Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 60. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 60.

 Hakuna Marefu Yasiyo na Ncha.

S

iku ya tatu usiku wakiwa bado hawajafungua wakisindikizwa na mchungaji aliyewajua hao watoto tokea enzi za uhai wa mama yao na yeye marehemu mama yao alikuwa akitumika kwenye kanisa analochunga huyo Mchungaji, akiwa na yeye amefunga, wakaongozana kwenda nyumbani kwa mzee Ngoi na mkewe Zelda. Kwa hakika Zelda alishituka sana. Akataka kumshawishi Ngoi awafukuze kwa kuja bila taarifa, lakini ilivyo ya kushangaza kwa mara ya kwanza Ngoi akawa kinyume naye. Akamwambia angependa awasikilize.

Wakakaribishwa ndani. Hilo likawa kosa, hata maji walikataa kunywa, wakasema wanaanza kwa maombi. Maombi yaliyopigwa hapo ndani, Ngoi na mkewe wakaanza kulipukwa mapepo. Zelda akawa anataka kukimbia kichaa. Wakamkamata na kumfunga kamba. Kazi ya kumuombea Ngoi ikaanza. Akatolewa mapepo akawekwa huru asielewe kinachoendelea. Hawakutaka kupoe. Wakaendeleza maombi ya nguvu ndipo Zelda akaanza kulipuka mapepo mengine yaliyoanza kuzungumza na kufanya msiba uanze upya. Alikiri mengi mno yaliyowaliza ndugu hao mpaka Ngoi mwenyewe. Prisca akamuomba mchungaji amuulize ni wapi anaficha uchawi wake. Kila alipokuwa akisema, wanaenda kutoa hirizi na madawa. Alikuwa amechimbia madawa kwenye kila kona ya hiyo nyumba.

Zelda akiwa bado amefungwa kamba akilia kama kichaa huku akiwaonya wasithubutu kuangamiza kitu hata kimoja wapo, lakini mchungaji hakumsikiliza. Wakakusanya yote mpaka madawa na hirizi alizokuwa ameficha ndani na kuchoma moto, watoto wao wakimchukua video kwa kila ukiri aliokuwa akikiri na kila mahali aliposema amefukia au kuficha hizo dawa, walikuwa wakienda kufukua uchawi huku wakichukua video.

Ilikuwa wote wafe kasoro Willy. Zelda alisema yeye Willy hakuwa kinyume naye, alikwenda mpaka kwenye harusi yao. Ila aliyekuwa akifuata kufa ni Prisca. Ikazidi kuwaumiza na kujuta kutochukua hatua mapema, pengine wangebakiwa na ndugu zao! Walipochoma kila kitu ndipo sasa ikaanza kazi ya kutoa hayo mapepo ya Zelda mpaka akawekwa huru. Ngoi alikuwa akimuogopa mkewe kupita kiasi. Hakutaka hata amsogelee. Walichofanya ni kumpeleka polisi usiku huohuo.

 Kwa kuwa walijua kesi za uchawi ni ngumu kuendeshwa kwa sheria za nchi, basi wakatoa ushahidi wote mpaka wa video ili tu kusaidia kuhukumiwa kwake kihalali. Kesi ya Zelda ikaanza. Wakimshitaki kwa mauaji aliyokiri mwenyewe kufanya kwa njia ya kutuma mapepo kuua. Wazazi wake Zelda wakaja hapo wakiwatisha kuwa kitawapata kitu kibaya kama hawatamtoa Zelda. Nao wakawashitaki na hivyo vitisho vyao. Wakapewa onyo kisheria na kuambiwa chochote kitakachoipata hiyo familia tena, hata kwa bahati mbaya, basi wao watakamatwa na kushitakiwa kuhusika moja kwa moja. Wakapoa.

 Hakuna aliyesikia kilichowapata hiyo familia wasitake kuwasaidia kwa hali na mali, mpaka maombi, na kisheria pia. Wakapata uungwaji mkono mkubwa, Zelda hakuweza kutolewa hata kwa dhamana. Kesi yake ikawa ikiendelea, yeye yupo rumande ila mtoto wake alichukuliwa na mama yake Zelda. Willy akaahidi nilazima baba yao atakuwa akimtunza huyo mtoto na kuhakikisha anakua vizuri na kusoma bila shida. Hilo likakaa sawa. Wakashukuru sana wasiamini kama hawatamtelekeza huyo mtoto.

Mungu Wa Yasiyowezekana Kwa Akili Za Kibinadamu..

S

abrina alipofikisha mimba ya miezi saba, mumewe akateuliwa kuwa naibu waziri wa fedha baada ya aliyekuwa naibu waziri kutolewa na raisi. Jack alikuwa akifurahia asiamini kama yote hayo yanamtokea yeye. Safari hii wakaenda kuapishwa ikulu. Jack akakusanya tena timu yake mpaka Dar. Na walishukia nyumbani kwao kwani walishaanza kujaza nyumba yao kwa thamani za ndani wakitaka kuwa wakiitumia pindi wanapokuwa jijini maana kuendelea kushukia majumbani kwa watu ikawa shida, familia yao ishakuwa kubwa. Kwa wakwe bado hawajapatana na Sabrina, wakaona bora wawe na kwao, iishe hivyo. Ikawafaa sana kwa wakati huo pia. Na kama kawaida yake, mama Msindai akaleta yeye nguo za Jackson. Wala Sabrina hakulalamika. Akamuacha tu afanye kile anachotaka kwa huyo mwanae.

          Baada ya shuguli hizo zote, wakajua nilazima sasa kuhamia Dar kwa kuwa sasa majukumu ya Jack kikazi yalimtaka awepo huko. Ikawa ngumu sana kwa Sabrina. “Itakuaje kule Singida, Jack?” “Tutarudi kuzungumza nao na kuwaambia majukumu yanatushikilia huku lakini mimi bado ni mbunge wao, nawawakilisha huku. Na tutakuwa tukirudi kuwatembelea mara kwa mara. Na wewe utaendelea kufanya nao kazi kwa karibu.” Wakaweka mipango iliyofanya hata Sabrina kujiridhisha kuwa wameacha jimbo kwenye hali nzuri. Walipotulia, wakarudi Singida kuwaaga na kuzungumza nao vizuri. Ikawa ni jambo la kuwahuzunisha kuwakosa huko Singida lakini pia lakuwafurahisha wakijua wamepata uwakilishi mzuri huko bungeni.

Kila Kitu Mwangani.

B

ado Sabrina hakuwa amewasiliana na nyumbani kwao ila habari za mafanikio ya mumewe haikuwa siri. Hata wao walijua mafanikio ya Jack waliyembeza aliposhindwa ubunge wa Afrika ya Mashariki. Madaraka ya Jack yakaibua kuchimbuliwa kwao. Minong’ono juu ya familia ya Jack ikaanza. Kitendo cha kuonekana na aina ile ya watoto ndio iliyoibua minong’ono mitandaoni. Familia yenye watoto wa kizungu wakati hapakuwa hata na mweupe kwa wazazi hao! Nani kati yao alizaa na mzungu ndipo akaja nao kwenye ndoa!!!?? Naibu waziri au Sabrina? Ukawa utata. Ilianza minong’ono ya chinichini tu, ila iliweza kusikika, na hapakuwa na jibu.

          Picha za mapacha zikaanza kuenea na kufananishwa mpaka wakajua ni watoto wa Sabrina. Nani baba yao!? Nalo likawa jambo lakutafutiwa majibu. Lakini sasa unampata wapi Sabrina kujua habari zake? Hajaajiriwa popote, na sio mtoto wa jiji, hakuna anayejua habari zake kwa undani. Hana Instagram wala Facebook. Habari zake zikaanza kusakwa bila kuchoka. Nani yupo karibu na familia hiyo inayoweza kutoa mambo ya ndani! Kwa upande wa familia ya Msindai ikawa ngumu kuingia ili kuweza kutoa mambo ya familia ya Naibu waziri mpya, ikaanza kusakwa familia ya Sabrina. Amezaliwa wapi! Ndugu zake kina nani! Ilimradi tu kujipatia habari. Mswahili mnyime chakula lakini si neno.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Bado Max alikuwa kifungoni na kesi yake haikuwa imesomwa. Hajahukumiwa bado, kila wakati kesi yake ilikuwa ikisogezwa mbele. Mkewe alishahamia Dodoma, akisubiria kustaafu aondoke serikalini na kiinua mgongo chake sio mikono mitupu.

Adui Za Mtu Ni Wale Wa Nyumbani Kwake.

{Mathayo 10:36}

A

lipofikisha majuma 36 ya ujauzito wake, Sabrina bila hila akijua akifikisha majuma 38 lazima kufanyiwa upasuaji mwingine na akajua hataweza kutoka ndani kwa muda mrefu akijiuguza kidonda na kulea hao mapacha wake wa nje, akaamua kwenda kuona wazazi. Nyumbani ni nyumbani, wazazi ni wazazi. Akaamua kwenda kuwaona na kuweka amani. Akakusanya watoto wake na dereva maana ni kweli mambo yalibadilika kati yao. Mapenzi ya kila wakati wakishikana huku na kule, kuongozana kila mahali, yakapungua, Jack alishapewa majukumu mazito, hawezi kuzembea kwa sababu hakutaka kuharibu kwa la unaibu waziri, akitaka kuja kuaminiwa na makubwa zaidi. Akaongeza nidhamu ya kazi zaidi ya kawaida yake. Kwa hiyo mtindo wakufuatana kila mahali ukakoma. Mara chache tena ikilazimu ndipo utawakuta pamoja.

Sabrina alijifungasha vizuri akiwa amewanunulia wazazi wake zawadi za kutosha, akaondoka mjini muda mzuri tu akielekea Chalinze nyumbani kwao. Ilikuwa siku ya jumamosi. Akashangaa mazingira ya nyumbani kwao! Kulionekana kumebadilika sana. Hali ya neema ya ajabu! Nyumba iliwekwa geti zuri na la kisasa. Akashangaa kidogo na kumpongeza Sabina nafsi mwake. Akamwambia dereva asubiri pengine watafunguliwa baada ya kupiga honi. Wakatulia garini wakisubiria kuona. Na kweli akaja kijana ambaye Sabrina hakuwa akimfahamu, akafungua geti wakaingia ndani. Macho ya Sabrina yakapokelewa na barabara iliyotandazwa mawe mazuri kuanzia hapo getini walipoingia mpaka kwenye ngazi za nyumba! Ngazi zenyewe ni kama zilijengwa mpya sio alizoacha Sabrina za kawaida tu. Halafu ngazi hizo zilijengwa na kuzungushiwa rembo nzuri za vinguzo vyenye muundo mzuri za kuvutia pamoja na rangi yake. Halafu sakafu ikajengewa marumaru za kisasa, safi. Kuanzia ngazi ya chini mpaka kuingia ndani. Sabrina akashangaa sana.

Dereva akamsaidia kushusha watoto, Sabrina akawaambia wale wakubwa mapacha wambebee pochi yake waanze kuingia ndani wakati akijaribu kumuweka sawa Brayan ambaye hata mwaka hakuwa ametimiza. Ila dereva akamtoa kwenye kiti chake, Sabrina akawa amemshika mkono akimtaka atembee mwenyewe sio kumbeba. Basi akawa akijivuta taratibu kutokana na tumbo lake na hatua za Brayan.

“Umeona yanakushinda huko, yamewalemea, ndio unajidai kurudi ulikokua umetususa!” Sabrina akatoa macho kwa mwanae na kumuangalia mama yake aliyekuwa akizungumza bila karibu hapo barazani. Sabrina akahisi pengine anazungumza na mtu kwenye simu au mtu mwingine, sio yeye. “Shikamoo mama.” Sabrina akasalimia na kurudisha macho haraka kwa Brayan asije akaanguka. “Mimi naona tubebane tu. Lasivyo tutafika huko mwakani.” Sabrina akamwambia Brayan na kumnyanyua mwanae. Kuangalia, bado mama yake anawatizama.

Akacheka. “Unavyotushangaa! Umependeza mama Sabina.” “Ulivyotususa, ulifikiri tutaaibika?” Sabrina akakunja uso. “Kwamba gafla mimi nataka muabike!?” Sabrina akauliza na tabasamu la mshangao. “Kumbe! Ulivyotutupa, ulidhani tutayumba! Mungu wetu yupo Sabrina. Na tumeyaanza maisha kabla wewe hujaja hapa duniani. Ona kinachokutokea sasa hivi! Yamekushinda huko ndio unarudi huku kuomba undungu! Undugu hauombwi wakati wa shida. na kwa taarifa yako tu, kama umeshindwa wewe kututambua sisi kama ndugu zako, sio waonavyo walimwengu. Habari zako zinatafutwa ulikozaliwa. Sasa hata ukitukimbia sisi kwa sababu unatuona si wasomi na hatufai kama kina Msindai, lakini jua bado sisi ni wazazi wako. Ulizaliwa hapa na kukuzwa hapahapa. Hapa ni mtakuja. Hata uende wapi, hapa ni mtakuja tu.” Sabrina na wanae wakabaki hata kwenye ngazi ya kwanza hawajapandisha. Mama Sabina anaongea kwa jazba kupita kiasi, Sabrina haelewi.

“Kwanza hata hao kina Msindai hawakutaki. Unaa..” “Mama Sabina, huyu mtoto hata ndani hajaingia mke wangu! Ona hali yake! Ni mjamzito huyo na ana mtoto mkononi, kweli unashindwa kumpokea wakati amekuja nyumbani kutuona!?” “Amekuja kutuona au kaja kutusanifu na kutufunga mdomo! Sasa hapa lazima haki itendeke. Tino apate haki yake. Hatuwezi kunyamazia ukweli huku mkitesa watoto wake wakati yeye mwenyewe yupo na ana uwezo wa kuwalea!” “Acha nikupokee mtoto.” Dereva akamsogelea na kumuomba Sabrina kwa heshima. Sabrina akageuka. “Nashukuru. Naomba nisaidie kurudisha wote ndani ya gari, hapa jua kali sana.” Sabrina akamkabithisha Brayan kwa huyo dereva ambaye wanae walishazoea kumuita anko Chali. “Jeiline, mama, nenda kwa anko Chali, atakusaidia kupanda kwenye gari. Mnisubirie nakuja sasahivi. Sawa Keiline?” Wakakubali na kuanza kumfuata Chali. “Hata ukiwakimbiza hapa…” “Subiri kidogo mama. Sitaondoka hapa mpaka umalize dukuduku lako. Lakini naomba nitoe wanangu juani. Tafadhali mama yangu.” Akamgeukia dereva. Alipomfunga Brayan kwenye kiti chake, akaanza kuingiza wale mapacha garini. Alipoingia na yeye na kuwasha gari, Sabrina akamgeukia mama yake.  

“Nakusikiliza mama, japo kwa hakika hata sielewi ni nini unazungumzia!” “Utajijua!” Mama yake akajibu. “Jamani wazazi wangu mimi nilikuja kuwaona, ni hilo tu sina jingine. Nilitaka kuwajulia hali nikijua Mungu akinipa uzima nikijifungua,..” “Ili nije kukusaidia kulea watoto wa watu wasio na utu! Binadamu walionyimwa utu, wanatumia vyeo vyao vibaya! Wanamfunga mtu aliyekuwa akitaka kumsaidia Tino! Kwa kosa lipi mno! Sasa na sisi kwa kuwa Tino ametuonyesha utu na ubinadamu, anatambua sisi ni ndugu za watoto wake, anajali na kukumbuka nyumbani sio huyo mwanaume ana kazi ya kukuzalisha tu, hajui kama una wazazi! Sasa na sisi kama familia, tutasimama na Tino mpaka apate haki yake. Popote na kwa yeyote yule, tutazungumza ukweli.” Kidogo ni kama Sabrina akaanza kuelewa.

Akaangalia yale mazingira kisha akarudisha macho kwa wazazi wake. “Kwa hiyo haya mabadiliko ninayoyaona hapa, ni kazi ya Tino hii?” Sabrina akauliza. “Yeye ndiye aliyebaki mwenye uti je! Ulifikiri na yeye atakuwa kama huyo mwanaume wako wa magazetini tu, wala chamaana hatuoni!” “Sawa mama. Nyinyi endeleeni na Tino.” “Unatudharau ukidhani tutashindwa hiyo kesi? Sasa Sabina amekubali kutoa ushahidi wote. Na mimi nitaeleza jinsi huyo Jackson alivyowatelekeza watoto wa Tino zaidi ya mwezi, hajui walipo, wanakula nini wala wanavaa nini mpaka Tino akaingilia kati kuwasaidia. Hakika tutasema.” “Haikufika hata mwezi mama yangu!” “Utajijua mwenyewe. Lakini na mimi nilikwepo, shahidi wa Tino. Nitasema ukweli wala sitaogopa. Alikutelekeza na watoto mpaka Tino akaja kukusaidia. Aliposhindwa ndio akajirudi na kumpokonya mwenzie watoto wake.”

“Huyo mwanadamu gani kama si mnyama tu! Yakimuendea sawa anawatelekeza. Yakimdodea anarudi! Ona ulipofikishwa. Tumbo linakulemea na watoto wote upo nao peke yako, yeye anazungushwa kwenye magari ya kifahari! Sasa safari hii ujue wazi kabisa, Tino anachukua watoto wake.” Sabrina hata hakuwa akijua kama kuna kesi inayoendelea dhidi yao. Akabaki kimya akimsikiliza. Baba yake naye kimya. Mama huyo akaongea mpaka akayamaliza. Alipoona Sabrina kimya na hakuna uungwaji mkono kutoka kwa mumewe, akataka kurudi ndani.

Sabrina akamuita. “Naomba unisikilize kidogo tu mama yangu.” “Kwa lipi?” “Sina jipya mama yangu. Ila nilitaka kuwapa angalizo.” “Hututishi.” “Hata kidogo mama. Mimi sina nguvu. Nilishashindwa muda mrefu sana ndio maana nilimuachia Yesu wangu atawale na anipiganie.” “Huo ni unafiki Sabrina. Kama wewe kweli unamjua huyo Yesu, basi mpeni Tino haki yake.” “Baba, naomba wewe unisikilize ili badaye kusiwe na majuto.” “Uta..” “Hapana mama. Kama wewe huwezi kunisikiliza, tafadhali  mwache baba anisikilize. Nisikilize tu baba yangu.” Sabrina akasihi.

“Najua Sabina anategemewa sana hapa nyumbani. Ni nguzo yetu tokea zamani.” “Kumbe unalijua hilo na…” “Mwache amalize.” Baba yake akaingilia. “Nawasihi wazazi wangu, hata kwa kupiga magoti nitapiga, mwambieni Sabina asijiingize kwenye vita na Jack.” “Atamfanya nini?” “Baba na mama. Hata kama mmezoea kunipuuza, lakini naomba isiwe katika hili. Tafadhali sana wazazi wangu. Baba, mwambie Sabina, asianze vita na Jack. Hata nyinyi, chochote mnachopanga kinyume na Jack, acheni kabisa. Acheni vita ya Tino, apigane mwenyewe, nyinyi isiwahusu.” “Huyo Jack atatufanya nini? Ni kwa kuwa amekua naibu waziri wa fedha ndio anakuchanganya akili?” Mama yake akaendelea kupayuka.

Sabrina akamgeukia baba yake. “Baba, umenisikia? Vita yeyote mnayopanga dhidi ya Jackson, mjue mnapigana na kina Msindai wote. Nimeishi na wale watu, nimewasoma. Katika mapungufu yao yote ambayo mnayajua wanayo wao, basi iwe ya ndani wenyewe kwa wenyewe watakuwa sawa na kuyanyamazia, ila si nje. Huwa hawakubali mmoja wao ashindwe. Ukimgusa Jack, umegusa kina Msindai wote na kwao si kitu kidogo hata kidogo, Kwa kuwa unawachafulia jina lao ambalo wanalilinda kwa sababu wana malengo nalo kwa mpaka watoto wao. Unapomuona Jack leo ni kiongozi, hajajikuta tu, wazazi wangu. Wale wanaandaliwa kuwa viongozi tokea watoto wadogo. Uongozi wa hii nchi kwao si kwa Jackson na kaka yake tu, ni mpaka watoto wao. Macho na masikio yao yapo kila mahali wakilindana mchana na usiku. Popote linapotajwa jina la Msindai inakuwa ni kama umegusa antena zao, wanasikia na hawapuuzi.” Sabrina akaendelea.

“Baba, mnamtegemea sana Sabina. Nakusihi baba yangu, mwambie Sabina aachane na kina Msindai. Hata kama ameanza, akatangaze huko kuwa, ameacha. Hamtawaweza kina Msindai.” “Sisi tunatetea haki ya Tino.” “Sawa mama. Lakini hakika hii siku ikumbukwe. Msije sahau kama niliwaonya. Baba umenisikia?” “Acha kututisha Sabrina. Unataka kutufunga mdomo ili…” “Kuwaokoa, ili mbakie salama.” Sabrina akamalizia kwa mama yake na kuendelea. “Mimi sijui huwa Tino anawaambia nin…” “Ukweli. Ukweli mtupu. Ameongea ukweli na ameomba msamaha mpaka kwa vitendo. Ndio maana anajenga hapa ili ikitokea watoto wake wanatelekezwa tena, wasihangaike. Yeye ni binadaamu.” “Hakika Mungu awasaidie wazazi wangu.” Sabrina akawahurumia sana.

“Atusaidie mara ngapi?” Mama yake akaendelea. Sabrina akatulia kama anayefikiria mbele ya wazazi wake. Akatulia kabisa kwa muda akiwa ameinama, mama yake akizungumza kishabiki. Akaongea mengi kwa jazba akiropoka. “Kama hayo unayozungumza mama ni ya kweli na ndiyo yanayoendelea huko mitandaoni na mtaani, basi..” “Inamaana wewe Sabrina ndio unasikia haya!?” “Kabisa baba na Mungu wangu nishahidi, mpaka naogopa. Mimi nilitingwa na shuguli nyingi kwa kuwa tulihamia hapa nikaacha mambo yangu Singida hayajakaa sawa. Nikawa nipo hapa na kule nikihangaika kule kupaweka sawa maana niliacha hata biashara zetu hazijakaa sawa. Sasa akili ikawa Singida japo niko huku nikifanya mambo kwa haraka ili nitakapojifungua, nipate muda wa mapumziko. Na nikajiambia leo lazima kila kitu kisimame, nije niwaone kabla lakutokea likatokea nikajifungua, nikashindwa kuja kuwaona. Haya mama anayoongea hapa, sina hata habari nayo! Na ndio maana najiambia kama mama haongezi chochote, ni kweli kama ilivyo, basi kwa ukimya wa wakina Msindai, ujue si jambo zuri.” “Muongo. Kaja kutuchota.” “Subiri kwanza mama Sabina.” Muwe akamtuliza.

“Twende taratibu Sabrina. Inamaana mumeo hajakwambia chochote juu ya haya?” “Jack hawezi kuniambia baba kwa sababu kama unavyoniona. Nilipata huu ujauzito mshono ukiwa mbichi kabisa. Huyu unayemuona hapa ni dereva tuliyepewa na Jacinta, dada yake Jack. Sina ninapokwenda bila huyu kaka mpaka nimeogopa kwa sababu ya cheo cha Jacinta. Inawezekana kwa hicho kinachoendelea, huyu ninayedhani mimi kama ni dereva, wala si dereva yupo hapa akilinda hawa watoto wa Jack.” “Wengine ni wa Tino. Usije jisahau.” “Vile atakavyokuaminisha Tino ukaamini, sina jinsi ingine nikakuweka upande mwingine ukakubali mama yangu. Lakini ninachotaka kusema, Jack hataki nipandishe pressure kabisa nafikiri ndio maana wananificha na mimi si mtu wa kushika simu kujua kinachoendelea mitandaoni. Kwanza kushika simu kwenye ni shida. Hapa kwenyewe nilipo hata sijui simu yangu ilipo, mpaka naanza kujilaumu najiambia itabidi nibadilike.”

“Kujibu swali lako baba yangu, sijui. Nipo hapa kuwaona tu. Sijui chochote, na Jack yupo kimya juu ya hili ila sasa ndio mmenifanya nifikirie. Kumeongezeka umakini sana pale nyumbani. Hata aina ya ulinzi sio kama zamani. Mimi nilidhani ni kwa kuwa Jack amekua Naibu waziri amepewa ulinzi na serikali, kumbe ni kuzuia hao watu wa habari wanaokuja huku kwenu, wanaotaka kunihoji mimi wasitusogelee pamoja na huyo aliyekuwa mke wa Tino, Lela ambaye mmesema ananitafuta kujua ukweli juu ya watoto wa Tino. Sasa hivi ndio naelewa huo umakini wa wakina Msindai.” Sabrina akafikiria tena kidogo na kuzidi kufunguliwa macho.

“Wazazi wangu, hiyo vita mliyoanzisha na kina Msindai, hawatakubali. Na inamaana hata hapa nyumbani wanajua kinachoendelea.” “Watatufanya nini?” “Msipoachana nao, kwa hakika mtajua kwa vitendo.” Sabrina akamgeukia tena baba yake ambaye naye ni kama aliingizwa kwenye jambo hajui chakufanya tena. “Baba, kila linapofika kwenye swala la Msindai hata mmoja wao, ile familia hawafanyi kama hivi sisi. Huwa wanaweka tofauti zao pembeni, wanasimama pamoja. Usimuone yule mzee ni mkimya vile, yule mzee ni mtu wa usalama wa taifa wa miaka mingi mno. Anajua mambo ambayo yatakushangaza, baba yangu.”

“Anawafundisha mpaka wajukuu zake jinsi ya kumjua mtu mwenyewe kwa uhalisia ni kwa kumsikiliza kwa makini, na kutopuuzia taarifa yeyote ile anayotoa mdomoni mwake hata kama ndogo ya kiasi gani. Kwa kumsikia mwenyewe akiwaambia wale wajukuu zake, neno lolote linalotoka kinywani mwa mwanadamu, halijatoka mdomoni bali moyoni. Anawafundisha wale watoto wadogo kuwa wakimsikia mtu yeyote akizungumza kwenye mazungumzo yasiyo rasmi kama hotuba zilizoandikwa na kuandaliwa, ila yale mazungumzo ya kirafiki tu, basi kunyamaza ili kusikia moyo wa huyo mtu. Mpaka akanifanya niwe makini sana kuzungumza nao wale watu. Na kuna jambo anasisitizia wanae, taarifa yeyote wanayosikia, wasiwe wepesi kujibu na kuchukulia hatua.”

“Huwa anarudia kusema bila kuchoka, hata kwenye kuapishwa kwa Jack mara hii ya pili baada ya kutoka Ikulu, tulipokusanyika kama ndugu tu, Junior akamuomba tena aongee chochote cha kumjenga Jack, yule mzee akarudia tena, akasema siri ya kushinda jambo ipo kwenye kutulia, kufikiria hatua zote utakazochukua ndipo kuchukua hatua. Yeye anasema, kuchukua hatua za haraka ambazo hazijafikiriwa, mara nyingi ndipo kushindwa kirahisi. Ni maneno ya yule mzee kwa kumsikia mwenyewe, mbele ya wajukuu zake na wanae. Yule mzee sio mkimya na mjinga wazazi wangu, ila yupo makini mno, na analinda familia yake kuliko nitakavyowaambia au mtakavyomuona yupo mkimya vile mbele ya watu. Si mjinga. Amewafundisha watoto wake kutokukurupuka kwenye lolote. Hiki mnachowafanyia kina Msindai, na mnaona wapo kimya, sio kwamba wameshindwa! Hata kidogo. Wapo kwenye mipango yao na sidhani kama itawaletea nyinyi matokeo mnayotarajia.” “Wat..” “Subiri kwanza mama. Nakaribia kumaliza.” Sabrina akamkatiza mama yake kwa haraka.

Akaendelea taratibu tu. “Wazazi wangu, najua mimi nimekuwa mtoto ambaye hamridhishwi na mambo yangu. Ndio maana mpo tayari kusimama na mtu baki kama Tino ili tu ashinde dhidi ya upande niliopo mimi. Lakini naomba mchukulie ujio wangu huu ni Mungu amenituma kwenu. Si safari hii na si katika hili. Nitafuteni kuniangamiza mimi kama Sabrina lakini si kwa vita na kina Msindai. Nawahakikishia wazazi wangu, hamtashinda.” “Hii nchi ni ya haki. Sheria itasimama na haki itatendeka.” “Sawa mama. Jambo la mwisho, nilikuja na zawadi. Je, mtazipokea?” “Ili mje mseme hamkutelekeza nyumbani! Mnatujali kama Tino? Maana siku zote mlitutupa, Tino ndiye anayetujali. Leo mnajirudi ili kupata ushahidi wa kuja kusema eti na nyinyi mlikuwa mkitujali?” “Kama nimekuelewa vizuri mama, ni umekataa kupokea vitu nilivyokuja navyo. Si ndiyo?” “Hatuna shida. Kamwambie mumeo, amekumbuka shuka kumekuchwa.” “Kwa hiyo hutakuwa na shida hata ukiona nakwenda kumpa mama Jabiri huyo jirani yetu? Maana nilinunua, nikaombea kuwa iwe baraka kwa mpokeaji.” “Hatuna shida.” “Mama Sabina!” Mumewe akashangaa sana kuwa wanawezaje kukataa!

Wakati akikataliwa zawadi zake za vyakula dereva naye alikuwa amemfuata tena. Sabrina akageuka alipomsogelea zaidi. “Simu yako ilikuwa ikiita sana, mwishoe nimepigiwa mimi. Ni mumeo anataka kuzungumza na wewe. Anakwambia pokea simu.” “Nashukuru. Nakuja sasahivi, acha niage tuondoke.” Akabaki amesimama. Sabrina akamgeukia akimshangaa kwa nini haondoki! “Nimekwambia nakuja. Wewe tangulia tu kwenye gari.” “Ameniambia nirudi na wewe kwenye gari. Nafikiri sababu ya jua.” Akajua Jack ameshajua kinachoendelea. “Haya wazazi wangu. Mimi naondoka na kuwaacha na amani ya Bwana.” “Ilikuwepo na itaendelea kuwepo.” Sabrina akaondoka hapo kwao hata ndani hajakaribishwa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akaingia garini akakuta Jack amempigia zaidi ya mara tatu. “Naomba tushushe hivi vitu hapo kwa jirani. Siwezi kurudi navyo nyumbani.” Akamuona yule dereva kama anasita kumwambia kitu. “Ni nini? Niambie tu Chali.” “Nina familia kubwa hapo kwangu, mama Msindai! Ni kama ukoo mzima umehamia hapo mpaka namuhurumia mke wangu. Kama nyumbani wamekataa, basi naomba na mimi kidogo.” “Basi ni vyako vyote. Mungu alikusudia kukubariki wewe. Ila naomba uturudishe sisi nyumbani kwanza ndio upeleke hivi vitu kwako.” “Mungu akubariki.” “Amina.” Akaamua kurudisha simu ya mumewe.

“Sikujua kama leo unakwenda nyumbani!” Jack akawa kama analalamika. “Sikupanga kukaa muda mrefu. Nilitaka kuwaona kabla sijajifungua.” “Pole.” Sabrina akataka kama kumuuliza lakini akasita na kunyamaza. “Kwa hiyo mnarudi nyumbani?” “Naona nikapumzike tu.” “Upo sawa lakini?” “Nafikiri.” Akajibu Sabrina na kutulia. “Basi nitakuona jioni, tutazungumza vizuri.” “Sawa.” Sabrina akakata simu akiwa na maswali mengi hajui aanzie wapi kuuliza na hakuwa akijua kama mambo ndio yapo yalivyo! Akataka kujilaumu, lakini akaona haitasaidia. Akaumia sana kuona familia yake inavyojipanga kushindana naye wala si kumtetea.

Dereva akaendelea kukanyaga mafuta kuwatoa huko Chalize kuwarudisha nyumbani. Sabrina aliomba hata redio izimwe. Dereva akaizima, kukawa kimya kabisa. Akarudisha kiti nyuma, akabakia amejilaza hapo akisugua tumbo lake taratibu. Wanae wote wakapotelea usingizini, kukaendelea kuwa kimya hapo garini. Dereva akaendesha taratibu kwa makini mpaka kwake. Bado ilikuwa mapema tu mida ya saa saba mchana wakati mlinzi akiwafungulia geti. “Naomba niitie kina dada, wawachukue hawa wote.” “Wewe hushuki?” “Hapana. Nataka nikamuone daktari mara moja.” “Kwema?” “Kwema tu.” Sabrina akajibu na kurudi kujilaza kitini, kimya.

Wakaitwa wasichana wa kazi, wakachukua watoto. Wote wakiwa bado wamelala. Sabrina akatoa maelezo na kuondoka na dereva, mpaka hospitalini. “Wewe niache hapa. Endelea na shuguli zako. Nikimaliza nitakuita.” “Unaweza kukisia muda?” “Sijui. Lakini wewe usiwe na wasiwasi. Unaweza hata kwenda nyumbani ukashusha mizigo yako. Nitakutaarifu kutokana na nitakavyozungumza na daktari.” “Sawa. Nakushukuru sana dada yangu.” “Karibu.” Dereva akaondoka Sabrina akaingia ndani, akamwambia mtu aliyemkuta hapo mapokezi kuwa hajisikii vizuri, anahisi pressure ipo juu, anaomba kumuona daktari, zaidi daktari anayemuona kwa maswala ya ujauzito. Akaambiwa yupo kliniki na kina mama wengine, ila anaweza kuanza kupimwa.

Akakubali, vipimo vikaanza. Kupimwa, pressure ikawa juu sana. Wakamwambia daktari ambaye huwa anamuona kwa kliniki za ujauzito. Akafika hapo alipopumzishwa Sabrina, kitanda cha sehemu ya mapokezi tu. “Huyu mtoto bado kidogo, mama Msindai.” “Basi nipe dawa nipumzike kabisa. Nimekuwa na hekaheka nafikiri ndio maana imepanda. Nikitulia itatulia.” “Nitakupa dawa na nitawaambia wakuwekee maji. Nataka ulale mpaka yaishe kabisa. Halafu nitakuja kukupima tena baadaye.” “Sawa.” Akamtumia ujumbe yule dereva afike hapo kumchukua saa 11 jioni kisha akatulia kabisa ili asisababishe madhara kwa mtoto wake. Alipopewa tu dawa akalala kabisa hata hakutaka kujua linaloendelea duniani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ambacho hakuwa akijua Sabrina, moto ulishawaka na mama Msindai alikuwa kooni kwa wanae mchana na usiku. “Sikuwaambia mimi hawa watoto wa kizungu watatuletea matatizo?” “Hakuna tatizo mama. Naomba utulie. Hii fujo yote inakaribia kufika ukingoni. Na safari hii tumeamua kuikomesha kabisa.” “Hakika Mungu akusaidie Junior. Hii familia inaangamia mikononi mwako hivihivi!” “Hakuna kuangamia mama. Tafadhali nipe muda wakurekebisha bila simu za kila wakati! Unanifanya nashindwa kufikiria.” “Siwezi nikatulia hivihivi sijui kinachoendelea!” “Basi naomba muda, nitakuwa nikikupa muendelezo kwa kila hatua nitakayokuwa nikifikia.” Junior akamuaga mama yake. Na kumpigia simu Jacinta.

“Umefikia wapi? Nashindwa kufanya kazi sababu ya simu za mama.” “Mimi nimeacha kupokea simu zake mpaka nikamilishe hili. Nilifikiria huyu askari kanzu atoke huko jela mwishoni mwa juma hili, ili kujua msimamo wa mwisho wa Max atakapozungumza na huyo mwanasheria wake.” “Mbona ni kama ulisema amejiridhisha kuwa Max amekataa kuwapa ushirikiano?” Junior akasikika kuchoka kusubiri. “Anasema ni kama wanaanza kumshawishi na anashawishika zaidi kutokana na ndugu wa Sabrina kuonekana kutoa ushirikiano. Wanaye mngojea ni Tino ambaye inasemekana anatarajia kurudi siku za karibuni. Hawajampa tarehe kamili. Ila ndugu wa Sabrina ndio wanaomshawishi na wamemwambia safari hii Tino pia yupo upande wake na wao wanao ushahidi wa kutosha kumtetetea.” “Daah!” Junior akachoka kabisa.

“Nilikwambia jana, Junior. Pengine umesahau.” “Nina mambo mengi Jacinta! Tafadhali nisaidie hili liishe nimtoe mama mgongoni kwangu.” “Nyinyi mmetaka kulimaliza moja kwa moja bila madhara, Junior. Mngekubali kutumia njia yangu, sasahivi tungekuwa tumeshasahau.” “Daah!” “Hawa watu wanataka kuharibu. Lazima kuwadhibiti. Sasa kama wewe na baba mnataka kwa njia zenu, juwa itachukua muda mrefu. Lazima kuwa wavumilivu. Ukitaka vya haraka, mwambie baba mniachie mimi.” “Acha nifikirie, jioni nitakupigia simu.” “Sawa.” Jacinta mjeshi, hacheki na kima, hajui kubembeleza. Junior mtaratibu, anataka mambo kwa hekima kama baba yake na Jacinta alimjua kaka yake akawa akimchukulia taratibu na kufanya vile anavyotaka yeye akijua mwishoni atachoshwa tu. Akamuacha mpaka asalimu amri mwenyewe. Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jioni Sabrina akarudi nyumbani na kupitiliza kuoga ndipo akaomba aletewe watoto wote. “Huyu ummemlisha nini mbona kitumbo kimejaa hivi! Eti Brayan.” “Pina ametoka kumpa uji sasahivi.” Sabrina akabaki ametulia hapo kitandani wanae wakicheza mpaka Jack aliporudi. “Vipi?” “Sasahivi nipo sawa. Nilijipandisha pressure. Nafikiri mshituko na kuumia.” “Nisikilize Sabrina. Usinichukie kwa sababu sikutaka kukuumiza. Nilijua ungejua mipango ya kwenu yakutaka kumsaidia Tino kupata watoto ingekuumiza sana.” “Najuta Jack! Najuta sana. Nahisi mimi mwenyewe ndiye niliyesababisha kumleta Tino karibu yao.” “Hata kidogo. Mwenzio nimejifunza kutoka kwa kaka kuwa makini. Acha niwatoe hawa nje, tuje tuzungumze.” Jack akacheza na wanae kidogo, akawatoa nje na kuwaambia wasubirie wakiwa na michezo yao.

Akarudi kwa Sabrina. “Tino ndiye aliyemtafuta Sabina kwa mara ingine tena akamkabidhi begi lenye vitu alivyotaka wapewe watoto, ukakataa, akalichukua mama yenu.” Sabrina akatulia akisikiliza. “Ukiwa kwenye harusi ya Pendo huna taarifa, Sabina na mama yenu walikutana na Tino ambaye tayari anayo restrain order. Si ndivyo ulivyoniambia?” “Lakini nilikaa Villa na hotelini kwa pesa ya Tino, Jack. Usilisaha hilo. Ni kama mimi mwenyewe nilijirudisha tena kwa Tino! Najitetea vipi?” “Hizo taarifa zilishafutwa. Hakuna sehemu inayoonyesha ulikaa Villa wala hotelini.” “Jack!” Sabrina alishituka mpaka akakaa.

“Si kazi ndogo. Sabina, mama yako na Tino walirudi pale hotelini na kwenye Villa kutafuta ushahidi kuonyesha nilikutelekeza wewe na watoto ndipo Tino akawasaidia.” “Jack!” “Kweli tena. Sijui ni kwa nini ndugu zako wanataka kuniangamiza, Sabrina.” “Ni njia ya kunikomoa mimi tu. Ukiona jinsi Tino alivyotengeneza pale nyumbani! Unaweza potea. Amewabadilisha kwa mahela anayowapa, nafikiri ndio maana wanamng’ang’ania.” “Ila Sabrina, mwisho sio mzuri. Nasikitika kusema hivi kwa kuwa ni ndugu zako, lakini mwisho si mzuri hata kidogo. Hivi tunavyozungumza, yupo mtu wa usalama wa taifa yupo alikofungwa Max,  kama na yeye ni muhalifu, akifuatilia kila kitu.” “Jackson Msindai!” “Kabisa Sabrina. Hawa watu wamepanga kutuangamiza, baba hawezi kukubali. Wanafuatiliwa kupita kiasi. Namsikitikia Sabina. Amejiingiza pabaya mno. Hawawezi kumuacha.” Jack akaendelea.

“Walimpa kila sababu ajitoe ili asiangamie na Tino pamoja na Max, lakini inavyoonekana yeye Sabina ndio yupo  mstari wa mbele, akiunganisha pande zote ambazo zipo kinyume yetu. Mara kwa mara anaonekana huko rumande akimshawishi Max, akiwa ametumwa na Tino.” Sabrina akaumia sana. “Hivi tunavyozungumza, Sabina amemtafuta aliyekuwa mke wa Tino.” “Lela?” “Nafikiri huyohuyo. Sasa kwa kuwa nafikiri wamegundua simu zao zinasikilizwa, wameacha kuzungumza kwa simu. Lakini Sabrina, hili nakwambia wewe kwa kuwa imeshajulikana kuwa unajua, nimeombwa kuzungumza na wewe ili tuwe ukurasa mmoja. Tafadhali usipandishe pressure kwa ajili ya haya.” “Wewe niambie tu. Maana mama alizungumza hata juu ya Lela, lakini akiwa na jazba sana. Na naumia kuona kumbe ni Sabina mwenyewe ndiye aliyemtafuta Lela! Hakika ndugu zangu wananichukia Jack. Nilijua chuki dhidi yangu imeisha, nipo upande woa, lakini hili limewaanika wazi kabisa! Wamemchagua Tino, Max na wengine dhidi yangu! Tena Sabina ndio mstari wa mbele akishindwa hata kuwasiliana na mimi nikijua yupo busy na kazi kumbe ana muda wa kuzunguka ili kuniangamiza!” Sabrina akazidi kunung’unika.

“Nikikwambia Sabina anafuatiliwa, ni anafuatiliwa kila aendapo. Walikutana na huyo aliyekuwa mke wa Tino. Sabina amemwambia kuwa Tino alimsaliti wakiwa kwenye ndoa, akazaa na wewe. Kwa hiyo amshitaki Tino.” “Sasa mbona tena wanageukana na Tino?” “Wajanja sana. Hiyo ni akili waliyopewa na Max wakiwa na wakili wao. Bila kujua, Max aliporudi ndani huko rumande waliposhikiliwa na huyo askari kanzu, akamueleza kila kitu, mipango yote wanayopanga. Ndio maana sasahivi kila wakienda kumtembelea Max, na huyo askari kanzu anatembelewa. Anakaa nao karibu kujua wanachopanga na kuwarikodi. Sasa tulitaka kuachana na Max ila baada yakupewa onyo kali. Max alionekana kukataa mwanzoni. Ila sasahivi ni kama ameanza kushawishika ndio sasa na yeye kesi yake inataka kusomwa ili ahukumiwe kwa makosa yake. Nasikitika kwa kuwa hata mkewe hatabaki salama.” “Jamani Tino anaangamiza wengi!” Sabrina akasikika kuumia zaidi.

“Sana Sabrina. Kaka na baba wamesema wanataka haki itendeke bila kuonewa mtu wala kuachwa mtu ili kukomesha hili kabisa.” “Mzee Msindai!” “Ni vile mama hajui kama baba anashugulikia hili kwa undani. Nikikwambia amefanya, ni zaidi nitakavyokwambia na baba huwa akifanya jambo anafanya kikamilifu mpaka likamilike sio nusunusu. Akikwambia anaweka kikomo, ujue anaweka kikomo. Ameshampata yule daktari. Amehojiwa kisheria kabisa. Ameeleza kila kitu juu ya mipango waliyokubaliana  na Max juu ya kuuwa hawa watoto. Na amefungiwa mahali mpaka kesi ikamilike.” “Jackson!” Sabrina akazidi kushangazwa jinsi mambo makubwa na mazito yanavyoendelea yeye akiwa hana hata habari!

 “Baba hataki kufanyike kosa. Wakimfikia na kumbadilisha mawazo au hata kumdhuru ili ashindwe kutokea mahakamani kutoa ushahidi wake!” Sabrina akabaki ametoa macho. “Amekusanya ushahidi wote tena kwa haraka na kumkabidhi wakili wetu. Aliyekuwa akisubiriwa ni Jacinta, upande wa Max na kujaribu kumtoa Sabina. Lakini kwa jinsi nilivyoona, imeshindikana. Sabina amekusudia kwelikweli. Na inavyosemekana amewahakikishia mama yenu yupo tayari kutoa ushahidi pia, ili kumsaidia Tino kwamba wakati mimi nimewatelekeza, eti yeye na Tino ndio walikuwa wakiwalea wewe na watoto.” Sabrina akazidi kuumia. “Naomba turudi kwenye swala la Lela.”

“Ndio hivyo walivyokuwa wamepanga kama kumtibua Lela. Max amewahakikishia popote kwenye harufu ya pesa, Lela anakuwa kama mwendawazimu hawezi kutulia. Kwa hiyo wamemchokonoa tu, ili aanzishe tena kesi ya madai. Itabidi uchunguzi ufanyike ili kujua kama kweli Tino alizaa nje ya ndoa. Watatafutwa watoto walipo. Mahakama itaamuru watoto wafanyiwe vipimo ili kujua kama kweli ni wa Tino, si itabidi sasa DNA ifanyike kwa kuwa mahakama imeamuru! Ikishajulikana ni watoto wa Tino ndio sasa wao waendelee kuanzia hapo mpaka Tino aje apate watoto. Kwa hiyo Lela atakuwa ni kama anachokonoa tu. Sasa inavyosemekana, au walivyosikia hao watu wakati Sabina akizungumza na Lela ni kuwa, Lela akutafute wewe, akuulize. Na ndio maana nimetumwa kukwambia ili ujiandae.” “Mimi sitaki kukutana na Lela. Sitaki kabisa Jack. Kwa sababu najua anachotaka ni kujua kama kweli nilikuwa na mahusiano na Tino na kama nilizaa naye. Sipo tayari kulijadili hilo tena. Na yeyote yule, sitaki. Nataka nitulie kabisa mpaka siku za huyu mtoto kufika, azaliwe.”

“Leo niliingiwa hofu nilipoona pressure ipo juu na daktari kuniambia mtoto bado!” “Daktari!?” “Ilibidi kwenda mimi mwenyewe kujisalimisha Jack. Nilitoka nyumbani nikiwa nimechafuka kwelikweli. Ile kukaa njiani mpaka hapa nikiwafikiria watu wa nyumbani kwetu, ikanipandisha pressure ikabidi kwenda tu hospitalini. Ndio nikaambiwa pressure ipo juu, na mtoto hayupo tayari.” “Kwa nini hukuniambia?” “Nilitaka anipe dawa, nilale kabisa. Sikutaka kuzungumza na yeyote yule. Tafadhali na wewe nisaidie Jack. Niweke mbali na hao watu au kesi, angalau mpaka nijifungue salama. Haya mambo yapo tu. Hizi kesi zipo tu. Lakini nikimpoteza huyu mtoto ndio nimempoteza kabisa, hasara yangu mimi.” “Ni hasara yetu. Na mimi nataka mwanangu azaliwe salama. Ila nakuelewa. Nitamwambia kaka wakuache mpaka mwisho kabisa itakapolazimu. Hata kama itabidi kuivuta hii kesi, iendelee kuvutwa tu, ili utulie tupate huyo mtoto.” Sabrina aliingiwa na hofu hakujua kama mambo ni makubwa kwa kiasi hicho.

“Nikuulize kitu Sabrina?” “Juu ya nini?” “Ujue Tino atafungwa na anaweza akahukumiwa kifungo cha maisha kwa kusudio la kutaka kuua?” “Hakika sijali Jack. Acha Mungu ashugulike nao. Sina kosa, ni kwa nini wanataka kuniangamiza bila sababu? Tino hakutaka hawa watoto kabisa. Kwa nini leo anafanya hivi? Na upande wa Sabina, yeye ni dada yangu mimi, kwa nini asinisaidie kama hivi wewe unavyosaidiwa na watu wa nyumbani kwenu! Wote wamesimama na wewe hata kama wanaona hustahili, lakini wapo kukusaidia. Kilichowashinda wao kunilinda ni nini mpaka wakamuacha Mungu wangu ashuke, apigane vita yangu? Acha Mungu ajitukuze hata katika hili Jack. Sikutaka kuua viumbe wake, ndio ilikuwa kosa langu! Acha ashuke yeye mwenyewe Mungu anitetea. Wamemtafuta Mungu mpaka ameitika. Acha ashugulike nao. Na leo nimemuonya baba nikimwambia amwambie Sabina aache hila. Sasa sijui!” “Nahisi wameshachelewa.” Hilo likamshitua Sabrina.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kikulacho Ki Nguoni Mwako. Kila Pande Imejipanga. Nani Mshindi?

 Nani Mwenye Kisu Kikali? Usikose Muendelezo

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment