“Mbona umepata ushahidi
mzuri tu, lakini umejawa wasiwasi?” “Hapana.” Akajibu Jack macho kwenye video.
“Ni nini?” “Mbona Phina hatoki, kaka? Maana mimi nilimwambia atoke, nikapitiwa
na usingizi. Na Mungu wangu ni shahidi kaka, nilipoamka hakuwepo.” “Mbona
alionekana kutoka! Sogeza mbele, nafikiri ni baada ya kama dakika…” “35 hivi
baada ya kuingia.” Akadakia yule bosi wake na kurudi kusogelea laptop yake.
Acha nikusogezee mbele maana hata sisi pia tulisogeza mbele.” Akavuta ile laptop
akasogeza mbele. “Huyu hapa anatoka. Tena inaonekana bado ni usiku, hata lisaa
halikuisha! Mwendawazimu kabisa huyu mwanamke. Ameonjeshwa asali anataka
kujenga mzinga! Mpuuzi wa mwisho!” Jackson akapumua kwa nguvu kusikia kiongozi
wake yupo upande wake.
“Sasa dogo, acha mimi
niwaache nikaweke mambo yangu sawa kabla ya safari. Naona mzee ameshaanza
mchakato, mtawasiliana naye.” “Nashukuru kaka.” “Halafu hujaniamia Msindai. Ile
dili ilitiki?” “Wapi! Nasukumana nao mpaka…” Jack akaona atoke maana walirudi
kwenye mambo yao, akabaki kama msikiliza mambo yasiyomuhusu, akatoka taratibu
na kuondoka bila yakuaga.
~~~~~~~~~~~~~~
Alipoingia tu ofisini
kwake, ujumbe kutoka kwa baba yake na namba ya simu. ‘Mtafute
huyu jamaa, ndiye atakayesimamia kesi yako. Weka mazingira ya kukutana naye leo
bila kukosa. Nataka mwishoni mwa hili juma, niwe nimefunga hizi kesi zako.
Zinanichukulia muda mwingi sana.’ ‘Naweza kukupigia?’ Hakujibiwa, ila
baada ya dakika 15 akaona baba yake akimpigia. “Nakushukuru
sana baba na samahani kwa usumbufu wote. Ila naamini umethibitisha
sijadanganya.” “Umefanya kosa Jackson. Kosa linalonigarimu sana.” “Naelewa baba
yangu. Na narudia tena kukuomba msamaha. Naahidi haitakaa itokee tena.” “Kutana
na huyu mwanasheria mapema.” “Nampigia sasahivi nikiagana na wewe. Ila naomba
nikuulize, baba.” Jack akawahi kabla baba yake hajakata simu maana
alijua ni jumatatu inamaana juma ndio linaanza kwa mzee Msindai mwenye majukumu
mengi, na hospitali yake kubwa anayoendesha. Hata Jena mwenyewe kuna siku tatu
za juma hufanya kazi kwenye hospitali ya baba yake.
“Juu ya nini?” Mzee Msindai akauliza. “Hatima yangu na hii kazi. Nianze kutafuta kwingine?” “Hakuna
mtu atakufukuza kazi. Tuliza akili kazini, usiharibu majukumu uliyopewa.”
Hilo likamtuliza kabisa Jackson. Akajua kumbe baba yake tokea mwanzo alijua
hatafukuzwa kazi! “Jambo la mwisho. Ni juu ya Sabrina.
Yeye hajawahi kuniloga.” Baba yake akamuelewa. Lilikuwa ni kama swali
akitaka uhakika, lakini kama anayeogopa ukweli, halafu kama anayemtetea. “Nampenda Sabrina tokea chuo na sijawahi kuacha kumpenda.”
“Sabrina hajawahi kukuloga, Jackson.” Jack akavuta pumzi kwa nguvu kama
aliyetuliwa mzigo mzito. “Nakushukuru baba yangu.”
“Acha woga. Ongeza nidhamu kwenye hiyo ofisi.” Simu ikakatwa.
Kwa Waili, Wakili wa Msindai
Aliyemtoa Jasho Jackson.
B |
ila ya kuchelewa Jack akampigia simu huyo wakili
ila akakuta ameshajua nini chakufanya. “Nilikuwa
nikimalizia kuangalia video yako nikilinganisha na malalamiko ya Phina.
Nimeshayatoa kopi malalamiko yake yote huko mitandaoni na ninalinganisha na hii
video. Baada ya muda mfupi sana Ibra na Phina watapokea barua zao za mashitaka.”
“Nashukuru sana. Ungehitaji kuniona?” “Hakuna sababu. Ila ningependa kukusikia
wewe binafsi kwanza ndipo nijue ninaendelea vipi kuanzia hapa.” “Unataka
kusikia nini?” “Kuanzia mwanzo wako mpaka mwisho. Usiache chochote ambacho
unajua kitanisaidia kwa haraka dhidi ya hao watu wawili. Mzee anataka tufunge
hii kesi kwa haraka sana.” Jack akavuta pumzi kwa nguvu akifikiria
pakuanzia.
Wakati akifikiria, ujumbe
kutoka kwa Sabrina ukaingia. ‘Nataka kumtuma Chali apeleke
matumizi nyumbani. Kwa jinsi nilivyozugumza na baba, wana hali mbaya.’
Jack akausona na kufikiria kwa haraka akarudi kwenye simu. “Naomba nikupigie baada ya muda mfupi. Nataka kuzungumza na
mke wangu.” Kabla Waili hajamjibu, Jack akakata simu na kumpigia mkewe,
akimuacha huyo wakili akishangaa. Anawezaje kukatiza mazungumzo muhimu kama hayo!
~~~~~~~~~~~~~~
“Wote mliamka
salama?” “Wote tupo salama. Vipi kikao?” Sabrina akauliza. “Kilienda vizuri.
Nilikuwa kwenye simu na wakili atakayeniwakilisha kwenye kesi yangu. Ndio
nimemwambia anisubiri ili nizungumze na wewe.” “Ushanichanganya! Una kesi gani
tena?” “Mzee Msindai amepata ile video. Anataka tumshitaki Phina kwa uongo
anaosambaza mtandaoni na Ibra.” “Kwa maana nyingine baba amepata kitu
alichokitarajia kwenye hiyo video?” “Sijadanganya, Brina.” Sabrina akaanza kucheka.
“Umepoteza
imani kabisa na mimi!” “Acha kuanza kukasirika bwana Jack! Sasa unasemaje juu
ya ujumbe niliokutumia?” “Wewe mtume tu.
Unataka msaada wowote?” “Hapana. Nina kila kitu nilitaka tu kukutaarifu.” “Basi
acha niendelee na huyu wakili. Tutazungumza baadaye.” “Asante kwa kujali na
kupiga.” “Nakupenda Brina.” Sabrina akacheka. “Ndio utulie.”
Sabrina akajibu hivyo na kukata.
Jack akampigia tena. “Tulia Jack, fanya kazi.” “Jana ulinipa wakati mzuri Brina,
leo unataka kunichanganya tu, niharibu kila kitu!” “Haya nakupenda Jack, mume
wangu. Baba watoto wangu. Mupenzi. Umeridhika?” “Kama unamaanisha!” “Namaanisha
Jack. Usikasirike bwana! Tena leo nimefunga kwa ajili yako ili kila kitu kiende
sawa. Mungu akufanikishe hata ambako hustahili” Hapo akamtuliza Jack. “Nashukuru Brina. Basi nitakupigia baadaye kukupa taarifa ya
kinachoendelea.” “Sawa. Na usiogope.” Akakata. “Jack!” Sabrina akabaki
akimfikiria mumewe. “Sasa sijui kama anakumbuka kama yeye ndio amenikosea!
Anataka tena mimi ndio niwe nambembeleza tena!” Sabrina akawaza na kucheka
akimfikiria mumewe.
~~~~~~~~~~~~~~
Akarudisha simu kwa
wakili ambaye hata sura hakuwa akimfahamu. “Nataka
kukupa historia fupi kati yangu mimi, Ibra na Phina.” Jack akaanza moja
kwa moja mara baada ya Waili kupokea. “Nakusikiliza.”
Akamuelezea kuanzia walipokuwa chuoni, walipomaliza na kumtafutia Phina kazi.
Urafiki wake ulipoisha na Ibra. “Subiri kidogo Mheshimiwa.
Naomba turudi nyuma kidogo. Inamaana kilichomkasirisha Ibra ni wewe kumuoa tu
Sabrina, au kulishakuwa na matatizo mengine?” Akauliza huyo wakili.
“Pengine kama
mimi sikuyagundua mapema. Ila ninachokumbuka ni yeye kutoafikiana na mimi
kumuoa Sabrina, tena akiwa mjamzito wa mimba ya mtu mwingine.” “Kwa maana
ingine hata yeye alijua kama unajua kuwa Sabrina ni mjamzito kabla ya kumuoa?” Waili akataka uhakika
kutokana na shutuma zinazoendelea mtandaoni. “Ndiyo. Na
mimi ndiye niliyemwambia. Kwa hiyo sasahivi wanadanganya kusema eti mimi
nilimwambia Phina kuwa nataka kumuacha mke wangu kwa kuwa alinibambikizia
mimba! Si kweli. Na yeye Ibra nishahidi yangu maana hicho ndicho kilichomuudhi
zaidi akisema inawezekana Sabrina ananiloga. Si kawaida. Na hata kwenye harusi
alikataa kabisa kuja.” Akatulia kidogo kama anayeandika.
“Okay.
Endelea.”
Jack akaendelea kumsimulia mpaka siku wanakutana na Phina nchini Uswiz. “Na kilichoendelea ni kama ulichokiona kwenye video.” “Video
haina sauti Mheshimiwa Msindai. Nataka kujua mlichozungumza tokea anagonga
mpaka mnaachana.” Ikabidi Jack asimulie tena. Hakuacha neno hata moja
japo kwa mkewe hakutaka kumwambia Phina alichomwambia ila kwa wakili wake
akaongea yote aliyoambiwa mpaka kumdhoofisha na kumrukia Phina bila kufikiria
mpaka alipofunga goli ndipo akili ikamrudia kuwa ameoa, na amefanya
mapenzi na mwanamke asiye mkewe.
“Mimi si
dhaifu. Ila sijui ilikuaje!” Jack akajitetea na kuendelea kueleza kilichoendelea mpaka
Ibra kufanikisha kumleta Phina nyumbani kwake. “Inamaana
wewe hukujua kama Phina atakuwepo miongoni mwa marafiki wanaokuja kuwatembelea
nyumbani kwako?” “Phina sio rafiki yangu mimi wala wa mke wangu. Mahusiano
yaliishia chuoni.” “Ulimtafutia kazi na kulala naye tena baada ya kuoa.” Waili
akamrekebisha. “Lakini hapakuwa na muendelezo hata
wakuhisi kama anaweza kuja kunitafuta baadaye kwa hitimisho tulilokuwa nalo
nchini Uswiz!” “Baada ya mapenzi?” Hilo swali likamuudhi Jack.
“Unataka
nikwambie kilichokuwa kikiendelea au?” Jack akauliza kwa jazba kidogo. “Lazima tuwe ukurasa mmoja na uelewe aina ya maswali, maana
haya ninayokuuliza unaweza kuulizwa na wakili wa Phina akitaka kuthibitisha
anachokizungumzia Phina na Ibra. Kuwa ulimuahidi ndoa baada ya kumuacha mke
wako, na ndio maana ulimkaribisha nyumbani.” Akamuweka sawa na kuendelea.
“Huyu Phina alikuwa mpenzi wako wakati ulipokuwa na
Sabrina. Si ndiyo?” Jack kimya.
“Kwamba kuna
kipindi ulikuwa na hawa wanawake wote wawili kwa wakati mmoja. Na palikuwa
hakuna mipaka kati yao. Kwamba Sabrina aliweza kufika ulipokuwa na Phina na
Phina hivyohivyo. Si ndivyo?” “Hapana! Sivyo.” Jack akakanusha kwa hasira.
“Sabrina ni mke
wangu! Hata kama nimechanganyikiwa kwa kiasi gani, nisingeweza kumleta Phina niliyekosea
naye karibu ya mke wangu!” “Lakini kama nilikusikia vizuri na hakuna
nilichokosa kutoka kwenye maelezo yako ya muda mfupi uliopita, unaweza
kunirekebisha lakini.” “Juu ya nini?” “Kwamba ulishakuwa na mahusiano ya kimapenzi
na Phina, na Sabrina alikuwepo karibu yenu.” Kimya. “Na kwa kuangalia
hii video ulionekana wewe mwenyewe kumfungulia mlango.” “Si nimekwambia
aliniambia ana kitu muhimu cha kuzungumza na mimi! Au hukusikia?” Jack
akauliza kwa hasira.
“Utanirekebisha tena, Mheshimiwa
Msindai. Mlikuwa hotelini, ambako kuna mgahawa sehemu ya chini. Lakini
ulikubali mazungumzo yenu myafanyie chumbani kwako ambako kwa maelezo yako, tayari
ulikuwa nusu uchi! Ni kama mtu ambaye hukutaka kuweka mipaka kati yenu! Na ni kama
ambaye ameshazoezwa, tena na wewe mwenyewe kufika popote pale. Ndio
maana hapakuwa na shida kufika nyumbani kwa mkeo.” “Hiyo sio kweli.”
Jack akakanusha.
“Narudia tena.
Mimi nipo upande wako Mheshimiwa. Lakini nataka ujiandae, haya ninayokuuliza
unaweza kuulizwa na wakili wa Phina kuthibitisha kuwa nyinyi bado mlikuwa
kwenye mahusiano. Kwa msichana wa kawaida tu, ambaye hampo kwenye mahusiano,
asingeweza kumfuata Naibu Waziri kwenye chumba anacholala, tena usiku ambao
anajua ameshalala! Isipokuwa hawa watu wapo kwenye mahusiano ya karibu sana.
Sijui kama unanielewa?”
Kimya.
“Kilichoendelea
ndani, baada ya wewe kumfungulia mlango inamaana kilitarajiwa kati yenu wote
wawili. Halikuwa jambo geni, na Phina hakuonekana kuvuka mipaka kwa kuwa
hakuvunja mlango, wewe ulimfungulia. Hakukubaka au kukufanyia fujo, ila matokeo
ambayo inaonekana mliridhia nyinyi wote wawili na ndio maana palikuwa na ukimya
kati yenu mpaka swala la ujauzito lilipotokea. Si ndivyo?” Kimya.
“Naomba tuzungumze
Mheshimiwa Msindai. Maana hii kesi mzee wako anataka ifungwe kwa haraka.”
“Nakusikiliza.” “Kwa hiyo unaelewa ninachozungumzia?” “Sasa unataka kunisikia
nikikwambia nini?”
Na yeye Jack akamuhoji kwa jazba. “Uelewe kile ambacho
kinapelekea jamii kubwa kumuunga mkono Phina. Nimefuatilia posti zake na kusoma
kila comments kutoka kwa mashabiki wake. Nataka na wewe uwe upande ambao
hujajifunga, ila ukiwa na akili wazi ili tuweze kumaliza hili jambo.” “Mimi
nakwambia ukweli wa mambo ulivyokuwa.” “Basi tuendelee.” Jack akataka
kumkatia simu ila akakumbuka na yeye yupo kazini, anatakiwa kurudisha majibu ya
kueleweka kwa mzee Msindai. Akajaribu kujirudi na kuendelea.
“Ndio akafika
na Ibra. Wakamkabidhi mke wangu bahasha na kumwambia Phina ni mjamzito wa mimba
niliyompa mimi.”
Jack akaelezea kwa ufupi akificha yale waliyoyafanya akisaidiwa na Jacinta. “Kwa hiyo unakubali kuwa Phina alikuwa na mimba yako?”
“Hapana! Hata kidogo. Sikumkuta ni bikra na wala sijui kama ni mimi peke yangu
ndiye niliyekuwa nikijamiiana naye kwa wakati huo.” “Uliona picha za Ultrasound
ya mtoto aliyekuwa amebeba?” “Hapana. Na pia sio kithibitisho kuwa alikuwa ni
mtoto wangu na ndio maana nilimwambia nipo radhi kupima DNA mtoto atakapozaliwa
kuthibitisha kama mimi ndio baba wa mtoto, lakini sikutaka kufanya naye vipimo
akiwa mjamzito kama ni kweli alikuwa mjamzito ili tusimzuri mtoto. Kwa kifupi
hakuna aliyethibitisha kama kweli alikuwa mjamzito. Na nikweli nilimwambia
tutafanya DNA mtoto akizaliwa. Sasa kama ningekuwa nataka kuanzisha naye
familia, ni kwa nini nitake tena kufanya DNA?” “Pengine hukutaka kurudia kosa
kama anavyosema ulifanya kosa kwa mkeo, ukamuoa akiwa mjamzito
akakudanganya mimba ni yako lakini si yako!” Jack akafunga macho kwa
hasira.
Hakujibu. “Mheshimiwa Msindai?” Waili akaita akitaka kujua kama bado
yupo au alishakata simu. “Kwa kuwa sio kweli!” Jack akajibu. “Hakimu
na wengine wote hawajui hilo. Sijui kama unanielewa? Anaweza kusema kutaka
kufanya DNA ilikuwa ni njia sahihi kwako ili usirudie kosa, uanze naye pazuri.”
“Naomba nikuage kwa sasa?” “Sawa. Lakini nilazima kumalizia haya mazungumzo
na…” Jack akakata simu.
~~~~~~~~~~~~~~
D |
akika 10 hazikuisha, akaona simu ya mzee Msindai.
Akajua ameshapata taarifa. Akajaribu kutulia ndipo akapokea. “Kabla hujaongea chochote baba, jua na mimi nimekasirika
sana. Wakili uliyenitafutia ni kama ananihukumu na wala si kunisaidia!”
“Ulielewa chochote juu ya kutaka kwangu kumaliza hii kesi kabla ya juma hili
kuisha?” “Nilielewa baba, lakini..” “Simu inayofuata kutoka kwa Waili iwe
yakutaka muongozo baada ya kumalizana na wewe, Jackson. Umenielewa?” “Ndiyo.”
“Hakikisha yeye ndiye anayekuaga. Nikimaanisha kusiwe na muingiliano wowote
mpaka atakapomaliza yeye.” “Sawa.” Jack akakubali, simu ikakatwa.
Akatamani kuirusha ile simu lakini akakumbuka huyo wakili anasubiria simu yake ili
arudishe majibu kwa mzee Msindai. Akapoa.
Mtaka
Cha Mvunguni, Sharti Ainame.
Kwa Wakili
Tena.
Akampigia tena Waili, ikapokelewa
kwa haraka kama aliyekuwa akimsubiria na simu mkononi. “Uliishia
kukubali kumsaidia mpaka atakapojifungua, ndipo mkafanye DNA.” Bila
kupoteza muda Waili akapokea na huo muendelezo. “Lakini
ilikuwa ni njia ya kumfanya atulie ili nijipange.” “Narudia tena. Hayo ni
maneno yako wewe, lakini vitendo na anachozungumza Phina, ulishakubali hata
kulipia kliniki yake, na kumtunza yeye kama yeye akiwa mjamzito.” “Ni kweli.”
“Hiyo inamaana mlikuwa kwenye mahusiano ya kama wazazi mpaka ulipomkimbia.”
“Ndiyo.” Jack akajibu kwa jeuri na kunyamaza.
“Sasa huu ndio
ushauri wangu na nitakutaka usimamie hapo. Chochote kilichoendelea kati yako na
Phina baada ya kulala naye Uswiz, futa kana kwamba hakijawahi kutokea wala
kuzungumzwa kamwe hapa duniani. Sijui kama unanisikiliza?” Kimya, Jack akisikiliza
upande wa pili bila ya kumjibu, yeye akaendelea akijua amekasirika. “Wewe hukujua swala lake la ujauzito wala hukumuahidi kumlea
yeye na mtoto. Unanielewa Mheshimiwa Msindai?” “Na swala la kuja nyumbani?”
“Hilo nimeshazungumza na mzee, hapa nasubiria waraka nitaletewa mapema tu, kuwa
walikuja kukufanyia fujo nyumbani ukiwa haupo, wakatolewa na mlinzi, na uliwashitaki.
Safari hii wanapopelekewa shitaka lao la kudanganya na kukuchafua mtandaoni
Phina akitumia siri za ofisi, kwa upande wako na hilo litakuwa moja wapo.
Watashitakiwa kwa kuvamia familia yako na kufanya fujo nyumbani kwako kisha
kukimbilia mtandaoni na kusambaza uongo.” Akamueleza mengi wakijipanga kwa
hiyo kesi ambayo inamashabiki wengi, mpaka kweli akaridhika na kumuaga. Jack akabaki
ametulia hapo mezani simu mkononi asiamini jinsi alivyopozwa na hiyo starehe ya
muda mfupi!
~~~~~~~~~~~~~~
Akabaki akifikiria watu aliowaingiza
matatizoni kwa kushindwa kusema hapana kwa tamaa iliyomuwaka na kuituliza kwa
starehe iliyogeuka kuwa chungu kuliko shubiri. Akamuhurumia sana Phina. Akajua
kwa hakika atalipa anachokifanya, tena atalipa kwa uchungu mkubwa sana. Alijua
baba yake hawezi kumsamehe. Lazima atamuadhibu vibaya sana. Akatamani
angemuokoa tokea mwanzo hutoka huko anakopitishwa na Ibra, na yeye mwenyewe
kujianika mitandaoni. Alimjua Phina. Alikuwa msichana mtaratibu sana, ila
akajua kwa kushindwa kwake kusema hapana kwa tamaa ya mwili iliyomuwaka
gafla na kumrukia kimapenzi, kumeleta maafa makubwa kwake na kumtibua
moyo wake, akajiachia na yeye shetani anatumia uchungu wake na hasira, kumtesa
akihaha huko mitandaoni. “Phina yupo kwenye uchungu wa kupoteza mtoto pia na
kutolewa kwenye ofisi iliyokuwa ikimneemesha.” Jack akajikuta akimuhurumia
badala ya kumchukia vile anavyomchafua. Aliziona siku zake ambazo hatakuwa na
hao mashabiki tena, mzee Msindai amemfikisha kwenye adhabu yake! Jack akajikuta
akivuta pumzi kwa nguvu na kutulia.
Majuto yakamrudisha kwa
mama yake na adhabu anayopokea kutoka kwa baba yao. “Jena!” Japokuwa
mengi alijitafutia mwenyewe Jena, lakini yeye alitoa sababu ya anguko lake.
Hekaheka anayoingiza familia nzima! Kaka yake aliacha shuguli zake, akaja hapo
ili tu kuongeza uzito kwenye mazungumzo yake na bosi wake! Kweli ilisaidia,
lakini ni usumbufu wa starehe ya muda mfupi sana aliyoipata. “Jacinta!”
Akazidi kuhesabu maafa aliyosababisha hata kwa huyo dada yake na kumuhurumia,
akijua yeye ndio miguu na mikono ya baba yao. Inamaana hapumziki yupo kwenye
kutekeleza tena kwa haraka kila anachotumwa na baba yao ili kusafisha maafa
aliyoyasababisha mbali kabisa na nchi! Hapo ndipo akamfikiria baba yake kwa
kumuhurumia. Muda na pesa nyingi anayotumia kwa ajili ya hilo tu! “Umri alio
nao alipaswa kupumzika na kutumia uzee wake vizuri!” Jack akazidi
kujihukumu.
“Masikini Sabrina wangu!” Akamuhurumia mkewe. Yupo
kwenye mfungo akiwa ananyonyesha ili tu kusaidia yeye kusafisha uchafu wake!
Aibu aliyomuingiza. Maneno machafu yaliyosambaa mitandaoni wakimfananisha
muonekano wake na Phina. “Wamemchafua Sabrina wangu kwa starehe iliyogeuka
kuwa chungu kuliko shubiri!” Akawaza na kuumia sana moyoni.
Akatamani hiyo kesi iishe
kwa haraka kila mtu apumzike. Lakini hofu nayo ikaanza kumsumbua akijiuliza
iweje Phina apate wakili mzuri atakayemuhoji zaidi na alivyohojiwa na Waili! “Akinibana
kwa maswali magumu zaidi mpaka nikashindwa kujieleza!” Jack akajiuliza kwa
hofu. “Inamaana hii hali haitakaa ikaisha! Bado kutaendele….” Jack
akabaki akiwaza siku ya mahakamani. Akaona mamilioni ya watu watakavyojaa na
kushuhudia aibu yake. Akazidi kuingiwa na hofu akijutia kumfungulia mlango
Phina usiku ule. “Bora ningefanya kama alivyosema Waili. Kwenda kuzungumza
naye chini sehemu ya Mgahawani kuliko nilivyomfungulia mlango! Kweli zinaa ni
ya kukimbia.” Akazidi kuwaza Jack asijue…
~~~~~~~~~~~~~~
Majuto, ni Mjukuu…
0 Comments:
Post a Comment