Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu Ya 25. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu Ya 25.

Kwa Nanaa!

Wakati yupo hospitalini akiuguza, Nanaa akaanza kupokea jumbe na picha kutoka kwa mtu aliyejitambulisha kama Rita. Akafungua. Akamuona Geb akiwa amevaa vizuri, amekaa mezani na chupa yake ya maji. ‘Naitwa Rita. Nipo na mpenzi wangu sasa hivi.’ Nanaa akasoma. Moyo ukampasuka kama unaotaka kutoka. Akaamua asijibu. Akatulia. Baada ya muda zikaanza kuingia zile picha za Rita akiwa uchi chumbani na Geb hana shati. ‘Hivi ndivyo tunavyomalizia siku yetu.’ Huo ndio ukawa ujumbe wa mwisho.

Kituo Cha Polisi!

Mama G na familia yake wakaingia pale polisi wakiwa hawaelewi. Wakaulizia jina la Geb, wakapewa maelezo yaliyowashangaza. HAIWEZEKANI!! Wote walikataa kwa pamoja. “Hata wahudumu wa pale wanasema yule dada aliondoka pale mezani akiwa analia. Akimlalamikia Geb kuwa anamsaliti. Mashahidi wanasema yule dada alijaribu kuondoka lakini Geb alimkimbilia. Ndipo wakachukua chumba. Baada ya muda, ndipo wakapokea simu ya kuitwa chumbani kwao. Mimi nilikuwepo kwenye tukio.” Huyo polisi waliyemkuta hapo kituoni alisistiza.

“Tulimkuta huyo binti yupo uchi kabisa, na kijana wenu hivyo hivyo.” Mama G alitamani akae chini sakafuni. Walipoomba kumtoa kwa dhamana, walikataliwa. Kwanza waliambiwa siku ile ni ya jumapili, pili aina ya kesi aliyoshitakiwa na Rita ni kesi ya mauaji. Hawezi kupata dhamana. Mpaka mahakama iamue.

Mama G na familia yake walitoka pale wakiwa hawaamini. “Haiwezekani!” Kila mmoja alisema kwa wakati wake. “Danny. Naomba usimwambie mtu yeyote juu ya hili jambo. Tafadhali sana. Naomba nifichie aibu yangu mpaka nizungumze na Geb mwenyewe. Bado moyo wangu unasita.” Mamaa G aliongea kwa uchungu sana wakati wanaingia tu ndani nyumbani. “Siwezi mama. Sithubutu.” Danny akajibu. “Basi nashukuru.” Mama G akajibu.

Grace alikuwa kama amepigwa na butwaa. “Sasa unaenda wapi mama?” Danny akamuuliza. “Nakwenda kumuita Mungu wangu. Yeye baba wa yatima na mume wa wajane. Nitamuita, mpaka aniitike. Hakika atanitetea.” Yule mama akaingia chumbani kwake akiwa ameshabeba kosa la mwanae na kuanza kuomba.

~~~~~~~~~~~~~~

Mama G alikesha usiku kucha akiomba huku akimuuliza Mungu afanye nini. Grace na Danny walimsikia akilia kwa uchungu sana huku akiomboleza. Hakuna aliyeweza kulala. Yule mama alikuwa akilia akiomba bila kunyamaza mpaka panapambazuka. Alikuwa akilia kwa uchungu sana huku akinung’unika. Kuna wakati Grace aliingia akamkuta amelala sakafuni kabisa analia. Alimmiliki huyo Mungu, usiku kucha kana kwamba ni wake peke yake. Kuna wakati alimlilia kama baba yake akimkumbusha yeye ni yatima. Alimpokonya ndugu, ndugu zake ni hao watoto.

Wakati mwingine alimtambua kama mume. Akimkumbusha alimchukua mumewe. Hana kimbilio ila yeye tu mume wa wajane. Akamsihi achukue nafasi ya marehemu Magesa, baba yake Geb, ili akamtoe mtoto wao huko jela. Yule mama alilia na kugaragara mpaka asubuhi.

Mungu Ajibuye Maombi.

Palipo pambazuka tu ni kama wazo likamjia. Akatoka kwa haraka. “Danny! Naomba nipeleke nyumbani kwa kina Rita.” Mama yule aliwasimamia kina Danny na mkewe, kitandani kwao bila hodi. Walitoka wote bila hata kuoga. Fili alikuwa kwenye nguo zake za kulalia. Lakini alibebwa hivyo hivyo. Mzee Simba na mkewe walikuwa wakiishi Mbezi ya Kibaha. Danny alikuwa akipakumbuka. Saa 10 na nusu asubuhi wakawa wamewasili nyumbani kwa Mzee Simba. Mama G akashuka haraka kwenye gari akaenda kugonga. Akafungua Mzee Simba akiwa na mshangao. “Kuna nini!?” Mama G akapiga magoti huku akilia. Aliinama mpaka kwenye miguu ya yule baba huku wanae waliokuja nae wakimwangalia. “Nisaidie baba yangu. Nisaidie.” Mama G alisikika akiombeleza huku ameshika miguu ya Mzee Simba. Mkewe akatoka.

“Mama Magesa! Kuna nini!?” Ndipo Danny akasimulia. Mzee Simba na mkewe wakaangaliana. “Hebu ingieni ndani. Wala huna haja yakulia. Rita amekuwa mwehu. Utusamehe sana mama Magesa.” Ndipo wakapewa historia nzima ya Rita. Wote wakabaki mdomo wazi.

Kisa Cha Wehu Wa Rita.

Sio kwamba Rita aliolewa na mwanaume tu wa Canada. Alihakikisha anaolewa na mwanaume mwenye pesa ili anufaike kote. Akabahatika kupata kijana mwenye pesa na pia alikuwa akitokea kwenye familia ya watu wenye pesa sana. Kwahiyo maisha yao yalikuwa mazuri huko nchini Canada. Aliishi kwenye jumba la kifahari na kuendesha magari mazuri.

Baada ya kukamilisha mambo yake ya ‘Permanent Resident’ huko nchini Canada, ndipo alipotoa makucha yake. Starehe zikaanza kunoga kwa Rita. Hata shule akaacha bila mumewe kujua. Club na yeye, yeye na club. Starehe mchana na usiku. Anavaa nguo za madizaina na nywele za aghali kweli. Kwa kuwa mumewe alikuwa mtu wa mshahara tu, akaanza kulemewa na garama za maisha. Rita akiwa amezama kwenye ulevi wa kumpindukia ndipo akaanza utapeli.

Kukopa kila mahali kwa kutumia jina la mumewe na kufuja pesa kwa kutumia Credit Card za mumewe. Haikuchukua muda mrefu yeye na mumewe kufilisiwa. Isivyo kawaida kwa familia za wenzetu, ikabidi wahamie ukweni tena wakiwa hawana kitu. Wizi wa vito vya thamani kwa wakweze ukaanza. Anaiba hapo nyumbani na kutoroka hata siku mbili tatu, akimaliza pesa, anarudi nyumbani. Walipewa Basement/Sehemu ya chini kabisa ya nyumba ya gorofa ambako ndiko alipokuwa akiishi na mumewe.

Walipochoshwa naye, wakamtegeshea kamera, wakapata ushahidi wakutosha, ndipo Rita akapelekwa jela. Mumewe alimtafutia mwanasheria wakumtetea, baada ya miaka miwili Rita akatolewa na talaka juu. Akaanza kuzunguka nchini Canada kama chokoraa. Leo kwa mtanzania huyu, kesho Kanisa hili. Ilimradi shida tu.

Ndipo habari zikamfikia Mzee Simba. Akatuma nauli na kumtaka arudi nyumbani. Rita alirudi nchini akiwa kama mwehu. Starehe tu. Na hawezi kulala bila kunywa. Lazima alewe ndipo alale. Mchafu na yupo tayari kulala na yeyote. Swala la kwenda kuchukuliwa na wazazi wake baa, walishachoka wakaamua kumuacha. Mara nyingi alikutwa akiwa kama sio vifichoni akiwa amebakwa, basi amerudishwa mpaka hapo nje akiwa hajitambui na wazi alionekana amebakwa. Hakusikia la mtu na wala hakuwa akijali. Mzee Simba na mkewe walishazungumza naye mpaka wakachoka. Tapeli wa mchana na usiku. Anajulikana kila mahali hapo mtaani. Hata wenye maduka walishakatazwa na Mzee Simba wasimruhusu kukopa.

~~~~~~~~~~~~~~

“Wewe sio wakwanza kulizwa na Rita. Hivi umewahi tu. Hodi zote za humu ndani ni mashitaka yake huyo Rita!” Mama Simba aliongeza. “Basi hayo mliyoyasema. Naombeni mkawaambie polisi ili wamtoe mwanangu. Tafadhali mama Simba. Nihurumie mwenzio. Ndio mwanangu wa mwisho huyo! Hajui hata kupiga mtu kofi! Naomba umuokoe. Nitawalipa chochote kile.” Tayari mama G alikuwa amepiga magoti. “Wala huna haja yakutulipa. Ingekuwa nikulipwa, naona sasa hivi tungekuwa mamilionea hapa mjini. Vilio kama vyako hivyo haviishi humu ndani kwetu. Si vijana, si wazee. Vilio ni vya huyo Rita. Mnatofautiana tu majanga. Ni msalaba wetu huyo! Tunabeba mpaka na sisi Mungu atakavyotusaidia. Maombi ya kila mtu ni Rita. Twendeni tuwahi wasije muhamishia jela.” Mzee Simba na mkewe wakavaa na kutoka pale sebuleni.

~~~~~~~~~~~~~~

“Lakini jamani, hatuwezi kufuta kesi mpaka tuelewane na Rita mwenyewe.” Mama G akakumbuka. “Wala usipate shida. Ngoja nimuamshe.” Mama Simba akarudi ndani kwenda kumuamsha. “Lakini lazima mjue atataka pesa. Atadanganya chochote kile ili awatoe pesa.” “Hamna neno Mzee Simba. Tutampa tu.” Mama G akajibu.

Rita akaja. Akionyesha bado anapombe kichwani. Baba yake akamwambia lazima waongozane wakafute hiyo kesi. “Lakini ameniharibia simu yangu na kuniumiza. Lazima anilipe.” “Kiasi gani unataka?” Akaitaja hiyo pesa bila kuuma maneno. “Bila hivyo sifuti kesi.” Mzee Simba akatingisha kichwa kwa majonzi. “Unaniona mimi muongo?” Rita akauliza kwa ukali. “Kama huniamini basi.” Rita akataka kuondoka kurudi ndani. Baba yake akasimama kwa haraka. “Usiondoke Rita.” Baba yake akamuwahi. “Tutamlipa hiyo pesa Mzee Simba. Bora hiyo kesi ifutwe.” Mama G na Grace wote wakasimama.

“Rita mwanangu wewe! Hakika Mungu akusaidie” Baba yake akaongea kwa uchungu akimuhurumia huyo binti yake. “Kwa hiyo wewe unawatetea wao badala unitetee mimi?” Rita akauliza. “Twende mama. Wamesema watakupa hiyo pesa. Twende sasa hivi ukawaambie polisi unafuta kesi. Na ubadili maneno yako kuwa Geb juu ya Geb kutaka kukuua.” “Mimi sikusema hivyo.” Rita akakataa kabisa kama sio yeye aliyekuwa akijiliza kwa polisi. “Haya. Twende mama. Twende.” Baba yake hakutaka kesi.

Wakatoka tena pale mpaka polisi.

Kwa Mungu Wa Yasiyowezekana.

Rita alikana kila kitu. Akawashangaa wale polisi waliwezaje kuchukua maneno yake. “Kwanza nilikuwa nimeshalewa! Wewe vipi?” Mama G na kina Danny hawakuamini. Mpaka saa tatu asubuhi, kesi ya Geb ikawa imefutwa, akatolewa. Geb alitoka nje akilia kama mtoto mdogo. Mama G alipomuona anatoka, ni kama na yeye alipandwa na kitu. Akapiga magoti palepale nje ya kituo cha polisi mbele ya mama Simba na mumewe, akaanza kulia, mpaka Grace naye akaanza kulia. Alilia mama G mpaka Mzee Simba akamnyanyua na kumsindikiza kwenye gari ya Danny. Wote wakiwa wanalia kasoro tu Danny.

“Sasa ile pesa yangu?” Rita akauliza bila hofu wala kuonyesha kujali. “Naona mnanisahau wakati mimi ndio nimemtoa huyo Geb!” Rita akaongeza. “Hatujasahau Rita. Na tunakushukuru sana. Sasa naomba tuongozane tena mpaka Sea cliff nikachukue gari ya Geb, halafu mimi na wewe twende benki.” Rita akakubali. Waliongozana magari mawili  la Mzee Simba na gari ya Danny mpaka Sea cliff hotel alipokuwa ameacha Geb gari yake siku iliyopita. Danny, Mama G, Fili na Geb wakaondoka kurudi nyumbani baada ya kumuacha Grace hapo ili achukue gari la Geb na kumalizana na Rita. Ndipo Grace na familia ya Simba wakaelekea benki baada ya Grace kulipia na hapo pia maana hawakuwa wamelipia hata chumba alichokuwa amechukua Rita na ile Wisky. Ndipo Grace akatoa hicho kiasi cha pesa alichodai alipwe kutoka kwenye akaunti yake, akamkabidhi Rita. Wakaachana.

~~~~~~~~~~~~~~

“Mama!” Geb akaita wakati wapo njiani. “Umewasiliana na Nanaa?” “Alinipigia jana asubuhi kabla sijakwenda kanisani. Ilibidi kumrudisha Zena hospitalini. Anaonekana ni mgonjwa sana.” Geb akanyamaza. “Pole baba. Pole sana.” Mama yake alimshika mkono. Alimuona machozi yakimtoka. “Sijui kama Nanaa atanisamehe!?” Walimsikia akilalamika. “Naomba pata muda wakupumzika Geb. Mengine utajua baadaye.” “Unajua muda wote nipo pale rumande nilikuwa nikimuwaza Nanaa, mama! Nilimfanyia kitu cha ajabu sana. Najua nitakuwa nimemuumiza vibaya sana.” “Mimi nashauri kama mama, Geb. Umepitia masaa machache magumu sana kwenye maisha yako. Twende ukalale. Ukiamka, utajua kitu chakufanya.” Danny akashauri tena.

Geb akainama kwa muda. Kisha akainua kichwa. “Unajua nilishindwa hata kumtambulisha kwa Rita! Sijui nilipatwa na nini jamani!” Geb akasimulia kuanzia mwanzo wa kukutana na Rita akiwa na Nanaa, mpaka alipoishia polisi. “Masikini Nanaa wangu!” Geb aliendelea kulalamika wengine wakiwa kimya. Wasijue ndio yupo kwenye mshituko au la. Aliongea bila kuulizwa. “Nilimkuta amekaa pale nje ya geti peke yake! Na pia nikashindwa kuzungumza naye chochote juu ya mabusu na kukumbatiwa na Rita! Sikutegemea kama na mimi naweza kumfanyia hivi Nanaa, tena kwa mwanamke kama Rita! Kweli nimeumia sana. Nahisi adhabu ya jela, inanistahili kabisa. Tena baada ya kumuahidi..” Geb akanyamaza.

“Pole Geb.” Ikabidi mama yake arushie neno. “Mimi sistahili pole mama. Nanaa ndiye anastahili pole. Sijui niliingiwa na nini!?” Geb bado alikuwa ameinama anajisugua mikono. “Amekwambia kama atarudi?” Baada ya muda akamuuliza tena mama yake. “Geb! Lazima atarudi.” “Lini?” Akauliza tena. “Nafikiri mpaka mgonjwa apone.” “Wapo hospitali gani?” “Hakunitajia. Amesema Zena hataki mtu yeyote ajue. Hata hivyo amesema wakati anamnyanyua Zena, simu yake ikaanguka. Anahisi imepata matatizo. Amesema Yasini amemwambia ataichukua kuipeleka kwa fundi. Inawezekana hana simu kwa sasa.” Geb akabaki kimywa.

~~~~~~~~~~~~~~

Walirudi nyumbani. Geb akaoga. Akanywa uji na kujitupa kitandani. Alilala mpaka saa moja usiku akaamka. Akamkuta mama yake jikoni. “Nanaa amerudi?” “Hawezi kurudi leo Geb. Yule binti ni mgonjwa sana.” “Amekupigia simu?” “Hapana. Lakini wewe umelala vizuri?” “Nimelala.” Geb akavuta kiti pale jikoni akakaa. “Mama!” Mama yake akamgeukia. “Najua uliniombea. Asante.” Mama G akaanza kulia. “Pole mama na samahani.” Geb akasimama kwenda kumbembeleza mama yake. Alimuona vile alivyokuwa ameumia. “Pole mama. Pole sana mama yangu.” Geb akaendelea kumbembeleza. Grace akaingia akawakuta wanabembelezana. Akasimama pale kwa muda mpaka mama yao akatulia.

“Pole mama.” Grace naye akaongeza. “Pole na wewe Geb.” “Asante.” “Na nyinyi poleni kwa hekaheka.” “Asante. Ulipata muda wakupumzika?” Grace akauliza. “Nililala.” Geb akajibu kwa upole. Grace akataka kutoka. “Grace!” Grace akarudi. “Vipi?” Akamuuliza kaka yake. “Nanaa amekutafuta?” “Alinipigia simu jana asubuhi kuomba ruhusa ya kazini. Alisema rafiki yake mgonjwa sana. Yupo kwenye matibabu. Daktari amewaambia inaweza kuchukua siku tatu ndipo akaruhusiwa.” “Okay. Asante.”  Geb akanyamaza.

“Jaribu kutulia Geb. Kila kitu kitakuwa sawa.” “Sidhani. Sidhani tena.” “Kwa nini unakata tamaa Geb!?” “Nahisi Rita amemtumia picha. Na sijui atakuwa alimwambia nini?” “Amepataje namba ya Nanaa?” “Aliniomba simu yangu wakati anakula. Alisema hajawahi kushika simu kama hii. Akawa anaigeuza kulia na kushoto. Nikahisi anasoma kitu, ndipo nikamuomba anirudishie. Baada ya hapo kila mazungumzo yaliyoendelea akawa anamlaumu Nanaa. Hata kulia kote kule akitaka niende naye chumbani nikafanye naye mapenzi, alikuwa akimlaumu Nanaa. Nilihisi ananipiga picha. Wakati namkimbiza ili nimpokonye simu nione, ndipo akajikwaa na kuanguka. Alikuwa amelewa sana. Yaani sijui pale Sea Cliff nitakuwa nimeacha deni kiasi gani!? Maana alichukua chumba Presidential Suite.” “Nimelipia kila kitu, mpaka Whisky!” Grace akacheka.

“Usicheke G. Nimempoteza Nanaa.” “Utamuelezea, ataelewa tu.” “Ni heri angesikia kutoka kwangu mimi kwanza. Kuliko kusikia kutoka kwa yule mwendawazimu kwanza! Maneno yangu yatakuwa hayana nguvu tena.” “Mungu atakutetea Geb.” Mama yake akamfariji. “Naamini hivyo mama. Japo nimetenda kila kitu kwa upumbavu, lakini naomba Mungu anirehemu.” Geb aliongea kwa upole huku akifikiria.

Huko Kwa Nanaa Na Zena.

Mpaka inafika siku ya jumanne, ndipo walipofanikiwa kushusha homa ya Zena. Ilipofika jioni Yasini alipokuja kumuona alimkuta Zena amechangamka tofauti na alivyokuwa amemuacha asubuhi. Yasini na Zena walimshukuru sana Nanaa. Wasijue hata yeye alishukuru kwa siku zile alizokuwepo pale ili kupata muda wakufikiria zaidi. “Daktari amesema kesho ataniruhusu.” Zena akamwambia Yasini. “Afadhali. Nilikuwa na hamu na wewe Zena.” Zena akaanza kulia. “Nilifikiri utakuwa umenichoka, hunitaki tena.” “Zena wewe! Unawezaje kufikiria hivyo?” “Sijui Yasini.” “Hapana. Ila nimekuonea huruma.” Nanaa akatoka kama kuwapa nafasi.

Alijua wazi angeweza kurudi nyumbani usiku ule. Lakini akaaamua alale tu na siku hiyo palepale hospitalini mpaka kesho yake. Alikaa pale nje akiwaza. Akakumbuka maneno ya Geb. Akakumbuka picha alizotumiwa na Rita mpaka wakiwa chumbani. Nanaa akacheka. “Kweli mimi sina mkosi. Bali mimi mwenyewe ni mkosi. Khaa! Haiwezekani jamani!” Nanaa alijiwazia akiwa amekaa pale nje peke yake. Wauguzi walishamjua kuwa yupo kwenye chumba cha Zena akisaidia kuuguza. Kwa hiyo hata walipomuona amekaa pale kwenye makochi, sehemu ya wageni, hakuna aliyemsumbua.

Alikaa akiwaza, mpaka Yasini alipomuita. “Zena anakuita.” Nanaa akanyanyuka. “Nakushukuru sana Nanaa.” “Karibu Zena na pole.” “Asante.” Zena akashukuru tena. “Naombeni niwashauri mimi kama rafiki tu.” Wote wawili wakamtizama. “Nyinyi wawili mnakitu cha kipekee sana kati yenu. Sidhani kama utofauti wa dini unaweza kuwatenganisha. Nashauri hayo mahusiano myafikishe kwa wazazi. Yasini, binafsi namuomba Mungu nipate mwanaume kama wewe. Unampenda na kumjali sana Zena. Nilidhani ungemkimbia baada ya mimi kuwa naye hapa hospitalini, lakini nimeona jinsi ulivyokuwa ukihangaika naye. Kutafuta damu bila kuchoka. Nashauri hofu ya dini isikunyime mke. Mfikishe Zena kwa wazazi. Muone watawashauri vipi.” “Asante sana Nanaa. Nitaanza kuzungumza na Mzee wangu kwanza.” Yasini akajibu.

Palipo pambazuka siku hiyo ya jumatano, Nanaa akaoga hapo hapo hospitalini. Akavaaa haraka. Yasini alipokuja kuleta uji wa mgonjwa, akaomba lifti. “Nishushe popote nipate daladala za Kariakoo niwahi ofisini. Najua Zena atatolewa leo kama mambo hayatabadilika. Na ninaomba yasibadilike.” Wakacheka. “Nitakupigia simu mchana kujua alipo ili jioni nije kumuona ndio nirudi Tabata. Lakini naaamini atakuwa ametoka.” “Amina.” Yasini akampeleka mpaka ofisini kwake, akamshusha nje.

Kuliko Ungua Mpini.

Nanaa alifika kazini hata Grace bado hakuwa amefika. Kwa kuwa Grace ndiye aliyekuwa akikaa na funguo za chumba hicho cha muhasibu, Nanaa akaamua kwenda kukaa na kijana wa stoo, ofisini kwake. Wakiwa wanaongea, Grace naye akaingia. Ilikuwa saa mbili kasoro. “Pole kwa kuuguza Nanaa.” “Asante.” Nanaa akacheka. “Unaonekana umechoka!” “Sana. Zaidi hofu. Hakutaka tuwaambie wazazi. Basi nilikuwa nashindwa hata kulala nikihofia kupitiwa na usingizi akazidiwa nisijue.” Grace akacheka. “Nilikuwa sitaki hata kusinzia! Lakini ni kama amepona. Leo watamruhusu. Nikitoka hapa nitakwenda kumwangalia ndipo nirudi nyumbani.” “Afadhali. Sasa ungewashauri waoane.” “Wamesema wanaanza kuwaambia wazazi kwanza. Lakini namuhurumia Zena. Baba yake ameshika sana dini. Sidhani kama atakubaliwa. Anyway, nakushukuru kwa ruhusa. Nimeona nirudi haraka usije nifukuza kazi au ukatafuta mtu mwingine.” Grace akacheka. “Siwezi.” Akamfungulia ofisi, siku ikaanza.

Siku ilikuwa nzito sana kwa Nanaa kuliko siku nyingine. Alikuwa akisinzia kama mlevi. Ilipofika saa kumi ilibidi aage tu. “Hali mbaya Grace. Kichwa kizito kama kinaanguka kwa usingizi!” Grace akacheka taratibu akimwangalia. “Nenda kapumzike.” “Nitakwenda. Lakini nataka nimpitie kwanza Zena nyumbani kwao, ndipo niende nyumbani.” “Mvua itakuwa kubwa. Imeshaanza manyunyu.” Grace alimtahadharisha. “Nikiona kubwa sana, nitalala tu kwao mpaka kesho. Hamna shida.” “Sawa.” Wakati anatoka, akamkuta Geb mapokezi. Hakujua kama alifika pale muda gani.

“Habari yako?” Nanaa akasalimia. “Nzuri.” Alipojibu tu, Nanaa akampita. Akarudi ofisini kwake kwenda kuchukua pochi yake, Geb akamfuata. “Nimesikia unaondoka sasa hivi.” Nanaa akainuka. Maana alikuwa ameina kuchukua pochi yake, akamgeukia. “Ndiyo.” Akajibu kwa kifupi tu. “Tunaweza kuongozana?” Geb akauliza. Nanaa akakunja uso kidogo kama anayemshangaa. “Wapi!?” Geb akaingia akafunga mlango.

“Namaanisha nikusindikize huko unapokwenda, halafu turudi wote nyumbani.” Safari hii Nanaa akaweka uso wa mshangao kabisa. “Kwa nini!?” Akamuuliza Geb. “Mvua inaonekana itakuwa kubwa. Utasumbuka swala la usafiri.” “Hapana. Nitakuwa sawa tu. Nakushukuru.” Nanaa akataka kutoka, Geb akawa bado amesimama mlangoni. “Samahani, naomba kupita.” Nanaa akaomba kiustarabu. “Naomba twende wote Nanaa.” “Mbona kama unalazimishia kitu Geb? Kuna nini!? Mimi naenda kumuona Zena ndipo nirudi nyumbani. Unanizuia mlangoni!” “Mvua itakunyeshea.”

 “Kweli Geb? Ujue unazungumza na Nanaa. Sijui wala sijazoea maisha ya gari mimi. Kwangu si mvua wala jua ni hatari kwangu hata kidogo. Sina tatizo la kunyeshewa na mvua. Kama unahofia mimi kuloa, usiwe na wasiwasi hata kidogo. Na nitahakikisha nakauka, kabla yakuingia nyumbani kwako ili nisiloweshe chochote kile.” “Simu yako ipo wapi? Nimepiga haipatikani.” “Yasini alinipelekea kwa fundi. Niliiangusha. Imepasuka. Lakini nilimpigia simu Grace kumuomba ruhusa yakutokuja kazini, sababu ya kuuguza. Kwa hiyo anataarifa. Hata mama anajua kama nauguza.” Nanaa alikuwa akiongea kwa jazba kidogo, na Geb akajua amebeba hasira.

“Mbona mimi hukunipigia?” Hapo Nanaa akanyamaza na kuinama. “Nanaa!” Kimya. “Mbona mimi hukunipigia?” “Nilijua unahitaji muda.” Nanaa akajibu kwa upole akiwa ameshajirudi na jazba imeisha. “Ni kweli nilihitaji muda.” Geb akajibu na yeye kwa upole. “Samahani.” Samahani ya Geb ikamfanya Nanaa atulie na kumwangalia vizuri. “Mbona unaonekana umechoka? Upo sawa?” Nanaa akamuuliza kwa kujali huku akifuta machozi. Geb akavuta pumzi kwa nguvu huku amefunga macho. “Geb!” Nanaa akamuita. “Upo sawa?” “Hapana Nanaa.” Nanaa akakausha machozi, kisha akamshika mkono. “Pole Geb. Naanimi kila kitu kitakuwa sawa. Pole.” Geb akataka kumkumbatia lakini akasogea nyuma kidogo kama kumkwepa. Na Geb akajua.

“Nitakuona baadaye kidogo. Naomba niwahi Sinza nikamuone Zena.” “Naomba nikupeleke Nanaa.” “Hapana Geb. Haya ni maisha yangu. Nimeshazoea hivi. Naomba niache niishi hivi. Huko bado sijafikia. Nitakuona nyumbani baadaye.” Alikataa kwa upole, bila jazba. Akampita pembeni yake, akafungua mlango, akatoka. Alimuacha Geb amesimama palepale ofisini kwake.

~~~~~~~~~~~~~~

Alitembea mpaka kituo cha Fire, akapata daladala za Sinza. Alimkuta Yasini anapika, akamwambia Zena amelala ndani. “Basi nisimwamshe. Mwache apumzike tu. Nitampigia simu hata kesho.” “Lakini ujue simu yako bado haijawa tayari.” “Mpaka lini?” “Nimepitia jioni hii, sikumkuta fundi.” “Hamna shida. Nitawatafuta kwa simu ya mtu yeyote yule atakayekuwa karibu yangu.” “Nashukuru sana Nanaa. Asante kwa kila kitu.” “Karibu. Muwe na usiku mwema.” Wakaagana, Nanaa akarudi tena kutafuta daladala.

~~~~~~~~~~~~~~

Alipanda daladala nyingine mpaka kituo kikubwa cha Mwenge ili kupata daladala ya Tabata. Hapo angalau hakupata shida ya kupata daladala. Lakini alipoingia tu ndani ya daladala, mvua ikamwagika. Nanaa akacheka moyoni. Akajua hiyo ameikwepa. Yakabaki maombi kuwa ikatike hapo njiani ili akifika Mwenge asilowe. Lakini ikawa tofauti. Mvua ilizidi kunyesha. Magari hayaendi. Mpaka anafika kituoni Mwenge, tayari giza limeshaingia.

Ilimlazimu kushuka hivyo hivyo na mvua ili kutafuta daladala za Tabata. Sababu ya mvua, daladala zikawa za shida sana. Nanaa akabaki hapo anasubiri. Ilipokuja, ikabidi tu na yeye agombanie kuingia ili atoke pale kituoni. Maana ni kama alisikia wakitangaza ndio daladala ya mwisho kwenda Tabata. Akapata nafasi ya kusimama. Safari ikaanza. Ilichukua zaidi ya masaa mawili kumfikisha Tabata Barakuda kwenye kituo cha mabasi ya karibu na nyumbani kwa Geb. Foleni ilikuwa kubwa sana.

Akavuka barabara huku anakimbia mpaka getini kwa Geb. Akashangaa geti linafunguliwa mara tu alipojitambulisha kuwa yeye ni Nanaa. “Labda wameanza kulijua jina langu.” Nanaa akawaza wakati anaingia. Alishakuwa amelowa sana, akaona hamna sababu ya kukimbia tena. Akaanza kujivuta taratibu mpaka ndani. Kwanza alikuwa amechoka. Wakati anavua viatu na kuacha pochi yake ili ajikaushe, Geb akatoka na taulo lake. “Pole.” “Asante.” “Sasa mbona ulikuwa hukimbii?” “Niliona haina haja tena. Nilishaloa.” Nanaa akajibu. “Jikaushe na taulo.” Nanaa akapokea. “Asante.” “Njoo ndani.” “Nachuruzika sana maji. Ngoja yapungue kidogo. Nitalowesha nyumba nzima.” “Utakohoa Nanaa. Ingia ndani. Tutakausha tu.” Nanaa akabaki akifikiria huku akijikausha taratibu. “Nanaa! Acha ubishi basi.” Akacheka kidogo, kisha akaingia ndani. Alikuta kila mtu yupo hapo sebuleni wamejifunika na vikombe vya chai pembeni.

“Shikamoo mama.” Akamsogelea mama G. “Poleni na kazi.” Akimaanisha Danny na Grace. “Marahaba. Simu bado haijapona?” “Mimi nahisi huyu fundi ananichezea mama. Kesho naenda kuchukua simu yangu hivyo hivyo.” Nanaa akaendelea. “Kwani nilipokupigia si tulisikilizana kama kawaida?” Nanaa akauliza. “Nilikuwa nakusikia vizuri tu.” “Basi naenda kuichukua simu yangu, asinichezee akili.” “Si umesema imepasuka?” Mama G akaendelea kuhoji. “Nitaifunga na tape.” Mama G akacheka. “Nanaa wewe!” “Wanaweza kuniharibia zaidi bure, wanitie hasara ya mwaka. Wakati mimi sina bajeti ya simu sasa hivi. Ujue naweza kusoma jumbe na kuona kila kitu?” Geb moyo ukampasuka. “Basi hiyo nzima kabisa.” “Sasa je?” Mama G akacheka.

“Nenda kabadili nguo uje ule.” “Hilo ni kosa ambalo sitafanya.” Nanaa akajibu huku akielekea chumbani kwake. “Nina usingizi, nusura nipitishwe kituo mama. Yani nilisimama mpaka kituo kimoja kabla ya kushuka ndipo nikapata kiti. Ile kukaa tu, usingizi mpaka konda ilibidi aniamshe kuniuliza. Nikajihisi nililala kizembe labda akaniona.” Mama G akacheka. “Kweli mama! Sasa kwa nini anifuate mimi?” “Au labda ulikuwa ukikoroma sana mpaka ukasumbua abiria wengine?” Nanaa akacheka mpaka akasimama huko koridoni.

“Mama wewe!” “Kumbe! Sasa kwa nini uamshwe wakati sio mwisho wa daladala?” Nanaa akatulia kidogo akifikiria aliyosema mama G, kisha wakamsikia akicheka huko koridoni. “Umekubali mwenyewe.” “Bwana sijakoroma mama! Acha kunitia hofu ukanifanya nishindwe kulala.” “Kula kwanza ndio utalala vizuri.” “Hapa nipo hoi mama yangu. Hamna jinsi naweza kupitisha chakula hapo kooni kikapita kwenda huko tumboni. Natamani tu kitanda. Acha tu nilale mpaka kesho.” Nanaa akaanza kukohoa.

“Nimekusikia unakohoa Nanaa! Kunywa hata chai upate joto. Mvua hiyo.” “Sidhani. Huko hospitalini walikuwa wanawasha AC kwenye baridi kali kweli. Ili kushusha homa ya Zena. Nahisi huko ndiko nimepata hiki kifua. Usijali mama yangu. Nitapona tu.” Wakamsikia amefungua mlango wa chumbani kwake. Alikuwa akiongea na mama G akiwa nje ya chumba chake.

Hata hakuoga. Alivua tu zile nguo. Akavaa nguo za kulalia, akajitupa kitandani. Geb akagonga, akaingia na blangeti. “Hapo utakuwa umenisaidia. Mbona asante!” Geb akacheka. Akamfunika. “Zito hilo! Mpaka raha.” Nanaa akasifia. “Asante Geb.” Geb akabaki akimwangalia. “Nasinzia mwenzio.” “Wewe lala tu.” Hapo hapo Nanaa akalala. Geb akamkusanyia nguo mbichi, akatoka nazo pale chumbani.

Habari Mbaya Huenea Kwa Haraka.

Aliamka asubuhi ya saa 4. Nusura achanganyikiwe. “Mungu nisaidie! Nimefukuzwa kazi tayari!” Akatoka nje. “Mamaaa!” Akaanza kuita. “Nanaa!” Akatulia baada yakusikia sauti ya Geb. “Geb!” Geb akasogea. Alikuwa sebuleni. “Uwiii! Nimepitiwa na usingizi. Grace ataniona sipo serious na kazi! Atatafuta mtu mwingi..” “Nanaa!” Geb akamwita tena akiwa anamwangalia. “Nimepitiwa Geb. Ngoja nijiandae nie..” “Nanaa!” Geb akamuita tena kabla hajarudi ndani akiwa na zile nguo za kulalia.  “Abee!” “Tumeamua leo kukuacha upumzike. Usiwe na wasiwasi.” Nanaa akatulia kidogo. Akarudi pale alipokuwepo Geb.

“Sasa mbona wewe haupo kazini!?” “Nilitaka kubaki na wewe.” Nanaa akakunja uso huku na tabasamu. “Yaani uache kwenda kazini, ubaki na mimi!?” “Ndiyo.” Nanaa akatoa kicheko cha sidhani, huku akifikiria na kumtizama Geb kama hana uhakika na anachozungumza. Akaondoka kurudi chumbani kwake bila kuongeza neno na kumuacha Geb amesimama palepale.

Akaoga vizuri. Akavaa gauni la kawaida tu lakini lilimkaa vizuri. Ni moja ya magauni aliyojinunulia mwenyewe. Akaweka mafuta ya mdomo yenye rangi nyekundu kidogo. Akapulizia body sprey aliyonunuliwa na Geb. Ilibidi kuachia nywele zake kwa kuwa bado zilikuwa mbichi. Alikuwa amesukia rasta ndogo ndogo. Kwa hiyo akazifungua ili zikauke na upepo tu. Akatoka akiwa amependeza.

“Njaa inauma!” Nanaa aliongea huku akielekea jikoni. “Mama amekuachia kitu cha kula hapo jikoni.” Geb na yeye akasimama, akamfuata huko jikoni. Akasimama na kumgeukia Geb. “Umependeza.” Geb akamuwahi kabla hajazungumza kitu. Nanaa akamuona anawasiwasi usoni.

“Ni nini kinaendelea Geb!?” “Tupate kifungua kinywa kwanza ndipo tuzungumze.” “Kama nikuhusu Rita, usiwe na wasiwasi. Hata yeye nilimwambia asiwe na wasiwasi na mimi. Wewe endelea tu Geb. Huna haja yakuacha kwenda kazini kwa ajili hiyo.” “Subiri kwanza Nanaa. Unasema ulizungumza na Rita!?” “Ndiyo. Si yule mpenzi wako mliyekumbatiana na kupeana mabusu mbele yangu? Ukanionea haya hata yakunitambulisha jina tu kwake! Ndiye huyo huyo alinifuata mpaka hospitalini baada ya kunitumia picha zenu, na jumbe zenu zote mlizokuwa mkitumiana siku ya jumapili asubuhi kabla ya kukutana.” Nanaa akaendelea akiwa ametulia tu bila jazba.

“Amenitumia picha za familia yake na yenu. Tokea Fili ni mtoto mchanga. Amenieleza kwa undani na kwa kituo juu ya mapenzi yenu na mahusiano ya kifamilia mliyokuwa nayo. Urafiki kati ya mama yenu na mama yake. Picha zao. Akaniomba niachane na wewe. Nimemuhakikishia mimi si mpenzi wako. Na haitakaa ikatokea nikaja kuwa mpenzi wako. Nimemuhakikishia hata kama kulikuwa na wazo lolote juu yako, nikamuahidi Rita, NIMEFUTA. Nimemuomba msamaha na amenielewa. Akaondoka na kuniacha kwa amani.” Geb alitamani kukaa chini.

“Kwa hiyo kama uliacha kwenda kazini kwa ajili hiyo, naona mpenzi wako amekupunguzia kazi. Wahi tu kazini. Maana hata mimi nikimaliza tu kula, naenda kazini. Nashukuru kwa ofa ya mapumziko ya leo, lakini sina sababu ya kujilaza hapa kama mgonjwa.” Nanaa akatulia kidogo, akajishika tumbo. “Halafu unajua nini? Nahisi tayari nimeshiba. Ngoja tu niende kazini.” Nanaa akatoka pale jikoni. Aliingia chumbani kwake akachukua nauli ya daladala, akatoka bila hata kugeuka nyuma. Akaenda kazini.

~~~~~~~~~~~~~~

Geb alibaki amesimama palepale jikoni. Akaamua kumpigia simu mama yake. “Vipi Nanaa? Mmeweza kuzungumza naye?” “Nimeshindwa kabisa mama yangu. Kumbe Rita alimfuata mpaka hospitalini! Amemueleza kila kitu. Nanaa anahabari zote juu yangu na Rita. Mahusiano yako na wazazi wa Rita. Alimtumia picha za wakati ule tunakwenda kwao. Mbaya zaidi ameambiwa na Rita sio mimi. Najuta mama, natamani kama mimi ndio ningekuwa nimezungumza na Nanaa kwanza.” Geb alisikika amechoka sana.

“Umekula?” Ndilo swali mama yake alilomuuliza. “Nilikuwa namsubiria aamke tule naye. Lakini ameshindwa hata kula! Amesema ameshiba, ameenda kazini.” “Nisikilize Geb. Wewe unamtaka Nanaa kwa kiasi gani?” “Nampenda Nanaa, mama yangu. Ndiye mwanamke anayenijali mimi binafsi hata kama nimemuudhi, ananijali. Anataka kuniona ninafuraha wakati wote. Namtaka Nanaa, mama yangu. Nikuchanganyikiwa tu. Nilikosa sana.” “Basi nataka ukae chini. Kula vizuri ushibe. Usichanganyikiwe. Nanaa anahabari ya upande mmoja tu kutoka kwa Rita. Hajakusikiliza wewe. Ukishamaliza kula, mfuate kazini. Hakikisha unarudi naye hapo nyumbani akusikilize. Usikubali kushindwa na Rita, ambaye ni mwehu tu.” Mama yake akasisitiza.

“Unamaanisha nikamfuate Nanaa?” “Ndiyo.” “Namwangaliaje?” “Tena hakikisha anakuangalia machoni. Unanisikia Geb? Nanaa anakupenda. Sema amekasirika tu. Lakini ukifanikiwa kumtuliza, umempata. Kula uende.” “Asante mama yangu. Nakwenda sasa hivi.” “Hapana Geb. Nimesema kula kwanza.” “Siwezi mama.” “Basi ndio umemkosa Nanaa. Mimi nakujua Geb. Ukiwa na njaa huwezi kuongea kabisa. Kula kwanza. Hata usiku hujala. Ungekuwa umeshiba wewe, Nanaa asingekuponyoka hapo. Kaa chini kula.” “Sasa nile nini?” “Vyakula vyote vipo mezani.” Geb akamshukuru mama yake akakata simu.

Akakaa, akala. Tena hakunywa uji. Akala chakula cha mchana alichokuwa ametayarishiwa na mama yake. Akala matunda, akaongeza na juisi ndipo akatoka. Hakumaliza hata lisaa tokea Nanaa atoke, na yeye akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Grace akashitukia Nanaa anaingia ofisini kwake. “Uchovu umeisha?” Nanaa akacheka. Lakini Grace alijua ile sio cheka ya Nanaa. “Ungeniona nilivyoamka nikagundua ni saa nne asubuhi, ungenihurumia! Nusura nichanganyikiwe. Samahani mwaya.” “Ungepumzika tu Nanaa.” “Grace wewe! Huko sijafikia mwenzio! Yaani siku ya kazi kama sasa hivi eti nimekaa nyumbani napumzika! Uwiii! Baada ya kufanya nini? Acha nifanye kazi tu.” Grace akacheka. “Haya. Funguo za ofisi yako hizi hapa.” Nanaa akazichukua na kuingia ofisini kwake. Akakaa.

~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda kidogo, akasikia mlango mkubwa unafunguliwa Geb anamuulizia kwa Grace. “Nanaa amefika hapa?” “Yupo ofisini kwake.” Akamsikia akielekea kwenye ofisi aliyokuwepo. Akainamia kompyuta kama aliyetingwa na kazi nyingi. “Na mimi nina haki yakusikilizwa Nanaa.” Geb aliingia na kuanza kuzungumza bila hata salamu. Nanaa akabaki tu kimya. “Kama uliweza kumsikiliza Rita, na mimi lazima unisikilize.” Kimya. “Nanaa!” Kimya. NANAA! Geb akaongeza sauti. “Nipo kazini Geb! Naomba tuzungumze baadaye.” “Kwa hiyo umekubali tuzungumze?” “Si unataka nikusikilize tu?” Nanaa akamuuliza. “Ndiyo.” “Basi nitakusikiliza baadaye. Naomba niache nifanye kazi.” Geb akavuta kiti pembeni yake akakaa.

Wakatulia kwa muda, Nanaa akishangaa haondoki. Akamuacha tu. “Lakini nataka ujue, muda wakati Rita anazungumza na wewe, alikuwa ameniweka jela.” Hilo likamshitua mpaka akamgeukia. “Rita!?” “Ndiyo. Rita alinisingizia kosa la mauaji. Nikafungwa siku hiyo ya jumapili nikatolewa jumatatu. Tena baada ya mama kuwafuata wazazi wake kuwabembeleza. Rita akataka alipwe pesa. Amelipwa mamilioni ya pesa na Grace ndio mambo yakaisha.”

“Pole Geb. Pole sana.” “Ningefungwa kifungo cha maisha Nanaa. Huwezi amini muda wote nipo huko rumande, nilikuwa nakuwaza wewe. Nilikuwa nafikiria vile..” Geb akainama. Akaona machozi yanamtoka. Akamuhurumia huku na yeye ameingiwa na hofu asijue ni hofu ya nini! Kwa mwanamke kulia ni jambo la kawaida. Tena wakati mwingine wengine huchukulia kama ni ishara ya unyenyekevu. Inapendeza. Lakini sio mwanaume, tena wakiafrica! Ukiona chozi lao na hawapo msibani au mbele za Mungu, basi ujue kuna jambo zito limemsibu.  

Akasimama na kumkumbatia. Ikawa zamu ya Geb kupata faraja mikononi mwa Nanaa. Ni kama aliyekuwa amebeba mzigo mzito kifuani. Geb kwa mara ya kwanza akajikuta anapoteza uasili wa mtoto wa kiume wa kiafrica. Akalia bila kujizuia mbele ya mtoto wa kike, tena anayempenda. Nanaa alimsugua mgongoni mpaka akatulia.

“Nina hamu na wewe Nanaa!” “Sijui nisemeje Geb.” Geb akasimama. “Naomba niamini hakuna kilichotokea kati yangu mimi na Rita. Na wala sikuwa nimekusudia kufanya chochote na Rita. Sema nilikutana naye kwa gafla. Halafu nikashindwa niseme nini wakati sikuwahi hata kumtaja kwako! Wakati mara ya mwisho kuagana naye, tuliagana naye vizuri sana. Kiukweli alikuwa mpenzi wangu. Sijui alikwambia nini, lakini tulikuwa na mahusiano mazuri kuliko uliyonikuta nayo na Liz. Wazazi walijua kwa hakika tutaona. Nilitaka tukutane naye siku ya jumapili, niwekane naye sawa ndio tuzungumze. Aliiba namba yako kwenye simu yangu. Baada ya kutaka nifanye naye mapenzi nikakataa, ndipo akaanza kukulaumu wewe. Alinitia aibu yule msichana, hujawahi ona!” Nanaa akacheka kidogo. Geb alimsimulia kila kitu akamuacha Nanaa na mshangao.

“Nisamehe Nanaa.” “Naelewa mimi bado mgeni sana kwako Geb. Una maisha uliyoishi nyuma. Na mimi hivyo hivyo. Hatuwezi kuambiana kila kitu kwa wakati mmoja. Lakini niliumia uliposhindwa hata kunitambulisha!” “Ni kweli nilikosa Nanaa. Lakini nilikuwa sijui niseme nini! Nilijua nikianza utambulisho, hata kwake kwako. Ingebidi niseme ni mpenzi wangu. Wakati tulitengana zaidi ya miaka mitatu, nafikiri.” Geb akafikiria kidogo. Kisha akaendelea.

“Mara ya mwisho tuna agana na Rita, yeye akirudi nchini Canada kwa ahadi akirudi tuoane. Kwa kifupi hakuwa tu kama Liz. Rita alikuwa mchumba wa kuja kumuoa. Baada ya ukimya wa miaka yote hiyo ndipo na mimi nikamuona tena siku ile. Nilikuwa kwenye mshituko Nanaa. Nilitaka kwanza nimsikie ndipo nijue jinsi yakumtambulisha kwako.” Nanaa akanyamaza.

“Sijui umenielewa?” “Nina swali Geb. Na ninaomba uwe mkweli kwangu.” “Uliza tu.” Geb akajiweka sawa kupokea swali. “Endapo Rita asingekugeuka kwa kiasi hicho, inamaana mngerudiana. Si ndiyo?” Geb alivuta pumzi kubwa akaishusha taratibu. “Naomba niwe mkweli kwako. Kidogo nilishawishika. Lakini kadiri masaa yalivyokuwa yakisogea bila wewe. Huku nikijiambia ndio nitaachana na wewe niwe naye, ndivyo ugumu ulipoanza Nanaa. Nimegundua siwezi tena kuishi bila wewe. Nakuhitaji wewe kuliko kitu kingine chochote. Najua nilikosea tangia mara ya kwanza nilipomuona. Nakiri nimekosa. Nisamehe.” Nanaa akanyamaza.

Akarudi kukaa alipokuwa amekaa tokea mwanzo. “Nanaa! Nimeomba msamaha!” “Yameisha Geb.”“Unajua sio ninachokuulizia Nanaa!” “Unataka kunisikia nikisema nini Geb?” “Nimekuwa muwazi kwako! Usiniadhibu. Unajua wazi ningeweza kukudanganya. Lakini kwa kuwa nakupenda, sikutaka kukudanganya. Usiniadhibu kwa hilo.” “Sikuadhibu Geb.” “Ila ni nini?” “Mbona nimesema yameisha!?” “Nanaa!” Geb akalalamika.

Nanaa akamgeukia. “Nipo kazini Geb. Sina maisha yakueleweka. Naomba niache ni focus. Nisaidie shule yangu iishe na pia nisiharibu hapa kazini. Sitaki kujichanganya sasa hivi.” “Sitakubali uchanganyikiwe Nanaa.” “Unakumbuka hiyo ni moja ya ahadi ulizonipa ijumaa, jumamosi ukaishia kwenye mikono ya mwanamke mwingine? Nakuamini vipi tena?” Nanaa alimuuliza bila jazba. Geb akabaki kimya.

“Nimesoma jumbe zako na zake mlizokuwa mkitumiana siku ya jumapili asubuhi kabla yakukutana. Tena nimesoma kwa kurudia rudia, ili nisije kukuelewa vibaya. Kilichonishangaza ni vile ulivyoweza kuamka jumapili asubuhi, ukawasiliana na yeye, sio na mimi tuliyeachana nikiwa sina raha Geb! Hukujali hisia zangu ila zake. Nimesikiliza mazungumzo yenu asubuhi ya jumapili. Ulimwambia unamsikiliza yeye. Achague muda na wakati anaotaka yeye ili mkakutane kwa kuwa alikwambia anahamu sana na wewe. Geb, tuwe wawazi. Mimi sio mtoto mdogo. Mimi nimekuwa kimbilio pale unapohitaji. Lakini wanapokuwepo watu wa muhimu kwako, nakosa maana. Hukunipa uthamani wowote kwa Rita.” Nanaa aliongea kwa upole bila hata hasira. Lakini alijua ujumbe wake unafika. Akaendelea.

“Sidhani kama ulikosea Geb. Nafikiri hakuna hisia za penzi la dhati kwangu. Hujali hisia zangu. Na sishangai. Wewe sio wa kwanza. Wanaume wote wanakuwa hivyohivyo kwangu. Nafikiri sikuwahi kubahatika kupata mwanaume ambaye ananipa mimi kipaumbele. Ninachoogopa kwako zaidi, ni kwa sababu nahisi naanza kukupenda. Utaniumiza na kunichanganya zaidi Geb. Tafadhali naomba niache nitengeneze maisha yangu. Angalau hii shule iishe. Ili na mimi niwe na kitu mkononi mwangu. Tafadhali Geb. Unajua nilikotoka.” Nanaa akacheka kwa kujihurumia.

“Unakumbuka mvua ya jana uliyokuwa ukihofia nitalowa? Tena mvua ya jiji la Dar, kwenye joto! Basi mimi nilikuwa nikilazwa nje. Kilimanjaro! Kwenye baridi na mvua inaninyeshea usiku kucha ili nimalize kazi zangu. Asubuhi wakiamka ndipo naruhusiwa kuingia ndani. Sio kulala, ninaingizwa ndani kuanza kazi za ndani tena. Ujue hapo ni siku ya shule. Sio weekend. Na hapo ilikuwa ni juu yangu mimi. Niamue kurudi kulala baada ya wao kuondoka au niwahi shule pengine nitakuja kukutana na hicho kitanda usiku kama nitabahatika. Hakuna wakukulazimisha usome. Lakini ilinilazimu mimi mwenyewe kwenda shule. Bila kujali kama nililala nikinyeshewa. Na hapo bado mvua inanyesha nje. Ilinilazimu kujibidisha mwenyewe kwenda shule. Nimefika hapa kwa shida sana Geb. Acha nisiharibu sasa hivi. Na nina hakika sio nia yako kuniharibia maisha.” Nanaa aliongea taratibu bila jazba. Geb akatoka akiwa amenywea kama maji.

 ~~~~~~~~~~~~~

Nanaa aamua kuachia ngazi. Mapenzi yameshindikana kwa Geb ampendaye. Nini kitaendelea akiwa bado anaishi nyumbani kwake?

Usikose Muendelezo.



 

 

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment