Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 50. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 50.

 Willy kwa Junior.

Jackson alipotoka tu Willy akampigia simu Junior. “Samahani kaka. Najua usiku na umepumzika. Ila nimekwama. Nina shida.” “Hamna shida. Karibu.” “Naomba unisimamie harusi siku ya jumamosi, ila kesho ambayo ni siku ya kazi tunahitajika kwa mchungaji mida ya saa nne na nusu asubuhi. Nimekwama kaka, ndio maana nakuomba wewe. Sina watu. Nilipoteza ndoa na marafiki pia.” “Pole sana. Labda niulize kwa Jackson imekuaje tena? Nilisikia yeye na mkewe wangewasimamia!” “Kwanza  nafikiri Sabrina anakaribia kuwa aliyekuwa mkewe, pili Jackson kesho ana mambo ya Ubunge wa Afrika Mashariki. Kesho ndio siku yenyewe.” “Hebu twende taratibu Willy.” Ikabidi Junior akae sawa.

          “Ndio hivyo kaka.” “Tuanze taratibu. Unasema Jackson Msindai anagombania kwenye Ubunge wa Afrika Mashariki!?” “Ni siri yake na mama yenu hata sisi wenyewe tumejua leo. Hata mkewe amesikia leo wakiwa hospitalini, Jena aliropoka tu kama kawaida yake unavyomjua Jena.” “No way! Yaani Sabrina mwenyewe amejua leo!?” “Acha kaka, ni mambo yakusikitisha.” “Sabrina amehangaika sana na Jackson!” Kidogo kikaonekana kumsumbua Junior. “Ndio chakuumiza na hapa tunavyozungumza, yupo kwa mama yake, ameacha mzazi hapa.” Willy akamueleza mengi mno ya uchungu na kumshangaza sana Junior.

          “Kwa hiyo nimekwama kaka. Naomba msaada wako unisimamie.” “Hilo halina shida. Lakini naomba nikuombe kitu Willy.” “Nakusikiliza kaka.” Walimjua Junior kwa hekima. Akatulia akitaka kusikia hizo hekima zake usiku huo akiwa hajui hatima yake na msimamizi wake. “Tafadhali usimkatie Jackson tamaa. Naomba mvumilie. Najua unaweza usimuelewe sasa hivi, lakini atakuwa kwenye kipindi kigumu sana, ambacho atatuhitaji tu. Naomba mimi nije kesho hapo kanisani. Nifanye yote yanayohitajika, ila kwa niaba ya Jackson, na nitamwambia mchungaji. Mafundisho yote mimi nitarikodi kwa ajili yake. Akishindwa kutokea kabisa kesho, basi akimaliza shughuli zake nitampa ajue ni nini  mchungaji alitaka asikie yeye kama msimamizi.” “Sasa na jumamosi siku yenyewe ya harusi asipotokea?” Willy akasikika kutoridhika.

          “Atakuwepo kwenye harusi. Na kama asipokuwepo basi mimi nitasimama badala yake. Tafdhali Willy. Nikuombe kwa niaba yake. Sisi ni ndugu, tusikatiane tamaa. Na unamjua Jack. Anampenda mke wake na watoto wake, pamoja na familia yako. Katika hili naomba tumsaidie. Ili jambo jema lisigeuke kuwa baya.” “Ndio nashangaa sasa!” “Ni kweli anachofanya ni kitu kizuri sana, ila utekelezaji wake ndio umekuwa mbaya tu. Lakini anafanya kitu sahihi. Tafadhali mvumilie.” “Nimekusikia kaka. Na asante. Najua unamajukumu mengi.” “Hata hilo ni moja ya jukumu la muhimu sana. Ndoa ni msingi wa kila kitu. Nakupongeza sana.” Willy akacheka akisikika ametulia sio jazba kama alivyoanza. Akashukuru na kukata simu akiwa ametulia kabisa.

Jacinta.

M

ida ya saa 12:30 asubuhi Jacinta akawa amefika hapo nyumbani kwa Pendo. Sifa akamfungulia. “Wote bado mmelala? Nimekuja kumuona mzazi kabla siku haijawa na mengi.” “Mimi na bibi tulishaamka. Hata dada Pendo yupo macho chumbani kwake, amepita hapa sasa hivi kutoka kumwangalia mzazi.” “Basi acha nianzie kwa Pendo.” “Umependeza dada!” Jacinta akacheka. “Asante Sifa. Mama shikamoo.” Mama Sabina akaitika na kutoka kusalimiana na Jacinta. “Na kweli umependeza.” “Asante. Acha nizungumze na hawa warembo wawili kabla sijachelewa kazini.” “Karibu dada Jacinta. Kama kawaida yako umependeza.” “Asante. Sasa mbona asubuhi asubuhi na mifuko?” Jacinta akamuuliza Pendo. “Nampelekea Sabrina. Twende, yupo macho.” “Hatutaamsha watoto?” “Wanae wana mida yao yakuamka. Hapa tulikuwa tukizungumza tokea saa 11 asubuhi usingizi uliponiishia.” “Naona mtakuwa na kazi yakucheka tu.” Willy naye akatoka chumbani kwake na kumsalimia Jacinta, ndipo wakaelekea chumbani kwa Sabrina.

          “Karibu. Nasikia sifa za kupendeza kwako, nikawa nakusubiria. Shikamoo.” “Marahaba Sabrina, hujambo?” “Mimi naendelea vizuri, namshukuru Mungu.” “Mshono?” “Naona unaendelea vizuri kwakweli. Njoo ukae hapa kitandani, usisimame muda mrefu na kiatu kirefu.” “Nishazoea. Majukumu niliyonayo yanataka kiatu kirefu muda wote kazini. Usijali. Ila nakaa ili mniambie nini kilitokea jana hospitalini.” Sabrina na Pendo wakaangaliana. “Ni nini?” “Sabrina hataki kusema eti anaogopa kuwa mchonganishi.” “Wala si uchonganishi, ni ili na wewe ueleweke Sabrina. Umesikia wifi yangu?” Sabrina akanyamaza.

          “Usiache watu wakakusema vile watakavyo. Iwe wamechagua tu, lakini ukweli ujulikane. Niambie nini kimetokea.” “Mama Msindai hataki hawa wanangu wawili, wifi.” “Unamaanisha nini?” Jacinta akakaa pembeni ya kitanda. “Acha mimi nikusimulie dada.” Pendo na yeye akakaa. “Jana sisi wawili tulikwenda kutembea kama mazoezi, tukawaacha Jena na mama yenu wakiwa na mtoto. Jack alikwenda kulipia. Wakati tunarudi tukawasikia wakimsema Sabrina vibaya sana. Pamoja na mimi.” Pendo akamasimulia Jacinta mwanzo mpaka mwisho, Jacinta akabaki ametoa macho.

          “Haiwezekani!” “Ila hata Jack hajui haya.” Sabrina akaongeza. “Kwa nini?!” “Wifi, Jack yupo kwenye ushindani. Mama yake akitaka afanye anachotaka, sitaki tena mimi nikazidi kumchanganya halafu ikawa lawama. Acha afanye anayoshauriwa na mama, mpaka afike mwisho, nisije laumiwa baadaye.” “Wala hutaacha kulaumiwa.” “Asante dada Jacinta. Na mimi nimemwambia hivyohivyo Sabrina.”

          “Nisikilize Sabrina. Mimi namjua mama. Ulipo hapo na Joy, wifi yetu alifikishwa kasoro tu, Junior sio mtoto wa mama kama Jack, ndio maana Joy alipita. Mumewe alisimama naye mpaka mama akaelewa kuwa Junior hataki mchezo kwenye ndoa yake. Sasa kwa Jack ni tofauti. Jack ni mtoto wa mama yule ambaye hakui, na ni marafiki wa kuzungumza hata saa sita usiku. Kwa miaka yote unayojua Jack anayo, mama ni rafiki wake wakaribu mno, ndio maana unamuona safari hii amekamatwa na hana jinsi yakujitoa. Nilimkuta jana nyumbani, Jackson  hakuwa na furaha kabisa. Ni kama aliyekuwa njia panda. Na mama akahakikisha anatuonya kabisa na kututenga na Jack. Hakutaka kabisa tujue kinachoendelea.”

          “Yaani mimi, ndio nimeambiwa na Junior jana usiku baada ya kuzungumza na Willy kuwa Jack anagombea Ubunge na wewe hujui. Ndio tukaelewa ni nini kinaendelea, ila hatukujua kama mama hakutaka watoto waende pale, ndio maana mimi na Junior tukaona nije tuzungumze vizuri na wewe. Na ujue ni kweli mama hataki kumshiriki Jack na yeyote yule hata sisi ndugu zake pia hataki. Mimi na Junior ndio maadui wakubwa wa mama sababu ya Jackson. Na anafanya hivyo kwa mapenzi tu aliyonayo kwa Jackson. Naomba umsamehe Jack. Tafadhali Sabrina. Muhurumie tu na uelewe alipo sasa hivi. Mama ana ushawishi wa hali ya juu, najua kwa sehemu na wewe umeshamfahamu.” Sabrina akacheka na kunyamaza.

          “Na wote tunajua jinsi Jackson anavyokupenda Sabrina. Si kwa kinafiki, Jack anakupenda. Alikosana na mama kwa ajili yako. Ili tu kukuoa.” Sabrina akajifuta machozi. “Kweli. Mimi nilikuwepo wakati Jack akikugombania. Yupo kwenye wakati mgumu na haya yote pia anaona yatakuwa na manufaa kwenu wote ndio maana unamuona ameangukia kwenye mtego kirahisi. Na mama ametumia hiyo njia makusudi akijua udhaifu wa Jackson. Mama yetu anaakili Sabrina, anayo akili ile ya kufikiria kwa haraka na mbali. Ngumu kumshinda, mpaka uwe na akili na moyo kama wake, ndipo utamuweza. Hivihivi, sio mrahisi. Kwa hiyo vumilia tu. Ila huu ndio msimamo wetu mimi na Junior.” Sabrina akamwangalia.

          “Safari hii hatutazungumzia chochote kama mama anavyotaka. Tutawaacha tu waendelee mpaka mwisho. Akifanikiwa, tutatoa pongezi kama wengine, ili mama apate huo utukufu anao uhangaikia, pengine atatulia. Hatutazungumza lolote ila kuwa watizamaji tu. Kwa hiyo tunaomba na wewe usikate tamaa. Ukweli jambo analofanya ni zuri sana tu. Ubunge wa Afrika Mashariki sio jambo baya, na lingemuongezea sifa na bado angerudi kugombania huko Singida. Ila tu mama amelifanya liwe baya mpaka kutenganisha familia! Tena bila sababu mpaka linashangaza! Ukitaka chochote kile, mimi na Junior tupo kwa ajili yako.” “Nashukuru Wifi yangu. Ila naomba mimi nikasubirie huko Singida.” Sabrina akajifuta machozi.

          “Naweza kurudi huku kama itahitajika, lakini tuna miradi mingi na muhimu sana tulianzisha na Jackson. Siwezi kuiacha katikati tu! Mimi ndivyo nilivyo wifi. Nikianza jambo najisikia lazima kumaliza.” “Inaeleweka Sabrina, na hiyo nayo ni sifa aliyokusifia Jack pale nyumbani.” Sabrina akacheka na kuinama. “Sasa kwa muda gani?” Akauliza Pendo.

          “Ni kwa muda tu dada. Ikishasimama, tukapata wasimamizi wazuri, sio ikafa mara tu tutakapoondoka! Nikijiridhisha ipo sawa na imesimama, na Mungu amenipa kibali chakuondoka, basi nitaondoka. Lakini sio sasa, tena ghafla! Sitaweza.” “Basi popote ulipo jua mimi na Junior simu yako itapokolewa wakati wowote.” “Nashukuru sana wifi yangu, na asante kunisikiliza.” “Karibu na acha kulia. Usilie tena. Una watoto wanao kuangalia. Tulia kabisa fanya kile unachoweza kufanya. Mengine yatasubiri tu.” Sabrina akajifuta machozi na kutulia. “Ewaa!” Wakacheka vile Jacinta alivyosema kama kufurahishwa na Sabrina kutulia kwake. “Basi acha mimi niwahi kazini, tutaonana baadaye. Pendo unitafutie wine bwana. Nikitoka kazini niikute.” “Usijali dada yangu. Nikitoka kanisani nitaenda kukununulia, uikute hapa.” “Hayo ndio maneno.” Jacinta akatoka.

Kanisani.

P

endo na Sabrina walitoka nyumbani bila yakuchelewa kwa makubaliano wakutane na Willy pamoja na Junior huko kanisani. Wakamkuta Willy alishafika. Pendo akaanza kucheka. “Kweli mpenzi wangu ameamua kuoa jamani!” Sabrina akacheka wakati wakiegesha gari. Waliwahi dakika 20 kabla ya miahadi na mchungaji, kwa hiyo hata mchungaji hakuwa amefika bado. “Acha nikamchokoze wakati wewe unasubiria hapa.” “Msalimie.” Pendo akaegesha gari vizuri na kushuka, akamuacha Sabrina amepoa garini.

          Baada ya muda kidogo wakaona gari ya Junior ikiingia. Akaegesha na yeye, kisha akatoka kwenda kumsalimia Pendo na Willy, akazungumza nao kidogo akamfuata Sabrina pale garini alipokuwa amekaa. “Niambie shemeji! Umemuacha wapi kaka?” “Babu yake alipokuja kumuona jana usiku, akampima mapafu, akasema ni wa kupewa jembe akalime uwele. Si wakupakata tena.” Junior akacheka sana. “Kama mtaalamu Msindai ametoa baraka zake, basi anastahili kwenda shamba.” Wakacheka kidogo.

          “Naomba niingie garini tuzungumze kidogo.” “Karibu shem.” Junior akapanda garini. “Hapa mlipo wewe na Jack, mimi na Joy tulishapitishwa. Ila sisi tukasimama, Joy akanivumilia mpaka mama akaelewa. Ninachotaka kukwambia ni hivi, Jackson anakupenda sana, mnayo ndoa nzuri mno, usikubali kuipoteza. Na usifikiri ni kwa hili tu, itachukua zaidi ya hili na mengine mengi mpaka mje kuwa ukurasa mmoja na mama, na pengine pia mnaweza isije ikatokea mkawa ukurasa mmoja kwa maisha yenu yote, lakini simama na mumeo.” “Nasimama naye vipi wakati sijui linaloendelea shem!? Mimi nimesikia jana! JANA! tena kwa bahati mbaya, hata Jack hakuju kama nipo chooni, Jena aliropoka tu.” Sabrina akalalamika.

          “Kwanza nataka ujue hiki anachokifanya Jackson ni jambo zuri sana. Binafsi natamani angenishirikisha ili nimshauri vizuri na kumsaidia maandalizi mazuri akajiongezea nafasi kubwa yakushinda! Lakini imetokea kama ulivyoona. Hakuna jinsi yakubadilisha tena. Sasa hivi yupo huko, amenipigia kuniomba nikutafute hata kwa simu nijue unaendeleaje kisha nimjulishe.” Sabrina akaona machozi yanamtoka. “Naweza kuelewa wakati mgumu alionao yeye Jack, zaidi hofu yakuona ameharibu na anajisikia kama ni msaliti. Mimi na Jacinta tumeamua kutomwingilia kabisa mpaka mwenyewe azungumze. Asipolizungumzia, hatutamuuliza wala hatutataka kujua.” Sabrina akanyamaza.

          “Kwa sasa, unahitaji kitu chochote?” “Labda nikuombe msaada wakunirudisha mimi, watoto na mama yangu, Singida. Kama nilivyomwambia wifi Jacinta, kuna mambo nasimamia. Nikiyaacha sasa hivi, kazi yote ile mpaka na nyinyi mkaja kutuunga mkono, itakuwa bure kabisa. Naomba nisaidie hilo tu.” “Unataka kuondoka lini?” “Sitaki Pendo na Willy watoke kwenye fungate, wakute nyumba yao bado imejaa. Hata yule msichana wao wa kazi wamempa likizo. Baada ya harusi tu, anakwenda kwao. Na mimi naomba iwe hivyo. Ikipatikana ndege ya jioni, ningeshukuru.” “Na mshono huo utaweza kusafiri?” “Kabisa shem. Acha nikatulie nyumbanni na wanangu walipopazoea na patulivu. Huku kwenye majumba ya watu ni kama wanakuwa kero.” “Basi acha niangalie, nitakujibu jioni nikija kumuona kaka na dada zake.” “Nashukuru sana.” wakamuona mchungaji amefika, wakashuka garini. “Acha nimuwahi nizungumze naye.” Junior akaongeza mwendo kwa haraka akimfuata mchungaji.

          “Waziri Msindai!” “Heshima yako mzee wangu.” Akampa mkono. “Unafanya nini hapa!?” Wengine wakasogea. “Nikuombe tu. Jackson, mdogo wangu, ndiye msimamizi wa hii harusi. Amebanwa kwenye majukumu mida hii ameshindwa kufika hapa. Naomba niwepo hapa kwa niaba yake. Nichukue hekima zote kutoka kwake, kwa makini mpaka na kukurikodi kabisa, kisha nikamuhamishie yeye. Tafadhali sana mchungaji. Najua sio utaratibu wenyewe, ila nikuombe tu.” “Haina shida kabisa. Na kama ningejua, tungebadili muda.” “Willy anataka kuoa. Hilo lakubadili muda tumelitoa kwenye mjadala.” Wakataniana kidogo, ndipo wakaingia ofisini na kuendeleza ratiba ya siku hiyo.

 Nyumbani kwa Pendo.

I

lipofika jioni chumba alichopewa Sabrina kikawa kimejaa kelele na vicheko. Joy na wanae walifika hapo mara baada ya kuwatoa tu shule. Jacinta naye akafika hapo na kudai wine aliyoagiza. Akawa amekaa akinywa huku wakicheka, Willy naye alitoka kazini akawepo hapo, na Junior naye akafika hapo. Vicheko vikaendelea wakati Sabrina amejilaza. Mara na Jack naye akaingia. Binti zake walikuwa wakicheza na Claire, wote walipomuona ameingia wakanza kilio wakimtaka. “Hapo tena habari imebadilika. Si mlikuwa mmetulia nyinyi!?” Jacinta akawachokoza lakini hata hawakumwangalia. Wote wakamsogelea Jack, akawabeba na kuwabusu. “Hata mimi nimewasi. Mnaendeleaje!” Wote wakambusu kwa pamoja, watu wote wakacheka.

          “Haya mabusu ndio nayamisi zaidi. Haya, mbusuni tena dad!” Wakarudia tena na kujipigia makofi, kila mtu akacheka. Angalau akakuta mazingira ya hakuna anayemwangalia tofauti, akasogea nao mpaka pale kitandani. “Vipi Brina?” “Safi tu.” Akajibu Sabrina kwa sauti ya chini macho kwa watoto wake. “Sasa hayo machozi si mjifute nyinyi wawili!” Wakajifuta na kushangaza wote. “Kumbe wanaelewa!?” “Wanaelewa sana. Ila tu wamegoma kuongea. Sasa sijui sababu ya shuguli!” Sabrina akaongeza. “Brayan anaendeleaje?” Jack akaendelea kuuliza. “Naona huyu mlalaji. Na kelele zote hizi hajaamka hata kidogo.” “Kunyonya?” “Ukimsogeza kwenye ziwa anafungua mdomo na kunyonya bila shida.” “Hata chupa yake ni hivyohivyo. Ukimuwekea tu mdomoni, ananyonya.” Akaongeza mama Sabina. “Afadhali.” Akamalizia Jackson, na kurudisha macho kwa binti zake.

Stori zikaendelea na vicheko. Jack kimya na binti zake wakatulia hapo begani kwa baba yao. Uchangamfu wao ulitegemeana na baba yao. Akiwa amechangamka, na wao wanachangamka, Jack akitulia, na wao wanatulia. Wakatulia kimya wengine wakizungumza mpaka bibi yao alipowataka wakale, Jack akatoka nao kwenda kuwalisha. Sabrina hakuwa hata akimwangalia Jack.

Ilipofika kwenye saa mbili baada ya wote kumaliza kula Joy akaaga na watoto wake kwa ajili ya shule kesho. “Kuna watakaolia kuamka hapa kama wasipopata usingizi wakutosha.” “Ni Claire huyo! Mimi siliagi.” “Sasa kwa nini umtaje ili aanze kulia hapahapa! Utalia wewe Clei!” “Mimi siliagi asubuhi. Muongo tu Clei.” Akaanza kulia Claire. Watu wote wakaanza kucheka. “Umefurahi sasa?” Mama yake akamtisha, Clei akakimbia pembeni. “Basi mwanangu. Lakini pia naona muda wako wa kulala umeshaanza kupita. Si hata macho yameanza kuwa ....” “Na machozi.” Akamalizia Clei kwa baba yake nakufanya wazidi kucheka.

“Hakika uatalia Clei wewe!” Clei akakimbilia nje, mpaka baba yake akacheka. “Mimi macho hayajajaa machozi mimi!” Hapo Claire anaongea machozi yapo kifuani. “Njoo mama. Wanakusingizia?” Baba yake akamuuliza, kidole akapeleka mdomoni akamwendea baba yake akilia. “Kwani dad mimi macho yangu yamejaa machozi?” “Njoo mama. Mimi nilitaka kusema yamejaa usingizi. Si ndiyo?” Akatingisha kichwa kukubali. Shangazi yake akawa anacheka mpaka machozi. “Mimi naona kuna wanao onewa kwa kuwa wakweli.” Akaongea Jacinta kwa sauti ya chini.

“Clei mchokozi, anti. Anapenda kunichokoza tu.” “Na mimi nimemuona anti. Usilie basi, asije sema kweli macho yako yamejaa machozi.” Mpaka mama yake akacheka. “Mimi silii tena.” “Nakujua wewe sio mliaji, Claire wangu.” “Clei ananisingizia?” Akamuuliza anti wake akiwa amepakatwa na baba yake. “Nikuulize Claire, kipenzi changu?” Jacinta akamuuliza kwa upendo, akatingisha kichwa kukubali, kidole mdomoni. “Eti kwani ukiamshwa asubuhi kwenda shule wewe huwa unalia?” “Kidogo tu, halafu nanyamaza.” Walicheka wote mpaka Sabrina akashika tumbo asitoneshe mshono. Walicheka sana. “Mimi naona dad atusindikize kwenye gari, asije akalala hapahapa. Si ndio Claire mwanangu?” Akamkubalia mama yake kwa kutingisha kichwa, Junior akasimama na mwanae huku akicheka.

“Sasa maadamu nishakula hapa, nikifika ni kuoga na kulala, siku imeisha. Nashukuru Pendo mdogo wangu. Mzazi wewe, kesho tena. Acha na mimi nikalale naona na mimi macho yameanza kujaa usingizi.” Wakacheka tena. “Basi raha yake Clei ni kumuona mwenzie analia hivi kila wakati.” “Sasa kaka yao mbona mtulivu sana?” Sabrina akauliza. “Huwezi kumsikia.” Akaongeza Jacinta akisimama. “Yupo kama baba yao, ukimya.” “Halafu nahisi anajiona mkubwa sana kwao hawa wawili, hawafuati nyuma kama hivi unavyomuona Cleiton kutwa nyuma ya Claire mwanangu akitafuta chakumliza. Halafu anapenda sana kusoma vitabu. Hapo yupo chumbani kwa Willy amekutana na vitabu huko, ndio maana umemuona amekuja hapa kwa baba yake, amemuonyesha kile kitabu na kumuuliza kama kinafaa kusoma. Baba yake alipokiangalia na kukipenda, ndio ukamuona anamnong’oneza Willy, pale alikuwa akimuomba kile kitabu.” “Kumbe!” “Ndivyo alivyo mwanangu yule. Hapo anakisoma, hatatoka hapo mpaka amalize au nikamtoe huko. Huwezi kumkuta akimfanyia fujo dada yake.” “Kwanza hataki kumuona hivi akilia.” Akaongeza Junior kwa mkewe.

“Sasa starehe ya Cleiton yeye ni mpaka mwenzie alie.” Wakaendelea kucheka. Junior na Jacinta wakijiandaa kutoka. “Usiku mwema Sabrina. Ulale salama na watoto. Na mimi naona niondoke nao hawa, tufike nyumbani pamoja.” “Nashukuru shem. Mungu akubariki. Na Joy asante kwa supu. Nzuri kweli naona mwenzangu Pendo ana kazi yakuongeza tu!” Wakacheka. Wote wakawa wakiondoka. Willy na Pendo ikabidi kuwasindikiza, Sabrina akabaki hapo na mtoto wake.

Jack akarudi ndani kwa haraka. “Jana nilikuja nikakuta mlisha lala.” Sabrina akatulia tu. “Naona nyumba imejaa sana, mpaka unalala na mama hapahapa!” akaendelea Jack, Sabrina kimya hata hakuwa akimtizama. Akamuweka sawa mtoto, akasimama kuelekea chooni. “Vipi maumivu?” “Naendelea vizuri.” Hapo Sabrina akajibu. Jack akawa anamfuata nyuma. Ikabidi Sabrina asimame na kumgeukia. “Nakwenda chooni Jack!” “Najua. Ila nakupenda Brina. Mimi sitakusaliti. Na mimi sio kama Tino.” “Nimebana haja ndogo kwa muda mrefu sana sababu ya wageni. Naomba nikajisaidie tafadhali.” “Sawa. Ila kaka alinitumia mafundisho yote ya kanisani, harusi nasimamia mwenyewe.” Ikabidi Sabrina aondoke tu.

Choo kilikuwa nje tu ya chumba hicho anachotumia na wanae. Jack akaendelea kumfuata hata Sabrina hakugeuka tena. Akamfuata mpaka chooni, akasimama nje ya choo. “Kungekuwa na nafasi hapa, leo ningelala hapa. Ila naona nyumba imejaa! Au tuhamieni wote kule kwa mama?” Jack akaendelea kuzungumza, Sabrina akawa akimsikiliza kule ndani chooni. “Nimewamisi Brina. Nina hamu na wanangu. Kwa nini tusiende wote kule kwa mama?” Sabrina kimya, mama yake akisikiliza tu asielewe.

“Brina!” Sabrina akatoka na kumpita hapo mlangoni. “Basi mimi niondoke na kina Jeiline. Maana nimeambiwa wanalala chini.” “Usithubutu. Nilipo mimi ndipo na wao watakuwepo. Hata kama ni sakafuni.” Sabrina akajibu huku akirudi chumbani, Jack akimfuata nyuma. Pendo na Willy wakarudi ndani. Pendo akapitiliza chumbani kwa Sabrina, akamkuta na Jack akataka kutoka. “Njoo dada, unisaidie kitu.” Sabrina akamuwahi kabla hajatoka.

“Nini?” “Huu mfuko ulioniletea sijaelewa.” “Sasa mwenzio hizo zilikuwa zikinifaa haswa. Maana nilikuwa nikianza hedhi ni mpaka kwenye mashuka. Basi nikivaa hizo pullup diaper, nalala bila wasiwasi yakuchafuka. Kwa hiyo jaribisha. Utalala vizuri.” “Kwani bado unapata hedhi nyingi?” Hakuna aliyemjibu Jack. Sabrina na Pendo wakaendelea kungalia mfuko. “Nenda ukaoge, ujaribu.” “Kweli nikaoge ndio nije ninyonyeshe.” “Au turudi hospitalini, Brina.” Jack akaendelea bila kuchoka akijikomba. Sabrina akachukua taulo na nguo pamoja na mfuko, akarudi bafuni, Jack naye akamfuata. “Unataka nikusaidie nini, Brina?” “Kunyamaza Jack!” “Mpaka saa ngapi?” Sabrina akanyamaza. “Brina?” “Nenda kapumzike Jack, tuache wenye nyumba na wenyewe wapumzike, tafadhali.” “Basi niogeshe watoto ndio niondoke.” “Bibi yao ameshawaogesha ndio maana unaona wapo kwenye nguo za kulalia.”  “Kweli!” “Hii nyumba tunawahi kulala na hatutaki kelele na wewe unajua Jack. Nenda kwenu.” Pendo akamfukuza.

“Namsubiria Sabrina.” “Huna haja yakusubiria. Nenda kalale.” Sabrina akajibu. “Haya nenda ili Willy wangu afunge milango, tulale. Kesho anakwenda kazini kama kawaida.” “Halafu kaka Junior alinitumia mafundisho yote ya kanisani. Nishayasikiliza na nimeyafanyia mazoezi.” “Wewe nenda bwana Jack. Unakuwa msumbufu tu. Unakuja mida watu tunataka kulala!” “Basi acha nimsubirie Brina nimuage.” “Nakusikia Jack.” “Kesho basi. Nikujie na nini?” “Sihitaji kitu.” “Basi kesho. Mlale salama. Acha nikaage wanangu. Nahisi wapo chumbani kwa Sifa.” Kimya. Jack akaondoka bila ya kujibiwa.

Ijumaa.

Siku ya ijumaa Jackson hakutokea kabisa pale nyumbani wala hakupiga simu. Mida ya mchana Sabrina na Pendo walikwenda saluni kufanyiwa matengenezo ya nywele, kucha na uso kwa sababu harusi ilikuwa asubuhi ya siku inayofuata, hawakutaka kuchelewa kanisani wala kwenye chakula ambako ndipo walipokuwa wamealika wageni wao wote. Willy alikwenda kazini kama kawaida, likizo yake ilikuwa ikianza rasmi siku ya jumatatu.

Alirudi nyumbani wakaanza kusaidiana na mama yake kufungasha sababu ya safari ya kurudi Singida kesho yake. Mama yake akashindwa kuvumilia, ikabidi kumuuliza Sabrina. “Nataka tu kujua Sabrina mwanangu. Ni nini kinaendelea kati yako na Jackson? Maana ulitakiwa ukakae huko kwao kwa uzazi, umerudi hapa na yule mama simuoni wala mumeo!” Ikabidi Sabrina akae chini amueleze mama yake. “Una maumivu?” “Hata. Naona nipumzike wakati nakwambia. Kiiuno kinauma.” Sabrina akaweka na nguo za mtoto pembeni alizokuwa akikunja.

“Jack ni mtoto wa mama yule wakuambiana siri zile za ndani. Mama yake hataki mtu yeyote awe karibu na Jack isipokuwa yeye. Jack kunipenda mimi ambaye nilishamkataa mara nyingi tu na yeye kujua, akaja kunioa wakati nina mimba ya hawa mapacha, na Jack kunisifia kuliko yeye, kinamuuma yule mama. Haamini kama ni jambo la kawaida ila natumia nguvu za giza kwa mwanae. Ndio vita hiyo iliyokuwepo. Na naomba kukwambia tu ukweli mama yangu. Maana nimekuona umesimama na mimi kwenye ulezi wa watoto wote bila kuchoka. Yule mama ameshindwa kabisa kupokea hawa watoto wakizungu.” Ikabidi mama Sabina akae sasa.

“Maadamu umeanzisha haya mazungumzo, acha niulize. Maana nilikuwa sijui naulizaje.” “Kujibu maswali yako yote na mengine ambayo pengine utashindwa kuniuliza, hawa watoto nilipata mimba mtaani tu. Baba yao amezaliwa na mama mwenye asili ya kizungu kama unavyowaona hawa. Hawa ndio wamebeba damu kali ya huko kwa bibi yao kuliko hata huyo baba yao. Sasa huyo baba yao hakutaka nizae hawa watoto ila kutoa mimba. Mimi nikaachana naye, nikaamua kutunza hawa watoto yeye akiwa ameridhika niliitoa mimba maana aliniacha hospitalini akidhani nimetolewa mimba kumbe nilimuomba daktari tumdanganye. Kufupisha stori, Jack aliniomba anioe na ujauzito wa hawa kina dada wawili, ndio mama yake anahangaika sasa hivi.” Sabrina akaendelea.

“Nilimkuta Jack kule Singida panamshinda. Nikamtia moyo na kuanza kufanya mengi kwa upande wa mambo ya siasa. Kama unavyomsikia Jack kwenye vyombo vya habari akimshukuru sana mkewe, bila hila na kwao hivyohivyo, basi yule mama anatafuta na yeye kuyafuta yote hayo abakie akisifiwa yeye na Jack.” “Mmmh! Sasa atafanyaje?” “Kwanza kumtenganisha na huyu kaka yake waziri na huyu dada yake unao waona kutwa wapo hapa kunitembelea. Maana wao wanamshauri tofauti na anavyotaka yeye kummiliki. Na pili, kumtafutia aina nyingine ya ubunge ambao yeye mama Msindai ndio atajulikana amemwezesha, apate sifa. Ndio hekaheka unayoona inaendelea, Jack hayupo, yupo kwenye kinyang’anyiro cha Ubunge wa Afrika Mashariki. Tena kwa siri wote tulikuwa hatujui.”

“Mbona jambo la kheri analifanya vibaya!” “Kila mtu anashangaa mama yangu! Sasa kujibu swali jingine ulilouliza mwanzoni, yule mama hataki hawa watoto wangu wa kizungu wakaishi pale kwake. Tuliwasikia wakinisema na wanangu kule hospitalini kuwa hawawataki wakaishi pale kwake, eti wawe wanakuja kunisalimia mimi na Brayan kwa muda mimi nitakao kuwa pale. Ndio na mimi nikawaambia sitakwenda tena kwake. Nilipo mimi, ndipo watakapokuwepo wanangu wote!” “Haiwezekani!” “Hakika mama.” “Sasa Jackson akasemaje?” “Hakuwepo na wala hajui. Hapo alipo anahasira kwamba nimembadilikia, sikwenda kwao. Ndio maana unamuona hivyo.” Mama Sabina akazidi kushangaa.

“Sasa kwa nini na wewe hukumwambia?” “Asante mama.” Pendo akaingia. Sabrina akacheka. “Da Pendo na wewe umo!” “Mama amekuuliza swali kama la dada Jacinta. Mjibu.” “Nisikilize vizuri mama yangu. Jack tayari yupo kwenye siri na mama yake. Wapo kwenye mipango ambayo mama yake amefaulu kumteka moyo mpaka amekubali. Sasa wameshaanza mchakato, sitaki nikawa sababu ya mimi kuwachonganisha katikati ya haya yote, akashindwa huko, nikaonekana mimi ndiye niliyeingilia na kumchanganya. Nimemuomba Jacinta na yeye asiwaingilie kabisa. Tubakie sisi ni wabaya mpaka hili la Ubunge liishe. Kwani ubaya huwa unajificha mama yangu? Utakuja kujulikana tu.” “Mimi nakuunga mkono Sabrina. Mahusiano ya mama na mtoto huwa hayaishi hata iweje. Usijiingize katikati yao. Acha yawashinde wenyewe.” “Asante kunielewa mama yangu.

“Mwache yeye akatae wajukuu zangu wa kizungu. Ninavyojivunia mimi!” Pendo na Sabrina walicheka sana. “Hakika tena. Hata magazetini wanitoe nao. Nawapenda kweli! Na naona wenzangu kila kukicha wanazidi kuwa wazungu!” Sabrina alicheka sana. “Basi mimi nilikuwa nikimuomba Mungu siku moja waje waamke weusi.” “Koma wee!” Mama Sabina akamkemea mwanae kwa mshituko kabisa. Pendo alicheka mpaka akakaa. “Mama hutaki tena weusi?” Akauliza Pendo akicheka. “Kwani yeye Sabrina ndiye kawaumba! Asitafute balaa. Muumbaji mwenyewe kataka wazaliwe wazungu, leo unaomba nini! Si hao wanakuwa bila huyo mama? Watakuwa tu, na lile alilokusudia Mungu juu yao litatimia.” “Amina mama yangu. Nakushuru. Na asante.” “Amina.”  Na Pendo naye akapokea neno la baraka wakaendelea kufungasha.

 Ilipofika jioni ndugu wakaanza kuingia tena. Upande wa Pendo na Msindai. Bwana harusi yuko wapi?” Pendo akaanza kucheka. “Sitaki Nancy.” “Mbona mimi nimeuliza kwa wema tu.” “Kaenda harusini.” Watu wakaanza kucheka. “Mzee Ngoi kapatikanika!” “Willy katoka kunipigia simu, anasema kumbe ni harusi ya ukumbini kabisa. Anakaribia kurudi. Anasema kuna shangwe utafikiri Zelda anaolewa na kijana!” “Waw! Ndugu zake je?” “Anasema hajawaona mahakamani labda ukumbini hapo baadaye. Ila Willy mwenyewe nimemlazimisha angalau atokee tu.” “Bora. Mambo mengine ni kuepuka lawama tu. Mzee kama yule kupiga simu kabisa si jambo dogo.” “Halafu bado ni baba yao. Hata wafanye nini bado ni baba tu.” Akamalizia baba yao hapo kwa mkewe.

Stori zikaendelea Jack hakuonekanika na hakuna hata aliyemzungumzia hata kumuulizia kama alitokea pale. Bado mama Msindai na Jena pia hawakutokea pale, ila mzee Msindai alifika tena kumwangalia mtoto na Sabrina. Akampakata mtoto na kucheza na wajukuu zake wengine, kisha akaondoka.

Kumbuka Shuka Kumekuchwa!

M

zee Msindai alipoondoka tu Sabina akamsogelea Sabrina na begi dogo alilokwenda kulifuata kwenye gari wakati Mzee Msindai akiaga, akamkabidhi Sabrina. “Ni nini hii!?” “Amenipa Tino.” Sabrina alishituka karibia kutupa chini. “Nakushauri upokee tu Sabrina. Tino ametoka Italy amenitafuta na kunisihi nikukabidhi hili begi kwa wema tu,  si matatizo.” Hapo akavuta masikio ya kila mtu hapo chumbani kwake ambako walikusanyika na bibi harusi mwenyewe akiwa amelala na mzazi. “Amesema hakuna haraka. Ila amesema itakusaidia sana. Hata kama ni baada ya miaka hata mitatu, anashauri ubaki nalo tu, uje ulifungue na kuona alichoweka humo ndani. Ameahidi hatakusumbua kwa lolote lile. Ila ameomba upokee hilo begi.” Wala Sabina hakuwa akizungumza kwa sauti kubwa, ndogo tu kama kunong’ona, lakini kila mtu aliweza kusikia.

“Kuna leo na kesho mdogo wangu. Akili kumkichwa.” “Kwani wewe umezungumza naye!?” Sabrina akamuuliza kama anayetaka kujua kama anajua kilichoendelea kati yake na Tino!  “Sana tu. Tena hakunificha kitu hata kimoja. Mimi mpaka ikabidi kuomba hekima za mama. Tino yupo na hali mbaya ya majuto kupita kiasi. Anasema ameandika barua kabisa akikiri watoto ni wako na hakuna atakayekusumbua tena, ila anataka kukusaidia akitambua malezi ya watoto wawili ni gharama na mengine mengi amesema ameandika vipo humo ndani. Nia anasema ni kusaidia tu si kukuvuruga. Anasema alifanya kosa ambalo linamgharimu mno maishani, ila hataki kuendelea kutenda kosa.” Sabrina akabaki kama amepigwa na butwaa.

~~~~~~~~~~~~~~~~

v  Mungu Wa Sabrina Safari Hii Anajibuje?

v  Sabrina Ataelewaje Majibu Ya Mungu Wake Aliyemuomba Kwa Mara Ingine Tena, Akiwa Kwenye Uchungu Akiwa Hospitalini, Akiwa Na Maumivu Ya Makali Ya Kujifungua Mtoto Kwa Upasuaji Na Kusemwa Vibaya Na Mama Mkwe Na Wifi, Pamoja Na Jack Aliyemficha?

v  Nini Kitaendelea Kwenye Ndoa Hii Iliyoingiliwa Na Mama Mkwe Kukiwa Na Ahadi Nzito Ya Mafanikio Kwa Jack?

v  Wakati Jack Akiwa Kwenye Kinyang’anyiro Cha Ubunge, Tino Arudi Kwa Upya?

       Usipitwe Na Muendelezo.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment