Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 59. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 59.

 Wakati Wa Mungu.



iku inayofuata walikutana kwenye viwanja vya bunge ikiwa mapema tu. Kila mtu alikuwa amependeza kwa shuguli nzima. Jack akawapa habari za kifo cha mtoto wa kwanza wa Ngoi. Junior akapiga simu kwa Willy wote wakatoa pole wakiwa wamebakisha muda mfupi waingie bungeni. Ukweli ilisikitisha. “Kesho tutakuwa hapo kukuunga mkono Willy. Poleni sana.” Junior akamalizia ili waingie ndani, wasichelewe. Wakaagana na kuanza kuelekea ndani.

Wakamuona Jack anamvuta mkewe pembeni. “Umeipenda hii suti?” “Nimeipenda na umependeza sana Mheshimiwa Msindai.” Jack akacheka. “Asante Brina.” “Asante ya nini tena!?” “Kunifikisha mpaka hapa. Hakika usingekuwa wewe watu wote hawa wasingekuwepo hapa leo wakifurahia hivi. Ushauri wako wakuendelea kubakia kwenye siasa kule Singida ndio umenisogeza hapa. Nakushukuru.” “Karibu.” Angalau hilo likamfurahisha Sabrina. Katika wanaume wote aliosimama nao, Jack amemtambua.

“Hayo mabusu mheshimiwa Msindai ungeyaendeleza ukitoka huko kuapishwa.” Jacinta akafanya wote wakawageukia wakamkuta Jack akiwa anambusu mkewe. Sabrina akacheka na kusogea.  Jackson akawaaga wanae vizuri na kuwaacha mama yao amewashika mkono, akaingia sehemu nyingine akiwa na kaka yake, waziri Msindai wakati wageni wao wakielekea sehemu wanayofikia wageni hapo bungeni.

Jackson Msindai akafanikiwa rasmi kusimama ndani ya bunge, akiwa anakaribia kuwa mmoja wao. Ikawa ni ndoto yake iliyotimia akiwa anajua kabisa aliyefanya yote hayo ni Sabrina. Alikaribia kupishana na huo muujiza akiwa amefunga, ameomba na mkewe, wakasubiri bila kuona mabadiliko yeyote huko chamani. Jackson ambaye alitegemea mfungo wake ulete matokeo ya haraka ikawa sivyo mpaka akakata tamaa na kutaka kuachana kabisa na mambo ya siasa. Lakini kumbe pale alipokuwa akipatizama yeye, sipo Mungu alipokuwa amemkusudia kwa wakati ule. Mungu alimuwazia mema zaidi, tena kwa haraka. Ikawa amepata zaidi ya alivyoomba tena kwa haraka sio kusubiri mpaka wakati wa uchaguzi mkuu miaka ijayo, ndipo agombanie tena.

Vikafanyika viapo hapo, Jackson Msindai akaapishwa rasmi kuwa mbunge wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Baada ya hapo ikawa tafrija fupi. Ukweli kulikuwa na amani. Hapakuwa na maneno maneno. Ikawa kama mama Msindai naye anajihami na Sabrina. Sabrina naye hata hakumsogelea. Jacinta akawa karibu naye kila wakati. Wakati wanakaribia kuondoka Sabrina akacheka na kumuangalia Junior.

“Nini?” Junior akauliza na tabasamu. “Mimi nina swali linalonisumbua kidogo, shem. Nilikuwa nikisubiria wakati Claire hayupo nikuulize.” Wakamuangalia Claire pale alipokuwa na watoto wa Sabrina na Clei wakiendelea na yao. Wakawa wakicheka zaidi kumcheka Claire. “Mwanangu mtu mzuri sana tu, ila Clei ndio anamchokoza.” Joy akafanya wacheke zaidi. Junior akamgeukia Sabrina. “Karibu.” “Eti mimi nimekuona. Sijui kama nipo sahihi! Katika kila ugomvi wa Claire na Cleiton, huwa huingilii kabisa. Hata mziwanda wako alie, hutawaingilia utambembeleza tu. Ni kwa nini?” “Asante Sabrina. Na mimi nilishamlalamikia huyu Junior. Nikamwambia akimkemea Clei mara moja tu, ataacha kunilizia mwanangu. Clei ananifanya mimi kama bibi yake, ananichezea hanisikilizi.” Joy akalalamika.

“Ngoja nikwambie ukweli Sabrina. Katika kila baraka Mungu anayokupa, kuna jinsi ya kuishi nayo. Junior mume wa Joy wa kabla hajawa waziri, sie mume huyu aliyekuwa waziri. Kuna garama zake tunalipa ambazo kama mimi na yeye Joy hatujakaa sawa, tukakubaliana, familia yetu ingeyumba sana. Na wewe utakuja kuona. Jack yule aliyekuwa muhasibu wa Singida, hatakuwa huyu aliyeapishwa leo. Ni jambo zuri, lakini hii baraka itakuja na mabadiliko mengi sana, lazima ujiandae haswa.” “Ni kweli mwaya.” Hapo hata Joy akakubali.

“Maisha ya Jack sijui kubeba watoto na kukumbatia hivi kila wakati, yatapungua kwa asilimia karibu na 80 kwa sababu ya majukumu atakayokabidhiwa. Kipo kipindi hatakuwepo nyumbani, itakulazimu kulea peke yako. Hayo anayokufanyia sasahivi kwa ukaribu hivyo, hataweza kuyafanya japo atatamani. Vipo vipindi utauguza watoto peke yako. Kwa asilimia 88 utaishia kulea hao watoto peke yako, kwa maisha yao ya kila siku. Ndicho kinachotokea kwangu na Joy. Hata nikiwa pale Dar, nakuwa na majukumu ambayo yananinyima muda wa kuwa na watoto kwa karibu kama hivi Joy. Napata nao muda mfupi sana, na sitaki nikiwa nao niwe mtu wa kesi tu.” “Lakini kweli. Maana unaweza kujikuta watoto wanakuona kama mwalimu mkuu wa shule zile tulizosoma sisi za kuchapwa sio kama hawa watoto wa siku hizi wanaonywa kwa maneno tu.” Jacinta akaongeza na kucheka wakikubaliana naye.

“Ewaa! Yaani wewe ukirudi nyumbani ni kesi na adhabu tu! Watoto hawajakuona muda mrefu, wanahamu na wewe, na wewe unarudi nakuanza mashitaka na adhabu! Hakuna mahusiano mengine isipokuwa kujibu mashitaka! Hapana. Mimi huwa namwambia Joy awaadhibu yeye mwenyewe anayeishi nao kila siku. Anajua wapi pakukemea na wakati gani wakupooza. Sasa mimi nikiwaadhibu, naondoka nikiwa nimegombana nao, nakuwa sina muda mwingine wakutengeneza mahusiano mengine.” “Cleiton atasikia kila kitu lakini si kwenye swala la Claire jamani! Sijui yukoje yule mtoto jamani!” Wakacheka.

 “Lakini ukweli, wao wenyewe. Huyu Joy na Claire hawawezi kuwa sehemu bila Cleiton.” Wakaanza kucheka. “Huwa wanamuita wao wenyewe.” CJ akaongeza, Joy akazidi kucheka. “Nyumba inapooza bwana!” “Umemsikia sasa Joy mwenyewe?” Junior akauliza. “Wanaweza wakawa na safari zao wao wawili, Joy na Claire, lakini hawawezi kwenda bila Clei. Hata kama mwanangu anashuguli zake, basi watambembeleza mpaka waongozane nae.” “Nikienda sehemu ananisaidia kuniangalizia mwanangu wakati nafanya mambo yangu.” Wakazidi kucheka.

“Kwa hiyo shem ushawaona hawa ni waarabu wa pemba?” Sabrina akauliza akicheka. “Haswaa! Wanajuana kwa vilemba. Huyu Joy hawezi kuwa popote bila Clei. Popote alipo Joy, atamtaka na Clei awepo. Muda na wakati wowote Clei akiwa hayupo shule, ukipiga simu basi ujue atakuwa yupo na mama yake. Na hapo ujue lazima Claire naye yupo hapo akinyonya vidole vyake huku akimshikashika mama yake. Sasa na yeye Clei akiwa katikati yao hawa, hana chakufanya kwa kuwa michezo yake na Claire haiendani, basi mchezo wake ni vile anavyomchokoza mwenzie, akilia ndio anaona raha. Wakimfukuza ni dakika 10 tu.” “Tena hizo ni nyingi dad. Wao wenyewe huwa wanamuita.” CJ akaongeza nakufanya wazidi kucheka.

“Kumbe!” “Muulize Joy huyu hapa. Hawajiwezi bila Clei. Lakini kingine na kikubwa mimi shida yangu si Cleiton. Shida yangu ni huyu dada yao. Claire. Claire anakipaji cha uongozi kama huyu anti yake. Mbali na vilio vya Clei, muulize CJ jinsi anavyojua kujipangia mambo yake na kuyasimamia mpaka huwa anatushangaza.” “Kwani si ndiye aliyetufanya tusije huku siku moja na mama! Anasema alikuwa tayari ameshamuahidi rafiki yake atahudhuria birthday yake, eti alishanunua mpaka zawadi, lazima yeye aende huko. Halafu alivyo sasa, ananiambia.” Jacinta akacheka na kutingisha kichwa kwa masikitiko. Wakaanza kucheka.

“Eti, wewe anti tangulia tu na kina bibi. Usimuache Clei. Halafu utatutafutia usafiri mimi na mama pamoja na CJ utufikishe Dodoma kesho yake.” Walicheka sana. “Nikampigia simu baba yake. Nikamwambia mwanae ananipanga! Na kashaniagiza kesho nimtafutie usafiri wake, mama yake na CJ. Ila Clei naweza kutangulia naye tu.” Wakazidi kucheka. “Akiwa na jambo lake, hana kusitasita.” “Halafu ni msafi sana, kila kitu chake anapangilia vizuri huwezi kukuta vitu vyake vinazagaa hovyo.” CJ akaongeza. “Na kweli anti yangu ni msafi haswa. Anajipenda kweli!” “Namuona. Kila wakati vitu vyake visafi kama mama yake.” Sabrina akaongeza. “Mwenyewe anasema yupo kama anti yake wala si mimi!” Joy akaongeza.

 “Basi hata akiwa shule yupo hivyohivyo. Very smart mpaka huwa anasifiwa. Mungu akimjalia, anaweza kuwa kama anti yake Jacinta.” “Mimi nimemwambia nataka awe zaidi yangu.” Jacinta akafanya wacheke. “Na mwenyewe anapenda sana kuongoza hata shuleni kwoa ni kiongozi. Sasa huwa namwambia watu kama kina Cleiton wapo wengi tu kila mahali. Lazima yeye mwenyewe ajue jinsi ya kumkabili kama anti yake anavyoongoza wanaume wenye kila haiba na hashindwi.” “Lakini anasema Clei amezidi sana.” Joy akamtetea nakufanya wazidi kucheka.

“Shemeji yangu unahekima!” “Inabidi kumuandaa! Yeye amezaliwa mwanamke mwenye kipaji cha uongozi. Atafanyaje akiwa analia mbele yao huku ananyonya vidole?” “Jamani mwanangu ataacha kunyonya vidole! Bado mdogo.” “Sawa Joy.” Junior akakubali bila shida. “Ni vile anampenda.” Sabrina akaongeza. “Tena nakwambia anampenda sana Clei. Japokuwa hakawii kumliza, lakini hasikii raha bila ya kumuona. Nikimuita sasahivi hapa Clei, nikampa kitu cha kufanya hapahapa, dakika tano nyingi. Claire ataacha kila mchezo pale na kuja kumfuata hapa. Yeye mwenyewe anamfuata Clei. Sasa ndio nimemuachia kuwa Clei iwe ni jukumu lake mwenyewe. Hawezi kumkwepa Clei kama vile uwe bosi kwenye ofisi, halafu upate watu wa chini yako wabovu. Utaacha kazi?” “Hapana.” Akajibu Sabrina.

“Basi ndio nimemuachia Clei awajibike naye yeye mwenyewe. Lazima kesi zake ajue jinsi ya kuzikabili yeye mwenyewe. Hatuwezi kumsaidia kukabiliana na kila matatizo kwenye maisha yake. Atahangaika naye hivyohivyo mpaka atakuja kummudu tu. Na akisha mmudu basi ataacha kulialia hovyo. Atakua hamsumbui tena. Ila Clei akizidisha kwa mdogo wake huwa CJ naye anammudu Clei, anajua jinsi ya kumtuliza.” “Tena wakati mwingine anamsikiliza CJ kuliko mimi, mpaka mimi huwa ndio maana namrushia viatu maana kumkimbiza simpati.” Wakazidi kucheka.

Wakapata wakati mzuri ndipo wakaondoka hapo na mumewe kurudi hotelini. Walikuwa wakikaa hapo kwa siku ambazo bunge linaendelea. Safari hii Sabrina aliaga chamani huko Singida. Hakutoroka na bado alikuwa akiwasiliana nao kwa simu. Ila hawakuwa na uhakika kama Jack na mkewe watakuja kurudi tena Singida. Likabakia fumbo huko Singida japo Sabrina na Jack waliwahakikishia pale ni nyumbani lazima warudi tu.

Siku inayofuata Jack na familia yake wote wakaondoka Dodoma kwenda Dar. Ila Jack na Junior walikuwa wakienda msibani kwa siku moja tu kisha kurudi tena Dodoma kuendelea na shuguli za Bunge. Sabrina akabakia hotelini na wanae wakimsubiria Jack arudi, amalize shuguli zake za Bunge warudi kwao Singida.

Hakuna Msiba usiokuwa na Mwenzie.

J

ack na Junior wakarudi hapo Dodoma wakiwa bado hawajamzika kaka yake Willy. Waliamua kusubiria ndugu wengine kwa mazishi. Sabrina akawa akibakia hotelini wakati Jack akihudhuria vikao vya bunge. Alijawa furaha huyo, Sabrina akawa akimcheka tu. Juma hilo nalo likaenda Sabrina akiwa anapata mapumziko yake na wanae. Juma lilipofikia ukingoni, wakiwa wametoka kumzika tu mtoto wa kwanza wa mzee Ngoi, Patric, dada yao mkubwa, Stella, akiwa anaoga bafuni, kutoa vumbi la makaburini, na yeye akaanguka na kufa papohapo huko bafuni. Nazo zikawa habari za kushitua sana. Huyo dada alikuwa na pressure inayopanda, akahisiwa pengine ilikuwa juu ila akashindwa kutumia dawa zake sababu ya msongo wa msiba wa kaka yake.

          Pendo akampigia tena simu Sabrina. Akamuelezea kila kitu. “Lakini dada, naomba muombe. Msipuuze. Hii roho ya mauti umefunguliwa, ipo kuangamiza. Tafadhali mwambie Willy asipuuze. Ombeni ulinzi wa kimungu.” “Inahuzunisha wewe! Stella ameacha binti wazuri! Mmoja anaenda chuo kikuu mwaka huu! Hata hajamuona mwanae akimaliza jamani! Inauma sana. Japokuwa Stella hakuwa akinipenda lakini bado wanae wanamuhitaji, Sabrina!” Akalia hapo Pendo, Sabrina akimtuliza.

          Baada ya ndugu kukusanyika, naye huyo dada akazikwa. Likawa jambo la kuumiza na kushangaza kila mtu. Vifo viwili vyakufululiza! Sabrina akaona sio sawa. akampigia mama yake Pendo. “Mama, naomba unisikilize. Najua kwa sasa Pendo ametingwa na uzazi pamoja na ulezi, lakini ipo roho ya mauti inayotembea kwenye familia ya Ngoi. Niliiona kabla ya kifo cha yule kaka yao Patric. Nikamwambia Pendo, lakini alisahau. Naomba zungumza nao, Willy akae sawa na Mungu, ili apate ulinzi wa ki Mungu. Na kama upo karibu na Prisca naye uzungumze naye amkimbilie Mungu.” “Na mimi nilihisi sio kawaida jamani! Vifo mfululizo hivyo! Nitazungumza na Pendo pamoja na Willy. Hiki sio kitu cha kawaida jamani! Wataisha wote!” Wakazungumza na mama Kenton mpaka Sabrina akaridhika kuwa huyo mama amemuelewa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

          Baada ya Bunge kuisha Jack na Sabrina wakarudi Singida. Safari hii wakapokelewa kama mashujaa kwelikweli. Hakuna aliyeamini kama wangerudi, wasijue bado Jack anamasilahi makubwa sana kwenye hilo jimbo na Sabrina analishikilia hilo jimbo kwa maombi. Safari hii waliporudi chamani hata wale waliogeuzwa mioyo wakawa upande wa Jack. Jack huyu aliyerudi ni Mheshimiwa Jackson Msindai. Heshima ikaongezeka na bado akawa akitoa ushirikiano wa karibu sana hapo chamani na kwenye ofisi alikokuwa akifanyia kazi kuhakikisha anapaacha salama. Hilo nalo likamuongezea heshima.

          Falme Zote Zipo Kazini Zikitenda Kazi Na Watu.

B

ado walikuwa wakipokea pole za kuondokewa na ndugu zao hao wakubwa kwa kufa kwa kufuatana, bila kupumzika. Mtoto watatu wa Ngoi naye akiwa baa na rafiki zake wakinywa, gafla akaanguka na kufa papohapo. Ukawa mshituko mkubwa, kwani alinguka mbele ya wenzake wakadhani ni pombe imemzidia. Kumuangalia pale chini ikawa ameshapoteza uhai. Usiku mkewe akiwa anakaribia kulala, akiwa ameshazoea tabia ya mumewe kuchelewa kurudi nyumbani, akapigiwa simu na marafiki zake waliozoea kunywa naye kuwa mumewe amepelekwa hospitalini akiwa si mgonjwa ila maiti. Usiku huohuo Willy akapigiwa tena simu. Na Pendo naye akampigia Sabrina. “Naomba tuombe wote sasahivi Sabrina. Inakua kama tunapigwa na upofu hivi, tunasahau kuomba kabisa. Inakua kabla hatujakutana wote na kuomba, basi jambo lakutuchukua akili linatuingilia, tunashindwa kuomba, basi ndio tunasahau mpaka mtu anaanguka tena na kufa! Wanaanguka kama upupu jamani! Sasahivi amebakia Willy wangu tu na Prisca! Hapana Sabrina. Lipo jambo.”

          “Tutaomba dada, lakini nakusihi sana mwambie Willy asimame kama yeye mbele za Mungu ili Mungu mwenyewe aweke ulinzi wake kwake. Shetani hana kazi ingine isipokuwa kuua, kuharibu na kuangamiza. Sina jinsi nyingine ya kuwasihi ila hiyo. Dada, shetani anawinda watoto wa Ngoi. Ni kwa nini, mimi na wewe hatujui.” “Mimi mpaka namuhisi ni Zelda. Na hivi alizaa mtoto wa kike na akaona sasahivi ni kama watoto wa Ngoi wamemgeuka, ndio anawatoa wampishe.” “Basi usipuuze dada, OMBENI. Roho ya maangamizi imetumwa kwenye hiyo familia. Hakikisha haipiti nyumbani kwako.” “Naomba tumuombee sasahivi Willy wangu. Tafadhali Sabrina.” Wawili hao wakaanza maombi kama zamani.

          Hilo juma Pendo na Sabrina wa zamani wakarudia maombi yao ya zamani. Kila siku walikutana kwa simu na kuomba. Japokuwa Prisca hakuwa akimpenda Pendo na wote walijua, lakini Pendo alimpigia simu na kumtaka afike kwake wazungumze. Pendo akazungumza naye taratibu kwa kina mpaka Prisca akakubaliana naye waombe pamoja. Prisca naye akaingia kwenye kundi la Sabrina na Pendo. Maombi yakaendelea huku bado wanasubiri kuzika. Willy na yeye akaanza kuomba na mkewe. Mtindo wa kusema wapo busy, ukakoma. Mungu akawekwa mbele.

Hapohapo msibani, nyumbani kwa marehemu walikuwa wakianza kuomba hapo, mpaka wanasahau kama ni msibani. Mke wa marehemu kaka yao Patric, shemeji yao mume wa Stella, na watoto wao, mke wa huyo marehemu, kina Pendo, Willy, na Prisca walikuwa wakiomba haswa hapo msibani. Wakawa wakiomba ulinzi wa Mungu huku wakivunja roho ya mauti. Walikuwa wakisubiria mida ya usiku ambapo wale wageni wanao ondoka hapo msibani wakiondoka, basi wao wenyewe na watu wao wa karibu ndio inapoanzishwa sala ya nguvu, mpaka kunapambazuka. Walifanya hivyo mpaka walipozika. Zelda hakuwa akilala msibani. Na walimuona hapo kama mara moja tu, akarudi siku ya mazishi. Na walipozika akaondokea hukohuko makaburini hakurudi tena hapo msibani.

Baada ya kumzika huyo kaka yao, siku inayofuata Willy akampigia simu baba yake akiomba ndugu wakutane nyumbani kwao, yaani kwa mzee Ngoi kwa ajili ya mazungumzo. Lakini Zelda akakataa akiweka ugumu akisema kuwa hataweza kukaribisha wageni hapo nyumbani kwake kwa kipindi hicho. Akatoa sababu nyingi zisizo na mashiko. Willy hakutaka kubishana naye, akashukuru na kukata simu. Lakini baada ya kukata tu simu Willy akawaambia ndugu zake waliokuwa wakisubiria jibu wakiwa wamekusanyika hapohapo msibani kwa maombi kuwa watakwenda hivyohivyo ila kwa kumshitukiza yeye ambaye ndio mlengwa mkubwa. Walitaka mazungumzo lakini lengo kubwa ni kufanya maombi na yeye Zelda akiwepo.

Wakatangaziana siku tatu za mfungo. Familia nzima wakaingia mfungoni wakijitakasa na kutaka kujisogeza zaidi patakatifu kwa Mungu kwa ajili ya ulinzi wakijua vita inayowakabili mbeleni. Kuanzia familia ya marehemu kaka yao Patric mpaka familia ya mtoto wa mwisho ambaye ni Prisca, walikubaliana wote na watoto wao wafunge isipokuwa wale watoto wadogo kabisa. Mpaka watoto wao wakakubali. Wote wakaingia mfungoni, Sabrina naye akawasaidia. Akaungana nao kwenye maombi. Wakawa wakijiandaa kwa maombi kama wanao kwenda vitani kumbe kwenye nyumba waliyozaliwa na kukulia watoto hao wanao uwawa mchana na usiku, ila safari hii Zelda akiwa mama mwenye nyumba siye mama yao aliyechimba hilo kaburi na kuishia kuingiza wanae mwenyewe wala si Pendo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usikose Muendelezo Kujua Nani Anabaki Kwenye Familia Ya Ngoi, Nani Anamfuata Marehemu Mama Yao Pamoja Na Ndugu Zao waliotangulia Mbele Ya Haki!

Hatima Ya Yote Ni Nini?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment