Sabrina alikuwa amekufa
ganzi miguu haiwezi kusogea. Akili imegoma hata kufikiria! Masikio yakawa
hayasikii kabisa, akawa amepigwa na bumbuwazi. Alikuwa akiona ni kama dunia
iliacha kuzunguka kwa muda. “Dada, mtoto analia! Ameamka, nimembadilisha, ila
anaendelea kulia, nahisi ni njaa.” Ikabidi Phina amshitue tu, maana alikuwa
kama hayupo pale wakati kilio cha mwanae kilikuwa kikisikika kwa sauti ya juu
tu. Ndipo akagutuka na kumsikia Brandon akilia. Akasimama hapo kochini na
kukabidhiwa mwanae. Hiyo nyumba ilikuwa imejaa watoto, kila akipita yupo mtoto.
Akamchukua na Brayan aliyeanza na yeye kumlilia akiwa anaelekea chumbani. “Huyu
atakuwa na usingizi Phina. Naomba uje umbadilishie nguo zake za kulalia hapa
chumbani wakati nikimnyonyesha mdogo wake. Akilala ndio uje umchukue.
Ney&Felix.
L |
ilikuwa ni tukio ambalo hata wao hawakuwa
wamelitarajia hata kidogo. Walichokuwa
wamejiandaa nacho ni wakati nzuri wakukutana baada ya majukumu mengi ya mjini
kwa Ney, Felix na Jack. Pamoja na kupotezana kwa muda mrefu na Ibra. Japokuwa
hao wawili walikuwa wakifanya wizara moja na Jack, lakini Jack alirudi kuwa
bosi wao tena. Busy, kukutana naye si kama ilivyokuwa chuoni. Ibra yeye alipotea
hawakumsikia kwa muda mpaka alipompigia Felix yeye mwenyewe. Ila wote
walichukulia ni ubusy wa maisha. Kila mmoja mjini kuhangaika na maisha,
wakajua na yeye yupo busy na wao wakawa busy. Amani ikaendelea
kila mmoja na majukumu yake.
Walipomaliza Chuo wote
hawakupangiwa Wizara ya Fedha hapo Dar, kama walivyokuwa wakitamani. Wao watatu
walikwenda kuripoti na kufanya kazi kwenye vituo vyao vya kazi japo wawili hao
hawakupenda, lakini si Jack. Felix alipangiwa Gundu. Watoto hao wajiji walikuwa
wakimcheka sana maana hawakujua hata Gundu ilipo. Lakini Felix alikwenda.
Akafanya kazi miaka miwili ndipo akapata uhamisho kurudi Dar. Ibra yeye
alipangiwa Mpiji, alikasirika nakuona amedharauliwa. Hakutaka hata kwenda.
Akajiingiza kwenye biashara. Neema yeye akapangiwa Mkuranga. Akawa na kazi nyingine
ngumu ya kwenda asubuhi Mkuranga na kurudi kwake Chang’ombe usiku kwa karibia
mwaka. Haikuwa rahisi hata kidogo, lakini alikusudia kubaki Wizarani akiamini
atakuja kurudi tu alipopataka. Akaendelea hivyo bila kulalamika na kweli akaja
kufanikiwa kurudi jijini. Jack na yeye alipangiwa Singida ila yeye ni kwa
kutaka kwake. Kaka yake Junior ndiye aliyemsaidia mpaka akapangiwa huko, kwani
alitaka kwenda Singida kupafahamu zaidi. Alikuwa na malengo nako ya Ubunge kama
hivyo.
“Hakika Jack
atanilaumu sana.”
Felix akampigia Ney mara tu walipoondoa magari yao hapo nyumbani kwa Msindai
kwa kufukuzwa na askari wanaolinda hapo. “Ila Jack
amefanya uchafu wa kupitiliza. Hakika sikumtegemea!” “Yeye ni binadamu bwana!
Kukosea kumo. Halafu si umeona Phina mwenyewe alivyozidi ku...” “Acha ujinga
Felix. Unatetea nini? Kwa hiyo atakuwa akilala na kila mwanamke aliy..” “Basi
na sisi tusianze kugombana Ney. Nishauri chakufanya.” Akamtuliza maana
na Ney alishaanza kuwaka. “Kwa kuwa wewe ndio umemletea
ile fujo mle ndani na kumsogezea janga kwa mkewe, muwahi kabla hajarudi
nyumbani.” “Acha masihara Ney!” “Kumbe! Wewe unataka afike pale kwake na kukuta
ile hali wakati sisi tulijua!” “Aisee kweli.” Felix akaona ampigie simu
Jack.
Mjumbe
Hauwawi.
J |
ack alipokea simu ya Felix bila yakuchelewa. “Nakaribia nyumbani mzee, mbona huna subira?” “Aisee egesha
pembeni, usiende nyumbani kwako kwanza mpaka tuzungumze.” “Kuna nini wewe?” “Acha
ubishi Jack. Hili unatakiwa kulisikia ukiwa huendeshi kaka.” Jack akiwa
haelewi akatafuta mahali pazuri na kuegesha gari. “Kuna
nini Mkuu?” “Wewe ulipolala na Phina, mkiwa Uswiz, ulijua kama anakupiga
picha?” Jack alishindwa hata kujibu. Felix akaona aendelee. “Sasa ile ya Ibra kunitafuta ili nimlete kwako ilikuwa njia
ya kupajua kwenu, ili waje na Phina maana Phina anasema umemfungia simu zake
zote hakupati ili kukwambia ni mjamzito. Hapa tunapozungumza mkeo amepewa picha
mlizokuwa kwenye chumba mlicholala huko Uswiz na Phina. Mimi na Ney tulikataa
kuziangalia, ila ameachiwa mkeo. Hapa tumetolewa na askari wako tena kwa mtutu
maana tulianza kushikana na Ibra. Alikuwa akikutukana matusi mabaya mpaka
wafanyakazi wako wote wa nje na ndani na watoto wakaja pale sebuleni wakawa wakitusikiliza,
ikabidi kumtuliza kwa ngumi.” “Mungu wangu!” Hivyo ndivyo Jack alivyosikika.
“Ibra mshenzi
sana. Amenitumia mimi kutimiza azma yake! Halafu anaonekana anatumindi sisi
kuwa Wizarani pamoja wakati yeye mwenyewe alikataa kafanya kazi serikalini, sasahivi
anaona tunamdharau! Anatukana kama mwehu! Na anawaambia wanawake zako kuwa huo
ndio mchezo wako. Ukiwa na Phina unakuwa na Sabrina, ukiwa…” “Sio wanawake
zangu. Mke wangu ni mmoja tu, Sabrina. Phina ilikuwa mara moja tu na hata yeye
nilimwambia nilifanya kosa na.…” “Sasa hapo kaka umeangukia pua. Hiyo mara moja
naona ukafanikiwa na mtoto.”
“Phina ni
mjamzito na mkeo kapewa mpaka kopi za ultrasound. Na amesema yupo tayari
kufanyiwa DNA hata kesho ili kuhakikisha kuwa mtoto aliyebeba ni wako.” “Mungu
wangu!” “Na naona ujiandae kiongozi. Hayo madai wanayokutaka, mpaka nikamwambia
Ibra anataka kutajirika kwa jasho lako! Amemwambia Sabrina, mtoto wa Phina
anataka akue kwenye mazingira mazuri kama yale wanayokulia watoto wako pale
nyumbani kwako na Sabrina. Halafu Jack.” Felix akaendelea kufikisha ujumbe.
“Wamekupa siku
tatu tu wanataka wakusikie. Tena wakusikie na mipango inayoeleweka kwa mtoto
wako na Phina lasivyo wamesema wanakupeleka Ustawi wa Jamii, na utawasikia
magazetini wakidai haki yao. Nimeona nikuwahi usije kufika nyumbani, moto
ukawaka, ukashindwa kuupata huu ujumbe nakushindwa kuutekeleza kwa wakati
waliokupa, halafu wakakuchafua magazetini. Fanya ufanyalo hili ulimalize
kinyumbani, kaka. Mtafute Phina.” Kimya. Jack akishindwa hata kujibu. Felix
akakata simu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jack na yeye akapata kama
hali iliyompata Sabrina. Alibaki hapo garini zaidi ya lisaa, hajui alipo, hajui
chakufanya. Ila yeye aliona tofuati. Dunia nzima ilikuwa ikizunguka kwa spidi
ya ajabu sana mpaka akafunga macho ili kujaribu kujituliza. Napo haikusaidia. Huko
mawazoni ikawa mbaya zaidi. Kila kitu kikawa kimepinduka. Juu chini na kikienda
kwa mwendo kasi kuliko gari ya mashindano. Akafungua tena macho. Alibaki pale
hajui chakufanya mpaka saa nane usiku wa giza nene na saa mbili alikuwa
akitakiwa tena ofisini.
Akajua muda huo Sabrina
atakuwa amelala. Akarudi nyumbani. Akakuta ile bahasha pale sebuleni kwenye
kochi. Akaichukua mikono ikitetemeka kama anayeiba akihofia kukamatwa, kumbe
inamuhusu. Kweli Phina alikuwa amempiga picha wakiwa wameonekana kitandani, ila
yeye ndio alikuwa amelala usingizi kabisa, pembeni ya Phina. Jack akazirudisha
kwa haraka kwenye bahasha yake na kwenda kuziweka kwenye gari yake. Akarudi
kukaa hapo sebuleni. Aliposikia mtoto wao akilia, akanyata na kutoka kabisa
hapo ndani na kurudi kazini muda huohuo akijua Sabrina ataamka tu.
Siku hiyo Jack hakusikika
na yeyote hata kwa salamu kutaka kujua familia yake inaendeleaje. Aliingiwa
hofu kwa Sabrina, alishindwa hata kutaka kumsikia. Aliogopa hata kuiona sura
yake! Alikuwa akitetemeka kila akimkumbuka Sabrina. Alikaa ofisini siku nzima
na wala Sabrina hakumtafuta.
Adui Wa Mtu.
K |
inyume na walivyosema nyumbani kwa Jack, hata
mbele ya Felix na Ney, hata siku tatu walizompa Jack hazikutimia, jioni ya siku
inayofuata, wawili hao wakatokea ofisi za Ustawi wa Jamii. Huko nako Ibra akazungumza
mengi mno akisema wanakusudia kumshitaki Jack kwa kumtelekeza Phina akiwa amebeba
mtoto wake. Siku hiyo ilivyo mbaya kwa Jack, akitaka kufikiria ajue ni
jinsi gani atalikabili hilo, akaamua kwa siku hiyo afunge simu kabisa atulie.
Kumbe na watu wa Ustawi wa Jamii wakawa wakimpigia simu bila mafanikio. “Na
nyinyi mmekuwa mashahidi! Si mmeona hapatikanini kwa simu? Sisi tunaenda
kufungua mashitaka polisi.” Ibra akazidisha jazba.
“Jamani mimi nafahamiana na mama Msindai.
Acheni nizungumze naye kwanza kabla haya mambo hamjafikisha mbali. Nipeni muda
tafadhali.” Mama mmoja mtu mzima ambaye naye walimkuta tu hapo kwa bahati,
akaingilia. “Tusipowasikia na nyinyi mpaka kesho, sisi tunakwenda mbele,
kudai haki. Maana najua kwa kuwa wao wameshika hii nchi basi mnajisikia
kuwabeba tu.” Ibra akatishia. “Wala hatutafika huko. Usiwe na wasiwasi.”
Wakaondoka.
Kwa Mama
Msindai.
Ilishakuwa jioni, akaanza
kwa kumtumia ujumbe mama Msindai. ‘Mama Msindai, najua
unaweza usiwe unanikumbuka kwa karibu. Lakini nina jambo zito, naomba tafadhali
tuzungumze kwa haraka.’ Hapohapo mama Msindai akampigia. “Nazungumza na nani?” Huyo mama akajielekeza lakini
mama Msindai akashindwa kabisa kumkumbuka. Lakini akamwambia anamfahamu kupitia
mama Mkapa. Kuna kipindi walikutana kwenye washa aliyokuwa ameandaa mama Mkapa
mwenyewe. Akamtambulisha kwake ndipo akamuomba namba kipindi yupo waziri wa
afya. Lakini hakuwahi kumtafuta.
“Yaani leo
nikiwa kwenye ofisi za Ustawi wa Jamii niliposikia jambo linalokuhusu, nikasema
ulinipa namba yako kwa heshima, sio vibaya leo nikaitumia kwa jambo la msingi,
kukusaidia!” “Jambo gani hilo?” “Ndicho nataka kuzungumza na wewe kwa kuwa
nimewaambia mimi nakufahamu, nimeomba kuzungumza na wewe kabla mambo hayajapelekwa
mbali kwa kuwa na mimi ni mzazi.” “Kuna nini, mbona husemi!?” Mama Msindai akasikika
kupotezewa muda.
“Amekuja
msichana, amejitambulisha kwa jina la Phina, anasindikizwa na kijana,
aliyejitambulisha kwa jina la Ibra, akasema ni kama kaka yake Phina, tokea chuoni.
Na kwa aina ya mazungumzo yao, inaonekana walisoma na kijana wako huyu Naibu Waziri,
Jackson Msindai.” “Wote hao wawili nafikiri ndio hao ninao wafahamu. Ibra ni
rafiki wa karibu sana wa Jack.” “Mmmh! Si kwa alichokisema anakusudia
kukifanya endapo Phina hatapewa haki yake.” Hapo akamtia wasiwasi zaidi mama Msindai.
“Hapo
unanichanganya!” “Inavyoonekana Phina yupo kwenye mambo ya protocal, sijui
mipango huko serikalini.” “Nafahamu, Jack alimuomba kaka yake amsaidie
kumtafutia hiyo kazi, ndio akapewa hiyo nafasi. Kuna nini?” “Anasema kama miezi
miwili iliyopita, na yeye alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wameandaa safari
ya Naibu waziri wa fedha na kamati yake walipokwenda nchini Uswiz kwenye kikao.
Anasema Jack alifika huko akakutana naye, wakalala chumba kimoja mpaka asubuhi,
nafikiri mpaka hapo wewe mtu mzima umeelewa kilichoendelea kati yao.” Mama Msindai kimya
mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi. Huyo mama akaendelea.
“Sasa Ibra
analalamika anasema ilipofika asubuhi kijana wako akiwa amemtumia Phina usiku
kuchwa, eti asubuhi ndipo akamfukuza, tena vibaya sana. Na kuanzia hapo akawa
amemfungia simu zake. Hata Phina alipotaka kumwambia alishika mimba, hakuwa
akimpata Jackson.”
Mama Msindai kimya.
“Mama Msindai,
nashauri hili jambo mlimalize kinyumbani. Hawa vijana wanaonekana wapo tayari
kuzungumza na vyombo vya habari wakihofia usalama wa Phina kwamba ikitokea
anajulikana anadai haki yake chochote kibaya kinaweza kumpata kikisababishwa na
nyinyi.” “Kwanza kuna uthibitisho gani wa hicho anachokisema huyo Phina?” Mama Msindai akauliza
akisikika kumtetea mziwanda wake. “Mama Msindai, hawa
vijana wamejiandaa aisee. Inaonekana huyu binti alipiga picha za kutosha tu
wakiwa wamelala na kijana wako huko hotelini nchini Uswiz. Na zina tarehe mpaka
muda.” “Kwa hiyo ndio inamaanisha ni mimba ya Jackson!?” Mama Msindai
akazidi kuhoji kwa hasira.
“Ndio nilikuwa
nikienda kwenye point ya pili. Wana picha za ultrasound za huo ujauzito ambao
una majuma saba unakwenda nane.” “Sasa picha hizo ndio zitathibitisha kuwa mtoto
ni wa Jackson!?”
Mama Msindai akazidi kuhoji. “Ndio nilikuwa nikiendelea kuzungumza! Mimi nimewaomba muda
wa kuzungumza na wewe ili kukusaidia na mimi nikiwa mzazi kama wewe tu, mwenye
vijana kama wako. Sina nia mbaya. Ni mjumbe niliyejitolea ili tu kuwatuliza
pale Ustawi wa Jamii, ili na nyinyi mjue jinsi ya kujipanga.”
“Nilitaka
kuwatuliza tu, maana nilikuwepo hapo wakati wakivuta watu kwa kuongea kwa jazba,
zaidi yule kijana anayesema ni kaka yake Phina, Ibra. Amesema yupo tayari Phina
kupimwa DNA hata kabla mtoto hajazaliwa. Mimi nikamuuliza anayajua madhara ya
kumchokonoa huyo mtoto huko tumboni ili kufanyiwa hiyo DNA kabla hajazaliwa?
Akasema ameshafanya uchunguzi wake, ameshazungumza na Phina na yeye Phina ameelewa.
Wameshajua njia salama za kufanya hiyo DNA ambayo haitamdhuru huyo mtoto
anayemuita Msindai. Haitakuwa hapa nchini, amesema siku hizi Jackson
anayo pesa. Watataka njia salama kwa mtoto wao. Na kama mkikata apelekwe nje ya
nchi kwa hivyo vipimo ili kuthibitisha kuwa ni mtoto wa Jackson, basi amesema wataomba
mahakama imsaidie Phina. Narudia tena, mimi ni mjumbe tu mama Msindai. Nimeona
nikusaidie kabla mambo hayajakwenda mbali. Maana wanalalamika kwamba walianzia
nyumbani kwa kijana wako, hawa…” “Unamaana kwa mkewe!?” Hapo mama Msindai
akashituka sana.
“Walivyosema
walimkuta mkewe, kijana wako hakuwepo. Wamezungumza na mkewe na kumuachia
maagizo yote pamoja na hizo picha. Huyu Ibra anacholalamika ni kuwa inamaana
Kijana wako amewadharau. Amepata ujumbe lakini bado ameshindwa kuwatafuta. Wao
walitegemea hata usiku uleule angemtafuta Phina wazungumze, lakini imekuwa
kimya. Wao wanahesabu kuwa ni dharau. Ndio maana wamekuja hapa na wapo tayari
kwenda mbele ya haki zaidi. Ni hilo tu.” “Nashukuru. Asante. Nikutakie jioni
njema.”
Akakata.
Kwa Mzee
Msindai.
M |
zee Msindai akiwa katikati ya kuona wagonjwa wake
ambao ni watoto, akaona simu ya mkewe. Kabla hajatoa salama. “Saa mbili kamili, nataka kukuona hapa nyumbani wewe na
watoto wako wote bila kukosa.” “Leo nina wagonjwa mpaka saa nne, mama! Kwa
nini…” “Na Msindai, namaanisha saa mbili kamili na watoto wako wote.
Nisipomuona mtoto hata mmoja hapa!” Mama Msindai akaweka mkwara. “Junior ndio amerudi leo, mama. Hata nyumbani hajakwenda. Kwa
nini hicho…” “Hawa watoto wananidharau mimi! Junior hapokei simu zangu lakini
anazungumza na wewe! Na Jacinta hivyohivyo! Jackson ndio simu zake zote hazipo
hewani. Msindai onya watoto wako!” “Saa mbili na nusu tutakuwa hapo mama.
Lakini wewe ni mzima?” Simu ikakatwa.
Kabla hajasahau akampigia
simu Jacinta haikuita hata mara mbili, akapokea. “Baba
mzazi!” “Naomba muunganishe na Junior.” Mzee Msindai akaendelea na mtoto
aliyekuwa naye hapo akimuhudumia. Jacinta akamuunganisha kaka yake kwa haraka. “Mama yenu ameagiza saa mbili na nusu amuone kila mmoja wenu
pale.” “Kuna nini tena baba jamani! Mimi ndio nimerudi tu, hata sijamuona mke
wangu!” Junior akalalamika. “Linaonekana ni
jambo la msingi hawezi kusubiri. Na Jacinta.” “Nipo baba.” “Jackson
hapatikaniki kwa simu. Naomba taarifa zimfikie, na hakikisha saa mbili na nusu yupo
nyumbani.” ‘Sawa baba.” Jacinta akakubali. “Sasa
mimi nipo na kijana mzuri sana hapa. Anataka niendelee kuzungumza naye.
Nitawaona nyumbani.” Hiyo simu nayo ikakatwa. Junior akajua ndio ni
lazima kuhudhuria kikao.
Kwa Sabrina.
Akiwa ananyonyesha
mwanae, ukaingia ujumbe kutoka kwa mama mkwe. ‘Kuna
kikao cha familia saa mbili na nusu usiku wa leo. Tafadhali fika bila kukosa.’
Sabrina akasoma na kutulia akifikiria. Akataka asiende, lakini rohoni
akasukumwa kwenda. Akajibu. ‘Sawa mama.’ Hapakuwa
na ujumbe mwingine. Na yeye akatulia tu. Mpaka hapo hakuwa amemuona Jack.
Bahari
Imetibuka.
K |
wa makusudi kabisa, Sabrina akachelewa kwenda
kama kwa dakika 10 hivi hakutaka awahi hapo ajikute na huyo mama peke yake,
wengine hawajafika. Kwa kuwa aliwajua familia hiyo ni watunza muda, akajua
baada ya hizo dakika kumi, wote watakuwa hapo. Dereva akamshusha nje. Akakuta magari
yote mpaka la Jack. Akaingia. Tokea yupo mlangoni alikuwa akimsikia mama Msindai
akigombesha wanae. Sabrina akajivuta taratibu alipoingia tu hapo mzee Msindai
akamuwahi. “Karibu mama.” “Asante baba. Shikamoo.” “Marahaba. Umeacha wapi
wenye mji?” “Nimeona nikija na ile timu yote, hatutasikilizana hapa. Brayan
siku hizi anapatwa wivu akiona nimemshika mdogo wake. Analia na yeye anataka
nimbembe.” “Amepokonywa ziwa je! Lazima alie wivu.” Akadakia Jacinta na kufanya
kidogo atulie.
“Wengine wote shikamooni.
Mama samahani nimechelewa kidogo.” “Hamna shida tunaelewa. Na wala hujachelewa
sana. Maana nilikuwa nikizungumzia swala la mawasiliano. Naona kuna kupuuzwa.”
“Kwa hilo tumelielewa mama. Na tumeomba msamaha.” “Hamjaomba msamaha. Acheni
kunifanya mimi mtoto mdogo. Mnapuuzia simu zangu halafu..” “Sabrina mama, kaa. Kaa
chini.” Mzee Msindai ikabidi aingilie. Jack alikuwa ameinama.
“Asante.” “Karibu Shem.
Umetukuta katikati ya kikao. Karibu sana.” Akaenda kukaa pembeni ya Jacinta
ambako kulikuwa na nafasi, Jack alikuwa ameinamia magoti, anachezesha mguu
mmoja kwa wasiwasi. “Mama, samahani kwa kutopokea simu. Nilikuwa katikati ya
mambo mengi. Nimetua tu nchini na kukimbilia mambo ya ofisi hata nyumbani
sijafika.” “Mimi nilikuwa na vikao siku nzima. Na asubuhi pia natakiwa kuwahi
Pugu. Hivi itabidi kuwahi kuondoka.” “Muongo Jacinta. Anachaguaga simu za
kupokea. Tunakujua sana tu.” Jena akaingilia. Jacinta hata hakumjibu. “Kwani
mimi simjui! Anachagua simu ipi apokee na kwa wakati wake yeye ndio anaweza
kurudisha simu uliyompigia.” “Samahani mama.” Jacinta akamuwahi ili asiendelee
kulalamika.
“Wala humaanishi! Unanifunga
mdomo tu ili nifanye haraka uondoke.” “Mtoto ameomba msamaha mama, si..” “Hata
iweje hutaacha kumtetea Jacinta, wewe! Hata kama ana kosa, basi unaona bora
wewe ubebe kosa lake yeye aachwe. Lakini hivyo unavyofanya Msindai si sawa.”
Mzee Msindai akanunua ugomvi. “Hawa watoto wananidharau mimi na wewe unajua,
huwakemei! Junior anarudi tu hapa nchini anakutafuta wewe kukupa ratiba zake
zote, mimi hajanijulia hata hali wakati hajawasiliana na mimi kwa muda mrefu
sana!” “Nilikupigia simu juzi usiku mama! Labda kama umesahau.” “Juzi usiku
ndio leo?” “Nimeomba msamaha mama yangu.”
“Hata mimi naomba tena msamaha
mama. Halafu nina swali.” “Jacinta wewe mtoto!” Mama yake akamnyoshea kidole
kumuonya kwa ukali. “Jamani baba!” Jacinta akamgeukia baba yake akitaka tena
utetezi. “Sio ungemsikiliza swali lake kwanza!” Kama kawaida yake hapo mzee
Msindai akaingilia tena. “Najua swali lake. Hapa ni nyumbani kwangu. Mimi ndio
nimewaita. Naongoza mimi kikao. Sitaki kuulizwa kama hili ndilo nililowaitia.
Nachagua ni wapi nianzie na wapi nimalizie.” “Kuwa huru mama. Hapa kwako na
sisi watoto wako, lazima tukusikilize.” Jena akawakera kwa makusudi. Sabrina
kimya. Alishaijua hiyo familia. Akabaki ametulia tu. Jacinta akajirudisha
nyuma, akatulia. Mama Msindai akalalamika mpaka akamaliza.
“Sasa tumepata tatizo
linaloonekana limekwenda mbali tena kwa kasi. Nishapata simu zaidi ya tatu kwa
muda mfupi tu. Inaonekana inasambaa vibaya sana.” Hapo wote wakaongeza umakini.
“Jack ameingia matatizoni.” Hapo akamuumiza Sabrina. Kwa jinsi alivyoongea, ni
kama ilikuwa ajali! “Matatizo gani!?” Akauliza mzee Msindai na wote
kumgeukia Jack. Alionekana amejawa wasiwasi haswa, mguu anachezesha bila kutulia.
“Na katika hili lazima
kusimama kwa pamoja. Sisi wote tuwe pamoja. Nikimaanisha mpaka Sabrina
anatakiwa awe ukurasa mmoja, na asimame upande mmoja na Jack, ili kulinusuru
hili jambo “Naomba muache Sabrina, mama.” Jack akaingilia. “Kama ungekuwa
unataka kumlinda tokea mwanzo, usingefanya umalaya hovyo.” Hapo akamtibua mama
yake. “Ulipokuwa ukilala na wanawake bila kinga, ulitegemea nini?” “Ni bahati
mbaya mama! Sio kwamba ni kitu nilipanga ndio kikatoke!” Jack akajiteta. “Twende
taratibu. Kuna nini kinaendelea!?” Akauliza mzee Msindai.
“Nimetoka kuzungumza sasa
hivi na mama Mkapa. Yani hii habari imeenea na yeye amenipigia simu akimiambia
lazima tukae kama familia tulizungumze na tuwe ukurasa mmoja. Phina huyo
aliyepewa mimba na Jack, na Ibra huyo anayemsindikiza Phina kila mahali,
wamekusudia kumuangamiza Jackson kabisa. Walianza jana usiku nyumbani kwa Jack
mpaka wakampa mkewe uthibitisho wa Jack kuwa na huyo Phina huko Uswiz
walipokuwa wamelala mpaka akashika hiyo mimba. Na picha hizo za Ultrasound za
ujauzito zinazoonyesha umri wa huo ujauzito kulinganisha na tarehe za kwenye
picha zao huko Uswiz. Sasa aliyenitafuta wa kwanza ni mtu aliyemsikia Phina na
Ibra huko Ustawi wa Jamii wakilalamika kuwa Jack amefungia simu za Phina zote
baada ya kulala naye.” Mama Msindai akaeleza yote mpaka mwisho.
“Wanaonekana wanasambaza
haya maneno makusudi eti wanahofia tusije kuwaziba mdomo.” “Tafadhali sana mama
J. Siku nyingine unaponiitisha kikao cha dharula na watoto, kiwe kikao cha
dharula kweli.” Mzee Msindai hapo akawaka mpaka akashangaza wanae. “Hii ni
dharula Msindai!” “Dharula ni ile niliyoacha watoto wagonjwa, ili kuja hapa
kuzungumzia starehe za mtu mzima huyu aliyeamua kuishi kama mnyama tu!”
“Usiseme mtoto ni mnyama, Msindai! Hili jambo limetoea. Bahati mbaya zipo na
Jackson sio wa kwanza. Mtoto atakayezaliwa ni Msindai kama kina CJ. Atataka
kujua familia yake na kukuzwa kama watoto wote wa wakina Msindai humu ndani,
ajue ndugu zake na asili yake.” Hapo akawa kama amewasha taa ambayo hakuwa hata
akiifikiria kwenye fahamu za Sabrina. Akakaa sawa akimtizama mama Msindai
anachokizungumza.
“Na Phina mwenyewe
anaonekana yupo tayari kuwa mmoja wa hii familia. Mtoto wake awe Msindai
kwelikweli. Kwa hiyo lazima kuwa upande mmoja kujua jinsi ya kulikabili hili.
Kulimaliza kifamilia.” “Narudia tena mama J. Umenikosea na hili sitalinyamazia.
Hatuwezi kuokoa kazi ya mtu ambaye amekataa kuwajibika kwenye jamii, huku
tukiharibu kwa wengine. Uliponipigia simu nilikwambia kabisa, ninao wagonjwa wakuwaona
mpaka saa nne usiku. Inamaana usiku huu sisi tukiwa hapa tukijadili starehe
zake huyu aliyechagua kuwa mbinafsi, akifuatisha tamaa zake za mwili kama
mnyama tu, bila kujali familia yangu nzima ya Msindai, yupo mama anahangaika
usiku huu na mtoto mgonjwa! Nimerudisha watoto wagonjwa kwa ajili ya upuuzi
huu! Isiwahi kurudiwa tena.” Hapo kila mtu akajua kwa mara ya kwanza mzee
Msindai amekasirika kupitiliza. Hakuna aliyewahi kumuona hivyo, hata mama
Msindai hapo akanyamaza.
Akanyanyuka, akachukua
funguo zake za gari na kutoka. Pakazuka ukimya. “Jamani, nilikuwa safari kwa
muda mrefu, sijamuona mke wangu. Nimemuomba anisubiri, asilale mpaka nifike. Naomba
na mimi niwahi nyumbani.” Junior akasimama. Hiyo haikuwa ishara nzuri kwa Jack
hata kidogo. Junior hajui kumnawia mtu mikono. Inamaana katika hilo hakuwa na
la kusema. “Na mimi kama nilivyosema mwanzoni, kesho natakiwa PUGUUUU!” Jacinta
naye akasimama.
“Kwa hiyo mnamkimbia
mtoto?” “Kwa jinsi nilivyokusikiliza tokea mwanzo, wewe mama hutahitaji msaada
wetu hata kidogo. Unaonekana ushafikiria hiki alichofanya Jack. Umeshamtetea,
usha.” “Sija..” “Si umetaka kusikia? Basi subiri.” Jacinta naye akawa mkali
gafla. “Mbele ya mkewe hapa, umesema yeye sio wa kwanza. Phina ametaka kuwa
mmoja wa familia yeye na mtoto wake. Sisi tuwe ukurasa mmoja ili kuunga mkono hiki
kitu. Kuna nililoongeza hapa au unataka sisi tubishe, halafu na wewe ubishe kwa
hasira mwishoe wewe ndio uonekane mshindi, kwa kuwa kile ulichotaka kimekua?”
Jacinta akauliza kwa ukali kabisa.
“Familia umesema ni yako.
Umetoa muongozo kile unachotaka kifanyike, tena kwa baraka zako. Ulitaka wote
tukwame hapa tukibishania starehe za mwanao huyo! Na kukusaidia tu, mimi
sitaingia aibu kwa starehe za Jack, wala haitakuwa Junior. Junior anajulikana
kwa kuthibitishwa na kila mtu, halali na mwanamke isipokuwa mkewe na ndio maana
iliposikika tu mipango ya Max na mkewe, watu walinifuata haraka kuniambia
wanataka kumuharibia kiongozi. Uungwaji mkono niliopata mpaka mimi mwenyewe
nikashangaa. Watu wanajitolea kwa Junior kupita nitakavyokwambia wote mkaelewa.
Linapofika swala la Junior mpaka mimi huwa nashangaa, na wala sihangaiki. Watu wanamuhangaikia
mimi naletewa ripoti tu. Kwa hiyo usiwe na wasiwasi juu yetu. Kila mmoja
atabeba msalaba wake mwenyewe.” Jacinta akachukua pochi yake na kuondoka.
Akafuata Junior, akatoka kwa haraka kama akimbie.
Akabakia hapo mama
Msindai, Jena, Jack na Sabrina. Sabrina kimya. “Sasa wanazira nini? Kwani wao
hawakosei! Wanajidai watakatifu!” Jena akaanza. “Hata wakizira huyo mtoto
atazaliwa na yeye atakuwa Msindai tu.” “Na hilo ndilo nilitaka tuwekane sawa,
lakini naona kama…” “Wewe mama usiyumbe. Maji yashamwagika, hayazoleki. Sisi
nikuendelea. Mimi mwenyewe nitamtafuta Phina. Kwanza msichana mwenyewe mzuri
yule. Moyo wake safi, hana shida. Nitazungumza naye na kumkaribisha kwenye
familia. Hata babyshower ya mtoto mimi nita…” “Acha kuzungumza ujinga
Jena!” “Ujinga ni upi kati yangu mimi niliyekubali ukweli bila shida au nyinyi
mnayetaka kufanya mambo yakuzwe? Na kwa taarifa yako tu, kwa kadiri
unavyojichelewesha kwenye kukubali ukweli, ujue unajiharibia mwenyewe. Pokea
mtoto wako, tunza damu yako.” “Jena yupo sahihi.” Mama Msindai akadakia.
“Jamani wakati nyinyi mnapanga
mipango ya Phina na Msindai mpya, naomba mimi nikaendelee na yangu. Ila naomba
nitoke na Jack kidogo.” “Sasa unaondoka na Jack…” “Atarudi wala usiwe na
wasiwasi Jena.” “Mimi sina wasiwasi ila..” Sabrina akachukua pochi yake wakati
anataka kutoka, Jena akamuwahi tena. “Unadharau na utaona tutakachomfanyia
Phina. Wewe si ulikuwa ukiringa kama vile ni mwanamke peke yako kwa Jack? Sasa
Jack mwenyewe amekuonyesh....”
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Itaendelea…
0 Comments:
Post a Comment