“Shem najua. Safari hii nilijiambia sitapitwa
na kitu hata kimoja. Nina uhakika kwa asiliamia 100 bila hata Jack kukanusha
kwangu, Jack hajazungumza na Phina juu ya kina Keiline. Kwa kuwa nayajua mahusiano
ya Jack na wale watoto. Hata ukimuamsha Jackson usingizini, ukamuuliza kwa
haraka baba ya wale watoto wakizungu ni nani, hatamtaja Tino, ila yeye mwenyewe.
Najua kwa kuishi na Jack, kwa hiyo najua kwa hakika, hata kama alikuwa
na shida ya kiasi gani ya kulala na Phina, hilo asingeweza kusema kwa kuwa yeye
Jack halipo akilini mwake hata kidogo. Phina amemsingizia Jack. Hayo mambo ya Tino
na watoto hajayapata kutoka kwa Jack. Ila nahisi, sina uhakika, nahisi kuwa
habari za watoto wetu wamezipata kwa Lela, aliyekuwa mke wa Tino, ambaye na yeye
hajasikia kutoka kwa Tino ila aliambiwa na Sabina.” “Upo sahihi kabisa.” Mzee
Msindai akaafiki.
“Asante baba. Mimi
nilijua kwa hakika Jackson hajazungumza hayo yote na Phina. Ni habari ambazo
ninauhakika sasahivi wanazisaka kwa kila jinsi, ili kuzitumia vibaya. Kwa
upande wa Phina ni ili kuendelea kutengeneza stori yake. Na kwa upande wa Ibra
ni ili kuendelea kumchafua na kumvuruga Jack.” “Sio na wewe!?” “Sio mimi hata
kidogo wifi. Mimi shida yangu ni Jack. Nimeshajua bado mume wangu ananipenda na
anataka familia, sina hofu na ungurumaji wa shetani. Na ninajua inaweza kuwa
mbaya zaidi ya hapo kwa kuwa sasahivi Phina yupo kwenye uchungu wakumpoteza
mtoto wa Jack, aliyejua ni kama alikaribia kumpata tena mume wangu. Tena safari
hii akiwa na mtoto wake! Kwamba watakuwa na mahusiano yasiyovunjika tena, kwa
kuwa wamezaa!”
“Kwa hiyo najua sasahivi
ataweza kuongea chochote na kufanya chochote kwa kuwa yupo kwenye hasira na uchungu.
Na Ibra akimsaidia kukusanya taarifa zetu ili kupanga jeshi kinyume na Jack. Hilo
halinisumbui jamani. Nayajua maneno ya mkosaji jinsi yanavyoweza kuwa machungu
kuliko chubiri, na sumu kali kuliko sumu ya nyoka. Najua kwa kupita kwenye hizo
hali. Najua jinsi mwanadamu anavyoweza kugeuka akawa mkali na hatari kuliko
simba. Ni nguvu ya ajabu sana mwanadamu alipewa na Mungu. Hiyo sina wasiwasi hata
kidogo. Namwacha ahangaike tu huko mitandaoni na popote pale anapotaka yeye,
mimi sitajali ilimradi Mungu amenirudishia mume wangu, inatosha.” Sabrina
akaendelea.
“Shida yangu mimi ni hali
aliyonayo Jack. Tafadhalini naombeni mumsikilize na mume wangu.” Sabrina akamgeukia
baba yao. “Baba, hata kwa magoti mimi nitapiga. Najua alichokifanya Jack. Wala
mimi si mjinga. Najua amekufedhehesha sana, na kwa mara ya kwanza ameharibu
sifa nzuri ya familia. Ila baba, shetani anatumia hili tukio kama fimbo ya
kumchapa kila mmoja wetu hapa. Tafadhalini nawasihi, kama mnaweza kumsikiliza
Phina, basi mpeni na mume wangu nafasi awaeleze upande wake. Na mjaribu kuvaa
viatu vyake pale alipo sasahivi. Tusiruhusu akaingilia hata kazi yake.”
“Hivi unajua cheo cha mumeo ni chakupewa,
shem?” Junior akaendelea kama ambaye bado hajamuelewa Sabrina vizuri au anahisi
Sabrina hajaelewa uzito wa hilo jambo. Akaendelea kumuweka sawa kwa maswali
yatakayomfanya afikirie, kama anayetaka Sabrina aelewe taarifa sahihi kabla hajaongea
sana.
“Kwamba aliyempa anaweza
kumpokonya wakati wowote kwa kuwa hii ni siasa, Sabrina! Acha nikwambie ukweli
Sabrina. Kitendo alichokifanya Jack si kigeni katikati ya watu wanao tuzunguka.
Nawaona wakifanya hayo tunapokuwa tukiishi huko Dodoma kipindi cha Bunge, na
hata kwenye hizi safari zetu tunazokwenda nje ya nchi. Kwao ni jambo la kawaida
sana kulala hovyo na wanawake, hata wenyewe kwa wenyewe, kwao si jambo la hatari.
Ila matokeo yao wao hayana madhara
kwenye siasa zao na wengine. Lakini hapa, katika hili la Jack,
unamgusa moja kwa moja Raisi aliyempa haya majukumu! Anachafuliwa yeye moja kwa
moja kuwa mfanyakazi wake anaharibu, tena anaharibu vibaya akitumia mali ya
umma! Sasa wewe fikiria, amchafulie hivyo, na yeye ana mpango wa kurudi tena
madarakani, unafikiri Jackson atabaki salama?” Junior akamuuliza tena taratibu
tu.
“Nimeshalifikiria hilo na
hata Jack pia. Lakini ni BORA apoteze hiyo kazi lakini si sisi tuliokaa kwenye
hii meza.” Kila mtu pale mezani akamshangaa Sabrina, mpaka Joy mwenyewe ikabidi
amuangalie vizuri. “Jamani, hiyo itakuwa mbaya zaidi.” “Kwa maana nyingine hata
akipoteza hayo madaraka wewe huna shida?” “Hata hilo na yeye aliniuliza wifi
yangu. Mimi nitakuwa muongo, eti leo Unaibu Waziri huu aliopewa Jack juzi,
ndio iwe ngao ya familia yetu! Hakika sijali. Kipato kitapungua, lakini
mkumbuke tulipotoka mimi na Jack jamani! Singida kule, na watoto wetu wote!
Kasoro huyu Brandon ndiye hakuwepo. Lakini tulikuwa hivihivi na hatujawahi kulala
njaa, wala kuhisi kupungukiwa. Haya majukumu aliyopewa sasahivi sikatai
yameongeza kipato, lakini sio kila kitu jamani! Eti kiasi ya kwamba eti
sasahivi ndio tukose utu! Tupaniki na kumtupa Jack kwa sababu ya hofu ya
kupoteza haya madaraka tu!”
“Hapana jamani! Mimi
naombeni tuanze na Jack kama Jackson Msindai kwanza. Yeye mwenyewe na mtu wake
wa ndani, acheni mengine yajijibu kwa kadiri ya muda unavyokwenda. Nashukuru
ushauri wa baba, sitajibu mtu. Mimi huwa namwangalia Mungu wangu. Hata katika
hili atajibu tu. Atamsamehe Jack na atamrejeshea furaha aliyopoteza alipofanya
kosa. Ni hilo tu. Naombeni mumsamehe Jack. Kabla ya kuwaza na kushugulikia watu
ya nje, naombeni tumfikirie Jack mwenyewe, kwanza. Naombeni macho yetu yarudi
kwa Jack mwenyewe.” Sabrina akaendelea bila kuchoka.
“Shem, naomba nyosha tena
mkono, niokotee mume wangu pale alipoanguka, ili asimame tena. Naomba usimuache
chini. Tafadhalini sana. Ni hilo tu.” Sabrina akawafanya watulie na kujirudi.
Maana wote walikuwa wakihangaikia mambo ya nje na kumsahau Jack mwenyewe.
Pakatulia hapo mpaka muhudumu akarudi kuuliza tena vinywaji. Mzee Msindai
akataka aongezewe juisi, akaondoka na kuwaacha kimya.
~~~~~~~~~~~~~
Jack naye akawa anarudi
na Brayan akilia. Sabrina akasimama kuwafuata. “Sasa kaka mkubwa naye analia
nini?” “Ameanguka.” Claire akajibu. “Ila mimi nimemfuta vizuri, kumtoa
mchanga.” “Wewe ni dada mzuri Claire. Asante.” Sabrina akambeba. “Nionyeshe
ulipoumia.” Brayan akamuonyesha akilia. “Pole kaka mzuri. Pole sana.” Akawa
anambembeleza. “Mimi nahisi huu ni usingizi Jack. Tule, turudi nyumbani
wakawahi vitanda vyao, kabla timu nzima haijaanza kilio.” Wakarudi hapo mezani.
“Mkeo amekuagizia
chakula. Tunaweza kuzungumza wakati tukisubiria?” Jack hakuamini. “Kabisa kaka.
Nashukuru sana.” Akajikuta akishukuru bila hata kujua anaitiwa nini. “Sasa huyo
aliyelala si…” “Mlete mimi ni mbebe.” Mzee Msindai akawahi. Jack akamkabidhi baba
yake na kuondoka kwa haraka akimfuata kaka yake. Pakazuka ukimya wakimwangalia
Sabrina akipanga watoto wake hapo mezani. Wakamsikia Jacinta akicheka. “Naona Sabrina
kazi ya umama unaiwezea! Umetuliza ghasia yote kila mtoto ametulia
anakuangalia!” Sabrina akacheka. “Ndio ofisi yangu mwenzio.” Sabrina akajibu
akicheka
“Ila hawa wawili
wanakusikia Sabrina!” “Sana. Kwa hilo namshukuru Mungu, Joy. Hakuna
utakachowaambia ukarudia sana. Imenisaidia kulea hawa mapacha wangu wa nje
kiurahisi. Hata dada zao hawapati nao shida. Wanasema chochote unachowaambia
kufanya, ilimradi wakuelewe tu. Watafanya bila shida.” Jeiline na Keiline
walikuwa wamekaa kwenye kiti wakimwangalia mama yao kila anachokifanya,
wametulia kimya. Mpaka chakula kilipoletwa, zoezi la kula likaanza, Jack na
kaka yake hawakuwa wamerudi.
Waliporudi tu Sabrina
akamuomba Jack wao waondoke. “Nimeomba wakufungie chakula.” “Nashukuru.” Jack
akasimama kwa muda kama aliyetaka kuzungumza jambo, akagairi akaishia kuaga tu.
Mzee Msindai akasimama na mtoto. “Naona sisi watatu tutangulie kwenye gari.” Wakaelewa
anamaanisha yeye, Brandon na Jack. Wakijua anataka kuzungumza na Jack. Sabrina
akaona asubiri kidogo kama kumpa nafasi. Akarudi kukaa akimshukuru Mungu kuwa
wamemsikiliza na wanampa nafasi Jack.
Mzee
Msindai Kwa Jack.
M |
zee Msindai alipomfunga mtoto kitini akamwambia
Jack awashe gari, ndipo wazungumze nje. Jack akawasha gari akaacha inawaka na
A/C akatoka kuzungumza na baba yake. “Sijui umezungumza nini na mkeo! Lakini amekutetea
sana, Jackson. Na ameomba nikusaidie. Sasa, kabla hatujaendelea mbele baada ya
hapa, nakupa nafasi ya mwisho ya kuniambia ukweli bila kunidanganya. Kwa sababu
utakaponiambia neno lolote sasahivi, huna nafasi ya kurekebisha tena, na
nitakuadhibu vibaya sana.” Hofu ikamuingia Jack. Akameza mate akimtizama baba yake na yeye mzee Msindai akatulia akimwangalia.
“Sidanganyi chochote baba. Na wala Sabrina sijamdanganya ili aniamini. Nimesema
ukweli.” Jack akajibu midomo ikimcheza mbele ya baba yake. Mzee Msindai akabaki
akimwangalia machoni kama anayemsoma. Jack naye akatulia akijikaza kumtizama.
“Kwa maana nyingine,
nitakapoletewa video iliyorikodiwa na kamera zilizokuwepo nje ya vyumba vya
hoteli mliyolala nchini Uswiz, siku ulipolala na Phina, nitamuona yeye akiingia
chumbani kwako na sivinginevyo?! Na kabla hujajibu, nakuonya Jackson, uwe na
uhakika. Kwa sababu nitatumia muda na pesa nyingi sana kuhakikisha naipata hiyo
video.” “Labda kama wai wai…” “Jackson?” Baba yake akagomba kwa sauti. “Kama
hawajabadilisha, hakika agiza baba. Mimi nasema ukweli. Na hakikisha ni kweli
ni chumba changu wasije…” “Nimeianza hii kazi kabla hujazaliwa.” Mzee Msindai
akamjibu hivyo na kuondoka akionekana anatoa simu yake ili aanze mawasiliano.
Shetani Hana
Zawadi Ya Bure
Kidogo Jack akashukuru
Mungu akahisi pengine hiyo video inaweza kuwa mtetezi wake kufuta shutuma mpya za
Phina hata kwa mkewe. Maana alijua kwa hakika asubuhi hiyo atakuwa amemmaliza
kabisa kwa kila mtu hata wale waliokuwa wamebakiwa na asilimia chache za imani
kwake, watakerwa zaidi. Kwani asubuhi hiyo mitandaoni, alitoka na jipya akisema
anataka kuongea ukweli wote wa kilichoendelea kati yake na Jack huko nchini Uswiz.
Akaeleza kuwa Jack ndiye
aliyemfuata chumbani kwake akiwa amelala. Akamlilia shida kwenye ndoa yake,
kuwa watoto hao wakizungu ndio wanaleta shida. Kwamba Sabrina aliingia kwenye
ndoa akiwa amemdanganya Jack kuwa mimba
ni yake. Siri ilifichuka walipozaliwa watoto wa kizungu. Na fujo inayoendelea
kwenye ndoa yake kwa sababu ya Tino aliyejitokeza kama baba wa hao wa watoto wakizungu.
Kwamba imezua tatizo
kwenye ndoa yake, Jack ndio anataka kumuacha Sabrina. Hataki kuingia kwenye
vita na Tino. Anataka kuoa tena. Na alimuomba yeye rasmi aanze naye upya kwa
kuwa walishakuwa na mahusiano ya kimapenzi, na yeye hakuwahi kumsaliti kama
Sabrina. Ndipo Phina alipojiachia mpaka kushika mimba.
Akaendelea kueleza kupokelewa
kwake ramsi na wakweze, wakimkaribisha yeye na mtoto kwenye familia ya Msindai.
Na ahadi hata ya babyshower ambayo haikuwa hata siri huko mtandaoni. Wifi
yake Dokta Jena Msindai aliliweka wazi bila kificho. Na alimfuta yeye kibinafsi
na kumwambia mama Msindai ndiye atakayemfanyia babyshower ya huyo mjukuu
aliyembemba kama njia yakumkaribisha mtoto kwenye familia.
Huku Nyuma Walipoachwa na
Sabrina.
“Kila nikizidi kukufahamu
wifi yangu, nazidi kuelewa kwa hakika ni kwa nini Jack alikung’ang’ania akuoe
wewe!” Sabrina akacheka tu. “Kweli Shem. Umefanya wote sisi tujirudi. Sijui
upande wa Jacinta, ila kwa jinsi nilivyomuona baba, haya mazungumzo nafikiri
wote tulihitaji kuyasikia Shem. Ni jambo lililotupata kwa mshituko. Hakuna
aliyetegemea. Tukajikuta tukisumbuliwa na habari za mitandaoni, tukamsahau
Jackson mwenyewe.” “Ila kwa upande wangu aliniudhi zaidi nikijua ameanza
umalaya.” Jacinta akaongeza. “Hilo nalo.” Junior akakubaliana na dada yake.
“Kwa sababu madaraka na
pesa huo vina mtindo wa kumuanika mtu na kumfichua kabisa. Hata kama alionekana
anatabia fulani, akishapata nafasi, ndio anaanza kutoa makucha yake.
Hilo mimi lilinikera sana. Halafu akaniudhi zaidi akionekana tena hajui
chakufanya! Hapo ndipo nikachukia kabisa. Yaani ameanza uchafu wake, halafu hajui
jinsi ya kuishi nao huo uchafu! Hapo ndipo aliponikera nikawa nikimkwepa
kabisa. Maana nilijua akinisogelea, naweza kumchapa makofi bure kama mtoto
mdogo.” Jacinta akaongeza na kuendelea.
“Lakini hiki
ulichokizungumza, na mimi nimekua kama Junior. Nimeshukuru kukisikia. Kwa
asilimia kumbwa sana kimenituliza. Hata sasahivi ninapo shugulika na hili jambo
zima, la huyo Phina, nishaona utofauti. Si kwa..” “Kupaniki.” Akadakia Junior.
“Kabisa Junior. Si kwa paniki au hofu. Na mimi naanza kumuona ni kama mfa maji
tu. Na nakwambia ukweli, sijui labda iweje, inaweza isiwe kubwa kama
tunavyotaka kujiogopesha.” “Na hata ikiwa kubwa wifi, bado nawaomba mbaki na
Jack.” “Sabrina alivyomng’ang’ania mumewe!” Joy akafanya wacheke.
“Kwa kuwa namjua Jack
wangu jamani! Hajabadilika ila amekosa tu.” “Basi shem. Tumekusikia.” Wakazidi
kucheka. “Nawashukuru sana. Asante shem na samahani kuwaharibia mapumziko
yenu.” “Na kweli umeyaharibu!” Joy akadakia. “Joy naye! Huwa waungwana wanasema
usijali!” “Mimi najali. Junior wangu huwa simpati kwa muda mrefu na jumatatu
usiku anasafiri tena!” Junior akazidi kucheka akimwangalia mkewe. “Basi
ondokeni sasahivi na nyinyi msitukere. Msichomalizaga nyinyi ni kipi mno!
Mapumziko hayaishi!” “Kwanza hapa kikao
kimeshaisha. Twende Joy.” Junior akasimama kabisa.
“Wazazi nyinyi hata
sijawapatia mfano! Watoto wenu bado wanakula, nyinyi mnataka kukimbia!” “Nani
anataka kurudishwa na anti Jacinta nyumbani?” Junior akauliza. “Mimi naweza
kurudi na anti.” CJ akajibu taratibu tu kama aliyeelewa nia ya wazazi wao kwa
haraka. “Na wewe Claire mwanangu mzuri hutaki..” “Hakika siamini! Kweli nyinyi
mnauza watoto!” Jacinta akawashangaa Junior na Joy, wao wakazidi kucheka. “Baki
na anti na umwambie akupitishe kule madukani kwenye vibanio vizuri. Mkanunue na
ice cream ndio mrudi nyumbani. Umesikia Claire mtoto mzuri?” “Mimi sinunuliwi
kitu?” Cleiton akauliza baada ya Claire kutingisha kichwa akikubali. “Na wewe
Cleiton mwambie anti atakununulia chochote unachotaka.” Wakaondoka kwa haraka,
Jacinta akiwaangalia. Sabrina hana mbavu, kwa kucheka.
“Huna neno wifi yangu?” Sabrina
akamuuliza akicheka. “Tufanye nina neno. Ushawaona wazazi wenyewe?” Sabrina
akazidi kucheka. “Msiwe na wasiwasi wanangu. Tukitoka hapa, tunaenda kuangalia
movie, tunanunua na popcon kabisa. Tunakula popcon huku tunaangalia movie. Tukichoka
tunaenda madukani, halafu ndio nawarudisha nyumbani. Au mnasemaje?” Wote
wakakubaliana na anti yao, babu yao akawa anarudi.
“Mbona Junior na mkewe
wameacha watoto?” “Nawapeleka movie na kumnunulia Claire vibanio vya nywele.”
Mzee Msindai akacheka akikaa. “Nakushukuru baba yangu, acha sisi twende, hawa
wakalale.” “Karibu mama. Na tunashukuru na wewe kwa kila lililoendelea hapa.
Mfike nyumbani salama.” Jacinta akamsaidia kubeba watoto na mizigo, wakaenda
garini. Wakamkuta Jack garini amekaa, kimya. Wakapandisha watoto garini,
Jacinta akaenda upande wa dereva alipokaa Jack. “Kula na ulale vizuri ili uwe
na uwezo wa kufikiria. Umezeeka gafla!” “Sasahivi naweza hata kulala!” “Ndio UKOME.”
“Nilishakoma dada.” Jacinta akamuangalia na kuondoka bila yakujibu.
Shetani
Hanaga Usingizi!
W |
akati wanaingia getini, Sabrina akamuona baba
yake amesimama na walinzi. Hakutegemea kumuona baba yake nyumbani kwake! Akamwambia
Jack amshushe. Akasimamisha gari, Sabrina akashuka, yeye akavuta gari ndani na
kuita wasichana wakazi watoke wachukue watoto maana wote walishakuwa wamelala. Na
yeye akarudi getini alipomuacha mkewe akawakuta kwenye mazungumzo. Akapenyeza
salamu na kumkaribisha baba mkwe huyo ambaye hawakuwa wameonana kwa muda mrefu.
“Karibu ndani.” Mzee alionekana amechoka haswa. “Naomba tukazungumzie ndani
baba.” Sabrina akaweka msisitizo na kutaka kutangulia. “Mimi sitakaa sana,
nilitaka tu…” “Kwa hiyo unataka uishie getini!?” Sabrina akashangaa sana.
“Kwa nini iwe hivyo!?
Kuna uadui gani huo mkubwa kati yangu mimi na nyinyi wazazi wangu mpaka
nikifika kwenu mshindwe kunikaribisha ndani, na mkija kwangu pia mshindwe
kuingia ndani!?” “Ni vile nimekuja bila miahadi sikutaka kusumbua. Ila nilikuwa
na jambo muhimu sana nataka kukutahadharisha. Na ninaharaka yakurudi
nyumbani. Wala si kwa ubaya kati yetu.” “Sasa ndio unataka hilo ‘jambo muhimu’
tulizungumze hapa nje tumesimama wimawima?! Kwa haraka gani hiyo hata ndani
usiingie?!” Jack alipoona Sabrina ameshawaka akaona aingilie. “Tafadhali karibu
ndani. Husumbui mtu yeyote. Jisikie upo nyumbani, karibu. Sio sawa uishie nje.”
Wakaongozana mpaka ndani.
“Karibu mzee wangu. Sisi
tulikuwa tumetoka, acha tuangalie chakula ndani.” Akamtizama Sabrina kama
anayetaka aongozane naye. Sabrina akaelewa na kuongozana nae chumbani. “Naomba
tulia mama.” “Kwa nini wananifanyia hivyo!? Nilichowakosea mimi ni nini
jamani!?” “Naomba tulia, tujue kilichomleta. Tafadhali mama.” Sabrina akatulia.
Akatoka kwenda jikoni, akamwambia msichana wake wa kazi aanze kuandaa meza kwa
chakula cha baba yake, yeye akarudi chumbani kubadili nguo.
~~~~~~~~~~~~~
Alichoshangaa Sabrina,
alipomkaribisha baba yake chakula, hakujivunga hata kidogo. Akahamia mezani
kula. Alionekana na njaa na amechoka. “Mama anaendeleaje?” Sabrina akatupia
hilo swali wakati akimpangia mumewe chakula sehemu ya sebuleni. “Hali sio nzuri.”
“Mgonjwa?” Sabrina akauliza. “Mmmh!” Akamsikia akiguna tu na Sabrina akanyamaza
kama kumpa nafasi amsikie. Maana mara ya mwisho alimfukuza hakutaka hata aingie
ndani. Sabrina alipoona hazungumzi akaenda kumuita mumewe chumbani ili atoke
aende kula maana wakati wao wakila, yeye alikuwa kwenye mazungumzo na kaka yake.
Akamkuta amejiinamia.
~~~~~~~~~~~~~~
“Ni nini tena!?” “Daaah!
Kwanza sijui umezungumza nini na kina kaka, naona nimepata uungwaji mkono
mzuri. Ameniambia kesho atakuja ofisini kunichukua, tukazungumze na Waziri wa
Fedha mwenyewe. Atamuomba leo, ili kesho anipe nafasi yakunisikiliza upande
wangu ili atushauri. Baba ametoka kunitumia ujumbe kuniambia ushauri wa Junior
ni mzuri, nitengeneze mazinga yakutekeleza hilo kutokana na muda wa Junior
kabla hajasafiri.” “Sasa mbona ni jambo zuri na wewe unaonekana kukosa tena
raha?” “Kwa upande huo hamna shida. Kwanza nakushukuru. Asante Brina.
Umerudisha mioyo yao kwangu! Naona hata kaka amenipa pole na kunitia moyo. Na
baba anashugulikia video ya Uswiz iletwe.” Hapo akamchanganya Sabrina.
“Sijaelewa! Video gani
tena?” “Si unajua haya mahoteli makubwa huwa yana Surveillance cameras?”
Sabrina akabaki ametoa macho. “Kwamba yanarikodi matukio yote kila wakati ndani
na nje ya hoteli. Sasa baba anataka kuagiza rikodi ya siku na muda ule wa usiku
kwenye gorofa nililolala mimi na gorofa aliyokuwepo Phina ili kuthibitisha
hicho alichosema Phina kuwa eti mimi ndiye niliyemfuata chumbani kwake na
kumwambia maneno yote hayo. Najua na wewe umemsoma leo asubuhi mtandaoni. Unajua
shutuma zake mpya.” “Unauhakika baba hatakuta vinginevyo?” Hilo swali
likamuumiza Jack.
“Kwa hiyo huniamini?” “Mimi nakuuliza Jack.
Maana najua ukimdanganya mzee Msindai, safari hii hatakusamehe. Nilimuona ni
kama amelainika baada ya mazungumzo yetu jioni hii, sitaki umtibue zaidi.”
“Sidanganyi Brina! Mungu wangu ni shahidi, yeye ndiye aliyenifuata chumbani
kwangu. Tena ndio vizuri hata baba athibitishe sio kwamba nililala chumbani
kwake usiku kuchwa kama anavyodai yeye.” Jack akaongea kana kwamba kulala na
mwanamke asiye wako kwa muda mfupi ni bora kuliko kulala naye usiku kuchwa!
Sabrina akamwangalia akaona amuache tu. Aendelee asijetoka kwenye pointi.
Akarudia swali lake. “Ndio nauliza, tatizo ni nini tena? Maana ni
kama hayo yote yanakwenda sawa!” Jack akamwangalia na kutingisha kichwa kama
anayesikitika. “Ni nini Jackson!?” “Nina wakati mgumu Brina! Naomba usikasirike
zaidi na kunikimbia. Nitarukwa na akili uki…” “Jackson Msindai, baba yangu yupo
sebuleni na yeye anasema kuna jambo anataka akanitahadharishe, na chakula chako kipo tayari kinaendelea kupoa. Tafadhali
nipunguzie hii hali ya wasiwasi unayotaka kuniongezea.” Jack na yeye akasimama
kama mkewe na kuzidi kumtia wasiwasi.
~~~~~~~~~~~~~
Inaendelea….
(Thank You God For The Gift Of Life. Nov 7th)
{Ufamle Wako Uje, Na Mapenzi Yako Yafanyike Hapa Duniani Nilipo Mimi, Kama Huko Mbinguni}
{HAPPY BIRTHDAY TO ME}
0 Comments:
Post a Comment