Akiwa anavuja damu pale kitandani wakati Alex
amekimbilia dukani kununua pedi, Nanaa aliendelea kugugumia maumivu. Kwani ni
kama Alex hakuwa amemuelewa Nanaa, pale alipokuwa akimsihi afanye
taratibu. “Naomba uwe mwangalifu Alex. Mwenzio sijawahi kufanya
mapenzi.” Akiwa amejawa hofu, binti huyo wa sekondari alimsihi Alex aliyekuwa
chuoni. Akiwa na tumaini la kuja kuolewa. Lakini Alex alimwingilia kama
aliyekuwa anapambana. Na bado Nanaa alivumilia mpaka mwisho wa Alex akapiga
bao. “Nilijua kwa hakika Alex anganioa! Nilijua ni wangu! Lakini
aliamua kuzaa na Viola! Nina kasoro gani mbaya hivyo inayowafanya wanaume
kunikimbia?” Hakukumbuka kufurahishwa kimapenzi na Alex hata mara moja!
Na wakati wote Alex hakuonyesha kama anajali furaha ya Nanaa kwenye tendo hilo.
Ilimradi yeye amefanikiwa, aliishia kumshukuru kwa juhudi zake.
Mawazo yakamrudisha kwa Jamal. “Jamal
ndio alinionyesha ni kama alikuwa akipunguza haja zake tu, mwilini mwangu.
Hapakuwa na penzi lolote pale. Hata nilipomwambia ninafahamu kuwa ana mke,
hakuonyesha kujali hisia zangu. Mbona sina bahati? Ni nini wanakutana nacho
huko kwenye mwili wangu kinachowachefua na kushindwa kunithamini?” Nanaa
aliendelea kuwaza moyoni akijiumiza nafsi yake kwa kujitupia lawama zote yeye
kama wanawake wengi wafanyavyo kunapotokea matatizo kwenye mahusiano. Mara
nyingi hupenda kujitafuta kosa/tatizo wao wenyewe, hata kama aliyekosea ni
mwanaume!
~~~~~~~~~~~~~~
Walikutana na foleni kubwa kwenye njia
yakuingilia Tabata. Wakasimama. Ndipo Nanaa akajua wanaelekea Tabata.
Alishindwa kuuliza wanaelekea Tabata ipi, kwani hakuwa amemuongelesha chochote
dereva wake, tokea amfunge mkanda. “Hivi nilisema hata asante kweli?” Nanaa
akajiuliza na kujishangaa. “Ustarabu ni kitu kidogo sana Nanaa jamani!
Hata ‘asante’ hukusema!” Akajisuta kidogo. “Nitakuwa nimesema
bwana!” Akajitetea tena nafsini mwake. “Hata kama sikusema,
nani alimwambia anifuate na mgari wa ajabu? Kwanza abiria huwa hawatakiwi
kufunga mkanda. Ajali ikitokea? Au kwa nini basi mikanda iliwekwa?” Nanaa
aliendeleza vikao vya mashitaka, utetezi, kujisuta na mengine mengi huko kichwani
mwake nakuonekana mtulivu zaidi kwa nje.
~~~~~~~~~~~~~~
Simu ya Geb ikaanza kuita. Nanaa akagutuka kutoka
mawazoni, na kujiweka sawa. Alishangaa mlio unalilia kwenye spika za gari.
Akatulia kidogo. “Huo sio mziki bwana! Hata kama ni ushamba sio kwa
kiasi hiki! Niache kujifanya mjinga wakupita kiasi.” Akaona Geb
anabonyeza kwenye kitufe kilichopo kwenye usukani wa hilo gari. “Kuna foleni kweli. Lakini tupo njiani tunakuja.” Geb
aliongea. “Amejuaje aliyempigia?” Nanaa akajiuliza huku
akitafuta kusoma kama kuna sehemu iliandikwa jina la mpigaji. “Mbona
anazungumza naye bila mwenzie kujitambulisha? Au namba imetokea mahali ndio
akajua? Lakini wapi sasa!?” Nanaa aliendelea kujiuliza asijue
anaonyesha hata nje jinsi anavyochungulia.
“Kama hutajali naomba upitie
matunda sokoni. Nilimtuma Danny, amesahau.” Alikuwa ni Grace. Nanaa akatambua sauti ya
bosi wake. “Lakini amemjuaje mpigaji? Maana ameanza kuongea moja kwa
moja baada ya kupokea tu!” Akaongeza juhudi za makusudi kuchungulia
kwa makini kwenye dashboard kuona kama kuna mahali kunaonyesha namba au
jina. “Hamna shida. Tunaweza kupitia sokoni.
Lakini ujue tutazidi kuchelewa. Kuna foleni kubwa kweli!” Geb
alijibu. “Ni afadhali mchelewe lakini mje na hayo
matunda. Fili ameshaanza kuulizia juisi yake. Nimemzungusha lakini naona
anaanza kunibadilikia.” “Sawa.” Geb akajibu na kukata simu.
Walikuwa wakizungumza kwa kutumia spika ya gari, kwa hiyo hata Nanaa alikuwa
akiwasikiliza. Grace aliongea kwa utulivu kama Geb. “Watakuwa wanaishi
wote na dada yake.” Nanaa akawaza.
“Naona twende hapo Buguruni sokoni, itakuwa
karibu zaidi.” Geb alimgeukia Nanaa, macho yao yakagongana. “Sawa.” Nanaa
alijibu na kukwepesha macho kwa haraka. “Lakini alijuaje aliyempigia?” Bado
Nanaa aliendelea kujiuliza lakini hakutaka kujiabisha zaidi. Aliona Geb anahama
upande mwingine kurudi barabarani ili kuelekea Buguruni sokoni. “Kwani
huko kwao hakuna magenge wanayouza matunda!?” Nanaa akaendelea kujiuliza.
Zena Kwa Nanaa
Tena.
S |
imu
yake ikaanza kuita. Yake haikutolea mlio kwenye spika za gari, bali kwenye
kipochi chake kidogo alichokuwa amekipakata. Akaitoa ikiwa imeshakatika.
Aliposoma jina la aliyempigia, akaguna kwa sauti. “Mmmh!” Geb
akamtizama. Ikaanza kuita tena. “We Zena? Umekosea
namba au ulitaka kunipigia mimi?” Nanaa aliuliza mara baada ya
kupokea. “Nanaa naye!?” “Nini?” “Nakupigia wewe
bwana. Za siku?” “Nzuri.” Nanaa akajibu, wazi alionekana bado yupo
kwenye mshangao. “Sasa mbona hata huniulizi na
mimi!?” “Nipo bado kwenye mshangao Zena! Siamini kama umenipigia mimi simu!”
“Hamna bwana! Nimekuwa na hamu na wewe. Ulishaanza field?” “Wewe Zena? Hebu
acha kunidanganya bwana. Niambie una shida gani?” Alizungumza naye
akijua walivyojawa hila kwake.
“Nakujulia hali tu shoga yangu.”
“Yameanza lini? Kwani Tia ameenda wapi?” “Nanaa naye?” “Zena? Usinifanye mimi
mtoto mdogo. Najua unashida. Wewe niambie tu.” “Mpaka naona aibu.” Nanaa akacheka. “Aibu ya nini sasa? Wewe niambie. Mimi nilielewa. Wala
usijali.” “Mmmh Nanaa wewe! Kweli?” “Kabisa Zena. Wala usijali. Niliwaelewa
kabisa wewe na Tia.” Walifika sokoni.
Geb aliegesha gari. Akabaki ametulia. Nanaa
hakuwa ameelewa ule ukimya. “Naomba usubiri kwanza
Zena.” Akamgeukia Geb baada ya kubonyeza sehemu ya MUTE ili Zena
upande wa pili asisikie. “Tumefika sokoni.
Unaweza kunisubiri tu kwenye gari. Nitajitahidi kuwahi kurudi.” “Hutataka
msaada?” Nanaa akauliza. Geb akafikiria kidogo. “Hapana.
Nitarudi baada ya muda mfupi sana. Nisubiri tu.” Akashuka na kumuacha
Nanaa ndani ya gari.
Akaendelea na Zena. “We
Zena?” “Kwani uko wapi?” “Buguruni sokoni. Kwani vipi?” Nanaa akauliza. “Kwanza nikuombe radhi shoga yangu. Nilikukosea.” Nanaa
akacheka. “Mbona kama huamini?” “Nakusikiliza.”
“Umenisamehe?” “Wewe Zena? Nimekwambia nilielewa. Mbona kama nahisi shida yako
ni kubwa sana? Unanianzia mbalii!” “Wala sio uongo shoga yangu. Nimepata
mwanaume.” Nanaa akaanza kucheka.
“Usicheke bwana. Sasa Tia yupo mbali.
Jamaa mwenyewe anaonekana yupo vizuri. Natamani anioe.” “Hongera Zena.” Nanaa alimpongeza
mwenzie bila hila. “Lakini nataka uje leo tutoke
wote. Na yeye akiwepo. Kisha kwenye mazungumzo yetu, nitagusia maswala ya ndoa
kwa ujumla, halafu wewe naomba uulize maswali kwa makini. Kama swala la kumpima
na mengineyo. Sitaki kupoteza naye muda.” “Ujue una kichaa wewe Zena?”
“Nisaidie shoga yangu. Mimi kama namuogopa!” “Sasa utaolewaje na mwanaume
unayemuogopa? Mtazungumzaje mkisha oana? Au utataka nihamie kwenu?” Zena
aliendelea kumbembeleza Nanaa, huku akimsikiliza hoja zake. Baada ya muda Geb
akarudi na mifuko mingi ya matunda.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akafungua mlango wa nyuma. “Subiri kwanza Zena.” Nanaa akamuweka tena kwenye
Mute na kumgeukia Geb. “Naweza kukusaidia? Naweza hata kuyapakata hapa
mbele.” Nanaa aliuliza na kuendelea kutoa ushauri wake wa kizamani! Mambo ya
kubeba mizigo ndani ya gari! “Haina haja. Nitayaweka tu hapa kwenye boksi
kubwa, yasikuchafue wala kuchafua gari.” Geb alijibu. Akaanza kuyapanga
huko nyuma ya gari kwa uangalifu huku Nanaa akimtizama akiwa amegeuka nyuma,
akabaki akimtizama vile anavyoyapanga kwa makini na usafi. “Anaogopa
kuchafua gari ya dada yake. Wala sio mimi.” Nanaa alijisemea moyoni.
“Labda atakuwa hana kazi ya maana, ndio maana
dada yake anamtumatuma.” Nanaa aliendelea kuwaza. “Wakati mwenzake
anasoma na kujiendeleza sijui yeye alikuwa wapi!? Kweli duniani watu hawafanani!
Yaani hawa ni mapacha, mmoja kafanikiwa, mwingine mzurulaji! Atakuwa na kazi ya
kujitengeneza kama mtoto wa kike, na kulala na kila mwanamke anayempitia.
Mwanaume gani kucha zimelingana kama anafanya kazi saluni ya kutengeneza kucha! Ananukia
kama mtoto wa kike! Mimi mwenyewe mwanamke lakini sinukii hivyo. Nywele
utafikiri anafanya kazi kwenye saluni ya kinyozi! Ndevu zimejipanga mstari,
utafikiri askari wa Uingereza! Basi kazi yake itakuwa ndio hiyo tu. Kujitengeneza
na kuzunguka na gari ya dada yake. Na macho hayo, wanawake watakuwa wanapangwa
mstari mpaka wanachoka.” Nanaa aliendelea kuwaza huku akimwangalia Geb
aliyekuwa ameinama nyuma ya gari akiendelea kupanga matunda.
~~~~~~~~~~~~~~~
“We Nanaa!? Akamsikia Zena akiita.
Akakumbuka kama amemsahau shoga yake kwenye simu. “Zena?”
“Uko wapi wewe!? Mbona sikuelewi?” “Nimekwambia nipo Buguruni sokoni.” “Mbona
patulivu hivyo? Soko hilo soko gani!?” “Nipo ndani ya gari na wewe.” Zena
akaanza kucheka. “Siku hizi shoga yangu umepata
bwana mwenye gari lenye AC?” “Leta dharau zako, uone kama nitakusaidia.” Geb
akafungua sehemu nyingine kwenye boksi, palepale nyuma ya gari alipokuwepo
akatoka na chupa mbili za maji. Akarudi ndani ya gari, akafungua ile chupa ya
maji, akamkabidhi Nanaa. “Naona jua kali sana. Karibu maji.”
“Asante.” Nanaa alishukuru akapokea yale maji yaliyokuwa
baridi. “Karibu.” Geb naye akajibu.
“Asante ya nini na wewe Nanaa?” Zena akauliza. “Siongei na wewe!” Geb akakunja uso. “Sio
wewe. Samahani ni...” Nanaa aliongea huku akinyoosha kidole kwenye simu.
Geb akaelewa. “Nani? Uko na nani wewe
Nanaa?” Zena aliendelea kudadisi upande wa pili wa
simu. “Nimesahau kuikausha hiyo chupa. Chukua hii napkins itakusaidia
kuikausha hiyo chupa, usilowe.” “Asante.” Baadhi ya matone kutoka kwenye
chupa aliyopewa ya maji ya kunywa, yalishaanza kumdondekea Nanaa. Akapokea zile
napkins. Geb akafunga mkanda, akaondoa gari.
“Mbona unasena asante kila mara? Umepata
bwana mwanajeshi nini? Naona nidhamu imeongezeaka!” “Zena! Naomba nikupigie
simu baadaye.” “Nanaa wewe! Tafadhali shoga yangu.” “Si umtafute Tia?” “Tia
yuko mbali na ameshaanza field. Hawezi kuja.” “Nitakufikiria.” “Acha kunifanyia
hivyo Nanaa. Kwanza Terry anakutafuta.” “Mmmh! Mimi ndio wakula makombo?” Nanaa aliuliza. “Sio makombo. Terry alinikataa kabisa. Anakutaka wewe.”
“Naona umesahau shida yako wewe.” “Basi. Naacha habari za Terry. Njoo basi leo
nyumbani tuzungumze.” “Kuna mahali nakwenda jioni.” “Mbona sasa hivi mapema tu.
Njoo kabla hujakwenda huko. Tupange mambo yetu vizuri. Tena ana best yake na
yeye hajaoa. Ukikubali tutoke wote, nitamwambia aje naye. Mambo yao safi.
Siwezi kukuunganisha kwa wanafunzi kama kina Terry.” Nanaa
akacheka.
“Akikusikia Tia.” Zena na yeye
akacheka. “Hawana hela bwana. Kutwa chips mayai!
Mtoko huu ni wa uhakika shoga yangu. Tutaenda kwenye mahoteli makubwa ya maana.
Usijivunge. Au ushapata bwana?” “Wapi? Nipo tu.” “Basi njoo nyumbani tuzungumze
vizuri. Lazima kieleweke.” “Ntakuja baadaye.” “Ndio maana nakupenda.” “Acha
kunidanganya. Nitakuwa siji!” “Nanaa naye!” Nanaa akacheka
kidogo. “Haya Zena. Nashukuru kunikumbuka.
Nitakuona baadaye.” Alimsikia Zena akipiga kelele za kushangilia.
Nanaa akacheka na kukata simu.
Alibaki na tabasamu usoni. Gafla akakumbuka
mazungumzo yake na Zena. Tabia yake yakumuunganisha na wanaume. “Mungu
wangu! Sijui amenielewa huyu?” Nanaa akawaza. Akaamua kumtumia ujumbe
Zena baada ya kufikiria tena kidogo. ‘Sina uhakika
kama umenielewa vizuri Zena. Naomba usiniunganishe na yeyote, yule. Hata
aweje. Bado nipo mapumzikoni. Naomba nikusaidie ishu yako tu, basi. Sitaki
mwanaume kwa sasa.’ ‘Nanaa naye!’ ‘Kweli tena Zena. Tafadhali sana. Nimeamua
hivyo na naomba ibaki hivyo. Nitakuja kwa ajili yako, basi.” “Lakini…” Wakaendelea
kujibizana mpaka wakawekana sawa. Baada ya majibizano hayo ya jumbe na
kuridhika kuwa Zena ameelewa, hatamtafutia mwanaume, akarudisha simu yake
kwenye pochi. Alishangaa kuona wamesimama mbele ya geti kubwa tu. Akajua wamefika.
Akajua ameongea na Zena kwa muda mrefu, au
hawakuwa wakikaa mbali na hapo sokoni. Labda maeneo ya Tabata ya mwanzoni! Pia
hakuuliza. Geti likafunguliwa, wakaingia ndani. Nyumba ilionekana bado mpya.
Kulimwagwa vitofali vizuri. Kuanzia getini mpaka mlangoni. Baiskeli ndogo
ilikuwa pembeni, akajua itakuwa ya Fili tu.
Kwa Mara Ya
Kwanza, Nanaa Nyumbani Kwa Bosi Wake.
“Karibu.” Nanaa alifungua
mkanda. “Asante. Nikusaidie nini?” “Nisubiri tu twende wote ndani.
Nitabeba tu mwenyewe, sio vitu vingi.” Geb alitoa boksi zima. Lilikuwa ni
boksi la plastiki, lenye mishikio miwili. Lilionekana ni maalumu kwa kubebea
vitu kama hivyo. Akafunga mlango akamkaribisha ndani. Wakaongozana mpaka ndani
sebuleni.
“Karibu Nanaa, nipo huku jikoni. Msichana wa kazi
ameondoka leo asubuhi, amefiwa. Natayarisha chakula cha mchana, tukishakula
ndio tuanze kufunga zawadi.” Nanaa akamfuata Geb huko jikoni kulikosikika
sauti ya Grace. “Asante na pole kwa shuguli.” Nanaa
akaingia. “Asante mwaya.” Grace alijibu na tabasamu. “Mama yuko
wapi?” Geb akauliza mara baada yakutua mzigo. “Alikuwa anasinzia
hapa, Fili amempa nyanya, kala nusu, nusu amekufunikia hapo kwenye meza.
Ameniambia ukija uile.” Grace aljibu, Geb alinawa mkono akasogelea hiyo
sahani. “Halafu nimempatia maparachichi.” “Atafurahi kweli. Alikuwa
ananiambia anahamu nayo.” “Tena nimepata yale mazuri anayopenda.” Geb
aliendelea kukila kile kipande cha nyanya huku akiongea na dada yake.
“Fili yuko wapi?” Nanaa akauliza. “Yupo
na bibi yake huko chumbani. Na anavyopenda kuongea mwanangu yule, sijui kama
mama atakuwa ameweza kulala!” Nanaa akacheka. “Ngoja nikamwangalie
mama. Nitakuja kukusaidia kutengeneza juisi.” Geb alitaka
kutoka. “Ungenielekeza tu mimi, nitatengeneza.” Nanaa akamuwahi kabla
hajatoka. “Anza basi kuosha matunda mawili mawili kutoka kwenye hilo
boksi. Nikirudi nitakutolea tangawizi na Blenda, nikuonyeshe tunavyosaga. Ni
rahisi tu.” Geb alitoka akamuacha Nanaa anaanza kuosha matunda.
“Pole.” “Nimeshazoea. Wasichana huwa
hawakai hapa kwangu, sijui kwa nini! Mwanzoni nilifikiria wanalemewa na kazi,
tukawa tunawasaidia, lakini wapi. Nikafikiri ni sababu ya Fili.” “Kwa nini Fili!?”
“Mtoto ni mtundu huyo, hujawahi kuona. Yupo kama baba yake. Akianza kuongea
mpaka kichwa kinauma na anataka umsikilize. Nahisi ndio maana wanatukimbia,
wanachoka! Nikataka kumuanzisha shule mapema ili niwe natoka naye asubuhi na
kurudi naye jioni, ili kuwafanya wasichana wa kazi wasitukimbie, lakini Danny
hataki aanze shule kabla yakufikisha miaka 5. Kwa hiyo wasichana wa kazi
wakitukimbia, inabidi wote tupeane zamu ya kubaki naye hapa. Lakini bibi yake
ndio huwa anakuwa naye zaidi, kwa kuwa hachoki.” Nanaa akacheka.
“Kweli tena. Bibi yake anatabia kama za Geb. Huwa
hawachoshwi na kelele nyingi, wanawezana naye. Kwa hiyo muda mwingi hata tukiwa
na mfanyakazi, bibi yake huwa anachelewa kwenda kwenye shuguli zake.
Anamuhudumia Fili. Anahakikisha amemuogesha, anamuacha amekula ndio anaondoka,
ili msichana wa kazi asiwe anahusiki sana na mtoto, nayo pia haikusaidia!”
“Poleni.” Nanaa akaona ampe pole tu.
“Haya na anko wake pia akaanza kazi ya kufua nguo
zote. Mara mbili kwa juma. Tena wakati mwingine akiona nguo nyingi anafua mpaka
usiku na kukunja nguo zote, anampangia Fili kabatini kwake, na mimi nakuwa
napika chakula cha usiku mara nyingi, ili tu kumpunguzia msichana wa kazi
majukumu, lakini pia naona hawakai. Sasa sijui itakuaje, lakini kwa kuwa
ametimiza miaka mitano, ni heri aanze tu shule, nitachanganyikiwa bure.” “Pole.
Na Danny?” Nanaa aliuliza baada yakuona dad mtoto hayupo kwenye ratiba ya
ulezi.
“Huyo sitaki akae na mwanangu siku nzima.
Mwanangu anakuwa hana raha! Mkali sana kwa Fili. Anamlea kama mtu mzima bwana!
Hapana. Yaani nikimuacha mwanangu na Danny hata masaa mawili tu, tumbo linauma!
Kila saa nampigia simu au naomba Geb arudi aje awaangalie. Najikuta kazi
zenyewe zilizonipeleka ofisini sifanyi, nina kazi yakumpigia simu Danny,
kumkumbusha umri wa Fili. Ndio tumeona tuache kumpa yeye hiyo kazi ya ulezi
tubaki nayo sisi tu.” Nanaa alikuwa akicheka sana.
Geb alirudi akiwa amembeba Fili
mabegani. “Usimuweke hapo juu bwana! Ataanguka. Si unamjua hawezi
kutulia?” “Nimemtoa kule kwa mama ili apumzike kidogo. Anaruka ruka tu
kitandani mama hawezi kulala.” “Tulia basi kidogo Fili mwanangu. Huchoki? Au
nimpigie simu dad arudi aje akuchukue?” “Hapana mama. Natulia” “Basi tulia.
Tumalize kazi haraka ili tuwahi kwenye birthday yako.” Tayari Grace
alionekana kulemewa. Alishika hiki na kuacha nusu.
“Mwache bwana. Mimi si nipo? Hawezi kuanguka.
Haya nenda kamsalimie Nanaa, halafu uje ukae hapa kwenye meza.” Alienda
kusimama mbele ya Nanaa akabaki akimtizama huku anacheka. “Anajua
kuchanganyikiwa vibaya huyu! Sasa unacheka nini badala usalimie?” Mama
yake alidakia huku akiendelea na shuguli zake. “Hapo anataka uiname,
akubusu.” Geb aliongeza, wakacheka. Fili alienda kuvuta kiti mpaka karibu
ya Nanaa, akapanda na kumfikia Nanaa. “Ningeinama tu.” Nanaa
akacheka. “Uiname umpunguzie shuguli? Anapenda shuguli huyo!” Grace
aliongeza. Fili akambusu shavuni kisha akamkumbatia. “Asante
Fili.” Nanaa alishukuru na tabasamu la aibu usoni. Hakuzoea.
“Karibu. Umekuja kuishi na mimi?” Fili akauliza. “Nitakuchukua
twende tukaishi wote kwangu.” “Afadhali. Umchukue moja kwa moja. Lakini James
anaweza kumrudisha usiku huyo.” Grace aliongeza na kufanya Nanaa
acheke. “Wewe ndio uje uishi hapa kwetu.” Fili aliongeza. “Kwa
nini?” “Dad amesema nisubiri mpaka nisome, nipate mahela mengiiiii.” Fili
alionyesha ukubwa wa pesa anazotakiwa awe nazo kwa kupanua vimikono vyake. “Halafu
ndio amesema nikishapata pesa niende kwa anko James, tumlipe hela, nikuchukue.
Lakini amesema nikikuchukua nisirudi hapa, nikupeleke kwangu.” Walicheka
sana.
“Yaani Danny jamani!” Grace akalalamika
akicheka. “Lakini wewe ukija hapa sasa hivi, usimwambie kama mimi ndio
nimekwambia uje tuishi wote hapa. Wewe umwambie umeamua kuja kuishi hapa na
mimi, wala sijakuita. Halafu hawezi kukufukuza.” Fili aliongeza na
kuwafanya wote wazidi kucheka, Geb alikuwa akitingisha kichwa. “Hapa kazi
ipo! Akili ya ujanja ujanja kama baba yake. Wewe? Tulikwambia nini juu ya
kusema uongo?” “Hapo anko nitakuwa mimi sijadanganya. Nanaa atakuwa ndio
amekuja hapa.” Fili alijitetea.
“Kwa hiyo unamfundisha Nanaa kusema uongo?”
“Hapana anko.” “Na hapo pia unasema uongo. Si umemfundisha aje hapa asikutaje
kwa dad wako kama wewe ndio umemkaribisha?” Fili alinyamaza kidogo kisha
akauliza. “Kwani huo ni uongo?” “Sasa je? Hakuna kusema uongo.” “Basi
Nanaa. Usiseme tena. Samahani anko.” “Haya, nenda kacheze, usubiri mpaka upate
hela kama alivyokwambia dad, ndio utaenda kumlipa anko James, umchukue Nanaa,
umpeleke kwako sio hapa. Sawa?” Fili akapooza. “Sawa anko. Kwani
utamwambia dad?” Akauliza kwa upole. “Ukirudia tena kumfundisha Nanaa
kusema uongo, ndio nitamwambia.” “Mimi sirudii tena. Usimwambie dad wangu.”
“Ujue nitakuwa nakusikiliza kila neno unaloongea. Usirudie tena. Haya
nenda.” Alishuka kwenye kiti, akatoka.
“Afadhali umemuweza. Fili anaongea jamani! Halafu
hasahau jambo kama baba yake. Hapo ataenda kumsimulia kila mtu kuwa anataka
kuoa lakini dad amemwambia atafute kwanza pesa.” Wote waliendelea kucheka
wakati Grace akisimulia vituko vya mwanae, Geb anatengeneza juisi. “Sasa
si atarudi tena kwa bibi yake?” Nanaa aliwakumbusha, Geb akatoka kwa
haraka kwenda kumtafuta, akarudi amemshika. “Alishafika chumbani kwa bibi
yake nakuanza kumsimulia habari zake zisizo isha. Nimekwambia kaa
hapa.” Geb akampandisha tena juu ya meza. “Msimulie Nanaa badala ya
bibi.” Fili akaanza kusimulia huku akiruka ruka hapo juu ya meza.
“Utaumia Fili mwanangu! Tulia basi.” “Naweza
kuruka hapa, mama. Juu mpaka chini. Muulize anko.” Fili
alimchonganisha anko wake. “Wewe Fili?” Geb alimshitua huku
akimkonyeza anyamaze lakini hakunyamaza. “Namwambia ukweli mama yangu.
Mwenzio anko sio muoga. Ananiruhusu nipande halafu niruke.” Nanaa alicheka
sana. “Geb jamani!” Grace akalalamika. “Hawezi kuumia bwana!
Huyu ni Spider man. Acha hofu.” “Usikubali awe anaruka!” “Hana neno
bwana. Kwanza hapo pafupi.” Geb alitetea. Alikuwa akimruhusu kuruka kwa
siri, akiona mama yake hayupo. Alikuwa akivaa nguo zake za Spieder man
na kumuomba anko wake aruke kama Spider man.
“Kwani ni lazima aruke? Tafuta mchezo
mwingine. Umesikia Fili?” “Spider man lazima aruke mama.” “Hapana Fili
mwanangu. Mwambie dad au anko wakutafutie kazi nyingine za Spider man,
ufanye. Kuliko kuruka. Ukivunjika, mama ataumia sana.” “Basi mama yangu.
Nitaruka kidogo tu.” Geb na Nanaa wakacheka. “Kwani lazima kuruka
Fili? Acha tu mwanangu. Utaumia!” Mama yake alisisitiza huku akimpa juisi
aliyokuwa ametengeneza Nanaa. Alimuwekea kwenye chupa yake maalumu yenye picha
za Spider man, akaanza kunywa, ndio akanyamaza. Geb alimbeba na kutoka
naye pale jikoni akabaki Nanaa na Grace wakimalizia usafi.
Grace alipanga chakula mezani, akamuita kila mtu
aje kula. Wakati wamekaa mezani ili wale, mama yao naye akatoka chumbani.
Umbile alifanana sana na Grace kama alijizaa huyo mwanamke, hata rangi
alifanana na watoto wake lakini sio yale macho. Nanaa akasimama. “Nilikuwa
naambiwa mchumba umefika.” Yule mama alitoa mkono na kumpa Nanaa, wote
wakacheka. “Naona sasa hivi kila mtu anamfahamu Nanaa. Kila anayepiga
simu, anakaribishwa kwenye birthday na kuambiwa Nanaa atakuwepo. Mwanangu
amependa jamani!” Grace alidakia. Wote wakacheka. “Shikamoo
mama.” Nanaa alisalimia huku akicheka. “Marahaba. Karibu
sana.” Yule mama alikaa.
“Mbona sahani yako haina nyama?” Mama yao akamuuliza
Geb. “Nimeshakula zote.” Geb akajibu. “Chukua na hizi zangu.”
“Kula bwana mama! Nikitaka nitaongeza. Mbona bado zipo tu nyingi.” “Basi chukua
hii moja.” Walibishana kwa muda, mwishowe Geb akachukua nyama kutoka
kwenye sahani ya mama yake. “Hajawahi kukua huyo kwa mama. Utawazoea tu.
Mama akila kitu, anataka na mwanae ale. Hata kama hayupo nyumbani, anakula
nusu, nusu anamuwekea.” Grace alimwambia Nanaa, Nanaa akacheka kidogo na
kuinama. “Mvivu sana wakula huyu. Usipomsisitiza kula, ndio basi tena.
Hizo nyama zilizofanikiwa kuingia huko tumboni ndio kashamaliza hapo. Huo mdomo
hautapitisha tena kitu kingine.” Mama yao alimtetea Geb, Nanaa alicheka
tena kidogo na kuinamia sahani yake tena, akaendelea kula bila yakuongeza neno.
“Watakuwa wanamdekeza ndio maana hataki
kutoka nyumbani kwa dada yake, akaishi peke yake ajitegemee. Amenikalia
kudeka!” Nanaa aliwaza. Wakala lakini hawakuwa wakizungumza sana,
mpaka Danny alipoingia ndio akaanza kuongea nakuwafanya wote waanze kucheka.
Kitu kidogo, Danny alikikuza, akakisimulia kwa mbwembwe nyingii na kuwafanya
wote wacheke. Fili alianza kusinzia, Grace akambeba kwenda kumuogesha ili
amlaze angalau apate usingizi wa mchana. Nanaa alitoa vyombo pale mezani
wakisaidiana na Geb.
“Acha niwasaidie tu kusafisha. Sio
vingi.” Nanaa alitaka Geb ampishe pale kwenye sinki. “Ni vyakupanga
tu hapo kwenye mashine. Huwa mashine inatusaidia kuosha. Labda sufuria ndio
zakuziosha. Ngoja nikuonyeshe.” Geb alisuuza kidogo, akavipanga vyote
kwenye mashine iliyomtoa macho Nanaa, hakuwahi kuona mashine yakuoshea vyombo.
Ili kuepuka mshangao usoni, akaamua aanze kuosha sufuria. “Sasa kwa
nini wasichana wa kazi hawakai kama kuna mpaka mashine za kuoshea vyombo!” Nanaa
akazidi kushangazwa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Simu ya Geb iliita. Akatoa mfukoni na
kupokea. “Vipi?” Aliuliza. “Nimetoka kazini, nimechoka.” Akasikia sauti ya
kike upande wa pili. “Njoo upumzike hapa kwetu.”
“Fili anakelele bwana!” Yule msichana akalalamika, Geb
akacheka. “Ameenda kulala, hatakusumbua.” “Acha tu
niende kwangu. Nipumzike, nikiamka ndio nijiandae kuja kwenye birthday yake.”
“Njoo basi, angalau nikuone, Liz!” Geb akambembeleza. “Kwani una hamu na mimi?” Liz akauliza. “Si ndio maana nataka uje?” Liz alisikika
akicheka. “Niache nikalale kidogo, Geb. Nimechoka.
Tukitoka kwenye sherehe tutakuwa wote, mpaka utanifukuza.” “Sawa mama. Baadaye
basi. Ulale unono.” Liz alisikika akicheka tena. “Asante.” Wakakata simu.
~~~~~~~~~~~~~~~
Mara Grace akaingia. “Usinge hangaika
kuosha hayo masufuria, Geb angeosha tu.” “Hamna shida. Kwanza namalizia.” “Basi
ukimaliza uje tukae hapo sebuleni, tupumzike kidogo. Fili amelala.” “Mbona Fili
mwenyewe sio mtundu wa hivyo?” Geb na Grace wakaangaliana na kucheka. “Kweli!
Nipeni mimi siku za jumamosi niwe nakaa naye.” “Kama ulikuwa unatania ujue ndio
imekula kwako. Na hivi sina msichana wa kazi, jumamosi ijayo asubuhi na mapema,
nakuletea kwako.” Nanaa akacheka. “Kweli tena, wewe mlete tu. Ndugu
yangu ana mtoto wa kiume, yule mtoto ndio mtundu. Huwa kaka akienda nyumbani
Moshi kusalimia, huwa anachoka. Anasemaga ameshaona watoto watundu, lakini pale
mwisho.” “Mtoto wa Viola?” Grace akauliza na kumfanya Nanaa kushangaa
kidogo.
“Kumbe unawafahamu dada zake
James?” Wakacheka. “Alishawahi kufika hapa. Zamani kabla ya kupata
mtoto. Alimpenda sana Geb, lakini tatizo la Geb kazubaa. Sasa hivi angekuwa na
mtoto mkubwa tu na Viola.” Nanaa alitulia kidogo kama anawaza. “Tena
hata Vai pia alishafika hapa. Walikuja kumtembelea kaka yao hapa Dar, James
akawaleta waje watusalimie.” “Kumbe! Sikuwa nafahamu kama mnafahamiana vizuri
hivyo!” “Sana tu.” Grace akaitika bila shaka. Nanaa alikosa raha asijue ni
kwa nini. Alikausha mikono, akabaki amesimama kama aliyeduwaa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Kumbukumbu za mateso ya nyumbani kwa mama yake
mkubwa zilimjia. Vile Viola alivyompokonya mwanaume wake, akazaa naye, huku
akipongezwa na mama yake bila kujali machungu aliyomsababishia. Alimkumbuka
Alex, ahadi walizokuwa wamewekeana, majina ya watoto waliyokuwa wameamua kuwapa
pindi watakapo jaliwa watoto hao. Lakini akaishia kuzaa na Viola!
Alex alifanikiwa kulipa mahari kama alivyoahidi,
Viola akabaki akimsubiri amalize chuo ili wafunge ndoa, lakini walikuja kusikia
Alex alioa mwanamke mwingine, kwa haraka sana, mara tu baada yakumaliza chuo
chake. Ilimchukua muda mrefu kwa Nanaa kuja kurudi nyumbani kwa mama yake
mkubwa, Moshi. Kila James alipokuwa akienda kusalimia, Nanaa alikataa kurudi.
Alimuomba ampe kwanza muda wakupona. James alikuwa akimletea habari zote ya
kinachoendelea nyumbani kwao, lakini Nanaa hakuwa akienda kusalimia na alikata
mawasiliano kabisa.
Yalikuwa ni majuma machache sana yaliyopita kabla
yakuanza kazi kwa Grace ndipo alipoona ni vyema kuungana na James, kwenda
kusalimia nyumbani kwao. Siku alipokwenda kusalimia, alijuta. Asubuhi ya siku
inayofuata baada ya kutua tu Moshi, mama yake mkubwa alimuita kutoka chumbani
alipokuwa amelala na kumtaka aende hapo sebuleni kwa mazungumzo. Nanaa alivaa,
akaosha uso, na kwenda kukaa alipokuwa amekaa yeye na watoto wake. Bila hata
kujua linaloendelea kwenye maisha ya Nanaa ambaye hawakuwa wameonana kwa zaidi
ya miezi 24, tena waliachana katika hali ya machungu, yule mama alianza kumsema
sana Nanaa.
James na baba yake walikuwa wametoka, kwa
hiyo alimsema vile atakavyo. Alimsema Nanaa bila kupumzika tena akitumia maneno
machafu ambayo asingethubutu kumsema mtoto wake aliyemzaa. Alimsema vile
alivyonyimwa shukurani. Amefanikiwa kidogo tu na kusahau alipotoka. “Usifikiri
hapo ulipo umefika mwenyewe! Hata hapo unapoishi sasa hivi ni kwa James, mtoto
wangu. Tulimsomesha na kumtunza kwa jasho letu. Sasa hivi wewe usiye na
shukurani ndio unafaidi jasho la mtoto wangu! Umekuwa mzigo kwenye maisha yake
mpaka anashindwa kumsomesha mdogo wake, anakusomesha tu wewe mtu baki!”
“Huna shukurani kabisa! Umeondoka hapa,
unashindwa hata kunijulia hali! Mwenzio anashindwa kusaidia nyumbani kwao, kwa
kuwa wewe umekuwa mzigo kwake! Unajidai msomi kwa kuwa umefika chuo kikuu! Tutakuona
utafika wapi.” Alimsema Nanaa mpaka aliposikia gari ya mumewe wakirudi
nyumbani na James, ndipo akanyamaza na kubadilika kuwa mwema kwake kana kwamba
sio yeye na kubadili mazungumzo mara James alipoingia tu ndani.
“Nanaa amemshauri Vai mrudi naye Dar na yeye
akatafute shule asome.” Alimuwahi James kabla hajakaa, na tabasamu usoni. James
alipoona sura ya Nanaa alijua kilichokuwa kikiendelea na kujua ule ulikuwa
uongo. “Mbona baba ameniambia kuwa Vai anataka kuolewa? Sasa anasoma lini
na kuolewa lini?” James akauliza huku akikaa. “Kwani mtu akiolewa
hawezi kurudi shule?” “Nini kinaanza sasa?” James akauliza
tena. “Vyote vinaweza kwenda kwa wakati mmoja.” Mama yake
alimjibu. “Basi kama ndio hivyo akasomee kwake na mumewe
amsomeshe.” James alijibu.
“Mwanaume mwenyewe hana pesa! Sijui
tutaishije?” Vai aliongeza. “Nanaa twende nikakuonyeshe
kitu.” James hakutaka kuingilia kabisa. Alishawazira wadogo zake.
Alichukia vile mama yao anavyowakingia kifua, hata walipokuwa wakikosea,
hakutaka waonywe. “Sasa utaondoka na Vai, ili aanze kujiandaa na
safari?” Mama yake alirudia tena. “Hapana.” James alijibu bila
hata kufikiria. Kama aliyekuwa ameshaandaa jibu tayari.
“Kwa nini!?” Mama yao aliuliza kwa mshangao
na hasira. “Yaani upo radhi kumsaidia huyu mtu baki na sio mdogo wako,
ambaye ni damu yako?! Tumeshamsaidia huyo Nanaa vyakutosha. Ni
wakati sasa atafute maisha yake, apishe nafasi ya wenzie wapate msaada. Kwanza
bibi yako ana shida.” “Nimeshazungumza na bibi na nimeshamtumia pesa za
matumizi.” “Sasa nini kinachokushinda kumchukua Vai?” James alirudi kukaa
kwenye kochi.
“Unakumbuka Viola na Vai walishakuja Dar ili
waishi na mimi? Unakumbuka kuwa mimi ndiye niliwarudisha? Nilikueleza sababu
zote za kwa nini nawarudisha nyumbani. Nilishindwa kuishi nao. Nafasi
niliyotaka kuwapa wao, sasa hivi nimempa Nanaa na anaitumia vizuri. Nanaa
amekuwa msaada kwangu. Tunaheshimiana. Hawa watoto wako walinitia aibu kwa
marafiki zangu, mpaka ikabidi niwafukuze. Kila mwanaume walikuwa wakimtongoza
wao, mpaka waume za marafiki zangu waliwatongoza! Kama rafiki zangu wangekuwa
watu wasio na ndoa za kueleweka si wangevunja ndoa zao? Na pia hawana uwezo
wakufanya kazi za nyumbani kama Nanaa. Wakati naishi nao, Viola na Vai,
ilinilazimu kuwatafutia msichana wa kazi wakuwahudumia wao, wakati wao wamekaa
tu, wanaangalia tv, mchana na usiku. Shule walikataa, wakaishia kuniingiza
hasara zakulipa ada bila wao kuhudhuria darasa hata moja. Nanaa amekubali
kusoma. Anahangaika na shule, amebakiza kidogo tu amalize.” James
alijieleza kwa kituo bila jazba, ili mama yake aelewe.
“Watu wanabadilika James. Dada zako wamebadilika
sana.” “Basi watafute chuo hapahapa Moshi waanze kusoma. Kama baba ameshindwa
kuwasomesha, mimi nitatuma hiyo pesa itakayohitajika ya ada.” “Sijashindwa
kumsomesha hata mmoja wao hapo. Muulize Viola kama sijambembeleza ajikaze arudi
shule. Tena nilimwambia nitamsaidia kumtafuta mtu wakumlelea mtoto wake, wakati
anasoma, lakini amekataa. Ni week iliyopita tu nilimkumbusha tena, akakataa.
Jana pia nilizungumza nao wote wawili kutaka warudi shule, lakini wamekataa.
Sijashindwa kuwasomesha hata kidogo.” Baba yao aliingilia. “Nanaa
twende.” James akasimama na kutoka nje kumsubiria Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Alikumbuka yale maneno yote. Akakumbuka vile
Grace naye alivyosema anawafahamu vizuri sana. Aibu na hofu ikaanza
kumwingia. “Sasa sijui walimtaka mume wa Grace, Danny au wote wawili?
Aibu gani hii! Kumbe muda wote nipo hapa wananiangalia tu, kumbe wanazijua
habari zetu! Sijui niage niondoke?” Nanaa alibaki ameduwaa, huku Grace
na Geb wakizungumza palepale jikoni, akasikia wanacheka. Akagutuka kutoka mawazoni.
“Twende basi.” Grace alitoka pale
jikoni, akamfuata nyuma, wakaenda kukaa upande wa sebuleni, Nanaa akiwa
amepotelea kwenye mawazo. Zile kumbukumbu za maneno ya mama yake mkubwa
zilishamuharibia utulivu wa moyoni. Akabaki kimya nakushindwa kuchangia lolote.
Geb naye alitoka akaenda kukaa pale akisaidia kufunga zawadi.
Mara waliona mlango unafunguliwa. “Liz!” Geb
alishangaa. “Si ulisema una usingizi?” “Nimekubali ile ofa ya kuja kulala
hapa hapa. Shikamoo bibi wa Fili.” Liz alimgeukia mama yao
nakusalimia. “Marahaba. Karibu.” Alijibu kwa ufupi tu mama huyo akanyamaza. “Njaa
inauma, nina usingizi, sijui nifanye lipi niache lipi?” “Nilikwambia napika.
Chakula tumekirudisha sasa hivi kwenye friji. Wewe nenda kale ndio
ukalale.” Grace alijibu, Geb akasimama, Liz akambusu
midomoni. “Twende nikusindikize ukale, ndio ulale.” Wakaondoka na Geb
kuelekea jikoni, akamsikia Liz akiongea na kucheka akiwa na Geb huko huko
jikoni. Akajua ni wapenzi.
“Liz! Liz!” Grace akaita kama aliyekumbuka
kitu. “Nimesahau kukutambulisha kwa Nanaa. Njoo.” Liz akatoka. “Huyo
ndio Nanaa.” “Mchumba wa Fili?” Liz akauliza na kuamsha kicheko. “Amemng’ang’ania!
Kabla hajalala alikuwa anamfundisha Nanaa uongo wakumwambia baba yake ili
ahamie hapa.” “Aje amlee?” Liz akauliza. “Naona. Maana wasichana wa
kazi wote wanamkimbia. Lakini Geb akamgombesha aache uongo, naona akapooza
mpaka akapata usingizi.” Wakacheka tena.
“Sasa Nanaa ujiandae. Mume yule hamna kulala
sababu ya maneno mengi. Sura ya upole kama mama yake. Akikuangalia hivi na
macho yake yale, utafikiri ni malaika ambaye hajaanza kuongea. Lakini ngoja
afungue mdomo, ndio utajua ni mtoto wa Danny. Jana amenipigia simu ananieleza
habari zako, mpaka nikapitiwa na usingizi. Mtoto hachoki! Kila nikimuaga
ananiita, ‘Anti Liz, nimekwambia Nanaa ni
mzuri?’ Namwambia ulishaniambia zaidi ya mara hamsini,
anasema ‘Ndio unatakiwa usisahau sasa’.” Kila
mtu alikuwa akicheka. “Sasa Nanaa ujiandae. Hajuagi kuongea kwa kifupi
huyo mumeo, na hachoki.” Liz alirudi jikoni, baada ya kula wakaongozana na
Geb chumbani.
~~~~~~~~~~~~~~~
Japokuwa alikuwa akicheka, lakini moyoni
alishakosa amani, asijue ni nini kinachomsababishia ile hali. Kama ni maneno ya
kashfa aliyokumbuka kuambiwa na mama yake mkubwa, au ujio wa Liz, au aibu ya
ndugu zake hapo kwa kina Geb, hakujua ni lipi, lakini moyoni alikuwa amechafuka
kabisa. Alibaki kimya mpaka walipomaliza. Grace alikuwa akiongea na mama yake
huku Danny akiangalia mpira.
“Naona tumemaliza mapema na bado tuna muda mwingi uliobaki wa sherehe ianze. Naomba niondoke, kuna mahali nataka nipitie kabla ya kuja huko kwenye birthday.” Nanaa aliaga baada yakumaliza. “Basi ngoja nimuite Geb akupeleke.” Grace alitaka kusimama. “Hapana. Mwache tu apumzike. Ningependa kwenda peke yangu.” Grace akacheka. “Haya Mkwe wangu. Lakini usimsaliti tu mwanangu!” Grace alirudi kukaa, akamfanya Nanaa acheke kidogo. “Wala usijali. Nitakuja kwenye sherehe, nicheze naye.” Nanaa alichukua pochi yake akamuaga mama yao na Danny aliyekuwa akishangilia mpira kwenye tv, akatoka na sononeko moyoni.
~~~~~~~~~~~~~~~
Kwa
mara ya kwanza Nanaa akiwa amekusudia kuachana na mapenzi. Akiwa ameumizwa
vyakutosha, anapatwa na hisia za ajabu kwa Geb ambaye anamvutia kwa ajabu
asijue ni nini! Hamfahamu Geb hata kidogo, ila kwa hakika anajua ana mpenzi
wake, Liz. Liz si msichana wa vichochoroni. Anafahamika mpaka kwa mama yake
Geb. Anaonekana kufahamiana na Grace vizuri tu. Na ni Anti wa Fili!
v
Nini atafanya?
v
Je, atatupilia mbali hisia hizo ngeni zinazomliza na kumuumiza moyo?
v
Nini kitatokea kwenye sherehe ya Fili?
v
Na, Je, Zena ataheshimu ombi la Nanaa?
Usikose Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment