Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 66. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 66.

“Niliamuru asafirishwe na ndege ya leo usiku. Wakati nakuja kwako, nimepata ujumbe kuwa wamefanikiwa kumtoa hapa nchini.” Sabrina akaanza kulia tena. “Nimemwambia asirudi hapa nchini na wala asikutafute mpaka baada ya miezi sita kuanzia leo. Na hii nimefanya kwa sababu yako tu. Isingekuwa wewe, na hichi alichokutendea Jack, bado Tino angekuwa kifungoni. Na asingetoka mpaka kifo chake.” Sabrina akazidi kumuogopa mzee Msindai. Usiku huo alivaa sura ambayo hajawahi muona nayo!

“Nimemuahidi nyumba yake italindwa mpaka atakapokuja kurudi. Nataka utulie Sabrina. Maamuzi yoyote utakayoyafanya sasahivi, yanatoka kwenye hisia zilizoumizwa na hofu, unaweza usipatie sana. Tulia. Nataka utulie kabisa, mimi nipo kwenye kutengeneza. Baada ya miezi sita kuanzia sasa ukiona bado unahitaji Tino awe karibu na watoto, hapo utakuwa na akili safi ya kujua uweke mipaka gani. Na yeye Tino nilimwambia. Amepoteza haki ya ubaba kwa hawa watoto, ataishi nao kwa kauli yako. Kwa hiyo tulia. Fikiria kisha baada ya miezi sita kuanzia sasa, tutazungumza tena. Sawa?” “Nashukuru, usiku mwema.” Sabrina akazidi kulia akielekea kwenye gari ya Jacinta akitamani bora asingepanda humo.

Wakati Jacinta akimsubiria Sabrina aingie garini, ujumbe kutoka kwa baba yake ukaingia kwenye simu yake ya kazini, ‘Singida, HAPANA.’ Akaelewa mara moja. ‘Nimeelewa baba.’ Akarudisha hayo majibu na kuweka simu pembeni. Sabrina akapanda garini akilia.

“Nisikilize Sabrina. Wewe una watoto wachanga watupu. Wote wanakuhitaji wewe kama mama. Tulia ulee watoto wako. Hakuna atakayeruhusu ukapata shida ya kuishiwa pesa. Usiogope. Tulia kwa kipindi hichi ulichoumizwa, pata muda wa kufikiria ili utoe maamuzi sahihi. Unanielewa?” Sabrina akatingisha kichwa akilia kwa uchungu akiumia kwa nini wamfukuze Tino.

Alilia mpaka akafikishwa kwake, analia na kushindwa kunyamaza. “Nisikilize kabla haujashuka garini. Pina nenda kampe huyo kaka maziwa ya kaka Brayan, alale ili mama yake naye aje apumzike.” Pina akashuka garini na mtoto. Wakabaki wao wawili. “Mambo ya Phina yamemtingisha sana baba. Ni jambo lililotekea bila kutegemea. Analalamika kumuamini sana Jack, alidhani yupo kama Junior. Sasa, kwa jinsi lilivyolipuka hili la Phina, na Tino naye akawa anaonekana na watoto mtaani, ikawa ni fujo, hatujui tutulize wapi, tuache wapi. Na madhara yake si kwenu tu, ni familia nzima kama ulivyomsikia baba. Katika watoto wa Msindai, Junior amekuwa kioo cha jamii kwa muda mrefu sana. Hapajawahi kutokea skendo yake hata mara moja. Na mkewe hivyohivyo. Joy hana mambo mengi. Biashara na kupigizana kelele na wanae kama vile unavyomuona, hata marafiki hana.”

“Ilibidi kwenu baba mwenyewe aingilie kati kwa sababu nyinyi wenyewe mlionekana kuharibu zaidi kuliko kutengeneza. Sijui kama unanielewa?” Sabrina akaanza kujisikia aibu. “Mimi nitakwambia tu ukweli wifi yangu, nikijua unajua nakupenda. Si ndio Sabrina?” Akajifuta machozi akikubali. “Mlikuwa mkiharibu zaidi kila inapoitwa leo. Katikati ya yote hayo eti Tino aliyekuwa amefungwa jela, anatokea Wizara ya Vizazi na Vifo na barua kutoka kwa Sabrina Msindai, akitaka watoto wabadilishwe majina! Kutoka kuwa Msindai, sijui waitwe nani sijui! Ilimshitua sana baba na kuamuru Tino apelekwe alipo.” “Baba alijuaje wifi!?” “Nakwambia hivi, hakuna jina la Msindai likatajwa mahali kwa hila, asisikie. Ana masikio kila mahali. Ndio maana ikabidi kuingilia kati yeye mwenyewe alijua nyinyi wote mnatengeneza mkiwa mmepaniki.” “Nimeelewa. Na samahani. Ila naomba nikuombe kitu.” Sabrina akajifuta machozi.

“Nini?” “Ikitokea nakufa wifi, naomba angalia wanangu. Popote walipo, jicho lako liwe kwao.” “Hilo nakubali. Lakini nataka uondoe mawazo ya kufa ila kuishi ulee wanao mwenyewe. Unanisikia Sabrina?” “Nasikia, ila inatokea. Na inaweza kutokea.” “Hilo nimekuahidi nitafanya kama na mimi nitakuwa hai. Lakini nataka uanze mabadiliko yako wewe binafsi. Sasahivi nenda kapumzike. Lala kama mtoto mchanga kabisa. Usiku wa leo Pina atalea watoto. Nitaenda kuzungumza naye. Nakupa dawa za usingizi. Kalale kabisa. Naomba jaribu kutulia, upone. Umekonda, umechoka, usiruhusu watu kukuita kinyago kwa makwazo ya Jack. Hastahili. Unanielewa Sabrina?” Sabrina akatingisha kichwa kukubali.

“Naomba anza kwa kutoa hizo nywele kichwani. Hazijakupendeza hata kidogo. Kesho asubuhi badala ya kukimbilia Singida na kwenda kujionea huruma huko, anza kwa kwenda saluni. Suka nywele nzuri, pendeza. Jitengeneze, mimi nitakulipia garama nzima, ni ofa yangu.” Sabrina akacheka akiwa ameinama. “Kesho ni alhamisi. Ijumaa tunatoka kwa chakula cha jioni. Mimi, wewe, Joy, na Pendo. Bila watoto. Tunakwenda kula na kunywa mpaka tuchoke ndio tunarudi makwetu. Hakuna kurudi Singida. Kama hujaelewa, ndio mzee Msindai amekutambua ramsi.” “Kweli!?” “Wewe mpaka ametangaza wanao ni warithi wake! Unafikiri ni kitu kidogo?” Sabrina akabaki kimya akisikiliza.

“Kwa mara ya kwanza baba ametoa wosia wake mbele ya Junior ambaye wote tunajua  ndio mrithi wake. Na amefanya makusudi kuwatangaza mbele ya watu wote mpaka mama mwenyewe amepoa! Wewe na Joy ni Msindai. Baba anatambua watoto wako wote, Sabrina. Anza kuishi kama unayejielewa, au kama vile Joy. Hakuna kumpisha mtu hapa mjini. Mjini haondoki mtu labda ndani ya jeneza.” Sabrina akacheka. “Pambana kufa kupona mpaka wewe ndio ubaki umesimama. Usikimbie hovyo. Mimi nipo na wewe, na hao warembo wako ni jukumu langu nalipokea kwa asilimia zote.” Sabrina alifurahi sana, hakutegemea. “Muda na wakati wowote, nipigie. Unanielewa?” “Nashukuru wifi yangu. Ila kweli natamani ningeyasikia haya muda mrefu, wifi. Haya yote yamebadili hata mtazamo wangu na imeniondolea hofu. Nahangaika kwa ajili ya wanangu wifi! Sikutaka kuacha wanangu hawa wawili pabaya.” “Babu yao achasema tusichanganywe na hiyo rangi yao. Na wao ni warithi wa Msindai. Sasa kama ni warithi wa Msindai mwenye mali zote hizo, unafikiri watakuja kupata shida?” “Sasa hivi nimeridhika wifi yangu. Roho yangu imeanza kutulia. Na hivi na wewe najua umeshawachukua, hata Jack akiniua kesho sina wasiwasi.” Safari hii Sabrina akasikika ametulia.

“Hawezi. Sasa hivi jicho la baba lipo kwake mpaka namuhurumia aisee!” Wakatulia kidogo. “Haya twende ukanywe dawa, nataka ulale mpaka ukorome kabisa. Usiku wa leo watoto wakilia, si jukumu lako. Kesho saluni siku nzima. Hawa kina Msindai watakua sawa tu, usitie shaka.” Sabrina akacheka na kushuka garini. Jacinta naye akashuka, wakamkuta Jack amejiinamia hapo sebuleni. “Nataka usiku wa leo Sabrina alale kabisa. Nampa dawa ya usingizi, nataka alale atulie kabisa. Hata kama unajambo lako unataka kuongea, unyamaze Jackson. Maana wewe ni msumbufu.” “Sawa.” “Na usaidie alale. Sio waanze kumgongea nakuanza kumuamsha wakiuliza maswali ya watoto. Hakikisha wewe unaweka sawa mambo yote. Asubuhi uondoke hapa pakiwa pako sawa, maana akiamka, anakwenda saluni. Ijumaa kama ulikuwa na mipango yako, uahirishe ujue unakibarua chakulea, sisi tunatoka na Sabrina.” “Hata hivyo sikuwa na mipango mingine.” Jacinta akamtizama kama mchape kofi. Sabrina akapitiliza chumbani. “Nashukuru dada.” Jack akanong’ona. Jacinta akaelewa ameshukuru kumfanya Sabrina abaki. “UKOME.” “Nishakoma.” Jacinta hakumjibu akamfuata Sabrina chumbani.

Sabrina alikuwa amechoka, zaidi mawazo na mshituko mpaka maziwa yakakata. Na kwa kuwa hakuwa mnywaji pombe, dawa aliyopewa na Jacinta, ilimchukua kwa haraka sana hata asijue alipo. Alilala kama mama asiye na vichanga ndani ya nyumba. Alikuja kuamshwa na kilio cha Brandon, akadhani ni usiku kumbe saa nne asubuhi ya siku inayofuata. Akataka kutoka kitandani, akasikia kizunguzungu, akarudi kujilaza na kumuita Pina. “Mlete.” Akashangaa anaingia Jack na mtoto. “Huyu mtoto anakataa maziwa anayopewa na dada yake.” “Ngoja nijaribu kumnyonyesha.”

“Nikuletee supu? Pina amekupikia.” Jack akaongea kwa kujali akisikika kujikomba kabisa. Sabrina hakumjibu akaendelea kumnyonyesha mwanae  mwishoe akamuita Pina na kutaka aingie. “Naona sina kitu cha kumpa huyu mtoto. Anajibembeleza tu hapa na ziwa. Naomba supu, ingine nifungashie na uji ule uliokuwa ukinipikia wakuongeza maziwa, nitaondoka navyo. Kisha nipe maziwa ya Brandon nimjaribishe huyu.” “Amekataa kabisa.” “Wewe nipe mimi nitampa.” Jack akabaki amesimama hajui chakufanya.

Sabrina akafanya yake, akapaacha hapo vizuri, mtoto wake akalala akiwa ameshiba, ndipo akaondoka kuelekea saluni. Alimuacha Jack hapo nyumbani, hata hakumuuliza muajiriwa huyo, muda huo anafanya nini nyumbani siku ya kazi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Akaelekea saluni yake ya zamani ambayo walikuwa wakimsuka mtindo wake ambao huwa anapendeza, huna jinsi ukaacha kumsifia. Wakaenda kumtoa zile nywele, kazi ya ukarabati ikaanza. Mpaka inafika saa nne usiku, Sabrina hakuwa amerudi nyumbani.

Jack akamtumia ujumbe. ‘Upo salama huko?’ Sabrina akasoma akafikiria, akaona tu ajibu. ‘Bado nipo saluni. Brandon analia sana?’ ‘Babu yake amemletea maziwa amesema apewe hayo hayatamsumbua tumbo. Naona amelala. Nilikuwa nakuangalia tu, kujua kama upo sawa.’ ‘Bado kama lisaa hivi wanimalize.’ Hivyo tu kujibiwa, kukamfanya Jack afarijike. ‘Sawa. Usiwe na wasiwasi watoto wote wapo sawa. Wewe malizia tu.’ Hapo hakujibiwa tena. Akatamani amtumie ujumbe mwingine, akaona asiharibu. Akatulia.

Usiku huo Sabrina alirudi kwake saa tano na nusu, akamkua Jack sebuleni. Akataka kupitiliza, Jack akamuwahi. “Umependeza.” Sabrina hakumjibu. Akapitiliza jikoni, akaweka vyombo na kupitiliza chumbani kwenda kuoga. Alipotoka akakuta Jack amemuwekea supu. “Naomba unywe hii supu ndio ulale. Baba ameleta kuku wa kienyeji, anasema itakusaidia.” Sabrina akaiangalia, akaibeba na kutoka nayo pale chumbani, hakumsemesha kitu. Jack naye akaona anyamaze. Akaenda nayo chumbani kwa Brayan na Brandon. Akawakuta wamelala vizuri. Akajua wameshiba. Na yeye akakaa kabisa sakafuni, akaanza kuinywa hiyo supu. Aliposhiba, akajilaza hapohapo sakafuni akitafakari, akapitiwa na usingizi.

Jack akajua ndio analala huko, akamfuata. Wakati anatoa vyombo alivyokuwa ameacha pembeni yake, akaamka. “Nahisi nimechoka. Bado dawa za wifi zinanipa usingizi. Nilikuwa nikisinzia siku nzima huko saluni.” “Naomba ukalale kitandani, Sabrina. Mimi naweza kulala hata kwenye makochi.” “Sawa.” Sabrina akanyanyuka hapo na kuhamia kitandani hata meno hakusafisha. Akalala hivyohivyo.

~~~~~~~~~~~~~~

Asubuhi na mapema, Jack akaingia hapo kwa kunyata ili asimuamshe, akajitayarisha kwenda kazini, akatoka. Ijumaa hiyo ndiyo ilikuwa ya Sabrina kutoka kwa chakula cha usiku na wifiye pamoja na Pendo na Joy. Angalau alikuwa amepata kitu cha furaha akikitizamia. Akawa na kazi ya kutafuta nguo zitakazoendana na kamwili kake. Akatamani kupendeza zaidi, maana hizo nywele zilishambadilisha. Ungeweza sema ni mwanamitindo wa kutokea Los Angeles, Hollywood, aliyefanya juhudi za makusudi kupungua kwa ajili ya hilo jukumu.

Phina.

Cha Mtu, Mavi!

P

hina alikuwa na furaha ya kupokelewa ukweni yeye na mwanae, kwa ahadi ya kufanyiwa babyshower na mama Msindai! Ikawa kama ndoto ambayo hajawahi hata kuiota. Hana ajualo, akaanza siku yake na amani rohoni. Ungemuona Phina, ungejua kuna jema tu linaloendelea maishani mwake. Akaingia ofisini amependeza kwelikweli. Furaha imejaa, anazaa na Jackson Msindai, shida iko wapi? Mimba hiyo changa ikaanza kutunzwa kwa kula vyakula bora. Akaagiza hapo vitu vyake alivyoona ni bora kwake na mwanae, baada ya muda akaletewa. Akaanza kwa matunda, ndipo akaja sasa mayai, firigisi na mengine mengi akitaka mwanae akue vizuri. Akasukumia na maziwa yaliyowekwa Milo. Phina akaridhika, siku ya kazi ndipo ikaanza sasa.

Akiwa ndio ameenza tu kazi akapewa barua. Akaifungua akiwa amekunja uso, haelewi ni ya nini. Hakuamini alipoisoma. Wizara ilimtaka aripoti Lindi, Nampunga. Phina alishituka sana, hakutegemea. Akataka kupaniki lakini akakumbuka hayupo tena peke yake. Akaamua kumpigia simu Jackson Msindai, Naibu Waziri, baba mtoto, ili amsadie. Akatafuta namba ya Jack kwenye orodha ya majina kwenye simu yake, hapakuwa na hiyo namba wala jina la Jackson Msindai. Phina akashangaa. Akaona aingie kwenye jumbe zake za zamani alizokuwa akichat na Jackson, ili amtumie ujumbe kuwa ni jambo muhimu na ampigie kwa haraka, hapakuwa na chati. Phina alishangaa karibu macho yamwagike. Akatafuta tena na tena akahisi kuna mazingaombwe kwenye simu yake, maana hapakuwa na ujumbe hata mmoja kana kwamba hajawahi ku chat na Jack kabisa!

Akajaribu kukumbuka namba ya Jack. Kila namba aliyokumbuka na kupiga haikuwa ikienda kana kwamba hiyo namba haikuwahi kutumika! Akaanza kuingiwa na wasiwasi. Nani wakumsaidia! Akahangaika, hasira zikampanda. Akakumbuka picha alizompiga walipokuwa wote nchini Uswiz, akaona huo ndio wakati muafaka wa kuzitumia kama fimbo ya kumsaidia kubaki mjini. Akaanza kuzisaka. Akashangaa hakuna hata moja kwenye simu yake wakati hakuwa amezifuta!

Tumbo likaanza kukoroga. Akakimbilia chooni. Akaanza kutapika. Akajua mambo ya mimba changa. Likazidi kuuma kama yupo kwenye siku zake. Hajakaa sawa, tumbo la kuharisha likaanza. Akaanza kuhara mfululizo kama aliyekula kitu kibaya. Mara ya pili anajisaidia, damu zikaanza kutoka. Alishituka Phina, karibu aanguke chooni. “Inamaana mimba yangu imeharibika!” Akawa haamini. Kila alipojifuta, akawa anakutana na damu. Akawaambia wenzie wamsaidie kwenda hospitalini ili kujaribu kuwahi kuokoa hiyo mimba. Mpaka anafika hospitalini akawa hatapiki tena wala tumbo la kuhara hakuna, limepo kabisa, ni siku zake tu! Ikawa kama aliyesafisha tumbo, basi. Phina alikuwa akilia kama amefiwa na mtoto aliyekwisha nyonyesha.

Daktari aliyemuhudumia akamuuliza “Kwani ulikuwa na mimba ya miezi mingapi?” “Miwili!” “Au ulipitisha tu siku zako, maana hakuna dalili ya kutoka mimba ila hedhi ya kawaida tu!?” Phina akazidi kulia. Akasema anao mpaka ushahidi wa ultrasound. “Ilikuwa ni mimba kabisa!” Hapakuwa na chakufanyiwa. Akashauriwa akapumzike na kutumia dawa za maumivu endapo maumivu yataendelea. Phina akaondoka hapo hospitalini asiamini kama yamempata hayo! Alishajiona vile atakavyotembea na tumbo kubwa akijulikana amebeba mimba ya Jackson Msindai. Alishaona heshima atakayopewa siku ya babyshower yake! Alishaona vile atalea huyo mtoto na Jackson! Leo anarudi nyumbani hana kitu! Ulikuwa msiba mkubwa sana kwake. Aliona ndoto zake zikipotelea chooni, akishuhudia kwa macho yake.

Kitu cha kwanza alipofika nyumbani kwake ni kutafuta picha za ultrasound kuthibitisha kweli alikuwa mjamzito. Phina alitafuta mpaka chini ya godogo, kila mahali, hapakuwa na hizo picha. Akashangaa sana. Akaamua kumtafuta wifi yake Jena angalau azungumze naye na amsaidie kumuunganisha na Jack, naye Jena hakuwa akipatikanika kwa simu. Ikawa kama Jack! Hata jumbe walizowahi kuchati na Jena hakuzikuta.

“Mimi sichanganyikiwi jamani!” Akaongea peke yake. Akaona aingie Istagram ili amtumie ujumbe huko. Napo hakukuta akaunti ya Dr. Jena Msindai. Akafuatilia post na comment zake na Jena. Hazikuwepo! Akazidi kuingiwa na wasiwasi akahisi ni mazingaombwe kweli. Akatamani kumtafuta Ibra, akasita asijue kinachompata yeye na Ibra kilishampata mpaka kuonekana muongo kwa kila alipokwenda kumchafulia Jackson Msindai, kwa kuwa hakuwa na ushahidi!

Ijumaa hiyo ikawa chungu kwa Phina. Amepoteza kazi ya ulaji, halafu uhamisho huko Lindi! “Hakika siendi. Nani akakae kijijini!” Phina akakumbuka shule aliyonayo kichwani, akajiambia hiyo, hakuna wakumnyang’anya. Atabanana nao hapohapo mjini asijue jicho la mzee Msindai lipo naye kuhakikisha anamlipa ubaya kwa kumuanika kila mahali akiwa anasindikizwa na Ibra, kisha Jena! Mzee Msindai alijimbia atahakikisha kila anapoomba kazi hapo mjini, hapati, mpaka alipe ipasavyo.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati Phina akiomboleza kupotelewa na mtoto, Sabrina yeye aliacha wake nyumbani na kutoka na kundi lake. “Sasa hapo unawakilisha jina Msindai vizuri.” “Kweli wifi yangu?” “Mbona ningeshakwambia! Si unanijua mimi?” Angalau Sabrina akacheka. “Na wewe umependeza sana wifi yangu.” “Mwenzio kawaida yangu.” Sabrina alicheka mpaka machozi, Jacinta kimya. “Wifi!” “Wewe sema ni lini umenikuta hovyo.” “Hata siku moja.” Sabrina akamjibu. “Ndio ujue ni maamuzi tu. Sijiweki kihasara hasara mimi! Kwa nini!?” “Nitabadilika wifi yangu.” “Na ubadilike kweli. Mjini hapa, watu hawana kazi ila kuongea ndio ajira yao. Sasa wewe akili kichwani. Ukienda saluni wamekutendeza kitu hakijakaa sawa akili mwako, waambie watoe hapohapo. Usitoke ukiwa unajishuku.” “Wifi!” “Kwani ulikwenda kutengeneza udugu au kutengenezwa upendeze?” “Nipendeze.” Sabrina akajibu na cheko. “Ndio hivyo. Wasikutoe kituko.” Akaja Joy, amependeza haswa. Jacinta akaanza kucheka.

“Mumeo amekuona na hilo gauni?” “Nimetoka hajarudi. Nikaona nijiwahi na gauni langu. Nililinunua gali, lakini nimeshindwa kulivaa.” Joy akalalamika. “Sasa kwa nini hujawahi kulivaa gauni zuri hivyo!?” Sabrina akauliza akiwa haelewi. “Si Junior huyo!” “Mumewe ana wivu yule, usimuone vile. Halafu mkoloni.” Joy akaanza kucheka. “Hataki nivae nguo za kubana, matako na hips vikachorwa hivi! Hataki.” Sabrina akaelewa maana hapo hips zote na tako la Joy vilikuwa vikionekana. “Sasa na wewe Jacinta sio umuite hapa, aje atulipie. Atanikuta na hili gauni, akasirike, usiku wa leo mume wangu alale amenuna.” “Sasa wewe ulilivalia nini kama si kutaka kumuuudhi mumeo?” “Sehemu yenyewe hii ya hadhi wifi yangu. Mtoko wenyewe kama hivi ni mpaka wifi yangu uamue huko kichwani kwake, ndio tunatoka. Nikajiambia acha nipanie.” Stori zikaanza. Akaja na Pendo. Vicheko vikaendelea hapo.

Mara simu ya Junior ikaingia kwa Jacinta. “Huyu ukishatoka na mkewe, kazi yake ndio hii.” Jacinta akaongea na kupokea. “Njoo Mheshiwa Msindai uje ulipe.” “Mimi nilijua tu. Sasa kwa nini unamuita, mwache akapumzike bwana!” “Kapiga mwenyewe. Njoo kaka yangu. Tule na kunywa vya mjini.” Junior akaongezeka. “Mke wangu kapendeza!” Akamsifia. “Asante mpenzi wangu. Pole na kazi.” “Jacinta, mpigie mzee Msindai mwambie naoa upya. Nataka mahari ingine ya Joy!” Joy alicheka mpaka machozi. “Unanioa tena!” “Kabisa.” Jacinta akampigia kweli baba yake.

“Baba mzazi, inatakiwa mahari ingine ya Joy. Junior anataka umsindikize ukweni, ukamuolee tena.” “Joy huyohuyo?” Mzee Msindai akauliza. “Mwambie tena safari hii ajiandae zaidi, maana ashanizalia watoto watatu.” Junior akajibu, Joy hana mbavu. “Mzee Msindai umesikia?” Jacinta akamuuliza baba yake. “Acha nijikusanye tena, mama.” Mzee Msindai akajibu.  “Usikubali mwaya baba yangu. Hawa wawili watakufilisi. Lala baba yangu mzazi. Kesho.” Jacinta akakata simu, Junior akambusu mkewe. “Kama mzee Msindai ameishiwa, mimi mwenyewe nitakulipia tena mahari ingine.” Akambusu tena, safari hii mdomoni kabisa. “Hawa nao wanaboa!” “Acha wivu wifi yangu. Mapenzi kupendwa.” Stori zikaanza, Sabrina hapo akapoa akimwangalia Joy na mumewe. Ungejua tu Junior anampenda mkewe.

Walikaa hapo mpaka usiku mwingi tu, Sabrina mawazo. Bado moyo ulikuwa hauna raha kila akikumbuka yupo Phina na mtoto wake katikati ya ndoa yake. Aliweza kucheka kidogo, lakini wakati wote akili zilimkumbusha Phina. “Hivi ndio itakuaje, jamani! Mtoto akiumwa ndio Jack awe nao mpaka apone!” Hilo swali likaendelea kupita kichwani mwake. Mwishoe akaaga.

~~~~~~~~~~~~~~

 Pendo akamsindikiza mpaka garini. Wakaanzisha kikao kingine. Sabrina akamsimulia kila kitu. “Nimechanganyikiwa dada, sijui chakufanya!” “Bora wewe upo hapo na watoto nyumbani. Mwenzio niliachwa na sikuwa na watoto. Lakini unakumbuka jinsi ulivyonibeba bila kuchoka?” “Sasahivi ndio nakuelewa dada. Ila naona bora wewe ulikuwa angalau unapata muda wa kulia unapunguza uchungu. Mwenzio sipumui sababu ya majukumu ya watoto. Usiku wa jana angalau wifi alinisaidia. Akapanga ile timu yangu, ndio nikaweza kulala mpaka asubuhi. Nimechoka dada! Zaidi nafsi. Sijui itakuaje! Sijui ndio ndoa yangu itachukua sura gani! Hata sielewi! Jack anakuwa baba wa mtoto wa Phina pia. Inamaana anahaki zote za umama kama mimi, na Jackson anatakiwa kuwajibika huko kama huku kwangu! Haya watoto wote wakiugua kwa wakati mmoja, huyo Jack anakwenda kwa yupi na yupi atabaki kupewa pole ya kwenye simu! Sijui itakuaje dada! Nimeazima matatizo yote ya kesho, naishi nayo leo kwa wasiwasi na siwezi kujisaidia.” “Pole Sabrina.” Pendo akaamua na yeye amuazime masikio. Atoe la rohoni kama alivyomfanyia yeye wakati ameachwa na Willy.

“Lakini nashukuru Jacinta amekubali kupokea wanangu. Ameniambia hata nisipokuwepo hapa duniani, jicho lake litakuwa na kwao pia. Hilo limenifariji na kuniondolea hofu.” “Mmmh!” Wakazungumza hapo, Sabrina akaondoka kurudi kwake.

~~~~~~~~~~~~~~

Alifika kwake akamkuta Jack sebuleni, akamsalimia na kupitiliza chumbani kwa Pina na mwenzie. “Nimewaletea kuku choma. Wapo jikoni. Mkitaka mle kesho au…” Wote wakaruka kitandani nusura wamuangushe mlangoni. “Kwani  hamjala usiku, nyinyi!? Mtaniangusha bure mnivunje.” “Kuku wa kuchoma mpaka asubuhi dada na wewe! Kweli?” Pina akajibu akikimbilia jikoni. “Basi mtaamsha watoto wote humu ndani!” “Tunakula kimya kimya.” Akajibu Pina akiwa washafika jikoni na cheko limewajaa wote wawili. “Mfuko huo mwingine sio wenu. Chakula cha baba.” Jack akasikia ila akashangaa yeye hajakaribishwa. Akatulia tu.

‘Harusi ya kesho ni ya familia nzima. Na bado sijapata majibu ya vipimo vyako.’ Ujumbe kutoka kwa baba yake ukaingia. Jack akajua ndio anatakiwa kwenda na Sabrina. Akatulia akijua baba yake anasubiria majibu. ‘Kwa kuwa bado sijaenda kupima, baba. Nitaenda kesho asubuhi.’ Jack akarudisha hayo majibu. Kimya. Akajua ameyapata. Na lazima kesho aende kupima. Akabaki ametulia kochini akifikiria.

Wema Hauozi.

S

abrina akaenda chumbani akatoka akiwa ameoga. “Nilileta samaki wakuchoma kama vile unavyopenda na ndizi za kuchoma pia. Unataka kula sasahivi au uwekewe utakula kesho?” “Asante kujali. Lakini naona nile tu kesho. Usiku umeshakuwa mwingi.” Sabrina akaenda kuweka kwenye friji na kurudi chumbani kwa watoto. Akataka kumuamsha Brandon anyonye lakini akaona amuache tu. Maziwa yalishaanza kujaa tena. Hakuwa amenyonyesha kwa msaa mengi. Akachukua vifaa vyake vya kukamulia, akahamia hapohapo chumbani kwa wanae akaanza kukamua.

 Jack akamfuata. Alipoingia tu, akajifunika kwa haraka. “Kumbe maziwa yameanza kutoka!” “Ndiyo.” Sabrina akajibu nakurudisha mawazo kwenye kukamua huku amejifunika. Akashangaa Jack haondoki. “Wewe nenda tu kalale chumbani. Mimi nitalala hapahapa ili akiamka usiku, nimuwahi kujaribu kumnyonyesha kabla Pina hajampa maziwa mengine. Nataka aendelee na maziwa yangu. Kwa hiyo nenda tu kalale kitandani, mimi nitakuwa hapa. Usilale kwenye makochi. Si sawa.” Jack akaenda kukaa pale pembeni yake.    

“Sabrina!” Akajaribu kuita. “Wakati ule tupo chuoni, na ulipokuwa Moshi nilipokufuata, yale maneno uliyoniambia, hayakuwa yakileta maana mpaka sasahivi!” Sabrina akamwangalia na kukunja uso. “Nimeingiwa na hofu, Brina! Sina jinsi nikakwambia ukaelewa. Nina wakati mbaya ambao sijawahi ishi kabla. Najisikia fedheha nashindwa hata kuangalia ndugu zangu usoni. Nimeingiza kila mtu kwenye shida, Brina. Nimepatwa na ile hali kama wewe. Moyo unapasuka kila wakati kama kumeangushwa chuma!” Sabrina akatulia, akajua ndio anamkumbusha jinsi yeye alivyokuwa akimbeba kwenye shida.

“Nimekwama Brina. Sijui nifanyaje! Dhambi yangu inanililia, nashindwa kutulia.” Jack akatulia kidogo, Sabrina na yeye akatulia. “Najua kwa swala la mume kwa sasa itakua ngumu, lakini naomba turudi kuwa marafiki wakubebana!” “Kwa hiyo leo ndio umekuja kudai fadhila zako?” “Hapana Brina. Hata kidogo. Lakini nipo pabaya! Halafu mbaya zaidi sina mtu. Nipo kama hivi.” “Na Phina?” “Sina mawasiliano naye na sidhani kama tutakuja kuwasiliana tena.” “Mpaka ajifungue?” Sabrina akamuuliza kwa wivu.

“Baba ametoka kunitaarifu kuwa ile mimba iliharibika leo.” Sabrina alishituka nusura amwage maziwa yote. “Ni nini kilitokea!?” “Hata sijui! Ila baba ananiambi alionekana hospitalini leo asubuhi akilia anaumwa na tumbo, na kuanza siku zake. Basi.” “Poleni sana.” Sabrina akajikuta akitoa pole bila hila. Jack akanyamaza. Wakatulia kila mtu akiwaza lake, Sabrina akakumbuka alikuwa akikamua, akaendelea mpaka akamaliza bado Jack yupo hapohapo.

“Nenda kalale Jackson. Najua upo kwenye maumivu ya kufiwa na mtoto wenu, lakini nenda kajaribu kupumzika. Tena kitandani kabisa, sio kwenye makochi. Itakusaidia. Ile usiku wa jana mimi kulala vile angalau imenisaidia kidogo. Kajaribu kupumzika pengine kesho utaamka na akili ya kujua nini mfanye.” “Hakuna maisha kati yangu na Phina. Tafadhali naomba uamini hatukuwa tumepanga kukutana.” “Si umesema ni bahati mbaya wewe!? Ndio hiyohiyo bahati mbaya imewakutanisha tena huko Uswiz mpaka na mtoto juu! Sasa unakataa nini?” “Sasa sasahivi nimtafute tena wa nini? Sikuwa nataka mahusiano na Phina, Sabrina. Naomba nisamehe. Ilitokea…” “Kwa bahati mbaya.” “Basi mama. Kama umekataa kunisaidia na mimi, basi Brina. Acha mimi niendelea kulipa garama ya makosa yangu. Ila ingekuwa mimi nisingekuacha Brina. Japokuwa unakuwa umeniumiza, lakini huwa sitaki uwe peke yako matatizoni.” Sabrina kimya. Jack akanyanyuka, na kutoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Sabrina akakaa pale akaanza kuumwa na dhamira. Akakumbuka Jackson alivyombeba wakiwa chuoni. Japokuwa alimuabisha, lakini akaweka tofauti zao pembeni akamsaidia. Akakumbuka na kutulia. Kumbukumbu zikamjia jinsi alivyokuwa ameishiwa chuoni, Jack huyohuyo akawa akihangaika naye mpaka kula yake. Akapoa. Kumbukumbu ikamrudisha alipokuwa Moshi. Ile hofu aliyokuwa nayo mpaka Jack akaenda kumchukua na kumsamehe akiwa mjamzito! Akatulia.

Mungu akamrudishia ile furaha aliyokuwa nayo na kushindwa kuamini Jack kumuoa na ujauzito! Jinsi alivyombeba na tumbo lake. Heshima aliyompa kwenye jamii kwa kumchumbia kwa heshima na ujauzito wake. Ikaja harusi ya kifahari! Na Jack kubaki naye hospitalini baada ya ndugu zake kuona amejifungua watoto wa kizungu. Sabrina akatulia kidogo. Hasira zikaanza kushuka.

~~~~~~~~~~~~~~

Akatoka, akakuta taa ya sebuleni imezimwa, akajua Jack amefuata ushauri wake. Ameenda kulala chumbani. Akajishauri hapo! Ingekuwa sio kukumbushwa fadhila, angelala chumbani kwa watoto. Lakini usiku huo Jack amerudi kukusanya malipo ya wema wake. Baada ya muda Jack akamsikia ameingia hapo chumbani. Akajizungusha hapo wee, Jack kimya akitaka kujua mwisho wake, ila akajua anajishauri. Akaingia chooni. Akamsikia anaoga tena, wakati alishaoga. Akatulia kabisa, wala hakulala ili amuone. Akatoka hapo akamuona anapaka lotion, hamalizi. Jack kimya wala hakumsemesha.

~~~~~~~~~~~~~~

Alichokiunganisha Mungu, Mwanadamu Asikitenganishe. 

Inaendelea..

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment