Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu Ya 28 - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu Ya 28

Siku inayofuata ya jumapili James ndio alikuwa kama amechanganyikiwa. Alimtafuta Nanaa, kila eneo la pale Mlimani City, bila mafanikio. Akaamua kurudi tena pale benki ya CRDB kuzungumza na yule askari. Hakumkuta. Akaambiwa atakuwepo tena pale kazini kesho yake usiku. Siku ya jumatatu usiku James akarudi tena pale akiwa na Geb na Danny. Wakamuhoji tena kwa upya kutaka kujua kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Ndipo wazo likamjia Geb, “Kuna mtu mwingine alimpigia simu mbali na mimi?” “Nilimwachia simu. Sasa sijui.” Juhudi zikagonga mwamba. Wakaondoka.

Siku ya jumanne asubuhi sana kama saa 11, Geb akarudi tena pale CRDB kuzungumza tena na yule mlinzi kabla hajatoka kazini. Akamuomba simu yake. Akakuta alifuta namba zote zilizotoka kwenye simu yake siku ya jumamosi. Hakukata tamaa. Akamwambia atamlipa pesa, kama atakubali kuongozana naye mpaka kwenye kampuni ya simu awaombe wampe historia yote ya simu yake. Namba zilizotoka siku ile, muda wa karibia na muda Geb alipokuta Missed call, kutoka kwenye simu ile ya yule askari. Yule askari akakubali bila shida. Wakaongozana mpaka kampuni ya simu. Akaombwa kitambulisho, kuhakikisha yeye ndio mmiliki wa ile namba.

Akapewa namba mbili tu kwa muda ule alioonyesha Geb. Muhudumu wa hapo akawaambia ndizo zilizotoka usiku ule. Akaziandika, akamkabidhi yule askari. Yule askari akachukua kile kikaratasi akamkabidhi Geb. Ilikuwa namba yake Geb na nyingine hakuwa akiifahamu. Geb akamlipa yule askari, akamshukuru wakaagana.

Atafutaye Hachoki.

Geb akarudi kwenye gari ili kupiga ile simu. Iliita mara kadhaa ndipo ikapokelewa na lafudhi nzito ya kichaga. Geb akasalimia na kumuuliza kama anamfahamu Nanaa. Antii akamwambia kwa wakati huo yeye ndio ametoka TMJ alipolazwa Nanaa, hali yake sio nzuri. Alisema alikwenda kumpelekea uji asubuhi hiyo lakini Nanaa alishindwa kabisa kula. Ameacha ndio wanamuongezea dripu ya maji. Kwani hajawahi kuingiza kitu mdomoni tokea afike hapo.

Geb alitoa gari pale huku akimpigia simu James kumtaarifu habari za Nanaa. Akampigia na Danny. Wakati Geb anaingia TMJ hospital yupo mapokezi, Danny na James nao wanaingia pale hospitalini. Kwa kuwa Danny na James walikuwa wakifanya ofisi moja, waliongozana. Pale mapokezi kulikuwa kumejaa sana muda ule wa asubuhi na muhudumu alikuwa mmoja. Walikaa pale, mwishowe wakaamua kumpigia tena Antii kuuliza alipolazwa Nanaa. Antii akawaelekeza. Baada ya muda kidogo, akaingia Grace na Mama G.

Wakaongozana mpaka alipo Nanaa. Wakakuta amelala huku amezungushiwa mashine kila pande. Kila mtu akashituka. Daktari akaingia wakauliza kulikoni. Akawaambia aliletwa hawezi kupumua kabisa na anavichomi vikali sana. Aliwekewa oxygen kwa matumaini ya kumsaidia kuhema kwa muda, huku wakidhani ni pumu, lakini asubuhi yake Nanaa alianza kupandisha homa. Wakajua ni pneumonia. Akaendelea kueleza kuwa, Nanaa ameanzishia matibabu ya hiyo Pneumonia siku iliyopita, lakini hapakuwa na nafuu. Wanamwangalia siku hiyo, kama bado hali itakuwa ni hiyo hiyo itabidi juhudi za kupasuliwa na kufyonzwa maji yaliyopo kwenye mapafu, yanayosababisha homa hiyo kali ifanyike. Ili maji hayo yatolewe kabisa.

James alibaki kimya akimwangalia dada yake akiwa amelala pale kitandani. “Umejaribu kuzungumza naye?” “Hawezi kupumua. Kwa hiyo tunamwacha apumzike. Ili asitumie nguvu chache alizonazo. Anaonekana ana maji mengi kwenye mapafu. Hana nguvu.” Geb akamsogelea akamshika mkono. Ilikuwa ya baridi sana. “Nafikiri anasikia baridi. Naomba afunikwe.” “Walimpunguzia mashuka sababu ya homa. Ilikuwa juu sana.” Geb akaanza kusugua viganja vya Nanaa huku akivipulizia ili vipate joto. Akapandisha shuka lililokuwa kiunoni mpaka shingoni. Wakabaki wote wameduaa. “Mkihitaji kitu chochote, mtatuambia.” Daktari akaaga. “Asante sana.” James akashukuru.

~~~~~~~~~~~~~~~

 “Yaani mimi huwa nasema, kama kuna mkosi humu duniani, au bahati mbaya, basi dada yangu huyu amepata! Namuona anavyojitoaga kwa watu. Anajituma, upendo kwa watu, lakini wote wanamtendea unyama! Hajawahi kupata mtu au watu wakampa kipaumbele. Wakati wote huwa anapewa nafasi ya mwisho. Sijui ni kwa nini?” James akalalamika. “Nyinyi mpo pale. Watu wazima watatu, kweli jamani mnashinda kumjali mtu kama Nanaa! Hamkuwahi hata kuhisi kama ni mgonjwa?” “Nanaa alikuwa mzima kabisa James. Yaani alianza kulalamika baridi tulipokuwa njiani kuelekea pale Mlimani City. Akasema anasikia baridi kali mpaka kwenye mifupa.” Mama G, alijibu kinyonge kama kutetea, kumbe ndio anaharibu.

“Na bado ukamuacha nje!?” James akauliza kwa kulaumu. “Mmemtoa nyumbani, mkaenda kumtupa pale Mlimani City! Mnawezaje kumfanyia unyama kama huo?” “Nikupitiwa James. Mambo yalikuwa mengi pale.” “Usiniudhi zaidi ya hivi, Danny. Kwa hiyo mnachoniambia sasa hivi ni kuwa, baada ya mambo yenu mengi kuisha ndio anakuja Nanaa!? Nilipowaona pale ukumbini vile mnavyosherehekea, nikajua mmeamua kumuacha nyumbani! Kumbe mnakula na kunywa, wakati mmemuacha dada yangu nje! Tena bila kujali!? Nyinyi ni binadamu wa namna gani jamani?” James alikuwa akitetemeka. Wasijue ni hasira au hofu. Maana dada yake alikuwa mahututi pale. Taarifa alizopewa ni kuwa hawezi hata kuhema na ana maji kwenye mapafu.

“Naomba unisamehe James. Nisamehe mwanangu. Sijui nilipitiwa kivipi baba. Lakini muda wote akili yangu ilikuwa inaniambia Nanaa yupo ndani ukumbini. Kwani nilishamuaga kuwa mimi nitakaa meza ya wazazi, yeye akasema atakaa nyuma kabisa. Miguu inauma baba. Hata chakula si uliona Grace ndiye aliyeniletea? Naomba radhi James mwanangu. Nisamehe baba. Lakini nampenda sana Nanaa. Na yeye anajua.” James akatoka nje, baada yakuona machozi yanamtoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Zilipita siku tano bado Nanaa anahema kwa mashine na bado homa ipo juu. Daktari akamshauri James akubali wajaribu kumfanyia upasuaji kufyozwa maji. Ilikuwa ni uwamuzi mgumu tena wa hatari, lakini ilibidi James akubali kusaini makaratasi ya upasuaji kwani hali ya Nanaa ilizidi kuwa mbaya. Kuachwa bila upasuaji ilionyesha infection itazidi kusambaa na kuziba kabisa njia ya upumuaji. Ilikuwa lazima apasuliwe asafishwe, japo hali yake ilikuwa dhaifu sana. Kwa hali yake ilivyokuwa, kuingizwa chumba cha upasuaji kulikuwa na hatari yakutotoka hai.

“Kwa hiyo mmesema vyote ni hatari?” James akauliza tena kabla ya kusaini. “Upasuaji ni hatari na kuachwa hivyo pia ni hatari. Lakini angalau kupasuliwa kunaweza kuokoa maisha yake kama atatoka salama.” James aliomba tena dakika kumi za kufikiria kabla ya kusaini. Alizunguka na yale makaratasi huku akijiambia ni kama anaweka saini ya kifo kwa dada yake. Alikuwa kama amechanganyikiwa.

Alirudi kuuliza tena na tena, huku rafiki zake wakimwangalia nakushindwa chakufanya. Hakuna aliyeweza kufanya kazi siku nzima. Walikuwa wakipokezana kwenda kukaa na James pale hospitalini. Daktari alimlazimisha kutoa maamuzi, kwani alimwambia kadiri wanavyochelewa kumpasua, ndivyo nafasi ya kumtoa Nanaa hai huko chumba cha upasuaji, zinazidi kupungua. Ndipo ikabidi James aweke saini kuidhinisha upasuaji huo, akiwa ameelewa madhara yote.

Taarifa kwa marafiki wa karibu wa James na wake zao zilishaenea kila mahali. Wakawa wakifika pale hospitalini, watu mbali mbali  kumtizama Nanaa ambaye alikuwa hajaweza kuzungumza hata kidogo, muda wote alikuwa amelala. Geb alishindwa hata kufanya kazi. Hakuonekana ofisini kwake, BOT wala kwenye biashara zake. Muda wote alikuwa hospitalini na James. Angalau James alikuwa akitoka mchana na kwenda kuchungulia ofisini, lakini sio Geb. Hakuzungumza chochote kile. Si kumlaumu mama yake wala kuomba msamaha kwa James. Alikuwa kimya muda wote. Alikuwa akiingia na kukaa akimtizama Nanaa tu huku ameshika viganja vyake wakati wote.

Nanaa afanyiwa upasuaji.

Siku Nanaa anaingizwa chumba cha upasuaji marafiki wote waliokuwepo kwenye harusi, mpaka Malii na mkewe walikuwepo hapo kusubiria kama Nanaa atatoka hai. James alikuwa akizunguka huku akisikika akivuta pumzi nakuzishusha kwa nguvu mara kwa mara kama kutoa wasiwasi kifuani. Grace na mama yake walikuwa kimya tu. Hamna aliyemsemesha mwenzake. Kadiri muda ulivyozidi kwenda, dada yake akiwa chumba cha upasuaji, ndivyo hali ya James ilivyokuwa ikizidi kuwa mbaya. Mikono ilikuwa kichwani wakati wote akitembea huku akiliita jina la Yesu amsaidie. Alitia wasiwasi kila mtu aliyekuwepo pale.

Baada ya muda daktari akatoka na kumwambia James mambo yamekwenda vizuri. Hapakuwa na madhara mengi. Na wanaamini kama ataendelea hivyo, Nanaa atapona tu. Ndipo James alipoanza kulia huku ameweka mikono kichwani. Akainama huku ameshikilia magoti yake. “Uuuuu! Uwuuuuu!” Alisikika kijana huyo wa kichaga, James akivuta pumzi huku akilia kwa sauti ya chini. “Asante Mungu wangu. Hata sasa hujatuacha. Asante.” James aliendelea, akapiga magoti huku machozi yakimtoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda kidogo, Nanaa akatolewa chumba cha upasuaji akiwa kwenye kitanda chake kurudishwa wodini. Bado alikuwa amelala. Baada ya muda, akashituka. Akafungua macho. Akataka kujigusa usoni, Geb akamuwahi mkono. “Unamashine ya kupumulia. Usitoe.” Akamwambia taratibu. “Pole.” Nanaa akafunga macho. James akamsogelea. “Pole Nanaa.” Nanaa akafungua macho. Akamuangalia kaka yake kwa macho ya usingizi, wakaona machozi yanamtoka. “Pole sana. Utapona. Umesikia?” James akamshika na yeye mkono wakushoto. Akafunga macho na kurudi kulala. Daktari aliwaomba watu wote waondoke ili kumuacha apumzike, mpaka tena baadaye.

~~~~~~~~~~~~~~~

Walipotoka tu nje, James akawaita Geb, Danny, Grace na mama yao. Akaomba azungumze nao. “Niliwaomba mnisaidie kuishi na Nanaa kwa muda wakati nikijiweka sawa, ili nimtafutie sehemu ya kuishi. Nashukuru kwa kumpokea na kumuhifadhi kwa kipindi hicho. Nitakuja kuchukua vitu vyake nitakapotulia. Naona niendelee naye mimi mwenyewe tu. Naomba kwa sasa mumuache kabisa.” Kimya.

 James akawatizama kwa zamu, akaona wanamuangalia kama wasioelewa. “Namaanisha hivi, sitaki kuwaona tena hapa hospitalini. Kwa kuwa tunaheshimiana, naomba mnielewe na msiniudhi zaidi.” “Naomba utusamehe James. Tafadhali sana.” Grace alijaribu kabla James hajaondoka.

James akarudi na kumgeukia Grace. “Unakumbuka niliwaambia nini tulipokuwa Marangu?” Kimya. “Mmemuona mama yangu mzazi hapa?” Kimya. Hakuna aliyethubutu kujibu. “Mama yupo hapa Dar, hajarudi Moshi. Lakini hata yeye nimemkataza kufika hapa. Na ninaomba mnielewe na msirudi tena jamani. Urafiki wenu upo na mimi tu. Hilo mmeliweka wazi, na mimi ninaliheshimu. Narudia, Nanaa ni jukumu langu. Nitamlinda dada yangu na kila hatari, hata ikibidi mama yangu mzazi. Mlishindwa kuishi na Nanaa akiwa mzima, msikae hapa kumkejeli dada yangu na kudanganya uma. Naombeni muondoke kabla sijakasirika zaidi.” James akarudi chumba alicholazwa Nanaa.

~~~~~~~~~~~~~~~

Alikaa hospitalini akiwa analala tu kwa muda wa siku tatu mbele baada ya upasuaji, homa ikashuka. Akaanza kuhema bila mashine. Kwa siku hizo nane tu, tayari Nanaa alionyesha amedhoofu mpaka usoni. Kwa kuwa mapafu yalikuwa yakimuuma, akaendelea kupewa chakula kwa mrija. Antii alikuwa akijituma sana. Hakuacha kumletea vyakula vya kusagwa. Alionyesha yeye ndio muhusika haswa wa Nanaa. Alikaa siku 15 hospitalini ndipo akaruhusiwa. Antii alionyesha utayari wa kuendelea kuishi naye nyumbani kwake. Alimuahidi James kujitahidi kumlisha ili arudishe mwili.

Alitoka pale sauti haitoki kabisa. Mpaka usikilize sana ndipo ungeweza kumsikia. Alirudi nyumbani kwa Antii, moja kwa moja akaingizwa chumbani, akalala. Alilala akaamshwa na ndoto ambayo ilikuwa siku ya harusi ya Malii. Kumbukumbu zilimchukua mpaka vile Geb alivyokuwa anaingia na Liz ukumbini. Akashituka. Akamuona Geb amekaa pale pale chumbani. Akamtizama kwa muda mrefu kama akijaribu kujua kama ni ndoto au ni kweli anamuona Geb. Kwanza ilikuwa usiku sana. “Pole Nanaa.” “Asante.” Nanaa alijibu kwa sauti ya chini sana. Akaanza kutokwa na machozi. Geb alivuta shuka, akamfunika tena vizuri. “Pole sana.” Nanaa akarudi kulala asijue kama bado anaota au ni kweli!

Alipoamka, Geb hakuwepo, akajua ilikuwa ndoto tu. Antii akaingia na chakula akimtaka kula. Akajitahidi, lakini akashindwa. Zilipita siku nyingine 7, ndipo Nanaa aliweza kujaribu kukaa na kuweza. Alikondo, akawa kama katoto. Alipokuja James, akamuomba ampeleke Tabata, nyumbani kwa Geb, akachukue mizigo yake. Chuo kilikuwa kimeshafunguliwa. Wenzake walishafanya usajili, lakini Nanaa bado alikuwa amedhoofu sana hakuweza kwenda.

Kulikoungua Mpini, Kukabaki Shoka.

Baada ya kazi siku hiyo ya ijumaa, James alimfuata Nanaa na kumrudisha Tabata, nyumbani kwa Geb. Bado sauti haikuwa ikitoka, na bado mwili ulikuwa unachoka sana. Mpaka wanaingia ndani ya geti nyumbani kwa Geb, Nanaa hakuwa hata na habari! Alishakuwa amelala muda mrefu sana tokea hata James hajaondoa gari pale nyumbani kwa Antii. James akaenda upande wake. Akamuamsha kwa muda mrefu ndipo akaamka.

Akatembea taratibu mpaka mlango wa kuingilia ndani. Kaka yake akamfungulia, akabaki ameshikilia ule mlango, ili Nanaa aingie. Akaweza kupanda ngazi kwa shida, akaingia mpaka ndani. Akaenda kukaa moja kwa moja kwenye kochi.

“Vipi mama?” Mama G, akamuuliza. Kwani aliwakuta wote wapo sebuleni. James alishawaambia angemleta kuchukua vitu vyake. “Pole.” “Asante, mama.” Nanaa akajibu kwa sauti iliyosikika kwa mbali sana, akajiegemeza kichwa kwenye kochi akafunga macho.

 “Unakula vizuri?” Grace akamuuuliza. “Najitahidi lakini mwili hauna nguvu, naona na sauti imekataa kutoka!” Nanaa akajibu huku amefunga macho na kichwa bado amekilaza kwenye kona ya kochi. “Pole sana Nanaa. Kazana kula utapata tu nguvu.” Akatingisha kichwa kukubali, akatulia. “Tukuletee chakula?” Mama G, akauliza kwa upendo. “Hapana. Nina maji kwenye gari. Ndio hayo nabembelezana nayo niyamalize. Lakini nimefuata documents zangu. Nimeweka kwenye kabati. Chuo kimefungua, nataka niwaombe kina Zena, wanisaidie kunifanyia usajili. Nimechelewa, lakini nataka nijaribu tu.” Nanaa alikuwa akiongea kwa shida sauti ya chini mpaka wakazima tv kabisa ili kuweza kumsikia. James alikuwa kimya tu.

 “Si ungeahirisha huu mwaka ili upone kabisa?” Mama G, akatoa wazo. “Hii shule haijawahi kusubiri mama. Lazima nimalize tu. Nitamaliza tu mama yangu.” “Tunakuombea Nanaa mwanangu.” “Asante.” Nanaa akashukuru akafunga tena macho. “Nanaa! Jikaze twende nikakusaidie kukukusanyia vitu.” James akamsogelea dada yake. “Ulipotuambia unakuja leo kuchukua mizigo yake, tuliikusanya vizuri. Ipo yote kwenye mabegi na masanduku yake. Kasoro hizo documents. Ngoja nikazitafute. Nitaleta na mizigo yake yote. Mwache apumzike tu.” Grace akanyanyuka. “Asanteni sana.” Nanaa akashukuru huku akipandisha miguu kwenye lile kochi dogo alilokuwa amekalia. Akaikunja miguu yake ndani ya sweta alilokuwa amevaa, akaegemea kwenye kochi, akalala. Alilala pale pale wakimwangalia.

Hakuwa akisikia kitu chochote kinachoendelea. Wakapandisha vitu vyake vyote kwenye gari, bila hata Nanaa kujigusa. Wazi alionekana bado ni mchovu.  James akarudi kumchukua. “Nanaa! Nanaa!” James alimwita, lakini hakuitika. Akaamua kumtingisha kidogo. “Nanaa!” Akafungua macho. “Vipi?” “Nasikia kuchoka kaka!” “Unalala mchana lakini?” “Nalala. Hapa nimelala siku nzima, lakini bado mwili umechoka sana.” “Unataka nikubebe?” James akamuuliza Nanaa, akacheka. “Tutaanguka wote!” James akacheka. “Siwezi kukuangusha bwana! Kwanza umerudi kuwa kama katoto! Enzi zileee upo la kwanza. Sijui kama unajua hilo?” Nanaa akacheka. Akatoa miguu kwenye sweta. “Acha tu nitembee, nijipe mazoezi. Ninalala sana.” Akavaa kandambili zake alizokuwa amevua wakati anapandisha miguu.

“Geb!” Nanaa akaita, Geb akamwangalia. “Nakushukuru sana kwa kunipokea.” Geb hakujibu alibaki kimya. “Jamani, nikipata nguvu nitarudi kuwasalimia. Nashukuru sana kwa kuishi na mimi vizuri na kwa upendo. Nashukuru. Asanteni.” Grace alibaki ameinama. “Uje kutuona tena Nanaa.” “Nitakuja mama. Lazima nitakuja. Ngoja nipate nguvu, akili iwe shuleni. Mambo yakikaa sawa, nitakuja angalau niwasalimie.” “Naomba usiache kurudi kuja kutuona, Nanaa.” “Usijali mama yangu.” Nanaa akatoka na kaka yake.

Alipompandisha kwenye gari na kumfunga mkanda, James akarudi ndani. Bado akakuta wenyeji wao wamekaa vile vile kama alivyowaacha kinyonge. James akaingia na kusimama katikati yao. “Naomba kuweka msisitizo. Kama mlivyomsikia Nanaa. Shule yake haijawahi kusubiri, na amekataa isisubiri. Kwa hali mliyomsababishia nyinyi, bado ameamua kurudi tena shule na kuendelea na masomo yake. Tafadhalini.” James akawaangalia mmoja baada ya mwingine. “Narudia tena, TAFADHALINI jamani. Mwacheni Nanaa amalize hiyo shule. Kumuingilia kwa namna yeyote ile, ni kutangaza vita vikali sana na mimi.” James akatoka bila kutaka kujibiwa.

~~~~~~~~~~~~~~

Alirudi kwa Antii, moja kwa moja akapanda kitandani akalala. James akataka kumuamsha. “Muache tu alale. Mchana alikula vizuri. Muache alale. Akiamka nitampa maziwa.” James aliingiza vitu vyote ndani, akakaa kidogo. Kisha akaondoka akimfikiria dada yake na kumuhurumia sana asijue amsidie nini tena! Alishamaliza dawa zote alizokuwa ameandikiwa.

Baada ya siku 5 nyingine, aliweza kwenda kwenye ofisi za utawala kuzungumza nao. Mwezi ulishapita tokea chuo kifungue. Antii alikuwa amemsindikiza. Akaonyesha vyeti vya hospitalini. Wakaangalia matokeo yake ya miaka iliyopita, akaruhusiwa aendelee. Yule matron alishamtafutia chumba hapo hosteli, tokea chuo kinafunguliwa, Nanaa alishakuwa na chumba hapo hostel. Kwa hiyo hakupata shida. Mbali na yote, alitakiwa pia kuwakilisha repoti ya field aliyofanya na bado alipambana kusoma kwa kasi ili kufikia wenzie darasani. Alijitahidi kuchukua notes kutoka kwa wenzake. Mchana na usiku Nanaa alikuwa busy kusoma. Alishaondoka kwa Antii, akawa anaishi hosteli.

Nanaa Arudi Ofisini Kwa Grace

Akatoka siku hiyo mchana, hakuwa na kipindi. Akaenda ofisini kwa Grace. Alimkuta Grace ofisini kwake. “Nimefurahi kukuona Nanaa!” “Asante.” “Mwili umegoma kurudi?” Grace alimuuliza, Nanaa akacheka. “Naona angalau sauti inasikika kidogo.” “Najitahidi.” “Karibu.” “Asante. Nipo kwenye kutengeneza ripoti yangu ya field. Naomba nisaidie barua ya kuthibitisha kama nilikuwa hapa na nilimaliza muda wote niliokuwa natakiwa kuwepo hapa.” “Hamna shida kabisa. Ila na mimi naomba nikuombe kitu kimoja Nanaa.” Nanaa akajiweka sawa.

“Naomba utusamehe.” Nanaa akajaribu kufikiria. “Tusamehe kwa chochote kibaya tulichowahi kukutendea.” “Usijali Grace. Mimi nipo tu sawa.” Nanaa alijibu kiuungwana. “Mbona sasa hujarudi nyumbani? Mama hana raha Nanaa!” “Ukweli mambo yamekuwa mengi tu. Nimerudi chuoni nimekuta wenzangu wapo mbali kweli! Imebidi kuanza upya, tena peke yangu. Halafu na vimitihani vya chuo! Si unaelewa?” “Nakumbuka.” “Lazima nitarudi kuja kuwaona, najitahidi kupunguza mambo. Nikikaa sawa, nitakuja tu. Naomba mwambie mama asiwe na wasiwasi hata kidogo. Mimi mwenyewe namkumbuka. Ila akili haijatulia Grace. Bado napambana na afya yangu na shule. Naomba mtulize mama. Mwambie bado nampenda tu. Ajiandae nikija nitakuja na mazawadi kibao.” Grace akacheka.

          “Nitamwambia. Naona kidogo atatulia.” “Msalimie na Fili wangu. Na Danny. Wote nawakumbuka.” “Mnawasiliana na Geb?” Nanaa akatulia kidogo, na kuinama. Uso wake ukabadilika kabisa, hata Grace akamuona. “Hapana Grace. Hata yeye sijamuona muda mrefu!” “Naomba na yeye ukiweza umtafute.” “Nakuahidi kufanya hivyo Grace. Acha nijiweke sawa ili kunusuru hii shule. Ndio mwaka wa mwisho huu. Sitaki chochote kibaya kitokee nishindwe kumaliza.” “Nimekuelewa Nanaa. Na nitawafikishia nyumbani salamu zako.” “Hapo umenifurahisha na kunituliza. Mungu atasaidia hili la shule likiisha, nitakuwa huru.” Baada ya kukamilisha mambo yake yote akaondoka pale kurudi chuoni.

~~~~~~~~~~~~~~~

Alijitahidi na mambo ya shule, mchana na usiku akipambana ili kufikia wenzake. Baada ya mwezi mwingine, akajikuta yupo sawa na wenzie darasani. Tena yeye ndiye alikuwa akifanya vizuri zaidi kwani aliweka juhudi za ziada ili asipitwe. Kila matokeo ya test na assignments zake zilipokuwa zikitoka, Nanaa alikuwa na alama za juu sana mpaka akawa anajishangaa. Hakuwahi kuongoza kwenye darasa lolote. Akabaki akifurahia.

Mambo ya shule yalipokaa sawa, ndipo akili zake zilipotulia na kuanza hata kujifikiria yeye mwenyewe. Akaenda saluni kutengeneza nywele na kucha. Kidogo akaanza kurudia hali yake. Miezi miwili na majuma kadhaa yalishapita tokea apate wakati mzuri na Geb kimapenzi. Kitendo cha kusahauliwa nje siku ya harusi, kilimuuma sana Nanaa. Hasa akizingatia Geb alikuwa na Liz! Tena alimshuhudia akiwa amemshika mkono! Nanaa alisema wengine wote wangeweza kumsahau, lakini si Geb. Zaidi ya masaa 4 hakumuona ukumbini, asijali  na hata alipompigia simu hakupokea! Nanaa alizidi kuumia na kushindwa kuwatafuta familia ya Geb na Geb mwenyewe. Hata week ambazo hakuwa na mitihani, aliamua kukaa tu chuoni. Alishindwa kwenda kuwatembelea kabisa.

Siku zikazidi kwenda, ndipo akagundua hajatumia pedi kwa muda mrefu. “Mmmh!” Akaguna baada ya kuwaza.  Akajiangalia vizuri hakuona kitu cha ajabu. Kwa kuwa alikuwa amekonda sana, akajiambia mwili unarudia hali yake. Akaanza kujiuliza mara ya mwisho kuona siku zake. Akakumbuka alipata siku zake alipokuwa nyumbani kwa Geb. “Kaaa! Hata kama nimeshika mimba ya Yesu, ingetoka tu. Madawa yote yale niliyokunywa na operation juu! Hii sio mimba. Mwili umeshituka tu sababu yakuugua muda mrefu. Ndio maana nimepitisha siku zangu.” Akajifariji huku moyo wake ukiwa na wasiwasi sana.

Marefu Yenye Ncha.

Alipoona hofu inazidi, akaona asijitese. Akaenda duka la madawa kununua kipimo cha kupimia mimba ili kujipunguzia wasiwasi, ndipo akagundua ni mjamzito. Hofu ilimuingia asijue Geb atapokeaje lile jambo na yeye ndio alikuwa mwaka wa mwisho. Hakuwahi kuruhusu kitu kiingilie shule yake. Kama ni mwanaume aliyekuwa akimsumbua na akajua atahatarisha masomo yake, Nanaa alimuacha bila kufikiria mara mbili. Aliazimia lazima shule yake iwe mkombozi wake, kwa hiyo hakuruhusu muingiliano wa aina yeyote. Kitendo chakujigundua ni mjamzito, tena akiwa anamalizia chuo, kilimshitua sana. Zaidi mimba ya mwanaume ambaye hawajawasilina kwa muda mrefu na alishajua Geb alirudiana na Liz.

~~~~~~~~~~~~~

Tokea augue, hakutaka kuwasha simu yake. Alipopona kabisa ndipo alipopata nguvu ya kufungua mizigo yake akiwa hapo hostel. Akakuta  Grace alimfungashia vitu vyote. Kuanzia laptop mpya aliyokuwa amenunuliwa na Geb. Simu yake mpya pia ilikuwepo. Nguo zote mpya na zazamani zote zilikuwa kwenye masanduku na mabegi mapya. Mengine alikumbuka alinunuliwa na Geb, lakini mengine akahisi labda walimnunulia ili kuhifadhi vizuri vitu vyake. Ulishapita mwezi, hata James hajamuona. Alishamwambia anahitaji kutuliza mawazo chuoni tu. Kwa hiyo James akamuacha.

Kwa Geb.

Akaichukua ile simu, akaiwasha. Ujumbe wa Geb ukaingia. ‘Naomba kukuona Nanaa. Tafadhali. Japo kwa muda mfupi tu. Geb.’ Wakati anasoma ule ujumbe, simu ya Geb ikaingia. “Haloo?” Nanaa aliitika. “Unaendeleaje?” “Naendelea vizuri.” “Umepata ujumbe wangu?” Geb akauliza. “Ndio nimewasha simu na wenyewe ukaingia. Sikuwa nimeiwasha muda mrefu. Nilitaka kutulia chuoni. Nilichelewa sana kuanza chuo. Nikakuta wenzangu wapo mbali. Ilibidi kutulia ili niwafikie.” “Umefanikiwa?” “Kwa asilimia kubwa. Lakini mambo ni mengi kweli! Nahitaji kutulia kweli ili hii shule iishe.” “Pole.” “Asante.” Wakatulia.

 “Nanaa!” “Bado nipo.” “Ninahamu sana na wewe.” Nanaa akaanza kulia. “Naomba unisamehe kwa kukusahau.” “Nilikuona siku ile ya harusi. Ulikuwa na Liz. Tena umemshika mkono.” “Hapakuwa na kilichoendelea zaidi ya kule kumshika mkono, Nanaa!” “Ndio maana ulinisahau Geb. Unajua nilikaa pale nje zaidi ya masaa manne? Nikimuomba Mungu angalau uhisi mle ndani sipo, ili utoke uje unikute pale mlangoni.” “Nisamehe Nanaa. Ule utaratibu wa kusimamia harusi ulipangwa zamani sana. Hapakuwa na jinsi ya kubadilisha. Na wala Liz hakuwa sababu ya kukusahau. Nilizungumza na Mama, akaniambia umekaa kiti cha nyuma.” “Kama kweli unanijali basi ni kwa nini hukunitafuta kama ulivyoniahidi? Nilikuwa saluni, wakati unanilazimisha kuja! Nilikuja kwa ajili yako Geb. Ukaniahidi utanitafuta, hutaniacha peke yangu.” Nanaa akazidi kulia.

“Naomba niambie ulipo ili nije. Nipo safarini. Kesho ninarudi nyumbani. Nitakufuata ili tuzungumze vizuri.” Geb alibembeleza. “Hapana Geb. Acha nitulie nimalize hii shule. Nakushukuru kwa kila kitu.” “Nanaa please! Nakuomba kukuona!” “Hamna cha kuona tena Geb. Mwili bado umeisha, hamna tena nyama.” “Sijawahi kukupendea umbile lako Nanaa! Nilikupenda kabla hata sijakuona!” “Mimi najua kupenda kunaambatana na kujali Geb. Mara zote umekuwa ukimtanguliza Liz, mimi ninafuata. Unakumbuka Marangu? Nilikuacha ukiwa unamkumbatia. Kwenye harusi ulikuwa umemkumbatia. Ungekuwa unanijali mimi na hisia zangu, usingefanya uliyofanya Geb. Hujawahi kunipenda kwa mapenzi ya kweli. Na nina uhakika ingekuwa mimi ni Liz, usingenisahau nje ya ukumbi. Hujawahi kufikisha thamani yangu kama ulivyomthamani Liz. Alikuwa akiweza kunitukana mbele yako, lakini hukuwahi hata kunitetea mbele yake!” “Ukisema hivyo unakosea Nanaa! Nimemuacha Liz, ili niwe na wewe!” “Ni lini umemuacha Liz, Geb? Maana mpaka mara ya mwisho nimewashuhudia mmeshikana mikono kama wapenzi. Labda uniambie utakuja kumuacha kwa ajili yangu. Lakini haukuwahi kumuacha Liz.” “Nanaa, nakupenda wewe.” “Asante, na kwa heri Geb. Uwe na wakati mzuri, na safari njema wakati unarudi nyumbani.” “Nanaa!” Nanaa akakata simu huku akiendelea kulia.

~~~~~~~~~~~~~~~

Alikaa pale akilia. Mishowe akajiambia lazima ampe mwanae haki ya kuwa na baba. Akajiambia hata kama hatakuwa na mahusiano na Geb, basi mwanae apate haki ya kuwa na baba. Na lazima Geb ajue mapema, ili ikitokea anakufa chumba cha kujifungulia, kama mama yake, basi mwanae achukuliwe na baba yake. Akaazimia kesho yake kwenda nyumbani kwa Geb. Akasoma kidogo, akalala.

Aliamka asubuhi, akakimbilia maktaba kujisomea tena, kisha akaendelea na vipindi vingine kama kawaida mpaka ilipofika jioni akaingia kwenye mtihani. Alitoka kama kwenye saa moja na nusu usiku akiwa amechoka, lakini akakusudia lazima akamuone Geb wazungumze. Alirudi kwenye chumba chake, akaacha madaftari akachukua pochi yake, akaondoka kwenda nyumbani kwa Geb.

Hakuna Msiba Usiokuwa Na Mwenzie.

Kwa kuwa walinzi walishamfahamu, hawakuhitaji kupiga simu ndani kuuliza kama Nanaa aruhisiwe. Akawasalimia pale getini, akaingia. Alikuta magari mawili tu. Moja analifahamu ni la Geb, jingine hakuwa akilifahamu. Akaamua kuingia tu ndani. Alipofika sebuleni hakumkuta mtu. Wasiwasi ukamwingia. Lakini akahisi labda ni la Geb, amenunua gari nyingine. Akaamua kumfuata Geb chumbani kwake. Haikuwa kawaida ya Nanaa kuingia chumbani kwa Geb. Mara chache sana, tena ilikuwa kama ametumwa na Mama G, kwenda kuweka kitu. Hasa nguo safi. Ile kufungua tu mlango  akamkuta Liz yupo uchi kitandani kwa Geb. Akabaki ametoa macho. Kabla hajakaa sawa, Geb naye akawa anatoka bafuni akiwa uchi na taulo mkononi anajikausha. Nanaa akawaangalia wote kwa zamu, kisha akatoka pale chumbani.

“Nanaa!” Alimsikia Geb akimwita. “Nanaa!” Nanaa akaendelea kutembea. “Nanaa! Naomba simama tuzungumze.” Nanaa akaendelea kutembea. Akataka kufungua mlango wa kutoka nje kabisa. Pale barazani. “Nanaa! Sio kama inavyoonekana.” Nanaa akasimama, akamgeukia. “Sio kama inavyoonekana. Naomba usiondoke. Nisikilize.” “Huo mchezo nimeshachezewa tokea nipo sekondari Geb. Nina uzoefu nao.” “Mchezo gani!?” “Huo unaoufanya sasa hivi.” “Sio kama inavyoonekana!” Nanaa akacheka akafungua mlango akatoka.

“Nanaa! Naomba usiondoke.” Geb akakimbilia mbele yake, Nanaa akasimama. “Nakwenda shule Geb. Kitu ninachokifanya bila kuingiliwa na mtu, na ndio kitu pekee nilicho nauwezo wa kukitawala na kukiongoza. Namshukuru Mungu pia nina uwezo wa kukilinda. Hakuna mtu anaweza kuniingilia kwenye shule yangu. Nilazima niisome na nimalize. Haiuhusiani na mwanaume yeyote wala hisia zangu. Ni moja ya kitu ambacho nilazima nimalize.” “Nanaa!” “Mbona sikuelewi Geb!? Nini?” Akampita pembeni na kuanza kuondoka akielekea getini.

“Sio kama inavyoonekana, naomba usiondoke.” Nana akamgeukia Geb akasimama vizuri.  “Katika kumbukumbu zako, mara ya kwanza kulala na mimi ulinikuta bikra?” Geb kimya. “Basi walipita wenzako kama wewe, wengine wenye stori kama zako. Wewe sio wa kwanza. Kwa kusema hivi, namaanisha nina uzoefu wa hizi habari. Najua utaanzia wapi na kuishia wapi, ili kunidanganya. Usifikiri umeniumiza Geb, hata kidogo. Wewe ni ukurasa niliousoma, nimeuelewa, nakufunika, naendelea na maisha yangu.” Ni kama alimfunga Geb mdomo. Akashindwa ajitetee vipi.

Ila akajikaza kuuliza.“Kwa hiyo unatupilia mbali kila kitu?” Nanaa akakunja uso. “Ni nini chakutunza kati yetu? Eti Geb? Nini cha kuweka kumbukumbu? Kama ni mapenzi tulifanya na wewe kama nilivyofanya na wanaume wengine. Uliridhika na mimi nikaridhika. Sasa hivi unaendelea na mwanamke wako na mimi ipo siku nitapata mwingine, nitaendelea. Tatizo liko wapi? Hunidai, sikudai. Nakuruhusu endelea na maisha yako kwa amani, na mimi naendelea na maisha yangu. Nakushukuru kwa kuniweka nyumbani kwako kwa muda niliohitaji msaada, basi. SITAKI unitafute, na mimi sitakutafuta.” Geb akabaki kimya, haamini.

“Huna tofauti na matapeli wengine wote niliokutana nao maishani mwangu. Tofauti yako wewe ni pesa tu basi. Labda na good sex. But am sure, one day I will find the BEST one.” “Kwa hiyo hutaki nikutafute tena?” “Kwa nini unitafute!? Na usifikiri naongea kwa hasira Geb. Nilitoka kwa Jamal kama hivi ninavyotoka kwako. Nilikusanya vitu vyangu, nikaondoka bila ugomvi wala maneno mengi, maisha yakaendelea. Nilimuacha na mkewe, na wewe nakuacha na mwanamke wako. Nikarudi chuoni nikatuliza mawazo, nikasoma na nikamaliza mwaka wa pili. Ndio na wewe hivyo hivyo. Naomba uniache nikaendelee na maisha yangu. Hutaniumiza kichwa wala roho yangu.”  Nanaa akageuka, kama utani akaondoka. Geb hakuamini.

~~~~~~~~~~~~~

Alitegemea fujo na kelele. Kulia na lawama, lakini Nanaa alitoka akionyesha amemdharau na kama hakuwa na hisia zozote juu yake, kitu kilichomuuma sana Geb. “Yaani Nanaa alikuwa akinitumia tu? Hakuwa na hisia zozote kwangu!?” Geb alibaki akiwaza kwa kuumia sana utafikiri yeye ndio amemfumania. Alirudi ndani akajikuta anapitiliza jikoni badala yakurudi chumbani alipomuacha Liz. Asijue anafuata nini huko. Akavuta kiti na kukaa hukohuko jikoni. Akiwa amezama mawazoni wala asijue anayeingia na kutoka, akasikia sauti ya Grace. “Naomba ukavae nguo Liz. Danny yupo hapo nje anaingia sasa hivi na mtoto. Tafadhali sana.” “Namtafuta Geb.” “Basi kavae nguo ndio utoke. Huwezi kujiacha uchi mbele ya mume wangu! Hapo tutakosana! Tafadhali sana.” Geb akatoka.

 “Naomba uondoke Liz.” Geb alikuwa amekasirika sana. Hata Grace alimuona usoni. “Wewe Geb vipi?” Liz akajilalamisha, hakutaka kuondoka. “Geb na Liz, wote mpo uchi. Fili na Danny wanaingia sasa hivi. Naomba muingie chumbani kwenu. Tafadhali sana.” “Sio chumbani kwetu. Ni chumbani kwangu.” “Sijali utakavyopaita, naomba ingia ndani. Fili hawezi kukuta hapo na boxer.” Grace akambadilikia hata kaka yake. Geb akaondoka kuingia chumbani kwake, Liz akafuata.

Maisha Ya Nanaa Shule Na Ujauzito.

Ni kweli kwa Jamal aliondoka na maisha yakaendelea, lakini sio safari hii, alipokuwa na mtoto wa Geb tumboni. Siku zilizidi kwenda, akijaribu kujiliwaza, lakini yule mtoto naye alizidi kumkumbusha ukurasa aliotaka kuufunga. Ulikuwa haufungiki. Kila akicheza, alimkumbusha yeye yupo, na ni mtoto wa Geb. Mwanaume aliyeacha historia kubwa sana ya mapenzi mwili mwake, tofauti na wanaume wengine wote. Hakuna siku Geb alishika mwili huo asimridhishe Nanaa visivyo vya kawaida. Iwe ni katikati ya usiku akiwa amelala, au siku zile alizomwingilia chumbani kabla hata hajalala. Geb aliutendea haki mwili wake.

Ndiye mwanaume aliyemuonyesha anahitaji mwili wake visivyo vya kawaida na kuuthamini. Alimuonyesha mwilini mwake ndiko anapopata starehe aliyokuwa hata hatarajii! Mambo mengi aliyasimamisha ili tu kwenda kufaidi mwili huo.

Ndoto akiwa amelala na Geb nazo hazikukawia. Mara nyingi aliota Geb yupo akichezea kifua chake, au akichora mgongo wake, huku akimbusu mara kadhaa. Mabusu ya shingoni ndiyo yalikuwa yakimsisimua na kumtoa usingizini. Alikuwa akishituka na kukaa kitandani kwake, nakubaki akiwaza.

~~~~~~~~~~~~~

Hakutaka kuanza kliniki mapema, mpaka alipomsikia mtoto wake alipoanza kucheza tumboni, ndipo alipojua nilazima aanze kliniki. Alianza kliniki katika hospitali ya taifa ya Muhimbili na huku akipambana na masomo. Mimba haikumsumbua sana ila upungufu wa damu ndio likawa tatizo kubwa la kumsumbua yeye, lakini si mtoto. Mtoto alikuwa akikua salama bila shida. Akashauriwa na daktari wake huko kliniki kuongeza kula vyakula vyakuongeza damu na kunywa bila kukosa vidonge vya kuongeza damu.

Hilo likamtia hofu na kumuongeza umakini. Hakutaka aje afe amuaache mtoto wake kama yeye alivyoachwa na mama yake. Akaweka juhudi za makusudi kujitunza vizuri bila kupuuzia dalili yoyote anayoona ni hatarishi kwake.

Akajitahidi kuweka mazoea na huyo daktari anayemuona kwa kliniki kwa makusudi ili tu awe msaada. Alimuelezea historia ya maisha yake. Vile alivyozaliwa bila kukutana na mama yake. Maisha ya upweke anayopambana nayo, akamsihi huyo daktari amsaidie bila kumpuuza. Huruma ikamuingia huyo daktari, akawa akimfuatilia kwa karibu kama mtu anayemuhusu haswa, ili kuhakikisha anabeba hiyo mimba na kujifungua salama.

Na yeye akaweka juhudi ya kula vizuri kutokana na uwezo wake, na kuendelea kufuata ushauri wa huyo daktari. Kila wazo aliloona litamuharibia mudi yake, au kumchafua moyo, alijitahidi kuliepuka ilimradi tu kujituliza.

~~~~~~~~~~~~~

Kila James alipomtaka wakutane, alimkwepa. Wakati mwingine James alitaka kumtoa kwa ajili ya chakula cha mchana au kumpa ofa ya kutaka kumnunulia gauni au kiatu. Tena wakati mwingine James alimpigia akiwa amejawa furaha. “Leo nina pesa Nanaa. Pesa ya kufa mtu. Twende ukapate hata kiatu tu!” Nanaa alikuwa akicheka tu. Akitamania kukutana na kaka yake lakini hakutaka kabisa amgundue kuwa ni mjamzito. Akazidi kumkwepa kwa maneno ya busara na kumuaminisha shule ndio kipingamizi. “Ni miezi kama 6 tu imebaki kaka yangu. Naomba nijikaze hii shule iishe. Ikiisha tutakuwa wote. Mungu ni mwema atajalia.” Hiyo ndio kauli kwa kaka yake.

Kwa hiyo kila alipokuwa akimpigia simu labda akitaka kumtoa au amtembelee, alimtajia muda uliobaki. “Imebaki miezi miwili tu kaka yangu, hii shule iishe. Acha nikazane. Hata mimi nina hamu ya kutoka. Lakini siku 60 sio nyingi.” Alikuwa akiweka hiyo line yenye namba ya simu mara moja moja sana akitaka kuzungumza na kaka yake tu, na kila alipomaliza kuzungumza naye, alitoa hiyo namba na kuweka namba mpya ambayo hata James hakuwa akiifahamu. James aliendelea kumtunza dada yake. Alimtumia pesa kila mara, na kwa kuwa Nanaa alifanya kazi ofisini kwa kina Grace, alikuwa na akiba iliyomfanya aishi maisha ya kawaida tu bila shida yeyote.

 Na Walimwengu Hawakosi Yao.

Maisha yakaendelea, tumbo likawa bayana. Kila mtu aliyemuona alijua ni mjamzito, lakini hakuonyesha wasiwasi hata kidogo. Hata rafiki zake walipomuuliza baba wa mtoto wake, jibu lake lilikuwa moja tu, “Mama yake ndio mimi.” Wakajua safari hii kwa hakika Nanaa amepatikana. Ameachwa kama walivyozoea kumuona akiachwa, ila safari hii ameachwa na mtoto juu.

Kwa kuwa hakuwa akienda popote hata siku za likizo, kwa hiyo wakawa wakiambiana amefukuzwa hata kwa kaka yake sababu ya ile mimba. Walio mcheka walimcheka, na kumsema. Alijua lakini hakujali. Alijitahidi kuweka mawazo yake shuleni tu bila hata kuweka wasiwasi wa kuwaza pakwenda mara baada yakujifungua. “Kila kitu nitakijua mbele ya safari.” Nanaa alikuwa akijiambia hivyo.

~~~~~~~~~~~~~

Penzi la Zena na Yasini lilikolea. Yasini alikuwa akimtunza vizuri sana Zena. Akapendeza. Zena alijawa na furaha. Kila walipokuwa pamoja, Tia na Nanaa, Zena hakuacha kueleza uzuri wa Yasini. Alipendeza akawa mtu wa vipya kila wakati. Kama sio nguo mpya basi Zena alirudi na viatu vipya au pafyumu, chochote kile kizuri ambacho lazima awaambie vile Yasini anavyomjali yeye. Yale maisha ya Nanaa aliyokuwa akiishi wakati wapo na Jamal, kuondoka ijumaa na kurudi jumatatu akayaanza kuyaishi Zena. Tena hakuondoka kimya kimya. Alikuwa akiaga darasani kwenye kipindi cha mwisho. Nanaa alikuwa akimsikia akisema kwa sauti tu. “Jamani eeeh! Naenda kulea penzi. Naona na mume anasubiri nje. Hapa tena ni mpaka jumatatuuuu!” Basi hapo Zena atasimama kwa mikogo na kutoka.

Tia na Evan nao pia penzi likawa lakaribu. Evan alishamaliza shule yake huko mjini Morogoro akawa yupo jijini. Kwa hiyo kutoana kwa chakula cha mchana siku za weekend likawa jambo la kawaida kwao. Kutoka asubuhi siku za jumamosi na kurudi usiku au hata kesho yake wakichukua chumba nyumba za kulala wageni, likawa jambo la kawaida tu kwao.

Kwa kuwa mashoga hao wote walikuwa na wapenzi, ikabidi Yasini na Evan wafahamiane. Kwa hiyo wakati mwingine walitoka kama couple. Nanaa akaachwa na tumbo lake. Hata alipokuwa akikaribishwa, alikuwa akikataa. Wakajua anajificha sababu ya kupewa mimba. Tia alikuwa akimcheka anapokuwa na Zena.

“Alivyokuwa akimringia Terry vile! Lazima ajifiche.” Tia aliongeza kwa Zena. “Wewe hukumuona alivyokuwa akimringia Jeff. Jeff hakutaka kuzungushana naye, akatafuta mwanamke mwingine. Tulipoenda Kigamboni kwenye birthday ya Yasini, bwana Jeff mtoto wa mjini alimfanyia shoo hiyo! Asikwambie mtu Tia. Ilikuwa shoo yakufunga mwaka. Mbona aliaga!” Zena alimsengenya. Wala asisimulie msaada aliopewa wakati mgonjwa. Ushoga na Tia ukarudi kunoga zaidi, Nanaa hakumtaka tena. “Ulinisimulia! Acha ajifungie. Sura ile ataficha wapi? Alitingisha wanaume, sasa hivi kachina!” “Bi dada hata kwa kaka yake kafukuzwa.” Waliendelea kucheka.

“Unafanya mchezo na wanaume wa mjini?” “Lakini sasa hivi atakuwa anajuta. Jeff alitaka kumuoa ki ukweli. Akamringia! Sasa ona yaliyompata. Anazunguka na tumbo lisilo na baba.” Wakacheka. “Ujue hata likizo haendi mahali?” “Kweli!?” Zena akashangaa. “Kweli tena. Alibaki hapa hapa chuoni.” Wasijue Nanaa alikuwa katikati ya kundi lililokuwepo pembeni yao wakijisomea. Na wao walikuwa wamekaa wawili tu chini ya mti huo mkubwa wakipena habari za weekend iliyopita. Watu wote waliokuwa wakisoma na Nanaa walikuwa wakisikiliza jinsi Zena na Tia wanavyomsema rafiki yao. Nanaa akacheka tu, akanyamaza. Walimsengenya mpaka wakachoka. Hawakusoma kitu chochote pale, wakaondoka wakicheka na kupongezana.

~~~~~~~~~~~~~

Hakuacha kwenda kliniki. Tena bila kukosa. Alitaka kujua maendeleo yake na ya mtoto wake huyo waliyekuwa wakizungumza kila wakati. Alimgeuza kuwa ndiye rafiki yake wakaribu. Kucheka na kumuongelesha kwa kila jambo.

 Wasiwasi ulimwingia pale alipopewa tarehe ambazo anatakiwa ajifungue. Zilikuwa zikiendana kabisa na tarehe zake zakuanza mitihani yake yakumaliza chuo kikuu. Akabaki kumuomba Mungu utokee muujiza apitilize siku zake zakujifungua ili ajifungue akiwa ameshamaliza chuo. “Inabidi upunguze shuguli humo ndani ili ukae mpaka nimalize mitihani. Umesikia? Ukija sasa hivi, mama atakuwa na mambo mengi hatutapata muda wa pamoja. Umesikia kipenzi cha Nanaa?” Nanaa alikuwa akiongea na mwanae kila akimsikia akizunguka tumboni. Alilishika tumbo lake na kulipapasa kama anampapasa mtoto wake. Jina kubwa alilokuwa akimwita huyo mtoto ni kipenzi cha Nanaa.

Kila alipoamka, alishika tumbo lake kwa upendo nakuzungumza na mwanae. “Umeamka salama kipenzi cha Nanaa?” Alimuuliza mwanae. “Amka umsalimie mama, basi.” Atapiga piga tumbo lake taratibu huku akizungumza na mtoto wake mpaka mwanae acheze huko tumboni ndipo afurahi. Atamwambia mipango yake yote ya siku hiyo. Wapi watakwenda na nini watafanya ndipo atoke kitandani. Hivyo hivyo ikifika usiku wakati analala. Atampa pole ya mahangaiko ya siku hiyo. Mafanikio yake kwa siku hiyo na changamoto zinazomkabili. Basi atazungumza na huyo mtoto hapo mpaka wanalala.

Ujauzito huo ukawa faraja tofauti na wenzie walivyofikiria. Wakati wao wakimcheka, Nanaa alikuwa amepata rafiki mzuri kuliko wao. Rafiki huyu hawakuwa wakigombana kwa lolote. Alimsikiliza kila wakati na kuongozana naye kila mahali. Hata akisikia kiu ya maji, basi atamwambia mwane huko tumboni. Akichoka au akisikia usingizi pia, atamshirikisha mwanae. Hakukosa kitu cha kuzungumza na huyo mtoto.

Miezi 9 Ya Mimba Ya Nanaa.

Miezi tisa ikatimia na mitihani ikawa imefika. Nanaa alikuwa amejiandaa vizuri tu na mitihani yake, hakuwa na wasiwasi. Kwa kuwa hakuwa na mtu wakumfikiria ila yeye na mtoto aliyekuwepo tumboni, basi alisoma vizuri bila shida. Msichana aliyekuwa naye chumba kimoja, alikuwa ametulia sana. Alikuwa ni dada aliyekuwa ameolewa, lakini hakuwahi kupata watoto. Alimuacha mumewe mkoani Lindi, akaja chuoni hapo kujiendeleza. Alikuwa akimsaidia sana Nanaa. Alishazoea mazungumzo ya Nanaa na mwanae hapo chumbani. Si asubuhi si jioni alikuwa akimsikiliza Nanaa akiongea na mwanae nakuishia kucheka tu.

Alishanunua vitu vyote anavyohitaji siku ya kujifungua na begi la mtoto wake lilikuwa tayari. Furaha ilimjia pale alipoenda kliniki akaambiwa mtoto wake yupo salama. Japokuwa siku za kujifungua zilikuwa zimetimia, lakini walipompima wakakuta  njia bado haijafunguka. Aliambiwa ni kitu cha kawaida kwa kuwa alikuwa ni mtoto wake wa kwanza. Alimshukuru sana Mungu. “Ukae humo humo ndani mpaka mama amalize mitihani. Sawa eeh!” Nanaa hakuacha kumsisitiza mtoto wake kila alipomsikia anazunguka nakumletea vichomi.

“Kwanza huko ndio utakuwa salama. Unakuwa na mama kila wakati na kila mahali. Hakuna kutengana. Usishawishike kutoka huko.” Nanaa alikuwa anamsisitiza mwanae kila wakati. “Nitakupenda sana mwanangu. Mimi ndio nitakuwa rafiki yako wa kwanza hapa duniani. Tulia tumuombe Mungu atujalie sote maisha marefu. Tuje tuonane, nikulee mimi mwenyewe.” Basi hapo Nanaa huanza kuomba na mwanae huku ameshika tumbo akilipapasa.

~~~~~~~~~~~~~

Roho ya umama nayo haikukawia. Hakuacha kumuombea na kumtabiria mambo mengi mazuri. “Uwe na akili kama za dad. Uwe mpole na hekima kama anti Grace. Usikubali nywele zangu. Nina kipilipili kibaya sana. Utanilaumu maisha.” Hapo Nanaa ataanza kucheka naye. Na kama ukimkuta, basi ungedhani anazungumza na mtu. Hata akisoma, atamuelezea anachosoma. Kama nikigumu atamlalamikia. Kama ni kitu anachokipenda atamuelezea hicho kitu. Na wakati wote alipotaka kuingiza kitu kichwani kikae, alimshirikisha mwanae. “Lazima umsaidie mama kukumbuka kwenye mtihani.” Basi hapo atasoma kwa sauti, huku akimuelezea mwanae. “Umeelewa lakini?” Atamuuliza.

Mara nyingi alitamani kumuona mtoto wake. Alikuwa na wasiwasi naye. Jinsi atakavyokuwa baada ya yeye kunywa madawa yote yale makali wakati mgonjwa. “Hata ukiwa vipi, bado utakuwa ni mwanangu tu. Nitakupenda sana. Unajua sifa yako kubwa?” Nanaa alimuuliza mtoto wake. “Wewe ni jasiri kama simba. Upo kama mti wa mzeituni. Unamea jangwani. Umeweza kushinda mauti! Basi wewe huwezi kushindwa na  changamoto za haya maisha. Mungu alikutuma kwangu kwa makusudi. Wewe ni faraja yangu.” Nanaa hakuacha kumsifia mwanae.

~~~~~~~~~~~~~

Week inayofuata Nanaa akaanza mitihani. Aliingia kwenye mtihani wake wa kwanza, ilikuwa asubuhi akatoka bila shida ila kiuna kilianza kumuuma. Akajiambia kwa kuwa ni miezi tisa na ametoka kwenye mtihani mgumu labda ndio sababu. Akaamua kurudi chumbani kwenda kulala. Alikuwa amepata chumba kilichopo gorofa ya juu kabisa, kwa hiyo mazoezi yake yalikuwa yakupanda ngazi hizo kila siku kama alivyoshauriwa. Wakati amemaliza ngazi zote anataka kuingia chumbani kwake, chupa ikapasuka.

~~~~~~~~~~~~~

Karibu Na Ukingoni Mwa Mkakati wake wa SHULE, Ambao Haukuwahi Kuruhusu Ivunjike Au Ibadilike, Mtoto Anakuja. Hana Mtu Wa Karibu Wa Kumsaidia Kwa Wakati Huo.

Ni Nini Atafanya ? Nini Kitaendelea?

Usikose Muendelezo.

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment