Damu nzito kulikio maji.
Sabina alishapanga
na Tino usiku uliopita mara tu alipotoka nyumbani kwa Pendo, kuwa kesho yake
atapokwenda kumchukua mama yake na watoto, wakati Sabrina yupo harusini, basi
wao wakutane sehemu ili Tino apate muda na watoto wake. Sabina alichofanya ni
kushusha vitu vya kina Sabrina na wanae pamoja na mama yake nyumbani kwake, na
kuondoka nao wote mpaka sehemu Tino aliyojua watoto wake watapata sehemu ya
kucheza na kaka yao kukaa bila shida. Wakakutana hapo bila hata kumwambia
Sabrina. Hata Sabrina alipopiga simu kujua hali ya wanae, hawakumwambia sehemu
walipo.
Tino
alifurahi kuwaona hao watoto mpaka machozi. “Wamefanana
sura na mama yao ila damu ya kwetu kabisa! Hizo nywele nyingi mpaka kwenye
ngozi ni za kwetu. Si umemuona mama yangu mdogo? Ananywele hivyohivyo.”
“Hata mama yako alikuwa na nywele nyingi.” Sabina akaongeza maana alimuonyesha
picha za marehemu mama yake pia. “Kabisa, kama mama pia. Nimefurahi Sabina!
Asante sana. Sikujua kama naweza kuja kupata nafasi ya kuja kuwasogelea kwa
karibu hivi.” Mama yake Sabina kimya akiwatizama hao watoto na Tino.
“Nifanyaje
ili wanisogelee?” “Hawa watoto wanapenda michezo ya kimyakimya. Kama hivyo
unavyoona wanajenga hapo, sasa usianze maneno mengi. Kajenge nao, hapo ndipo
utaweza kuwavuta.” Mama Sabrina akamsaidia Tino. “Hawajaweza kuzungumza tu!?”
“Bado. Ila wanaelewa kila kitu, wazito tu wakuzungumza.” “Kama Tino mwenyewe.”
Sabina akaongeza. “Katika moja ya vitu nilivyomwandikia Sabrina pia ni hivyo.
Kuwa anapoona wanachelewa kuzungumza, asiogope, sisi kwetu huwa tunachelewa
sana kuongea, ila tunavipaji vikubwa sana vya uchoraji. Ndio kazi ambayo
hata mama mdogo inayomtajirisha. Kwa hiyo tupo hivyo.” Hayo Tino anazungumza
macho kwa watoto hao wakizungu.
Mwishoe
akawasogelea. Bibi yao alikuwa akitembea na begi lao la michezo kama mama yao
ili wasisumbue mtu. Na kweli wakiwa na michezo yao, utakachosikia ni kupiga
makofi tu na kucheka. Watajenga vitu vyao kimyakimya bila kuzungumza wala
kusumbua mpaka wachoke. Walikaa nao hapo mpaka jioni kabisa bila kumsikia
Sabrina kitu kilichomshangaza mama yao na kuanza kumpigia wakiwa njiani kurudi
nyumbani kwa Sabina.
~~~~~~~~~~~~~~~~
W |
alifika nyumbani
kwa Sabina na kumkuta amekaa tu nje, amejiinamia. Alipowaona akasimama kwenda
kusaidia kutoa watoto kwenye gari. “Hawa watoto wananukia harufu ya
Tino. Mlikuwa na Tino?!” Mama yake na Sabina wakaangaliana kwa hofu maana
Sabrina aliuliza swali la moja kwa moja. Sabrina akapata jibu. “Haya naomba
umpigie nataka kuzungumza naye.” “Naomba utulie Sabrina. Aliniomba tokea jana,
nikaona kwa kuwa hautakuwepo, mimi ndio niwapeleke.” “Una namba yake ya simu?”
“Naomba adhabu yake unipe mimi Sabrina. Tino yupo kama mgonjwa, mimi ndiye
niliyemruhusu. Anakuogopa kupita kiasi. Tafadhali Sabrina. Naomba..” “Unanipa
namba yake au hutaki?” “Mimi naona umpe tu.” Mama yake akamwambia Sabina
lakini akiwa amepooza kama na yeye ameingiwa hofu.
Sabrina
akarudisha watoto kwenye gari na kuwafunga vizuri, akachukua namba ya Tino na
kumpigia hapohapo. Tino akapokea. “Haloo!” “Mimi
Sabrina.” Pakazuka ukimya. “Unakumbuka pale
tulipokuwa tukiishi Moshi, ukaniacha peke yangu ukiwa umejiridhisha nimeshaua
hawa watoto?” Kimya. Sabina na mama yake wakaangaliana wakiwa bado ndani
ya gari.
“Wewe Tino? Unasahau pale tulipokuwa tukiishi Moshi mpaka ukawa
unanilazimisha niue hawa watoto?” “Nakumbuka Sabrina. Na ninaju..” “Sasa,
sehemu kama ile kwa hapa Dar, naweza kupata wapi? Kwa mwezi mmoja tu, nataka
nikodi, nikae wakati najiuguza.” Kidogo
Sabina na mama yake wakatulia. “Zipo sehemu nyingi tu,
inategemea unataka kuishi mtaa upi.” “Sasa sio unitajie sehemu za mamilioni ya
pesa, maana mimi ni mama wa watoto watatu, ukichanganya na wale uliotaka niwauwe.”
“Sabrina jamani!” “Asije akafikiri wale aliotaka niwauwe
niliwauwa. Ndio namwambia pale aliponiacha hospitalini, akakimbilia huku Dar
akiwa amejiridhisha nishaua watoto wangu, bado ninao.” “Mimi naona wewe
Sabina ungenyamaza maana mnaharibu zaidi.” Mama yao akaingilia.
“Najua sehemu ya pesa nzuri tu. Ulitaka kwa lini?” “Si ndio
nimekupigia simu hapa!” “Kwa hiyo usiku huu?” “Unakumbuka nilipokuja mjini
kupumzika nikaishia kukuuguza wewe mchana na usiku bila kupumzika,
halafu MIMI ukaniacha matatizoni?” Wote
kimya. “Basi tokea wakati ule mpaka leo sijapumzika,
nakimbizana tu. Sasa sijui kwa hali hiyo ulitaka iwe lini?” “Iwe haraka
Sabrina.” Akajibu Tino kwa upole.
“Sasa mimi nina wazo. Unakumbuka ile hoteli tulikaa pale kabla ya
kwenda Moshi?” Tino akauliza kwa uzuri tu, Sabrina
akampokea. “Pale kwenye ile hoteli tulipokuwa pamoja,
ukawa ukinidanganya kama unanipenda sana, umri na mali si tatizo. Tutaendelea
tu na tutakuwa na maisha mazuri na matulivu, kumbe ulikuwa uongo wa kutaka
kunitumia tu ili uweze kujitegemea halafu unitupe bila kuacha
chochote kwangu, hata watoto niue?”
Kimya kidogo. “Wewe Tino? Si pale siku ile ukakasirika
na kulia kabisa ukidhani nimekuacha kumbe nilikwenda tu saluni nikaacha sim...”
“Ni hapohapo Sabrina. Hapohapo. Nilikuwa nikishauri pengine usiku huu ukalale
hapo na watoto, wakati tukishughulikia hiyo Villa. Mimi natangulia hapo
kukuchukulia chumba, utanikuta hapo.” “Sasa sio
tumekubaliana hapa, ukaanza ule mtindo wako wa kubadilika badilika kama
kinyonga. Mtu usiye na msimamo. Unaongea hili leo, halafu kesho unapanga mauaji
kabis...” Mama yake akaenda kumpokonya simu. “Inatosha Sabrina.” “Sawa.”
Bila shida Sabrina akakubaliana na mama yake na kugeukia wanae.
“Nani
anahamu na mama?” Akauliza wanae, mapacha wakaanza kupiga makofi. “Muanze
kuongea nyinyi warembo, tuwe tunawasiliana. Mkoje nyinyi! Ona mlivyojaa
michanga! Haya twendeni mkapumzike na mama. Mama anataka likizo ya mwezi mzima,
mbali na kelele za watu. Nani anakwenda na mama?” Wakajipigia tena makofi na
cheko kubwa. Sabrina akacheka. “Naomba nisogeze mpaka sehemu ya taksii dada,
mimi na mama tukapumzike.” “Mbona unabadili mawazo wakati tulikubaliana
vizuri!?” Sabrina akatoa kichwa garini.
“Naomba
nisikilize dada yangu. Maisha yangu yote yamekuwa kuhangaikia watu bila kushukuriwa
ila lawama tu. Sijawahi tenda jema hapa duniani, ikabakia sifa ila karaha.
Nikakaa nikajifikiria leo siku nzima. Ni kwa nini niendelee kuteseka hivi!
Sijapata jibu. Nikajiambia nawajibika mimi mwenyewe kwa Sabrina. Acha nijipe
raha. Hii hangaika na mishono ya uzazi mpaka Singida, sasa hivi, kwa nini
haswa!” Mpaka Sabina akacheka.
“Sabrina!”
“Kweli dada. Sasa twende mama yangu, ukalee uzazi kitajiri, kwenye mahoteli ya
wenye pesa zao. Tukipata Villa, nitakwambia umelete na baba, apumzike na yeye hata
mwezi tukihudumiwa na sisi kama wagonjwa. Tukitoka huko ndipo tutajua
chakufanya. Ila sasa hivi, sitaki kelele kabisa. Mimi na watoto wangu tu.
Sitaki kumsikia yeyote yule ila wanangu. Na wewe dada wakikutafuta, tafadhli
tafuta hekima yakuwajibu, ila chonde, usiwaambie mimi na mama tulipo.
Acha nipumzike kidogo, nipate tena nguvu ya kuendelea na haya maisha, lasivyo
nitarukwa na akili, niache wanangu wakiteseka.” “Mimi nipo na wewe Sabrina. Ila
kumbuka umeolewa mama, na mahari ya watu tulichukua.” “Usijali. Hayo tutakutana
nayo baada ya hata mwezi. Acha nijiuguze mimi mwenyewe kwanza nipone. Au dada
utashindwa kunifichia siri? Kama utaona shida, basi hata usijue ninapokwenda.”
“Siwajui, hawanijui. Wewe ndio unanihusu Sabrina. Siwajibiki kwao.” “Asante dada
yangu.” Wote wakaondoka hapo kwa Sabina, wakiwa na vitu vyote vya Sabrina na
watoto wake, pamoja na mama yao kuelekea huko hotelini.
“Jamani
Brayan ni mpole mwanangu! Amelia kweli huyu leo?” “Kidogo tu. Lakini kimya
hivyohivyo.” “Ubakie mpole hivyohivyo mwanangu, mama apumzike.” Sabrina
akamvuta mkono na kumbusu. Akamfunika vizuri akatulia. “Sijui tunapokwenda
Sabrina.” Sabrina akamtajia. “Haiwezekani Sabrina!” “Kasema mwenyewe Tino. Acha
nikapumzike dada. Nilihangaika naye sana yule mwanaume.” “Ila anaonekana hata
huko amefanikiwa!” Sabina akaongeza. “Nimemsikia kwenye mazungumzo yake.” Mama
yake akaongeza tena. Sabrina kimya ametulia
na watoto wake kiti cha nyuma.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakafika hotelini na kumkuta Tino
akisubiria nje kama Valet. Sabrina alishituka sana alipomuona Tino.
“Natamani kukuuliza lakini nimejikumbusha kuwa hayanihusu.” “Hongera kwa mtoto.
Mtulivu kweli.” Sabrina akamwangalia na kushusha wanae kwenye gari. “Acha
nikusaidie kuwabeba hawa wawili.” “Sitaki. Sihitaji msaada wako.” Tino akajivuta
nyuma. “Kwanza ile barua ya restrain order bado unayo au nikakutafutie
nyingine?” “Nimewapatia chumba kizuri, nenda kapumzike na watoto.” Sabrina
akamwangalia na kurudisha uso ndani ya gari kufungua wanae. Sabina na mama yake
kimya wakisikiliza.
“Nasubiri
ushushe watoto na mizigo ili nikaegeshe gari.” Sabina akaongea akiwa bado
amekaa kwenye kiti cha dereva. “Nenda tu kapumzike dada. Uje kesho asubuhi tuwe
wote.” “Kweli hamtahitaji msaada kwa sasa?” “Hapana dada. Najua unasubiriwa
mahali. Nimesikia ukiambiwa kwenye simu wakati tupo njiani. Wewe nenda, mimi na
mama tutakuwa sawa kabisa. Kesho.” “Sawa. Ila mkiwa na shida mnipigie.” “Sawa.”
Sabrina akakubaliana na dada yake. Mama yake akashuka garini baada ya kuagana
na Sabina.
“Basi
ngoja mimi nikalete Cat yakubebea mizigo.” “Ukiongea hivyo unasikika kama mtu
mzuri, usiyejawa hila na huwezi hata kufikiria mabaya kwa viumbe wasio na
hatia!” Tino akaondoka kwa haraka, kweli akarudi na Cat, gari yakubebea mizigo.
“Acha mimi nikusaidie kuipanga hapa na kukuingizia ndani.” “Sitaki Tino. Kwanza
ondoka.” “Umetoka kufanyiwa upasuaji Sabrina, acha kubeba vitu vizito! Acha
nikusaidie, nitaondoka tu. Mimi silali hapa.” “Sasa hivi ndio unataka
kunisaidia wakati uliniacha hospitalini na dripu ya maji, huku ukinipokonya
vitu vyako na ukiwa umeridhika nimefanya uovu wako.” “Sasa unataka niendelee
kuwa mtu mbaya au mzuri?” Sabrina akamwangalia na kunyamaza.
Akatoa watoto wake garini, wakike akawasimamisha pembeni ya gari, Tino na mama
yake wakaanza kutoa mizigo garini huku wakipanga kwenye kigari chakubebea
mizigo.
Walipomaliza
Tino akamuita muhudumu na kumuomba yeye ndio asukume ile Cat ya mizigo. “Naomba
nikusaidie kubeba watoto Sabrina. Kwanza wanasinzia, sio sawa kutembea mpaka
huko chumbani na wakati...” “Sitaki. Kwanza wameshazoea. Na bibi yao
yupo hapa. Akiona wamechoka atawabeba. Usiguse watoto wangu. Kwanza ondoka
Tino.” “Sasa huko chumbani utapajua?” “Wewe nielekeze, uondoke. Nipe
kadi ya chumba, uondoke.” “Nakusaidia tu, Sabrina! Sina nia ya kuendelea
kukukera.” “Unakumbuka uliponiita mimi ni mnyanyasaji?” “Kwa nini
nisibebe watoto mpaka chumbani, kisha niwaache mkiwa ndani, kuliko kuwaacha
hapa nje! Watu wanapita hapa wanatuangalia! Ona mpaka mlinzi hapo
mlangoni hatuelewi! Mpe mama mtoto huyo mdogo, mimi nibebe hawa wawili,
twende.” “Wewe mwenyewe umechoka, sidhani hata kama unanguvu yakubeba watoto
wawili. Utaniangushia wanangu bure!” Mama yake akaenda kumchukua Brayan
mikononi mwa mama yake.
“Naomba
mimi mnionyeshe huko chumbani, huyu kaka akabadili nguo, ale, alale vizuri.”
Bibi yao akaongoza njia. “Niwabebe?” Tino akaendelea kusihi. “Hawataki kubebwa
na wewe.” “Au tuwaulize wenyewe?” “Hawaongei.” “Ila wanaelewa kila kitu hawa
watoto. Wanaufahamu mkubwa sana.” Sabrina akamtizama, na kuondoka. Tino akabeba
wanae na kumfuata. “Mmechoka sana?” Tino akawauliza kwa upendo, wakajilaza
begani. Akaendelea kutembea kumfuata Sabrina kwa haraka ili yeye ndio aongoze
njia.
“Na
kesho usirudi hapa, wewe Tino. Sitaki wanangu wakuzoee. Wewe ni mpita njia, na
ubakie hivyohivyo.” “Ile Villa yakuishi japo kwa mwezi nimeanza kushugulikia.”
Tino akatupia akitembea nyuma yake. “Basi usirudi hapa mpaka uwe umekamilisha.”
“Sitaki kukuudhi zaidi, Sabrina. Nitafanya kila kitu unachotaka, ila ukumbuke
mimi nipo.” “Na hilo ndilo tatizo langu.” Sabrina akajibu. Wakawa wamefika
kwenye lift. Wakaingia wote na mama yake Sabrina. “Ungeniacha nimalizie. Kwamba
ukihitaji kitu chochote, muda wowote hata kama ni usiku, nipigie.” “Nataka
ufute ule uongo na utapeli wako wote ulionidanganya wakati unashida na...”
“Namba ya simu nimeandika kwenye simu ya mama, Sabrina. Hata ukitaka dawa ya
maumivu, kurudi hospitalini kwa uangalizi tu, wewe nipigie, nitakupeleka.” “Leo
ndio unakumbuka kuwa kama wanadamu wengine? Uliniacha hospitalini wewe.”
“Najutia mpaka nimekuwa mgonjwa Sabrina.” Sabrina akamwangalia.
“Kweli
Sabrina. Najutia na naugua kwa huo ubaya. Sijawahi kumtenda mtu ubaya
niliokufanyia wewe na watoto wangu. Huwa nashituka usiku, nikikumbuka,
nashindwa kurudi kulala, mpaka kwa madawa. Sili vizuri, Sabrina.” Sabrina
akamwangalia vile alivyokonda kama mgonjwa na kunyamaza. “Ila nashukuru Mungu
nilikosa nikiwa na wewe Sabrina. Kama ningekosa kwa ukubwa ule
nikiwa na mwanamke mwingine, sasa hivi tusingekuwa na hawa watoto.” Hapo
Sabrina akawa amefungwa mdomo kabisa. Akanyamaza. Mama yake kimya ametulia hapo
ndani ya lift na Brayan akiwa amelala kama dada zake begani kwa baba yao. Wote
wakanyamaza mpaka wakafika kwenye chumba.
“Asante.”
Sabrina akashukuru na kupitiliza chumbani. Tino akatabasamu tu. “Nikusaidie
nini mama yangu? Naona hawa wamejaa michanga sana. Naweza kukusaidia kuwaogesha
na kuwabadilisha nguo, wakati wewe ukimsaidia Sabrina kwa huyo kaka yao.” “Una
uhakika Tino? Umekuwa nao siku nzima, sijakuona ukila vizuri! Nashauri
ukapumzike.” “Usijali mama yangu. Hata hivyo mimi si mlalaji wa mapema hivi.
Acha nikusaidie kidogo tu. Nipe nguo zao zakubadili baada ya kuwaosha.” “Sawa.”
Tino akaelekea kwenye moja ya bafu la karibu na vyumbani akijua huko yapo
mataulo pia. Sabrina na yeye akaingia kuoga kwenye bafu la moja ya chumba, master.
Wakati
amejilaza baada ya kuoga, Tino akaingia. “Unajisikiaje?” Sabrina akabaki
akimwangalia. “Kuna aina moja ya shampoo na conditioner, nzuri sana kwa ajili
ya aina ya nywele zao hawa. Naomba nilete kesho asubuhi pamoja na aina nzuri ya
brashi kwa ajili ya aina ya nywele zao pia.
Nimeona aina ya chanuo mnachotumia, sio kwa ajili ya aina ya hizo nywele
zao. Itawasaidia hata wao.” “Hebu njoo
hapa karibu Tino.” Tino akasogea na hofu kidogo. Sabrina akakaa.
“Unashida
gani wewe? Unataka nini tena!? Tafadhali naomba niambie, usinipotezee
muda.” “Najutia nilichofanya Sabrina. Nimepata kila kitu mpaka ile leseni
niliyokuwa nikihangaikia ya Italy. Sasa hivi nauza picha zangu kimataifa. Kazi
zangu zinauzika vizuri. Nina hela Sabrina, lakini majuto yananifanya
kuwa kama hivi unavyoniona. Mgonjwa nisiye na dawa, ndio daktari amenishauri
nirudi, nitengeneze na wewe kwanza, niweke amani na wewe niliyekukosea kwanza,
ndipo tuone tunaendelea vipi!” “Unataka nikusamehe kwenye lipi Tino? Msamaha
huo unataka ufike wapi?” “Popote utakaponisaidia kunisamehe Sabrina. Nimekosa,
naomba nisamehe.” Tino akapiga kabisa magoti.
“Tafadhali
acha kunikosanisha na Mungu wangu. Usinipigie mimi magoti ila Mungu tu. Simama.”
Tino akasimama. “Nimekosa kwako zaidi na nitakavyokiri hapa. Najuta Sabrina.”
“Sasa naomba uniache nipumzike Tino. Nipo kwenye wakati ambao hata mimi
mwenyewe siuelewi. Nahitaji muda wakutafakari mengi kwenye maisha yangu. Kwa mara ya kwanza
nataka nijifikirie mimi kwanza.” “Naahidi sitakubughudhi Sabrina. Nataka tu
kusaidia. Najua sistahili, lakini najua kwa hakika hata wewe hustahili kulea
peke yako. Watoto wawili si kazi ndogo! Kuanzia kiuchumi na hata maisha yao ya
kila siku. Naomba upokee kila msaada nitakaoweza kukupa, kwa muda nitakao weza.
Ni hilo tu. Naondoka, nashauri na wewe ufikirie juu ya hili.” “Sawa.” Hilo
likamfurahisha Tino, hakutegemea. “Nashukuru sana Sabrina. Basi nitakuona
kesho. Na ninachukua kadi moja ili nikirudi asubuhi nisisumbue.” Sabrina
akamwangalia na kurudi kujilaza bila kumjibu.
Tino
aliondoka hapo akiwa amejawa furaha asiamini kama hajafukuzwa tena. Sabrina
alikuwa kama amepoa kwa kiasi fulani, kitu kilichomtuliza na yeye na kumfanya
angalau usiku huo akalale kwa amani.
Kwa Kina Msindai.
J |
ack
alikuwa kama amepigwa na butwaa hajui afanye nini tena. Alikuwa amemkasirikia
Sabrina akidhani amemsaliti, kumbe mama yake ndiye amemdanganya. Ameshaharibu
mpaka hapo, akaona ni bora amalize tu, ndipo amtafute tena Sabrina angalau
akiwa ana habari njema za kuwa Mbunge. Alijua kwa hakika atafanikiwa tu kwenye
swala la ubunge. Upepo wote ulikuwa ukionyesha unavuma kwa heri kwake. Akaona
arudi kwa Sabrina akiwa ameshamaliza yote na ahadi ya kutulia naye. Alijua kwa
hakika Sabrina hana pakwenda, amejifungua na ana watoto watatu wadogo, akajua
yupo tu, amalize yake, atamkuta tu. Alishaambiwa na kaka yake kuwa Sabrina
anampango wa kurudi Singida na watoto, akaona atulie mpaka akitoka Dodoma ndipo
arudi Singida.
Baada
ya kufukuzwa harusini, na yeye akaenda kutafuta sehemu akakaa huko mpaka giza
lilipoingia ndipo akarudi nyumbani kwao akiwa ametulia kabisa. Hakutaka kesi
wala kumuuliza mama yake. Alimkuta chumbani kwake, baba yao sebuleni tu akisoma
magazeti kama kawaida yake na kuangalia taarifa ya habari. Akamsalimia na
kupitiliza chumbani kwake. Akabadili suti aliyokuwa amevaa, akatoka na yeye
akakaa hapo sebuleni. Kimya. Hakuna aliyemsemesha mwenzie mpaka Jack alipoaga
kwenda kulala. Mama yake hakutoka chumbani.
Asubuhi
siku ya jumapili alichelewa kutoka chumbani mpaka kwenye saa 4 asubuhi
alipomsikia baba yake akimgongea chumbani kwake. “Huendi kanisani?” “Hapana
baba. Shikamoo.” “Marahaba. Basi ungetoka upate kifungua kinywa.” “Naelekea
Dodoma muda si mrefu.” “Basi uwe na safari njema. Acha mimi niwahi. Mama yako
naye yupo chumbani.” “Asante baba.” Mzee Msindai akaondoka. Akaenda kuoga na kuchukua
mizigo yake baadhi pamoja na suti nzuri akatoka hapo chumbani kwao na kwenda
chumbani kwa mama yake. Akakuta amemaliza kifungua kinywa, sinia lipo pembeni.
“Shikamoo
mama, mimi ndio nakwenda Dodoma.” “Uwe na safari njema.” “Asante.” Jack
akaondoka bila kuzungumzia jingine lolote. Akapewa lifti na dereva wa hapo
nyumbani kwao kumpeleka uwanja wa ndege kuelekea Dodoma. Akiwa kwenye ndege
alibaki akifikiria jinsi alivyokuwa amefurahia hilo swala la ubunge na jinsi
lilivyomgeukia vibaya sana. Amepata ukweli wote wa kilichoendelea kati ya Sabrina,
mama yake, Jena na Pendo. Akajidharau kupita kiasi kujiona safari hii amewezwa
kirahisi hivyo! Hakuwa na wa kumlaumu ila yeye mwenyewe.
Alifika
hotelini. Sehemu nzuri tu, lakini akaanza kusikia upweke wa hali ya juu.
Akamkumbuka Sabrina na watoto wake. Akasikia kummisi. Ghafla kila kitu kikakosa
maana. Akasikia mzigo mkubwa moyoni, hata huo ubunge na ahadi zake vikakosa
maana. Jack asiyejua kumuudhi mtu ghafla anaangukia kumuumiza mwanamke moja tu
na wa pekee aliyempenda na kumsubiria kwa muda mrefu sana. Mama yake akilijua
hilo, anampokonya! Akasikia hasira asijue anamkasirikia mama yake au yeye
mwenyewe aliyeamini kwa haraka na kusahau maneno ya Sabrina tokea mwanzo kuwa
angependa babyshower ya Brayan na pia japokuwa asingekuwa huru ukweni,
lakini alimwambia wazi kwa ajili yake atakwenda tu, kwa uzazi huo wa Brayan. Alisahau
vipi na kuamini kuwa Sabrina ni kigeugeu! Akapoa.
Jumapili.
H |
uku kwa
Sabrina mida ya saa nne asubuhi, Tino aliingia hapo na mifuko mingi ya vitu vya
watoto wake. Akakuta bibi yao akiwapa kifungua kinywa. “Acha nikusaidie.”
Akakaa yeye na kuanza kulisha binti zake huku akiwaongelesha na kucheka
walivyokuwa wakicheka. Sabrina alikuwa ametulia kimya chumbani akiwasikiliza na
mtoto wake wakiume amelala. Alishaamka akala na kunyonyesha na kurudi kujilaza.
Tino anaingia hapo alimsikia muda wote.
Ilikuwa
ni hoteli nzuri sana na Tino aliwachukulia suite. Chumba na sehemu ya
sebule yenye kila kitu. “Sabrina na mtoto wameamkaje leo?” “Vizuri tu. Naona
amerudi kulala. Alikuwa hapa na wanae, akaenda kupumzika.” “Jana nilihisi kama
yupo na maumivu, anazo dawa?” “Mmh! Sabrina si mzungumzaji wa matatizo yake. Ngumu
kujua. Ukimuuliza atakwambia tu yupo sawa. Na ndivyo alivyonijibu hata asubuhi
hii kuwa yupo sawa. Ila ameniaga hapa kuwa anakwenda kupumzisha mgongo. Sasa
nikusubiri mpaka aseme mwenyewe.” “Sabrina ni mtu mzuri sana mama. Aliniuguza
nikiwa sina mtu. Natamani kumsadia sasa hivi, lakini najua ni ngumu kwa
niliyomtendea.” “Sabrina ni msiri sana. Sana. Si kama Sabina au watoto
wangu wengine. Sasa mpaka afunguke yeye mwenyewe, ndipo utajua kinachoendelea.
Mchukulie taratibu tu.”
Tino
akabaki akilisha binti zake huku akifikiria. Akamgeukia mama yake Sabrina.
“Unafikiri Sabrina atakubali nitoke na watoto wakaogelee kidogo? Nimewanunulia life
jackets. Hawawezi kuzama au kudhurika. Nitakuwa nao majini.” “Muulize
mwenyewe.” “Tunaweza kwenda wote. Na wewe ukakaa pale na kupata chakula wakati
sisi tukiogelea.” “Mimi nashauri uzungumze na Sabrina mwenyewe Tino. Hata jana
nilikwambia, si sawa kuchukua watoto bila idhini ya Sabrina mwenyewe. Hata kama
umerudi sasa hivi, lakini usisahau amehangaika nao hao watoto tokea
hawajazaliwa. Nashauri kwenye kila jambo linalohusu hawa watoto, zungumza naye
yeye mwenyewe.” Tino akanyamaza.
Walipomaliza
kula, akasaidia kuwasafisha kisha akaenda chumbani. “Vipi Sabrina?” “Hao watoto
sijawahi kuingia nao kwenye maji kwa kuwa mimi mwenyewe ni muoga sana wa maji.
Hata baba yao huwa namkataza asiwaingize majini tukiwa ziwani.” “Nimenunua lifejackets
za kuwavalisha wakiwa ndani ya maji na mimi najua kuogelea. Watakuwa salama.
Ila kama ukikataa, sitalazimishia.” “Unataka kwenda nao wapi?” “Kwenye pool ya
hapahapa hotelini. Nitakwenda na mama pia.” “Naomba uwe mwangalifu Tino.
Tafadhali sana.” “Usiogope, watakuwa sawa kabisa. Kuna muda maalumu unataka
niwarudishe?” “Lazima waje wapate usingizi wa mchana. Ikifika kwenye saa 7 na
nusu watakuwa wapo tayari kwa usingizi. Naomba warudishe mapema kidogo ili
waoge pia na kula.” “Sawa ila naona nitawalisha hukohuko. Unataka uletewe
chakula gani?” “Naomba uwe mwangalifu tafadhali. Kusiwe na bahati mbaya
huko.” Tino akaelewa hataki amuulize chochote juu yake.
“Sabrina.”
Akamuita taratibu, Sabrina akamwangalia. “Nashukuru.” Sabrina akanyamaza wala
hakumjibu. Tino akabaki akimwangalia. “Unazo dawa za maumivu?” “Ninazo.
Asante.” “Una kila kitu unachohitaji kujihifadhi wewe binafsi?” “Kwa sasa
ninavyo, pengine mpaka kesho.” “Niandikie ili nikiondoka jioni, nikajaribu
kutafuta madukani.” “Huhitaji kufanya hivyo. Mimi nitaenda kujinunulia
mwenyewe.” “Najua unaweza. Lakini kwa kuwa mimi nina usafiri na ninapita huko
madukani, naweza kukuchukulia.” Sabrina akanyamaza. “Basi acha niandae watoto,
watakuja kukuaga.” “Sawa.” Tino akatoka.
Baada
ya muda wakaingia watoto wake na bibi yao. “Jamani mmependeza!” Wakajipigia
makofi. Sabrina akacheka na kukaa vizuri. “Sasa hizo kofia za nini tena?”
“Nywele zisiwasumbue zikiingia maji. Niza kuogelea.” Tino akajibu akiwa nje ya
chumba. “Unashughuli wewe na hawa watoto! Sasa vyote hivi umenunua?” “Jana
nilipotoka hapa. Kila kitu walichovaa hapo ni salama kwa ajili yao. Hata hivyo
viatu ni maalumu ili wakiloa, wasiteleze. Bibi yao ameniambia hawapendi kubaki
miguu tupu bila viatu au soksi.” “Sio hawapendi tu, hawatembei kabisa hao.
Lazima miguu iwe angalau na soksi ndipo wanasimama.” “Niliwaona jana wakati
Sabina alipowavua na kuwaambia watembee mchangani, wakagoma. Sasa hivyo
vitawafaa maana wanaweza kuingia navyo majini na pia wakatembea navyo nje.
Nimewanunulia na sun screen cream kwa ajili ya kulinda ngozi yao wakiwa
juani, wasiungue.” “Ukiondoka, uniachie hiyo sun screen cream, maana
ilibidi kuwabadilishia muda wakuwapeleka ziwani, iwe jioni kwa sababu
wanababuka wakikaa sana juani.” “Basi utaona leo wakirudi, hawataumia kabisa.”
Sabrina akawaangalia na kucheka.
“Hivi
mnajua mnakwenda wapi?” Akawauliza na kucheka, wakajipigia makofi. “Muanze kuongea
bwana! Njooni mumbusu mama, na msimsumbue bibi pamoja na Tino. Muwe wasikivu.
Sawa?” Wakaenda kupanda kitandani. “Tarabu kaka amelala.” Wakamwangalia mtoto.
Tino akaenda kuwasaidia kupanda vizuri hapo kitandani. “Mnaanza kuongea lini?” Wakacheka.
“Watazungumza tu. Mama mdogo ameniambia nikwambie huwa kwetu watoto wa kike
wanachelewa sana kuzungumza. Hata yeye na mama walichelewa kuzungumza mpaka
mama yao akaingiwa na wasiwasi. Bibi akajaribu kuwatafutia wataalamu wa speech,
matamshi, lakini na yeye bibi akaambiwa na mama yake ni vya kuridhi.”
Sabrina akabaki akimsikiliza.
“Ila
kwetu tunakipaji cha uchoraji, Sabrina.” “Sitaki watoto wangu wateseke kama
wewe Tino. Wewe unaamini njia yakufanikiwa ni moja tu, huo mkono wako na si
vinginevyo. Hapana Tino. Sitaki wanangu wawe watumwa.” “Si utumwa! Na
hata hili mama mdogo ameniambia nikwambie, kwetu ni wachoraji sana.
Angalia hawa watoto unapowapa michezo yao. Kama umekaa chini ukachunguza, jinsi
wanavyopangilia blocks zao, ni kifasaha si kama watoto wengine. Ni
kipaji Mungu amekiweka kwetu, huwezi kuwazuia. Hawa hawajafundishwa na
mtu. Angalia hata wakikuta hata na vyombo au viatu mahali, ona jinsi wanavyopangilia
vizuri! Ni kipawa kipo ndani yao. Ni aidha kukitambua na
kuwasaidia kukikuza au kitakuja kujitokeza baadaye sana, kwa kuchelewa.”
Sabrina akawaangalia wanae na wao wakawa wanamwangalia. Wote wakacheka.
“Sasa
nyinyi mnacheka nini?” Wote wakaenda kumbusu mama yao kwa pamoja. “Halafu hawa
wanao Sabrina, utafikiri ubongo wao upo sehemu moja! Wanafanya mambo mengi kwa
pamoja tena bila kuambizana.” Mama yake akaongeza. “Na Jack alishasema hivyo.
Kuna mambo wanafanya kama kope za macho. Bila kupanga, wanafanya pamoja.”
“Nakufanana mpaka mimi mwenyewe huwa kuna wakati nawachanganya. Wakitoka kuoga
ndio kabisa mpaka niwaite majina kama ulivyonifunisha. Naanza na Keiline
anayeitika kwa haraka, najua ndio yeye na kumtia alama hata ya kitu kidogo tu.”
Wakacheka.
“Nikija
kurudi tena nitakuletea vitu vya kuwasaidia kwenye makuzi yao. Vyakuchora,
kuzungumza na mengine mengi kutokana na akili yao. Watakua vizuri tu.” “Sasa
huko kuzungumza ni mpaka lini? Na wakianza kuzungumza ndio itakuwa kama hivyo
wewe!” Mpaka mama yake akacheka. “Ndiyo na hapana. Upande wa wanaume hawana
shida ya matamshi, mimi ni makuzi mabovu ndiyo yaliyonifanya kushindwa
kuzungumza. Mama mdogo yeye ni mzungumzaji mzuri tu. Ipo siku utamsikia, lakini
anasema yeye na mama ni kweli walichelewa sana kuongea.” Wakatulia kidogo.
“Acha sisi twende kabla jua halijawa kali sana.” “Mama, naomba macho kwa
wanangu tafadhali.” “Na Sabina naye anakuja. Usiwe na wasiwasi.” Wakambusu tena
mama yao, wakaondoka.
Siku
hiyo Sabrina alijikuta hapo chumbani yeye na mwanae huyo wa wakina Msindai,
wengine wote wakashinda sehemu ya kuogelea karibu siku nzima. Ilipofika mchana
mama yake alirudi kumwambia wanae wana wakati mzuri, anashauri awaache tu,
wakichoka ndipo wawarudishe. Sabrina alikubali akijua hata yeye mama yake amefurahia
huko walipo. Akawaacha tu.
Jumatatu.
W |
akati
Sabrina yupo mapumzikoni akiepuka maneno ya mama Msindai akimpa nafasi na
mwanae na mapumziko ya uzazi, akifurahia pesa ya Tino huko hotelini, na kumpa
Tino mwenyewe wakati mzuri wakulala usiku huo baada ya kuwa na wanae siku nzima
na kupigia simu ndugu zake huko Italy akiwatambulisha wanae akitaka wawasalimie
na kuwatambua, huko kwa Jack jijini Dodoma ilikuwa tofauti. Alishindwa kulala
kwa mawazo. Akajaribu kumtumia ujumbe usiku huo. ‘Nipo mpweke
Brina, moyo unauma. Sijui chakufanya! Natamani ungekuwa hapa na mimi, Brina.
Nimeharibu, sijui chakufanya.’ Akautuma huo ujumbe na kusubiri ufike
lakini akasubiri zaidi ya lisaa, ukawa haujafika.
Akampigia
na kugundua simu yake imefungwa asijue Sabrina alifanya kwa makusudi. Alimtumia
ujumbe Pendo na kumwambia anajipa likizo ya mwezi mzima, atamtafuta baada ya
hapo. Akamtakia mwanzo mwema na Willy, ndipo akazima simu rasmi. Jack
akaangalia simu kwa muda akisubiria kuona ujumbe unafika, mpaka akachoka.
Akaweka simu chini na kuanza kufanyia mazoezi yale atakayokwenda kujibu bungeni
kwenye usahili. Akajiuliza maswali na kujibu akiangalia muda asipitishe
akaongea mengi yasiyo na maana. Akajikosoa kwa hili na lile, ilimradi tu
kujinoa vizuri. Ilipofika karibu saa 11 alfajiri ndipo usingizi ukaanza
kumsumbua. Akasinzia kidogo na kuwahi kwenye usahili akiwa anataka kufanya kwa
ajili yake na familia yake.
Baada
ya wenzake kadhaa kuingia na kujieleza mbele ya wabunge wote na yeye akaitwa
kuwa imefika zamu yake, akaingia. Ukweli alijitahidi kwa kadiri ya uwezo wake
akiamini atafanikiwa tu na jina lake pia alijua linambeba. Msindai! Kaka
naye yupo kwenye uongozi! Akajua nafasi ni yake. Alikuwa amekaa hapo huku macho
kwenye simu akitegemea kuona ujumbe umefika kwa Sabrina lakini mpaka mida hiyo
wakiendelea kwa usahili yeye na wenzie, hakuona ujumbe kufika. Akajua kama
kawaida ya Sabrina kumblock anapokuwa amemkasirikia. Akaomba simu ya mtu
mwingine, akajaribu kumpigia na kumkosa.
Usahili
uliisha wakasubiria hapohapo majibu kuona nani amepita nani amekosa, Jack akiwa
ametulia hana wasiwasi ila tu kwa familia yake. Ila si kwa kinyang’anyiro hicho
alichokuwa amejiaminisha na kuaminishwa hata na mama yake kuwa NI
LAZIMA atashinda tu. Muda wa matokeo kufika, Jack akawa hajafanikiwa. Hakupata
nafasi ya Ubunge wa Afrika Mashariki. Alishituka na kubaki kama amemwagiwa maji
ya baridi. Hakuna kupinga ila kukubali tu matokeo. AMESHINDWA.
~~~~~~~~~~~~~~~~
0 Comments:
Post a Comment