubusu nakumuweka mbele ya uso wake. “Unalala
sana Liv jamani! Mpaka tunakuwa na hamu na wewe!” Geb aliongea na mwanae, Liv
alibaki akimwangalia baba yake. Geb akambusu mara kadhaa huku akimchezea.
“Manywele haya, tutaanza kuyakata na kuyauza. Tufanye biashara. Eti Liv wangu?
Naona yanazidi kujaa kichwani.” Geb aliongea akisikika akimsifia mwanae. Nanaa
akacheka. “Naona mimi nitakuwa mteja wenu wa kwanza.” Geb akacheka. “Eti Liv?
Tuanze biashara? Mteja wa kwanza tumeshampata.” Geb aliendelea kumchezea.
“Changamka basi mama! Mfanyabiashara gani mpole hivyo?
Tuchangamkie pesa, mchana kweupeee!” Liv alianza kucheka na kumfanya Geb azidi
kucheka kwa furaha.
“Angalau roho imetulia. Sasa hivi nenda
kanyonye, halafu tukacheze, tumpishe mama apumzike.” “Kesho hutakwenda kazini?”
Nanaa akauliza, akishangaa kwa nini Geb achelewe kulala wakati kesho yake ni
siku ya kazi. “Kesho sitakwenda kazini.” Nanaa akafurahi sana. Akajua mambo
yake yatakaa sawa. Atamuachia mtoto, yeye akamalizane na Zac. Hata hivyo
alikuwa na hamu naye. “Kesho nikakate kiu.” Nanaa aliwaza akatoa
tabasamu aliloliona Geb. Akaona ni bora atoke ili kumpa nafasi ya kunyonyesha
kwa uhuru si kujifunika. “Nitakuwa hapo chumbani.” “Sawa, nikimaliza,
nitamleta.” Geb akatoka.
Nanaa na yeye akacheza na mtoto wake kwa muda mrefu, Geb
akiwasikiliza Nanaa akiongea na kucheka. “Hamna kunyonya mpaka tuongee leo.”
Nanaa alisikika. Alimuimbia taratibu huku akimtania mtoto wake, mwisho akasikia
anapewa ziwa. “Njoo ule mwanangu. Usilale ili ukacheze na dad. Sawa Liv? Hamna
kulala.” Nanaa aliendelea, kimya kikazuka, Geb akajua ameshaanza kunyonya.
Akacheka.
Hakumaliza hata dakika mbili, tayari Oliva alisharudi kulala.
Nanaa aligutuka kutoka mawazoni akichezea nywele za mwanae, aliyekuwa amelala
bila habari. Akagundua alishalala
“Jamani Liv wewe! Amka bwana!” Lakini hata hakufungua macho. Kila mama
yake alipomkuna miguuni ili aamke, yeye aliongeza kunyonya kwa nguvu bila
kufungua macho. Akamuona ameachia chuchu, akajua ameshashiba. Akamuweka begani
ili ateuke. Akateuka. Akamwangalia tena diaper, akamuweka kitandani kwake,
akabaki akicheka. “Unaturingia wewe!” Nanaa akatoka.
~~~~~~~~~~~~~
“Geb!” Akasikia sauti tulivu mlangoni kwake. Akakaa. “Ingia
tu.” “Nilihisi umelala, kumekuwa kimya!” “Hapana. Nawasubiri wewe na Liv.”
“Mwanao amelala hana hata habari!” Wote wakacheka. “Ndio atakuwa haraka.
Ilimradi ananyonya, mwache alale. Karibu.” Nanaa alishangaa anakaribishwa.
“Asante. Ngoja nikuache upumzike.” “Nanaa!” Geb aliita kwa utulivu akabaki
akimwangalia Nanaa aliyekuwa amesimama pale mlangoni, ameshikilia mlango.
“Abee.” Akaitika kwa upole na heshima zote. Alivaa nguo nzuri ya kulalia.
Ilikuwa na kitambaa cha silk, nyeusi. Kilikuwa kigauni, kama shumizi. Geb
alibaki akimtizama kwa uchu, Nanaa akainama. Alibana nyele zake sehemu moja ili
zisimsumbue wakati analala. Alivutia kumtizama. Ukimya wa muda ulipita.
“Usiku mwema.” Nanaa alinyanyua uso, akaaga. “Nilikuita
Nanaa.” Nanaa alibaki akibabaika asijue aongee nini, Geb akabaki akimtizama.
“Abee.” Akarudia tena kuitika huku akimtizama kwa shida. Nanaa alipenda
kuangaliwa na Geb. Macho yake yalikuwa kama moto unaoyeyosha matatizo yote
moyoni mwake, hasa akimwangalia akiwa ametulia kama wakati huo. Akaingia ndani,
akafunga mlango na kusimama mlangoni huku amekusanya mikono yake pamoja asijue
aseme nini. Akamkumbuka Zac. Kwa kuwa Geb hakuwa amesema kitu, akaona avunje
ukimwa ili kuyatoa macho yake kwenye mwili huo wenye nguo ya kulalia tu.
“Geb!” Nanaa akaita akanyanyua uso, macho yake yakagongana na
Geb aliyekuwa bado amejiegemeza kitandani akimwangalia. “Kesho umesema huendi
kazini?” “Ndiyo.” “Naomba asubuhi nitoke nikuache na Liv kwa muda mfupi kidogo,
nitakwenda mahali, kama baada ya lisaa au lisaa na nusu nitakuwa nimerudi.
Nitajitahidi nisichelewe.” Mapigo ya moyo yalianza kwenda kasi. “Unarudi tena
kwa Zac?” Geb aliuliza swali la moja kwa moja lililombabaisha Nanaa,
nakushindwa aseme nini. Akajua mama yake amemwambia kila kitu, akainama.
“Eti Nanaa? Umeamua kurudi tena kwa Zac?” “Sijui Geb.” “Hujui
nini?” “Nilikutana naye leo nilipokuwa na mama, akaniomba tukutane tuzungumze.
Zac yeye ananonekana bado ananihitaji kwenye maisha yake.” Lile neno lilizidi
kumuuma Geb. “Nilikwenda kuonana naye jioni hii nilipokuaga, lakini nilishindwa
kuzungumza naye.
Ameomba kuniona tena
kesho.” “Kwa hiyo unaenda?” Nanaa hakujua anamaanisha nini wakati ametoka
kumuomba abaki na Liv, yeye atoke. Wazi alishamjulisha anakwenda kukutana na
Zac. “Sasa anamaanisha nini tena!?” Nanaa akajiuliza.
“Naona nimekimbia vyakutosha Geb. Najihisi ni wakati mwafaka
wa kusimama na kusikia ukweli. Umri umekwenda. Sitarudi tena kuwa msichana
mdogo. Siwezi kubadili yaliyotokea, kwa kuwa nimekuwa nikikimbia bila kujua
ukweli. Japokuwa naumia, lakini naona nimpe Zac, mwanaume aliyeonyesha
kunipenda na kunijali, nafasi ya kumsikiliza.” “Ili muanze naye maisha?” Geb
akauliza. “Sijui Geb! Sijui atanipa sababu gani ya kwa nini alilisaliti penzi
letu.” Geb alitamani kuchanganyikiwa.
“Halafu kwa Zac sitakuwa naanza Geb. Nitakuwa nikiendelea.
Nilikwambia jinsi Zac alivyokuwa akinipenda na kunijali. Hajabadilika. Mpaka
naachana naye leo, alinionyesha ananipenda na kunijali, mimi.
Nimejiuliza kwa nini arudi tena kwangu, tena baada yakunikosea. Au kwa nini
amenitafuta tena? Jioni hii wakati nimemuacha pale mgahawani, nilimpiga
marufuku asinitafute tena. Lakini Geb, Zac amenitafuta tena. Zac ananionyesha
kwa vitendo ananihitaji. Hawezi kulala vizuri, akihisi nitalia. Hawezi kuniacha
ninalia, hata kama itamlazimu kuahirisha mtihani au vipindi, atabaki na mimi
mpaka nitulie ndio ataondoka! Zac alikuwa akitaka kunisikia kila wakati!” Nanaa
akaendelea taratibu.
“Japokuwa alinisaliti, lakini Geb, nimeshakaa na wanaume
baada ya Zac, nimeona wachumba wa rafiki zangu, bado sijapata wakumlinganisha
na Zac. Anafurahia akiniona ninafuraha. Hata kama ananidanganya, lakini
najisikia furaha na amani katika huo uongo. Napata kile ninachokitafuta, ndani
ya huo uongo wake. Zac ananithamini kuliko ambavyo nitakueleza. Nimeamua kumpa
nafasi ya kumsikiliza. Ikitokea anaomba radhi, najihisi kuruhusu nafsi yangu
kumpa nafasi ingine tena. Ili nione tutakapofika tena.” Geb alikuwa ametulia
pale kitandani kama aliyekufa ganzi. Nanaa akaendelea.
“Sina
chakupoteza tena, sina haraka. Sasa hivi nina Liv, na yeye amempenda mtoto
wangu. Nimemueleza maisha yetu. Mimi, wewe na Liv. Zac amekubali na ameahidi
tutafikia muafaka tu ili nisimkose Liv kama nikiwa naye. Amepata ahadi ya kazi
yenye mshahara mzuri. Ameniambia Mungu akimbariki hiyo kazi, itatusaidia
kipindi hichi ninacholea. Amenishauri kama nitamsamehe, nakurudiana naye,
ameniahidi tutafunga ndoa. Kisha tutakuomba badala yakuajiri msichana wa kazi,
basi unipe mimi kazi ya Liv.” Nanaa alianza kulia.
“Atakuwa akinileta nyumbani asubuhi na mapema
kabla hujaenda kazini. Nitakuwa na Liv siku nzima mpaka usiku atakapokuja
kunichukua Zac, turudi nyumbani. Sitataka chochote kutoka kwako, Geb. Nitafanya
kwa bure kabisa. Ilimradi tu unipe nafasi ya kumlea Liv kama sasa hivi. Na
sitazaa mtoto mwingine, mpaka Liv awe mkubwa. Nitafanya chochote utakacho
ilimradi tu naomba unipe kazi yakumlea mwanangu.” Geb alishangaa na yeye machozi yanamtoka.
Nanaa akashituka kidogo. Akakausha ya kwake. Akabaki hajui ni
nini kimempata, ‘Bosi dad wake’. “Geb!
Sio kwa haraka. Pata muda wakufikiria.” Geb hakujibu. Nanaa hakuwa anaelewa.
Alisogea mpaka pale kitandani, akakaa. Geb akainama, akafuta machozi.
“Nimekosea?” Nanaa akauliza kwa upole na wasiwasi. “Geb! Nimekosea nini?
Nimekuudhi?” Nanaa
akauliza tena. “Kama ni juu ya Zac, usiwe na wasiwasi naye. Sitamruhusu hata
amsogelee Liv. Nitamwambia asifike hata ndani nyumbani kwako. Kama
nikunishusha, atanishusha nje ya nyumba yako. Hataingia.” Kimya. “Tafadhali
Geb, niambie kitu chochote. Usiniache njia panda, nikiwa sijui unawaza nini!”
Nanaa akabembeleza. Asijue wivu na hukumu aliyoiacha kwenye moyo wa Geb.
~~~~~~~~~~~~~
Anajirudije tena kwa Nanaa baada ya vituko vyote
alivyomfanyia? Ndilo swali lililomziba mdogo Geb, nakushindwa kutoa neno hata
moja na kwa mara ya kwanza kujikuta akitoa machozi mbele ya mwanamke, tena
baada ya kujiapia hatalizwa tena na mwanamke. Historia inajirudia tena!
Anaachwa na mwanamke mwingine, kwa sababu ya mwanaume mwingine. Geb aliinama.
Akajikuta machozi yakimtoka tena. Hisia zilimrudisha kwa msichana wake wakwanza
aliyemlilia mpaka karibia kutaka kujiua.
Sasa hivi tena ni Nanaa. Lakini Nanaa hakuwa na kosa.
Alimfukuza yeye mwenyewe. Anajirudije tena kwa msichana, aliyekwisha muomba
msamaha wa machozi kiasi kile, nakushindwa kumsamehe? Leo Nanaa anatangaza
kurudi kwa mpenzi wake wa zamani, atamzuia vipi? Si utakuwa ubinafsi tu!
~~~~~~~~~~~~~
Geb alishindwa hata kunyanyua uso kumuangalia Nanaa. Nanaa
aliogopa hata kumshika. Walikaa pale kwa muda, Nanaa akiwa pembezoni kabisa ya
kitanda, Geb amekaa katikati ya kitanda chake ameinamisha kichwa chake.
Alipotulia tu, Nanaa akasimama kama mshale. “Usiku mwema. Nitakuona kesho.” Akatoka,
bila kujibiwa.
Nanaa alikwenda kulala,
asijue kinachomliza Geb. Akajiuliza maswali mengi akihisi amemkosea, lakini
akajiaminisha kuna lake linamliza sio yeye. “Asubuhi nikiamka tu, naenda zangu
kwa Zac.” Nanaa alijiambia wakati anapitiwa na usingizi. Geb aliendelea kuwaza
hili na lile akihesabu hasara zote. Akijutia hili na lile. Akaliona anguko lake
kwenye maisha. “Ndio maana Zac mwenzangu
amerudi. Hakuna mwanaume aliyeishi na Nanaa, akamuacha na kufanikiwa kimaisha.
Nimekwisha Geb, mimi.” Geb aliendelea kuwaza huku machozi
yakimtoka.
~~~~~~~~~~~~~
Ilishakuwa saa nne
asubuhi wakati Geb alipoamshwa na maongezi ya Nanaa na Liv. “Hakuna kulala tena
Liv. Lazima dad akuone. Amebaki leo kwa ajili yako. Usinichekee bwana! Twende
tukampikie dad uji. Nitakufundisha ili uwe unampikia kila siku, asiwe analala
na njaa. Umesikia Liv? Twende.” Geb aliwasikia wakitoka chumbani, akatoka.
“Jana hukula Geb.” Nanaa alimuwahi mara Geb alipotoka chumbani kwake. Geb
akabaki akimwangalia Nanaa. Alipendeza, akionyesha wazi yupo tayari kutoka.
“Mama ameleta vyakula, vipo mapokezi.” “Jamani mama yangu!
Anahangaika kweli! Angeacha tu nikapika. Halaf..” Nanaa akanyamaza kidogo kama
anayefikiri. “Kwa nini aache vyakula mapokezi, asiingie humu? Ni nini
nimemuudhi? Au..” Nanaa akapooza. “Nimekosea? Niambie ukweli Geb. Sitaki
kumuudhi mama, wala wewe. Nilipokesea nitarekebisha haraka. Nini kimemuudhi mama, nakushindwa kuja kuniona mimi na
Liv!? Sio kawaida yake!” Nanaa akaanza kulia kama kawaida yake, machozi
ya karibu. “Hajawahi kuacha kuniona tokea nimerudi
na Liv.” “Nanaa! Nanaa!” Geb alimkatiza kutaka atulie asiendelee kulia.
“Mimi ndiye nimemuomba leo asije.” Nanaa akafuta machozi
akamwangalia Geb kwa kushangaa. “Kwa nini!?” “Sikujua kama unamiahadi mingine
tena na Zac. Nilimuomba mama leo anipe nafasi na nyinyi. Nilitaka muda na wewe
Nanaa, pamoja na Liv. Nilimuomba jana kabla hujanitaarifu kuwa unakwenda na leo
kukutana na Zac!” Hilo likamtuliza. “Niliingiwa na wasiwasi nikajua
nilimkosea!” Akamsogeza Liv kwa baba yake. “Naona anakaribia kusinzia huyu. Leo
ameamka mapema! Nimeona bibi yake anachelewa kuja kumuogesha, nimecheza naye tu
sikutaka nimuogeshe. Maana akioga tu angelala kabla hujamuona. Na akilala sasa
hivi, atachukua muda kuamka. Pata naye muda sasa hivi kabla hajarudi kulala.”
Nanaa akamkabidhi. Geb akamtizama kidogo, akarudisha macho kwa mwanae.
~~~~~~~~~~~~~
Alijua Nanaa anamkwepa. “Nitarudi muda sio mrefu. Nakwenda
kufuata hivyo vyakula mapokezi.” Nanaa akaaga, hakusubiri jibu, akatoka.
Alipofika tu mapokezi kabla hajamfikia muhudumu, Zac naye akasogea. “Hee!
Ulilala hapa hapa!?” Nanaa akamuuliza kwa mshangao. “Nimefika muda sio mrefu.”
Akamsogelea na kumkumbatia kwa upendo. Akiwa kifuani kwa Zac, akajikuta machozi
yakimtoka. “Zac anaonekana kunipenda sana. Kwa
nini alinisaliti?” Hilo swali bado lilimsumbua na kumfanya ashindwe
kujizuia. “Natamani ingekuwa kama zamani Zac!”
Nanaa aliongea kwa upole akiwa bado amekumbatiwa. Zac alisikia, akamvuta mbele
kidogo akabaki amemkumbatia huku akimwangalia. “Nilikosa Nanaa.” “Hilo ndilo tatizo Zac.” Nanaa aliendelea kulia
taratibu huku macho yake yakiangalia kifua cha Zac, kama aliyeinama. Zac alitoa
mkono mmoja nyuma ya mgongo wa Nanaa na kuanza kumfuta machozi.
“Ndio umekuja ili tupate muda wa mazungumzo?” Zac akauliza. “Hapana. Nimefuata chakula.” Nanaa akajibu huku
bado amekumbatiwa. “Unataka tukae hapa tule wote?” “Geb
leo yupo nyumbani. Hiki chakula mama yake ndio ameleta sio chakununua. Huwa
hali vyakula vya kununua, kwa ufupi hapendi kula kwa hiyo vyakula vyake vina
jinsi yakupikwa.” Akatoa tabasamu. “Kwa hiyo
mama yake huwa anampikia mara zote. Ngoja nikichukue, nimpelekee. Nimemuacha na
Liv. Nitarud..” Akamuona Zac ametoa macho yake anaangalia kwengine kama
aliyeona kitu.
Akiwa
bado amekumbatiwa na Zac, akageuza kichwa, ndipo alipomuona Geb na Liv na wao
wanaingia hapo. Kidogo alibabaika, lakini akagundua hana kosa analofanya. Geb
si mpenzi wake tena, ni mzazi mwenzake tu. Lakini akakumbuka alimuaga anakwenda
kuleta chakula, akaishia kukutwa amekumbatiwa! Akajitoa mikononi kwa Zac.
“Samahani nimechelewa kurudi.” Ndilo neno lililofanikiwa kutoka mdomoni mwake huku
akionyesha wasiwasi na hofu ya wazi kabisa. Akahisi anashikwa mkono taratibu.
Akamgeukia Zac, akamkuta na tabasamu lililoashiria kumtuliza, asiogope. Nanaa
akamgeukia Geb aliyekuwa amesimama na yeye akiwaangalia kwa utulivu tu bila
paniki.
“Naenda kuchukua sasa hivi, nikilete ndani.” Nanaa akarudia.
“Hamna shida. Niliamua kukufuata ili kumtoa Liv ndani. Nataka kumtembeza kidogo
asirudi kulala kwa haraka.” Geb alirudisha macho kwa mwanae, ukimya ukapita.
Nanaa akahisi mkono wake umeminywa na Zac, akageuka akamtizama. Bado walikuwa
wameshikana mikono. “Geb! Huyu ndio Zac.” Nanaa alimtambulisha kwa unyonge, Geb
alinyanyua macho kutoka kwa mwanae akayatupia kwa Zac bila kusema kitu. Nanaa
alivyoona hivyo, akageuka kwa Zac. “Huyo ndio Geb, baba yake Oliva.” “Asante
kwa utambulisho. Nimefurahi kumfahamu.” Zac alimjibu Nanaa, tena kwa
kumwangalia yeye wala sio Geb. Kimya.
“Ngoja nikachukue chakula, halafu nikamnyonyeshe Liv, ndio nitakuja
tutoke.” Nanaa akaaga. “Sawa, nitakusubiri. Lakini kuna zawadi zako kwenye
gari. Nilikununulia kabla sijarudi hapa nchini. Naweza kukusaidia kuzibeba
mpaka ndani, kama utakuwa na mzigo mkubwa. Tuziache kwako, sitaki kuendelea
kuzunguka nazo.” Nanaa akacheka kwa deko. “Ulijuaje kama utanipata sasa?”
“Penye nia pana njia Nanaa, mbona unakuwa msahaulifu?” Wote wakacheka kidogo.
“Haya bwana, asante kunikumbuka. Nenda basi kafuate zawadi wakati mimi nachukua
chakula. Nitakusubiri hapa.” Zac alitoka kwenda kwenye gari lake, Nanaa
akaelekea mapokezi bila hata kumtizama Geb.
Baada ya kusalimiana na kijana aliyemkuta hapo mapokezi,
akamuomba mzigo wao. Geb akamsogelea. “Kama ni mzito, naweza nikakusaidia
kubeba.” Nanaa akageuka baada yakusikia sauti ya Geb nyuma yake. “Wewe mbebe
Liv, mimi nibebe hivi vyakula. Kwanza atakuwa na hamu na wewe. Muone
anavyoshangaa.” Wote walirudisha macho kwa Liv aliyekuwa amebebwa kwa kugeuziwa
mbele ili asilale kifuani kwa baba yake. “Eti Liv? Ulikuwa na hamu ya dad?” Geb
alimtekenya kidogo na kumbusu mgongoni. Wakati makapu mawili ya vyakula
yamewekwa juu ya kaunta, Geb na Nanaa wakishangaa vyakula vilivyo vingi, Zac
naye akarudi na mfuko mzuri, ulionekana ni wa zawadi.
Nanaa akamgeukia vizuri na kucheka kumuonyesha amefurahia ile
zawadi, kisha akarudisha macho kwenye vile vikapu vya vyakula. “Jamani mama!
Sijui hata kama amelala leo. Vyakula vyote hivi! Nitampigia simu nimshukuru.
Kwanza nimeshapatwa hamu naye. Lazima aje atuone kidogo. Siku haiwezi pita bila
kuonana na mama.” Nanaa aliendelea kuongea peke yake bila kujibiwa na mtu.
Wanaume wote wawili walikuwa wamemsimamia pale nakumfanya azidi kubabaika.
Kuongea pekee ndiko kulikokuwa kukimtoa hofu.
Akamgeukia Zac akampa tena tabasamu. “Nashukuru, lakini
hukuwajibika kufanya hivyo bwana.” “Wewe nenda kafungue kama hujarudi
unarukaruka kwa furaha. Mambo yako matupu humo ndani.” Zac alimfanya Nanaa
acheke zaidi. “Haya Zac. Nashukuru.” “Niwasaidie kubeba mpaka ndani?” Zac akauliza,
Nanaa akamgeukia Geb, Geb akamtazama Zac.
Shilingi Imepinduka.
“Naweza kuwasaidi mizigo.” Zac akarudia huku akimtizama Geb.
“Hukaribishwi kwetu, na wala nisingependa kukuona karibu ya mlango wa nyumbani
kwetu.” Geb alijibu kwa utulivu huku akimtizama Zac machoni. Nanaa akashituka
sana, nakuogopa zaidi. “Nimekosa nini!?” Zac akauliza kiungwana. “Kucheza na
hisia za Nanaa, hilo ndilo kosa lako. Unamdanganya. Huna mapenzi ya kweli kwa
Nanaa. Kwa kuwa unamfahamu anataka nini, shida yake ni ipi, ndio maana unacheza
na hisia zake vile utakavyo. Unajua ni lugha gani sahihi utakayo itumia kwa
Nanaa na kumfurahisha au kumfanya ashindwe kufikiria kitu kingine chochote ila
wewe na uongo wako tu.” “Sio kweli. Mimi nina mapenzi ya dhati kwa Nanaa.” Zac
akajitetea kwa ujasiri.
Geb akamuweka mtoto vizuri, kisha akaendelea. “Unatumia
machozi ya Nanaa, kujinufaisha naye. Unatumia upweke wake, kujinufaisha nae.
Tena kwa muda, ukiwa huna mipango ya kudumu na Nanaa. Acha kumdanganya Nanaa,
na sitakuruhusu uendelee kucheza na hisia zake.” “Sichezi na hisia za Nanaa.
Nampenda Nanaa.” “Kama kweli unampenda Nanaa, mwambie ukweli wa maisha yako
yote. Usimdanganye.” “Ndio nataka nikamwabie ukweli.” “Anza kwa kuwa muwazi
sasa hivi. Hapa hapa mbele yangu. Anza kwa kitu kidogo tu. Anza kwa kumweleza
ukweli kati yako wewe na Ndina.” Wote
wakashituka na kumgeukia Geb.
Nanaa akarudisha macho kwa Zac. “Amemfahamuje Ndina?” Nanaa
akamuuliza Zac kwa upole. “Naomba umuulize maswali sahihi, Nanaa.” Geb
akaingilia. Nanaa akamuangalia Geb kisha akarudisha macho kwa Zac. “Zac! Ukweli
gani juu yako wewe na Ndina?” “Ulitaka kujua kipengele gani?” Zac aliropoka, na
kumchanganya zaidi Nanaa, Geb akacheka kwa kicheko cha kumkejeli. “Kipengele
tena? Kwani vipo vingapi!?” Nanaa akauliza, lakini Zac alinyamaza akamgeukia
Geb. “Shida yako ni nini Geb? Kwa nini unafanya hivyo?” Zac akamlaumu Geb.
“Kwani mnafahamiana na
Zac?” Nanaa akauliza. “Kama kweli unampenda Nanaa, mwambie ukweli.” Geb
akajibu. “Ni habari ndefu Nanaa, twende tukazungumze.” Zac akabembeleza. “Hata
sio ndefu! Msimulie tu kwa kifupi. Akikubali na kukuelewa, akaondoka na wewe
sasa hivi, sitakuwa na neno. Lakini sitakuruhusu utoke na Nanaa leo, kabla
hajajua ukweli wote. Mtatoka naye tu, endapo utamwambia ukweli, akakujua
vizuri, halafu bado akaamua kutoka na wewe.” Geb aliongea huku akimsogelea yule
kijana pale mapokezi.
“Naomba
nisaidie kikombe.” Alizungumza na muhudumu. Alipopewa kikombe, akachukua kapu
lililokuwa na chupa ya uji, akakaa kwenye meza ya pembeni yao akafungua chupa
ya uji, akajimiminia na kuanza kunywa uji aliokuwa ameletewa na mama yake
taratibu huku akiwatizama. “Unamfahamu Zac?” Nanaa akamuuliza Geb kwa upole.
“Ndiyo. Lakini sikujua kama Zac huyu, ndiye Zac uliyekuwa ukimzungumzia wewe.
Mpaka hivi leo nilipowakuta mmekumbatiana hapa. Ndio nikajua Zac huyu
unayemwita wewe mpenzi wako, ndiye…..
~~~~~~~~~~~~~
Usikose Muemdelezo.
Zac Ni Nani?
Amefahamiana Vipi Na Geb?
Yote Na Mengine Mengi Yapo Mbeleni.
0 Comments:
Post a Comment