“Unaniletea ujinga mimi!? Unafikiri watoto
wanakuzwa na maziwa tu? Kama ndio hivyo si kila mwanaume ungemuona hana mke ana
watoto tu! Kama unafikiri hizo pesa ndio kila kitu, mbona nilivyowazaa baba
yenu asiwachukue akawalea nyinyi kwa maziwa ya kopo au ya ng’ombe kwa kuwa
alikuwa mfugaji? Acha ujinga wako. Umenisikia Geb?” “Nanaa alikuwa anatoroka.”
“Kinachomuweka hapa nini, nawakati wewe umekuwa kama mwehu? Hata mimi
ningetoroka. Nipe hizo funguo haraka. Unamfungia mzazi nje? Hata damu ya uzazi
haijakatika, unamfungia nje na baridi hii! Umechanganyikiwa wewe!? Huyo mtoto
hata kitovu hakijakauka unataka kumtengenisha na mama yake! Umelaaniwa wewe?
Haraka sana nipe funguo.” Geb akampa funguo mama yake.
“Ulipokuwa ukizunguka naye kwenye mahoteli,
nakujiiba kuingia chumbani kwake usiku, unafurahia, hukuwa ukijua kutunza? Ulitaka
kujiridhisha tu halafu umuache, utegemee akae anakulilia wewe?” “Nanaa mwenyewe
ndio alinikataa mama, sio mimi.” “Kama wewe mwanaume kweli kwa nini hukwenda
kumtafuta na kumbembeleza? Si alikuwa hapo chuo kikuu? Sasa hivi ndio unajidai
kulalamika umefichwa! Umefichwa! Umefichwa nini wakati ulijidai wewe unakiburi?
Wenzio tunajua kubembeleza ndio maana amesamehe.” Mama G alikuwa akiwaka kama
moto. “Sasa nikusikie tena.” Mama G akamchimba mkwara. Geb akanyamaza
akionyesha amekasirika sana.
Akatoka
pale chumbani kwa Geb kwa hasira kuelekea nje kwa Nanaa. Alifungua milango yote
akamnyanyua Nanaa pale alipokuwa amekaa chini, aridhini akilia. “Njoo Nanaa
mwanangu.” “Geb
amenifukuza mama.” “Acha kusema
uongo Nanaa. Sio wewe uliondoka humu ndani tena huku ukinitukana?
Nilikubembeleza ubaki, ukasema unaondoka mimi ni ukurasa uliofunga! Leo unataka
kuondoka tena na mwanangu, umpeleke kwa mabwana zako! Hujui kutulia sehemu moja
Nanaa. Umezoea kuruka ruka, unataka ukaanze kuhangaika na mwangu!” Mama G akamwingiza
ndani.
“Wewe ndio muongo. Uliniahidi nini
tulipokuwa Morogoro? Uliniahidi utakuwa na mimi wakati wote.” “Sasa kwa nini uliondoka
kama uliamini? Wewe uliniambia ungekuwa mlinzi wangu. Sijakuona ukilinda
chochote zaidi ya kukimbia kimbia!” “Ulitaka
nikulinde hata ukiwa na mpenzi wako?” “Nilikwambia Liz, ni msichana
niliyekuwa naye zamani na hata yeye nilishamwambia basi! Tukaachana kwa
ajili yako.” “Sasa mbona niliwafumania?” “Hujawahi
kunifumania Nanaa, acha uongo. Mimi sio muhuni. Najiheshimu. Siwezi nikawa na
lala na wewe huku na lala na Liz. Sina ujinga huo, naomba uniheshimu. Kama wewe
unaweza kufanya hivyo ni wewe, acha kuniingiza kwenye huo uchafu.” Nanaa
akashangaa sana.
“Unataka kukana nini wewe Geb
wakati niliwakuta wote mpo uchi chumbani kwako?” “Leo ndio unauliza, wakati siku ile
nilikubembeleza unisikilize ukakataa ukasema nitakudanganya kama wanaume
wengine waliokudanganya! Sasa hata nikikwambia, kitakachokufanya uniamini leo
ni nini? Kutukuta uchi ndio umenifumania? Tena unazidi kudanganya wakati
nilikuomba usidanganye!” “Sasa hapa nimedanganya
nini?” “Wewe siku ile umemkuta Liz yupo uchi kitandani kwangu, na mimi
natoka bafuni kuoga. Sasa hapo ndio ulinifumania?” “Sasa
je? Kwa hiyo ulitaka mpaka niwakute mkifanya mapenzi?” Mama G alitafuta
mahali akaaa ili asikilize vizuri.
“Sasa nisikilize Nanaa. Wewe sio mtu wa
kuaminika. Hujui kupenda wala hujui kutulia sehemu moja. Kitu ambacho
sitaruhusu kitokee kwa mtoto wangu. Wewe hangaika na wanaume wote unaowataka
hapa duniani. Fungua kila kurasa na kufunga. Hama kitanda kimoja mpaka kingine
mpaka uje ufe kwa magonjwa. Lakini sio na huyu mtoto wangu. Umenielewa Nanaa?
Nakupa nafasi ya mwisho. Nataka uchague wewe mwenyewe, tena ukijua wazi, huyu
mtoto hapa ni kwao. Hatawahi kuishi kwenye nyumba za kupanga na wanaume zako.
Hatakaa atoke humu ndani bila idhini yangu. Nilikufungulia mlango mpaka wa moyo
wangu, ukaamua kunitesa na kuniacha nikiwa nakuhitaji. Nilikuwa silali nakuja
hospitalini na nyumbani kwa Antii usiku kucha nipo na wewe nikikuuguza bila
kulala. Japokuwa James alinifukuza lakini sikuacha kuwa na wewe Nanaa. Kama
ningekuwa na Liz, kwa nini nilikufuata niwe na wewe wakati hukuwa hata unajua
kama nipo?” Nanaa akanyamaza hakujua hata kama Geb alimuuguza. Akanywea kabisa.
“Umepona hata kunitafuta! Nimekuwa na kazi ya
kukupigia kama mwehu! Unawasiliana na watu unaowataka wewe, mimi unanipuuza.
Nimekuwa kama mwehu kwa ajili yako! Mara ya mwisho nimekupigia simu,
ukanishutumu. Nilijaribu kukuelezea kila kitu na kukuomba msamaha wa kukusahau
pale nje siku ya harusi. Usifikiri kukuacha nje ukumbini ni kitu nilichokifurahia
Nanaa. Kiliniuma kuliko ambavyo ningefungua mdomo wangu kukueleza. Nilikwambia
nina hamu na wewe, ukanikatia simu. Matokeo yake ukaja hapa, ukanisingizia na
kuniacha huku ukinitusi na kunifananisha mimi na wanaume zako wengine. Sijakusamehe
kwa hilo, kwa kuwa ulinidhalilisha sana. Mimi sina mchezo wa kuhama vitanda na
wanawake tofauti tofauti, halafu nikajisifia. Naumia sana kuona naachana na
mwanamke ambaye nilishamvulia nguo. Naumia sana Nanaa. Mimi sio kama wewe.
Sijisifii kubadili wanawake. Inaniuma sana. Hasa wewe kwa kuwa nilikupenda kwa
dhati, na nikakutanguliza kwenye kila kitu. Umenisaliti Nanaa. Na ninarudia
tena, sijasamehe.” Mama G ndio alikuwa akisikia mambo mengine kwa mara
ya kwanza. Akawa anasikiliza kwa makini.
“Sasa, leo
mbele ya mama. Nakupa nafasi ya mwisho, ili ukiharibu na mama awe shahidi
yangu. Na pia ili usinikosanishe na mama yangu.” Nanaa alibaki
akilia.“Unakubali kukaa hapa ili kulea mtoto wangu kwa masharti yangu au
hutaweza kuishi hapa? Sitakusumbua na wanaume zako, ila ujue saa 12 jioni uwe
umeingia humu ndani. Ikipika hata dakika moja hujapita pale getini, usirudi
tena siku hiyo. Siku utakayorudia kutoka na mtoto bila idhini yangu, ndiyo siku
yako ya mwisho kukanyaga humu ndani. Hutakaa urudi na ndio utakuwa mwisho wako
na huyu mtoto. Nitakushitaki kwa kuzaa mtoto wangu na kumficha hosteli za chuo
akiwa hana uangalizi mzuri. Na wala huna mahali pa kumuweka. Najua nitashinda
kesi kwa kuwa huna hata uwezo wa kifedha wa kumlea huyu mtoto, wakati mimi nipo
na nina uwezo.” Huo ulikuwa ukweli ulioanza kumuogopesha Nanaa.
Geb akaendelea.
“Haruhusiwi kuleta mwanaume yeyote humu ndani, isipokuwa James, kaka yako. Sasa
je, unabaki humu ndani au unaondoka ukaendelee na maisha yako uliyokwisha
kuzoea kuyaishi?” Kimya, Nanaa alisikika akilia kwa uchungu sana. “Naomba tusipoteze muda Nanaa. Unaondoka au
unabaki.” “Mimi sio malaya.” “Ulinimbia
mwenyewe, tena kwa kujisifia. Sasa, unaondoka au unabaki?” Mama G, alikuwa
kimya akiwasikiliza.
“Namtaka
mtoto wangu Geb. Nipe nikamlee hata miaka mitano tu, ndio umchukue.” “Haitakaa ikatokea Nanaa.
Kama kuna mwanaume ulimdanganya huyu ni mtoto wake, nashauri tafuta uongo kama
uliokuwa ukinidanganya mimi, na yeye ukamdanganye. Nina uhakika atakuamini tu.
Maana na mimi nilikuamini.” “Sijawahi kukudanganya
Geb, na Mungu ni shahidi.” “Nanaa! Naomba tusirudie mambo. Mimi
nikiongea sana, mdomo na kichwa vinaniuma. Nataka jibu la mwisho. Unabaki au
unaondoka?” “Naomba
kubaki.” Nanaa alijibu kwa upole
huku akiendelea kulia. “Tafadhali zingatia masharti. Sitakusamehe endapo
utavunja hata moja wapo.” Geb akarudi ndani chumbani kwake, akawaacha hapo sebuleni.
~~~~~~~~~~~~~~
“Mama, mimi sio muhuni na wala
sijamdanganya Geb. Mungu wangu ni shahidi.” “Naomba utulie Nanaa. Umechagua jambo zuri,
kubaki na kumlea mtoto wenu. Naomba akili zako zihamie kwa mtoto tu, hayo mambo
mengine yaache kwanza. Lea mtoto wako. Ni bahati ambayo wanawake wengi
wanatamani kuipata. Lakini wengine wanakufa hata kabla hawajanyonyesha watoto
wao. Wengine wanashindwa uwezo, hamna mazingira mazuri ya kulea watoto wao. Na
mambo mengine mengi najua wewe unajua. Maadamu Mungu amekupa nafasi hiyo, upo
hai, unamaziwa, na afya njema, weka kila kitu pembeni, mlee mtoto wako tu.
Umesikia mama?” Mama G akaenda kumnyanyua pale na kumuingiza chumbani.
Alikuwa amejaa michanga
mwili mzima kwa kugaragara chini alipofungiwa nje na tayari alishakuwa amelowa
damu. Akamchemshia maji ya moto, akaenda kumsaidia kuoga na kumkanda,
akamrudisha kitandani. Akamfunika mashuka mengi na blangeti juu, akampa uji,
akanywa, akarudi kulala.
~~~~~~~~~~~~~~
Aliamshwa na Geb.
“Mchukue mtoto, naenda kununua vitanda.” Nanaa alikuwa amepooza. Geb alimpa maneno
ya hukumu, akajuta siku ile kuondoka bila kumsikiliza Geb, aliyekuwa akimsihi
atulie wazungumze. Hakuwa hata akijua kama Geb alikuwa akijiiba kukaa naye
usiku wakati mgonjwa. Alimpokea mtoto,
Geb akatoka. Akakumbuka wosia wa Grace. Alimwambia asikubali hisia zake zimtawale.
Alijuta. Akatamani kama angerudisha siku nyuma, abaki amsikilize Geb. Alijiona
mjinga vile alivyoteseka na mimba ya mwanaume ambaye alitaka mtoto wake.
Alikejeliwa na wanafunzi wenzake, bure tu. Akabaki akiwaza.
~~~~~~~~~~~~~~
Alirudi na kitanda kama kilekile alichokuwa akilalia
mwanzoni, godoro jipya, mashuka mapya na kitanda cha mtoto wake
kilichokamalika. Alitoa kile kitanda cha zamani, akaweka kipya. Na kitanda cha
mtoto wake alikifunga pembeni ya kitanda chake, chumbani kwake. Akaingia
chumbani kwa Nanaa, akamkuta amelala kitandani amemkumbatia mtoto wake.
Akamchukua yule mtoto na kutoka naye.
Nanaa alianza kulia tena. Alilia kwa muda mpaka
akasikia mlango unafunguliwa tena, Geb akarudi. “Sikuwa
nimeenda kwa mwanaume mwingine, Geb! Naomba usiniadhibu bila kosa.” “Nimebadili
kitanda kizima. Kila kitu ni kipya. Nimemnunulia Liv kitanda chake. Kipo
pembeni ya kitanda kikubwa, chumbani kwangu. Na hii ni monitor yake
akiwa amelala, unaweza kumuacha kwenye kitanda chake, wewe ukaenda popote ndani
ya hii nyumba ukiwa na hii monitor, akiamka utamsikia. Kama utataka
kulala pembeni yake, unakaribishwa kulala kwenye kitanda ambacho sijalalia
na wanawake zangu.” “Kwa nini tumlaze mtoto
peke yake Geb? Naomba nilale na mwanangu!” “Huyu mtoto atakuwa mkubwa
zaidi ya hivi alivyo sasa, na si muda wote atakapotaka kulala na wewe utakuwa
unataka kulala. Huwezi kumuacha kwenye kitanda peke yake, ataanguka. Ndio maana
nimemnunulia kitanda chake ili aanze kuzoea kulala peke yake.” “Kwa hiyo kwa sasa naruhusiwa kulala naye?” “Sasa
hivi nitakuwa naye. Ukitaka kumnyonyesha, unaruhusiwa kuja kumnyonyesha na
kumuacha kwangu. Kila siku usiku nitakuwa nalala naye mimi, mchana namlaza
kwenye kitanda chake.” “Yaani mimi siruhusiwi
kulala na huyo mtoto?” Nanaa aliuliza huku akilia. Geb akatoka.
Baada ya muda mfupi Mama G akaingia. “Unalia nini
tena?” “Geb amenipokonya mtoto mama.” Nanaa
akamuelezea kila kitu. Mama G, akacheka. “Wala usilie. Yatamshinda tu.” “Hawezi mama. Jana usiku kuchwa alikaa pale kwenye kochi
amemkumbatia mwanae.” “Wewe tulia wala usilie. Fuata kila kitu
anachotaka, mpaka mtoto wako achangamke, akufahamu wewe vizuri. Jifunze kucheza
na kucheka na mwanao. Mfanyie vitu ambavyo ni wewe tu unaweza kumfanyia.
Akishakuelewa wewe, nitakufundisha kitu kingine. Sasa hivi jifanye mjinga,
fuata kila anachokwambia. Mimi namjua Geb akiwa amekasirika. Huwa najua ni wapi
pakumbania. Wewe tulia kabisa. Achana na tabia za kulialia. Akikuita
umnyonyeshe mtoto, wewe nenda tena ukiwa umetulia.” “Kaniletea
kimashine hiki hapa! Eti mtoto akiamka nitamsikia. Inamaana anachojaribu
kuniambia hatakuwa akiniita, nikimsikia mtoto ameamka niende mimi mwenyewe.”
Mama G alicheka akatingisha kichwa.
~~~~~~~~~~~~~~
Mama G akamtuliza akatulia. “Kwani siku hizi
hafanyi kazi tena huko BOT?” “Aliacha kazi. Siku hizi anafanya biashara tu.
Kanunua jengo moja la gorofa hapo Ubungo, kalitengeneza vizuri. Ofisi zote
kahamishia kwenye hilo jengo. Hata ofisi ya Grace ipo hapohapo. Chini
ametengeneza maduka, juu ndio zipo ofisi zao. Kila duka la hapo chini
linamwingizia pesa nzuri tu. Ana sehemu amejaza mashine ya kutolea kopi, anauza
vitabu na mambo kama hayo ya Stationary.
Upande mwingine ameweka duka la jumla la vinywaji. Siku hizi anasambaza
vinywaji karibia mji mzima huu wa Dar. Upande mwingine anauza mazao kwa jumla
na rejareja. Kama lile duka langu, lakini yeye ameongeza mafuta. Anakusanya
mafuta ya kila namna kutoka vijijini, anakuja kuyaweka kwenye madumu ya kila ujazo,
kisha anauza. Kuanzia mafuta ya mawese, alizeti, mzeituni, na mengineyo. Ana mashamba
ya asali huko Tabora. Kwa hiyo anauza ile asali nzuri. Watu wengi wanapenda
asali yake, wanasema ni nzuri hachanganyi na vitu vingine. Ndio na huo Mchele,
mahindi, na maharage pia anauza.” “Na ile ofisi ya Grace kule kwa zamani?”
Nanaa aliendelea kuhoji.
“Si unajua pale walikuwa
wanakodi?” “Sikujua!” “Pale walikuwa wanakodisha kutoka kwenye kampuni ya
muhindi mmoja hivi. Wamepaachia. Akahamishia hiyo ofisi kwenye hilo jengo hapo
Ubungo. Tena aliamua kununua godauni huko Buguruni, naona huko ndiko
wanakohifadhia mazao na dada yake. Pakubwa sana. Ndiko wanakoweka mali zao
zote. Naona mambo yao sio mabaya. Grace anapesa kweli siku hizi. Na siku hizi
Geb hasafiri sana kama zamani. Amefungua ofisi huko mikoani, ameweka
wafanyakazi wanao msaidia kumkusanyia mazao na kumtumia huku. Kila mkoa ambapo
anapata mazao mengi, amefungua ofisi.” Nanaa akanyamaza.
~~~~~~~~~~~~~~
“Wewe
usiwe na wasiwasi hata kidogo. Ni hasira tu za kumuacha. Hana lolote!” “Sikumuacha
mama. Siku nilipokuja kumwambia ni mjamzito, ndio siku nilimkuta chumbani na
Liz, tena wote wako uchi. Nilishituka sana mama yangu. Nahisi sijui ni hasira,
sikutaka hata kumsikiliza, nikaondoka. Matukio kama hayo yameshanitokea mara
nyingi sana kwenye maisha yangu. Sijawahi kubahatika kupata mwanaume
mwaminifu.” Nanaa akafikiria kidogo.
“Unajua siku ile ya harusi mliponiacha pale nje,
nilimuona Geb na Liz wakiingia pamoja huku wameshikana mikono! Geb aliniahidi
wakati nipo saluni kuwa japokuwa atasimamia harusi, lakini atakuwa akija tukae
wote. Nilikaa pale nje zaidi ya masaa 4, mama! Hakuna hata aliyetoka kunitafuta!
Zaidi Geb aliyejua nipo pale kwa ajili yake! Nikajua ni kwa sababu yupo na Liz.
Kuja tena kumkuta tena yupo uchi na Liz, nikajua ni yaleyale. Sikutaka
kudanganywa tena mama. Nikaamua niondoke tu. Hata hivyo nilijiona mimi ndiye
niliyeingilia mapenzi yao. Nilianza mahusiano na Geb, mimi nikiwa sababu ya
kuvunjika hayo mahusiano yao. Nikajua waliamua kusameheana, ili waendelee na mapenzi
yao.” Mam G akashangaa kidogo.
“Ngoja kwanza Nanaa. Wewe unahusika vipi kwa
kuvunjika kwa mahusiano yao?” “Moja ya masharti ambayo Liz alimpa Geb, ili
waendelee kuwa wapenzi, ni kunitoa mimi hapa ndani. Ndio Geb akamwambia
hatanifukuza mimi humu ndani kama ulivyomsikia Danny akisimulia siku ile
asubuhi ya harusi ya Malii, pale jikoni. Hilo ndilo lilikuwa sharti mojawapo na
mengine.” “Yapi?” Nanaa akasita kumwambia Mama G. Akaona anyamaze tu.
“Naomba nisikwambie mama yangu. Tuyaache tu.
Lakini Geb aliniambia kuwa alipomkatalia ndio akasema basi, hawezi kuendelea
tena na Geb. Yeye hawezi kuishi kwenye nyumba yenye watu wengi.” “Yule msichana
ni mwehu tu. Hata hivyo nisingekubali aolewe na Geb.” “Mama wewe!”
“Nakuhakikishia. Geb asingethubu kumuoa. Niliwaacha tu nikijua ni mambo ya
muda. Unafikiri ingekuwa kuolewa si angeshaolewa muda mrefu sana? Huyo Geb
anasubiri nini sasa hivi asiyeoa tukapumzika? Au mabinti wa watu nao
wakapumzika? Anatongozwa mchana na usiku mpaka unawahurumia hao wanawake! Huyo
Liz nilimuona sio mke wa kuwekwa ndani. Hafanani na maisha yetu hata kidogo.”
Nanaa akamwangalia asiamini.
“Sasa Geb angemng’ang’ania amuoe?” “Nakwambia asingemuoa.
Au kwa kuwa unaniona nipo kimya? Naangalia kila kitu. Kinachotokea ni kwa kuwa
nakiruhusu. Geb na Grace hawawezi kufanya chochote bila kuniambia.
Wananiambia kila kitu, na hawawezi kufanya jambo mpaka waone nimewapa
baraka zangu. Kwa hilo namshukuru Mungu nimepata watoto wanao nisikiliza.
Kwanza ujue mimi huyo Liz sijawahi kumuona tena humu ndani tokea siku ile
alipokuja akataka kuingia chumbani kwa Geb, Geb akamkatalia?” “Kweli mama!?” Nanaa hakuamini.
“Kweli tena. Tangia siku
ile, sijamuona Liz humu ndani. Na wala sijamsikia Geb akimtaja. Geb hanifichi
kitu. Mimi ndio msiri wa Geb. Na pia sikutaka akuchezee wakati nilijua yupo
Liz. Ikabidi kumuhoji mapema. Ndio akanihakikishia aliachana na Liz kabisa na
hata iweje hatamrudia tena. Na mimi namjua Geb, anamsimamo sana. Hawezi
kujipinga na si muhuni hata kidogo. Kama ingekuwa wamerudiana, angeshaniambia.
Kuna kilichotokea tu siku hiyo na Liz. Mwache kwanza.” Nanaa akabaki
akiwaza. Mama G, akacheka.
~~~~~~~~~~~~~~
“Unacheka nini?” “Geb ananikumbusha sana baba
yake. Mzee alikuwa mkorofi yule! Hujawahi kuona. Halafu mkali kama pilipili. Geb
amerithi kila kitu kutoka kwa baba yake, kasoro ukimya. Ukimya wao hawa
wawili, yeye na dada yake, umezidi. Baba
yao alikuwa akiweza kugomba haswa mpaka nyumba ikatikisika sio kama Geb
anayekasirika kimya kimya. Lakini tabia hizo za hasira za Geb, ni kama baba
yake. Hivyo hivyo. Kabla yakunifanya kuwa wake, alinijaribu sana.” Mama G
akacheka tena huku anavuta hisia.
“Hakika alinijaribu yule Mzee! Isingekuwa kuwa
mkorofi, na nina msimamo, nisingefanikiwa.” Nanaa akajiweka sawa huku akicheka.
“Acha umbea wewe mtoto!” “Bwana nisimulie.” “Na usicheke.” “Kidogo tu mama.”
Mamaa G, akaanza kucheka tena. “Ona. Wewe mwenyewe yanakuchekesha!” “Yaani
nakaaga mwenyewe najiuliza hivi akili zangu Mungu aliziumbaje!? Huwa sielewi.
Nilifanya kituko cha mwaka. Mimi mwenyewe nilikuwa najishangaa.” “Ilikuwaje?”
Nanaa akahoji kwa shauku zaidi.
Historia ya Mama G.
“Mimi hivi unavyoniona, sijui kabila langu wala
sijui wazazi wangu. Nasikia tulizaliwa mapacha. Mwenzangu alikuwa wakiume.
Unapajua Peramiho, ipo Songea?” “Nimeshawahi kupasikia.” “Basi hapo Misheni
ndipo tulipoenda kutupwa mimi na mwenzangu wa kiume. Aliyetutupa hatumjui.
Wanavyosema, itakuwa tuliachwa hapo usiku, padre aliyekuwa ameenda kufungua
kanisa, akatukuta hapo. Kwa kifupi mwenzangu alifariki masaa machache tu
tulipofika hospitalini, mimi nikaishi. Ndio chanzo huyo padre kunipa jina la
Oliva. Kama vile Olive tree. Unajua asili ya miti ya mizaituni inastawi vizuri
kwenye udongo usio na rutuba. Ukiweka kwenye udongo wa rutuba, haitengenezi
mafuta mazuri. Sasa kaka yangu alikufa sababu ya mazingira yale mabaya, lakini
wanasema wakanikuta mimi nipo nacheka.” Nanaa akacheka.
“Nikarudishwa pale kituoni nikaanza kulelewa.
Unaambiwa nikawa kama mtoto wa kila mtu. Unibebe, uniweke chini, mimi nipo sawa
tu. Siumwi wala silii. Chakula chochote kile mimi nakula. Nikawa napenda vile
vitu vya hatari zaidi. Ukiniambia nisishike moto ni hatari, basi ndio kama
umenituma! Nikaendelea hivyo mpaka nimekuwa. Mkorofi kweli kweli. Masista na
padre wote walikuwa wakinijua Oliva.
Nikaanza shule. Lakini nikajikuta sipendi sana shule. Nikamaliza darasa la 7
kwa shida sana. Tena kwakusukumana na masista. Wakataka kuniingiza kusomea
usista, nikawaambia mimi nataka mwanaume.” Nanaa akacheka sana.
“Usicheke. Tena nilikuwa nikiwaambia bila woga.
Nikakataa kwenda sekondari. Wakanilazimisha kwa kuwa nilikuwa nimefaulu vizuri,
nikachaguliwa kwenda Kilakala Sekondari. Wao wakaamua kunihamishia Songea girls
ili niwe karibu nao. Nikasoma mwaka wa kwanza, wa pili mwishoni nikatoroka
nikaamua kuhamia Dar. Hapo napasikia tu. Simjui mtu yeyote yule. Nikawa nasikia
sifa zake kuwa jiji la Dar ni zuri sana, ila maisha ni magumu. Nikasema
napataka hapohapo. Shule zikafungwa, badala ya kurudi kwa masista nikaamua
kutorokea Dar.” “Mama wewe! Sasa shule?” “Nimekwambia mimi shule nilikuwa
sipendi. Sio kwamba nilikuwa mjinga, lakini sikupenda tu kukaa darasani.” Nanaa
alikumbuka aliambiwa na Geb mama yao ni mkorofi. Akaanza kumwangalia mara mbili
mbili huku akicheka.
“Bahati yangu ilivyokuwa nzuri, wakati nipo
njiani kuja huku jijini nikakaa na kijana mmoja hivi. Alijitambulisha kwa jina
la Chalii. Lafudhi ilikuwa ya kichaga kabisaa. Kama kawaida yangu nikaanza
kumchokoza kwa kuwa nilijua amenipenda. Hapo binti mdogo, umbile kama vile
unavyomuona Grace. Akachanganyikiwa kweli kweli. Akaanza kujisifia alivyo na
pesa na nikimkubali atanitunza. Basi nikamwambia akitaka nimkubali, anitafutie
kazi. Akasema dada yake na mumewe wana shamba kubwa sana nje kidogo ya jiji la
Dar, Kibaha. Wana kituo cha maziwa hapo hapo Kibaha, atanitafutia kazi hapo.
Basi nikamuahidi kama akinitafutia kazi na sehemu ya kuishi, ningefanya naye
mapenzi. Ahadi hiyo nampa usiku, tupo njiani. Tunakuja Dar. Wakati huo mabasi
yanasafiri usiku. Kuja kupambazuka aliponitizama vizuri, akazidi kuchanganyikiwa.
Basi akawa kama kapagawa. Akaninulia vyakula njiani huku anajigamba kweli
kweli. Mimi nimetulia tu namsikiliza.” Nanaa akabaki anatingisha kichwa.
“Tukashukia Kibaha, akanitafutia chumba kwenye
nyumba za kulala wageni. Eti na yeye akataka tulale naye.” Mama G akaanza
kucheka. “Ulifanyaje mama wewe!” “Nilimuadabisha! Hakika hatasahau. Nikamwambia
makubaliano ni anitafutie kazi kwanza na mahali pakuishi ndio nitampa mapenzi.
Basi akaondoka pale chumbani na maumivu. Kesho yake akaja kunifuata akaniambia
natakiwa kwenda kwenye usahili wa kazi. Basi, ilikuwa asubuhi tu. Nikatoka
naye. Kwanza sikuamini kama atarudi jinsi nilivyomfanyia usiku uliopita.”
“Kwani ulimfanyaje?” Nanaa akazidi kudadisi.
“Mbea huyu!” “Bwana niambie mama!” “Nilimpiga
teke la nguvu huku chini. Alilala chini kama dakika 5, anaugulia maumivu.”
“Mama wewe!” Nanaa akaanza kucheka. “Kumbe! Makubaliano yetu ilikuwa anitafutie
kazi na sehemu yakuishi. Sasa leo iweje atake kuvunja makubaliano? Nikampiga
nakumfukuza.” Nanaa akazidi kucheka.
“Ehe?” Baada yakutulia Nanaa akataka aendelee.
“Basi, akanipeleka mpaka kwa Mzee Magesa.” “Baba yake Geb!?” Nanaa akauliza na
mshangao kidogo. “Ndiyo! Yaani ile kumuona tu yule Mzee, nikajiambia lazima
yule ndio aje awe mwanaume wangu wa kwanza.” Nanaa akaficha uso. “Sasa
ulimpendea nini?” Nanaa akauliza kwa aibu. “He was tough. In every way. He was
tough and very handsome. Yaani kwa kumwangalia tu, unaona vile mwanaume yule
alivyokuwa amesimama na nguvu kama dume kwelikweli. Macho yake ndio
yalinimaliza kabisa! Tena nilimkuta anagombesha wafanyakazi wake. Chalii
akanitambulisha, akamwambia anipeleke ofisini kwake, nikamsubirie huko.
Nikaenda, nikakaa. Baada ya muda akaja. Akawa anafanya mambo yake hapo kwenye
meza yake huku mimi namwangalia. Akaandika wee, huku amekunja uso.” Mama G
akacheka.
“Yaani yule mzee hakuwahi kunisahau. Unajua
wakati anaandika na mimi nikamwambia naomba kalamu na karatasi. Akanyanyua uso
kunitazama. Nikarudia, ‘Naomba kalamu na karatasi nataka kuandika kitu.’ Yule
mzee akanipa. Nikaanza kuandika.
Nikaandika huku nasema, ‘Chai nzito au maziwa ya cocoa, maji ya kunywa,
juisi, nyama za kukaanga pamoja na kitafunio kizuri. Mboga za majani.’ Yule
Mzee akaacha kuandika alichokuwa akiandika, akabaki akiniangalia, maana
nilikuwa naongea kwa sauti.” “Ni nini sasa?” “Yule Mzee naye akaniuliza hivyo
hivyo.” Mama G akaanza kucheka.
Kisha akaendelea. “Nikamwambia naandika vitu
ambavyo kama mimi ningekuwa mkewe, ningehakikisha unavipata asubuhi kabla
hujaja kazini. Nikaandika tena chini huku akinitizama. ‘Kufanya akili zake
zitulie, ili ajifikirie yeye mwenyewe.’ Kisha nikamaliza.” “Mama wewe!” Nanaa
akatoa macho kwa mshangao.
“Ujue yule Mzee alibaki kama hivyo wewe unavyo
niangalia! Ni kamwambia tena. ‘Lakini hiki cha mwisho kinaweza kuwa cha kwanza.
Ukijifikiria wewe mwenyewe, utajaribu kutafuta mazingira ya kula vizuri, kulala
vizuri, kunywa maji ya kutosha, halafu utajithamini wewe kuliko pesa. Kwa kuwa
pesa hainunui uhai. Kwa hiyo nitahakikisha unaondoka nyumbani ukiwa umetulia.
Ili ukija huku kazini ukikutana na watu wajinga kama hawa wafanyakazi wako,
hujimalizi mwenyewe kwa kukasirika. Kwa kuwa kila ukikasirika, unapunguza muda
wa kuishi hapa duniani. Halafu unagombesha watu ambao hawastahili.’ Nikamaliza
nikabaki nikimwangalia.” “Jamani mama wewe!” “Ujue yule Mzee alikaa kama dakika
tano ananiangalia hanimalizi. Nikamsogezea kile kikaratasi.” Nanaa alikuwa
haamini.
“Akasemaje?” “Akaniuliza jina langu nani.
Nikamwambia Oliva. Akaniuliza jina kamili. Nikamwambia bado ndio najaribu
kulitengeneza. Yule baba alibaki hanielewi. Akaniuliza, ‘Unatengeneza jina
lako?’ Nikamwambia, ‘ndiyo’. Akabaki ananiangalia. Akaniuliza shule ulikuwa
ukitumia jina la nani? Nikajibu kwa kifupi tu ‘la Padri’. Yule baba alizidi
kutonielewa. ‘Una miaka mingapi?’ Akauliza tena. Nikamwambia andika mwaka
wowote lakini uishie na 1, au 3, au 5 au 7. Akaniuliza kwa nini hizo namba.
Nikamjibu huwa sio rahisi kugawanyika. Ni ngumu, na hazigawanyiki kwa mbili.
Yule Mzee akabaki ananitizama.” “Jamani wewe mama ni mkorofi!” “Sana.
Sijajipatia mwenzangu. Hivi nashukuru nilikutana na Yesu. Lasivyo!” Wakacheka.
“Akaniuliza tena. ‘Kwani una miaka mingapi?’ Nikaanza
kufikiria. Akaniuliza kwa hiyo hata umri wako hujui? Nikamwambia kuna umri
walinipa, lakini siamini. Nahisi walinipunja. Akaniuliza unataka uwe na miaka
mingapi? Haraka sana nikamjibu 19. Akacheka na kutingisha kichwa. Akauliza
tena, ‘unasoma Oliva?’ Halafu akajijibu yeye nwenyewe baada ya mimi kubaki nikimwangalia.
Akasema ‘ndio maana unatafuta kazi kwa kuwa husomi’. Nikamjibu, ‘Exacalty!’
Akazidi kutingisha kichwa. Akaniambia ‘wewe ni mtoto mdogo sana, kwa nini haupo
shuleni unatafuta kazi?’ Nikamwambia sipendi kukaa darasani. Naona nitafanya
vizuri kazini kuliko darasani. Yaani nikifanya kitu kinachoniingizia pesa ndio
naweza kufanya vizuri kuliko kukaa darasani. Akabaki akinitizama kwa muda.
Akauliza tena, ‘wazazi wako wako wapi?’ Nikamjibu kwa kifupi tu ‘sijui.’
Akabaki ananiangalia.” “Sasa ulikuwa huogopi?” “Mimi sio muoga Nanaa. Labda mtu
aumwe, lakini sio vinginevyo.” Nanaa alitingisha kichwa.
“Kufupisha stori, yule baba akaniajiri, Chalii
akanipangishia chumba. Nikaanza maisha. Eti akaja Chalii anadai haki yake. Acha
nimbadilikie kama simjui. Hapo nilishamzungusha mpaka basi. Ashanitambulisha
kwa mkewe Magesa ambaye ni dada yake sasa. Anajisifia kwa watu eti mimi mkewe.
Nikawa namsikiliza tu. Pale kazini nikawa nachapa kazi mpaka Mzee Magesa mwenyewe
hakuwa akiamini kama sijasoma. Kazi zikawa zinaenda, ukali akapunguza. Lakini
hapo nikawa namchunguza. Nikamjua kila kitu juu ya maisha yake.” Mama G
akaendelea.
“Wakati akili zangu zimezama kwa Magesa na kazi
zake, Chalii naye akawa ananisumbua. Nikampiga marufuku aache kunifuatilia. Eti
akataka kujiua kwa ajili yangu. Eti nimemsaliti. Usiku huo nyumbani kwa dada
yake, yaani nyumbani kwa Mzee Magesa eti akajidai amekunywa sumu juu yangu.
Akaacha na ujumbe. Akapelekwa hospitalini wakagundua sijui amekunywa dawa mbili,
sijui tatu! Dada yake akanifuata asubuhi pale kazini mbele ya mumewe eti kwa
nini nimemsaliti mdogo wake! Nikamwambia, ‘Kwanza, usiniletee habari za mtaani
kazini kwangu. Pili sikujui na wewe hunijui. Kama ungenijua hata kidogo, ungetambua
kuwa mimi sio mwanamke ninayeweza kuwa na mtu kama mdogo wako.’ Akauliza kwa
nini. Nikamwambia ‘He is weak.’ Ujue Mzee Magesa hakuamini. Akaondoka yule baba, mkewe akamfuata nyuma.
Nikaendelea kufanya kazi zangu.” “Mama!” Mama G, akacheka.
“Sikuishia hapo. Yule mama alivyoondoka tu
nikamfuata mumewe. Nikamuuliza mbona wewe hujaniuliza kama mkeo? Mzee Magesa
aliishia kuniita jina langu, ‘Oliva!’ Nikamwambia wewe niulize tu. Akanitizama,
kisha akaniuliza, ‘Kwa nini umemsaliti Chalii.’ Nikamsimulia mwanzo wetu mpaka
mwisho na nikamwambia nilikuwa namdanganya ili anipe kazi. Kwa hiyo sijamsaliti
ila nimemdanganya.’ Yule Mzee alitingisha kichwa. Akauliza tena, ‘Sasa kwa nini
unakataa hata wanaume wenye uwezo? Ujue Chalii ni mfanyabiashara mkubwa tu.
Anamaduka pale Kibaha kituo cha mabasi.’ Nikamw..” “Kwani kuna wengine walikuwa
wakikutongoza?” “Nilikuwa gumzo. Vijana kwa wazee walikuwa wananifuata pale
kazini. Wapi useme Oliva usisimuliwe umbo langu! Ilikuwa si mchezo. Oliva
nilikuwa natingisha kweli kweli.” Nanaa akacheka sana.
“Sasa ukamjibu nini wakati ulimfuata mwenyewe?”
“Nikafungua kijitabu changu, nikaanza kumsomea. Nikamwambia, ‘Nina mpenda
mwanaume mmoja tu. Lakini, 1. Ni mume wa mtu. 2. Ana watoto wanao lingana na
mimi. 3. Ni mcha Mungu sana na ni Mzee wakanisa. Nimeambiwa kuwa hajawahi
kumsaliti mkewe. Japo mkewe sio mtu wa mapenzi, anajua kusaka pesa tu. 4. Hata
yeye mwenyewe sio mtu wa mambo ya mapenzi, nasikia anapenda sana pesa. 5. Kwa
asili hana tamaa ya wanawake. Hata wanawake wakimtongoza, huwa hakubali.’ Yule
baba alibaki akinitizama. Nikamwambia, ‘huo ndio uchunguzi nilioufanya juu ya
huyo mwanaume ninayempenda mimi na ndiye atakuwa baba wa watoto wangu. Wawili.’
Yule baba alinitizama, akanyanyuka na kuondoka. Hakurudi siku ile. Siku inayofuata,
mkewe akaja na kunifukuza kazi.” “Mama!” Nanaa akashangaa.
“Kabisa! Nikamwambia nipe pesa yangu niondoke.
Sikutaka hata kujua sababu. Ile nimetoka tu, nikasimamishwa na baba mmoja,
alikuwa mteja wa hapo. Na yeye anachukua maziwa hapo kwa Magesa kwa bei ya
jumla anayauza kwa kuyasambaza maeneo ya Kibamba mpaka Ubungo. Alikuwa na
magari yakusambazia. Basi akaniambia nipande kwenye gari yake. Nikapanda bila
woga. Akanitongoza. Nikamwambia simpendi lakini nataka anisaidie. Anipe pesa
nianze biashara. Kama utani, yule baba akanipa pesa, akanishusha kwangu.” Mama
G akaendelea.
“Sikuamini. Alinipa pesa yote bila shida.
Nikatafuta sehemu, nikafungua duka la kuuza ‘yogurt.’ Nikawa nanunua maziwa kwa
Magesa, nakuja kutengeneza ‘yogurt’, kisha nauza. Nikaajiri vijana wawili.
Ndani ya miezi 6, kitu kimechanganya. Nikaongeza vijana wengine wawili ambao
wakawa wananiuzia kwenye kituo cha mabasi pale standi. Pesa ikaanza kuwa
nyingi. Nikabuni njia nyingine ya kufunga hizo yogurt kwenye vilailoni kama ice
cream. Nikawa nauza kweli. Nikahama Kibaha sababu ya usumbufu wa wanaume,
nikahamia Kibamba. Nikakodi kinyumba kidogo. Nikaanza maisha. Hapo hata
sijatimiza miaka 20.” “Mama una akili!” “Sana.” Nanaa akacheka kwa sauti.
“Nakumbuka ni kama mwaka ukawa umepita, tokea
niache kazi kwa Magesa na mkewe. Siku hiyo ya jumamosi sikwenda kazini, nilikuwa
sijisikii vizuri. Niliamka sijisikii vizuri, nikarudi kulala ili kuona kama
nitajisikia vizuri hapo nikiamka tena ili niende kazini. Nikaamka mchana mchovu
zaidi na homa ipo juu. Nikawapigia simu wafanyakazi wangu kuwa sitakwenda hata
jioni kwa kuwa nina homa. Ukifika muda wakufunga, wafunge tu mmoja aniletee
funguo na mahesabu. Ilikuwa mchana. Nikarudi kulala tena.”
“Ilipofika jioni nikaamshwa na mtu anagonga.
Nikajua nikijana wa dukani analeta funguo. Nikaamka kichwa kinauma kweli,
nikafungua mlango. Ana kwa ana na Magesa. Nilisimama pale mlangoni
nikimwangalia. Akaniambia, ‘naomba kuingia ndani’. Nikamwambia, ‘nimebadili
mawazo, naomba uondoke’. Akaniambia ‘acha ukorofi Oli, nipishe mlangoni
niingie.’ Nikajikuta naanza kulia. Sikuwa nimelia sijui zaidi ya miaka hata
mitano. Nikalia wee, nikampisha. Akanishika mkono akanivutia ndani. ‘Una homa
kali Oli. Umekunywa dawa?’ Nikanyamaza. ‘Oli?’ Nikanyamza.” “Alikuwa anakuita
Oli?” Nanaa akauliza.
Mama G akacheka kama anayekumbuka mbali. “Yeye
ndio alikuwa akiniita Oli. Na ungependa kumsikia akiniita.” Nanaa akazidi
kucheka. “Basi, nikaendelea kulia nikamwambia, ‘ulinifukuza
kazi. Umeniacha peke yangu kwa mwaka mzima! Sikutaki tena. Naomba uondoke.’
Akaniambia, ‘Sijawahi kukuacha hata siku moja. Njovu ni kijana wangu.
Umemuajiri lakini ni kijana wangu na ninakufuatilia kila kitu. Leo ameniambia
unaumwa ndio maana nimekuja kwa haraka. Leo sio siku niliyotaka kuja.’
Akajaribu kunituliza. ‘Sasa lini ulitaka kuja?’ Nikamuuliza. ‘Hivi unajua nina
mke na watoto, Oli? Nina maisha niliyojenga kwa muda mrefu sana. Sidhani kama
ulitegemea ni kurupuke tu, na wewe bado mdogo na ni binti mzuri unayetakwa na
kila mtu! Ilibidi kukuchunguza Oli.’ ‘Kwa hiyo umeonaje sasa?’ Nikamuuliza. ‘Si
ndio maana nipo hapa?’ Akanijibu.” Mama G, akatulia.
‘Umekunywa dawa?’ Akaniuliza tena. Nikamjibu
sijanywa dawa na wala sijala. Nikamwambia huwa siumwi. Kwa ufupi ndio ilikuwa
mara yangu ya kwanza kuugua. Nikashangaa akanichukua akanipeleka hospitalini.
Nikakutwa na UTI. Nikapewa dawa, akanirudisha nyumbani. Akahakikisha nimekula
na kunywa dawa, ndipo akaondoka. Hakuna usiku niliolala vizuri kama huo.
Nilifurahi sana. Kesho yake asubuhi siku ya jumapili alipotoka kanisani akaja
tena. Akaniletea chakula. Nakumbuka alikaa na mimi mpaka usiku ndipo akaondoka.
Jumatatu nilirudi kazini nikiwa na nafuu, akaja, akaniletea chakula na
kuniambia nijiandae, siku ya jumamosi tunasafiri mimi na yeye tu. Akaniambia
nimuachie Njovu maelekezo mazuri yakutosha kwa kipindi ambacho sitakuwepo.
Basi.” Uso wa mama G ukajawa furaha mpaka Nanaa akamuona nakucheka.
“Basi, siku ya jumamosi asubuhi akanipitia
nyumbani mpaka uwanja wa ndege. Ndio ilikuwa mara yangu ya kwanza kupanda
ndege. Tukaenda Arusha. Tulikaa huko hotelini kwa juma zima. Hakuna kutoka, ni
mimi na yeye tu. Sijawahi kupata wakati mzuri hivyo maishani. Japo aliniudhi,
lakini nilifurahia sana.” Nanaa akacheka.
“Sasa alikuudhi nini tena?” “Yule baba alijua
kabisa mimi ni jeuri. Mkorofi wa asili, lakini..” Mama G akaanza kucheka.
“Nini?” “Kwanza tulipoingia tu chumbani ujanja wote ukaniishia. Sijui mapenzi
wala sijawahi kufanya mapenzi. Sasa sijui natakiwa nifanye nini! Nikaanza
kuhangaika sasa. Mara nitoe nguo zote kwenye begi nianze kupanga upya. Kwa mara
ya kwanza nikaingiwa hofu. Natetemeka. Mara nikunje mataulo ya bafuni, mara
niyatoe. Sasa yule baba kumbe amekaa tu ananiangalia. Akajua. Lakini akataka
kunikebehi, akaacha nihangaike mpaka nisalimu amri. Nikawa nimeishiwa sasa vitu
vya kufanya, na yeye akajidai anaandika vitu vyake kama hanioni. Nikamuuliza,…”
Mama G akaanza kucheka.
“Nini?” “Sasa si sijui! Kusema naona aibu, sababu
yakujidai mjuaji eti nikamuuliza, ‘Wewe unapenda kuvuliwa nguo au unavua
mwenyewe?’ Akabaki akiniangalia. Nikarudia, lakini safari hii natetemeka mpaka
naonyesha. Nikamuuliza, ‘Wewe unapenda kumvua mwanamke nguo au unataka ajivue
mwenyewe?’ Yule mzee akaanza kunicheka. Akaniambia, ‘Sikujua kama kuna
mazingira huwa yanakufanya ukawa mtoto mzuri hivyo! Njoo kwanza hapa.’ Nikabaki
nimesimama. ‘Njoo Oli. Njoo tuzungumze kwanza.’ Nikamuuliza, ‘Kwani
nimeharakisha sana?’ Akazidi kunicheka. Nikamwambia, ‘usinicheke bwana! Nielekeze.’
Yule Mzee alicheka mpaka basi.” Hata Nanaa na yeye alikuwa akicheka.
“Basi, akaniuliza, ‘Ujanja wote huo hujui kabisa
maswala ya mapenzi?’ ‘Sasa ningelala na nani?’ Nikamjibu kwa kumuuliza swali.
Hapo nimepooza kama sio mimi! ‘Sasa ulipokubali kuja huku, ulikuwa na picha
gani?’ Akauliza. ‘Nilijua nikifika tu huku ingekuwa rahisi, ningejifanya najua
halafu tungelala, lakini kumbe ni ngumu hivi!’ Alizidi kucheka. ‘Usicheke
bwana. Mwenzio sijawahi kuvua nguo mbele ya mtu. Hata wasichana wenzangu huwa
sikai uchi mbele yao.’ Nikajitetea. ‘Kweli Oli?’ Akauliza. Na nikweli. Sikuwahi
kujiweka uchi mbele ya mtu yeyote. Yaani wale masista walikuwa wakiniambia tokea
napata akili zangu, nilikuwa naogopa hata paja langu lisikae nje. Wakati wote
nilitaka nguo ndefu.” “Na ulivyo na mguu mzuri mama!?” Nanaa akashangaa.
“Wakati
nipo msichana kila mtu alikuwa akiniambia hivyo! Lakini wapi. Nguo hajafika
chini, siivai. Yaani wanaume walikuwa wanahangaika, moyoni nilikuwa najiambia
nia yao ni kunivua tu nguo wanichungulie, wajue ndani nikoje. Nikajiambia si
thubutu. Tena nikikuona unahangaika sana na mimi ndio nakuchukia kabisa. Nakuona
wewe dhaifu. Ndio maana naona nilitulia sana kwenye swala la wanaume.” Nanaa
alibaki akimwangalia.
“Basi, yule baba akaja akanichukua pale
nilipokaa. Nafikiri akanihurumia, akajisikia vibaya. Akaniambia yeye ni mkubwa
sana kwangu, sina sababu yakufanya naye mapenzi. Naweza kuendelea kujitunza tu
mpaka nitakapo olewa. Nililia. Nikajua ananikataa kwa kuwa sijui mapenzi.
Nikamwambia asinikatie tamaa nitajifunza. Akaniambia anafanya vile kwa ajili
yangu sio yeye. Hapo nilikuwa mdogo. Kumbuka niliishia kidato cha pili
nikatoroka. Nikafanya kazi kwake muda mfupi, mkewe akanifukuza kazi. Ndio
nikaanza biashara zangu. Na walinianzisha shule mapema kwa sababu ya utundu na
ukorofi. Masista waliona ni heri waniingize darasani kuliko kuniacha nje.
Nilikuwa sisikii kama sina masikio! Kila nilichokuwa nikiambiwa nisifanye ndio
nilikuwa nafanya. Jeuri, kweli kweli!” “Sasa ulirudi tena?” Nanaa akauliza.
“Sikuwahi kurudi tena.” “Sasa si watakuwa
walikutafuta?” Kidogo akamuona Mama G, amepooza. “Sidhani. Kwa kuwa yule padre
aliyetuokota mimi na kaka yangu au pacha wangu akanipa jina la Oliva, alikuwa
ni mtu wa kutoka Italy. Alianza kuugua akataka arudi nchini kwao. Lakini
akasema hawezi kuondoka bila mimi. Alikuwa akinipenda sana. Nakumbuka tokea
nakua alikuwa akinifundisha kusali na kuimba. Sasa katika harakati
yakukamilisha utaratibu wakunichukua kutoka hapa nchini kunipeleka nchini kwao
kama mtoto wake, akaja kufa gafla kabla hata mambo ya safari yangu
hayajakamilika. Jamani walinitesa wale watu. Walinitesa sana. Nikawa
sisikilizwi tena. Hakuna mtu ananiangalia. Ndipo nikajua ule uangalizi
niliokuwa nikipata wakati ule ni kwa sababu ya yule padre. Nilipoona wanazidi
kunionea na mimi siwezi kujishusha ndipo nikaondoka.”
“Nafikiri pia walichangia kuondoka kwangu, au ni
mimi tu mwenyewe na jeuri yangu! Sijui. Lakini sikurudi na wala sikutaka
kuwatafuta tena mpaka leo. Yule padre akanipa jina lake. Alikuwa akiitwa padre
Angelo Romano. Akaandika vyeti vyangu vyote vya kuzaliwa, Oliva Angelo Romano.
Niliumia sana alipokufa yule padre. Sana. Lakini nilishindwa hata kulia.”
“Kwani wewe mama si mlizi?” “Hata iweje. Aliyekuwa akiweza kuniliza ni baba
yake Geb tu. Basi.” “Labda kwa kuwa ulimpenda sana.” “Sana. Mzee nilimpenda
yule! Karibia kurukwa na akili.” Nanaa akacheka sana mpaka akajisahau.
“Kweli. Na sikuja kuwahi kupenda tena. Na
sikuwahi kuwa na mahusiano mengine ya mapenzi. Alikuwa wa kwanza na nikajiambia
ndio wa mwisho.” “Kwa nini mama!?” Nanaa akauliza kwa mshangao. “Nilijua
wengine watanichafua tu. Sikutaka tena. Yule mzee alinipenda Nanaa! Sijawahi
pendwa hivyo. Alijidhalilisha sana kwa ajili yangu. Kwanza alikuwa akifahamika
yale maeneo ya Kibaha, huko Picha ya Ndege mpaka kuja huku Kibamba. Alifahamika
kama chumvi. Wapi upite usisikie Magesa!”
“Alikuwa anapesa mnooo. Hilo shamba lake la
mifugo, lilikuwa gumzo. Lilikuwa kubwa sana na akafanikiwa kufanya ufugaji ule
wa kisasa. Walikuja watu kutoka Denmark, wakawa wanatafuta sehemu nzuri
yakufanya majaribio ya uwekezaji wakisasa kwa kutumia mashine. Serikali ikamteua
yeye kupokea hao wazungu. Kwa kuwa alikuwa na eneo kubwa sana na tayari alikuwa
na ng’ombe wengi wakisasa. Wale wazungu wakamuinua zaidi. Kwa hiyo alikuwa na
mashine za kumsaidia mambo mengi sana kwa ufugaji. Alikuwa akitangazwa sana
kwenye vyombo vya habari kwa ufugaji wa kisasa. Sasa wakakutana na mama wa Kimachame
anayejua pesa, basi usiseme. Enzi hizo kuendesha Cruzer ilikuwa sio kitu
kidogo. Sasa yeye alikuwa nalo la silver. Akipita mtajua tu ni yeye Magesa
amepita. Jeuri kama hivyo unavyomuona Geb. Mkali kama pili pili.” “Sasa
ikawaje?” “Mmbea wewe!” Nana akacheka.
“Bwana nisimulie mama!” “Basi, akanikatalia.
Akaniambia mimi bado mdogo sana. Hawezi kuwa ndio mwanaume wangu wa kwanza.
Nikaanza kuvua nguo zangu zote. Nikamwambia basi ajue yeye ndiye mwanadamu wa
kwanza kuniona nipo uchi. Nikamwambia tokea napata akili zangu, nilikuwa naoga
mwenyewe ili tu mtu mwingine asinione. Nikamwambia hata kama hataki mahusiano
na mimi, basi anisaidie yeye ndio awe mwanaume wangu wa kwanza. Alisadiki kwa
sababu alishanijaribu sana.” “Ki vipi?” Nanaa akauliza.
“Kumbe tokea siku ile ofisini nilipomwambia juu
ya mwanaume ninayemtaka mimi nikimaanisha yeye, akaondoka, kumbe akaanza
kunijaribu. Mkewe ndiye wakati wote alitaka nifukuzwe kazi.” “Kwa nini?” Nanaa
aliuliza. “Unakumbuka Chalii alitaka kujiua kwa ajili yangu halafu yule mama
akanifuata, nikamjibu mbovu?” “Oooh!” Nanaa akakumbuka nakuanza kucheka. “Basi
ndio akanichukia. Lakini yule baba, mumewe, Mzee Magesa alikuwa hataki
kuniachisha kazi kwa kuwa nilikuwa nikifanya kazi sana. Kwa asili mimi sio
mvivu wala sio mwizi. Alishanitega mpaka akaridhika kuwa mimi sio mwizi.
Wafanyakazi wake wengine walikuwa wakimwibia sana. Wanadanganya lita za maziwa
wanazopokea kutoka shamba, wanaandika kidogo, halafu zile zinazozidi wanauza.
Lakini mimi sikuwa nafanya hivyo. Akajua. Nilipokuwa mimi, aliona mahesabu yake
yapo sawa.”
“Haya, akawa akinitumia vijana kuja kunitongoza.
Au anawashawishi marafiki zake wanitongoze. Nikawa nawalia pesa zao tu lakini
siwapi mapenzi. Wakaanza kujua mimi ni tapeli. Habari zikamfikia Magesa. Kuwa
Oliva anatapeli wanaume lakini hataki kufanya nao mapenzi. Ndio kipindi hicho
nilipokuwa naye hapo hotelini, akaniambia ni lazima tukirudi niwalipe pesa zao.
Nikakataa. Akaniambia, ‘Sio ombi Oli, nilazima. Utamtafuta mmoja mmoja, utaomba
msamaha, na kuwarudishia pesa zao.’ Nilihisi kuchanganyikiwa.”
“Sijui
watu wanaombaje msamaha! Nikamwambia. Akasema kama nampenda kama ninavyosema,
nitafanya hivyo. Na akaniambia ni lazima kuacha hiyo tabia. Hataki kusikia tena
natapeli watu.” Nanaa akacheka sana.
“Mama wewe! Ulikuwa unawatapeli?” “Sana. Ukija
kichwa kichwa, nakulia pesa yako, halafu hupati penzi. Sasa ole wako uniguse.
Utajuta.” Nanaa akabaki anamwangalia. “Unashangaa nini sasa?” “Nisimulie
bwana.” “Hivi wewe mtoto ujue mimi ni mama yake Geb?” Nanaa akajificha uso.
“Yaani unataka kujua habari za mapenzi za baba na mama yake Geb! Shika adabu
yako.” Nanaa akacheka sana kwa aibu. “Lakini imenoga mama. Si unimalizie tu?
Usiniche katikati mama!” “Sitaki. Ila ujue ndio muda huo nikawa muwazi kwake.
Nikamuelezea historia yangu ya maisha. Akaniambia hata yeye ananipenda lakini
kuna garama kubwa sana ya kulipa ili tuweze kuwa naye.” “Garama gani tena?”
Nanaa akauliza.
“Kwanza alijua itagundulika. Watu watataka kujua umri
wangu. Tayari nilikuwa ni mtoto sana kwake. Nafikiri nilikuwa nalingana na
mtoto wake wa pili, wakike. Alikuwa na watoto wakike wawili tu. Kingine alijua
ndoa yake inaweza kuvunjika, lawama itakuwa kubwa kwenye jamii. Alijua jina
lake litaharibika sana. Kwa kujulikana anamahusiano na mtoto anayeweza kumzaa.
Akaniambia ndio mambo yaliyomfanya akae mbali na mimi kwa muda wote huo,
kuhesabu hasara, na kujua kama ninastahili kulipiwa garama yote hiyo! Kwa
kifupi ni kama aliamua kutoa maisha yake kafara, kwa ajili yangu.” “Masikini!”
Nanaa akamuhurumia.
“Akanielezea umbali aliotoka na yule mwanamke.
Kwa nini alimuoa. Akakiri ni kweli haikuwa mapenzi. Ila akasema mkewe ni
mwaminifu sana, na ni mchapakazi. Ndio kitu kikubwa alichompendea mara tu
alipofika hapo Kibaha na kukutana naye. Akasema kwa kuwa alikuwa na uchu na
pesa, akajua akiwa na yule mwanamke watafika mbali. Akasema hakukuwa na mapenzi
makubwa kati yao, lakini haikuwahi kuwa shida kwake, kwa kuwa na yeye hakuwa
mtu wa wanawake. Shida yake ilikuwa pesa tu.”
“Alisema ndoa yake haikuwa na matatizo makubwa
kwa kuwa hakuna aliyetarajia cha ziada kutoka kwa mwenzake, zaidi ya pesa.
‘Sikuwahi kulalamika juu ya kitu fulani kwa mke wangu na yeye hivyo hivyo.
Ilimradi pesa inaingia. Mazungumzo yetu ni juu ya biashara zetu basi.
Mfanyakazi huyu anaendeleaje. Biashara hii inaingiza pesa kiasi hiki, na kwa
nini? Ni nini tufanye ili tuongeze faida, na nini tuwekee mkazo. Basi. Hayo
ndio mazungumzo yetu kwa jumla. Na kwa kuwa wote tunakuwa tunachoka na kazi’ .”
Mzee Magesa aliendelea.
“Hata ufanywaji mapenzi sio kipaumbele kwetu.
Mara chache sana. Tena ikibidi. Mke wangu sio mtu wakupenda mapenzi. Ni haki
yake, kwa kuwa anafanya kazi sana. Akijitupa kitandani ni saa 5 au 6 usiku, na
yupo hoi kwa kuwa anaamka mara nyingi saa 11 asubuhi kuwahi kwenye miradi.
Hatuna utaratibu wa likizo. Kwa kuwa hatuna mtu tuna mwamini na miradi yetu.
Labda ndio maana tumefanikiwa sana katika hilo eneo la pesa lakini si kindoa.
Ila narudia tena, hatujawahi kuona tatizo, kwa kuwa hakuna aliyetarajia kitu
cha ziada kwa mwenzake.’ ‘Kwa nini hukuwahi kutafuta mwanamke wa nje? Nimesikia
wanawake wengi wakisema washakujaribu sana, lakini umekuwa ukikataa. Mpaka
wasichana wadogo na wazuri.’ Nikamuuliza.”
“Alisema, ‘Najua watu wengi wananipendea pesa.
Kila mtu anajua akiwa na mimi ataneemeka. Kitu ambacho nakipata kwa mke wangu.
Hata yeye akiniona, anaona kichwa kitakachofikiria haraka na kumpa ufumbuzi wa
matatizo yake ya kipesa. Hajui kufanya kitu bila kuniuliza. Kwa kuwa Mungu
alinijalia akili ya haraka ya kufikiria, na hekima katika maamuzi. Ndio maana
nategemewa sana katika jumuiya. Iwe kanisani, au kwenye jamii, watu
wananitegemea sana.’ Nilimuhurumia. Nikasimama, nikaanza kuvaa nguo zangu.
Akaniuliza kwa nini nafanya hivyo? Nikamwambia sitaki kumuharibia maisha.
Nimeelewa kwa nini hataki kufanya mapenzi na mimi.’ Mama G aliinama kidogo,
akafikiria.
“Nakumbuka alisimama, akanikumbatia na kuniweka
kitandani. Akaniambia, ‘Oli! Wewe ni mtu wa thamani sana kwangu. Wakati wote
umeonyesha kunijali mimi kuliko pesa yangu.’ Yeye ndio mtu pekee aliyekuwa
akiniita Oli. Kila alipokuwa akija kazini, nilihakikisha anakunywa chai.”
“Mama! Ulikuwa ukimtengenezea?” “Nilijua hali vizuri Nanaa. Na hasira zile
zilikuwa ni njaa. Kwa hiyo nikawa nampikia vitafunio nyumbani, na kaanga mayai
au nyama. Naenda navyo ofisini. Akija tu, nampashia maziwa moto, namuwekea
Cocoa, namtayarishia namuwekea mezani kwake, ofisini kwake.” “Sasa wenzio
walikuwa hawakusemi?” “Mimi huwa sijali Nanaa. Nilimpenda yule baba, kama
mwehu. Nilikuwa nikimuona amekasirika, nilikuwa naumia sana. Nilikuwa
nahakikisha anakunywa maji kila wakati.” “Sasa wangemwambia mkewe?” “Mimi
sinaga hayo maswali na majibu ya kesho. Ninaloliweza kulifanya leo, nafanya.
Kesho napambana nayo ikifika.” “Nimekuheshimu mama.” Mama G akacheka kidogo.
“Basi. Akaniambia mimi ndio nilikuwa mtu wa
kwanza kumjali na kumthamini kama yeye. Lakini akaniambia umri wake umekwenda.
Akaniambia ananihurumia kunianzishia jambo halafu akaniacha nateseka peke
yangu. Akili ikanijia kwa haraka. Nikamwambia mimi sitegemei chochote kutoka
kwake isipokuwa mapenzi. Nikamwambia naweza kujitunza. Na hata kama nikipata
watoto, naweza kulea wanangu bila yeye. Nikamwambia ninachotaka maishani ni
yeye tu kuwa mpenzi wangu. Yule baba hakuwa akiamini Nanaa. Alibaki akiniangalia.
Nilikuwa mtoto, halafu navutia kwa kila kitu. Akabaki ananiuliza, ‘Kwa nini
mimi!?’ ‘Sijui. Lakini najua nakupenda wewe. Na ninataka wewe ndio uwe mwanaume
wangu. Nitaacha kukusumbua tu, endapo utaniambia nakuharibia maisha yako.
Nitaondoka na sitakusumbua tena.’ Nikamwambia hivyo. Alikuwa akiniangalia na
macho yake yale, nazidi kuwa mdogo. Ujeuri wote unaniisha.” “Kama Geb.
Anamakusudi kweli. Anayajulia macho yake. Basi akikuangalia hata kama unampango
wakusema hapana, unajikuta unasema ndiyo. Halafu unataka akubusu
tu.” Mama G akacheka mpaka machozi.
“Kweli
mama. Mimi hata sikuwa na mpango wa mwanaume mpaka nimalize chuo. Kwanza
nilivyomwambia Zinda, sikuwa nimemdanganya. Sikuwa nataka wanaume kabisa.
Nilishakinahiwa. Lakini Geb akitaka jambo lake, hutoki mama.” “Basi na baba
yake yupo hivyo hivyo. Na hana papara ya mambo. Mkikaa hapo kitandani, hutataka
mtoke.” Nanaa alificha uso. Akawa anacheka. Alimkumbuka Geb. Hakuwahi kupata
mwanaume mjuzi wa mapenzi vile. Geb aliweka historia mpya na nzuri kwenye
maisha yake.
“Nimalize basi mama.” “Basi. Ndio tukakubaliana.
Akaniomba tusubiri kwanza swala la watoto, ili na yeye apumzike kidogo.
Aliniambia hajawahi kuishi hayo maisha ya mapenzi. Anataka ayafurahie kidogo
kabla watoto hawajaja. Ukweli yeye hakuwa akitaka watoto kabisa. Mimi ndiye
nilimuomba. Mapenzi yakaanza. Nikawa kile anachokitaka kwa kuwa yeye ndio
alikuwa mwalimu wangu. Akaja kuwa kama mjinga na yeye. Kutwa yupo mlangoni
kwangu. Asubuhi na mapema, anakuja kwangu, Kibamba.”
“Maneno yakaanza kuenea kwa kuwa gari yake ikawa
inaonekana mitaa ya Kibamba, nyumbani kwangu. Wakati mwingine mchana ananifuata
kazini, ananirudisha nyumbani. Ananiomba niwe naye hata kwa lisaa tu. Mchana,
kweupe! Asubuhi anatoka kwake, anakuja kwangu. Wakati mwingine nakuwa hata
sijaamka, nashitukia anapanda kitandani kwangu. Maana alichongesha funguo za
kwangu. Akawa anaingia na kutoka vile atakavyo. Maneno yalivyozidi,
akanihamishia mjini. Akanichukulia nyumba mitaa ya Kinondoni. Akanunua kila
kitu. Sikufurahia sana, kwa kuwa kulikuwa mbali na kwake.” “Yeye alikuwa
akiishi wapi?” Nanaa akauliza.
“Alijenga bonge ya jumba huko Picha ya ndege,
karibu na shamba lake. Kibaha ndio kulikuwa na kiwanda chake cha maziwa.
Nikalalamika. Lakini akasema ni kwa usalama wangu. Lakini atajitahidi kila siku
lazima tuwe tunaonana.” “Biashara yako sasa?” “Aliifunga. Maneno yalikuwa mengi
sana. Na yeye alikuwa hawezi kujizuia. Nakwambia mchana kweupe, anaonekana
amekuja kunifuata kazini, ananichukua kwenye gari yake, ananirudisha nyumbani
kwangu. Tutakaa hapo kitandani mpaka jioni. Ananirudisha tena kazini kwangu,
yeye anaendelea na shuguli zake.” Nanaa akaanza kucheka.
“Watu wakawa wanatufuatilia. Wakawa wananisema
kuwa ninakataa vijana wenzangu, halafu nimemkubali yeye Mzee sababu ya pesa.
Chalii ndio alizidisha fujo. Analalamika kuwa shemeji yake kampora mwanamke
wake. Ndio sasa Magesa akanilazimisha kuhama. Akanifungulia sehemu nyingine ya
biashara ileile ya Yogurt, maeneo ya posta. Nilikuwa natengeneza pesa, kama
nini sijui! Sasa hapo sina mtoto, sina ndugu. Pesa yangu ni yangu. Na Magesa
naye akawa ananipa pesa.”
“Kwanza
tuliporudi kutoka mapumzikoni Arusha, baada ya miezi michache tu, akanizawadia
gari akasema ni zawadi ya kujitunza. Ilikuwa Toyota Corola. Enzi hizo waendesha
magari wachache sana, tena wanahesabika. Sasa uje kukuta ni mwanamke! Ndio
kabisaa. Nilikuwa Oliva kweli kweli. Nikipita mahali utajua nimepita. Sisikii
la mtu, ni Magesa tu.” Nana alikuwa akicheka kama sio yeye aliyepokonywa mtoto.
“Nakumbuka siku hiyo akaja nyumbani amepoa. Kila nikimuuliza kulikoni hasemi, anatoa
tabasamu huku ananiambia nisiwe na wasiwasi. Nikamwambia yeye ananijua huwa
sina wasiwasi isipokuwa yeye akiwa kwenye matatizo. Nikambembeleza siku hiyo,
ndio akaniambia yupo kwenye matatizo na watoto wake. Wamejua kama anamwanamke
mwingine. Tena mtoto umri wao. Wanataka kujua ukweli. Kwa kuwa mama yao hana
raha. Nikamuuliza aliwajibu nini? Akasema alishindwa kukubali au kukataa.
Nikamwambia mimi sitakuwa tayari kumuona yupo kwenye hali ile. Nipo tayari
kumuacha aendelee na maisha yake. Au hata akitaka tuachane kwa muda, mpaka
aweke mambo yake sawa. Nikamuahidi nitamsubiri tu.” “Maskini mama! Kumbe
ulimpenda sana!” Nanaa alimwingilia.
“Yaani Nanaa, nilikuwa nahisi kurukwa na akili
nikimuona yule Mzee hana raha. Basi. Nikamwambia namruhusu aondoke. Sitamtafuta
wala kumsumbua mpaka atakapoweka amani nyumbani kwake. Nikamwambia lakini kabla
ya kuondoka lazima tuagane. Maana alikuja kama mgonjwa. Nikambembeleza mapenzi,
akakubali tukiambiana ndio tunaagana kwa muda. Tukajisahau siku ile, tukashitukia
pamepambazuka. Akatoka kama amechanganyikiwa. Sikumuona tena mpaka baada ya
miezi kama 5 hivi.”
~~~~~~~~~~~~~~
Nini
Kiliendelea? Usikose Kufuatilia.
0 Comments:
Post a Comment