James alimuona vile alivyoumia.
Alimuelezea kwa kuumia sana tofauti na vile alivyokuwa amemueleza juu ya
kusalitiwa na Alex. “Kwa hakika huyu nilijua ni wangu!” Nanaa
alimalizia kwa kaka yake huku amenyong’onyea pale kwenye kochi. Ilibidi James
achukue nafasi ya umama na kuanza kumtia moyo ili asiharibikiwe zaidi. James
akiwa ameumia na yeye akitamani kama wanaume wangeona uthamani wa mdogo wake,
alizungumza naye kwa upendo kama mama au dada kwa mdogo anayempenda na kumjali.
Akamkumbusha wajibu alio nao kwa wakati ule. Kwanza ni shule, ndipo ije ndoa
kama Mungu atamjalia mwanaume atakayemthamini. Alimwambia kwa wakati huo ni
lazima kutuliza mawazo na kufanya ile mitihani. Akamfaraji mpaka Nanaa
akatulia.
~~~~~~~~~~~~~~
Mungu akamsaidia tena kipindi hicho
kigumu cha machungu na kusalitiwa kikapita. Angalau akaanza kulala mpaka
asubuhi bila kugeuka geuka kitandani. Akapata nafuu, akarudisha akili shuleni,
akaanza kujiandaa kurudia mitihani hiyo wakati wenzake wakiwa likizo.
Tia na Zena wao walifaulu vizuri tu.
Tena kwa alama za juu sana. Walihakikisha habari zinamfikia Nanaa, ili ajue wao
wamempita kielimu. Kwa hiyo hawakuwepo kwenye kundi la wanao takiwa kurudia
mitihani. Baada yakumaliza mitihani, Tia alibaki jijini kwa muda. Akarudi
kuishi nyumbani kwa kina Zena. Walihakikisha wanajua kinachoendelea.
Tena kutoka kwa rafiki wa Karibu wa Zac.
Vicheko viliwajaa kujua kilichompata
Nanaa. “Yako wapi!? Yako wapi shoga yangu?” Zena alicheka mara baada
ya kukata simu waliyokuwa wameweka kwenye ‘loud speaker’ wakimsikiliza
rafiki wa Zac, akieleza mkasa mzima. “Kitanda hakiangalii kiuno chembamba,
wala rangi ya mwili. Ukilalia tu, mchezo unachezwa.” Tia alizidi kupasua
mbavu huku machozi yakimtoka kwa furaha ya kumcheka Nanaa. “Alivyoshushuka!
Ndio maana kujidai kote kulimwisha!” “Alikuwa hawezi hata kututizama!” “Kwa
mabusu yale na zawadi! Hata mimi ningenyong’onyea.” Wakaendelea
kupokezana. “Kawa mdogoooo! Eti Zac atanioa. Yako wapi? Ndoa Bongo?” Zena
akaongeza huku akicheka na kuongeza. “Halafu Zac alivyomshenzi, umeona
mwanamke aliyelala naye? Ndio ujue havichagui sura wala umbile.” Walizidi
kucheka na kugonga mikono wakifurahia anguko la penzi la waliyemwita shoga yao.
“Zena bwana! Eti havichagui
kiuno.” Tia aliongeza na kuzidi kucheka akiunga mkono hoja ya shoga yake. Gafla
akakumbuka jambo. Zena akapoa. “Ni nini tena?” “Nimekumbuka hizo sio habari
njema sana kwangu.” Akili ilimrudia Zena wakiwa wanamcheka mwenzao. “Terry
akijua kama sasa hivi Nanaa hana mtu si ndio atahamisha majeshi kwake?” Zena
aliingiwa na hofu ya gafla. “Ataambiwa na nani huyo Terry? Hakuna
kumtafuta tena Nanaa. Akakae huko huko kwao. Anaweza kurudi na hasira,
akatembea na wanaume zetu wote. Akuu! Atuondolee balaa lake na mkosi. Hata simu
zake hakuna kupokea tena.” Tia aliongea kwa hakika akijihami.
Mikakati ya kumkwepa tena Nanaa
ikakamilika. Kipindi hicho kabla Tia hajarudi kwao, akiwa jijini kwa kina Zena,
walihakikisha wanamkwepa kabisa Nanaa. Hawakumpigia tena simu. Kwa hiyo kila
walipokuwa wakitoka, hawakutaka kumwambia Nanaa. Evan alikuwa akienda
kuwachukua wao wawili tu. Na kila Terry alipouliza alipo Nanaa, walimwambia
yupo na Zac. Utulivu ukawepo. Zena akaendelea kujisogeza kwa Terry bila uwepo wa
Nanaa.
Jamal.
M |
aisha ya kuamka asubuhi nakujisomea yakaanza tena. Wakati mwingine
anarudi chuoni kusoma na kukutana na wenzie wanaorudia mitihani hiyo. Wanasoma
pamoja. Akichoka anapanda daladala mpaka maktaba ya jiji, anaanza kujisomea
tena. Hiyo ilikuwa kama njia yakutoa uchovu na kubadili mazingira kuanza
kujisomea upya. Kisha jioni anarudi nyumbani. Akaendelea kufanya hivyo
akiongeza bidii ili kutimiza lengo. Ilikuwa ni lazima amalize chuo.
Akiwa kwenye maandalizi hayo,
akajikuta anakutana na kijana mmoja hapo hapo kwenye hiyo maktaba. Eneo
analopenda kujificha yeye kusoma, ndilo huyo kijana naye alikuwa akipendelea
kwenda hapo. Nanaa alimuona akitua vitabu vyake na kuanza kujisomea. Hakuwahi
kumuona na mtu yeyote, ila yeye tu akijisomea mwenyewe. Wakajikuta kila siku
kwenye kona hiyo wao wawili tu. Kila mmoja kimya, akisoma kivyake.
~~~~~~~~~~~~~~
Wakaanza kusalimiana kila mmoja wao
anapomkuta mwenzake na kuagana kila mmoja wao anapoondoka na kumuacha mwenzake.
Ikabidi kufahamiana majina. Nanaa akajitambulisha kwa Jamal. Siku hiyo nayo
ikapita kwa kujuana majina tu.
“Naona haya ndio maeneo yako ya
kujidai! Hukosi!” Nanaa akatabasamu. Akanyanyua uso akiwa amezama
kitabuni. Alijua ni Jamal tu ndiye aliyezoea kuwepo hapo, japo siku hiyo
alichelewa kidogo. “Inanilazimu. Nimeshikwa. Lazima kurudia mitihani
ya chuo.” Nanaa akawa muwazi. “Pole. Inatokea kabisa. Lakini kwa
juhudi hizo, lazima utapita tu.” Jamal akamtia moyo. “Nashukuru. Na
hayo ndio maombi yangu.” Ikawa siku ya kwanza angalau kumuongelesha
kidogo. Akavuta kiti sehemu yake, Jamal akapotelea kwenye vitabu vyake.
Siku nyingine tena, Jamal aliingia na
kumkuta Nanaa alishaingia hapo makitaba. Akamsalimu na kuvuta kiti pembeni
yake. “Vipi?” “Safi tu. Habari za kutwa?” Nanaa naye akatoa
salamu. “Nzuri, namshukuru muumba.” Jamal akajibu, Nanaa
akatabasamu. “Mbona na wewe huishi kuja hapa?” Na yeye
siku hiyo Nanaa akauliza. “Elimu ya utuuzimani. Tulikimbia shule wakati
vijana, sasa hivi maisha yanaturudisha huku.” Jamal akajibu kwa kifupi.
Nanaa akacheka lile jibu. Kwani Jamal hakuwa hata na dalili ya uzee. “Haya
bwana. Hongera.” Nanaa hakuhoji zaidi. Akaishia hapo.
~~~~~~~~~~~~~~
Taratibu wakaanza kutoka muda mmoja.
Jamal anapanda gari yake na kuondoka, Nanaa anaelekea kituo cha daladala
kusubiri usafiri wa kumshusha kituo kilichopo karibu na nyumbani kwa kaka
yake. Baada ya siku mbili, Jamal akajitolea kumsindikiza kituo cha
daladala na kumsubiri mpaka apande kwenye daladala ndipo na yeye aondoke.
Alimwambia hajisikii vizuri kumuacha tu bila kuwa na uhakika amepata usafiri na
kuondoka pale salama. Nanaa akamwangalia kwa tabasamu, akakubali kusindikizwa.
Napo hapakuchukua siku zaidi ya mbili. Baada ya kusubiri kituoni kwa muda mrefu
siku ya tatu, Jamal akaona amsogeze tu, japo hakuwa akielekea pande hizo.
Nanaa hakuona sababu. “Daladala
huwa zinachelewa tu. Lakini nitapata usafiri. Wewe usijali. Nenda tu, mimi
nitaendelea kusubiria.” Nanaa alijaribu kukataa lifti hiyo. Lakini Jamal
akasisitiza. “Siwezi kukuacha mrembo kama wewe barabarani hapa na kiza
hichi! Ukipatwa na janga? Vijana wamjini hawawezi kujizuia kwa mrembo kama
wewe. Acha nikusogeze japo mpaka karibu na nyumbani.” Nanaa
akacheka. Wakaongozana mpaka kwenye gari ndogo ya kawaida tu ya Jamal.
Kuanzia hapo, lifti zikaendelea.
Ikajengeka tabia ya kurudishwa mpaka kituo cha daladala karibu kabisa na
nyumbani kwa kaka yake. Hapakuwa na mazungumzo mengi humo garini. Kila mmoja
akiongea kwa kujiwinda. Lakini Jamal uzalendo ukamshinda. Akaamua kuvunja
ukimya. Alimwambia alivutiwa naye, na angependa wazidi kufahamiana zaidi.
Ukweli Nanaa alikuwa ni dada mwenye
vitu vya kuvutia macho ya mtu yeyote kwa haraka. Hakuwa gumzo la jiji, lakini
ukifanikiwa kuwa naye karibu, lazima utavutiwa tu. Nanaa akacheka kwa aibu
kidogo wakati anakaribia kushushwa kituoni. “Ni sawa baada ya kusoma siku
ya jumamosi, tukaelekea nyumbani kwangu?” Tayari uchu ulishamlemea Jamal.
Kumbeba Nanaa kwenye gari lake na kukaa pembeni yake na kuyaona mapaja
yaliyotulia kitini kila akibadili gia, halikuwa jambo rahisi. Rangi nyeupe
usoni aliyokuwa akiiona ikiwaka, akajua ndivyo atakavyokuta ndani pindi
atakapomfunua. Anavumiliaje tena?
“Sitakuchelewesha. Nitakurudisha hapa
muda kama huu.” Jamal akasisitiza. “Hee! Kwa hiyo unataka nishinde
kwako siku nzima? Maana unajua siku za jumamosi huwa namaliza kusoma mapema.” Nanaa
alihoji na tabasamu la soni, usoni. “Nakuahidi kutokuchoka.” Nanaa
akainama kwa muda kama anayefikiria. “Ana nyumba na gari! Ngoja nikajionee.
Huwezi jua.” Nanaa akawaza. Akanyanyua sura na kumtizama Jamal
aliyekuwa akisubiria jibu lake. “Lakini sitakaa sana.” “Ukitaka
nikurudishe wakati wowote ule, utaniambia. Lakini ukitaka kulala pia, sitakuwa
na neno.” “We Jamal!” Nanaa akashangaa kwa pozi.
“Hakuna neema kubwa kama kumiliki
Kito cha thamani kwenye maisha ya mwanadamu yeyote yule hapa duniani. Nitakuwa
nimenyimwa shukurani na Mungu hatanikumbuka tena, kama nikikataa baraka ya
uwepo wako nyumbani mwangu. Sasa Mungu anipe nini tena?” Nanaa akamtizama
kama kuhakiki yale maneno, akabaki natabasamu asijue ajibu neno gani kwa maneno
mazito kama yale. Jamal alijua wazi amekubaliwa.
S |
iku hiyo ya jumamosi Nanaa akawahi kufika hapo maktaba akiwa na
shauku ya kumkuta Jamal. Mpaka inafika saa sita kasoro, Jamal hakuwepo.
Wasiwasi ukampata. Akajuta kujirahisisha kwa kiasi kile. “Kwa nini
nilimkubalia?” Akajilaumu huku ameinamia vitabu vyake. Mara akasikia
mtu anamgusa begani. Akageuka. “Jamal!” “Ahadi ni deni Nanaa. Saa sita
ndio hii. Nimekuja kukuchukua.” Nanaa akacheka kwa furaha. “Mbona
hukuja tokea asubuhi?” “Si kwa ugeni nilio nao mimi!” Jamal alijibu na
kumfanya Nanaa acheke. “Kwa hiyo ulikuwa ukijiandaa na ugeni?” Nanaa
akauliza. “Kumbe!? Sio mgeni wangu anafika nyumbani, hamna chakula wala
maji! Sikulelewa hivyo.” Jamal alikuwa na lafudhi iliyomvutia Nanaa.
Lafudhi ya watu wa pwani. Akatabasamu na kurudi kukusanya vitu vyake vyote
vilivyokuwepo hapo mezani. Naye akamsaidia kubeba, na kutoka pale maktaba.
Akaendesha mpaka nyumbani kwake
Temeke. “Huku ndiko nilikopata sehemu ya kuishi.” Aliongea wakati akimfungulia
Nanaa mlango. Nanaa ambaye hachagui sura ila mtu tu wakuwa naye, hakuona shida.
Ilikuwa nyumba ndogo tu. Kwa haraka Nanaa akajua anaishi peke yake. Palikuwa
pasafi sana. Akaona asiwe mchoyo wa sifa. “Jamal wewe unaonekana ni msafi
sana.” “Subiri mpaka uangalie kila mahali ndipo usifie. Unaweza ukajuta
baadaye.” Nanaa akacheka.
Akaingia na kutaka kukaa. “Twende
nikutembeze kila mahali. Sitaki tena siku nyingine ukawa mgeni humu ndani!”
“Kwani unampango wa kunikaribisha tena?” Nanaa akauliza na tabasamu
limemjaa usoni. “Hata! Nataka siku nyingine na mimi uje unikaribishe.”
“Humu humu ndani?” Nanaa akauliza huku akicheka. “Kumbe? Na mimi
nataka siku nyingine nikirudi, nisikute makochi yakinitazama. Bali nikukute na
wewe kitini unanisubiri.” Nanaa akacheka sana.
“Au hutaki?” “Sijui!” Nanaa
akajibu kwa aibu. “Yaani unataka leo ndio iwe mwisho!? Haiwezekani Nanaa.
Nimekukaribisha hapa, kwa kuwa nimekuheshimu na ninakuona ni mtu utakayenifaa.
Si ningekukaribisha tu hata baa? Kukuleta hapa kwangu, ujue nimekuheshimu mno.”
“Nakushukuru.” Nanaa akasuuzika roho. Mungu ampe nini tena? Nyumba, gari
na Jamal anayemtangazia wenyeji mchana kweupee!
“Twende sasa nikuonyeshe kila
mahali. Au njaa inakuuma?” “Hapana. Nipo sawa tu.” “Kwa hiyo unaniruhusu
nikutengee chakula baadaye?” “Hamna shida.” Nanaa alijibu kwa kuridhika
kabisa kitu kilichomfurahisha Jamal aliyekuwa akimezea mate mapaja aliyokuwa
akiyaona ndani ya gauni. Sasa hivi yapo ndani ya nyumba yake! Nanaa si mtoto! Akarudi
kumshika mkono kumuongoza atakapo yeye Jamal. Bila hiana, Nanaa akafuata kwa
tabasamu.
Walifanikwa kuona chumba cha kwanza,
choo cha wageni wakaishia chumbani kwa Jamal. Humo ndipo alipojua ni kweli
Jamal alikuwa na uchu naye. Chumba kile kisafi, Jamal alikitumia ipasavyo
kukata kiu. Na Nanaa naye hakumzuia. Akajituma ipasavyo. Hapakuwepo tena na Zac
wakumfanya ashindwe kumvulia nguo Jamal. Akamkumbuka Terry, akajiambia kama
angekuwepo wakati ule, yeye ndio angefaidi. Lakini akakumbuka uchu wa Zena kwa
Terry. Akaona ajiachie tu. Akahangaika siku nzima kumfurahisha Jamal kwenye
kitanda hicho bila hata kujali hisia zake ila lengo lake tu.
~~~~~~~~~~~~~~
Wakati akijituma hapo kitandani,
akaanza kujifikiria jinsi atakavyokuwa mama wa ile nyumba, na kwa usafiri ule
aliokuwa nao Jamal, sio pabaya sana kuanzia maisha. Hakuona chakupoteza kama
akitoa penzi lake kwa Jamal, pengine atamvutia zaidi. Na kweli, hapakuwa na
jinsi ungesema Jamal hakumfurahia Nanaa siku hiyo pale kitandani. Nanaa alitoa
ujuzi wake wote siku ile kumfurahisha Jamal bila hata kujijali yeye. Alijituma
kwa kadiri ya uwezo wake. Yale aliyokuwa akimfanyia Zac, ndio alipewa Jamal
siku ile tena kwa juhudi huku akiongeza mautundu, asije kukimbiwa tena. Kwa
Nanaa alikuwa ni kama yupo kazini. Lengo moja tu, ndoa. Awe na kwake,
aepukane na kuishi au kuwa mzigo kwa mtu. Yeyote mwenye mafanikio kidogo ya
maisha, huyo alimfaa. Hapakuwa na vigezo eti mwanaume mrefu. Sijui kifua
kipana. Rangi sijui iweje! Hapana. Bora mwanaume, basi.
~~~~~~~~~~~~~~
Mapenzi yakachanganya, ratiba za
maktaba zikaanza kuongezeka. Siku ambazo Jamal haendi kazini, siku hizo za
jumamosi, Nanaa alifika nyumbani kwake asubuhi. Walipata kifungua kinywa
pamoja, mapenzi kidogo, kisha kujisomea. Ikifika jioni, mapenzi tena yakuagana,
ndipo anamrudisha Nanaa nyumbani kwao.
Mambo yakaenda vizuri, wakiwa
wanatumia muda mwingi kusoma na mapenzi. Hapakuwa na maongezi mengi sana kati
yao, kwani Jamal alionekana kumtaka zaidi Nanaa kitandani kuliko kitu kingine.
Kile kitendo chakuonyeshwa anahitajika na mtu, kilimfariji sana Nanaa. Simu na
ujumbe wakutakiwa usiku mwema, huku akiambiwa ni jinsi gani anasubiriwa kesho
yake wakafanye hiki au kile havikuisha. Pengo la Zac likazibika kwa haraka
sana. Yale aliyokuwa akifanyiwa na Zac, akakutana nayo kwa Jamal. Tena
akimsifia vilivyo huku akimlaumu kumuacha akiwa bado anamuhitaji kwa mapenzi
zaidi.
~~~~~~~~~~~~~~
Muda wa Nanaa wa kurudia mitihani
yake ukafika. Akafanya akiwa ametulizwa kwenye penzi la Jamal aliyekuwa akimpa
vihela vya hapa na pale vyakujikimu. Matokeo yakatoka, yale masomo akawa ameyafaulu,
akaendelea mwaka wa pili na penzi la Jamal.
Kina Zena walipogundua si hatarishi tena kwani anaye mwanaume
mwingine, urafiki ukarudi tena kati yao. Kwani Nanaa aliwaambia juu ya Jamal
baada yakumuona anapilika pilika zisizoisha. Kama hakuwepo kwenye simu, basi
anakuja kuchukuliwa na kuondoka. Ndipo Tia akamuuliza kulikoni. Ikabidi
kuwaambia habari za kuvutia za mpenzi mpya mwenye gari na nyumba, si kama Zac.
Asijue amempa Zena habari za
kumchafua zaidi kwa Terry, ili kumvuta kwake. Nanaa hakuwa akitoka nao tena,
kwani alikuwa akija kuchukuliwa mara baada ya kipindi chao cha mwisho siku ya
ijumaa. Kila alipokuwa akitoka kwenye lecture siku hiyo ya ijumaa,
alimkuta Jamal akimsubiri nje. Alikuwa akimchukua siku za ijumaa anakuwa naye
nyumbani kwake mpaka jumatatu asubuhi wakati Jamal akienda kazini ndipo
anamshusha chuoni.
Nyumbani kwa kaka yake alikuwa
akienda siku ya jumapili. Atakaa naye kidogo, na kumuaga. Kulala nyumbani kwa
kaka yake akapunguza. Kama siku hiyo ya jumapili akienda kumtembelea kaka yake
akapakuta pachafu, basi atamsaidia kusafisha na kufua. Akishaacha kila kitu
sehemu yake na chakula, ndipo anaondoka kurudi kwa Jamal mpaka siku inayofuata,
jumatatu.
Ilimbidi kuongeza juhudi ya kusoma
hizo siku za kati kati ya juma. Maana siku hizo anazokuwepo kwa Jamal, kuanzia
hiyo ijumaa jioni mpaka jumatatu asubuhi wanapotoka hapo kwa Jamal, Nanaa
alikuwa mke kweli kweli. Kujituma kumpikia na penzi kitandani. Kufua na kufanya
usafi kwenye kijinyumba hicho kidogo, ambacho Nanaa alishajiona ni mama mwenye
nyumba. Yaani yupo kwake.
Asubuhi za hizo siku za jumatatu pia
Jamal alimuaga kwa kujiridhisha kweli kweli akimwambia kwa kujifidia kwa siku
hizo ambazo Nanaa hatakuwepo hapo. Walifanya penzi la kufidia jumanne, jumatano
na alhamisi. Ijumaa usiku alirudishwa kitandani hapo. Na jumatatu asubuhi
alitoa penzi la nguvu ndipo wanapooga, nakuanza siku. Jamal kazini, Nanaa
chuoni. Maisha yakaendelea.
~~~~~~~~~~~~~~
Penzi alilokuwa akipewa Jamal
halikuwa kama la Zac. Kwani Zac alipewa kwenye hosteli na nyumbani kwa rafiki
yake. Hapakuwa na uhuru. Alipewa penzi la kimya kimya wakijua wapo wanachuo
wengine wanapita nje ya chumba chao, au wengine wapo chumba cha jirani. Wakiwa
nyumbani kwa rafiki yake Zac, pia iliwalazimu kuwa wastaarabu japo walijua
anajua kinachoendelea huko chumbani. Lakini hapo kwa Jamal, Nanaa alikuwa huru.
Kwanza ni nyumba anayoishi peke yake.
Majirani wapo mbali. Jamal hakuwa na maneno mengi. Alimuonyesha wazi anamtaka
kitandani tu. Kila asubuhi anapokuwepo hapo nyumbani kwake, nilazima amwamshe
kwa kumtaka kimapenzi. Tena penzi la haja. Jamal hakuwa mvivu hata kidogo
katika hilo eneo. Kitu kilichomlazimu Nanaa mwenyewe kujituma kweli kweli hata
kama ni asubuhi. Ndipo aamke akaandae kifungua kinywa. Na baada ya hapo tena
warudi tena kitandani kama si siku za jumatatu. Kwa hiyo ikawa yupo kazini
kwelikweli wala si mapenzi kuwa anayafurahia kama Jamal aliyemuhisi si mzima
kwa jinsi alivyokuwa akiendekeza kitanda! Kama aliyekuwa akitumiwa, na wala si
nguvu zake mwenyewe!
~~~~~~~~~~~~~~
Alikuwa akimshangaa vile Jamal
alivyokuwa mkimya. Hakuwa mzungumzaji sana. Kama sio wanafanya mapenzi, basi
wanaangalia mpira. Mechi za timu za nchi za bara la Ulaya au tamthilia za hapo
hapo nyumbani. Alikuwa akikodisha movie mbalimbali ambazo pia walikuwa
wakiangalia kila wanapokuwa pamoja. Na alimuonyesha wazi, pindi anapoangalia
vitu vyake kwenye luninga, angependa kusikia na maneno. Kwa hiyo kunakuwa na
utulivu wa aina yake. Hilo nalo Nanaa akalikubali na kuliheshimu ilimradi tu
kuendeleza maisha bila kutaka kumuudhi, asije akakosa ndoa. Maisha yakaendelea.
~~~~~~~~~~~~~~
Katika hiyo hali ya kuchukuliana na
kumvumilia Jamal akifanya mambo bora liende, siku moja ya jumapili wakati Jamal
anaogo na Nanaa yupo kitandani, baada ya shuguli nzito hapo kitandani. Tena
Nanaa akiwa anaugulia maumivu kwa mapenzi ya muda mrefu. Simu ya Jamal ikaanza
kuita akiwa yupo bafuni. Nanaa akiwa hoi hapo kitandani, akigugumia maumivu ya
michubuko mingi aliyoipata katikati ya tendo, nakushindwa hata kusema, au
kumwambia Jamal ili tu kumfurahisha. Alibaki hapo kitandani akigugumia maumivu
sehemu za siri huku akiitazama simu ya Jamal iliyokuwa ikiita na kukata.
~~~~~~~~~~~~~~
Tokea siku ya ijumaa wanafika hapo
nyumbani mpaka siku hiyo ya jumapili, Jamal alionekana anataka kufanya mapenzi
tu. Tangia anamchukua chuoni, Nanaa alishamuona hayupo sawa. Alipoingia kwenye
gari akajua kuna tatizo. Nanaa alimsalimia kama kawaida. Akarudisha salamu kwa
kifupi tu. Baada ya kuona amekuwa kimya sana au mzito wa maongezi, akaamua na
yeye anyamaze. Walipofika tu nyumbani siku hiyo ya ijumaa, akamshusha nakutoka
kufuata chakula. Hakutaka Nanaa apike. Alimwambia aoge, nakumsubiria.
Ndipo mapenzi yakaanza bila maongezi
mengi. Kila alipomuuliza kulikoni, alimbusu, na kuanza tena mapenzi.
Jumamosi nayo ikawa hivyo hivyo. Anatoka kwenda kununua chakula. Baada ya muda
anarudi, kazi inaendelea. Kwa ukavu ule aliokuwa akikutana nao kwa Nanaa
nakuendelea kufanya naye mapenzi bila kujali, wala kutaka kumlainisha kwanza,
japo Nanaa alishamjua si mtu wa kujali anachojisikia yeye wanapokuwa kwenye
mapenzi, lakini siku ile alizidisha. Hapakuwa na mapumziko marefu wala
maongezi. Wakati wote alitaka Nanaa amchezee na kuanza mapenzi tena na tena.
Nanaa alijua lipo jambo. Alimchubua vilivyo. Mpaka inafika siku hiyo ya
jumapili, Nanaa hakuwa na hamu tena yakuwepo pale.
Mara hiyo ya mwisho kabla yakuingia
bafuni kuoga na kumuacha hapo kitandani, Nanaa alihangaika naye sana ili
kumfikisha. Alishasahau hata walianza saa ngapi. Alifanya naye huku akigugumia
na kujikaza sana. Alishamuomba Mungu wake amkumbuke kipindi kile, Jamal
amalize, apumzike. Mpaka anafanikiwa, Nanaa hakuwa na hamu. Alilala pale
kitandani akiwa hoi na maumivu makali sana akiwaza kama amuage Jamal na
kumwambia amepata zarula anatakiwa kuondoka, au amwambie ukweli kama anavidonda
vinavyompa maumivu makali sana. Hataweza kufanya tena mapenzi siku ile. “Ataniona
sifai. Heri niendelee kujikaza, lakini nimkwepe mapenzi leo. Angalau nijiuguze
mpaka tena ijumaa ijayo atakapokuja kunichukua. Nitakuwa nimepona.” Simu
ya Jamal ikaita tena na kumtoa kwenye mawazo.
Nanaa Alizwa
Tena.
Akamwita Jamal mara kadhaa kumuuliza kama ampelekee simu hiyo huko bafuni au ajibu yeye, lakini Jamal hakusikia. Ikaita mara tatu, kisha ujumbe ukaingia. ‘Mtoto bado ni mgonjwa, mume wangu. Pesa uliyonitumia haijatosha matibabu na chakula. Uliniahidi kuja leo. Mpaka sasa hujafika na simu hupokei. Nimeamua kwenda kwenu ili wanisaidie. Mama yako ameamua kumrudisha Fatma hospitalini, Barabara ya kwanza, ili afanyiwe vipimo upya. Homa ipo juu sana. Hapa tulipo tupo hospitalini. Naomba upokee simu mume wangu. Unatutia wasiwasi, hasa baba.’ Nanaa alikaa kwa mshituko.
Wakati anafikiria na kurudia ule
ujumbe, Jamal aliingia pale chumbani. “Mbona umeshika simu yangu bila
ruhusa!? Unatafuta nini?” Jamal aliiuliza kwa hasira. “Kwa nini
hukuniambia kama umeoa na unafamilia!?” Nanaa akauliza. “Uliuliza?” Jamal
alijibu kwa kuuliza swali lililomfunga Nanaa mdomo. Alitamani kulaumu, lakini
akakumbuka hamfahamu Jamal hata kidogo. Ni kweli hakudanganywa. Alitamani
kulia. Lakini akajisuta moyoni. Anamlilia nani pale? Jamal hakuonyesha
kufumaniwa hata kidogo.
Alichukua simu yake kutoka kwa Nanaa
bila kuonyesha kuna la ajabu ila hasira ya Nanaa kushika simu yake. Akavaa
pensi yake, akatoka pale chumbani bila hata maelezo ya ziada kwa Nanaa. Hakutaka
kupoteza muda wake zaidi hapo ndani, Nanaa akavaa haraka haraka, akakusanya
vitu vyake nakutoka bila hata yakuoga. Alikutana na Jamal nje akizungumza na
simu, akampita na kuondoka bila ya kumsemesha neno hata la kwaheri.
~~~~~~~~~~~~~~
Kwa kutumia pesa alizokuwa amepewa na
Jamal siku chache zilizopita, akachukua taksii kurudi chuoni. Hakutaka hata
kupeleka sura yake kwa kaka yake. “Vipi Jamal? Mbona umerudi leo badala ya
kesho?” Zena alimrushia swali mara alipofika chumbani kwao.
Aliwakuta wakiangalia tamthilia, kila mmoja akiwa kitandani
kwake. “Wewe Nanaa? Si huwa unarudi jumatatu asubuhi?” Nanaa aliingia
na kujitupa kitandani kwake bila kuongea chochote.
~~~~~~~~~~~~~~
Kwanza alikuwa na madonda ya penzi
alilokuwa akilitoa tokea siku ya ijumaa alipochukuliwa hapo chuoni. Kwa hiyo
alikuwa na maumivu makali sana. Alijichukia na kujidharau sana vile alivyokuwa
akimvumilia, ili kumridhisha yeye Jamal. Alijinyima raha yeye, ili kumpa furaha
mume wa mtu! Kwa kipi! Kwa nini!
Pili alijichubua yeye mwenyewe donda
la moyoni. Kwa haraka gani jamani! Hata muda wakutosha kutulia na kutafakari
wapi anakosea, nini afanye cha tofauti ili kufanikisha lengo lake, haukuwa
umepita tokea atendwe na Zac, akajitupa kwa Jamal. Bila kumfahamu Jamal, siku
ya kwanza tu kukaribishwa nyumbani kwake, tayari kitandani, tena kwa sarakasi
kibao! Nikulogwa au ujinga ulioje! Haraka hiyo ya kujigawa hivyo kama karanga
za kwenye kapu zinazoonjeshwa kwa kila mtu, ili zinunuliwe hata kwa wasiokuwa
na lengo nazo, ni za nini?
Hayo yote yakazua ububu kwa Nanaa
kila akijiuliza bila kujipa jibu yeye mwenyewe. Hakujua awaeleze nini wenzake.
Walishamshuhudia akiwa kwenye mahusiano ya mapenzi na wanaume wawili tofauti
tofauti tena kwa muda mfupi mfupi, ndani ya mwaka mmoja, tena
walijua ni mahusiano mazito. Kwani Nanaa alikuwa akihama kabisa na
kwenda kuwaridhisha hao wanaume huko wanakochagua wao. Halafu mahusiano yote
hayakudumu! Anawaambia nini wao waliokuwa wakimsifia uzuri wa kila kitu? Alijua
hata marafiki zake watamshangaa.
~~~~~~~~~~~~~~
Tia bado alikuwa kwenye mahusiano na
Evan. Na hakuwahi kumsikia akimlalamikia huyo Evan hata mara moja. Habari za
Evan zilizokuwa zikiletwa humo chumbani, ni sifa zake tupu. Vile anavyojua
kumjali na kumpenda, basi. Tena Tia msichana wa kawaida kabisa. Hakuna cha
rangi nyeupe wala umbo namba 6 au 8. Hakuna alikopita wanaume wakageuka au hata
kuhisi kama amepita msichana wa ajabu. Lakini alitangaza kuenziwa na mwanaume
aliyeanza naye tokea yupo kidato cha 5. Sasa yupo chuoni mwaka wa pili. Tena
sio na mwanaume wa kijijini. Evan! Mtoto wa jijini. Ametoka kwenye familia ya
wasomi, wenye exposure kubwa tu. Anajua warembo na sifa zake. Lakini Tia
alijisifu vile alivyotulia kwake. Akazidi kupata ububu na aibu.
Alinyamaza pale kitandani, akijuta
kwa nini aliwasaidia kutafuta chumba. Tena kuwafanya waishi nao chumba kimoja!
Kama isingekuwa kuwasaidia kuwatafutia chumba, wala mwaka huo wa pili wasingeishi
chumba kimoja tena. Usiku huo angekuwa na watu wengine. Wasiojua historia yake
ya mapenzi. Na wala wasingejua kinachoendelea kwake. Nanaa akajuta sana. Akajua
kwa mara nyingine tena, hao mashoga wawili watabaki kuwa mwiba wake kwa mwaka
huo mzima tena.
~~~~~~~~~~~~~~
Akataka kujilaumu zaidi lakini
akajifariji kuwa hakuwa na jinsi. Kwani kipindi yeye yupo hapo chuoni
akijiandaa na kurudia mitihani yake, Zena alimtafuta na kumuomba awasaidie
kutafuta chumba kwa kuwa yeye alikuwa maeneo ya hapo chuoni, na walijua kuna
matron alikuwa akimpenda sana Nanaa, wakajua wakimpanga vizuri Nanaa, watapa
chumba hapo hapo Main Campus, wanapopapenda, tena kwenye sehemu nzuri. Nanaa
na moyo wake wa kusamehe, akawasaidia mpaka kujikuta nao tena pamoja.
~~~~~~~~~~~~~~
Alinyanyuka kwenda kuoga baada ya
maumivu kuendelea. Akaona akajisafishe labda maumivu yatatulia. Akanywa na dawa
na kurudi kulala huku mikakati mikali ikiendelea kichwani mwake. Alishahangaika
akidhani atapata mwanaume atakayempenda na kumthamini, akaishia kujidhalilisha
tu. Alishagawa penzi kwa wanaume hao, lakini hakuna aliyeona uthamani
wake. “Mhhh! Inatosha sasa.” Nanaa alijisemea moyoni. “Labda
kweli shule ndio itakuwa mkombozi wangu pekee. Mapenzi yamenikataa. Nitulie,
nishike moja. Shule tu.” Nanaa aliazimia moyoni.
~~~~~~~~~~~~~~
Alipopona tu madonda aliyoachiwa na
Jamal, tena alijiuguza kwa kujipaka mafuta tu kila wakati bila kumwambia mtu.
Huku asijue kama inasaidia au la! Kama anajiongezea sumu mwilini au la! Kila
alipooga na kujisafisha, alipaka mafuta mpaka akapona. Maswali ya hofu yalipita
kichwani mwake akijiuliza mbali na madonda yale, ni nini kingine Jamal
alichomuachia!? Yalimtesa sana. Mwishowe akaona asijichoshe na maswali ambayo
anaweza kupata majibu yake.
Akapiga moyo konde mpaka hospitali ya
kulipia. Mbele ya daktari aliyemkuta siku hiyo akamwambia shida yake ni moja
tu, kujua kama ameathirika au la! Alipomuuliza kwa nini hakwenda kwenye vituo
vya Ushauri Nasaha, akasema moyo wake ulimtuma hapo. Hataki kuulizwa maswali
wala hataki kushauriwa. Yeye anataka kupimwa UKIMWI, apewe majibu yake, basi.
Mengine atajua mbele ya safari.
Kwa kuwa ilikuwa ni hospitali ya
kulipia, pesa yake tu. Nanaa akapimwa. Alikaa pale akisubiria matokeo yake huku
mawazo yakizunguka huku na kule. Yalipotoka na kuambiwa hajaathirika, akatoka
pale bila kuaga. Akajiwekea mikakati yake. Akajiambia lazima kuitimiza hata
iweje.
~~~~~~~~~~~~~~
Na kweli Nanaa aliamua kutulia na
shule tu. Aliachana na kila aina ya marafiki na vishawishi vitakavyoingilia
shule yake, akatuliza mawazo shuleni tu. Muda wa kuwepo hapo hosteli ukapungua.
Akaanza kuishi nyumbani kwa kaka yake zaidi labda kuwe na test au ni kipindi
cha mitihani. Alifanya hivyo ili kupunguza kero za wanaume walioanza kumfuata
mpaka pale chumbani anakoishi na kina Tia.Walipojua tu Nanaa ameachwa tena na
Jamal, Tia na Zena wakaanza kumkwepa tena huku wakimcheka waziwazi. Nanaa
akajua. Akaamua kujitenga nao kabisa.
Wakiwa wanamsengenya Nanaa kwa
mafumbo bila kujua Evan dereva wao aliyekuwa akiwaendesha anawasikiliza, Zena
na Tia wakiwa wamekaa kiti cha nyuma wakicheka bila habari. Wakajikuta
wanaropoka jina la Nanaa na kusema kuwa ameachwa tena. Evan hakuchelewesha zile
habari. Wakiwa wamesimama kwenye mataa, Evan akamtumia ujumbe Terry kwa haraka
sana. ‘Naona Mungu amesikia sala zako. Nanaa hana mtu tena. Nasikia
ameachana na huyo mwanaume mwingine. Changamka. Huu ndio wakati wako kabla
hajakupiku mwingine.’ Evan alituma ule ujumbe palepale wakati Zena na Tia
wanaendelea kumcheka Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~~
Terry akamtafuta Evan, wakapanga
weekend inayofuata lazima Evan arudi jijini ili kumsindikiza hosteli, kwenye
chumba cha Tia na Zena wakijua ndipo watakapompata Nanaa, kwa kuwa walijua
wakipanga kuwaita Zena na Tia mahali, Nanaa hatakwenda. Na kweli siku ya ijumaa
usiku Evan alitoka chuoni SUA akaenda moja kwa moja nyumbani kwa kina Terry.
Wakazungumza na kupanga asubuhi na mapema waamkie chuo kikuu cha Mlimani. Ili
tu Terry ambaye alikuwa akisubiri muujiza wake, akamuone Nanaa.
Siku inayofuata, Evan rafiki watokea
utotoni wa Terry akawasili nyumbani kwao. Akamchukua, safari ya Mlimani
ikaanza. Njiani alikuwa kimya. Evan alijua wazi anapanga hoja zake pindi
atakapofanikiwa kumkuta Nanaa ambaye hawakuwa wamemuona kwa kipindi kirefu.
Kila alipokuwa akimuulizia, Zena alimtinga na majibu aliyodhani yatavunja moyo
wa Terry, lakini asijue ndio alikuwa akiongeza shauku ya Terry kuja kummiliki
Nanaa.
Mungu alikuwa upande wao, walifika
kwenye chumba cha kina Tia, saa nne asubuhi. Wakamkuta kweli Nanaa yupo. Lakini
alikuwa kwenye simu. Mtu wa upande wa pili akiongea, ambaye alikuwa James.
Nanaa alishawasalimia kwa kuwapungia mkono mara walipoingia chumbani hapo,
akiwa na simu sikioni imeshikiliwa na mkono wa shoto. Wakulia ndio ulifanikiwa
kuwapungia wakati wanaingia, akaendelea kukusanya baadhi ya vitu huku
akizungumza kwenye simu.
Terry alijawa na furaha baada ya
kumkuta Nanaa hapo ndani na kupata tabasamu lililosindikizwa na dimpozi nzuri
za Nanaa. Akafarijika moyoni. Wakaendelea kusalimiana na Zena na Tia wakati
Nanaa bado yupo kwenye simu. Ndipo wakasikia Nanaa akijibu, “Pole sana kaka
yangu. Basi nakuja kukusaidia. Labda uji utakaa tumboni.” Hapo
hapo Nanaa akachukua kijibegi chake kama pochi. Akawapungia tena mkono. Safari
hii alikuwa akiwaaga, akatoka akiwa bado anazungumza kwenye simu.
~~~~~~~~~~~~~~
Haikuwa weekend nzuri hata kidogo kwa
Terry. Pale pale alibadilika. “Twendeni basi.” Zena aliongea kwa
sauti ya kuchangamka. Kwani waliingia na ofa ya kuwachukua na kuwapeleka kwenye
kifungua kinywa. Terry alishabadilika mpaka alionekana usoni. “Hata mimi
nipo tayari.” Tia naye aliongea huku akimsogelea Evan mpenzi wake. “Naombeni
niwe muwazi. Mimi sitaongozana na nyinyi. Nilimfuata Nanaa, naona na yeye
ameondoka. Sina kawaida ya kwenda kupata kifungua kinywa asubuhi asubuhi kwenye
mabaa. Kwanza mimi sio mlevi, na pili kwetu wanakuwa na kifungua kinywa kizuri
sana zaidi ya mahoteli mengi sana hapa mjini.” Akiwa na hasira, Terry
akatoka.
Zena aliumia sana. Hapo hapo na yeye
akakubaliana na matokeo. Kuwa hata iweje, Terry hawezi kumpenda. Wala hatawahi
kuwa wake. “Nilidhani Terry atakuwa wangu!” Zena aliwaza
moyoni, akiwa amejawa simanzi usoni. Japokuwa alishamuonyesha wazi kuwa
anamtaka awe mpenzi wake, lakini Terry hakuonyesha kumtaka hata kidogo. Akakubali
pia kosa halikuwa la Nanaa. Nanaa alishajitoa kwao muda mrefu sana. Na alikuwa
na uhakika Nanaa na Terry hawakuwa wakiwasiliana kabisa. Kumuwekea kinyongo
Nanaa alijua ni kumuonea tu. Nanaa mwenyewe alishamruhusu amchafue vile
atakavyo kwa Terry ili tu kumvutia kwake. Alielewa maumivu aliyonayo
Terry kwa wakati ule, ‘kupenda asipopendwa!’ Inauma. Akamuhurumia
kwani na yeye ndipo alipokuwepo kwa wakati huo. Alitamani ingekuwa vinginevyo
ili mambo yawe tofauti. Lakini mapenzi ni kitu cha ajabu. Akaamua awaache tu
Tia na Evan watoke wao peke yao. Yeye akabaki.
Mapinduzi.
A |
kiwa njiani yale yaliyokuwa yakiendelea pale chumbani akiwa
anazungumza na kaka yake kwenye simu yakamjia. Akakumbuka jinsi Zena
alivyobabaika mara Evan na Terry walipoingia. “Zena bado anaonekana
hajafanikiwa kwa Terry.” Nanaa akawaza. “Inabidi nijiweke nao
mbali kabisa. Hata pale chumbani nihame. Nisije nikarudi, akapata sababu
yakunichukia zaidi.” Nanaa alishajua wanamchukia. Hakutaka wamrushie
yeye lawama. Akakusudia kutulia nyumbani kwa kaka yake moja kwa moja. “Hakuna
kulala kwengine tena isipokuwa kwa kaka tu.” Akakusudia kuhama kwenye
hicho chumba ambacho ni kama yeye ndio aliwakaribisha wenzake. Akaanza
kuhamisha kitu kimoja baada ya kingine bila kuaga.
Sio wanafunzi wa mwaka wa tatu
wala wa kwanza waliokuwa wakimtafuta Nanaa tu. Hata wenzake wa darasa moja
walimtafuta. Alikuwepo kama hayupo. Akiwa mahali alinyamaza kimya kama hayupo.
Kwanza angezungumza nini wakati habari zake zilishasambazwa kila mahali na kina
Zena na Tia. Wakidhani wanamuharibia zaidi, kumbe ndio wanaamsha wale waliokata
tamaa kwenda kujaribu bahati zao na wao kwa Nanaa.
Lakini Nanaa alikusudia. Alikataa
katakata swala la shule na mapenzi. Hata uwe na pesa na kumuahidi kumpa yeye
gari, Nanaa asingekubali tena. Waliposhindwa kwa Nanaa mwenyewe, waliwafuata
marafiki zake ili wawasaidie kuwatongozea kwa Nanaa. Alipoona fujo za Zena na
Tia zinazidi, wanachukua pesa za watu kwa lengo la kugawa namba yake kwa watu
asiowafahamu, akabadili namba na kuhamisha vitu vyake vyote pale chumbani.
Maana wakati mwingine wa mchana, alikuwa akirudi kujipumzisha pale chumbani
kwao, na ndipo hapo kina Zena hutoa habari kwa wanaume kuwa yupo chumbani.
Akaamua kukusanya kila kitu chake mpaka kalamu. Na kweli akaacha kabisa kulala
nje na nyumbani kwa kaka yake. Ikawa ni nyumbani kwa kaka yake James ambaye
alikuwa kama ndiye ndugu wa pekee na mzazi wake Nanaa. Basi. Iwe karibu ya
mitihani au la, Nanaa alihakikisha usiku analala nyumbani kwa kaka yake.
Ikitokea anachelewa kumaliza kujisomea na wenzake, alimsihi James awe anamfuata
chuoni ili arudi naye nyumbani.
~~~~~~~~~~~~~~
Hakika Nanaa hakuwa ametania.
Alikusudia. Mpaka kina Tia wakaanza kuwa na hamu naye na kuanza kujirudi.
Lakini aliyeng’atwa na nyoka, kang’atwa tu. Nanaa akawa makini kwa kila mtu
anayemsogelea. Hakuonyesha hasira, lakini aliishi na kila mtu kwa tahadhari.
Maisha yake ikawa shule, na nyumbani. Zena na Tia ndio waliobaki kusumbuliwa na
wanaume. Na ndio waliokuwa wakipokea hongo ili kusaidia kumtongoza Nanaa,
lakini Nanaa alibaki akiwacheka. “Mtakuja kubembwa juu juu nyinyi! Endeleeni
kupokea pesa za watu.”
“Sasa kama huyu kaka mwingine kwa
nini unamkataa?” Tia alimuuliza. “Hana lolote. Anataka
anivue nguo tu, ili aniangalie hili tako likiwa halina nguo. Anichezee halafu aje
kuniumiza moyo wangu tu! Sitaki.” “Bwana huyu kaka anachanganywa na miguu
yako.” “Sio miguu tu. Anasema anapenda kiuno cha Nanaa.” Zena
alidakia. “Basi mpeni pole. Mwambieni atakiona kwenye gauni, lakini
hatawahi kuniweka kitandani.” “Basi nenda hata kazungumze naye, Nanaa shoga
yetu. Tumekula pesa yake.” Nanaa alicheka sana. “Mtajijua wenyewe.
Aliyewaambia mpokee nani? Nishamaliza kazi ya kuvulia wanaume nguo. Kama
hawakubahatika kipindi kile cha mgao, wapeni pole. Waambieni Nanaa ameshamaliza
mgao.” Akawacheka na kuondoka mapema kabla giza halijaingia kuwahi kwa kaka
yake.
~~~~~~~~~~~~~~
Kweli
mapenzi ni kitendawili!
Je ni mara
zote, au mara nyingi, “Utapenda usipopendwa, na
kupendwa, usipopenda”?
Nani wa Nani?
Mengi mazito yapo mbeleni.
0 Comments:
Post a Comment