Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 63. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 63.

Kabla Jena hajamalizia Jack akasimama kama mshale akamrukia na kumpiga ngumi tatu mfululizo, mama yao akaingilia, Sabrina akatoka. “Niliwaonya mumuache Sabrina. Mama na Jena, hakika nawaonya. Katika kusaidia kwenu katika hili, iwe ni kusaidia kweli, isiwe si kushindana na Sabrina. Mimi nilifanya kosa, acheni kumuadhibu mke wangu kwa makosa yangu. Na usinijibu Jena. Sijalala nina usingizi, naweza nikakumalizia wewe hasira bure!” Jena akanyamaza. Jack akatoka.

Chachu Ndogo Imechachua Donge Zima.

J

ack akamkuta Sabrina ndani ya gari. “Panda nyuma ya hii gari.” Sabrina akamuamuru mumewe. “Tunakwenda wapi na kwa nini niache gari yangu hapa!?” “Nikimalizana na wewe, utarudi kuchukua gari yako. Panda.” Jack akapanda asijue wanapokwenda ila yeye Chali alishajua maana Sabrina alimwambia mara tu alipopanda garini wakati Jack akimpiga dada yake ndani. Chali akatoa gari hapo. Njiani kimya. Jack akashangaa wanaendesha mpaka kituo cha polisi Ostabay. “Shuka.” Sabrina akaamuru tena. “Kwa nini tupo hapa!?” Sabrina hakumjibu, akashuka na pochi yake na kufunga mlango.

Sabrina akaongoza njia mpaka ndani kituo cha polisi, mapokezi. Jack akamfuata. “Mimi na mume wangu tunataka kufuta kesi na kuondoa restrain Order kwa Constatino Mandari.” “No way Sabrina! Haiwezekani.” “Usinitanie Jackson. Futa kesi zote za Tino, na nataka atolewe jela usiku huu.” “WHAT!? Hata kama unaniadhibu lakini si kwa..”  “Ushaona wapi mtu anaadhibiwa kwa kupata starehe?” Askari wa pale mapokezi wakabaki wanashangaa. Ni Naibu Waziri wa fedha na mkewe. Kina Msindai!

Sabrina akamvuta mkono na kumtoa nje kabisa ya pale mapokezi mbali na masikio ya watu. “Kwa maisha uliyochagua kuishi wewe, ndiyo nayaendeleza. Wewe unalala na wanawake nje bila kinga. Unataka uje uniue mimi, halafu binti zangu ndio waje wapate shida!” Sabrina akaanza kugomba. “Yaani mama yako leo amenifungua macho na amenithibitishia wakina Jeilini hawatakaa kuwa wakina Msindai. Amewakataa. Ndio maana leo yupo radhi kumpokea mtoto wa Phina, lakini si wangu! Sasa ulitaka wewe uendeleze umalaya huko nje bila hofu ukijua hata ukifa kesho wanao watapata pakukimbilia halafu wanangu wao ndio waje wapate shida baadaye, ukiwa mimi mama yao ushaniua, baba yao umemfunga jela, hawajui ukoo wao kama hivi mama Msindai anavyotaka mtoto wa Phina ajulikane kwenye ukoo wa Msindai!? Acha ushenzi na ujinga. Tunafuta kesi zote za Tino. Na sijui utafanyaje Jackson Msindai, namtaka Tino HAPA. Usiku huu, LEO.” “Tino anakabiliwa na makosa mengi likiwepo la kukamatwa na madawa ya kulevya.” Sabrina akashangaa sana.

“Umechanganyikiwa Jackson, wewe!?” “Amekamatwa, sio mimi.” “Sasa nisikilize Jackson. Namtaka Tino ambaye amefutiwa makosa yake yote likiwepo hilo mlilomsingizia.” “Sio…” “Nisikilize Jackson, maana katika hili huna chaguzi. Badala ya kupoteza muda hapa, anza kukusanya jopo lako lote, mjue jinsi ya kumtoa Tino ndani.” “Hayupo hapa.” “Popote mlipomfungia, utamleta hapa nillipo mimi. Maana hapa sitaondoka bila TINO. Ukishindwa wewe, mimi nitamtafutia mwanasheria wakumtetea. Waseme leo, ni kifaa gani hicho maalumu walichonacho uwanja wa ndege wa nchi kama Tanzania, ambacho hawana nchi zilizoendelea kama Itali, kilichoshindwa kugundua madawa ya kulevya kwenye sanduku la Tino wkati akiyatoa huko, eti hapa Tanzania ndio waweze kumkamata!” Jackson kimya akijua akili ya Sabrina bado inafanya kazi japo amekasirika.

“Usinitanie Jackson! Kamlete Tino hapa, lasivyo mimi na kina Jeiline, tutafika mpaka mahakamani kwa ajili yake.” Kimya.  “Na ujue kabisa Jackson, Tino akilala ndani, mimi nitakuwa hapa nikimsubiria mpaka atoke. Hata kama itachukua miaka, nitakuwa hapa. Usilete michezo ya kijinga hapa! Na uanze kwa kumfutia mashitaka yote, hapa, tena sasahivi. Usitake kunitania mimi!” Sabrina akazidi kuwaka.

“Unataka wewe watoto wako uwatunze, au watambue ukoo wao, halafu eti mimi wangu nije kuwaacha hapa duniani wakitangatanga kama mimi mama yao nilikuwa mjinga tu, sijielewi! Namshukuru sana mama Msindai na Jena kunifungua ufahamu wangu leo! Sasa kama wewe unakataa, ondoka niache hapa.” Sabrina akataka kuondoka, Jack akamuwahi. “Sabrin..” “Acha kuzungumza na mimi. Nataka vitendo tu. Sina shida ya kukusikia.” Simu ya Sabrina ikaanza kuita akapokea kwa haraka maana ilikuwa ni simu ya nyumbani kwake.

“Dada, mtoto analia sana.” Alikuwa Phina. “Nilikamua maziwa na kuyaweka kwenye friji kabla sijaondoka. Kwa hiyo mpe hayo maziwa. Pasha moto angalia yasiwe moto sana akaungua ulimi.” “Tuliyamaliza tokea saa nne.” “Mmmh!” Sabrina akaangalia saa, ilikuwa ikienda saa sita. “Usiwe na wasiwasi, baba yake anakuja na maziwa.” “Acha kuadhibu watoto Sabrina. Huyu mtoto bado ni mdogo, hajaanza kunywa maziwa mengine. Turudi nyumbani, tukazungumze.” “Wewe ulikimbia nyumba tokea jana! Leo unataka kuniambia nini!?” “Nilirudi ila sikujua ni jinsi gani ya…” “Basi kwa kuwa leo upo tayari kurudi, nenda na wewe kalee wakati na mimi nikishugulikia mpango kando kama wewe. Wewe unashugulikia mipango kando yako huko nje ya nchi wakati mimi nikilea. Sasa na wewe nenda kalee wakati na mimi nahangaika na mpango kando wangu. Nikimaliza na mimi nikawa tayari kurudi nyumbani, nitarudi. Ila hapa sitoki bila Tino.” Jack akaondoka hapo kurudi garini. Sabrina akarudi kwa Phina. “Usiwe na wasiwasi baba yao anakuja. Na ukiwa na swali lolote la watoto mpigie yeye simu.” Sabrina akakata simu na kuizima kabisa na kurudi ndani kituo cha polisi, akaenda kukaa kwenye benchi mbele ya mapokezi, akainama.

“Mama Msindai, karibu usubirie hapa ofisini.” Mkuu wa kituo alishaitwa na kuambiwa kina Msindai wapo hapo, akatoka na kubaki hapo mapokezi akijua kwa alichoambiwa na maaskari wa hapo, watarudi tu. Akawa akiwasuriria hapo. Ndipo aliporudi tu Sabrina, akamuwahi kwa ukaribisho. “Hapana, nashukuru. Kama hamtanifukuza, basi hapa panatosha.” “Hapa pako wazi kwa msaa 24. Ila huku ndiko kwenye mazingira mazuri.” “Nashukuru, lakini acha hapa patoshe tu.” Sabrina akarudi kujiinamia, kumuashiria amemaliza mazungumzo na yeye.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jack akabaki garini akifikiria pakuanzia kumtoa Tino. Kitendo cha baba yake kuondoka vile, akigomba mbele yao, akajua kwa mara ya kwanza amemvunja sana moyo. Akaona asimtafute. Junior! Akakumbuka Junior aliondoka pale hata hakumtizama wala kuchangia lolote juu ya hilo. Akaona amtafute Jacinta ambaye yupo jikoni. Akarudi ndani kwa Sabrina. “Njoo mara moja hapa nje.” Sabrina akasimama na kumfuata. Waliporidhika wapo mbali na watakaposikika, Jack akaanza. “Inamaana unataka mpaka Sabina aachiwe!?” “Umenisikia nikitaja jina Sabina usiku wa leo mimi?” “Kwa hiyo upo radhi ndugu…” “Acha kunipoteza malengo. Futa kesi zote za Tino, na ninataka hati yake ya kusafikiria ije naye pamoja na mizigo yake yote.” Sabrina akaweka msisitizo.

“Kwa nini tusishugulikie haya mambo kesho? Sasa hivi ni usiku sana.” “Tokea lini giza limekuwa tatizo kwako na kushindwa kufanya yako? Usinitanie Jackson. Na usicheze na upande ninaokuwepo mimi! Wewe unajua kabisa, walio upande wangu huwa hawashindwi, sasa usinijaribu nikahamia kambi pinzani. Hutataka kuwa mahakamani ukishindana na mimi pamoja na kina Keiline! Nakuonya Jackson!” Jack akarudi garini, Sabrina akarudi kukaa ndani.

Kwa Jacinta.

Akampigia simu Jacinta. Ikaita mara kadhaa mpaka ikakata. Akajua ameamua asipokee simu zake. ‘Tafadhali, ni muhimu, lasivyo nisingethubutu kupiga.’ Akaona amesoma hajajibu. Jack akafikiria kitu kinachoweza kumfanya dada yake azungumze naye. Akakosa. Akafikiria kwa muda ni nini kinamfanya Jacinta kuwa kama mwanadamu au mwanamke wa kawaida! Maana wote walimjua Jacinta ni katili, mkorofi haswa. Masikio yake huwa yanamsikia baba yao vizuri na kumuelewa yeye bila kurudia kuliko mwanadamu mwingine yeyote na huwa hamuogopi mtu ila kuamua kukustahi tu. Ila Junior huwa wanapatana sana na kuheshimiana tokea wadogo. Ni kama Junior alishamjualia na akajua jinsi ya kuishi naye.

 Jackson akamfikiria dada yake, mpaka akapata jibu. Akarudi kuandika kwa haraka. ‘Ni jambo la kuhusu Sabrina.’ Hapo Jacinta akampigia. “Sabrina yupo hapa kituo cha polisi cha Ostabay, amesema hataondoka mpaka Tino atolewe na afutiwe kesi zake zote na aletwe na mizigo yake yote ikiwepo hati yake ya kusafiria.” “Mwambie Tino atakuwa hapo baada ya dakika 45.” Simu ikakatwa. Jack akashangaa sana asiamini anawezaje kumuachia Tino kirahisi hivyo! Akajua kweli Jacinta amekasirika na anafanya makusudi kumkomoa.

Akarudi ndani, akamuita tena Sabrina. Sabrina akatoka na kumfuata nyuma. “Tino atakuwa hapa baada ya dakika 45. Nashauri urudi nyumbani kwa watoto.” “Nitakuwa hapa mpaka nimuone Tino kwa macho yangu haya ya nyama. Akiwa mzima nitakuwa na mazungumzo naye. Akiwa mgonjwa nitahakikisha nampeleka hospitalini. Anatibiwa mpaka apone kabisa, nipate muda wa mazungumzo naye ndipo mengine yatafuata. Kwa hiyo usiwe na wasiwasi juu yangu. Inaonekana usiku ndio mzuri wa kufanya mambo kukiwa kumetulia. Ila wakati wewe unakusanya watoto wa nje, nasikia kuna anayelia kule nyumbani. Jitahidi kuwahi.” Jack akataka kutoka.

“Nashauri usiondoke bila kufuta kesi na vipingamizi vyote vya Tino, Jackson. Maana kesho nakwenda naye Ustawi wa Jamii, na mimi nafanya kama Phina.” “Sabrina umekasirika. Nashauri utulie.” “Hata kidogo Jackson. Mama yako amenipigia kengele inabidi niamke. Na nimeshaona hatari ya wewe kuja kuniua nikaacha binti zangu wakihangaika. Katika hili, hamna hasira hata kidogo.” “Sabrina!” “Nakusisitiza Jackson, futa kesi za Tino. Sikutishi, nakuonya.” “Kila kitu kimeshashugulikiwa. Tino analetwa hapa na vitu vyake…” “Basi nashauri uwahi nyumbani. Brandon akianzaga kulia bila kutulizwa akatulia, anaamsha watoto wote. Hapa tunapozungumza, watakuwa nyumba nzima wapo sebuleni. Wahi. Na naomba uniachie Chali. Asisogee pale alipo. Tafuta usafiri mwingine wa kukutoa hapa.” Jack akatoka. Sabrina akarudi ndani.

Sabrina&Tino Tena .

Sabrina akiwa amejiinamia askari kanzu wawili wakaingia hapo na Tino. Tino alikuwa amechoka haswa na mandevu mengi. Wakamfungua pingu. “Mama Msindai!” Sabrina akasimama. Tumeambiwa tukukabidhi na mizigo yake ipo kwenye gari. “Mimi sitaki tena kesi Sabrina.” “Sasa hivi ndio unajidai hutaki kesi? Ulipokuwa ukikusanya watu kinyume changu na mume wangu! Sikukuonya wewe?” Sabrina akamgombeza. “Nimejifunza.” Sabrina akamwangalia na kurudisha macho kwa wale askari. “Naomba muhamishie mizigo yake kwenye gari yangu. Twendeni. Na wewe unifuate. Acha kujitilisha huruma hapo wakati ulijitafutia mtatizo wewe mwenyewe.” Akatoka, wote wakamfuata nyuma. Wakamkabidhi Tino vitu vyake vyote, Sabrina akawashukuru na kubaki amesimama na Tino.

“Mimi sitaki tena kesi Sabrina. Naondoka hapa nchini na hutakaa ukaniona tena. Ila naomba nikuachie ile nyumba. Na kabla hujakataa naomba nisikilize.” “Nani amekwambia nakataa!” Tino akashangazwa na hilo jibu. Hakutegemea! Ikambidi kusimama wima na kumtizama vizuri, aina hii mpya ya Sabrina. “Ulikuwa ukisema?” Sabrina akataka aendelee, aache kumshangaa. “Ile nyumba baba yangu alinisaidia kuijenga makusudi ili na mimi niwe na kwetu. Na ndio maana nilimwambia Lela, nitampa kila kitu lakini si ile nyumba.” “Wakati umemtibua sasahivi? Unataka kuniachia ugomvi?” “Usiwe na wasiwasi na Lela. Hana chake tena. Tulishamalizana. Max alisema tumchokoze tu kama kuchokonoa mambo lakini alituhakikishia kwa hakika, hana lake tena. Kwanza mimi ndio kama namdai. Kwahiyo chukua wewe ile nyumba ili Jeiline na Keiline wapate kwao.”

“Sasa nisikilize Tino. Kwanza umeangamiza watu wengi sana kwa upuuzi wako ambao nilishakuonya. Huwezi kushindana na kina Msindai wewe. Nilikwambia.” “Hakika nimejifunza Sabrina. Basi. Utakaponihurumia naomba uje unitambulishe kwa wanangu. Lasivyo najiweka pembeni kabisa.” “Mbona safari hii hujaugua huko ulikokuwa umefungiwa?” “Jeiline na Keiline ndio wamenifanya nitulie, Sabrina. Wale watoto wamenipa sababu ya kutoka hivi japo njaa inauma sana. Lakini kila nilipokuwa nikikumbuka wanangu, nilikuwa nikijiambia nina sababu ya kuwa hai. Sikuruhusu kuugua hata kidogo. Ila nilifungiwa pabaya sana. Kulikuwa kunatisha, na hofu ya mashitaka niliyosomewa ndio zaidi!” “Umesomewa mashitaka gani?” Akamtajia Sabrina.

“Sasa nisikilize Tino. Nimekuombea kwa kina Msindai, haya mambo yaishe. Ila..” “Asante Sabrina. Hakika ningefia jela! Nakuahidi sitasumbua tena.”  “Nisikilize Tino. Nimeona siwatendei haki wanangu. Kuna leo na kesho. Nataka kina Jeiline wakufahamu kama baba yao na watambue wanapotoka.” Tino akaanza kulia hapo kama mtoto wa kike. “Nashukuru Sabrina. Nakushukuru sana. Niambie vile unavyotaka, mimi nitafanya.” “Wewe ndio haupo hapa nchini. Ndio niambie hii hangaika yote hii, mpaka ukafanikiwa kugeuza ndugu zangu kinyume yangu, ulipanga nini baada ya kufanikiwa kupata hao watoto?” Sabrina akataka kujua mipango yake.

 “Acha kwanza mimi mwenyewe ndio niombe msamaha kwa upande wangu kwa kuwa watoto ni damu yangu. Lakini Sabrina, halikuwa wazo langu. Ipo siku tutazungumza vizuri. Ila kwa mara ingine tena, mlipoondoka usiku ule pale Vila, mama yako na Sabina walinitaka nirudi usiku uleule kabla sijaondoka nchini, nikarudi. Walizungumza na mimi mambo mengi sana mpaka wakanibadili moyo wangu nikaona nakimbia wanangu sababu ya hofu tu. Nikajisikia nina jukumu la kupambana ili kukomboa wanangu, wakiwa wamenihakikishia Jackson hawezi kuwa baba mzuri kwa hao watoto. Wakasema hana msimamo. Atakuja kukimbia watoto kama alivyofanya, kisha wanangu wakapata shida. Waliniambia mengi juu yenu ya ndani kabisa, mpaka nikakuhurumia, nikakumbuka jinsi ulivyosimama na mimi  bila kuchoka wakati sijiwezi, japo Lela alikuwa akikukatisha tamaa. Lakini bado ukabaki na mimi.”

“Nikajua ile tabia yako ndio unayoendelea nayo kwa Jack pia, mwishoe wanangu watakuja kuteseka. Nikajiambia nina jukumu la kusaidia wanangu, ambalo siwezi kulikwepa hata kama Jack kwa wakati huo anaonekana yupo, lakini na mimi lazima niwepo, ili atakapokuja kukubadilikia, basi niwepo.” Sabrina akajiambia ndio utabiri umetimia hivyo. Akajisikia vibaya, akapotelea mawazoni, Tino akizungumza.

“Anyways, nikataka kuwalaumu kwa kuwa niliwaonya, lakini wakati nimefungiwa hivi nilivyokamatwa, ndio ni kama nikapata muda wakutulia na kutafakari zaidi.  Ni kama na mimi nimeungana nao kukuangamiza, Sabrina! Nimejichukia sana. Na sikwambii hivi kwa sababu unanipa watoto, ila tu kukwambia, nilivyofikiria. Nikajiambia nilikuwa nikikimbia bila kufikiria, nikaungana nao. Ile hali ya utayari wao kuwa kinyume nawe na mimi nikiwasaidia kimali, ndiyo ikanikumbusha zamani ulipokuja pale kwangu kuja kunisaidia nikiwa mgonjwa, uliniambia juu yao. Jinsi mahusiano yao na wewe yalivyo na mimi nikaungana nao. Kwa hiyo makosa ni yangu Sabrina. Acha mimi niombe msamaha. Nimekukosea tena. Ila lengo ni wanangu, Sabrina.”

“Wale watoto wananikumbusha haiba ya mama yangu mzazi ndio maana nashindwa kuwaacha. Nahisi kama Mungu amenirudishia mama kupitia wale watoto. Anti alikuwa akiwaangalia kwenye video, anasema wapo kama yeye na mama walivyokuwa. Hiyo ndio ikazidi kunichanganya. Nataka kuwa na mahusiano na wanangu, Sabrina.”

“Kivipi?” “Kwa kadiri utakavyoniruhusu. Wana vipaji vikubwa sana ambavyo vinahitaji pesa na mtu anayeelewa kuviendeleza. Nilikuwa natamani hiki ulichosema, lakini sikuwa najua jinsi ya kukitekeleza.” “Kipi?” “Siku moja niende nao kule kwa ndugu zetu, niwatambulishe. Wapafahamu tulikotoka na ndugu zao ili wasijikute waajabu katikati ya familia yenu. Sitajali hata wakiendelea kumtambua Jack kama baba yao. Sitawaingilia vile watakavyokua, ila nataka wajue nilikosa, nimerudi na nataka kuwatunza.” “Leo umechoka na kuna mengi utazungumza sababu ya hofu na mimi sitaki kudanganywa.” “Sita…” “Hapana Tino. Nenda kalale. Pumzika kabisa ukiwa na uhakika hakuna atakayekugusa tena. Huna kesi inayo kukabili. Kisha nitafute baada ya siku tatu kuanzia sasa.” “Kwa maana nyingine, kuanzia leo upo tayari kupokea msaada wowote wa watoto nitakao kupa?” “Kabisa. Na nitataka uwe na mahusiano nao, ili ikitokea leo na kesho mimi sipo, basi wawe na pakwenda.” Tino akamtizama Sabrina vizuri.

Sabrina akainama kama anayefikiria. “Kuna nini Sabrina!?” “Nafikiria maisha ya binti zangu, Tino. Mimi si Mungu kwamba nitakuwepo hapa duniani milele. Sitaki waje kumangamanga mtaani wakitesema na wewe umerudi ukiwataka! Siwezi kufanyia hivyo wanangu. Wewe nenda kapumzike, tutazungumza vizuri.” “Usinielewe vibaya Sbrina, ila naomba kuuliza kwa uhakika. Hichi unachoniambia umekifikiria vizuri?” “Kabisa Tino.” “Sabrina?” “Ni kweli na ndio maana nilitaka utolewe na ufutiwe kesi zote, uwe huru. Nimeona nitajidanganya, na wanangu ndio wataishia kuumia. Hakika usingekaa ukatoka jela Tino.” “Hilo najua. Najua kabisa.” “Basi ujue upo huru kwa sababu ya watoto. Nataka uwepo hapa duniani, ili siku moja wawe na kimbilio.” “Daah! Utanifanya niwe makini sana.” Wakatulia.

“Nakuahidi nitakuwa makini Sabrina. Kwa hiki unachonipa, sitakuangusha. Najua utafurahi. Nipe namba yako ili tuweze kuwasiliana.” Sabrina akamtajia. Tino akashika kwa kichwa. “Sitakupeleka kwako Tino. Ingekuwa hospitalini hapo sawa. Hii gari ni ya Msindai, siwezi nika…” “Naelewa kabisa. Kama hawatakuwa wamenidanganya, basi inamaana wamenirudishia kila kitu changu. Nitakuwa sawa tu. Nitachukua taksii hapa.” “Usiku mwema.” Sabrina akaingia garini akamwambia Chali amrudishe nyumbani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Sabrina alifika kwake akakuta pako kama mchana. Watoto wote wapo sebuleni  na baba yao, wamechangamka, mdogo analia na kunyamaza. Wote wakataka kumkumbatia alipoingia. “Mama yenu ni mchafu na ninanuka. Subirini hapahapa nikaoge kwanza. Nakuja.” Sabrina akakimbilia kutoa  nguo na kuoga kwa haraka akatoka na kumchukua Brian aliyekuwa akilia mikononi kwa baba yake. “Haya Jeiline  mshike Brayan mkono twende chumbani kwao.” Jeiline akasimama na kumshika mkono kaka yake. “Keiline wewe mtoto mzuri ukaniombee maziwa ya Brayan kwa dada, halafu uyalete chumbani kwao.” Keiline akakimbilia chumbani kwa kina Pina    , baada ya muda hiyo nyumba Jack akashangaa ipo kimya kama haina mtu. Akavuta pumzi kwa nguvu na kujiegemeza kwenye kochi. Akapitiwa na usingizi mzito asijue alipo.

Ilipofika asubuhi Jack akashitushwa na wasichana wa kazi waliokuwa wameamka wakianza majukumu yao ya siku. Ikabidi atoke hapo sebuleni kuwapisha wasafishe. Akaingia chumbani kwa kunyata akamkuta Sabrina ananyonyesha, pako kimya. Hakumsemesha, akaingia kuoga, akatoka na kuvaa kwa haraka na kutoka hapo.

 Kwa Phina.

N

jiani akampigia simu Phina. “Ni nini kinaendelea Phina!? Mbona imekuwa ni kama umekusudia kuniangamiza kana kwamba nilikubaka au nilikurubuni ili ulale na mimi?” “Mimi mwenyewe nahisi kama Ibra ndiye anayekuza, Jack. Mimi sikutaka kukuharibia wala yafike mbali, ila nilipokuwa nikikutafuta, nikakukosa ndio nikampigia simu Ibra kumuulizia kama ana namba yako ingine.” Jack kimya akimsikiliza.

“Akasema siku hizi kukupata ni shida, ila naweza kumwambia chochote atanisaidia. Ukweli sikuwa na jinsi Jack. Nikijua Ibra ni mtu wako na anatufahamu tokea chuo nikamwambia kama tulikutana Uswiz, tukalala wote, nimeshika mimba.”

“Subiri kwanza Phina. Wewe unavyoiweka ni kama ulilala na mimi usiku kuchwa na wakati bado ilikuwa mapema tu. Na baada ya pale nilikwambia wazi kabisa, nimefanya kosa. Sikutakiwa kulala na wewe kwa kuwa mimi nimeoa, nampenda mke wangu. Nimefanya kosa ambalo sitataka lijirudie tena. Uondoke urudi chumbani kwako. Nilikuacha unavaa Phina! Nikapitiwa na usingizi. Lakini nashangaa kukuta picha ulizopiga na mimi tukiwa tumelala kitandani! Imekuwa kama ulinitega makusudi!” Jack akasikika kulalamika.

“Mimi nakupenda Jack. Na hilo unalijua tokea chuoni.” “Na ndicho ulichoniambia hata siku ile uliponifuata chumbani kwangu. Ukanilainisha kwa maneno mengi, akili imekuja kurudi nimesha msaliti mke wangu! Na wewe nilikwambia ni kosa! Ni kwa nini unipige picha bila idhini yangu?” “Nahisi ni kutaka kutunza kumbukumbu yetu, Jack.” “Kumbukumbu yetu unayoitumia kuniangamiza na kuisambaza kila mahali ukinichafua! Unamfuata mke wangu nyumbani na kumuonyesha picha chafu vile!” “Hakika ni Ibra. Sio mimi. Ibra ndiye aliyeanzisha hilo na ndiye aliyempa Sabrina.” Phina akajitetea.

“Kwanza hakuwa akiamini kama kweli unaweza kuwa umelala na mimi. Akasema wewe ni muadilifu sana, huwezi ukalala na mwanamke mwingine ukiwa kwenye mahusiano.” “Lakini hivyo sivyo anavyosema! Hata kwa Sabrina amemwambia tofauti!” “Na mimi siku ile pale nyumbani kwako nilishangaa. Ni kama alinibadilikia! Lakini katika kupinga huko ndio nikamwambia ninao ushahidi, mimi nililala na wewe tulipokuwa nchini Uswiz. Akitaka aje nimuonyeshe. Nilikuwa nimekasirika Jack, Ibra aliniona mimi muongo. Nakuzushia tu! Ndio ikabidi kumwambia ninao ushahidi. Ibra aliendesha mpaka kwangu kuja kuona huo ushahidi. Nikampa simu yangu akawa anaangalia zile picha zetu. Sasa wakati namwandalia kinywaji niliporudi akaniambia eti ameona ajihamishie zile picha. Nikamuomba asije kuzisambaza. Akaniambia nisiwe na wasiwasi.” Phina akaendelea.

“Sasa juzi mchana akanipigia simu kuwa amejua pakukupata kwa urahisi, atanisindikiza. Ndio akanifuata baada ya kutoka kazini, akaniambia twende. Mimi sipafahamu kwako, wala kwake Ibra. Kwahiyo hata sikujua ni wapi tunaelekea. Nikashitukia tunaingia nyumba ambayo Sabrina yupo, Ibra akaanza hasira kwa kina Felix na Ney na kuniambia niseme. Sasa mimi nikasita kuzungumza pale kwa kuwa niliona hayawahusu pale, ila Ibra yeye akasema kila kitu, nikashangaa ametoa na picha kabisa. Wakaanza kutukanana na Felix. Felix na Ney wakaanza kumchangia kwa maneno, wakaanza kurushiana ngumu nafikiri msichana wa kazi akaenda kuita mlinzi au sijui mlinzi alisikia fujo, ndio tukatolewa wote pale. Ila sio mimi.” Phina akajitetea.

“Sio wewe ndio ulikwenda Ustawi wa Jamii ukidai haki yako? Wakati mimi sijakataa chochote na wala sikuwa nikijua kama umeshika mimba! Kwa nini unafanya hivyo Phina?” “Ni Ibra. Mungu wangu ni shahidi, Jack. Ibra ndiye ananipelekesha mpaka ananiogopesha! Amejawa na hasira na ninahofia atatumia zile picha vibaya. Ila tulipotoka pale Ustawi wa Jamii, nilimwambia, atulie, tupunguze spidi. Tunawasha moto bila sababu. Akasema yeye anaijua nguvu ya kina Msindai. Wanaweza kunizima nikapotea hivihivi. Mimi nimemwambia kuanzia sasahivi sitataka kwenda naye popote. Nitakusubiria wewe.” “Labda nikuulize Phina. Baada ya kushika hiyo mimba, unatarajia nini kutoka kwangu? Maana wewe unajua kama nimeoa na nampenda Sabrina. Nilichofanya kwako nilikosea. Na nilikwambia Phina! Sijakurubuni. Sasa wewe ulitaka nini au unatarajia nini kutoka kwangu?” Kimya.

“Tafadhali kuwa muwazi. Unachotaka ni pesa?” “Unajua sina shida na hela Jack. Mimi pesa ninayo. Ninachotaka ni umtambue kuwa huyu mtoto ni wetu. Hilo tu. Ujue ni damu yako na uhusike kama baba, kama hivyo unavyofanya kwa watoto uliozaa na Sabrina.” Jack akahisi giza. “Sitaki mwanangu aje afichwe. Nataka atambuliwe kuwa na yeye ni Msindai.” Phina akaongea bila kuuma maneno. “Sasa hii fujo unayofanya ukizunguka na Ibra, tutakuwa na mahusiano gani na huyo mtoto? Mimba yenyewe hata miezi miwili bado, unafanya fujo nchi nzima!? Unataka mimi niharibikiwe ili iweje? Unaungana na Ibra kuniangamiza huku unataka mtoto aje akute baba! Unataka akutane na baba niliyeshindwa majukumu yangu, sina kazi, siwezi hata kusaidia siku anapohitaji msaada wangu!” “Nimeongea na Ibra. Na nitamuomba leo tukutane tuzungumze ili afute hizo picha aache kuzisambaza.” Phina akasikika kunyenyekea.

“Nahisi umeshachelewa Phina. Mimi na wewe hatukuwahi kushindwana jambo. Hata tulipomaliza chuo, japo nilijua hatutakuwa wote, lakini nilihangaika mpaka ukapata kazi inayokuingizia pesa nzuri mpaka sasa!” “Na mimi hilo sijasahau Jack. Na nilikwambia sitakuja kusahau huo wema wako.” “Sasa kwa nini katika hili mimi umenifanyia ubaya?” Jack akauliza kwa kuumia kama aliyebakwa.

“Ulifungia simu zangu Jack! Ulitegemea nini?” “Wewe ulitegemea nini Phina? Eti kwa kuwa tumelala wote mara moja, basi tuanze kuchat na kurudisha mawasiliano kama vile sijaoa? Hivi unajua shida niliyopata baada ya kufanya lile kosa?” “Mimi sijui Jack.” Phina akajibu kinyonge akisikika wivu, kana kwamba hakujua analala na mume wa mwenzie. “Nina hukumu yakupitiliza. Sabrina amekuwa muaminifu sana kwangu. Mno. Sikutakiwa kumtenda nilichomtenda.” “Kwa hiyo unanilaumu?” “Nilikwambia tokea mwanzo, kuwa mimi ndiye niliyefanya kosa. Sikukubaka, hukunibaka. Nilikosa. Hapakuwa na jinsi baada ya pale eti tukaendeleza mazungumzo kati yetu, kwa ile hukumu niliyokuwa nayo, Phina.”

“Sasa kuanzia sasahivi nikiwa na shida nakupataje?” Phina akauliza kwa hasira. “Shida gani tena Phina na wewe umesema huna shida na pesa unachotaka ni mtoto akizaliwa niwe na mahusiano naye?” “Kwa hiyo ndio sitakusikia tena mpaka nijifungue?!” Phina akauliza kwa kuhamaki. “Nimetoka kukuuliza Phina. Unataka nini kutoka kwangu? Ni nini unatarajia kutoka kwangu? Kumbuka nimeoa, nina familia na nina majukumu ya kazi pia. Ulitaka nifanye nini na huyo mtoto bado hajazaliwa?” “Kwa hiyo unaamini kama ni mtoto wako?” Ikawa swali la kama kumtisha tena Jack. Akatae, aanzishe kingine.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kila Kazi Na Malipo Yake. Hakuna Kunakopandwa, Kusivunwe Hata Magugu!

Makosa! Makosa! Makosa!

Nani Atavuna Nini?

Usikose Muendelezo…

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment