Wapi akafanye field! Akaanza kuhangaika kutafuta
maofisi ambayo angefanya field hiyo lakini angalau wamlipe pesa kidogo ya
kumsaidia hata nauli na hata wakiweza kumuajiri mpaka chuo kifungue, lakini
akakosa. Hapo ndipo ikambidi azungumze na kaka yake, ili amsaidie kumtafutia sehemu yakufanya
field. James akamwambia ampe muda kidogo wa kutafuta.
Baaada ya kama siku mbili akamwambia amefanikiwa
kumpatia kazi mahali. Amepata ahadi ya kazi kwa muda ambao muhasibu wa hiyo
ofisi atakapokuwa likizo ya uzazi. Nanaa alifurahi sana na kumshukuru Mungu
wake.
~~~~~~~~~~~~~~
S |
iku
hiyo ya jumamosi asubuhi Nanaa alisikia watu wakicheka na kaka yake sebuleni
kwao. Ndio na yeye alikuwa ameingia tu chumbani kwake baada ya kumaliza shuguli
zake. Akaona atoke aangalie ni kina nani wanao mfanya kaka yake acheke hivyo.
Alikuta ni mtu na mkewe. Wakitaniana sana na James. Akajua lazima watakuwa
marafiki wa James. “Njoo Nanaa usalimie na uongee vizuri na Grace. Ndiye
atakuwa bosi wako. Hakikisha unamuelewa usibaki unayashangaa hayo macho yake, akamaliza
kuongea hujaelewa kitu.” Nanaa akamtizama Grace vizuri. Kweli alikuwa na
macho yakuvutia. Akacheka.
“Usicheke mtoto wa kichaga. Tumekuja mjini
kuzisaka pesa. Changamka na usipumbazwe na hayo macho na sauti hiyo, ukashindwa
kuomba pesa kubwa. Maana wakati tupo pale chuo kikuu cha Mlimani, huyo Grace
alizungusha vichwa vya wasomi wenye shahada zao, wafanyakazi,
maprofesa, na wafanyabiashara wa jiji. Watu wazima tukabaki kama
wehu. Muulize Danny. Mimi mwenyewe nilitaka kuoa, lakini nikashindwa. Kila
alipokuwa akiniangalia, maneno yalikuwa hayatoki. Mwenzangu Danny akaamua kufa
kiume, lakini karibia tumkimbize Mirembe kwa kuchanganywa na Grace.” Wote
walianza kucheka tena. Lakini Nanaa akawa ameshapata utambulisho
wakujitosheleza. Danny ni mume wa Grace bosi wake. Marafiki wa kaka zake
waliosoma pamoja.
“Achana nao hao. Wanapenda kunichokoza tu.
Tutaelewana Nanaa, usiogope.” Grace alijibu huku akicheka. “Ashindwe
kuelewa Danny mpaka leo, ataelewa mdogo wangu huyo? Kwanza hayo macho kwa mara
ya kwanza yakikuangalia unakuwa kama unapumbaa hivi. Sasa Danny ndio alikuwa
anatuchosha. Pesa hana, anamtaka Grace. Ukiangalia mgongo wa Grace, Danny
alikuwa anazidi kuchanganyikiwa. Basi tukajua pakumpatia Danny. Tukitaka
kumchanganya, tunamtisha, tunamwambia tumemuona Grace amepakizwa kwenye gari
zuri sana, halafu huoni ndani, vioo vyeusi. Basi weee, Danny
anapagawa!” James aliongeza nakuwafanya wazidi kucheka.
“Nakwambia nilipambana mpaka
nikafanikiwa.” Danny akaongeza. “Na usifikiri akikwambia
alipambana anadanganya? Nilikuwa sina raha. Alikuwa ananisumbua kupita maelezo.
Yaani namgombesha mbele za watu, labda asubuhi, lakini mchana utamuona huyo
amerudi. Angekuwa hasomei Eletronics huyu, watu wangesema hana akili
vizuri.” Grace alijibu kwa sauti yake ya upole. “Mimi nakwambia vile
ulivyokuwa ukinigombesha huku unanifukuza, nilikuwa nasikia raha. Nilikuwa
narudi kwa kina James nawaambia Grace ameniongelesha.” Walizidi kucheka.
“Yaani anagombeshwa, lakini yeye anasikia raha.
Danny mjinga sana huyu! Yaani mpaka tulikuwa tunamuhurumia.” “Halafu sasa
suruali yake ni moja tu ya jinsi. Tisheti tu ndio alikuwa anabadili. Marafiki
zangu walikuwa wananicheka. Halafu alivyo sasa Danny, anakufuata mpaka kwenye
lecture, mbele za watu. Eti ananijulia hali! Nilikuwa nakasirika mpaka basi.” Grace
aliwafanya wazidi kucheka. “Mvumilivu hula mbivu. Huoni niliibuka mimi
mshindi? Namiliki chombo mwenyewe. Nimewapiga bao watu na pesa
zao.” Mumewe akajibu.
“Hawa wawili hawa, na wenzao wenye akili kama
zao, walisoma sekondari pamoja. Wakachaguliwa hapo chuo kikuu cha Mlimani.
Wakawa chuo kimoja, mwaka mmoja, darasa moja, na sasa hawa wawili
katika kundi lao, wanafanya kazi sehemu moja. Hawana jipya. Wananikera na macho
yangu, sina raha. Huyo James kaka yako, na wenzake, walikuwa wanamsindikiza Danny
kunitongaza. Basi James na wenzake walikuwa wanasimama mbali kidogo,
wanatuangalia mimi na Danny tunavyoongea. Walikuwa wananiudhi kundi lao hawa!
Sina hamu. Twende mwaya Nanaa tukazungumze hapo nje. Maana yule muhasibu wangu
amepitisha siku za kujifungua, muda wowote ule anaweza akajifungua, nikabaki
nahangaika. Ofisi yenyewe sio kubwa, lakini yeye ndiye anamajukumu
mengi.” Wakatoka nje. Kuzungumza.
Grace alizungumza naye taratibu. Kwa kumsikiliza
tu, Nanaa akavutiwa na bosi Grace. “Sasa upo tayari kuanza kazi
lini?” Grace akauliza. “Hata kesho. Sina kitu chakufanya sasa hivi.”
“Mbona wewe utanifaa! Ndio vizuri uanze mapema akuelekeze kila kitu, ili
ikitokea anajifungua, tusikwame.” Nanaa akafurahi sana. Wakakubaliana
mshahara, Grace na mumewe wakaondoka.
“Naona ulivyofurahi.” James alimchokoza dada
yake. “Kasema atanilipa.” Nanaa alijibu huku akicheka. “Ni watu
wazuri sana, hawana shida. Nina uhakika utafurahia kufanya kazi na Grace. Ni
dada muungwana sana.” “Ni kweli ulitaka kumuoa? Mzuri kweli!” James
akacheka. “Hapana. Huwa tunapenda kumchokoza tu. Danny, mumewe ni mtundu
sana. Halafu Grace ni mpole. Wakati mwingine tunamchokoza tu ili aongee. Tokea
shule huwa tunapenda vile anavyoongea kwa upole. Usipomchokoza Grace,
hazungumzi hata. Atabaki kimya tu.” “Kwa hiyo Danny ni rafiki yako tokea
zamani?” “Danny ni mtu wa watu sana. Alikuwa au tuseme ni rafiki wa
kila mtu. Alituunganisha marafiki tuliokuwa tukisoma pamoja tokea sekondari.
Tukajikuta tuna kundi letu. Utakuja kuwaona wengine. Danny hawezi kupoteza mtu.
Mmoja wetu akipotea tu, atamtafuta mpaka tujue alipo. Mwishowe tumejikuta
lazima kukutana mara kwa mara. Tulipotezana kwa muda, wakati yeye alipoamua
kurudi chuoni kufanya shahada ya pili. Akawa kimyaa. Alipomaliza akatukusanya
tena. Ameajiriwa pale ofisini kwetu. Hata mwaka hajamaliza pale kazini, lakini
kila mtu anamfahamu. Mpaka wafagizi wanamjua Danny. Kila anapopita anatengeneza
marafiki anaowafanya wawe karibu yake. Mtundu sana na haishiwi
maneno.” Waliendelea kuzungumza wakicheka vituko vya Danny alivyokuwa
akisimulia James.
Mwanzo Mwengine Mpya.
N |
anaa
akaanza kazi kipindi huyo muhasibu anafunga mahesabu na kutengeneza ripoti ya
mwezi. Walifanya kama siku mbili tu, Nanaa akiweka juhudi na kuuliza maswali
mengi kadiri awezavyo. Akijua ile si field tu, sasa ni kama kazi. Na kama
akiongeza juhudi, ni sehemu anayoweza kurudi kuomba ajira pindi atakapomaliza
chuo. Mshahara wa mwanzoni tu ulimvutia. Akajua akirudi na vyeti,
basi mambo yake yatakuwa safi. Kabla huyo muhasibu hajakamilisha ripoti, na
Nanaa kuona inakuaje mpaka mwisho, chupa ya uchungu ikavunjika wakiwa ofisini.
Wote walifurahi kwa kuwa huyo mtoto alikuwa akisubiriwa na watu wote pale
ofisini lakini sio Nanaa. Yeye alitaka waendelee kuwa naye ili amfundishe mpaka
mwisho ili asije haribu, lakini ndio katikati ya mafundisho, chupa ikavunjika.
Grace alimkimbiza hospitalini huku akiwa amempigia simu mumewe awafuate
hospitalini. Nanaa alibaki pale hajui chakufanya.
~~~~~~~~~~~~~
Alikaa hapo mpaka jioni wakati anakaribia
kufunga, akasikia sauti ya mtu akiongea nje ya ofisi yao, akiwa
mapokezi. “Sasa hivi siwezi kufanya kitu cha
maana G. Nimechoka na nina mambo mengi. Akili haijatulia. Kwa nini nisije siku
ya jumamosi?” Alimsikia mtu akiongea taratibu kama Grace. Lakini
huyu sauti yake ilikuwa nzito, nzuri ya kiume. Akasikia kimya kama
mtu anayesikiliza upande wa pili. “Bwana wewe ni
muoga tu, G. Unaweza.” “Siwezi. Wewe msaidie.” Nanaa alishitukia
yule mtu amefungua mlango amemsimamia mbele ya meza yake na sauti ya Grace
ikasikika kutoka kwenye simu. Moyo wa Nanaa ukapasuka. Akabaki kimya asijue kwa
nini! Akabaki ameduaa.
“Labda jumamosi. Leo nitakuharibia
kazi. Jumamosi akili itakuwa imetulia, au usubiri baada ya week ijayo.” Yule kaka aliendelea
kuongea kwenye simu huku akivuta kitabu cha invoice mbele ya meza ya yule
muhasibu, akaanza kuangalia taratibu. “Kwanza wala
huna transanctions nyingi! Acha uvivu G. Fanya mwenyewe.” Waliendelea
kuzungumza, Grace akisikika akimsisitiza yeye ndio afanye. “Basi nitakuja hiyo siku ya jumamosi, wewe zungumza naye
muelewane. Nikifanya leo, nitamchanganya tu.” Grace aliendelea
kuzungumza upande wa pili. “Sawa. Hamna
shida.” Akaitikia na kukata simu, na kumuangalia Nanaa.
Nanaa hakuhitaji utambulisho, alijua wazi ni kaka
yake Grace bosi wake. Walifanana sana na Grace. Macho yao yalikuwa yakifanana
sana. Makubwa kiasi na yakusinzia. Aliongea kwa utulivu kama Grace, yaani haiba
ya utulivu kama Grace. Mweusi na nywele nyingi zilizoonekana alifanya juhudi za
makusudi kuzitengenezea mustachi mzuri kuzunguka midomo yake na usoni. Nanaa
alibaki akimtizama.
“Naitwa Geb, kaka yake Grace.” Akampa Nanaa
mkono na kuendelea. “Alitaka nimalizie kazi ya muhasibu wake, lakini leo
nimechoka sana. Nikisema nikae hapa, nitashindwa kukuelekeza vizuri. Ingekuwa
nafanya peke yangu, hapo sawa. Lakini inaonekana G, anataka nikufundishe na
wewe.” “Kwani ni ngumu sana? Naweza kukuangalia wakati wewe unafanya. Huna haja
yakuongea sana.” Nanaa aliuliza, yule kaka akakaa kwenye kompyuta ya yule
muhasibu na kuanza kuangalia bila kujibu kwa muda.
“Huyu mwenzako nilitumia karibia mwaka mzima
kumuelekeza kutengeneza hii ripoti tu. Mpaka kipindi fulani nikawa natengeneza
mwenyewe. Nafikiri kama nikuweza vizuri, amefanikisha kama ripoti mbili za
mwisho, nyingine zote ilikuwa lazima nizirekebishe sana. Ni kama nilikuwa
nafanya mwenyewe tu.” Aliendelea kuperuzi kwenye kompyuta ya huyo muhasibu
huku Nanaa amekaa meza ya pembeni isiyokuwa na kompyuta.
“Yaani mpaka hapa tu, naona nitahitaji siku
nzima. Vitu vingi sana havijakamilika.” Aliendelea kuperuzi huku Nanaa
akiwa kimya. “Daah! Kuko hovyo sana.” Aliendelea kuzungumza mwenyewe
akiendelea kuperuzi.
Akaingia dereva wa hiyo kampuni. “Mzima
bosi?” Geb alisalimia. “Kumbe mkuu mwenyewe upo hapa?”
“Nipo.” Geb alijibu na kurudisha macho kwenye kompyuta. “Kama upo
basi ipo neema. Maana nina mzigo hapa, natakiwa kumkabidhi muhasibu kisha
anikatie kiasi.” “Usinitie matatizoni bwana. Mimi sina pesa. Na sitaki kukaa na
pesa ya mtu.” Geb alijibu huku akiendelea kuangalia kompyuta kwa makini.
“Unanikatalia bure bosi wangu. Najua wewe huna
shida na pesa ndogo ndogo kama hizi.” “Unamuongelea Geb wa jana, leo hali
mbaya. Mpigie simu bosi wenu umuulize chakufanya.” Yule dereva aliendelea
kuzungumza na Geb wakionekana kufahamiana. Kwani walitaniana kidogo, mwishowe
Grace alimpigia simu Nanaa. “Pokea pesa kutoka kwa
huyo dereva, kisha uumpe elfu 10. Hakikisha mnaandikishana na anaweka saini
sehemu kuthibitisha amepokea hiyo pesa ya malipo yake na amekupa pesa yote ya
ofisi.” “Sawa nitafanya hivyo. Kwani hutarudi tena?” Nanaa
akauliza. “Nitakuwepo hapo kesho. Geb bado yupo?”
“Yupo.” “Sawa. Analalamika amechoka, hawezi kukusaidia kufunga mahesabu.
Anataka kuja kufanya jumamosi. Utaweza?” “Saa ngapi?” “Atakwambia
mwenyewe. Hapendi kufanya kazi siku za jumamosi asubuhi asubuhi, kwa
hiyo haitakuwa asubuhi sana, usiogope.” Nanaa akacheka kidogo. “Sawa.” Alimuelekeza kidogo Nanaa,
wakaagana.
Yule dereva aliondoka na kumuacha Nanaa na Geb
pale ofisini. Geb alipiga simu kitengo cha stoo kuomba transctions
zote. “Mbona nilishatuma?” Dada
aliyekuwepo kwenye kitengo hicho alijibu. “Ni sawa
kama nikikuomba utume tena?” Geb aliomba kiustarabu sana. Nanaa
akabaki akimwangalia kwa kujiiba. “Sawa. Nitafanya
hivyo.” “Asante sana na samahani kwa usumbufu.” “Hamna shida.” Akakata
simu na kusimama.
“Nilikwambia naitwa Geb?” “Ndiyo.”
“Samahani. Akili zimechoka. Sasa bosi wako ameniambia huwa hufanyi kazi siku za
jumamosi. Mimi nitakuwepo hapa asubuhi ya saa nne. Ukiweza kuja kutizama
ninachofanya ni sawa. Ukishindwa, nitakuelekeza wakati mwingine. Haina haraka.”
“Sawa.” Geb alimtizama kwa macho yaliyomfanya Nanaa abaki ameduwaa, asijue
kama aliulizwa swali na kama alijibu sahihi. Akakumbuka kaka yake alimwambia
asili ya macho yale yakikuangalia kwa mara ya kwanza, hupumbaza.
Nanaa akajiweka sawa baada ya kuona bado
anamtizama. “Si umesema jumamosi utakuwa hapa, saa nne ya
asubuhi?” Nanaa akauliza kama kupata uhakika. “Ndiyo. Na wewe umesema
sawa. Sasa sawa hiyo nitegemee utakuja au utataka kujifunza wakati mwingine?”
“Nitajitahidi kuwepo.” Nanaa akaongeza. “Basi usiku mwema. Tutaonana
Mungu akipenda.” Geb akatoka. Ndipo Nanaa akapumua kwa nguvu kama
aliyepata aghueni. Alihisi tokea Geb amtazame ni kama alishindwa kupumua.
Akabaki anababaika. “Si kwa macho yale. Daah!” Nanaa
alijiambia huku akijicheka.
~~~~~~~~~~~~~
Isivyo kawaida yake, Nanaa ambaye hakuwahi hata
kumfikiria mwanaume kwa umbile, akajikuta anabaki na taswira ya Geb. Kutoka
kwenye kuapa hataki tena mwanaume, lakini akajisikia shauku ya kutamani
jumamosi ifike haraka akamuone tena Geb. Hiyo ilikuwa siku ya jumatano Geb
alipowatembelea ofisini. “Hivi hata jina nilimtajia kweli? Sijui ameoa
au ana mpenzi? Daah! Yule akikutamkia ndoa, unasamehe hata mahari.” Nanaa
aliwaza wakati amejilaza kitandani kwake. Alitamani Geb arudi tena pale ofisini
au ajue habari zake zaidi, lakini hakujua amuulize nani.
~~~~~~~~~~~~~
Siku ya jumamosi ilipofika, Nanaa alimka asubuhi
na mapema nakuanza kujiandaa. Kila nguo siku hiyo haikumpendeza. Alivaa
yakumbana, “Mmh! Ataona najirahisisha sana.” Akavua na kuvaa
kubwa kidogo. “Hii hapana. Hata kiuno changu hakionekaniki! Wakati hiki
ndicho kinawachanganya wengi!” Akacheka na kuvua. Alihangaika kuvua na
kuvaa, mpaka akaishia kuvaa gauni la kawaida tu kwa kuwa muda ulikuwa umeisha,
akaona atachelewa na kuonekanika sio msomi.
Alitoka akiwa na haraka, akabahatisha
daladala mpaka ofisini. Akakuta walinzi tu, na watu wa stoo waliokuwa wakipokea
na kutoa mizigo. Aliingia ofisini kwa muhasibu akakaa akisubiri mpaka saa nne
na nusu ndipo akamsikia Grace na Geb wanaingia.Walipita moja kwa moja ofisini
alipo Nanaa, wakiwa na mtoto mzuri sana wakiume, mwenye macho yanayo fanana na
wao. Rangi yake pia alikuwa mweusi kama wao. Nanaa akabaki akijiuliza kama ni
mtoto wa Geb au Grace.
Alimsalimia Nanaa kwa heshima akabaki akimwangalia.
Nana akacheka. “Wewe vipi Fili?” Grace alimuona vile alivyobaki akimkodolea
macho Nanaa. Akampa ishara ainame ili amnong’oneze. Grace akacheka na kuinama
kumpa sikio. Yule mtoto alimnong’oneza kitu Grace nakumfanya acheke sana.
Akatoa simu na kupiga, kisha akaweka sauti kubwa.
Alipopokea tu, Grace akaanza . “James! Umepata shemeji.” “Nani?” Upande wa pili
aliuliza ambaye ni James, kaka yake Nanaa. “Fili
amesema Nanaa ni mchumba wake.” Wote walicheka mpaka Geb. “Kwa kuwa naonana na Danny jioni, mwambie Fili nimemkabidhi.
Nitamalizana na dad hukuhuku.” Ndipo Nanaa akajua kuwa yule ni
mtoto wa Grace wala si Geb. Roho ikatulia. “Labda bado hajaoa.” Nanaa
akawaza kwa haraka huku akicheka.
Nanaa alikuwa akicheka kwa aibu kwani bado Grace
alikuwa akicheka huku akimwangalia mwanae. Akampigia simu Danny mumewe na
kumsimulia. “Mwanao anataka kumuoa Nanaa.” “Sasa
huko ndiko kuingizana umasikini. Mwambie kabla hajafikiria kuoa atafute kwanza
kazi, ili apate pesa ya kumlipa James ya mahari. James atataka nyumba yangu
bure.” Grace aliendelea kucheka na mumewe akilalamika.
Baada ya muda Danny akamuunganisha James kwenye
simu wakawa wote watatu. “Hapa nishaanza kutafuta
mteja wa nyumba yangu ile mbavu za mbwa. Mahari ya Nanaa ni mjengo wako
Danny.” James aliongea mara baada ya kupokea simu. “Si nilikwambia Grace? Mtoto anataka kuniingiza umasikini
huyo. Mahari yenyewe si umesikia?” “Acha kumuogopesha mwanangu bwana James!
Hata kwa mkopo sisi tutaoa tu.” Grace alimtetea mwanae. “Tena Grace uishie hapo hapo. Mwambie Fili kama
anamtaka Nanaa, awe na pesa yake. Mtoto anataka vitu vizuri huyo! Hajui vizuri
garama?” Wote walicheka. “Mpango wangu
ilikuwa nimpeleke huyo Fili kijijiniii. Nikamchukulie mke kwa joo mbili tu,
basi.” Danny aliongeza. Waliendelea kutaniana, huku vicheko
vikiendelea. Ikabidi Grace awaage.
~~~~~~~~~~~~~
Akamgeukia Nanaa. “Huyu anaitwa Geb. Mdogo
wangu.” “Kaka yako bwana!” Geb alimkatisha. “Kwa kupenda ukubwa huyu!
Mimi ndio mkubwa, nimempita kwa lisaa lizima.” Ndipo Nanaa alipojua kuwa
ni mapacha. “Kwani ukiniita kaka unapungua wapi, G?” “Haya. Na hivi
unanisaidia, acha niwe mpole. Huyu ni Geb, anko wa Fili. Ndiye anayenisaidia
mambo ya mahesabu kwenye maisha yangu yote. Usifikiri ni hapa ofisini
tu.” Nanaa akacheka kidogo kama asiyesadiki. “Usifikiri nakutania.
Nachukia sana hesabu, lakini yeye ni mtaalamu sana wa mambo ya mahesabu tokea
watoto yeye ndio alikuwa mwalimu wangu. Halafu huwa hachoki kufundisha.
Atakuelekeza mpaka wewe mwenyewe ndio utachoka. Nitakuacha naye hapa. Ukichoka
wewe uondoke tu, maana yeye anaweza kulala hapahapa.” “Siwezi kulala bwana. Saa
kumi jioni mwisho. Naenda mazoezini.” Geb alidakia tena huku macho yakiwa
kwenye makabrasha yaliyokuwepo hapo juu ya meza.
“Haya Nanaa, kazi kwako. Mtumie vizuri kumuuliza
maswali yote, ili jumatatu ukiachiwa ofisi, usipate shida.” “Sawa,
asante.” Nanaa alishukuru. “Nitakuja baadaye kumchukua Fili twende wote
mazoezini. Au unasemaje?” Geb alimtizama Fili, akampa 5. “Ewaa!
Ujiandae na uvae kabisa ile jezi yako na viatu. Nikija tu,
tunaondoka.” Wakaona Fili anababaika wala hafurahii tena kwenda mpirani na
anko. “Nini?” Geb akamuuliza. “Unabaki naye?” Fili akauliza
nakuwafanya wote wacheke. “Yaani huyu mtoto kama Danny!” Geb alicheka
huku akitingisha kichwa. “Nanaa yupo kazini. Anatoka jioni. Ukimtaka
umtafute kesho, hafanyi kazi. Sawa?” Geb alimjibu
Fili. “Sawa.” Fili alijibu kwa kuridhika kwa ahadi ya kuonana na
Nanaa kesho yake.
“Tutamtafuta kesho?” Wakati wanatoka
walimsikia Fili akimuuliza mama yake na kumfanya Nanaa na Grace
wacheke. “Wewe Nanaa umemchanganya mwanangu. Wala hakuwa hivi!” Grace
aliongea huku akifungua mlango wakutoka nje ya ofisi, wakasikia wakifunga
nakutoka.
~~~~~~~~~~~~~
Palipita hali ya ukimya kidogo, Geb akiendelea na
shuguli zake, na Nanaa akifikiria chakufanya. “Nimeshajisahau! Naendelea
bila kukuonyesha. Sogeza kiti uone jinsi ninavyokusanya kila kitu, na
kupangilia mpaka kupata ripoti nzima.” Nanaa akasogeza kiti na kukaa naye
meza moja, kazi ikaanza. Kulikuwa na utulivu wa namna yake pale ofisini. Mara
kadhaa Geb alitaka kujua kama bado wapo pamoja au alimuacha mbali, na mara zote
Nanaa alisema anaelewa.
“Kama una swali lolote, usisite
kuniuliza.” Geb alimgeukia kuona kama bado Nanaa yupo au alishahama pale.
Yale macho alitamani yaendelee kumuangalia kwa muda. “Naelewa.” Nanaa
alijibu kwa utulivu. “Na ujue mwezi ujao hii ndio kazi utatakiwa kufanya.
Kwa hiyo uelewe kweli kweli. Ukiwa na swali uliza. Usisite. Na hakuna swali
dogo au kubwa. Yote ni ya msingi.” “Sawa.” Nanaa akajibu akijaribu kutulia.
Nyongo
Kutumbuka Pabaya!
Waliendelea na kazi pakiwa na utulivu wa namna
yake. Nanaa akifurahia kuwepo pale kwa wakati huo wala asijue ni furaha ya kuelewa
kazi au ni mwalimu mwenyewe ndiye anayefurahia uwepo wake! Lakini akajisikia
kutulia rohoni kwa namna yake mpaka akajishangaa! Ilipofika saa 7:30 mchana,
Grace akampigia kaka yake. “Nikuletee chakula?”
“Nataka nimalize kabisa. Nikila sasa hivi nitapata uvivu.” “Ndio maana hunenepi!”
“Niwekee chakula changu, nikirudi nitakuja kula.” “Mama anasisitiza uwahi
kurudi. Usikae huko ukajisahau kula.” “Sasa unataka nikumalizie kazi yako au
unataka nije kula?” Grace alisikika akicheka.
“Liz amesema atakuja baadaye.” “Mfanye
anisubiri, asiondoke mpaka nije.” “Changamsha mikono sasa.” “Sitachelewa.”
“Vipi Nanaa?” “Yupo. Anaonekana kuelewa.” “Mruhusu akale.” “Sawa. Nitakuona
baadaye, lakini usisahau kumfanya Liz anisubiri.” “Nitampa hiyo kazi Danny.
Amuongeleshe mpaka umkute.” Geb alicheka kidogo na kukata simu.
Baada ya Nanaa kusikia kuna Liz tu, alichafukwa
na roho kupita kiasi. Hasira za kusalitiwa zikampanda. Kumbukumbu za juhudi
zake kujitoa kwa wanaume nakuishia kujidhalilisha zikamjia. Akaamua atoke
pale. “Vipi!?” Geb aliuliza baada ya kuona Nanaa anavuta kiti chake
kwa nguvu na kusimama bila taarifa. “Ni muda wa kula, si ndio?” Nanaa
akauliza kishari kidogo. Geb akabaki akimtizama. “Nakwenda
kula.” Nanaa akaaga nakutoka bila kuongeza wala kujibiwa.
Hakuna chakula kilichopita kooni, akajikuta
akitokwa na machozi asijue ni kwa nini. Aliingia chooni akakaa humo kwa muda,
akarudi tena jikoni akatengeneza chai, lakini akaishia kuimwaga kwenye sinki.
Alishikwa na hasira za ajabu, akashindwa kujizuia. Chuki kwa wanaume
ikamwingia, akaamua kurudi ofisini.
Alifungua mlango akapokelewa na macho matulivu ya
Geb. “Kwema?” Geb akauliza kwa utulivu. “Najisikia vibaya,
naondoka naenda kupumzika.” Alijibu kwa kifupi. Akachukua kipochi chake,
nakutoka. Geb alibaki ameshangaa. Lakini lilikuwa jukumu lake kumaliza kazi
aliyokuwa amepewa na dada yake. Akabaki akifanya ile kazi, asielewe
kilichompata mwanafunzi wake. Kilikuwa kitendo cha muda mfupi. Hakujua kama ni
maumivu ya gafla au alikuwa nayo kwa muda mrefu! Anamuuliza nani na Nanaa
alishaondoka! Akabaki haelewi.
~~~~~~~~~~~~~
Alitoka pale akarudi nyumbani. Akashukuru
kutomkuta James nyumbani, akaingia chumbani kwake nakuanza kulia. Alilia kana
kwamba Geb alikuwa mpenzi wake akamfumania. Na wala hakuwahi kulia vile hata
alivyowafumania wapenzi wake wote. Alilia kwa kusononeka kutoka moyoni, huku
akikubali kushindwa.
Alilia kukosa ambacho wala hakuwahi kumiliki na
wala hakuwa akimfahamu Geb! Labda ni juhudi alizoweka kwenye kuvaa akitaka
kumfurahisha? Ni kweli Nanaa kwa mara ya kwanza amependa? Amependaje mtu kwa
kumuona tu? Hamfahamu Geb. “Sasa kwa nini
nilie wakati hanifahamu na mimi simfahamu? Ana maisha yake na mimi ninayo
yangu. Huu ni ujinga.” Aliwaza na kujikashifu. Akaamua kulala
tu.
~~~~~~~~~~~~~
Sababu ya kulia muda mrefu, alipitiwa na usingizi
mzito mpaka akaamshwa na simu ya James. “Pole. Nasikia
uliondoka kazini ukiwa unaumwa. Vipi?” James akauliza. “Sasa hivi najisikia vizuri. Nilipatwa na kizunguzungu cha
gafla, tumbo lilikuwa linauma.” “Unataka nije nikupeleke hospitalini?” “Hapana
kaka yangu. Nimepumzika angalau sasa hivi najisikia vizuri.” “Pole sana.”
“Asante.” Ukimya ulizuka kidogo.
“Unauhakika utakuwa sawa bila kwenda
hospitalini?” Bado
James alionyesha wasiwasi. “Usiwe na wasiwasi.
Nikijisikia vibaya nitakupigia. Lakini sasa hivi najisikia vizuri.” “Basi
nitamjulisha na Grace. Amenipigia simu akiwa na wasiwasi.” Nanaa
alijisikia vibaya kwa jinsi alivyoondoka, hata yeye hakujua kilichompata. “Naomba uniombee msamaha. Niliondoka gafla.” “Afadhali
uliwahi kuondoka kuliko kuzidiwa ofisini. Basi pumzika, usihangaike na kupika.
Mimi nitakula hukuhuku, nitakuletea na wewe.” “Asante. Lakini usiwe na
wasiwasi, nipo sawa tu.” “Sawa. Basi pumzika.” Nana akavuta pumzi
akajirudisha kujilaza vizuri.
Wakati amejilaza hapo kitandani ujumbe
ukaingia. ‘Vipi, unaendeleaje? Geb.’ Nanaa
aliusoma ule ujumbe na kuufuta palepale bila hata kutaka kujibu. “Hayamuhusu.” Akajisemea
na kuiweka simu yake pembeni kwa hasira. Akarudi kulala mpaka James alipokuja
kumgongea kuwa amerudi na chakula. Aliamka kula na kurudi kulala. Siku
inayofuata alilala karibia siku nzima. Aliamka jioni na kujikuta peke yake,
James hayupo. Akapika na kuosha vyombo, akarudi chumbani kwake.
Ilipofika usiku akasikia sauti ya Grace, Danny na
James wakiingia huku wakicheka kwa sauti ya juu. “Nenda kamuamshe tujue
anaendeleaje?” Alimsikia Grace akimtuma James. “Una wasiwasi
wakupoteza mfanyakazi nini?” Danny aliuliza huku akimcheka
mkewe. “Ninavyomuhitaji huyo Nanaa! Sitaki yule dereva awe analala na
pesa. Ataanza kuzitumia. Nenda bwana James.” Alimsikia James akisogelea
chumba chake huku akicheka. “Nanaa! Bosi wako amekufuata.” Nanaa
akafungua mlango. “Nilikwambia uwaambie najisikia vizuri, kaka! Wasiwe na
wasiwasi.” “Wewe njoo uwasalimie, labda wataridhika.” Nanaa akatoka
kuelekea sebuleni akiwa na majuto na alichokifanya siku iliyopita.
“Tumekuletea na mchumba wako. Labda
utapona.” Grace alimuwahi Nanaa mara alipotokea, akacheka. Fili alikuwa
amepakatwa na Geb kwenye kochi dogo, wametulia kimya. Halafu Grace na Danny
wamekaa kwenye kochi kubwa. “Nimepona. Nilimwambia kaka James akwambie, ili
usiwe na wasiwasi.” “Afadhali. Pole sana. Tulikuwa tunamwambia James, tunaanza
kupunguza mahari, tumekuletea Ice cream.” Nanaa akacheka, akaenda kupokea
kopo dogo la Vanilla Ice cream. “Sijui kama utapenda! Tumechukua tu.”
“Asanteni sana kwa kujali, na poleni kwa usumbufu.” “Hamna shida. Kwanza ndio
tumepata sababu ya kuja hapa.” Danny alidakia nakumfanya James acheke.
“Sasa unataka nini hapa kwetu?” James
akauliza huku akicheka. “Si basi tu. Kwani hujawahi kuona wale watu
wasiopenda kwao?” Danny aliongeza nakufanya wote wacheke kasoro Geb,
alibaki akimbembeleza Fili aliyekuwa amelala kifuani kwake.
Aliendelea kupitisha mkono wake mgongoni kwa Fili taratibu. Nanaa
alijifanya kama hajamuona na wala na yeye hakuzungumza chochote, alibaki kimya
tu akibembeleza mtoto.
Jumatatu.
A |
lifika
ofisini siku ya jumatatu akaendelea na shuguli zake kama kawaida. Ilipofika
mchana, akasikia sauti ya Geb akiwa ameingia hapo ofisini akiongea na dada yake
wakiwa mapokezi. “Utakuwa hunidai.” Alimsikia Geb akimwambia
Grace. “Mbona nakushukuru! Nimeipitia ripoti nzima, naona mambo sio
mabaya.” “Lakini bado nikiangalia nafikiri unaweza kutengeneza faida kubwa
zaidi, G.” “Umeniambia. Tupate basi muda tuzungumze zaidi ili unishauri
chakufanya.” Geb akaaga, na kuondoka bila hata kusogelea ofisi ya Nanaa,
akamsikia Grace anakuja ofisini kwake. “Geb ametuletea Bank Statement ya
mwezi uliopita. Naomba uitunze, atakuja kudai wakati wakutengeneza ripoti.”
“Sawa.” Nanaa akaipokea na kuiweka kwenye faili lake husika.
Yalipita majuma mawili mfululizo bila kumuona Geb
pale ofisini wala hakutuma tena ujumbe. Nafsi ikaanza kutapatapa. Akatamani
kumfahamu zaidi kama anakofanya kazi, na mambo mengine mengi lakini akaishia
kujiambia haina sababu. Akabaki anataka, hataki
~~~~~~~~~~~~~~
Siku hiyo ya ijumaa wakati anakaribia kutoka,
akiwa anarudisha mafaili mengine pale mapokezi, akamuona Grace anaongea na simu
kwenye mlango wakutokea nje ya ofisi. “Nanaa!” Grace akamuita. Nanaa
akamsogelea. “Kesho ni birthday ya mchumba wako. Tutamfanyia sherehe ndogo
tu. Unaweza kuja na James kama huna kitu kinachokufunga.” “Saa ngapi?” “Saa
kumi na nusu jioni. James anafahamu hoteli ambayo huwa tunafanyia. Nitamwambia
mje naye.” “Anapenda zawadi gani?” Nanaa akualiza. “Mmh! Wala
usihangaike. Ana michezo mingi sana, naona hata mingine hachezei. Wewe njoo tu.”
“Nije mikono mitupu!?” Grace akacheka kama anayefikiria.
Akawa amepata wazo. “Basi njoo nyumbani uje
unisaidie kuandaa zawadi zakuwapa watoto watakao hudhuria hiyo
party, halafu tutaondoka wote kuelekea huko kwenye sherehe na hizo zawadi.”
“Hapo sawa.” Wote wakacheka. “Mnakaa wapi?” “Nitamtuma Danny au James
wakulete nyumbani. Usiwe na wasiwasi. Utafikishwa tu.” Nanaa alifurahia
kuona amepata kitu chakufanya siku inayofuata.
Jumamosi.
Siku hiyo alimka na furaha akiwa anakumbukumbu za
kualikwa kwenye shuguli ya Fili. Aliamka asubuhi na mapema akafua nguo zake na za
kaka yake. Akasafisha nyumba, baada ya kuandaa kifungua kinywa, akabaki amekaa
chumbani kwake akimsubiria James aamke ili ajue ni saa ngapi atampeleka
nyumbani kwa Grace. Alimsikia James ameamka, anamwita. Akatoka. “Nahisi
Grace atakutaka mapema. Danny amenipigia kuniambia msichana wao wa kazi
ameondoka leo asubuhi.” “Utanipeleka?” “Ngoja nile kwanza. Nimeamka na njaa.
Nitakupeleka kwenye saa tano hivi.” Nanaa akarudi chumbani kwenda kujitayarisha,
akamuacha James anapata kifungua kinywa huku akiongea na kucheka kwenye simu.
~~~~~~~~~~~~~~
Ilipofika saa tano na nusu, Geb aliwasili pale. “Niambie
Mkuu!” James akamuanza. “Nipo kaka. Nimetumwa kumfuata Nanaa.” “Pole
kwa usumbufu. Kuna mahali natakiwa kwenda sasa hivi. Nikaona mpaka nimalize
huko, nije nimchukue hapa na kumleta huko kwenu, nitachelewa.” “Hamna
shida.” Geb akajibu na kutulia.
James akaenda kumuita Nanaa ambaye tayari mapigo
ya moyo yalikuwa yakimwenda mbio baada yakusikia sauti ya Geb ndani ya nyumba
yao. “Nilimuomba Grace amtume mtu akufuate. Kuna mahali natakiwa kwenda.
Geb ndio amekuja kukuchukua. Tutaonana jioni kwenye shuguli.” “Hamna
shida.” Nanaa alitoka akamkuta Geb amekaa kwenye kochi akimsubiria.
Hakuwa amemuongelesha tokea siku alipomuacha
ofisini, tena kwa hasira na hata alipofika siku ile akiwa na familia ya dada
yake, Nanaa hakumsalimia. “Habari yako?” Nanaa
alisalimia. “Nzuri.” Geb alijibu kwa ufupi tu. “Mimi nipo tayari.” Nanaa
akaongeza, Geb akasimama. “Sasa kaka?” Geb alimgeukia
James. “Tutaonana jioni. Acha mimi nikasake pesa.” James akajibu. “Sawa.
Baadaye basi.” Geb aliaga nakutoka, Nanaa akamfuata nyuma baada ya kuagana
na kaka yake.
~~~~~~~~~~~~~~
Alikutana na gari ya rangi ya silver, aina
ya ‘Cadillac Escalade, SUV’ ikisubiri
nje. Nanaa alibaki ametoa macho. Hakuwahi kuona gari nzuri vile. Akabaki
anashangaa. Alisikia Terry na Evan pamoja na marafiki zake wakishindana
kutajiana aina ya magari ambayo ndio ndoto zao. Na kama endapo watafanikiwa
kimaisha watanunua magari hayo. Nanaa hakuwa hata anaelewa hayo majina. Hakuwa
kwenye ulimwengu huo wakuwaza aina ya magari wakati hata pakulala ilikuwa shida!
Hakujua aina ya magari, na hakuona umuhimu wa mtu kupoteza pesa nyingi eti kwa
ajili ya kununua tu gari, mpaka alipokutana na ile gari pale nje. Ndipo
akaelewa kwa nini kuna aina ya magari, na watu wanapenda aina fulani.
Wazo la kwanza alifikiria kama angepiga picha
kwenye lile gari. “Hata nikipiga picha itasaidia nini? Niache ushamba.” Nanaa
akajisuta. “Khaaa! Sio kwa uzuri huu wa gari jamani!” Alibaki
akikodoa macho. Geb alipoona amezubaa pale nje, akarudi upande wa abiria.
Mlango wa mbele, akamfungulia mlango. “Karibu.” Akamkaribisha kama kumtaka
waondoke. “Asante.” Akasogea. Tayari miguu ilikuwa ikicheza. “Ndani
litakuaje? Hizi nguo haziendani na hili gari hata kidogo!” Nanaa
aliendelea kuwaza wakati anasogelea mlango. Akaingia, Geb akafunga mlango.
Geb alijua wazi Nanaa amebabaika na lile gari.
Alitegemea. Akamcheka moyoni kwani alishindwa kuzuia mshangao wake. Alishangaa
mpaka mdomo aliacha wazi. Geb hakujua kama Nanaa alijijua jinsi alivyoachama
mdomo na kutoa macho baada ya kuona lile gari. Alicheka tena moyoni, akatulia
tu usoni.
Alimsubiri ajifunge mkanda ndipo aondoe gari.
Nanaa hakujua hata kama anatakiwa kujifunga mkanda. Akabaki ametulia kwenye kiti
huku akishangaa ile dashboard/mbele ya gari kwa ndani. Akagundua safari
haijaanza. Wapo pale pale. Akamgeukia dereva wake. “Nasubiri ufunge
mkanda.” Haraka sana, Nanaa akajiangalia gauni alilokuwa amevaa. Lilikuwa
la lastiki kiunoni. Ni kweli lilikuwa na vijinyuzi vyembamba pembeni.
Vyakupitishia mkanda wa gauni. Lakini hakuwa amevaa mkanda. Alivaa bila mkanda.
Lilikuwa la kuchanua chini. Kigauni cheusi. Polka dots za gold. Kilikuwa kina
mikono mifupi iliyoshuka chini kidogo ya mabega. Kilimwagika vizuri sana chini
ya kiuno.
“Sikupataga mkanda unaofanana na hili
gauni.” Nanaa akajitetea. Bado Geb alikuwa akimtizama wakati anajiangalia
na kuendelea kuvuta lile gauni na kulikusanya chini ya mapaja kama
kulikalia. “Kwa hiyo hapa sina mkanda.” Aliendelea kujieleza,
akionekana kupaniki tayari. “Namaanisha mkanda wa gari. Kwa ajili ya
usalama wako barabarani.” Geb aliongea kiungwana. “Oooh! Mkanda wa
gari. Nil..nil …nilifikiri..” Akaanza kupambana kuvuta mkanda wa hilo gari
pembeni ya hicho kiti alichokuwa amekalia. “Nikusaidie?” Geb akauliza
baada yakuona anatumia nguvu nyingi kwa kuvuta mkanda ambao hata Fili huwa
anavuta bila shida.
~~~~~~~~~~~~~~
Nanaa alijisikia aibu mara mbili. Sio kosa lake.
Amepanda wapi gari zuri hivyo? Kaka yake James ana gari nzuri. Lakini ni ya kawaida
tu, na huwa Nanaa mwenyewe hapandi mara kwa mara kwa kuwa James anatumia gari
ya ofisini siku za kazi, na hawaongozani na Nanaa. Wanafanya kazi pande mbili
tofauti za Dar. Ofisi za kina James zipo njia yakuelekea Kawe kutokea Morocco.
Na ofisi ya kina Nanaa, ipo Kariakoo karibu na Fire. Siku za weekend James
anakuwa na mishuguliko yake na gari yake, Nanaa anabaki nyumbani. Akiwa na
safari basi daladala itahusika.
Mwanaume mwingine aliyekuwa naye na mwenye gari
alikuwa Jamal. Jamal alikuwa na gari aina ya Mark 2. Nayo ilikuwa ya kawaida
sana. Tena ilionekana ni ya zamani. Jamal aliinunua kwa mfanyakazi
mwenzake akiwa ameshaitumia kwa miaka mingi tu. Na huyo mfanyakazi mwenzake
alinunua ikiwa imeshatumika hata huko Japan aliko iagiza. Vioo vilishaharibika.
Hakumbuki hata kama lilikuwa na mkanda. Milango ya hilo gari ya Jamal ilikuwa
lazima ufunge kwa nguvu. Tena wakati mwingine mara mbili au tatu.
~~~~~~~~~~~~~~
Akaendelea kupambana na mkanda wa kiti chake
mpaka alipochoka. Akakubali kushindwa. Geb alikuwa ametulia kimya, akimsubiria
achoke ndipo amsaidie. Kwa kuwa alijua kwa uvutaji ule, lazima mikanda iji lock.
Kwa hiyo alimuacha apambane mpaka aache ndipo arudie tena kuuliza kama angetaka
msaada. “Naona mikanda mibovu.” Nanaa aliongea kwa upole, baada ya
kupambana na ule mkanda na kushindwa.
Geb akamsogelea. Mapigo yake ya moyo yakaanza
kwenda kasi. “Ananipa pole kwa kunibusu!?” Aliwaza
harakaharaka huku mapigo ya moyo yakienda kasi wakati Geb akijivuta upande
wake. Akanyoosha mkono kwa tahadhari kama asiyetaka kumgusa. Akavuta ule mkanda
kwa urahisi sana, akamfunga. Nanaa alivuta pumzi kwa nguvu. Akajiweka sawa pale
kitini huku aibu imemlemea.
~~~~~~~~~~~~~~
Kwenye nyumba aliyopangisha kaka yake, hapakuwa
na geti. Kwa hiyo ilikuwa rahisi kuingia na kutoka bila shida. Hakujua aseme
nini tena. Alishajidhalilisha vyakutosha. “Sio kosa langu. Sijazaliwa kwenye
magari. Hata yeye kuna mambo hajui. Kwani yeye ni Mungu kuwa anajua kila kitu?
Wala sio jambo la ajabu nililolifanya!” Nanaa alijitetea kwenye nafsi
yake. “Lakini nisingesingizia kuwa mkanda ni mbovu! Gari yenyewe
inaonekana mpyaaa! Aibu gani hii! Lazima nibadili mazungumzo. Kuondoa hii
aibu.” Akawaza kama ajieleze juu ya ujumbe ambao hakujibu au vile
alivyomuacha pale ofisini bila maelezo ya kutosha, na pia akamfuata nyumbani
kwao, akashindwa hata kumsalimia! “Labda nitulie tu.” Nanaa akaendeleza
kikao kichwani mwake, akijiuliza na kujijibu.
Akajifunga mkanda wake na yeye, kisha akaondoa
gari bila ya kuongeza neno wala kuuliza swali, aliendelea kuendesha akiwa
ametulia kimya kana kwamba yupo peke yake garini. “Itakuwa gari ya dada
yake hii! Grace anapesa sana.” Nanaa aliendelea kuwaza wakati Geb akiendelea kuendesha.
Akakumbuka ripoti ya mwezi uliopita ilivyoonyesha faida kubwa
waliyoingiza. “Hakika Mungu amembariki yule dada.” Nanaa
akaendelea kuwaza.
Alishangaa kuona wanapita Ubungo, wakielekea njia
ya Mabibo Hosteli. Akamkumbuka Zac, mpenzi wake wazamani. Kidogo akaanza kukosa
raha. Akajiweka sawa na kugeukia dirishani. Akaegemeza kichwa vizuri hapo
dirishani, akabaki akiangalia nje ya dirisha. Mawazo yalimpeleka moja kwa moja
mpaka siku alipomfumania Zac. “Mmmh!” Alipumua kwa nguvu huku
ameshika shavu. Geb akamtizama, lakini akagundua hayupo pale kimawazo maana
hata kubabaika pale kitini kuliisha. Akatulia kabisa macho nje gari.
~~~~~~~~~~~~~~
Usikose
Muendelezo….
0 Comments:
Post a Comment