Oliva
alilia mpaka baba yake akasalimu amri. “Naomba nisaidie mama. Mtoto wangu
anapandisha homa.” Mama G, akashitukia
Geb amemsimamia pembeni ya kitanda chake, amechoka kama anayetaka kulia na
yeye. Geb huyu ni baba wa mtoto anayempenda sana lakini kwa usiku huo yeye
mwenyewe na vyote alivyonavyo vimeshindwa kumsaidia mwanae. “Nakusaidia vipi
wakati hutaki nimshike mwanao?” Akaona machozi yanamtoka. Akajua
ameshapatikanika. Geb si mliaji kama Grace. Akajua ubaba umemuingia kama si
majuto.
“Naomba niambie alipo.” “Kwani maziwa ya kopo
ameyakataa kabisa?” “Mama jamani! Si umeona pale
amekataa!” “Kamjaribishe tena.” Mama G alikuwa akimkejeli tu. “Naomba niambie Nanaa alipo. Tafadhali mama!” Akajifuta
machozi. “Si umpigie simu mwenyewe umuulize kama atakubali umfuate? Kama yupo
na mtu wake wanataka kupata muda mtulivu je?” Alizidi kumkera. “Sina namba ya
Nanaa?” “Hee! Huna namba yake!?” “Naomba usiniadhibu mama. Ujue unamuadhibu
mjukuu wako mwenyewe?” “Lini umelitambua hilo? Si ulikuwa ukininyima huyo
mtoto? Leo iweje ukumbuke kama ananihusu?” “Nimekuomba msamaha!” “Msamaha wa
nini?” Geb alitamani kulia tena lakini mwanae akamzidi. Alikuwa akilia
kupita kiasi. Akatoka kwenda kumchukua.
Akarudi. “Naomba msamaha wa kukugombesha na kukukatazia mtoto.” Geb
akamalizia hapo. “Usinitanie Geb!” “Sasa nimefanya nini tena!?” “Uliniambia
nini juu ya Liz? Kwa nini alikutwa uchi humu ndani?” “Na mimi nilimkuta
uchi pale pale kitandani kwangu. Mungu wangu ni shahidi, mama. Nilikuwa
nimetoka safari, nimechoka, sikutaka hata kuzungumza naye, na mimi nikapitiliza
bafuni kuoga. Nimetoka bafuni na Nanaa anaingia. Nilijaribu kumtuliza Nanaa ili
tuongee lakini hakutaka, akaondoka.”
“Ulijua amekasirika. Kwanza hamkuwa mmemaliza
tukio la kukuona umemshika Liz mkono siku ya harusi, na ukamsahau. Pili
akakukuta naye wote mpo uchi. Tena na wewe unajua alishadanganywa na wanaume
wengi kwenye matukio kama hayo, kwa nini hukumtafuta tena baadaye ukaweka mambo
sawa, tena baada ya kujua atakuwa mjamzito?” “Sikuwa bado nimepata uhakika kama
ameshika mimba. Na nilijiambia hata kama alishika mimba itakuwa ilitoka kwa ile
hekaheka ya kufanyiwa upasuaji na madawa makali aliyokuwa akipewa. ” Geb
akajaribu kujitetea.
“Kwa
nini hukumtafuta?” “Kwa nini tusiendelee na kesi baadaye ukaniambia mahali
alipo Nanaa, nimpeleke mtoto?” “Wewe kama una haraka ya kuondoka hapa, jibu
maswali yangu yote.” “Nilikosea mama. Nilikuwa nimekasirika. Niliona
ananiadhibu bila kosa! Tena ukumbuke ndio nilikuwa nikijiiba kwenda kuwa naye
usiku kucha wakati mgonjwa.” “Mwenzio wala hajui kama ulikuwa ukikesha ukimuuguza.”
“Ndio nimekuja kugundua hilo mama. Hakuwa hata akijua kama nilimuuguza muda
wote huo. Sikufikiria vizuri mama yangu na kipindi hicho na mimi nilikuwa na
mambo mengi ya kupanua kwenye biashara ili niache kazi. Nilikosea. Naomba
unisamehe kwa kumfukuza Nanaa, najisikia vibaya sana. Najua nimekosea.”
Akamsikia mama yake anapumua kwa nguvu kama amepata aghuheni. Akajua ameshasamehe.
Akamwambia Nanaa alipo. Geb akatoka kwa haraka.
~~~~~~~~~~~~~
Bado
Nanaa alikuwa akiwaza anakopitia wakati ule, asiamini kama anaweza kunyang’anywa mtoto wake kirahisi kiasi hicho! Usingizi uligoma kuja kila
alipofikiria usiku huo atalala mbali na mtoto wake. Aliendelea kukumbuka shida
alizopata wakati wa ujauzito wa Liv! Leo Geb anammiliki mwanae yeye anakuwa
kama mtu baki tu! Akachukia umasikini kupita kiasi. Alijuta kutokubaki siku ile
alipomkuta na Liz, ili kuyamaliza. Alikuwa amejilaza hapo kitandani akiwaza
wakati muhudumu wa mapokezi alipompigia simu chumbani kwake, kwa kutumia simu
ya mezani ya hotelini hapo.
Simu yake ilishazima kabisa mara baada ya
kumtumia ujumbe wa mwisho Mama G, kumtaarifu alipo. Nanaa alishituka aliposikia
simu ya mezani ikiita. Akafuta machozi, akapokea. Ndipo alipoambiwa ana mgeni anataka kwenda hapo chumbani kwake,
kumuona. Akasikia sauti ya mtoto akilia sana kwenye simu, akajua ni mtoto wake.
Bila kujibu Nanaa alitoka huku anakimbilia mapokezi na yeye akilia. Alimkuta
Geb amembeba Liv akilia kama kengele. “Namuomba nikusaidie kumbembeleza.” Geb akampa
bila ubishi.
Nanaa akampokea mwanae, akamkumbatia huku akilia
sana. Alilia huku akimbembeleza na kumbusu mtoto wake. Gafla yule mtoto
akanyamaza. “Naomba
nikamnyonyeshe.” Aliomba kwa
upole huku akilia kwa uchungu sana. “Naona atakuwa na njaa sana.” Geb akajibu
kwa upole kama sio yeye! Nanaa akaongoza njia mpaka kwenye chumba alichokuwa
amekodisha. Haraka haraka bila hata kupoteza muda, akamtolea mtoto ziwa, Liv
alilipokea, nakuanza kuvuta kwa nguvu. Ulisikika mlio wa Liv tu akinyonya kwa
uchu. Nanaa alianza kumchezea nywele zake huku akifuta machozi yake. Alishika
mikono ya Liv huku akiibusu. “Pole Liv.” Nanaa
aliongea kwa sauti ya chini akimbembeleza mtoto wake kwa upendo.
Geb alibaki amesimama na begi la mtoto begani. “Samahani nimechelewa kurudi.” Nanaa akaomba
msamaha huku akilia. “Nilikutana na foleni. Saa 12
imenikuta bado nipo barabarani. Siku nyingine sitachelewa.” Geb alizidi
kujisikia vibaya. “Hamna shida.” Geb akajibu. “Hata hivyo uliondoka muda mbaya.”
Nanaa hakuamini. Tokea arudi nyumbani kwake, hiyo ndio ilikuwa sentensi ya
kwanza na ndefu sana, tena yenye amani kuizungumza kwake. Akajifuta machozi,
akabaki akimwangalia mtoto wake. “Naona anahoma!” Nanaa
aliongea taratibu huku akimpapasa mwanae. “Nafikiri ni sababu ya kulia. Amelia
sana leo. Sikujua kama ni mkali hivyo!”
“Geb!” Nanaa aliita kwa upole huku machozi
yakianza kumtoka tena. “Nakuomba uniruhusu leo
nilale naye. Tafadhali sana. Akipona nitamrudisha.” “Unaondoka!?” Geb
alishituka sana kama siye yeye aliyemfukuza. “Bado
sijapata chumba. Labda kesho ndio naweza kufanikiwa.” “Kwa hiyo ukipata
chumba utaondoka?” Nanaa alianza kulia
tena kwa uchungu sana. Akijua ndio anafukuzwa rasmi. “Naomba
nikae naye kidogo. Angalau akiacha kunyonya ndio naweza kuondoka. Tafadhali
Geb. Niache nimlee hata akifikisha mwaka ndio unifukuze kwako. Nitajitahidi
kufuata kila masharti, ili tu nilee mwanangu. Naomba usimkuze hivi kama hana
mama! Ni ngumu! Mimi nimepita huko. Nina uhakika hutataka Liv akue hivyo. Ni
maisha mabaya sana! Tafadhali usinitengenishe na mtoto wangu.” Nanaa akaendelea.
“Sikukusudia kukuficha Geb. Siku
niliyokuwa nataka kukwambia ndio siku nilikufumania na Liz. Nilikuja kukwambia
lakini nikashindwa. Naomba unisamehe.” “Mungu wangu ni shahidi Nanaa, na mimi nilimkuta
Liz yupo uchi pale kitandani kama ulivyomkuta wewe. Sikutaka kubishana naye kwa
kuwa nilikuwa nimechoka sana, na njaa ilikuwa ikiniuma. Nikaamua nioge, ndio
nitoke niende jikoni kutafuta chakula. Nimetoka kuoga, ndio na wewe unaingia
pale. Sikumgusa wala kumuongelesha Liz. Mpaka ulipoondoka ndipo nikamuomba
funguo zangu za nyumba, na kumwambia asirudie kufanya kitendo alichokifanya
tena. Aliomba msamaha, akanipa funguo zangu za nyumba na chumba, akaondoka.
Sisemi uongo.” Nanaa alishikwa na kigugumizi asijue anatakiwa aseme nini.
Machozi yakakauka gafla, akabaki kimya kwa muda.
“Kwa hiyo naruhusiwa kurudi nyumbani kwako?”
Nanaa akauliza kwa wasiwasi kidogo. “Muda na wakati wowote.” Nanaa akakunja uso
kidogo, akainama kama anawaza. “Hata ukitaka sasa hivi tunaweza kurudi wote.”
Nanaa akamwangalia Geb kama asiyeamini. “Kweli!?” Nanaa
akauliza huku machozi yakimtoka tena.
“Kweli Nanaa. Huyo mtoto siwezi kumlea peke yangu na sitaki akue hivyo
bila wewe. Liv anaonekana anakuhitaji wewe zaidi sasa hivi kuliko hata mimi.”
Nanaa aliinama nakulia sana. Alilia kwa kwikwi na kushindwa kujizuia.
“Naomba nisamehe Nanaa. Nimekukosea sana.
Nashindwa hata nianzie wapi! Naomba unisamehe. Nisamehe kwa masharti niliyokuwa
nimekuwekea. Nisamehe kwa kukufukuza kinyama. Nisamehe kwa kukupokonya mtoto. Nisamehe
kwa kutokutafuta tena baada ya kunikuta siku ile na Liz, nikakuacha ukiteseka
peke yako. Nisamehe kwa kushindwa kutunza ahadi yangu kwako.” Kwa wakati huo Nanaa
hakuwa akikumbuka tena ni ahadi gani anayoizungumzia. Akamwangalia akiwa na uso
wa kuuliza ni nini anazungumzia. “Nilikuahidi mimi nitakuwa nikikufuta machozi
daima. Lakini nimeshindwa. Ile hali yakunikataa huku ukinitukana iliniumiza
sana, nikashindwa kujizuia. Iliibua hasira kali sana moyoni kuona mimi
nakupenda kwa dhati kumbe mwenzangu huthamini chochote kile! Niliumia sana
Nanaa. Yote nilifanya kwa hasira tu.” Nanaa aliinama na kuendelea kulia. Geb
alijirudi, akajishusha mpaka akamshangaza, asijue kinachoendelea.
“Naomba
unisamehe. Nisamehe kwa kila kitu. Nimekukosea sana. Naahidi nitabadilika.
Nahisi ninahasira sana. Nina tabia yakuweka vitu moyoni na kushindwa
kuviachilia kwa haraka.” Baada ya kulia kwa muda, Nanaa akaamua yaishe ilimradi
apate mtoto wake. Akafuta machozi akatulia huku akimshukuru Mungu kumpata mtoto
wake. “Yameisha Geb.” Geb akabaki na maswali kwa ukubaliji ule wa jumla.
“Yameisha umesamehe au umekubali yaishe?” “Vyote. Chamsingi ni mtoto wetu akue
na tumpe yale sisi tuliyoyakosa. Nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kumlea tena mwanangu.
Nakuahidi kuitumia vizuri.” Geb alipooza toka rohoni. Akaelewa Nanaa ndio
anachora mstari bayana. Haitakuwa kama zamani, ameharibu kwa Nanaa. Hawezi
kumpokea tena kama mpenzi ila mzazi mwenzake.
“Kwa hiyo usiku wa leo tunafanyaje? Unaniruhusu
kulala naye hapa halafu asubuhi ndio nirudi naye nyumbani kwako au
unataka turudi sasa hivi?” Nanaa akauliza. Lile swali liliendelea kuonyesha
wazi msamaha ule ni wakurudiana kama wazazi wa mtoto lakini sio wapenzi.
Akakumbuka ile hali aliyoiacha pale nyumbani kwake. Meza zilizovunjwa na pacha mwenzie,
makochi yalivyochanwa akaona asimrudishe pale Nanaa. “Ngoja nitoke kidogo,
nitakuwa hapo nje kuna simu nataka kupiga. Kisha nitarudi na jibu kamili.” Geb
akatoka.
Baada ya muda akarudi. “Kuna kitu nataka
kurekebisha pale nyumbani. Naomba nivumilie kwa siku chache, tutarudi nyumbani.
Lakini naomba tuhame hapa hotelini twende kwenye Apartment kwa muda. Nimepata
nafasi, wameniambia tunaweza kwenda hata sasa hivi. Hapa kuna kelele za baa, siwezi.”
Nanaa akacheka kidogo. “Nilipachukua kwa kuwa bei ni rahisi, halafu nilipanga
kulala usiku wa leo tu.” “Kwa hiyo ni sawa tukihama?” “Hamna neno. Ila bado
sijamaliza mambo ya chumba, Geb. Nilazima kesho nikamilishe, nifunge mkataba wa
kile chumba. Nihakikishe napewa funguo kabisa. Kuna watu wengine
wanakigombania. Nikikamilisha hilo, nitaenda kuchukua vitu vyangu kwa Antii,
nivifungie hapo. Nikikamilisha hilo nakuahidi nitatulia. Vitu vingine vya hicho
chumba, nitanunua taratibu. Siku ambazo najua utakuwepo nyumbani kama jumamosi
na jumapili, ndio nitakuwa nikitoka kwenda madukani. Sitarudia kutoka tena
jioni. Hata kesho nataka kumuomba huyo mwenye nyumba, tukutane asubuhi.” Geb
akanyamaza kwa muda.
“Nitajitahidi nisichelewe kurudi.” “Ni wapi?”
“Kipo mtaa wa Temeke, karibu na benki ya NMB. Ni chumba kizuri tu.” “Utataka
tukusindikize mimi na Liv?” “Mmh! Wewe na mwanao huyu mmekaa kitajiri sana
bwana. Mtaniponza kama wakati ule. Unakumbuka?” Geb akacheka kidogo.
“Unatukimbia mimi na Liv?” “Mwanao huyo ndio kabisaa. Nikienda naye watajua
nimezaa na mzungu mwenye pesa. Labda nimvue hizo cheni na hereni zake za
dhahabu. Nimfunge kitambaa kichwani na..” “Basi. Mimi naona wewe uende tu.”
Nanaa akaanza kucheka.
“Utarudi, Nanaa?” “Kwa nini unauliza hivyo Geb,
jamani!?” “Nauliza tu.” “Hata nikitaka niondoke, sina pakwenda. Lazima nirudi
kwa Liv. Nimekuwa bila mama, Geb. Najua ugumu wake, na umuhimu wake. Nitalipa
garama zote kuwa na Liv. Hata ikigarimu furaha yangu! Sitajali, nitakaa na
mwanangu. Niambie tu muda gani utakuwa na nafasi ili uje ukae na mtoto mimi
niende. Nitajitahidi kufanya haraka sana ili nirudi.” “Natamani kukuomba tena
usitafute chumba!” Nanaa akanyamaza.
“Nina nyumba mbili za kuishi, Nanaa.” “Ni zako
Geb. Mimi siku ile uliponifukuza na kuniambia nitoke, nilikuwa nikilia mengi! Kwanza
nilikuwa sijui niende wapi asubuhi ile. Kulikuwa na baridi na tayari nilikuwa
nimeshachafuka kwa damu. Pili niliingiwa na hofu ya mtoto wangu. Ile baridi
pale nje ilivyokuwa ikinipiga, nilikumbuka vile mama mkubwa alivyokuwa
akinifungia mlango nje, ananiambia nilazima nifue mpaka nimalize ndipo nirudi
ndani. Sitasahau Geb. Ilikuwa ni baridi kali mpaka vidole vilikuwa vikiganda.
Unakuta hapo sina sweta, na nimeambiwa nifulie nguo nje. Upepo mkali, unafua
huku unatetemeka baridi! Na huwezi kufua vibaya, kwa kuwa ukimaliza, unatakiwa
kumwita atoke nje akague kwanza, ndipo akiridhika uingie ndani uendelee na kazi
za ndani. Ukichelewa kumaliza ukakuta mlango umefungwa, ndio ujue nitalala hapo
nje mpaka kesho yake asubuhi wao wakiamka, ndio wanifungulie.” Nanaa akaanza
kutokwa na machozi.
“Nilikuwa nikilia
siku ile pale nje kwako, nikiomba Mungu anirehemu. Nilikuwa nikimwambia Mungu
ni heri angeniua siku namzaa huyo mtoto, kuliko kuruhusu nipokonywe. Niliingiwa
hofu, nikawa najiambia ukifungua mlango, nitakuomba hata unipe kazi ya
kusafisha kama wale vijana wanokuja pale kukusafishia nyumba yako, ili tu niwe
karibu na Liv wangu. Na nikajiambia, kama hutanifungulia mlango, ule ndio
ungekuwa mwisho wangu. Ningejiua Geb. Nilijua hamna mtu angepata hasara, na
hamna mtu angejua. Nilipanga nikajiulie sehemu ya mbali ili watu wasihangaike
na maiti yangu. Ndio maana hata ulipokuwa ukinipokonya mtoto, hutaki nilale
naye kitanda kimoja, nilijiambia ni afadhali hivyo kuliko kukosa kabisa.” Geb
akanyamaza kimya na Nanaa akanyamaza, akabaki akifuta machozi.
“Tunaweza kuondoka sasa hivi?” Geb akavunja
ukimya. “Hamna shida. Lakini bado hujaniambia kesho utakuja kukaa na mtoto saa
ngapi ili niweke miahadi na huyo baba mwenye nyumba.” “Nafikiria swala la Liv.”
“Nitahakikisha nakuachia maziwa yakutosha.” “Hataki chupa kabisa huyo mwanao.”
Nanaa akamwangalia mwanae aliyekuwa amepitiwa na usingizi huku chuchu ya mama
yake ipo mdomoni. Akabaki akimwangalia nakumpapasa taratibu. “Asante Geb.” “Kwa
nini tena? Maana najisikia vibaya sana Nanaa. Natamani kama ningebadili lile
tukio.” “Nakushukuru kwa nafasi uliyonipa ya kumlea mwanangu.” Geb akabaki
kimya, akashindwa hata kujibu.
Nanaa &
Geb Kwenye Apartment.
W |
alitoka
hapo, wakahamia kwenye apartment nzuri na ya kisasa. Ilikuwa na vyumba viwili
tu, jiko zuri na sebule iliyojazwa na kupangwa makochi na meza nzuri. Nanaa
alienda kukaa sebuleni akiwa amempakata mtoto wake. “Kabla sisi hatujaenda
kulala, naomba simu yako nimtaarifu mama kuwa tupo hapa.” Geb akamwangalia
kidogo, akampa simu yake. Nanaa akampigia Mama G. “Pole mama, nimekuamsha?” “Wala
usijali mwanangu. Umemuona cha ulizi wako? Wamekuletea huko huko.” Nanaa akacheka. “Mimi sijui huyu Liv amefuata
wapi kulia hivi! Mimi si mlizi hivi. Amelia hoteli nzima wakajua kama amefika!” Mama G, akacheka. “Jike la nguvu huyo. Akifika
mahali lazima watu wote wajue kama Oliva Magesa yupo. Sio watu wakae kihasara
hasara.” “Mwenyewe huyooo!” Nanaa alimtania Mama G.
“Kumbe! Unamuona kwa wasiwasi?” “Hata kidogo, mama. Basi
alivyo huyu mjukuu wako, ametulia sasa hivi kama sio yeye. Hataki hata kuamka.
Tumehama hotelini tumehamia kwenye apartment, njia nzima namwita aamke ili
tuongee, ameninyamazia kimya. Tabia gani hiyo!?” “Mwache apumzike. Amelia
sana.” “Jamani Liv wangu! Siku nyingine sitamuacha tena.” “Wakati kesho unamuacha
tena!?” Geb akaingilia mazungumzo.
“Halafu kweli. Ujue amekataa kunyonya kwenye chupa?”
“Ameshakujua huyo. Na unavyombembeleza wakati ananyonya, basi anajua ndio
anatakiwa afanyiwe hivyo hivyo! Mbona unae huyo.” Nanaa akacheka. “Naona raha mwenyewe!”
“Nakusikia hata sauti imebadilika.” “Asante mama yangu.” “Asubuhi
nitakupitishia chakula.” “Mama wewe! Pumzika bwana! Nitaagiza chakula hapa
hapa, kuna sehemu ya mgahawa.” “Basi maziwa yatakauka. Huko hotelini hawawezi
kukutengenezea uji kama ninaokupikia mimi! Mbona unataka kunipunguzia shuguli?” Nanaa alicheka mpaka
machozi.
Geb akabaki akimtizama anavyoongea na mama yake. “Mimi nilitaka upumzike.”
“Hata! Acha nimuhudumie wajina wangu. Nataka awe kama mimi. Mungu amjalie afya
njema, ampe umri mkubwa, ashike wajukuu na vitukuu vyake.” “Amina mama yangu.
Basi nakusubiri hiyo kesho.” “Nikuletee nini?” “Ngoja nitakutumia kwenye
ujumbe.” Wote
wakacheka, wakaagana.
~~~~~~~~~~~~~
“Mama amefurahi sana kumpa mtoto jina lake.” “Eti
eeh!” “Sana. Lakini pia anakupenda. Mama anakupenda sana Nanaa.” “Ni kweli.
Nilihisi hivyo. Ndio maana nilipokwama na mtoto, yeye pekee nilijua ndio
atakuwa kimbilio langu. Na wala hakubisha. Nilimpigia tu nikamwambia naomba
uje, nina shida sana. Hakuuliza hata maswali mengi, akaja. Alinifariji sana.
Bila yeye nahisi nisingeweza kufanya mtihani. Nilikuwa namfukuza aondoke
akapumzike lakini hakutaka kuniacha peke yangu na mtoto. Alihakikisha
aninisaidia na Liv mpaka wewe alipokuja kumchukua. Namshukuru sana Mungu kwa
kunipa mama kama huyu, sikuwahi kupata mtu kama yeye.” Geb akabaki kimya.
“Geb!” Nanaa akaita. “Naomba kesho mama akija,
anisindikize kwenye hicho chumba nikiwa na Liv ili nisimuache tena peke yake.
Kama ukikubali, nataka nimuombe mama twende naye, halafu abaki na Liv kwenye
gari, mimi wanishushe mbali kidogo, nitatembea mpaka kwa huyo mwenye nyumba.”
“Naomba mimi nilipie, Nanaa.” “Hapana Geb. Una mambo mengi sana. Usiwe na
wasiwasi na mimi, nina pesa.” “Unapata wapi pesa na wewe huna kazi?”
“Unakumbuka nilikuwa na mkopo wa chuo wa asilimia 85? Kaka naye alikuwa
akinitumia pesa, halafu ule mshahara mliokuwa mkinilipa wakati ule nawafanyia
kazi kwenye kampuni yako, nilikuwa najiwekea akiba. Halafu Liv nilijifungulia
hospitali ya serikali, wala sikutumia pesa nyingi. Kwa hiyo ninayo pesa
yakujitunza kwa sasa. Wewe mwangalie mtoto wako tu. Usinifikirie mimi hata
kidogo. Nipo sawa kabisa.” “Wala hunisaidii hivyo. Unazidi kuniumiza.” “Naomba
kabisa uwe na amani Geb. Kwa sasa ni kweli sihitaji msaada wa mtu yeyote yule.
Nilichokuwa nataka ni mtoto wangu, na umenipa. Asante.” Geb akanyamaza.
“Hujajibu Geb.” “Ni sawa. Nyinyi nendeni tu.”
Nanaa akatulia tena kidogo. “Naomba nikuombe kitu cha mwisho.” Geb
akamwangalia. “Naomba usiku wa leo nilale na Liv. Kesho nitakuachia, lakini angalau leo tumfanye asilie tena.” Tayari
machozi yalishaanza kumtoka Nanaa. Geb aliinama kwa muda. “Naomba iwe kwa usiku wa leo tu. Tafadhali Geb.” “Ni
sawa. Hamna neno. Hata hivyo sasa hivi naona anakufahamu na kukuhitaji wewe
zaidi.” “Asante. Nakushukuru sana.” Nanaa
akajifuta machozi, akanyanyuka na mtoto wake.
“Sisi
tutachukua hiki chumba kidogo.” Nanaa aliongea akiwa katikati ya hivyo vyumba
na Geb yupo sebuleni lakini hakujibu. Akaingia kwenye hicho chumba, akamlaza
mtoto wake vizuri baada ya kumbadilisha, akapanda kitandani. Akamkumbatia mtoto
wake, akaanza kulia taratibu. Geb alisimama nje ya mlango akimsikiliza jinsi
anavyolia. Alikuwa akitoa kilio cha sauti ya chini. Lakini alilia kwa uchungu
sana. “Nakupenda Liv. Unakumbuka nilikuahidi
hatutaachana? Ona Mungu ametusaidia tupo wote pamoja! Na leo tunalala wote tena.
Mungu akitusaidia hatutatengana kwa muda mrefu. Nakuombea uzima mwanangu. Hata
hapa tutapita tu.” Aliendelea kuzungumza na mwanae kwa upendo, kwa sauti
ya chini yenye kilio. Geb alisimama pale akisikiliza, uzalendo ukamshinda
akaamua kuingia.
Nanaa akakaa kwa haraka kama aliyekosea. Akabaki
anababaika. “Nimekushitua?” Geb akamuwahi kama kumtuliza, akaenda kukaa kwenye
kile kitanda. Nanaa akajiweka sawa, akamfunika mtoto wake vizuri na kumsogeza
pembeni kidogo kama kumuonyesha Geb kuwa hakuwa amemkumbatia. “Naomba
unisamehe, nilikukosea.” “Yameisha Geb! Hakika
nimesamehe.” Alijibu huku akifuta machozi. “Unauhakika?” “Kweli Geb. Nimeshatendwa sana. Nimeumizwa mnoo.
Nikajifunza kusamehe kabla sijaombwa msamaha. Nilielewa na kukusamehe kabisa.
Huwa nafanya hivyo kwa ajili yangu mwenyewe. Nimejawa na furaha ambayo siwezi
kueleza. Siamini kama nimepata bahati ya kulala na mwanangu hivi. Niliingiwa
hofu sana. Sikujua kama ipo siku nitarudi kulala na Liv wangu na kumkumbatia
kwa uhuru hivi. Niamini kuwa nalia kwa furaha, sio kwamba nina uchungu na
wewe.” “Sasa kwa nini hukutaka mama aniambie kama una mtoto wangu kama
ulishanisamehe?” Nanaa akafuta machozi, akajiweka sawa.
“Unakumbuka nilikwambia niliwaona siku ya harusi
mmeshikana mkono mnaingia ukumbini pamoja? Tena mlionekana mmetulia kama
wapenzi tu. Kuja kunisahau pale nje, huku nikijua upo na Liz ndani, ukweli
niliumia sana. Nakumbuka tulizungumza kwenye simu muda mfupi kabla ya pale
ukumbini. Ulijua wazi nilikuja pale kwa ajili yako Geb, na bado ukanisahau!
Halafu kilichoniumiza zaidi ni wewe Geb unayesifika kutosahau! Nikajiona kweli
nina mkosi. Mtu aliyeumbiwa kutosahau kila kitu ila Nanaa tu! Kwa hiyo ikaniuma
na bado nilikuwa na hasira. Lakini nikajiambia ni haki yako na Liv kufahamiana.
Nikaamua kuja kukwambia tu. Sasa tena nikaja, nikawakuta tena na Liz! Halafu wote mpo uchi! Nilijua
mlisameheana na kuamua kurudiana. Nikaona nisubiri kwanza ili nisije kuonekana
kama natumia mtoto kama chambo ya kukuvutia kwangu. Kumbuka nilikwambia nilimtaka
mtu anayenipenda mimi kama Nanaa. Awe anajua madhaifu yangu yote, na bado
anichague mimi.” Nanaa akaendelea taratibu.
“Sikuta kuja kuishi na wewe sababu ya mtoto.
Lakini ningekuja kukwambia siku moja baada ya kutulia. Sikutaka kujichanganya.
Yaani nipo kwenye mitihani, halafu niwe
nakabiliwa na kesi za kujibu kwako au ndugu zako! Sikutegemea kama Liv angekuja
katikati ya mitihani Geb. Ulikuwa mshituko kwangu. Halafu sikujua
utamchukuliaje. Kama utamkubali au la. Kwa hiyo hayo yote nilijiambia nitakuja
kujua baadaye. Nikiwa nimeshatulia kwangu, nimepata kipato cha kueleweka ndipo
ningekutafuta kukutaarifu tu, sio kuanza kukulia shida.” Nanaa akafikiria
kidogo, kisha akaendelea.
“Sikutaka kuzunguka na
Liv kama mzigo ambao nataka kumuachia mtu, halafu akaishia kukataliwa kama mimi
nilivyokataliwa au ninavyokataliwa na watu. Geb, niamini nikikwambia kuwa
inauma sana kujua watu wanakukataa. Wanakuona mzigo, hawakutaki! Inauma kuliko
kitu chochote. Na maumivu yake hayana tiba hata iweje, hayaponi. Inaathiri kila
eneo la maisha yako. Sikutaka Liv apite nilipopita mimi. Kwa kuwa nilishafanya
kosa kama la mama yangu kumleta duniani bila makubaliano au tuseme bila ndoa,
sikutaka kuendelea kurudia historia yangu na mama yangu kwa Liv. Sijui
umenielewa?” “Nimekuelewa Nanaa. Nahisi hata mimi ningefanya hivyo hivyo.”
Wakatulia kwa muda. “Tutaongea zaidi kesho. Pata muda wa kupumzika. Naomba
usilie.” Nanaa akanyamaza. “Usiku mwema.” “Asante na wewe.” Geb akatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Asubuhi Mama G alifika hapo na vyakula. Geb
alipata kifungua kinywa akaondoka kwenda kazini na kuwaacha hapo. Vilijaa
vicheko kati yao, mwishowe wakatoka. Alisindikizwa na Mama G, akakamilisha
mambo yake ya chumba. Alilipia pesa na kukabidhiwa funguo. Alirudi kwenye gari
alipokuwa amemuacha mama G na mwanae, machozi yakimtoka. “Ni nini tena? Umekosa
hicho chumba?” Mama G akauliza. “Sasa hivi na mimi
nina kwangu mama. Nanaa naye ana kwake!” Mama G akacheka. “Nimelipia kila kitu. Nimemalizana na dalali pamoja na
mwenye nyumba wangu. Ona funguo hizi hapa. Funguo za nyumbani kwangu mama.
KWANGU!” Nanaa akaweka msisitizo. “Hongera.” Mama G alikuwa akicheka
huku akimwangalia jinsi alivyofurahia.
“Naomba unisindikize kuchukua tena mizigo yangu.
Au umechoka?” “Mimi leo nipo kwa ajili yako. Nizungushe utakavyo.” Nanaa
akacheka. “Basi twende kwa Antii.” Mama G akaondoa gari, Nanaa akamuelekeza
mpaka nyumbani kwa Antii, Chuo Kikuu cha Mlimani. Walipofika, Nanaa akamwambia
mama G asisumbuke, akae tu kwenye gari yeye ataleta vitu. Akashuka. Hakumkuta
Antii, lakini alijua wapi pakuchukua funguo. Akaanza kuingiza vitu vyake kwenye
gari ya mama G, huku akivipanga vitoshee. Bado Liv alikuwa amelala.
Nanaa akaendelea kusombelea na kuvipanga taratibu
kwenye gari ili asimsumbue mtoto wake mpaka akamaliza. “Nimemaliza mama. Naomba
kabla hatujavipeleka hivyo vitu vyangu kwangu, tupitie kwenye ofisi za utawala,
kuna kitu nataka nikaweke sawa.” Nanaa akatoa tabasamu aliposema neno ‘kwangu’. “Naona umefurahi!” “Sana mama
yangu. Angalau sasa hivi nina kimbilio. Hata nikifukuzwa, ninapo pakwenda.”
“Sasa mbona huna hata kitanda?” “Taratibu mama. Kwa kuwa sasa hivi ninapo
pakuishi, nitanunua vitu vyangu kimoja baada ya kingine mpaka nikamilishe kuwe
kwa kueleweka.” Nanaa alijibu kwa upole lakini akiwa amejawa na furaha.
“Nakuhakikishia Nanaa, Geb hawezi kurudia tena
upuuzi alioufanya. Anajutia sana.” Nanaa akanyamaza wakati mama G akiendelea
kuendesha wakielekea kwenye ofisi za Utawala chuoni hapo. “Msamehe.”
“Nimesamehe mama, hata yeye nimemwambia nimeshasamehe kabla hata hajaomba
msamaha. Huwa nafanya hivyo kwa ajili yangu mwenyewe, mama. Nimepita pagumu
sana. Kama ingekuwa kuweka visasi moyoni, nisingeweza kuwa hapa. Ningeshindwa
kuendelea na maisha.” Nanaa akacheka kidogo. “Nimejiwekea kama katabia. Kama
mtu ameniumiza sana, nikaumia, huwa namtafutia sababu ya kwa nini alinifanyia
hivyo, ili tu kupata sababu ya kusamehe, kujipa amani moyoni, au kujifariji ili
niendelee na maisha.” Mama G akamuhurumia sana Nanaa.
Walifika kwenye ofisi za utawala, Mama G
akaegesha kwenye kivuli, Nanaa akashuka akamuacha Oliva akiwa bado amelala
kwenye kiti chake. “Kama watu sio wengi, sitakawia mama yangu. Nivumilie.”
“Wewe usiwe na wasiwasi na sisi. Maliza mambo yako kwa utulivu.” Nanaa akatabasamu
huku akichukua pochi yake, akaondoka. Alibahatisha kujikuta yupo peke yake pale
ofisini. Akamuulizia muhusika ambaye angeweza kumsaidia kumpatia matokeo yake
yote ya nyuma. Trascript. Akaambiwa lazima kujaza kwanza form baada ya
siku mbili ndipo arudi kuchukua transcript yake. Alipomaliza kujaza,
akatoka.
Wakati akiliendea gari ya Mama G, aliangusha
karatasi na kalamu alizokuwa ameshika mkononi. Akainama kuokota, lakini
karatasi ilianza kupeperushwa na upepo. “Ngoja nikusaidie.” Kijana mmoja
mtanashati alianza kukimbiza karatasi ya Nanaa huku akiacha harufu nzuri nyuma,
alimfanya Nanaa asimame abaki akimsubiria arudi na ile karatasi, na Mama G
alibaki akiwaangalia kwani Nanaa alikuwa amekaribia kabisa garini. Kila
aliposogelea ile karatasi na yenyewe ilisogea, na yeye hakukata tamaa. “Lazima
nikupate wewe karatasi, huwezi kunishinda.” Walimsikia akiongea, Nanaa akacheka
taratibu huku akimwangalia kwa nyuma. Alihangaika mpaka akaikamata. “Told you!”
Yule kaka alianza kuiongelesha ile karatasi kwa sauti ya ushindi baada ya
kuiokota. Nanaa akacheka akainama huku ameficha mdomo kwa kiganja.
Ya Kale…
“Penye nia, pana njia.
Karatasi yako hii hapa.” Nanaa akanyanyua kichwa kupokea. “Zac!” Nanaa alishituka
sana, hakutegemea. “Nanaa!” Yule kijana alijibu. Alikuwa Zac, kipenzi wa zamani
wa Nanaa. “Zac!” Nanaa alirudia safari hii
akiwa na machozi. “Nanaa mpenzi!” Zac alimkumbatia. Hakuwahi kuruhusu Nanaa
alie mbele yake.
~~~~~~~~~~~~~
Mara ya mwisho wapenzi hao waliachana Zac akiwa
amepiga magoti nje ya daladala, Nanaa ndani ya daladala akilia. Zac aliumia
kumuona Nanaa akilia na yeye kushindwa kumbembeleza. Alishawishika kuingia na
yeye ndani ya daladala, lakini akajua Nanaa anarudi nyumbani kwa kaka yake,
hakutaka mwanzo wa mahusiano yake na shemeji yake uwe wa habari ya fumanizi
lake. Alimbembeleza Nanaa ashuke wayamalize, lakini Nanaa hakutaka hata
kumgeukia. Aliendelea kulia ndani ya daladala hiyo akikumbuka ahadi kemkem
alizokuwa ameahidiwa na Zac. Penzi alilokuwa akipewa na Zac. Kitanda kile kile
alichokitumia kumridhisha Zac, ndicho hicho hicho alikitumia classmate
mwenzake Zac, kumpa yale yale aliyokuwa akiyapokea kutoka kwa Nanaa. “Nibaki au
nirudi? Ili iweje wakati anauwezo wa kupokea kwa msichana mwingine, kile
nilichodhani ni cha thamini, alichoahidi kukipata kutoka kwangu tu?” Nanaa alijiuliza wakati akiendelea kulia ndani ya
daladala.
Ni
kweli alijua kwa hakika Nanaa ndiye atakaye kuwa mkewe. Lakini ni nini
kilimpelekea kulala na msichana mwingine, tena aliyemjua Nanaa kwa muda wote?
Ni swali ambalo alishindwa kuwajibu wengi walio yajua mahusiano mazuri
aliyokuwa nayo na Nanaa na wengi waliitamania couple yao. Walishangaa
kuweza kumsaliti msichana kama Nanaa aliyekwisha kujigamba kwa kila mtu kuwa ni
lazima atamuoa yeye. Kwa kumwangalia tu Nanaa, utajua ni binti aliyetulia. Hata
rafiki wa Zac walimpongeza na kumsifia Zac wazi wazi kuwa Nanaa ni ‘wife
material’. Kwamba ni mke wa kuoa na kuweka ndani. Zac naye alishajisifia
nyumbani kwao kuwa akimaliza tu chuo, atawapelekea kifaa chakufunga mwaka. Kwa
hiyo hata nyumbani kwa kina Zac, walishazisikia habari za Nanaa, wakabaki
wakisubiria atokee.
~~~~~~~~~~~~~
Zac alizidi kumkumbatia Nanaa kwa nguvu akimvutia
karibu kabisa na mwili wake, huku ameinamisha kichwa chake kwa Nanaa akimbusu
kichwani, kwenye nywele zake. “Nanaa!” Zac aliendelea kuita taratibu kwa sauti
iliyojaa hamu, mapenzi na hakika alionekana ni mwanaume anayempenda Nanaa.
Nanaa aliendelea kulia huku amekumbatiwa. Alikuwa na machungu ambayo alijua kwa
Zac, ndio sehemu sahihi ya kuyatolea. Zac alijua kumbembeleza.
Mama G alikaa sawa akabaki akiwaangalia na
kusikiliza. Kwa hakika vile walivyokumbatiana haukuonyesha kama ni ukaribu wa
kawaida. Mama G, alijua wazi walikuwa wapenzi. Nanaa alishindwa kujitoa kwenye
mikono ya Zac. Wazi alionekana ni mahali anapofurahia kuwepo. Alijisahau kabisa
kama yupo mbele ya macho ya mama yake Geb. Alilia huku akikumbuka shida zake
zote tokea waachane na Zac. Zac alijua kumtuliza Nanaa. Kwa kilio kile, Zac
alijua wazi lipo jambo kwa Nanaa. Je bado anamaumivu ya kumfumania au kuna
jingine linaendelea ndani yake? Hilo ni swali Zac aliendelea kujiuliza wakati
akishindwa kumuachia.
“Lakini
anaonekana na hali nzuri sana kimaisha! Nanaa amependeza zaidi. Hiki kilio ni
cha nini tena kwa mpenzi wangu?” Zac alijiuliza huku akiendelea kumkumbatia na
kumbusu Nanaa aliyekuwa akiendelea kulia kwa kwikwi. Aliendelea kumkumbatia
huku akipitisha mikono yake mgongoni taratibu, kama kumbembeleza huku akimbusu
kichwani. Nanaa alitamani kuongea kitu lakini akashindwa. Ni kama kitu
kilimkaba kooni.
Zac alimvuta mbele kidogo kumwangalia. “Pole
mpenzi wangu. Nimekuacha peke yako!” Mama G, alisikia Zac akimwambia Nanaa
aliyebaki ameinama huku akifuta machozi. “Sijawahi kukusahau Nanaa. Bado
nilijua nitakupata tu. Umeolewa?” Nanaa akatingisha kichwa kukataa. “Una
mchumba?” Mama G akajiweka sawa kusikia jibu la lile swali. Alitamani kujua
Nanaa atajibu nini. “Nanaa!” Zac akaita tena. “Naomba usilie mpenzi. Unajua
nachukia kukusikia ukilia.” Nanaa akafuta machozi.
Zac alivuta mkono wa kushoto wa Nanaa. Alipoona
hauna pete, akaubusu. “Afadhali. Nilidhani nimeshachelewa!” Nanaa akacheka huku
akifuta machozi. “Nilizimiss hizo dimpozi zako!” “Nilibahatika
kupata mtoto.” Nanaa akaongea kwa upole. “Hongera.” Nanaa akatoa
tabasamu, wakabaki wakiangaliana kwa muda. “Nina hamu na wewe Nanaa!” Nanaa
akanyamaza, kama anayefikiria kitu. Alipokonya simu ya Nanaa, akajipigia na
kuandika namba yake. “Sitaki kukupoteza tena.” Kisha akamrudishia na busu la
kichwani. “Usilie Nanaa wangu. Usilie mpenzi.” Nanaa akajifuta machozi.
“Unafanya nini hapa?” Nanaa akauliza taratibu.
“Nimekuja kufuatilia transcript yangu. Yakwanza nilipoteza, nikaandika
barua ya kuomba nyingine. Leo waliniahidi itakuwa tayari, ndio nimeifuata.
Umependeza sana Nanaa.” Nanaa akacheka na kuinama. “Na wewe unafanya nini
hapa?” “Na mimi nilifuatilia transcript.” “Unataka kuendelea na chuo?”
Zac akauliza. “Hapana. Hali yangu haijabadilika sana Zac. Ni Nanaa yuleyule
uliyeniacha. Naishi kwa rehema za Mungu. Sina uwezo wakurudi tena chuo. Sasa
hivi nimepata bahati ya kumlea mwanangu, nalea, akikua kidogo nahisi baba yake atamchukua, ndipo naweza kutafuta kazi.” Zac
aliona machozi yakimtoka tena Nanaa.
Zac
alikunja uso. “Baba yake akimchukua tena? Sijaelewa.” “Ni habari ndefu Zac.
Lakini kwa sasa, naishi na baba wa huyo mtoto wangu. Kwa ajili ya kumlea mtoto
wetu. Ni mdogo sana, bado nanyonyesha, ndio maana nipo nao. Lakini..” Nanaa akashindwa kuendelea kuongea
akainama nakuanza kulia kwa kwikwi. Zac akamuhurumia, akajua yapo mengi
yanaendelea. Nanaa alikuwa mpole kwa asili. Alimvuta tena akamkumbatia.
Alimbembeleza kwa muda. “Naweza kuingia hapo
ofisini nikachukua hayo matokeo yangu, kisha twende mahali?” “Hapana Zac. Nipo
na mama yangu na mtoto, wapo…” Nanaa akageuka ili kumuonyesha alipokuwa
ameiacha gari ya Mama G, akashituka sana kujikuta kumbe wamesimama hatua chache
sana kutoka lilipo gari hiyo. Wakabaki wakiangaliana na Mama G. Zac
akamwangalia Mama G, akamwangalia Nanaa aliyekuwa ameinama.
“Nanaa! Umesema mama!?” Zac aliuliza kwa mshangao
kwani aliijua historia ya Nanaa vizuri sana. “Ni mama yake huyo mzazi mwenzangu.
Lakini nimemzoea sana, mpaka najisahau.” “Ohh! Nimeelewa. Shikamoo mama.” Zac
akasalimia. “Marahaba Zac mwanangu.” Nanaa akashituka akanyanyua uso
kumwangalia Mama G. “Amelifahamu vipi
hilo jina la Zac, wakati bado sijamtambulisha?” Akajiuliza, Zac akatoa
tabasamu la mshangao huku akimwangalia Mama G, Nanaa aliona.
“Kwani
mnafahamiana?” Nanaa akauliza kwa upole. “Nimesikia jina lake sasa hivi wakati
unamtaja.” Mama G, alijibu akiwa ametulia kabisa. Nanaa aliinama akajua wazi
Mama G, amesikia kila kitu. Ukimya ukapita kwa muda kati yao, huku Nanaa akiendelea
kupokea taarifa kuwa yule alikuwa mama yake Geb. Akabaki ameinama akifikiria
itakuaje baada ya hapo. Alikumbuka vile alivyokuwa akilia kifuani kwa Zac, na
kupokea mabusu mfululizo muda mfupi uliopita, tena bila kupinga.
Ukweli mama G alikuwa mama yake Geb. Alimpenda
Nanaa kwa upendo uliokuwa ukimfanya Nanaa asahau kama yule si mama yake. “Itakuaje tena baada ya hapa? Bado
ataendelea kunipenda na kuniheshimu kama zamani? Atamsimulia Geb! Lakini
sitajali hata kama Geb akijua. Sio mpenzi wangu na amenionyesha wazi
hanihitaji. Liv wangu je? Bado atampenda?” Nanaa aliendelea kuwaza.
“Nanaa!” Zac akamuita kama kumtoa mawazoni.
“Abee!” Aliitika kwa upole akanyanyua uso huku ameegemea gari ya mama G.
“Naomba tuonane baadaye.” Zac aliomba kwa utulivu. Sauti yake ilionyesha
mapenzi makubwa kwa Nanaa. “Saa ngapi?” Bila kufikiria, Nanaa alijikuta
akiuliza swali lililomshangaza Mama G, wazi alionyesha anataka kumuona tena
Zac. “Muda na wakati wowote. Niambie wewe.” Nanaa akafikiria kidogo. “Hata sasa
hivi.” Zac akaongeza. “Sasa hivi sitaweza, Zac. Kwa mara ya kwanza nimepata
kwangu.” Nanaa alimtolea Zac kicheko. Zac akaonekana kuelewa kile kicheko.
“Finally!” Zac alijibu kwa kucheka. “Finally, Zac! Hatimaye na mimi nina
kwangu.” Nanaa aliweka msisitizo. “Hongera sana. Am proud of you!” Nanaa
akacheka.
Kama aliyekumbuka kuwa kuna mama Geb pale
anawasikiliza, akaacha kujichekesha. Akaendelea. “Kwa hiyo leo ndio
nimekabidhiwa funguo. Usifikiri ni nyumba, ni chumba!” Zac akacheka. “Hata kama
ni chumba kimoja, bado nakupongeza Nanaa.” “Asante.” Nanaa akajibu kwa furaha.
“Kwa hiyo leo ndio nahamia huko.” “Naweza kukusaidia kuhama.” Zac aliongeza
nakumfanya Nanaa acheke. “Hujabadilika Zac!” Zac akatabasamu. “Nifanye niwe
mikono yako. Wewe ongea tu, nitakuwa nakufanyia kila kitu. Nitakubebea vitu
vyako, na tukifika nitakupangia.” Nanaa akacheka, akainama kama anayekumbuka
kitu.
~~~~~~~~~~~~~
Mawazo yalimrudisha zamani akiwa na Zac. Wakati
mwingine alikuwa akimuomba kazi. “Naomba nipe kazi, Nanaa.” Zac alikuwa
akimwambia nakumfanya Nanaa acheke. Wakati mwingine alipokuwa akila, alimuomba
kazi yakumlisha, huku akimwambia yeye afanye kazi ya kutafuna tu. Na alimlisha
mpaka chakula kinaisha. Siku alizokuwa na Zac, hakujigusa. Zac alimfanyia kila
kitu. Yeye alikuwa akilala kitandani tu, huku Zac akimuomba amtume. Zac
alimpenda na kumtumikia Nanaa bila kuchoka. Ndiye mwanaume aliyeonyesha
kumsikiliza kila wakati na kujali hisia zake. Hakuchoka kumtafuta na kumjulia
hali. Tena endapo atapiga na kumkuta Nanaa hana furaha, ni lazima atamtafuta
ili ajue kulikoni. Swali ni kwa nini alimsaliti, ndilo lilimtesa sana
Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~
Alinyanyua uso ukiwa na tabasamu, akakuta wote
wanamtizama. Akajaribu kujibaraguza kwa kujishika hapa na pale akitafuta neno
la kuongea tena, akababaika kidogo kwa kuwa Mama G, alikuwa ametulia ndani ya
gari akimtizama tu. Akakumbuka ombi la Zac. “Sina vitu vya kuhamisha Zac. Ndio
naanza maisha.” “Hata kitanda tu nitabeba.” Zac akaendelea kubembeleza. “Huwezi
amini hata kitanda sina. Naanza kupeleka urithi wangu, upo hapo nyuma ya gari.
Vitabu na madaftari.” Zac akakunja uso.
“Utalala wapi sasa?” Akamuuliza. “Nilikwambia kwa
sasa naishi kwa mzazi mwenzangu, nikimlea mtoto.” Nanaa akajibu nakuongeza.
“Njoo umuone mwanangu Zac.” “Ngoja kwanza Nanaa, sasa kama unaishi naye,
nitakuona vipi? Akikukatalia kuja kuniona?” Tayari Zac alipatwa na wivu na
Nanaa akajua, akacheka. “Tutaonana tu. Usiwe na wasiwasi. Tunaishi naye tu, sio
kama tuna mahusiano. Na sio kwamba tunaombana ruhusa. Hapana. Ni kuagana tu.
Hata yeye huwa akitoka hasemi anakwenda wapi, au anarudi saa ngapi. Kikubwa ni
mimi niwepo pale na mtoto, au yeye mwenyewe awepo na mtoto. Hajali wapi
ninakwenda, ilimradi nisichelewe kurudi.” Zac akashangaa sana, lakini kwa
upande mwingine akashukuru Mungu.
“Daah! Lakini afadhali yangu.” Nanaa akacheka.
“Nitakuona jioni, Zac. Ngoja tuwahi, nisimuweke mama.” “Saa ngapi sasa?” “Mpaka
yeye arudi, ili nimuachie mtoto, ndipo nitakutafuta.” “Una uhakika Nanaa?
Naomba usinidanganye.” “Sina sababu ya kukudanganya. Hata mimi nataka kukuona.”
Zac akacheka kwa furaha. “Basi nitakuwa na simu karibu sana kusubiria simu yako.
Naomba nimuone mtoto.” Nanaa akasogea mpaka mlango wa nyuma, akafungua na
kumpisha Zac.
Zac alisimama pale akabaki akimwangalia yule
mtoto. “Anaitwa Oliva.” Zac alivuta pumzi kwa nguvu, akatulia. Alimwangalia Liv
kwa muda. “Alitakiwa kuwa ni mtoto wangu huyu!” Zac aliongea kwa sauti ya chini
kama anayejutia. “Unakumbuka jina tulilokuwa tumepanga kumpa mtoto wetu wa
kike?” Zac alimgeukia Nanaa aliyekuwa kimya nyuma yake akimsikiliza, akamuuliza
lile swali. Nanaa akabaki tu kimya. “Daaah! Nilichezea shilingi chooni. Najuta
sana, Nanaa. Natamani nirudishe ile siku, lakini siwezi. Hamna siku inapita
nisijutie. Maisha yangu yameharibika kweli baada ya kuachana na wewe. Lakini
tutapata muda tutazungumza.” Nanaa akanyamaza, Zac akarudisha macho yake kwa
yule mtoto, akabaki akimtazama akiwa ametulia.
“Unamtoto mzuri sana Nanaa. Jamaa amebahatika,
ameibuka mshindi! Natamani ndio ningekuwa mimi!” Nanaa akacheka kidogo.
“Hongera mpenzi wangu.” Zac alitoka pale akasimama nje ya gari akimwangalia
Nanaa. “Asante Zac.” “Nategemea kukuona
jioni, Nanaa. Tafadhali usiache kunitafuta.” “Nitafanya hivyo.” Zac akatulia
kwa muda kama anayefikiria kisha akaongeza. “Nimefurahi sana kukuona Nanaa.
Sana.” Nanaa akacheka. “Tutaongea zaidi baadaye. Uwe na wakati mzuri. Mungu
akutangulie.” Ni usemi wa Nanaa aliokuwa akiupenda sana kwa Zac. “Amina mama.
Nimeshaanza kusubiria simu yako.” Nanaa akacheka. “Hata hatujaachana!?” “Ndio
ujue ni kiasi gani nina shida ya kuongea na wewe.” Nanaa akacheka tena. “Haya.
Akija tu baba yake Liv, nitakupigia tukutane.” Waliagana, Zac akaondoka
kuelekea ofisi za Utawala, Nanaa akapanda kwenye gari asijue anaanzia wapi na
Mama G.
~~~~~~~~~~~~~
Alitamani kama Liv angekuwa ameamka ili
ajibaraguze naye, lakini Oliva alikuwa amelala kama malaika! Akajiweka sawa
kitini. “Lakini hakuna nilipokosea.”
Akajitetea nafsini mwake. “Kwa hiyo huyo ndio Zac?” Alishituliwa na swali
kutoka kwa Mama G. “Ndiyo.” Nanaa akajibu kwa upole. “Anaonekana anakupenda
sana.” Mama G akaongeza. “Kipindi nipo naye, kama hata Mungu angeshuka,
akaniambia Zac asingekuwa mume wangu, ningesema sio Mungu. Alikuwa…” Nanaa
akatulia kidogo. “Nashindwa hata kusema. Alinipa mapenzi ambayo sijawahi pata
maishani. Hakutaka hata anihisi nilikuwa ninalia. Nikilia alikuwa anachanganyikiwa.
Alikuwa akipiga simu kutaka kusikia sauti yangu kila mara ili apate nguvu ya
kuendelea kufanya alichotaka kukifanya. Kama hakuwa akipiga simu, basi atatuma
ujumbe. Alikuwa akipenda kunisikiliza nikiongea, nikicheka ndio kabisaa.” Nanaa
akacheka na kumfanya Mama G, na yeye acheke kidogo. Aliongea kwa hisia.
“Una sauti nzuri, Nanaa. Inatia raha kusikiliza.”
“Sio kwa kila mtu mama.” Nanaa akajibu nakuinama. Mama G, akajua anamaanisha
sio kwa Geb. “Nini kilitokea?” Mama G akauliza swali. “Na yeye nilimfumania.”
Mama G alishituka kidogo, akamgeukia Nanaa, Nanaa akacheka. “Kweli mama.
Nilimfumania akifanya mapenzi na msichana waliyekuwa naye darasa moja! Tena
kwenye kundi moja la kujisomea! Wakati mwingine alikuwa akimfuata Zac
amfundishe peke yake. Lakini sikuwahi hata kuhisi. Kwa kuwa yule msichana
alikuwa na pete ya uchumba kidoleni, yaani alikuwa anasubiriwa na mchumba wake
amalize chuo, wafunge ndoa. Mchumba wake alikuwa akifanya kazi. Hakuwa
mwanafunzi kama sisi. Na vikao vya harusi vilishaanza. Yaani sikuwa hata
nikiwahisi chochote. Alijitahidi sana kujificha.” “Unafikiri walikuwa na
mahusiano ya muda mrefu?” “Sijui mama. Na wala sikusubiri kutaka kujua
ilikuaje. Niliondoka pale pale.” Nanaa akacheka.
“Mbona unacheka?” Mama G akatupia swali jingine.
“Nakumbuka vile Zac alivyokuwa akinikimbiza huku yupo nusu uchi. Kweli Zac
alinipenda mama. Alikuwa akinikimbiza kama mwehu huku ananiita mpaka kituoni.
Tulipofika kituoni mimi nikapanda ndani ya daladala yeye alibaki amepiga magoti
nje ya daladala akinisihi nishuke tuzungumze. Hakutaka niondoke nikiwa nalia.
Lakini nilishindwa kushuka mama.” “Kwa nini?” “Sikutaka anidanganye na pia
sikuwa tayari kwa ukweli, ili asinivunje moyo. Kwa kuwa nilijiambia lazima nije
kuolewa na kuanzisha familia. Niwe na watoto, niwape kile nilichokikosa.” Akatulia
kidogo.
“Unajua mama, ipo hisia ndani yangu inaniambia au
najihisi kuwa nina upendo mkubwa sana ndani yangu. Naona kama nikibahatika
kupata mume na watoto, ninajiona nina uwezo mkubwa sana wakupenda. Nikawa mke
na mama mzuri tu. Najihisi hivyo. Sitaki kuja kuishia kwenye mikono isiyo
sahihi ya mwanaume asiyenithamini mimi, mama. Nimeteseka sana tangia nazaliwa
mpaka leo. Nahangaika kupata pumziko ambalo nahisi hakuna mwanadamu atanipa
tena, labda mimi mwenyewe. Naogopa kusema nimekata tamaa.” “Na wala huna sababu
ya kufanya hivyo.” “Unafikiri hivyo mama?” “Kabisa Nanaa mwanangu. Huna sababu
yakukata tamaa.” “Asante mama yangu.”
“Eti hata hivi kuonana na Zac, na kuonyesha bado
ananijali, imenifurahisha kidogo! Angalau nimefarijika. Nitamtafuta tena ili
nipate naye muda wakumsikiliza.” Mama G, akabaki kimya kama aliyenywea. Alijua
utabiri wake umetimia. Mwanae ndio ameshakosa.
~~~~~~~~~~~~~
Walifika kwenye hicho chumba ambacho Nanaa
alikuwa akimiliki kwa wakati huo. Akashusha vitu vyote kwa haraka bila hata
kuvipanga. Akafunga mlango, akarudi kwenye gari kwa haraka. “Pole mama yangu.
Nakusumbua eeh?” “Wala usijali. Kwanza mbona kama vitu vyenyewe ulikuwa ukivitupa
tu. Umepanga kweli?” Nana akacheka huku akihema kama mtu aliyekuwa akikimbia.
“Nimefanya haraka ili nisiendelee kukuweka mama yangu. Na wewe ukapumzike.
Nitarudi hata jioni au kesho kuja kuvipanga vizuri. Nafikiria nivinunulie
kwanza kabati. Kitanda kisiwe kitu cha kwanza. Maadamu sasa hivi mimi nina
pakulala, basi vitabu vyangu na vyenyewe nivisitiri. Nitavinunulia kabati zuri,
nivipange humo. Ndipo ninunue kitanda. Lakini pazia zuri kwanza na….” Nanaa akaendelea
kutaja vitu alivyoona angehitaji nakumuacha Mama G, akiwaza vyake.
~~~~~~~~~~~~~
Mara simu ya Nanaa ikaingia ujumbe. Akaona uso wa
Nanaa ulivyojawa furaha. Haraka sana Nanaa akajibu huku na tabasamu limejaa
usoni. Waliendelea kujibizana kwa ujumbe kwa muda mrefu. Wakati mwingine
alimuona Nanaa akicheka nakugeukia dirishani kama anayekumbuka kitu, kisha
anarudisha macho kwenye simu yake na kuendelea kuandika ujumbe mwingine, kisha
anatulia kama anayesubiri majibu. Mama G alijua wazi atakuwa akiwasiliana na
Zac tu. Kwani ni jana yake tu Geb alimwambia hakuwa hata na namba ya simu ya
Nanaa! Na alimsikia Nanaa akimwambia Zac kuwa hawana mawasiliano na baba watoto
wake. Nanaa alishamwambia hata Geb akiondoka asubuhi huwa hamuagi.
Na kweli mama G alishuhudia hata alipokuwa mbali
na nyumbani, anapotaka kuulizia hali ya Liv, alimpigia yeye wala si Nanaa.
Alizidi kukumbuka vile Nanaa
alivyomwambia kuwa Geb hakuwa akimuongelesha. Na hata alipomuomba msamaha,
hakuwahi kujibu. Kwa hakika aliyekuwa akiwasiliana naye kwa wakati ule hakuwa
mwanae Geb, ni Zac tu. Mwanaume aliyeonyesha kwa muda mfupi sana alipowaona
pamoja, kumpenda na kumjali sana Nanaa. Nanaa aliendelea kuchat na Zac
nakujisahahu kabisa alipo na yupo na nani mpaka walipofika.
~~~~~~~~~~~~~
“Tumefika mwanangu.” Alishitushwa na sauti ya
Mama G. Akaangalia nje, akagundua kweli wamefika kwenye apartment. “Asante
mama.” Nanaa akashukuru tena kama kawaida yake. “Asante hizo zinakaribia
kumwagika kwenye pipa.” Nanaa akacheka. “Bwana mama! Usichoke. Kweli
nakushukuru, na ninakuahidi leo mwisho kukufanya dereva wangu.” “Wala usijali.
Ndio nafurahia kupata muda na nyinyi wote wawili.” Akamsaidia kumshusha mtoto,
yeye akabeba vitu vingine.
“Huyu naye itabidi kumuamsha anyonye.” Mama G,
aliongea wakati anaweka kiti cha Oliva kwenye kochi. “Jamani Liv analala! Mpaka
ananitia wasiwasi.” “Na baba yake alikuwa hivyo hivyo. Nyumba inakuwa kimya
kama hamna mtoto. Nenda kaoge, uje umnyonyeshe.” “Utamuamsha?” Nanaa akauliza.
“Lazima. Amelala sana. Lazima aamke anyonye.” Mama G alianza kumchezea wakati
mama yake yupo bafuni akioga, mpaka akaamka.
Alitoka akamkuta mwanae ameamka. “Muone vi macho
vyake! Unalala mpaka nakuwa na hamu na wewe! Njoo kwanza unichekee ndio nikupe
nyonyo.” Nanaa akamchukua. Akambusu na kumkumbatia kifuani. “Na anaonekana ana
njaa kweli!” Mama G, akaongeza. “Lazima awe na njaa. Analala sana.” Alibaki
akimtizama Nanaa na mwanae. Alikuwa akimuongelesha kama watu wanao elewana
vizuri.
“Eti Liv! Huna hamu na mama!?” Alimuweka chini,
akawa akizungumza naye huku akimwangalia mwanae. Nanaa huyu wa sasa hivi
aliongezeka furaha na uchangamfu sio kama alivyomkuta asubuhi. “Ngoja mimi niwaache. Naondoka.” Mama G,
aliaga akiwa amenyongea moyoni. Ilishakuwa jioni. “Si tukae kidogo?” “Nataka
nipite dukani nikaangalie kidogo kabla hawajafunga mahesabu ya siku.” “Haya
mama yangu. Nakushukuru sana, tena sana. Mungu akutangulie. Ukute kila kitu
kipo sawa huko kwenye biashara yako.” Mama G akacheka. “Amina.” Akatoka.
~~~~~~~~~~~~~
Alitaka kuondoa gari, lakini akashindwa kabisa.
Mawazo yalimrudisha Chuo Kikuu cha Mlimani, akamuona Nanaa vile alivyokuwa
amekumbatiwa na Zac. Akazima gari. Alikaa pale zaidi ya nusu saa, Mama G
akisikilizishwa na mawazo yake, ile sauti iliyojaa penzi, ya Zac kwa Nanaa.
Akakumbuka miahadi ya Nanaa na Zac. Maneno ya Nanaa akimwambia Zac maisha yake
na Geb jinsi yalivyo. Kwa Nanaa aliongea kama kitu cha kawaida sana, lakini yeye
aligundua udhaifu mkubwa au mapungufu ya
mwanae yatakayomkosesha mke mzuri kama Nanaa. Kwa Nanaa kuongelea sifa za Zac
kwake, akajua ndio udhaifu wa Geb, mtoto wake kipenzi. “Hasira imemponza mwanangu!” Akawaza kwa kumsikitikia kiziwanda
wake.
Geb Kwa
Mama Yake.
Simu yake ilianza kuita, akaitizama, ilikuwa
ikitoka kwenye duka lake. Akajua wafanyakazi wake wanamtafuta. Akabaki
akiingalia. Hakuwa na nguvu hata yakutoka pale. Bado alikuwa ameegesha gari
yake kwenye majengo hayo marefu ya apartment. Akakumbuka furaha ya Nanaa akiwa
kwenye gari wakati ana chat na Zac. “Mhh!”
Simu ya Geb ikaingia. Akaipokea. “Shikamoo mama.” “Marahaba.” “Mnaendeleaje na mtoto?” “Kwa
nini unaniuliza mimi na sio mama yake?” Geb akatulia kidogo. Hakutegemea kusikia hivyo
kutoka kwa mama yake. Kwani alijua Oliva mwanae ndiye anayemfanya mama yake
acheke na kuongea hata kama amechoka.
“Wewe Geb?” “Mbona leo hivyo mama!?” Alihisi sauti ya ukali
kwa mama yake. “Tokea umeondoka nyumbani, umempigia simu Nanaa kumjulia
hali yake yeye mwenyewe binafsi na mtoto?” Kimya. “Utajuta Geb wewe! Shauri yako.” “Basi mama. Mimi mwenyewe nitarudi
nyumbani muda sio mrefu. Nitamuona mwanangu.” Mama G, aliona kwa wazi utofauti kati ya
mwanae na Zac aliyekuwa akimwangalia Nanaa kama alumasi.
“Nikuulize swali Geb?” “Uliza tu.” Geb akajibu akiitambua
sauti ya hasira kutoka kwa mama yake. “Hivi unampango tena na Nanaa au ndio kama ulivyotuonyesha
kuwa yupo kwa ajili ya mtoto tu?” “Kwa nini unaniuliza hivyo, tena unasikika
ukiwa na hasira? Kwani nimefanya nini tena!? Mbona kama nilishakuomba wewe
msamaha na kumuomba Nanaa mwenyewe msamaha! Tena wote mkasema mmenisamehe!
Grace pia leo nimezungumza naye na kuomba msamaha! Sasa natakiwa kufanya nini
tena? Eti mama?”
Geb akawa haelewi.
“Nisikilize Geb. Nanaa ni msichana ambaye hutakaa ukapata
mwanamke kama yeye. Yule mtoto unampuuza Geb.” “Simpuuzi mama jamani! Tulikuwa
na matatizo ndio nipo kwenye kuweka mambo sawa.” “Kwa njia ipi, na mpaka lini?
Utachelewa, uje kukuta mwana sio wako! Wewe fanya mchezo. Wanaume wenzako
wanaotambua uthamani wa yule binti, hawachezi kama wewe. Wewe umeondoka tokea
asubuhi hujui alipo, yupo na nani, anaendeleaje au hata basi kutuma ujumbe tu! Kwanza hata huwa
unamuaga wakati unapokwenda kazini au unapotoka tu kwenda kwenye shuguli zako?” Kimya.
“Mimi ni mama yako Geb, nakwambia utanikumbuka. Fanya mchezo
tu. Huyu binti leo amekutana na mpenzi wake wazamani, anaitwa Zac. Kijana
kachanganyikiwa, anamtaka mpenzi wake. Nimesikiliza mazungumzo yao. Mmh! Sijui.
Sijui Geb mwanangu. Nakuhisi kama umeshachelewa. Zac anaonekana anampenda sana
Nanaa, na ni kama anafanikiwa kumpa Nanaa alichokuwa anahitaji maishani. Nanaa
uliyemuacha leo asubuhi, siye Nanaa niliyemuacha sasa hivi hapo ndani mida hii.
Mwanaume anatuma ujumbe kila wakati na anaonekana anamjulia Nanaa. Nanaa
amejawa na furaha usoni. Nimejaribu kumuuliza maswali machache, anaonekana ni
kijana anayempenda sana. Hata leo nilivyokuwa nikiwatizama, sio uongo, pale
lipo penzi la kweli.” Mama
G, alimsimulia kila kitu Geb, mwanae kipenzi. Tena kwa kituo. Neno kwa neno.
Kila Zac alichokuwa akimfanyia Nanaa, na vile Nanaa alivyokuwa akilia kwa
furaha, na kuonyesha amepata sehemu ya kutulia mzigo wake. Geb alibaki kama
amenyeshewa mvua kwenye baridi.
“Nakwambia mzee Magesa atakuwa akizunguka huko kaburi. Wewe
sio mtoto aliyetegemea uwe. Hakukutabiria hivyo. Hakujua kama utakuwa mwehu
wa kiasi hicho!” “Naomba usiseme hivyo mama!” Geb akalalamika. “Nakwambia kama Mungu
angemfufua baba yako leo, akampa dakika moja ya kuzungumza na wewe, hakika
angekukana kama wewe sio mwanae. Na wala asizungumze na wewe tena maishani.
Baba yako alikufundisha kwa vitendo, wewe mtoto! Uliona kule tulikopita na baba
yako lakini akasimama kama mwanaume. Umerithi macho tu hayo, ukamuachia busara
zote.” Mama
G akakata simu bila kutaka kumsikiliza tena mwanae. Hata hivyo Geb alishukuru
vile alivyokata simu. Alijua kama angeendelea kuongea, angemtukana zaidi ya
vile.
~~~~~~~~~~~~~
Ni kweli kila Geb alipojilinganisha na Zac
aliyesimuliwa na mama yake, akajiona ni kama ameshachelewa. Ni kama mchana na
usiku. Alimkumbuka Zac aliyekwisha kusimuliwa na Nanaa. Zac aliyejua kumjali
Nanaa. Akabaki kimya upande wa pili. Afanyaje tena wakati alishakosea kwa kiasi
kile? Aanzie wapi kurekebisha baada ya kumfanyia unyama mkubwa Nanaa aliyekuwa
amejitoa kwake kwa kiasi kile? Ni kweli Nanaa alikuwa na haki ya kumkasirikia
baada ya kumfumania kama Zac. Lakini angalau mwenzake alionyesha kujali, akamkimbiza
Nanaa mpaka kituo cha daladala, akiwa uchi, akitubia kosa. Lakini yeye hakuweza
hata kumtafuta tena Nanaa. Alimkasirikia.
“Lakini na yeye
Zac alikuwa wapi miaka yote hiyo!?” Geb aliwaza baada ya kukatiwa simu na mama yake.
“Huyu ni shetani kabisa anataka
kuniharibia mipango yangu yote!” Aliendelea kuwaza, akachukua funguo zake
za gari kwenye droo, akatoka kuwahi nyumbani.
Kakumbuka Shuka,
Kumekuchwa..
G |
eb
alifika nyumbani, ilishakuwa tayari ni saa 11 jioni. Akafungua mlango akaingia
ndani akamkuta Nanaa amekaa upande wajikoni akiwa anajibu jumbe zake kwenye
simu na tabasamu usoni. Ukweli alikuwa amependeza. Hakuwa amevaa nguo za
kuonyesha amekamia kwenye hiyo safari yake. Lakini alivaa jumpsuit ya rangi
moja nyeupe tupu. Iliishia juu ya maziwa, bila mkanda wowote. Ili isianguke,
fundi aliyeitengeneza hiyo nguo aliiunganisha na lastiki pana iliyopita
kuzunguka mgongoni na kujichora vizuri juu ya matiti ya Nanaa yaliyokuwa
yamejaa vizuri. Bila shaka ukubwa uliongezwa sababu ya kunyonyesha. Nywele zake
alichana bila kuweka mtindo wowote, akaziachia tu. Ile nywele yenye mawimbi
mazuri, ilianguka mgongoni, ikafunika mabega yake. Hakuwa na mkufu wowote
shingoni. Labda sababu ya hereni ndefu alizokuwa amezivaa zikakaribia kushika
mabega. Aliweka rangi nyekundu kwa mbali kwenye midomo yake, iliyofanya azidi
kuwaka usoni.
Akasimama kwa haraka alipomuona Geb. “Pole na
kazi.” Mwili mzima wa Geb ulisisimkwa, asijue kama ni wivu au ni la! Alishaambiwa
na mama yake kuwa anasubiriwa, aachiwe mtoto ili Nanaa akaonane na Zac. Nanaa aliongea kwa sauti iliyoonyesha hofu
kwa Geb. Taratibu ile sura ya furaha aliyokuwa nayo, ikaanza kubadilika.
“Nikupokee?” Aliongeza Nanaa baada yakuona kimya. “Hapana. Asante.” Nanaa
akatulia kidogo huku akijaribu kuweka simu yake chini kwa tahadhari.
“Vipi mmeshindaje, wewe na mtoto?” Geb akavunja
ukimya. “Liv ameshinda vizuri. Amelala karibu siku nzima! Imebidi mama amuamshe
ili anyonye. Nimejitahidi kumuweka macho ili angalau ukija umkute, lakini
amelala muda sio mrefu.” Nanaa alijibu kama anamjibu mwalimu wake au anatoa
ripoti kwa bosi wake. Tena bosi mnoko! Haikuwa hivi tokea zamani. Geb na
Nanaa walikuwa wapenzi, tena alimfanya ajisikie vizuri. Wakati ule kila
wakiangaliana walitoleana tabasamu.
“Geb!” Nanaa akaita kwa upole. “Naomba nitoke.
Sitakuwa mbali. Kuna mtu nakutana naye hapo kwenye mgahawa wa apartment.
Sitakawia kurudi. Lakini ikitokea Liv anaamka kabla sijarudi, na ananihitaji,
tafadhali naomba unipigie simu. Nitarudi kwa haraka. Chakula chako kipo mezani.
Na uji pia upo.” Kitu kilimkaba Geb, akashindwa ajibu nini. Anamkatazaje leo,
wakati alishamruhusu kwenda kwa mabwana zake lakini asichelewe kurudi?
Anamuuliza anakwenda wapi, wakati hata yeye kuwa anaondoka bila kuaga?
Tena hata hakuwa akimwambia anapokwenda!
Wakati mwingine Nanaa alimsikia akimuaga mama
yake, sio yeye. Alimpa ruhusa yakutoka, lakini isizidi saa 12 jioni. Tena
akitamka wazi huku akimpa baraka zake na kumuonyesha hajali hata kama anakwenda
kwa wanaume wengine, yeye hana neno. Alianzisha hiyo tabia baada ya Nanaa
kurudi na mtoto nyumbani, akiwa amemkasirikia.
Aliondoka asubuhi bila kumuaga na wala hakumpigia
simu. Ujumbe uliingia kwenye simu ya Nanaa. Nanaa akachukua simu yake. Akarudisha
majibu ya ule ujumbe ulioingia, kisha akamgeukia Geb. “Sitachukua muda mrefu,
nitarudi.” Wazi Nanaa hakuwa akiomba ruhusa, na alionekana ni safari ambayo
lazima aende. Kwanza alionekana alitumia muda wakutosha kwenye kioo.
“Nimeandika namba yangu ya simu hapa kwenye
kikaratasi kama ikitokea inabidi unipigie kama mtoto akiamka.” Nanaa aliongeza.
Inamaana huyu Geb hakuwa hata na namba ya simu ya Nanaa! Hata yeye mwenyewe
alijisuta nafsini mwake. Hakuwahi kumpigia simu hata mara moja tokea arudi na
mtoto. “Umependeza sana.” Ndilo neno pekee alilofanikiwa kulitoa Geb,
nakumfanya Nanaa ajiangalie kidogo na tabasamu. “Asante, hata mimi nilifikiri
hivyo.” Alijibu kwa sauti yake nzuri na ya upole. Akapita pembeni ya Geb
aliyekuwa amebaki amesimama vilevile, akatoka. Geb alimsindikiza kwa macho.
Akabaki akikodolea macho mgongo wa Nanaa.
Hiyo jumpsuit ilimkaa vizuri sana mgongoni. Kiuno
chembamba cha Nanaa kilionekana kwa nyuma, huku kikishikiliwa na supu nzuri ya
kumtoshea. Hips zake ziliungana na matako na kutengeneza duara zuri lililokuwa
limetuna na kushiliwa na jumpsuit hiyo ambayo ilimchora vizuri na kuruhusu
yeyote kuona na kuvutiwa. Urefu wa Nanaa uliongezeka kwani nguo hiyo ilikuwa
ndefu mpaka chini kabisa. Haikuonyesha kumbana kwa chini, isipokuwa hapo
katikati ya kiuno na mapaja tu. Geb alibaki ametoa macho asiamini aliwezaje
kuruhusu hasira kumtenga naye. Ni yuleyule Nanaa. Mwanamke aliyezaa naye.
Aliyeruhusu hasira zikubali kulala chumba cha pili yake. Ashindwe kupokea msamaha
wake, yaishe, akafaidi kile anachoenda kupewa Zac jioni hiyo.
~~~~~~~~~~~~~
“Hata kama hatampa mapenzi kwa usiku huu, lakini mwenzangu ataliwazwa.
Watacheka na Nanaa. Atapata nafasi kuyaona kwa karibu yale niliyojidai
nimeyasusa. Pengine atambusu!” Geb alianza kuwaza akiwa amesimama palepale.
Akakumbuka midomo mitamu ya Nanaa. Iliyokuwa ikimtoa ofisini kwake BOT na
kuifuata popote alipo Nanaa, na kuinyonya hata kwa dakika 5 tu, huku
amemkumbatia. Alivuta pumzi, akaenda kukaa kwenye kochi.
Sio kwamba ilihitaji Visa kukutana na Nanaa.
Nanaa alikuwa hapohapo kwenye eneo la apartment, tena analala chumba cha
pembeni yake. “Nimechelewa
kidogo tu. Leo ndio nilipanga nizungumze na Nanaa kila kitu. Ni heri jana
nilipomkuta akilia, ningeongea yote, labda angenielewa kwa haraka, kuliko nije
kuanza tena baadaye, tena akiwa na penzi jipya la Zac! Ameshindwa hata kujibu
swali dogo tu la ‘umeshindaje
wewe na mtoto’! Akaishia kumzungumzia Liv, yeye akajitoa kabisa!” Geb aliendelea kuwaza
akiwa amejiweka kwenye kochi. “Daah!”
Alijikuta akiongea mwenyewe kwa sauti. Giza lilianza kuingia mpaka sebuleni,
lakini hakuwasha taa, akabaki amekaa tu gizani. “Kweli Mzee Magesa atanikana. Sio kwa
upuuzi huu!”
Geb akajikejeli mwenyewe.
~~~~~~~~~~~~~
Ukisema cha Nini, Zac analilia
atakipata Lini!
Zac amerudi kwa kasi mpya. Na Nanaa
naye hana kipingamizi.
Alishaomba msamaha mpaka amechoka. Geb
alimuonyesha hana shida naye. Usikose mwendelezo kujua yatakayojiri.
0 Comments:
Post a Comment