Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 55. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 55.

Alipomaliza kuzungumza na Tino tu, akaelekea jikoni bila ya kumsemesha Jack. Na yeye  Jack akasimama kwa haraka na kumfuata. “Naomba tulia Jack, ili nipike.” “Kwani wewe ulikuwa hata ukiniwaza?” Sabrina akaendelea nashuguli zake. “Mimi nilikuwa naangalia simu usiku kuchwa, Brina! Najiambia pengine Brina wangu hasira zitakuwa zimeisha, sasa hivi anahamu na mimi. Nikawa nikikutumia ujumbe mchana na usiku!” Sabrina kimya. “Bado umekasirika?” “Hapana Jack.” “Kwa hiyo umenisamehe na bado unanipenda?” Sabrina akaendelea na shughuli zake.

“Hata iweje, sitakaa nikakuficha kitu tena, Sabrina wangu. Siri ni kati yangu mimi na wewe tu. Kwanza tutakuwa hatuwaambii watu mambo yetu.” Sabrina kimya. “Nimekoma Brina. Halafu hata ubunge wenyewe nilikosa. Sasa hivi sitaki tena mambo ya siasa. Nakutaka tu wewe Sabrina wangu. Au unasemaje?” “Maswala ya kazini umeyaachaje Jack?” “Nimeyaacha na sijali. Nimekufuata wewe.” Sabrina akamwangalia na kuchoka kabisa. “Kwa nini hukuomba ruhusa hata ya bila malipo?” “Hivi unajua inachukua muda mrefu kujibiwa? Na mimi sikuwa na muda wa kusubiri nilijua nikija kukupoteza tena safari hii, naweza nisikusikie tena.” “Hivi ukoje Jack wewe jamani?!” “Sasa wewe kwa nini uliniblock kila mahali? Nilijua ndio unaniacha moja kwa moja!” Jack akaendelea.

“Nimeingia aibu Brina! Ubunge wenyewe nimekosa!” “Sasa aibu ya nini tena?” Sabrina akamuuliza huku akiendelea na mapishi. “Huoni ni kama nimejidhalilisha tu? Nahisi Mungu amenilaani. Wanasema laana ya mke inashika, Sabrina! Mungu amenilaani na kunidhalilisha ndio maana nimekosa.” “Nisikilize Jack. Wewe hujaalaniwa na yeyote kati yangu na Mungu. Na mimi sioni kama umejidhalilisha hata kidogo.” “Kweli Sabrina, au unanitia tu moyo?” Sabrina akamgeukia vizuri Jack.

“Lipi bora, kujaribu na kushindwa au kutojaribu?” “Lakini si kwa jinsi kama hii! Mpaka nikakuudhi!” “Mimi sikukasirika kwa wewe kugombea huo, Jack! Kwa kuwa sipo kwenye mashindano na mama yako. Siku ile nilikuwa nimeumizwa na maneno mabaya sana ya mama yako pamoja na Jena. Sijali kama utabadili mawazo. Nafanya kila kitu kwa ajili yako nikitambua kile Mungu ameweka ndani yako. Ukisema leo hutaki tena ubunge, mimi sina neno. Lakini isiwe sababu ya kukata tamaa. Hapo hapana. Umejaribu huko, bado zipo nafasi nyingi tu. Inawezekana hiyo siyo njia Mungu aliyokuandikia Jack.” “Kweli Brina?”

“Kabisa. Wewe sio Mungu kwamba unajua kila kitu! Unajaribu huku ukimtumaini Mungu. Ukikosa, unajaribu tena mpaka mlango wako aliokusudia Mungu ufunguke. Kile alichokuandikia Mungu lazima kitatimia tu. Usikate tamaa.” Hapo akamtuliza Jack. “Nashukuru Brina. Nilikuwa nakuonea aibu nikajua utakuwa ukinicheka!” “Jack! Kwa nini? Hata kidogo! Kushindwa kwako wewe ndio mimi. Haijalishi njia gani unatumia. Iwe mama yako, kaka yako, yeyote  ile, ilimradi tu kufanya jambo sahihi. Umefanya jambo sahihi lakini halikuwa lako. Basi, tushukuru katika hilo na kusubiria jingine.”

“Mwenzio nilijua umeniacha.” “Nilitaka kupumzika. Nikajua mambo yako na mama yako nikiwepo, naweza nikakuchanganya, bora nikuache na mimi nitumie muda  huo kupumzika. Nilikuwa naumwa sana, nikaona nikiendelea vile, sitakuwa msaada kwa yeyote.” “Sasa hujakasirika nilivyokuficha?” “Umenishangaza sana na kuniumiza. Ila nimeona na wewe ni binadamu tu kama wanaume wengine waliozoea kuniumiza na kujirudi.” Hilo likamuuma sana Jack.

“Usiseme hivyo Brina!” “Kweli Jack. Ungekuwa ukiniheshimu kweli, na kunipenda kwa dhati, ukijua mimi nipo na wewe ukurasa mmoja, nakuwazia mema wala si mabaya, nipo Singida, mkoa ambao hata sikuwaza kuja kwenda, ila naishi kwa ajili yako, kama ungethamini hilo, usingenificha. Ni ile hali ya kunidharau kama wengine wote ukijua utarudi kwa wakati wako, utanikuta, utatoa sababu nzuri iliyokusababisha ukafanya ulichokifanya, kwamba makosa hayakuwa yako, mtu mwingine ndiye amekusababisha ufanye ulichofanya, kisha ukataka yaishe kwa wakati wako wewe unapoona inafaa kujirudi kwangu, kisha na mimi nielewe tu, nikubali yaishe tuendelee. Si ndivyo hivyo unavyotegemea au nimekosea?” Kimya.

“Hapa umerudi na sababu kuwa mama Msindai ndiye amekufanya ufanye mlichofanya. Uliniacha na watoto nyumbani kwa Pendo kwa siku za kutosha tu, nikiwa mgonjwa na mtoto mchanga, ukaendelea na mambo yako bila hata ujumbe kunijulia hali, mpaka ukamaliza, ndipo uliponitafuta kama wengine wote waliopita kwenye maisha yangu, ndivyo hivyohivyo ulivyonifanyia Jackson. Huna tofauti ila sema kwako imenishangaza zaidi. Imekuwa mshituko mkubwa sana kwangu, kwa kuwa wewe nilijua upo tofauti Jack! Hata Tino nilimwambia, wewe sio kama wengine. Ila umeishia kuwa kama wengine tu.” Hapo Jack akaishiwa nguvu na kupoa kabisa. Sabrina akaendelea kupika.

Tino akapiga simu. Sabrina akapokea. “Nipo hapa nje.” “Unataka nije kukusaidia?” “Hapana. Nataka kujua kama naruhusiwa kuingia?” “Karibu Tino! Sasa hao kina dada si wamelala?” “Nitawabeba tu, ni kama wanasinzia.” “Wamechoka. Walete walale.” Baada ya muda Tino akagonga na mguu, Sabrina akakimbia kwenda kufungua mlango, akakuta amewabeba wote wawili. “Waone! Ujanja wote umewaishia.” Waliposikia sauti ya mama yao, wakatoa vichwa begani kwa Tino, na ndipo wakamuona Jack kwa nyuma. Wakaanza kumlilia wote wawili.

“Hata mimi nilikuwa na hamu na nyinyi. Njooni.” Jack akaenda kuwapokea wote wawili na kuwabusu wakilia. “Msilie sasa. Mnausingizi?” Wakabaki wakimwangalia Jack na machozi mpaka mashavuni. “Wamekula?” Jack akauliza akiwaangalia watoto. “Wamekula kidogo. Watakuwa wameshiba, tuliwalisha uji mwingi asubuhi. Hata nilipowaongezea...” Jack akaondoka wakati Tino hata hajamaliza! Sabrina akamwangalia, akajua amekasirika.

“Acha nikachukue mizigo yao kwenye gari.” “Mimi nipo huku jikoni, napika.” Tino akatoka na kurudi na mizigo ya watoto, akaiacha sebuleni na kumfuata Sabrina jikoni, Jack akiwa chumbani na watoto. Wakasikia mlango mkubwa ukifunguliwa. “Sabrina?” “Shikamoo baba. Nipo jikoni. Mbona mapema?” “Naona Sabina amewaongelesha hao vinyozi mpaka wakalainika, nimenyolewa kwa haraka, nimemaliza, nikaona nirudi tu. Mama yako na Sabina nimewaacha hukohuko, wamesema wakimaliza wanakwenda madukani.” “Basi kaa niivishe sasa hivi, ule.” “Wala usiharakishe kwa ajili yangu, labda wengine. Mimi bado nimeshiba.” “Sawa baba yangu.” Sabrina akarudi jikoni alipokuwa amemuacha Tino.

Ukweli, Mchungu.

 “Naweza kujaribu kuja jioni nione kama naweza kupata nafasi ya kuwaaga?” “Sijui kama Jack atatoka nao au la! Na kwa sasa hivi alivyo sidhani kama ni wazo zuri kumuuliza. Ila umekuwa nao siku nyingi Tino!” “Daah! Najuta Brina! Najuta sana. Napatwa uzito wakuondoka, na kazi zinanisubiri. Hapa nilikuwa nikifanya kazi usiku ili mchana niwe nao hawa. Na bado naona haijatosha! Unafikiri nikija kurudi tena wakati mwingine nitapata nafasi kama hii?” “Siwezi kukuahidi. Sitaki kukupa tumaini ambalo linaweza lisiwepo.” Tino akatulia kidogo.

“Lakini Sabrina, kila siku namshukuru Mungu nilikosea nikiwa na wewe.” Sabrina akanyamaza. “Kwa hakika namshukuru Mungu. Ingekuwa mtu mwingine angefuata ushauri wangu, hiyo furaha tunayoipata sasa hivi tusingekuwa nayo. Asante sana na samahani. Ila ujue najutia.” “Lakini labda mimi nikuulize Tino, unajutia nini? Upande upi haswa?!” “Kila kitu Sabrina.” “Kwa kuwa leo tunazungumza, hebu fafanua kidogo. Kuwa tu muwazi. Maana umezungumza kwa kurudiarudia kuwa unajuta. Ni nini unajutia?” Sabrina akamuuliza bila jazba.

“Maamuzi niliyoyafanya nilipokuwa na wewe Sabrina. Huwa nakaa peke yangu, au nakuwa nimelala, nikikumbuka yote yaliyoendelea Moshi, huwa nashituka kama narushwa gorofani jinsi moyo wangu unavyovurugika! Nikikwambia hali niliyonayo nilikwenda mpaka kwa wataalamu wanisaidie, ujue sidanganyi. Lakini mwishowe imenibidi tu kurudi japo mliniwekea restrain order, lakini nilijiambia nilazima nije kukiri kosa.” “Naomba tukae kidogo Tino. Tafadhali, ili tuzungumze, maana nahisi unachanganya habari ambayo haipo. Njoo hapa kwenye meza, sehemu yakulia chakula.” Sabrina akazima kabisa jiko na kuhamia mezani, baba yake akiwa sehemu ya sebuleni.

“Twende taratibu tu. Maana hatugombani. Leo tumepata huu wasaa, tuwekane sawa. Pengine kuna kitu wewe unachanganya hujaelewa au ni mimi.” Tino akatulia. “Uliponiacha hospitalini Moshi, ulisema unakuja hapa Dar, kwenye maswala yako ya kupigania mali zako, kisha kwenda kutibiwa nchini Italy. Hutaki ijulikane kama nina mimba yako au hata kama tulikuwa na mahusiano mengine yeyote yale bali kukufanyia kazi kama Lela alivyonipa ajira ya kukuuguza tu, ili asije akashinda kesi. Na ukasema waziwazi kabisa, huna muda wakulea. Unataka ukatibiwe mkono, ambao ndio chanzo chako cha pesa. Maswala ya watoto au mtoto kwa wakati ule tukijua ni mmoja, ulisema hutaki. Si mara moja, ni kwa kurudiarudia ulisema hiyo kauli, tena ikaanza kwa ukali kabisa ukinifoka kwa nini sitaki kutoa mimba! Ukanichukia kabisa, hutaki tuzungumzie chochote hata kukujulia hali isipokuwa kutoa mimba.”

“Haya. Ukawa hutaki hata kukaa sehemu niliyopo au nikufuate popote kwa hasira kwamba ni kwa nini nang’ang’ania mimba ambayo wewe hutaki! Tukaendelea ukiwa kimya kwangu, mwingi wa hasira na kunikwepa. Ukifungua mdomo au ukiniona swali likawa nimefikia wapi juu ya kwenda kutoa mimba. Haya, ukabadilika jinsi ya utakaji wa kutolewa mimba. Ukaja kwa kunibembeleza sasa, ukinisihi nitoe mimba, ili tuachane ukiwa umeridhika, hujaacha kitu kwangu. Kwa kurudia rudia hayo maneno ukinieleza hutaki kuniacha na mimba itakayojulikana wewe ndiye uliyenipa. Si ndivyo ilivyokuwa au umesahau?” Tino akawa mwekundu kabisa, kimya.

“Kuthibitisha ulichopanga na kuniambia ni kweli ulikusudia, uliniacha hospitalini ukiwa umejiridhisha nimeshatoa mimba na umetengeneza ushahidi kuwa mimi nilikuwa mfanyakazi wako tu. Ukanisainisha karatasi yakuwa nilikuwa nikikufanyia kazi na si vinginevyo, na kuwa nilipokea malipo yangu kwa hundi kabisa ili kubakiwa na ushahidi kuwa nilipokea ile pesa au  benki ionyeshe hundi yako ilitoka kwenye akaunti yako kuingia kwangu kama niliyekuwa nikikufanyia kazi tu! Sijui kama unakumbuka hayo yote Tino?” Kimya.

“Kuendelea kuthibitisha unamaanisha, hukunitafuta tena. Sikubadili namba ya simu kwa zaidi ya miezi miwili nafikiri mpaka akaja kunichukua Jack pale Moshi, tena nakumbuka njiani ndipo nilitoa ile namba. Lakini kwa kipindi chote hicho hukuwahi hata kuuliza ninaendeleaje?!  Hata kwa ujumbe tu, hukukosea.” “Lela alikuwa akikutafuta sana ili umsaidie kumtetea. Akawa anawinda simu yangu na akapata watu wa mtandaoni wanaofuatilia simu zangu.” “Tino! Kweli hiyo ndio sababu yakushindwa kumjulia hali mtu kama mimi kweli! Vipo vibanda vya simu vingapi hapa jijini, au watu wangapi hapa Dar ambao ungeweza hata kuazima tu simu ukanijulia hali? Na kama kukumbusha tu Tino, uliweza kudai gari yako ukiwa uliniacha hospitalini. Tukawasiliana kuwa yule uliyemtuma kuja kuchukua gari amefika, na nikakutaarifu kuwa nimeshamkabidhi gari yako. Katika mazungumzo hayo Tino, ulishindwa vipi hata tu kuulizia hali yangu? Si kama mpenzi, ila tu ubinadamu! Au umesahau haya ninayokwambia?” Sabrina akauliza taratibu tu.

“Tafadhali nijibu Tino, usijekuwa unajutia kitu kisicho.” “Nilikuwa kwenye hali mbaya Sabrina. Unakumbuka hata ile hali ilinipata siku ile tuliagana wewe unakwenda saluni mimi polisi? Nikashindwa kabisa kufikiria? Nahisi akili yangu haikuwa sawa Sabrina. Hata maamuzi yangu mengi niliyafanya wakati ule hayakuwa sahihi nikishindikizwa na Max tu au yeye akiniongoza vile atakavyo. Na ndio maana hata nilipofika Italy ikabidi kupelekwa kwa daktari wa mambo ya saikolojia kutibiwa.”

“Mmmh! Kwa hiyo hata mazungumzo mengi tuliyozungumza mimi na wewe wakati tupo pale hotelini hayakuwa yakitoka kwako kama Tino huyu ambaye akili yako sasa hivi unasema imetibiwa, ila yalitoka kwa Tino ambaye akili ilikuwa imechanganyikiwa? Kwamba yote na vyote tulivyofanya pamoja, nilikuwa nipo na Tino ambaye hakuwa na akili timamu, ndivyo hivyo?” Sabrina akahoji.

Tino kimya. “Sasa hebu jiulize Tino, kama ulipatwa na tatizo la akili, uliwezaje kumshinda Lela aliyekuwa amejiandaa vile, huko mahakamani mpaka ukapata mali zako zote na kuachana naye bila hata kulipwa fidia yeyote ile na wakati alikuwa mkeo wa zaidi ya miaka miwili?” “Max ndiye aliyekuwa akiendesha mambo yote.” Sabrina akamwangalia huku amekunja uso. “Kweli Sabrina.” “Mimi sijui unapenda kujiaminisha nini ili kujipa amani kwenye maamuzi yako uliyoyafanya na unayoendelea kuyafanya, ila huwa watu wanasema, na nafikiri ndivyo na wewe unavyoishi kuwa, maishani huwezi kupata kila kitu Tino.”

“Ulipiga mahesabu yako vizuri sana. Tena kwa kunitamkia waziwazi kuwa hutakuwa na muda na mimi wala watoto.” “Sabrina!” “Unakataa nini Tino?! Hukuniacha Moshi wewe ukisema hutakuwa na muda na..?” “Nilikwambia ni kwa sababu nataka nikatibiwe, na ningerudi kukutafuta.” Sabrina akacheka kwa kuumia sana. “Kweli Sabrina. Nakumbuka kukwambia hivyo.” “Sasa akili yako haikuwa ikifanya kazi katika lipi na lipi ilikuwa ikifanya kazi? Mbona umekusudia kugawa yale matukio kwa mafungu ili tu kujipa amani?” Kidogo hasira zikaanza kumpanda Sabrina.

“Ulifanya mambo yako kwa umakini sana Tino. Jack anakuja kunichukua pale Moshi, wewe ulikuwepo nchini, na kesi ulikuwa umeshashinda na imefungwa! Uliishi Dar, mimi umenitelekeza Moshi, na haukuwa mume wa Lela! Wewe sema umepatwa tamaa baada yakuona hawa watoto.” “Sio tamaa.” “Nitamaa tu Tino. Unataka upate vyotevyote kwa gharama hata waliyolipa watu wengine, kitu ambacho sidhani kama ni sawa. Hawa watoto wamezaliwa wakisubiriwa na Jack kwenye chumba cha kujifungulia. Wafika hapa duniani, amewashika yeye kwanza hata kabla yangu!”

Gharama aliyowalipia Jackson hao watoto niliozaa wakizungu, wewe ulishindwa Tino. Jackson amepoteza mahusiano muhimu sana na mama yake, sababu ya hao watoto. Wapo hivyo walivyo kwa kukuzwa na mshahara wa uhasibu, tena wa serikalini, halafu wilayani Singida, sio Dar, ni Singida. Mshahara huo anaolipwa Jack ndio umewafikisha hao watoto hivyo! Watoto wawili, Tino! Jackson anawalisha na kuwavalisha kwa kamshahara kadogo anakolipwa. Hao watoto unawaona hivyo walivyo wakivutia ni kwa kulelewa na Jack. Jackson anaajira ya jumatatu mpaka ijumaa. Saa moja na nusu anatakiwa ameshatoka nyumbani. Na jioni akirudi nyumbani kutoka kwenye kazi ya uhasibu ni kazi ya watoto mpaka kuwaogesha na kulea mpaka anawaweka kitandani kipindi nipo mjamzito! Jack analea hao watoto kwa jasho lake. Kwa hali na mali bila msaada wa yeyote yule ila kabiashara tulikokaanza tena kachanga hata hakajafika umri wao hao watoto. Wanaishi kwa jasho la Jackson.”

“Wakati wewe unasoma na kutafuta leseni za kimataifa huko nje ya nchi, huyu Jackson alikuwa akibana kapesa kake, ili mimi na hawa watoto tuishi vizuri. Alichagua kufanya kile ambacho wewe ulikataa kufanya Tino! Tena kwa kunitamkia zaidi ya mara moja, ukimaanisha kabisa. Kuwa, HUNA MUDA WA FAMILIA KWA WAKATI HUO ILA MALI NA KUJITIBU. Uliniacha bila hata kujua naendeleaje, ila Jackson alinichukua akaanza kulea mimba yao hawa, nikijua ni mmoja tu. Nilichanganyikiwa nakulia, nilipojua ni mapacha, nikijua sina uwezo, na Jack ni kijana tu. Lakini huyu Jack akaniambia nimbembee tu, yeye atalea, nisiwe na wasiwasi hatashindwa kulea hawa watoto.” Sabrina akajifuta machozi.

Mama yake Jackson anadhani namloga mtoto wake, kwa mapenzi aliyonayo kwa hawa watoto! Si kawaida! Anawajali, kuliko nafsi yake mpaka mama yake anaumia. Na mimi naelewa. Jackson sio milionea. Hana biashara ya maana, hata tuliyoanza bado haitulipi kihivyo ila mwajiriwa tu, tena wa serikali. Mimi sina kazi namtegemea huyohuyo Jack! Hata mimi mtu angemfanyia hivyo huyu Brayan wangu, ningeumia.” Sabrina akajiweka sawa.

“Sijui kama unanielewa Tino? Mama yake anatafuta njia yakurudisha akili ya Jackson, ili aweze kufikiria kama hivyo wewe, Tino! Haamini kama Jack ni mzima kwa anayoyafanya kwa hawa watoto. Na hajifanyi wala kujitahidi, ni wake. Tokea wapo tumboni, Jack alikuwa akiwaambia anawasubiria kwa hamu, ila hatukujua kama watazaliwa wakizungu! Ndugu zake walimkimbia hospitalini huyu Jack baada yakuzaliwa hawa watoto wakizungu, Tino! Nikisema kikimbiwa namaanisha kukimbia kabisa, tena kwa maneno mabaya sana yakumkatisha tamaa. Lakini Jack alibaki na sisi pale hospitalini mpaka tuliporuhusiwa. Akatuchukua tena sisi wote watatu na kuturudisha nyumbani kwake ambako anatangaza ni kwetu wote.”

“Tumenunua nyumba hapa Dar, anashughulikia hati ya nyumba iwekwe jina langu kwa ajili ha hawa watoto! Jack anasema kuna leo na kesho. Hataki akija kuondoka hapa duniani hawa watoto wakapata shida, au hata baadaye wakija kukua, wapate sehemu ya kurudia. Nyumbani kwao!”

“Hapo walipo anajua wanalazwaje kitandani ili wasiumie usiku au wasihangaike. Akikohoa hata mmoja wapo hapo, Jack anajua kikohozi cha kila mmoja wao hao kwa majina kitu ambacho hata mimi mama yao mzazi sijui! Kwanza sijawahi ona umuhimu. Akikohoa hata mmoja wao hao usiku chumbani kwao au hata mchana wakiwa sehemu, Jack atakwambia ni nani anakohoa, na atamwita. Akija ni kweli ni yeye ndiye aliyekuwa akikohoa huko walipokuwa. Anaamka katikati ya usiku, tukiwa wote tumelala, kwenda kuwaangalia jinsi walivyolala. Kila siku usiku lazima awaangalie wakiwa wamelala, nakuwafunika au kuwaweka sawa. Mimi mwenyewe siwezi!”

          “Ninachotaka kukwambia Tino, huna haja yakujutia. Ni maamuzi. Na kila maamuzi yanazo gharama zake. Jack analipa gharama mpaka hivi sasa tunavyozungumza, analipa gharama yakunipokea mimi na hao watoto. Hao watoto wamemtoa Jackson kwenye familia iliyokuwa ikimpenda sana. Mama anayemjali kupita nitakavyokwambia. Jack ni wale watu wanaozungumza na mama zao hata mara tatu kwa siku. Nimemkuta Jackson hajui hata bei za nguo za ndani. Mama yake anamnunulia na kumtumia popote alipo. Lakini yote hayo ameyapoteza kwa kuwachagua hao watoto. Na kumuona leo hapa, inamaana bado amewachagua tena wao, wala sio familia yake!”

          “Tafadhali usiseme unajuta Tino, kwa kuwa ulichagua ulichonacho. Mungu amekupa, tena amekupa kwa uaminifu mkubwa sana. Una afya njema, ajira nzuri kwenye kampuni ya kimataifa, unauza picha zako kwenye soko la kimataifa! Vilevile kama ulivyoniambia huna nafasi kwa wakati ule sababu ya kutaka ulichopata! Tafadhali usikufuru! Mimi na wewe tunamlaumu Max, lakini wote tunajua Max anahusika kwa asilimia ndogo sana, kama washauri wengine wowote wale ambao tunaamua kutofuata ushauri wao. Ila tupo hapa, mimi na wewe, kwa maamuzi yetu au chaguzi zetu tulizofanya tukiwa pamoja. Wewe ulichagua ulichochagua, na mimi nikachagua nilichochagua. Mungu ameweka mkono wake kwenye kila chaguzi zetu, akatupa na watu wakusimama na sisi, sasa kwa nini tena kurudi nyuma na kuchanganya watu?”

          “Hiyo sio nia yangu Sabrina.” “Tafadhali naomba niambie nia yako, Tino. Tafadhli sana. Nia ni nini? Ni kusafisha dhamira yako au?” “Kusaidia.” “Unamsaidia nani?” Sabrina akauliza. “Watoto wawili sio kazi ndogo, Sabrina! Acha nisaidie?” “Kwa nini umchague Keiline Jackson Msindai na Jeiline Jackson Msindai na sio vituo vya watoto yatima vilivyojaa kote ulimwenguni?” Hapo Sabrina akauliza swali lakini kufikisha ujumbe. “Eti Tino? Kwa nini uchague kusaidia watoto wa familia yetu?”  Kimya, macho mekundu haswa.

          “Najua hili usingependa kulisikia Tino, lakini watoto ulioacha kwangu, TULIUA Moshi na ushahidi wote wa tulichofanya pale kwenye ile hospitali inayoua watoto upo na Jackson. Anao.” “Naomba usiseme hivyo Sabrina.” “Sina jinsi nyingine rahisi ya kukwambia Tino, ukaelewa, na kuendelea na sisi kuanzia hapa, usipokuwa na uelewa huo. Ukielewa hivyo, nahisi  mbeleni mnaweza mkakutana na Jack, angalau mkaelewana. Lakini si kwa uelewa mwingine wowote ule.” “Nipeni hata masharti.” “Nilikwambia, leo Jack hayupo vizuri. Jibu lolote atakalokujibu leo, hutalipenda. Tafadhali mwache. Shukuru muda uliopata nao, basi kwa sasa itoshe tu.” “Haiwezi kuwa basi Sabrina! Tafadhali nisaidie.” “Sawa Tino. Ila kumbuka na hili, nimekuonya. Jack amepoteza mambo na vitu vingi sana sababu ya hao watoto.” “Mimi sitaki ugomvi ila naomba.”

          “Kama mimi nimemuelewa Sabrina. Labda niingilie na kukusaidia Tino.” Wote wakamgeukia baba yake Sabrina aliyekuwa amekaa kimya sebuleni akisikiliza muda wote. “Kwamba kwa sasa, itoshe tu. Acha mpaka wakati mwingine tena. Na yapo madhara ya kulazimishia mambo kwa wakati usiofaa. Nashauri utulie.” “Naondoka kesho mzee wangu. Sijui nampataje Sabrina!” “Na kwa sababu yeyote ile, hata kwa kukosea Tino, usiwasiliane na mke wangu.” Jack akatoka chumbani na hilo onyo.

Sikutishi, ila nakuonya ili usije kulaumu baadaye. Hiki nilichokikuta hapa kwa mke na watoto wangu, ni mara ya kwanza na HAITAKAA ikatokea tena. Kumtafuta Sabrina kwa kutumia yeyote yule kwenye familia yao, mkawasiliana nyinyi wawili au kupitia mtu yeyote kwenye familia yao kwa sababu yeyote ile, huko nikunitangazia vita mbaya sana. Na sitakubali kushindwa.” Sabrina kimya, ameinama akijua na yeye anafikishiwa ujumbe wake.

          “Sabrina ni mke wangu wa ndoa ya kanisani na nililipa mahari kabisa kwamba hakuna mwanaume mwingine atasogelea nyumbani kwao tena juu ya Sabrina, mimi nilifunga hiyo biashara tena kwa heshima zote na ushahidi upo wa kukabidhiwa Sabrina kihalali na wazazi wake au ukoo wao wote waliridhia mimi Jackson Msindai, kumchukua Sabrina mpaka kifo.” Na baba yake Sabrina akafikishiwa ujumbe wake. Kimya yeye na binti yake waliompokea Tino kinyume cha Jackson Msindai.

Ulimuacha vibaya sana Sabrina, nilimkuta mpweke na amejawa hofu pamoja na majuto. Tumejenga familia yetu kitu ambacho hukutaka. Acha kuchanganya watu!” Jackson akasogea karibu.

“Nilikwambia Tino, na ninarudia. Litakapofika swala la familia yangu, nitanguruma, hakuna mwenye sikio akaweza kunisikiliza. Nampenda mke wangu, napenda watoto wangu. Nywele zao na hiyo rangi waliyobeba, isikuchanganye hata kidogo. Hawa mabinti wawili ni kina Msindai kama Brayan. Na kukusaidia tu, SIJASHINDWA kutunza familia yangu, kwa hiyo tunza pesa yako.” “Sitaki kukuudhi Jack. Nakushukuru kwa kila kitu.”  Unanishukuru kwa lipi NILILOKUTENDEA?!” Jack akawa mkali haswa mpaka sauti ilisikika ni ya ukali.

“Sikujui, hunijui. SINA chako. Sijakusaidia chochote kile. Mimi naendesha familia yangu! Nilimuonya Max asimsogelee mke wangu, hakunisikiliza. Unajua kilichompata Max?” Sabrina kimya. “Naomba tusifikishane huko Jack. Na samahani kama nimekuudhi. Naona kweli niondoke. Samahanini sana.” “One Man’s Trash, is another Man’s Treasure. Uliona ni takataka yakutupa, ukatupa. Mimi nikachukua akiwa yupo peke yake, Moshi. Peke yake hakuna hata anayemjulia hali Sabrina! Nilimkuta mpweke kama yatima jangwani! Sasa hivi unaona vinang’aa, vinapendeza, ndio unarudi kinyumenyume kuleta vurugu? Ulikuwa wapi siku zote hizo? Unamdanganya Sabrina unaumia? Kwa lipi!?” “Naomba niondoke jamani. Samahanini sana.” “Na usiwahi kusahau, macho yaliyokuwa yakimtizama Max, mpaka kumtia nguvuni, sasahivi yamehamishwa kwako wewe, Tino. Usinijaribu tena. Hii iwe mara yako ya mwisho.” "Najua na ndio maana unaona nimefuata kila sharti la Sabrina. Nimekuwa nikirudisha watoto kwa wakati aliotaka yeye Sabrina." Tino akajaribu kujitetea asijue anazidi kumuudhi Jack.

"Tino nakuonya wewe! Hakika NAKUONYA. Na leo hata Sabrina atakua shahidi wa hili. Hata kwa kushawishiwa na Sabrina mwenyewe, huruhusiwi kugusa binti zangu kwa kuwa wewe ni muuwaji na ushahidi ninao. Nikianzana na wewe kisheria, adhabu utakayohukumiwa wewe, kwa huruma sana ni kifungo cha maisha kama si kunyongwa. Tafadhali waambie ukweli hao wanao kusogeza karibu na binti zangu. Waambie ulikusudia kuwauwa, ila Mungu akawalinda. Uliwafikisha mpaka kwenye kifo, na ukaridhika kuwa wamekufa. Nakuonya, na onya wanaokusaidia kukusogeza kwa binti zangu." Tino akaondoka kwa haraka. Jack akarudi chumbani, Sabrina jikoni. Baba yake Sabrina na yeye akapokea ujumbe wake na familia yake wote. Jack aliwasema kwa heshima na mafumbo lakini alielewa na Jack akajua atafikishia wengine ujumbe. Maana ni kweli walimtelekeza Sabrina. Jackson anamfuata Sabrina, Moshi, hakuwa hata na mawasiliano na ndugu zake hata mmoja! Leo wanakusanyika hapo chini ya Tino! Jack alikasirika sana. Pakazuka ukimya mkubwa haswa hapo ndani, hata tv haikuwashwa.

~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment