Akaamua kwenda mwenyewe hospitalini. Alichukua
taksii iliyompeleka mpaka hospitalini. Alikutana na muuguzi mcheshi sana.
Alimpokea begi la mtoto wake, akampa kitanda. Alipopimwa, akaambiwa njia
imeanza kufunguka. “Lazima huyu mtoto azaliwe leo.” Alimwambia yule muuguzi
aliyemkuta pale, akacheka. “Kwa nini?” “Nina mtihani siku ya jumatano.” “Si
uarishe?” “Hapana. Hii shule haijawahi kusubiri, na haitakaa ikasubiri. Lazima
iishe. Nilijua huyu mtoto ndie angesubiri mpaka nimalize, naona anataka tuonane
mapema. Amechoka kunisikiliza tu. Anataka kuiona sura ya mama yake. Sasa leo
lazima utoke, tuonane.” Nanaa aliongea huku akijipapasa tumbo. Akashauriwa
atoke nje ajaribu kutembea tembea ili kusaidia kufunguka kwa njia zaidi. Nanaa
akatoka nakuanza kutembea. Alizunguka mpaka alipohisi maumivu makali sana,
akarudi tena kuangaliwa njia. Nesi alipoona imefunguka vizuri, akamuingiza
chumba cha kujifungulia.
~~~~~~~~~~~~~~
Alisukuma mara kadhaa tena kwa
ujasiri bila hata yowe huku akijiambia ni lazima aishi alee mtoto wake. “Lazima
nitoke kwenye hichi chumba, nikalee mwanangu mimi mwenyewe. Sitakufa, bali
nitaishi.” Nanaa alikuwa akijiambia kila akijitahidi kusukuma mtoto. Kama
aliyekuwa kwenye mchezo, akayapita maumivu yote kwa kuwaza uzima wake na
mtoto, akajikaza kwa mara ya mwisho,
akasukuma mpaka mtoto wa kike akatoka. Hapo ndipo alianza kulia. Alilia kama
amefiwa. “Mtoto wako ametoka na nywele zote na kucha! Mtoto mkubwa kweli!”
Nanaa alipata muuguzi mzuri sana. Japokuwa yeye aliisha, lakini alizaa mtoto
mwenye afya nzuri. Nywele nyingi kama baba yake, na macho ndio hukuhitaji
kuuliza. Geb mtupu.
Nanaa alipewa mtoto wake huku akilia.
Alikuwa mtoto mkubwa sana. Akarudishwa naye wodini, mtoto akaanza kunyonya.
Ilipofika mchana muda wakuona wagonjwa, jirani yake alikuja kutembelewa na mume
wake, Nanaa akamuomba akamsadie kumnunulia chakula. Yule baba hakukataa,
akaenda kumletea chakula kwa ahadi ya jioni atajitahidi kuleta kingi ili ale na
mkewe. Na kweli, jioni akaletewa uji kama jirani yake.
Alikula akawa
ameshiba, lakini alijikuta akilia usiku kucha. Alijiuliza ni kwa nini yule
mtoto amekuja wakati ule. “Si angesubiri tu mpaka nimalize mtihani
jamani! Nitafanyaje mitihani na huyu mtoto!?” Nanaa aliendelea kuwaza huku
akimwangalia mwanae aliyekuwa amelala vizuri bila hata wasiwasi. Watoto wengine
walikuwa wakilia lakini sio mwanae. Yeye ndio alikuwa akilia wakati mtoto wake
amelala. Kila mtu alimsifia huyo mtoto. Alichukua rangi ya mama yake, ila
nywele ndio zilikuwa nyingi sana. Nyeusi na mviringo kama mtoto wakiarabu.
Mkubwa, mrefu kama mtoto aliyekuwa ameshatimiza mwezi. Kila alipokuwa
akimwangalia yule mtoto alimkumbuka vile Geb alivyokuwa akipenda kumlalia
kifuani kwake ili amchezee nywele zake. Alizipenda sana nywele za Geb, na
hakuchoka kuzishika. Alikuwa akitulia wakati Nanaa akichezea nywele zake mpaka
analala.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Aliruhusiwa asubuhi wakati madaktari
wanapita round mawodini. Akarudi chumbani kwake. Alishukuru Mungu kukuta
mwenzake amemuachia ujumbe kuwa amehamia kwa marafiki zake kwa kipindi hicho
cha mitihani kwa ajili ya kusoma nao. Yule dada alikuwa mwalimu, alijiunga hapo
chuoni ili kuongeza elimu. Alikaa kitandani akamuweka mtoto kwenye ziwa huku
anasoma. Alimnyonyesha kwa muda mrefu kwa kuwa maziwa hayakuwa yakitoka mengi.
Alipolala, akamuweka kitandani na kuendelea kujisomea huku akiwaza pakumuweka
huyo mtoto kesho yake akiwa anaenda kufanya mtihani, ambao ulikuwa mchana.
Mpaka panapambazuka siku ya jumatano,
siku ya mtihani, Nanaa hakuwa amepata mtu. Wazo lilimjia la kumtafuta Mama G.
Aliangalia saa, akajua atakuwa kwenye biashara yake, dukani kwake. Geb
alimfungulia mama yake sehemu kubwa yakuuza mchele kwa bei ya jumla na
rejareja. Alikuwa na wafanyakazi wanao msaidia, kwa hiyo alikuwa akienda muda
na wakati anaotaka yeye.
Mtaka Cha
Mvunguni.
A |
kaweka line yake yazamani, akapata
namba ya mama G. Akapiga. Iliita mara moja tu, akapokea. “Hujambo Nanaa,
mwanangu?” Nanaa alishindwa kujibu akaanza kulia. Alilia kwa muda, “Vipi mama?
Hujambo?” Mama G aliendelea kumbembeleza kwa upendo lakini Nanaa aliendelea
kulia. “Umenitupa mama yako!” “Nina shida sana mama yangu. Naomba
msaada wako.” “Unataka nini?” “Nahitaji msaada wako kwa masaa kama matatu tu.
Lakini usimwambie mtu yeyote kama unakuja kwangu na tumewasiliana.” “Unataka nije
wapi?” “Hapa chuoni. Tukutane ofisi za Utawala. Saa sita kamili.” “Nitakuja
mama. Usiwe na wasiwasi.” Nanaa akamshukuru na kukata simu. Aliendelea kulia kidogo,
akajiambia anapoteza muda.
Nanaa na
Mama G.
Ilipotimu saa 5:50 asubuhi, Mama G
alikuwa akiegesha gari karibu na ofisi za Utawala hapo chuo kikuu cha Mlimani.
Yaani dakika kumi kabla ya muda wa miahadi yao. Alitafuta sehemu yenye kivuli
ndipo akaegesha gari yake. Akabaki ndani ya gari akimsubiria Nanaa. Ilipofika
saa sita na dakika tano, Mama G akashangaa mtu anagonga kwenye kioo chake cha
dirisha. Akashusha kioo, akabaki anamshangaa Nanaa na mtoto. “Nipo kwenye
mtihani mama yangu. Naingia saa sita na nusu. Nisaidie kukaa na mwanangu wakati
nafanya huu mtihani. Nikitoka nitamchukua mwanangu.” Mama G akiwa na mshangao
mkubwa sana, akakubali. “Hamna shida. Utanikuta hapahapa.”
“Nakuomba mama, usimwambie mtu. Ibaki
siri yetu tu.” “Wala sitasema.” Nanaa akambusu mwanae, akamfunua kidogo ili
amuongeleshe. “Nitarudi muda sio mrefu. Unisubiri. Umesikia eeh? Mama
hatachelewa.” Alimuongelesha mwanae kwa upendo. Akambusu tena mtoto wake huku
Mama G akimwangalia. Akamkabidhi yule mtoto kwa Mama G, akabaki akimwangalia
mwanae. “Nenda usiwe na wasiwasi naye. Atakuwa salama tu.” “Asante
mama.” Akashukuru huku machozi yakimtoka. “Nenda kawahi mtihani. Utanikuta
hapahapa na mwanao.” Nanaa akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Cha kwanza alichofanya Mama G, ni
kuanza kumchunguza huyo mtoto aliyeachiwa. Alibaki akimgeuza asimalize.
Alimkumbatia nakushindwa kumuweka chini, akabaki akimwangalia kwa muda wote.
Huku machozi yakimtoka. Alianza kuomba. Akamshukuru Mungu kwa karibia nusu saa
huku machozi yakimtoka. Alianza kumuombea yule mtoto huku akimbariki bila
kuchoka. “Asante Mungu umekumbuka uzazi wangu. Asante Yesu kunipa huyu
mtoto.” Akaendelea kushukuru huku amemkumbatia huyo mtoto kwa upendo
sana.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Baada ya kumaliza tu mtihani wake,
Nanaa akarudi. “Pole mama. Amekusumbua?” Nanaa aliongea akiwa amesimama
dirishani upande wa dereva alipokuwa amekaa mama G. “Hata kidogo. Kwanza
hajaamka!” Nanaa alikuwa akimwangalia mwanae. “Analala sana. Inabidi niwe
namuamsha ili anyonye.” “Naomba uingie ukae hapo kwenye gari, Nanaa.” Nanaa
akaingia kiti cha mbele. Nakukaa.
“Umejifungua lini?” “Juzi.” Nanaa akajibu,
na kumuacha yule mama akiwaza. “Mtoto anaitwa nani?” “Sikuwa hata nimefikiria
bado. Maana mtoto mwenyewe nimejua jinsia yake siku amezaliwa. Halafu sikumtarajia
kama angekuja kipindi hiki ambacho nina mambo mengi. Mitihani inayonilaza macho.
Nilijua atasubiri mpaka nimalize mitihani, pengine akili ingekuwa imetulia na
kuweza kufikiria. Sikutaka kukurupuka tu na kumpa jina. Nilitaka mpaka nitulie
ndio nifikirie vizuri jina la kumpa. Au wewe unajina lolote ungependa nimpe?”
Nanaa alimuuliza huku akimwangalia mtoto wake.
Mama G akacheka. “Labda tumpe langu.
Oliva.” “Liv! Zuri sana. Basi hilo hilo ndio atakuwa akiitwa. Nikimaliza chuo
nitaenda kumuandikisha hilo la Oliva.” Nanaa alimchukua mtoto wake.
“Nakushukuru sana mama.” “Mitihani imeisha?” “Bado mama yangu. Kesho ninao
mwingine asubuhi. Nilitaka kukuomba uje tena, kama utaweza.” “Hamna shida.
Lakini Nanaa, kwa nini tusiende wote nyumbani? Nitakuleta asubuhi.” “Hapa nipo
naishi vizuri tu, nipo kwangu.” “Ulikodi chumba mtaani?” “Hapana mama. Ni
hapahapa hosteli. Ila nipo chumbani mimi na Liv tu. Mwenzangu amehama chumba.
Anajisomea na wenzake kwa ajili ya mitihani. Ila kama hutaweza hamna shida
nitatafuta mtu mwingine.” “Nitaweza Nanaa. Unajua sina kitu chakufanya sasa
hivi. Grace na familia yake walishaondoka pale, wanaishi kwao. Nipo mimi na Geb
tu. Sina chakufanya. Nitakuja.”
“Asante mama. Lakini naomba usije
kumwambia mtu. Nitahitaji msaada wako kwa masaa machache tu, ambayo nitakuwa
kwenye mtihani, baada ya hapo unaweza kuondoka tu.” “Basi nitawahi kidogo,
nitakuletea uji. Unywe kabla yakuingia kwenye mtihani.” Nanaa akacheka. “Asante
mama yangu. Nitakuona kesho.” Alimuacha
Mama G amekaa kwenye gari yake akiwaza. Hakuwa amezima hilo gari tokea afike
hapo, akawa amewasha AC kiasi kwa ajili ya mtoto.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Alitoka hapo na kuanza kununua vitu
vya mtoto na vyakula vya kumpikia Nanaa. Alipofika tu nyumbani akaingia jikoni.
Geb alimkuta mama yake anahangaika jikoni. “Una wageni?” “Hapana? Kwani vipi?”
“Naona unamasufuria zaidi ya mawili hapo jikoni. Halafu chupa za chai kubwa,
tena mpya na hotpots mpyaa!” Akanyamaza, kitu kilichomtia wasiwasi Geb na
kurudi tena pale jikoni. Akafungua mlango akaingia mpaka ndani kwani mwanzoni
alisalimia, akawa anaongea naye akiwa anaelekea chumbani kwake.
“Mama!?” “Sufuria hili la supu ya kuku, hili
lina mifupa ya nyama ya ng’ombe ili nipate supu ya kupikia mtori. Na hapa
naandaa kupika mtori, pale ni uji wa kawaida.” Geb akakunja uso. “Vyote hivyo!?”
“Kwani shida yako wewe nini?” “Basi mama. Mbona mkali?” “Nakuona maswali hayakuishi!”
“Ujue nimekuuliza swali moja tu mama.” “Bwana eeh!” Geb akacheka, akatoka,
baada ya kuoga akarudi jikoni kwa mama yake.
“Mchana nilipita pale dukani,
sikukuona?” “Nilitoka.” Mama G, alijibu kwa kifupi huku akiendelea kupika.
“Najua ulitoka mama yangu, ndio nataka kujua ulikwenda wapi wakati uliniita,
nikakwambia nitakuja wakati wa chakula cha mchana!” Mama G, akasimama kidogo
akiwaza, akajua ameshagonganisha magari. “Kwani leo vipi, mama?” “Kuhusu nini?”
“Upo kama una wasiwasi. Uso wako haujatulia kabisa! Au kuna kitu unahangaika
kunificha?” “Wewe naona umechoka leo. Hebu nipishe bwana nimalizie kupika.” Geb
akaamua kunyamaza.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Mama G aliamka asubuhi na mapema,
akamalizia kupika kila kitu na kupasha moto vyakula vya jana yake, akaviweka
kwenye zile chupa za chai, na hotpots. Akaanza kuweka kwenye gari yake. Geb
aliamka baada ya kukurukakara nyingi za mama yake. “Nikusaidie?” “Hapana.
Nishamaliza.” “Kwani una mgonjwa?” “Mbona una maswali mengi wewe Geb? Unashida
gani na mimi?” “Mbona mkali hivyo mama yangu? Mbona swali ni dogo tu?” “Ndiyo
nina mgonjwa. Na sitaki swali jingine.” Geb akacheka nakurudi chumbani kwake.
“Siri hizo Mama G, wewe! Zitakutokea puani.” “Hayakuhusu. Wewe nenda kazini.”
“Haya mama yangu.” Geb alijibu akiwa chumbani kwake na Mama G jikoni.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Alifika sehemu ile ile aliyokubaliana
na Nanaa, akaegesha gari. Baada ya muda mfupi Nanaa akaja na mtoto wake.
“Sijalala mama. Mtoto ameanza kulia.” “Hashibi. Mlete nikae naye hapa, wewe kula.
Nimekuletea vyakula. Kula kwa haraka vikiwa vya moto, ili maziwa yatoke.” Bila
kujivunga, Nanaa akamimina uji, akaunywa wote. “Nikirudi nitakula tena.
Nilikuwa na njaa sana. Asante mama yangu.” “Wewe nenda, niachie wajina wangu.”
Nanaa akatoka baada ya kumbusu mwanae mara kadhaa akiwa ameshikwa na mama
G.
Baada ya mtihani akarudi na kukuta
yule mtoto ni kama ameogeshwa. “Umemuogesha?” “Nimemfuta tu. Nimenunua kila
kitu, nazunguka navyo kwenye gari. Nilichemsha maji kabisa, nikaweka kwenye chupa.
Kwahiyo nimemfuta, nikambadilisha nguo kabisa. Vipi mtihani?” “Hivyo hivyo
mama, itaisha tu. Nataka nikalale ili baadaye niamke nisome.” “Twende wote
nikakae na mtoto ili wewe ulale.” Nanaa akaanza kulia.
Alilia kwa muda mrefu. “Naomba
utusamehe Nanaa. Tulishindwa kukuthamini mwanangu. Wote tulijilaumu sana. Zaidi
mimi niliyekuacha nje. Nisamehe mwanangu. Nilipitiwa.” “Hamna neno
mama. Hata hivi nakushukuru kwa kuja kunisaidia. Ngoja sisi twende.” “Siwezi
kurudi na hivi vyakula vyote Nanaa. Nimekupikia wewe mwanangu. Naomba
uvichukue.” “Sina pakuviweka mama!” “Basi naomba uniruhusu twende wote
mpaka huko unapoishi. Nikusubiri ule, ulale, wakati nakushikia mtoto. Ukiamka
ukaoga na kula tena, nitaondoka.” Nanaa alianza kulia tena.
“Najua tulikuudhi mwanangu. Lakini
sasa hivi unahitaji msaada ili umalize salama. Acha nikusaidie ili juhudi zako
zote za miaka yote zisiende bure. Umejinyima vingi sana ili umalize. Kubali
nikusaidie mtoto, ili wewe uzingatie mambo ya shule tu. Ukimaliza mitihani,
ukinifukuza, wala sitakusumbua.” Nanaa akacheka na machozi yakimtiririka. “Haya mama
yangu.” Wakaongozana mpaka chumbani kwake.
Akala tena na kulala wakati Mama G
anambadilisha mtoto wake. Aliamka akampa tena chakula, akajaribu kumnyonyesha
mtoto wake, maziwa yakaanza kutoka kidogo. “Kazana kula. Yatatoka tu.” “Sasa
umemletea nguo zote hizo, nitaziweka wapi?” “Nitakuwa naondoka nazo kwenda
kufua, asubuhi narudi nazo.” Nanaa akacheka. “Umeamua kuhamia hapahapa?”
“Nakushikia mpaka mitihani iishe.” “Mmh! Kwani unampango wa kuhamia hapa?”
“Hapana. Nakuja asubuhi, naondoka usiku.” “Kwa hiyo huondoki sasa hivi?” “Saa
mbili au tatu usiku mwisho. Naondoka.” “Kweli umeamua kunisaidia mama yangu.”
“Ili usilemewe. Wewe waza mambo ya shule tu. Mtoto kazi yangu. Mnyonyeshe tu, mengine
yote ni mimi” Nanaa alimshukuru sana Mungu kwa hilo. “Asante mama.”
Bila kupoteza muda, akaoga, akala,
nakurudi kusoma. Siku hiyo alikaa na Mama G, mpaka usiku. Alihakikisha Nanaa
ameshiba, akamuachia uji wakunywa usiku kama ataamka nakusikia njaa. Akambadili
mtoto nguo, akamlaza vizuri. Ndipo akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Kesho yake tena mama G akarudi.
“Nakushukuru kwa chakula mama. Maziwa yameanza kutoka. Liv amelala vizuri kwa
kushiba.” Nanaa alimuwahi Mama G, mara alipoingia, akacheka. “Basi nipe
nimshike, wakati wewe unakula. Kazana kula, yatatoka mengi zaidi.” “Unamizigo
mingi! Ni nini tena umeleta?” “Matandiko yake huyo. Vitambaa vyakumshikia na
kumsafishia. Mashuka yake, na kichandarua kidogo, ili mchana akilala
nimuwekee.” Nanaa akacheka.
“Naona nimekupa kazi kubwa! Pole mama
yangu.” “Ndio nafurahia mwenzio!” “Kwa hiyo huoni kama usumbufu?” “Naona
umeniheshimu sana Nanaa. Wewe kula, usome. Mengine tutaongea wakati mwingine.”
Alimpisha pale kitandani ili amtandikie mjukuu wake, yeye akahamia mezani
kula.
Alikula, akaoga na kuanza kusoma tena
wakati Mama G, akimsafisha mtoto kitomvu. “Kitaanguka mapema kweli!” “Sasa
hivyo unavyomsafisha, haumii?” “Angelia. Lazima kumsafisha vizuri ili kisioze.”
“Vitu vyote hivyo umekuja navyo!?” Mama G, akacheka. “Shuguli imenipata! Na
hivi umempa jina langu, basi ndio na mapenzi yanazidi.” Nanaa akaendelea kucheka
akimtizama vile anavyohangaika na huyo mtoto.
Siku hiyo hakuwa na mtihani.
Wakashinda hapo chumbani pamoja, Nanaa akila na kusoma huku Mama G, akimlelea
mtoto. Ilipofika usiku akaondoka na kumuacha Nanaa ameshiba. Akaondoka na nguo
chafu za Nanaa na za mtoto wake. Akarudi nazo nyumbani.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Alimkuta Geb amekaa sebuleni.
“Natamani kukuuliza habari za huko ulikokuwa mpaka unarudi usiku kila siku!
Lakini najua hutanijibu.” “Sasa si unyamaze!” Geb alinyanyuka kwenda kumpokea.
Alikuwa na mizigo mingi na begi ambalo hakutaka Geb ashike. “Wewe nenda
kanioshee hivi vyombo vyote. Chupa za uji na chai, hizo hotpots na hayo
mabakuli. Halafu bandika nyama. Nakuja sasa hivi.” Geb hakuongeza neno, akapokea
na kwenda jikoni.
“Mama G! Naona mapenzi yako yameisha
kabisa kwangu. Natamani kumjua huyo aliyechukua nafasi yangu! Siku hizi hata
hunitafuti kwa la kheri wala la shari. Hunipigii kuniuliza kama nimekula au la!
Haya, nikikufuata tukale pia sikupati!” Mama yake alikuwa akimsikia mwanae
alipokuwa jikoni yeye anafua kwenye mashine, lakini akanyamaza. “Najua
unanisikia mama.” Akamsikia mama yake anacheka.
Akarudi pale jikoni. “Mbona shuguli
zimekuzidi Mama G, vipi?” “Mmbea wewe? Unachonifuatilia ni nini?” “Mimi na wewe
Mama G?” “Huna lolote. Nipishe nipike bwana wee. Umemsikia Grace?” “Alipita
hapa na mwanae, kukuangalia. Anasema hakupati kwenye simu.” “Yaani nyinyi
wawili, mtafikiri bado mnanyonya! Kutwa mpo mgongoni kwangu! Niacheni na mimi
nipumue.” “Yamekuwa hayo?” “Ndiyo. Niacheni. Kutwa mnataka kunisikia! Na mimi
nina maisha yangu.” “Mwenyewe huyo Mama G!” “Ukisikia mwingine ujue kopy. Mjini
nipo peke yangu.” Geb akaanza kucheka
akimwangalia mama yake.
“Nikusaidie?” “Sitaki. Mbona
umenikazania hivyo?” “Basi mama. Nakaa hapo pembeni nakusubiria. Sikuongeleshi
tena.” “Bora.” Mama G, alimaliza kupika haraka. Akaenda kuoga na kulala.
Hakuongea sana na Geb, Geb alimuona amechoka.
Hakuna
Siri Duniani.
Asubuhi tena akaamka na kaunza upishi
wake. Geb alitoka akanywa uji aliokuwa amemtayarishia, akabeba chupa yake ya
uji akamuaga mama yake akatoka. Aliondoka akaenda kuegesha gari mbali kidogo na
nyumbani kwake. Kama baada ya lisaa akamuona mama yake akitoka, akamfuata nyuma
kwa siri. Akashangaa anaelekea chuo kikuu cha Mlimani! Aliendelea kumfuata bila
mama yake kujua. Akaona ameegesha gari nje ya moja ya hosteli, akaanza kushusha
vile vitu kutoka kwenye gari lake, na kupandisha navyo juu.
Kwa kuwa Geb alishasoma hicho chuo,
hakupata shida kuficha gari yake na kumfuatilia mama yake mpaka juu. Alimuona
mama yake akimalizia mzigo wa mwisho. Akamfuata taratibu na yeye akipandisha
ngazi huku akijificha na gazeti usoni. Akawa kama mtu anayelisoma. Alipanda
naye bila mama G, kujua msoma gazeti nyuma yake ni mwane Geb, mpaka akaingia
chumbani kwa Nanaa, Geb akapitiliza mbele kidogo, akawa anachungulia.
Pakatulia. Geb akaanza kufikiria kama aingie au la. Mara akamuona Nanaa anatoka
akiwa na haraka. Akasubiri kidogo tu akagonga.
Damu Nzito Kuliko Maji.
“Umesahau nini?” Mama yake akafungua
mlango huku amebeba mtoto. Alishituka sana baada ya kumuona Geb. “Kumbe huku
ndiko unapokuwa unakuja?” Geb aliingia akakaa kwenye kiti. Mama yake akafunga
mlango kimya kimya akijua ameshakamatwa.
Akarudi akaanza kumsafisha mtoto
vizuri, akambadilisha nguo. Akabaki amempakata mtoto bila hata kumsemesha Geb.
Alipomlaza tu kitandani, Geb akaenda kumchukua pale kitandani. Akampakata,
akamuangalia kwa muda mrefu huku akimgeuza geuza bila yakusema kitu.
Aliporidhika akachukua kitambaa akajifunika kifuani kisha akamlaza yule mtoto
kifuani kwake, akanyoosha miguu kwenye kiti kingine, akanyamaza.
“Nanaa aliniambia nisimwambie mtu.”
Mama G akaanza kama kujitetea lakini Geb hakujibu. Aliendelea kumpapasa yule
mtoto taratibu mgongoni kama anayembembeleza. “Lakini nilipanga baada ya
kumaliza mitihani yake ndio nikwambie. Yupo kwenye mitihani, sikutaka kumkera
akashindwa kufanya mitihani yake.” Geb hakumjibu kitu. Akajivuta nyuma
akajiegemeza, akafunga macho akiwa amemuweka mwanae kifuani kwake.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Baada ya masaa mawili, Nanaa akarudi. Alikaribia kuanguka baada ya
kumkuta Geb amebeba mtoto wake huku amefunga macho, palepale kwenye kiti. Akamgeukia
Mama G. “Pole na mtihani.” Nanaa akabaki kimya. “Kaa chini unywe supu.” “Maziwa
yanamwagika. Nataka nikaoge, nije kumnyonyesha.” Nanaa alitoka, baada ya muda
akarudi akiwa amejifunga khanga. Akamchukua mwanae kutoka kifuani kwa Geb bila
hata kumsemesha Geb, akaanza kumnyonyesha. Liv alinyonya mpaka alipomaliza,
Nanaa akamuweka begani ili ateuke lakini Geb akaenda kumchukua, akamuweka yeye
begani kwake. Alizunguka naye pale chumbani mpaka akasikia mtoto ameteuka,
akarudi kukaa naye palepale, na mtoto
kifuani kwake.
Mama G, alimuwekea supu kwenye
bakuli, Nanaa akaanza kunywa. “Nguo inalowa, Nanaa!” “Maziwa yamekuwa mengi.
Itabidi kukamua. Ningekuwa na friji ningekuwa nakamua, nakuweka kwenye friza
kama nilivyofundishwa kliniki.” Pakazuka ukimya mwingine. “Jilaze mama kidogo.”
Nanaa alimuhurumia Mama G aliyekuwa akifika pale asubuhi sana, nakuondoka
usiku. Na wazi alionekana anaamka alfajiri ili kupika vyakula vyote vile.
Alikuwa amebadilika kama sio yeye mama G. Alirudi kuwa msichana. Mwili
ulipungua sana. Nanaa aliona, lakini hakuwa na muda wa mazungumzo ya ziada,
zaidi ya kuomba msaada na kupokea kile anachopewa. Alitaka akili zitulie ili
amalize mitihani yake, basi. Sio kuanzisha stori za zamani.
“Wewe ndio unatakiwa kulala Nanaa.
Upumzishe huo mgongo.” “Nina mtihani wa mwisho kesho. Lazima nisome.
Nitapumzika baadaye. Wewe lala kidogo. Najua umechoka.” Mama G akajilaza
kitanda cha mwenzake Nanaa, akalala muda huo huo. Alikuwa na uchovu wa kuamka
asubihi asubuhi.
Nanaa aliendelea kusoma bila
yakusemeshana chochote na Geb. Liv naye alilala kama masaa manne tena ndipo
akaamka. Nanaa alimchukua, akamuangalia diaper yake, akambadilisha na nguo,
ndipo akaanza kumnyonyesha tena. Walikaa pale mpaka usiku. Kama kawaida Mama G
akachukua vyombo na nguo chafu, akaondoka, akamuacha Geb pale amembemba mtoto
wake huku amemfunika ili asing’atwe na mbu. Nanaa alishangaa usiku unazidi
kwenda lakini Geb haondoki pale na wala haongei chochote.
Yeye akapanda kitandani akalala
wakati Geb yupo na mtoto. Alimuamsha mara mbili kunyonyesha na kila alipomaliza
kumnyonyesha mtoto, yeye Geb alimchukua huyo mtoto na kumrudisha kifuani. Mpaka
asubuhi mama yake alipokuja, ndipo na yeye Geb akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Nanaa alipumua kwa nguvu. “Kwa nini
umenigeuka mama jamani!? Nilikwambia usimwambie mtu!” “Mungu wangu ni shahidi
Nanaa, Geb amenifuata bila ya mimi kujua. Nimesikia mlango unagongwa mara tu
ulipotoka hapa jana. Nikadhani ni wewe unarudi labda umesahau kitu, kumbe ni
yeye. Amenikasirikia hataki kuniongelesha. Nimejaribu kumuelezea kuwa nilikuwa
nafuata matakwa yako kuwa nisimwambie mtu, lakini hajanijibu. Amenikasirikia
sana.” “Pole na samahani mama. Lakini leo ndio mwisho. Nikitoka kwenye huu
mtihani utakuwa huru, nitamlea mwanangu mwenyewe. Kwenye saa kumi nitakuwa
nimemaliza na wewe uwahi kurudi nyumbani.” Mama G, akanyamaza.
Nanaa akala nakurudi kujisomea mpaka
kwenye saa sita, Geb akarudi na mashine ya kukamulia maziwa, akaweka mezani
bila ya kumsemesha mtu. Mama yake akaichukua, aliposoma akamkabidhi Nanaa.
Ilikuwa nzuri na ya kisasa yenye chupa zake kabisa ya kuhifadhia maziwa.
Ilikuwa na cooler box yake, ya kutunzia hayo maziwa yasiharibike. Nanaa
akakamua maziwa yake. Kwa kuwa alikuwa na maziwa mengi, akafanikiwa kujaza hizo
chupa zote alizokuwa ameletewa na kuzihifadhi ndani ya hiyo cooler boksi. Muda
wakwenda kwenye mtihani wa mwisho ulipofika, akaondoka na kumuacha Geb amembeba
mwanae.
Shilingi
Yapinduka…
Kumbe Geb alirudi na kiti cha gari
chakumuweka mtoto. Car seat. Nanaa alipotoka tu kwenda kwenye mitihani,
Geb naye akakusanya vitu vya mtoto wake na maziwa aliyoyaacha Nanaa, akataka
kutoka. “Unaenda wapi na mtoto? Naomba usiondoke na huyo mtoto, Geb. Nanaa
atachanganyikiwa. Huyo mtoto ni roho yake! Anazungumza naye usiku kucha.
Tafadhali usimchukue huyo mtoto.” “Mwambie sasa hivi ni zamu yangu. Alishakaa
na mtoto wangu miezi 9 tumboni bila kuniambia. Akamzaa pia hakuniambia. Mwambie
sasa hivi na mimi ni zamu yangu. Nitamtafuta baada ya miezi 9, ndipo tutajua
hatima ya mtoto.” “Huyo mtoto ni mdogo sana Geb. Bado anamuhitaji mama yake kwa
maziwa. Ananyonya. Acha ukorofi kama baba yako.” Geb akatoka bila kuongeza neno.
~~~~~~~~~~~~~~
Nanaa alitoka kwenye chumba cha
mtihani akiwa anafuraha zote. “Sasa hivi unaweza kwenda mama yangu. Nakushukuru
sana kwa msaada wako.” Akashangaa Mama G, ameinamisha kichwa. Nanaa akaangalia
kitandani. “Mtoto wangu yuko wapi, mama?” “Geb amemchukua.” “Unamaanisha
nini!?” Nanaa alishaanza kulia kweni alielewa lakini alikataliana na
alichokielewa. “Anasema ulikaa na mtoto wake miezi 9 tumboni bila kumwambia,
ukamzaa pia hukumwambia. Amesema atakutafuta baada ya miezi 9 ya kukaa na huyo
mtoto kama wewe.” Nanaa alikaa chini nakuanza kulia. “Namtaka
mtoto wangu, mama! Mpigie simu Geb.” “Hapokei.” “Naomba
nipeleke nyumbani kwake.” Wakatoka huku Nanaa akilia sana.
Mtakuja!
W |
akafika getini mlinzi akawaambia Geb amesema asimfungulie mtu
yeyote geti. Mama yake akamwambia aende akamwite Geb, amwambie mama yake yupo
getini. Geb akasema geti lifunguliwe. Nanaa na Mama G, wakaingia. Wakamkuta Geb
yupo sebuleni. “Namtaka mtoto wangu Geb.” Nana aliendelea kulia. “Mtoto yupo
amelala. Na hapa ni nyumbani kwao, amelala. Unakaribishwa kumpa huduma zote
unazotaka kumpa mtoto wangu, lakini hapahapa ndani. Unaruhusiwa kutoka na kuingia
utakavyo, ila mwisho ni saa kumi na mbili jioni. Ukizidi huo muda haujarudi,
ujue utalala nje. Na hutaruhusiwa kutoka na mtoto wangu.” Geb alimbadilikia
Nanaa kama sio yeye.
“Huwezi kufanya hivyo Geb!” “Basi subiri
baada ya miezi 9, ndipo na mimi nitakutafuta tuzungumzie hatima ya huyu mtoto
inakuaje. Sasa hivi na mimi nalipizia muda wote uliokaa na mwanangu bila
kuniambia. Ukikubaliana na hayo masharti nakukaribisha uishi hapa ili
kumuhudumia mtoto.” Geb akaingia chumbani alikokuwa mtoto na kumuacha Nanaa akilia
palepale na mama yake yupo kimya.
Baada ya muda walimsikia mtoto
ameamka, Geb anambembeleza. Nanaa akamuomba Mama G khanga. Akamtolea khanga na
vitenge, akaingia bafuni kuoga ndipo akaingia chumbani kwa Geb. Alitaka
kumchukua yule mtoto atoke naye, Geb akamkataza. “Nimekwambia huyu mtoto hapa
ndio amefika.” “Nataka kwenda kumnyonyesha.” “Nimekwambia unakaribishwa
kumuhudumia humu humu ndani kama utaweza. Kama huwezi, basi. Lakini hatatoka
humu chumbani. Ninayo maziwa yakumtosha mtoto wangu. Na yakiniishia, nitaenda
kumnunulia. Kwa hiyo kama unahitaji muda wa kwenda kufikiria, mlango uko wazi.
Ila ikifika saa kumi na mbili kamili jioni, ujue hutaruhusiwa kurudi, mpaka
tena kesho.” Nana alitamani kuchanganyikiwa. Alikaa kwenye kochi pembeni ya kitanda,
akaanza kumnyonyesha mtoto wake. Mtoto
alitulia akaanza kunyonya, lakini Nanaa aliendelea kulia kwa kwikwi.
Alipomaliza kunyonya Geb akamchukua
akamuweka begani ili ateuke. “Unakaribishwa kitandani kulala.” Geb aliendelea
kumbembeleza mtoto wake huku akimwambia Nanaa. “Sina shida. Wanawake zako
unalala nao hapohapo. Halafu unataka mimi na mtoto wangu pia tuje kulala
hapohapo ulipokuwa ukilala na wanawake zako! Uchafu wa namna gani huo?
Humthamini hata mtoto!” Nanaa aliendelea kulia. Geb akanyamaza kimya, mtoto alipotoa mlio
kama ametoa hewa, akamrudisha mtoto kwa Nanaa, akatoka.
Baada ya muda akarudi. “Usiku wa leo
mtalala kule kwenye chumba chako. Nimeshawatayarishia. Kesho nitaenda kununua
kitanda kingine, nitakuja kumchukua mtoto.” Nanaa akasimama na mtoto wake
akatoka huku akilia.
Alipoingia tu kule chumbani Mama G,
naye akaingia. “Naomba utulie Nanaa. Sio vizuri unavyolia huku umebeba mtoto.
Unamtia simanzi huyo malaika wa Mungu asiye na hatia. Huyo mtoto anahitaji
mapenzi yako sana. Naomba utulie ulee mtoto wako.” “Sio humu
ndani, mama.” “Unataka kwenda wapi? Maana pale hosteli chuo kikifungwa
mtatakiwa kuondoka, utaenda wapi na mtoto mdogo hivyo?” “Nina pesa
ya kukodisha chumba.” “Ulishapata hicho chumba?” Nanaa akashindwa kujibu akaendelea
kulia.
“Eti Nanaa?” “Nitapata
tu mama.” “Basi mimi naomba utulie mpaka utakapo weka sawa mambo yako ndio
ufikirie chakufanya. Lakini sasa hivi naomba utulie na mtoto. Pata muda
wakupumzika, jilaze hapo kitandani na mtoto wako.” Nanaa alipanda kitandani na
mtoto wake huku akilia kwa uchungu. Akamkumbatia kwa upendo huku akiendelea
kulia mpaka akapitiwa na usingizi.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Aliamshwa na Mama G akitaka ale.
“Sisikii kula mama.” “Lazima ule. Lasivyo hayo maziwa yatakauka yote, halafu
mwanao atateseka. Kwanza umelowa. Kaa uyakamue, tumuamshe na Liv anyonye.”
“Mmemuita mwanangu jina gani!?” Kumbe Geb alikuwa amekaa pembeni. “Nanaa
alinipa ruhusa kumpa jina lolote ninalotaka, ndio nikampa la kwangu. Olivia.
Lakini mama yake analifupisha anamwita Liv. Ila kama hujapenda, unaweza kumpa jingine
unalotaka wewe.” “Mimi, mama yake nimelipenda hilo la Olivia. Ataitwa Olivia
sitaki jina jingine.” Geb akacheka, akasimama. Akamsogelea mtoto wake
akamchukua pale kwa mama yake, akaanza kumuangalia tena.
“Mtoto amefanana na mimi huyu! Mpaka
raha.” Geb akajisifia. “Wala hajafanana na wewe kitu chochote! Kwanza nashangaa
kwa nini unafikiri ni mtoto wako.” “Haya macho ni alama ya kwanza na ya pekee.
Muulize mama, hata baba yetu alishindwa kutukana tulipozaliwa. Fili mwenyewe
alizaliwa na haya macho, hayaepukiki na hakuna mwenye haya macho. Utazunguka
sana, utagundua ni sisi tu ndio tuna haya macho. Haya hilo moja, na kubwa na la kwanza. Kingine
hii nywele ni yangu kabisaa! Halafu mrefu kama mimi. Sasa kama kuna
uliyemdanganya huko, ataandika maumivu. Huyu mtoto hapa amefika kwao. Hataishi
kwengine ila humu ndani. Sasa huyo baba mwingine uliyemdanganya umemzalia
mtoto, mtafutie stori nyingine.” Nanaa akaanza kulia tena.
“Hivi wewe Geb umechanganyikiwa
lakini? Kwa hiyo unaona raha hivyo Nanaa anavyolia huku ananyonyesha?” “Kwani
mimi nimesema jambo gani baya? Nimemwambia ukweli unaomuuma. Hapo analia kwa
kuwa amedanganya huko nje. Sasa ananikasirikia mimi kwa kumchukua mtoto wangu,
hana mtoto mwingine wakwenda kumuuza. Hii ni damu yangu, hakuna mtu wakuifanyia
biashara. Hata kama na wewe mama ulishiriki kunificha, lakini damu yangu
ilinililia mpaka nikaipata.” Nanaa akaendelea kulia.
“Sasa atanyonyeshaje mtoto akiwa
analia hivyo?” “Mimi sina shida. Akishindwa kunyonyesha, nampa mwanangu maziwa
ya kopo. Kwani yeye ndio atakuwa mtoto wa kwanza kukuzwa na maziwa ya kopo? Eti
Liv wangu? Twende tukatafute maziwa unywe.” Geb akataka kutoka. Nanaa akasimama
kwa haraka akamkimbilia Geb kabla hajatoka mlangoni. “Namuomba
mwanangu Geb!” Mama G, akatafuta mahali akakaa vizuri kujiangalizia. “Wala
usivunje mguu. Ukitaka kumnyonyesha mnyonyeshe tu, ukishindwa pia hamna shida.”
Nanaa akamchukua mtoto akarudi kukaa kitandani na kuanza kunyonyesha.
Mama G alijua wazi Geb amemkasirikia
sana hataki kumsemesha wala kumsikiliza, akaamua kunyamaza. Baada ya kunyonya,
Mama G akamchukua Liv, akamteusha. Akambadili nguo akataka kumuweka kitandani
alale. “Namuomba mtoto wangu.” “Utamfanya huyo mtoto azoee mikono, Geb! Atakuwa
anataka kushikwa muda wote.” “Kuna tatizo gani? Mbona alikaa tumboni kwa mama
yake miezi 9 bila shida? Kitakachotushinda kumshika sasa hivi ni nini? Namuomba
nimshike mtoto wangu. Tena ndio vizuri azoee mikono yangu.” Mama G akamnyanyua
pale kitandani, Geb akampokea, akamuweka kifuani kwake, akajiegemeza vizuri
kwenye kochi, akamfunika Liv, akatulia. “Naomba na wewe ukaoge, ule ulale, ili
upumzishe huo mgongo.” Mama G, alibaki akiongea na Nanaa.
Nanaa alimaliza kila kitu akapanda
kitandani. “Namuomba mtoto nilale naye.” Geb akafungua macho akamtazama Nanaa.
“Nimesema namuomba mtoto wangu, ni lale naye.” “Sasa hivi ni zamu yangu na
mimi. Ulilala na huyu mtoto miezi 9, tena kwa siri, bila kuniambia baba yake
ili uwe huru kufanya unayoyataka. Sijui amezaliwa wapi! Sijui alikuwa akilishwa
nini na nani kwa miezi yote hiyo 9! Sijui alikuwa akishikwa au ulikuwa ukilala
na nani wakati mtoto wangu alipokuwa tumboni! Uliamua kunificha mtoto wangu,
kwa sababu unazozijua wewe. Sasa na mimi ni zamu yangu. Nitafanya kile
ninachotaka na mtoto wangu, tena bila mtu yeyote kuniingilia. Unaona huwezi,
mlango huo hapo, ondoka.” Mama G, akasimama akaondoka kwenda chumbani kwake
kulala. Nanaa akajirudisha kitandani kulala.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Kwa kuwa alikuwa amekamua maziwa
mengi, ameweka kwenye friji, wakati mwingine alipoamka usiku akitaka
kumnyonyesha, Geb alimwambia alishamnywesha maziwa. Nanaa alikuwa anahasira
asijue afanyaje. Geb alimuonyesha wazi hamuhitaji yeye mle ndani. Asijue
amemkasirikia kwa kutomwambia ni mjamzito au maneno aliyomwambia mara ya mwisho
wakati anaondoka huku Geb akimsihi abaki! Nanaa aliondoka humo ndani kwa jeuri
sana, akimtamkia wazi Geb ni ukurasa uliopita kwenye maisha yake, na hana shida
naye tena, anakwenda kuanza ukurasa mpya na wanaume wengine. Alimuacha Geb
amesimama nje na boxer tu, akaondoka huku akimbembeleza.
Mbio
Za Sakafuni.
N |
anaa aliamka asubuhi ya saa 11, akakuta amewekewa mtoto wake
pembeni. Akakaa vizuri kuangaza macho kulia na kushoto, akajikuta yupo peke
yake. Akavaa harakaharaka, akamvalisha na mtoto wake vizuri, akamfunika na
vitambaa vingi ili asiingiwe na baridi, akatoka pale chumbani huku akinyata.
Nyumba ilikuwa imetulia kabisa kuashiria watu wote walikuwa wamelala. Akasogea
mpaka sebuleni, hakukuta mtu. Akajaribu kufungua mlango wa ndani kwa kutumia
funguo zilizokuwa zimening’inia hapo mlangoni, zikafungua bila shida. Akafungua
mlango wa pili wa barazani na geti dogo nje ya mlango wa barazani, na wenyewe
ukafunguka bila shida. Nanaa alikuwa akitetemeka kwa hofu. Alivuta pumzi,
akaangalia tena ndani akakuta kumetulia. Ndipo akatoka kwa haraka kukimbilia
getini.
Alipofika tu getini, alipokelewa na
walinzi wawili. “Unaenda wapi?” Nanaa alibabaika kidogo, akajikaza.
“Namuwahisha mtoto hospitalini. Naomba utupishe.” “Bosi mwenyewe anafahamu?
Maana amesema huyo mtoto akiwa ndani, sisi tutakuwa nje, lakini huyo mtoto akiwa
tu nje bila idhini yake, basi sisi tutakuwa ndani. Sasa je, anafahamu kuwa huyo
mtoto anatoka?” Nanaa alinyamaza na kuanza kulia. Mmoja akaenda kumgongea Geb
dirishani, Geb akatoka. Nanaa alikuwa amekamatwa, amewekwa kwenye kibanda cha
walinzi.
Alimsikia yule mlinzi akizungumza na
Geb, “Tumemuweka chini ya ulinzi.” Hakusikia Geb akijibu kitu, kumbe alikuwa
akimfuata pale getini. Alienda kumchukua mtoto wake pale alipokuwa amekaa
Nanaa, akaondoka na kumuacha Nanaa pale chini akilia sana. Aliingia ndani
akafunga milango yote kwa ndani. Nanaa alinyanyuka kurudi ndani, akakuta
amefungiwa. Alihisi anaota. Alilia kwa sauti kama amechinjwa. “Geb!
Namtaka mtoto wangu. Geb fungua mlango.” Nanaa aliendelea kulia,
~~~~~~~~~~~~~~~~
Haya Tena, Geb & Nanaa. Sasa
Hivi Ameongezeka Mtoto Wakiwa Hawapo Kwenye Maelewano. Geb Anadai Mtoto Wake, Nanaa
Naye Anamtaka Mtoto Wake. Lakini Mwenye Kisu Kikali….
Nanaa Amefungiwa Nje, Mtoto
Ndani. Hatima Yao Ni Nini? Geb Asiyejua Kuzungumza Ila Hasira Tu, Tena Safari
Hii Hasira Ya Kukataliwa Penzi Alilokuwa Akilisubiri Tokea Anasoma Sekondari.
Itakuaje?
0 Comments:
Post a Comment