Jack hakujisumbua hata kumtaarifu mama yake akijua atayapata tu matokeo. Akarudi hotelini. Ile hali ya uchovu ikachanganyikana na mshituko. Akawa amechoka ila hana njaa wala usingizi. Akaanza kufuatilia swala la usafiri wakumrudisha Singida kesho yake.
Jumanne.
Aliondoka
mji mkuu wa Tanzania akiwa ameshindwa. Alichohangaikia mpaka kuvunja
mahusiano mazuri aliyokuwa nayo na kaka yake, Jacinta dada yake pamoja na
Sabrina, watu wake wa karibu sana, hajapata! Hakuwa amewasiliana na hao watu
wala na wao hawakumtafuta kama waliojionya kama walivyoonywa na mama yao. Kama
isingekuwa hivyo, wangeshampigia na kumpa maneno yakumtia moyo. Jack alikuwa
amepoa lakini na tumaini la familia. Akajua hata kama Sabrina atakuwa
amemkasirikia, basi angalau hiyo likizo aliyokuwa amechukua kumsaidia kulea
mtoto, basi atalea watoto kwa juhudi zake zote, mpaka kumfurahisha Sabrina,
asijue Tino ndiye ameshika usukani.
Walikuwa
na mipango mzuri, lakini kosa dogo tu, likabadilisha kila kitu na kujikuta
akimrudishia Tino asiyestahili, damu yake. Jambo zuri na la maana, likakosa
baraka za Mungu, mke, hata jamii yake ya karibu kwa sababu ya ushindani
wa mama yake.
Alifika
Singida moja kwa moja mpaka nyumbani kwake na kushangaa hakuna mtu. Akazunguka
kila chumba kukaonyesha wazi ni kama alivyopaacha mara ya mwisho alipoondoka
baada ya kumruhusu na msichana wao wa kazi aondoke na yeye kwa likizo mpaka
watakapokuja kurudi hapo nyumbani ndipo na yeye wangempigia arudi. Msichana wa
kazi aliondoka na kumuacha Jack peke yake hapo ndani kwa siku chache akijiandaa
kwenda kuungana na familia yake huko Dar ndipo ikatokea kujifungua Sabrina kwa
gafla, Jack akaondoka hapo bila kuweka sawa. Kwa hiyo akakuta nyumba vilevile
kama alivyoacha. Akaanza kazi ya kupiga simu ya Sabrina bila mafanikio. Jioni
mlinzi alipokuja hapo kwa ajili ya kulinda, alimwambia Sabrina hakufika hapo na
watoto. Hakuna aliyeingia hapo. Jack akaanza kuingiwa hofu.
~~~~~~~~~~~~~~~~
H |
uku kwa
Tino na Sabrina pamoja na watoto, aliwaacha wakakaa hapo hotelini kwa muda wa
siku 6 ndipo wakahamia kwenye Villa nzuri sana. Hapo napo wakapapenda. Ilikuwa
sehemu ya vyumba viwili, ndipo Sabrina akamuomba baba yake na yeye aende
wakapumzike. Maisha hapo yakaendelea kwa utulivu tu, Sabrina na watoto wake, na
Tino akisaidia kwa hali na mali.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Huku
kwa Jack juma lilipoisha akaamua kurudi jijini kumsaka mkewe na watoto akijua
kwa hakika Pendo atakuwa akijua walipo. Jack alitua jijini moja kwa moja
nyumbani kwa Pendo. “Usinisumbue Jack. Umeshindwa na mipango yako na mama yako,
ndipo unamkumbuka Sabrina sasa hivi! Alitoka hospitalini akakaa hapa hata
kuhumtafuta, sasa hivi ndio unajidai kumtafuta?” “Naomba niambie alipo.” “Sijui,
na hata ningejua, nisingekwambia.” Jack akaondoka hapo nyumbani kwa
Pendo njiani akawatumia ndugu zake wote ujumbe akiomba wakutane kwa wazazi wao
jioni.
Akaelekea
mpaka ofisini kwa Sabina mida hiyo ya karibu kutoka kazini siku ya ijumaa.
“Sabrina na watoto wako wapi?” “Ni swali gani hilo Jack, au umechanganyikiwa
wewe!?” Sabina akaweka mshangao mkubwa. “Unaniuliza swala la mkeo, kwani mimi
ndiye niliyemuoa?!” “Sabrina hayupo nyumbani.” “Yuko wapi?! Na umewaambia
wazazi?” Hapo Jack akaingiwa hofu kidogo. “Wewe Jack? Tokea lini?” Sabina
akazidi kumkaba. Jack kimya. “Kwani mlikuwa na matatizo? Kwa maana mimi
nilihisi tatizo tokea alipojifungua. Eti mtu kajifungua kwa upasuaji, eti
ukamuacha na watoto wote akiishi kwa Pendo, nikaambiwa wewe huishi pale
unaishia kwenu! Mama akajiuliza na kushangaa sana. Akasema hata kama wewe ni mnyama
wa kiasi gani, basi ungeamua kumuacha angalau akiwa amepona! Unamuacha mzazi na
kidonda kibichi!” “Nilikuwa sijamuacha. Kulitokea kutoelewana tu.” “Ndio hasira
mpaka ukamtelekeza mke na watoto! Yaani baba yako aliweza kufika kuangalia
mtoto, wewe mwenye mtoto umekasirika unajificha kwenu! Sasa hasira zimeisha au
unataka kumpa talaka yake?” Sabina akaendelea kumkaba.
“Hapana!
Nani amesema nataka kumuacha Sabrina!?” “Wewe mwenyewe kwa vitendo vyako. Au
umegairi kwa kuwa umekosa ubunge?” Jack akaona aondoke. “Sasa wazazi
wapo kwa mdogo wangu yule wakiume, wameenda kumtembelea. Wapigie simu, uwataarifu
kutoonekana kwa Sabrina na wajukuu zao.” Jack akatulia kidogo na kugeuka tena
akiondoka. “Mbio za sakafuni, zimeishia ukingoni. Ulifikiri utashinda kwa kuwa
wewe ni Msindai, ukamtelekeza Sabrina, umeshindwa ndio unaanza kumtafuta tena!
Muulize Pendo uliyemuachia familia yako.” Jack alikuwa amesimama na
kumgeukia tena Sabina wakati alipoanza
kuzungumza tena kwa kumkejeli, akabaki amesimama tu, Sabina akarudi zake
ofisini, akamuacha hapo nje.
Kwa Kina Msindai.
I |
lipofika majira
ya saa mbili na nusu ndipo Jack akaingia nyumbani kwao na kukuta ndugu zake
wakimsubiria. Akasalimia na kukaa. “Samahanini kwa kuchelewa.” Akaanza Jack.
Kimya. “Nakumbuka mwanzo niliposema namuoa Sabrina, mama alipinga kabisa akiwa
ametoa sababu zake. Nikalazimishia mpaka nikamuoa Sabrina. Alipojifungua wale
watoto, napo ikaleta shida sana, nafikiri wote tunakumbuka. Mama akakata
mawasiliano na mimi mpaka Sabrina aliposhika mimba ya Brayan na maswala yale
aliyoyafanya Sabrina kule Singida yalipoiva, Brina akashauri nimpigie mama
simu, ili asipitwe kwenye vitu muhimu sana vinavyotokea kwenye maisha yangu.”
Kila mtu kimya akisikiliza.
“Sikutegemea
kwa ule ushauri. Nikamuuliza Brina kama anao uhakika, akasema yeye anajua mama ananipenda
sana, na amehangaika sana na mimi mpaka kufika pale. Hadhani kama ni
sawa mama akapitwa na mambo yangu ya muhimu. Tofauti zake na mama, akaniambia hazinihusu
mimi. Hataki kumnyima Brayan mapenzi ya bibi yake au kuvunja mahusiano
yangu na mama, kwa makosa aliyofanya yeye nyuma. Kufupisha habari, nilimtafuta
mama, yeye mwenyewe mama akaomba kufika nyumbani kwetu akiwa na zawadi za Jeiline
na Keiline. Nikajua amefika mahali, amewapokea.”
“Ukaanza
mchakato wa babyshower ya Brayan. Kuhofia kilichotokea kwa mapacha
kisitokee tena, mimi nikakataa kabisa. Sabrina akanilazimisha na kurudia tena
usemi wake uleule, maisha na maamuzi mabaya aliyofanya yeye, yasimnyime Brayan
baraka kutoka kwa bibi yake. Nikamwambia mbona kama kuna upendeleo! Akasema
watoto wote ni wake, haimsumbui kama mmoja akipendelewa.
Sisi wazazi tutafute jinsi ya kubalansi huo upendo, lakini tusimnyime Brayan
alichoandikiwa na Mungu. Tukakubaliana kila kitu na mama alichotaka ila bila
kujua kwamba ukaribisho huo hapa nyumbani si kwa wale mapacha!” “Unaaza ufitini
Jackson. Mimi ndivyo nilivyokwambia au unaleta maneno ya mtaani hapa nyumbani
kwangu?” “Naomba nimalizie mama.” “Sitaki ufitini mimi.” “Sawa.” Jackson
akaendelea.
“Ukaja
mchakato wa Ubunge wa Afrika Mashariki. Ukaanza kama unakuwa siri. Nikauliza ni
kwa nini hata kaka asiambiwe, yeye ndio mshauri wangu. Sasa baada ya kukaa
baada ya haya yote kutokea ndipo nagundua kulikuwa na hila nyingi tu
ndani yake tokea mwanzo. Hata majibu niliyojibiwa wakati ule nashindwa
kuyaeleza hapa. Ndipo nikalazimishia kusema nilazima nimuulize kaka, anishauri.
Nikaonywa nisiende kwa undani ili kuepusha kuja kuonekana kuna upendeleo.” “Na
mkeo?” Akauliza Jacinta. “Si amesema asiingiliwe huyu Jack? Sasa maswali ya
nini?” “Swali hili ni la Jack, Jena. Acha kunijibiza.” “Wote tumeitwa hapa.
Nani amekuweka wewe ndio muuliza maswali?” Jena akamuuliza dada yake.
“Kwa
Sabrina niliambiwa nisimchanganye. Sio mbaya kuuwa ndege wawili kwa jiwe
moja. Nikimwambia kabla ni kama kumvunja moyo kwenye juhudi tunazoweka
Singida. Nifanye kimyakimya, nikishafanikiwa ndipo nimwambie. Ila kwa hakika
sikujua kama zile simu za kuulizwa mchana na usiku kama nimemwambia Sabrina,
zinahusiana na ushirikina. Kwamba anahisiwa kuwa ataniloga
nisifanikiwe.” Junior na Jacinta wakacheka kwa kusikitika. Mzee Msindai kimya,
ametulia kabisa.
“Mnachocheka
kwa dharau ni nini?” Mama yao akauliza, hawakujibu, wakanyamaza kabisa.
“Kufupisha habari nzima, binafsi nilishangaa sana hili jambo lilivyokuja
kugeuzwa kuanzia hata na Jena huyu hapa mbele ya Sabrina! Ikawa tena kama kuna ushindani!”
“Acha kuniingiza kwenye mambo yako Jackson. Mkeo mwenyewe yamemshinda, analia
wivu.” “Sawasawa. Tukubaliane kabisa kuwa Sabrina ni mchawi, mbaya
sana kwangu, ana watoto wa kizungu ambao ni aibu kubwa sana kwa hii
familia. Hata hivyo ameondoka na watoto wake.” Wakashangaa sana.
“Ndiyo.
Sabrina ameondoka.” “Ameona umeshindwa Ubunge, ndio amekukimbia.” “Hivi
wewe Jena kichwa chako kimejaa wadudu au unafikiria kweli?” “Ningekuwa daktari?
Nafikiria, na mimi naongeaga ukweli, si mnafiki mimi. Ameona mwenzie ameshindwa
ndio ameondoka.” “Labda mimi nisaidie kwenye kuongeza ubaya wa Sabrina hapo kwa
Jena kwa kusahihisha. Tokea alipoondoka siku ile ya harusi ile ya kina Pendo,
hata kabla sijakwenda Dodoma kwenye kinyang’anyiro hicho cha ubunge, sijawaona
tena.” “Hakwenda Singida kama alivyosema?!” Kaka yake akauliza kwa mshangao.
“Hapana kaka. Hakuna aliyemuona Sabrina na wanangu kule Singida tokea
walipokuja huku kwa ajili ya harusi ya kina Pendo, babyshower ya Brayan
na kujifungua. Lakini hilo sio tatizo. Nimewaomba mfike hapa ili muwe
shahidi.” Wote wakatulia.
“Nimefanya
mengi mno aliyokuwa amenishauri mama. Nafikiri tokea mtoto, jibu analojua mama
kutoka kwangu ni ‘ndiyo’. Na nimekuwa mwaminifu sana hata katika hili la
Ubunge japokuwa nilikuwa nimevurugukiwa haswa, nikajiambia nitii tu.
Nifanye kile anachonishauri.” “Kwani na wewe mwenyewe hukutaka? Acha kunigeuka
kama vile nilikulazimisha! Kama ni kokosa huo Ubunge safari hii ni wengi
tu wamekosa, halafu nafasi nyingine zipo tu zinakuja. Utapata.” “Sawa mama.”
“Halafu sio kila kitu alichokushauri mama umefanya wewe Jack. Alikwambia nini
juu ya huyo Sabrina na ukang’ang’ania?” Jena akaongeza bila aibu.
“Hivi
wewe Jena huwa unafikiria lakini kabla hujazungumza kweli?!” “Subiri kwanza
kaka. Ni kweli kabisa Jena. Sasa ndio nimerudi hapa kwa mama na wewe Jena.
Nimekuwa peke yangu kwa zaidi ya siku 10. Tokea Jena ulipomwambia Sabrina kuwa
amepitwa, nyinyi wote mnajua swala la ubunge kasoro yeye, mpaka leo sina
familia. Nipo Singida peke yangu. Sina hata wakuzungumza naye. Sasa ndio
nimerudi kuomba mawasiliano ya yule mwanamke mnayeona atanifaa, niombe tena
nioe.” Hapo pakawa kimya. Jack akatoa simu.
“Sabrina
ameondoka na wale watoto wake wakizungu na hata huyu wangu. Sasa sasahivi nipo
huru kuoa kabisa. Tena hata sheria ipo upande wangu kwa kuwa Sabrina yeye ndiye
aliyeondoka. Sijamfukuza. Sasa katika wale wanawake ambao mlikuwa mkinishauri,
yupi ambaye sasa hivi mama, unadhani atakufaa awe mkwe wako?”
“Unanivunjia heshima Jackson!?” “Hata kidogo mama yangu. Ninachotaka ni hiki
kilichotokea kwa Sabrina kisitutokee tena. Safari hii nioe chaguo
lako, ili wote tupumzike. Sasa hivi nipo tayari kwa yeyote
utakayemchagua wewe, nitajie tu, nianze kutongoza upya, nioe.” “Utajijua
mwenyewe!” “Nilijijua mwenyewe, ukaingilia mama, mpaka sasa hivi nimekimbiwa.
Nilikuwa nikiheshimika nina familia nzuri. Kule Singida kila mtu alikuwa
akinipongeza kwa heshima Sabrina aliyokuwa ameniwekea kwenye jamii. Sasa kama
nilipata heshima kwa mwanamke mbaya ambaye hafai vile, bila shaka kwa huyo utakayenichagulia
wewe, itakuwa zaidi.”
“Mimi
sijakwambia umuache mkeo.” “Hata kidogo mama yangu. Ameondoka yeye
mwenyewe kwa kuwa yamemshinda. Viwango vyetu vitukufu vimemshinda yeye
aliyezaa watoto wa kizungu, akaloge kwingine. Ndio naomba sasa ushauri wa
mwingine hata bikra, mimi nitaoa.” “Naona umeanza kunitukana.” Akasimama mama
yake. “Naomba usubiri mama. Kwa maana nyingine. Kuondoka kwako hapa leo, mbele
ya familia, ni kwamba unasema swala langu na mwanamke nitakayeoa tena, halikuhusu?”
“Linanihusu vipi mimi!?” “Tafadhali naomba fikiria majibu yako na
uyakumbuke siku utakapokuja kunikuta na mwanamke wangu. Narudia tena
mama, naomba nipe mwanamke ambaye wewe unajua ni mcha Mungu, asiye na mimba,
atakayenipenda na kunihudumia kwa uvumilivu kuliko Sabrina.” “Kwani na wewe
mwanamke ni mmoja tu? Siku zote tulivyokuwa tukikushauri juu ya Phina hapa!?
Mama alikushauri mara ngapi hapa ukaishia kwa....” “Subiri Jena.” Jack
akamkatiza na kuchukua tena simu yake.
Jack
kwa Mke, Chaguo la Mama Yake.
W |
akamuona
anapiga simu na kuweka kwenye spika. Wote kimya. “Upo
mzima Phina?” “Mzima Jack. Mama watoto na kichanga wanasemaje?” Akauliza
Phina vizuri tu akisikika ametulia na yupo kwenye mzingira tulivu. “Tumeachana ndio maana nimekupigia.” “Aisee pole. Ndio maana
ile shower ilifutwa! Maana nilisikia tu watu siku za mwishomwisho
wakisema hawatakuja, nikasikia mpaka mama Mkapa naye amegairi, ndio nikauliza
kwa nini tena na tumealikwa na mama Msindai mwenyewe! Sikupata majibu
yakueleweka, kumbe ndoa ilishindikana! Pole Jackson. Inatokea.” Wote
hawakuwa wakijua hata kama watu wengi wakubwa aliotaka mama Msindai wahudhurie
kwenye hiyo tafrija, walitoa udhuru wakutohudhuria. Kumbe tena walimkatalia siku
za mwishoni, akabakia kumlaumu Sabrina tu.
“Huyo
naye atakuwa mbeya.” Kwa haraka Jack akabonyeza Mute ili Phina asimsikie
mama yake. “Wala hakuna aliyeghairi kuja! Ni vile Sabrina alivyokataa ndipo
nikaifuta. Lakini wageni wote nilioalika walikuwa tayari kuja. Mbeya tu.”
“Tena! Mkwe mwenyewe anayependwa tena na yeye mbeya!?” Jacinta akauliza
na kuanza kucheka. “Upo Jack?” Wakamsikia Phina
akiita kwenye simu. Jack akamtoa kwenye mute. “Nipo.
Samahani nilikuweka kwenye mute. Sasa kwa kuwa tumekuwa tukifahamiana
kwa muda mrefu, na umezoeleka hapa kwenye familia, naomba tuoane.”
Wakamsikia Phina akicheka.
“Sikutanii Phina. Kweli. Ukikubali, mwezi ujao tunafunga ndoa.”
“Acha masihara Jack! Yaani wewe siku zote hizo, ushakuwa mpaka na watoto ndio
unataka unipe mimi wegazi! Ulikuwa wapi miaka yote hiyo! Akuu! Na uache utani
wa usiku usiku bwana! Pole kwa matatizo, lakini mimi sina mpango wakuingia
kwenye ndoa za namna hiyo. Sina shida kihivyo! Yaani ushindwe ndoa ya mwanamke mliyepambana
vile siku ya harusi, mkae mpaka mzae, mje mshindwane ndipo uje kwangu! Acha
masihara wewe! Mimi mwenyewe nataka mume wangu, tuje tulee watoto wetu,
sio wegazi! Naamini utaelewa tu Jackson. Sitaki kuwa chaguo la pili
kwa yeyote yule. Na umama wa kambo sio wito wangu.”
Jack alikuwa ametulia kabisa akisikiliza, na kuweka speaker kila mtu asikie.
“Hata
hivyo na yeye ni mtu mzima sana. Hee!” Mama Msindai akaongeza, wakasikia simu
imekatwa. “Naomba ushauri wa mwingine ambaye si mtu mzima, mama.” “Wewe tulia
utapata mwanamke mzuri tu. Acha haraka.” “Wala si haraka mama. Sirudi kuwa
mdogo na kama ulivyosikia ni kama soko langu linaanza kuisha sokoni sababu si
kijana tena.” “Sasa na wewe huyo Phina ni mwanamke wa kutulia na kuoa huyo?”
Jacinta akacheka sana.
“Na
huyo naye pia hamfai Jack? Maana ndiye aliyekuwa chaguo lenu wewe na Jena,
ghafla amekuwa mtumzima? Wakati ukimng’ang’aniza Jack amuoe, hukujua
kama ni umri wa Jena?” “Hayakuhusu Jacinta wewe! Acha kunivunjia
heshima.” “Samahani mama yangu. Nimefurahi tu.” “Kwahiyo...” “Naomba turudi
kwangu mama. Kwa hiyo huna ushauri mwingine tena?” “Mimi nilikuwa nakusaidia
Jackson. Unaweza kuwa umekasirika kwa kuukosa huo Ubunge uliokuwa ukiutaka
sana. Lakini...” Jack akacheka na kutingisha kichwa kwa masikitiko, kisha
akauliza. “Mimi ndiye niliyekuwa nikiutaka sana Ubunge na si wewe
mama? Hukunikuta nimetulia na ndoa yangu, tukiwa na mipango inayoeleweka na
Sabrina, umenivunjia ndoa na mipango yote, sasa hivi nimerudi kuwa kama kijana
niliyemaliza chuo! Nipo sifuri kabisa!” “Wewe rudi ukatulie, endeleza jimbo
lako. Uchaguzi unakuja baada ya miaka michache sana. Upo pazuri. Huko Singida
huwezi kushindwa. Sabrina si Mungu wako. Alikuwa akikutafutia sababu, ameipata
kwa haraka na ndio maana amekukimbia.”
“Mimi
labda niulize japokuwa unaweza ukanichukia sana mama.” “Sasa kwa nini uulize?” Mama
yake akamuuliza Junior. “Humuhurumii Jack hapo ulipomfikisha? Kwamba huhisi
kama unahusika kumfikisha hapo alipo?” “Kwa lipi!? Sijamwambia Sabrina
andoke mimi! Yeye kama si mchawi, anakimbia nini? Anakimbia kwa aibu
zake, kuona amegundulika ubaya wake! Na swala la watoto wa kizungu kwani ni
uongo? Hata Jack akijidai kuwapenda, kweli wale watoto si wake. Na ni mzigo
unaomgharimu Jackson. Kwa pesa ipi anayoingiza Jackson itakayomtosha kutunza na
watoto wa wanaume wenzie waliopita hapo kwa Sabrina? Mimi ni
mama, lazima niumie. Sasa kosa langu ni kutoa malalamiko yangu? Yeye huyo
Sabrina hakumtaka Jackson tokea zamani, ila Jackson ndiye aliyeenda
kumlazimisha.” Jackson akashangaa sana.
“Mzee
Msindai, upo baba yangu?” “Nipo Jacinta, mama. Za kazini.” “Mimi naendelea
baba. Nachapa kazi. Umekula baba yangu au nikuletee chakula hapohapo ulipokaa.”
“Nitashukuru.” Jacinta akasimama kwa haraka na kuanza kumpangia baba yake
chakula. “Umemuuliza Pendo kujua Sabrina na watoto walipo?” Junior akamuuliza
Jack. “Hajui. Nimemfuta na Sabina, pia hajui.” “Kwa wazazi?” Akauliza baba
yake. “Hawapo Chalinze. Wazazi wapo kwa yule kaka yao. Acha mimi nikapumzike.”
Jack akasimama, wakamuona anatoka. “Wapi tena!?” “Naona hapa nimekosa mke,
baba. Acha nikatulie hotelini kesho nirudi Singida, nikaanze kazi, nisije
nikakosa vyote. Usiku mwema.” Hakuna aliyejibu, kimya. Jack akaondoka.
Jacinta
akamaliza kumpangia baba yake chakula. “Sasa wewe kula baba yangu, na mimi
nikapumzike, kesho nina vikao vya kuanzia alfajiri. Nitakupigia mchana.”
“Nashukuru mama yangu mzazi. Uwe mwangalifu huko barabarani.” “Nitafanya hivyo.
Sasa muheshimiwa Msindai?” Akamgeukia kaka yake. “Acha na mimi niondoke pengine
nitamuwahi Joy kabla hajalala. Usiku mwema baba.” “Na wewe. Salimia familia,
zaidi Claire.” “Huyo sijui kama nitamkuta sasahivi. Nitamwambia kesho akupigie
kwa kuwa haendi shule.” “Hapo sawa.” Wawili hao wakaondoka na kumuacha baba yao
akila hapo sebuleni peke yake, mke chumbani.
Singida.
J |
ack
akarudi Singida na kuanza kazi. Lakini
na huko Singida nako akakuta habari zake za kukosa ubunge wa Afrika Mashariki
zimeenea tena zikisambazwa vibaya sana na mmoja wa mwanasiasa ambaye naye
aliona muelekeo wa kurudisha hilo jimbo kwa chama chao, akatamani yeye ndio awe
mbunge hapo lakini akakuta Jack ameshajijengea sifa na ni kama kila mtu
alishajua yeye ndio atachukua jimbo pale. Kitendo cha kugombania ubunge wa Afrika
Mashariki bila hata kuwaambia vijana wake wa chama wale wa karibu tu, huyo
mpinzani wa Jack wa ndani ya chama hichohicho akatumia huo mwanya vibaya sana. Akawatangazia
watu kuwa Jackson Msindai ni msaliti kwa watu wa hapo. Alikuwa na tamaa ya pesa
na alikusudia kuwakimbia pindi atakapopata ila Mungu alimuweka mwangani. Na
kweli majina yote ya walioingia kwenye kinyang’nyiro hicho yalikuwa yakitembe
tu mitandaoni, walioshindwa walijulikana kwa wazi tu, na waliochaguliwa
kuiwakilisha nchi ya Tanzania kwenye Bunge la Afrika ya Mashariki majina yao yalitangazwa
na pongezi zao ziliendelea kumiminika.
Akamchafua
Jack vilivyo akipita kugeuza mioyo ya wapambe wa Sabrina na Jack akitaka
wamgeukie au wawe upande wake ili yeye aje achukue nafasi ya Jackson Msindai
kwenye hilo. Akaweka chuki na ufitini. Singida pakaanza kuwa pachungu kwa Jack.
Hana majibu ya kueleweka juu ya alipo Sabrina na wanae, na wala hakuwa na sababu
ya msingi ya kutoweka wazi nia ya kugombea Ubunge wa Afrika ya Mashariki,
ambalo hata halikuwa jambo baya kama anavyosema Waziri Msindai. Jambo jema,
wakalifanyia hila bila sababu! Na kama wangeliweka kwa wazi, kushindwa kwa Jack
wala isingekuwa jambo la ajabu. Ni kawaida tu, na si Jackson Msindai peke yake
ambaye hakuchaguliwa!
Jack akabaki hajui chakufanya tena. Mama yake ameshamaliza
yake, hataki kupandishwa presha. Alichokitaka kwa kijana wake kwa kiasi fulani
kimetimia. Mwanae yupo Singida akiingiza pesa yake anayolalamikia ni ndogo, sasa
safari hii haitumiwi na Sabrina wala watoto wake Sabrina. Kumetulia. Lake na
Jena limetimia. Sabrina amewapisha kwenye maisha yao.
Watu
wawili waliokuwa wakiendesha familia moja na kusaidia jamii, shetani ameingilia
kati. Si wao tu wanaojiharibia familia yao, na jamii ambayo ilikuwa ikiwatizama
kwa muongozo kiajira, kwenye miradi walioanzisha wao wenyewe, Sabrina na Jack.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Je, Sabrina ameyarudia matapishi yake?
Usikose Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment