Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 64. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 64.

 Jack akatumia akili ya haraka kumjibu maana alishatoka kwenye mapenzi akimbembeleza, akaanza jazba. Akajua hatima yake nzuri inategemeana na huyo Phina. Akitulia, patatulia.  

“Nisikilize Phina. Huyo mtoto awe ni wangu au asiwe wangu, cha muhimu ni usalama wake. Hichi anachokwambia Ibra mfanye, mimi sitakataa, ila si salama kwa mtoto. Kwa kuwa mimi nililala na wewe, na umesema mimi ni muhusika, kwa sasa nakubali kuwajibika kwa vile utakavyotaka wewe, ila tafadhali kuwa muungwana kama Sabrina alivyokuwa muungwana kwako wakati tupo wote kule chuoni. Sabrina alikuheshimu sana akijua nipo na wewe kwenye mahusiano.” Jack akasikika kusihi.

“Najua Jack, na mimi sikukusudia kumvunjia heshima Sabrina. Nilikueleza.” “Basi naomba kuanzia sasa kuwe na maelewano. Na ndio maana nauliza, unataka nini kutoka kwangu?” “Labda tua
nze swala la kliniki. Nisaidie kulipia kliniki sehemu nzuri na kwa daktari mzuri, nijifungue sehemu nzuri.” “Sawa. Wewe tafuta hiyo sehemu, niambie garama zote, nitalipia. Na nini tena?” “Nitakuwa nikikwambia vipi sasa maendeleo ya mtoto wetu?” Jack akachoka kabisa. Kwa hakika alichokitafuta akajua atakipata tu. Akajaribu kutulia ili amjibu kwa utulivu, atulie.

“Naomba hilo tulifanye kuwa kila ukitoka kliniki unachoambiwa juu ya mtoto, basi uwe unanijulisha. Na ikitokea unaugua, unahitaji msaada, nijulishe. Hii simu sitafunga tena.” Hapo akamgusa Phina. “Nashukuru Jack. Na ninakuahidi nitazungumza na Ibra na nitahakikisha anafuta picha zote. Na mida ya saa nne nitatoka kazini kwenda Ustawi wa Jamii kufuta kila kitu.” “Utahakikisha vipi kama Ibra amefuta picha?” “Acha nifikirie. Maana bila mipango yakueleweka, anaweza kunigeuka, akakataa na kuamua kutumia zile picha vile anavyotaka yeye.” “Na huo ndio wasiwasi wangu, kama hatujachelewa.” “Naamini hilo nitalimaliza.” “Nafikiri na mimi ninahaja ya kukutana naye, tukazungumza. Nafikiria hivi.” Jack akapata wazo.

“Safari hii usimfuate peke yako ila usimwambie. Muombe mkutane naye sehemu. Kisha mimi na wewe twende wote. Usigusie swala la kutotaka kuendeleza mikakati yake, wala swala la picha mpaka tutakapokutana naye pamoja.” Hapo Phina alishakuwa mama watoto wa Jack, akaona anajaliwa na Jack, hakuna atakachoambiwa na Jack akakataa. Anataka mahusiano na baba mtoto wake! Akakubali bila shida. Wakajipanga kama kitu kimoja, ndipo wakaagana.

Kwa Jacinta.

J

ack akafikiria na kuamua kumtumia ujumbe dada yake. ‘Dada, najua nimekuangusha vibaya sana. Naomba msamaha. Ila nipo kwenye kutengeneza. Na safari hii nitatengeneza mimi mwenyewe bila kumtumia mama. Ila nahitaji msaada wako.’ Akatuma huo ujumbe. Kimya. Ila akaona amesoma. ‘Naomba kuzungumza na wewe dada yangu. Ukinitupa tu, ujue safari hii nitaumiza vibaya sana familia yangu.’ ‘Nitakupigia baada ya lisaa.’ Alipopata hayo majibu, akafurahi sana. Akaondoa gari mpaka kazini.  

Baada ya dakika 45, akaona simu ya Jacinta ikiingia nusura aruke kutoka kitini. Akaomba faragha ofisini kwake, waliokuwepo ndani wakatoka. “Nashukuru kunipi..” “Nenda kwenye pointi tafadhali. Usinipotezee muda.” “Nataka kukusimulia kilichotokea.” “Acha kuniambia uchafu wako Jackson! Wewe ni mchafu unashindwa hata kufikiria familia yako! Hata kama wewe ni malaya wa namna gani, unalala hovyo tu bila kinga!?” “Ni kitu kilichotokea mar…” “Unahitaji nikusaidie nini?” Jacinta akasikika kikazi haswa mpaka Jack akarudiwa na hofu.

“Ibra alijichukulia picha alizopiga Phina nikiwa nimelala kutoka kwenye simu ya Phina na kujihamishia kwenye simu yake. Phina anasema anaonekana ni kama analengo la kutaka kuzitumia vibaya. Nimemwambia Phina amuombe tukutane naye, asimwambie kama mimi nitakuwepo. Kama tumvamie tu. Ndio naomba askari ambao watatusaidia kupokonya simu yake illi kuzifuta.” “Akiwashitaki kwa kumpokonya simu?” Hapo Jack akakwama.

“Umelala kweli wewe? Au unausingizi unaokufanya unashindwa kufikiria! Maana naona unaongea ujinga!” “Nisaidie dada. Nimekwama na sikukusudia kuzaa na Phina.” “Nakuuliza hili swali nataka ulifikirie kabla hujanijibu na kama huna jibu, ni bora unijibu baadaye.” “Juu ya nini?” Jack akauliza kwa wasiwasi. “Unataka kuzaa na Phina?” “Hapana dada na wewe unaju..” “Jackson Msindai, unaongea sana bila kufikiria. Unataka mtoto na Phina? Jibu lako nipe ukiwa umetulia. Na naomba usionekane TENA na Phina sehemu yeyote ile.” “Sawa dada.” “Nitumie namba yake ya simu na ya Ibra. Huwa hatupokonyi watu simu ili kufuta taarifa.” Simu ikakatwa na kumuacha Jack akitafakari. Lakini kwa haraka sana akamtumia Jacinta namba ya simu ya Phina. Akabaki akifikiria. Jibu alilojibu kwanza, hakuwa na wasiwasi nalo. Anauhakika nalo. Ila agizo la kutoonekana Tena na Phina, analitekeleza vipi wakati Phina ametulia akijua anakutana naye ili amsindikize kwa Ibra! Akili ya Jack ikawa ikichemka akijitahidi kucheza karata zake kwa akili ili asiharibu zaidi.

~~~~~~~~~~~~~~

Akampigia simu Phina. “Ibra anatumia namba gani?” “Anazo mbili. Unazitaka?” “Zote tafadhali.” Hapohapo akamtumia. “Umeshamtafuta?” “Hapana. Nimeona nianzie pale Ustawi wa Jamii kwanza. Nipaweke sawa ndipo nimtafute.” “Unawekaje sawa?” Jack akaendelea kumchota taratibu. “Naenda kufuta kila kitu tulichosema jana. Zaidi mambo aliyozungumza Ibra. Nataka kuwaambia haikuwa idhini yangu. Yeye ameongea tu. Mimi sitaki kesi.” “Nakushukuru sana Phina. Asante.” “Samahani Jack. Nimeumia kuona imekua hivi! Nimekumbuka jinsi ulivyonisadia kupata hii kazi na mengine mengi. Sikukusudia.” “Haina shida. Naomba kuanzia sasa tuwe upande mmoja.” “Nitakutaarifu muda na sehemu tutakayokutana na Ibra, ili tuwe na wewe pia. Angalau nikuone, nikuombe msamaha unione ninavyo maanisha.” Phina akaonyesha utayari wa kuwa huo upande mmoja na Jack. Jack na yeye akawa akimsikiliza na kumuitikia kwa makini ila kichwa kikichemka jinsi ya kumtoka bila kuharibu hiyo hali ya utulivu aliyoipata mpaka utayari wa kwenda kurekebisha huko Ustawi.

“Sawa. Ila naomba usikasirike ikitokea nashindwa kufika Phina, mama. Nina mambo yananishikilia hapa ofisini. Sitaki kuharibu na hapa.” “Usijali hata kidogo, Jack. Nakuelewa kabisa baba watoto wangu.” Hapo moyo wa Jack ukawa kama wa Sabrina. Mpaka akaelewa anavyosema Sabrina moyo unapasuka inakuwa kama chuma kimeanguka sakafuni! “Baba watoto wake! Mungu nisaidie!” Akachoka kabisa na kuzidi kuingiwa hofu kana kwamba hakuyapanda, hapo anavuna! “Sawa. Tutawasiliana.” Jack akamjibu lakini huku akiyafanya yote. Mpaka wanaagana na Phina, alishamaliza kumtumia dada yake hizo namba na kumjibu ujumbe wake. ‘Nitakujulisha kazi itakapokamilika.’ ‘Asante dada. Na bado jibu ni lileile, sikuwa nimekusudia kuendesha familia mbili.’ Hakujibiwa. Ila aliona ujumbe umefika.

Phina.

K

uanzia Phina anatoka nyumbani kwake, hakujua kama kuna watu wanamfuatilia na kuripoti kwa Jacinta. Akaingia Ustawi wa Jamii, kuzungumza nao. Wakati anakaa tu, akaingia msichana mwingine na yeye akakaa sehemu nyngine. Phina akajieleza akikanusha kila kitu walichosema jana yake mpaka akawashangaza wale aliowakuta pale mwanzo. “Au umetishwa!?” “Hivi mnavyoniona naonekana ni kama mtu niliyetishwa?” Phina ametoka kuzungumza na Jack, wana mipango yakulea mtoto, roho safi. “Yale mambo ni ya yule niliyekuja naye. Kwanza hata sio kaka yangu! Ana bifu na Jackson Msindai. Anataka kumuharibia, ndio akaniambia nije tumuharibie. Jack alikuwa mpenzi wangu wa chuoni.” “Kwa hiyo zile picha mlizopiga Uswiz ni…” “Mjini hapa mama yangu. Mambo yanatengezwa.’ Phina akaongea mengi mpaka akawaweka sawa, Ibra akabaki kichekesho. Akatoka hapo akiwa ameridhika amemtengenezea Jack, atamfurahisha.

 ~~~~~~~~~~~~~~

Akamtumia ujumbe Ibra akimuomba wakutane kwa chakula cha mchana. Akakubali kwa haraka sana. Wakapanga muda na sehemu. Hapohapo Phina akamtumia ujumbe Jack kumtaarifu kila kitu. Jack akashukuru Mungu hilo la Ustawi wa Jamii limekaa sawa. Sasa kukutana ndio akatafuta hekima yake ili asije kutibuka tena atakapoona hajatokea. Akijua wazi hatakwenda, lakini akamwambia kwenye mida ya saa nne atampa jibu la hakika kama atakwenda au atamuomba yeye amuwakilishe. Phina akazidi kufurahia akijua wapo ukurasa mmoja na Jack, kumbe Jack yupo kwenye mikakati ya kujitoa kwake moja kwa moja. ‘Usijali Jack. Mimi naelewa. Wewe chapa kazi.’ Akamrudishia hayo majibu.

Hata hivyo kwa asili Phina alikuwa mtaratibu. Mzuri sana wa sura na umbile pia. Kwa muonekano ukweli alivutia kwa haraka sana. Jack akamtumia dada yake muda na sehemu watakayokutana Ibra na Phina. Akaona ujumbe umefika, lakini hapakuwa na  majibu. Alitegemea. Akatulia.

Sikio Halizidi Kichwa.

I

lipofika mida waliyokubaliana kukutana, Phina akaenda hapo, akamkuta Ibra akimsubiria. “Vipi mrembo?” “Mimi naendelea vizuri. Za tokea jana?” “Nzuri tu, lakini nilikuwa nazungumza na jamaa hapa kwa simu, anaonekana anaweza kutusaidia swala la Jack.” “Kwa njia gani?” “Hata kwa kumshitaki kisheria! Yeye si anajidai mjanja? Sasa sisi tumuwhi kisheria. Tunamshitaki kuwa Jackson Msindai anatumia mali ya serikali kufanya…” “Subiri kwanza Ibra. Kwani kimetokea nini kati yako na Jackson!?” Mpaka ikabidi Phina kuuliza maana Ibra alionekana amebakiwa na ajenda moja tu maishani. Ajenda, ‘Angamiza Jackson Msindai’!

“Jamaa mshenzi yule!” “Amekuudhi nini hicho ambacho upo tayari kumuharibia kwa kiasi hicho?” “Usitake kuniambia kama umebadili mawazo, Phina!” “Sio kubadilli mawazo ila nataka tu kujua mlipokosana na Jack kwa kiasi hiki ulicho tayari kumuona ameharibikiwa mpaka amefika chini kabisa!” “Nisikilize Phina, mimi nakusaidia wewe.” Phina akakunja uso kama akimshangaa.

“Katika mazungumzo yangu ulinisikia nikisema Jack alinibaka!” “Phina wewe vipi!?” “Hapana Ibra. Katika vita yako na Jack, jua na mimi utaniangamiza tu. Unapotaka kumshitaki kutumia mali ya umma kufanya uchafu wake, ujue aliyefanya naye uchafu ni mimi. Jack atakapofukuzwa kazi au atakapoharibikiwa, inamaana na mtoto wangu ataharibikiwa.” “Wamekufikia nini ndio maana unaongea hivyo!? Wamekuahidi nini?” Ibra akaanza kupandisha hasira zaidi kana kwamba ni kaka yake kweli Phina!

“Hapana Ibra. Wewe fikiria tu bila jazba. Sina mahali nilipolalamika juu ya kubakwa. Na sio kwamba nimekutana na Jack, nikamwambia swala la ujauzito, akanikana. Nimefikiria nimeona nakwenda mbali mpaka napotea lengo.” Wakaanza kubishana. Wasijue yupo mtu meza ya karibu kabisa na wao, ameshaingia kwenye simu zao, ameshapata mafaili ya picha, anaendelea kufuta vitu kwenye simu zao, wao wakiendelea kubishana, hawajijui.

“Hapana Ibra. Mimi mwenzio bado nampenda Jack.” “Kwa hiyo unajidanganya kwa kubeba huyo mtoto ndio atakurudia?” “Hata asiponirudia lakini nitabaki mama watoto wake, daima. Kwamba nimepata sababu ya kuwa na Jack kwa karibu kama mzazi mwenzie. Nampenda Jack, na Mungu amenisaidia atakuwa baba mtoto wangu, nataka afanikiwe zaidi. Nakuonya achana na mambo yangu na Jack.” “Basi wewe achana nayo, mimi naendelea kivyangu.” “Unaendelea vipi na mimi mlengwa nishakwambia sitaki! Wewe vipi Ibra!?” Ibra akanyanyuka na kuondoka hapo kwa hasira kabisa mpaka akamshangaza Phina.

Alichokuwa hajui Ibra mpaka hapo ananyanyuka na kuondoka kwa hasira akipania kwenda kumuharibia Jackson Msindai, hana ushahidi tena wa kuwa Jack alilala na Phina. Kitendo cha kukaa tu hapo, nyumba yake, gari na hiyo simu vilivamiwa kama nyuki bila yeye kujua. Na walihakikisha wanatafuta mpaka chini ya godoro! Kwa makini ili akirudi asijue kama kuna mtu aliingia hapo kwake. Gari yake ilipekuliwa kila mahali. Uzuri nyumbani kwake alikuwa akiishi peke yake. Ikawa rahisi.

Picha zilizokutwa zikachukuliwa na gari yake kufungwa pamoja na nyumba kurudishwa kama alivyoiacha kwani huwa wanapiga picha kabla hawajagusa. Kwa hiyo wanaporudisha wanahakikisha hata kama uliacha kijiko kichafu kitandani, basi utakikuta vilevile kana kwamba hakuna aliyepita hapo kumbe ilifanyika kazi kwa kina bila kupuuzwa sehemu yeyote mpaka ndani ya mto, lazima mkono upite na jicho lihakikishe hakuna wanachokitafuta.

~~~~~~~~~~~~~~~

Phina akamtumia ujumbe Jack. ‘Nimetoka kuzungumza na Ibra. Hatujaishia pazuri na ameshatafuta mtu atakayemsaidia kukushitaki.’ Jack akasoma huo ujumbe akatulia kidogo kama dakika kumi hivi, kumuonyesha kweli yupo busy, wakati hapo akili yake haifanyi kazi kwa hofu ya mkewe na aibu aliyotia familia. Alikuwa akisubiria safari moja ya nje ya nchi ambayo hakuwa na uhakika kama atapewa yeye au atasafiri Waziri mwenyewe. Akatamani iwe ni yeye angalau atoke hapo nchini, akapumue kwa muda. Pengine ataweza kulala kitandani, maana hakuwa akilala kitandani kwa hofu ya mkewe. Akajiambia akipata usingizi hata wa masaa 6 tu mfululizo, pengine akili itafanya kazi. Akabaki akifikiria hapo mwishoe akamrudishia ujumbe. ‘Usijali. Rudi kazini ukatulie kabisa. Usijipandishe presha. Inatosha.’ ‘Nashukuru kujali, Jack. Asante na samahani.’ “Usijli.” Phina akafurahi akarudi kazini roho imetulia.

~~~~~~~~~~~~~~~

Jack alikuwa amekaa ofisini kwake hana afanyalo isipokuwa macho kwenye simu akimsubiria dada yake na kujua kama anasafiri au la. Akiwa mawazoni, ujumbe kutoka kwa Jacinta ukaingia. ‘Labda kuwepo na picha nyingine sehemu ingine, lakini hizo picha zimefutwa kwenye simu zao. Mpaka nakala alizokuwa ameficha nyumbani kwake na kwenye gari lake zote zimeharibiwa.’ Jack akapumua kwa nguvu, wakati akitaka kumshukuru dada yake akapata wasiwasi mwingine. ‘Kama je zimebakia kumbukumbu huko studio alipoenda kutoa kopi?’ Jack akamuuliza dada yake. ‘Wapi?’ Hapo Jack akajua hilo swali linataka majibu ya uhakika. Akamtafuta tena Phina kujua ni wapi walienda kutoa zile picha, akawa hajui. ‘Nimekwama dada. Phina hajui.’ ‘Angalia kwenye bahasha au nyuma ya picha walizokuletea. Wanaweza wakawa wameacha jina la hiyo kampuni. Iwe haraka kuwahi kabla hazijatolewa nyingi zaidi tukashindwa kudhibiti.’ Jack akakimbilia kwenye gari kuchukua ile bahasha. Bahati nzuri dada yake alikuwa sahihi. Akamtumia. ‘Hizo picha zisiwahi kuonekana na jicho lolote, hata lako.’ ‘Naziharibu sasa hivi.’ Ujumbe ulifika ila haukujibiwa.

Jioni akiwa amebaki peke yake ofisini ukaingia ujumbe mwingine. ‘Na studio pia zimeharibiwa. Isiwahi kutokea tena kuniomba nifaye ujinga kama huu. Iwe mwisho.’ ‘Nashukuru dada na nakuahidi haitatoke...’ ‘Na baba ameamuru yule daktari wa Moshi aachiwe huru. Kesi zako zote hataki kuzisikia tena. Zimefutwa.’ Jack akaumia sana, akajua baba yake ndio anamnawia mikono. ‘Nilikosea sana dada yangu. Najuta. Najua nimeabisha familia na nimeharibu familia yangu mwenyewe. Lakini naahidi nitarekebisha.’ Huo ujumbe haukujibiwa tena. Akabaki pale akifikiria kitu chakufanya.

Nyumbani kumekuwa moto. Anamuogopa Sabrina, kuliko alivyowahi dhania anaweza muogopa mwanadamu. Akajua Tino ndio amerudishiwa watoto. Akatamani ingekuwa ni kosa jingine amefanya ili ampigie simu kaka yake apate hekima zake, lakini naye akamuogopa. Akaona atulie. Dhambi yake aliyofanya mbali, nje ya nchi kabisa, ikanuka kuliko waasherati wote na wazinzi wote aliowahi kuwafahamu. Akajifananisha na mfalme Daudi wa kwenye bibilia, alipolala na mke wa Uria. Mungu akamuadhibu vibaya sana. Jack akajua na yeye anapata aina ileile ya adhabu aliyopewa mfamle Daudi {2Samweli12:12,18}. 12.Na mimi niliyofanya sirini, hakika Mungu ameniadhibu hadharani.” Jack akawaza. 18.Na mimi nimepoteza binti wazuri, wawili!” Kila Jack alipohesabu starehe aliyopata alipomuweka Phina kitandani mpaka anamalizana naye, na madhara anayoendelea kuyapata, akazidi kuingiwa hofu. “Hakika hii ni laana kutoka kwa Mungu mwenyewe kwa maombi ya Sabrina. Mungu nisamehe.” Hapo mpaka Jack akatubu.

Akabaki akisuburia muda aliojua Sabrina na wanae watakuwa wamelala, ndipo na yeye akarudi nyumbani. Akafanya hivyo kama siku mbili mfululizo. Anakwenda usiku mwingi na kuondoka alfajiri, tena analala kwenye kochi.

Tino.

B

aada ya siku tatu kama alivyoambiwa na Sabrina, Tino akamtumia ujumbe Sabrina. ‘Tunaweza kukutana tukazungumza?’ ‘Saa ngapi na wapi?’ Sabrina akarudisha majibu. ‘Muda wowote ambao utakufaa kwako wewe na watoto. Kuna chakula nataka niwapikie, ni Pasta tu, chakula cha kiitaliano. Mje kula hapa nyumbani kama kuwakaribisha rasmi Jeiline na Keiline kwenye familia. Kama ni sawa lakini.’ ‘Basi nitawaleta na njaa, mida ya saa 10 jioni wakiamka, nitakuacha nao mpaka kwenye saa moja hivi ndipo nitarudi kabla hawajaanza kulia usingizi. Na hapo ndipo tutapata muda wa mazungumzo.’ Tino akapoa kidogo, inamaana Sabrina amejitoa kwenye huo ukaribisho. Akatulia kidogo ila baadaye akajibu. ‘Hata hivyo nashukuru Sabrina. Asante kunipa nafasi na watoto.’ Sabrina akasoma huo ujumbe, akajua amemuelewa. Akatulia akifikiria bila yakumjibu tena.

Ilipofika mida ya saa 10:30 jioni, Sabrina akawa amewasili nyumbani kwa Tino. Siku hiyo alimruhusu Chali mapema sana. Akamwambia kwa siku hiyo kazi yake imeisha, anaruhusiwa kuondoka. Sabrina akawa akiendesha wanae mwenyewe. Mlinzi akafungua mlango wakamkuta Tino ndio anatoka mlangoni. Alishanyoa, akarudi yule Tino wakuvutia. Sabrina akavuta gari mpaka karibu kabisa ya aliposimama. “Sasa hao wananjaa. Kila mmoja wao anakibegi chake hapo. Wakianza tu kulia, nipigie. Nitakuwa saluni. Nikimaliza nitakuja.” “Sasa mbona wananiangalia tu hawataki kutoka kwenye viti? Watakubali kweli?” “Zungumza nao kwanza. Hawawezi kushuka tu. Halafu pia bado wana usingizi.” “Basi anza kuwaambia wewe Sabrina.” Sabrina akawageukia wanae nakucheka.

“Wanavyokuangalia! Keiline?” Keiline akamgeukia mama yake na Jeiline akamgeukia pia. “Anko Tino ana kitu kizuri anataka kwenda kuwaonyesha. Mnataka kwenda kuona?” Wote wakatingisha kichwa kwa pamoja kukataa. “Mnataka kwenda na mami?” Wakakubali. “Basi acha niweke gari vizuri nishuke nao, wakichangamka ndio niondoke ili upate nao muda. “Nashukuru. Lakini kwani huwa wanakataa watu?” “Nilidhani wewe wangekukumbuka. Nahisi sababu ya kukaa tu ndani, hawajazoea watu. Acha niweke gari vizuri nishuke nao.” Tino akafunga huo mlango wa nyuma walipokuwa wamekaa hao watoto, wamefungwa kwenye viti vyao Sabrina akasogeza gari.

Kaegesha vizuri na kushuka na wanae. Wakaingia wote ndani, akakaa nao chini kabisa na kuwaambia watoe michoro yao waanze kuchora. Tino akabaki akiwaangalia. “Wamekua! Wameweza kuzungumza?” “Wanaongea wakiamua. Ila wanaelewa kila kitu na wakitaka kitu chao watakwambia tu. Wanatumia vitendo zaidi kuliko maneno.” Tino akabaki akiwaangalia. Kila mmoja wao akafungua begi lake na kutoa vifaa vyake. Tino akashangaa sana. “Hivi vitu umepata wapi Sabrina!?” “Jack huyo. Kila akienda safari, anarudi navyo. Ila Tino, hawa watoto wanakipaji cha ajabu sana mpaka wanatushangaza! Chagua kitu chochote unachotaka. Kiweke mbele yao, halafu waambie wakichore. Utashangaa.” “Kweli Sabrina?” “Wewe si utakua nao hapa, wajaribishe na usiwe na haraka. Kwa muda wao watarudi na kuchora.” Tino akafurahi sana.

“Wakati wanachora, unaweza kuja hapa sehemu ya kula tuzungumze kidogo au watalia?” “Ilimradi wajue nipo, hawatakuwa na neno. Tena ngoja niwaambie. Wamesahau kusalimia.” Akageukia wanae. “Keiline, mmesalimia?” Wakaangaliana, halafu wote kwa pamoja wakasema, “Shikamoo anko Tino!” Tino akashangaa mpaka akafunika mdomo. “Sabrina! Inamaana walikusikia…” “Na kuelewa pale garini. Kwahiyo walivyotingisha kichwa kukataa, haukuwa usingizi. Kweli walikuwa hawataki.” “Ungewalazimisha?” “Wana machozi hao, hujawahi ona. Na wakilia utasikia uchungu maana wanalia kwa huzuni mpaka dada yao anawajua! Hataki walie.” Sabrina akaanza kucheka akiwaangalia.

“Na mbona unamuita sana au unamuanza Keiline katika kila jambo?” “Upo makini, Tino!” “Nimekuona tangia wakati ule kwenye Villa.” “Alinifundisha Jack, akasema Keiline ndiye mtiifu na mwitikiaji wa haraka. Hata wakitoka hapa wakaenda chooni. Ukimuita Keiline, atakuja kwa haraka sana. Ila ukimuita Jeiline, unaweza ukarudia hata mara tatu ndio anakuja. Na ujue wanafuatana kila mahali. Kwa hiyo ndio siri hiyo.” “Oooh!” “Waitikie sasa salamu yao halafu waulize maswali. Nikiondoka, jifunze wanachofanya, halafu fanya nao ila usiongee sana. Ukizidisha tu maneno, wanaondoka na kukuacha.” Tino alicheka sana.

“Kweli Sabrina?” “Wajukuu wote wa Msindai wamewajua. Michezo yao hawa, hawataki maneno mengi. Ukiongea tu sana, wanaondoka kimyakimya. Kwa hiyo mara nyingi wanakuwa wao peke yao.” Tino akawasogelea karibu na kuwatizama kwa kutulia. Wakamwangalia. “Gosh! You girls are so beautiful!”  Tino akajikuta akiwasifia tu hao watoto jinsi walivyo wazuri! Wakacheka wote kwa pamoja. “Kwani wameelewa!?” “Sijui!” “Kwani mnawaongelesha lugha gani?” “Unanitania wewe Tino? Kiswahili.” Akarudisha macho kwa wanae. Akakuta wakimwangalia. “Nimefurahi kuwaona tena. Nilikuwa na hamu na nyinyi!” Wakatulia wakimwangalia. “Endelee na mnachofanya, acha nizungumze na mami, halafu nakuja mnifundishe mnachofanya.” Wakakubali.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakahamia sehemu ya kulia chakula. “Kabla sijaanza mengine naomba nikwambie swala la hii nyumba. Ni kweli nimekusudia kuwapa hawa binti zangu. Nilisaidiwa kujenga na baba yangu, na mimi nawaachia. Sitaishi tena hapa nchini. Nimeamua. Naona huko nilipo ndio nafanya vizuri kuliko hapa. Nataka wanangu wawe na kwao. Hapa palinifaa sana nilipofukuzwa nyumbani kwa baba na mkewe. Nimeishi hapa kwa miaka mingi sana. Pamefanyika kama nyumbani.” “Nashukuru Tino.” Tino akasimama kuelekea chumbani kwake, akarudi na kilekile kibegi alichokuwa amempa Sabina.

“Ulivyokikazania hicho kibegi!” “Ilibidi nikakifuate Chalinze japo nafikiri upande wa pesa, hapako vizuri.” Sabrina alimjua dada yake. Akajua yeye na mama yake watakuwa walizitumia zote. “Nilikwenda benki, hali si nzuri. Sasa sijui kama kuna mtu aliiba taarifa au vipi, lakini nimekuta pesa zimetumiwa vibaya sana. Ila nimeshazifunga. Nataka kukuomba kama utanipa hawa. Niende nao kesho huko benki. Niwafungulie akaunti zao.” “Kesho saa ngapi?” Tino mwenyewe akashangazwa na utayari wake. Alibadilika sana Sabrina.

“Ni wewe tu na muda wako.” “Lakini Tino, hizo kadi za benki safari hii nataka zitunzwe sehemu ambayo haitaguswa mpaka itakapolazimu sana.” Sabrina akafikiria. “Nimeyajua maisha kwa picha ya tofauti. Huwezi kuyatabiri ndio maana imebidi nijiandae. Nilipojifungua mtoto wangu huyu wa mwisho, niliugua sana.” “Pole. Nini?” “Nilipata infection, nilikuwa nikipandisha homa, nilidhani ningeondoka. Sasa nafikiria siku nikiondoka, hawa watoto wakizungu, watakwenda wapi! Ndio imebidi nijirudi japo wewe ni mtu wa mwisho kabisa natamani kukaa na wewe kama hivi na kuzungumzia jinsi ya kuwalea hawa.” “Bado hujanisamehe tu, Sabrina!?” “Hakika ni kwa kuwa wewe ni baba yao Tino, na wamezaliwa wapo hivyo kama walivyo na kugoma kuchukua uswahili kabisa. Lakini wewe!” “Basi Sabrina. Naomba usipandishe hasira.” “Na kweli.” Sabrina akasimama.

“Sijamaliza.” Sabrina akamgeukia. “Unafikiri unaweza kuja kunipa siku moja niende nao Italy.” “Nilikwambia siku ile usiku kuwa, nataka wafahamu walipotoka. Kwa hiyo ndiyo. Ila bado hawana hati za kusafiria.” “Ukinipa mimi taarifa zao zinazotakiwa huko wizarani, nitashugulikia hizo hati kwa haraka sana.” Sabrina akakunja uso. “Kwani ulitaka kwenda nao lini?” “Wakati wowote utakapokuwa tayari.” “Hawa watoto hawajakuzoea Tino, na bado wanahitaji msaada. Mimi nakujua wewe ni mtu wakutumikiwa. Watateseka sana ukiwachukua sasa hivi. Tafadhali acha wakuzoee kwanza.”

“Nisikilize Sabrina. Tino uliyekutana naye wakati ule si huyu. Hakika nimebadilika na nimeacha ubinafsi.” “Hilo ulitakiwa kulishugulikia kwakweli. Kama umefaulu hapo, hongera. Maana…” “Utapandisha hasira Sabrina. Hapo paache hivyohivyo. Ninachotaka kusema ni kwamba, hawa watoto ndio wamesababisha nitoke kifungoni safari hii nipo mzima. Ni kama sasahivi naishi kwa ajili yao. Nakuahidi nitajifunza kuwa baba mzuri kwao. Nielekeze tu. Na ukiwa unanipa nikiwa hapa, basi wakilia nitakuwa nikikupigia mpaka wanizoee.” “Hapo sawa. Una kingine? Maana nataka kwenda saluni.” “Hiki kingine naomba ukae.” Sabrina akarudi kukaa.

“Hali ya wazazi kule si nzuri.” Sabrina akabaki akimwangalia. “Umenisikia?” “Nakusikiliza.” “Waliambiwa kwa barua kuwa Sabina ameshikiliwa na kufungiwa sehemu sababu ya aina yake ya makosa. Mchochezi na mvunja amani. Anapanga mbinu za uvunjaji amani. Hawataweza kumtoa mpaka siku ya hukumu yake. Ametengwa na jamii. Wazazi wanalalamika kwamba si sawa. Kwa nini iwe hivyo kwake?” “Sasa si washitaki serikali?” Sabrina akauliza kwa ukali. Tino akajua tayari amemtibua.

“Nilikwenda pale nyumbani…” “Wameniambia Sabrina. Wamenisimulia kila kitu.” “Na unajua kwamba wewe ndio unahusika kuwafikisha wote pale walipo? Maana wewe unaneema yako mpaka huwa namshangaa Mungu. Linapofika jambo lako, huwa Mungu anaweka mazingira mpaka anakutoa kwenye mdomo wa simba. Ona ulipo sasahivi na walipo mashabiki wako.” “Ila Max na mkewe sijahusika Sabrina. Wao wenyewe walinitafuta na kupanga mipango kinyume na kaka yake Jack.”

“Sabina?” “Nilikwambia Sabrina. Na usifikiri siku ile nilikuwa nikizungumza kwa kuwa nilikuwa nikijitetea! Ni kweli. Sikuwa nimekudanganya.” “Juu ya nini?” “Kweli unataka kujua kwa undani?” “Umeanzisha mwenyewe. Ndio useme sasa.” “Tokea waliponiita siku ile kule kwenye Villa na kuniambia niliyokwisha kukwambia, mimi nilibaki mtoa pesa tu, lakini nilikuwa nikitembea kwenye mipango ya Sabina mpaka mimi nikamwambia tupunguze mwendo ni kama tunakwenda mbali sana. Akasema ameshawasoma kina Msindai, anajua aliposhindwa Max, yeye hawezi kuanguka kama Max. Nifanye anachoagiza, yeye na mama watanisaidia kupata mtoto.”

“Mpaka kujenga pale kwenu ni wazo lao wenyewe wakisema ni moja ya ushahidi kuonyesha kuwa mimi najali nyumbani kwenu kuliko mumeo. Basi mimi nikawapa hiyo pesa. Lakini Sabrina, Sabina yupo nilipomuonya atakuwepo kama hajajipanga vizuri. Akanihakikishia kwamba, hawatamuweza. Nakuhakikishia Sabrina, nilimuonya Sabina.” Sabrina akazidi kuumia. “Basi, watoto wakianza kulia, nipigie. Vinginevyo nikimaliza saluni, nitakuja kuwachukua.” “Sawa.” Sabrina akatoka akiwa amezidi kuumizwa. Nyumbani kwao vita. Ukweni vita. Mume ambaye ndiye aliyekuwa ngao yake, ndiye huyo! Akatoka hapo na maumivu kweli.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akaenda saluni kujitengeneza. Hakuwa amekwenda kwa muda mrefu kidogo. Akaona atulie hapo. Wakaanza kumshugulikia. Akataka asuguliwe mpaka miguu. Akatulia hapo akiwa amepotelea mawazoni hata asijue kinachoendela hapo saluni. Nani anasemwa, nani anasifiwa. Yeye kimya mpaka wakamaliza, ilikuwa saa mbili usiku. Akarudi nyumbani kwa Tino, akakuta watoto walishalala, wamemuegemea Tino. “Sasa kwa nini hukunipigia?” “Nasikia raha hivi walivyonilalia. Nilikuwa naogopa hata kusogea wasije wakaamka. Nimeongea kwa video na anti na ndugu wote wakiwasalimia hawa naona mpaka chaji imeniishia, simu imezima.” “Walikula vizuri?” “Naona chakula chenyewe nilichowapikia hawajapenda. Anti amekiona anasema ningefanya Pasta laini zaidi na ningeongeza sauce pengine wangekula.” Sabrina akacheka akiwaangalia vile walivyolala. “Watakwenda kuongezea na maziwa ndio watalala vizuri mpaka asubuhi.” Tino akasaidia kuwapandisha garini, Sabrina akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Mpaka wanafika nyumbani ni saa nne na nusu na Jack naye akawa anaingia getini. Akawa ameshampigia simu Pina na mwenzie watoke kumsaidia kubeba hao watoto. Jack akabaki kwenye gari akiangalia kinachoendelea. Akagundua ni watoto wa kike tu, na ndio wanarudi mida hiyo na mama yao. Inamaana alikuwa kwa Tino. Jack akaumia sana. Ingekuwa siku chache zilizopita angeuliza na kukemea, gafla akahisi amepoteza mamlaka kwenye familia iliyokuwa ikimtizama kama kichwa cha familia. Akatulia hapo garini akifikiria mpaka wakaingia wote ndani na yeye ndipo akaingia na kukaa sebuleni kama mgeni rasmi.

Sabrina akarekebisha mambo yake na watoto. Akarudi sehemu ya kula akakaa na kuanza kula. “Kesho nasafiri.” “Hata kama mama yako amekwambia anatambua watoto unaozaaa huko nje, nakushauri ukumbuke kinga. Utakufa ukiwa umemuachia mama yako watoto kila kona. Fanya umalaya ukiwa na akili timamu. Sio kwa kuwa mwanamke amekubali kulala na wewe, basi ndio unajiachia tu hovyo ukijua hata ukizaa kama paka, mama yako atakusaidia kulea.” “Sa…” “Acha kunijibu. Nakusisitiza, kumbuka KINGA. Hata kama starehe zimekunogea huko, kumbuka mpaka sasa una watoto watatu. Brayan, Brandon na huyo wa Phina. Kuwa mwangalifu.”

“Usifurahie vile dada yako anavyokushangilia na kumwambia mwanamke wako eti atamfanyia babyshower na yeye Phina anashangilia huko mitandaoni akijiona mshindi, ukadhani ni sifa. Unaendelea kumwaga mbegu hovyo. Utakufa uache hawara zako na watoto bila baba. Shauri yako.”

“Nilimuonya Jena aachane na mambo ya babyshower. Sasa kama yeye…” “Hilo tu ndilo unaona ndilo lakuelewa? Elewa swala la kinga, Jackson Msindai. Babyshower ya Phina, haina madhara, ila haitakuwa na maana kama hata huyo mtoto atakuja kuzaliwa, halafu aje asikukute. Binadamu wazuri ukiwepo. Hata Jena anashabikia sasahivi ili tu kuniumiza. Sasa usifikiri ushangiliaji huo au juhudi hizo zitaendelea ukiwa wewe mwenyewe haupo! Hamu ya ushindani itamuisha kwa kuwa watakuwa wamekuzika. Kwa hiyo huko Mungu anakokutuma akiwa amekuamini, na wewe unaamua kuanzisha agenda zoko nyingine, ndio nakusisitiza, KUMBUKA KINGA.” Sabrina akasimama na kuondoka hapo hata chakula hakumaliza.

Jack akatamani kama akamtafute Jena usiku huo, lakini akajua ataishia kumpiga mpaka amuumize kwa kummalizia hasira. Alikuwa na safari aliyokuwa akiitamani mpaka akamuomba bosi wake yeye ndio aende akamuwakilishe, bila shida Waziri akampa yeye. Jack akalifurahia hilo akijua anaondoka kesho yake, anakwenda kupumzika kwa muda na kumuacha Sabrina pengine atatulia lakini imekuwa tofauti. Safari yenyewe imegeuka kuwa chungu kupita alifadhania. Anaacha kwake moto unazidi kuwaka na dada yake akisaidia kuchochea kuni. Inamaana hata akirudi, atakuta mambo palepale, hapajapoa.

Safari zote zinakuwa nzuri na anaagwa kwa maombi, ila safari hii maneno machungu! Akabaki pale kwa muda, akaamua kuingia chumbani na kuanza kufungasha, Sabrina kitandani amejilaza, macho kwenye simu.

Akaanza. “Mwanamke wako amejaa huko Instagram akisaidiwa na wifi yake Jena. Dada Pendo amenitumia. Ameshatuma picha za Ultrasound na tarehe ambayo wanapanga na Jena kufanya babyshower.” Jack akasimama wima kwa mshituko, hakutarajia. “Unataka kuona au ndio unakwenda kuchezea tumbo lenyewe live?” Sabrina akamkejeli akicheka kwa uchungu. “Siendi na Phina.” “Kwa hiyo safari hii unaenda na mwingine tena!?” Jack kimya. “Mheshimiwa Msindai, utajaza wajawazito huko Insta, mpaka mfungue nchi yenu wenyewe.” Jack kimya.

Sabrina akarudisha simu yake pembeni ya kitanda, akatulia. Jack akaendelea kufungasha. “Ni safari ya siku 6 tu, nitarudi Brina. Na tutazungumza vizuri.” “Unataka unisimulie jinsi ulivyomfaidi mrembo Phina, wakati mimi nikijiuguza hapa nyumbani peke yangu? Nilikuwa nimejawa hofu ya kifo kwa kujifungua kwa upasuaji na kupata infection kali, nahofia na kukuhurumia kukuachia watoto peke yako, kumbe mwenzangu huna hata wasiwasi maisha yako yanaendelea, tena si  kama kawaida, kwa starehe tupu! Hakika Mungu aingilie kati katika hili.” “Sabrina, ilitokea bahati mbaya, sio kitu nilipanga mke wangu. Naomba usinilaani!”

“Mtoa laana ni Mungu Jackson. Wala si mimi. Ila ujue umepoteza vigezo vyote vyakuwa baba kwa binti zangu. Wewe endelea kukusanya watoto huko nje, mwache Tino na yeye achukue wake, mambo yaishe. Unaniacha mimi naugua hapa na katoto kachanga, bado Brayan mdogo kabisa ananililia hajui kama naumwa au nina mdogo wake, na wewe unajua tulizaa karibu karibu, ukaniacha hapa, unakwenda kuendeleza umalaya wa kizembe huko nje!  Hakika Mungu aingilie kati.” Sabrina akatoka kabisa hapo.

Jack akajua hicho alichokiona huko Istagram ndio kinamuumiza zaidi. Akaamua na yeye aangalie. Akachukua simu ya Sabrina na kutafuta ujumbe aliotumiwa na Pendo. Akakuta ni kweli mpaka na tarehe na jina la ‘wifi Jena’ halafu Jena Msindai aka like ile post na comment. Akabaki amesimama pale na simu mkononi. Sabrina hakurudi mpaka asubuhi anaondoka, akasikia Brandon amelia kidogo, akatulia. Akajua Sabrina yupo chumbani kwao. Akaenda. “Mbaki salama.” Hakujibiwa. Akaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment