Sabina akiwa ofisini
kwake, siku ikiwa imeanza kama kawaida, akasikia ana mgeni mapokezi. Akatoka
akiwa hana hili wala lile kumbe arobaini zake zimefika. Alipofika tu
mapokezi akadakwa na askari. Wakamfunga pingu na kumwambia yupo chini ya
ulinzi. Kabla akili haijakaa sawa, Sabina akavutwa vibaya sana na kupakizwa
kwenye difenda ya polisi, watu wote wasielewe. Ni Sabina, mdada wa kuheshimika
sana hapo kazini! Alipoingia tu garini akafunikwa kichwa asiweze kuona atakapopelekwa.
Askari mmoja akaamuru pochi yake na vitu vyake vingine vyote viletwe hapo. Wafanyakazi
wenzake wakasaidiana kukusanya vitu vyake vyote na kuwakabidhi hao askari
lakini lengo ni kupata simu yake ili kujua mawasiliano yake na Tino.
Walipojiridhisha kwenye hivyo vitu ipo simu yake, ndipo wakaondoka.
Gari ilitolewa pale kama
amekamatwa jambazi sugu anapelekwa kufungiwa. Akiwa hajui ni kwa nini anakamatwa,
maana ni kweli walijitahidi sana kuwa makini kwenye mipango yao wakijua
wanasikilizwa, Sabina asijue watu wa Usalama wa Taifa wapo kila mahali na
huwezi kuwatambua kwa kuwaangalia. Japokuwa alikuwa akifanya kazi kwenye
kampuni ya kutoka nje ya nchi, lakini walikuwepo pia watu wa Usalama wa Taifa
wakifanya nao kazi wasiwajue. Na wenyewe walikuwa wakiendelea kumchota taratibu
kujua kila kitu kinachoendelea na yeye alikuwa akisema kwa kujisifu, asijue
alikuwa akijishitaki wakati wote.
Sabina alipelekwa sehemu
na kufungiwa kwenye chumba, asijue alipo ila hofu. Aibu ya kutolewa
vibaya sana mbele ya watu akiwa ofisini! Akabaki akitetemeka kwa hofu zaidi ile
yakuvutwa na kutupiwa kwenye hicho chumba chenye giza, kikatili. Wakati amekaa
hapo chini sakafuni, akaingia mtu na kuamuru taa iwashwe. Ikawashwa. Alionekana
mtu mwenye mamlaka mpaka akamtisha Sabina. “Upo chini ya ulinzi kwa kosa la
kula njama za kufanya uhalifu. Unajihusisha na mtuhumiwa anayeshikiliwa na
makosa makubwa na hatari sana kwa jamii ikiwepo kusudio la kutaka kua. Njama ya
kumuangusha kiongozi mkubwa sana, aliyeaminiwa na raisi wa nchi yetu. Kwa kuwa
yeye ameshikiliwa yupo ndani, anashindwa kuhitimisha nia yake, wewe ndiye
anayekutumia kufanya uhalifu huku nje. Kutaka kuangamiza watoto wasio na hatia
pamoja na uchochezi.” Sabina alikuwa akilia sana huku akibisha.
Akamtolea picha zake
akiwa gerezani akizungumza na Max. Zaidi ya mara moja. Siku zote alizokuwa
akienda kumtembelea Max, alikuwa akipigwa picha akiwa na Max mwenyewe na wakili
waliyemtafutia Max. “Je, unapinga kwamba huyu sio wewe?” Sabina akaendelea kujitetea
huku akilia akisema safari zote alizokuwa akimtembelea Max, zilikuwa za
kirafiki tu. Akaanza kusikilizishwa mazungumza yao alipokuwa akimtembelea Max huko
rumande. Sabina hakuamini vile alivyokuwa akijisikia vizuri bila shida wakati akimshawishi
Max akubali kusimama na Tino, apinge shutuma zote anazotuhumiwa na aseme
anamjua Tino na Sabrina kwa muda mrefu.
Alimtaka aseme kuwa alikuwa
nao hao wawili tokea mwanzo wa mahusiano yao, pale Lela alipomtelekeza Tino.
Tino alimpenda sana, ila Sabrina ndiye aliyekuja kumgeuka Tino pale alipoondoka
tu nchini kwenda kwenye matibabu, na kumpa watoto Jack. Akajisikia vile
anavyomuhakikishia Max kuwa endapo atamsaidia Tino katika hilo, na akaweza
kupata watoto wake, basi Tino atalipia garama zote za mwanasheria wa aina
yeyote anayemtaka yeye, atakayemtetea mpaka na yeye akashinda kesi dhidi ya
Msindai pia.
Kisha akajisikia tena vile
alivyomwambia Max kuwa, Tino ameahidi kumlipa yeye malipo makubwa zaidi pindi atakapopata
watoto wake. “Mimi ndiye ninayemuwakilisha Tino hapa
nchini. Sasahivi anafanya chochote ninachomwambia mimi. Ukikubali tu, ujue
maisha yako yamebadilika Max. Usiogope.” Akajisikia vile alivyokuwa
akiweka ushawishi zaidi na zaidi ili Max amkubalie. Hapo Sabina akaongeza sauti
kama aliyefiwa na mama yake mzazi.
Kisha akasikilizishwa tena
mazungumzo kati yake na Lela pia. Sabina akajisikia vile alivyokuwa akimchochea
Lela, akimwambia kishabiki kuwa asikubali hata kidogo. Hata kwa kuandamana,
adai haki yake. Tino amlipe zaidi ya alivyolipwa wakati wa kutengana. Hapo
Sabina akazidi kulia na kuogopa zaidi. Hata yeye alijisikia vile alivyokuwa
akizungumza kama aliyepagawa akichochea mambo ambayo hata hayakuwa yakimuhusu! “Wewe
ni mvunjaji wa amani, kwenye nchini yenye amani. Wewe ni mchochezi. Unakula
njama na wauaji.” Sabina alikuwa akilia, akashindwa hata kujitetea zaidi maana
alipewa ushahidi ambao hakuwa hata akihisi kama walikuwa wakirokodiwa na watu
wa Usala. Ukweli walijitahidi kuwa makini ili hicho kinachotokea, kisitokee.
Wakasahau kina Msindai masikio yao yapo kila mahali, ni kiasi cha kusikiliza
tu.
Yule aliyekuwa akimsomea
mashitaka akatoka na kuamuru taa izimwe tena kitu kilichomuongezea hofu zaidi. Alikuwa
akitetemeka kwenye chumba hicho kibaya, ila kilikuwa na baridi ya kawaida tu,
lakini yeye alihisi ni kama amewekwa kwenye friji. Giza na akawa peke yake
asijue alipo. Alikuwa akitetemeka kana kwamba amepigwa shoti ya umeme mpaka
meno yalikuwa yakigongana.
Mama Kundi.
J |
acinta alipoachiwa afanye vile anavyojua yeye
kuharakisha mambo, hakutaka kuchelewa zaidi. Wakati askari wake wakimkamata
Sabina, tayari alishatuma wengine Dodoma. Wakamfanyia kama walivyomfanyia
Sabina. Mama Kundi akiwa ofisini, hata kazi zenyewe hakuwa akifanya kwa hofu na
mawazo ya kile kinachowakabili yeye na mumuwe, askari wakamtia pingu. Ila sasa
yeye ikawa tofauti. Aliwekwa nyuma ya gari, safari ikaanza. Alishangaa ule
mwendo kasi, asijue anapokwenda ila akashangaa hawafiki. Baada ya masaa kama
mawili kupita ndipo akili ikamjia kuwa, anarudishwa Dar. Mama huyo alikuwa
amejawa hofu kupitiliza kwani yeye alishayajua makosa yake, ila akashangaa ni
kwa nini hakuwa amekamatwa bado mbali ya kuhamishwa kituo cha kazi!
Siku
hiyo ndio akajua arobaini zake zimefika. Akatulia hapo garini akitamani
mauti imfike, shutuma zake zisije someka magazetini. Alikuwa akilia akihurumia
watoto wake na aibu watakayoingia. Uzuri walikuwa na watoto wakubwa na wanaojua
maisha. Waliwaacha pazuri kimali. Ila aibu ya wazazi wao baada ya uovu waliokuwa
wakipanga kuja kuwekwa hadharani, huyo mama alisononeka na kujuta sana. Kwa
upande fulani yeye alijua hiyo siku ingeweza kufika ila akawa akimsihi Max
asimamie kwenye kuomba msamaha na kukiri kutorudia tena, asijue Sabina na
wakili waliyemtafutia mumewe waliuza sera zao mpaka mumewe akapotea lengo. Kwa
mara ingine tena, Max anamuingiza matatizoni.
Gari
iliendelea kwenda mpaka akasikia likisimamishwa kwa ajili ya kuongezwa mafuta.
Akaulizwa kama angetaka kujisaidia. Akakataa. Baada ya hapo, gari liliondolewa hapo
ikaendeshwa kwa masaa kadhaa, mpaka sehemu fulani. Ikasimamishwa tena,
wakaingia askari wengine wawili hapo nyuma alipokuwa ametupwa tu, na kuachwa
peke yake amelala chini na pingu zake mkononi kwa muda wote tokea wanatoka
Dodoma. Kisha hiyo gari ikaondolewa tena. Aliweza kuona kwa kuchungulia kwa
chini ya ile soksi aliyokuwa amefunikwa kichwani, wale askari walikuwa
wamesimama kabisa. Gari ikaondolewa tena kwa mwendo kasi mpaka baada ya kama
dakika 45 hivi, akaanza kusikia hiyo gari ikipigwa honi mfululizo kama
inayotaka ipishwe barabarani. Akajua wameshaingia Dar na ndio maana
waliongezeka askari wenye risasi kuongeza ulinzi. Mama Kundi alikuwa
akitetemeka vilivyo asiamini kama na yeye amegeuka kuwa kama jambazi!
Na
yeye akashushwa na kwenda kutupiwa kwenye chumba chenye giza. Hata alipotolewa
ile soksi kichwani, hakuwa akiona kitu. Alikaa hapo akitetemeka kwa hofu mpaka
baada ya masaa kama manne mbeleni. Akaingia mtu hapo ndani na kuamuru taa
iwashwe. “Uko chini ya ulinzi kwa kosa la kukusudia kutenda kosa la kumsingizia
UBAKAJI, kiongozi aliyeteuliwa na raisi, na kupewa majukumu mazito ya kiserikali.”
Mama Kundi alikuwa akitetemeka nakushindwa hata kujibu. Na yeye
wakamsikilizisha mazungumzo yake na mumewe siku Max alipompigia akiwa na hasira
ya Jackson uwanja wa ndege. Yule mama alijisikia vizuri kana kwamba walikuwa
wakizungumza kwenye kipaza sauti. Akajisikia jinsi alivyokataa mwanzoni na
kumuonya mumewe. Mumewe akasikika kuweka ushawishi mpaka akakubali kabisa
mipango ya kumtoa Waziri Misindai mjini. Hapo mama Kundi alilia sana. Yule
aliyemsomea mashitaka akatoka na kuamuru taa zizimwe tena. Akabaki peke yake.
Tino.
S |
iku Tino anatua nchini hakuwa akijua kama
anasubiriwa vilivyo. Usalama wa Taifa walikuwa hapo muda muafaka wakisubiria
ndege yake ifike. Akiwa uwanja wa ndege akisubiria mizigo yake ili atoke
uwanjani hapo, akasogelewa na askari wanne. “Wewe ndiye Costantino?” Tino
akashituka kidogo. “Tufuate.” “Mnanipeleka wapi!?” “Tumesema ongozana na sisi.
Au unataka tukuvute?” “Hapana! Kwani nimefanya nini!?” “Twende.” Wawali
wakatangulia, Tino akafuata, wengine wawili wakafuata nyuma. Tino alijua mambo
yameshaharibika, na yeye arobaini zake zimetimia.
Wakamuingiza kwenye moja
ya chumba hapohapo uwanja wa ndege ambapo nje kulikuwa na mbwa wakubwa wale wapolisi wanao tumiwa kunusa ili
kujua kama kuna kitu kimefichwa mahali hata kama ni ndani sana. Akakuta
masanduku yake yote yapo juu ya meza. Akazidi kuchanganyikiwa. “Haya ni masanduku yako?” “Ndiyo! Kuna nini!?” “Hati
yako ya kusafiria inaonyesha sasahivi unatokea nchini Italy. Na umeingia nchini
na kutoka kwa muda mfupi sana zaidi ya mara 5. Unaweza kueleza unajishugulisha
na nini?” “Kwanza kwa nini mnihoji juu ya maisha yangu binafsi!? Inawahusu
nini?” Wakaangaliana kisha wakamtizama kwa cheko la kejeli kama vile kumwambia tutakuonyesha.
Akafunguliwa sanduku lake
moja, vitu vyake vyote vikatupwa mezani kishwa akaonyeshwa kuwa chini kabisa
kulichanwa. “Sisi ndio tulichana hapa baada ya mbwa kupata harufu ya hii na
mashine kuthibitisha kuwa umeficha bidhaa haramu.” Akaonyeshwa mfuko wenye
madawa ya kulevya. “No way! Hayo sio madawa yangu.” “Lakini umesema masanduku
ni yako. Si ndivyo?” “Hilo sanduku ni langu lakini madawa si yangu!” “Kwa hiyo
haya madawa yamejiingiza tu humu ndani?” “Hapana. Yupo aliyeyaweka hapo lakini
sio mimi.” Tino akazidi kuingiwa hofu. “Costantino upo chini ya ulinzi kwa kosa
la kuingiza chini madawa ya kulevya.” Tino akafugwa pingu na kutolewa pale kama
mtuhumiwa na yeye akaenda kufungiwa sehemu peke yake.
Yeye walimfanyia tofauti.
Sababu alianza kwa jeuri, walimuacha siku hiyo nzima bila mtu kumzungumzisha. Na
siku ya pili nayo ikaisha akiwa peke yake. Gizani haswa hajui kama huko nje ni mchana
au usiku. Hofu iliyokuwa imemkamata Tino, alishindwa hata kufunga macho gizani.
Baada ya siku tatu kujua jeuri yake imeshuka na ameelewa ipo nguvu kubwa juu
yake hapo nchini ndipo na yeye akafuatwa na mtu yuleyule aliyewasomea mashitaka
Sabina na Mama Kundi.
Likaanzwa kosa la kuingiza
madawa ya kulevya nchini. Hilo alionyweshwa ushahidi wa picha. Sanduku lake
lilivyochanwa, akaonyweshwa madawa ya kulevya yakiwa kama yamefichwa chini
kabisa ya hilo sanduku lake. Tino akazidi kuingiwa hofu na kujua hana jinsi ya
kujitetea tena maana wazi yale madawa yalionyeshwa ni kama kweli yametolewa kwenye
sanduku lake bila ubishi.
Akasomewa shitaka la kusudio
la kutaka kuua watoto aliokuwa amebeba Sabrina. Akaonyeshwa ushahidi wa malipo aliyomlipa
yule daktari wakiwa moshi na ukiri w daktari mwenyewe. Akasikilizishwa
mazungumzo yake na Max alipomshawishi arudi nchini kudai watoto, akakataa
akisema watoto ni wa Sabrina. Lakini akaja kuitishia familia ya Msindai mpaka
wakamuwekea restrain order, ila baadaye kukiuka onyo hilo la kutosogelea
watoto wa Sabrina na Jackson Msindai. Akaambiwa tarehe na muda aliochukua
watoto wa Sabrina akisaidiwa na Sabina kinyume na matakwa ya wazazi wao.
Akaonyweshwa picha zake akiwa na hao watoto siku na tarehe yenyewe ikionekana
pichani. Tino alishituka, hakulitegemea hilo. Asijue utafiti ulifanyika mpaka
wakajua hoteli waliyokwenda siku hiyo, na kuamuru hoteli kuangalia kwenye
kamera zao za ulinzi wakitishwa kuwa wao ni Usalama wa Taifa. Walipowaona wakatoa
hizo picha kama ushahidi. Hapo walizidi kumuogopesha Tino.
Lakini akajikaza na
kujitetea. “Jackson Msindai alitelekeza watoto wangu. Nyinyi mlitaka niache
damu yangu ipate shida kwa kuhofia restrain Order? Kipi bora, mimi kuwa jela,
au kuwa huru na kuendelea kutesa watoto ambao nilishatenda kosa?” “Utapata
nafasi ye kujitetea mahakamani. Hiyo ni haki yako ya msingi, lazima utapewa.”
Akamjibu hivyo na kuendelea na kosa jingine.
Akamtajia kosa la kumsaidia
kifedha, akiwa ameshamtafutia na kumlipa wakili atakayepinga mashitaka ya muhalifu
Max. Yeye Tino akitaka Max awekwe huru ili amsaidie kuendelea kuifanyia fujo
familia ya Jackson Msindai akitaka kuiba watoto wake ili baadaye, yeye na Max
sasa, waje watimize kusudi la kutaka kuua watoto hao. Akaonyeshwa picha
alizotumiwa mwanzoni kabisa na Max, wakati mapacha wa Jack ni wadogo na ukiri
wake mwenyewe kuwa watoto si wake ni wa Sabrina. Akaonyeshwa kopi ya restrain
order aliyopewa na kusaini kuwa alipokea onyo hilo alilopewa, baada ya
kujipinga yeye mwenyewe aliposema, watoto si wake ni wa Sabrina lakini
akarudi kudai watoto hao kwa vitisho. Akaonyeshwa tena picha ambazo alishawahi
kwenda kumtembelea Max rumande. Mpaka anamaliza kumsomea mashitaka yake, Tino
akajua ndio mwisho wake wa uhuru hapa duniani.
Kwa
Sabrina.
S |
abrina akawa kama amejionya, akataka kutulia
kabisa asiharibu hiyo mimba. Akawa mtu wa kulala kama vile alivyokuwa akifanya
Pendo. Hajigusi kwa chochote, na hatoki hapo ndani. Alikuwa amebakisha siku
kama tano tu ili afikishe majuma 38 ambayo daktari alimwambia hawatasubiria
uchungu, ila kutoa huyo mtoto. Akawa na kazi ya kula na kulala tu. Hata simu
akafunga kabisa ili asisikie lolote isije kujipandisha pressure. Siku mbili
kabla hajaenda hospitalini kujifungua, usiku ikabidi azungumze na Jack. “Tokea
najifungua mapacha mpaka Brayan, hapajawahi kutokea amani ninapokuwa
hospitalini nikijifungua. Nimekuwa nikifuatwa na maneno yakuniumiza tu bila
sababu. Safari hii tulikataa babyshower tokea mwanzo na wakaelewa. Sasa naomba ukawaongezee
na hili, SITAKI mtu kule hospitalini.” Jack akashangaa sana.
“Haiwezekani Sabrina!”
“Hakika hakikisha inawezekana Jackson. Na katika hili sitaki utani wala
masihara. Wanataka mtoto, wasubiri nijifungue. Mungu akinitoa chumba cha
upasuaji salama, na mtoto akatoka salama, tutarudi hapa. Ndipo waje hapa waone
mtoto. Najua hapa hata wakiwa na lakunisema, watayakusanya yote, watasubiri
wakanisemee makwao sio hapa kwangu.” “Na baba kuangalia mtoto?” “Tungekuwa
Singida angefanyaje?” Jack kimya akifikiria.
“Maana hii mimba
nilishika tukiwa Singida na tukasema tunyamaze waje washitukie tuna mtoto
mwingine. Sasa kilichobadilika hapa ni nini?” Jack kimya. “Mimi sitaki fujo
Jack. Kwanza ni mtoto wa nne. Najua kila kitu. Halafu Mungu amenipa Pina,
ananijulia mimi na makinda yangu yote. Huyu msichana mwingine atafanya kazi za
humu ndani akisaidiana na kaka. Nishapanga timu yangu, wote wameelewa. Sitaki
msaada wa mtu mwingine yeyote yule maana ndio wanakuja kunisimanga baadaye.
Mungu amenihurumia amenipa hao watu, inatosha.” “Chakula?” “Nitakula cha
hospitalini pamoja na uji atakao kuwa akinipikia Pina na kumpa Chali au wewe uniletee
hospitalini. Nimemaliza.” “Hata Pendo pia?” “Huyo nishazungumza naye na
ameniunga mkono kwa asilimia 100. Wanachofanya wakija hospitalini nikiwa
najifungua ni kunitesa tu. Sitaki mtu. Mungu atamsaidia mwanangu atazaliwa
salama hatahitaji hekaheka za madaktari kama za Brayan.” Jack akapoa.
“Hakika naomba uniahidi
utalisimamia hilo Jack.” “Sasa hata mama nisimwambie?” “Utampelekea watoto.
Lasivyo nikwambie kabisa Jack, kesho mimi naondoka nakwenda kujifungulia
Singida, nikatulie kabisa kule. Sitaki fujo mimi.” “Basi nitawaambia kama
unajifungua ila nitawaambia wasije hospitalini.” Sabrina akanyamaza.
“Sasa mbona hujibu?”
“Nishaona wewe utanisumbua. Acha tu kesho mimi niondoke. Nakwenda kuzungumza na
yule daktari wangu wa Singida, anisaidie kujifungua. Nikipata nguvu ndio nakuja
huku.” “Basi Sabrina.” “Unataka kunichanganya bila sababu Jack. Kuna ulazima
gani wakuwaambia kuwa najifungua kama vile yupo mtu ananijali sana, kwamba
atakuulizia Sabrina yuko wapi, kama si kutaka kunijazia watesi wangu
pale hospitalini?” “Lakini ni kama wamebadilika.” “Basi ndio wasubirie na wewe
utulie.” Akanyamaza.
“Jackson Msindai?” “Basi
hata tuagane.” “Hapana Jack. Wewe unakwepa kuahidi tu. Niambie kama umeelewa na
ume..” “Sasa si tuagane kwanza?” “Hapana. Tunaagana hapa kila siku na
hatumalizi! Leo tufunge huu mjadala.” “Sawa nimeelewa. Hutasumbuliwa.” “Acha
kujibu harakaharaka ili uanze michezo yako bwana, Jack!” Jack akaanza kucheka.
“Michezo yetu mama. Mbona unajitoa wakati na wewe nakuona siku hizi mpaka
asubuhi unakumbushia kuagwa!” Sabrina akacheka sana. “Naona kila siku hali
inabadilika! Hakika sitoki chumba cha upasuaji bila kufunga kizazi, lasivyo
baada ya miezi 9, habari hii itajirudia.” Wakakubaliana na Jack itoshe hivyo.
Mungu amewapa watoto wanne, itoshe. Wawili hao makubaliano hayo yakasindikizwa
na penzi, wakiambiana wanaagana. Maana Sabrina anakwenda kujifungua kwa
upasuaji kwa maana ingine inabidi wasubiri mpaka apone.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kwenye mida ya saa nne
asubuhi siku ya kujifungua kwa Sabrina, Jack akiwa anatokea kazini akamfuata
hospitalini maana Sabrina alipelekwa na dereva tu, akamwambia amuache hapo.
Lakini Chali alikuwa akipatana na kila mtu hapo kwa Sabrina. Akamwambia
atamsubiria mpaka aone atakapolazwa ili apate mtu wa kumtuma kabla hajapelekwa
wodini. Sabrina hakukataa akajiambia inawezekana hayo ndiyo maagiza aliyopewa,
asimuache hapo peke yake. Chali alikaa hapo na Sabrina mpaka akapewa kitanda,
akaenda kukaa naye mpaka Sabrina alipomwambia arudi nyumbani pengine Pina
atakuwa akimuhitaji amtume, ndipo Chali akaondoka. Ilipofika saa nne sasa ndio
Jack naye akaingia.
“Sasa wewe sahizi huku, na kazi?” “Sikutaka
uwe peke yako!” “Mimi nipo mzima kabisa, nilikuwa na Chali hapa tunaongea.
Ameondoka muda si mrefu ili nipumzike. Wewe nenda kazini.” “Hapana bwana
Sabrina! Hata kama ni kazi ndio hata nisiwepo hapa!” “Hata ukiwepo hapa, kwenye
chumba cha upasujia hutaingia na kwa jinsi nilivyoambiwa nafasi yangu ni mpaka
saa nane. Leo dakatri ana watu wengi wakuwazalisha. Sasa utakaa hapa mpaka saa ngapi?”
“Nakuonea huruma, Brina wangu. Umekataa watu.” “Mwenzio nina amani na Mungu
wangu. Nishaombea kila kitu, hapa nilikuwa nimelala ili nisifikirie chakula.”
“Njaa imeshaanza?” “Nafikiri kile kitendo cha kuambiwa nisile chochote ndio
kinaniongezea njaa.” “Pole.” “Acha kuniangalia kwa huruma bwana!” “Sasa unataka
nifanyaje? Nikusaidie nini?” “Hakuna kwakweli. Kama huna lakufanya sasahivi huko
kazini, basi tukae tu. Ila kama una mambo mengi, nenda kapunguze uje hata hiyo
saa nane.” “Basi muda ukibadilishwa niambie. Si unajua hapo kazini sio mbali na
hapa, nitakuja mara moja.” “Nakuaminia Mheshimiwa Msindai.” Jack akacheka.
“Huogopi?” “Naomba
uondoke Jack. Unataka kuanza kuniingizia hofu zako.” “Nakuuliza tu!” “Sitaki.
Mimi nakujua wewe. Hapo ushawaza pengine naweza kufa huko chumba cha upasuaji,
usinione tena ndio maana umekimbilia hapa.” Jack akapoa.
Akajua ni kweli. “Njoo Jack.” Akamsogelea karibu.
“Wewe tuliomba jana usiku. Ukamwambia Mungu mengi. Kwa nini unakosa imani?”
“Nina imani na hofu pia, Brina! Aisee utoke huko.” “Mungu atanisaidia. Vipi
lakini?” Zikaanza stori, wala Jack hakuondoka.
Wakakaa hapo mpaka mida
ya saa 6 Sabrina akaja kuchukuliwa kupelekwa chumba cha upasuaji wakicheka tu
na Jack. Akamsindikiza mkewe mpaka nje ya mlango akamwambia anamsubiria yeye na
Brandon, mtoto wao wa mwisho. Japokuwa watu hawakuja hapo, lakini kila mtu
nyumbani kwa kina Jack alijua siku hiyo Sabrina anajifungua. Mzee Msindai akawa
ameshatayarisha daktari wa mtoto wa kumuangalia pindi atakapozaliwa na kuomba
apewe taarifa zake.
Baada ya muda mtoto
akatolewa ndipo baadaye Sabrina naye akatolewa. “Umemuona Brandon?” Sabrina
akauliza akisikika bado ana madawa ya usingizi mwilini. “Nimemuona. Naona
amefanana na wewe huyo! Sura kama dada zake!” Sabrina akacheka wakati
wakimrudisha chumbani kwake. “Vipi maumivu?” “Nimeanza kuyasikia.” “Tukimuweka
tu kitandani tutamchoma sindano ya maumivu.” Baada ya kumuweka sawa na kumchoma
sindano, wauguzi wakatoka. “Nasinzia Jack.” “Lala.” “Na wewe usisite kuondoka.
Nikiamka nikawa na shida nitabonyeza kengele, watanisaidia tu, usiwe na
wasiwasi. Acha nipumzike.” “Basi nitarudi jioni na uji.” “Sawa.” Sabrina
akarudi usingizini.
Alikaa pale hospitalini
akisaidiwa na wauguzi kwa siku tatu ndipo akaruhusiwa kurudi nyumbani na mtoto
wake. Hakuna aliyefika hapo hospitalini kumuona isipokuwa Jack tu ambaye
alikuwa akipita asubuhi na chakula na kurudi tena jioni akitokea kazini.
Wanakaa hapo wanazungumza na kumsaidia kutembea kidogo kisha anaondoka usiku
kurudi nyumbani kwa watoto mpaka akaruhusiwa.
Aluta
kontinyua…
B |
rondon alikuwa ameshafikisha miezi miwili, lakini
bado Sabrina akawa mtu wakukaa ndani kwani aliugua sana baada ya kujifungua. Akaanzishiwa
madawa ya makali ya antibiotic ili kuua infection, kwahiyo ndio akawa kama ndio
amepona tu. Siku hiyo akiwa amejipumzisha tu nyumbani Jack akampigia simu kumtaarifu
kuwa kina Ibra watafika hapo nyumbani kuwaona. “Sikujua kama mmerudi kuwasiliana
na Ibra!” Sabrina akashangaa sana. “Maana si alikuwa hataki mimi niwe na wewe
ndio mpaka akashindwa hata kuhudhuria harusi yetu na kukata mawasiliano na wewe
muda wote huo! Sasa leo anakuja kutuona kwa lipi!?” “Mimi mwenyewe nilishangaa.
Ila Felix ndiye aliyeniambia kuwa ni Ibra mwenyewe ndiye aliyempigia simu na
kumwambia imekua muda mrefu hajawasiliana na sisi, anaomba yeye na Ney wamsindikize
kuja kutuona. Ndio ikabidi Felix ampigie simu Ney kumuuliza kama leo ananafasi
ya kuja huku, Ney akakubali bila shida.” “Makubwa!” “Hutaki wageni mama
Msindai?” “Mimi nashangaa tu. Maana sijamsikia huyo mtu hata kwa kuropokwa
nilipo mimi!” “Na mimi ndio leo nimemsikia tena. Kila kitu kikiwa sawa mida ya
saa mbili nitakuwa nimeshafika hapo.” “Haya waambie wakaribie tu.” “Ila
usijichoshe sana. Watakula watakachopika kina Pina.” “Usijali.” Wakazungumza
yao, wakaagana.
Ikabidi Sabrina kutoka
kitandani akijua ana wageni jioni hiyo, lazima kupikwe vizuri na maandalizi
yakae ya kigeni. Akatoka kutoa maagizo nini kipikwe na kitayarishwe kwa ajili
ya wageni watakaowatembelea usiku huo. Ukweli Sabrina alikuwa na wasichana wa
kazi wazuri, waliojua kujipanga kiasi chakumpa pumziko zuri huyo mzazi mwenye
mapacha wa nje na ambaye ndio alikuwa akirudisha nguvu baada ya kuugua kwa muda
mrefu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ilipofika mida aliyojua
wageni wanakaribia kurudi na mumewe, Sabrina akatoka kuangalia vyakula.
Akasaidia kupanga ndipo akarudi kuoga na kujitengeneza vizuri angalau na yeye
afananie na ile nyumba. Wanae wakawa wasafi, wakatoka kusubiria wageni.
Wakaanza kuingia Neema na Felix. Zikaanza stori Sabrina akicheka hana mbavu
wakikumbushiana mambo ya chuoni na habari za mtaani. Mwisho akaingia Ibra na
Phina. Japokuwa hawakuwa wakimtegemea Phina hapo, na hata Sabrina mwenyewe
alishangaa ujio wake pale, mpenzi huyo wa zamani wa baba mwenye nyumba hiyo
lakini Sabrina akawa muungwana, akasimama
kabisa na kuwapokea kwa furaha zote, bila hila.
Felix na Ney wakawa kama
bado hawajaelewa. Ibra alipiga simu akisema yeye ndio anaomba wamsindikize hapo
kusalimia familia ya Jack, sasa anawezaje kufika nyumbani kwa Jack na mpenzi wa
Jack wa zamani! Hicho kikawasumbua kidogo. Lakini walipoona Sabrina hajajali,
na wao wakaona wanyamazie. “Mama wewe umependeza. Tena umependeza mnoooo!”
“Acha kunisanifu bwana Sabrina!” “Eti Ney, huyu Phina hajapendeza kweli?” “Sasa
anakataa nini? Basi umetisha! Acha kujishaua.” “Achana na Ney. Mwaya umependeza
na unazidi kuvutia. Karibuni mkae, tuendelee kucheka.”
“Naona mzee ulijificha!”
Felix akamrushia neno Ibra. “Maisha tu. Vipi Ney?” “Nipo Ibra. Tupo na serikali
yetu.” “Naona huko mnagawana tu mihela ndio maana hamtukumbuki!” “Wewe si
ulikataa serikalini mzee! Malalamiko ya nini?” Felix akaingilia bila nia mbaya,
ila utani tu. “Kwa hiyo sasahivi unaona sisi tunalia tu njaa, hatuna maana?”
Kidogo vicheko vikapungua. “Maana mmeshapata nyinyi, wengine mnatuona..” “Mbona
povu mkubwa wakati mimi nakutania tu!?” Felix akauliza na cheko la mshangao
kidogo.
“Phina zungumza mama, upo
sehemu sahihi. Sema tuondoke. Naona wanaleta dharau kwa kuwa wanajiona wao
wamepata, siku hizi mambo yao wao safi, wanakula na wakubwa wa hii nchi, ndio
wengine hatuna maana! Yaani Jack ndio wakukataa kupokea simu zangu mimi!? Yaani
mimi ili kumpata yeye ni mpaka wewe!” Hapo wakajua hao wawili hawajaja kwa wema.
Utani ukaisha kabisa, wakanyamaza kuwasikiliza. “Sema Phina tuondoke zetu.”
Wote wakamgeukia Phina kusikia hicho anachotaka kusema.
“Au labda nimsubirie Jack
mwenyewe, nizungumze naye yeye? Hapa naona kama si sehemu yake!” “Sehemu ingine
ipi na bosi wao hawa analeta dharau! Ongea usiogope.” Akawa kama anampandisha
morari, ila Phina amejawa hofu, akainama. Kimya wakimtizama yeye na kuwasikiliza.
Phina aliponyanyua kichwa kuwaangalia, akakuta wakimtizama kumuonyesha wanamsubiria
yeye aongee lililowaleta na kutaka kuja kuzungumza na Jack tu! Akaanza
taratibu. “Mimi sio kwamba ni mvurugaji. Ni vile Jack amenifungia simu zangu na
sina jinsi ya kumpata.” “Basi unabahati nzuri. Amerudi nchini. Yupo hapa mjini!
Muda si mrefu atakuwa hapa.” Sabrina akamtuliza bila hila. Kidogo Phina akapoa.
“Acha kusita Phina! Ni
haki yako. Unaogopa nini? Hata kwa wazazi wake mimi nimekwambia nitakupeleka.
Waache dharau.” “Kwani kuna nini? Kama kuna jambo ambalo unaona naweza
kukusaidia, tafadhali usisite Phina. Sisi tumetoka mbali. Na tumesaidiana
katika mengi.” Sabrina akajaribu kumtuliza ili azungumze lakini akadakia tena
Ibra. “Mengi sana, nashangaa eti sasa hivi ndio wanaleta dharau!” “Kiongozi
vipi mbona jazba tena!?” Felex akauliza na Ney akaanza kucheka. “Acha hasira
Ibra. Kama kuna jambo la kuzungumza, acha tuzungumze kwa amani.” “Amani ipi
wakati Jackson anatumia madaraka yake vibaya, kisha analeta dharau?” Kimya
wakimpa nafasi huyo Ibra maana alionekana analo jambo analotaka lazima Phina aliseme,
lakini ni kama Phina naye anasita. “Sema usiogope, Phina.” Akazidi kumsisitiza
Phina.
“Kuna nini Phina?”
Sabrina akamuuliza Phina kwa upendo tu akimbembeleza. “Jack kampa mimba
Phina, halafu anamkimbia!” Ibra akajibu kwa haraka, moyo wa Sabrina ulishituka
kama kumeanguka chuma sakafuni. Akaona kama giza kwa sekunde kadhaa.
“Anatafutwa, halafu anafungia namba za Phina zote! Anatumia watu tu vile
atakavyo! Amelala na Phina usiku kuchwa, eti asubuhi ndio kama anakumbuka
alifanya kosa, anamfukuza Phina! Uzuri Phina alimpiga picha na ushahidi anao
wakiwa hotelini Switzerland walipokutana na Jack.” Ibra akasimama na bahasha
kubwa tu aliyokuwa ameishika tokea wanaingia hapo akaenda kuiweka pembeni kwa
Sabrina kama kumpa ushahidi.
“Huo ndio ushahidi wa
Phina. Mpe mumeo anayejua kuchezea wanawake vile atakavyo. Alipokuwa na Phina,
akawa na wewe pia. Nikamuonya Jack, hakunisikia. Akakuoa. Sasahivi yupo na
wewe, analala na Phina. Si ushenzi huo? Sasa mwambie Jack aanze kuweka mikakati
juu ya mtoto wa Phina. Tunampa siku tatu tu awe amewasiliana na Phina na kuweka
mipango ya kueleweka lasivyo sisi tunatangulia Ustawi wa Jamii kudai
haki zetu, na atasikia habari zetu magazetini.” “Labda mimi nikuulize Ibra,
wewe unaongea hapa kwa jazba kama nani?” “Hayakuhusu Ney.” “Mbona mimi ndio
naona kama wewe Ibra ndio hayakuhusu?” Akadakia Felix.
“Twende Phina. Ila Sabrina, jua mtoto wa Phina
naye anataka alelewe kama hivi hao watoto wako wanavyolelewa hapa. Wawekewe
ulinzi kama huo waliowekewa watoto wako na aishi kwenye nyumba kama hii.” Felex
akakasirika sana. “Wewe ni mshenzi Ibra na naona maisha yamekupiga mjomba,
unataka uponee hapahapa kwa Msindai.” Nusura ngumi zianze. Matusi yakaanza
hapohapo mpaka wasichana wa kazi na watoto wakajongea hapo sebuleni kujua
kulikoni. Sabrina kimya palepale alipokuwa amekaa.
“Umenitumia mimi
kukusogeza kwenye familia ya watu ili mje kufanya fujo! Yeye Phina hakujua
analala na Jack mume wa mtu na ana majukumu mengine mbali ya kupokea simu zake
malaya huyu.” Felix alikuwa amekasirika kwelikweli akigomba, Ibra naye
anamtukana Jack matusi ya nguoni hapohapo mbele ya mkewe na watoto wake kama aliyekuwa
na hasira kali sana kwa Jack. Chakushangaza Felix ndiye aliyekuwa akigombana
naye, lakini yeye anamtukana Jack mpaka mlinzi akaingia na kuwatoa wote mpaka
kina Ney.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Nini Kitaendelea? Usikose Muendelezo..
0 Comments:
Post a Comment