Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 54. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 54.

Jack aliachiwa nyumba na mshahara aliokuwa akilalamikia mama yake kuwa Sabrina na wanae wanamaliza. Miradi yote pamoja na biashara waliyokuwa wakifanya na Sabrina ambayo nayo iliwaongezea kipato, vyote vilikuwa hapo, Jack akifanya na kuona vyote havina maana tena. Tumaini la kuja kugombea tena na kushinda vikamuishia kabisa, ikawa kama ameingiwa hofu ya kujaribu tena. Kwanza hata kwenda chamani ikawa ni jambo la kujikaza jinsi alivyokuwa amechafuliwa kwa shutuma zinazofanana na ukweli. Ujasiri ukamuisha kabisa hata kuongoza ikawa ni jambo la hofu, anaona watu hawawezi kumsikiliza tena jinsi mwenzie alivyokuwa amejaa na kustawi kwenye mafanikio yake na Sabrina ambaye ni kama alikimbia miradi michanga kabisa iiyokuwa ikihitaji usimamizi, wakaishia kuiacha, mwenzao akafika hapo na ujasiri na kutawala kana kwamba alikuwepo kwenye msingi wa hiyo miradi. Jackson alipoa, usingeweza kuona tabasamu usoni mwake. Maswali ya mke na watoto walipo, likawa jambo la kumuondoa katika kila mazungumzo.

Hakuacha kumtumia ujumbe Sabrina kila siku asubuhi kumjulia hali yake na watoto. Na kila siku ikawa kazi ya kuangalia hizo jumbe kama zimefika. Juma la pili lilipoisha akaongeza ujumbe wa usiku. Kumtakia usiku mwema yeye na watoto. Nia ni kupata kitu cha kuangalia kwenye simu yake, na sababu ya kujua kama Sabrina amefungua simu yake. Akaendelea kusubiria mchana na usiku bila kuona kama jumbe zake zimefika.

Zilipita siku 21 bila mawasiliano kati yake, Sabrina, mama yake wala ndugu zake. Kukawa kimya kabisa, ila baba yake hakuacha kumpigia kumjulia hali. Angalau mara moja kwa juma na hawakuwa watu wa mazungumzo marefu, ila salamu tu.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku moja usiku akiwa ametoka kuoga, akasikia ujumbe umeingia. Akakimbilia simu akiwa na taulo tu. ‘Sisi tunaendelea vizuri, namshukuru Mungu. Naulizia kama Singida kuna mtu. Naona nguo za kaka nilizokuwa nazo zimeanza kuwa ndogo. Sasa kabla ya kufanya manunuzi mapya, nilitaka kujua kama naweza kupata nguo zake na za dada zake. Ikishindikana, hamna shida. Nitafanya manunuzi mengine.’ Jack alisoma na kukaa kitandani. Zilishapita siku 25 tokea amuone Sabrina. Nyumba ilijaa vitu vya familia, lakini alikuwa peke yake.

Akampigia lakini hakupokea ila akamtumia ujumbe. ‘Kaka na dada zake wamelala. Siwezi kuongea. Tafadhali nijulishe kwa ujumbe tu.’ Jack akasoma na kupiga tena na tena lakini haikupokelewa. ‘Naomba pokea simu, Brina.’ ‘Sio lazima Jack. Nitanunua upya. Usiku mwema.’ ‘Tafadhali toka hata nje tuzungumze.’ Jack akaona amemtumia tena ujumbe wa pili. Kaka na dada zake wamelala. Siwezi kuongea. Tafadhali nijulishe kwa ujumbe tu.’ ‘Nilisoma huo ujumbe, Brina. Naomba tuzungumze.’ Hakupata ujumbe mwingine ikawa kimya. Akapiga tena, simu haikuwa hewani.

Jack akasubiria kuona kama atapigiwa tena, ikawa kimya. Kesho yake asubuhi akatumia akili akamtumia ujumbe. ‘Ulitaka kupataje hivyo vitu? Mimi nipo Singida ila ijumaa nitakuwa Dar. Unataka kuvipata kabla au unaweza kusubiri nikaja navyo Dar? Na kama kuna vitu vingine ungehitaji, niandikie, niviweke pamoja.’  Huo ujumbe haukuonyesha kufika mpaka usiku akapata majibu. ‘Nashukuru. Ni vya watoto tu. Wanakuwa kwa haraka vikikaa muda mrefu vinaweza visiwafae tena.’ ‘Nivilete wapi?’ Jack akauliza kwa haraka. ‘Kwa Pendo tafadhali. Nitavifuata kwake.’ ‘Nimwambie lini utavifuata?’ ‘Nitazungumza naye. Sina uhakika. Pengine ijumaa au jumamosi.’ ‘Sawa. nisalimie wanangu.’ Kimya na ujumbe haukufika. Akajua ameshazima simu, ila furaha aliyokuwa nayo, akajiambia hataondoka nyumbani kwa Pendo mpaka amuone Sabrina.

Atafutaye, Hachoki.

J

ack aliondoka asubuhi siku ya ijumaa kuelekea Dar, na basi tu akiwa na mabegi kadhaa yaliyojaa nguo za watoto wake. Akatua jijini Willy akaenda kumpokea kituo cha mabasi, jioni hiyo. Walijua atakuwepo nyumbani kwao. “Vipi maisha ya ubachela?” “Naomba usinidhihaki Willy.” Willy akaanza kucheka. “Mbona hasira Jack na haupo hapo kwa bahati mbaya ila maamuzi tu!?” Jack hakumjibu hilo ila kuuliza jingine. “Sabrina amefika leo pale kwa Pendo?” “Mimi nimetokea kazini ndio nimekupitia hapa kituo cha mabasi. Kwa hiyo sijui.” “Kwani hujazungumza na Pendo?” “Mpaka muda mfupi niliotoka kuzungumza na Pendo, na yeye hajamuona wala kumsikia Sabrina kama mimi tu, tokea siku ile ya harusi akimwambia anakwenda kupumzika kwa muda, anamuombea, na atamtafuta mapumziko yakiisha. Basi.” Jack akanyamaza.

Walifika nyumbani kwa Pendo wakamkuta amejilaza chumbani kwake. Willy akamsaidia Jack kuingiza mizigo yake mpaka kwenye chumba alichokuwa akilala Sabrina na  wanae. Wakati wapo humo ndani ya hicho chumba wakamsikia Pendo akicheka mlangoni. “Hiki chumba nacho kinakaribia kuitwa mtakuja.” Jack akamgeukia vizuri. “Umezungumza na Sabrina?” Jack akauliza. “Sabrina alilala chumba hikihiki karibia siku 5 wewe ukiwa kwenu hata kumtumia ujumbe wakumjulia hali ukaona shida, sasa hivi unataka kusumbua tu watu. Chakula kipo mezani. Nenda kale. Twende zetu Willy.” “Na mimi nilikuwa nimemkasirikia Sabrina kwa kujua amenigeuka bila kujua ukweli.” Akajitetea Jack.

“Wewe mwanaume gani, au baba gani unanuna kama toto dogo na kuzira mpaka watoto! Hiyo ni akili kweli au ujinga huo?” Pendo akamuuliza. “Mama yako anammalizia hasira Sabrina kwa watu kumsusia shower, kwa kushindwa kwake mwenyewe! Halafu anamsingizia Sabrina kumbe hata mgeni rasmi aliyetaka awepo siku ya shughuli alighairi, halafu eti anasingizia babyshower haikufanyika sababu ya Sabrina!” “Sijaelewa Pendo.” “Ndio utajijua mwenyewe wewe usiyetaka kutumia akili ila hisia.” Pendo akaondoka, Jack akamkimbilia.

“Nini wewe?” “Umezungumza na Sabrina lini?” “Leo. Na kesho mida ya saa nne anakuja hapa kuchukua mizigo yake. Tulia.” “Nampenda Sabrina.” “Basi vitendo vyako vinazungumza tofauti.” Pendo akamjibu na kugeuka. “Kwa hiyo wewe unapenda mimi nikiachana na Sabrina?” Pendo akamgeukia na kumwangalia kwa sekunde kadhaa, akaondoka zake akijisukuma na tumbo lake bila ya kumjibu

Mtakuja...

Siku Inayofuata.

K

wenye majira ya saa tatu na nusu wala si saa nne Sabrina akawa anaingia hapo getini kwa Pendo. Sifa akafurahi kumuona. “Umependeza dada! Hizo nywele umesuka si itakua garama sana?” “Na muda mrefu haswa. Kwa hiyo kama umezipenda ujiandae kukaa chini.” “Mmmh! Itakua mihela mingi. Akuu!” Sabrina akamcheka Sifa jinsi alivyojilalamisha. “Nimemsikia dada akizungumza chumbani, atakua ameshaamka, ngoja nimuite.” “Sasa na wewe unamwagilia maua jua lishatoka!?” Sifa akachekaa. “Leo nimepitiwa na usingizi. Nikupokee mtoto?” “Mwache tu, alichomwa sindano jana, naona hajisikii vizuri. Acha tuendelee kupendana tu.” Sifa akaingia ndani na kibegi cha mtoto na pochi aliyompokea Sabrina, akaenda kumgongea Pendo, akatoka kwa haraka.

“Mama huko ulikojificha naona kumekupenda! Umependeza Sabrina!” “Asante dada. Ninapumzika vizuri, halafu huyu kaka mpole, kwa hiyo uzazi mzuri. Nakula vizuri, napumzika vyakutosha. Naona na wewe unazidi kuongezeka!” Wakacheka wawili hao kwa furaha. “Ndoa tamu.” Wakaendelea kucheka. “Kabla sijakaa, niambie mizigo yangu kama ililetwa? Maana nguo za huyu kaka sikuwa nazo nyingi, na hata nilizoziacha Singida nahisi ni kubwa, maana bibi yake aliniambia nisinunue nguo, yeye atanunua. Nikaanza kununua za miezi minne kwenda juu tena kwa hamu tu. Sasa siku ile nilipowaacha kwenye tafrija yako, nikasema nisifanye haraka, nikakosa mengi. Nikamtumia ujumbe mama Msindai kumuuliza kama hiyo shower bado ipo, kimya.” “Haiwezekani Sabrina?!” Pendo akashangaa sana.

“Kwamba huamini kama nilimtumia ujumbe? Tena nilipoona kimya nikampigia kabisa ila hakupokea.” “Sabrina wewe!? Na maneno yote yale machafu aliyokutupia na kukuzulia bado ulimtafuta?” “Mimi ndiye mbaya wake lakini si mjukuu wake dada. Lakini nilipoona hajanipokea simu yangu wala kujibu ujumbe tena, nikaona nitulie tu. Nikajua na yeye amesusa mtoto kama mwanae. Nimenunua nguo baadhi, lakini naona nahitaji zaidi. Ndio nimeomba zile za Singida ziletwe nichambue. Nikikosa, nimnunulie nyingine.” “Mmmh! Sabrina wewe una moyo wa ajabu! Mimi nisingeweza.” “Nafanyaje dada, si mtoto wangu peke yangu. Lakini kama hivi wamemsusa, basi. Nalea mwenyewe na Mungu wangu hajaniacha wala kunipungukia.” “Nakuona ulivyopendeza.” Wakacheka kwa kushangilia.

“Mama, umependeza haswa! Naona na mwili safari hii umekubali.”  Wakacheka zaidi. “Nashukuru dada yangu lakini kwa uzazi wa wale mapacha nao ilikuwa hivihivi. Mwili ulikuja, wakati nashangilia kunenepa, ukanywea wote. Hapa nahesabu tu siku.” “Wakati ule ulikuwa mzazi na hekaheka za huko Singida. Safari hii huna la kukuzungusha, mwili na wenyewe utabaki tu.” “Na kweli dada. Nahisi safari hii Mungu ameamua kunipumzisha kitajiri haswa!” Wakacheka tena na kugonga kwa ushindi. Willy akatoka chumbani. “Mzima Sabrina?” “Mimi mzima Willy, namshukuru Mungu. Vipi honeymoon imeisha?” “Haiishi.” Willy akajibu na kumfanya Sabrina na Pendo kucheka zaidi.

“Warembo wako wapi?” “Wapo na Tino. Leo ameomba ashinde nao, maana kesho anaondoka. Ndio na bibi yao amepata nafasi ya kwenda saluni, na mimi wamenishusha hapa, ndio maana nimewahi mapema, nimeomba lifti wanilete hapa. Naamini sijawaamsha au kusumbua.” “Hata kidogo. Karibu.” “Subiri kwanza Sabrina. Tino, Tino?” “Huyohuyo dada, mwingine nani? Kajirudi na msamaha mpaka kwa wazazi ameomba msamaha, nikajiambia kwanza mimi mwenyewe mkosaji namba moja na wakati wote Mungu amekua akinisamehe. Amekua akinifutia midhambi yangu na kunirehemu. Nawezaje kubakia na Tino moyoni nikimchukia na kweli wanae ninao! Nikamwambia Mungu yeye ndio ashugulike naye, mimi nimtue tu, nimalize kinyongo naye kwanza hata jinsi ya kupata hao watoto wote tulikuwa tukimkosea Mungu, lakini amenirehemu. Wale watoto hawajawahi hata kuugua wakanywa dawa! Wazima. Sasa huyo si Mungu tu.” “Kweli mwaya.” Pendo akaafiki.

“Halafu dada, watoto wenyewe wanakataliwa huko kwengine, na kufukuzwa waziwazi, hawatakiwi! Nawezaje kuwang’ang’ania mimi mwenyewe, nitaweza wapi dada? Kuna leo na kesho. Siku chache zilizopita hapa ilionekana waziwazi, nikaachwa hapa, kila mtu akashuhudia. Sasa nijidai kichwa ngumu, nimeachwa peke yangu, nafanyaje?” “Lakini kweli mwaya.” Pendo akaendelea kuafiki.

“Najua leo mnapumzika, wala sitaki kumpunja Willy kwa kuchukua muda wenu. Mimi nitarudi jumatatu dada, wakati Willy yupo kazini, tuzungumze vizuri. Nipe mizigo yangu niondoke.” “Jack yupo.” Sabrina akanyamaza. “Alikuja jana usiku.” Kimya, na Willy kimya. “Sabrina?” “Hata sijui dada!” Kisha akamgeukia Willy. “Samahani Willy, naomba mwambie Jack nimekuja kuchukua mizigo kama alifanikiwa kuja nayo, mimi niondoke, mtoto akapumzike.” “Mzima lakini?” “Mzima. Ila jana tulimpeleka kupata sindano ya chango, naona ndiyo ilimpa homa kidogo, ndio maana unaona tumekumbatiana hivi.” Wakamchungulia, alikuwa amelala kifuani kwa mama yake amebebwa, kwa kufungwa mbeleko maalumu ya kubebea, ila amemuweka kwa mbele. “Mwanangu huyu si mlizi. Akilia ujue kuna jambo. Usiku hakulala vizuri, na vilio vya hapa na pale, na ameamka akilia kidogo ndio maana unaona tupo kwenye kupendana hapa.”

“Sasa hivi anayo homa?” Akatoka Jack na hilo swali, Sabrina akajua alikuwa akisikiliza. “Nampa dawa kila baada ya masaa 8 ili kufanya isipande tena.” Akajibu Sabrina macho kwa mwanae wala si Jack ambaye hakuwa amemuona kwa muda mrefu. “Amekua!” Pendo akasifia huku akimchungulia pale alipofungwa kifuani na mama yake. “Hana utani na chakula huyu. Ni mlaji mzuri sana na mlalaji, ndio maana bibi yake anasema anakuwa na mwili.” Jack akasogea mpaka pale alipokaa Pendo na Sabrina aliyekuwa amempakata huyo mtoto lakini bado amemfunga na mbeleko hapo kifuani kwake.

“Kweli amekua.” Jack akataka kumchukua. 

“Nashauri ungemuacha kwa sasa. Analialia na si kawaida yake. Hajatulia vizuri. Hapo amepitiwa na usingizi muda si mrefu ndio maana unaona nasita hata kumtoa hapo kifuani.”  “Nina hamu naye, acha nikupokee tu, akilia nitambembeleza.” Sabrina akafungua ile mbeleko, akamkabidhi. “Basi wakati wewe umemshika, acha mimi nikangalie nguo zake. Kubwa nitaziacha hapahapa kwa dada, nitakuja kuchukua wakati mwingine.” Sabrina akaelekea kwenye chumba alichojua Jack ndipo alipopewa hifadhi.

Jack akamfuata nyuma. “Swala la Ubunge binafsi sikujua kama kulikuwa na hila nyuma yake, Brina.” Akaanza Jack akimfuata Sabrina nyuma, wala hakugeuka. “Mama alinishauri kwa hekima kwamba nisikwambie ili nisikuvunje moyo kwa juhudi unazoweka kule Singida. Niingie kwenye kinyang’anyiro tu. Nikishinda ndipo nikwambie ili tuwe na chaguzi mbili.” “Begi lipi ndilo lenye nguo za watoto?” Sabrina akamuuliza. “Jeusi.” Akajibu Jack na kuendelea.

“Yaani mimi siku ile pale hospitalini sikujua kama yalishasemwa maneno mabaya, na mama hataki watoto wafike nyumbani kwake, ndio maana na mimi nikakasirika kuona unanibadilikia kwa hasira kiasi kile na hutaki kunisikiliza, wakati mimi najua mama aliweka mipango mikubwa kwenye shower yake huyu, bila kujua kumbe na wageni wenyewe walishatoa udhuru. Kwamba hata shower yenyewe isingefanyika hata kama ungekuwepo au pengine ingekuwa ni watu tu wa familia, asiniambie hivyo. Akabaki kusema wewe ndio umesababisha isifanyike.” Sabrina kimya. Akiendelea na alichokuwa kifanya.

“Unanisikiliza Sabrina?” “Ulichukua nguo zote za Brayan, sehemu zote nilizokuelekeza?” Sabrina akamuuliza na yeye. “Kwani tunahamia huku Dar?” Sabrina akasimama na kumwangalia vizuri. “Nilikuelekeza sehemu zote nilizoweka nguo za mtoto, Jackson. Ulichukua?” “Ukiniita hivyo jina langu lote najua umenikasirikia. Unakuwa kama unanisomea hukumu. Najua.” “Umechukua nguo zote au umeacha?” “Nimeacha nyingine nikijua tunarudi.” “Sasa zile ulizoziacha ndio za muhimu zaidi, maana hizi ulizoleta ni za umri mkubwa. Sizihitaji.” “Kwani tunarudi lini nyumbani kwetu?” Jack akauliza.

“Sijui wewe, lakini mimi, nikizungumzia mimi nawakilisha...” “Watu watatu. Najua.” “Hapana. Watu wanne.” Sabrina akamrekebisha. “Tupo mapumzikoni.” Sabrina akamalizia. “Mapumziko yetu yanaisha lini?” Jack akauliza swali akijiongeza na yeye. “Yetu sisi ni kwa mwezi mzima, yakiisha hayo ndipo nitajua chakufanya. Sijui wewe!” “Kwa maana nyingine umebakiza siku kama 6 tu umalize hayo mapumziko. Na mimi nakusubiria hapahapa Dar, yakiisha hayo mapumziko ndipo tujue chakufanya pamoja. Kama tunabaki wote hapa Dar, au tunarudi Singida.” Akamuona anarudisha nguo kwenye begi alilokuja nalo mpaka akamaliza.

“Haya namuomba mtoto, sisi tuondoke, nikamnunulie nguo.” “Tunaondoka wote Sabrina. Tukapumzike wote mpaka huo mwezi ukiisha ndipo tujipange tena upya lakini nilitaka unisikilize.” “Nikwambie ukweli Jack, sina shida yakujua mipango yako na mama yako. Hainihusu hata kidogo. Sijui kama unanielewa?” “Nilitaka kukwambia kilichotokea!” “Sihitaji Jackson. Tafadhali mimi naomba mtoto niondoke. Acha kunipotezea muda na kutaka kunichanganya. Nina vichwa vitatu vinanitegemea mimi, kila siku wanayopewa na Mungu. Mimi nikiyumba tu, na kumuongeza na mama yako kwenye mipango yangu, tutajikuta wote tunakwama tukisubiria amri kutoka kwa mama yako. Mimi sina huo muda. Mpo watoto wanne kwa mama yenu, nafikiri mnatosha kumsikiliza na kufuata hekima zake. Naomba na mimi usiniingize huko tafadhali. Sitaki na sitafanya hivyo. Au niseme sitakuruhusu. Namuomba mtoto.”

“Basi tuendelee na mipango yetu. Mimi na wewe na familia yetu.” “Jackson Msindai, acha kunipotezea muda na kuniyumbisha tafadhali. Kama unataka kubakia na mtoto, sawa. Nakuachia ila ujue bado ananyonya na sijatembea na maziwa yake. Sasa je, nikuachie mtoto au unanipa mimi niondoke hapa? Siku ya leo ni ya Pendo na mumewe, wenzetu bado wapo honeymoon. Naomba usiniharibie ratiba yangu. Nishamwambia dada Pendo leo nakuja kuchukua tu mizigo, sitakaa.” “Basi nisubiri tuondoke wote.”

“Unakwenda wapi!?” “Huko kwenye mapumziko.” “Hapana, huwezi. Kwa sababu kama ileile iliyokushinda kuwepo hapa kipindi natoka hospitalini.” “Pale nilikuwa...” “Naishi kwenye villa ya vyumba viwili tu. Chumba kimoja natumia mimi na watoto wangu wote, na kingine nilimuomba baba aje akae na mama, ili mama atulie, anisaidie kulea watoto. Sina nafasi ya kukuweka.” “Nitalala kwenye makochi.” “Hapana Jackson. Hapa nako kulikuwa na makochi lakini ulishindwa kulala. Acha kuwa myumbaji.” “Basi naenda kukodi Villa ya vyumba vitatu, wote tuhamie hapohapo.” “Sina sababu yakuhama mimi. Sitahama.” “Basi twende wote, nikakodi Villa yangu ya peke yangu, ila karibu na nyinyi. Au hutaki Tino akatuona tupo pamoja? Ulimwambia nimekuacha ili mrudiane?” Sabrina akamwangalia na kuchoka kabisa.

“Maana naona unanikwepa, na maisha yako sasahivi ni Tino tu. Sasa mimi sijasema nataka nikaishi na wewe pamoja na huyo Tino. Nachukua Villa ya pembeni yenu ambapo sipafahamu. Ninachokuomba ni unifikishe mpaka hapo mnapoishi na mimi nikakodi Villa yangu. Nalo hilo pia hutaki?” “Basi naomba ufanye haraka, tuondoke.” “Sawa. Umekula lakini?” “Ndiyo.” “Basi nisubiri nikusanye vitu, tuondoke.” Akamkabidhi Sabrina mtoto pale alipokuwa amekaa, akaanza kukusanya vitu vyake.

“Mimi nipo tayari, sijui tunaondokaje hapa?” “Mimi, nilimuomba Tino asiwe mbali na hapa ili nikichukua vitu, anisaidie kunirudisha.” “HATUTAONDOKA na Tino hapa.” Jack akaongea kwa sauti ya juu kwa hasira. “Sawa.” Sabrina akabaki akimwangalia. Akaonekana akifikiria kidogo, kisha akatoka. “Willy!” Akamsikia akiita. Willy akaitika. “Naomba nisaidie tena usafiri.” “Wewe ni msumbufu Jack. Mimi naomba Sabrina uchukue gari yangu, atumie akiwa hapa mjini na watoto. Nitazungumza naye mwenyewe juu ya kurudisha.” Pendo akajibu kabla ya Willy. “Asante Pendo.” “Sitaki Jack. Na sijakupa wewe gari, ni Sabrina.” Jack akarudi chumbani alipokuwa amemuacha Sabrina na mtoto.

“Tumepata usafiri.” “Sawa.” Jack akaanza kubeba mabegi yote. “Mimi naomba mizigo uliyonijia nayo hapa Dar niiache hapa kwa dada Pendo. Sina nafasi yakujaza mizigo nisiyotumia.” “Nitaiweka kwenye Villa nitakayokodi mimi, au umesahau siku hizi tuna mahela yakuishi kwenye Villa mbili hapa mjini? Bado nyumba tuliyonunua ya hapa Dar inatusubiri na Singida pia?” Akamuuliza kwa kejeli akiwa amekasirika. “Sawa Jack. Wewe beba mizigo unayotaka.” “Nabeba yote.” Sabrina akatoka na kurudi sebuleni alipokuwa amekaa Pendo  na Willy.

“Dada, acha sisi twende, nikajaribu kumlaza huyu kaka, nitakuja jumatatu.” “Basi nitakusindikiza na madukani, usiende peke yako.” Wakaanza kucheka. “Mimi mwenyewe nilikuwa na hamu na wewe dada yangu. Nitakuja kukufuata basi jumatatu.” “Hayo ndio maneno.” Sabrina akatoka, Pendo akimsindikiza. Jack akarudi ndani kumuaga Willy, kisha akatoka kumfuata Pendo na Sabrina ambao walishafika garini. “Kapumzike dada. Tutaongea zaidi jumatatu Mungu akipenda.” “Sawa.” Pendo akarudi ndani.

“Tunaelekea wapi?” Sabrina akamuelekeza. “Unanitania au kweli!?” “Ndipo ninapoishi. Nilitaka kupumzika.” Jack akamwangalia na kuendelea kuendesha mpaka kwenye hizo Villa. “Kweli wewe unayo pesa! Au ndio mambo ya Tino haya?” “Naomba unisikilize Jack. Nimetaka mapumziko ya mwezi tu katika maisha yangu. Mbali na kelele pamoja na masimango. Nimebakiza siku chache sana, unafikiri unaweza kusubiri au mimi na watoto tuondoke tena?” “Hata maswali ya kawaida...” “Naomba uyatunze utakuja kunihoji wakati mwingine isiwe sasa.” Jack akatulia.

“Na kukusaidia tu, ofisi za wanapokodisha hizi Villa, tumeziacha kule getini, upande wa kushoto. Naomba unishushe mimi na mtoto karibu na mlango, nikambembeleze nione kama atalala, wakati wewe ukishughulikia Villa yako.” “Mimi sidhani kama nitapamudu hapa. Na hivi nitakaa hapa bila likizo ya kazini, naweza nikajikuta nafukuzwa kazi. Kwa hiyo twende tu hapo kwenu, nitalala hata jikoni.” Sabrina hakumjibu. Alitegemea yote hayo. Akamuelekeza mpaka kwenye kinyumba wanachoishi.

“Ndio mnalipia kiasi gani hapa?” “Wewe ni msumbufu bwana Jack! Ni kwa nini huwezi kuwa msikivu?” “Hata swali kama hilo nilakutunza!?” “Nenda ofisini ukaulize.” Jack akanyamaza. Wakafika, Sabrina akashuka na mtoto hata pochi hakuchukua. “Karibu.” “Sasa mbona ukaribisho wenyewe ni kama hujafurahia?” “Nazungumza kwa sauti ya chini sababu ya mtoto Jack! Acha kulalamika kama mtoto mdogo bwana! Karibu.” “Sasa mizigo yangu ndio niweke wapi?” “Popote unapotaka wewe.” “Chumba chetu na watoto ni kipi? Nisije nikaweka chumbani kwa wakwe.” “Jikoni ni pale ndani.” Jack akaanza kucheka.

“Kweli sitakiwi humu ndani!” “Si ulisema mwenyewe!” “Ni kiuungwana tu! Hapo ulitakiwa wewe uniambie, ‘hapana mume wangu, tutajibana tu na watoto’! Mapenzi yote yale yamekwenda wapi Brina wangu?” “Naomba punguza kelele, Jack. Huyu mtoto hajalala vizuri usiku.” “Sawa. Kwa hiyo akilala ndio tutapata muda wetu?” Sabrina hakumjibu akapitiliza chumbani.

          Akaingiza mizigo yote hapo chumbani, Sabrina kimya akibembeleza mtoto. “Nimekumiss Sabrina.” “Acha kelele Jack, bwana!” “Mbona sasa hata mtoto mwenyewe unayembembeleza ameshalala! Pata muda na mimi Sabrina! Hujui hata nilikuwa naendeleaje! Nilikuwa na hali gani! Kwa nini mimi hunijali tena?” “Najuta kukutafuta Jackson Msindai jamani! Heri ningemaliza likizo yangu ndio nikakutafuta jamani!” “Nijali hata kidogo tu!” “Unaendeleaje Jackson?” “Usiniite hivyo. Niite vile vizuri kwa upendo.” “Basi nenda kasubiri hapo sebuleni, mimi nimlaze mtoto.” “Kwa hiyo unakuja tupate muda wetu kama familia?” “Naomba toka Jack.” “Ukichelewa mimi narudi. Maana nahisi nimeshasahauliwa. Sijaliwi tena!” Akakaa.

          “Kweli karibu mwezi mzima hujui nilipo wala nakula nini, Brina jamani! Maisha yangu yamekuwa mabaya. Naishi peke yangu kwa kosa dogo tu. Mimi nilikasirika nikaenda kulala kwa mama, lakini nilikuja kukuangalia. Ila nikasafiri. Mimi hunipendi Brina. Sio kama mimi ninavyokupenda. Siwezi kuishi bila wewe, hata nikiwa nimekasirika, nataka niwe na wewe tu. Hata ukinitendea jambo baya la namna gani, mimi nakutaka tu wewe. Mimi sio kama wewe Brina. Siwezi kuku block kwa kuwa nataka kukusikia tu wewe. Mimi nakupenda wewe kuliko mtu mwingine yeyote hapa duniani. Lakini wewe hunipendi Brina.” Sabrina akabaki akimtizama tu, na mtoto mkononi.

“Unaweza kulala bila kujua kama mimi ni mzima au la! Nimekula au la! Maisha...” “Naomba ukanisubiri hapo sebuleni, ili umalizie malalamiko yako Jack. Acha nimlaze mtoto kukiwa kimya ili asiamke wakati namuweka chini.” “Na mimi nataka kujaliwa. Unanipuuza Brina.” “Haya nenda, nakuja kukusikiliza.” Akatoka na kurudi. “Hivi hata ulishakuwa na wasiwasi kujua mimi naendeleaje  au niko wapi?” “Nilikuacha mikononi salama kwa mama yako, Jack. Naomba tulia kule kwenye makochi.” Hapo akapoa kidogo akatoka, lakini akamsikia akiendelea kulalamika kwa sauti ya chini kama mtoto mdogo. Sabrina alimjua Jack, akajua ameongeza mtoto mwingine hapo kwenye Villa.

“Maisha yangu yamebadilika kabisa, nimekuwa kama sijao sababu ya kosa la kutaka maendeleo!” Sabrina akatoka na kufunga mlango wa chumbani. “Mimi ningefanikiwa, ungefurahi Sabrina.” “Nani alikwambia sikuwa na furaha?” “Namaanisha zaidi.” Sabrina akamwangalia na kurudisha macho kwenye simu. Akapiga. “Sasa mbona mimi hunisikilizi tena!?” “Nampigia simu Tino, kumruhusu aende atakako, asibakie maeneo yale akidhani bado nahitaji...” Wakati akimjibu Jack huku kwenye simu Tino akapokea.

“Halow!”  Akamsikia Tino. “Mimi nilishatoka maeneo ya huko, Tino. Wewe kuwa huru kwenda utakako. Nilipata usafiri.” “Sijui kwa nini! Jeiline amelala kabisa! Mpaka naona shida kumwamsha.” “Jana alikaa ndani ya maji muda mrefu sana. Atakuwa amechoka. Nashauri uwarudishe tu.” “Nikiwarudisha sasa hivi, utanipa tena jioni tukaangalie movie?” “Baba yao yupo hapa, Tino. Sijui atasemaje tena!” Tino akanyamaza na kushindwa chakujibu. Lakini Jack akafurahi sana.

“Mimi nashauri uwarudishe kwa sasa, halafu tujipange tena.” “Hata hivyo nakushukuru sana, Sabrina. Asante. Nahisi sababu ya furaha ya kuwa nao, nilikosa kuwa na kiasi kwao, nikawashindisha majini kwa muda mrefu.” “Na wenyewe wanapenda maji, ila wamelemewa.” “Basi tunarudi.” “Sawa.” Sabrina akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Nani Anabakia Baba Kwa Hao Mapacha Wasiotakiwa Na Mama Msindai? Itakuaje Kwa Tino, Sabrina Na Jack Aliyerudi? Wanakutana kwenye Villa anayolipia Tino.

Inaendelea..

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment