Watoto wote walikuwa
wamelala wakati wanaingia hapo nyumbani kwao. Wakasaidiana kuwaingiza ndani na
kuwalaza. Mizigo yao ilibahatika kuondoka siku iliyopita na basi la mwisho
kabisa kutoka Dar. Jack akajua itakuwa imeshafika, akachukua gari kuifuata,
Sabrina alipojiridhisha amebaki peke yake, akapiga magoti hapo chumbani, na
kuanza kulia mbele ya Mungu. Alijawa hofu juu ya ndoa yake. Jack alikuwa mtu wa
kusamehe kwa haraka na kumtaka kimapenzi wakati wote. Lakini walilala hotelini
hata hakugusia kabisa swala la mapenzi. Alikuwa amepoa kupita kawaida yake. Akakumbuka
mara zote alizomuomba msamaha tokea wapo Dar, hakusema kama amesamehe.
Sabrina anayependa kumpa
Yesu mtatizo yake, akamwambia mpaka hapo ameharibu, hajui chakufanya, anaomba
msamaha na msaada. Akajifikisha maeneo yake ambayo hapo huwa hakosei. Magotini.
Akatubu kwa machozi na kuomba rehema, Mungu asimchoke, amkumbuke tena, amrehemu
na kumrudisha moyoni kwa Jack. Akaomba mpaka akakumbuka anajukumu hapo kama
mama na mke, na hana msaada. Akanyanyuka na kuanza majukumu ya kinyumbani,
zaidi kupika.
Jack alipitia na sokoni.
Kwa hiyo akachelewa kidogo kurudi. Akamkuta Sabrina ameunganisha masalia ya
kwenye friji na stoo, anapika. “Nisadie nini?” Jack akauliza baada ya kuingiza
kila kitu ndani na kupanga. “Labda kuniangalizia Brayan. Anaweza akawa ameamka
na kutulia tu.” “Ndio mpole hivyo?” “Wewe utamuona. Kama haupo makini, ni rahisi
kumsahau.” Jack akaondoka. Ila chakushangaza hakurudi tena jikoni kama Sabrina
alivyozoea. Alivyotoka kumuangalia mtoto akaenda kukaa sebuleni.
Sabrina wakati akipanga vyakula mezani,
akamuona amekaa sebuleni amejiinamia wala hajawasha tv. Akamuacha akijua watoto
wanakaribia kuamka. Mazungumzo yeyote watakayoanzisha, hawatamaliza kabla
yakuingiliwa na watoto. Na kweli
haikuchukua muda mrefu watoto wote wakaamka. Wakasaidiana kimya kimya mpaka
watoto walipoenda kulala, na yeye Jack akajiwahi kuoga na kujiweka kitandani.
Akamkuta kitandani amejilaza hata simu amezima. “Nimezungumza na Pina,
nimemuomba arudi atusaidie kazi.” “Umefanya vizuri. Tutahitaji msaada.” Akajibu
hivyo, Sabrina akaona bado mazungumzo kati yao yamekua mazito.
Akajiweka kitandani na
yeye baada ya kuoga bila kuzima taa. “Jack, umeshalala?” “Nipo. Nafikiria
inamaana nisingekufuata inamaana mpaka leo ningekuwa hapa peke yangu! Na
nikiangalia mazingira niliyoyakuta pale, ni kama nimewaingilia Brina. Maisha
yenu yalikuwa yakiendelea kama kawaida, tena vizuri kabisa bila mimi. Nahisi
ndio maana mama yako amenichukia sana. Ananiona mimi mvurugaji.” Jack akazungumza
akilalamika.
“Najua nimekosa na
nimekuumiza, Jack. Lakini naomba utulie na ujaribu kufikiria tu. Weka hasira
pembeni na ufikirie. Fikiria tu tafadhali.” Jack akamwangalia. “Hivi kweli wewe
ulifikiri nilikutafuta kweli ili unipe nguo za Brayan, kweli?” Jack akatulia
kidogo bila ya kujibu. Baada ya muda akamuona anakunja uso kama anayepingana na
jibu lake. Sabrina kimya akimtizama pale alipojilaza kitandani kwa huzuni. Kisha
akajibu. “Lakini ndivyo ulivyoniambia Brina!” “Kwa hiyo wewe unavyofikiria kule
Dar hakuna nguo za watoto wa kiume mpaka Singida?” Jack akanyamaza.
“Unakumbuka wewe
uliondoka na kunitelekeza na watoto wote ukaendelea na mipango yenu na mama
yako?” “Ukisema hivyo inasikika vibaya!” “Ndivyo ilivyokuwa, Jack. Sasa
ningejuaje kama umeamua kuturudia mimi na makinda yangu?” “Wewe Sabrina!
Si ilikuwa ni...” “Mimi ningejuaje mipango yako na mama yako? Kama ni moja kwa
moja au utaturidia? Sikujua safari hii mama yako amefanikiwa lipi na kwa undani
gani kwako! Kumbuka maneno machafu aliyoyasema juu yangu, halafu nikaja kukuona
upo naye. Ulikuja kwa Pendo, nikakuona mara moja tu, tena hukuzungumzia chochote
kwenye swala la Ubunge. Hata hukutaka kujieleza lolote juu ya hilo. Sikujua
umeamini nini na utaamua nini juu yangu na wanangu! Halafu ukweli nilikuwa
nikiumwa na niliumia Jack. Nikaona nije huku, nikuache tu mpaka umalize, uje ututoe
mimi na wanangu kwenye hii nyumba. Sikupanga hata kukaa kwenye Villa, na Mungu
ni shahidi.” Sabrina akaendelea.
“Sasa siku ile ya harusi
nilipoondoka pale, hata hukunifuata nyuma, nikajua moja kwa moja umekubaliana
na mama yako mimi ni mzigo. Umekusudia kuachana na mimi.” “Nilitaka kukufuata
lakini Pendo akanirudisha na kutaka kuniambia ukweli.” “Sasa mimi sikujua yote
hayo. Nilijua moja kwa moja uliamua kuachana na mimi. Na naomba ukumbuke
historia yangu, Jack. Wanaume wote huwa napambana kuwasaidia kwenye ndoto zao,
wakishafanikiwa huwa wananitupa. Mimi moja kwa moja nikajua na wewe utakuwa
hivyohivyo. Nilitoka pale nikaenda sehemu kuomba. Nikiwa sijui tena chakufanya,
nikijua umekusudia kuachana na mimi. Nilikaa pale kwa muda mrefu sana,
nikimuomba Mungu lakini ukweli nilikuwa nimepoteza dira. Baada ya kujihisi
nimechafuka na maumivu ya tumbo kunizidia, nikaamua kurudi kwa dada Sabina,
maana nilipanga tulale pale na watoto pamoja na mama, kesho yake nije huku.”
“Nilifika pale, sikuwakuta.
Nikakaa nje tu mpaka wakarudi. Nilipowashika kina Jeiline nikapata harufu ya
Tino. Nikajua walikuwa na Tino maana nilishapata habari za kutaka kujirudi
kwake, lakini mimi nilimkatalia. Sasa muda ule nikijua umeamua kuachana na
mimi, halafu nilikuwa mgonjwa, sina pakwenda.” “Na huku?” “Sasa huku
ningerudije wakati tukio la harusi kwa Pendo kutonifuata likawa
limeshanithibitishia unaniacha? Watoto watatu, sikuwa na pakuwaweka na wewe
hukuwa hata ukikosea kwa ujumbe angalau kutujulia hali! Nikajua umeingiziwa
maneno, safari hii yamekuingia.” “Nahisi hapo ndipo nilipokosea.” Jack akakiri.
“Basi nikajiambia ni bora
nimtumie Tino aniweke mahali wakati nikijipanga upya. Mungu nishahidi
Jack, sikuwa hata na mpango wa kurudiana na Tino, na wala hakuna lililokuwa
likiendelea kwa muda wote tuliokuwa pale. Kwanza ananiogopa mno. Hapakuwa na jingine
isipokuwa kuomba kuona watoto tena wakati mwingine hata alikuwa akimtuma mama
amuombee kwa jinsi anavyoniogopa. Yaani jana, kwa mara ya kwanza na wewe ukiwa
pale kwenye Villa ndio angalau nimeweza kukaa naye chini kuzungumza naye. Tangu
anitelekeze yule kiumbe, sijawahi kupata naye muda wakuzungumza naye. Moyo
wangu ulisita kabisa kuwa naye karibu kwa muda mrefu. Alichokuwa akifanya ni
akifika pale, akiniomba kitu nikiwa chumbani, nikimruhusu anatoka. Au akinikuta
nina maumivu alikuwa akiogopa hata kunisogelea, anamtuma mama.” Jack akawa
anasikiliza tu.
“Tino kama yeye kwa
hakika nilikuwa nikimtumia na yeye nilimwambia kabisa kuwa namtumia
kujipumzisha. Haikuwa siri hata wazazi niliwaambia ananilipa kwa kumtumikia
alipokuwa yeye mgonjwa, hii ni safari yangu na mimi anilipie pale nikijiuguza.”
“Lakini alihusika na wanangu, Brina. Mpaka kuwalisha?” “Nisikilize Jack, na naomba
uamini. Hiyo picha iliyokuingia kichwani haikuwa hivyo. Hapakuwa na maisha ya
Tino na hao mapacha wako. Haikuwepo kabisa. Unaposikia aliwalisha, sio
kwamba ilikuwa ni mpango ulikuwa ikifanywa ili awalishe au asaidie kazi zao.
Kwanza Tino sio kama wewe, hayawezi. Anachopenda ni zile show
pale. Atayarishiwe watoto ndio atoke nao. Ni mtu wakutumikiwa. Nahisi pengine
atakuwa alimkuta mama akiwalisha, akasaidia kwa vijiko vichache tu. Hapakuwa na
maisha yaliyokuwa yakiendelea kama familia pale.”
“Ninachojuta na nafikiri
ni kosa nililifanya kwa kuwa nafikiri nimekosa imani na Tino kabisa.” “Kosa
gani?” Jack akauliza. “Najuta kule kumtuma mama kila mahali awe na Tino
anapokuwa na watoto. Na nafikiri huko ndiko alikomuingia mama moyoni. Maana nilikuwa
sina amani ya kumuacha peke yake na watoto wetu. Kwa hiyo nikawa nikimuomba
mama atoke nao. Halafu sio mara nyingi. Alikuja mwanzoni aliponisaidia hoteli,
nilipohamia kwenye Villa na yeye akaondoka. Nilimsikia akimwambia mama, tena
mimi nilikuwa chumbani, kuwa anasafari ya kwenda kwenye kuuza picha zake
mnadani. Hata sikujua ni nchi gani, ila aliondoka. Amerudi nafikiri hata siku
saba hajamaliza. Ameomba wale watoto kama mara tatu tu. Na jana tena lakini ndio
wanao wakamgomea, ndio maana akawarudisha.”
“Kwa hakika nilihitaji
kupumzika Jack, kwa kuwa sikuwa nikijua hatima yetu japo nilihisi kwa asilimia
79 utakuwa umeniacha. Sasa nafanyaje na watoto watatu ambao hata bibi yake huyu
Brayan amemsusa? Ndio sikuwa najibu, nikajiambia nikapumzike kidogo, nijiuguze,
nipone ndipo nijue chakufanya. Wapi pakuanzia, sikuwa nikijua ila
nilishakusudia Tino hatarudi kuwa mbadala hata iweje. Japokuwa
anajitilisha huruma, lakini ni mtu mwenye roho mbaya sana. Ni chui mwenye ngozi
ya kondoo. Nilimuona wakati tukiwa Moshi. Na ni mtu anayeweza kubadilika vibaya
sana pindi anapoamua jambo lake. Hata kama usingenirudia Jack, Tino asingekuwa
mbadala.”
“Anyway, katika
hizo asilimia chache zilizokuwa zimebakia kwako ndio nikajiambia nikujaribishie
swala la nguo kwanza nione msimamo wako.” “Sabrina!” “Nishakataliwa sana Jack.
Sikuwa tayari kwa wakati huu kukataliwa tena. Nilijiambia nikiona majibu yako
hayaeleweki, basi natulia Dar na wanangu, nianze tena maisha mengine.” “Mimi na
wewe mpaka kifo Brina. Na wewe nilikwambia.” “Hayo maneno yanasikika vizuri
sana siku ya harusi, lakini kuja kuyaishi ndio mambo kama haya yaliyotupata
mimi na wewe. Wakati mwingine ni rahisi kuyatilia shaka.” “Mimi nitayashikilia
mpaka kifo.” Sabrina akamwangalia nakuendelea.
“Swala la kukublock
kwenye simu. Ni kosa. Lakini Jack, ukitulia na kufikiria, sijakublock.”
“Unawezaje kusema hivyo?!” “Najua usingependa kusikia hili, lakini na kwako
nilifanya kama kwa Tino. Simu yangu ilikuwa hewani tokea namzaa Brayan,
naruhusiwa na kutoka hospitalini kwenda kwa Pendo, mpaka siku ya harusi ya
Pendo, natoka pale nakuhamia kwenye hoteli. Haikuwahi kutokuwa hewani. Lakini
Jack, ni mara ngapi hata ulinitumia ujumbe kunijulia hali mimi na watoto?” Jack
akababaika sana mwishoe akakumbuka.
“Lakini nilikuja siku ile
pale kwa Pendo, mpaka nikakuomba nichukue watoto niende nao! Ulikataa lakini nilikuja
kuelewa baadaye ni kwa nini ulikataa. Ila siku ile unanikatalia watoto sikuwa
nikijua ni kwa nini. Na mimi nikaendelea
kukasirika na kushindwa kujua hata nikikutafuta nakwambia nini?” “Sasa
umekubaliana na mimi sio kwamba nilikufungia mawasiliano ila hapakuwa na
mawasiliano kati yetu kutokea mwanzo? Nilichofanya ni kupumzisha tu simu za
watu ambao nao niliona nipumzike, zaidi wa huku Singida. Sikujua nawaambia nini
nikiwa sijui hatima yetu! Sikutaka niongee jambo likaja kukuharibia, ndio maana
nikaona nitulie tu. Hata kama utaniacha, basi wewe nitakayekuacha huku ubakiwe
na hekima ya kuzungumza juu yangu na watoto.” “Nakushukuru kwa hilo, ila nahisi
nilifeli tokea mwanzo kwenye swala la mawasiliano na wewe, Brina.” “Ni kweli.
Na mimi najutia maana hata dada Pendo alinisihi sana nikwambie. Nikidhani
nitakuchanganya, kumbe naharibu zaidi. Naomba unisamehe Jack, mpenzi wangu.
Mimi nakupenda sana na nimekuchagua wewe. Nisingekutafuta kama sina mpango wa
kurudi huku. Na huo ndio ukweli.” Akamuona ameridhika.
“Naomba na mimi unisamehe
Brina. Nilikukosea. Sikupaswa kukufanyia nilichokufanyia. Ila ujue sikuwa na
mpango wa kukuacha hata kama ningefanikiwa huo Ubunge wa EALA. Na naomba
uniamini japo najua unaweza kusema naongea hivi kwa kuwa nimekosa.” “Kwangu
yameisha. Na wewe?” “Yameisha. Ila naona kuanzia sasa, tubadilike jinsi
tunavyoishi na watu, turudi kama zamani. Mambo yetu ni sisi tu. Sio kama sasa
hivi. Tumejianika vibaya sana. Kila mahali tunaonekana hovyo! Nimejichukia
sana.” Sabrina akatoka hapo kitandani na kuzima taa akijua wameshapatana.
“Sasa mimi nilijua
tunapata penzi la upatanisho! Si unajua jinsi inavyokuwa nzuri? Mkigombana
halafu mnamalizia kwa…” “Unakumbuka chochote tulichoambiwa na daktari juu ya
mapenzi baada ya kuzaa kwa upasuaji?” “Yale mambo ya baada ya majuma 6 ujue ni
kwa wale wanaume walevi na wale waliorafu. Kuhofia kuumiza wake zao. Mimi
mstaarabu Brina.” Akajua akili zimeshamrudia. Jack wa zamani amerudi.
Yashaisha. Akamshukuru Mungu kwa moyo wake huo wakumpenda na kutaka mambo
yaishe waendelee.
“Acha kunishika Jack
bwana!” “Kwani wewe huna hamu na mimi?” “Ninayo ila sasa ujue mshono wa ndani
haujapona. Japo nje inaweza kuonekana kama nimepona.” “Acha niwashe taa basi
niangalie hata huo mshono.” “Iwe tu kuangalia Jack. Usiende mbali. Sijajikinga
na chochote kile. Ukianza tu mambo yako hapa nashika mimba usiku huu huu.
Naomba kuwa mvumilivu.” “Mimi siwezi kuvumilia.” “Jack!” “Kweli tena. Yaani
mara ya mwisho ni vile ulivyoniaga hapa siku unakwenda Dar, napo havikuwa vya
muda mrefu ulisema ushachelewa.” “Lakini usiku wake si tuli..” “Acha kukumbushia
mambo ya zamani, Brina! Mimi hali mbaya. Nitulize hata kidogo tu.” Jack
akawasha taa na kurudi kitandani.
“Hapana Jack. Ushaanza
kunishawishi, na mimi najiona kama sina nguvu nyingi za kukukatalia. Bora hata
nisikuonyeshe.” Jack akacheka sana. “Tena leo ningekupa yale mambo yako yote
unayapenda mpaka unaniita jina langu.” Sabrina akacheka, nakucheka sana.
“Yote?” “Hakika nisingekubakisha. Kwanza ningekupa kwa pole ya kujifungua na
kujiuguza mwenyewe. Halafu kukushukuru kusimama na mimi japo nimeshindwa mambo
ya ubunge.” “Hujashindwa bwana.” “Sawa Brina wangu. Lakini ujue usiku wa leo ungepoozwa
vilivyo.” Jack akajiweka kitandani na kupiga magoti mbele ya alipokuwa amekaa Sabrina.
Akaanza kumbusu. “Ningekushukuru kwa kurudi na mimi huku, kunichagua na kuni…”
“Huko huo mkono unapokwenda, utulie hukohuko usitoke.” Jack akaanza kucheka.
“Vipi yale majuma 6?”
“Huyu daktari asinitanie kabisa. Wewe endelea kunishukuru. Ila na wewe sio fujo
sasa mpaka usiku wa leo tuhamie hospitalini!” “Mie mstaarabu. Taratibuuu…”
yakaanza mapenzi usiku huo. Jack na mkewe ambaye hana hata kitanzi. Akajiachia
wakati mwanae hata hajafikisha siku 30. Lakini kweli Jack akawa mstaarabu
haswa, alihakikisha hamuumizi. Baada ya hapo stori zikaanza sasa. Jack akimpa
kinachoendelea hapo.
“Sasa hakuna kupaniki.
Tutembeze siku tatu za mfungo.” “Si unanyonyesha wewe?” “Usijali. Mwanao
atapata chakula.” “Na wewe?” “Nitakuwa nikinywa chai tu. Siku tatu mpaka
tumsikie Mungu akitupa dira.” “Nakushukuru Brina. Asante mama.” “Tulale, kesho
uende kazini kama kawaida.” “Nilikuwa nikifikiria nichukue likizo nikusaidie
kazi.” “Usijali. Pina atakuja kesho kutwa kutusaidia. Tuendelee na maisha yetu
kama kawaida.” Wakazungumza na kupanga mengi, wakalala.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jack akiwa anajua
amebakiwa na Sabrina tu, hakuna tena cha mama, akaongeza mapenzi kwa mkewe.
Sabrina naye akijua anasubiriwa viharibike kwa Jack achekwe kwao, akaongeza
umakini kwa Jack. Wakashikana wawili hao, ule ukaribu wake na Pendo ukawa
kidogo umepungua. Pendo amempata Willy wake, akawa na muda mwingi na mumewe si
Sabrina tena. Sabrina naye alipoona Jack amepunguza ukaribu na kina Willy,
ikawa shida kupiga simu kwa Pendo zaidi Jack akiwepo. Akahamishia mtindo wa
kuomba kwa Jack. Yale mazoea ya kupiga simu na kuomba mara kwa mara na Pendo
ikawa ni Jack sasa. Mara waombee watoto, mara mambo ya chama, wakati mwingine
biashara zao. Ikawa wao wawili zaidi, Pendo yupo likizo na mambo ya Mungu,
anafurahia majibu ya maombi yake. Analea ndoa na mimba.
Sabrina hakuharakisha
kutoka ndani mpaka siku 40 za tokea ajifungue zilipoisha ndipo akatoka. Akaanza
taratibu kwenye mambo ya chama ila akakuta ukinzani mkubwa sana. Uzuri wanawake
wa pale hawakuwa wakipikika chungu kimoja. Kwa hiyo wakati akijaribu kujirudi,
akagundua wenyewe kwa wenyewe walishagombana, hawasemeshani, hawawezi kufanya tena
kazi pamoja. Mashitaka yakaanza kwa Sabrina. Hilo nalo akaona ni muujiza.
Hapakuwa na jinsi ya kutapanya pesa kwa sababu bado Jack alikuwa lazima aweke
saini ili kutoa pesa. Kwa hiyo hata huyo mpinzani alipokuwa akiwachanganya,
hawakuweza kuiba pesa.
Sabrina akarudisha nguvu kwenye mambo ya chama
haswa, akifanya kwa juhudi huku akikataa majungu. Hakuwahi kutaka kumsema huyo
mpinzani mbele ya hao watu akijua jinsi wanavyopenda kusambaza maneno. Akawa na
kazi ya kuwasikiliza na kujitahidi kuwarudisha kazini bila mafanikio makubwa
sana kwani haikuwa rahisi kama mwanzo. Kulikuwa na mgawanyiko mkubwa sana. Huyo
mpinzi alishafanikiwa kuwaingia akilini na kuifanya kazi yao kuwa ngumu zaidi
kuliko mwanzoni walipokuwa hawana upinzani wa ndani. Kila siku wakawa wakikutana
na jambo zito na gumu huko chamani. Lakini Sabrina hakuwa akikata tamaa mpaka
akawa anamshangaza sana Jack.
“Mama unapambana! Kila siku najiambia pengine safari
hili litamkatisha tamaa Brina wangu ataacha kabisa mambo ya chama kwa
sababu mimi mwenyewe nilikuvunja moyo na mambo ya mama kutaka kushinda, nikajua
huu ugumu tunaokutana nao sasahivi, utaona ni mimi na mama yangu ndio
tulikufikisha hapa, utaamua kuacha lakini nakuona kila siku ukikutana na jambo
unatafuta njia, huachi!” “Kwanza naomba uelewe kitu kimoja Jack. Sishindani na
mtu yeyote, zaidi mama yako. Kokote utakapofanikiwa kutimiza ndoto zako, sina
shida ilimradi ufanikiwe wewe. Mimi nakujua na nimetambua kitu Mungu ameweka
ndani yako ndio nafanya kazi na Mungu kuhakikisha unafanikiwa kufika pake
alipokusudia. Siwekezi nguvu ili ufanikiwe kupitia huku iwe eti ni mimi! Hapana
Jack. Mimi sina huo uwezo wa kukufanikisha ila Mungu wako mwenyewe aliyekupa
kicho kipaji.” “Basi mimi mpewa kipaji naona nishachoka Brina. Hakika nimekinahiwa.
Hila na vijambo haviishi! Kila siku kuna hili! Najiambia hivi ni
kwa nini nahangaika hivi! Sioni sababu.”
“Mimi mwenyewe nilifika
hapo. Lakini kuna mambo mawili Jack. Kwanza, tunalipa garama ya makosa yetu
wenyewe. Isingekuwa siri zako na mama yako, tusingekuwa hapa leo.” “Nimekuahidi
hamna tena siri. Kwanza sasa hivi nimetulia na wewe tu, hata sizungumzi na kina
Msindai labda baba tu tena mpaka apige mwenyewe.” Sabrina akashangaa kidogo,
lakini akaona aendelee na lake.
“Ninachotaka kukwambia, tunalipa
garama. Tulifungua mlango sisi wenyewe, huyu mpinzani wako akaingia. Kwa wewe
kuweka usiri wako, na mimi kufunga mawasiliano hata na viongozi tulioacha huku.
Ikawa ni kama tumewatelekeza. Tukamwacha huyu mpinzi akawa kiongozi wao, sisi
tuko likizo. Shetani haitaji siku nyingi kuharibu, kama kujenga. Ameingia na
kufanya uharibifu wake kwa muda mfupi sana wakati sisi wenyewe tukiwa tumetengana.
Mungu anaamuru baraka kwenye umoja. Imeandika hata kwenye Zaburi 133. Ipo baraka katika umoja wetu mimi na wewe.
Mungu alipoona mwanzoni ule umoja wetu, na juhudi zetu mimi na wewe, akaweka
baraka zake. Tulipotengana tu, na shetani naye akaingia.” “Sirudii tena.” Jack
akaongeza.
“Basi lazima kumuonyesha
Mungu tulikosa na tumekusudia kutorudia tena.” Sabrina akaendelea. “Kwa hakika
tumesamehewa. Lakini tumwambie Mungu kwa maneno na vitendo kuwa tunastahili na
tunaweza nafasi ya pili kama ataturudishia tena. Sisi hatuna kimbilio jingine
kama wengine, isipokuwa Mungu. Njia yetu ni nyembamba na imesonga. Kiongozi wetu
ni Yesu. Lazima tubakie hapo na tukubali kufundishika. Tunyenyekee hapahapa,
tufundishike mpaka ajue na kuona kweli tumetia adabu. Na tunastahili kwa
makubwa. Hapa hatutatoka kwa maombi tu
ni mpaka kumuhakikisha Mungu akitukabidhi kitu kikubwa sana, basi tunauwezo wa
kutenda naye kazi. Na hatutakimbia tena. Ukikimbia tu, atampa mtu mwingine bila
shida.” “Basi natulia mama.”
Na kweli wakatulia
wakaendelea kutumika kwa shida hivyohivyo wakiambiana waliyataka wenyewe. Wanavuna
walichopanda. Ukaribu wao ukaongezeka. Hawakumsikia mama Msindai, mama Sabina
na watu wote wa nyumbani kwa kina Sabrina, wala Tino mwenyewe. Msichana wao wa
kazi, Pina, naye alirudi na kuwa msaada mkubwa sana kwa Sabrina, akimsaidia
swala la watoto wakati yeye Sabrina akizunguka kwenye biashara zao pamoja na
mambo ya chama bila kukata tamaa huku akimuomba Mungu na kumshangaza zaidi Jack.
Maombi ya kufunga na kuomba kati yao likawa jambo la kawaida mpaka Jack akaanza
kuelewa mambo ya Mungu kwa ukaribu. Japokuwa hapakuwa na mabadiliko makubwa
huko chamani, mambo ni kama yaliendelea
kuwa magumu tu, lakini jinsi Sabrina alivyokuwa akizungumza naye, Jack mwenyewe
akabakia akifanya kazi na Sabrina tu na kumuunga mkono japo hapakuwa na tumaini
tena. Ni kama Jack alishaona mwisho wa kushindwa mwanzoni ila hakumwambia
Sabrina ili asimkatishe tamaa.
Ugumu wa maisha haukusikika kati yao kwa
juhudi alizoongeza Sabrina akitambua anao watoto wawili wa ziada, hakutaka
kumlemea Jack. Hakutumia pesa ya Tino, kwani alimuachia mama yake kile begi alichotaka
Tino akichukue Sabrina akisema kina kadi za benki za watoto na vitu muhimu
vitakavyomsaidia kwa malezi. Siku Sabrina anaondoka pale kwenye Villa,
alimwambia mama yake amrudishie Tino. Na hakutaka kujua kama alimrudishia au
la. Akaachana nao kabisa.
Ila hakuna kati yao
aliyekuwa na hamu ya kurudi tena Dar wala kuwasiliana na watu wa nyumbani kwao.
Kila mmoja kati yao ni kama alikinahiwa na hekaheka za jijini la Dar. Wakatulia
kabisa Singida. Ila kila walipopata pesa ya ziada, hawakuacha kulipa deni kwa
ajili ya mkopo wa nyumba waliyonunuliwa na Junior na mkewe huko Dar. Walipeleka
pesa benki kimya kimya na kutunza resiti.
Kwa Pendo.
M |
ungu
alimsaidia Pendo akafikisha miezi 9 bila shida, nao huo ukawa muujiza mwingine.
Sabrina alimwambia Pendo yeye atakwenda kutembelea tu watoto, sio kuwepo siku
ya kujifungua kwa sababu ya wegazi wake. Inamaana akiondoka yeye, abebe watoto
wote watatu na msichana wa kazi. Akamwambia Pendo wakifika huko watajikuta
wakilea timu ya watoto wake nakushindwa kuangalia watoto wapya. Hata hivyo
Pendo alikuwa na uungwaji mkono mwingi. Watoto wake walikuwa wakisubiriwa kwa
hamu na kila mtu! Nyumba yake isingetosha na Sabrina alimwambia huo ni wakati
wake na yeye wakulelewa na watoto wake tu. Kwamba macho na masikio ya kila mtu
yanatakiwa yawe kwake yeye tu na wanae. Pendo asiye na mengi akawa akicheka tu
bila shida.
Kukiwa
kunaonekana kuna amani na utulivu, shetani naye akihangaika kivyake, muda wa
Pendo nao ukafika, naye akajifungua bila tatizo bila shida. Kwa salama kabisa
akiwa na mumewe hospitalini. Sabrina na Jack na wao wakawepo kwa njia ya video
kushuhudia safari nzima mapaka hao watoto wakazaliwa. Ukweli walikuwa ni watoto
wazuri sana. Kwa afya na muonekano pia walikuwa wakivuti kuangalia. Wazuri kwa
muonekano kama Pendo na Willy wenyewe. Ilikuwa furaha yakupitiliza kwa wawili
hao. Muujiza ambao hawakuutegemea. Na kweli mtoto wa kike walimuita Sabrina na
wakiume Samweli kama alivyopanga mama yao.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Sabrina
akiwa anatoa salamu za pongezi kwa Pendo, tayari alishajigundua ni mjamzito.
Walipopiga mahesabu na Jack, wakagundua ni siku ya kwanza waliporudi hapo
nyumbani wakafanya mapenzi ndio siku hiyohiyo Sabrina alishika mimba. Kabla
Brayan hajatimiza miezi miwili, mama yake alishashika mimba, na ina mwezi mmoja
tayari. “Iweje sasa mshono ufunguke, tumbo lipasuke halafu…” “Naomba
usiniingizie hofu bwana Jack! Wewe tulia.” “Iweje..” “Haitakua chochote.
Nitakua sawa. Na kama wewe unaogopa, usiniambie. Unataka kunitia tu hofu,
wakati haitasaidia tena.” “Basi usiogope.” “Wakati wewe mwenyewe humaanishi?
Ona ulivyoingiwa hofu! Ningejua nisingekwambia kama mimba ya Brayan.” “Hapo
ungeniudhi kupitiliza.”
Safari hii hawakuchelewa kwenda kwa daktari. Halikuwa
jambo la hatari sana, ila waliambiwa wawe makini tu na daktari kuwa karibu ya
Sabrina. Sabrina akawa na kazi ya kliniki zake kama mama mjamzito na za Brayan
mtoto mchanga na mapacha wake. Alikuwa akienda kliniki anacheka mwenyewe kama
mazuri. “Hii ni aibu ya mwaka! Tunaonekana kabisa ni wazazi tusiofikiria.” “Hapana
bwana. Huu ndio uzazi wetu wa mpango. Tunazaa na kumaliza, halafu tunalea.” “Hakika
huyu ndio wa mwisho Jack.” “Na mimi nakubaliana na wewe. Wanne inatosha.”
Maisha
yao yakaendelea kimya kimya wala wasimwambie mtu chochote kinachoendelea kwao.
Jack akawa kimya na familia yake. Mambo yao wao wawili tu. Sabrina hakuwa
amemsikia mama yake na wala yeye hakumtafuta hata Sabina. Ikawa hivyohivyo kwa
upande wa Jack. Kimya maisha yao yakiendelea na watoto wao, msichana wa kazi
akiwa msaada mkubwa kwa Sabrina.
Mungu Wa Yote Katika
Yote
S |
iku moja
Jack alipokuwa kazini akapata simu kuwa kulikuwa na nafasi ya ubunge kwa viti maalumu,
raisi hakuwa ameijaza, yeye ameteuliwa na raisi kuijaza nafasi hiyo. Alipata
ububu nakushindwa kuongea. Mpaka anayempa maelezo na kumwambia siku ya kuapishwa
kwake anakata simu, Jack ndio akawa kama amerudiwa na akili. Akatulia kwa muda,
akagutuka na kutaka kumpigia simu kaka yake kwanza, ila akaoana mpigie kwanza
Sabrina mkewe anayehangaika naye kumuombea. “Brina!” “Tokea
wanao waanze kuita ‘dad’ na kujua ‘hodi’, naona wamekuwa kama wewe! Hakuna kupumzika!”
Jack akacheka nakushindwa hata kumwambia alichompigia simu maana Sabrina alimtanga
na maneno.
“Pokea video nikuwekee uwaone. Wamenikuta nikiomba hapa, naona
wameanza na ‘dad’ na maneno mengine mengi. Sina ninachowaelewa, nimebaki
nimewakodolea macho, pengine wewe dad mtu unayezungumza nao kila wakati utawaelewa.”
Jack akawa anacheka na kuweka video. Akaanza kuzungumza nao. “Naomba niwapeleke sebuleni, muendelee kuzungumza mimi
nimalize maombi Jack. Kuna kitu kinaendelea kwa kina Pendo, nasikia kuwaombea.”
“Ni nini tena?” “Sasa tutazungumza vipi wanao wamejaa kwenye simu?” Jack
akawaangalia wanae, nakuzidi kucheka maana walichukua simu ya mama yao, wao
ndio wakawa wamejaa hapo, hata hakuwa akimuona mama yao ila wao. “Nakuja. Nina habari
njema.” “Sasa wewe usikate. Zungumza nao hapo sebuleni, mimi niombe tena
kidogo.” Akawatoa hao watoto hapo, akarudi chumbani kuomba.
Baada
ya muda Jack akaja. Sabrina akatoka. “Kuna nini, mbona mapema?” Jack
akamsimulia juu ya ile simu aliyopata. “Jackson Msindai!” “Kweli tena. Siamini Brina.”
“Umemuuliza Shem kama ni kweli?” “Bado. Nilitaka kuzungumza na wewe kwanza.
Inamaana na kazi hapa ndio basi.” Jack akawa anacheka kwa furaha. Akampigia kaka
yake. Junior akamwambia na yeye alisikia fununu lakini akataka asikie yeye
mwenyewe kwanza. Na atakuwepo Dodoma wakati wakipishwa. Akampa pongezi na
kumueleza mengi. Mpaka wanakata simu, Sabrina akawa anajua mumewe ameshapewa
ubunge. “Wewe ni Mungu, badala yako hakuna mwengine.” Akasikika Sabrina
akianza kushukuru na kumtukuza Mungu. Jack akidhani milango ya hapo ya miaka
miwili ijayo kuja kugombania hapo Ubunge imeshafungwa, Mungu wala hasikii tena,
kumbe Mungu anawawazia makubwa na mazuri zaidi, tena kwa haraka.“Kweli
tumshukuru Mungu. Mwenzio nilishakata tamaa, nikawa nikifanya bora liende.
Nilikuwa nakusubiria tu na wewe uchoke, tuondoke kwenye huu mji tukaendeleze maisha
Dar, niachane na siasa kabisa.” “Tungepishana na majibu yetu.” Wakashikana
mikono wawili hao na kumshukuru Mungu mpaka wakamaliza.
“Afaddhali
tunahama hapa.” Akaanza kushangilia tena Jack ambaye alishachoka huo mji. “Kaa
hapa chini Jack, acha kukimbiakimbia kila wakati.” “Hakika naondoka Singina,
Brina. Hatuna haja ya kubaki hapa! Kwa nini!?” “Naomba usijisahau Jack. Huu ubunge
ni wa kuteuliwa. Aliyekupa, anaweza kukupokonya muda na wakati wowote
akiamua. Hilo ni moja. Nakuomba uvumilie ili hii iwe njia ya kwanza ya kukupatia
cha kwako, yaani ubunge wa hili jimbo, kama kaka yako alivyojipatia ubunge kwenye
jimbo lake kwa kuchaguliwa na wananchi. Ukifika hapo, basi ujue hakuna mtu wa kukupokonya.
Hiyo moja, lakini pili, kuendelea kuishi hapa japo umekuwa mbunge iwe njia ya
kurudisha mioyo ya watu wa hapa, kwako. Wathibitishie kwamba haukuwa na nia ya
kuwakimbia tokea mwanzo. Wewe ni Mbunge wa viti maalumu, lakini pia unakwenda
kuwawakilisha wao. Kwamba upo pamoja nao kwa nyadhifa yoyote ile utakayoshika. Tukiondoka
tu sasahivi, uchaguzi ujao hatutashinda.”
“Brina!
Hutamani kuishi Dar?” “Mimi natamani kuishi na wewe, popote ulipo na Mungu
alipotupa.” Hapo akamgusa Jack mpaka akarudi kukaa. “Kweli Brina?” “Wewe sio
Junior Msindai, Jack. Junior yupo mbali sana kwenye siasa. Ameshajijenga na amethibitishwa
na Mungu mpaka Mungu ameridhika naye ndio maana unamuona mpaka baba yako
anamsifia kila wakati. Wewe bado upo chini. Tafadhali tuendelee kujijenga kwenye
huu msingi. Hapa ni kwetu na Dar ni kwetu. Hatuna haraka ya kukimbilia popote.
Mungu ameweka mkono wake hapa. Tusikimbie.” “Kweli Mungu alikusudia kukuweka
kwenye maisha yangu Brina. Ingekuwa mwingine angetamani kwenda kuishi kwenye
ile nyumba kubwa na nzuri kule Dar. Au angetamani yale maisha kule. Lakini naona
mwenzangu unafikiria mbali kuliko mimi! Basi tutabaki hapahapa kama ulivyosema.
Ila tujiandae kwenda Dodoma kuapishwa. Tunabeba watoto wetu wote. Tunaenda nao.”
“Kwahiyo kazi tena basi?” “Ndio nimepewa kazi ingine mama. Ila sio uhasibu.” “Hongera
muheshimiwa Msindai.” Sabrina akamfanya Jack ajisikie vizuri sana. “Sasa
hii pongezi urudie nikishaapishwa. Sasahivi twende ukanipe pongezi ya vitendo. Au
umefunga?”
“Usiku.
Usiku lazima nikupongeze. Acha sasahivi niombe Jack. Ipo roho ya mauti naiona
kwa kina Pendo. Sijui kama ni kwa familia yake moja kwa moja na Willy, au
familia ya Ngoi? Sijui. Nipo kwenye kumsihi Mungu awalinde na kuwaepusha na roho
ya uharibifu inayowanyemelea.” “Umemwambia Pendo mwenyewe?” “Hapana. Ila nitamwambia.
Najua bado yupo kwenye kusherehekea uzazi.” “Uzazi huo mpaka leo miezi mitatu!
Mungu anaona ameshamaliza mapumziko, arudi kazini.” Sabrina alicheka sana
hakutegemea Jack aseme hivyo.
“Basi
hapa kwa kuwa hakuna mapenzi, acha nikasubirie barua ramsi ya kuteuliwa, ndipo
na mimi nifanye taratibu za kuacha kazi. Nataka nipaache pale vizuri mpaka
atakaekuja nyuma yangu atambue Jackson Msindai alikaa hapa na alipatendea haki pale
kwenye ile ofisi, sio nitoke kama nakimbizwa.” Jack akatoka, Sabrina na yeye
akarudi kwenye maombi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
0 Comments:
Post a Comment