Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 65. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 65.

Tino hakulazia damu bahati yake. Mida ya saa nne, akaenda sehemu karibu nanyumbani kwa Sabrina, Sabrina akampelekea watoto. “Tafadhali wakilia tu, uwarudishe. Halafu usihangaike chakula sasahivi. Wameshakula. Subiria mpaka baada ya masaa matatu watakuwa na njaa, chochote utakachowapa watakula.” “Sawa. Utawataka saa ngapi?” “Utakapokuwa tayari kuwarudisha.” “Hata usiku?” “Ila isizidi saa mbili, ili walale kwa muda wao waliozoea.” “Nakushukuru. Na nitakuwa mwangalifu.” “Hilo ndilo la msingi.” Tino akahamishia watoto kwenye gari yake, akawafunga vizuri.” “Naona mpaka umenunua car seats zao!” “Sikutaka vipingamizi vidogovidogo.” Sabrina akaaga wanae, akaondoka kurudi nyumbani.

Hilo juma zima, Tino alikuwa akifanya hivyohivyo. Anakuja kuwachukua asubuhi, na kuwarudisha usiku wakiwa wameshalishwa na kubadilishwa nguo. “Unavyojitahidi! Unawarudisha wasafi!” “Ungemuonea huruma anti. Kuanzia nawapikia, nawasaidia kula na kuwaogesha nakuwa naye kwenye video akinipa maelekezo. Mpaka kuzibrashi nywele zao vizuri na kuzifunga hivyo ni yeye.” Sabrina akaangalia wanae na kucheka. “Ila leo nimefanya mwenyewe bila msaada wake.” “Sawa. acha wakapumzike.” Sabrina akaondoka.

Siku Ya Sita.

T

okea waachane na shemeji yake siku ile nyumbani kwao, siku hiyo akaona simu ya shemeji yake inaingia. Akaiangalia kwa muda akijishauri kama apokee au la, karibia ikatike akapokea. “Unaendeleaje na watoto Shem?” “Tunaendelea vizuri, namshukuru Mungu.” Sabrina akajibu lakini Junior alisikia sio sauti aliyoizoea. Na yeye akaona ayafanye marefu kuwa mafupi. “Sasa sitachukua muda wako mrefu. Mimi ni mjumbe tu, baba ameitisha kikao kingine nyumbani. Leo usiku saa mbili. Ameomba nikufikishie ujumbe.” “Mimi sidhani kama nitaweza kuhudhuria shem. Naona mimi inatosha. Nyinyi endeleeni tu.” “Naomba usikatae wito shem. Waswahili wanasema kataa maneno.” “Hayo maneno machungu ya huko kwenu ndio ninayokataa, shem. Naishia kudhalilishwa bila sababu shemeji yangu. Acha tu nikae pembeni. Mama Msindai hatazungumza lugha ingine nikaja kuelewa zaidi ya msisitizo kuwa amenikataa. Na naona na kijana wake ndio kama hivyo. Jack ameanzisha familia inayotambulika na kukubaliwa na mama yenu. Mimi nakuja huko kama nani?” Sabrina akaongea taratibu tu.

“Ingekuwa ni wakati ule Jack ni mume wangu, hapo sawa ningesema navumilia sababu ya mume wangu. Lakini…” “Bado Jack ni mume wako. Mlioana ndoa takatifu ya kanisani.” “Kanisani kule ni ndoa ya mke mmoja, mume mmoja. Siwezi ndoa za mitala, shem. Nina watoto wadogo sana. Sasahivi nikijiingiza kwenye mapenzi ya kitajiri hayo anayoanzisha Jack huko, hatujui huko kwa wapenzi wao wengine na wao wanaishije! Mwanamke anayekubali kulala na mwanaume bila kinga, si inamaana analala na wengine hivyohivyo bila kinga!” Sabrina akaendelea taratibu tu.

“Shem, Jack aliniacha hapa nina homa kali, inapanda haishuki. Natetemeka baridi, nimeharibikiwa kidonda cha mshono wakujifungua, ameniachia watoto wadogo, anakwenda kulala nje bila shida! Halafu akaficha. Alishindwa hata kukiri mpaka Phina alipojitokeza, inamaana hiyo ndio tabia yake. Mwanamke wake asingejitokeza, hakuna ambaye angejua, na angeendeleza tabia yake hiyo anayotaka kuaminisha watu ni bahati mbaya. Hizo bahati mbaya zingeendelea tu kutokea mpaka mnakuja kushitukia tunakufa kwa maradhi! Hapana shem. Nilimpenda Jack, lakini si kwa kuja kuniua. Hata bibilia inaniunga mkono, jamani! Kosa la uzinzi! Hilo naruhusiwa kutoka kwenye hii ndoa.”

“Halafu mama yake hanitaki mimi na watoto niliozaa! Wanatangaza kumpokea Phina na mtoto wake mpaka huko mitandaoni, mimi wamenikataa kabisa! Nimegeuka mimi kichekesho! Wamechagua kuniumiza bila sababu, shem! Hapana shemeji yangu. Acha itoshe hivyo. Kwa nini niendelee kujitesa jamani! Acha tu Jack aendelee na maisha yake yenye mafanikio na mwanamke wake. Mimi inatosha.” Junior kimya akisikiliza.

“Hata hivyo, mwambie baba, sisi kesho tunakwenda Singida. Najiandaa usiku wa leo kwa safari ya kesho na watoto.” “Kwema?” “Nahisi kutakuwa kwema mimi mwenyewe nikienda huko. Ni mambo ya biashara tu.” “Mimi nimekusikia Sabrina. Pole sana.” “Nashukuru shem. Muwe na usiku mwema.” Junior akajua ndio anaambiwa anakata simu. “Basi nitamfikishia baba ujumbe. Uwe na safari njema kesho.” “Nashukuru.” Sabrina akakata simu.

Mzee Msindai!

Sabrina akiwa chumbani kwake, akasikia sauti ya mzee Msindai akizungumza na watoto sebuleni kwake. Alishituka karibu aruke kitandani. Akaangalia saa ya ukutani, akagundua ni saa tatu usiku. Akavaa kwa haraka na  kutoka. “Karibu baba.” “Asante. Vipi unaendeleaje?” “Tunaendelea vizuri kabisa. Wote hatujambo. Ila kesho alfajiri tunasafiri.” “Nimeona masanduku yapo mpaka mlangoni!” Sabrina akanyamaza. “Mwambie dada achukue watoto tuzungumze.” Phina akakusanya jeshi lote la Sabrina akawapeleka chumbani, Sabrina mapigo ya moyo yakienda kasi. Amefuatwa na mzee Msindai!

Akakaa kochi la pembeni ya mkwe wake. “Junior alikupigia simu kukwambia kuna kikao. Tumekusanyika pale nyumbani, hukutokea, ndio maana nimekuja mimi.” “Samahani baba. Ila nilimwambia shemeji sitaweza kufika.”  “Ndio maana nipo hapa.” Sabrina akatulia macho chini. “Siku ile ya kutolewa mahari yako nyumbani kwenu, unakumbuka kuniona mimi?” “Nakumbuka baba.” Sabrina akaanza kulia na hofu. “Unakumbuka maneno niliyosema?” Sabrina akaanza kufikiria. “Nilisema nimekuja kuoa kule kwenu. Nilimuolea Jackson mke. Ile mahari ni jasho langu mimi wala si Jackson. Niliwasindikiza mpaka kanisani. Nikaona baraka mlizopewa kama mke na mume. Leo unapoitwa mama Msindai, si kwa kukubali kwa Jack. Ni kwa kuwa mimi nilishakuchunguza hata kabla Jackson hajakutamka nyumbani.” Sabrina akashangaa kidogo.

“Siwezi nikakubali kila mtu akaitwa Msindai. Lasivyo kungekuwa na Msindai wengi tu. Lakini wanaotokana na Msindai mimi, MIMI mwenyewe ndiye ninayechagua. Ndio maana niliposikia habari za Tino akisumbua, sikutaka kuwa nikipewa taarifa, mimi mwenyewe nilikuwa mstari wa mbele, ili utulie na ubaki umetulia kama mama Msindai.” Sabrina kimya.

“Kwa umri wangu huu, mpaka sasa, sijawahi kuita mtu, akakataa wito wangu kwa sababu mimi kama mimi huwa sitoi sababu ya mtu kunikatalia jambo. Unanielewa Sabrina?” Mikono ikaanza kumtetemeka Sabrina akifuta machozi. “Samahani sana baba.” “Basi. Kila mtu yupo nyumbani, nimewaambia mtu asiondoke, na kikao hakitaanza, mpaka wewe uwepo.” “Tunaweza kwenda sasahivi. Ila naomba nibebe huyu mtoto mdogo kwa kuwa sina maziwa. Na siwezi kukamua, maziwa yananikauka.” Sabrina akaongea kwa sauti ya chini. Basi mbebe na Pina, ili akusaidie kumshika wakati wamazungumzo. Nitakutaka wewe pale muda wote.” “Sawa baba. Na samahani sana.” “Hilo limekwisha. Na leo mimi ndio nitakuwa dereva wako.” Sabrina akacheka kwa wasiwasi na kwenda kukusanya vitu na kubeba mtoto wake na Pina. Wakatoka.

Jungu Kubwa, Na Ukoko Wake.

S

abrina alifika hapo akakuta pako kimya. Kila mtu yupo mpaka Jack! “Lete nikupokee mtoto.” Jack akamuwahi alipoingia na mwanae mkononi. “Acha nikamlaze maana akiamka hapa, atataka maziwa na mimi sina, ndio nimetoka kumnyonyesha, ameyamaliza yote mpaka yajae tena, itachukua muda ndio maana nataka tusimsumbue, akiamka akutane na maziwa.” “Umekonda sana Sabrina! Unakula wewe?” “Nakula wifi yangu.” “Mmmh! Huo mwili hauwezi kutoa maziwa. Umekauka sana. Kazana kula, au sasa mwanzishie huyo maziwa mengine.” “Mwanangu bado mdogo wifi. Najitahidi naye hivyohivyo nimsogeze kidogo.” Sabrina akajifuta machozi. “Basi hataacha kukulia. Ni aidha wewe ubadilike, uanze kutoa maziwa, au umuanzishie maziwa. Huna jinsi ingine.” Sabrina akamwangalia mwanae vile alivyolala.

“Naomba nikamlaze hapo chumbani kwa dada, nakuja sasahivi.” “Kwa nini ukamlaze huko na vyumba vimejaa hapa ndani!” Mzee Msindai mwenyewe akamuita msichana wa kazi na kumtaka amwandalie huyo mtoto chumba. Sabrina akashukuru na kumfuata msichana wa kazi. Kimya. Mama Msindai kama hayupo hapo.

Baada ya muda Sabrina akarudi na kwenda kukaa pembeni ya Jacinta. “Samahani kuwaweka muda mrefu.” “Usijali. Hiki kikao ililazimu uwepo hapa ndio maana unaona mpaka Joy yupo hapa.” Akaanza Mzee Msindai.

Wamjua Msindai Mwenyewe.

“Wote mliokaa hapa ndani, ni kina Mzindai kwa kuwa MIMI Msindai niliruhusu muwe kina Msindai.” Mama Msindai akamwangalia na nyusi akapandisha juu. “Wengine kwa kuolewa na wengine  kwa kuzaliwa. Jinsi nilivyoenda kukuposa wewe Sabrina, ndivyo nilivyofanya hivyohivyo kwa Joyce. Na Joy amefanyika binti yangu tokea siku ile, na ndivyo ilivyo hata kwako wewe Sabrina. Kitu ambacho nyinyi hamjui, nilimjua Sabrina na kumchunguza hata kabla Jackson hajaja kumtambulisha hapa nyumbani.” Wote wakamtizama.

“Ilikuwa hivyohivyo kwa Joy. Na ninafanya makusudi kabisa kwa sababu sitaki aina nyingine za Msindai kwenye hii familia isipokuwa nyinyi. Jackson na Junior mnanielewa?” Wote wakaitika kuwa wameelewa.

 “Jena!” Jacinta akafurahi sana akajua usiku huo atakipata. “HURUHUSIWI. Huna ruhusa, wala mamlaka yakukaribisha mtu yeyote kwenye hii familia bila idhini yangu. Unanielewa?” Kimya. “Jena?” Akamuita kwa ukali. “Wewe ni Jena Msindai mpaka sasa kwa kuchagua kwako vinginevyo ungekuwa mtu mwingine kwenye familia ingine. Acha ndoa za kaka zako.” “Msindai..” “Ninaongea mama J. Tafadhali nisiingiliwe.” Jacinta akatamani kupiga vigelegele.

“Kitendo cha kuwa mtandaoni, ukimkaribisha Phina kwenye hii familia, bila idhini yangu, UMEKOSA sana. Umeingiza hii familia aibu na wote sisi umetufanya tuonekane tumekubaliana na maisha ya kinyama aliyoamua kuishi Jackson.” Jack akainama. “Hata Jackson mwenyewe, HARUHUSIWI kukaribisha mtoto yeyote kwenye familia yangu, kama hajatokana na Sabrina, tena ndani ya ndoa yako. Mtoto yeyote utakayezaa nje ya Sabrina, niliyekwenda mimi kukuolea, tafuta jina na ukoo wakumtambulisha, lakini kwa Msindai mimi, NIMEMKATAA. Unanisikia Jackson?” “Ndiyo baba.” “Unanisikia Jena?” Kimya.

“Katika hili sina utani Jena. Nataka nikusikie. Kama hutanisikia, nitakutaka uondoke hapa ndani, wewe si mmoja wa Msindai anayetokana na mimi.” “Msindai unakwenda mbali.” “Hujanielewa mama J. Mimi ndiye Msindai, nachagua nani anaingia kwenye hii familia na si vinginevyo. Anayeshindwa, anaruhusiwa kuondoka, ila ujue Jena, nitakupokonya majina yangu yote. Ukitoka kwenye huo mlango bila kunitii, ujue huna cheti hata chakuzaliwa chenye jina la Jena Msindai.” “Msindai!” Mama Msindai akashangaa sana. “Kama huamini, mwambie Jena atoke kwenye huo mlango sasahivi. Nimenyamaza lakini naona mnataka kuharibia kila mtu!” Mzee Msindai akaendelea kugomba.

“Wewe Jena hujui hata maisha ya ndoa ni nini, upo mitandaoni unashangilia uchafu huo?” “Na nilimuonya. Muulize mama, mpaka mimi nikampiga hapa. Nikamwambia aache kumuadhibu mke wangu kwa makosa yangu. Sasa mimi namjua Jena. Alichokifanya mtandaoni, ni kunikomoa mimi, makusudi tu.” “Umedhalilisha familia nzima! Simama Jena.” Baba yake akarudia, safari hii kwa amri zaidi mpaka Jena akasimama. “Umenielewa au unaondoka?” “Nimeelewa.” Jena akajibu.

Jena akaanza kusomewa hukumu yake. “Kuanzia leo, huruhusiwi kuwa na akaunti yeyote ile ya social media. Na akaunti uliyokuwa nayo Istagram imefungwa. Huruhusiwi kuchangia chochote mitandaoni.” “Baba J, hapo umezidisha.” “Hakika katika hili sina utani na sitabadilika. Akishindwa yupo huru akawe kingine lakini si mmoja wetu. Siku atakapomtangaza mwanamke mwingine yeyote, popote pale, bila idhini yangu, mbali na Joyce na Sabrina, nitakuadhibu vibaya sana.” Jacinta alitamani asimame ashangilie.

“Labda uwe kwa jina jingine si Msindai. Umenielewa Jena?” “Ndiyo.” “Na uwe na adabu kwa wake za Msindai, sisi wote sasahivi tunaonekana ni wanaume tusiojua majukumu! Yaani sisi wanaume watatu hapa ndio tumegeuka gumzo huko mitandaoni! Hapana Jena. Usiwahi kurudia. Ukiona wifi zako wapo sehemu ambayo huwezi kuwa nao pamoja, usifike. Na wewe hatutakulazimisha ufike. Natangaza ramsi, leo tunakuruhusu kutokuwepo katikati yetu. Ukijisikia kuja, basi uje na adabu zako zote. Ukishindwa, usifike. Kaa kwako. Unanielewa Jena?” “Ndiyo.” “Rudi kukaa.” Akakaa.

Mzee Msindai akaendelea. “Swala la watoto.” Jacinta akamtizama Junior. Junior kimya japo alimuona dada yake. “Narudia tena. Mtoto yeyote, aliyezaliwa ndani ya ndoa ya Msindai, ni Msindai. Awe wa kijani, bluu, njano, rangi yeyote ile ni Msindai. Unanielewa Sabrina?” Wakajua zamu yake na yeye imefika.

“Ndiyo baba.” “Watoto uliozaa ndani ya ndoa ukiwa Msindai, mimi nikalipa mahari kwa jasho langu bila kusaidiwa na mtu hata shilingi, watabakia Msindai. Hilo hata Tino nimemwambia.” Sabrina alishituka mpaka mate yakapita kwenye njia ya hewa. Akapaliwa na kuanza kukohoa mfululizo. Jacinta akaenda kumletea maji. Akanywa wakimsubiria mpaka akatulia. “Pole.” Jack akarushia pole yake. “Asante.” “Nimezungumza naye na nimemuonya vikali sana. Nimemwambia, siku atakayothubutu kuwabadilisha wajukuu zangu majina, hata kwa kuongeza herufi yake kwenye majina yao, nimemwambia nitamuadhibu vibaya sana. Na nikamwambia hakuna atakapojificha akataja jina la Msindai hata kwa kunong’ona, nisisikie kama alivyofanya leo. Popote hilo jina linapotajwa kwa hila, linagusa antena zangu, na ninasikia.” Sabrina kimya.

“Unanielewa Sabrina?” “Ndiyo baba.” “Jamani, msichanganywe na rangi ya wale watoto. Hata Tino nimemwambia hili. Wale watoto nilibeba mimi mwenyewe wakiwa hata hawajafikisha masaa 24 hapa duniani! Niliwabeba mimi kwa mikono yangu, nikawakaribisha kwenye hii familia. Hakuna atakayenipokonya.” Sabrina akaanza kulia tena taratibu.

“Kama alivyo mrithi Claire kwenye hii familia, ndivyo alivyo Jeiline na Keiline. Na Tino nimemwambia. Atakachorithi mtoto wa Joyce kutoka kwenye mali zangu, ndicho atakachorithi mtoto wa Sabrina. Hiyo nawaambia mimi nikiwa hai. Unanisikia Junior.” “Ndiyo baba.” “Jeiline na Keiline, hawatabadilishwa majina yao ya mwisho, hata kwa idhini ya Sabrina mama yao mwenyewe, mpaka watakapoolewa, au watakapofika umri wa kuwa wakubwa, wakaamua wenyewe. Hapo hatutakuwa na upinzani. Lakini si sasahivi. Ni kina Msindai. Unanisikia Junior?” “Ndiyo baba.”

“Yanayoendelea mkiwa hapa, ndani ya nyumba hii, sina mamlaka nayo kwa kuwa ni kwa mama yenu. Lakini haibadilishi uhalisia wa mambo.” Jacinta akajua zamu ya mama yao lakini yeye anaambiwa kiutuuzima. “Wote mliokuwepo hapa ni kina Msindai. Na kina Msindai, tuna nia mamoja. Tunaweza kuwa na mapungufu yetu, lakini linapofika swala la kupigana nje, tunasimama pamoja mpaka Jackson alipoleta utaratibu wake mwingine.” Wakajua zamu ya Jack.

Nimemuonya, na ninarudia kumuonya. Maisha anayotaka kuyaishi nikiwa hai, hataruhusiwa kuyaishi. Unanisikia Jackson?” “Nimeelewa baba.” “Uelewe na usiwahi kusahau. Labda na wewe ubadilishe, usiwe Msindai. Nitakufuta kila mahali na hutakaa ukawa hata na cheti cha darasa la saba. Mpaka chakuzaliwa nitachukua, kwa kuwa ni mali yangu. Itabidi uanze upya, ukiwa na jina jingine. Kuanzia leo.” Hukumu yake ikaanza. “Utapewa namba mpya ambayo kwa muda mpaka mambo yatakapokuwa sawa, hutampa mtu mwingine yeyote zaidi marafiki zako. Itabakia nyumbani na kazini. Ujue itakuwa ikifuatiliwa. Safari za kikazi ambazo si lazima wewe uende, tutakuombea ruhusa ubaki ukifanya majuku yako hapahapa nchini, kwa muda mpaka mambo yako yakae sawa. Rudi nyumbani baada ya kazi. Unanielewa Jackson?” “Ndiyo baba.” Jackson akaitika kwa haraka kwa unyenyekevu.

 “Kwa wengine wote, nimeeleweka?” “Tunaruhusiwa maswali?” Akauliza mama Msindai. “Kwa nini hili langu halijajibiwa kwanza?” Kila mtu akamshangaa mzee Msindai. Alimbadilikia kila mtu mpaka mkewe. “Eeeh! Msindai vipi leo!?” “Nauliza, katika niliyozungumza mimi, nimeeleweka?” Akaweka msisitizo. “Mimi nimeelewa baba.” Jacinta akajibu. “Na mimi nimeelewa baba, na naomba msamaha. Naahidi nitaongeza umakini.” Akaongea Sabrina na machozi kibao. “Hilo ndilo nilitaka kulisikia kutoka kwako. Jua unalea watoto uliozaa wewe, lakini si wako peke yako. Huwezi kufanya kile unachotaka! Hapana Sabrina.” “Nimeelewa baba.” “Kama ni hivyo nashukuru.”

“Na mimi nimekuelewa baba. Kina Msindai wengine tutakao pokea kwenye hii familia ni kutoka kwa kina CJ, Cleiton, Brayan na Brandon.” “Naona hapo nimeacha maagizo yangu sehemu sahihi. Na ibaki hivyo.” “Sawa baba.” Junior akaitika. “Mmmh!” Mama Msindai akasikika akiguna. Hakuna aliyemwangalia.

“Namalizia juu ya Phina.” Mzee Msindai akaendelea na hukumu ya Phina. Kila mtu akataka kujua. “Jackson na wengine wote. Mimi nikiwa hai na nikiwa nimekufa, Phina haruhusiwi kukanyaga hapa.” “Heee!” Mama Msindai akashituka sana. “Hana adabu. Hana maadili, hawezi kuwa mmoja wetu. Ni mwizi asiye na aibu. Ameitia familia yangu aibu na kunifedhehesha vibaya sana. Amenichafua kila mahali na yupo mtandaoni akijisifia uovu wake kwa ndoa ya mwenzie! Sitamtaka hapa kwangu na popote nilipo mimi. Siku nitakayokusikia umerudi kulala na yule mwanamke, usiwahi kurudi hapa Jackson. Nitakuweka mbali kama nitakavyomuweka mbali Phina.” Hapo kila mtu akaingiwa hofu. Nitahakikisha hakuna atakayemsikia tena. Kama vile jina la Msindai lilivyomuinua juu, ndivyo litakavyomshusha chini. Unanielewa Jackson?”

“Nimeelewa baba na naomba msamaha kwako na wote. Najua nimewaingiza aibu na kuifikisha familia hapa tulipo. Nimekosa baba. Naahidi haitakaa ikatokea tena.” Kimya. “Nimekosa baba. Najutia kosa langu, ni hivyo siwezi kurudisha siku nyuma nikarekebisha. Nimekosa baba yangu. Sio kitu hata kilikuwa kichwani kwangu kwamba nilikuwa nikipanga. Hata na mimi sijui ilikuwaje, naahidi kuongeza…” Brandon akaanza kulia kwa ukali. Akalia tena na tena mpaka baba yake akashindwa kuzungumza. “Baba, naomba mimi nikamchukue.” “Sabrina, huyo mtoto hashibi. Kilio hicho si chakutoka usingizini. Mtoto huyo ananjaa. Unanisikia?” Jacinta akamuuliza kwa msisitizo.

“Najitahidi kunyonyesha.” “Sidhani kama kwa sasa unamaziwa yakumtosha huyo mtoto. Lazima kumuongezea chakula wakati wewe ukirudisha mwili. Au ukubali tu kuwa alivyonyonya Brayan si Brandon, basi aanze kupewa maziwa mengine. Au baba wewe unasemaje?” Jacinta akamuuliza baba yake kama mtaalamu wa watoto. “Kwa hivyo alivyo mpaka aje arudishe maziwa yakumshibisha huyo mtoto, itakuwa muda mrefu na mtoto ataendelea kuteseka. Nenda kamtulize kwanza.” Sabrina akaenda.

“Ona ulipomfikisha mkeo! Sabrina alipendeza na mwenyewe anaasili ya maziwa mengi kwa wanae. Uchafu wako unatesa mpaka watoto wako! Wewe unaacha mkeo anakuwa kichekesho mitandaoni kwa kushindwa kuwa mwanaume kama Junior! Mchafu, unalala hovyo, unajaza wanawake wajawazito mitandaoni!” “Huyu mtoto ameomba msamaha jamani!” “Hapana mama. Acha kumtetea Jackson. Amekosa SANA. Na kama si baba kutaka kuzungumza leo hapa na Jena, hakika nilipanga kumfuata nyumbani kwake nikazungumze naye.” Junior akaendelea. “Jena, angalia maneno ya kinywa chako tafadhali. Acha chuki kwa wake zetu. Hawaishi na wewe, ni nini kinakusumbua wewe?” “Kwani..” “Ukinijibu tu, leo mimi nitakupiga.” Mpaka Joy akashituka. Junior alibadilika kama baba yake.

“Umekosa adabu kabisa wewe! Unatangaza mtoto wa uzinzi mitandaoni wakati wewe umeshindwa hata kutunza mwanaume hata mmoja?” Jena akaanza kulia. “Junior unapitiliza!” “Hapana mama. Huyu ndiye amefikisha familia hapa. Amemtia hofu Sabrina, mpaka akaanza kuwatafutia watoto wake baba, akihangaika usiku magerezani!” “Mbona hamumsemi mama yeye aliyesema huyo mtoto anatakiwa kutambuliwa hapa na akaribishwe kama Msindai?” “Jena acha mdomo wewe.” “Mimi nilifanya kutokana na alivyosema mama. Nikamtafuta Phina na kuzungumza naye kutokana na alivyosema mama, lakini sasahivi mimi ndio naonekana mbaya.” “Mbaya sana wewe Jena.” Jack na Jacinta wakamchangia.

“Mnafiki tu. Ulienda kumtafuta Phina ukitaka kunilipiza kisasi sababu nilikupiga.” “Mbali ya hivyo, amekakaa tu kuvunja ndoa za  wenzie! Mdomomdomo tu.” “Mdomomdomo gani na wewe Jacinta kama si..” “Sasa leo umeonywa. Na UBADILIKE. Badilika kabisa, wake za wenzio wapumzike. Tukienda kuoa majumbani kwao tunakuwa wema, wakishaingia tu humu ndani ndio tunageuka mwiba! Acheni watoto wawatu watulie makwao jamani! Acha kuunganisha waume zao na wanawake wengine. Junior kashamuoa Joy, mwach...” “Kwani mimi nimemuunganisha Junior na nani?” “Jack! Jack ndiye anayekuuma mpaka unashangaza hata mashoga zako! Acha kujidhalilisha Jena. Wewe mtu mzima, tulia. Ni hilo tu mimi nilitaka kukwambia. Kakae ufikiri.” “Sina muda wa kipuuzi.” “Hakika nakushauri utulie na utafakari Jena. Umevuka mpaka ambao huna nafasi nyingine ya kukosea.” Baba yake akaweka msisitizo, wakanyamaza.

Sabrina akatoka na mtoto. “Vipi?” “Kweli naona nikamuanzishie tu maziwa mengine. Hajapata kitu, amejibembeleza tu na nyonyo amelala, hana muda mrefu ataamka tena.” “Hapa sisi tumemaliza mama. Naweza kukurudisha nyumbani.” “Naona nitakusumbua baba. Acha nimuombe mnyonge wangu.” Jacinta akacheka na kutingisha kichwa. “Mimi naweza kurudi nao nyumbani.” “Nataka kuzungumza na wifi. Wewe endelea tu na ratiba zako.” Sabrina akamkatalia mumewe. “Nisindikize wifi yangu najua na wewe natakiwa kukupa maelezo.” “Haya twende.” “Pina beba vitu turudi nyumbani.” Akatulia kidogo, kisha akasema.

“Mimi nashukuru kwa kila kitu. Asante baba. Asante kunisamehe. Ila nilitaka kuwaaga rasmi. Sisi kesho asubuhi  tunaondoka, tunarudi Singida. Tutakuwa huko nikiendelea kufanya biashara zangu. Hapa mjini naona sitapaweza.” Wote kimya. Sabrina akamgeukia mzee Msindai. “Naomba kukuuliza swali baba yangu.” “Karibu.” “Naomba iwe hapo nje.” Mzee Msindai akasimama wakati anataka kutoka, mkewe akaanza kulalamika macho kwenye simu.

Na mama Msindai hakuachwa salama. “Mbona simu zangu zote hazifanyi kazi!?” “Eneo zima la kuzunguka huu uzio, hapatakuwa na mawasiliano ya simu pamoja na internet.” “HAPANA Msindai! Haiwezekani uniadhibu mimi kama mtoto mdogo!” “Kwa hiyo hakuna simu itakayoweza kufanya kazi mara unapoingia pale getini, isipokuwa yangu na Jacinta tu kama na yeye atatumia ya kazini.” Akamalizia mzee Msindai. “Hakika huwezi kunifanyia hivyo.” “Nashauri utulie mpaka nitakaporekebisha hii hali. Kila mahali kumechafuka. Hatuwezi kuzuia haya madhara kama wote humu ndani tukiwa wasemaji. Naomba mpaka nitakaporekebisha madhara aliyoyasababisha Jackson, mimi peke yangu ndio nibakie msemaji wa hii familia. Na Junior, endapo nitamtuma mimi.”

“Unanivunjia heshima Msindai!” “Ukitulia, utakuja kugundua nipo kwenye kutengeneza, na simu zako na marafiki zako zinanishika miguu. Kwa kuwa wapo kukuchota maneno na kuyasambaza.” “Hapana Msindai! Mimi ni mtu mzima, najua nini chakuzungumza na nini chakuto….” “Unakumbuka majibu yako ya kwanza kabisa kwenye simu ya mtu aliyekupigia kukutaarifu habari za mwanao huyo, alizozisikia kutoka kwa Ibra na Phina huko Ustawi wa Jamii?” Mama Msindai akatulia kidogo akijaribu kuvuta kumbukumbu. Wote kimya.

“Mwanamke wa kwanza kabisa aliyekupigia simu akikwambia anataka kukusaidia kama mzazi akitaka kuzuia mambo yasiende mbali. Unamkumbuka?” “Mbona nilimjibu vizuri tu!?” “Kama ulimjibu vizuri ni kwa nini mama Mkapa na yeye alikupigia akikushauri mmalize mambo kinyumbani? Hilo moja, pili, umeshajiuliza yeye mama Mkapa aliyajua wapi hayo kwa muda mfupi vile? Na kama aliyemwambia alikuwakilisha vizuri kwake, kwa nini akupigie na kukusisitiza umalize mambo kinyumbani?” Mama Msindai akakunja uso.

“Naomba tumalize haya mazungumzo baadaye, ili mimi nikaongee na Sabrina, akawahi kumpa mtoto chakula.” “Kwa hiyo nikitaka kuzungumza na simu zangu inabidi nitoke hapa?” Hukumu ingine kwa mama Msindai. “Utachukua likizo kwa muda, utulie humu ndani.” “Hakika huwezi kunifungia humu ndani Msindai, eti kwa sababu ya makosa ya Jackson! Sitakubali.” “Tayari kuna ulinzi getini. Siruhusu mgeni yeyote humu ndani wala mtu kutoka mpaka nitakapoweka mambo sawa huko mtandaoni.” Mzee Msindai akatoka nje.

“Hakika baba yenu hawezi kunifanyia hivi mimi! Hawezi kunifungia mimi humu ndani! Junior, nenda kazungumze na baba yako. Mwambie..” “Kabla hujaanza kutishia mama, jua baba amesikilizishwa majibu yako yote ulipozungumza na yule mwanamke aliyekupigia simu. Na baada ya kuachana na wewe, alipompigia mama Mkapa pia baba amesikilizishwa mazungumzo yao. Yule mama hakusemi vizuri. Anasema unamtetea kijana wako kwa tabia zake chafu. Anasema hukujali swala la kwa nini amelala nje ya ndoa, bali ulionyesha unalalamikia kusingiziwa kwake mimba na mengine mengi. Ni mbaya mama!”

“Na mbaya zaidi ni kama mkalithibitisha hilo kwa kuongeza swala la Phina. Jena ameenda kukuwakilisha kwa Phina pia.” “Acha kunisingizia Jacinta.” “Wewe unafikiri ni kwa nini baba amekasirika? Huyo shoga yako Phina, anatangaza amepokelewa na mama yake Jack na wifi yake. Na wewe umemwambia mama atamfanyia babyshower. Pinga nikamuite baba.” “Lakini ndivyo mama alivyosema! Mimi nilizungumza na Phina mambo yote aliyoongea mama.” “Mnafiki mkubwa wewe na mbea! Hata kama nilisema, nani alikutuma ukaongee mambo ya ndani, huko nje!?” “Ulisema Phina ameshakuwa mmoja wa familia. Hata kama wamekasirika, lakini Phina amembeba Msindai, na ni mtoto wa humu ndani. Wewe utampokea kwa baraka zote na utamkaribisha. Ulisema hutamtupa huyo mjukuu. Bisha mama.” Wakaanza kubishana hao wawili wakijua wameshakamatwa. Jack kimya ameinamia magoti, kichwa chini.

Sabrina alipoona hawamalizi, akamuita msichana wake. “Pina tangulia kwenye gari ya anti Jacinta. Nakuja, sisi tuondoke.” “Nipe vitu vyenu nitangulie navyo kwenye gari. Mimi mwenyewe natoka hapa. Sitaki kusikiliza ujinga huu.” Jacinta akachukua kibegi cha mtoto mkononi kwa Pina aliyekuwa amebeba mtoto na begi. Wakatoka. “Usiku mwema jamani.” Sabrina akaaga nakutoka. Joy akabaki ameinama, hakuzungumza neno hata moja tokea anaingia hapo. “Twende Joy.” Junior naye akaondoka na mkewe.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Sabrina akamfuta mzee Msindai mpaka alipokuwa amesimama. “Nimeshajichanganya baba yangu, hata sijui nitafanya nini!” “Juu ya nini?” “Hiki ulichokuwa umekizungumza leo, natamani kama ningekisikia muda mrefu. Niliingiwa na hofu juu ya hatima ya binti zangu, ikabidi kuomba au nisema kudai Tino atolewe, ili angalau awepo ikitokea nakuja kufa kwa maradhi basi yeye awepo kulea watoto ambao nilijua hapa wamekataliwa. Tino alipotolewa, nikamrudishia watoto na baraka kwamba, hata hivi anavyotaka kuondoka, anaweza kwenda nao, ila awarudishe baada ya juma moja. Tukakubaliana hivyo. Sasa sasahivi nitafanyaje?” “Kabla sijakujibu swali lako, naweza kukuuliza swali na naomba uwe muwazi tu.” “Sawa.” Sabrina akakubali akiwa na wasiwasi. Huyo mzee alibadilika usiku huo akawa Mafia wakutisha. Alitembeza hukumu hapo, kila mtoto akabaki kupokea hukumu yake mpaka kumshangaza Sabrina, hiyo mamlaka kubwa hivyo anapata wapi! Alidhani 

“Bado unataka ndoa na Jackson?” Hapo Sabrina akaanza kulia tena. Mzee Msindai akabaki kimya akimsubiria amalize, ampe jibu lake. Sabrina akalia mpaka akatulia mbele ya baba mkwe wake. “Nimeingiwa hofu ya maradhi na sijui tutakuwa na ndoa ya namna gani akiongezeka Phina katikati yetu. Usinielewe vibaya baba. Hata sasahivi Tino nimemwambia watoto watabaki kumuita tu anko. Nilitaka kuwa na familia moja ndio maana nilipoona Tino anaanza fujo, nikaona sio mbaya akadhibitiwa. Sasa kuja kugundua kumbe mwenzangu ana maisha mengine huko nje, imenishitua sana na kuniogopesha. Kitendo cha mama Msindai kupokea mtoto wa Phina huku akikataa wangu, pia nimeogopa baba. Ndio nikamtafuta Tino.” 

“Wewe unataka nini?” “Nimezungumza sana na Tino, na naona ameongeza adabu. Ameahidi kufanya nitakachomwambia. Naomba safari hii achukue watoto, atawarudisha.” Akamuona mzee Msindai anafikiria. “Nitakwambia habari zitakazokushitua na kukuumiza kidogo.” Sabrina akatulia akimwangalia. “Nimemuondoa Tino hapa nchini.” Sabrina alishituka sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment