Sabrina
akapika mpaka akamaliza, pakiwa kimya vilevie, akajua Jack amelala na watoto
huko chumbani. Akamuwekea chakula baba yake
na kwenda kumuangalia. Chakushangaza akamkuta Jack amekaa tu pembeni ya
kitanda amejiinamia. Sabrina akaenda kukaa pembeni yake. “Nilijua umelala?”
Jack akamwangalia tu. “Twende tukale au unataka nikuletee hapa?” “Nimekasirika
sana, siwezi kula.” Sabrina akakaa vizuri na kumwangalia vizuri.
“Sasa
umekasirika nini?” “Kila kitu. Nimekasirika na nahisi umeniadhibu au umenilipa
kisasi kwa kumrudisha Tino kwa wanangu makusudi.” “Sio kweli Jack!” “Ni hivyo
tu. Ukijua wazi nilimfukuza huyu mtu, tena kwa kumpa mpaka restrain order,
wewe unakwenda kinyume yangu na kumpa watoto kwa baraka za wazazi wako!?
Umenidhalilisha kupita kiasi Brina. Katika yote ningetegemea, ila si kwenda
kinyume nami kwa kiasi hicho! Na sijajua ni ujumbe gani unataka kunifikishia?”
“Tafadhali usiende mbali Jack. Uliondoka na sikujua kama unger…” Jack
akasimama. “Si umetaka tuzungumze? Sasa mbona unaondoka?” “Nimekasirika na
kuumia sana Brina. Kwa sasa siwezi kuzungumza na wewe chochote, tukaelewana.
Acha nikatembee kidogo.” Jack akataka kutoka akawa kama amekumbuka kitu,
akageuka.
“Ni
kama nahisi nilijipa au ulinipa nafasi ambayo nahisi siyo! Na kama ndiyo basi ni
kwa vile upendavyo wewe. Unanipa hiyo nafasi na kunipokonya vile unavyopenda au
kujisikia wewe. Nikiwepo ni sawa. Nikiondoka basi pengo langu linaweza kuzibwa
bila shida, tena na yeyote yule hata kwa mtu kama Tino! Unanifungia mimi simu
zangu kila wakati unapojisikia kutozungumza na mimi, bila kunifikiria mimi,
lakini si kwa watu wengine wanao kuumiza! Umeniacha mimi mpweke kule, huku ukilea
na Tino! Mmeanzisha familia yenu na wazazi wako wakiwepo, huna wasiwasi!
Unatangaza kumsamehe Tino, huku mimi umenifungia simu zangu? Kwamba mimi dhambi
zangu NI KUBWA MNO, huwezi kusamehe ila Tino yeye umeweza kumsamehe na
mnaendeleza maisha ya kitajiri huku! Mpaka naanza kuamini ni kweli nimependa
nisipopendwa.” Jack akarudia maneno ya mama yake na kutoka.
Kitendo
cha kuona watoto wake begani kwa Tino wamelala na Tino kusema mpaka aliwalisha
asubuhi hiyo, kilimuuma sana Jack nakushindwa kujizuia. Akasahau hata makosa
yake na kuona Sabrina amemtenda ubaya wakupitiliza kwa kumkaribisha Tino kwa
undani kiasi kile, mpaka kumpa watoto!
Sabrina
akahisi baridi inapita kuanzia juu mpaka chini kama vichomi, akashindwa hata
kusogea pale. Hakutegemea Jack aliyecheka naye alipoingia hapo kwa mara ya
kwanza, angembadilikia kwa kiasi hicho! Ni kama amebadilika gafla! Asijue alichokiona
kwa mapacha wake wakiwa na Tino ndio kimemvuruga. Akabaki amekaa kama sanamu.
Alikaa pale bila hata kusogea mpaka akamsikia mama yake na Sabina wamerudi, akatoka.
“Mbona umepoa hivyo!?” Mama yake akamuuliza. “Nipo tu sawa mama yangu. Sasa na
nyinyi mbona mmerudi mapema wakati nimesikia mnakwenda madukani?” “Kwanza
nisifie.” Sabrina na Sabina wakacheka. “Umependeza mama Sabina.” “Sasa
upendezaji huu Sabina ameona nisiupotezee mtaani, usiku anitoe mimi na baba
yake. Nimeona nije nipumzike, jioni tunatoka. Uzazi mzuri mwanangu!” Akajisifia
mama Sabina akitegemea Sabrina aendelee na cheko lakini akamuona Sabrina kama hayupo
tena pale kimawazo, na akili imevurugwa. Akamuangalia Sabina kumuona kama na
yeye amemgundua mdogo wake, kama hayupo sawa.
“Vipi
wewe Sabrina?” Ikabidi Sabina kuuliza asijue moto uliokuwa umewashwa hapo muda
mfupi uliopita. Baba yao kimya. “Kuna nini tena!?” Mama yao naye akaongeza
swali alipomuona hata mumewe amepoa, na chakula alichowekewa pia hajagusa. “Mimi
naona haya mapumziko yetu yameshaisha, sisi kesho tunaondoka.” Sabina na mama
yake wakashangaa sana. Hawakutegemea kabisa. “Wewe Sabrina, unaacha pesa yote
hiyo iliyolipiwa hapa!?” “Sina jinsi dada. Lazima niondoke. Jack yupo hapa,
nimerudi naye, nimemkuta akinisubiria kwa Pendo. Hali si nzuri, nahisi
sikufikiria vizuri kuja kukaa hapa. Nimemuumiza sana Jack.” “Mbona yeye alikutelekeza?
Sasa hivi yamemshinda ndio…” “Ni nani ambaye hajawahi kunitelekeza?” Sabrina
akamuuliza dada yake.
“We
Sabrina?” “Tuwe tu wakweli dada. Nani ambaye hajawahi kunitelekeza? Lakini si
wote mpo hapa na mimi? Tena wote wamekua wakinirudia mambo yangu yakishakuwa
mazuri. Lakini Jack amekuwa akinirudia nikiwa matatizoni na yeye ndio nimekua
nikimtenda vibaya kuliko wote! Linapofika swala lake huwa sijui ni kwa nini
najisahau nashindwa kufanya maamuzi sahihi! Halafu yeye huwa anaacha kila kitu,
na kunifuata! Hapo alipo amenifuata mimi na watoto hata kazini hajaaga amenikimbilia
huku ambako nimetangaza msamaha kwa kila mtu, huku nikiwa nimemfungia
yeye.” “Lakini ulitaka mapumziko Sabrina!?” “Wala usinifariji dada. Nimekosa.
Jack ni mume wangu. Mapumziko ni mpaka kifo. Halafu ukweli Jack hakuwahi kunichosha
ila kunibeba kwa hali na mali. Kusema nimejificha huku eti napumzika, nimekufuru
dada. Sikufikiria vizuri. Acha niondoke tu, nikajaribu kutengeneza kama
sijachelewa.” Akawageukia wazazi wao.
“Ila
baba na mama, mimi nashauri nyinyi mmbaki, muendeleze mapumziko mpaka muda
uishe, ndipo muondoke. Msiiachie hii pesa hapa.” “Mmmh!” Sabina akaishia
kuguna. “Naomba mnisaidie kukusanya vitu vyetu kokote vilipozagaa humu ndani. Nawasiliana
na dada Pendo, twende jioni tukawaage, kesho tuondoke.” “Na mimi nakuunga
mkono.” Wote wakamgeukia baba yao.
“Nafikiri
na sisi kama wazazi hatukufikiria vizuri.” “Juu ya nini!?” Mama Sabina akauliza
kwa mshangao na ukali kidogo kama anayejua ni nini anachouliza ila tu jazba. “Hiki
tulichokifanya hapa! Hakikuwa sahihi, mama Sabina. Sabrina ameolewa.
Tulimuozesha huyu kwa heshima kabisa. Kukaa naye hapa bila kuzungumza na mumewe
haikuwa sawa.” “Sasa yeye si alikuwa amemtelekeza! Tungefanyaje?” “Huyu kijana
alikuja na wazazi wake mpaka nyumbani kwetu, akatimiza taratibu zote za ndoa,
mama Sabina. Tusilisahau hilo. Akalipa mahari kabisa. Tulipaswa kufanya
mambo kiutu uzima, sio kuishia barabarani.” “Mimi sijaishia barabarani. Yeye
Sabrina alisema anataka kupumzika ndio atajua chakufanya! Sasa tungemuacha hapa
peke yake na mume alikuwa haonekaniki, anaendelea na mipango yake na mama yake
huko? Pengine ameona ameshindwa huko ndio amejirudi, lakini hana wakumlaumu ila
yeye mwenyewe.” Akajibu mama Sabina kwa jazba na kumuumiza Sabrina.
“Jamani
wakulaumiwa ni mimi mwenyewe, wala si Jack au nyinyi. Mimi ndio nilikosea.
Sikufikiria vizuri, na tokea mwanzo nilishindwa kuzungumza na Jack kumuweka
wazi ni nini kiliendelea kati yangu, mama yake na dada yake, tulipokuwa
hospitalini, yeye akiwa hayupo. Nafikiri hata dada Pendo alisema, kama
utakumbuka mama. Mimi ndio nikasema tumuache, tusimchanganye kumbe ndio
nimemchanganya zaidi na kumuumiza kwa maamuzi yangu ya tokea mwanzo. Tafadhali
msinunue matatizo yangu. Hili nahusika nalo mimi mwenyewe, tena moja kwa moja.
Kama mtabaki mbaki, ila mimi naondoka, narudi kwangu.” Sabrina akataka yaishe.
“Hata
hivyo umeshapumzika vyakutosha.” Mama Sabina akajibu kwa hasira akichukia kuona
anataka kupokonywa tonge mdomoni. Alishaonjeshwa maisha ya kitajiri hapo, hakuwa tayari kuyaachia. Akapumbazwa
na wema wa Tino aliowaonyesha muda mfupi tu aliokuwa nao hapo. Pesa alizokuwa
akimpa hata yeye mwenyewe huyo mama, akaona Jack anataka kumrudisha Chalinze
mapema sana! Hakuwa tayari kwani alishanogewa na maisha ya Tino, yakitajiri,
aliyokuwa akiwapa hapo, akasahau anawajibika yeye kama mama.
Sabrina
hakumjibu tena akarudi chumbani. “Sasa mtafanyaje mama?” Akamsikia dada yake
akiuliza. “Mihela yote hii tuiachie hivihivi eti kwa sababu yeye Jack amemaliza
yake na kuamua kurudi sasahivi! Hapana kwakweli. Hatuwezi kuyumbishwa kama
watoto wadogo. Mimi hapa siondoki mpaka tumalize muda wetu. Hatuwezi tukawa
tukichezea pesa kwa kiasi hiki. Hili ni jasho l…” “La Tino.” Sabrina akatoka chumbani
akiwa na nguo chafu za wanae na kumjibu hivyo mama yake.
“Kwani
hilo ndio tumelijua leo?” Akauliza mama Sabina kwa jazba. “Tokea tunahamia hotelini,
na Jack yupo kwenye mambo yake ya kinyang’anyiro tulikuwa tukijua ni jasho la
Tino na tukakaa kule kwenye lile lihoteli na kuhamia hapa bila shida. Leo
kashindwa na yakumshinda ndio aje atuvuruge na sisi? Mbona tokea mwanzo asiache
kila kitu kama kweli yeye ‘muachaji’ na kukufuata tokea wakati ule upo
mgonjwa, kidonda cha kujifungua ndio kibichi kabisa, upo pale kwa Pendo, nikihangaika
na wewe, iwe sasa hivi?” Mama Sabina akauliza. “Nakuuliza wewe Sabrina. Kama
yeye muachaji kweli kama unavyosema huwa anaacha mambo yote na
kukukimbilia, mbona asiyaache ya Ubunge wa huko Afrika ya Mashariki akakufuata
pale kwa Pendo, ndio anakufuata sasahivi, kama si kuchanganyana tu?” Sabrina
akazidi kuumia na kujilaumu kuweka mambo yake na Jack hadharani zaidi kwa
familia yake. Akaona hapo asijibu.
“Naomba
nitafutie tu tiketi za kesho dada yangu, niondoke kesho.” “Kwa hiyo unaacha
vitu vyote hivi? Maana kwenye ndege huwezi kubeba vyote! Acha kuondoka kwa
kukimbiakimbia wewe Sabrina. Alikuacha, amerudi. Basi sasa hivi ndio muondoke
ukiwa na wewe upo tayari! Usikubali kukimbizwa hovyo!” “Mizigo mingine
nitaiweka kwenye mabegi, na maboksi, itatufuata kwa basi. Tutakutana nayo
hukohuko mbele ya safari.” “Makubwa!” Sabina akajibu vile lakini Sabrina akawa
ameshaamua, mandalizi yakuondoka hapo yakaanza. Hakutaka kuzungumzia tena mambo
yake na Jackson.
Sabrina
akaingia bafuni kufua nguo za wanae. “Hakika hapa siondoki mpaka mwisho.” Akamsikia
mama yake akiongea kwa kupania, akisikika mwenye hasira mpaka akamshangaza
Sabrina. “Anamuacha mwanaume anayejielewa, wamaana hivi, anahangaika na mtu
ambaye hana hata msimamo!” Sabrina akashangaa sana na kuumia. Kwamba gafla
Jackson Msindai hana maana isipokuwa Tino! “Ndio ujue kila mtu na akili yake
mama. Hata kama Tino alikosa, lakini amejirudi. Na Tino ana watoto naye wawili!
Tena damu inayofanana na kwao kabisa! Huyu kijana mwingine hata maisha yenyewe
bado hayajamkalia sawa, anahangaika hajui pakushika!” “Siasa zenyewe ndio hizo.
Kupata na kukosa.” Akamsikia mama yake ameongeza kwa Sabina. “Na ndio kakosa
sasa.” Sabina akaongeza kishabiki.
“Halafu
analoshindwa kukumbuka na anajidanganya huyu mdogo wako kwa maneno ya huyu
kinaja asiyejielewa, anasahau kuwa huko ukweni hawamtaki yeye na hao wanae pia.
Mama Msindai hataki hawa watoto hata wakanyage nyumbani kwake! Sasa badala
aende na mwenye watoto, ambaye ameshasema huko amejijenga na maisha huko ni
mazuri, anataka kujichanganya, yamdodee tena, arudi nyumbani na watoto! Kama sio
kuandikiwa kukosa huko ni nini?” Akamsikia mama yake akiongea kwa sauti ya
chini kama kawaida yake anavyomuona mjinga, fungu la kukosa. “Ndicho
anachokitaka na atakipata tu. Mwache amwache Tino aondoke adhani yeye na hao
watoto ndio wamaana sana, aendelee kumringia Tino. Wenzake wanalilia hizo
bahati!” Akaongeza tena Sabina kwa sauti ya kumteta kama asiwasikie.
“Halafu mama huyu Tino analiliwa na wanawake
kibao!” “Kijana mzuri je? Mzuri na pesa anayo. Kinachomshinda kutulia na baba
watoto wake, wakalea watoto na kukuza watoto kama wazungu wenzao ni nini kama
si kuchanganya tu watoto?” “Wazungu wa Singida?” Akauliza Sabina kwa kejeli na
kucheka. “Hebu niambie jamani kama si balaa hilo ni nini? Kwanza kumbe hata
nywele zao zenyewe hawajazijulia mpaka alipokuja baba yao mzazi! Kawaletea
wanae vitu vya maana, angalau watoto wamefanania na utajiri wa kwao! Eti
sasahivi anataka kuwarudisha kwenye vumbi huko, kama si kuzisaka shida ni
nini?” Sabrina akaumia sana wasijue amewasikia vile walivyokuwa wakimsema kwa
kunong’ona.
“Twende
ukanichagulie nguo nzuri, tutoke, Sabina mwanangu.” “Mama huyumbishwi?” Akamsikia
dada yake akiuliza na kucheka kishabiki. “Hata kidogo! Kwa kipi mno? Hanitoi
hapa kwa kunikimbiza. Kwanza Tino alisema atakuja kutuaga na kutushukuru rasmi
kwa kusaidia kumlelea wanae. Sasa unafikiri atakuja na maneno matupu ya siasa
hapa?” Sabina akazidi kucheka. “Akijidai kuondoka tu na wanae, mimi nitakuja tukae
wote kwa hizo siku zilizobaki. Bahati kama hizi haziji mara mbili.” “Kumbe! Akisema
cha nini, wenzie wanalia tutakipata lini.” Mwishoe akawasikia wamehamia chumbani
huku wakiendelea kumsema.
Akaendelea
kufua mpaka akamaliza, Jack hakuwa amerudi na wanae wakawa bado wamelala.
Akatoka kwenda kumtafuta. Akamkuta amekaa sehemu, humohumo ndani ya uzio wa
Villa, lakini peke yake. Na yeye akaenda kukaa pembeni yake.
“Naomba
turudi na watoto nyumbani.” Jack akamwangalia. “Namaanisha Singida. Nimeshaanza
kufungasha ili kesho tuondoke.” “Nashindwa kurudi mle ndani.” Sabrina akawa ni
kama amemuelewa. “Kukaa mle ndani nasikia ni kujidhalilisha kwa hali ya juu.
Yaani na mimi nakuja kula na kulala kwa Tino! Natunzwa mimi na wanangu na
mwanaume kama Tino? Hata kama sina uwezo kama wake, ni bora niondoke mimi
ambaye sina uwezo, niwaache.” “Tutaondoka wote.” “Mimi sina pakwenda. Sina
mahela ya kukodi hapa.” “Kuanzia sasahivi popote unapokwenda, ujue tunakufuata
wewe.” Jack akamwangalia na kunyamaza.
“Hata
kama chini, twende tukalale wote. Popote pale. Sasa hivi tutakuwa tukipanga
mambo yetu pamoja. Na tabia ya kukublock naacha kabisa.” Jack kimya. “Nisamehe mume
wangu.” Hapo akamgusa Jack. “Sasa ndio tunakwenda wapi?” Jinsi alivyouliza,
Sabrina akajua hasira zimeanza kupungua. “Au tukalale kwa dada Pendo?” “Hapana.
Pendo alinitukana. Ananiona mimi mjinga. Sijielewi. Sitaki kurudi tena kwake
nikiwa na shida.” Katika mtu wa mwisho kutaka kugombana naye ni Pendo. Sabrina
alishampenda Pendo na kuona wanaendana katika kila jambo. Ila akaona kwa wakati
huo aache tu asimtibue zaidi.
“Na
kwa Sabina pia sitaki. Namuhesabu dada yako ni msaliti mkuu na amenidharau
kupita kiasi. Hawezi kumrudisha Tino kwako wakati akijua mimi ni mumeo! Hata kama
ulimjua Tino kupitia yeye, lakini angetambua nafasi yangu na kuiheshimu. Hiyo
ni dharau ya hali ya juu.” “Basi kwa kuwa tuna watoto, siwezi kukwambia twende
tukalale pale kwetu ambako hakuna hata kiti cha kukalia. Ingekuwa ni mimi na
wewe tu, ningekwambia twende tukalale hata chini. Lakini kwa kuwa tuna watoto,
nashauri twende tukatafute hoteli ya uwezo wetu, kesho turudi kwetu, Singida.”
“Unauhakika?”
“Kabisa Jack. Mimi nilitaka tu kupumzika. Nishapumzika vyakutosha, turudi
nyumbani tukaendelee na mipango yetu.” “Wala si kuendelea. Huko Singida nako
kumeharibika, hakufai! Nimeharibu kupita kiasi mpaka nafikiria kurudi kutafuta
kazi nzuri huku Dar. Tena safari hii sitaki tena serikalini. Nitafute kwenye
kampuni nzuri nilipwe vizuri huku Dar, si huko Singida kuendelea kudhalilishwa.”
“Ni nini tena?” “Hili swala la Ubunge wa EALA, imekuwa kama mkosi Sabrina. Nimejichafua
kupita kiasi. Nimerudi chini kabisa. Kama unadhani kuna kuendelea, basi ujue
hali ni mbaya kuliko vile ulivyonikuta mwanzo kabisa ulipohamia Singida.”
Akamuelezea kila kitu jinsi mpinzani wake anavyomchafua. “Sasa ubaya ni kwamba ni vita ya ndani kwa ndani! Heri
ingekuwa anatoka chama pinzani. Ila ni ndani! Amegeuza watu wote wapo upande
wake!” Akasikika amekata tamaa kabisa. Sabrina akazidi kujilaumu.
“Nisikilize
Jack. Shetani ni kama simba angurumae. Na huwa akinguruma, anaogopesha
sana. Lakini hana lolote, ni kelele tu. Ila sisi tunaye Simba wa kabila
la Yuda. Yeye akinguruma, kila kitu kinakaa sawa.” Jack akamwangalia.
“Usitishwe na kelele ya ‘kama simba’. Si simba huyo. Anakutisha tu ukimbie. Ni
kelele tupu.” “Sabrina! Ame…” “Nakwambia acha kutishwa na kelele, Jack. Hizo ni
kelele, na kamwe hatutakimbia mji kwa ajili yake. Tutaondoka Singida, Mungu
akimaliza shuguli zake kwenye ule mji kwa kututumia sisi. Mungu akisema
tuondoke, tutaondoka. Lakini si kwa kutishwa. Hatutakimbia, wala kutishwa. Hata
wifi Jacinta nilimwambia. Sijamalizana na Singida. Na mimi si mtu wa nusunusu.
Nikimalizana na Singida, ndipo nitaondoka. Tena tukiwa na baraka za Mungu,
lakini si vinginevyo.” “Hata mimi uliniambia hivyo. Lakini ilikuwa kabla ya
huyu mpinzani!”
“Tuliliweza
lile jimbo likiwa na yule mpinzani aliyetawala kwa kura za wananchi wengi, kwa
miaka mingi tu. Halafu eti leo tuje kukimbizwa na huyu mpuuzi ambaye hajawahi
kufanya chochote pale! Acha kutishwa Jack. Kwanza hukufanya kosa. Ubunge wa
EALA sio siri. Majina yalitangazwa tokea hata uchaguzi wenu kufanyika. Ilijulikana
na kila mtu kasoro kwetu ambao hatukuwa mitandaoni. Sasa siri hapo iko wapi?”
“Anasema mimi sikuwaambia pale jimboni.” “Tokea lini wewe umekuwa ukiwaambia
mipango kama si kuwaletea matokeo mazuri tokea mwanzo? Eti Jack?” Jack akaanza
kufikiria. “Miradi yote tuliyofanya pale Singida, ulikaa na mtu wa chama
mkapanga ndipo mkachukua nao hatua au waliyaona tu matokeo mazuri? Wao
wanajuaje kama ulikuwa ukihangaikia huu Ubunge kwa faida yao pia? Kwamba kama
ungeshinda inamaana ungekuwa na nguvu, pamoja na uwanja mpana wa kuwawakilisha
kimataifa?” Hapo akaanza kubadili hata mtazamo wa Jack mwenyewe.
“Kukimbia
ni kuhama mji kisha kwenda kugombania kwingine. Sisi tulikuwepo pale, miradi
ikiendelea, na wewe ukihangaika kutuwakilisha kimataifa. Hilo ni kosa au
ushamba wake huyo anayekuchafua, asiyejua mambo?” “Sasa kama unayajua yote hayo
kwa nini ulinifungia simu zangu ukaniacha mimi naabika sina majibu ya
kueleweka? Ulinitelekeza Brina.” “Nimekosa Jack. Nakuahidi sitarudia tena.
Najutia vibaya sana. Nahisi mimi nimechangia kufungua huo mlango wala si wewe.
Nisingepotea kwa muda wote huo, tusingetoa huu mwanya. Lakini naamini Mungu
ataturehemu tu. Turudi nyumbani kwetu Singida, tukaendelee wala tusikimbie.” Jack
akatulia.
“Twende.
Huna haja yakuingia ndani. Nabeba vitu vyetu, naingiza kwenye gari na watoto
wetu, naaga, tunaondoka.” Jack akabaki akifikiria. “Twende Jack. Nakuahidi kila
kitu kitakuwa sawa. Mungu atatusaidia. Hakuna kukimbia.” “Hata hapa sitakimbia.
Japokuwa ndugu zako wameniumiza, twende tu nikakusaidie kukusanya vitu, tuage
na kumshukuru mama kukusaidia kulea, tuondoke na watoto wetu.” Wakarudi pale
walipokuwa wakiishi kina Sabrina.
Bado
baba yake alikuwa amekaa sebuleni, Sabina na mama yake wapo chumbani. Jack
akapitiliza chumbani wala hakukaa hapo. “Sisi tunaondoka baba.” Sabrina akaaga.
“Sasa hivi?!” “Ndiyo.” “Unataka nikusaidie nini?” “Jack atanisaidia baba yangu.
Wala usihangaike. Kwanza wala si vitu vingi sana.” Mama yake akatoka. “Yaani
gafla mnaondoka sasahivi?!” “Ndiyo.” Sabrina akajibu. “Mnakwenda wapi sasahivi
watoto wote wamelala?” “Tutajua huko mbele ya safari, mama.” “Huko nikusumbua
watoto Sabrina. Nakwambia ukweli wala sitakuficha. Kuwa mama mwenye msimamo.
Ukiyumba wewe ujue unayumbisha watoto. Huwezi ukawa wewe ni mtu unayeyumbishwa
tu.” “Wewe usiwe na wasiwasi mama yangu. Hawa watoto watakuwa tu sawa. Acha
tusaidiane, tutoke.”
“Utakuja
kunikumbuka Sabrina wewe! Tena ukiharibikiwa safari hii ujue unao watoto
watatu! Uliachwa nao hao, ukajionea mwenyewe! Sasa wewe chezea bahati, kama
hujalia tena peke yako.” “Mungu atanirehemu.” “Si ndio amekurehemu! Unataka
rehema hizo upewe mara ngapi? Ulitelekezwa hapa. Tino amekusaidia. Kweli
unataka uondoke hapa bila hata kumpa nafasi aage watoto wake! Ubinadamu huo uko
wapi, Sabrina wewe? Utalaaniwa bure, bila sababu.”
“Hebu
subiri kwanza mama. Mbona gafla swala limekua Tino tu? Mbali na Tino kulipia
hapa, msaada gani mwingine aliotoa? Kaja juzi tu hapa kakuta watoto wakubwa
kabisa hawa, imekua nachezea bahati!? Bahati hiyo ni ya vyanuo vya kuchania
nywele hizi za hawa watoto?! Kama watoto wangekuwa wanakuzwa kwa vyanuo na
shampuu za nywele tu, si kila mtoto angekuwa na hali kama za kina Jeiline?” Sabrina
akawa amekasirika kabisa. “Hawa watoto wamekua au wapo hivyo walivyo na sabuni
za Jack, na mbona kila mtu alikuwa akiwasifia! Leo kaja Tino, na maneno ya kujitilisha
huruma, na vijisenti vyake ndio imekua nongwa?” “Wala si vijisenti.” “Basi hata
kama ni milionea, simtaki. Acheni nikaharibikiwe mwenyewe na watoto
wangu, pamoja na Mungu wangu. Kama mnawasiwasi na kuja kuachwa tena na hawa
watoto, nikaja kuwa mzigo kwenu, msiwe na wasiwasi. Sitarudi tena na
wanangu huko nyumbani. Nitahangaika nao mimi mwenyewe. Hata nikiwa na shida sitawasumbua
tena. Nitahangaika mimi mwenyewe na Mungu wangu ambaye huwa haniachi na wala
hajawahi kunichoka. Hamtapata mzigo tena kutoka kwangu. Endeleeni na maisha
yenu, acheni mimi ambaye situmii akili nikahangaike kivyangu.”
“Nani
amekwambia hutumii akili?” Akauliza Sabina. “Nimewasikia sana wewe na mama
mkisema situmii akili. Naachia bahati ya Tino. Niacheni na ujinga wangu na
wanangu.” “Utatukumbuka Sabrina wewe?” “Wala sijawahi kuwasahau dada yangu.
Nawajua vizuri sana.” Sabrina akaondoka hapo maana walishaamsha watoto wote,
akasikia wakizungumza ndani na Jack. Akajua sababu ya kuongea kwa sauti ya juu ameamsha
wanae. Jack hakuingilia kabisa japo alisikia kila kitu. Akajisikia fedheha ya
hali ya juu. Ila hakuwa na jinsi. Wakakusanya vitu vyao vyote, wakatoka hapo
baada ya Sabrina kuwaachia funguo zote za hiyo Villa na maagizo ya kuparudisha
pindi watakapokuwa tayari. Ndipo wakaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Walitafuta
hoteli ya kawaida tu. Jack akawaacha hapo na kutafuta vifaa vyakufungia mizigo
yao maana vitu vingine walikuwa kama wamevitupia tu kwenye gari. Akarudi na masanduku
pamoja na mabegi. Ikaanza kazi ya kufungasha tena. Walipomaliza kuweka mizigo
yao vizuri. Jack akatoka tena na mizigo waliyotaka iondoke na basi na kwenda kuituma
kituo cha mabasi ili iondoke kwa basi. Kisha kutafuta tiketi zao sasa za ndege.
Jack hakutaka kutumia tena mtu yeyote kumsaidia. Akayafanya yote yeye mwenyewe
ndipo usiku sasa wakaelekea nyumbani kwa Pendo kumrudishia gari yake na Sabrina
alimwambia nilazima akamuage.
Jack
alifika na kukaa sebuleni na wanae akiwa ameshachukua namba ya simu ya mwenye
taksii na kumwambia akiwa tayari atampigia afike hapo nyumbani kwa Pendo
kuwachukua. Pendo na Sabrina wakaingia chumbani kuteta kama kawaida yao.
“Mbona
sasa kama mnaondoka mbiombio? Shuguli zimemuisha mumeo na mama Msindai ndio
katulia sasa?” “Nilimuomba mwenyewe kwa Mungu huyo. Mungu akanipa kwa upendo na
heshima kubwa sana. Acha tu niende dada yangu. Hata hivyo nishapumzika
vyakutosha.” “Nimemuona alivyotulia pale sebuleni. Sasa mama yake?” “Amesema
anamwacha kwa muda kwanza. Naona mara ya mwisho hawakuachana vizuri. Mimi
nilimwambia sitajali, hata kama anataka kwenda na Brayan kumsalimia,
nitamfungashia maziwa ya mtoto aende naye akamsalimie bibi yake, naona amekataa.
Nimemuacha.” “Yanawarudi wenyewe. Nasikia wageni wenyewe aliokuwa amewaalika
kwenye babyshower ya Brayan walimsusia. Akajidai kukusingizia wewe.”
“Dada!” “Kweli tena. Ni kama akaingia mkosi baada ya pale hospitalini. Dakika
za mwisho kabisa, kila mtu akawa anampa udhuru. Nancy kayasikia huko mtaani.”
Pendo akamsimulia mengi, Sabrina
akashangaa na kunyamaza tu.
Mwishoe
Jack akaita taksii, wakaagana hapohapo, Sabrina na familia yake wakaondoka
kurudi hotelini. Kesho
yake tena wakaita taksii ikaja kuwachukua na kuwapeleka uwanja wa ndege.
Sabrina akarudi Singida na familia yake bila kuwasiliana tena na ndugu yeyote
upande wa Msindai wala kumsikia Sabina na mama yake. Waliondoka kimya kimya.
Hiyo nayo ikawa mara ya pili tena Sabrina kuondoka jijini akiwa amejifungua
bila maelewano mazuri na mama yake mkwe. Mwanzoni alidhania ni kwa sababu ya
watoto ambao si wa Jack, safari hii akamzalia Jack mtoto wa kiume pia
haikusaidia. Bado mama Msindai hakutaka kumsogeza karibu yake. Ila safari hii
ndio ikawa mbaya zaidi. Ikawa ndugu upande wa mke, mama mkwe na shemeji, wamemchukia
mume, hawamtaki tena Jack. Wanamtaka Tino aliyerudi na ahadi pamoja na pesa
nyingi. Na ndugu upande wa mume nao, mama mkwe na wifi wamemchukia mke. Kwa
hiyo Jack akaona hata asiendelee kumvuruga kaka yake. Akaona maamuzi yake
yanaishia kuleta kutoelewana kati ya mama yake na kaka yake, pamoja na Jacinta
pia. Akaona safari hii awaache kabisa. Wakaondoka jijini kimya kimya.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ugomvi Wa Wapendanao
Ukishirikishwa Nje, Wao Wakisameheana, Huacha Madonda Nje.
Nini Kitaendelea?
0 Comments:
Post a Comment