Jack alitoka kazini
akaambiwa yupo chumbani na ameomba asigongewe kwa muda. Akajua anaomba. Na yeye
akaliheshimu hilo akabaki sebuleni ameinama akimuhurumia mkewe. Akakaa hapo
kama dakika 20 mbeleni, ndipo akatoka. “Vipi?” “Safi tu. Upo sawa?” “Kabisa. Nipe
kama dakika 15 hivi, nipange timu yangu ndipo tutoke.” “Acha na mimi
nibadilishe nguo kabisa.” Wakajiandaa wakati wanatoka Jack akamwangalia.
“Umependeza sana, lakini
umechoka Brina wangu! Unakula kweli?” “Kesho ndio nitakula. Wala usijali. Nipo
tu sawa. Twende sisi walengwa tusije chelewa.” Wakatoka. “Nakuahidi sitarudia
tena Brina. Nimejifunza kwa uchungu sana.” “Nakuombea Jack.” Hivyo tu akajibu
na kunyamaza. Wakatulia mpaka kwao, Sabrina akiendelea kuombea hata kikao cha jioni
hiyo.
Wakati wanafika nyumbani
kwao gari la Jacinta na la Junior nayo yakawa yanaingia. Sabrina akashuka na
kuwasubiria. “Sasa sikiliza Sabrina, sio nilikwambia uwe unapania kila mahali!”
Sabrina alicheka mpaka akainama. “Kwani nimependeza sana!” “Sana shem. Upo
mzima lakini?” Junior akaongezeka. “Nipo mzima kabisa, shikamooni.” “Marahaba,
ila midomo imekukauka bwana!” “Nakunywa maji sijui kwa nini! Labda kwa kuwa
nailamba sana.” Sabrina akajibu akijilamba tena. Jack na yeye akasalimia. “Sasa
mzee Msindai leo sijamsikia vizuri.” Junior akanong’ona. “Kumbe na wewe umemgundua
eeh?” Jacinta akamuuliza kaka yake kwa kunong’ona. “Nimemsikia. Sasa naomba
tuingie ili saa 12:30 itukute tumekaa sebuleni kwake, hivi nilimtanguliza Joy
mapema, nikamwambia asichelewe, leo upepo sio mzuri sana.” Wakaingia wote
wanne.
Wote wakasalimia.
Walimkuta mzee Msindai, mkewe, Joy na Waili pia alishafika. “Jena bado
hajafika?” Akauliza Junior akikaa. “Ameniambia yupo kwenye foleni, lakini
anakuja.” Akajibu mama Msindai. “Pole na kazi, baba.” Junior akaendelea.
“Asante.” “Wakati tunamsubiria Jena, nikuletee chai, baba mzazi?” Jacinta
akamuuliza. Mzee Msindai akatulia akifikiria, wakajua kweli hayupo sawa. “Amekataa.
Dada amemuuliza mara mbili na kuamua kumletea kabisa kwenye sinia lake,
amekataa amemwambia arudishe. Ndio maana unaona wote tuna vinywaji yeye hana.”
Akajibu mama yao kama anayejitetea. “Wakati wote chai huwa haikudanganyi baba
yangu, mimi. Mimi naomba nikuletee.” Jacinta akasimama bila kusubiri jibu,
akaenda kuleta sinia lilelile lililokuwa limepangwa tayari sukari, kijiko chake,
chupa ya chai na kikombe anachokipenda kutumia mzee Msindai wakati wote wa chai.
“Mpaka hiki kikombe
kikiisha, utajisikia vizuri.” Akammiminia kwenye kikombe na kijiko kidogo
kimoja cha sukari kama kawaida ya baba yake. “Asante mama.” Mzee Msindai akashukuru.
“Junior, naomba mpigie Jena, mwambie watu wote tupo hapa tunamsubiria yeye.”
“Sawa, baba.” Junior akasimama na kutoka hapo kwa haraka. Baada ya muda mfupi
tu akarudi. “Naona anaingia getini.” Kimya. Jack akabaki ameinama.
Sabrina akamsugua
mgongoni na kucha, akamgeukia akiwa vilevile ameinama. “Nikuombee chai?” Sabrina
akamuuliza kwa kunong’ona. “Hapana. Asante. Wewe hutaki?” “Tena ipo nyingi tu
huko jikoni. Tumeandaa kabisa na chakula ili mle mkiondoka hapa mmeshiba ni
kwenda tu kulala.” “Asante mama. Shem nikuletee na wewe kikombe? Najua wifi
yangu yeye atataka glasi ya wine.” “Hapa nilikuwa najikaza tu. Maadamu umeamua
kutukarimu wifi yangu, glasi itahusika.” Jacinta akadakia yeye. “Basi na mimi
niombe glasi. Joy atakuwa dereva wangu leo.” Sabrina akasimama akicheka.
“Na wewe Joy?” “Kama
hujaelewa ndio nimeambiwa mimi nisinywe ili nimuendeshe.” Wote wakacheka.
“Sijasema hivyo bwana Joy!” “Wewe ushanichagua nikuendeshe, sasa mimi
nakunywaje?” “Labda kwa sababu ya majukumu yako ya kesho.” Kila mtu akazidi
kucheka. “Wewe huendi kazini kesho?” “Asante baba.” Joy akafanya wazidi
kucheka. “Mimi nakunywa glasi mbili tu, baba. Haziwezi kunishinda kuamka
asubuhi.” Angalau kidogo kukachangamka. Waili kimya.
Jena akaingia. “Samahani
baba. Nimekutana na foleni, nimechelewa.” “Kwa kuwa umechelewa kuanza safari ya
kuja hapa.” “Nilikuwa na mgonjwa baba yangu. Niliona ni bora…” “Ndio maana
nimesema hukuchelewa barabarani ila ulichelewa kutoka kazini, na wakati nilishakwambia
umuhimu wa hiki kikao! Junior mwenyewe imembidi aahirishe majukumu yake, leo
awepo nchini kwa ajili ya hili! Ninapotoa muda na kutaka wote muwepo si kwa sababu
nimebuni tu muda, Jena. Kila mmoja yupo hapa akiacha majukumu mazito
yanayotukabili kwa kuokoa fujo ulizomsaidia mdogo wako
kuziendeleza huko mtandaoni.” Watu wakajua huo usiku ushakuwa mchungu kwa hao
waliotajwa.
“Samahani baba yangu. Leo
sikutaka kukuudhi zaidi. Nilijua kwa hakika mimi ndio ningekuwa wa kwanza hapa.
Nisamehe baba.” Jena akajishusha na kusikika kama Jacinta kwa baba yake. “Sasa
na wewe Sabrina si unywe hiyo chai, itapoa! Yamoto itasaidia maziwa. Midomo
imekukauka sana. Kunywa. Au nimwambie dada akuletee yamaziwa?” Mpaka Jacinta
akakunja uso. “Nashukuru mama, asante. Naona hii ya rangi anayopenda baba
itanifaa na mimi. Nashukuru.” “Ongeza kula. Kazi yakunyonyesha dume sio kazi
ndogo!” Mama Msindai akaendeleza kuongea na Sabrina ili kumtuliza mumewe. “Na
naona ana kazi ya kula tu, mpaka mashavu yamekutana na shingo!” Sabrina akajibu
kidogo pakatulia.
“Ila umependeza! Umekua
kama kamodo!” Mpaka Jack akanyanyua uso na kumtizama Jena. Junior na Jacinta
wakabaki wamehamaki. Ni kama Sabrina na yeye hakutegemea akashindwa kujibu kwa
haraka. “Halafu aina hiyo ya nywele pia nzuri! Imekupendeza sana wifi yangu. Na
kwa kukuomba msamaha nimekuletea pochi nzuri hiyo! Najua lazima utaipenda tu. Sema
nimeiacha kwenye gari kwa haraka ya kuwahi hapa ndani.” “Mimi naomba kwa
heshima zote, baba, mruhusu huyu maneno mengi akalete hiyo pochi.”
“Jacinta unanianza!” “Wewe usitake ugomvi na mimi, kalete pochi.” “Sasa
unafikiri nadanganya?” “Wewe ungeacha maneno mengiiiii! Muombe baba, ukalete
hiyo pochi kama kweli ipo.” Junior naye akaongeza kwa Jacinta. Akamwangalia
baba yake. “Naomba ufanye haraka Jena.” Jena akasimama kwa haraka na kutoka
nje.
“Hakika ningejua leo, ningekuja
na mwamvuli wangu.” Mpaka Joy akacheka. “Kwamba mvua itanyesha, wifi?” Joy
akauliza akicheka. “Tena ile ya radi kabisa!” Junior akazidi kucheka. Kweli
Jena akarudi na mifuko mizuri tu ameshika mkononi. “Hii hapa pochi ya wifi
yangu, Sabrina. Na vibanio vya anti zangu wale mapacha wa Msindai. Keiline na
Jeiline.” “Baba ataniazima mwamvuli wake.” Wakazidi kucheka. “Na sijamaliza. Hivi
hapa ni vya mrembo Claire. Na huu mfuko huu pia ni wa....” Akachungulia ndani.
“Eehee! Hizi nguo za ndani za dada Claire na hizi nyingi za mapacha wetu.
Jeiline na Keiline.” “Asante Jena mdogo wangu.” Junior akashukuru, Joy akabaki
ametoa macho.
“Leo mpaka nimeitwa mdogo
wangu!” “Uwe unaleta hivi zawadi mara kwa mara dhambi zako zinakuwa
zinasamehewa.” Watu wote wakacheka. “Mimi nimeshasema nimebadilika. Halafu haka
kamfuko kadogo haka, ka mamilioni ya pesa, ni kababa mzazi.” Mzee Msindai
akacheka na kutingisha kichwa. “Hapa mimi leo siondoki baba. Nalala hapahapa.
Kesho navaa nguo za mama kwenda kazini.” Jacinta akafanya wakazidi kucheka.
“Wifi unaogopa hata kutoka?” “Hakika leo ni mvua ya mawe!”
“Sijali maneno yako
Jacinta. Hii saa ya baba. Baba yangu amenihangaikia sana, mpaka nimepata ile
nafasi!” Mpaka mama Msindai akasimama na kushangilia. “Kweli Jena?” “Waziri wa
Afya mwenyewe amenipigia simu, wameniambia katika wanawake tuliofanya usahili,
mimi peke yangu Reseach yangu imepita. Ila kwa ajili ya kushika hiyo
nafasi, nahitajika kwenda kusoma kwa miezi 6 tu kama kujiweka sawa, nikirudi ndio
nakabidhiwa rasmi kitengo cha mambo ya moyo kwa upande wa watoto.” “Sasa
utakwenda!?” “Sina kinachonizuia mama yangu. Kwa nini nisiende tu? Nitakwenda.
Nimefurahi, nikasema nitamwambia baba nikija sio kwa simu, maana ndiye
aliyehangaika na mimi kwenye kukusanya Data, kupitia Reseach Papers
zangu, akizisahihisha bila kuchoka. Kila niliporekebisha makosa na kumrudishia
asome tena na tena wala hajawahi kunikatalia, mpaka akaridhika. Halafu bado
akanifanyia mazoezi kitu cha kuzungumza nao hao walionifanyia usahili ili
kuwavutia na wanichague mimi. Akawa akinifanyia mazoezi mpaka nikaweza. Asante
baba.” “Hongera sana.” Mzee Msindai akampongeza na kupokea hiyo zawadi ya saa.
“Na nikirudi tu nchini tunafungua kitengo chetu
cha mambo ya moyo kwa watoto pale kwenye hospitali ya baba!” “Mama huyu kapata
mukari mpaka anapangia mahesabu pesa ya baba bila kumuuliza mwenyewe kama yupo
tayari na kitengo cha mambo ya moyo!” “Aliniambia baba mwenyewe wakati
nilipoenda kusomea mambo ya moyo. Aliniambia nikifanya vizuri huko chuoni,
anaweza kuongeza kitengo cha mambo ya moyo pale hospitalini kwake, halafu
akaniachia mimi nikiendeshe. Ila niliporudi nchini ndio nikawa na mambo mengi.
Ila sasahivi nishakuwa mtoto mzuri. Sasahivi sifanyi tena mambo yakumuudhi
bab..” “Na kila mtu.” Wote watatu wakadakia kwa pamoja.
“Wewe unakera kila
mtu Jena.” “Jacinta ujue wewe umenikazania wewe! Unataka kunianza! Baba
unamuona Jacinta?” “Sasa nyinyi wawili msianze kuchafua hali ya hewa hapa.” Mama
Msindai akawawahi. “Ni Jacinta huyo! Anataka kunikorofisha bila sababu! Mtu
nishasema nimebadilika lakini…” “Hata ukipewa kitengo na baba pia, ubakie
hivyohovyo. Usirudi kule kubaya. Maana sio uwe mwema sasahivi ili kumfanya baba
akuamini, halafu ukishakabidhiwa kitengo huko kwenye hospitali ya Msindai…”
Jena akaanza kulia. “Kwa nini hamumpi mwenzenu nafasi jamani!? Eti Junior?”
“Mimi namtahadharisha mama.” “Hapana Junior. Mtieni moyo. Sio mumzodoe. Amejirudi
kwa kila mtu, bado mnashindwa kutambua jamani! Si sawa.” “Nimekosa mama.
Samahani.” Junior akajirudi kwa haraka.
“Jena mdogo wangu, naomba
msamaha.” “Wewe hunipendi Junior, tokea zamani
unampendelea Jacinta. Mnanitenga kwenye kila kitu! Kila nikifanya jambo zuri
wewe huoni, unaona mambo ya Jacinta tu, tokea zamani sisi ni wadogo. Mimi sijui
niliwafanyia nini!” Jena akaongea kwa uchungu akilalamika na kulia. “Kila jambo unamsifia Jacinta, lakini sio mimi! Halafu
kwenye kila jambo la Jacinta unakuwepo lakini mambo yangu mimi huwa unatoa
udhuru.” Akendelea kulalamika. “Kila mtu
alikuja kwenye mahafali yangu ya kuhitimu mambo ya moyo, lakini wewe hukuja
Junior. Na nilimwambia mama kabisa, ingekuwa ni Jacinta, ungeahirisha kila kitu
kuhakikisha unahudhuria.” Akatoa mifano mingi akisema Junior
anavyompendelea Jacinta kuliko yeye.
“Kila siku
unaonekana unatoka na Jacinta, mimi hamniiti! Mnanitenga kama mimi sio ndugu
yenu! Mnanifanya nakuwa peke yangu naishia kuwa na mama tu! Kila siku, kila
mahali unakuwa na Jacinta sio mimi.” Jena akaendelea kulia akilalamika. Jacinta naye
akanyamaza kimya akiendelea kunywa. “Basi Jena, mdogo wangu. Kwanza nashukuru
kuniambia. Naomba msamaha, na ninakuahidi nitaongeza umakini kwako. Ila ujue Jacinta
huwa sitoki naye. Jacinta anatoka na mke wangu, halafu anaishia kunipigia
simu…” “Aje alipe.” Akamalizia Joy, wote wakacheka.
“Kweli baba. Yaani
ukitoka na Jacinta ujue umetoka na Junior. Wine zikishamuingia tu kichwani,
simu kwa kaka yake.” “Na samaki wa kuchoma kwa baba yake.” Mama Msindai
akaongeza na kufanya wazidi kucheka. “Samaki wa kuchoma na ndizi, hivyo
vinaagizwa akishalewa. Sasa Junior huwa anamwambia, baba sasahivi atakuwa
ameshalala. Hapo huna utakachomwambia wifi yangu. Ataagiza viletwe, na maagizo
yake ni yaleyale, kamkabidhi mlinzi getini, akagonge usiku huuhuu dirishani kwa
mzee Msindai, amwambie kitoweo kutoka kwa mama mzazi.” “Basi hayo
maagizo hata saa sita usiku utayasikia dirishani. ‘Kitoweo kutoka kwa mama
mzazi.’ Basi najua yupo baa tu.” Akamalizia mama Msindai wakazidi kucheka.
“Mimi naomba Jena mdogo
wangu, unisamehe. Si nimesema nitaongeza umakini?” “Ndiyo.” Jena akajibu.
“Basi tunaanza na kwenda kukupongeza kwa kupata kitengo. Unachagua popote
unapotaka, safari hii Jacinta atalipia.” Kidogo kukaanza kutulia. “Na mimi
naomba nikushukuru Jena. Binafsi nimechukulia ni jambo la kipekee na
nimefurahia sana kwa zawadi yangu, na asante kwa zawadi za kina Jeiline na
Keiline pia. Asante sana.” Sabrina akashukuru. “Karibu.” Jena akaitika
akisikika ametulia.
~~~~~~~~~~~~~~
“Haya, naomba tuokoe muda,
tumruhusu Waili aendelee. Kwanza tumeshatumia muda wake mwingi sana.” “Hakuna
shida kabisa mzee wangu. Maana hiki kilichoendelea hapa ni muhimu sana. Kuwa
ukurasa mmoja kwanza nyinyi kama familia. Zaidi kwa mke wa Jackson.” Sabrina
akakunja uso kidogo. “Mnaweza msitambue umuhimu wake kesho, lakini kwa hiki
kilichotokea kwa mumewe, uwepo wake yeye kama mke pale mahakamani, unanguvu
sana.” Waili akaendelea.
“Kama mtakumbuka mwaka
1998, ile skendo aliyoipata aliyekuwa Raisi wa wakati ule nchini Marekani.” “Raisi
Bill Clicton na yule mwanadada Monica Lewinsky?” Akadakia kwa haraka sana
Junior na kuongeza. “Mimi nakumbuka na mpaka vile mkewe alivyosimama naye.”
“Sawasawa Kiongozi. Na ile ilipunguza sana makali ya lile kosa lake. Jackson
atakapotokea kesho na mkewe ambaye walijaribu kumchafua na kuwachonganisha
mtandaoni, ile kuwaona tu pamoja wakiwa kwenye hiyo tu hali ninayowaona nayo hapa
sasahivi. Hata bila kuzungumza kitu juu yao, itasaidia sana. Maana sehemu yenye
upendo huhitaji kupatetea sana. Watu watawaona tu, na kuwadhoofisha walio
kinyume nanyi. Nianze na Dokta Jena Msindai.” Akamtambua kwa heshima.
“Kama tulivyozungumza na
yeye mwenyewe nataka na sisi hili litukae kichwani zaidi Jackson, kuwa hakuwahi
kuandika kitu mtandaoni, akaunti zake zote walizi hack. Kwa hiyo
huyo mtu aliyekuibia akaunti zako ndiye aliye kuwa akizitumia huko mtandaoni
mpaka ulipojua ndipo ukazifunga zote. Sijui kama tupo pamoja?” “Nimeelewa. Hata
hivyo mimi sikuwa mtumiaji sana wa akaunti zangu. Kwa hiyo nimeelewa.” “Kuna
swali?” “Ndiyo.” Jack akadakia na kufanya wote wamgeukie yeye.
“Karibu.” “Huyu Jena alimfuata Phina. Sijui
walikutana wapi! Sijui nani waliwaona pamoja!” Jack akazidi kuweka hali ya
wasiwasi akionekana wazi binafsi ameingiwa hofu ya kesho yake huko mahakamani.
“Jena na Phina hawajawahi
kukutana. Unakumbuka Jena?” “Nakumbuka.” Jena akajibu. “Kivipi tena!?”
“Jackson, naomba zingatia upande wako tafadhali. Ya Jena wewe hufahamu kama
hivi unavyoniuliza, tafadhali ibakie hivyo.” “Ikitokea wananiuliza?” Jack
akamuuliza Waili kwa mshangao mkubwa kama anayezungumza asichojua! “Nikuulize
swali mheshimiwa Msindai?” “Tafadhali niite Jackson.” Jack akawa ameshakasirika.
“Samahani.” Sabrina
akamkatisha. “Naomba utulie Jack. Nafikiri huyu wakili yupo hapa kukusaidia, na
nahisi kama sijakosea anataka kukupunguzia mzigo. Naomba usikasirike.”
“Nafikiri mkeo amenielewa kwa haraka sana.” “Ameanza na mimi muda mrefu sana,
wewe hujui tu Sabrina. Imekua kama ananiadhibu! Maswali yake kwangu ni ya
kunihukumu, kuliko kunisaidia!” Jack akazidi kupandisha hasira akiendelea
kulalamika.
“Ameharibu siku yangu
nzima kwa kunihoji kama yeye ndiye anayemtetea Phina na sio mimi! Na mimi
nimechoka jamani! Ananihoji kama mimi ndio mtuhumiwa wakati anatakiwa kuwa
upande wangu!” “Baba, naomba nizungumze na Jack kwa muda mfupi tu hapo nje. Hatutachelewa.”
Ikabidi Sabrina kuingilia kati. “Sawa.” Ile mzee Msindai anamalizia kukubali,
Jack alishafika mlangoni. Sabrina akanyanyuka na kumfuata. Ukimya ukazuka hapo
ndani
~~~~~~~~~~~~~~
Usikose Sehemu Ya Mwisho Ya
Simulizi Hii Kujua Hatima Ya Hukumu Ya Kila Mtu Na Makosa Yake.
0 Comments:
Post a Comment