Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAKOSA! – SEHEMU YA 49. - Naomi Simulizi

MAKOSA! – SEHEMU YA 49.

Pendo Bado Asimama Na Sabrina.

Alimkuta Pendo akimsubiria kwenye gari. “Mtoto yuko wapi!?” “Bado yupo na bibi yake.” Sabrina akajibu akipanda garini. “Pole Sabrina.” Sabrina akacheka taratibu ila mpaka usoni alikuwa amebadilika. “Umekunywa dawa za maumivu?” “Haya ni maumivu ya moyoni dada. Nimetoka kumuomba Mungu anisaidie. Maana naumwa! Kuliko nitakavyokwambia. Naumwa dada, ni Mungu ndiye aniponye, wala si dawa.” “Pole sana Sabrina. Pole.” “Nashukuru.” Sabrina akajiegemeza kwenye kiti akafunga macho, akatulia kabisa. Pendo akavuta pumzi kwa nguvu na kunyamaza. Kimya.

          Baada ya muda Jack akaja na mtoto. “Huyu mtoto aliandaliwa kila kitu kule kwa mama, Sabrina! Kwa nini hukusema mapema kuepusha usumbufu usio na sababu wa matayarisho yake? Kwanza pale nyumbani kwa Pendo hakuna nafasi yakutosha. Nyumba imejaa sasahivi.” Sabrina kimya kama Pendo. “Kama ni mambo ya Ubunge, sikukwambia kwa nia nzuri tu na kwanza ni kwa sababu ya kuwa na chaguzi nyingi. Hakuna ubaya kuwa na chaguzi nyingi.” “Tafadhali ukipata nafasi uniletee nguo zangu na za kaka pale nyumbani kwa Pendo.” Sabrina akaongea hivyo huku akimpokea mtoto.

          “Nashukuru kwa kila kitu Jack. Kunilipia gharama hapa hospitalini na...” “Mbona unaongea kama hatutakuja kuonana tena!?” “Naomba nisaidie kufunga mlango, tafadhali.” “Sasa mbona umemleta mtoto bila kiti chake na wewe Jack!?” Pendo akauliza kwa hasira kidogo. “Naomba tu twende dada. Natamani kulaza huu mgongo. Kiuno kinauma na tumbo nalo linakata. Nahisi nimechafuka tena.” “Wewe Sabrina! Tena!?” “Inatoka kama bomba!” “Si uliniambia usiku kuchwa hakuna iliyotoka?” “Sijui dada! Twende tu, labda nikitulia itapungua.” “Kwa nini tusimuulize daktari kabla yakuondoka.” “Nashukuru Jack, ila acha nikawahi wanangu. Twende dada.” Sabrina akaweka msisitizo, Jack akaweka mfuko wa dawa miguuni na kufunga mlango, Pendo akaondoa gari, Sabrina akiwa amepakata mtoto wake.

          “Kwa nini hukutaka kumwambia ukweli Jack?! Ungemwambia tu. Maana wenzio watamjaza maneno yasiyo ya kweli mwishowe wewe utaonekana mbaya.” Wakiwa njiani Pendo akaanza. “Tayari mimi ni mbaya dada. Historia yangu inajirudia tena. Ilikuwa hivihivi kwa Tino. Tulikuwa na mipango mizuri sana na Tino. Max alipoona Mungu ametenda, ndipo na yeye akaingilia ili kujinufaisha yeye binafsi. Sasa ndicho kinachotokea kwa Jack. Mama yake anatamani sana abakie yeye mwenyewe kwa Jack. Kama ulivyomsikia, anaumia kuona niliyomfanyia mimi Jack ndio yamekuwa makubwa na kuingia kwenye historia ya maisha ya Jack halafu yeye hatajwi. Anachotaka kufanya sasa hivi ni kumfanikisha Jack kwa njia alizobuni yeye, ili abakie yeye ndio amemfanikisha Jack kwenye aina hiyo ya Ubunge, si ubunnge wa Singida ambako atajulikana ni Sabrina, si yeye.” “Sabrina! Ujue ni kweli! Wewe umesema. Mama Msindai ni mtu wakupenda sana sifa.” Akaongeza Pendo kama aliyefunguliwa macho.

          “Hata kwenye ile babyshower ya mapacha wako alitaka kufanya ugomvi, sema wanamuogopa sana Jacinta. Jacinta akawa mkali na kumwambia waziwazi kabisa kama hawezi, aondoke. Aliumia mambo yalikwenda vizuri bila yeye kuhusishwa na akakuta kuna wakubwa wengi tuliwaalika siku ile wakakubali bila hata kumtumia yeye.” “Sasa ndicho kinachompata na kilichotokea Singida siku wa uzinduzi wa kile chama kwa upya. Dada ule mji ulifurika watu wazito wenye majina na vyeo ambao hata mimi sikutegemea! Halafu na yeye hakuhusishwa kuombwa akaribishe mtu hata mmoja. Yaani akaja kukutana nao pale kwenye shuguli. Mambo yaliyotendeka siku ile pale na watu kunitambua na mimi, hata mwanae pia kusema yote yasingewezekana bila mimi, kinamuuma sana mama Msindai, ndio maana anahangaika.” “Sabrina wewe umesema kweli!” Pendo akaendelea kuamini.

          “Lakini dada si mimi. Ni Mungu. Sabrina mimi sina uwezo hata wakuwa na mtu kama wewe dada!” “Usiseme hivyo Sabrina!” “Mimi sikudanganyi dada. Najijua mimi ni nani na kile Mungu ananitendea. Sina uwezo wowote ila Mungu.” “Sasa kwa nini humwambii Jack.” “Hata kidogo. Jack si mtoto mdogo, dada. Halafu mahusiano ya Jack na mama yake ni ya muda mrefu sana, hayatavunjwa na mimi kamwe. Sitataka mimi kuingia katikati yao. Mwache Mungu ashughulike nao. Sijawahi kufanikiwa kwenye kujitetea dada. Tokea mtoto mimi ni mbaya sana kwenye kujitetea. Sijui ni kwa nini! Tunaweza tukawa tumefanya kosa wote pale nyumbani, wenzangu wakajitetea na kupona, mimi nikaishia kuingia matatizoni na wazazi kunichapa kabisa. Nilipongundua huo udhaifu wangu, nikaacha kujitetea kabisa. Nilipomfahamu Mungu kwa undani, nikamuomba awe mtetezi wangi.” Mpaka Pendo akaanza kulia.

          “Hajawahi kuniacha hata kwenye yale magumu mno. Huwa ananitetea kimyakimya na kuniinulia msaada mpaka huwa nashangaa. Tino aliponiacha mjamzito, peke yangu, niliingiwa na hofu kubwa sana, na nilikuwa na maumivu kama hivi. Nililia dada, na mbaya zaidi nilijua nilimkosea Mungu. Niliishi na Tino kimapenzi nikiwa nimetoka kufunga na Mungu kunikutanisha naye. Nilimlilia Mungu kwa toba nikimsihi asiniache, mbona alinitumia Jack! Huyu Jack nililetewa na Mungu. Wala sitapambana nao, dada. Nilifanya mengi kwa Jack, si kwa ajili yake. Kama ilivyokuwa kwa Tino, ndivyo kwa Jack. Nilimtengenezea jina pale Singida, nikiwa najinyima mno na mimba ya huyu mtoto. Nikifunga na kuomba huku mjamzito, bila kumwambia Jack, mpaka Mungu akafanikisha kwa kiwango cha juu sana.” “Lakini Jack alisema. Bila wewe asingejulikana. Kabla ya kuanza kumuhangaikia, alikuwa tayari kurudi huku mjini.”

          “Sasa hicho ndicho kinachomuuma mama Msindai na kumshangaza mpaka anasema ni uchawi kumbe mwenzie naanzia magotini.” Hapo akamgusa Pendo. “Huyu simba wa kabila la yuda, dada!” “Si mchezo.” “Acha dada. Ana mtindo wa kunguruma! Akinguruma mahali, hamtabaki kama ilivyo. Watu wanachanganyikiwa. Wala si Sabrina. Ingekuwa mimi nisingeumia hivi. Lakini ni yeye ananguruma dada, mpaka na mimi naumia kwenye masikio ya rohoni! Ila acha dada. Nimetoka kumwambia pale hospitalini kuwa, amenguruma kupita kiasi, mpaka masikio yangu ya nafsi yameumia. Yeye ndio aniponye.” “Jamani Sabrina!”

          “Kweli dada. Ni yeye tu. Yesu aingilie kati. Maana kama isingekuwa yeye kujibu kwa MOTO, nani angeona moshi mkali hivi na kuwafanya watokwe na machozi yasiyo koma!” Pendo akacheka sana. “Sabrina una maneno!” “Nakwambia kweli dada. Moshi huwa unamtindo wakuumiza macho mpaka machozi. Ndicho kinachompata mama Msindai. Aliyoyatenda Mungu mpaka sasa masikio yanawasha, moshi unamuumiza macho yeye na Jena, wanalia bila kujijua. Namuachia Mungu. Nitanyamaza kimya, nimemsihi mtetezi wangu aanze kazi yake. Hakika atasimama na kunitetea TENA.” “Nilikuwa nimeumia Sabrina, lakini umeniinua nafsi yangu mpaka nakuhurumia wewe.” “Hata mimi huku kuongea hapa kumenifanya nimepata faraja.” Wakaanza kucheka.

          “Ila nasikia maumivu dada!” “Acha kabla hatujafika nyumbani kwenye ile fujo ya wanao, tupate muda wa maombi. Tumsihi mtuliza bahari, atulize dhoruba ndani yako.” “Niombee na ndoa yangu. Shetani anataka kupenya.” Pendo akatafuta sehemu wakaegesha gari. Yakaanza maombi hapo. Wawili hao waliomba zaidi ya nusu saa. Mpaka wanamaliza hapo, vicheko. “Mama wewe ni muombaji!” “Wewe hujioni?” “Wewe ndio umeniambukiza Sabrina.” Wakacheka. “Basi najisikia moyo umetulia kabisa mpaka mwili!” “Amen.” Pendo akatoa gari pale kuelekea kwake wakiwa wanacheka. “Mwanao mtulivu! Amelala hata hageuki!” “Halafu nahisi amejisaidia. Nitambadilisha nyumbani.”

~~~~~~~~~~~~~~~~

          Walifika nyumbani kwa Pendo na kuwashangaza, zaidi mama yake Sabrina. “Basi mimi nikajua uzazi huu, ukweni!” “Naona kazi bado unayo wewe bibi wa wajukuu watatu.” Akajibu tu hivyo Sabrina wakacheka. “Haya mlete kaka.” Mama Sabina kampokea Brayan kwa furaha zote bila swali la ziada. Wanae wakafurahi sana kumuona mama yao. Wakaanza kurukaruka. Sabrina akacheka. “Na mimi nilikuwa na hamu na nyinyi! Mmependeza! Nani amewasuka?” “Nimewavizia wakati wamelala.” “Asante mama. Wamependeza kweli. Waone na macho yao.” “Kweli wamependeza. Una watoto wazuri Sabrina!” “Sasa dada Pendo si useme tu wazuri kama mimi!” Wakacheka sana. “Siamini Sifa! Hata wewe unanipinga!” “Dada mimi nimefurahi kukuona.” “Mmmh!” Sabrina akaguna na kupitiliza chumbani.

          “Pendo dada yangu, naomba uje huku uzungumze na hii timu yangu, wakati naoga.” “Na mimi nakuja kujilaza hapohapo kwenye godoro lao.” “Si upande hapo kitandani tulale wote?” “Sasa si na wao watataka kupanda kitandani wakati kaka naye anataka kulala!” “Hapo kweli. Basi mama mwenye nyumba wewe karibia hapo kwenye godoro.” Wakacheka wakati Pendo na watoto wote wakimfuata Sabrina huko chumbani. Na mama yake akiwa na Brayan wakawa wanaingia ili kumbadilisha. Walipata chumba kimoja hapo kwa pendo. Sabrina na watoto wake wote wakapata chumba kimoja. Mama Sabina ikabidi ahamie chumbani kwa Sifa kwani alikuwa akilala hapo kwenye chumba na watoto wa Sabrina. Willy alikuwa na chumba chake. Pendo ndio anatumia chumba kikubwa humo ndani, master bedroom. Cha mwisho ndio hicho kilijazwa vitu vya watoto watarajiwa wa Pendo. Nyumba ikawa imejaa haswa. 

Kwa Msindai.

J

ioni Junior, Joy na Jacinta wakaelekea nyumbani kwao moja kwa moja wakijua Sabrina aliruhusiwa na kuelekea nyumbani kwa wazazi wao. Walimkuta Jena yupo hapo. “Wewe kazi vipi?” Kaka yao akauliza akikaa. “Nimefika na mimi muda si mrefu.” “Na hospitalini pia ulikuwepo?” Akauliza Jacinta. “Mbona maswali mengi hivyo!?” Jacinta akamwangalia na kuelekea kwenye kabati. “Hakuna wine huko. Nimeishiwa nategemea kesho ndio nikanunue.” “Nilivyo na kiu! Mzazi yuko wapi?” Jacinta akauliza na kumgeukia Jack aliyekuwa kwenye simu yake.

          “Kabadili mawazo, yupo kwa Pendo.” Akajibu Jack nakufanya wote wamgeukie. “Kwa nini tena!?” “Halafu kama yupo kwa Pendo kwa nini wewe uko hapa!?” Junior akaongeza swali kutoka kwa Jacinta. “Kwani kila alipo Sabrina ndipo awepo Jack!?” Akadakia mama Msindai na kumshangaza kila mmoja mle ndani. “Hebu subiri kwanza mama. Pengine mimi ndio hamjanielewa. Nauliza hivi, kama Sabrina yupo kwa Pendo, kwa nini Jack anaonekana yupo hapa?” “Tena anaonekana amekuwepo hapa na pensi yake hiyo anayoshindia hapa! Kuna nini?” Akaongeza swali Jacinta.

           “Kwa hiyo nyinyi ndio mnataka muwe mnajua kila kitu cha Jack kama nyinyi ndio mmemzaa nyinyi?” “Mbona ukali kwenye swali dogo tu mama Msindai?!” Junior akauliza akicheka. “Naona unataka kuendesha familia yako na ya Jackson!” Junior akakunja uso, mkewe akacheka kwa kuguna. “Unaguna nini na wewe Joy.” “Naomba wala nisijibu mama yangu. Nikuachie tu huyo Junior.” “Pengine kuna ziadi ya hili linaloendelea hapa, sisi tuliokuja sasa hivi hatujui. Maana naona mama umejiandaa kwa ugomvi! Eti Jackson Msindai, kwema?” “Jacinta unanitafuta wewe!”  Mama Msindai akawaka. “Hee!” Jacinta na Junior wakahamaki kwa pamoja.

          “Wanaumia kuona safari hii wamepitwa. Hawajui mambo ya Jack. Washazoea wao kuwa washauri wa Jack, wampotoshe vile wanavyotaka wao. Sasa mtajibeba.” Jena akasimama na pochi yake. “Una uswahili wewe kama sio daktari! Umejawa maneno maneno ya uchonganishi na ushabiki! Hujui unaongea nini wala na nani!” Jena akamcheka Jacinta na kuongeza bila kujibu shutuma zake. “Mmepitwa safari hii. Haya nendeni makwenu, Jack yupo na mama yake. Hamna wakumuharibu kichwa.” “Unazungumza nini wewe Jena!?” Akauliza Junior akionyesha hasira na sintofahamu. “Sitaki maneno na wewe Junior. Mimi nimeletwa na yangu, naondoka. Mambo ya Jack na familia yake, mwacheni Jackson mwenyewe. Yeye anajua nini chakufanya, acheni kumfuatilia kila wakati na kumwambia mnachotaka nyinyi afanye.” “Nani huwa anafanya hivyo kama sio umbea tu?” Akauliza Jacinta.

          “Nyinyi wawili. Junior na wewe Jacinta.” Akajibu mama Msindai, Jena akacheka sana kwa kuwakera. “Mwenye mtoto amekataa na mtoto wake. Kafanyeni yenu yanayowahusu.” Jena akaongeza na kutoka akicheka. Junior na Jacinta wakaangaliana. “Hata mkiangaliana, mtanifanya nini sasa?” Akauliza mama Msindai. “Jamani sisi tunaona tuondoke. Twende Joy mke wangu.” “Naona na mimi pia niondoke.” “Muwe na usiku mwema.” Akaongeza mama Msindai, Jack kimya ameinamia simu yake.

Kwa Pendo.

M

ama Sabina akashangaa mpaka giza linaingia Jack haonekaniki pale, ila Willy akarudi kutoka kazini, Pendo amelala kitandani na Sabrina. Willy akacheka. “Sasa hapa timu imekamilika.” “Umeona eeh! Hapa roho kwatu!” Akajibu Pendo. “Pole na kazi.” “Asante. Mzee Msindai atapita hapa muda si mrefu kumuona tena mtoto.” “Yule baba ana upendo jamani!” “Ni daktari wa watoto pia. Hataki kufanyike kosa.” Willy akajibu. “Lakini pia anao upendo wa kibaba.” “Mtu mzima pia. Hana mambo ya kitoto. Ila nahisi hata Junior amechukua moyo wake. Mstaarabu sana yule kaka.” Mama Sabina alikuwa akiwabadilisha nguo wajukuu zake hao wawili ili walale. Akabaki akisikiliza tu, Sabrina kimya amejilaza na mwanae.

          “Vipi na wewe Sabrina?” “Tumbo lilikuwa likiuma, ila limepoa. Nililala tokea nitoke hospitalini, ndio tumeamka na Pendo sasa hivi.” “Sasa mtoto! Mtamuua mtoto kwa njaa nyinyi wawili.” Pendo na Sabrina wakacheka. “Huyu Sabrina anabaraka ya maziwa. Yanamwagika kama bomba! Alikamua na kumuachia mama. Ndio akawa anayatumia kumpa mtoto wakati tumelala. Halafu mwanae mpole kweli. Si mlizi.” Wakati wanazungumza wakasikia sauti ya Mzee Msindai. “Ngoja nikamkaribishe.” Willy akasimama na kutoka.

          Baada ya muda wakaingia hapo ndani na kuanza kutania watoto kwanza. Aliwajulia watoto, mpaka kina Jeiline wakawa wanamchekea. Na yeye akapewa mabusu. “Hapo sasa roho imeridhika. Mbona mnapendeza usiku huu?” Wakajipigia makofi wakicheka. “Mwambieni babu urembo huu ni wakitandani!” Akajibu bibi yao. “Kweli nyinyi ni warembo! Hapo ndio mnakwenda kulala?” Wakajipigia tena makofi, Pendo na Sabrina wakazidi kucheka. “Hiyo ndio kazi yao hao. Kupiga tu makofi. Karibu baba.” “Kaka yao anaendeleaje?” “Mlalaji kweli!” “Acha nimwangalie kidogo.” “Nashukuru baba yangu.” “Karibu Mzee Msindai.” Pendo akamkaribisha akimpisha hapo kitandani. “Sasa na wewe Pendo unapata usingizi wa mchana au usiku.” Pendo akacheka. “Nishapata wa mchana, hapohapo, wa usiku naenda kuupata chumbani kwangu.” Wakataniana kidogo na Msindai, wakamuona anaanza kumpima mapafu.

          Akatulia akimsikiliza akitumia stethoscope. “Naona hiki kifua ni cha mkimbiaji kabisa! Apewe jembe akalime.” Wakacheka. “Nashukuru baba yangu.” “Karibu. Usiwe na wasiwasi kabisa. Huyu naona mzima kabisa. Baba yao yuko wapi? Simuoni hapa!” “Nilimuacha hospitalini na mama.” Akajibu tu hivyo Sabrina. “Basi naona kila kitu kinakwenda sawa. Mlale vizuri, nitakuja kuwaona tena kesho.” “Nashukuru sana baba yangu. Usiku mwema.” Akacheza kidogo na watoto, wakati Willy anamsindikiza nje, Jack naye akawa anaingia na mizigo.

          “Tuzungumze kidogo hapo nje Jackson.” “Sawa baba.” Willy akampokea mzigo na kutoka na baba yake. “Pole na kazi baba.” “Asante. Nilitaka kukushauri uongoze umakinifu kidogo tu. Unafanya vizuri, lakini kuwa makini zaidi. Ni hilo tu.” Jack alimjua baba yake si mwenye maneno mengi. “Naamini unaelewa.” “Katika nini? Labda unisaidie kufafanua kidogo.” “Familia ndio msingi mkubwa wa kila kitu. Nikimaanisha kila kitu. Mafanikio ya aina yeyote ile, yanaanzia kwenye familia. Ikishashindikana nyumbani, au familia ikiyumba tu, hakuna mafanikio yeyote yale huwa yanasimama. Hata kama yatasikika ni makuu sana, kama msingi wa familia ukiwa mbovu, hakuna kinachosimama.” Akatulia mzee Msindai akimtizama kama kumpa nafasi.

 “Sijui kama unanielewa?” “Nakuelewa baba.” Akajibu Jackson. “Hapo ulipo, Junior alipita lakini kilichomsaidia yeye ni msingi mzuri, ndio maana mpaka leo unamuona yupo kwenye mafanikio. Hana cha ajabu sana na watu wengine au mawaziri wengine, lakini msingi wa familia yake ndio unamuona ametulia vile. Akifanya mambo sahihi, na ufahamu wake upo wazi akiwa na uwezo mkubwa sana wa kuelewa mambo magumu, hata kuyafanya yaliyo magumu ndio maana hata wakimtafuta na kosa hawapati, ila siri ipo kwenye msingi. Pakiwa bado pabichi kabisa, tengeneza msingi mzuri na imara. Ni hivyo tu. Usiku mwema.” Mzee Msindai akaondoka na kumuacha Jack amesimama hapo nje akiwaza.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Mambo yalishaiva. Alishachukua fomu za kugombea ubunge wa Afrika mashariki kama alivyoambiwa na mama yake. Kesho yake ndio anatakiwa kwenda kujinadi. Alifanya kila kitu kama alivyoshauriwa na mama yake akimwambia asubiri asiseme lolote juu ya hilo mpaka atakapofanikiwa. Alipomwambia hawezi kumficha Sabrina, mama Msindai akatumia hekima ya kimama kwa kiziwanda wake mpaka Jack akakubali. Ila sababu kubwa aliyompa mwanae ni kumwambia kutosema kwa haraka ili asimchanganye Sabrina ambaye amewekeza sana huko Singida. Ahangaike kimyakimya mpaka akipata ndipo amwambie ili wachague pamoja ila lengo la mama Msindai ni kama alivyomgundua Sabrina. Ilikuwa ni hila tu.

 Kama kawaida yake alimpigia simu kaka yake kama mkongwe kwenye siasa na mwenye hekima akamuuliza tu kwa kifupi anachukuliaje aina hiyo ya Ubunge, Junior akajibu jibu la ujumla uzuri wa hiyo nafasi, faida zake, Jack akaridhika, asimwambie kama ameshauriwa na mama yake agombanie. Kwa hiyo hata Junior hakuwa akijua kinachoendelea. Ikabakia ni Jackson  na mama yake  wakiweka mikakati na Jena kama mpambe wao, ila mzee Msindai yeye alishasikia kwenye mazungumzo ya mikakati hiyo kwa simu kati ya Jackson na mama yake, kama kawaida yake mzee huyo hakuuliza. Alinyamaza tu.

Sasa Jackson akabaki akifikiria. Akahisi ameshakosea. Mambo yameshajulikana kabla. Sabrina amekasirika. Na pia hakupenda kabisa jinsi walivyoachana na kaka yake pamoja na Jacinta usiku huo nyumbani kwao. Akahisi amekuwa msaliti kwa watu waliosimama naye kwa kipindi chote hicho! Ghafla akajikuta kwenye kambi ya mama yake na Jena ambao wote wanajulikana ni wapinzani tokea mwanzo! Baba yake naye anampa maonyo ya mafumbo lakini alijua wazi ni nini anamaanisha. Asimamie wapi! Afanye nini! Akawaza Jackson. Mambo yameshafika mbali. Na yeye ameshashawishika. Ubunge anautaka tena kwa haraka. Na ahadi ya kuupata upo! “Hakika siwezi kurudi nyuma. Hangaika yote hii itakuwa bure kabisa. Nikishaupata na Sabrina akaona mafanikio yote haya, lazima yeye mwenyewe ataunga mkono tu!” Jack akafikia muafaka wa kuendelea. Alisimama hapo nje kwa muda akifikiria, ndipo akarudi kwenye gari aliyokuwa amekuja nayo na kuchukua mizigo mingine, akaingia nayo ndani.

~~~~~~~~~~~~~~~~

            Aliingia ndani akakuta nyumba imetulia kama kawaida ya nyumbani kwa Pendo.  Willy na Pendo walikuwa mezani wakila. Wao wawili tu. “Karibu Jack.” “Mimi nimeshakula. Sabrina yuko wapi?” “Naona wamelala na mama yake huko chumbani pamoja na watoto.” Akajibu Willy, Pendo kimya. “Hiyo mizigo labda uiweke tu hapo, na uitolee maelezo kama yapo. Vinginevyo Sifa ataiingiza huko chumbani kesho.” “Sabrina amelala muda mrefu?” “Ndiyo.” Akajibu Pendo akimtizama Jack kama aliyekwisha mkera.

          “Na naomba upunguze sauti Jack, watoto wamelala. Bibi yao amewabembeleza muda si mrefu na yeye anataka kumpumzika. Alikuwa nao hapa siku nzima kama Sabrina  tu. Ungetaka, ungewahi kuja. Acha kelele.” Pendo akawa mkali kwa Jack. Jack alibakia akimtizama na kumsikiliza. Pakatulia kwa muda. Willy na Pendo wakaendelea kula. “Usiku mwema.” Mwishoe Jack akaaga. “Sasa kesho tunatakiwa kanisani Jack, kwa ajili ya kukutana na mchungaji kwa mara ya mwisho kabla ya harusi. Nimesikia unamipango mingine ya ubunge kesho hiyohiyo. Sasa nataka kujua kama utaweza au nitafute mtu mwingine? Maana Sabrina amesema yeye ataweza, ukishindwa itaeleweka tu. Naweza kumuomba kaka Junior anisimamie badala yako.” Willy akaongea bila kubembeleza.

          “Ni saa ngapi?” “Tuliweka miahadi ya saa nne na nusu asubuhi.” “Hatuwezi kusogeza?” “Hapana kwakweli. Wa muhimu alikuwa Sabrina. Pendo alisema nilazima Sabrina, ndio maana tulimuomba mchungaji isiwe leo ila kesho. Mimi sina ulazima au chaguzi ya mtu wakunisimamia, nataka kuoa. Kwa hiyo sitaki kumyumbisha tena mchungaji kwa mara ingine tena. Ni kesho saa nne na nusu asubuhi. Kama hutaweza, uwe na amani kabisa, uniambie nitafute mtu usiku huu huu nikamilishe hili swala. Sitaki kuyumbishwa.” “Sikuwa najua Willy, ningejipanga! Muda huo nitakuwa kwenye..” “Kama nakuelewa sawasawa ni kwamba kwa muda huo hutaweza? Ndiyo au hapana. Nijibu kwa ufupi tu ili tujaribu kuokoa hili swala, nisikwame kwa ajili ya msimamizi.” Jack akawa kama amebanwa.

“Nafikiri mchungaji ataelewa kwa kutokufika kwangu kwa kesho tu. Ila jumamosi nitakuwepo.” “Wewe unataka kunikwamisha Jack na maswala yako ya sirisiri. Mimi katika hili sitayumbishwa aisee. Najua ninachotaka, na si siri. Nilikupigia muda mrefu tu kukuomba, ukakubali. Huu ujuaji unaotaka kuuweka mpaka kanisani kusema mchungaji ataelewa, hapo nikutaka jambo langu likwame wakati mambo ya siasa mimi nayajua. Nyinyi wanasiasa huwa mnaongea chochote hata kama mnajua kabisa si kweli, ilimradi tu kufanikisha mambo yenu. Sasa hapa unataka kunipiga siasa mimi, nikae nikijua na sisi tumepatana katika hili kumbe mwenzetu unamipango yako mingine ya siasa.” “Hakuna jingine Willy! Mbona hivyo!?”

          “Acha kuniuliza kama hujielewi Jackson. Swala la harusi yangu kuwa ni jumamosi wewe ulilifahamu tokea lini?” Kimya. “Zaidi ya majuma mawili! Kila anayenihusu alifahamu likawa wazi. Nikawauliza kabisa kama mtaweza. Sabrina akakubali, na wewe ukakubali. Wewe swala lako la huu ubunge ulilijua lini? Kinachoendelea kesho si chakushitukizwa kwako ila kwetu sisi uliyetukubalia! Huwezi ukaniletea siasa kwenye ndoa ninayoitaka Jack. Sio hapa, na si katika hili. Tafadhali nikushukuru tu, nitatafuta mtu mwingine. Wewe endelea tu. Acha nipige simu mbili tatu kuona mtu mwenye utayari.” “Mimi nipo tayari Willy. Acha hasira. Nitasimamia harusi yenu.” Willy akacheka akivuta simu yake.

          “Nakushukuru muheshimiwa Jackson Msindai, lakini hapana. Mimi siasa nazijua kaka. Huwa hazinaga macho. Haziangalii utu wala mtu, ni kufanikisha maswala ya siasa kwanza, mengine baadaye. Mimi nilishaharibu, nimepata neema, acha niitumie. Wewe kila la kheri Muheshimiwa. Ila katika hili ulilokwisha onyesha mashaka hata yakuwepo kesho kwa muda wetu, hapana. Hutanisimamia tena. Ila karibu harusini kama utakuwa na nafasi. Ibada ni saa nne asubuhi pale kanisani. Tukitoka hapo tunakwenda kwenye kupiga picha. Chakula cha mchana tutakuwa hotelini na ndugu wa Pendo, pamoja na Jacinta, Sabrina na watoto wake, na familia ya kaka Junior. Ukiweza karibu. Ukishindwa sisi wote waelewa tu. Siasa si ngeni kwetu. Wote tunajua ni mchezo mchafu.” Jack akacheka na kutingisha kichwa. Pendo akasimama na kuondoka kabisa pale mezani. “Wapi tena?” Willy akamuuliza. “Naenda kuoga. Nijilaze. Si utakuja.” “Nikimaliza kufunga milango baada ya Jack kuondoka.” Jack akajua ndio anafukuzwa. Akashangaa sana vile anavyogeukwa.

          “Isingekuwa hiyo ratiba ya kesho, hakika ningekuwepo kanisani Willy. Naomba usinielewe vibaya. Na ujue wazi jumamosi hakuna kitakachoharibika. Nitakuwepo.” “Kama mgeni, karibu. Ila si kama msimamizi wangu. Umeshindwa kesho, inatosha. Wale wasimamizi wetu wa ndoa ya kwanza nao walianza dalili kama hivi wewe, nikawafumbia macho, mwishoe wakaja kuwa tatizo kwenye ndoa yetu. Sasa wewe endelea tu. Nashukuru kwa maneno yako ya utayari.” Jack akaona aondoke. Ni kweli alikuwa kwenye wakati mgumu.

~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment