“Sabrina!?”
Sabina akamuita akitaka kujua msimamo wake. “Nipo kwenye wakati wakutulia mbele
za Mungu, anisaidie dada. Angalau nitulie kabisa, pengine akiongea yeye
Mungu nitamsikia nijue chakufanya. Kumekuwa na kelele nyingi, sijui nimsikilize
nani na niamue nini! Kwa hali niliyonayo sasa hivi, siwezi kufanya
maamuzi sahihi. Acha nimalize siku zangu za maombi kwanza.” “Wewe Sabrina kumbe
unafunga ndio maana huli! Si maziwa yatakauka!?” Pendo akashangaa sana. Wote
wawili na Sabina wakamgeukia Pendo, wakajua wanasikilizwa. “Nina maziwa mengi
dada! Mpaka mama ananishangaa. Hapa nimekamua, nimejaza chupa zote, na bado
yanamwagika.” “Mmmh! Ila kufunga katikati ya kunyonyesha!” “Na mimi namwambia
hivyohivyo, lakini hanisikii.” Mama yake akadakia.
“Naomba mjumbe nimalize ujumbe wangu ili
niwahi kuondoka, nina miahadi mahali.” Sabrina akamgeukia tena dada yake.
“Mwenzio amesema yupo anasubiri. Hataondoka kuona kama utapokea au unataka
nimrudishie vitu vyake. Anasema hilo begi lina vitu vya thamani sana ambavyo
hakuna pesa inaweza kununua.” Sabrina akakunja uso kwa mshangao. “Hataki vije
vitupwe tu. Amesema ukikataa, nimrudishie.” “Wewe, Sabina!” Wote wakamgeukia
mama yao. “Nipe mimi hilo begi nikae nalo wala usirudishe.” Wakabaki kimya
wakimshangaa yeye mama Sabina.
“Jamani
tusidanganyane. Kuna maisha na uhalisia wake. Si haya sasa hivi
tunayashuhudia! Wakati mwingine mapenzi yanashindwa na uhalisia
wa maisha. Leo mnakubaliana hivi, kesho tutakuja kumkuta Sabrina amebaki peke
yake kama hivi na watoto. Atafanyaje?” Chumba kizima kimya, maana ni kweli Jack
hakutokea hapo siku nzima.
Mama
Sabina alipoona ukimya mkubwa katikati ya wasomi hao, mama wa Chalinze, mtaji
wake ni watoto wake, akasimama yeye mwenyewe akaenda kuchukua hilo begi pale
alipokuwa ameliweka Sabina, kitandani ila amelishikilia. “Kamwambie Tino mimi
ninalo hili begi. Sabrina atakapokuwa tayari atalifuata nyumbani kwao.”
Akalichukua na kuanza kutoka. Wajukuu zake wote pale walipokuwa wamekaa karibu
na bibi yao wakicheza na Claire, wakaanza kumlilia bibi yao pale walipomuona
akitoka. “Naona mapenzi yamehamia kwa bibi!” Akadakia Pendo kwa nia nzuri tu,
kama kubadili ile hali ya hewa. “Ndiye niliyebaki! Watafanyaje?” Akajibu mama
Sabina. Ukimya mwingine tena ukapita. “Simameni sasa mumfuate bibi, acheni
kulia bwana.” Wakamgeukia mama yao. “Haya Keiline anza kusimama.” Kweli huyo
mtoto akasimama na dada yake akafuata. “Taratibu msianguke sasa, nendeni kwa
bibi.” Wakajipigia makofi, angalau watu wote pale wakacheka.
“Ila
humo ndani kuna kadi za benki za kila mtoto, amesema kuna pesa. Usizire
Sabrina mdogo wangu.” “Dada Sabina! Bado una ujumbe tu!” Wakacheka kidogo. “Nimekaa naye karibia masaa matatu
akijieleza. Na wewe unamjua Tino si muongeaji. Kwa hiyo lazima nimalize ujumbe,
ndio niondoke maana na yeye anasubiri jibu. Nimesubiri ili tubakie peke yetu,
naona hamna dalili. Sasa Tino anasema zitakusaidia kuwatunza watoto.” “Acha
nimuombe Mungu hekima dada. Najua wewe ni mjumbe, lakini natamani isingekuwa
wakati huu. Naomba tuyaache tu. Maadamu wanakua, na wanafuraha, naomba tuyaache
kama yalivyo kwa sasa. Ila nashukuru.” “Sawa. Na mimi nitakuwa nikiondoka.
Nitakuja kesho kuja kuwachukua.” “Nashukuru dada. Asante.” Sabina akaondoka,
Sabrina akaendelea kukusanya vitu vyake na watoto. Pakazuka ukimya wa muda.
Junior
akavunja ukimya. “Halafu Sabrina, usifikiri nimekusahau. Bado nashugulikia
swala la usafiri wa kukurudisha Singida.” “Hamna neno shemeji. Sisi tutakuwa
sawa tu.” “Utafanyaje!?” Akauliza Junior kwa mshangao kidogo. “Kesho wakati
tunakwenda harusini, nitamuacha hapa mama na hii chekechea yangu yote. Nikitoka
kwenye tafrija ya Pendo na Willy, nitarudi hapa. Sabina atatuchukua, tukalale
kwake, naona tuondoke siku ya jumapili nikiwa nimepumzika.” “Mtaondoka na
usafiri gani!? Ungesubiria niangalie hata ndege ya jumatatu!” “Sabina anaye mtu
anayefahamiana naye anakatisha tiketi za ndege. Amemuahidi anaweza kutupatia
tiketi siku ya jumapili. Ndio tunasubiria. Usihangaike tena shemeji yangu.
Najua una mambo mengi. Naona mimi na timu yangu tupo vizuri kabisa.” Pakazuka
ukimya mwingine.
Mkewe
Junior akavunja tena huo ukimya mwingine, akiaga. “Jamani tutaonana kesho
kanisani. Acha msimamizi wa harusi, akalale. Naona marafiki wameondoka
wamemuacha hapo, anasinzia.” “Naona na vidole vishawekwa mdomoni.” Pendo
akadakia. “Eti Claire?” “Mimi nitaenda kutengenezwa nywele zangu asubuhi. Mama
amesema ataniamsha kama nakwenda shule.” “Hutalia?” Shangazi yake akamchokoza,
wakacheka kidogo. “Ata...” “Cleiton, bora usijibu. Maana lasivyo!” Mama yake
akamkatisha kaka yake kwa haraka, Clei akaweka mkono mdomoni kama anayejiziba
mdomo nakufanya wote wacheke sana. “Mimi silii siku hizi. Nimekuwa dada mkubwa,
anti. Na mama amemwambia Clei akiwa ananichokoza na kunifanya nikalia, yeye
ndio atalia zaidi.” Walicheka humo chumbani kila mmoja akiwaangalia hao watoto
wawili. Siku hiyo nayo ikapita.
Harusi ya Willy & Pendo.
W |
akati wapo
kanisani, Jack akaingia kama aliyekuwa akikimbia. Ila amependeza haswa. Msafi
na amenyoa vizuri, suti safi. Sabrina alimuona ila akatulia tu. Ibada ilikuwa
nzuri, ila fupi tu yenye watu wachache. Wakatoka hapo na kwenda kwenye kupiga
picha, wakaelekea sehemu ya kula. Hakuna aliyemsemesha Jack hata hapo ndani ya
gari wakiwa maharusi na wao kama wasimamizi, yeye mwenyewe akaanza. “Vipi
Sabrina?” Sabrina akamwangalia. “Salama.” Akajibu taratibu tu. “Vipi na
watoto?” “Hawajambo kabisa.” “Mbona kama sijawaona hapa?” “Wapo na mama na
Sabina. Sikutaka vilio kwenye shughuli ya muda mfupi. Nikaona niwaache tu.”
“Nilikuwa Dodoma, nimeingia muda si mrefu. Na bado sijamaliza, natakiwa kurudi
tena.” Kimya. Hakuna aliyemjibu.
“Mimi
nishukuru kwa kutusimamia jamani. Sabrina, asante sana. Najua bado ni mgonjwa
na mambo ya operation, lakini ilikuwa lazima wewe uwepo ili nioe.” Pendo na
Sabrina wakacheka. “Usijali Willy. Mimi mwenyewe nimefurahi nimeshuhudia kuwekwa
historia kwa mara ya pili, tena kanisani! Sikujua kama ndoa za kanisani huwa
zinavunjika!” Sabrina akawa kama anashangaa. “Kiukweli hazikutakiwa ziwe
zinavunjika, hata maandiko hayaruhusu. Ni basi tu. Ni kosa, haitakiwi kuwa
hivyo.” “Lakini nyinyi Mungu aliwakusudia muwe pamoja. Ilikuwa lazima
awarudishe pamoja.” “Ni kwa neema
Sabrina. Hata sisi tunakiri ni Mungu tu.” Wakatulia mpaka wakafika sehemu ya
chakula.
Hawakuwa watu wengi. Walishaweka reservation.
Wakakuta meza yao ilishaandaliwa. Pendo hakuvaa shela, ila nguo nzuri tu ya
rangi ya maziwa. Wakakaa, Sabrina naye akakaa pembani ya Pendo, Jack pembeni ya
Willy, Sabrina akainama na kunyamaza. Wakaagiza vinywaji, wakati wanasubiria
vyakula wakitoa pongezi zao kwa Willy na Pendo, wakamuona mama Msindai na
mumewe wakiwasogelea.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Pakazuka ukimya. Maana hawakuonekana
kanisani. Hata Jena hakutokea kanisani. Hata maharusi wenyewe hawakumtegemea
huyo mama maana mara ya mwisho hawakuachana vizuri na bibi harusi mwenyewe,
yaani huyo Pendo. Walipofika hapo mezani, wakasalimiwa na kila mtu. Uzuri
kuliwekwa viti kwa idadi ya watu. Waliomba meza sehemu ya ndani, lakini ya
kuweza kukaa watu 25 mpaka watoto. Kwa hiyo waliweza kuonana.
Willy na Pendo wakasalimia kwa heshima
na kushukuru kufika kwao. “Asante kwa kufika.” “Ulifikiri kwa sababu umeungana
na huyo mwenzio kunihujumu kwenye shughuli yangu ndio sitakuja?” Akauliza mama Msindai
akiweka napkin yake vizuri. Pakazuka ukimywa wa ghafla, Sabrina macho chini.
“Wengine tukisema ‘ndiyo’ kwenye jambo, huwa tunasimamia ‘ndiyo’
zetu, hatuwi vigeugeu.” “Sidhani kama hii ni sehemu yake mama. Tafadhali mambo
mengine tuyazungumze wakati mwingine.” Junior akaongea kwa sauti ya chini kama
kumtuliza mama yake.
“Halafu hapa ni harusini jamani!
Tusisahau kama sisi tumealikwa.” Akaongeza Jacinta na kuharibu zaidi. “Kukiwa
harusini ndio watu hawazungumzi! Hee!? Tena nyinyi ndio mnampa kichwa huyo
mwanamke, ananifanyia jeuri mimi kwa kuwa nyinyi watatu na huyo Pendo mmeungana
kumkingia kifua.” Sabrina akamtizama.
“Hata unitizame kwa dharau, lakini
Mungu atakulipa wewe. Unanidhalilisha mimi hapa mjini! Naalika watu
kumfanyia shower mjukuu wangu, unanikatalia wakati tuliwafanyia shower
watoto wako!” “Mama! Unakwenda mbali pasipo sababu!” Jackson akashituka sana.
“Samahani, pengine sikuwa nimeeleweka au sikuwa nimeelewa. Mimi sijakataa shower
ya Brayan. Hata Jack nilimwambia, ningependa na Brayan afanyiwe shower.”
Sabrina akaongea taratibu tu.
“Huo ni unafiki mbele
ya watu ili uonekane mwema kumbe ni...” “Hapana mama. Acha kumtukana Sabrina.
Hata kama amekataa shower lakini...” “Samahanini jamani. Mimi naomba
niondoke, ili kuleta amani hapa.” “Umesha...” “Ila kama nilivyosema
hospitalini, muda na wakati wowote ule mtakaomtaka Brayan, tafadhali tuwasiliane
tu. Na sijakataa shower. Brayan ni mtoto wangu kama Jeiline na Keiline.
Sikatai baraka zozote kwa mtoto wangu. Tafadhali, mnijulishe tu. Ni lini, wapi
na muda gani natakiwa kufika na Brayan, bila shida nitafika ila kulala nilazima
nilale walipo watoto wangu wengine wote.” Sabrina akamalizia.
Akamnong’oneza kitu Pendo ambaye
alikuwa akilia, akachukua pochi yake na kuondoka taratibu. “Kweli mama Msindai,
kwa ajenda zako binafsi unakuja kuniharibia harusi ya mtoto wangu!?” Akalalamika
mama K. “Mimi nafahamiana na wewe mama Msindai na familia yako kwa muda mrefu
sana, lakini leo umevuka mipaka. Unakuja kumtusi binti yangu siku ya harusi
yake kwa kuwa tu amemchagua Sabrina kuwa rafiki! Umetuvunjia heshima vibaya
sana, mama Msindai.” “Mimi nahisi ametudharau sana. Pengine ametuona sisi wote
hatuna maana, ila hao wageni aliokuwa amewaalika kwenye hiyo babyshower
yake.” Akaongeza Kenton kwa mama yake.
“Umepokelewa kwa heshima kubwa sana
hapa, na ukashukuriwa. Umegeuza harusi ya mdogo wangu sehemu ya kutolea
dukuduku lako!? Kilichoshindikana ni nini kumuita Sabrina pembeni na kuzungumza
naye?” Akaendelea kulalamika Kenton. “Hakutaka kuzungumza ila kumuadhibu Pendo,
kwa kumpokea Sabrina. Kile kinachoendelea pale kwa Pendo, akilia kwenye harusi
yake, ndicho alichokuwa akikitaka. Na amekipata.” Akaongeza Nancy. Mzee Msindai
kimya.
“Hiyo ni dharau ya hali ya juu sana.
Kama wangekuwa wamekaa hapa kwenye hii tafrija, watu wa hadhi zenu nyinyi, kwamba
na sisi tungekuwa tumealika maraisi hapa, pamoja na wake zao. Mawaziri wenye
vyeo kama vyenu hivyo, kweli mama Msindai ungefanya ulichokifanya hapa?” “Kwani
nimeongea nini cha ajabu?” “Hivi unajua hii harusi ilibidi kusogezwa mbele ili
Sabrina awepo hapa na Pendo?” Akauliza tena Kenton. “Kwani mimi nimemfukuza
Sabrina? Dhambi zake mwenyewe ndizo zimemkimbiza!” “Jamani, acheni mimi
nimuwahi Sabrina. Yule binti amejifungua kwa upasuaji, nahisi leo ndio
amemaliza juma. Sidhani kama ni sawa...” “Nenda Jacinta. Tafadhali sana.”
Akadakia Junior, Jacinta akaondoka kwa haraka, Jack akawa kama ameduaa.
Jack
akasimama kama mshale. “Subiri kwanza Jack. Acha
kukimbia kimbia na wewe kama usiyejielewa.” Pendo akajifuta machozi. “Kwa kuwa mama yako ameanza kuvunja amani kwenye hii
tafrija akimshutumu Sabrina bila kosa.” “Pendo nakuonya wewe mtoto.” “Hapana mama Msindai. Umekwenda mbali mno na najua mwisho
wa haya yote ni kutaka kuvunja ndoa ya Jack.” “Navunja!” “Nyamaza mama Msindai. Umekuja mwenyewe kwenye shuguli
yangu na kuanza fujo. Heshima haiombwi.” Pendo akawa mkali mpaka
akashangaza wote. Willy akamshika.
“Pendo!”
“Kabisa mama Msindai! Unampotosha Jack kwa
kisingizio cha maendeleo huku ukipanda mbegu za chuki katikati yao!
Unamdanganya Jack ili kumchukia mkewe...” “Nilikuonya acha uzushi Pendo
wewe!” Pendo akamgeukia Jack. “Haya CJ, nenda na watoto kule baharini
mkacheze.” Mtoto mkumbwa wa Junior akachukua watoto wote wakaondoka kama
alivyoagiza mama yake.
“Sasa
wewe jidai unataka ubunge, halafu ukawa mbunge, ukajikuta huna mke wala watoto.
Mama yako anakudanganya Jack. Anachotaka ni ushindani, alichofanya Sabrina kule
Singida na kukusanya watu, ndio anataka na yeye akifanye apate sifa kama
alivyosifiwa Sabrina. Hapo alipo anachuki kwa kile alichokifanya Sabrina
Singida na kufanikiwa akasifiwa yeye Sabrina na si yeye.” ‘Unaongea nini wewe
Pendo?!” Jack akauliza. “Mnafiki huyo na mchonganishi.” “Sasa kama ni muongo,
si umuache amalize kuzungumza ndipo ukanushe? Eti mama Msindai? Umeanza
mwenyewe, tumekusikiliza mpaka mwisho, acha na Pendo naye azungumze. Kwanza ni
harusi yake, umeshaiharibu, hakuna cha ziada.” Akasisitiza Kenton.
“Haya
ninayokwambia Sabrina hatakwambia kwa kuwa amekataa. Hataki kukuchanganya,
anaona ni bora yeye abakie mbaya, ili utulie na mama yako. Mfanikiwe kwa hila
zenu. Lakini Sabrina si kigeugeu Jack. Mimi siwezi kukuficha. Alimsikia mama
yako na Jena wakimsema vibaya sana. Maneno machafu mno siwezi kurudia hapa
itakuwa kama kumdhalilisha tena Sabrina. Ila walikuwa wakilalamika kuwa wale
mapacha wanakufilisi wewe, na hawataki pale nyumbani kwake.” “Haiwezekani! Si
kweli Pendo. Mama aliwaandalia...” “Acha kuwa kama toto linalonyonya na wewe!
Tumia akili zako wewe Jack!” Pendo akawa mkali kabisa. “Siwezi kukaa hapa na
kusikiliza uongo wa kipuuzi mimi.” Mama Msindai akasimama.
“Ondoka
tu, lakini wote tunajua unakimbia ukweli.” Akamgeukia Jack. “Wewe ulifikiri
siku ile hospitalini mama yako alikuwa akiniomba niwe nawaleta kina nani pale
nyumbani kwake?” Jack akawa anajaribu kuvuta kumbukumbu. “Walikujaza maneno
mengi ya uongo wakimsingizia Sabrina eti anakataa kwenda kwake mama Msindai
kwakuwa ulimficha siri yenu ya ubunge wa EALA. Wakakujaza huo uongo ili
kukupoteza tu kwenye lengo. Lakini walitaka Sabrina aache watoto wake nyumbani
kwangu, yeye akaishi kwenu kama kuwaficha wale mapacha wake eti marafiki zake
hao waheshimiwa wasije kuona watoto wa kizungu pale kwenu.” “Haiwezekani!
Maana mama alishavuka huko kwenye swala la wale watoto, hata alikuja Singida
akakaa nao!” “Si huyo hapo akanushe.” Akaongea kwa hasira. “Sina muda wakujibu
shutuma za kijinga.” Mama Msindai akaondoka.
“Hawataki
kabisa wale watoto na anafanya kila awezalo kukutenganisha na Sabrina. Na kwa
taarifa yako tu unacheza mchezo wa hatari sana Jack, mpaka nakuhurumia.
Aliponitenda Willy, alinitenda nikijua ananipenda. Sikujua mapenzi ya
mtu mwingine isipokuwa ya Willy, aliyekuwa akinipigania kwao mchana na usiku
ndio maana tulirudiana kwa urahisi. Lakini wewe Jack, unapita kwenye moyo
uliojaa madonda. Hujaweka hata mizizi, hujatoa hata sababu ya msingi
yakuvumiliwa na kupendwa kweli mpaka kifo, unacheza michezo ya visa
vya mama mkwe wewe! Unachokifanya wewe unatofauti gani na Tino?” “Acha
kunifananisha na Tino, Pendo.” “Haa!” Pendo akakaa vizuri.
“Hujamuacha
Sabrina nyumbani kwangu akiwa na hedhi mbaya, mshono wa uzazi akiwa na watoto
watatu, wewe unanyonya kwa mama yako mkifichiana siri?” “Ni
jambo...” “Acha ujinga Jack. Wewe ni kama mdogo wangu. Lakini nakwambia ukweli
kabisa, samahani naongea hivi mbele ya baba yako na kaka yako, lakini sikujua
kama unaakili ndogo kiasi hiki!” “Pendo unanitukana.” “Hakika wewe ni mjinga wa
mwisho kabisa Jack. Kasirika mpaka urukwe na akili. Sijui utakuwa mbunge wa
namna gani unayeshindwa hata kufikiria! Unauchu wa madaraka mpaka unakuwa
mnyama wakupitiliza!” “Sio uchu wa madaraka.” “Ni uchu huo na mama yako
amegundua huo udhaifu wako ndio anaoutumia. Sasa nikwambie kabisa, umecheza
kijinga, na mama yako amekuingiza pabaya na wewe umeingia kama
likondoo.”
“Kwanza
wewe una katoto kamoja tu na Sabrina, pamoja na mama mkwe mwenye matusi makali
akimdhalilisha vibaya sana. Mwenzio Tino anao...” “Tino si mwenzangu.” “Na
kweli si mwenzako maana yeye anao watoto wawili na Sabrina, na amejirudi
akijutia makosa yake. Hana baba wala mama mkwe wakumkera Sabrina. Anamtaka
Sabrina na watoto wake, tena kwa machozi. Ndipo mtajua kama Sabrina ni mchawi
au ni Mungu wake. Sasa nenda Dodoma, nenda kokote ukawe mbunge, acha
wanaume wenzako waliokwisha shiba pesa, wakayaishi maisha, wakajua familia ni
bora kuliko mengine yote, wakushikie kile mama yako anachokuaminisha
hakina umuhimu. Tutakuona mitandaoni na ubunge wako. Huna aibu wala
shukurani kabisa wewe Jack.”
“Maisha
yako yote ulikuwa Msindai. Hakuna hata gazeti lililotaka kukuweka. Kaka yako na
mama yako si wapo na nyadhifa za juu za uwaziri! Mbona hukuwahi kuitwa bungeni?
Swala la ubunge wa afrika Mashariki kwani limeanza leo? Mbona hushangai mama
yako hakukuweka huko mpaka alipoona Sabrina amekutoa huko mavumbini Singida,
ndio mnaanza fujo za kipuuzi hapa! Mnajidai tu, lakini hamna lolote wanafiki
wakubwa nyinyi mnapenda kutumia watu bila aibu. Haya ondoka, nenda kamfuate
mama yako.” Jack akabaki amesimama.
“Baada
ya dakika 5 ukiwa umesimama hapo, nakuitia askari akutoe hapa kwa nguvu, kesho
uonekane magazetini. Toka na nisikuone tena Jack. Mbaya kabisa wewe, mwanaume
usiye na msimamo, ila uchu wa madara.” “Tulia Pendo mama yangu mzazi.
Utapandisha pressure.” “Hawa si watu baba. Wanyama kabisa, hawa! Huyu Jack
anahangaikiwa na Sabrina akiwa mjamzito mpaka anafanikiwa, hata mwaka
haujaisha, anajidai yeye ni Msindai, mtoto wa mama anamtelekeza Sabrina
akiwa mgonjwa! Huna akili kabisa Jack. Na kaburi mama yako alilomchimbia
Sabrina, linakuzika wewe mwenyewe tena ukiwa hai. Subiri utaona ‘Muheshimiwa Msindai!’
Siku yako inakuja.” Pendo akamdhihaki kwa kumwita ‘Muheshimiwa’.
“Na
msiba huo utalia mwenyewe, maana mama yako pamoja na Jena watakuwa busy
wakisherehekea ushindi wa kumrudisha Sabrina na watoto wake wakizungu
kwa Tino, wewe wamekukabidhisha huyo msichana wanaetaka umuoe.” “Tena naona
kama Tino ameshapata baraka za mama yake Sabrina!” Jack akakunja uso na kumgeukia
Nancy. “Mimi naona wewe upambane tu upate Ubunge, umfurahishe mama yako,
mheshimiwa Msindai. Naona maswala ya ndoa yanahitaji wanaume kwelikweli, wewe
huyawezi. Kapige tu siasa. Sasa kama alivyokwambia Pendo, hapa sisi njaa zinauma.
Tunaomba utupishe, sisi wanandoa tuendelee kudumisha ndoa, wengine siasa
hatuwezi.” Nancy akaongeza.
“Nashauri
Jackson uondoke.” Akaongeza mzee Msindai aliyekuwa kimya kabisa muda wote. “Na
pengine niombe radhi kwa wote. Najua hii si picha mliyokuwa nayo kwa siku ya
leo. Mtuwie radhi. Binafsi nishukuru kwa heshima mliyotupa, acha tupishe hapa,
ili mjaribu kuimaliza hii siku vizuri. Naamini Sabrina atakuwa salama. Muwe na
wakati mzuri.” Jacinta akarudi wakati baba yake ndio amesimama tu. “Jamani
sijampata Sabrina. Nimempigia simu baada ya kumkosa hapa, simu yake haipo
hewani. Na nimezunguka kila mahali hapa mpaka nikauliza walinzi wa pale nje,
hawajamuona. Mwenye simu ya Sabina, naomba.” “Mimi ninayo ya mama yake. Acha
tumjaribishe.” Ikabidi mzee Msindai
asubiri.
Pendo
akampigia mama Sabina. “Bibi harusi!” Ikabidi
Pendo acheke tu. “Mpo na Sabrina hapo?” “Alinipigia
muda tu kuniuliza kama bado tunamaziwa ya mtoto. Alipojua tulishaondoka pale
kwako na watoto wapo sawa, akaniambia anakwenda mahali, atatutafuta baadaye.
Nilifikiri mpo naye!” “Nashukuru mama yangu. Tutawasiliana.” Pendo
akakata bila kutaka kumtia wasiwasi. “Sasa atakuwa amekwenda wapi?” “Sasa hivi
ndio unajidai kuuliza!? Acha kunitia kichefuchefu Jack. Please.”
Akamjibu kwa hasira na kumgeukia Jacinta. “Nahisi naweza kujua alipo, lakini
sitawaambia. Yupo salama dada Jacinta. Nashukuru kujali.” “Unauhakika?”
Akauliza kwa kujali Jacinta. “Kabisa. Wewe kaa ule dada yangu.” “Na kunywa.”
Jacinta akavuta kiti na kukaa.
“Mbona
baba na mheshimiwa Msindai mmesimama?” Jacinta akauliza akivuta glasi yake ya magarita.
“Mimi nilikuwa nikiondoka, mama.” “Bila kula baba yangu!? Mambo yako yote yapo
hapa. Wanyama wa baharini, washaokwa, kazi kutafuna tu baba yangu. Au
nikawaombe wakufungie uende navyo?” “Wewe uniletee nyumbani.” “Usitie shaka
baba yangu. Nikilewa kiasi chakujua sitafika kwako, nitamuomba kaka yangu hapa
akupitishie.” Ikabidi wacheke. “Nashauri usiendeshe baada ya hapa.” “Hilo wazo
zuri baba yangu. Nitalifikiria.” “Naomba utilie maanani, Jacinta. Tafadhali
mama.” “Sawa baba yangu. Mimi mtiifu.” Jacinta akasindikiza za kinywaji
mdomoni, Mzee Msindai akamwangalia huyo binti yake nakuondoka.
“Tushatia
aibu hapa, bora tu kulewa, yaishe.” Jacinta akaendelea huku akinywa, wote
wakacheka. “Kunywa kidogo Junior, kaka yangu. Hamna jinsi.” “Natamani kama
kuondoka!” “Sasa hiyo ndio aibu mara mbili hapa. Au nadanganya Kenton?” Jacinta
akafanya wazidi kucheka. “Kweli tena. Ushaona watu wanaofanya fujo kwenye
harusi za watu, tena tupo tu wachache hapa, halafu tena tuondoke! Jamani
tunyweni, tu.” Akanyanyua glasi juu. “Jamani, kwa Willy na Pendo.” “Kwa Willy
na Pendo!” Wote wakanyanyua glasi na kugongesha.
“Pendo
naomba tuzungumze pembeni kidogo.” “Acha kunisumbua Jack. Nilikuwa nyumbani
tokea tulipoachana hospitalini. Ungekuja.” “Nashauri Jackson uondoke.” Kaka
yake akaweka msisitizo. “Unanisikia Jackson?” “Sawa. Lakini mimi si msaliti, nampenda
Sabrina na wala sijamtumia tu. Hapa nilitaka kujua Sabrina alip..” “Kwa
nini sasa hivi Jackson? Kwa nini iwe kwenye shughuli ya mwenzio?” Junior akawa
mkali kabisa. “Uharaka huo unatoka wapi?” “Basi kaka. Lakini nia ilikuwa nzuri
tu tokea mwanzo. Sikuwa nafanya siri. Ila..” “Nafikiri unazungumza na watu
ambao sio sahihi kabisa Jackson. Hayatuhusu. Sijui kama unaelewa?” “Sawa kaka.
Na samahanini sana jamani.” Kimya. “Mimi naona wewe ungeondoka tu, washawachoka
kina Msindai.” Jacinta akajibu akiendelea kunywa huku akizungumza. Jackson
akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
0 Comments:
Post a Comment