Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu Ya 31. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu Ya 31.

Mama G akaendelea. “Sikumuona tena mpaka baada ya miezi kama 5 hivi.” “Mama! Hukuogopa labda atakuacha?” “Hapana. Nilijua ananipenda sana. Asingethubutu kuniacha. Lakini nikajua hawezi kufikiria kama mimi nikiwepo kwenye picha. Alikuwa ananipenda zaidi nitakavyokueleza. Nakumbuka alikuja kurudi baada ya hiyo miezi mitano, ilikuwa mchana, na mimi ndio natoka kliniki. Nimechoka.” “Ulishika mimba?” Mama G, akaguna.

“Siku niliyomwambia tuagane, nilikusudia aniache nikiwa mjamzito. Mimba yenyewe ilikuwa ndio ya hao kina Geb. Tumbo kubwa. Halafu kumbuka hapo hata sijafikisha miaka 20. Akanikuta nimelala sakafuni nipo peke yangu. Alinihurumia sana. Akaniuliza, ‘kliniki wamekwambia nini?’ Nikamuelezea nikiwa nimelala pale pale chini. Nikamwambia watoto hawajambo. Wapo wawili. Wameona wakike. Mwingine amejificha. Hapo namjibu nikijua yeye anawatoto wakike tu. Akaniuliza kama nimekula, presha yangu ikoje. Nikamjibu nikiwa nimetulia, nachezea funguo zangu za gari bila hata kumwangalia. Akaniambia, ‘Sijakutupa Oli. Sikujua kama uliamua kushika mimba. Nilikuomba tusubiri ili niweke mambo yangu sawa. Nilipojua upo mjamzito, ilibidi kujipanga kwa ajili yako na watoto.’ Sikumjibu. ‘Oli!’ Akaniita. Nikanyamaza. Akasimama pale kwa muda, akatoka nje.”

“Nikamuona anaingiza begi lake, akarudi kukaa pale nilipolala. Ndio nikamwangalia. Alikuwa amekonda sana. Nikaanza kulia, nikakaa. ‘Mbona umekonda hivyo?’ Nikamuuliza. Akasema anaumwa. Alianza kuumwa miezi michache iliyopita. Lakini alishindwa kwenda hospitalini. Kwa kuwa kuna mambo ilimbidi aweke sawa. Akaniambia alipojua ni mjamzito, ikabidi akamwambie mchungaji wao. Akakiri kila kitu mbele ya kanisa. Wakamwambia kwa umri wake na jina alilojijengea kwa jamii, ni lazima aniache. Kwanza ni aibu. Anasema alikataa. Akasema mimi ni mkewe pia, na amekusudia kunioa mahakamani.” “Mama!!” Nanaa akashangaa.

“Hata mimi sikuamini Nanaa. Basi, wakamtenga na kumwambia asifike kabisa pale kanisani kwa kuwa anawafedhehesha. Kurudi nyumbani mkewe na watoto wakamuita kikao, na kumwambia ni lazima achague kati yangu na wao. Ndipo ikabidi awaeleze kuwa tayari mimi nilikuwa mjamzito, tena wamapacha.” “Mama! Alijuaje wakati mlikuwa hamuonani!?” Nanaa akauliza kwa mshangao.

“Asingeweza kuniacha bila kujua linaloendelea Nanaa. Yule Mzee alinipenda kwa dhati. Kwanza wafanyakazi wote aliokuwa amewaajiri pale walikuwa vijana wake. Sijui alikuwa akiwatoa wapi, lakini walikuwa wake. Njovu nilihama naye kutoka Kibaha, akaja kunifanyia kazi pale Posta. Na yeye ndio alikuwa mtu badala yangu pale kazini, na alikuwa kijana wa Magesa. Kwa hiyo alikuwa akituma ujumbe kwa Magesa kumueleza kila kitu kinachoendelea. Nani ananitongoza. Kama nimekubali au la. Kwa hiyo nilijua ananiulizia. Basi. Akawaambia wanae hayupo kwenye hali yakuchagua tena. Yeye ni baba kwao na kwa watoto hao wasio na hatia. Ambao hawakuchagua wazaliwe na nani. Hapo anasema ni mwezi uliopita, na alishaanza kuumwa.”

“Basi, wakamfukuza pale ndani, na kumwambia hawamtaki tena awe baba yao. Na mkewe akampokonya mali zote, akasema kwa kuwa yeye ndio anaondoka, lazima aache kila kitu. Akawaomba wampe muda wakufikiria, wakamwambia akiwachagua wao ndio arudi, lasivyo wao wanaondoka kwenda kuishi na wazazi wa mama yao huko Machame. Basi anasema ikabidi yeye ndio atoke kuliko kuwaharibia watoto wao maisha. Alikuwa akipenda sana binti zake. Anasema aliishi hotelini huku akijaribu kuweka mambo sawa ya nyumbani kwake, lakini hakufanikiwa. Walimwambia nilazima aachane na mimi. Sasa wakajua kama alininunulia gari na amenipangishia nyumba. Mbaya zaidi ile biashara iliyokuwa inashamiri hapo Posta.” “Sasa walijuaje?” Nanaa akahoji.

“Mtu yeyote anayekuletea habari za umbea wewe, ujue hashindwi kutoa habari zako na wewe na kumpa mwingine. Hao hao vijana wake ndio walikuwa wanamgeuka Magesa. Kila kitu kilichokuwa kikiendelea kati yetu, walikuwa wakimwambia yule mama na wanae. Sasa wakataka Magesa aninyang’anye vile vitu. Magesa alikataa kata kata. Wakashitakiana kila mahali, Magesa akakataa kuninyang’anya. Uthibitisho wa zile documents zote za kununua gari yule mama alikuwa nao. Akawa anawaomba wazee wamuulize Magesa gari alilolinunua kwa pesa wanayohangaika wao wawili, mchana na usiku, liko wapi?” “Mama!” Nanaa akashangaa.

“Yule mama alikuwa na haki, Nanaa. Walihangaika na Magesa mchana na usiku bila kupumzika! Magesa akakiri kuwa ni kweli amenikabidhi mimi. Lakini hawezi kunipokonya. Ni heri atoe gari yake awape, kuliko kuchukua gari aliyonipa mimi. Hawakuamini. Gari ya Magesa ilikuwa nzuri sana. Mpyaa. Safi sana. Akatoa funguo akamkabidhi yule mama. Yule mama hakukubali. Akamshitaki Magesa kuwa hamuamini tena na mali zao, kwa kuwa ameanza kuhonga nje. Kumbe muda wote huo alikuwa kwenye heka heka! Magesa anasema hakutaka ugomvi na mkewe, akakiri kosa huko mahakamani. Na kukubali mali zote ziende kwa jina la mkewe. Wakili wake akamwambia ni lazima iwe kwa majina yao yote mawili, lakini Magesa akakataa. Akamwambia mali zinatafutwa, lakini sio kitu alichonacho kwangu. Nililia Nanaa. Nililia siku ile. Sikuamini kama Magesa amenichagua mimi na kuyatupa maisha yake.” “Jamani mama! Kwa hiyo wakamfilisi?” Nanaa alitaka aendelee.

“Yaani vile alivyokuwa ameingia siku ile, ndio alikuwa amemaliza.” “Hukujuta?” “Nilifurahi sana. Kwamba ndio mimi nimesusiwa Magesa! Mungu anipe nini? Kwanza ukumbuke kuanzia mwanzo niiyekuwa namtaka ni yeye. Sikuwahi hata kuchanganywa na mali zao. Alikuwa mgonjwa, na mimi mjamzito, lakini sikumuachia siku ile. Kila saa ananiweka pembeni, ananiuliza, hivi umeelewa nilichokwambia? Namwambia nimeelewa kuwa sasa hivi wewe ni wangu. Magesa akawa anacheka tu. Akaniuliza akitokea mwanaume mwenye pesa zaidi yangu. Nikamjibu kuwa hao wapo tu, na wala hawataisha. Niligaragara naye hapo chini nafurahia siamini. Usiku nikampeleka hospitalini. Sijakaa sawa tupo tunamsubiri daktari, akaanguka nakupoteza fahamu.” “Uwiii!” Nanaa akashituka.

“Acha Nanaa. Nilikuwa namdai Mungu kama namjua vile au kama yupo hapo. Eti Magesa kapoteza fahamu siku tatu! Nilizicheza ngoma zote. Nikamwambia Njovu awaambie familia yake wajue kama baba yao mgonjwa, unajua walijibu walishafuta undugu naye! Mkewe akasema hataki kumsikia yule baba. Nanaa, nilikuwa nazunguka pale Muhimbili kama mwehu. Tumbo kubwa, namwambia Mungu namtaka Magesa. Muda wa kuona wagonjwa ukifika, naenda kupiga magoti pembeni ya kitanda chake. Kuomba sijui, mtoto niliyelelewa na masista.”

“Tena hapo mwizi wa mme wa mtu! Sijali. Namwambia Jesu ulizungumza na yule mwizi pale msalabani, basi naomba azungumze na mimi. Watu wanajua ninamlilia baba yangu, kumbe mme.” Nanaa akaanza kucheka gafla. “Tumbo kubwa kama nataka kuzaa, kumbe ni miezi 5 tu. Tako na lenyewe limeumuka, nikipita unaona tumbo na tako tu. Nilikuwa natembea pale Muhimbili asubuhi mpaka asubuhi. Njovu akawa anakuja kunitoa pale kwa nguvu, ananirudisha nyumbani. Saa 11, nipo hospitali ya Muhimbili kwa Magesa. Alikaa pale karibia mwezi ndio nikarudi naye nyumbani. Nilimlisha, mpaka anatoka pale akawa kama kijana.”

“Bwana Magesa alinawili! Kazi yake ilikuwa kula kulala. Mapenzi mazito. Sitaki mambo yakumkera. Usiku Njovu anarudi nyumbani, analeta pesa, nyingine anakuwa ameshaweka benki.” “Mlikuwa mkiishi na Njovu?” Nana akauliza. “Yule baba asingekubali niishi kule Kinondoni, peke yangu. Alikuwa na wivu Magesa kuliko nitakavyokwambia. Njovu aliwekwa pale kama mlinzi. Lakini alitusaidia sana na Magesa. Halafu alikuwa mwaminifu sana.”

“Yuko wapi sasa hivi?” “Alikuja kufa kabla hata ya Magesa. Alikuwa muhuni sana. Alikuwa anapenda sana wanawake. Ndio ulikuwa ugonjwa wake. Magesa aliumia sana alipo athirika. Alikufa mikononi mwetu. Halafu wakati ule madawa hayakuwa mengi kama sasa hivi. Ukiathirika unakufa kwa haraka.” “Jamani! Eehe?” “Nanaa mtoto mbea huyu!” “Bwana  nimalizie.” Mama G akacheka.

“Maisha yakaanza. Mimi na Magesa wangu. Kuanzia asubuhi mpaka usiku. Kila kitu tunafanya pamoja. Kuanzia kuoga, mpaka kulala. Mtoto deko, nadekezwa. Biashara yetu ya Posta ikachangamka. Si nilikwambia Magesa ana akili sana?” “Kama mwanae Geb.” Mama G akacheka. “Hivyo hivyo. Na alimwambia Geb. ‘Wewe una akili sana. Lakini utafanikiwa zaidi ukiwa mfanyabiashara’. Naona hicho kitu kikamwingia sana Geb. Basi, tukaanza kuendeleza ile biashara. Akaanza kuuza tena maziwa. Lakini safari hii akawa anauza yaliyokwisha fungwa kwenye paketi. Kabla hata sijajifungua, akawa amepata sehemu maeneo ya Chang’ombe. Anasambaza maziwa ya paketi jijini. Mtindi kwa fresh. Kumbuka alianza biashara kwa pesa tuliyokuwa tunapata au niliyoikusanya pale kwenye biashara ya Posta. Alichukua pesa yangu yote benki akaiwekeza. Alikuwa na akili yule mwanaume, hujawahi ona Nanaa. Ukimuona amenyamaza anaandika, mwache,  ujue kuna kitu cha maana anaandika.”

“Basi siku za kujifungua zikafika. Nikashindwa kuzaa. Watoto wakubwa.” “Naona na Grace pia mrefu!” Nanaa akaongeza. “Kama baba yao. Magesa alikuwa mrefu sana. Basi nikafanyiwa upasuaji, Grace akatoka wa kwanza, akaja Geb wakiume ambaye hata sikumtegemea. Mimi na Magesa tukamshukuru Mungu kwa pamoja. Akasema ni kwa rehema za Mungu tu ndio alitupa wale watoto, hatukustahili. Ndio akamwita Grace, na mdogo wake akampa jina la Geb. Lina asili la ki Egypt kuwa ni mungu wa ulimwengu huu. Akamtabiria kuwa kila atakachoshika katika ulimwengu huu, kitastawi sana.” “Kumbe majina ya wanao yanamaana kubwa hivyo!” “Magesa huyo.” “Lakini hata lako mama. Wakati umesema tumwite Oliva mwanangu, nikakubali kwa haraka sana nikasema tutamwita Liv kwa kuwa aliishi hata katikati ya yale matatizo. Walinifanyia mpaka upasuaji, na kunipa madawa makali. Lakini akatulia tuli mwanangu mpaka akazaliwa. Tena bila kasoro. Na uliponipa maana ya Oliva, naona kama mnafanana! Wote mnastawi kwenye mazingira magumu.” Mama G, akacheka.

“Ikawaje sasa mama?” “Wewe Nanaa! Nenda kanyonyeshe wewe mtoto acha umbea!” “Nimalizie bwana.” “Sasa wewe mtafutie Geb sababu. Nenda kamchungulie mwanao. Unasubiri mpaka uuitwe! Shauri yako.” “Kwa hiyo niende?” Nanaa akauliza. “Wewe si umekaribishwa huko chumbani? Nenda. Mshike mwanao, jizungushe kisha toka.” Nanaa akasimama. “Lakini utakuja kunimalizia stori?” “Yatakushinda wewe Nanaa!” Nanaa akatoka anacheka sio kama vile alivyokuwa akilia.

~~~~~~~~~~~~~~

Kweli, Nanaa alitulia akaanza kumlea mtoto wake. Akimsikia ameamka kwenye monitor, anaamka na yeye anakwenda chumbani kwa Geb. Anamchukua mtoto, anakaa naye kwenye kochi, anamnyonyesha, huku amemkumbatia kwa mapenzi na kumshika shika. Wakati mwingine alitulia akiwa anamtolea tabasamu na kumchezea vidole vyake vya mkono wakati ananyonya. Wakati mwingine alipokuwa akimsikia mtoto ameamka, anapokwenda, anamkuta Geb anampa maziwa ya chupa aliyokamua.

Siku zikazidi kwenda, Liv anakunywa maziwa ya mama yake kwa chupa na kunyonya. Taratibu yule mtoto akaanza kumjua mama yake. Akimuona Nanaa, au akimshika anatulia kabisa na kuonyesha kufurahia. Tayari alishamaliza miezi miwili, akawa amechangamka, lakini bado Geb hakuwa akimuongelesha Nanaa. Nanaa alishaomba msamaha akaamua anyamaze. Kwa asili Geb ni mkimya, ukichanganya na kiburi alichonacho, haikumsumbua kunyamaza.

Alikuwa akilala na mtoto wake. Asubuhi wakati anaenda kazini anamuacha kitandani kwake, akijua lazima mama yake atakwenda kumchukua na kumuhudumia. Na alitaka akirudi mchana au jioni amtawale mtoto wake. Nanaa alilielewa hilo, kila siku asubuhi alipomsikia Geb anaingia chumbani kwake na kumuachia pesa za matumizi kabatini kwake, alijua ndio anaondoka, na yeye ndipo alipokuwa akiamka kwenda chumbani kwa Geb anamchukua mtoto wake, anarudi naye kulala naye akiwa amemkumbatia chumbani kwake siku nzima mpaka akisikia gari ya Geb.

Ilikuwa kila akisikia gari ya Geb, anambemba na kumrudisha kitandani kwake kwa haraka, kabla Geb hajamkuta. Liv alikuwa mtoto mzuri wa kutochosha kumwangalia. Kwa kuwa alikuwa akinyonya sana, alikuwa na mwili mzuri, mkubwa. Hata Geb alipokuwa akimpeleka kliniki alikuwa akisifiwa kuwa anamtunza vizuri. Alikuwa na nguo nyingi sana, hakuwa akirudia. Kila Geb aliporudi kutoka kazini alikuja na nguo mpya na vitu vya huyo mtoto. Macho yalikuwa kama ya Geb. Alikuwa na nywele nyingi sana kama baba yake. Kwa kuwa alichukua rangi ya mama yake, kwa haraka sana mtu ungeweza kusema ni mtoto aliyechanganyia na damu ya kiarabu.

Geb alimpiga picha za kila namna na kutundikwa katika kila kona ya hiyo nyumba. Nyingine zilikuzwa zikawa kubwa sana, nyingine za rangi ya nyeupe na nyeusi, ilimradi tu ile nyumba ilijaa Liv. Muda mwingi aliutumia nyumbani na mtoto wake. Na akiwa nyumbani, hakutaka kuingiliwa, alikuwa yeye na Liv tu. Bado alikuwa haongeleshani vizuri na mama yake, kidogo alimuogopa kwa kumgombeza siku alipomfungia Nanaa nje. Lakini afadhali yeye alimsalimia lakini sio Nanaa. Alipofungua mdomo wake kuongea na Nanaa, ilikuwa ni kumpa maagizo tu. Hapakuwa hata na salamu.

~~~~~~~~~~~~~~

 “Sasa na wewe uache kuzunguka na khanga humu ndani.” “Naona rahisi kunyonyesha.” “Mambo yakishamba matupu hayo! Kwa hiyo unaenda chumbani kwa Geb na makanga!?” “Si nakuwa naenda kunyonyesha?” “Uwiii! Ndio maana hata ukimuongelesha hakujibu. Unamkera.” “Mama jamani!” “Kumbe! Kuzaa imekuwa nongwa! Ulikuwa unapendeza mwenyewe, rangi yako nzuri, umbile Mungu kakujalia, halafu unajiachia kwa mtoto wa kwanza tu! Wewe nenda kanunue vigauni vyako vizuri, na vya maana. Vyenye zipu au vifungo mbele. Nunua sidiria ya kunyonyeshea. Sio kutoa ziwa lote mpaka mtoto mwenyewe anakinahiwa!” Nanaa akaanza kucheka.

“Mama nyie!” “Sasa je! Tengeneza nywele, kuwa msafi.” “Mtoto ameanza kusumbua kunywa maziwa ya chupa. Nikitoka itakuaje?” “Tutaenda wote huko madukani.” “Geb hawezi kuruhusu tutoke na mwanae. Kliniki yenyewe anampeleka mwenyewe!” “Anajidai tu. Akitaka aache kazi aje akae na huyo mwanae hapa. Lakini lazima kesho tutoke. Nitamwambia.” Wakakubaliana.

Kesho yake Geb aliwahi kutoka kazini na kurudi kukaa na mtoto wake. Nanaa na Mama G, wakatoka kwenda madukani. Mama G akamnunulia nguo nzuri. Za kulalia usiku, na kuvaa wakati wa mchana. Akamnunulia sidiria nzuri kwa ajili ya kunyonyeshea. Wakapitia sehemu wanayosuka. Akaomba wasichana watatu, wafike nyumbani kwao asubuhi sana kwenda kumsuka Nanaa. Akawaambia aina za nywele anazotaka kusukwa, Mama G akamlipa mmoja wao kwenda kuzinunua hizo nywele, japokuwa zilikuwa za gharama sana, lakini Mama G alikubaliana naye kuwa zitakaa muda mrefu.

Walirudi nyumbani mapema tu, mtoto alikuwa bado amelala. Kama kawaida Nanaa alienda kuoga akaenda kumchukua mtoto wake na kuanza kumnyonyesha. Geb akatoka bila kuaga, wakajua amerudi kazini. Jioni akarudi, akamfuata Nanaa chumbani kwake. “Kesho utatoka tena?” Nanaa akamgeukia kama kutaka kujua kwa nini anamuuliza hivyo. “Kuna mahali nataka kwenda. Nitachelewa kurudi. Naweza kurudi usiku, na sitaki uzurule na mtoto wangu. Kama unasafari zako, nataka uniambie mapema, ili niahirishe safari zangu nije kukaa na mwanangu.” “Kesho sitatoka. Nitakuwepo.” Geb akatoka. Nanaa alibaki akijiuliza. Ndio kwa mara ya kwanza ametoka pale ndani tokea aingie, lakini Geb ameonyesha kutokufurahia!

~~~~~~~~~~~~~~

Geb alitoka asubuhi na mapema, Nanaa akamsikia akimuaga mama yake kuwa anakwenda Morogoro, lakini atarudi usiku. Kuna jambo anafuatilia. Lakini hakumuaga Nanaa, akaingia chumbani kwake, akamuwekea pesa juu ya kabati kama kawaida, akaondoka. Wasusi wote watatu walifika hapo saa moja asubuhi. Alitaka asukwe nywele ndogo ndogo sana, za kusukwa chini na kuachia juu, kwa kutumia “100% human hair”. Iliyomgharimu sana Mama G. Mpaka kufika saa tano asubuhi alikuwa ameshamalizwa.

Alipendeza sana. “Na hizo dimpozi huko mashavuni, umezidi kupendeza mwanangu. Hapo ukimshika Oliva ndio watakubali kabisa kama wewe ni mama yake. Maana manywele hayo ndio mmefanana zaidi.” Nanaa akacheka. “Asante mama yangu kwa kunipendezesha.” “Halafu mtu hawezi kujua kama sio zako! Zimekuwa kama zako kabisa!” Msusi mmoja aliongezea sifia. Walilipwa pesa yao, wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

 “Mbona vidole kwenye simu muda wote?” “Si unakumbuka jinsi nilivyoondoka chuoni? Sasa mizigo yangu yote nilimuomba yule matron anitunzie.” “Antii?” Mama G akauliza.  “Huyo huyo. Ndiye aliyekwenda kunichukulia pale chumbani kwangu, amenihifadhia kwake. Sasa ndio anauliza ni lini naenda kuvichukua? Nyumba yake ni ndogo kweli! Vitakuwa vinamkera.” “Si twende sasa ukavichukue uje uvihifadhi huko stoo!” Mama G. Akaonyesha utayari. “Sio hapa mama. Nipo kwenye makubaliano ya bei na dalali, anachumba. Lakini wapo watu kama watatu wanakitaka hicho chumba. Ndio nimemuomba akazungumze na mwenye  nyumba, kama atanipa mimi.” “Kwa nini ukakodishe chumba wakati nyumba hii ipo?” Nanaa akaanza kutokwa na machozi.

Hapa sio kwangu mama. Unakumbuka jinsi nilivyofukuzwa siku ile? Nilifungiwa nje! Nipo hapa ndani kwa masharti makali sana. Itakuaje siku nikiyavunja halafu vitu vyangu nimefungia humu ndani? Hiyo mizigo niliyoiacha kwa Antii, ndio juhudi yangu yote. Kuna vyeti vyangu kuanzia darasa la saba mpaka kidato cha sita. Hivyo vyeti ndio ndugu, ndio mama yangu, ndio baba yangu. Ndio tumaini pekee nililobaki nalo hapa duniani. Nimevipata hivyo vyeti kwa shida sana mama. Kwa masimango, mateso, kulala bila kula, na dhiki ya kila namna. Kuna kipindi nilikuwa natamani kukata tamaa, lakini nilikuwa najiambia shule atakuja kuwa mkombozi wangu, ndio maana nilihakikisha nakosa kila kitu, lakini sio shule.” Nanaa akaendelea huku akilia.

 “Acha nivitafutie kwao, vikae hapo vikinisubiri. Hata siku nikija kufukuzwa tena hapa, nitajua vipo kwetu vinanisubiri. Vitakaa hapo kama ndugu. Acha na mimi niwe na kitu changu mama. Nimeshahangaika vyakutosha. Nimenyanyasika vyakutosha. Mungu akinisaidia nikapata cheti kizuri cha chuo, nitatafuta kazi, na mimi nianze kujitegemea.” “Na mtoto?” Mama G akauliza.

“Unafikiri nitakuwa na kazi gani tena hapa kama Liv akianza kula? Geb ameweka mpaka kabisa kati yangu na mwanangu. Amenionyesha kwa vitendo sihitajiki humu ndani. Ananihitaji kwa kumnyonyesha tu mtoto, tena wakati mwingine hataki hata nimguse mwanangu yeye akiwepo. Siku za jumamosi na jumapili kama unavyomuona. Anakuwa na mtoto kuanzia asubuhi mpaka asubuhi. Akilia anampa maziwa ya chupa. Ananiambia nikamue niweke kwenye chupa. Hebu niambie mama yangu, huyu mtoto akianza kula, nitahitajika kweli hapa ndani?” Mama G, akanyamaza kidogo.

“Ulimjaribisha tena kuzungumza naye?” Mama G, akauliza. “Japokuwa aliniumiza sana kunifukuza kwake na kunifungia nje, nilikubali yaishe ili kulea mtoto kwa amani. Nimeomba msamaha, mpaka nimeamua kuacha tu. Hanijibu kitu, akiongea na mimi ni kunipa maagizo tu. Hata akiingia chumbani kwangu ni kuacha pesa, basi. Tena kuna mahali huwa anaziweka, juu ya kabati langu. Kiasi chake ni kilekile, kila siku. Nimezikusanya, ni pesa nyingi. Hivi nimemkusanyia nitamrudishia.” “Usifanye huo ujinga hata siku moja, Nanaa. Wewe upo humu ndani, unalea mtoto, unafikiri pesa utapata wapi? Zitunze hizo pesa, hujui ni lini zitakusaidia.” Nanaa akanyamaza. Akaenda kuoga, akaenda kumchukua mtoto wake, akaenda kulala naye kitandani kwake.

Walikula hapo hapo chumbani huku wakiongea na Mama G, mpaka ilipofika tena jioni, Nanaa akapitiwa na usingizi akiwa amemkumbatia mtoto wake palepale kitandani. Hakusikia wakati Geb anaingia, akaenda kumtafuta mtoto wake kitandani akamkosa. Akaenda chumbani kwa Nanaa, akamkuta Nanaa amemkumbatia, wamelala. Aliingia kuoga akarudi kumchukua mtoto wake mikononi kwa Nanaa, Nanaa alishituka sana, akakaa na kuanza kulia alipomuona Geb amemchukua mtoto. “Nimekwambia mwache mtoto alale kitandani kwake kama mimi sipo. Usinijaribu Nanaa!” Nanaa akaendelea kulia huku ameinama bila kujibu kitu. Alilia, akarudi kujilaza.

Alishituka tena usiku akamsikia mtoto wake analia kuliko kawaida yake. Nanaa akaenda chumbani kwa Geb. “Kwa nini analia?” Akamkuta Geb anambembeleza. “Wewe ndio umeharibu kila kitu. Kwa nini unalala na mtoto unamkumbatia? Sasa hivi ni kama amechanganyikiwa haelewi anatakiwa kulala wapi!” “Naomba nimbembeleze.” Nanaa akasogea. Alipomshika tu nakumuongelesha kidogo, mtoto wake akatulia. Nanaa akakaa chini, akatoa ziwa na kuanza kumnyonyesha.

Aliponyanyua uso, macho yake yakagongana na Geb, alimkuta anamtizama kwa kujiiba. Akajitengeneza nywele zake vizuri, akavuta kitambaa, akajifunika yeye na mtoto, kama kujificha Geb asione matiti yake. Liv aliendelea kunyonya kama mwenye njaa sana. “Kesho nataka kutoka.” Nanaa akavunja ukimya wakati bado amempakata mtoto wake akinyonya. “Lazima niende kwanza kazini, nikirudi ndio na wewe utatoka kwenda kuzurula.” Nanaa hakujibu akainama na kuendelea kucheza na nywele za mtoto wake taratibu kama kumbembeleza wakati bado akinyonya.

~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake Nana alijiandaa, akamuaga Mama G, na kumwambia Geb akirudi tu, na yeye atatoka kwenda kufuatilia chumba, na kama akifanikiwa, atakwenda kuchukua mizigo yake na kuihamishia kwenye hicho chumba. Akachukua pesa zote alizokuwa akiziacha Geb juu ya kabati lake, akaenda kuziweka kwenye kabati la mtoto chumbani kwa Geb. Akatoka akawa amekaa na Mama G jikoni wakitaniana. “Leo sijui kama utarudi! Ulivyopendeza hivyo!” Nanaa alikuwa anacheka tu. “Wakikuona huko, lazima wakuibe.” “Hapana bwana mama. Na Liv wangu?” “Si yupo kwa baba yake!?” “Na kweli. Nitamtafutia mdogo wake.” “Na ulivyopendeza hivyo, atakuja mdogo wake kwa haraka sana.” Wakaendelea kucheka. Mara wakasikia mlango unafunguliwa, wakajua ni Geb, wakanyamaza.

Akaingia hapo jikoni akiwa na mifuko mkononi. “Ni nini hicho?” Mama G akamuuliza. “Maziwa ya Liv.” Nanaa akashituka sana. “Mimi bado nina maziwa mengi tu. Naomba usimuanzishie mtoto maziwa ya kopo.” “Kama unamaziwa mengi kwa nini jana nimekuta chupa moja tu?” Geb akauliza. “Liv ameanza kukataa kunyonya kwenye chupa, Geb. Nikiwa naye anataka nimnyonyeshe tu.” “Labda hataki maziwa yako yakiwa kwenye chupa, haya atayanywa.” “Tafadhali Geb, usimpe mtoto maziwa ya kopo sasa hivi wakati mimi mwenyewe nipo.” Nanaa alishaanza kulia.

“Wewe Nanaa, niangalie mimi. Huyo mtoto hatapewa maziwa ya kopo. Nyamaza uende uwendako ukiwa umetulia. Sio unakutana na watu macho yamevimba! Umependeza sana, acha kujiharibia siku yako. Toka na furaha yako, kafanye mambo yako uwahi kurudi umnyonyeshe mwanao. Si umeacha maziwa mengine?” “Nimekamua chupa tatu mama.” “Haya nyamaza, uende. Mwanao hatakunywa maziwa ya kopo, atampa ya kwako.” Geb akatoka mle ndani kwa hasira, wakamsikia akipigiza mlango. “Wewe nenda. Achana naye.” Nanaa akatoka akiwa ametulia.

Uchungu Wa Mwana, Aujue Mzazi.

Ilipofika saa 11 jioni Grace, Fili na Danny wakaingia. “Naona tumbo linakaribia kuanguka.” Mama yake akamchokoza Grace. “We acha tu! Watoto wenyewe wawili tu wapo humo tumboni, lakini utafikiri nimebeba jeshi!” Grace akakaa. “Anakula huyo! Utafikiri anakwenda vitani.” Danny akadakia. “Niache Danny. Unafikiri mimba ya watoto wa kiume mchezo?” Grace na mumewe waliingia wakiwa wanaongea, Grace akajitupa kwenye kochi, Mama yake akaanza kucheka.

Mara Liv akaanza kulia akiwa chumbani. “Hee! Hii nyumba ina mtoto au mlio wa simu?” Danny akahoji, ndipo wakanyanyua macho kuangalia ukutani. “Huyu mtoto wa kiukweli au ni zile picha za watoto za kununua ndio mkapamba ukutani?” Grace akahoji na kujipinga tena. “Hataa! Haya macho na nywele za huyu mtoto kama navifahamu! Fili alizaliwa hivi hivi kasoro rangi tu! Huyu mweupe.” Danny akaanza. “Geb! Geb weee! Hebu njoo bwana. Acha kutufanya mimi na mke wangu kama machizi, tunaulizana na kujijibu wenyewe!” Geb akatoka amembeba mtoto. Wote wakanyamaza kwa gafla, macho yakawatoka.

“Huyu mtoto ni wa nani!?” Baadaye Grace akauliza na mshangao mkubwa machoni. Akavuta suruali ya Geb ili amsogelee karibu, amuone huyo mtoto. “Hebu nipe mimi huyu mtoto.” Akapewa, akaanza kumchunguza taratibu. “Kwa kuwa huyu mtoto sio wangu, basi ni wa Geb.” Grace akanyanyua uso na kumtizama mama yake. “Anaitwa Oliva.”  Mama G, akaongeza. “Si ni jina lako mama?” Grace akaendelea kuhoji. “Ndiyo.” “Kwa hiyo ni mtoto wa Geb?” Kimya. “Mbona kama kunakufichwa hapa?” Danny akalalamika.

“Ndiyo ni mwanangu.” Grace akamwangalia kaka yake kwa kukunja uso. “Sijaelewa. Yaani wewe Geb una mtoto, halafu huniambii mimi wakati tunaonana karibia kila siku na tunakuwa wote siku nzima!?” “Acha kunikasirikia Grace, huyu mtoto na mimi nilikuwa sijui kama yupo.” “Wewe ulijua lini kama huyu mtoto yupo?” Grace akauliza akisikika ameshakasirika. “Miezi miwili sasa.” Mama yao akajibu kishabiki.

“Ngoja kwanza mama. Yaani wewe upo na huyu mtoto humu ndani, unashindwa kutuambia? Undugu umeisha kati yetu?” “Wala usiende mbali Grace. Humu ndani kuna hekaheka, sio mchezo.” Mama G, akasogea akakaa pale kwenye makochi. “Yaani Grace, pakikucha au pakiingia usiku mkapanda kitandani kwa amani, mnashukuru Mungu. Kumegeuka kuwa kambi ya jeshi. Vilio haviishi, ubabe ndio usiseme.” “Ngoja kwanza mama. Tuanze kwa hatua. Mama yake huyu mtoto ni nani, na yuko wapi?” Danny akauliza.

“Mama yake huyo mtoto anaitwa Nanaa, dada yake James.” Kila mtu akamwangalia Geb, aliyekuwa ametulia kimya, mikono yake mfukoni. Grace akachukua headphone kutoka kwa mumewe, akamvalisha Fili baada yakumuwashia simu acheze game. “Hebu endelea mama. Maana nahisi ni stori!”“Huyo Nanaa katoka hapa muda sio mrefu. Lakini kutokana na masharti aliyopangiwa humu ndani, haruhusiwi kurudi tena leo. Labda mpaka tena keshoo kabla ya saa 12 jioni. Sasa hivi, yaani mida hii, katoka kunitumia huu ujumbe hapa.” Mama G, akachukua simu yake akaanza kusoma.

‘Mama, nimetoka hapo nyumbani muda mbaya. Nimepelekwa kwenye hicho chumba. Ukweli nikizuri sana, na tupo watu kama watatu tunakitaka. Ikabidi kumfuata mwenye nyumba, nyumbani kwake ili nizungumze naye, mimi mwenyewe kujaribu kumshawishi ili anikodishe mimi. Ameniambia nifuate jibu kesho. Lakini foleni ni kubwa sana mama yangu. Sasa hivi ni saa kumi na mbili kasoro. Hakuna muujiza wa kufika hapo nyumbani kwenu kabla ya saa 12. Ili nisimuudhi zaidi Geb, na nisivunje sharti jingine, nikakosa hata hiyo nafasi yakunyonyesha, naona heri nichukue tu chumba hotelini, nilale kwa usiku huu. Kesho nitajitahidi kuwahi kurudi mapema. Nimeacha maziwa yakutosha. Nina uhakika yatamtosha Liv hata mpaka kesho. Tafadhali mama yangu, hakikisha Liv wangu hanywi maziwa ya kopo. Tafadhali sana mama. Simu inaishiwa chaji. Nazima mpaka nikipata hoteli ya kulala usiku huu, ndipo nitawasha ili kukutaarifu nilipo mama yangu. Mbusu mwanangu kwa niaba yangu. Mwambie ninampenda sana.’

~~~~~~~~~~~~~~

Mama G akamaliza kusoma na ukimywa mzito ukatanda. Grace alisikika akivuta pumzi kwa nguvu akajiegemeza kwenye kochi vizuri. Danny akamchukua yule mtoto kutoka kwa mkewe. “Bwana toto zuri hili, kama toto la kimanga! Macho yake mazuri kama ya mke wangu!” Danny akaendelea kusifia huku akimwangalia Liv. “Mbona kama nimechanganyikiwa zaidi ya mwanzo! Ni nini kinaendelea?” Grace akauliza. “Acha nikueleze mwanangu, maana mimi nipo kwenye uchungu wakupitiliza. Nimeongea na Nanaa kwa kituo. Akanieleza mambo yote.” Mama G akaanza kuelezea kuanzia mwanzo anaitwa na Nanaa chuoni.

“Yaani ndio alikuwa ametoka kujifungua!?” Grace akahoji kwa mshangao mkubwa. “Haswaa. Alijifungua Jumatatu alipotoka tu kwenye mtihani, sasa jumatano asubuhi ndio akanipigia simu nikamshikie mwanae, kwa sharti nisimwambie mtu. Nikaona ameniamini mimi na kunisamehe. Kumbuka tokea nimuache nje kwenye ile harusi ya Malii, sikubahatika kupata muda naye nikaomba msamaha. Sasa kuja kunipigia simu na kunitaka msaada, nikajiona nimebahatika na amenisamehe. Sasa nikasema nisivunje Imani yake kwangu. Nimsaidie mpaka amalize mitihani ndipo tuzungumze naye.” Mama G akaendelea.

“Nikaanza kazi ya kupika hapa na kwenda kukaa naye na mtoto. Tena hapo nilimbembeleza kweli, baada ya kumuhurumia. Maana alitaka msaada kipindi anaingia kwenye mtihani tu. Muda mwingine alisema atakaa na mwanae, nisiwe na wasiwasi. Nikamuhurumia sana. Kwanza alikuwa amekonda sana. Huku ananiambia alikuwa akila kama mchwa lakini manesi walikuwa wanamcheka kuwa mtoto ndio alichukua chakula chote. Kazaa mtoto mkubwa kweli.” “Hata sasa hivi huyu mtoto ni mkubwa, hafananii na wa miezi miwili. Ehhe?” Grace akataka aendelee.

“Pili nikakumbuka jinsi Nanaa alivyohangaika kumaliza chuo. Mnakumbuka alipokuja hapa kuchukua vitu vyake ili aende chuo?” “Nakumbuka. Alikuwa kama anataka kukata roho!” “Ewaa. Sasa yote hayo nikayakumbuka. Nikasema maadamu ameniita, lazima nimsaidie. Huku nikijitahidi kukukwepa wewe na Geb. Sikutaka mtu yeyote amuingilie na mipango yake ili atulie amalize mitihani yake.”  Mama G akaelezea kila kitu mpaka Geb alipomfukuza Nanaa, akamfungia nje, jinsi anavyomnyanyasa Nanaa na mtoto wake, masharti aliyomuwekea Nanaa.

“Wakati na mimi nilishangaa siku ile kumkuta Liz yupo uchi humu ndani wakati Geb ameanza mahusiano na Nanaa!” Grace akaanza kulia. “Hata mimi nilikasirika sana, nikamwambia Danny. Tena nakumbuka nilikutana na Liz yupo uchi hapo koridoni, na mwenzie huyu yupo na boxer. Nikawalazimisha warudi chumbani wakavae, kwa kuwa Fili na Danny walikuwa wakiingia. Na hiyo ndio ikawa moja ya sababu ya sisi kuondoka humu ndani kwa haraka.” Grace aliongeza huku akilia.

“Basi, ndio Nanaa anatafuta chumba, ili angalau awe na pakukimbilia. Vitu vyake aliviacha kwenye hicho chumba, huko hosteli. Antii, yule  matroni aliyemuhudumia sana hospitalini, alivichukua ili amuhifadhie. Kwa kuwa tuliondoka kama tunakimbizwa! Nanaa analia, anataka nimlete hapa kwa mwanae. Hakuchukua vitu vyake, akaacha hivyo hivyo. Nafikiri alijua atarudi kwa haraka.  Sasa miezi miwili mingi, kukaa na mizigo ya mtu! Si rahisi. Ndio amemtafuta anamtaka akachukue vitu vyake. Sasa pakuviweka ndio shuguli.” Mama G akamalizia.

“Si angevileta hapa!?” Grace akauliza huku akifuta machozi. “Sasa avilete hapa wakati mwenye nyumba ashamuonyesha hapa ni mpitaji? Nilimuuliza hivyo hivyo. Akaniuliza swali gumu kweli yule mtoto, lililonifanya nije kulia mwenyewe baadaye, na kumshukuru Mungu kwa uzima alionipa. Japokuwa sikuwa na uwezo, lakini nikashuru Mungu alinipa uwezo wa kuwalea. Unajua Grace, unaweza usione umuhimu wa uhai wako, lakini jilinganishe na Nanaa. Mtoto ambaye hakuchagua kuzaliwa akiwa hana mama. Yule mtoto aliniambia maneno yananiuma mpaka leo. Si unamjua Nanaa, alivyo na sauti ya upole? Akaniambia hiyo mizigo yake ina vyeti vyake. Ambavyo kwake yeye ndio ndugu na kimbilio la pekee. Akaniuliza itakuaje aje avilete hapa ndani, halafu Geb aje amfukuze tena? Atavipataje tena? Akaniambia, ‘Mama, acha niwe na kwangu, sehemu ya kukimbilia. Sina ndugu wala sina rafiki wakunihifadhi, itakuaje nikija kutupwa tena nje?’ Nilishindwa chakujibu ikabidi nimuache. Maana ni kweli nilimkuta hapo nje, asubuhi, amepiga magoti, yule mtoto analia na kuomboleza afunguliwe mlango.”

“Nilikuwa nimelala, niliamka, sikuamini! Ile picha inanitesa mpaka leo. Naamka usiku natubu kwa niaba ya Geb. Namwambia Mungu amsamehe mwanangu, asimlaani. Naweza nikaamka nikajikuta machozi yananitoka. Nasema labda ndio angekuwa Grace wangu, labda na mimi ningekuwa nimekufa, wangemfanyia hivyo mwanangu! Kila siku usiku ile picha inanijia Nanaa akilia na kuomboleza pale nje. Huu ni mwezi wa pili, kazi pia imenishinda, nipo naye humu ndani namliwaza.” Grace alikuwa akilia kama mama yake Nanaa.

“Lakini Grace, Mungu yupo. Yule mtoto naona ana roho ya tofauti. Sijui kwa kuwa ameshapitia mengi! Amekubaliana na yote, ametulia, na amependeza kweli kweli. Ukimuona hutaamini kama ni Nanaa yule aliyekuwa amechoka. Si unajua ana ngozi nzuri? Basi amekuwa kama mtoto. Nilikuwa namlisha mchana na usiku ili angalau arudishe mwili. Sasa naona na uzazi umemkubali. Amependeza sana.”

“Lakini bado utamuhurumia. Asubuhi mwenye mtoto akiondoka, anaingia kule chumbani kwa Geb, anaenda kumchukua mtoto wake, analala amemkumbatia kama paka. Huwa nabaki kulia mwenyewe. Akisikia tu gari ya Geb, hata kama yupo usingizini, ataruka kama swala. Anakimbia haraka kumrudisha mtoto kitandani kwake, hapo baba yake anapotaka awekwe. Lakini hajaacha ukarimu wake kwa Geb. Japokuwa nampikia vyakula vya uzazi, lakini asubuhi lazima aamke asubuhi na mapema, anampikia Geb uji, na jioni atahakikisha Geb anachakula ndio anarudi chumbani kwake.”

“Lakini mbona husimulii jinsi alivyonitendea mimi Mama!? Mbona kama unanilaumu tu? Nanaa alinikimbia tena kwa kunitukana!” Grace alinyanyuka kama simba. Akapiga teke meza ya kioo iliyokuwepo mbele yake. “Wewe ni mbwa Geb. Mshenzi wa washezi. Unakimbiwa na pesa, una uwezo wa kulala maporini kuzisaka pesa, mpaka unazipata, iweje leo unashindwa kumtafuta Nanaa hapo Chuo Kikuu Mlimani? Tena baada ya kukufumania?” “Usinitukane Grace. Nanaa alitukuta uchi, hakunifumania.” Geb akajaribu kujitetea.

Grace alichukua kinyago cha kimasai kilichokuwa kimepabwa pembeni ya makochi, kizito, akaenda kupiga meza ya kioo yakulia chakula. “Pesa zimekufanya kuwa mnyama wewe Geb. Kumbuka sisi tulipotoka. Kumbuka Mungu alipotutoa. Mavumbini, chini kabisa. Kumbuka mateso tuliyopitia kabla hatujapata pesa.” Grace alivunja ile meza, akahamia kwenye madirisha. “Leo unapata pesa unamfukuza Nanaa? Unamuacha nje? Jeuri hiyo unapata wapi wewe?” Grace alikuwa akivunja vitu huku akilia na kuongea.

“Mkeo atazaa leo.” Mama G, akamwambia Danny. “Waache watoke. Mimi mwenyewe nimechoka kusubiri.” Danny akajibu. “Unafikiri watoto wanalelewa na maziwa ya kopo?” Grace aliingia jikoni akatoka na yale makopo yote ya maziwa, akaanza kuyafungua na kuyamwaga chini kwenye miguu ya Geb. Aliyamimina yote, mpaka akamaliza. “Mshenzi mkubwa wewe. Unafikiri watoto wanalelewa na maziwa peke yake? Ingekuwa hivyo kila mwanamke sasa hivi ungemkuta ana mtoto.” Akaenda kwenye friji akatoa maziwa yote aliyoyaacha Nanaa, baada ya kuyakamua, akaenda kumwagia Geb mwilini mwake, akatupa nje zile chupa baada ya kuzipasua pasua.

“Wewe si mwanaume? Mnyonyeshe sasa huyo mtoto leo. Mtoto anahitaji joto la mama, wewe unalala na mtoto! Una joto gani wewe la kumkuza huyo mtoto? Unampangia Nanaa muda wakurudi nyumbani halafu unakaa na mtoto wake? Unadai miezi 9 aliyokuwa na mtoto wako tumboni kwake!? Hivi unajua unachoongea wewe au unaropoka tu? Unajua shida na taabu mama anazopitia kwa hiyo miezi 9? Ungepewa wewe mimba na mwanaume uliyemfumania, nina uhakika wewe ungeitoa hiyo mimba. Nakujua wewe Geb. Usingevuka hata miezi 3 ile ya mwanzo. Hivi unajua shida ya kubeba mimba ya mwanaume unayejua analala na mwanamke mwingine? Unajua shida yake wewe? Ulimuacha nje kwenye harusi, na bado akakufuata hapa na kukuta na Liz. Ulitaka akufanyaje? ” Grace akaanza kuchana na makochi.

“Sasa hapo Danny mchukue mkeo. Tutakaa wapi?” Mama G akashituka sana. “Mwache mke wangu aongee bwana! Anajua anachoongea. Hapo ana usingizi wa siku kibao! Hawezi kulala chali, hawezi kulala ubavu, havilaliki jinsi hao watoto huko tumboni wanavyomuendesha! Na Geb analijua hilo. Umeshindwa kumuenzi mwanamke aliyekuzalia mtoto mzuri hivi!?” Danny akauliza.

“Tena ngoja niwaambie nyinyi wote kama hamumfahamu Geb. Halali na mwanamke kihasara. Liz alikuwa ananiambia, Geb alikuwa anajua mzunguko wake wa hedhi wa mwezi. Yaani yeye mwenyewe Liz alikuwa akisahau, anamuuliza Geb. Na mara zote Geb alikuwa akitumia kondomu na Liz, ila zikiwa siku za hatari, hata hakuwa akitaka kumgusa Liz. Liz alikuwa akiniambia, haamini hata kondomu huyo kwa jinsi alivyokuwa akiogapa mtoto na Liz. Mimba ya Nanaa haikuwa ya bahati mbaya. Nina uhakika Geb alipanga mpaka na jinsia ya mtoto. Geb anapenda sana watoto wa kike, na alikusudia kuzaa na Nanaa. Alimpa mimba msichana wa watu kwa makusudi, halafu sasa hivi ndio anajiliza hapa, eti ‘Nanaa alinikimbia’! Tena ulijua alikukimbia na mtoto wako tumboni kwa nini ulimuacha ateseke peke yake?” Grace aliendelea kufanya fujo pale nyumbani kwa Geb.

“Tumeishi chumba kimoja sisi wote hapa tena na marafiki zako. Muulize mama au rafiki zako kama kuna aliyewahi kuwekewa sharti hata mmoja. Ubinadamu umekuisha kabisa sababu umepata kinyumba hiki! Huna aibu, hukumbuki ulipotoka wewe?” Mtoto akaanza kulia. “Mnyonyeshe sasa. Wewe si mwanaume? Mnyonyeshe na umbembeleze mpaka anyamaze leo.” Akamchukua mtoto kutoka kwa mumewe, akamkabidhi Geb.

 “Na mama, hakuna kumsaidia huyu, akome na ndio ajue uthamani wa mama.” Mtoto aliendelea kulia. “Unashangaa nini? Si wewe unajidai unagubu wewe. Huwezi kuongea jambo likaisha, unabeba visasi? Sasa mbembeleze huyo leo mpaka anyamaze. Na hakuna wa kukusaidia.” “Jamani, ngoja mimi nikaoge, nilale.” Mama G akasimama.

“Mama unaondoka?” Danny akauliza akicheka. “Kumbe! Kazi yangu mimi ni Nanaa. Nanaa naye kachelewa kurudi, kafungiwa geti. Huyo mtoto anashikwa na yeye mwenyewe tu. Mimi hataki nimshike mwanae kwa kuwa kanikasirikia. Kama Nanaa anatoka humu ndani, basi ni heri aache kazi, aje akae na mwanae. Hataki hata nitoke naye! Juzi nilimuomba nitoke naye Liv, ili nikamnunulie mama yake nguo, akanikatalia bila aibu. Akaja kukaa na mwanae mimi nikatoka na Nanaa. Sasa sina chakufanya hapa.” Mama G akaanza kuondoka.

“Kamnunulie maziwa mengine ya kopo.” Mama G alitoa ushauri wa kumsanifu, kisha akaondoka. “Naombeni twendeni Danny, nisije nikaleta madhara makubwa zaidi bure.” Grace akamshika mwanae mkono bado alikuwa na headphone masikioni. Alikuwa amezama kwenye game zake hakuwa hata anajua kinachoendelea. Alimtoa pale kwenye kochi taratibu ili asikanyage vioo alivyovunja mama yake.

“Na kazini kesho siendi. Nenda kafanye kazi zako mwenyewe. Ukijidai kulala hapa na huyo mtoto wako, ujue kesho unaingiza hasara ya mamilioni ya pesa.”  Grace akatoka na familia yake. Alimsikia akivunja meza nyingine ya kioo ya barazani. “Hivi vitu ndio vinamtia wazimu huyu. Sijui nichome moto hii gari yake mpya?” Geb alimsikia dada yake akiuliza. “Twende bwana Grace! Hasira zote hizo ni usingizi tu wala sio Nanaa.” “Usiniudhi zaidi Danny! Unajua shida ya kubeba mimba na kuzaa wewe? Tena maumivu yanazidi unapomzaa halafu upokonywe! Yule binti yupo kwenye hali ngumu zaidi.” “Basi mama, twende.” Baada ya muda akasikia gari ikitoka.

Nani Kama Mama!

Oliva alianza kulia kama amechapwa. Aliongeza sauti na kulia kama kengele. Geb alimbembeleza huku anazunguka nyumba nzima. Mwishowe Mama G akasikia wanatoka. Baada ya muda wakarudi huku mtoto bado analia sana. Mama G, akatoka kwenda jikoni akijidai anataka kunywa maji ili aone tu kinachoendelea. Akamkuta Geb amenunua maziwa mengine ya kopo na chupa za maziwa. Akatengeneza yale maziwa, akayapima kama yana joto zuri. Mama G akavuta kiti cha palepale jikoni akakaa huku anamwangalia. Akamfuta mtoto wake machozi, akampa ile chupa.

Liv akapokea ile chuchu kwa haraka sana. Alipoweka tu mdomoni, akatema na kuanza kulia upyaa. Mama G akaanza kucheka. “Watu na mama zao! Hataki ujinga huyo mtoto. Unamdanganyishia unga wa viwandani wakati maziwa ya mama yake yapo!” “Sasa Grace si kayamwaga.” “Basi leo jasho litakutoka. Kama namuona sasa hivi Nanaa. Kalala kwenye kitanda kisafi. Hakuna manyanyaso, hakuna ubabe wa usiku. Kwa raha zake!” Mama G akaanza kucheka tena.

“Sasa ngoja apate bwana anayejua kubembeleza, ampe mimba ya pili. Wee! Kama nakuona na mwanao huyo unayejidai nae. Mtachina hapa. Na lile toto lilivyo zuri, tena sasa hivi ndio limezidi kuiva, limenona! Akicheka na zile dimpozi utafikiri anakuita! Akiongea utafikiri anakubembeleza! Sasa apate dume lenye upendo, likamkabidhi hata funguo za chumba kimoja tu. Akamwambia Nanaa, hapa kwangu ndio kwako, kuwa huru. Hutakaa ukamuona humu ndani. Atakuachia mtoto huyo, mbaki mnabembelezana mchana na usiku.” Mama yake akazidi kumkera.

“Tena wanaume wenye akili walivyo, wakimpata mtoto kama yule, hawamuachii mpaka wamzalishe mara mbili au tatu ndio wanamuachia. Si umemuona Danny mwenzio? Anahangaika na Grace mpaka leo. Basi unaona mwenzako mjingaa! Haya baba. Wewe si ulitaka mtoto ukadhani anachotaka mtoto ni maziwa ya kopo tu? Sasa Nanaa kakuachia mwanao. Huyooo! Wewe mwanaume wa shoka, hangaika naye leo. Ujue kazi ya mama ni nini.” Mama G, alimuacha hapo jikoni akihangaika na mtoto wake.

Liv alikuwa kama ametumwa! Hakuweka kituo, aliendelea kulia. Akarudi naye chumbani akamuwekea michezo yote kitandani, lakini hakunyamaza. Akakumbuka hajambadilisha diaper. Akahisi ndio sababu. Wakati anakwenda kwenye kabati ya mtoto, akakutana na pesa. Akafikiria kidogo, akajua Nanaa ndio aliziweka pale. Akajua ni zile pesa zote alizokuwa akimuachia Nanaa. Akasimama pale kwa muda akifikiria. Akashituliwa na sauti ya Liv akizidi kulia. Akaenda kumbadilisha diaper akaamua ambadilishe na nguo, lakini haikusaidia. Akamuweka kifuani kama alivyozoea zamani, lakini haikusaidia. Akazima taa zote ili chumba kiwe giza kabisa labda mwanga wa taa ndio unamfanya asilale, lakini haikusaidia. Liv alizidi kulia mpaka akapata joto. Yalishapita masaa matatu mfululizo Liv akilia tu.

~~~~~~~~~~~~~~

Jeuri Ya Geb Itaishia Wapi? Baada Ya Kumtenda Nanaa Kikatili, Hasira Ndio Zinamwisha Geb. Grace Amemjia Juu Na Kumfungua Macho Pamoja Na Mama Yake. Liv Naye  Anamkumbusha Baba Yake Kuwa Yeye Hakuokotwa, Anaye Mama Yake. Nanaa Yupo Kwenye Harakati Ya Kutafuta Kwake. Tena Safari Hii Akiwa Amehakikishiwa Pale Ni Nyumbani Kwa Geb, Na Yupo Kulea Tu.

·      Je Nini Kitaendelea Kati Ya Wazazi Hao Waliobeba Jukumu La Oliva?

·      Mahusiano Ya Geb Na Grace Yatakuja Kupona?

·      James Hana Habari Kuwa Geb Amemzalisha Dada Yake. Mara Ya Mwisho Ilikuwa Ni Onyo Tu, Lakumtaka Akae Naye Mbali. Leo Amemzalisha!

Nini Kitaendelea?

Usikose Muendelezo

 

 

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment