Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu Ya 26. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu Ya 26.

Nanaa akaendelea na kazi zake kama kawaida. Huwa kama Grace ndiye anayewahi kumchukua mtoto shule,  anawahi kutoka kidogo kwa ajili ya kuwahi foleni. Ili saa 11:30 jioni awe shuleni kwa kina Fili. Akaingia ofisini kwa Nanaa. “Unataka tuondoke wote? Naona mvua inataka kuanza kunyesha tena kama jana.” Nanaa akafikiria. “Kuna kitu nataka kumalizia. Halafu bado namsubiria dereva.” “Na kweli! Asilale na pesa. Lakini jitahidi akija tu, uwahi nyumbani.” “Sawa.” Grace akatoka.

Grace kwa Nana.

Baada ya muda kidogo akarudi tena. “Umesahau nini?” Nanaa akamuuliza. Akaingia ofisini hapo, akafunga mlango kwa nyuma. “Nataka kukwambia kitu.” Nanaa akajiweka sawa. Grace hakuwa muongeaji. Kwa hiyo akitaka kukusemesha kitu, nilazima utataka kumsikiliza tu. “Mimi ninavyojua. Naweza nikawa sipo sahihi. Lakini hata mama alinifundisha hivyo. Kuwa ili mahusiano yeyote yafanikiwe, yanahitaji juhudi za makusudi, za pande zote. Mama aliniambia kuna wakati inabidi kukana hisia za wakati huo ili kuwepo kwenye mahusiano ya aina yeyote yale. Hisia zina mtindo wa kudanganya Nanaa. Kuna wakati unaamka upo na furaha sana. Wakati mwingine hutaki hata mtu akuongeleshe. Na sio kwa kuwa unaumwa au mtu amekukosea, ni basi tu, hisia zinakuwa hivyo. Zina mtindo wa kubadilika badilika.” “Sasa unafanyaje?” Nanaa akauliza.

“Hakikisha unajua nini unataka. Nakuanza kukitendea kazi bila kufuatisha hisia. Ukisoma kwenye bibilia. Kitabu cha {waebrania12:2}, neno linaonyesha vile Yesu alivyostahimili mateso ya msalaba na aibu, lakini ni kwa sababu tu alijua mwisho, tokea mwanzo. Au niseme alijua mwisho wa shida yote hiyo ni nini atapata. Alijua lazima atembee kwenye mapito fulani ili kufikia heshima aliyonayo sasa na milele. Kama asingevumilia yote yale, inamaana leo asingepata heshima yote aliyo nayo. Asingewekwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu baba. Amepingwa na anaendelea kupingwa mpaka leo, lakini hajawahi kuchuja. Unafikiri kwa nini?” Nanaa akatulia.

“Alijua ni nini anataka. Akajua faida zake, ndipo akakubali kulipa garama. Akatembea kwenye hatua zote alizopitia mpaka kushinda. Haikuwa rahisi hata kidogo. Unakumbuka kabla ya mateso alilia pale bustanini akitaka Mungu amsaidie? Aliingiwa na hofu Nanaa. Sio rahisi kama watu wanavyodhania. Hakuna kitu kizuri ambacho ni rahisi kupata. Zipo garama za kulipa. Unamuona Yesu jinsi alivyokubali kutembea kwenye hatua za mateso? Mimi na wewe tungeweza kufikiri kuwa kipindi kile cha mateso makali ndipo kipindi ambacho Mungu angetakiwa kutembea naye. Au hata kutuma faraja. Lakini Yesu aliteseka yeye peke yake. Mpaka msalabani. Mbaya zaidi alijua yupo peke yake. Akamuhoji hata Mungu akiwa msalabani. Akilia ‘Mungu wangu Mungu wangu, mbona umeniacha!?’ Aliumia. Alisikia hali ya upweke. Lakini alihakikisha anamaliza.” Nanaa akaanza kutokwa na machozi.

“Kuna mapito mengine ni yako peke yako Nanaa. Hakuna mtu wala kiumbe mwingine anaweza kukuelewa unakopitia. Unaweza kuja kujikuta wakati mwingine upo peke yako maishani. Ukiwa umezungukwa na watu ambao ungedhani wanatakiwa kukusaidia, lakini wasikusaidie. Lakini utakata tamaa na kutupa kila kitu chini? Hapana Nanaa! Lazima kuendelea.” Grace akaendelea.

“Pambana bila kuchoka kuhakikisha unapata kile unachotaka na kujua ni chako. Usikimbie. Na wala usidhani yupo mtu atakusaidia! Wewe ndio unawajibika kwa Nanaa. Wewe ndio utampa Nanaa kile anachotaka. Na si vinginevyo. Usikubali kushindwa. Usikubali hisia zikakukosesha vitu vizuri. Usikubali hisia zikakurudisha au kukushikilia kwa muda mrefu. Umeelewa Nanaa mdogo wangu?” Nanaa akafuta machozi.

“Nimeelewa, lakini Geb ameniumiza Grace! Hajanithamini. Amenipuuza mbele ya Rita.” “Mimi sitaki kujua alichofanya Geb. Nataka kujua ulichofanya wewe. Wewe ulifanya nini Nanaa?” “Ningefanyaje Grace?”  “Kweli Nanaa!? Yaani unatoka na mtu wako. Anakutana na msichana mwingine, wewe umesimama tu! Haya, mnaondoka pale, njia nzima upo naye, kimya!? Asubuhi yake ulinitafuta mimi na mama, kwa nini hukumtafuta Geb kujua kilichoendelea? Mama aliniambia hakuna atakayeweza kumlinda Danny, ila mimi mwenyewe. Ni kweli Nanaa. Kama kweli unampenda Geb, na unataka awe wako, ujue unalazimika kumlinda mwenzio. Hakuna atakayekulindia Geb, ila wewe mwenyewe.” Vikaanza kumuingia Nanaa. Akakumbuka stori aliyosimuliwa na mama G, kuhusu Danny na Viola. Alijua lakini akamuacha Grace ashugulike na ndoa yake.

“Mtu anaweza asikwambie hili. Ila mimi nipo kwenye mahusiano ya ndoa, nakwambia ukweli Nanaa, kwa upande wako ulikosea mdogo wangu. Mimi sitazungumzia upande wa Geb, kwa kuwa Mungu ameshazungumza naye. Na amejifunza kivyake. Lakini na wewe Nanaa, umekosea. Na umeshindwa kulinda kilicho chako. Tokea mwanzo kabisa, umeruhusu hisia za wivu kukufunika mawazo yako na kushindwa kufikiria kwa haraka. Mimi si muongeaji kama unavyonijua. Lakini Danny hatoki kitandani kwangu bila kumshika mikono na kumuombea. Tena namuombea kwa sauti ili ajue kilio changu kwa Mungu. Ndio maana unamuona Danny yuko vile kama mwehu kwangu.” Nanaa akacheka huku ameinama nakufuta machozi.

“Mama alinifundisha kumlinda mume wangu. Tena alinikatalia kabisa eti kuja kuanza kuniambia habari za Danny za mtaani. Akaniambia nikizubaa, wengine watamchukua. Usifikiri hapati vishawishi! Yeye ni binadamu kama binadamu wengine tu, tena sasa hivi anapesa sana. Wanawake wengi wazuri na wadogo kuliko mimi wanamtongoza kweli, Danny wangu. Lakini namuombea Mungu amsaidie avishinde vishawishi na mimi nikijitahidi kwa upande wangu, kwa kila namna ili tu kumfanya asiingie vishawishini. Umenielewa?” “Nimeelewa Grace. Asante sana. Nakushukuru. Nilihitaji kusikia hivyo. Asante.” Nanaa akaona upande mwingine wa Grace. Grace akaondoka.

Kusamehe Ni Rahisi Kuliko Hasira.

Alimuacha Nanaa akiwaza na kujutia. Akabaki akiendelea kuweka mambo ya pale ofisini sawa. Alikuwa akifanya kazi, lakini akiendelea kukusanya taarifa ambazo alijua zingemsaidia kwenye kuandika ripoti yake ya chuo. Kwa hiyo alifanya vitu viwili kwa wakati mmoja. Akiwa amezama kwenye kazi, mlango ukafunguliwa. Alikuwa Geb. Nanaa akajiweka sawa. “Pole na kazi.” “Asante, na wewe.” “Asante.” Geb akavuta kiti akakaa.

“Vipi?” Geb akamuuliza. “Namsubiria dereva. Alikuwa Kariakoo, amesema kama baada ya nusu saa atakuwa amefika. Anapesa baadhi, nataka nizipokee kwanza ndipo nifunge mahesabu ya leo.” “Itamsaidia kumtoa kwenye vishawishi.” Geb akaongeza. “Vipi na wewe? Ulirudi kazini?” Nanaa akauliza nakumfanya Geb azidi kutulia maana ni kama amebadilika tofauti na walivyoachana mara ya mwisho alipokuwepo hapo.

“Yeah! Kuna mambo nilitaka kuyaweka sawa. Hii week sijafanya kazi vizuri. Nimekuwa nusu nusu.” “Pole.” “Asante. Na kesho nataka kusafiri.” “Unakwenda wapi?” Nanaa akauliza tena. “Morogoro. Kuna kazi ya kukamilisha siku ya jumamosi.” “Oooh! Ungekuwa unaondoka jioni, ningekusindikiza.” Geb akatabasamu kama haamini.

“Kweli ningekusindikiza ili usiwe peke yako njiani.” “Hata hivyo nitaondoka jioni sana, baada ya kutoka kazini.” Nanaa akanyamaza kwa muda kama anayefikiria. Geb akamsogelea, akamvuta mkono. “Samahani Nanaa. Naomba usinichukie.” Nanaa akakumbuka maneno ya Grace, akajishusha. “Na mimi naomba unisamehe Geb. Najua kuna nilipozembea mpaka ukaingia matatizoni.” Geb hakuamini.

“Asante Nanaa. Nakushukuru sana. Najua ni ngumu kusahau, lakini nakuhakikishia nimejifunza sana tu. Niamini haitakaa ikatokea tena.” “Na mimi nakuahidi tena nitakulinda Geb. Nitakuwa mlinzi wako.” Geb alihisi yupo ndotoni. Hakuamini. “Asante Nanaa. Asante sana.” Maagano hayo yakasindikizwa na mabusu.

Alivuta kiti chake karibu na Nanaa, akaanza kumbusu. Akaona yupo mbali zaidi, akamtoa pale kwenye kile kiti, akampakata kwenye kiti chake. Akamkumbatia huku akinyonya midomo ya Nanaa bila kupumzika. Alimpapasa kwa kadiri ya uwezo wake huku akinyonya midomo yake kwa nguvu zote. Alimpapasa kama kutoa hofu ya kuachwa ndani yake mwenyewe Geb. Hakuwa akiamini kama amepata hiyo nafasi tena. Alifukuzwa masaa machache sana hapo hapo ofisini. Safari hii anapewa ahadi ya kulindwa! Hakuna jinsi Geb angeachia mwili huo kwa haraka na nafsi ikaridhika.

Akaendelea kumpapasa kwa nguvu huku akimvutia mwilini kwake. Tayari hali ya Nanaa ilishabadilika. Alikuwa akitoa mihemo ya huba huku mikono yote ipo nyuma ya kichwa cha Geb aliyekuwa amempakata. Waliendelea kupeana mabusu ya haja, bila kuchoka. Mabusu hayo yalisindikizwa na msamaha, majuto na ahadi ya penzi la kweli kati yao.

Dereva aliingia akakuta wapo katikati ya ile hali. Geb amempakata Nanaa, huku mikono yake imemshikilia kwa nguvu akinyonya midomo yake. Nanaa alishituka, akataka kusimama, lakini Geb akamng’ang’ania kama kumvuta asiondoke. Akambusu kama sekunde 30 mbele ndipo akamuachia huku akihema. Nanaa akasimama, Geb naye akasimama kwa haraka. Akamvutia tena karibu yake zaidi, akamkumbatia kwa kupitisha mikono yake yote miwili mwilini kwa Nanaa. Dereva alishatoka.

Akarudia kumnyonya tena midomo yake huku akimpapasa kwa uchu. Nanaa alishapotelea hapo mikononi, hajiwezi. Akahamia shingoni kitu kilichomchanganya zaidi Nanaa na kutamani amalize kila kitu hata kwa chuma mboga ya haraharaka tu. Lakini Geb si wa papara. Jinsi alivyokuwa akinyonya hiyo shingo yake, kana kwamba anao muda wote ulimwenguni, asijue ndio anamaliza nguvu zote za Nanaa.

Geb aliendelea tena na tena, akarudi midomoni. Akapata ulimi kwa muda, kisha akambusu nje ya midomo yake kama mara tatu ndipo akamuachia. Akabaki amemkumbatia huku anahema mpaka alipotulia na kurudia hali yake. Maana hata Nanaa alimuona alishakuwa juu sana. Alijaribu kutulia huku amemkumbatia Nanaa na amefunga macho. Alimsikia akivuta pumzi mara kadhaa na kuzishusha taratibu. Kisha akamuachia. Geb akatoka, dereva akaingia.

~~~~~~~~~~~

Yule dereva aliweka pesa juu ya meza, akaondoka bila kusema chochote. Hakuwa amewafumania. Aliwakuta! Na ni kama Geb alitaka aelewe hivyo, na ni kama alimfikishia ujumbe. Hakuwa akiiba. Nanaa ni wake. Nanaa hakutegemea. Alijua labda Geb angemuachia kwa haraka sana baada ya yule dereva kuingia, lakini alionyesha wazi yeye ndio anatakiwa apishe. Kwani ameingilia. Akajisikia vizuri, akabaki akicheka moyoni kuona Geb anamtangaza ni wake.

~~~~~~~~~~~

Muda mfupi tu baada ya dereva kutoka, Geb akarudi pale ofisini. “Twende tukajiandae na safari ya kesho. Nitakuleta kazini kama kawaida, lakini mizigo yako utaacha kwenye gari. Nikitoka kazini nitakufuata ndipo tutaelekea Morogoro.” “Sawa. Nisubiri basi nimalizie hapa.” Nanaa akahesabu zile pesa mbele ya Geb. Akamtajia kiasi alichokuta, kwa kuwa dereva aliziweka tu akatoka. Kisha akaandika kila kitu, nakufunga mahesabu ya siku ile. Wakatoka.

~~~~~~~~~~~

Walipopanda tu kwenye gari Nanaa akaita. “Geb!” Geb akamgeukia. “Kuna kitu nataka kukwambia.” Geb akaogopa kidogo. “Nini tena!?” “Mwenzio nakupenda.” Nanaa aliongea kwa upole huku midomo ikimcheza kama anayeongea kwa hofu. “Nakupenda.” Akarudia tena. “Asante Nanaa. Tutapata muda mzuri sana tukiwa Morogoro.” Hilo ndilo aliloweza kujibu Geb. Aliogopa kuongeza chochote kwani ahadi zote alizoahidi siku chache zilizopita aliharibu kama Nanaa alivyomshutumu. Akaamua safari hii iwe ni vitendo tu.

Nanaa akabaki akifikiria. “Vipi? Umebadili mawazo ya kwenda na mimi?” “Hapana. Nafikiria sehemu ya kubebea vitu vyangu vya kusafiria. Unakumbuka kile kibegi nilisafiri nacho kwenda Marangu?” “Nakumbuka.” “Alinipa kaka. Lilichanika na kuharibika zipu. Sina sehemu ya kuhifadhia vitu vyangu kama tukisafiri kesho.” “Tupite madukani tukaangalie.” “Lakini naomba tusiende kwenye yale maduka yako Geb. Sina pesa nyingi.” Geb akacheka.

“Kwanza vuta huo mfuko hapo kwenye kiti cha nyuma. Ni wako huo.” Nanaa akageuka. Akakuta mfuko mkubwa nyuma ya kiti cha dereva. Akajaribu kunyanyua. Ulikuwa mzito kidogo. Akaongeza nguvu, akavuta akaupakata na kuanza kufungua kuangalia ndani. Kwanza akakutana na boksi la simu. Mikono ikaanza kutetemeka na kutoa jasho. Geb akamuona anatoa mikono ndani ya ule mfuko akajifuta jasho kwenye gauni lake, kisha akarudisha ndani akanyanyua kile kiboksi cha simu. Akafungua huku akitetemeka. Akakuta ni simu iPhone iliyokuwa imeingia wakati huo. Mpyaa! Akameza mate.

Akamwangalia Geb. “Umeipenda?” Akamuuliza. Nanaa akatingisha kichwa kukubali kwa kuwa maneno yaligoma kutoka. Akabaki na kigugumizi. Mwishowe akajifunika uso wake kwa viganja viwili.  “Angalia na boksi la chini.” Nanaa hakufungua. Akabaki amejifunika analia kwa furaha. Geb akaondoka gari.

Baada ya kutulia. Akajifuta machozi, akatoa ile simu. Akaweka mapajani. Akafungua tena lile boksi. Alijua kwa hakika ni laptop. Akafungua huku akivuta kamasi. Alijifuta mara kadhaa machozi kwa kutumia mikono yake, ndipo akaweza kufungua lile boksi ambalo tayari taa za barabarani zilishamuonyesha picha ya laptop ya Apple MacBook Air nayo ndio ilikuwa toleo jipya la Apple. Nanaa hakuamini. Akafungua ndani huku machozi yakiendelea kumtoka. Akakutana na laptop yenyewe ikiwa na accessories zote. Akafunika kila kitu. Akarudisha kwenye ule mfuko, akageukia dirishani akaendelea kulia taratibu. Alishindwa hata kusema asante. Alijua wazi hastaili vitu vyote vile vya thamani. Kwanza hakuwahi kulipiwa garama kubwa ya kiasi kile. Aliyemuona akihangaika naye ni James. Tena na yeye alifanya pale alipoweza. Kwa kiwango cha chini sana kwa majukumu yaliyokuwa yakimkabili. Alijua wazi Geb ametumia milioni ya pesa kwa kumnunulia vile vitu viwili tu.

Alilia Nanaa, wala asijue wapi wanaenda na wapo wapi kwa wakati huo. Akahisi wamesimama. “Twende tukaangalie kama tutapata mabegi mazuri yakusafiria.” Geb akavunja ukimya mara baada ya kuegesha gari yake. “Usilie bwana Nanaa. Mimi nataka kukuona umefurahi.” Nanaa akainama akajifuta machozi. Akaweka vile vitu pembeni, akashuka. Geb akamfuata ule upande aliokuwepo. Akampa busu moja tu la mdomoni.

Akampangusa machozi. “Twende tuingie hapo ndani. Tunaweza kupata mabegi mazuri.” Nanaa akatingisha kichwa kukubali. Akarudia kumfuta tena machozi vizuri, akamshika mkono. Wakaingia ndani. Hakuwa ameegesha gari yake mbali na hapo dukani.

~~~~~~~~~~~

Lilikuwa duka la pochi na mabegi mazuri na yakaonyesha ni ya thamani kubwa. Nanaa akajua na hapo tena pesa nyingi itamtoka tena Geb. Akaanza kusoma bei. “Nanaa! Naomba angalia aina ya mabegi unayopenda. Acha kuangalia bei.” Geb akamsogelea baada ya kuona anahangaika kusoma bei zake. “Naona hapa ni garama zaidi, Geb. Twende kwengine.” Akamnong’oneza. “Nanaa!” “Kweli tena.” “Inamaana hakuna set yeyote uliyopenda hapa? Achilia mbali garama.” Yale mabegi yalikuwa yakiuzwa kwa sets 3 mpaka mengine seti 5. Yaliwekwa kwa pamoja, kuanzia kubwa kabisa, mpaka kibegi kidogo kabisa chakubebea vitu vidogo vidogo kama vipodozi.

“Niambie ni ipi angalau umependa.” Nanaa akasita. “Nanaa?” “Sijui!” “Najua unajua lakini unahofia bei. Hivi vitu ni kweli ni vya garama. Lakini vinadumu muda mrefu. Ukinunua mabegi kama hayo, utakaa nayo kwa muda mrefu sana bila uhitaji wa mabegi tena. Kuliko kununua kila mwaka mabegi ya bei ya chini. Sijui umenielewa?” “Nimeelewa.” “Basi muonyeshe huyo kijana, ni lipi umependa, utanikuta pale mbele.” Nanaa akaanza kuzunguka tena mle ndani.

Akaona ni heri achukue set ya masanduku. Akapata seti ya masanduku 5 yenye ukubwa mbali mbali akapenda. Kabla hajachukua akamuita Geb. “Najua unataka kunisaidia kununua. Lakini naomba nilipie haya hapa, niliyoyapenda. Ninazo pesa. Halafu kumbuka ulishaninunulia vitu vingi. Ni kama ulinunua mahitaji yangu yote ya....” Geb akambusu juu ya mdomo mara moja tu, kama kumtuliza. Nanaa akacheka.

“Naomba kanisubiri hapo nje.” Akatoka huku akicheka. Geb akamuomba yule kijana amtolee yale masanduku. Akaingia stoo, akatoka na aina kama ile ya yale masanduku aliyoyapenda Nanaa. Yalikuwa na muundo kama ya plastiki iliyopakwa rangi ya dhahabu, nzuri sana. Kona zake zilikuwa za chuma. Ni kweli pesa ilimtoka Geb. Akalipia na kutoka na yale masanduku. Akamkuta Nanaa ameinama nje ya gari yake.

Akayaingiza nyuma ya gari, akamfungulia mlango. “Sijui niseme nini Geb!” Nanaa akaanza kulia tena mara walipoingia tu ndani ya gari. “Asante.” “Naomba usifikirie kama unanifilisi au ndio unaniingiza garama kubwa sana. Naomba huko usifike tafadhali. Wewe furahia umepata vitu ulivyokuwa ukivihitaji. Ni vyako wala havihusiani na mahusiano yetu. Hesabu ni kama Mungu amekupa mahitaji yako. Katika ile orodha yako, ni kama tumemaliza kila kitu. Si ndiyo hivyo?” “Tumenunua kila kitu sasa hivi. Nakushukuru sana.” “Sasa nashauri usisubiri ikafikia orodha kubwa hivyo. Ukiwa na shida na kitu chochote kile, tafadhali niambie. Na wala usifikirie mara mbili. Sawa?” “Nakushukuru Geb.” “Najua. Lakini umesikia nilichokwambia?” “Ndiyo.” Nanaa akaitikia na kujifuta tena machozi.

“Lakini naomba unisubiri. Kuna kitu nataka nimnunulie mama.” “Nanaa!” “Sio pesa nyingi. Nimeona pochi pale ndani. Inamfanania mama kweli! Itatoshea bibilia yake wakati anaenda kanisani. Nisubiri nakuja sasa hivi.” Geb akacheka. Nanaa akashuka. Baada ya muda mfupi akarudi na mfuko. “Twende.” Geb akaondoa gari.

~~~~~~~~~~~

Walipofika nyumbani, Geb akateremka. “Nimekwama Geb. Nisaidie ili nishuke.” Geb akakimbilia upande aliokuwepo Nanaa. Akafungua mlango wake. Akainama ili kuangalia mkanda wa gari aliokuwa amejifunga. Akafungua, Nanaa akamvuta kwa nguvu na kuanza kumbusu yeye huku akimpapasa nyuma ya shingo yake. Yeye alikuwa amekaa ndani ya gari, Geb amesimama nje. Akaendelea kunyonya midomo yake kama alivyokuwa akimfanyia Geb bila papara.

Hakuchukua muda mrefu sana midomoni kwa Geb, akamuachia. “Asante Geb.” Akamshukuru. “Nakushukuru kwa kila kitu.” Akarudia tena kwa sauti tulivu huku bado amemshikilia. “Daah! Huu usiku utakuwa mrefu sana kwangu Nanaa.” Nanaa akacheka akiwa amemuelewa. “Natamani kesho tuwahi kuondoka mapema kidogo. Unafikiri ni sawa?” “Nitamwambia nini Grace? Nani atapokea pesa?” “Nitamuomba yeye abaki. Danny ataenda kumfuata mtoto. Nakuhitaji Nanaa. Nataka tukapate muda wa kutosha. Yaani huwezi amini Nanaa. Muda wote nilipokuwa rumande, nilikuwa nikikuwaza wewe tu.” Nanaa akamkumbatia.

“Hakika nakupenda Nanaa. Lakini ipo siku utaamini. Najua sasa hivi ni mapema kuniamini na yale yaliyot..” Nanaa akamuwahi kwa busu. “Yamepita Geb. Mimi nimejifunza, na wewe umejifunza. Naomba yaishe.” Geb akarudisha mabusu. Walikaa hapo kwenye gari wakishikana na kunyonyana midomo. Alipenda vile mikono ya Geb ilivyokuwa ikimkamata kwa nguvu. Hamu ya kuwepo Morogoro kwa haraka ikamjia. “Nakutamania.” Geb alimsikia Nanaa akiongea taratibu. “Mwenzio hali mbaya! Hata sijui naingiaje ndani.” “Basi tutoke tutembee kidogo.” Nanaa akatoa wazo. “Lakini baada ya hii mara ya mwisho.” Geb akamvuta tena na kuendelea kumpapasa kwa uchu huku akimnyonya bila kuchoka. Mwishoe wakaachiana. Wakatulia ndipo wakaingia ndani.

~~~~~~~~~~~

Walishakuwa wamekaa hapo nje zaidi ya nusu saa. Na watu wa ndani walishajua walirudi. Kwani walisikia mlio wa gari ya Geb. Wakaingia wakiwa wanacheka na wote walionekana wamejawa furaha. Wakamkuta mama G, Grace na Danny hapo sebuleni. Mama G akaguna. “Sasa mama unaguna nini?” “Aaah! Nasafisha koo Nanaa, mwanangu. Kwani mimi nimesemaje?” Nanaa akacheka akainama. “Mbona mmechelewa kurudi? Kwema?” Nanaa akamwangalia Geb kama anayetaka azungumze yeye.

Geb akaelewa. “Kesho nina safari ya Morogoro. Nitawahi kutoka kazini. Nilitaka kumwambia Grace kuwa nataka Nanaa anisindikize. Kazi zake tutamalizia tukirudi jumatatu.” Watu wote wakawageukia. “Upo likizo!?” Mama yake akauliza. “Tutaondoka Morogoro alfajiri sana. Kwa hiyo nitawahi kazini.” Safari za Morogoro huwa Geb anafanya kwa siku moja. Anakwenda asubuhi na kurudi jioni. Tena wakati mwingine hata chakula cha mchana anakuwa anakula nyumbani. Nanaa akabaki ameinama.

“Hivi ulisema safari hii ni ya wapi tena? Morogoro au Iringa?” “Ni Morogoro, mama! Naona safari hii nitakuwa na kazi kubwa itakayonifanya nikae kidogo.” Geb alijibu huku akijua kabisa mama yake anachokoza tu.  “Oooh!” Mama G akaitika kwa kuwakejeli. Wote wakacheka. “Sasa mama hiyo ‘Oooh’ ya nini hapo?” “Si nimeelewa kuwa safari hii una kazi itakayokufanya ukae zaidi huko Morogoro. Unaondoka na Nanaa kuanzia ijumaa mchana mpaka jumatatu asubuhi. Au sijaelewa vizuri?” Danny, Grace na Nanaa walikuwa wakicheka. Geb alibaki akimtizama mama yake huku akicheka na kutingisha kichwa.

“Au mama ulitaka nibaki nikusaidie kitu?” Nanaa akauliza na tabasamu usoni. “Miye huyu!?” “Ndiyo mama. Wewe. Unataka nibaki nikusaidie kitu?” “Akuuu! Swali hilo ulipaswa uniulize kabla hujamkubalia Geb. Tuna mipango mingi sana mimi na wewe weekend hii. Tena mwenyewe ukajidai kuniambia, ‘basi usiwe na wasiwasi mama, kati ya jumamosi au jumapili tutakamilisha’. Leo naona mwenzangu umetoka shopping ya safari ya Morogoro! Bwana huyo kakusimamia pembeni, ndio unajidai kama umenisahau vile. Eti, ‘au mama unataka nibaki nikusaidie kitu?’ Yaani kama vile kujidai umesahau au hujui! Ili nikukumbushe. Ubaki hapa, nilaumiwe mimi. Akuuu! Wewe endelea na mipango yenu.” Nanaa alikumbuka akaanza kucheka.

“Basi jumamosi ile ya mwisho wa mwezi mama yangu. Maana hizi zinazokuja zinamipango na Geb tayari. Ile ya mwisho wa mwezi mpaka tukamilishe.” “Ile jumamosi ya mwisho wa mwezi ni harusi ya Malii, Nanaa. Na umenikubalia tunaenda wote.” Danny akaanza kukohoa. “Masikini mwanangu Zinda!” Watu wote walizidi kucheka. “Mama jamani! Usiseme hivyo!” “Aaah! Namuhurumia tu Zinda.” “Basi mimi siendi.” “Mama!?” Geb akashituka. “Atakwenda tu. Kwa lazima, utakwenda. Ushamkubalia Geb huko, ndio leo ujidai kunidanganya eti unamuhurumia Zinda, huendi na Geb!? Wakati unamkubalia Geb kwenda naye kwenye harusi, ulisahau ulimkatalia Zinda kwenda naye kwenye sendoff?” Kila mtu alikuwa akicheka.

“Nilisahau mama jamani!” “Kama ulivyosahau miahadi yetu?” Mama G, akauliza kwa kejeli. “Mwache Nanaa, mama. Atakuwa kasahau.” Geb akajaribu kutetea. “Na anasahau kweli! Tena anasahau kwa haraka sana. Naona mimi na mwenzangu Zinda tuandike maumivu.” “Usiwe na wasiwasi mama yangu. Nikirudi tutakamilisha mipango yetu. Tena mimi naona wala tusisubiri siku za jumamosi. Hata ijumaa tunaweza kukamilisha tu. Ijumaa ijayo nawahi kutoka, nakufuata kabisa kazini.” “Unakumbuka ijumaa tulipanga tutoke Nanaa.” Geb akamnong’oneza, wakasikia.

          “Basi jumapili hii. Wala tusingoje mama yangu. Tutakamilisha usiwe na wasiwasi.” Nanaa aliongeza kama kumfariji. “Usisahau jumapili hii ndio tunakwenda kule kwenye mradi wa Antii kutembelea wagonjwa mahospitalini.” Geb akaongeza. “Haya naomba muondoke. Sitaki kuendelea kudanganywa hapa!” Nanaa akazidi kucheka.

“Tutapanga mambo yetu tukiwa tumetulia. Mimi na wewe mama yangu!” “Sitaki. Unanidanganya.” “Mimi na wewe mama?” “Mmmh!” “Twende ndani nikakuonyeshe zawadi niliyokununulia. Nililipwa mshahara na bosi wangu Grace. Twende.” “Ndio umeninunulia zawadi ya kunipoza?” “Mimi na wewe hatukosanagi mama yangu. Haya ni mapenzi tu kwako.” Nanaa aliongea huku anapitiliza chumbani kwa Mama G. “Njoo basi.” “Nakuja. Wewe si unajua nyanyuka yenyewe mpaka niagane na nyonga?” Walimsikia Nanaa akicheka huko koridoni.

 

Maandalizi Ya Safari Ya Jiji Kasoro Bahari.

Aliamka asubuhi akaandaa kila kitu. Geb akatoka chumbani akiwa amechangamka, kila mtu alijua anafuraha. Akala, wakati Nanaa anajiandaa. Alijaza vitu vipya vitupu ndani ya sanduku hilo jipya na la thamani. Nanaa huyu sio Nanaa wa siku chache zilizopita. Kila kitu chake kilinukia pesa. Yeye mwenyewe alikuwa anasikia raha kupanga vitu vyake humo ndani ya hilo sanduku. Kuanzia nguo za ndani mpaka za usiku za kulalia zilikuwa mpya na za thamani. Bado alikuwa amevaa mkufu wake wa dhahabu aliokuwa amepewa na mama G.

Wakaondoka kuelekea kazini siku hiyo ya ijumaa. Lakini walishaweka mizigo yao kabisa kwenye gari. Kwa makubaliano wapite moja kwa moja, wasirudi tena nyumbani mpaka jumatatu jioni wakitoka kazini. Hilo Nanaa akaliafiki bila shida. Hata yeye alitaka muda wa faragha na Geb. Mwanaume aliyemsubiri kwa hamu, na kwa muda mrefu tu huku akimuwazia Liz alivyokuwa akimfaidi chumba kinachofuata.

Ilipofika saa tisa mchana, akamsikia Geb ofisini kwa Grace akisalimia. Wakaongea kidogo na dada yake ndipo akaingia ofisini kwake. Akarudishia mlango akamsogelea pale kwenye kiti na kuanza kumbusu huku amemuinamia. Nanaa alinyanyua mkono wake wa kulia mpaka sikioni kwa Geb. Mabusu yakaendelea huku akichezea sikio la Geb.

Grace akaingia, akakuta bado wanakiss. Nanaa alitegemea kuona Geb anakurupuka kumuachia. Lakini wapi. Yeye alishashusha mkono kwa haraka sana, lakini Geb aliendelea kidogo. Akabusu tena mara kadhaa nje ya mdomo ndipo akamgeukia dada yake aliyekuwa anataka kutoka. “Naomba saini yako ya pili kabla hujaondoka.” “Ni pesa ya nini?” Geb akauliza kana kwamba hakuwa amefumaniwa pale. Akapokea ile hundi, akaanza kuisoma.

“Dereva wa lori la Lushoto, ameomba afanye matengenezo madogo, kabla ya kuondoka kesho kutwa. Anasema itamuhakikishia kurudi kwa haraka bila kuharibikiwa njiani.” Grace akajibu. Nanaa alikuwa ameinamia kompyuta yake, akiona aibu kwa Grace.

Geb akasaini na kumrudishia Grace, kisha akamgeukia Nanaa, “Upo tayari twende?” Nanaa akatingisha kichwa kukubali. Grace akasoma ile hundi akatoka. “Usingenibusu hapa.” “Kwa nini!?” Geb akauliza. “Hili ni eneo la kazi Geb. Hawa ni wafanyakazi wako. Nimekuta ukiwa na sifa nzuri sana hapa. Wanakuheshimu. Sasa huku kutufumania kila mara!” “Hatujawahi kufumaniwa Nanaa. Wananikuta nakubusu wewe. Hawajawahi kunikuta nikimbusu mwanamke mwingine yeyote hapa kazini, wewe ndio wa kwanza. Wewe sio mke wa mtu, ni wangu. Ndio vizuri wajue na wakuheshimu.” “Geb!?” Nanaa akamshangaa lakini kafurahia moyoni. Akaanza kujifikiria vile watu wengine pale watakavyokuwa wakimchukulia yeye kama mpenzi wa mmiliki wa kampuni! Akacheka moyoni.

          “Kwanza Grace amekatisha. Nilikuwa nasikia raha ya kukunwa sikio.” Nanaa akacheka na kujificha uso. “Usiseme hivyo bwana! Ujue mwenzio Grace naheshimiana naye sana? Sasa aje akute naleta mapenzi kazini!” “Twende bwana. Mwenzio nimefanya kazi zangu kwa haraka ili nikuwahi wewe, tukapate muda wakutosha Morogoro.” Nanaa akacheka kwa aibu kidogo, akasimama.

Geb akamshika mkono mpaka ofisini kwa Grace. “Bosi, naomba nimchukue Nanaa, tuwahi safari.” “Nyinyi nendeni tu. Muwe na safari njema na Mungu awajalie wakati mtulivu.” Nanaa hakuamini. “Asante Grace.” Alijikuta akiropoka shukurani yake. Wakatoka. “Si nilikwambia usimuogope Grace?” “Nimefurahi mwenzio. Nilikuwa naogopa.” Grace aliwasikia wakiongea wakati wanatoka nje. Akacheka moyoni. “Nanaa bado mdogo!” Akajisemea mwenyewe wakati akiendelea na kazi.

~~~~~~~~~~~

Usipitwe Na Makubwa Ya Mji Kasoro Bahari.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment