“Huyu wa mwisho shem. Tumepanga wanne
tu.” Junior akacheka akitingisha kichwa kama anayesikitika. “Hamkutaka
kusubiria angalau Brayan afikishe…” “Tunataka kusomesha tukiwa vijana.” Akawahi
kujibu Jack, wote wakacheka. “Haya hongereni kwa familia nzuri. Ila Sabrina
usisahau ulizaa kwa upasuaji. Kuwa makini.” “Yupo daktari anamsaidia kwa
karibu. Hata baba anasema ni mzuri. Tusiwe na wasiwasi.” “Mzee ameniambia
mnazungumza sana siku hizi.” “Ni kweli, sio kama ilivyokuwa zamani. Nimemuona amebadilika
kweli! Alikuwa akinipigia mara kwa mara tokea nilipotoka nyumbani mara ya mwisho.
Na huwa anapiga kuulizia hali za wajukuu zake.” “Na yeye ndiye aliyeniambia
kama ulimpata Sabrina. Akashauri tukuache kwanza.” “Niliona nimwambie tu. Alikuwa
na wasiwasi sana na Sabrina kwa kuwa alizaa kwa upasuaji, halafu akaondoka na watoto wote. Nilipompata Sabrina ikabidi
kumtaarifu kuwa wote wapo salama.” Sabrina alikuwa kimya tu hapo akiangalia
watoto wakati wakizungumza.
“Umemwambia
mama juu ya hili?” “Hapana. Tokea siku ile pale nyumbani sijazungumza naye
tena. Hata hivyo najua atakuwa anajua. Hamna jipya.” Junior akanyamaza kama
anayefikiria. Jack akajua kuna anachotaka kuwaambia ila anatafuta hekima ya kuzungumza
naye. Nao wakanyamaza kabisa. Ni Junior, waziri, halafu mstaarabu sana. Wakanyamaza
mbele yake kama kumpa nafasi. Kisha akaanza. “Sabrina, shemeji yangu, najua hili
nilishakwambia. Lakini naomba nirudie tena.” Sabrina akamgeukia vizuri. “Naomba
msinichoke.” “Tushauri tu shem. Najua wewe unatuwazia mazuri na ulipo ndipo
Jack anataka kuwepo. Kwa hiyo tunakutegemea kwa ushauri, wala usisite kwetu.” “Kweli?”
“Kabisa Shem. Wewe unaweza kutushauri kwa chochote. Hata kutukemea kabisa.”
Jack akabaki kimya akiwa ameshajua ni nini kaka yake anataka kuzungumzia.
“Basi
kwa ruhusa hiyo, acha niseme tu.” Junior akaendelea. “Najua mama amewaumiza
sana. Na najua amekosa. Lakini bado ni mama.” “Lakini hanitaki mimi na hawa
watoto. Sasa tutafanyaje?” “Sijui Mungu atawasaidia vipi! Lakini nilimsikia
Jack akisema ulikubali kuwa haya mapito ni yako wewe na mama.” Sabrina
akainama. “Si umekubali niwaambie?” “Ndiyo.” Sabrina akajibu macho chini. “Basi
mwache Mungu ashugulike na mama, isiwe wewe. Wewe kama wewe umefanya kwa nafasi
yako na kila mtu anatambua juhudi zako na upendo wako kwa Jack. Huna hila. Mwache
yeye mama ahusike na Jack kwa vile atakavyoweza. Jack amejifunza kutokana na
kilichotokea. Nina uhakika baba ameshazungumza naye sana kama alivyozungumza na
mimi, na ameelewa. Jack mwenyewe atakulinda na mama.” Junior akaendelea
taratibu tu.
“Binafsi
baba alinifundisha sana juu ya ndoa yangu na jinsi ya kuishi na mama. Nafikiri ndio
maana mimi na Joy tumebaki salama. Haikuwa rahisi na wala si rahisi. Wote tungetamani
ingekuwa tofauti, lakini sivyo. Bado mama ni mama yangu mimi na mama mkwe wake Joy.
Haitabadilika. Basi mwache Mungu afanye. Ila kwa kitu kinachotokea kwa Jack
kesho kutwa, nina uhakika mama na baba wangefurahia kufanya kama
walichonifanyia mimi siku naapishwa kwa mara ya kwanza. Ile furaha niliyoiona
kwa mama usoni kwake siku alipokuwepo hapa Dodoma nikiapishwa, namuombea Jack kwako,
asije na yeye kuikosa. Imenisaidia sana kwenye huu uongozi na kunifanya nisibweteke
nikijua sijiwakilishi mimi tu na Joy, bali na mama yangu pamoja na familia
nzima ya Msindai, wananitizama na kunitegemea sana. Namuombea mama Msindai
kesho awepo hapa, Sabrina. Ashuhudie kuapishwa kwa Jackson kesho kutwa. Najua yeye
anaweza asiseme, lakini najua angetamani na zilikuwa ndoto zake kuwepo hapa
wakati Jack akiapishwa.” “Mimi sina shida shem. Hata kama uwepo wangu na watoto
wangu utamsumbua..” “Watoto wetu.” Jack akarekebisha.
“Namaanisha
hawa asiowataka mam.…” “Hawa watoto wote ni wangu mimi, kaka. Na hapo ndipo inapokuwa
tatizo. Mama akiwepo tu kwenye picha, basi kunaanza kuwa na matabaka. Mimi hilo
ndilo nisilopenda.” “Naomba utulie Jack. Ninachotaka kusema ni kwamba hili
jambo ni la heri sitaki tulifanye liwe sivyo. Mama anakaribishwa hapa. Bila shida
kabisa. Ila ikitokea uwepo wangu hapa utamsumbua kama siku ile kwenye harusi ya
Pendo na Willy, mimi na watoto tutaondoka bila shida.” “Sidhani kama safari hii
tutafika huko.” Junior akamtuliza Sabrina, lakini Sabrina hakujibu. Pakazuka ukimya.
“Acha
mimi nirudi chumbani nikambadilishe huyu kaka.” Sabrina akaaga kama kuwapa
nafasi. Jack kimya akiwa anajua kabisa anawapisha, Brayan hakuhitaji
kubadilishwa. “Basi nitakuja kuwaaga kabla ya kuondoka. Ila mna watoto
watulivu!” Wakawaangalia wale mapacha pembeni ya Jack. “Hao hivyo walivyo hapo
na hiyo michoro yao, hutawasikia wakizungumza wala kutoka hapo mpaka wamuone
baba yao ananyanyuka hapo ndio utawaona ni kama wamekatwa mikono.” Junior
akacheka akiwaangalia. “Hapo walipo ni kama hawapo hapa kabisa. Watachora na
kupaka rangi zao hapo mpaka wewe ndio utake watoke hapo, lasivyo unaweza
wasahau.” “Sasa wanachora nini?” “Jack aliwaagizia hivyo vitabu vyenye michoro kwenye
karatasi ya chini. Wanafuatisha kuchora kwenye karatasi ya wazi ya juu yake
kisha wanapaka rangi. Naona aliwafundisha jinsi yakufanya, wakaelewa ndio hao. Wanapenda
sana.” “Basi nikipaji chao.” Jack na Sabrina wakacheka tu. “Baadaye shem. Wewe weka
hekima zako zote kwa baba watoto wangu. Tunahitaji hekima zako.” “Kwa baraka
hizo, acha niwe huru.” Sabrina akacheka na kuondoka.
“Mama
ananiharibia familia, kaka.” Jack akaanza kulalamika mara baada ya Sabrina
kuondoka. “Wewe ndio unajukumu la kumlinda mkeo lakini si mama. Wewe unafikiri
wanapatana sana na Joy?” Jack kimya. “Ni hivyohivyo tu. Lakini ilinibidi
kusimama kiume haswa na kumuhakikishia mama kuwa Joy ni kila kitu changu, kwangu
na maisha yangu. Nikamchorea mstari ambao nilimuonyesha kila anapouvuka huo inakua
ni tatizo. Basi tunaendelea hivyohivyo. Siku nyingine kunakuwa shwari siku
nyingine ndio hivyo. Ila Joy naye ameshaweza kumzoea na kumchukulia. Huwezi kumkwepa
mama, Jackson. Ni mama yetu na ukiangalia katika yote ni kwa kuwa anakupenda
tu. Ila hajui ni jinsi gani yakufanya. Anakosea.”
“Hakika
nilipanga kumuacha kabisa.” “Najua. Na ndio maana nakwambia usifanye hivyo. Ila
kuwa makini na nini unamshirikisha tena, basi. Jua sasahivi yupo Sabrina,
huwezi kumshirikisha mama kila kitu. Na yeye muonyeshe hakuna usiri kati yako
na Sabrina. Atakujaribu tena na tena kwa hili na lile. Lakini akishaona
unamsimamo. Ataanza kuelewa mipaka yako na kuishi na wewe kutokana na mwanya utakao
mpa.” Jack akavuta pumzi kwa nguvu na kutulia.
“Mpigie
simu mkaribishe kesho.” “Kaka! Mama atafanya mke wangu aondoke!” “Mkaribishe na
Jacinta. Huwa anajua kumtuliza. Na mimi nitakuwepo karibu sana na Sabrina na
watoto. Na tukiwa bungeni, nitamwambia Jacinta asisogee mbali na Sabrina mpaka
mimi mwenyewe nitakaporudi au wewe utakapoungana nao tena.” “Daaah!” “Mpigie
simu.” Jack akatoa tena simu. “Lakini nilimkaribisha baba.” “Najua. Aliniambia na
unajua baba hawezi kuja bila mama. Mpigie simu mama.” “Ila Jena simtaki.” “Jackson!”
“Jena ni mkorofi kaka. Tutaishia kugombana bure hapa, tena hadharani.” “Wewe
utakuwa mbunge wa wapi unakwepa watu? Kiongozi wa namna gani ambaye huwezi
kutawala watu wa nyumbani kwako? Jena na ukorofi wake wote, ulishamsikia anamjibu
vibaya Joy?” “Si kwa kuwa anakuogopa wewe? Ni wewe peke yako ndio anakuogopa
pale nyumbani. Mimi haniheshimu.” “Nilikwambia nini juu ya heshima?” Jack
akakasirika na kusimama kwa kuvuta kiti kwa nguvu. Jeiline na Keiline wote
wakanyanyua vichwa wakimtizama baba yao kwa pamoja mpaka Junior akashangaa.
“Huo
ni ukweli na lazima ubadilike Jack. Acha kukimbiakimbia. Na rudi kukaa, unatia
wasiwasi watoto wako.” Jack akarudi kukaa watoto wake wakabaki wakimwangalia. “Tuone
mlivyochora.” Wote wakamkabidhi baba yao kwa pamoja. “Mmechora vizuri sana.” Jack
akawarudishia, wakaendelea kuchora na kupaka rangi. “Sasa hata wakikubali kuja,
watafikaje huku?” “Watakuja na Jacinta, usiwe na wasiwasi.” Kazi ya kupiga simu
ikaanza.
Akaanza
kwa Jacinta. “Mheshimiwa Msindai?” Jack
akacheka. “Hongera sana. Au niseme hongereni sana.” “Nashukuru
dada. Sasa ili hii furaha ikamilike, kesho kutwa wakati nikiapishwa lazima uwepo.”
“Mbona nilikuwa nakuja bila hata ukaribisho! Na nguo tayari ninayo.”
Jack akacheka sana kwa furaha. “Hapa nishakusanya timu
yangu yote sema dada mdogo ndio anatufanya tusiondoke leo.” “Claire huyo?”
Jack akaliza akicheka. “Huyohuyo! Anamipango mingi
kuliko baba yake waziri! Ndio tunamsubiria amalize leo jioni, kesho nambeba na
timu ya Joy nzima, tunatua jijini. Tupate nyama choma na kunywa usiku kuchwa,
asubuhi bungeni.” “Nashukuru dada yangu. Asante sana.” “Wala usijali.” “Acha
nimpigie simu na mama.” “Hiyo hekima. Hapo nakupongeza na ndio unatutangazia
upo tayari kwa majukumu mazito.” Jack akanyamaza. “Utakuwa sawa. Mimi mwenyewe nakuja. Kwa hiyo kesho na kesho
kutwa itaisha vizuri.” “Naamini hivyo.” Wakaagana.
Akampigia
simu mama yake. “Nimeteuliwa kuwa Mbunge wa viti
maalumu.” “Hongera sana.” Mama Msindai akajibu. “Kesho
kutwa naapishwa. Nilikuwa nakukaribisha.” “Nilijua hutaki nije!” “Ndio nimekupigia
mama!” “Kwani wewe huku kuapishwa ndio umejua leo?” “Mama Msindai!” “Inakua
kama unalazimishwa mimi niwepo! Kama unaona shida ya mimi kuwepo haina sababu.
Maana..” “Mama! Mama! Naomba unisamehe kuchelewa kukutaarifu. Naomba kesho uje,
na swala la usafiri dada Jacinta atashugulikia.” “Maana unaweza ona nitaharibu!”
“Nimeomba msamaha mama. Na naomba yaishe.” “Yanaisha yote au hili tu
lakuchelewa kunitaarifu mimi kama mtu baki wakati ni mama yako? Maana uliniitisha
kikao mimi mbele ya ndugu zako!” Jack akamwangalia kaka yake, Junior
kimya.
“Nia yangu ilikuwa nzuri lakini ukanitupia mimi lawama! Mimi sina
kipimo, na wewe huna kipimo chakumjua mtu. Sasa kwa nini mimi nisiongee moyo
wangu pale ninapopatwa nawasiwasi?” Jack
akaweka spika kaka yake asikie. “Mimi kama mama lazima
nikulinde kwa kila namna. Sasa kosa langu lipo wapi?” “Omba msamaha.” Junior
akanong’ona. “Kaka!” Jack akashangaa sana kwa kuumia. Junior akatingisha kichwa
akikubali akiweka msisitizo, Jack akatamani kulia. “Mimi
mke wangu sio mchawi. Brina ananipenda na ananiombea sana.” “Sasa hayo yakuwa
si mshirikina kwa hakika mimi ningeyajua wapi? Kama yalimpata Ngoi, kwa nini
mimi nisiwe na wasiwasi juu yako? Kitakachoshindikana kukupata wewe ni nini?” “Basi
mama, mimi naomba yaishe. Yaishe yote. Ila naomba muache Brina. Hivi nilivyo
mimi, napenda. Hata kama ananiloga, niachwe tu nilogwe.” “Sawa.” Akajibu
mama Msindai.
“Kwa hiyo unakuja?” Jack akamuuliza. “Sijui! Napatwa uzito maana ni kama watu wote wananiona mimi
sifanyi ilivyo wakati nia yangu ni nzuri.” Gafla mama Msindai akageuka
yeye ndio muhanga! Anaonewa! Ikabidi Jack ajishushe kumtuliza ila akisimamia
Sabrina ndio yeye, lazima hilo aelewe. Wakaongea hapo karibu nusu saa, mwishoe
akachangamka. “Nitakuletea tai na soksi.” “Nishanunua
tai. Tafadhali usianze mama!” “Muulize Junior. Kila akiapishwa lazima avae tai
niliyomletea mimi.” Akamtizama Junior, akamuona anacheka taratibu akiwa
ameinama anatingisha kichwa kwa masikitiko. “We Jack?” “Nipo
mama. Sasa kwa nini..” “Muulize hata Joy. Nilishamwambia na yeye akaelewa. Awamu
zote mumewe akiapishwa lazima avae tai nilizonunua mimi na soksi pia. Sasa wewe
unabisha nini?” “Sawa mama, lakini nilishapanga tai yangu.” “Tai gani hizo za
vichochoroni? Unataka kuniharibia utaratibu wangu! Hii tai nilishanunua muda
mrefu sana nikijua siku moja utakuja kuapishwa tu. Sasa unataka kunikatili bila
sababu?” “Sawa mama. Unakuja na tai pamoja na nini kingine?” “Mimi sina uhakika
sana na hiyo suti unayotaka kuivaa siku ukiapishwa.” Junior akaanza
kucheka.
“Kwa hiyo na suti pia unataka ulete wewe, yangu nisiivae?”
Jack akamuuliza. “Unaposimama pale kesho kutwa ujue
unawakilisha kina Msindai wote. Sasa unataka tuonekane sisi wote hovyo? Unavaa suti
ambazo hata hazijulikani zimeokotwa wapi! Mpaka unafanya watu wajute kukuchagua
bwana! Inakua…” “Sawa mama.” “Basi swala zima la mavazi ni juu yangu. Na umwambie
Junior mimi nataka nije nilale huko leo. Ili nijiridhishe kama nguo imekukaa
vizuri au la. Kama kunamarekebisho basi siku ya kesho nishugulikie ili kesho
kutwa utokee smati.” “Usiwe na wasiwasi. Yako isiponikaa
vizuri, ipo hii yangu.” “Mbona unafanya nijirudierudie? Nasema sina imani na
hiyo suti yako.” “Sawa mama Msindai. Nitamwambia kaka ahakikishe leo, unalala
Dodoma ili unijaribishe suti.” Junior akatingisha kichwa kwa masikitiko akicheka.
Wakaagana.
“Mama!”
“Ila nimemsikia amefurahi sana. Nashukuru kunitia moyo kumpigia. Aliniumiza sana.”
Wakaendelea kuzungumza wawili hao. Ila safari hii angalau kikaongezeka na
kicheko. Jena yeye akamtumia tu ujumbe wa kumkaribisha, hakutaka kuzungumza
naye alijua wataishia kugombana. ‘Nakuja sana. Wala
sipitwi.’ Akarudisha hayo majibu. Akamuonyesha kaka yake. “Huyu
usiwe na wasiwasi naye. Nitazungumza naye
hata kabla hajaondoka Dar. Nitamuonya kabisa ili akishindwa, basi asije huku.” “Naomba
nisaidie kaka. Brina ameshika mimba akiwa bado na mshono mbichi kabisa. Sitaki waanze
kumpandisha tena pressure.” “Usiwe na wasiwasi. Mimi na Jacinta tutajipanga.” Wakaendelea
kuzungumza.
Kwa Pendo.
S |
abrina
akaona ampigie simu Pendo. “Nimekuamsha dada yangu?” “Usijali.
Vipi maandalizi huko?” “Tumeshafika Dodoma. Tupo hotelini. Lakini dada, kuna
jambo nilikuwa nikisita kukwambia, lakini acha tu nikwambie. Sina nia ya
kukutisha ila kukufanya uwe makini na wewe uombe.” “Niambie tu. Ni nini?” “Nimeona
roho ya mauti ipo karibu na wewe pamoja na Willy. Nimekua nikiwaombea, lakini
hata Jack amenishauri ni lazima nikwambie mwenyewe.” “Sabrina!” “Naomba
usiogope dada. Mungu anapotuonyesha jambo si kwa kutaka kutuogopesha ila
kutenda kazi na sisi. Naomba uombe na wewe.” “Na nimepoa kweli! Sina maombi
yeyote sababu ya hekaheka ya kulea. Nimejisahau.” Pendo akakiri.
“Na hapo ndipo
shetani anapenda kupenyeza yake. Akishaona tumepokea majibu ya maombi fulani, tukabweteka,
basi anachokonoa kwingine. Yeye hasinzii wala kulala akijua muda wake wa hukumu
umefika. Basi kazi yake ni kuharibu ili watu waanguke na apate wafuasi wengi. Mimi
nakuombea dada, lakini naomba mwambie na Willy aombe pia.” “Nashukuru Sabrina. Ila
naomba usiache kuniombea. Nimekua mbali na Mungu, ila nakuahidi nitaomba.”
Wakazungumza kidogo na kuagana.
Jiji Kuu La Tz.
M |
ama Msindai
akatua jijini akionyesha alikuwa amejiandaa vilivyo. Junior alimchukulia hoteli
mbali na hapo alipokuwa Jack na familia yake. Jack na Junior wakaenda kumpokea
na kwenda naye hotelini. Sabrina alimwambia asiwe na wasiwasi yeye atakuwa tu
sawa hapo hotelini na watoto, yeye apate nao muda. Basi mazungumzo yakaanza. “Msindai
anakuja kesho na timu yake. Amefurahi huyo!” “Baba!?” Jack akauliza asiamini. “Huyohuyo
baba yako. Kafurahi sana na kataka nitangulie na suti yake kabisa.” Wakacheka. “Ni
hivyo tu anawagonjwa wake leo usiku, kama mnavyomjua hawezi kuwaacha, ila
angekuja na mimi.” Zikaendelea stori, pakaonekana pana amani tu wala hapakuongelewa
Sabrina wala wanae.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kesho yake Mzee Msindai, Jacinta, Joy,
Jena na watoto wote wa Junior wakatua jijini tayari kwa shuguli nzima ya
kuapishwa kwa Jack siku inayofuata. Hapo ikabidi jioni baada ya Junior kutoka
bungeni watu wote wakutane sasa kwa chakula cha jioni. Maana Sabrina alibaki
hotelini na watoto wake karibu siku nzima Jack alipokuwa hotelini na mama yake
wakijaribishana hizo nguo. Ila Junior alishazungumza na kila mmoja wao hapo
akiomba amani zaidi kwa Sabrina. Akawaambia mpaka hiyo shuguli iishe, basi
Sabrina na watoto wake wote nilazima wawepo ndipo Jack atatulia, lasivyo wataharibu
shuguli nzima.
Jack na Sabrina pamoja na watoto wao
wakawafuata walipokuwa wakikutania. Sabrina aliona ni kama wote wanamshangaa ujauzito
wake, lakini akaona kama walioonywa hakuna aliyemsemesha. Alisalimia kwa jumla
tu, wakakaa sehemu ilipoachwa wazi kwa ajili yake na watoto wao. “Mmependeza na
wanao!” Jacinta akawasifia. “Asante wifi yangu. Haya salimieni sasa!” Wakamwangalia
baba yao. “Kwani wameanza kuongea?” “Wanajua kusalimia sana tu. Ngoja Jack
awaambie naona yeye huwa wanamuelewa vizuri kuliko mimi.” “Au tuinamishe vichwa
watushike?” Babu yao akauliza. “Pina dada yao aliwafundisha kusalimia hivyo kwa
kushika vishwa, eti Jack akawakataza kusalimia kwa namna hiyo.” Wakacheka. “Sasa
wanasalimiaje?” “We Jack, waambie wasalimie bwana. Mbona wanajificha?” Jack
akawachungulia kule nyuma yake.” “Haya njooni huku mbele muangalie watu na
kuwasalia, hslsfu mkae.” Wakachungulia. “Bwana hawa watoto ni wazuri jamani!
Sabrina, hapa ulizaa.” Joy akasifia wote wakacheka.
“Mimi napenda nywele zao, anti. Wananywele
za kizungu.” Claire akafanya wazidi kucheka. “Lazima kusalimia na mseme asante.”
Mama yao akaweka msisitizo. Wakasalimia huku macho kwa baba yao. “Salamu za Singida
hizi. Ushamba tu sijui wakoje mwaya!” Sabrina akawaambia wanae, wakarudi nyuma
ya baba yao. “Mlitaka wanangu wafanyaje sasa? Mmetaka salamu, wamewasalimia. Bado
tu?” Jack akalalamika akiwaangalia binti zake wa kizungu. Sabrina aliwavalisha
vizuri na kweli walikuwa wamependeza. Wakaendelea kucheka wengine ila mama Msindai
na Jena kimya.
“Watakubali
kukaa na mimi hapa karibu na dad?” Claire akauliza. “Labda nihame nao hapo
karibu yenu. Lasivyo hawatakubali.” Jack akajibu. “Basi mama wewe na Clei
muhamie pale ili watoto waje hapa wakae karibu na mimi pamoja na dad.” Kila mtu
akaanza kucheka. Junior akawa akicheka huku akimtizama mkewe.
“Wala
sinyanyuki hapa. Mkitaka nyinyi ndio muhame, hee!” “Dad amechoka na kazi, mami.
Tusimsumbue.” Claire akamjibu mama yake taratibu akitaka yeye ndio aondoke,
kila mtu akazidi kucheka. “Basi wakati nyinyi mnajipanga bora mimi nikaanze
kucheza na watoto.” “Utalia Clei wewe!” Mama yake akaanza kumtisha. “Sasa yeye Claire
si hataki kuhama mpaka ahame na dad! Mimi nipo tayari kufuata watoto.” “Acha
kutaka kumliza mtoto bwana! Yeye ndio amewahi, mwache aende.” Kaka yao, CJ
akaingilia. “Clei yeye mchokozi.” “Usilie Claire.
Twende wote mimi nikae na wewe ucheze na watoto halafu ukichoka, dad
atakupakata.” CJ akaendelea kuzungumza naye taratibu Clei anacheka. “Usimwangalie,
niangalie mimi. Anataka uzidi kulia.” “Basi mimi
silii.” “Mbona machozi yana…” “Clei wewe utalia wewe mtoto wewe!” Clei
akanyanyuka haraka akahamia kwa babu yake.
“Muone!
Mwenzio anambembeleza asilie, wewe raha yako ni mpaka alie!” Baba yao mwenyewe
alikuwa akicheka taratibu. “Acha kushindana na mtoto. Njoo Claire.” CJ
akajaribu kumtuliza. “Na mimi nataka tucheze wote Claire.” Clei akaingilia tena,
makusudi tu. “Sitaki kucheza na wewe Clei.” “Junior
mkanye Clei, atalia huyu mtoto jamani!” “Sasa mimi si nataka kucheza naye tu! Nimekosea
wapi?” “Mimi sitaki kucheza na Clei, nataka kwenda
na CJ nikacheze na watoto.” “Yaani mpaka hilo bunge lenu mmalize hapo
kina Msindai, na watoto wenyewe hawawataki tena.” Jacinta akaingilia nakufanya
mpaka Joy acheke wakawaangalia. Wale mapacha walikuwa wamesimama pembeni ya
baba yao wamemshika kila mmoja mkono wake kama asiwakimbie. Kimya, wametulia wanawaangalia
vile Claire anavyolia.
“Vipi yeye mzee mwenzangu?” Mzee Msindai akauliza
akimwangalia Brayan pale kwenye kigari chake alipokuwa amelala pembeni ya mama
yake. “Kaka yupo tu. Bado mtulivu hivyohivyo.” “Bwana mtoto yule wa kiume wa
Pendo anajua kulia mpaka Willy jasho linamtoka.” Wakaanza kucheka kila
wakikumbuka mapacha wa Pendo. “Akianza kulia kaka mtu na dada yake anapokea
basi hapo Pendo utasikia, ‘mpaka mimi mwenyewe machozi yananitoka!’ Pendo huyo.”
Joy akaigiliza sauti ya Pendo nakufanya wazidi kucheka. “Pendo analia, na wanae
pia wanalia?” “Wewe si unamjua Pendo asivyopenda matatizo? Basi mama yake amekua
kama amehamia pale. Anasema akiondoka tu, simu zinamfuata juu ya wale watoto.” “Na
mimi mama K, aliniambia. Anakaribia kumuhamishia mumewe pale. Hana analofanya
zaidi ya kulea hao wajukuu.” Wakazidi kucheka.
Mzee
Msindai akasimama kwenda kumchukua Brayan na Cleiton naye akamshika shati. “Utamuangusha
babu yako bwana!” Baba yake akamuwahi. “Mama anataka kunipiga kwa kuwa kaka
mzuri kwa Cl…” “Usinitaje jina langu.” “Na ukimjibu tu unalia.” Mama yake
akamtisha tena. Cleiton akajiziba mdomo na kiganja kimoja mkono mwingine
amemshikilia babu yake. “Basi mtamuangusha huyo mtoto.” Mama Msindai
akaingilia. “Wewe ukitulia hutachapwa.” “Wananionea bure babu! Sijakosa.” “Basi
tulia hapa kwenye kiti changu na usinyanyuke. Hakuna atakayekufuata kwenye kiti
changu.” “Na kila mtu amesikia. Babu amesema hata mtu asinirushie kiatu.” Walicheka
mpaka mama yake akatokwa machozi. Mzee Msindai akaenda kumchukua Brayan, Junior
akamuhamishia kiti pembeni ya Cleiton. Baba yao akakaa akiwa amembeba Brayan.
“Mtulivu
huyo!” Jacinta akamsifia Brayan. “Halafu bado ameshikilia sura ya baba.” Junior
akaongeza. “Ndio inamaana amefanana na Jack au wewe Junior.” “Mimi nahisi
amepitiliza mpaka amebakia kwa baba, jamani! Yaani utafikiri yeye ndio mtoto wa
mzee Msindai!” Mzee Msindai akazidi kufurahi. “Basi hapo mmemuweza Msindai. Anaona
sifa!” Mama Msindai akafanya wacheke wakimuangalia mzee Msindai. Kweli alionekana
anampenda huyo mjukuu wake. Alikuwa amemshika vizuri. Zikaendelea stori wakaletewa
vyakula kila mtu alichopenda, kukawa na kula, kunywa na kusaza mpaka waliporidhika
watoto wamechoka.
Sabrina
akaaga kwamba anakwenda kulaza watoto. Jacinta, Joy na Junior wao walisema
wanabaki kunywa. “Mbaki na baba watoto wangu ila mumrudishe salama.” “Unauhakika
Sabrina?” Jack akamuuliza kama kweli abaki pale. “Kabisa. Sasa unataka na wewe
uende ukalale sasahivi kama Brayan?” Angalau wakacheka wakaamua watoto wote waondoke
na Sabrina akapumzike. Junior akatafuta dereva kuwarudisha watoto wake
hotelini, CJ kaka yao awaangalie kwa maelezo kwa chochote kuwa kikitokea
awapigie wazazi wao simu, hata hivyo hawakuwa mbali na hoteli waliyoshukia hao
kina Msindai wote. Kisha dereva alitakiwa kumpeleka Sabrina na wanae kwenye
hoteli waliyofikia wao. Wakaondoka na kuwaacha hapo, Mzee Msindai na mkewe,
Junior na mkewe, Jacinta, Jena pamoja na Jack. Ndio kukawa kumekuchwa. Wakaaanza
kikao kwa upya.
Penye Amani Na Utulivu, Na
Uharibifu Hunyemelea.
W |
akati Jack anaingia hapo chumbani kwao hotelini
akamkuta Sabrina akizungumza na Pendo. Akaingiwa na wasiwasi kwa sababu kwa
muda ule, usiku wa saa saba alitegemea Sabrina awe alishalala. Akajua haitakuwa
simu nzuri. Jack akasogea kusikiliza, Sabrina akaweka kwenye spika ili na yeye
asikie. Jack akamsikia Pendo akilia. “Najuta
Sabrina wewe! Najuta sana. Natamani muda uleule uliponipigia ningeomba. Pale ulivyokata
tu simu na mimi nikaingiliwa na vilio vya watoto. Nimekuja kukumbuka
ulichoniambia sasahivi Willy alivyopigiwa simu na kutaarifiwa kifo cha kaka yake.
Ameondoka hapa mbiombio.” “Poleni dada. Wanasema
ni nini?” Sabrina akauliza.
“Gafla tu,
hata hakuwa mgonjwa! Yaani ameanguka tu akiwa anatoka sebuleni usiku huu, anakwenda
kulala chumbani kwake. Mkewe anasema alirudi akaishia hapo sebuleni wakawa
wakizungumza mpaka wakaamua kwenda kulala. Yaani mkewe anasema amedondoka
akimuona hivi! Imekuwa kama aliyesukumwa wakati anaelekea chumbani. Amedondoka na
kufariki hapohapo.”
“Poleni dada.” Wakaagana lakini Pendo akisikika
mwenye majuto.
“Ni nani!?” “Kaka yake mkubwa Willy.” “Ulipomwambia aombe
aliomba?” “Kama ulivyomsikia hapa. Anasema ndio anakumbuka sasahivi baada ya
hizo taarifa.” “Inamaana alipuuza!” “Anasema alipitiwa. Nilipomaliza tu
kuzungumza naye ile jana, eti watoto wakaanza kulia, akasahau.” Jack akasikitika
sana. “Alikuwa na nguvu zake kabisa!” “Namkumbuka yule kaka. Nilimuona siku ya
msiba wa mama yao. Alikuwepo pale. Tena amefanana kweli na mzee Ngoi mwenyewe.”
Ikawa habari iliyowahuzunisha sana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Katikati Ya Mema Na Mabaya Hujihudhurisha.
Sabrina Aliona Roho Ya
Mauti, Akawataarifu Waombe. Kukawa Na Kujisahau Kwingi Wakiendelea Kufurahia
Majibu Ya Muujiza Wao.
Sasa Je, Hiyo Roho Ya
Mauti Iliyofunguliwa, Inakwenda Umbali Gani?
Nani Anaangamia? Nani
Anabaki?
Mwisho wa Ubaya ni Nini?
Familia Ya Msindai Nayo Ipo Jiji
Kuu La Tanzania Kushuhudia Kuapishwa Kwa Jack. Nini Kitaendelea kwenye siasa za
Jack?
Usikose Sehemu Ya 59.
0 Comments:
Post a Comment