~~~~~~~~~~~~~~
T |
erry
mtoto wa mama. Rafiki wa karibu sana na Evan. Watoto wa jiji. Lakini walicheza
kwa tahadhari. Wakilindana wasije wakapitiliza starehe, wakawaumiza wazazi wao.
Wote walitoka kwenye familia zenye hali nzuri, zinazojiweza kiuchumi. Wazazi
wasomi. Baba yake Evan alikuwa daktari katika hospitali kubwa ya Muhimbili,
wakati baba yake Terry alikuwa daktari katika hospitali binafsi waliyokuwa
wameanzisha yeye na marafiki zake. Wote walitoka kwenye familia ambazo hazikuwa
zikilia shida. Wazazi wanaoamini katika professinals, na wao walikuwa
wasomi. Kwa hiyo hata watoto wao walijua elimu ndio kila kitu. Hawakuzidisha
starehe na kusahau shule hata kidogo.
~~~~~~~~~~~~~~
Tokea mara ya kwanza Tia anamtambulisha Nanaa
kwenye kundi hilo. Yeye akiwa mgeni. Kwani Zena na Tia walishawahi kutoka nao
mara kadhaa kabla ya Nanaa. Walisha alikwa kwenye shuguli mbali mbali za wadogo
zao huko majumbani kwao. Iwe ni communion ya kwanza au kipaimara cha mmoja wa
wadogo zao kwenye kundi hilo la kina Evan, Tia na Zena pia walialikwa. Kwa hiyo
walijikuta wanafahamiana na wote kwenye kundi hilo kabla ya Nanaa kujiunga nao,
lakini Terry hakuonyesha hata uhitaji wa mwanamke mpaka alipokuja Nanaa.
Ilikuwa ni birthday ya mmpenzi wake Tia, Evan
ndipo Nanaa alipokwenda na yeye. Walianzia nyumbani kwa kina Evan. Walikuwa
ndugu, jamaa na marafiki wakaribu wa wasomi hao, wazazi wa wakina Tery na Evan.
Walikula na kunywa. Lakini Nanaa akaona jambo la pekee na ndipo akaja kuelewa
baadaye, ni kwa nini kina Evan na Terry, japokuwa ni watoto wenye uwezo wa
kujitosheleza majumbani kwao, lakini bado wamebaki kuwa ni vijana wenye kiasi.
Kabla ya kukata keki, wazee hao na wake zao, pamoja na ndugu, walimtaka Evan
aelezee alipo, anapofikiria kwenda, changamoto anazokabiliana nazo kwa wakati
huo, ni hatua gani amechukua mpaka hapo. Na nini anampango wa kufanyia kazi.
Basi hapo ndipo ataulizwa maswali na kuomba ashauri wenzake. Na kuelezea makosa
aliyoyafanya, na kushauri wasipite alikopita yeye au wasifanye kosa kama
alilofanya yeye.
Nanaa aliona ni kitu cha ajabu jinsi wazee hao
wanavyofanya kwa vijana wao, lakini akavutiwa sana. Walikuwa ni wakina baba wa
makamu, na walionekana wasomi tu. Wake zao hivyo hivyo. Lugha ya kingereza
ndiyo iliyokuwa ikitumika zaidi kati yao. Hata watoto wadogo kabisa walikuwa
wakitumia lugha hiyo kuashiria wote wanasoma kwenye shule za maana na kingereza
kwao sio lugha ya kujidaia. Ndio lugha ya mawasiliano kati yao.
Terry alimganda Nanaa jioni hiyo. Alimfuata kila
mahali na kutaka azungumze naye. Nanaa aliamua amuwahi mapema kabla
hawajaagana. “Ninaye mpenzi wangu. Anaitwa Zac. Anamaliza chuo mwaka huu. Tuna mpango
wa kuoana.” Terry alitabasamu. “Nilitaka kukukaribisha kwenye birthday yangu na
mimi jumamosi ijayo.” “Mmmh! Ningependa kuja, lakini kuanzia ijumaa nitakuwa na
Zac. Weekend hii nimeshindwa kwenda, kwahiyo weekend ijayo lazima tuwe wote.”
Nanaa alikataa kwa kujitetea. “Haitakuwa siku nzima. Ni jumamosi jioni. Ukiweza
kufika, nitafurahi kukuona Nanaa.” “Naomba nisikuahidi Terry. Huwa nikiwa na
Zac, hapendi niende mahali. Nakuwa naye mpaka jumapili jioni. Nashukuru kwa
mwaliko lakini.” Nanaa alitoa tabasamu na kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~
Terry alikuwa mwaka wa pili kwenye chuo cha IFM.
Ulishapita mwaka, tokea asalitiwe na mpenzi wake. Akaapa kutopenda tena. Lakini
hata wenzake waliona tofauti pale alipotokea Nanaa. Alikuwa akihangaika kupita
walivyomzoea. Evan alimshauri awe muwazi zaidi kwa Nanaa, kuliko vile
anavyojifanya katuni mbele za marafiki zake kila anapomuona Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~~
Siku ya birthday yake ilikuwa mbaya zaidi, kwani mpaka
sherehe inaisha Nanaa hakuwa ametokea. Alitoka na kwenda kukaa nje, nyuma ya
nyumba yao. Wakati wenzake wakifurahia ndani, wakila na kucheza, yeye alikuwa
nje mpaka watu wote wakatawanyika pale ndani nyumbani kwao. Hawakuwa wamemuona
Terry. Alijichukia kumpenda msichana ambaye kwanza alikuwa mgeni kwake.
Hamfahamu. Pili tayari anajua yupo na mpenzi wake. Tena mwanaume anayetarajia
kumuoa! Hicho ndicho kilimuuma zaidi. Lakini alishindwa kujisaidia. Anampenda
Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~~
Kidogo wivu ukaanza kwa Zena ambaye aliona anamstahili
Terry. Kwanza yeye kama ndiye wakwanza aliyemfahamu Terry kabla yake. Kila
walipokuwa wakikutana kwenye kundi hilo ambalo Tia ndiye alimkaribisha na
kukutana na kina kaka hao, palikuwepo na mazungumzo ya pamoja. Ukweli
hapakuwepo na mazungumzo binafsi kati ya Zena na Terry. Japo Zena alishaonyesha
kumpenda sana Terry. Kwanza alijua ni yeye peke yake kwenye kundi lile ambaye
hana msichana. Halafu ni Terry jamani! Nani asimpende?
Analishwa na kutuzwa vizuri na mama yake. Hana
mawazo ya kufikiria pesa, kama watu wengi. Mtoto wa mama. Hawezi kutoka
nyumbani mpaka mama yake ahakikishe amekula na ana nguo safi. Akitoka mama
akiwa kazini, basi atapigiwa simu kuulizwa. Na pengine kuambiwa apitie ofisini
kwa mama yake, akachukue pesa za matumizi ili mradi tu amuangalie hali ya
kijana wake kabla hajarudi chuoni japo ni hapohapo jijini. Gari anayotembelea
ni ya nyumbani. Hajui hata kama huwa inafanyiwa matengenezo au la. Hilo
lilikuwa jukumu la dad au mama, yeye kazi yake ni kulitumia tu.
Kwa nini usimpende Terry? Ngozi nzuri. Anaongea
lugha ya kingereza na tabasamu zuri usoni. Akionyesha ametulia. Hana shida ya
kumnunulia mtu yeyote zawadi kutoka kwenye pesa ya ziada anayopewa nyumbani.
Hawazi kutaliwa nini, wala kulipa garama yeyote. Ni yeye tu. Kila ijumaa
anarudi nyumbani na nguo chafu za juma nzima. Zinafuliwa na kupigwa pasi ndipo
zirudi tena hosteli. Shida hamna. Ila sasa ni mapenzi. Alisalitiwa, akampenda
Nanaa mchumba wa mtu, ambaye anamuumiza moyo wake.
Sukari Inaanza Kuingia
Shubiri.
W |
ivu
ukazidi kwa Zena kwani alishamshirikisha yeye na Tia jinsi anavyovutiwa na
Terry. Sasa hasira ilimpanda zaidi pale alipomkuta akizungumza na kucheka na
Terry upande wa baa wakati wengine wote wamekaa upande wa baharini walipokuwa
Kigamboni juma moja baada ya birthday ya Terry. Nanaa alitoka upande wa
baharini akiwaaga anakwenda maliwatoni. Baada ya muda kidogo, Zena akamuona
Terry na yeye amesimama anaondoka
kuelekea upande aliokwenda Nanaa. Akajua wazi anayemfuata ni Nanaa. Kwani Terry
alishindwa kabisa kuficha hisia zake kwa Nanaa. Hakuacha kumuuliza maswali
mbele yao na kuchangia chochote Nanaa anachozungumza.
Wakati Nanaa anatoka chooni, akamuona Terry.
Alimfanyia ishara ya kumuita, Nanaa akamfuata pale alipomkuta amekaa upande wa
baa kama anaagiza vinywaji. Kwa kuwa Terry alimualika kwenye birthday yake na
hakwenda, Nanaa akaona huo ndio wakati mwafaka wakuomba radhi na kuuliza mambo
yalikwendaje siku hiyo. Akiwa hajui jinsi alivyomuumiza Terry, Nanaa
aliongea kama jambo la kawaida huku akitaka michapo ya siku hiyo.
Wakiwa kwenye mazungumzo, hata hawajafika mbali,
Zena naye akawasogelea. Akiwa hajui hili
wala lile kinachoendelea si kwa Zena tu ambaye ni rafiki kipenzi, hata Terry
pia, Nanaa akatoa ahadi isiyo na hatia. “Basi kwa malipizi, itabidi nikutoe
kwa chakula cha mchana. Tusherehekee tena birthday yako. Nitakuletea na zawadi.
Ili ujue sikuwa nimekusudia kukosa birthday yako.” Nanaa aliongea huku
akicheka. “Nilishamwambia ilikuwa ni weekend ya Zac. Ulikuwa kwa mpenzi
wako.” Zena akaongeza kwa haraka. “Afadhali unitetee Zena shoga yangu. Terry
anajua nilikimbia.” Nanaa akaongeza akicheka.
“Tusirudi nyuma, tukaharibu ahadi ya kunitoa.”
Terry aliongeza. Nanaa akacheka. “Hilo tu? Usijali. Nakutafutia siku yako
maalumu.” Nanaa akaongeza akijua ni utani kabisa, akacheka na kuondoka.
Aliwaacha pale baa Zena na Terry. Wala asijue kwenye kundi walirudi baada ya
muda gani. Asijue kama Zena alirudi akiwa na furaha au la. Kwa kuwa muda
ulikuwa umeshakwenda, hata Zena alipowaambia Tia na Nanaa waondoke, Nanaa
hakuona kuna jambo la ajabu. Walishakula. Wakaongea na kucheka. Ilishakuwa
jioni. Akaona ni sawa kuondoka. Asijue kinachoendelea.
~~~~~~~~~~~~~~
Halikuwa kosa la Nanaa. Kwani wakati Zena
anawaambia jinsi anavyompenda Terry, wakiwa chumbani kwao. Kila mmoja kitandani
kwake, yeye Nanaa alikuwa aki chat na Zac. Ukweli alikuwepo pale, lakini
mawazo hayakuwepo pale hata kidogo. Alikuwa akipokea jumbe za mapenzi kutoka
kwa Zac. Akisifia penzi alilompa kabla hawajaagana siku hiyo ya jumapili. Zac
alimwambia alifurahishwa na hiki na kile, ilimradi tu kumfurahisha Nanaa. Kwa
hiyo akili ya Nanaa ikawa imezama kwenye simu yake akifurahia zile jumbe, huku
akifikiria na yeye maneno mazuri ya mapenzi ya kurudisha kwa Zac wakati Zena
akiendelea na yeye kueleza hisia zake kwa Terry. Hata hakuwa akiwasikiliza Tia
na Zena. Kwanza alijua ni mazungumzo yao binafsi marafiki hao aliowakuta.
Halafu pia alikuwa amechoshwa na mapenzi ya kujituma zaidi ya kawaida kwa Zac
aliyedhania kwa hakika atakuwa mume. Kuanzia ijumaa usiku mpaka jumapili hiyo
anarudi hosteli Nanaa alikuwa akijituma tu kitandani bila kuonyesha kuchoka ila
kufurahia kwa uongo.
~~~~~~~~~~~~~~
Siku hiyo walipotoka Kigamboni, Terry na Evan
ndio waliokuwa wakiwasaidia usafiri. Nanaa aliomba ashushwe kwa kaka yake, mtaa
wa Kijitonyama, karibu na Usalama wa Taifa. Inamaana Zena angebaki peke yake
kwa kuwa mara nyingi yeye Tia hubaki na Evan mpaka siku inayofuata ya jumapili,
Evan akirudi chuoni SUA, mjini Morogoro ndipo Tia anarudi hosteli.
Wakati Nanaa anashuka, aliwaaga kwa kicheko
asijue kinachoendelea. Aliwaacha Zena, Tia, Terry na Evan kwenye gari. Safari
ya kumpeleka Zena karibu na kituo cha daladala kumfikisha kwao ambako asigethubutu
kuonekana anarudishwa na mwanaume, ikaanza. Mazungumzo yote ndani ya gari baada
ya kushuka Nanaa, ilikuwa Terry akifurahia ahadi yakutolewa na Nanaa. Hata Tia
aliumia sana. Asiamini Nanaa anawezaje kumfanyia hivyo Zena! Tena baada ya
kuwaambia wazi vile anavyojisikia kwa Terry! Halafu tayari Nanaa alikuwa na
mpenzi wake Zac! Tia akaona vile Zena alivyoumia, ikamuuma zaidi mpaka
akabadili mpango wao. Akamwambia Evan waonane kesho ili yeye awe na Zena usiku
huo. Akaamua akalale na shoga yake ili amfariji. Evan hakuwa na tatizo.
Akawashusha kituoni, na hapo ndipo wakapata
nafasi ya kumsema vizuri Nanaa. “Tabia yake mbaya!” Zena alianza kutupa
shutuma. “Hatosheki na wanaume!” Tia akamuunga mkono shoga yake. “Amesahau sisi
ndio tumemtambulisha kwao? Ametawala kundi zima sasa hivi, utafikiri yeye ndio
mwenyeji wetu jamani!” Zena akaendelea kulalamika. “Hukumuona vile alivyokuwa
akijishaua kwa Terry. Niliwakuta peke yao kule upande wa baa. Nanaa akijinadi.”
Mashoga hao waliongea mapungufu yote ya Nanaa, wakakubaliana kumtema tu.
Mkakati wa
jumatatu kumtoa kwenye urafiki rasmi ukapangwa wakiwa hapo hapo kwenye kituo cha
daladala cha Tanki Bovu karibu sana na kwa kina Zena. Wakaadhimia kufuta kabisa
urafiki na wala wasiongozane naye popote ili inapofika siku ya kukutana na
kundi la kina Evan, Nanaa asiwepo. Baada ya kuafikiana na mkakati wao juu ya
Nanaa ambaye gafla amekuwa adui, ndipo wakaelekea nyumbani kwa kina Zena
ambako ni kama kwa kina Tia pia. Kwa kuwa wazazi wa Tia walishakuja kumkabidhi
Tia rasmi hapo kwa wazazi wa Zena, basi Tia hakumuhitaji Zena kufika kwa mama
Hiza. Akawa ameshazoeleka pale nyumbani. Urafiki wa wazazi uliokuwa unaelekea
kwenye undugu kati ya familia hizo mbili ukawa umeshakomaa.
~~~~~~~~~~~~~~
Akiwa hajui lolote Nanaa alirudi hosteli siku
inayofuata ya jumapili akiwa na tabasamu lake lote. Akawakuta Tia na Zena chumbani
kwao. Akaona wote wamenuna. Nanaa akaanza kuwatizama kwa zamu na kucheka.
“Mbona kama mmeninunia? Nimefanyaje tena!?” Nanaa aliwauliza huku akiwatizama
kwa zamu. Ndipo Zena alipomjibu kwa jazba vile walivyokerwa na tabia yake
yakutaka kumpora Terry wake. Wakashangaa Nanaa anacheka sana. Wakatulia kidogo.
“Unacheka nini sasa? Unafikiri mazuri?” Zena
aliuliza akiwa amepunguza jazba. “Kumbe unamtaka Terry?” Nanaa akauliza huku akicheka
akiwa amepuuzia kabisa. “Kumbe!” Zena akajibu kwa utulivu. “Aiii! Mimi sina
hata shida naye. Wewe tafuta neno baya lolote la kunichafua kwa huyo Terry,
halafu mwambie unampenda.” Wakaangaliana. “Kweli!?” Wote wakauliza kwa pamoja
wasiamini. “Sasa mimi wa nini huyo Terry? Zac mwenyewe ananishinda! Terry
nitamuweka wapi mimi na ratiba ngumu ya Zac? Ijumaa mpaka jumapili ananitaka
kitandani mpaka nimkimbie, kwa kisingizio cha kumwambia naenda kwa kaka!” Tia
na Zena wakajiweka sawa.
“Tena kukusaidia tu Zena, mimi niache kuja kwenye
mikusanyiko yenu. Akishajiona mpo naye, lazima atakuchangamkia. Kwanza unalipa
shoga yangu!” Roho ya Zena ikaanza kusuuzika, akaanza kucheka. “Sasa kwa nini
hukuniambia tokea mwanzo? Mimi hata sikuwa na wazo! Kwanza mbona nilishamwambia
Terry kuwa ninaye Zac?” “Niliwaambia.” “Basi mimi hata sikuwa na wazo. Labda
akili yangu haikuwepo. Sasa mlipanga kuninunia mpaka lini!?” Nanaa aliuliza kwa
kuwasuta. “Wala hatukuwa tumekununia.” “Mmmh! Aibu zenu wanawake.” Vicheko na
mikakati yakumpata Terry ikaendelea jioni hiyo mpaka wakaamua kutoka na kwenda
kujisomea.
Baada
Ya Kusalitiwa Kwa Mara Ya Pili.
N |
anaa
alitoka pale Mabibo hosteli moyo na mwili ukiwa kama umekufa ganzi. Asielewe
anatatizo gani. Kama uzuri, alisifiwa mpaka na wanawake wenzake. Kwa hakika
Ndina haoni ndani. “Nilijua Zac ni wangu!”
Nanaa aliendelea kuwaza kwa uchungu. Mapenzi aliyokuwa akionyeshwa na Zac, kwa
hakika Nanaa alijua amefika. Sifa zilizokuwa zikimwagiwa kwake, kuanzia umbile
na mambo wanayofanya pamoja, hakuwahi hata kuhisi kama Zac anaweza kugusa
mwanamke mwingine. Faraja aliyokuwa akimpa! Mbele za watu alimkumbatia na
kumbusu. Ni kama alikuwa akitangazia uma wote kuwa Nanaa ni wake. Anarudishaje
sura yake kwa watu waliokuwa wakiyajua mapenzi yale? Anaishije tena bila penzi
zito la Zac?
Zikiwa zimebaki siku chache za mitihani, Nanaa
akijaribu kujifikiria hatima yake kimapenzi, alishindwa kusoma kabisa. Kila
akiinamia vitabu, badala yakuona maandishi, macho yalimuona Zac na Ndina pale
kitandani. Akaamua awekeze muda mwingi wakujisomea kwenye makundi ya wenzake
wanao soma pamoja. Lakini pia haikusaidia. Mawazo yaligoma kuwepo pale.
Yalisambaa kwenye jumbe za mapenzi alizokuwa akitumiwa na Zac. Simu za kutakiwa
usiku mwema kila siku na maneno matamu kutoka kwa Zac. Si asubuhi si mchana,
Zac aliwasiliana naye. Hata akiwa kwenye vipindi, aliweza kumtumia ujumbe Nanaa
kumwambia kuwa anamfikiria yeye.
Leo anaishije bila hayo maisha matamu yaliyokuwa
yamejaa faraja? Mitihani yakumaliza mwaka wa kwanza ilimalizika kwa shida mno.
Matokeo yalitoka lakini yalikuwa mabaya sana kwa Nanaa. Alifeli masomo mawili
nakutakiwa kuyarudia. Na yale masomo aliyokuwa amefaulu ni kama alikuwa kwenye
mstari wa kufeli kabisa. Yote alipata alama ya “C”.
~~~~~~~~~~~~~~
Shule
ambayo aliapa kuwa mkombozi wake ipo matatizoni sababu ya mapenzi.
Ndoa anazolilia
kumtoa kwenye wegazi, hazionekani kutoa matokeo
mazuri kwa
Nanaa.
Nini
kitaendelea?
Usikose Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment