Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu Ya 5. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu Ya 5.



Ile hali ya kumfumania Zac ilimuathiri sana kiasi ya kwamba hakujua kama hata akirudia ile mitihani anaweza kufaulu. James alijua kuna tatizo tu. Maana alimuona amekuwa ni kama aliyepigwa na kibumbuwazi wakati wote. Wakiwa wamekaa sehemu, macho yake yakiangalia kitu, hayatatoka hapo hata kwa nusu saa. Ndipo James ikabidi kumuuliza kulikoni huku akimsihi asimfiche. Akawa mtu wa kwanza kumsimulia kilichompata. Hakuwa na ujasiri wa kumwambia mtu yeyote. Hata Zena na Tia hakuwa amewaambia. Ila walijua kuna tatizo. Kwani hapakuwa tena na simu za usiku wala za asubuhi kutoka kwa Zac. Simu ya Nanaa ilikuwa imefungwa kipindi chote cha maandalizi na wakati wa mitihani. Hawakumuona akisoma ujumbe tena.

James alimuona vile alivyoumia. Alimuelezea kwa kuumia sana tofauti na vile alivyokuwa amemueleza juu ya kusalitiwa na Alex. “Kwa hakika huyu nilijua ni wangu!” Nanaa alimalizia kwa kaka yake huku amenyong’onyea pale kwenye kochi. Ilibidi James achukue nafasi ya umama na kuanza kumtia moyo ili asiharibikiwe zaidi. James akiwa ameumia na yeye akitamani kama wanaume wangeona uthamani wa mdogo wake, alizungumza naye kwa upendo kama mama au dada kwa mdogo anayempenda na kumjali. Akamkumbusha wajibu alio nao kwa wakati ule. Kwanza ni shule, ndipo ije ndoa kama Mungu atamjalia mwanaume atakayemthamini. Alimwambia kwa wakati huo ni lazima kutuliza mawazo na kufanya ile mitihani. Akamfaraji mpaka Nanaa akatulia.

~~~~~~~~~~~~~~

Mungu akamsaidia tena kipindi hicho kigumu cha machungu na kusalitiwa kikapita. Angalau akaanza kulala mpaka asubuhi bila kugeuka geuka kitandani. Akapata nafuu, akarudisha akili shuleni, akaanza kujiandaa kurudia mitihani hiyo wakati wenzake wakiwa likizo.

Tia na Zena wao walifaulu vizuri tu. Tena kwa alama za juu sana. Walihakikisha habari zinamfikia Nanaa, ili ajue wao wamempita kielimu. Kwa hiyo hawakuwepo kwenye kundi la wanao takiwa kurudia mitihani. Baada yakumaliza mitihani, Tia alibaki jijini kwa muda. Akarudi kuishi  nyumbani kwa kina Zena. Walihakikisha wanajua kinachoendelea. Tena kutoka kwa rafiki wa Karibu wa Zac.

Vicheko viliwajaa kujua kilichompata Nanaa. “Yako wapi!? Yako wapi shoga yangu?” Zena alicheka mara baada ya kukata simu waliyokuwa wameweka kwenye ‘loud speaker’ wakimsikiliza rafiki wa Zac, akieleza mkasa mzima. “Kitanda hakiangalii kiuno chembamba, wala rangi ya mwili. Ukilalia tu, mchezo unachezwa.” Tia alizidi kupasua mbavu huku machozi yakimtoka kwa furaha ya kumcheka Nanaa. “Alivyoshushuka! Ndio maana kujidai kote kulimwisha!” “Alikuwa hawezi hata kututizama!” “Kwa mabusu yale na zawadi! Hata mimi ningenyong’onyea.” Wakaendelea kupokezana. “Kawa mdogoooo! Eti Zac atanioa. Yako wapi? Ndoa Bongo?” Zena akaongeza huku akicheka na kuongeza. “Halafu Zac alivyomshenzi, umeona mwanamke aliyelala naye? Ndio ujue havichagui sura wala umbile.” Walizidi kucheka na kugonga mikono wakifurahia anguko la penzi la waliyemwita shoga yao.

“Zena bwana! Eti havichagui kiuno.” Tia aliongeza na kuzidi kucheka akiunga mkono hoja ya shoga yake. Gafla akakumbuka jambo. Zena akapoa. “Ni nini tena?” “Nimekumbuka hizo sio habari njema sana kwangu.” Akili ilimrudia Zena wakiwa wanamcheka mwenzao.  “Terry akijua kama sasa hivi Nanaa hana mtu si ndio atahamisha majeshi kwake?” Zena aliingiwa na hofu ya gafla. “Ataambiwa na nani huyo Terry? Hakuna kumtafuta tena Nanaa. Akakae huko huko kwao. Anaweza kurudi na hasira, akatembea na wanaume zetu wote. Akuu! Atuondolee balaa lake na mkosi. Hata simu zake hakuna kupokea tena.” Tia aliongea kwa hakika akijihami.

 Mikakati ya kumkwepa tena Nanaa ikakamilika. Kipindi hicho kabla Tia hajarudi kwao, akiwa jijini kwa kina Zena, walihakikisha wanamkwepa kabisa Nanaa. Hawakumpigia tena simu. Kwa hiyo kila walipokuwa wakitoka, hawakutaka kumwambia Nanaa. Evan alikuwa akienda kuwachukua wao wawili tu. Na kila Terry alipouliza alipo Nanaa, walimwambia yupo na Zac. Utulivu ukawepo. Zena akaendelea kujisogeza kwa Terry bila uwepo wa Nanaa.

Jamal.

M

aisha ya kuamka asubuhi nakujisomea yakaanza tena. Wakati mwingine anarudi chuoni kusoma na kukutana na wenzie wanaorudia mitihani hiyo. Wanasoma pamoja. Akichoka anapanda daladala mpaka maktaba ya jiji, anaanza kujisomea tena. Hiyo ilikuwa kama njia yakutoa uchovu na kubadili mazingira kuanza kujisomea upya. Kisha jioni anarudi nyumbani. Akaendelea kufanya hivyo akiongeza bidii ili kutimiza lengo. Ilikuwa ni lazima amalize chuo.

Akiwa kwenye maandalizi hayo, akajikuta anakutana na kijana mmoja hapo hapo kwenye hiyo maktaba. Eneo analopenda kujificha yeye kusoma, ndilo huyo kijana naye alikuwa akipendelea kwenda hapo. Nanaa alimuona akitua vitabu vyake na kuanza kujisomea. Hakuwahi kumuona na mtu yeyote, ila yeye tu akijisomea mwenyewe. Wakajikuta kila siku kwenye kona hiyo wao wawili tu. Kila mmoja kimya, akisoma kivyake.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakaanza kusalimiana kila mmoja wao anapomkuta mwenzake na kuagana kila mmoja wao anapoondoka na kumuacha mwenzake. Ikabidi kufahamiana majina. Nanaa akajitambulisha kwa Jamal. Siku hiyo nayo ikapita kwa kujuana majina tu.

“Naona haya ndio maeneo yako ya kujidai! Hukosi!” Nanaa akatabasamu. Akanyanyua uso akiwa amezama kitabuni. Alijua ni Jamal tu ndiye aliyezoea kuwepo hapo, japo siku hiyo alichelewa kidogo.  “Inanilazimu. Nimeshikwa. Lazima kurudia mitihani ya chuo.” Nanaa akawa muwazi. “Pole. Inatokea kabisa. Lakini kwa juhudi hizo, lazima utapita tu.” Jamal akamtia moyo. “Nashukuru. Na hayo ndio maombi yangu.” Ikawa siku ya kwanza angalau kumuongelesha kidogo. Akavuta kiti sehemu yake, Jamal akapotelea kwenye vitabu vyake.

Siku nyingine tena, Jamal aliingia na kumkuta Nanaa alishaingia hapo makitaba. Akamsalimu na kuvuta kiti pembeni yake. “Vipi?” “Safi tu. Habari za kutwa?” Nanaa naye akatoa salamu. “Nzuri, namshukuru muumba.” Jamal akajibu, Nanaa akatabasamu. “Mbona na wewe huishi kuja  hapa?” Na yeye siku hiyo Nanaa akauliza. “Elimu ya utuuzimani. Tulikimbia shule wakati vijana, sasa hivi maisha yanaturudisha huku.” Jamal akajibu kwa kifupi. Nanaa akacheka lile jibu. Kwani Jamal hakuwa hata na dalili ya uzee. “Haya bwana. Hongera.” Nanaa hakuhoji zaidi. Akaishia hapo.

~~~~~~~~~~~~~~

Taratibu wakaanza kutoka muda mmoja. Jamal anapanda gari yake na kuondoka, Nanaa anaelekea kituo cha daladala kusubiri usafiri wa kumshusha kituo kilichopo karibu na nyumbani kwa kaka yake.  Baada ya siku mbili, Jamal akajitolea kumsindikiza kituo cha daladala na kumsubiri mpaka apande kwenye daladala ndipo na yeye aondoke. Alimwambia hajisikii vizuri kumuacha tu bila kuwa na uhakika amepata usafiri na kuondoka pale salama. Nanaa akamwangalia kwa tabasamu, akakubali kusindikizwa. Napo hapakuchukua siku zaidi ya mbili. Baada ya kusubiri kituoni kwa muda mrefu siku ya tatu, Jamal akaona amsogeze tu, japo hakuwa akielekea pande hizo.

Nanaa hakuona sababu. “Daladala huwa zinachelewa tu. Lakini nitapata usafiri. Wewe usijali. Nenda tu, mimi nitaendelea kusubiria.” Nanaa alijaribu kukataa lifti hiyo. Lakini Jamal akasisitiza. “Siwezi kukuacha mrembo kama wewe barabarani hapa na kiza hichi! Ukipatwa na janga? Vijana wamjini hawawezi kujizuia kwa mrembo kama wewe. Acha nikusogeze japo mpaka karibu na  nyumbani.” Nanaa akacheka. Wakaongozana mpaka kwenye gari ndogo ya kawaida tu ya Jamal.

Kuanzia hapo, lifti zikaendelea. Ikajengeka tabia ya kurudishwa mpaka kituo cha daladala karibu kabisa na nyumbani kwa kaka yake. Hapakuwa na mazungumzo mengi humo garini. Kila mmoja akiongea kwa kujiwinda. Lakini Jamal uzalendo ukamshinda. Akaamua kuvunja ukimya. Alimwambia alivutiwa naye, na angependa wazidi kufahamiana zaidi.

Ukweli Nanaa alikuwa ni dada mwenye vitu vya kuvutia macho ya mtu yeyote kwa haraka. Hakuwa gumzo la jiji, lakini ukifanikiwa kuwa naye karibu, lazima utavutiwa tu. Nanaa akacheka kwa aibu kidogo wakati anakaribia kushushwa kituoni. “Ni sawa baada ya kusoma siku ya jumamosi, tukaelekea nyumbani kwangu?” Tayari uchu ulishamlemea Jamal. Kumbeba Nanaa kwenye gari lake na kukaa pembeni yake na kuyaona mapaja yaliyotulia kitini kila akibadili gia, halikuwa jambo rahisi. Rangi nyeupe usoni aliyokuwa akiiona ikiwaka, akajua ndivyo atakavyokuta ndani pindi atakapomfunua. Anavumiliaje tena?

“Sitakuchelewesha. Nitakurudisha hapa muda kama huu.” Jamal akasisitiza. “Hee! Kwa hiyo unataka nishinde kwako siku nzima? Maana unajua siku za jumamosi huwa namaliza kusoma mapema.” Nanaa alihoji na tabasamu la soni, usoni. “Nakuahidi kutokuchoka.” Nanaa akainama kwa muda kama anayefikiria. “Ana nyumba na gari! Ngoja nikajionee. Huwezi jua.” Nanaa akawaza. Akanyanyua sura na kumtizama Jamal aliyekuwa akisubiria jibu lake. “Lakini sitakaa sana.” “Ukitaka nikurudishe wakati wowote ule, utaniambia. Lakini ukitaka kulala pia, sitakuwa na neno.” “We Jamal!” Nanaa akashangaa kwa pozi. 

“Hakuna neema kubwa kama kumiliki Kito cha thamani kwenye maisha ya mwanadamu yeyote yule hapa duniani. Nitakuwa nimenyimwa shukurani na Mungu hatanikumbuka tena, kama nikikataa baraka ya uwepo wako nyumbani mwangu. Sasa Mungu anipe nini tena?” Nanaa akamtizama kama kuhakiki yale maneno, akabaki natabasamu asijue ajibu neno gani kwa maneno mazito kama yale. Jamal alijua wazi amekubaliwa.

 Atafutaye Hachoki!

S

iku hiyo ya jumamosi Nanaa akawahi kufika hapo maktaba akiwa na shauku ya kumkuta Jamal. Mpaka inafika saa sita kasoro, Jamal hakuwepo. Wasiwasi ukampata. Akajuta kujirahisisha kwa kiasi kile. “Kwa nini nilimkubalia?” Akajilaumu huku ameinamia vitabu vyake. Mara akasikia mtu anamgusa begani. Akageuka. “Jamal!” “Ahadi ni deni Nanaa. Saa sita ndio hii. Nimekuja kukuchukua.” Nanaa akacheka kwa furaha. “Mbona hukuja tokea asubuhi?” “Si kwa ugeni nilio nao mimi!” Jamal alijibu na kumfanya Nanaa acheke. “Kwa hiyo ulikuwa ukijiandaa na ugeni?” Nanaa akauliza. “Kumbe!? Sio mgeni wangu anafika nyumbani, hamna chakula wala maji! Sikulelewa hivyo.” Jamal alikuwa na lafudhi iliyomvutia Nanaa. Lafudhi ya watu wa pwani. Akatabasamu na kurudi kukusanya vitu vyake vyote vilivyokuwepo hapo mezani. Naye akamsaidia kubeba, na kutoka pale maktaba.

Akaendesha mpaka nyumbani kwake Temeke. “Huku ndiko nilikopata sehemu ya kuishi.” Aliongea wakati akimfungulia Nanaa mlango. Nanaa ambaye hachagui sura ila mtu tu wakuwa naye, hakuona shida. Ilikuwa nyumba ndogo tu. Kwa haraka Nanaa akajua anaishi peke yake. Palikuwa pasafi sana. Akaona asiwe mchoyo wa sifa. “Jamal wewe unaonekana ni msafi sana.” “Subiri mpaka uangalie kila mahali ndipo usifie. Unaweza ukajuta baadaye.” Nanaa akacheka.

Akaingia na kutaka kukaa. “Twende nikutembeze kila mahali. Sitaki tena siku nyingine ukawa mgeni humu ndani!” “Kwani unampango wa kunikaribisha tena?” Nanaa akauliza na tabasamu limemjaa usoni. “Hata! Nataka siku nyingine na mimi uje unikaribishe.” “Humu humu ndani?” Nanaa akauliza huku akicheka. “Kumbe? Na mimi nataka siku nyingine nikirudi, nisikute makochi yakinitazama. Bali nikukute na wewe kitini unanisubiri.” Nanaa akacheka sana.

“Au hutaki?” “Sijui!” Nanaa akajibu kwa aibu. “Yaani unataka leo ndio iwe mwisho!? Haiwezekani Nanaa. Nimekukaribisha hapa, kwa kuwa nimekuheshimu na ninakuona ni mtu utakayenifaa. Si ningekukaribisha tu hata baa? Kukuleta hapa kwangu, ujue nimekuheshimu mno.” “Nakushukuru.” Nanaa akasuuzika roho. Mungu ampe nini tena? Nyumba, gari na Jamal anayemtangazia wenyeji mchana kweupee!

 “Twende sasa nikuonyeshe kila mahali. Au njaa inakuuma?” “Hapana. Nipo sawa tu.” “Kwa hiyo unaniruhusu nikutengee chakula baadaye?” “Hamna shida.” Nanaa alijibu kwa kuridhika kabisa kitu kilichomfurahisha Jamal aliyekuwa akimezea mate mapaja aliyokuwa akiyaona ndani ya gauni. Sasa hivi yapo ndani ya nyumba yake! Nanaa si mtoto! Akarudi kumshika mkono kumuongoza atakapo yeye Jamal. Bila hiana, Nanaa akafuata kwa tabasamu.

Walifanikwa kuona chumba cha kwanza, choo cha wageni wakaishia chumbani kwa Jamal. Humo ndipo alipojua ni kweli Jamal alikuwa na uchu naye. Chumba kile kisafi, Jamal alikitumia ipasavyo kukata kiu. Na Nanaa naye hakumzuia. Akajituma ipasavyo. Hapakuwepo tena na Zac wakumfanya ashindwe kumvulia nguo Jamal. Akamkumbuka Terry, akajiambia kama angekuwepo wakati ule, yeye ndio angefaidi. Lakini akakumbuka uchu wa Zena kwa Terry. Akaona ajiachie tu. Akahangaika siku nzima kumfurahisha Jamal kwenye kitanda hicho bila hata kujali hisia zake ila lengo lake tu.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati akijituma hapo kitandani, akaanza kujifikiria jinsi atakavyokuwa mama wa ile nyumba, na kwa usafiri ule aliokuwa nao Jamal, sio pabaya sana kuanzia maisha. Hakuona chakupoteza kama akitoa penzi lake kwa Jamal, pengine atamvutia zaidi. Na kweli, hapakuwa na jinsi ungesema Jamal hakumfurahia Nanaa siku hiyo pale kitandani. Nanaa alitoa ujuzi wake wote siku ile kumfurahisha Jamal bila hata kujijali yeye. Alijituma kwa kadiri ya uwezo wake. Yale aliyokuwa akimfanyia Zac, ndio alipewa Jamal siku ile tena kwa juhudi huku akiongeza mautundu, asije kukimbiwa tena. Kwa Nanaa alikuwa ni kama yupo kazini. Lengo moja tu, ndoa. Awe na kwake, aepukane na kuishi au kuwa mzigo kwa mtu. Yeyote mwenye mafanikio kidogo ya maisha, huyo alimfaa. Hapakuwa na vigezo eti mwanaume mrefu. Sijui kifua kipana. Rangi sijui iweje! Hapana. Bora mwanaume, basi.

~~~~~~~~~~~~~~

Mapenzi yakachanganya, ratiba za maktaba zikaanza kuongezeka. Siku ambazo Jamal haendi kazini, siku hizo za jumamosi, Nanaa alifika nyumbani kwake asubuhi. Walipata kifungua kinywa pamoja, mapenzi kidogo, kisha kujisomea. Ikifika jioni, mapenzi tena yakuagana, ndipo anamrudisha Nanaa nyumbani kwao.

Mambo yakaenda vizuri, wakiwa wanatumia muda mwingi kusoma na mapenzi. Hapakuwa na maongezi mengi sana kati yao, kwani Jamal alionekana kumtaka zaidi Nanaa kitandani kuliko kitu kingine. Kile kitendo chakuonyeshwa anahitajika na mtu, kilimfariji sana Nanaa. Simu na ujumbe wakutakiwa usiku mwema, huku akiambiwa ni jinsi gani anasubiriwa kesho yake wakafanye hiki au kile havikuisha. Pengo la Zac likazibika kwa haraka sana. Yale aliyokuwa akifanyiwa na Zac, akakutana nayo kwa Jamal. Tena akimsifia vilivyo huku akimlaumu kumuacha akiwa bado anamuhitaji kwa mapenzi zaidi.

~~~~~~~~~~~~~~

Muda wa Nanaa wa kurudia mitihani yake ukafika. Akafanya akiwa ametulizwa kwenye penzi la Jamal aliyekuwa akimpa vihela vya hapa na pale vyakujikimu. Matokeo yakatoka, yale masomo akawa ameyafaulu, akaendelea mwaka wa pili na penzi la Jamal.

Kina Zena walipogundua si hatarishi tena kwani anaye mwanaume mwingine, urafiki ukarudi tena kati yao. Kwani Nanaa aliwaambia juu ya Jamal baada yakumuona anapilika pilika zisizoisha. Kama hakuwepo kwenye simu, basi anakuja kuchukuliwa na kuondoka. Ndipo Tia akamuuliza kulikoni. Ikabidi kuwaambia habari za kuvutia za mpenzi mpya mwenye gari na nyumba, si kama Zac.

Asijue amempa Zena habari za kumchafua zaidi kwa Terry, ili kumvuta kwake. Nanaa hakuwa akitoka nao tena, kwani alikuwa akija kuchukuliwa mara baada ya kipindi chao cha mwisho siku ya ijumaa. Kila alipokuwa akitoka kwenye lecture siku hiyo ya ijumaa, alimkuta Jamal akimsubiri nje. Alikuwa akimchukua siku za ijumaa anakuwa naye nyumbani kwake mpaka jumatatu asubuhi wakati Jamal akienda kazini ndipo anamshusha chuoni.

Nyumbani kwa kaka yake alikuwa akienda siku ya jumapili. Atakaa naye kidogo, na kumuaga. Kulala nyumbani kwa kaka yake akapunguza. Kama siku hiyo ya jumapili akienda kumtembelea kaka yake akapakuta pachafu, basi atamsaidia kusafisha na kufua. Akishaacha kila kitu sehemu yake na chakula, ndipo anaondoka kurudi kwa Jamal mpaka siku inayofuata, jumatatu.

Ilimbidi kuongeza juhudi ya kusoma hizo siku za kati kati ya juma. Maana siku hizo anazokuwepo kwa Jamal, kuanzia hiyo ijumaa jioni mpaka jumatatu asubuhi wanapotoka hapo kwa Jamal, Nanaa alikuwa mke kweli kweli. Kujituma kumpikia na penzi kitandani. Kufua na kufanya usafi kwenye kijinyumba hicho kidogo, ambacho Nanaa alishajiona ni mama mwenye nyumba. Yaani yupo kwake.

Asubuhi za hizo siku za jumatatu pia Jamal alimuaga kwa kujiridhisha kweli kweli akimwambia kwa kujifidia kwa siku hizo ambazo Nanaa hatakuwepo hapo. Walifanya penzi la kufidia jumanne, jumatano na alhamisi. Ijumaa usiku alirudishwa kitandani hapo. Na jumatatu asubuhi alitoa penzi la nguvu ndipo wanapooga, nakuanza siku. Jamal kazini, Nanaa chuoni. Maisha yakaendelea.

~~~~~~~~~~~~~~

Penzi alilokuwa akipewa Jamal halikuwa kama la Zac. Kwani Zac alipewa kwenye hosteli na nyumbani kwa rafiki yake. Hapakuwa na uhuru. Alipewa penzi la kimya kimya wakijua wapo wanachuo wengine wanapita nje ya chumba chao, au wengine wapo chumba cha jirani. Wakiwa nyumbani kwa rafiki yake Zac, pia iliwalazimu kuwa wastaarabu japo walijua anajua kinachoendelea huko chumbani. Lakini hapo kwa Jamal, Nanaa alikuwa huru.

Kwanza ni nyumba anayoishi peke yake. Majirani wapo mbali. Jamal hakuwa na maneno mengi. Alimuonyesha wazi anamtaka kitandani tu. Kila asubuhi anapokuwepo hapo nyumbani kwake, nilazima amwamshe kwa kumtaka kimapenzi. Tena penzi la haja. Jamal hakuwa mvivu hata kidogo katika hilo eneo. Kitu kilichomlazimu Nanaa mwenyewe kujituma kweli kweli hata kama ni asubuhi. Ndipo aamke akaandae kifungua kinywa. Na baada ya hapo tena warudi tena kitandani kama si siku za jumatatu. Kwa hiyo ikawa yupo kazini kwelikweli wala si mapenzi kuwa anayafurahia kama Jamal aliyemuhisi si mzima kwa jinsi alivyokuwa akiendekeza kitanda! Kama aliyekuwa akitumiwa, na wala si nguvu zake mwenyewe!

~~~~~~~~~~~~~~

Alikuwa akimshangaa vile Jamal alivyokuwa mkimya. Hakuwa mzungumzaji sana. Kama sio wanafanya mapenzi, basi wanaangalia mpira. Mechi za timu za nchi za bara la Ulaya au tamthilia za hapo hapo nyumbani. Alikuwa akikodisha movie mbalimbali ambazo pia walikuwa wakiangalia kila wanapokuwa pamoja. Na alimuonyesha wazi, pindi anapoangalia vitu vyake kwenye luninga, angependa kusikia na maneno. Kwa hiyo kunakuwa na utulivu wa aina yake. Hilo nalo Nanaa akalikubali na kuliheshimu ilimradi tu kuendeleza maisha bila kutaka kumuudhi, asije akakosa ndoa. Maisha yakaendelea.

~~~~~~~~~~~~~~

Katika hiyo hali ya kuchukuliana na kumvumilia Jamal akifanya mambo bora liende, siku moja ya jumapili wakati Jamal anaogo na Nanaa yupo kitandani, baada ya shuguli nzito hapo kitandani. Tena Nanaa akiwa anaugulia maumivu kwa mapenzi ya muda mrefu. Simu ya Jamal ikaanza kuita akiwa yupo bafuni. Nanaa akiwa hoi hapo kitandani, akigugumia maumivu ya michubuko mingi aliyoipata katikati ya tendo, nakushindwa hata kusema, au kumwambia Jamal ili tu kumfurahisha. Alibaki hapo kitandani akigugumia maumivu sehemu za siri huku akiitazama simu ya Jamal iliyokuwa ikiita na kukata.

~~~~~~~~~~~~~~

Tokea siku ya ijumaa wanafika hapo nyumbani mpaka siku hiyo ya jumapili, Jamal alionekana anataka kufanya mapenzi tu. Tangia anamchukua chuoni, Nanaa alishamuona hayupo sawa. Alipoingia kwenye gari akajua kuna tatizo. Nanaa alimsalimia kama kawaida. Akarudisha salamu kwa kifupi tu. Baada ya kuona amekuwa kimya sana au mzito wa maongezi, akaamua na yeye anyamaze. Walipofika tu nyumbani siku hiyo ya ijumaa, akamshusha nakutoka kufuata chakula. Hakutaka Nanaa apike. Alimwambia aoge, nakumsubiria.

Ndipo mapenzi yakaanza bila maongezi mengi. Kila alipomuuliza kulikoni, alimbusu, na kuanza tena  mapenzi. Jumamosi nayo ikawa hivyo hivyo. Anatoka kwenda kununua chakula. Baada ya muda anarudi, kazi inaendelea. Kwa ukavu ule aliokuwa akikutana nao kwa Nanaa nakuendelea kufanya naye mapenzi bila kujali, wala kutaka kumlainisha kwanza, japo Nanaa alishamjua si mtu wa kujali anachojisikia yeye wanapokuwa kwenye mapenzi, lakini siku ile alizidisha. Hapakuwa na mapumziko marefu wala maongezi. Wakati wote alitaka Nanaa amchezee na kuanza mapenzi tena na tena. Nanaa alijua lipo jambo. Alimchubua vilivyo. Mpaka inafika siku hiyo ya jumapili, Nanaa hakuwa na hamu tena yakuwepo pale.

Mara hiyo ya mwisho kabla yakuingia bafuni kuoga na kumuacha hapo kitandani, Nanaa alihangaika naye sana ili kumfikisha. Alishasahau hata walianza saa ngapi. Alifanya naye huku akigugumia na kujikaza sana. Alishamuomba Mungu wake amkumbuke kipindi kile, Jamal amalize, apumzike. Mpaka anafanikiwa, Nanaa hakuwa na hamu. Alilala pale kitandani akiwa hoi na maumivu makali sana akiwaza kama amuage Jamal na kumwambia amepata zarula anatakiwa kuondoka, au amwambie ukweli kama anavidonda vinavyompa maumivu makali sana. Hataweza kufanya tena mapenzi siku ile. “Ataniona sifai. Heri niendelee kujikaza, lakini nimkwepe mapenzi leo. Angalau nijiuguze mpaka tena ijumaa ijayo atakapokuja kunichukua. Nitakuwa nimepona.” Simu ya Jamal ikaita tena na kumtoa kwenye mawazo.

Nanaa Alizwa Tena.

Akamwita Jamal mara kadhaa kumuuliza kama ampelekee simu hiyo huko bafuni au ajibu yeye, lakini Jamal hakusikia. Ikaita mara tatu, kisha ujumbe ukaingia. ‘Mtoto bado ni mgonjwa, mume wangu. Pesa uliyonitumia haijatosha matibabu na chakula. Uliniahidi kuja leo. Mpaka sasa hujafika na simu hupokei. Nimeamua kwenda kwenu ili wanisaidie. Mama yako ameamua kumrudisha Fatma hospitalini, Barabara ya kwanza, ili afanyiwe vipimo upya. Homa ipo juu sana. Hapa tulipo tupo hospitalini. Naomba upokee simu mume wangu. Unatutia wasiwasi, hasa baba.’ Nanaa alikaa kwa mshituko. 

Wakati anafikiria na kurudia ule ujumbe, Jamal aliingia pale chumbani. “Mbona umeshika simu yangu bila ruhusa!? Unatafuta nini?” Jamal aliiuliza kwa hasira. “Kwa nini hukuniambia kama umeoa na unafamilia!?” Nanaa akauliza. “Uliuliza?” Jamal alijibu kwa kuuliza swali lililomfunga Nanaa mdomo. Alitamani kulaumu, lakini akakumbuka hamfahamu Jamal hata kidogo. Ni kweli hakudanganywa. Alitamani kulia. Lakini akajisuta moyoni. Anamlilia nani pale? Jamal hakuonyesha kufumaniwa hata kidogo.

Alichukua simu yake kutoka kwa Nanaa bila kuonyesha kuna la ajabu ila hasira ya Nanaa kushika simu yake. Akavaa pensi yake, akatoka pale chumbani bila hata maelezo ya ziada kwa Nanaa. Hakutaka kupoteza muda wake zaidi hapo ndani, Nanaa akavaa haraka haraka, akakusanya vitu vyake nakutoka bila hata yakuoga. Alikutana na Jamal nje akizungumza na simu, akampita na kuondoka bila ya kumsemesha neno hata la kwaheri.

~~~~~~~~~~~~~~

Kwa kutumia pesa alizokuwa amepewa na Jamal siku chache zilizopita, akachukua taksii kurudi chuoni. Hakutaka hata kupeleka sura yake kwa kaka yake. “Vipi Jamal? Mbona umerudi leo badala ya kesho?” Zena alimrushia swali mara alipofika chumbani kwao. Aliwakuta  wakiangalia tamthilia, kila mmoja akiwa kitandani kwake. “Wewe Nanaa? Si huwa unarudi jumatatu asubuhi?” Nanaa aliingia na kujitupa kitandani kwake bila kuongea chochote.

~~~~~~~~~~~~~~

Kwanza alikuwa na madonda ya penzi alilokuwa akilitoa tokea siku ya ijumaa alipochukuliwa hapo chuoni. Kwa hiyo alikuwa na maumivu makali sana. Alijichukia na kujidharau sana vile alivyokuwa akimvumilia, ili kumridhisha yeye Jamal. Alijinyima raha yeye, ili kumpa furaha mume wa mtu! Kwa kipi! Kwa nini!  

Pili alijichubua yeye mwenyewe donda la moyoni. Kwa haraka gani jamani! Hata muda wakutosha kutulia na kutafakari wapi anakosea, nini afanye cha tofauti ili kufanikisha lengo lake, haukuwa umepita tokea atendwe na Zac, akajitupa kwa Jamal. Bila kumfahamu Jamal, siku ya kwanza tu kukaribishwa nyumbani kwake, tayari kitandani, tena kwa sarakasi kibao! Nikulogwa au ujinga ulioje! Haraka hiyo ya kujigawa hivyo kama karanga za kwenye kapu zinazoonjeshwa kwa kila mtu, ili zinunuliwe hata kwa wasiokuwa na lengo nazo, ni za nini?

Hayo yote yakazua ububu kwa Nanaa kila akijiuliza bila kujipa jibu yeye mwenyewe. Hakujua awaeleze nini wenzake. Walishamshuhudia akiwa kwenye mahusiano ya mapenzi na wanaume wawili tofauti tofauti tena kwa muda mfupi mfupi, ndani ya mwaka mmoja, tena walijua  ni mahusiano mazito. Kwani Nanaa alikuwa akihama kabisa na kwenda kuwaridhisha hao wanaume huko wanakochagua wao. Halafu mahusiano yote hayakudumu! Anawaambia nini wao waliokuwa wakimsifia uzuri wa kila kitu? Alijua hata marafiki zake watamshangaa.

~~~~~~~~~~~~~~

Tia bado alikuwa kwenye mahusiano na Evan. Na hakuwahi kumsikia akimlalamikia huyo Evan hata mara moja. Habari za Evan zilizokuwa zikiletwa humo chumbani, ni sifa zake tupu. Vile anavyojua kumjali na kumpenda, basi. Tena Tia msichana wa kawaida kabisa. Hakuna cha rangi nyeupe wala umbo namba 6 au 8. Hakuna alikopita wanaume wakageuka au hata kuhisi kama amepita msichana wa ajabu. Lakini alitangaza kuenziwa na mwanaume aliyeanza naye tokea yupo kidato cha 5. Sasa yupo chuoni mwaka wa pili. Tena sio na mwanaume wa kijijini. Evan! Mtoto wa jijini. Ametoka kwenye familia ya wasomi, wenye exposure kubwa tu. Anajua warembo na sifa zake. Lakini Tia alijisifu vile alivyotulia kwake. Akazidi kupata ububu na aibu.

Alinyamaza pale kitandani, akijuta kwa nini aliwasaidia kutafuta chumba. Tena kuwafanya waishi nao chumba kimoja! Kama isingekuwa kuwasaidia kuwatafutia chumba, wala mwaka huo wa pili wasingeishi chumba kimoja tena. Usiku huo angekuwa na watu wengine. Wasiojua historia yake ya mapenzi. Na wala wasingejua kinachoendelea kwake. Nanaa akajuta sana. Akajua kwa mara nyingine tena, hao mashoga wawili watabaki kuwa mwiba wake kwa mwaka huo mzima tena.

~~~~~~~~~~~~~~

 Akataka kujilaumu zaidi lakini akajifariji kuwa hakuwa na jinsi. Kwani kipindi yeye yupo hapo chuoni akijiandaa na kurudia mitihani yake, Zena alimtafuta na kumuomba awasaidie kutafuta chumba kwa kuwa yeye alikuwa maeneo ya hapo chuoni, na walijua kuna matron alikuwa akimpenda sana Nanaa, wakajua wakimpanga vizuri Nanaa, watapa chumba hapo hapo Main Campus, wanapopapenda, tena kwenye sehemu nzuri. Nanaa na moyo wake wa kusamehe, akawasaidia mpaka kujikuta nao tena pamoja.

~~~~~~~~~~~~~~

Alinyanyuka kwenda kuoga baada ya maumivu kuendelea. Akaona akajisafishe labda maumivu yatatulia. Akanywa na dawa na kurudi kulala huku mikakati mikali ikiendelea kichwani mwake. Alishahangaika akidhani atapata mwanaume atakayempenda na kumthamini, akaishia kujidhalilisha tu. Alishagawa penzi kwa wanaume hao, lakini hakuna aliyeona uthamani wake. “Mhhh! Inatosha sasa.” Nanaa alijisemea moyoni. “Labda kweli shule ndio itakuwa mkombozi wangu pekee. Mapenzi yamenikataa. Nitulie, nishike moja. Shule tu.” Nanaa aliazimia moyoni.

~~~~~~~~~~~~~~

Alipopona tu madonda aliyoachiwa na Jamal, tena alijiuguza kwa kujipaka mafuta tu kila wakati bila kumwambia mtu. Huku asijue kama inasaidia au la! Kama anajiongezea sumu mwilini au la! Kila alipooga na kujisafisha, alipaka mafuta mpaka akapona. Maswali ya hofu yalipita kichwani mwake akijiuliza mbali na madonda yale, ni nini kingine Jamal alichomuachia!? Yalimtesa sana. Mwishowe akaona asijichoshe na maswali ambayo anaweza kupata majibu yake.

Akapiga moyo konde mpaka hospitali ya kulipia. Mbele ya daktari aliyemkuta siku hiyo akamwambia shida yake ni moja tu, kujua kama ameathirika au la! Alipomuuliza kwa nini hakwenda kwenye vituo vya Ushauri Nasaha, akasema moyo wake ulimtuma hapo. Hataki kuulizwa maswali wala hataki kushauriwa. Yeye anataka kupimwa UKIMWI, apewe majibu yake, basi. Mengine atajua mbele ya safari.

Kwa kuwa ilikuwa ni hospitali ya kulipia, pesa yake tu. Nanaa akapimwa. Alikaa pale akisubiria matokeo yake huku mawazo yakizunguka huku na kule. Yalipotoka na kuambiwa hajaathirika, akatoka pale bila kuaga. Akajiwekea mikakati yake. Akajiambia lazima kuitimiza hata iweje.

~~~~~~~~~~~~~~

Na kweli Nanaa aliamua kutulia na shule tu. Aliachana na kila aina ya marafiki na vishawishi vitakavyoingilia shule yake, akatuliza mawazo shuleni tu. Muda wa kuwepo hapo hosteli ukapungua. Akaanza kuishi nyumbani kwa kaka yake zaidi labda kuwe na test au ni kipindi cha mitihani. Alifanya hivyo ili kupunguza kero za wanaume walioanza kumfuata mpaka pale chumbani anakoishi na kina Tia.Walipojua tu Nanaa ameachwa tena na Jamal, Tia na Zena wakaanza kumkwepa tena huku wakimcheka waziwazi. Nanaa akajua. Akaamua kujitenga nao kabisa.

Wakiwa wanamsengenya Nanaa kwa mafumbo bila kujua Evan dereva wao aliyekuwa akiwaendesha anawasikiliza, Zena na Tia wakiwa wamekaa kiti cha nyuma wakicheka bila habari. Wakajikuta wanaropoka jina la Nanaa na kusema kuwa ameachwa tena. Evan hakuchelewesha zile habari. Wakiwa wamesimama kwenye mataa, Evan akamtumia ujumbe Terry kwa haraka sana. ‘Naona Mungu amesikia sala zako. Nanaa hana mtu tena. Nasikia ameachana na huyo mwanaume mwingine. Changamka. Huu ndio wakati wako kabla hajakupiku mwingine.’ Evan alituma ule ujumbe palepale wakati Zena na Tia wanaendelea kumcheka Nanaa.

          ~~~~~~~~~~~~~~

Terry akamtafuta Evan, wakapanga weekend inayofuata lazima Evan arudi jijini ili kumsindikiza hosteli, kwenye chumba cha Tia na Zena wakijua ndipo watakapompata Nanaa, kwa kuwa walijua wakipanga kuwaita Zena na Tia mahali, Nanaa hatakwenda. Na kweli siku ya ijumaa usiku Evan alitoka chuoni SUA akaenda moja kwa moja nyumbani kwa kina Terry. Wakazungumza na kupanga asubuhi na mapema waamkie chuo kikuu cha Mlimani. Ili tu Terry ambaye alikuwa akisubiri muujiza wake, akamuone Nanaa.

Siku inayofuata, Evan rafiki watokea utotoni wa Terry akawasili nyumbani kwao. Akamchukua, safari ya Mlimani ikaanza. Njiani alikuwa kimya. Evan alijua wazi anapanga hoja zake pindi atakapofanikiwa kumkuta Nanaa ambaye hawakuwa wamemuona kwa kipindi kirefu. Kila alipokuwa akimuulizia, Zena alimtinga na majibu aliyodhani yatavunja moyo wa Terry, lakini asijue ndio alikuwa akiongeza shauku ya Terry kuja kummiliki Nanaa.

Mungu alikuwa upande wao, walifika kwenye chumba cha kina Tia, saa nne asubuhi. Wakamkuta kweli Nanaa yupo. Lakini alikuwa kwenye simu. Mtu wa upande wa pili akiongea, ambaye alikuwa James. Nanaa alishawasalimia kwa kuwapungia mkono mara walipoingia chumbani hapo, akiwa na simu sikioni imeshikiliwa na mkono wa shoto. Wakulia ndio ulifanikiwa kuwapungia wakati wanaingia, akaendelea kukusanya baadhi ya vitu huku akizungumza kwenye simu.

Terry alijawa na furaha baada ya kumkuta Nanaa hapo ndani na kupata tabasamu lililosindikizwa na dimpozi nzuri za Nanaa. Akafarijika moyoni. Wakaendelea kusalimiana na Zena na Tia wakati Nanaa bado yupo kwenye simu. Ndipo wakasikia Nanaa akijibu, “Pole sana kaka yangu. Basi nakuja kukusaidia. Labda uji utakaa tumboni.” Hapo hapo Nanaa akachukua kijibegi chake kama pochi. Akawapungia tena mkono. Safari hii alikuwa akiwaaga, akatoka akiwa bado anazungumza kwenye simu.

~~~~~~~~~~~~~~

Haikuwa weekend nzuri hata kidogo kwa Terry. Pale pale alibadilika. “Twendeni basi.” Zena aliongea kwa sauti ya kuchangamka. Kwani waliingia na ofa ya kuwachukua na kuwapeleka kwenye kifungua kinywa. Terry alishabadilika mpaka alionekana usoni. “Hata mimi nipo tayari.” Tia naye aliongea huku akimsogelea Evan mpenzi wake. “Naombeni niwe muwazi. Mimi sitaongozana na nyinyi. Nilimfuata Nanaa, naona na yeye ameondoka. Sina kawaida ya kwenda kupata kifungua kinywa asubuhi asubuhi kwenye mabaa. Kwanza mimi sio mlevi, na pili kwetu wanakuwa na kifungua kinywa kizuri sana zaidi ya mahoteli mengi sana hapa mjini.” Akiwa na hasira, Terry akatoka.

Zena aliumia sana. Hapo hapo na yeye akakubaliana na matokeo. Kuwa hata iweje, Terry hawezi kumpenda. Wala hatawahi kuwa wake. “Nilidhani Terry atakuwa wangu!” Zena aliwaza moyoni, akiwa amejawa simanzi usoni. Japokuwa alishamuonyesha wazi kuwa anamtaka awe mpenzi wake, lakini Terry hakuonyesha kumtaka hata kidogo. Akakubali pia kosa halikuwa la Nanaa. Nanaa alishajitoa kwao muda mrefu sana. Na alikuwa na uhakika Nanaa na Terry hawakuwa wakiwasiliana kabisa. Kumuwekea kinyongo Nanaa alijua ni kumuonea tu. Nanaa mwenyewe alishamruhusu amchafue vile atakavyo kwa Terry  ili tu kumvutia kwake. Alielewa maumivu aliyonayo Terry kwa wakati ule, ‘kupenda asipopendwa!’ Inauma. Akamuhurumia kwani na yeye ndipo alipokuwepo kwa wakati huo. Alitamani ingekuwa vinginevyo ili mambo yawe tofauti. Lakini mapenzi ni kitu cha ajabu. Akaamua awaache tu Tia na Evan watoke wao peke yao. Yeye akabaki.

Mapinduzi.

A

kiwa njiani yale yaliyokuwa yakiendelea pale chumbani akiwa anazungumza na kaka yake kwenye simu yakamjia. Akakumbuka jinsi Zena alivyobabaika mara Evan na Terry walipoingia. “Zena bado anaonekana hajafanikiwa kwa Terry.” Nanaa akawaza. “Inabidi nijiweke nao mbali kabisa. Hata pale chumbani nihame. Nisije nikarudi, akapata sababu yakunichukia zaidi.” Nanaa alishajua wanamchukia. Hakutaka wamrushie yeye lawama. Akakusudia kutulia nyumbani kwa kaka yake moja kwa moja. “Hakuna kulala kwengine tena isipokuwa kwa kaka tu.” Akakusudia kuhama kwenye hicho chumba ambacho ni kama yeye ndio aliwakaribisha wenzake. Akaanza kuhamisha kitu kimoja baada ya kingine bila kuaga.

 Sio wanafunzi wa mwaka wa tatu wala wa kwanza waliokuwa wakimtafuta Nanaa tu. Hata wenzake wa darasa moja walimtafuta. Alikuwepo kama hayupo. Akiwa mahali alinyamaza kimya kama hayupo. Kwanza angezungumza nini wakati habari zake zilishasambazwa kila mahali na kina Zena na Tia. Wakidhani wanamuharibia zaidi, kumbe ndio wanaamsha wale waliokata tamaa kwenda kujaribu bahati zao na wao kwa Nanaa.

Lakini Nanaa alikusudia. Alikataa katakata swala la shule na mapenzi. Hata uwe na pesa na kumuahidi kumpa yeye gari, Nanaa asingekubali tena. Waliposhindwa kwa Nanaa mwenyewe, waliwafuata marafiki zake ili wawasaidie kuwatongozea kwa Nanaa. Alipoona fujo za Zena na Tia zinazidi, wanachukua pesa za watu kwa lengo la kugawa namba yake kwa watu asiowafahamu, akabadili namba na kuhamisha vitu vyake vyote pale chumbani. Maana wakati mwingine wa mchana, alikuwa akirudi kujipumzisha pale chumbani kwao, na ndipo hapo kina Zena hutoa habari kwa wanaume kuwa yupo chumbani. Akaamua kukusanya kila kitu chake mpaka kalamu. Na kweli akaacha kabisa kulala nje na nyumbani kwa kaka yake. Ikawa ni nyumbani kwa kaka yake James ambaye alikuwa kama ndiye ndugu wa pekee na mzazi wake Nanaa. Basi. Iwe karibu ya mitihani au la, Nanaa alihakikisha usiku analala nyumbani kwa kaka yake. Ikitokea anachelewa kumaliza kujisomea na wenzake, alimsihi James awe anamfuata chuoni ili arudi naye nyumbani.

~~~~~~~~~~~~~~

Hakika Nanaa hakuwa ametania. Alikusudia. Mpaka kina Tia wakaanza kuwa na hamu naye na kuanza kujirudi. Lakini aliyeng’atwa na nyoka, kang’atwa tu. Nanaa akawa makini kwa kila mtu anayemsogelea. Hakuonyesha hasira, lakini aliishi na kila mtu kwa tahadhari. Maisha yake ikawa shule, na nyumbani. Zena na Tia ndio waliobaki kusumbuliwa na wanaume. Na ndio waliokuwa wakipokea hongo ili kusaidia kumtongoza Nanaa, lakini Nanaa alibaki akiwacheka. “Mtakuja kubembwa juu juu nyinyi! Endeleeni kupokea pesa za watu.”

“Sasa kama huyu kaka mwingine kwa nini unamkataa?” Tia  alimuuliza. “Hana lolote. Anataka anivue nguo tu, ili aniangalie hili tako likiwa halina nguo. Anichezee halafu aje kuniumiza moyo wangu tu! Sitaki.” “Bwana huyu kaka anachanganywa na miguu yako.” “Sio miguu tu. Anasema anapenda kiuno cha Nanaa.” Zena alidakia. “Basi mpeni pole. Mwambieni atakiona kwenye gauni, lakini hatawahi kuniweka kitandani.” “Basi nenda hata kazungumze naye, Nanaa shoga yetu. Tumekula pesa yake.” Nanaa alicheka sana. “Mtajijua wenyewe. Aliyewaambia mpokee nani? Nishamaliza kazi ya kuvulia wanaume nguo. Kama hawakubahatika kipindi kile cha mgao, wapeni pole. Waambieni Nanaa ameshamaliza mgao.” Akawacheka na kuondoka mapema kabla giza halijaingia kuwahi kwa kaka yake.

~~~~~~~~~~~~~~

Kweli mapenzi ni kitendawili!

Je ni mara zote, au mara nyingi,  “Utapenda usipopendwa, na kupendwa, usipopenda”?

 Usikose Muendelezo kujua kama ndoto za Nanaa kama zitakuja kutimia!

Nani wa Nani? Mengi mazito yapo mbeleni.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment