Nyumbani Ni Nyumbani.
Chali alirudi nyumbani
moja kwa moja akataka kuzungumza na Sabrina. “Mwambie azungumzie dirishani,
mimi nanyonyesha huku chumbani kwa watoto na mtoto ndio ameanza tu, siwezi
kumkatisha.” Sabrina akamtuma Phina. Baada ya muda akamsikia Chali dirishani.
“Mama Msindai upo?” “Nakusikiliza Chali. Kwema?” Akamsikia akicheka ila si
kicheko cha furaha. “Nini tena!?” “Bwana safari hii mimi nimepokelewa mpaka
nimekaribishwa ndani!” “Haiwezekani!” “Na chai nimekunywa.” Sabrina akacheka.
“Nani kakukaribisha?” “Alianza mzee. Nikahofia mama asije akatoka na
kunikimbiza. Lakini yeye ndiye aliyeniletea chai. Ila hali sio nzuri mama Msindai. Wazazi wanaonekana walihitaji kweli
msaada.” Sabrina akatulia.
“Kuna wadogo zako wapo
shule, nafikiri ndio nilikuwa nikitumwa kwako na baba, hana ada.” Sabrina
akanyamaza. “Wanahitaji pesa mbali na vyakula. Na sidhani hata kama wana umeme
pale. Kwa ufupi hali mbaya mpaka ikabidi nimuachie mzee pesa kidogo wakati
akinisindikiza.” Sabrina akaumia sana. “Ulimpa kiasi gani?” “Naomba nisikwambie,
wale ni kama wazazi wangu pia. Lakini jua wameishiwa kabisa. Mama anasema
ilibidi kuokoteza vifuu vya nazi atumie kama mkaa ili kunipikia hiyo chai. Sasa
unajua mtu mzima mpaka aongee hivyo, inamaana hali si nzuri.” “Nashukuru
Chali.” “Na cha mwisho, nafikiri kwa hali ilivyo, hata ukiwapigia au ukienda,
nadhani safari hii utapokelewa tu.” “Naona nianze kwa kupiga.” Chali akaondoka na kumuacha Sabrina
akifikiria familia yake.
Akajua wamepoteza msaada
kutoka kwa Sabina na huyo Tino. Kaka yake tokea zamani hakuwa mtu wa kusaidia
nyumbani. Akajua kwa hakika hali ya kwao sio nzuri. “Sabina atatolewa lini?”
Hilo likabaki swalli aliloogopa kuliuliza kwa sauti kwa kuwa bado hakujua akija
kutolewa, atafanya nini cha kuvuruga zaidi! Akabaki akiwaza huku akinyonyesha
mwanae.
Aliyetangulia,
Katangulia tu.
I |
likuwa bado ni mapema tu wakati Ibra na Phina
wapo sehemu wakila na kunywa pamoja na wapambe wao. Ibra alisikika akizungumza
kwa sauti ya juu iliyojaa ushindi. Akawasogelea mtu aliyetumwa. “Ibrahimu Kondo?”
“Nani anauliza?” Akauliza Ibra kwa kiburi. “Mjumbe. Nimepewa hii barua yako
nikufikishie, inakuhusu.” Akabaki ameishika, Ibra hajapokea. Akaiweka mbele yake
kwenye meza iliyokuwa na vinywaji. “Saphina Shija?” Phina akamwangalia. “Na
wewe huu ni ujumbe wako. Ni muhimu kusoma maana..” “Kama unatoka kwa kina
Msindai waambie hatutaki misamaha ya vificho. Sisi tumetoka hadharani,
wasijifiche, wajibu hadharani kwa heshima ya jamii nzima. Waache dharau.”
Akaongea Ibra kwa ujasiri na kiburi.
“Si dhani kama ni jambo
baya kupokea ujumbe. Nafikiri sauti zenu zimefika mbali, ndio wanataka
kuwasikiliza. Bado nashauri msikatae huo ujumbe.” Wakaanza kushangilia, yule
mjumbe akaondoka akaacha wakipongezana. Moja kwa moja wao wakajua wamewafikisha
kina Msindai magotini, maana bado Phina alikuwa akipokea pole huko mtandaoni,
na kujibu maswali.
Wakamtia morari Ibra
mpaka akafungua barua yake. Gafla wakamuona amebadilika sura mara aliposoma tu
kichwa cha habari kwenye waraka uliokuwa ndani ya bahasha. Ilikuwa ni shitaka
kutoka kwa Jackson Msindai yeye kama Jackson na Naibu Waziri. Alipewa siku 4,
ikiwepo hiyo siku ya jumatatu, ajiandae na ushahidi wake wote ili kufika
mahakamani siku ya ijumaa, kujibu shitaka lake la kumchafua mtandaoni kwa
habari za uongo yeye kama Jackson Msindai, kisha Naibu Waziri. Na shitaka
jingine ni kumvamia mkewe na watoto nyumbani kwake, na kufanya fujo
mpaka kutolewa na askari. Ibra akatulia na kubadilika sura kabisa. “Nini!?” Wapambe
zake wakamuuliza maana ni kama aligeuka kuwa shujaa kwenye jamii gafla.
Akijisifu kuwa hababaishwi na cheo cha mtu ila haki tu.
“Phina wewe yako inasema
nini?” Bado Phina alikuwa akisoma yake. “Nilikwambia Ibra, kadiri yule
mwanasheria anavyochelewa ndivyo anavyotuweka sisi pabaya! Ona sasahivi sisi
ndio tutasimama sehemu ya watuhumiwa na si yeye Jack!” Phina akaongea
akilalamika macho kwenye waraka wake. “Acha nimpigie. Usipaniki.” Ibra akatoa
simu na kuanza kumpigia simu mwanasheria ambaye walishazungumza naye juu ya
hilo tokea mwanzo hata Phina hajambadilikia na kurudi upande wa Jack. Walimfahamu
kwa jina lake la kwanza, Lioni. Mara ya kwanza simu ya Lioni iliita kwa muda
mrefu bila kupokelewa. Alipopiga mara ya pili ikaita mara mbili na kukatwa.
Akasimama kabisa na
kutoka pale katikati ya kundi ili akampigie simu nje, sehemu tulivu. Hilo zoezi
likaendelea kwa mara tatu mbeleni. Simu inaita kidogo na kukatwa. Phina
akamfuata. Akamkuta bado akipiga simu. Alipojaribu kupiga tena, ile simu ikawa
haipatikaniki tena. Haipo hewani! Ibra akashangaa sana. “Mbona simuelewi huyu
Lioni?” “Labda yupo na mteja.” Phina akajibu kwa wasiwasi. Wakaamua kwenda
kumfuata ofisini kwake. Wakaondoka hapo baa bila hata yakurudi ndani kuaga
wenzao.
Aliyeshika
Mpini.
Chakushangaza wakamkuta Lioni
amekaa ofisini kwake, hana hata mteja. Tena alimwambia sekretari aliyewapokea
mapokezi awaruhusu waingie ofisini kwake moja kwa moja. “Vipi, mbona hupokei
simu zetu!?” “Kaeni na fungeni mlango.” Phina na Ibra wakakaa wakiwa na
mshangao usoni.
“Ni nini kinaendelea
Lioni!?” Ibra akaendelea kuhoji. “Mimi nitakwenda moja kwa moja kwenye pointi
wala sitawapotezea muda wenu kwa kuwa sikutaka tuzungumze kwenye simu. Haya
mlipaswa kuyasikia tukiwa tunatizamana kama hivi. Kwanza wekeni simu zenu hapa
juu ya meza nihakikishe hamnirikodi.” “Acha kututisha bwana!” “Basi ondokeni.”
“Acha masihara!” “Hakika siwatanii. Si mlisema huyu Phina alimpiga picha
Jackson Msindai akiwa amelala?” Wote kimya. “Kwa hiyo mnataka mnichezee akili na
mimi mnirikodi, halafu mkanifanyie kama mnachomfanyia Jackson Msindai!” Wote
wakashituka na kushangaa jinsi anavyowabadilikia.
“Wewe tulikuja kwako
tukitaka kukupa kazi ndio maana tulikwambia mambo ya ndani, leo unayatumia
kinyume chetu!?” “Acha masihara kabisa Ibra. Kama huyu Phina aliweza kumfanyia
mwanaume aliyekuwa naye kwenye mahusiano ya muda mrefu, mpaka akaja kumtafutia
kazi, wamelala naye akijua ni mume wa mtu, wakaambiana mambo ya ndani
kwa kiasi hicho, kwamba kulikuwa na mahusiano mazito kati yao, lakini bado
ameweza kumfanyia anayomfanyia huko mtandaoni, atashindwa vipi
kwangu mimi ambaye hata hanifahamu!?” Hilo likamuuma sana Phina, akanywea na
kuinama kabisa. Lioni akaendelea akiwakazia macho kama asiyetaka utani nao.
“Ninachotaka kuwaambia ni cha undani tena kama
kuwasaidia tu nyinyi wawili. Siwaamini ndio maana sitaki kuja kubadilikiwa
baadaye. Mkaja kuniangamiza mimi. Maana kuna waliomea kwenye hii nchi mpaka
kuota mizizi kama mti wa muarobaini. Kwamba mizizi yao inaogopewa kila mahali,
na ikipita chini ya nyumba yako, haitoi tu nyufa, inapasua
kuta. Sasa uchaguzi ni wenu, mnaweka simu au mnatoka?” Ikabidi Phina na Ibra kuweka
simu zao mezani. Lioni akaziangalia kabisa kama anayezikagua, akajiridhisha
zimezimwa.
“Nianze na Phina. Mpaka
sasahivi unao ushahidi wowote ule kwa shutuma zako unazoziendeleza mtandaoni?”
“Mpaka sasa ni kama nimekwama ndio maana tumekutafuta, maana nimetoka kupokea barua
ya mashitaka niliyopewa inatoka kwa…” “Wakili wa familia ya Msindai INAKUSHITAKI, Moja, Upande wa
Jackson Msindai anakushitaki wewe kama Saphina Shija ukiwa na Ibrahimu,
ulikwenda nyumbani kwake na kumfanyia fujo mkewe mpaka mkatolewa na askari.” Lioni
akamalizia shitaka la kwanza vizuri kana kwamba yeye ndiye aliyeandika shitaka
hilo na kuwashangaza wote wawili. “UMEJUAJE!?” Wote wakauliza kwa pamoja.
“Subirini kwanza. Hiyo ni
kwa Jackson tu, na si bado Phina unayo mashitaka mengine kama ya kusema
uongo mtandaoni na kumchafua mkewe, watoto na yeye mwenyewe Jackson
Msindai kama mume na baba wa familia?” Phina kimya. “Si pia Phina umeshitakiwa
kwa kutumia nafasi uliyopewa na serikali, kutoa siri za viongozi wa nchi, uliokuwa
umepewa dhamana na Wizara uliyokuwa ukifanyia kazi, ili kuwahudumia kikazi, ila
badala yake unatumia siri za ndani za Wizara ukiwa umejua wapi walikuwepo
kikazi, nini walifanya siku nzima, umetumia hizo taarifa vibaya, kumchafua
bwana Msindai kama Naibu Waziri? Ukaingia chumbani kwake, na kupiga picha
unazotangaza wewe mwenyewe mtandaoni kuwa ulimpiga na zimeibiwa. Unashitakiwa
kwa kutumia wadhifa wako vibaya, kuchafua ofisi zao na kutoa mpaka siri
za ndani na mipango ya serikali? Mpaka hapo nimedanganya?” “Lakini..” “Subiri
Phina. Kwenye hiyo barua hujapata shitaka pia kutoka kwa Jena Msindai AKIKUSHITAKI kwa kumsingizia
mtandaoni na kumfuata kazini kumfanyia fujo?” “Haiwezekani! Kumbe ndio
mashitaka ya Phina hayo!?” Ibra akashangaa sana.
“Kwani Phina hajakwambia?”
“Hapana!” Phina akabaki kimya. “Mbali ya hayo ya Jackson Msindai, Jena naye anamshitaki
kwa kumtupia shutuma za uongo huko mitandaoni.” “Lakini ninao ushahidi wa watu
ambao pia waliona likes zake kwenye comments zangu na comment
yake pia.” Phina akajaribu kujitetea. “Kumbe huna taarifa? Jena anasema akaunti zake zote walizi hack.
Kwamba kuna mtu alikuwa akitumia akaunti zake zote mitandaoni ndio maana
alipogundua, amezifunga zote.” “Kuna mchezo wanatuchezea tu, si bure.” “Ibra,
umejiingiza kwenye vita mbaya sana mpaka nakuhurumia.” “Hakuna
watakachonifanya. Hii ni nchi yenye uhuru wa kuongea.” “Umeongea pabaya, kaka.
Mimi mwenyewe nimeosha mikono yangu!” “Usiniambie kama na wewe Lioni wamesha
kununua!” Ibra akauliza kwa kuumia.
“Nikuulize swali Ibra? Na
ufikirie kwa makini kabla hujajibu.” “Juu ya nini!?” “Na Phina unaruhusiwa kumsaidia
kujibu.” Wote wakaongeza umakini. “Mlishasikia vita yeyote. Mtu yeyote hapa
nchini, au Raisi yeyote aliyekwisha kuwepo madarakani, mkubwa wa polisi au
yeyote yule hata mwanasiasa mashuhuri, akigombana hadharani na mtu wa
Usalama wa Taifa?” Pakazuka ukimya. “Kwa ukimya huo, mjue nyinyi wawili
mmekanyaga kwenye moto.” Lioni akajiweka sawa.
“Ingekuwa vinginevyo
ningewashauri mkimbie, lakini hamna pakukimbilia. Na kwa taarifa yenu tu,
hakuna atakayekubali kuwasimamia kesi yenu, kwa sababu hakuna aliye tayari
kuhama hapa mjini. Kila mtu anataka kulisha familia yake sio kuanzisha vita na
watu wa Usalama wa Taifa. Kama hamniamini, tokeni hapa, katafuteni wakili
mwingine, kampuni ingine, ila si kwenye hili jengo. Hili jengo letu wote,
hakuna atakayechukua kazi yenu hata kwa mamilioni ya pesa. Haya jamani,
kwaherini.” Kimya.
“Tafadhalini naomba niendelee
na majukumu yangu.” “Umejishusha sana thamani, Lioni! Sikujua kama na wewe
unaweza kununulika kirahisi kwa kiasi hichi! Jamii nzima ipo nyuma ya Phina
ikimuhurumia!” “Sawa Mkuu. Lakini mwenye macho huwa haambiwi tazama. Dada
Phina, kila la kheri.” Akasimama kabisa na kuwafungulia mlango, akiwaashiria
watoke. “Hivi watu kama nyinyi mkiwa mnapokea rushwa, sisi wanyonge tunao tafuta
haki zetu tuende wapi?” “Umejiingiza kwenye vita isiyokuhusu Ibra. Wewe si mnyonge,
ila ni shabiki niliyekutahadharisha kutokea mwanzo kabisa uliposema unazo
picha za Jackson Msindai, amelala na Phina, na amempa mimba ila anamkimbia.
Nilikuomba ushahidi, ukashindwa kutoa ushahidi ila maneno tupu.” “Si kwa kuwa
wameiba!” “Unao ushahidi wa hilo unalotaka kulianzisha tena?”
Kabla hajajibu akamuongezea swali jingine. “Basi hata kama ushahidi huna, hiyo kesi
ya kuwa uliibiwa, uliiandikisha polisi?” Kimya.
“Jamani mnanipotezea
muda. Naombeni mnipishe nifanye majukumu yangu. Phina, nashauri ujiandae haswa.
Shutuma ulizotupa huko mitandaoni zimefika kwenye masikio hatari sana. Na sijui
mlipata wapi hiyo akili ya kusambaza mambo hadharani! Mmejitega wenyewe! Ndio
mnatakiwa ushahidi wa kila mlilosema. Mbaya sana, HAMNA!” “Ibra alitaka nisikike.”
“Ndio umesikika, unapewa nafasi ukasikilizwe vizuri. Naomba mnipishe.” Phina
akatoka akamuacha Ibra akimwangalia Lioni. Mwishoe Lioni akaamua arudi kukaa, akainamia
mafaili yake akaendelea na kazi kana kwamba Ibra hayupo pale.
~~~~~~~~~~~~~~
Phina na Ibra wakaanza
kuzunguka kutafuta wakili wakuwawakilisha hiyo siku ya ijumaa. Kila walipoenda
jibu kubwa walilopata ni kwa wakati huo wanamajukumu mengi, hawataweza kuchukua
kazi mpya kwa haraka. Ibra akawa mtu wa kumtia moyo Phina kwamba asiogope,
hakuna watakachowafanya. “Uzuri kesi ipo mahakamani. Hata hakimu akiwa mla
rushwa kiasi gani, kesi yetu imefuatiliwa sana mtandaoni. Jamii nzima ipo
upande wako Phina, ikikuunga mkono na kukuhurumia kwa unyama uliofanyiwa. Ni
kuhamasisha tu watu mtandaoni kuja kwa wingi mahakamani ili hata haki isipotendeka,
watutetee.” Hilo likamtia moyo Phina.
Wakarudi nyumbani kwa
Phina wakiwa wamechoka, wakaanza kuandika tena mtandaoni kuwa mawakili wote wa
jijini wamekula rushwa, hawataki kuwatetea wao wanao gandamizwa. Wakatoa
malalamishi yao wasijue wanazidi kuharibu na kuchafua ofisi za wanasheria pia.
Watu wakazidi kuunga mkono wakitoa mifano yao na wao jinsi sheria
inavyopendelea wenye uwezo na mengine mengi kila mtu akitoa lililokwisha
kuwapata na kutopewa haki zao.
~~~~~~~~~~~~~~
Siku zikazidi kwenda kila
mtu akijipanga kivyake. Sabrina akawa na kazi ya kusoma mtandaoni na kuendelea
kufunga na kumlilia Mungu wake huku Jack akimshirikisha kila kitu
kinachoendelea kwa upande wa Msindai. Yeye kama Sabrina akawa na maombi juu ya
mumewe na kesi inayomkabili dhidi ya Phina, na mambo ya familia yake yaliyokuwa
yamejikoroga na kujikanganya mpaka akawa hajui hata mwisho wao ni upi. Sabina
yupo jela. Kama asingekuwepo jela, inamaana angekuwa uraiani akisaidia
kumshinda yeye. Mama yake amekamatwa ndani ya nyumba ya mganga wa kinyeji
akitaka mumewe afe. Akabaki akilia mbele za Mungu hajui aseme nini juu ya
familia yake. Alishamtumia baba yake pesa siku ileile ya jumatatu Chali
aliporudi kutoka kwao na kueleza shida ya nyumbani kwao.
Kimeumana!
Kwa
Phina&Ibra.
S |
iku ya jumatano Phina na Ibra nao ikabidi kurudi
Ustawi wa Jamii kushitaki na kuomba msaada wa mtu wa kuwawakilisha. Huko ndiko
waligombana mpaka wakaondoka bila kuagana. Kwanza walimshangaa sana Phina.
“Wewe si ulirudi hapa na kukanusha mambo yaleyale ambayo unasambaza huko
mtandaoni!?” “Jack ndiye aliyenituma.” “Wewe binti unacheza mchezo hatari sana.
Kwa nini unachanganya hawa wanaume kwa kiasi hiki!? Ulikuja na Ibra, mkamsema
vibaya sana Naibu Waziri Msindai ambaye inasemekana alikuwa rafiki wa karibu
sana na huyu Ibra.” “Ni enzi hizo.” “Sawa. Lakini mwenzio huyu alirudi tena
hapa kukanusha yote mliyolalamika na kumshitaki Mheshimiwa Msindai! Tena yeye
mwenyewe alituambia hata picha mlizotuonyesha ni za kutengeneza tu! Na
Mheshimiwa Msindai ni mpinzani wako wa tokea zamani, hajui ni kwa nini wewe
unamchukia kwa kiasi hicho!”
“Haiwezekani Phina!” “Ni
vile nilivyokwambia Jack alinidanganya.” Phina akajaribu kujitetea lakini wazi
alionekana kupatikanika. “Ndio uje unichafue kwa kiasi hicho!?” “Tena si hivyo
tu maana na mimi nilikuwepo hapa.” Akadakia mwingine. Wakaeleza yote
aliyokanusha Phina, tena kwa undani zaidi kama waliokuwa wakitaka
kuwafarakanisha. “Halafu leo nashangaa mmekimbilia mtandaoni, hakika wewe binti
ni mwaribifu na kina Msindai hawatakuacha salama. Leo unazungumza hiki, kesho
unakuja kufuta! Umeanika mambo ya undani kama sio mwanamke wewe!” Akaongea kwa
kuumia mama mtumzima kidogo waliyemkuta hapo hata siku ya kwanza walipokwenda
kushitaki. “Ndio kazi zao hawa. Ndoa hawataki, wanasubiri kutuibia waume zetu
na kujaa nao mtaani! Sisi tunakazi ya kuwalisha na kuwatumikia, wao
wanakimbilia suruali tulizofua sisi. Wewe unajifananisha na mwanamke
aliyefikishwa kanisani wewe! Ona ulipo na alipo mwenye mume!” Phina akaondoka
bila ya kuongeza neno, na Ibra hivyohivyo, ila akiwa amekasirika vibaya sana.
Kwa Kina
Msindai.
Siku ya alhamisi mzee
Msindai akataka wakutane wote na huyo wakili. Kikao nyumbani kwa mama Msindai.
Sabrina alikuwa amefunga tokea siku ya jumatatu. Ilikuwa asubuhi mida ya saa
tatu akaona simu ya mzee Msindai ikiingia. Alishituka maana hakuwa amemsikia
huyo mzee tokea siku alipotoka kumshika mama yake uchawi. Akapokea kwa haraka. “Shikamoo baba.” “Marahaba mama. Wajukuu wote hawajambo?”
“Wote wazima.” Akajibu na kutulia. “Kesho ni
siku ya mahakamani, nafikiri umeshaambiwa na Jackson.” “Ndiyo baba.” “Sasa simu
hii nimekupigia kukuomba rasmi kama unaweza kuongozana naye.” “Huko
mahakamani!?” Sabrina akauliza kwa kushangaa na mshituko mkubwa mpaka
mzee Msindai akasikia.
“Ndiyo.” Akajibu mzee Msindai kwa
kifupi na kumpa muda wakujibu. “Mashabiki wote wa Phina
wale waliokuwa wakinitukana mtandaoni watakuwepo kesho. Wanasema watakuja
kumuunga mkono Phina. Halafu…” Sabrina akasita akisikika amepaniki.
Akajikuta machozi yakimtoka. Hakutaka kwenda kuonekana huko mahakamani mbele ya
mashabiki wa Phina. Mzee Msindai kimya
upande wa pili. “Unafikiri ni muhimu na mimi kuwepo
huko?” Akauliza na kukumbuka hapohapo kuwa anazungumza na mzee Msindai
aliyemuomba amsamehe mumewe na amsaidie. Akajirudi kwa haraka. “Nitakuwepo baba.” Na machozi akajifuta. “Nashukuru sana. Sasa jioni tunatakiwa kukutana na wakili
wake huyo Jackson. Nimemuomba tukutane nyumbani. Na Junior nimemuomba awahi
kurudi nchini ili kesho na yeye awepo mahakamani na Jackson. Mimi sitaweza
kuwepo mahakamani.” Sabrina akaona jinsi mzee Msindai alivyolichukulia
hilo jambo kwa uzito.
“Nyumbani
tunatakiwa tuje saa ngapi?” “12 na nusu nataka kila mtu awe ameshafika.” “Basi
sitachelewa.” “Haya mama. Uwe na siku njema.” Sabrina akakata simu na kubaki akiwaza
akitamani kikombe kingemuepuka asionekane na mashabiki wa Phina, ana kwa ana.
Wabakiwe kumsema tu ila si kumuona uhalisia wake. Akajisikia kunyong’onyea.
Akajisikia duni! Akaona ni kama anaenda kujianika zaidi. Alikuwa amefunga kula
ila kunywa tu, akiombea hiyo siku ya kesho. Ukweli alikonda zaidi ya kawaida
yake. Leo kuambiwa atokezee mahakamani na mumewe! Jack alikuwa amependeza na
kuvutia kama Naibu Waziri haswa, Sabrina hakuwa hata na nyama ya nyongeza.
Ikabidi kuanza kusaka nguo na kutafuta kujitengeneza.
Kwa Mama Msindai&Jena.
M |
zee Msindai akampigia simu Jena akamuunganisha na
mama yake. “Nipo katikati ya kazi. Jena, upo na mama
yako hapo.” Akaanza mzee Msindai. “Nakusikiliza
baba.” Jena akajibu kwa heshima zote. “Wakili
niliyekutafutia wewe na Jackson, ameshauri Sabrina ni lazima awepo kuonyesha
yupo pamoja na mumewe katika kila jambo. Nimezungumza na Sabrina amekubali
kutokea mahakamani kesho. Lakini kama nilivyowataarifu, nilazima tukutane jioni
na huyo wakili, tuzungumze na kujipanga ili kuwa upande mmoja. Na Sabrina atakuwepo
hapo nyumbani.” Wote wawili wakaelewa.
“Mimi
nimeshakuahidi baba, sitarudia tena.” “Ninachotaka atulie, kesho aonekane yupo
na mumewe si kwa kulazimishwa ila ni kwa kuwa anapenda kuwa na mumewe. Sabrina
ndiye aliyeturudisha sisi wote kwa mumewe akimuombea msamaha kwangu, Junior na
Jacinta. Yeye mwenyewe ndiye aliyetubu kwa makosa ya mumewe na kunifanya na
mimi nijirudi na kufikia uamuzi huu. Amekusudia kusimama na mumewe. Sasa naomba
usiku wa leo, kusiwepo mazingira ya kuharibu hiyo hali ndani yake. Sijui kama
mama Junior umenisikia?” “Ndiyo.” Akajibu mama Msindai kwa kifupi tu. “Jena?” “Na mimi nimebadilika baba na …” “Jena? Nataka
kusikia juu ya Sabrina, tafadhali. Nipo kazini.” Mzee Msindai akaongea
kwa ukali haswa akisikika hataki kupotezewa muda. “Nimeelewa
baba. Na sitaongea jambo la kuudhi mtu yeyote.” “Basi ni hilo tu. Muwe na siku
njema.” Simu ikakatwa kwa wote wawili.
~~~~~~~~~~~~~~
Maombi Ya
Sabrina Kwa Mumewe Yamepokelewa Kwa Uzito Mkubwa Sana. Amepata Uungwaji Mkono Na
Mzee Msindai Mwenyewe.
Na Mzee
Msindai Amekusudia Kufunga Kesi Siku Ya Ijumaa. Anapanga Timu Yake Vilivyo
Kuhakikisha Hakuna Kosa Linatokea Siku Hiyo.
Je, Atafanikiwa?
Bado Phina Anao
Mashabiki Wake Mtandaoni, Amepungukiwa Wakili Wa Kusimama Naye Mahakamani
Kupambana na kina Msindai.
Je, Nini Kitaendelea?
Usikose
Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment