Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu ya 4. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu ya 4.

 Kilichokuwa kikimuumiza Nanaa ni vile alivyokuwa amejitoa kwa Zac na kujiaminisha yeye ni watofauti. Akabaki kuwa muaminifu kwake. Hata rafiki wa Evan, Terry aliyekuwa akisoma IFM alipokuwa akimtongaza Nanaa, alikataa kata kata, huku akijigamba anaye mpenzi. Alimwambia Terry kuwa si kwamba anaye tu mpenzi, bali mume. Nanaa alijisifia siku hiyo mbele ya kundi hilo walipokuwa wamekwenda beach ya Kigamboni, kupumzika. “Nampenda Zac. Na yeye ananipenda kwa dhati. Sijaona wala hakuna mwanaume kama Zac.” Hayo ndiyo maneno ya Nanaa alipojisifu mbele ya marafiki hao wakiume wa Evan. Wote walimsikiliza na kufunga kinywa wakijua ule ujumbe ulitoka kwa Nanaa ukiwa hauna hila, ila ulimuumiza sana Terry. Ni kama alikuwa akiwatangazia umma, hayupo tena sokoni. Zoezi la kutafuta na kutafutwa lilishafungwa.

~~~~~~~~~~~~~~

T

erry mtoto wa mama. Rafiki wa karibu sana na Evan. Watoto wa jiji. Lakini walicheza kwa tahadhari. Wakilindana wasije wakapitiliza starehe, wakawaumiza wazazi wao. Wote walitoka kwenye familia zenye hali nzuri, zinazojiweza kiuchumi. Wazazi wasomi. Baba yake Evan alikuwa daktari katika hospitali kubwa ya Muhimbili, wakati baba yake Terry alikuwa daktari katika hospitali binafsi waliyokuwa wameanzisha yeye na marafiki zake. Wote walitoka kwenye familia ambazo hazikuwa zikilia shida. Wazazi wanaoamini katika professinals, na wao walikuwa wasomi. Kwa hiyo hata watoto wao walijua elimu ndio kila kitu. Hawakuzidisha starehe na kusahau shule hata kidogo.

~~~~~~~~~~~~~~

Tokea mara ya kwanza Tia anamtambulisha Nanaa kwenye kundi hilo. Yeye akiwa mgeni. Kwani Zena na Tia walishawahi kutoka nao mara kadhaa kabla ya Nanaa. Walisha alikwa kwenye shuguli mbali mbali za wadogo zao huko majumbani kwao. Iwe ni communion ya kwanza au kipaimara cha mmoja wa wadogo zao kwenye kundi hilo la kina Evan, Tia na Zena pia walialikwa. Kwa hiyo walijikuta wanafahamiana na wote kwenye kundi hilo kabla ya Nanaa kujiunga nao, lakini Terry hakuonyesha hata uhitaji wa mwanamke mpaka alipokuja Nanaa.

Ilikuwa ni birthday ya mmpenzi wake Tia, Evan ndipo Nanaa alipokwenda na yeye. Walianzia nyumbani kwa kina Evan. Walikuwa ndugu, jamaa na marafiki wakaribu wa wasomi hao, wazazi wa wakina Tery na Evan. Walikula na kunywa. Lakini Nanaa akaona jambo la pekee na ndipo akaja kuelewa baadaye, ni kwa nini kina Evan na Terry, japokuwa ni watoto wenye uwezo wa kujitosheleza majumbani kwao, lakini bado wamebaki kuwa ni vijana wenye kiasi. Kabla ya kukata keki, wazee hao na wake zao, pamoja na ndugu, walimtaka Evan aelezee alipo, anapofikiria kwenda, changamoto anazokabiliana nazo kwa wakati huo, ni hatua gani amechukua mpaka hapo. Na nini anampango wa kufanyia kazi. Basi hapo ndipo ataulizwa maswali na kuomba ashauri wenzake. Na kuelezea makosa aliyoyafanya, na kushauri wasipite alikopita yeye au wasifanye kosa kama alilofanya yeye.

Nanaa aliona ni kitu cha ajabu jinsi wazee hao wanavyofanya kwa vijana wao, lakini akavutiwa sana. Walikuwa ni wakina baba wa makamu, na walionekana wasomi tu. Wake zao hivyo hivyo. Lugha ya kingereza ndiyo iliyokuwa ikitumika zaidi kati yao. Hata watoto wadogo kabisa walikuwa wakitumia lugha hiyo kuashiria wote wanasoma kwenye shule za maana na kingereza kwao sio lugha ya kujidaia. Ndio lugha ya mawasiliano kati yao.

Terry alimganda Nanaa jioni hiyo. Alimfuata kila mahali na kutaka azungumze naye. Nanaa aliamua amuwahi mapema kabla hawajaagana. “Ninaye mpenzi wangu. Anaitwa Zac. Anamaliza chuo mwaka huu. Tuna mpango wa kuoana.” Terry alitabasamu. “Nilitaka kukukaribisha kwenye birthday yangu na mimi jumamosi ijayo.” “Mmmh! Ningependa kuja, lakini kuanzia ijumaa nitakuwa na Zac. Weekend hii nimeshindwa kwenda, kwahiyo weekend ijayo lazima tuwe wote.” Nanaa alikataa kwa kujitetea. “Haitakuwa siku nzima. Ni jumamosi jioni. Ukiweza kufika, nitafurahi kukuona Nanaa.” “Naomba nisikuahidi Terry. Huwa nikiwa na Zac, hapendi niende mahali. Nakuwa naye mpaka jumapili jioni. Nashukuru kwa mwaliko lakini.” Nanaa alitoa tabasamu na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Terry alikuwa mwaka wa pili kwenye chuo cha IFM. Ulishapita mwaka, tokea asalitiwe na mpenzi wake. Akaapa kutopenda tena. Lakini hata wenzake waliona tofauti pale alipotokea Nanaa. Alikuwa akihangaika kupita walivyomzoea. Evan alimshauri awe muwazi zaidi kwa Nanaa, kuliko vile anavyojifanya katuni mbele za marafiki zake kila anapomuona Nanaa.

~~~~~~~~~~~~~~

Siku ya birthday yake ilikuwa mbaya zaidi, kwani mpaka sherehe inaisha Nanaa hakuwa ametokea. Alitoka na kwenda kukaa nje, nyuma ya nyumba yao. Wakati wenzake wakifurahia ndani, wakila na kucheza, yeye alikuwa nje mpaka watu wote wakatawanyika pale ndani nyumbani kwao. Hawakuwa wamemuona Terry. Alijichukia kumpenda msichana ambaye kwanza alikuwa mgeni kwake. Hamfahamu. Pili tayari anajua yupo na mpenzi wake. Tena mwanaume anayetarajia kumuoa! Hicho ndicho kilimuuma zaidi. Lakini alishindwa kujisaidia. Anampenda Nanaa.

~~~~~~~~~~~~~~

Kidogo wivu ukaanza kwa Zena ambaye aliona anamstahili Terry. Kwanza yeye kama ndiye wakwanza aliyemfahamu Terry kabla yake. Kila walipokuwa wakikutana kwenye kundi hilo ambalo Tia ndiye alimkaribisha na kukutana na kina kaka hao, palikuwepo na mazungumzo ya pamoja. Ukweli hapakuwepo na mazungumzo binafsi kati ya Zena na Terry. Japo Zena alishaonyesha kumpenda sana Terry. Kwanza alijua ni yeye peke yake kwenye kundi lile ambaye hana msichana. Halafu ni Terry jamani! Nani asimpende?

Analishwa na kutuzwa vizuri na mama yake. Hana mawazo ya kufikiria pesa, kama watu wengi. Mtoto wa mama. Hawezi kutoka nyumbani mpaka mama yake ahakikishe amekula na ana nguo safi. Akitoka mama akiwa kazini, basi atapigiwa simu kuulizwa. Na pengine kuambiwa apitie ofisini kwa mama yake, akachukue pesa za matumizi ili mradi tu amuangalie hali ya kijana wake kabla hajarudi chuoni japo ni hapohapo jijini. Gari anayotembelea ni ya nyumbani. Hajui hata kama huwa inafanyiwa matengenezo au la. Hilo lilikuwa jukumu la dad au mama, yeye kazi yake ni kulitumia tu.

Kwa nini usimpende Terry? Ngozi nzuri. Anaongea lugha ya kingereza na tabasamu zuri usoni. Akionyesha ametulia. Hana shida ya kumnunulia mtu yeyote zawadi kutoka kwenye pesa ya ziada anayopewa nyumbani. Hawazi kutaliwa nini, wala kulipa garama yeyote. Ni yeye tu. Kila ijumaa anarudi nyumbani na nguo chafu za juma nzima. Zinafuliwa na kupigwa pasi ndipo zirudi tena hosteli. Shida hamna. Ila sasa ni mapenzi. Alisalitiwa, akampenda Nanaa mchumba wa mtu, ambaye anamuumiza moyo wake.

Sukari Inaanza Kuingia Shubiri.

W

ivu ukazidi kwa Zena kwani alishamshirikisha yeye na Tia jinsi anavyovutiwa na Terry. Sasa hasira ilimpanda zaidi pale alipomkuta akizungumza na kucheka na Terry upande wa baa wakati wengine wote wamekaa upande wa baharini walipokuwa Kigamboni juma moja baada ya birthday ya Terry. Nanaa alitoka upande wa baharini akiwaaga anakwenda maliwatoni. Baada ya muda kidogo, Zena akamuona Terry na yeye  amesimama anaondoka kuelekea upande aliokwenda Nanaa. Akajua wazi anayemfuata ni Nanaa. Kwani Terry alishindwa kabisa kuficha hisia zake kwa Nanaa. Hakuacha kumuuliza maswali mbele yao na kuchangia chochote Nanaa anachozungumza.

Wakati Nanaa anatoka chooni, akamuona Terry. Alimfanyia ishara ya kumuita, Nanaa akamfuata pale alipomkuta amekaa upande wa baa kama anaagiza vinywaji. Kwa kuwa Terry alimualika kwenye birthday yake na hakwenda, Nanaa akaona huo ndio wakati mwafaka wakuomba radhi na kuuliza mambo yalikwendaje siku hiyo. Akiwa hajui jinsi alivyomuumiza Terry, Nanaa aliongea kama jambo la kawaida huku akitaka michapo ya siku hiyo.

Wakiwa kwenye mazungumzo, hata hawajafika mbali, Zena naye akawasogelea.  Akiwa hajui hili wala lile kinachoendelea si kwa Zena tu ambaye ni rafiki kipenzi, hata Terry pia, Nanaa akatoa ahadi isiyo na hatia. “Basi kwa malipizi, itabidi nikutoe kwa chakula cha mchana. Tusherehekee tena birthday yako. Nitakuletea na zawadi. Ili ujue sikuwa nimekusudia kukosa birthday yako.” Nanaa aliongea huku akicheka. “Nilishamwambia ilikuwa ni weekend ya Zac. Ulikuwa kwa mpenzi wako.” Zena akaongeza kwa haraka. “Afadhali unitetee Zena shoga yangu. Terry anajua nilikimbia.” Nanaa akaongeza akicheka.

“Tusirudi nyuma, tukaharibu ahadi ya kunitoa.” Terry aliongeza. Nanaa akacheka. “Hilo tu? Usijali. Nakutafutia siku yako maalumu.” Nanaa akaongeza akijua ni utani kabisa, akacheka na kuondoka. Aliwaacha pale baa Zena na Terry. Wala asijue kwenye kundi walirudi baada ya muda gani. Asijue kama Zena alirudi akiwa na furaha au la. Kwa kuwa muda ulikuwa umeshakwenda, hata Zena alipowaambia Tia na Nanaa waondoke, Nanaa hakuona kuna jambo la ajabu. Walishakula. Wakaongea na kucheka. Ilishakuwa jioni. Akaona ni sawa kuondoka. Asijue kinachoendelea.

~~~~~~~~~~~~~~

Halikuwa kosa la Nanaa. Kwani wakati Zena anawaambia jinsi anavyompenda Terry, wakiwa chumbani kwao. Kila mmoja kitandani kwake, yeye Nanaa alikuwa aki chat na Zac. Ukweli alikuwepo pale, lakini mawazo hayakuwepo pale hata kidogo. Alikuwa akipokea jumbe za mapenzi kutoka kwa Zac. Akisifia penzi alilompa kabla hawajaagana siku hiyo ya jumapili. Zac alimwambia alifurahishwa na hiki na kile, ilimradi tu kumfurahisha Nanaa. Kwa hiyo akili ya Nanaa ikawa imezama kwenye simu yake akifurahia zile jumbe, huku akifikiria na yeye maneno mazuri ya mapenzi ya kurudisha kwa Zac wakati Zena akiendelea na yeye kueleza hisia zake kwa Terry. Hata hakuwa akiwasikiliza Tia na Zena. Kwanza alijua ni mazungumzo yao binafsi marafiki hao aliowakuta. Halafu pia alikuwa amechoshwa na mapenzi ya kujituma zaidi ya kawaida kwa Zac aliyedhania kwa hakika atakuwa mume. Kuanzia ijumaa usiku mpaka jumapili hiyo anarudi hosteli Nanaa alikuwa akijituma tu kitandani bila kuonyesha kuchoka ila kufurahia kwa uongo.

~~~~~~~~~~~~~~

Siku hiyo walipotoka Kigamboni, Terry na Evan ndio waliokuwa wakiwasaidia usafiri. Nanaa aliomba ashushwe kwa kaka yake, mtaa wa Kijitonyama, karibu na Usalama wa Taifa. Inamaana Zena angebaki peke yake kwa kuwa mara nyingi yeye Tia hubaki na Evan mpaka siku inayofuata ya jumapili, Evan akirudi chuoni SUA, mjini Morogoro ndipo Tia anarudi hosteli.

Wakati Nanaa anashuka, aliwaaga kwa kicheko asijue kinachoendelea. Aliwaacha Zena, Tia, Terry na Evan kwenye gari. Safari ya kumpeleka Zena karibu na kituo cha daladala kumfikisha kwao ambako asigethubutu kuonekana anarudishwa na mwanaume, ikaanza. Mazungumzo yote ndani ya gari baada ya kushuka Nanaa, ilikuwa Terry akifurahia ahadi yakutolewa na Nanaa. Hata Tia aliumia sana. Asiamini Nanaa anawezaje kumfanyia hivyo Zena! Tena baada ya kuwaambia wazi vile anavyojisikia kwa Terry! Halafu tayari Nanaa alikuwa na mpenzi wake Zac! Tia akaona vile Zena alivyoumia, ikamuuma zaidi mpaka akabadili mpango wao. Akamwambia Evan waonane kesho ili yeye awe na Zena usiku huo. Akaamua akalale na shoga yake ili amfariji. Evan hakuwa na tatizo.

Akawashusha kituoni, na hapo ndipo wakapata nafasi ya kumsema vizuri Nanaa. “Tabia yake mbaya!” Zena alianza kutupa shutuma. “Hatosheki na wanaume!” Tia akamuunga mkono shoga yake. “Amesahau sisi ndio tumemtambulisha kwao? Ametawala kundi zima sasa hivi, utafikiri yeye ndio mwenyeji wetu jamani!” Zena akaendelea kulalamika. “Hukumuona vile alivyokuwa akijishaua kwa Terry. Niliwakuta peke yao kule upande wa baa. Nanaa akijinadi.” Mashoga hao waliongea mapungufu yote ya Nanaa, wakakubaliana kumtema tu.

 Mkakati wa jumatatu kumtoa kwenye urafiki rasmi ukapangwa wakiwa hapo hapo kwenye kituo cha daladala cha Tanki Bovu karibu sana na kwa kina Zena. Wakaadhimia kufuta kabisa urafiki na wala wasiongozane naye popote ili inapofika siku ya kukutana na kundi la kina Evan, Nanaa asiwepo. Baada ya kuafikiana na mkakati wao juu ya Nanaa ambaye gafla amekuwa adui, ndipo wakaelekea nyumbani kwa kina Zena ambako ni kama kwa kina Tia pia. Kwa kuwa wazazi wa Tia walishakuja kumkabidhi Tia rasmi hapo kwa wazazi wa Zena, basi Tia hakumuhitaji Zena kufika kwa mama Hiza. Akawa ameshazoeleka pale nyumbani. Urafiki wa wazazi uliokuwa unaelekea kwenye undugu kati ya familia hizo mbili ukawa umeshakomaa.

~~~~~~~~~~~~~~

Akiwa hajui lolote Nanaa alirudi hosteli siku inayofuata ya jumapili akiwa na tabasamu lake lote. Akawakuta Tia na Zena chumbani kwao. Akaona wote wamenuna. Nanaa akaanza kuwatizama kwa zamu na kucheka. “Mbona kama mmeninunia? Nimefanyaje tena!?” Nanaa aliwauliza huku akiwatizama kwa zamu. Ndipo Zena alipomjibu kwa jazba vile walivyokerwa na tabia yake yakutaka kumpora Terry wake. Wakashangaa Nanaa anacheka sana. Wakatulia kidogo.

“Unacheka nini sasa? Unafikiri mazuri?” Zena aliuliza akiwa amepunguza jazba. “Kumbe unamtaka Terry?” Nanaa akauliza huku akicheka akiwa amepuuzia kabisa. “Kumbe!” Zena akajibu kwa utulivu. “Aiii! Mimi sina hata shida naye. Wewe tafuta neno baya lolote la kunichafua kwa huyo Terry, halafu mwambie unampenda.” Wakaangaliana. “Kweli!?” Wote wakauliza kwa pamoja wasiamini. “Sasa mimi wa nini huyo Terry? Zac mwenyewe ananishinda! Terry nitamuweka wapi mimi na ratiba ngumu ya Zac? Ijumaa mpaka jumapili ananitaka kitandani mpaka nimkimbie, kwa kisingizio cha kumwambia naenda kwa kaka!” Tia na Zena wakajiweka sawa.

“Tena kukusaidia tu Zena, mimi niache kuja kwenye mikusanyiko yenu. Akishajiona mpo naye, lazima atakuchangamkia. Kwanza unalipa shoga yangu!” Roho ya Zena ikaanza kusuuzika, akaanza kucheka. “Sasa kwa nini hukuniambia tokea mwanzo? Mimi hata sikuwa na wazo! Kwanza mbona nilishamwambia Terry kuwa ninaye Zac?” “Niliwaambia.” “Basi mimi hata sikuwa na wazo. Labda akili yangu haikuwepo. Sasa mlipanga kuninunia mpaka lini!?” Nanaa aliuliza kwa kuwasuta. “Wala hatukuwa tumekununia.” “Mmmh! Aibu zenu wanawake.” Vicheko na mikakati yakumpata Terry ikaendelea jioni hiyo mpaka wakaamua kutoka na kwenda kujisomea.

Baada Ya Kusalitiwa Kwa Mara Ya Pili.

N

anaa alitoka pale Mabibo hosteli moyo na mwili ukiwa kama umekufa ganzi. Asielewe anatatizo gani. Kama uzuri, alisifiwa mpaka na wanawake wenzake. Kwa hakika Ndina haoni ndani. “Nilijua Zac ni wangu!” Nanaa aliendelea kuwaza kwa uchungu. Mapenzi aliyokuwa akionyeshwa na Zac, kwa hakika Nanaa alijua amefika. Sifa zilizokuwa zikimwagiwa kwake, kuanzia umbile na mambo wanayofanya pamoja, hakuwahi hata kuhisi kama Zac anaweza kugusa mwanamke mwingine. Faraja aliyokuwa akimpa! Mbele za watu alimkumbatia na kumbusu. Ni kama alikuwa akitangazia uma wote kuwa Nanaa ni wake. Anarudishaje sura yake kwa watu waliokuwa wakiyajua mapenzi yale? Anaishije tena bila penzi zito la Zac?

Zikiwa zimebaki siku chache za mitihani, Nanaa akijaribu kujifikiria hatima yake kimapenzi, alishindwa kusoma kabisa. Kila akiinamia vitabu, badala yakuona maandishi, macho yalimuona Zac na Ndina pale kitandani. Akaamua awekeze muda mwingi wakujisomea kwenye makundi ya wenzake wanao soma pamoja. Lakini pia haikusaidia. Mawazo yaligoma kuwepo pale. Yalisambaa kwenye jumbe za mapenzi alizokuwa akitumiwa na Zac. Simu za kutakiwa usiku mwema kila siku na maneno matamu kutoka kwa Zac. Si asubuhi si mchana, Zac aliwasiliana naye. Hata akiwa kwenye vipindi, aliweza kumtumia ujumbe Nanaa kumwambia kuwa anamfikiria yeye.

Leo anaishije bila hayo maisha matamu yaliyokuwa yamejaa faraja? Mitihani yakumaliza mwaka wa kwanza ilimalizika kwa shida mno. Matokeo yalitoka lakini yalikuwa mabaya sana kwa Nanaa. Alifeli masomo mawili nakutakiwa kuyarudia. Na yale masomo aliyokuwa amefaulu ni kama alikuwa kwenye mstari wa kufeli kabisa. Yote alipata alama ya “C”.

~~~~~~~~~~~~~~

Shule ambayo aliapa kuwa mkombozi wake ipo matatizoni sababu ya mapenzi.

Ndoa anazolilia kumtoa kwenye wegazi, hazionekani kutoa matokeo

mazuri kwa Nanaa.

Nini kitaendelea?

Usikose Muendelezo.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment